NA DENIS CHAMBI, TANGA.

Wakala wa vipimo Tanzania ‘WMA’ mkoa wa Tanga imewataka wauzaji na wasambazaji wa mitungi ya gas ya kupikia  ya  jumla na reja reja kuhakikisha kuwa ujazo wa mitungi wanayowauzia wananchi inakuwa sahihi  na kuepukana na udanganyifu wa aina yeyote ile ili kujipatia faida zaidi kinyume cha sheria na taratibu zilizowekwa.

Wito huo umetolewa na  Afisa mwandamizi wa wakala wa vipimo Tanzania ‘WMA’ mkoa wa Tanga Ally Mtowa wakati akizungumza na waandishi wa habari kwenye maonyesho ya 10 ya  biashara na utalii  yanayoendelea katika viwanja vya Mwahako ambapo alisema katika kuwadhibiti wauaji wote wa mitungi ya gas ofisi hiyo imekuwa na utaratibu wa kutoa elimu kwa wafanyabaishara wote.

“Tumeshafanya semina kwa wadau ambao wanafanya biashara za kuuza gas  wakiwemo wale wanaojaza mitungi  viwandani pamoja na wale wauzaji wa jumla na reja reja wamepewa elimu  ya namna gani wahakikishe mitungi inakuwa na ujazo sahihi na anatakiwa wawe na mzani ambao umehakikiwa na wakala wa vipimo na apime ule mtungi wa gas kama una ujazo sahihi  kabla hajaanza kumuuzia mwananchi”

Aidha amewataka wafanyabiashara na wamiliki wa vituo vya mafuta kutokuchezea mizani wakati wa kuwahudumia wateja  akisema kuwa yapo  baadhi ya malalamiko kutoka kwa wateja wakiwemo wamiliki na madereva wa  vyombo vya usafiri wakilalamika juu ya changamoto hiyo ambayo inaenda kinyume cha sheria zilizowekwa .

Hata hivyo Mtowa alisema katika kutua changamoto  licha ya kuendelea kuwabana na kuwachukulia sheria wamiliki na wafanya biashara wa vituo vya mafuta  ofisi ya wakala wa vipimo mkoa wa Tanga imekuwa ikitoa elimu kwa wananchi mara kwa mara ili kuwa na uelewa pale wanapoenda kupata huduma hiyo huku akiwataka kutoa taarifa pindi wanapo baini udanganyifu wa aina yeyot. 

“Majukumu yetu zaidi ni kumlinda mlaji  na madhara yatokanayo na vipimo ambavo havina usahihi mfano katika vituo vya  kujazia mafuta tunahakikisha kipimo kinatoa mafuta kwa usahihi sheria zipo ambazo zinawaongoza na kuwabana wamiliki na wafanyabiashara wote wanaouza mafuta wapo ambao tumeshawachukulia  hatua ikiwemo kupigwa faini na kama kosa litajirudia rudia wanaweza kufikishwa mahakamani , nawaomba wawe waadilifu kuweza kuhudumia wananchi na wahakikishe kwamba muda wote vipimo vyao vinakuwa sahihi” alisema afisa huyo.

Pamoja na hayo alisistiza zaidi kwa wafanyabiashara wadogo wadogo wanaouza vyakula na vitu vya majumbani kuhakikisha kuwa mizani zao wanazotumia kupimia zinakuwa na ubora na zilizo hakikiwa n a ofisi ya wakala wa vipimo kadiri ya utaratibu uliowekwa hii ikilenga kutoa huduma zaidi kwa wananchi na kuwalinda na madhara ambayo yanaweza kujitokeza.

 “Tumekuwa tukitoa elimu mara kwa mara kwa wananchi kwahiyo tunajitahidi kwa kiasi kikubwa kuhakikisha kwamba tunamlinda mwananchi kwenye vipimo , tuna kaguzi za m iani ambazo zinafanywa na watendaji katika serikali za mitaa lakini na wao wafanyabishara wenyewe tunawaelimisha jinsi ya kutumia mizani na kama ni mwananchi wa kawaida uzingatia vitu gani na pindi unapoona kuna udanganyifu wa vipimo usisite kufika ofisni ili tuweze kuchukua  hatua zaidi” aliongeza.

Maonyesho ya biashara na utalii  ambayo hufanyika kila mwaka jijini Tanga yakihusisha makampuni na taasisi za kiserikali na zisizo za kiserikali mwaka huu  yakiwa ni ya 10 yamebebwa na kauli mbiu ya ‘Kilimo , viwanda utalii na madini ndio msingi wa maendeleo ya kiuchumi’
 
Afisa mwandamizi wa wakala wa vipimo Tanzania ‘WMA’ mkoa wa Tanga Ally Mtowa akizungumza na waandishi wa habari wakati wa maonyesho ya 10 ya biashara na utalii yanayoendelea katika viwanja vya mwahako jijini Tanga.
 


NA DENIS CHAMBI,TANGA

 WAKALA wa usajili wa  biashara na leseni  ‘BRELA’ imewataka wafanyabishara  wote wakubwa,  wakati na wadogo waliopo katika maeneo mbalimbali hapa  nchini  kufuata sheria na taratibu zilizopo ikiwa ni pamoja na kurasimisha  biashara zao ili kuweza kuchangia pato la Taifa  ambapo pia itawasaidia kupata mikopo kutoka katika taasisi za kifedha.

Rai hiyo ometolewa na afisa leseni kutoka BRELA Jubilate Muro wakati akizungumza na wanahabari katika maonyesho ya 10 ya biashara na viweanda yanayofanyika mkoani Tanga ambapo amesma kuwa wapo wafanyabishara wengi wanaofanya biashara wakiwa hawajarasimisha jambo ambalo ni kinyume cha sheria zilizopo ili kujenga uaminifu kwa wateja na wafanyabishara wengine

"Tunawaomba sana wafanyabishara wote nchini wasajili biashara zao kwasababu kuna faida kubwa kwa kufanya hivyo kuliko kutokusajili a lakini pia kuna huduma zingine mfanyabishara ,mmiliki wa kiwanda au kampuni atashindwa kuzipata kwa kukwepa kusajili biashara yake kupitia BRELA"

 “Lakini hii pia itamsaidia kujenga uaminifu kwa wateja wake na wafanyabishara wengine na hata kwenye  taasisi za kifedha ataweza kuhudumiwa kama atahitaji mkopo akiwa na leseni ya kibiahara vinginevyo anaweza kukosa huduma muhimu ambazo zinaweza kumleta maendeleo” 
alisema Muro.

Maonyesho ya biashara na utalii  ambayo hufanyika kila mwaka jijini Tanga yakihusisha makampuni na taasisi za kiserikali na zisizo za kiserikali mwaka huu  yakiwa ni ya 10 yamebebwa na kauli mbiu ya ‘Kilimo , viwanda utalii na madini ndio msingi wa maendeleo ya kiuchumi’

Kwa upande wake  afisa usajili kutoka BRELA  Julieth Kihwelu alisema kuwa mifumo hiyo ni mikuu pendwa ambayo mwombaji anatakiwa kutumia kuwasilisha ombi lake huku akieleza wanatoa huduma ya kuwafundisha namna ya kutumia mfumo huo kuweza kujisajili.

“Katika mifumo hii mwombaji anatakiwa awe na kitambulisho na Taifa,barua pepe aweze kujisaijili na nitoe wito kwa wajasiriamali nchini kuendelea kusajili alama za biashara zao kwa kuwa alama moja inamtumbisla mtu mmoja”Alisema

Hata hivyo aliwashauri wakazi wa Tanga na mikoa ya jirani waenda kupata huduma ya papo kwa papo ambapo kwa sasa wanaendelea kutoa huduma hiyo katika maeneo hayo.

“Tokea 28 mei mpaka Mei 31 tumekwisha kuwahudumia wananchi 35 na tukilinganisha mwaka jana na mwaka huu kuna utofauti na tunategemea kufikia watu wengi kwa kuwatembele kwenye mabanda hususani wajasiriamali kuweza kuwapa ushauri namna ya kuweza kusajili alama za biashara “Alisema Afisa huyo.
Afisa leseni kutoka wakala wa usajili wa  biashara na leseni  ‘BRELA’ Jubilae Muro akizungumza na waandishi wa habari kwenye maonyesho  ya 10 ya biashara na utalii yanayoendelea katika viwanja vya mwahako mkoani Tanga.
Wafanyakazi kutoka wakala wa usajili wa  biashara na leseni  ‘BRELA’ wakitoa huduma na elimu kwa wananchi waliotembelea banda lao kwenye maonyesho ya 10 ya biashara na utalii  yanayoendelea katika viwanja vya mwahako Mkoani Tanga.
 


 


MBUNGE wa Singida Mashariki Miraji Mtaturu,amechangia mjadala wa bajeti ya Wizara ya Nishati na kutoa ombi kwenye maeneo matatu ikiwemo kwa serikali kuja na mpango mahsusi wa kuendeleza mradi wa umeme wa upepo Mkoani Singida ambao utekelezaji wake umekwama.

Akichangia Mei 31,Bungeni Jijini Dodoma,Mtaturu amesema mradi huo ukifanya kazi utawezesha kuongeza umeme katika Gridi ya Taifa.

Amesema juzi amemuona Waziri wa Nishati Januari Makamba akisaini mkataba wa umeme wa jua pale Kishapu Mkoani Shinyanga jambo ambalo ni zuri na la kupongezwa.

“Mh Waziri hili ni jambo zuri sana,lakini tumekuwa na kilio cha muda mrefu cha umeme wa upepo,na umeme huu tumezungumzia Makambako,tumezungumzia Singida,hivi ninavyoongea kuna watu wameonyesha nia ya kuwekeza kwenye mradi huu lakini mpaka sasa bado hatujaona dalili yoyote ya kuanza umeme huu ,umeme huu ni wa uhakika,hautaangalia mabadiliko ya tabia nchi,

“Nikuombe sana unapokuja utuambie mipango mahsusi ya wizara ili kuunasua mradi huu,kumekuwa na siasa nyingi naomba hizo siasa tuziondoe tuhakikishe mradi ule wa Singida uanze mapema ili tuweze kuingiza umeme kwenye gridi ya Taifa wakati tunasubiri vyanzo vingine,”amesema.



SUALA LA WATUMISHI WA TANESCO.

Mtaturu amesema ili Shirika la Umeme Nchini(TANESCO),liweze kufanya kazi vizuri ni lazima kuwe na mitambo,mashine,teknolojia,fedha za kuwekeza na kuwa na rasilimali watu wenye furaha.

“Ukishakuwa na rasilimali watu wenye furaha,motisha na wenye kupewa msaada muda wote utafanya kiwanda ambacho ni TANESCO kifanye kazi vizuri ,kama ambavyo nimemsikia Mh Mkundi amesema asubuhi hapa kwamba kumekuwa na manung’uniko kidogo upande wa wafanyakazi wa Shirika hili,kumekuwa na dalili huwenda Shirika likapunguza wafanyakazi,

“Sasa Mh Waziri leo hii unao wateja Milioni 4 nchi nzima lakini unao wafanyakazi 9900,wastani wa mfanyakazi mmoja anahudumia wateja 424,maana yake ni kwamba kuna mfanyakazi mmoja anahudumia wateja wengi sana hivyo huwezi kutegemea tija pale,sasa unapotaka kwenda kupunguza wafanyakazi maana yake unaenda kupunguza uwezo wa kuwahudumia wateja,”amefafanua.

Amesema hivi sasa wanaendelea kutekeleza miradi ya umeme vitongojini maana yake kwamba wanaenda kuongeza idadi ya wateja,sasa unapofikiria kupunguza wafanyakazi usitegemee kuwa na huduma zenye tija.

“Tumeendelea kupata taarifa kwamba mnapita kwenye Mikoa kuwaambia wafanyakazi kuwa kuna mpango wa kuwapunguza,mfano Mkoa wa Ilala wa kitanesco una wafanyakazi 288 sasa unasema utabakiza wafanyakazi 86 watahudumia vipi,Mkoa wa Dodoma kadhalika una wafanyakazi 162 unategemea wabaki 86 watahudumiaje wateja wa mkoa huo,

“Hapa maana yake ni kwamba unaenda kuanguka,unaenda kufeli ,nikuombe sana Mh Waziri najua hili huna taarifa nalo ila kumekuwa na fukuto la ndani kwa ndani linaendelea kwenye menejimenti,lifanyie kazi waite vyama vya wafanyakazi mzungumze hili muwafanye wafanyakazi hawa waendelee kufanya kazi ambayo tunaitegemea,”amesisitiza.

Mkuu wa Mkoa wa Singida, Peter Serukamba (kushoto) akimnyoshea kidole Mhandisi wa Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni, Gabriel Mayaya (kulia) wakati akimsisitizia kukamilisha ujenzi wa miradi haraka iwezekanavyo kabla ya Julai 1, 2023 wakati wa ziara yake ya kuhimiza ukamilishaji wa miradi hiyo aliyoifanya leo Juni 1, 2023 wilayani humo. 

Na Dotto Mwaibale, Manyoni 

MKUU wa Mkoa wa Singida, Peter Serukamba amemtaka Mhandisi na Afisa Manunuzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni kuhakikisha wanakamilisha ujenzi wa wodi ya wanaume na wanawake pamoja na chumba cha kuhifadhia maiti (Mochwari) katika Hospitali ya Wilaya hiyo kabla ya fedha zilizotolewa kwa ajili ya kazi hiyo kurudishwa Hazina.

Serukamba ametoa agizo hilo leo (Juni 1, 2023) katika mfululizo wa ziara yake ya kukagua miradi ya maendeleo katika Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni kabla ya kumalizika  kwa mwaka wa fedha wa 2022/ 2023 ambapo zimebaki siku 19 kuisha.

Maofisa waliokali kuti kavu ni Mhandisi wa Halmashauri ya Wilaya  hiyo, Gabriel Mayaya ambaye alielezwa kuwa kama fedha za kutekeleza miradi ya maendeleo zilizoletwa kwenye wilaya hiyo zitarudishwa Hazina kutokana na kutokamilika kwa miradi hiyo kabla ya Juni 30, mwaka huu awe na uhakika kuwa atakuwa hana kazi.

"Mhandisi hakikisha unakamilisha ujenzi wa miradi yote kwa wakati na kama fedha zilizotolewa na Serikali kwa ajili ya miradi ya maendeleo zitarudishwa Hazina bila ya kukamilisha kazi hii utakosa kazi," alisema Serukamba kwa ukali.

Kwa upande wa  Afisa Manunuzi, Joseph Nswila alielezwa kuwa iwapo kesho (Ijumaa) atashindwa kupeleka mabati ya kuezekea chumba cha kuhifadhia maiti atamuweka ndani.

Serukamba alikerwa na kasi ndogo ya ukamilishaji wa miradi ya maendeleo inayotekelezwa katika wilaya hiyo kutokana na uzembe unaofanywa na viongozi kwa kushidwa kusimamia na badala yake wamewachia viongozi wa vijiji,kata na kamati za ujenzi jukumu la kusimamia.

 Mkuu wa Mkoa alisema serikali imeleta fedha nyingi kwenye halmashauri kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maendeleo hivyo ni lazima wakuu wa idara wagawane kuisimamia ili iweze kukamilika kabla ya Juni 30, mwaka huu.

Alisema itakuwa jambo la ajabu kama fedha hizo ambazo zimeletwa katika mkoa huu zitarudishwa Hazina kutokana na kutokamilika miradi na kwamba hali hiyo ikitokea maana yake viongozi watakuwa wamefeli na kushindwa kumsaidia Rais Samia Suluhu Hassani ambaye amehangaika kuzitafuta fedha hizo.

Miongoni mwa maafisa waliopata fursa ya kutembelea na kukagua miradi hiyo ni wataalam, watendaji wa kata, tarafa, wajumbe wa kamati ya ulinzi na usalama wa wilaya hiyo na viongozi wa Shujaa wa Maendeleo na Ustawi wa Jamii Tanzania (SMAUJATA) wilayani humo ambao ni Wales Shechambo, Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Mwembeni, Salutary Naaly na Hossen Kheri.

Miradi aliyoitembelea na kuikagua ni ujenzi wa wodi ya wanaume, wanawake na chumba cha kuhifadhi maiti katika Hospitali ya Wilaya ya Manyoni, kutembelea stendi ya mabasi na eneo itakapojengwa stendi mpya, ujenzi wa madarasa Shule ya Msingi Tambukareli,  ujenzi wa Zahanati ya Kijiji cha Mbwasa, Ujenzi wa Bweni la Wasichana Shule ya Sekondari ya Sasajila mradi ambao umefadhiliwa na Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) na ujenzi wa bweni la wasichana katika Shule ya Sekondari ya Kintinku na ujenzi wa madarasa katika Shule ya Msingi Chikuyu.

Kesho ziara hiyo itaendelea wilayani humo kwa kukagua miradi mbalimbali na kuwahimiza wahusika kuikamilisha kwa wakati. 

Mkuu wa Mkoa wa Singida, Peter Serukamba akikagua ujenzi wa wodi ya wanaume na wanawake katika Hospitali ya Wilaya ya Manyoni.
Diwani wa Kata ya Manyoni, akichangia jambo wakati wa ukaguzi wa eneo itakapo jengwa stendi mpya ya mabasi wilayani humo.
Mkuu wa Mkoa wa Singida, Peter Serukamba, akikagua ujenzi wa vyumba vya madarasa katika Shule ya Msingi ya Tambukareli.
Baadhi ya viongozi wa Shujaa wa Maendeleo na Ustawi wa Jamii Tanzania (SMAUJATA) Wilaya ya Manyoni ambao walishiriki katika ziara hiyo wakati wa ukaguzi wa ujenzi wa wodi ya wanawake na wanaume katika Hospitali ya wilaya hiyo wakiwa katika picha ya pamoja.
Muonekano wa stendi ya mabasi ya sasa ya wilaya hiyo, ambayo inatakiwa kuhamishiwa katika eneo jipya kupisha malori kuhamia eneo hilo kwa ajili ya kuanzisha chanzo kipya cha mapato wilayani humo ambapo malori hayo yametakiwa kuegeshwa hapo kuanzia kesho Juni 2, 2023 huku Mkuu wa Mkoa wa Singida, Peter Serukamba akitoa wiki tatu kwa mabasi yote ya abiria  kuhamia stendi mpya baada ya kujengwa kwa miundombinu ya choo na maji katika eneo hilo.
Muonekano wa madara yanayo jengwa Shule ya Msingi Tambukareli.
Muonekano wa eneo itakapo jengwa stendi mpya.
Mkuu wa Mkoa wa Singida, Peter Serukamba, akizungumza wakati alipokuwa akikagua eneo itakapo jengwa stendi mpya.
Muonekano wa Zahanati ya Kijiji cha Mbwasa ambayo ujenzi wake umekamilika kwa asilimia 95.
Muonekano wa madarasa yanayo jengwa Shule ya Msingi, Chikuyu.
Mkuu wa Mkoa wa Singida, Peter Serukamba, akizungumza wakati akikagua ujenzi wa bweni la wasichana katika Shule ya Sekondari ya Sasajila.
Muonekano wa bweni la wasichana linalojengwa katika Shule ya Sekondari ya Sasajila.
Muonekano wa bweni la wasichana linalojengwa Shule ya Sekondari ya Kintinku.
 

 


Na Farida Mangube Morogoro.

 Serikali imeahidi kuendelea kutatua changamoto zinazowakabli vijana kote nchi ili waweze kuendelea kushiriki shughuli za kiuchumi kwa lengo la kukuza pato lao na pato la Taifa.

 Hayo yameelezwa na Mkuu wa wilaya ya Mvomero, Mhe. Judith Nguli kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa huo Mhe. Adam Malima, wakati alipokuwa akizungumza kwenye kilele cha Maadhimisho ya Kumbukizi ya 18 ya Waziri Mkuu wa zamani Hayati Edward Moringe Sokoine, iliyofanyika katika  viunga vya Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo, mjini Morogoro.

Mhe. Nguli amesema kuwa serikali ya awamu ya sita imekuwa ikipambana na changamoto zinazowakabili vijana na kuwekeza nguvu kubwa katika maeneo ambayo vijana watafaidika kiuchumi. 

“ Kwa sasa kuna Mpango wa Mageuzi ya Kilimo (BBT), ambapo serikali imejipanga kisawasawa kuhakikisha kuwa vijana wanashiriki katika kilimo chenye tija kwa lengo la kuwawezesha kujiajiri katika sekta hiyo muhimu.” Alisema Nguli. 

Ameongeza kusema kuwa kwa mujibu wa sensa ya watu na makazi ya mwaka 2022 takwimu zinaonesha kuwa kundi kubwa la Watanzania ni vijana  hivyo serikali imeweka mikakati kuhakikisha kuwa vijana wanashiriki shughuli za uchumi kwa kuwawezesha kujiajiri katika sekta mbali mbali. 

“Ninawapongeza Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo kwa kuja na kauli mbiu nzuri ya maadhimisho ya mwaka huu inayosema kuwa "Mazingira Wezeshi kwa Vijana Kushiriki Katika kilimo Tanzania: Sera, Miongozo na na Utendaji" ni kauli mbiu muafaka kwani ndicho serikali inachokifanya kwa sasa kuwezesha kundi la vijana kuzalisha mazao ya kilimo na mnyororo wa thamani, sambamba na shughuli nyingine za uzalishaji”.Alisema

 Nguli akiwataka vijana kote nchini kuacha kubweteka kwa kuendekeza starehe na kujikita katika kufanya kazi ili waweze kuepukana na  utegemezi.

 Awali akizungumza katika maadhimisho hayo ya kumbukizi ya 18 ya Hayati Sokoine, Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo, Jaji Joseph Sinde Warioba, Alisema SUA itaendelea kuwa kitovu cha kuwajenga vijana Katika Kilimo.

 


Mkuu wa Wilaya  ya Arumeru  Mhe.Emmanuela Kaganda aelekeza miradi ya uboreshaji miundombinu katika shule za Msingi   kukamilika kwa Wakati na kwa ubora uliokusudiwa.

Mhe.Kaganda  amesema  hayo  wakati  wa  ziara ya kukagua utekelezaji wa  Miradi  ya  BOOST  katika Halmashauri ya  Wilaya  ya  Meru ambapo  Serikali imetoa milioni  961.5  za  uboreshaji  miundombinu ya elimu kwenye Shule  za Msingi.

Aidha, Mhe. Kaganda  amesema Serikali  ya  Dkt.Samia  Suluhu  Hassan  imejipanga vyema kuendelea kuwaletea  wananchi wake maendeleo ambapo imetoa  fedha nyingi za maendeleo katika sekta ya elimu,afya, maji nk

Mhe.Kaganda  amewataka   wataalum wa Halmashauri hiyo kuhakikisha wanasimamia vyema utekelezaji wa miradi hiyo  kukamilika kwa wakati na kuwa na ubora uliokusudiwa kwani anmza ya Serikali ni kuwawezesha Watoto wa kitanzania kupata Elimu bora katika mazingira rafiki.

Naibu Waziri wa Maji Mhandisi Maryprisca Mahundi (Mb) amemuagiza Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dodoma (DUWASA) Mhandisi Aron Joseph kuhakikisha anafikisha huduma ya majisafi, salama na yenye kutosheleza kwenye zahanati ya Ntyuka iliyoko kata ya Ntyuka Jijini Dodoma. 

Agizo hilo amelitoa wakati akizindua mradi wa maji wa Ntyuka-Chimalaa kwa niaba ya Waziri wa Maji Mheshimiwa Jumaa Aweso (Mb). Mradi huo umetekelezwa kwa gharama ya shilingi  Milioni 471.8

Amesema dhamira ya serikali ni kuhakikisha inamtua mama ndoo ya maji kichwani huku ikifikisha huduma ya majisafi na salama katika maeneo yote ya huduma za kijamii. Kwa maana hiyo Mkurugenzi ahakikishe Zahanati hiyo iliyoko katika eneo la mradi inafikishiwa huduma ya maji haraka iwekanavyo.

 Amewahakikishia wananchi wa jiji la Dodoma na Tanzania kwa ujumla kuwa serikali itaendelea na jitihada zake za kuhakikisha huduma za kijamii zinafikiwa na huduma ya majisafi na salama.

Aidha, amewapongeza Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa mazingira Dodoma kwa kusimamia vizuri hadi kukamilika kwa mradi huo.

Awali akitoa taarifa ya mradi Mhandisi Joseph amesema mradi huo unatekelezwa kwa awamu mbili ambapo awamu ya kwanza imekamilika na inahudumia wakazi wapatao 1,931 katika maeneo ya Ntyuka mtaa wa Chimalaa. 

Awamu ya pili inatarajiwa kutekelezwa katika mwaka wa fedha 2023/24 na itanufaisha wakazi wapatao 2,510 wa mtaa wa Nyerere na hivyo kufanya jumla ya wanufaika wa mradi huo kufikia 4,441.





Na Mapuli Misalaba, Shinyanga

Taasisi ya Flaviana Matata Foundation leo imekabidhi mradi wa vyoo viwili vyenye matundu 24 katika Shule ya sekeondari Mazinge iliyopo Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga vyenye thaman ya shilingi milioni 58 kama hatua ya kuunga mkono juhudi za serikali.

Akizungumza Meneja miradi wa taasisi ya Flaviana Matata Foundation Lineth Masala amesema mradi huo umelenga kuondoa changamoto ya upungufu wa matundu ya vyoo katika shule hiyo.

Amesema mradi huo umeanza kutekelezwa Mwezi Machi Mwaka huu 2023 ambapo umekamilika Mwezi Julai 2023 na kwamba taasisi ya Flaviana Matata Foundation inatekeleza miradi kupitia ufadhili wa Diamonds do good.

Akizungumza katika hafla ya kukabidhi vyoo hivyo mkurugenzi wa taasisi ya Flaviana Matata Foundation amesisitiza walimu na wanafunzi wa shule hiyo kutunza miundombinu ya mradi huo ili uweze kudumu na kuendelea kuwanufaisha.

Flaviana Matata ameisihi jamii kuacha mila potovu ambapo amewaomba wazazi kutimiza wajibu wao katika malezi bora kwa watoto huku akiwasisitiza wanafunzi kusoma kwa bidii ili waweze kutimiza ndoto zao.

“Tunamshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan tunaamini hivi tunavyovifanya kwa kushirikiana na serikali vitaenda kutatua changamoto zilizopo wazazi mpo walimu na wanafunzi niwaombe tuvunje mila potovu tuwaache watoto wa kike wasome tuache mimba na ndoa za utotoni hivi vyoo tumejenga kwa lengo la kutatua changamoto zilizokuwepo”

“Sisi tumejikita kuhakikisha tunatatua changamoto zinazomkabili mtoto wa kike ili aweze kupata elimu na kujikwamua kiuchumi na sisi tutaendelea kushirikiana na ninyi siku zote lakini niwaombe mvitunze ili vije kutumiwe na wadogo zenu wanaofuata na viongozi mtusaidia kutunza miundombinu lakini pia tutafurahi kuona matokea ufaulu unaongezeka”. Amesema Flaviana Matata

Kwa upande wake mgani rasmi kwenye hafla hiyo, Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Mhe. Johari Samizi ameipongeza taasisi ya Flaviana Matata Foundation kwa kutatua changamoto ya vyoo katika shule ya sekondari Mazinge ambapo amesisitiza wanafunzi kuongeza juhudi katika masomo ili kuwatia moyo wadau wa maendeleo wanaowekeza mazingira bora na salama.

“Niipongeze sana taasisi ya Flaviana Matata Foundation kwa kukabidhi mradi huu leo lakini  Mradi huu ambao umeletwa na taasisi ya Flaviana Matata Foundation wanafunzi wa shule ya sekondari Mazinge ni wanufaika wa moja kwa moja tunaamini mazingira haya yatasaidia kuongeza ufaulu darasani hasa kwa watoto wa kike ambao kipindi cha nyumba mlikuwa mnashindwa kufika shuleni, niwaombe wanafunzi wote mtumie vyoo hivi kama ilivyokusudiwa ili uweze kuishi miaka mingi tusiharibu miundombinu”.amesema DC Samizi

Mkurugenzi wa Manispaa ya Shinyanga Dkt. Jomaary Satura naye ameipongeza taasisi ya Flaviana Matata Foundation kwa kuendelea kuisaidia serikali kutatua changamoto zilizopo ambapo amesema   serikali Manispaa hiyo itaendelea kushirikiana na wadau wa maendeleo kwa kuruhusu uwekezaji hasa katika sekta ya elimu.

Naye Mkuu wa Shule ya sekondari Mazinge  Mwalimu James Msimba amesema vyoo hivyo vitakuwa ni chachu ya kuongeza ufaulu kwa wanafunzi na kwamba ameishukuru taasisi ya Flaviana Matata Foundation huku akiomba kuendelea kushirikiana katika kutatua changamoto zingine zilizopo.

“Uongozi na jumuiya ya shule ya sekondari Mazinge tunaishukuru serikali yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya uongozi shupavu wa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuweka mazingira salama kwa taasisi mbalimbali zisizo za kiserikali”

“Tunaishukuru taasisi ya Flaviana Matata Foundation kwa msaada wao wa kutujengea matundu 24 ya vyoo pia kwa msaada wa taulo za kike ambazo walitoa kwa wanafunzi wa kike 135 katika shule yetu Mungu awabariki sana kwa moyo wenu wa majitoleo na upendo”.amesema Mwalimu James mkuu wa shule

Baadhi ya wanafunzi wa shule ya sekondari Mazinge wamesema vyoo hivyo vitawasaidia kuondokana na changamoto zilizokuwa zinawakabili hasa kwa wanafunzi wa kike.

Taasisi ya Flaviana Matata Foundation leo Juni mosi,2023 imekabidhi vyoo viwili vyenye matundu 24 ambavyo vina thaman ya shilingi milioni 58 kama hatua ya kuunga mkono juhudi za serikali katika Shule ya sekeondari Mazinge iliyopo Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga

Mkurugenzi wa taasisi ya Flaviana Matata Foundation, Flaviana Mtata akizungumza kwenye hafla ya kukabidhi vyoo ya kisasa katika shule ya sekondari Mazinge Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga leo Juni mosi 2023.

Mkurugenzi wa taasisi ya Flaviana Matata Foundation, Flaviana Mtata akizungumza kwenye hafla ya kukabidhi vyoo ya kisasa katika shule ya sekondari Mazinge Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga leo Juni mosi 2023.

Mkurugenzi wa taasisi ya Flaviana Matata Foundation, Flaviana Mtata akizungumza kwenye hafla ya kukabidhi vyoo ya kisasa katika shule ya sekondari Mazinge Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga leo Juni mosi 2023.

Mgeni rasmi, mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Mhe. Johari Samizi akizungumza kwenye hafla iliyoratibiwa na taasisi ya Flaviana Matata Foundation kwa ajili ya kukabidhi mradi wa matundu ya vyoo leo Juni mosi 2023 katika shule ya sekondari Mazinge Manispaa ya Shinyanga.

Mgeni rasmi, mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Mhe. Johari Samizi akizungumza kwenye hafla iliyoratibiwa na taasisi ya Flaviana Matata Foundation kwa ajili ya kukabidhi mradi wa matundu ya vyoo yenye thamani ya shilingi milioni 58 katika shule ya sekondari Mazinge Manispaa ya Shinyanga.

Mkurugenzi wa taasisi ya Flaviana Matata Foundation, Flaviana Mtata upande wa kushoto na Mgeni rasmi, mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Mhe. Johari Samizi wakiteta jambo kwenye hafla ya kukabidhi vyoo vya kisasa shule ya sekondari Mazinge Manispaa ya Shinyanga.

Mkurugenzi wa Manispaa ya Shinyanga Dkt. Jomaary Satura akizungumza kwenye hafla iliyoratibiwa na taasisi ya Flaviana Matata Foundation kwa ajili ya kukabidhi mradi wa matundu ya vyoo yenye thamani ya shilingi milioni 58 leo katika shule ya sekondari Mazinge.

Meneja miradi wa taasisi ya Flaviana Matata Foundation Lineth Masala akizungumza kwenye hafla ya kukabidhi mradi wa matundu ya vyoo leo Juni mosi 2023 katika shule ya sekondari Mazinge Manispaa ya Shinyanga.

Mkuu wa Shule ya sekondari Mazinge  Mwalimu James Msimba akisoma taarifa ya shule kwa mgeni rasmi katika hafla ya kupokea mradi wa matundu ya vyoo 24 yenye thamani ya shilingi milioni 58.