TUME ya Nguvu za Atomiki Tanzania (TAEC) imetoa ufafanuzi namna ambavyo teknolojia ya nyuklia inavyoboresha sekta za kilimo, mifugo na rasilimali za maji hapa nchini.

Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania, Bw. Peter Ngamilo ameyasema hayo Agosti 2, 2022 wakati akizungumza katika Maonesho ya Nanenane yanayoendelea jijini Mbeya.
 
Amesema kuwa, Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania (TAEC) ina banda lake katika Maonesho ya Kilimo ya Nanenane yanayoendelea viwanja vya Nanenane jijini Mbeya ambalo linatoa nafasi kwa wananchi wote kujifunza mambo mbalimbali.

Amesema, TAEC inashiriki katika maonesho hayo ili kutoa elimu juu ya teknolojia ya nyuklia inavyoboresha Sekta za Kilimo, Mifugo na Maji, Afya, Nishati, viwanda madini na ujenzi.
Bw.Ngamilo amesema, teknolojia ya nyuklia hutumika kuboresha mazao ya Kilimo, Mifugo sanjari na utafutaji na uboreshaji wa rasilimali ya maji.

Amesema, matumizi ya Teknolojia ya Nyuklia duninai ni makubwa na teknolojia hii imekuwa mkombozi katika kutokomeza wadudu waharibifu katika mazao yatokanayo na kilimo na mifugo, hivyo kupunguza kuenea kwa wadudu na magonjwa, kuongeza uzalishaji wa mazao, kulinda rasilimali za ardhi na maji, kuhakikisha usalama wa chakula na kuongeza uzalishaji wa mifugo.

"Shirika la Chakula Duniani (FAO) na Shirika la Kimataifa la Nguvu za Atomiki Duniani (IAEA) ambapo Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania ni wanachama wamekuwa wakipanua maarifa na kuongeza uwezo katika eneo hili kwa zaidi ya miaka 50 na matokeo na mafanikio makubwa yanaonekana ulimwenguni kote kupitia teknolojia hii,"amesema.

Bw.Ngamilo ameainisha mifano mbalimbali ya jinsi ambavyo Teknolojia ya Nyuklia inavyoboresha kilimo na mifugo katika nchi wanachama wa Shirika la Nguvu za Atomiki Duniani kama ifuatavyo.

2.Uzalishaji wa wanyama na uboreshaji wa afya za mifugo

"Katika uzalishaji wa wanyama na uboreshaji wa afya za mifugo Teknolojia ya Nyuklia hutumika na kuleta mabadiliko makubwa kwenye sekta za kilimo na mifugo katika kuongeza uzalishaji wa mifugo, kudhibiti na kuzuia magonjwa mtambuka ya wanyama na kulinda mazingira," amesema Bw. Ngamilo.
Bw. Ngamilo ametolea mfano jinsi teknolojia ya nyuklia ilivyotumika Zanzibar na kuweza kupata mbegu bora ya mpunga aina ya Supa BC, ambapo amesema kuwa awali wakulima wa Zanzibar kabla ya utafiti na ujio wa mbegu hiyo, kwa wastani katika hekta moja mkulima alikuwa anapata gunia za mpunga sio zaidi ya kumi, lakini baada ya utafiti uliotoa matokeo ya mbegu ya mpunga ya SUPA BC, katika hekari moja mkulima ameweza kupata wastani wa tani saba na kuendelea.

"Mbegu ya SUPA BC inavumilia ukame, haipati magonjwa kirahisi, haishambuliwi na wadudu na mchele wake una ladha na kutoa harufu nzuri.
“Vilevile teknolojia ya nyuklia imetumika kumaliza Mbung’o ambao walikuwa wakitishia maisha ya mifugo huko Zanzibar ambapo mpaka sasa mafanikio yake ni makubwa na kufanya tatizo la Mbung’o kuwa historia tofauti na ilivyokuwa hapo awali,"amesema Ngamilo.

Akiendelea kufafanua, Bw.Ngamilo ametoa mfano wa nchi ya Cameroon kuwa imetumia vyema Teknolojia ya Nyuklia katika uzalishaji wa mifugo na kutokomeza wadudu waharibifu, hivyo kudhibiti magonjwa na kupelekea wakulima kuongeza mazao yao ya maziwa mara tatu kutoka lita 500 hadi 1500 na kutoa nyongeza ya dola Milioni 110 katika mapato ya mkulima kwa mwaka.

Pia imepunguza sana tukio la ugonjwa wa Brusela unaoambukiza sana, ambapo ugonjwa huo unaweza kutoka kwa wanyama hadi kwa wanadamu ambao hunywa maziwa yasiyochemshwa au kula nyama iliyopikwa kutoka kwa wanyama walioambukizwa.

3.Uboreshaji wa udongo na maji

“Teknolojia ya nyuklia sasa inatumika katika nchi nyingi ili kusaidia kudumisha mifumo bora ya udongo na maji, ambayo ni muhimu katika kuhakikisha usalama wa chakula kwa idadi ya watu ulimwenguni, kwa mfano, huko Benin, kuna mradi ambao ulihusisha wakulima 5,000 wa vijijini ambapo mavuno ya mahindi yaliongezeka kwa asilimia 50 na kupunguza kiwango cha mbolea inayotumiwa kwa asilimia 70.
"Vile vile, Teknolojia ya Nyuklia huruhusu wakulima kulima kidogo, kupanga umwagiliaji mdogo, na kuongeza mazao mara mbili wakati ambapo hutumia asilimia 55 tu ya maji ambayo kwa kawaida yangeweza kutumika maji mengi zaidi ya hayo katika umwagiliaji wa kawaida,"amesema.

4.Usimamizi wa Wadudu

Ameongeza kuwa Mbinu ya kuwahasi wadudu kwa Teknolojia ya Nyuklia (Sterile Insect Technique-SIT) inajumuisha kuwahasi na kukuza wadudu wa kiume kabla ya kusambazwa katika maeneo yalioathiriwa na wadudu. Mbinu hii hupunguza wadudu ambao tayari wamezalishwa au kuzuia kuanzishwa kwa spishi zinazovamia maeneo husika – na ni salama kwa mazingira na afya ya binadamu kuliko dawa za kawaida za wadudu.

Bw. Ngamilo ametoa mfano kwa kwenda mbali zaidi, kuwa Serikali za Guatemala, Mexico na Marekani zimekuwa zikitumia SIT kwa miongo kadhaa kuzuia kuenea kwa wadudu aina ya Medfly kutoka Ukanda wa Kaskazini mwa Maditerrania kuingia katika nchi za Mexico na Marekani. 

Amesema, Guatemala hutuma mamia ya mamilioni ya wadudu madume waliohasiwa kila juma kwa majimbo ya California na Florida ili kulinda mazao yenye thamani, kama matunda ya machungwa. Hivyo, kuhasi wadudu wa kiume, ni njia timilifu ya kuzuia uzazi wa wadudu.

5.Usalama wa chakula

Bw. Ngamilo amesema, mifumo ya usalama wa chakula na mifumo ya udhibiti wa ubora unahitajika kuwa thabiti kwa kiwango cha kitaifa kuwezesha biashara ya chakula salama na kupambana na udanganyifu wa chakula (Food Fraud), ambao hugharimu sekta ya chakula duniani kufikia hadi dola bilioni 15 kila mwaka.
Teknolojia ya nyuklia husaidia nchi zaidi ya 50 duniani kote kuboresha usalama wa chakula kwa kushughulikia shida ya mabaki na uchafu katika bidhaa za chakula na kuboresha mifumo yao ya ufuatiliaji na uchambuzi thabiti ili kuongeza usalama wa chakula.

Hivyo matumizi ya teknolojia ya nyuklia husaidia kukidhi viwango vya chakula vya kimataifa na kukuza sifa ya nchi katika biashara ya kimataifa ya chakula.

6.Mabadiliko ya hali ya hewa

Sekta ya kilimo hutumia teknolojia za nyuklia na zinazohusiana na kukabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa kwa kuongeza ufanisi wa utumiaji wa rasilimali na tija kwa njia endelevu.

Programu ya kuzalisha wanyama kwa kutumia teknolojia ya nyuklia nchi ya Burkina Faso ni mfano mzuri sana kwani imeweza kusaidia wakulima kuzalisha wanyama wenye tija na sugu ili kukabiliana na hali ya hewa ya nchi hiyo

"Programu hiyo inachangiwa na tathmini ya maumbile katika maabara nne za kitaifa, huku wanasayansi pia wakiweza kutumia teknolojia inayohusiana kutengeneza malisho ambayo ni makubwa zaidi," amesema Bw.Ngamilo.
7.Kuzuia njaa ya msimu

Bw. Ngamilo amesema kuwa kupitia programu za uzalishaji wa mazao kwa kutumia teknolojia ya nyuklia hapa nchini teknolojia ya nyuklia itasaidia vijiji vilivyo katika mazingira magumu kuhakikisha usalama wa chakula, kukabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa na hata kukabiliana na njaa ya msimu kwa Kupanda aina mpya za mazao yanayoweza kufupisha mchakato wa kukua, na hivyo kuwaruhusu wakulima kupanda mazao ya nyongeza wakati wa msimu wa ukuaji.

Ngamilo ametoa mfano kwamba katika miaka ya hivi karibuni, wakulima kaskazini mwa Bangladesh wamekuwa wakitumia aina ya mpunga inayokomaa kwa muda mfupi, inayoitwa Binadhan-7.l hivyo kuokoa muda wa mavuno na kupata mazao kwa wakati
Aina hii huzaa siku 30 haraka kuliko mchele wa kawaida, huwapa wakulima wakati wa kuvuna mazao na mboga zingine kwa msimu mmoja, uzalishaji wa mpunga nchini Bangladesh uliongezeka kutoka tani milioni 26.8 mnamo 2003-2004 hadi tani milioni 33.8 mnamo 2012-2013.

8.Ukabilianaji na Janga inapotokea dharura (Alama ya Taadhari ya Uwepo wa Mionzi)

Hofu ya matumizi ya teknolojia ya nyuklia imekuwepo kwa baadhi ya wananchi, lakini ifahamike ya kwamba mionzi iko katika kila kitu kinachotuzunguka, kutoka katika jua hadi udongo, hata mifupa ya miili yetu ina mionzi.

Lakini ikitokea dharura ya tukio la kinyuklia, juhudi za ziada inabidi kufanyika ili mionzi isiingie kwenye mazingira ili kupunguza athari kwenye bidhaa za kilimo. Kwa mfano wakati wa dharura ya nyuklia ya 2011 huko Japan, Shirika la Chakula Duniani (FAO) na Shirika la Nguvu za Atomiki Duniani (IAEA) walitengeneza taarifa pana na ya kuaminika juu ya chakula kilichochafuliwa na mionzi.

Taarifa hii ilisaidia kubadilishana habari na kuwezesha na kuelekeza njia sahihi ya kufuata ili kulinda wateja, katika sekta ya chakula na ulimwengu kwa jumla.

Kwa elimu zaidi TAEC inakukaribisha kwenye Maonesho viwanja vya Nanenane Jijini Mbeya na Viwanja vya Nanenane vilivyopo TASO Arusha ambapo pia TAEC inashiriki kikanda katika kuendelea kutoa elimu kwa wananchi juu ya majukumu inayoyatekeleza hapa nchini kwa mujibu wa Sheria ya Bunge Namba 7 ya Mwaka 2003.
Share To:

Post A Comment: