Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akiongea na Waandishi wa Habari kuhusu Miradi ya Maendeleo na Fursa za Vijana kwa Mwaka 2025/26, Jijini Dodoma.



Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) imeendelea kuongoza katika utoaji wa huduma za matibabu ya moyo katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kusini mwa Jangwa la Sahara, kwa kufanya zaidi ya upasuaji 3,000 wa tundu dogo kila mwaka.

Mkurugenzi Mtendaji wa taasisi hiyo, Dkt. Peter Kisenge, amesema mafanikio hayo yametokana na uwekezaji mkubwa wa Serikali katika sekta ya afya, pamoja na kuimarika kwa rasilimali watu, vifaa tiba na miundombinu ya kisasa.

Akizungumza na waandishi wa habari Aprili 9, 2026 jijini Dodoma, amesema Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) iliyoanzishwa mwaka 2015 kwa ajili ya huduma za kibingwa bobezi, tafiti na mafunzo, imefanikiwa kupunguza utegemezi wa wagonjwa kwenda nje ya nchi kwa matibabu ya moyo.

Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO), magonjwa ya moyo yanaongoza kwa kusababisha vifo duniani, yakigharimu maisha ya watu milioni 17.9 kila mwaka, huku asilimia 75 ya vifo hivyo vikitokea katika nchi zenye kipato cha chini na cha kati.

Dkt. Kisenge amesema Tanzania ni miongoni mwa nchi chache barani Afrika zilizoanzisha hospitali maalum za moyo kutokana na uwekezaji mkubwa unaohitajika.

Ameongeza kuwa JKCI hufanya zaidi ya upasuaji 3,000 wa tundu dogo kila mwaka pamoja na zaidi ya upasuaji mkubwa 800 wa kufungua kifua. Pia hutoa huduma za upasuaji tata kama TAVI, pamoja na upasuaji maalum kwa watoto ikiwemo Ozaki na Truncus.

Mafanikio hayo yameifanya Tanzania kuwa kitovu cha utalii wa matibabu, huku wagonjwa kutoka ndani na nje ya Afrika wakija kupata huduma katika taasisi hiyo.

Katika kusogeza huduma karibu na wananchi, JKCI imeanzisha matawi sita katika maeneo ya Tazara (Temeke), Kawe, Oysterbay, Kariakoo, Chato na Arusha. Hali hii imeongeza idadi ya wagonjwa kutoka wastani wa 400 kwa siku mwaka 2022 hadi zaidi ya 1,100 mwaka 2025.

Aidha, taasisi hiyo imepanua huduma za upasuaji kwa watoto kupitia ufadhili wa Serikali na wadau, ambapo mamia ya watoto wamefanyiwa upasuaji bila malipo.

Kwa upande wa teknolojia, JKCI inatumia mifumo ya kisasa ikiwemo DOZEE kwa ufuatiliaji wa wagonjwa pamoja na mfumo wa miadi kwa njia ya mtandao uliopunguza msongamano na muda wa kusubiri huduma.

Taasisi hiyo pia imeanza maandalizi ya kuanzisha huduma za upandikizaji wa moyo, zikitarajiwa kuanza ifikapo mwaka 2030.

Zaidi, Serikali imewekeza katika maabara ya kisasa inayotumia teknolojia ya akili mnemba na roboti, hatua iliyopunguza muda wa majibu ya vipimo kutoka saa tatu hadi saa moja.

JKCI pia imeingia makubaliano ya ushirikiano na nchi mbalimbali za Afrika katika kuboresha huduma na kujenga uwezo wa wataalamu wa afya. Aidha, imeanzisha mkutano wa kimataifa wa magonjwa ya moyo (CardioTan) unaowakutanisha wataalamu kutoka zaidi ya nchi 40 duniani.

Kupitia huduma za tiba mkoba, taasisi hiyo imewafikia wananchi zaidi ya 35,000 katika mikoa mbalimbali nchini.

Katika mwaka 2025 pekee, JKCI ilitoa huduma kwa wagonjwa 252,915 huku wagonjwa 2,710 wakifanyiwa upasuaji, wakiwemo 836 waliopata upasuaji mkubwa wa moyo.

Mbunge wa Jimbo la Kisarawe, Dkt. Selemani Jafo,akichangia makadirio ya mapato na matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zake kwa mwaka wa fedha 2026/27  leo Aprili 9,2026 bungeni jijini Dodoma.

Na.Alex Sonna-DODOMA

Mbunge wa Kisarawe, Dkt. Selemani Jafo, amedhamiria kuwasilisha hoja binafsi bungeni itakayolenga kuishauri Serikali kuanzisha mpango maalum wa mikataba ya ajira za muda mfupi kwa vijana ili kupunguza changamoto ya ukosefu wa ajira nchini.

Akichangia makadirio ya mapato na matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zake kwa mwaka wa fedha 2026/27 bungeni, Jafo alisema mpango huo unaweza kuwa na mfumo wa Ajira za muda (part time employment) utakaodumu kwa kipindi cha miaka mitatu mitatu hadi ifikapo mwaka 2050  ambapo vijana watapata ajira za mikataba na kujipatia uzoefu wa kazi.

Alimpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, kwa juhudi kubwa za kuongeza fursa za ajira kwa vijana tangu aingie madarakani, akisema serikali imefanya kazi kubwa katika kuwawezesha wananchi, lakini bado kuna haja ya kuja na mikakati mipya ya kukabiliana na wimbi la vijana wasio na ajira.

Jafo alibainisha kuwa changamoto ya ajira bado ni kubwa, huku akitoa mfano wa vijana wengi waliopo kwenye shughuli zisizo rasmi kama bodaboda, baadhi yao wakiwa na elimu ya juu ikiwemo stashahada,  shahada na kuendelea. Alipendekeza mpango maalum utakaolenga wahitimu hao ili kuwapa nafasi ya kupata ajira za muda na mikataba ya miaka mitatu.

Kwa mujibu wa mapendekezo yake, kila mwaka vijana 50,000 wanaweza kuingizwa kwenye mpango huo, ambapo asilimia 20 wawe wahitimu wa stashahada na asilimia 80 wawe wahitimu wa shahada na kuendelea. Aidha, alipendekeza malipo ya kujikimu ya Shilingi 500,000 kwa wenye stashahada na Shilingi 700,000 kwa wahitimu wa shahada.

Alisema gharama ya utekelezaji wa mpango huo inakadiriwa kufikia Shilingi bilioni 396, huku akisisitiza kuwa mpango huo utasaidia kukuza ujuzi wa vijana, kuongeza uzoefu wa kazi na kupunguza tatizo la ajira nchini.

Pia alipendekeza asilimia 10 zitoke katika mapato ya ndani ya kila Halmashauri, 10 ya gawio la Serikali kutoka kwenye mashirika ya umma, na fedha zingine zitokane na kubana maeneo mengine ya matumizi ya kawaida ya serikali(Recurrent Expenditure) ili zitumike kufadhili mpango huo. Aidha, alishauri mpango huo usimamie kupitia serikali za mitaa na Taasisi za Umma ili kurahisisha upatikanaji wa ajira katika halmashauri mbalimbali na Taasisi hizo za Umma.

Jafo alisisitiza kuwa mpango huo, kama utapitishwa, utaisaidia Serikali kuongeza wigo wa ajira na kuwawezesha vijana wengi zaidi kunufaika na fursa za kiuchumi nchini.

 



Na  OWM-SBUU -Morogoro


Serikali imezindua Kikosi Kazi cha Taifa cha Ufuatiliaji, Tathmini na Utoaji Taarifa (ME&R National Task Force) kwa lengo kuratibu utekelezaji wa Mwongozo Jumuishi wa Ufuatiliaji na Tathmini katika kusimamia utendaji wa shughuli za Serikali.

Kauli hiyo imetolewa leo tarehe 09 Aprili, 2026 na Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Dkt. James Kilabuko  wakati akifungua Kikao Kazi Cha Kikosi Kazi cha Taifa cha Ufuatiliaji, Tathmini na Utoaji Taarifa (ME&R National Task Force) kilichofanyika mkoani Morogoro.

Dkt. Kilabuko amesema, Ufuatiliaji na Tathmini ni dhana muhimu ya usimamizi inayotumika kwa lengo la kuhakikisha uwajibikaji na uwazi katika utekelezaji wa afua za maendeleo.

“Kikosi Kazi hiki kitakuwa chombo cha kitaalamu cha kusaidia kuratibu utekelezaji wa Mwongozo Jumuishi wa U&Tc, kuoanisha mifumo ya kitaifa ya utendaji, kuimarisha ubora wa takwimu na taarifa za Serikali na  kuandaa mapendekezo ya sera na maboresho ya kiutendaji” alisema Naibu Katibu Mkuu huyo.

 


Na Oscar Assenga, TANGA

Chama cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Tanga kimetoa maelekezo kwa Halmashauri ya Jiji la Tanga kuhakikisha maeneo ya kukusanyia taka katika soko la Mgandini yanaboreshwa kwa kujazwa kifusi ikiwemo kurekebisha barabara za ndani ili kuimarisha usafi.

Agizo hilo lilitolewa na Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Tanga Rajab Abdurhaman wakati wa ziara yake ambapo alisisitiza umuhimu wa kuhakikisha maji ya mvua yanaelekezwa ipasavyo kwenye mifereji ili kuepusha mafuriko na uharibifu wa miundombinu.

Ziara hiyo ilikuwa ni kufuatilia utekelezaji wa maagizo aliyoyatoa awali kuhusu kuboresha usafi wa soko hilo ambapo viongozi wa Jiji hilo walianza kuyafanyia kazi ikiwemo kuondosha uchafuzi uliokuwepo awali.

Awali, wakati wa ziara yake ya kukagua hali ya usafi, Mwenyekiti huyo hakuridhishwa na mazingira ya soko hilo na kutoa muda wa mwezi mmoja kwa uongozi wa Jiji kuhakikisha hali ya usafi inaboreshwa.

Akizungumza baada ya kufanya ziara ya ufuatiliaji, Rajab aliwapongeza Mstahiki Meya pamoja na viongozi wa Jiji kwa kuchukua hatua na kuanza kutekeleza maelekezo hayo ya CCM.

“Hatuhitaji viongozi wa kulalamika, tunahitaji viongozi wanaochukua hatua kutatua changamoto za wananchi. Mlichokifanya ni kutimiza wajibu wenu,” alisema.

Alisema kuwa hali ya uchafu iliyokuwepo awali haikuwafurahisha viongozi wala wafanyabiashara, hivyo hatua zilizochukuliwa zinaonesha uwajibikaji wa uongozi.

Hata hivyo Mwenyekiti Rajab alisisitiza kuwa atarejea kukagua maendeleo hayo baada ya wiki mbili na kuonya kuwa hataki kusikia visingizio badala ya utekelezaji.

“Ndani ya mwezi mmoja kuanzia Aprili 9 hadi Mei 9, tunatarajia kuona kazi imeanza. Hatutaki hadithi, tunataka vitendo,” alisisitiza.

Aidha, alieleza kuwa Jiji la Tanga ni taswira ya mkoa huo, hivyo linapaswa kuwa safi na lenye mpangilio mzuri.

Alikumbusha kuwa zamani Tanga ilikuwa mji unaojulikana kwa usafi na ustaarabu, hivyo ipo haja ya kurejesha hali hiyo.

Kuhusu huduma za vyoo katika soko hilo, Mwenyekiti alieleza kutoridhishwa na hali iliyopo, akibainisha kuwa choo kilichopo hakitoshelezi mahitaji kutokana na idadi kubwa ya watumiaji.

Alisema kuwa hali hiyo inasababisha baadhi ya watu kulazimika kujisaidia katika maeneo yasiyofaa, jambo linalohatarisha afya za wananchi na wafanyabiashara.

Alisisitiza umuhimu wa Jiji kutafuta suluhisho la kudumu, ikiwemo kuboresha mfumo wa maji taka ili kuendana na ongezeko la watumiaji.

Hata hivyo, aliwapongeza viongozi kwa kuanza mpango wa kujenga choo kipya chenye matundu 12 kitakachosaidia kupunguza changamoto hiyo, hasa katika kipindi hiki ambacho soko linatarajiwa kujengwa upya.

Pia alizungumzia changamoto ya msongamano wa magari yanayoleta bidhaa sokoni hapo, akielekeza kuwepo kwa utaratibu maalum wa magari kuingia na kushusha mizigo kwa mpangilio ili kupunguza msongamano na kuboresha usafi.


Alipendekeza magari yapaki katika maeneo maalum yaliyo nje ya soko, kisha yaingie kwa zamu kushusha bidhaa.

Katika hatua nyengine alisisitiza umuhimu wa kujenga mifereji ya maji ili kuzuia maji ya mvua kutuama au kuingia sokoni, hali inayochangia uchafu na uharibifu wa mazingira.


Alimalizia kwa kuwataka viongozi wa Jiji kuwa karibu na wananchi na kushughulikia changamoto zao kwa vitendo, akibainisha kuwa wananchi hao ndio chanzo cha mapato ya Jiji kupitia kodi.

Kwa upande wake, Naibu Meya Khalid Rashid alisema kuwa Jiji lina mpango wa kuboresha miundombinu ya ndani ya soko, ikiwemo njia za kupita ili kuondoa changamoto ya matope wakati wa mvua. Alibainisha kuwa kazi hiyo inatarajiwa kuanza ndani ya wiki moja.

Mwisho.

Na Munir Shemweta, WANMM NAIROBI

 

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeelezea mafanikio yake katika maendeleo ya miji na sekta ya makazi wakati wa Kongamano la Pili la Miji Africa (2nd African Urban Forum) linalofanyika jijini Nairobi, huku ikitoa wito kwa wawekezaji wa ndani na kimataifa kuchangamkia fursa zilizopo nchini humo.

 

Hayo yameelezwa jijini Nairobi na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo wakati akitoa tamko la Tanzania likielezea jitihada za Serikali katika kuchochea maendeleo endelevu ya miji na makazi, ikiwa ni pamoja na sera, mipango na mikakati inayotekelezwa kuboresha makazi na upangaji wa miji.

 

Amesema, Tanzania imepiga hatua kubwa katika utekelezaji wa Ajenda 2063 ya Umoja wa Africa, hasa katika maeneo ya miundombinu, upatikanaji wa nishati, utoaji wa huduma za kijamii na kuimarisha ushirikiano wa kikanda.

 

‘’Juhudi hizo zinaendana na mkakati wa Bara la Africa wa kuimarisha muunganiko, biashara na maendeleo jumuishi’’. amesema

 

Aidha, Mhe. Dkt Akwilapo alielezea pia mikakati ya serikali ya Tanzania katika kukabiliana na changamoto za ukuaji wa kasi wa miji pamoja na upungufu wa makazi, ambapo kwa sasa makazi yasiyo rasmi yanakadiriwa kufikia asilimia 67.3.

 

Amesema, katika kukabiliana na hali hiyo, serikali ya Tanzania inaendelea kutekeleza mageuzi ya sera, kuanzisha mifumo bunifu ya fedha, kuboresha umiliki wa ardhi pamoja na kuhamasisha uwekezaji katika makazi nafuu kupitia ushirikiano kati ya sekta ya umma na binafsi.

 

Aidha, amesema katika kuboresha upatikanaji mikopo ya nyumba, serikali imeanzisha Taasisi ya Tanzania Mortgage Refinance (TMRC) inayosaidia kupunguza gharama za mikopo, kuongeza muda wa marejesho na kutoa fursa kwa wananchi wengi zaidi kupata huduma za kifedha kupitia mikopo midogo midogo.

 

Waziri huyo wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi amesisitiza kuwa, serikali ya Tanzania itaendelea kutumia rasilimali zake za asili pamoja na kudumisha amani na usalama ili kuharakisha utekelezaji wa Ajenda 2063.

 

Vilevile, Dkt Akwilapo alitoa wito kwa washirika wa maendeleo na sekta binafsi kushirikiana na serikali katika kuwekeza kwenye sekta ya makazi aliyoieleza kuwa inao mchango mkubwa katika kukuza uchumi na kuboresha maisha ya wananchi.

 

Kupitia Kongamano hilo, Dkt Akwilapo alieleza salamu za dhati kutoka kwa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliyempongeza Mhe. William Ruto pamoja na wananchi wa Jamhuri ya Kenya kwa kuandaa Kongamano hilo muhimu.

 

Kongamano la Pili la Miji Africa limezinduliwa rasmi April 9, 2026 na Rais wa Kenya Mhe. William Ruto na linaongozwa na kauli mbiu isemayo “Adequate Housing for All: Advancing Socio-Economic and Environmental Transformation Towards the Realization of Agenda 2063,” ikilenga kuhamasisha mijadala inayotoa fursa kwa washiriki kutoka nchi mbalimbali za Africa kubadilishana uzoefu na suluhisho bunifu katika kukabiliana na changamoto za maendeleo ya miji na makazi.







 Kamishna wa Uhifadhi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro Bw. Abdul-Razaq Badru leo tarehe 9 Aprili, 2026 amepuliza rasmi Kipenga cha shindano la mwezi mmoja la Safari Field Challenge akisisitiza kwamba Ngorongoro ni nyumbani kwa kila binadamu kutokana na chimbuko la historia linalobainishwa kisayansi.


Akizindua shindano hilo Kamishna Badru amewashukuru washiriki nane (8) wa shindano hilo kwa kuitika wito wa Ngorongoro na kuwaeleza kuwa Hifadhi ya Ngorongoro ni zaidi ya Kreta hasa kutokana na kuwa na utamaduni, asili, chimbuko la binadamu wa kale, siri ya Binadamu na maisha yake, Nyayo za Laetoli zenye umri za zaidi ya miaka milioni 3.6, mchanga unaohama, kushuhudia pumzi ya kwanza ya Nyumbu eneo la Ndutu, kuona Wanyama wakubwa watano katika eneo moja, mlima Lolmalasian ambao wa tatu kwa urefu Tanzania, misitu, mimea na ndege mbalimbali.

“Karibuni Ngorongoro ambapo ni nyumbani kwa sisi sote, mtapata uzoefu ya maajabu mbalimbali, kuyahisi, kuyaishi, kufurahia, kuyahadithia na kuwasaidia kupata ujuzi ambao utawafanya muwe mabalozi wazuri kuwaelezea watu wengine mkusanyiko wa maajabu yaliyoko Ngorongoro” Alisema Kamishna Badu.

Kamishna Badru amewapa changamoto washiriki wa shindano hilo kuwa watundu wa kuifahamu Ngorongoro, kuisemea Ngorongoro kwa mtazamo mpya wa sauti moja ambapo kwa kushirikiana na Azam Media hadithi, historia, maajabu ya Ngorongoro itasimuliwa na kufika pembe nne za dunia kuwa Ngorongoro sio kivutio cha utalii pakee bali ni Nyumbani kwa kila Binadamu ambapo historia yao ilianza.

Kamishna Msaidizi Mwandamizi anayesimamia Huduma za Utalii na masoko Mariam Chuma Kobelo amewaeleza washiriki wa Safari Field Challenge kuwa Tanzania ina vitu vingi vya Kujivunia,lakini Ngorongoro kuna vingi zaidi na kuwasisitiza washiriki wa shindano hilo kwenda kujifunza, kuifahamu na kuisimulia Ngorongoro kuwa ni zaidi ya Kasoko ya Ngorongoro.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Tanzania Tour Guide Fondation (TTGF) Mosses Njole ameleza kuwa washiriki wote 8 wako timamu na wamejiandaa kikamilifu kushiriki shindano hilo na kuwapongeza Ngorongoro kwa kuwa wadhamini wakuu na wadau wengine wakiwepo Azam Media ambayo imekuwa sehemu ya kusimulia maajabu ya Ngorongoro.










Wananchi wa wilaya ya Same mkoani Kilimanjaro wamewaomba viongozi kuhakikisha tamasha la utalii la Same Utalii Festival linafanyika kila mwaka kutokana na mchango wake mkubwa katika kukuza uchumi wa jamii.

Wito huo umetolewa leo na kina mama lishe wakati wa joggin ya kuhamasisha tamasha hilo linalotarajiwa kufanyika Aprili 10 hadi 12 mwaka huu, likiwa ni msimu wa tatu tangu kuanzishwa kwake.

Akizungumza katika joggin hiyo, Anna Mzava, ambaye ni mama lishe katika stendi ya mabasi wilayani Same, alisema tamasha hilo limekuwa msaada mkubwa kwao kiuchumi.

Alisema mbali na kuhamasisha utalii, tamasha hilo limeongeza kipato kwa wafanyabiashara wadogo kutokana na ongezeko la watu wanaohudhuria.

“Tunaomba tamasha hili liwe endelevu kwani sisi wananchi wa chini tunafaidika nalo. Biashara zetu zinaenda vizuri na tunapata fedha zaidi. Kwa mfano, badala ya kupika mchele kilo tatu, wakati wa tamasha napika hadi kilo 10 na zote zinaisha,” alisema Mzava.

Kwa upande wake, Jumanne Idd alisema tamasha hilo limekuwa chachu ya kutangaza utalii wa wilaya ya Same pamoja na vyakula vya asili vya kabila la Wapare.

Aliongeza kuwa tukio hilo limechangia kuitangaza wilaya hiyo kitaifa na kuchochea ukuaji wa shughuli za kiuchumi wakati wa msimu wa tamasha.

Akizungumza katika joggin hiyo, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Same, Yusto Mapande, alisema wamejipanga kuhakikisha tamasha hilo linakuwa endelevu ili kuendelea kutangaza vivutio vya utalii vilivyopo wilayani humo.

Alisema halmashauri itaendelea kubuni na kuibua vivutio vipya ili kuongeza fursa za kiuchumi kwa wananchi.

“Faida kubwa tunazotarajia ni za kiuchumi.Panapokusanyika watu wengi ni fursa, kwani wanahitaji huduma mbalimbali na hivyo kuongeza kipato kwa wananchi,” alisema Mapande.