




Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Adolph Mkenda amesema Baraza la Mitihani la Tanzania (NECTA) limejiondoa jukumu la kusema shule ipi bora lakini takwimu za shule ipi bora zipo na kila mtu anaweza kuzipata.
Profesa Mkenda alkuwa akijibu muongozo wa Mbunge wa Bunda Vijijini Mwita Getere aliyetaka ufafanuzi kuhusu minong’ono iliopo mitaani kuhusiana na NECTA kushindwa kutaja viwango vya ufaulu kwa shule na wanafunzi waliofanya vizuri katika mitihani yao ya kidato cha nne iliyofanyika mwaka 2022.
Getere aliomba mwongozo kwa Mwenyekiti wa Bunge kwa kutumia kanuni ya 76 ya bunge na kutaka ufafanuzi kuhusu hatua hiyo ya Baraza la Mitihani la Tanzania kubadali utaratibu wake wa kutangaza matokeo kwa shule na wanafunzi bora.
Akijibu muongozo huo, Waziri Mkenda amesema kwa sasa watakua wakitumia mfumo wa kuangalia namna shule inavyoweza kuongeza elimu ya wanafunzi kutoka kiwango kimoja kwenda kiwango kingine na sio matokeo ya mwisho.
Profesa Mkenda amesema, pamoja na kuangalia viwango vya ufaulu lakini wataangalia pia mazingira ya kujifunzia ya mwanafunzi na shule ili kuona namna ambavyo hatua zimepigwa kuhakikisha mwanafunzi anafaulu licha ya mazingira ya kujifunzia kuwa magumu.
MASWALI NA MAJIBU MUHIMU
Zipi ni hatua za kufuatwa ili kuhakiki laini zangu za simu zilizosajiliwa kwa namba ya Kitambulisho cha Uraia?
JIBU: Ili kuhakiki namba zako zilizosajiliwa kwa namba ya Kitambulisho cha Uraia, fanya kama ifuatavyo: -
KWENYE SIMU YAKO:
Bofya *106#(kisha bonyeza kitufe cha kupiga simu kwa mtandao husika;
Menyu itajitokeza kwenye skrini ya kifaa chako cha mawasiliano ikiwa na vipengele vitano (5);
KUMBUKA: Menyu hii inafanana kwa mitandao yote;
Ikiwa una namba moja pekee kwa Mtandao husika, unashauriwa kuhakiki kama namba yako ya Kitambulisho cha Uraia ilitumika kusajili namba hiyo pekee, au namba nyingine usizozitambua;
Kutekeleza zoezi hili chagua kipengele cha Tatu (3) kwenye menyu inayoonekana kwenye skrini ya kifaa chako. Iwapo utabaini uwepo wa namba za simu usizozitambua fika kwenye duka la Mtoa Huduma wako, ili uzifute.
“Hakikisha unacho kitambulisho chako cha Uraia au NAMBA TAMBULISHI (NIN) ili kukamilisha zoezi hili”
Ikiwa unamiliki namba zaidi ya moja za Mtandao mmoja zilizosajiliwa kwa namba za kitambulisho chako cha Uraia, unapaswa kuzihakiki;
Kutekeleza zoezi hili, chagua kipengele cha Tano (5) kwenye menyu iliyotokeza kwenye skrini ya kifaa chako. Kisha, bofya kipengele namba (1) ili kuchagua Namba Kuu. halafu, rudia kwa kubofya kipengele namba (2) kuhakiki namba za ziada.
Ipi ni tarehe ya ukomo ya zoezi la Uhakiki wa Laini za Simu?
JIBU:
Awali Serikali kupitia Mamlaka ya Mawasiliano (TCRA) iliweka tarehe-ukomo ya zoezi hili kuwa Januari 31 mwaka huu. Kwa kuona Umuhimu wa kuhakikisha kila Mwananchi anaetumia huduma za Mawasiliano hakosi huduma hizo Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari kupitia Waziri mwenye dhamana, Mheshimiwa Nape Moses Nnauye (Mb.) alitangaza wakati wa Mkutano wake na Waandishi wa Habari Dodoma mnamo tarehe 24 Januari 2023 kuongeza muda wa zoezi hili kutoka tarehe ya awali Januari 31 hadi Februari 13, 2023 saa 10:00 jioni.
Mara baada ya tarehe ukomo kupita laini za simu ambazo hazitakuwa zimehakikiwa kwa kufuata utaratibu uliobainishwa zitazuiliwa KUTOA na KUPOKEA huduma/zitafungwa.
Zipi ni faida na hasara za kutohakiki laini zangu za simu?
JIBU: Faida za kuhakiki laini zako zilizosajiliwa kwa Kitambulisho cha Uraia ni nyingi, kama ifuatavyo: -
Uhakiki unakuhakikishia Usalama wako wewe kama mtumiaji wa huduma za Mawasiliano ya simu;
Ni utekelezaji wa matakwa ya Sheria ya Mawasiliano ya Kielektroniki na Posta (EPOCA) na Kanuni zake zinazoelekeza kwamba laini zote zisajiliwe kwa utaratibu bayana;
Zoezi hili litawezesha kuondoa kwenye ikolojia ya Mawasiliano simu-laghai zinazosababisha matukio ya uhalifu miongoni mwa watumiaji wengine wa huduma za Mawasiliano ya simu;
Uhakiki unakupa utambulisho thabiti (Digital identity). Unakuwezesha wewe Mwananchi kuwa mshiriki Madhubuti katika Ujenzi wa uchumi wa Taifa lako (Uchumi wa Kidijitali).
Kuboresha Huduma. Taarifa za watumiaji zilizokamilika zinaiwezesha Serikali kupitia TCRA kuhakikisha upatikanaji wa huduma bora za Mawasiliano.
Hasara za kutohakiki ni kama ifuatavyo:-
Utakosa huduma. Laini yako itafungwa.
Kuunganishwa kwenye jinai.
Vipi ikiwa nilimsajilia mtu mwingine Laini ya Simu?
JIBU:
Ikiwa ulimsajilia mtu mwingine laini ya simu, mtake akasajili laini yake kwa utambulisho wake mwenyewe, kwa kufuata utaratibu uliobainishwa; ikiwa ni pamoja na kupata namba ya kitambulisho cha uraia kutoka NIDA.
Wewe uliemsajilia unalazimika/ unapaswa kuwasiliana na mtoa Huduma ili afute usajili wa namba ya huyo uliemsajilia na kuhamisha usajili kwa kutumia utaratibu uliowekwa.
Izingatiwe kwamba: Kila mtumiaji wa Mawasiliano ya simu nchini, aliekidhi vigezo vya kuwa na kitambulisho wa uraia anapaswa kwa mujibu wa kanuni za usajili wa laini za simu, kusajili na kuhakiki laini zake kwa utambulisho wake husika.
Mnasema zoezi hili litapunguza Uhalifu, kivipi?
JIBU:
Ni sahihi kwamba zoezi hili litapunguza matukio ya utapeli mtandaoni kwa kuwa, itakuwa rahisi sasa kumtambua kila mtumiaji wa huduma za Mawasiliano ya simu. Utambulisho halisi wa kila mtumiaji sasa utakuwa umetunzwa vema katika Kanzidata.
Kwa sasa baadhi ya watumiaji wa huduma za Mawasiliano ya simu wenye nia ya kutenda uovu kwenye Mtandao wamekuwa wakijificha kwenye kichaka cha usajili wa watu wengine kwa kutenda makosa ya kimtandao kwa kuwa usajili wa laini za simu wanazotumia si wa kwao;
Hivyo, tukihakiki wote na kuondoa namba tusizozitambua na kuhakikisha wale tuliowasajilia wao pia wanasajili laini zao wao wenyewe tutafanikiwa kupunguza matukio ya utapeli mtandaoni kwani kila mtumiaji atatambuliwa kwa laini yake ya simu anayotumia.
Ilikuwaje watu wakawa na laini za simu zisizokuwa na utambulisho wao?
Baadhi ya mawakala wa watoa huduma hawakuwa waaminifu, walikuwa wakiwasajilisha wenye vitambulisho zaidi mara moja na kutengeneza laini za simu za ziada, tofauti na ile ya muhusika kisha kuziuza laini hizo, ambazo wenye nia mbaya wamekuwa wakizitumia kutenda makosa ya kimtandao;
Mawakala hawa wasio waaminifu TCRA tuliwadhibiti kwa kushirikiana na Watoa Huduma, na tukatoa maelekezo kwa Watoa Huduma kuhakikisha mawakala wao wanazingatia sheria na taratibu zilizopo wanaposajili laini za watumiaji wapya au wale wanaohitaji kuongeza laini za simu;
Nikufahamishe kwamba tumeendelea kuzifutia huduma laini hizi za simu zinazotenda makosa mtandaoni ambapo hadi Novemba mwaka jana 2022 tulifungia laini zaidi ya 52,000 zikiwemo zilizokuwa zikijihusisha na utapeli.
Baada ya tarehe ya mwisho kupita 13/02/2023 ndiyo itakuwa basi tena?
JIBU: Zoezi hili ni endelevu. Hata hivyo kwa wale wenye laini zinazotumika sasa, ikiwa hawatakuwa wametekeleza takwa la uhakiki tutaziondolea huduma itakapofika tarehe ya ukomo, ili kuhakikisha kila mtumiaji wa huduma za Mawasiliano, anatambuliwa na kumbukumbu yake inatunzwa kwenye Kanzidata, hii itawezesha Serikali yetu kuwa na takwimu sahihi na kamili za watumiaji halisi wa huduma za Mawasiliano ya simu, intaneti na huduma za kifedha mtandaoni.
Ikiwa nitabaini uwepo wa namba za simu nisizozitambua baada ya kutekeleza zoezi la Uhakiki, nifanyeje?
JIBU: Fika kwenye duka la Mtoa Huduma wako, kisha toa Taarifa ya namba hizo ili ziweze kufutwa kwa kuzingatia utaratibu wa bayometria na kuwasilisha namba za Kitambulisho chako cha uraia.
Je, mnafikiria kuongeza Muda zaidi?
Tayari muda umeongezwa kutoka tarehe-ukomo ya wali ambayo ilikuwa Januari 31, 2023 na sasa zoezi la uhakiki wa laini za simu zinazotumika limeongezewa muda hadi Februari 13, 2023.
Zoezi hili la kuhamasisha uhakiki wa laini za simu zinazotumika lilianza Desemba 2021.
Mnataka kufunga hilo zoezi mbona wananchi hatujapata Taarifa za kutosha?
Kampeni hii ya Elimu tunaiendesha kwa ushirikiano na watoa huduma wote wa huduma za Mawasiliano ya simu. Kwa upande wao wamekuwa wakitumia mitandao ya kijamii, pia wamekuwa wakituma ujumbe wa moja kwa moja kwa watumiaji wote wa Mawasiliano ya simu wakiwakumbusha kila mtumiaji wa huduma za Mawasiliano ya simu kuhakiki laini zao za simu. Hivyo, TCRA tunaamini kila mtumiaji wa Mawasiliano ya simu amepokea Taarifa hizi za uhakiki kupitia ujumbe mfupi uliotumwa na watoa huduma, au kupitia kurasa za mitandao ya kijamii ya TCRA, watoa huduma na Wizara ya sekta.
Zoezi linaendaje hadi sasa?
Zoezi linaendelea kwa mafanikio makubwa. Hadi sasa zaidi ya asilimia 90 ya laini za simu zinazotumika nchini zimehakikiwa. Hivyo hima! mtumiaji wa huduma za Mawasiliano wewe ambae bado hujakamilisha uhakiki wa laini zao za simu, tekeleza zoezi hilo sasa kwa kubofya *106# kisha fuata maelekezo.
Muhimu kukumbuka ni kwamba itakapofika tarehe 13 Februari 2023 kama laini yako haijahakikiwa itazuiliwa kutoa na kupokea huduma. Hakiki sasa!
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akimsikiliza Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Ridhiwani Kikwete, Bungeni
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akizungumza na Mbunge wa Jimbo la Sumve, Kasalali Mageni , Bungeni jijini Dodoma.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Uratibu na Bunge, George Simbachawene akizungumza na Waziri wa Viwanda na Biashara Ashatu Kijaji , Bungeni jijini Dodoma. Februari 1 2023.
Katibu Mkuu ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Tamisemi Profesa Riziki Shemdoe ameziagiza Halmashauri zote nchini zianze kufanya miradi ya uwekezaji ili kuziwezesha Halmashauri hizo kuongeza mapato na kuondokana na utegemezi mkubwa wa bajeti ya serikali kuu ili kuendesha shuguli zake.
Profesa Shemdoe alitoa agizo hilo mkoani Morogoro wakati akifungua mafunzo ya siku kumi kwa maafisa mipango kutoka katika Halmashauri kumi na tatu (13) ili kuwajengea uwezo wa kuandika miradi mikubwa na inayokopesheka na ambayo pia itaweza kusaidia kuongeza uwezo wa Halmashauri husika kukusanya mapato ya kutosha kwa ajili ya maendeleo.
Aidha Profesa Shemdoe amesema uanzishwaji wa miradi hiyo mikubwa inalenga kuongeza wigo wa ajira kwa watanzania na hivyo kupunguza malalamiko dhidi ya Serikali juu ya ukosefu wa ajira kwa vijana licha ya kuwa Halmashauri zitakuwa zimeongeza pia ukusanyaji wa mapato pamoja sambamba na kutoa gawio kwa serikali kuu.
“Kwa sasa Halmashauri zinazokusanya zaidi ya bilioni 10 ni chache sana ukilinganisha na idadi ya halmashauri tulizonanzo nchini laakini kikubwa ni kwamba kama tutatengeneza miradi ambayo tunaweza hata kuipangisha kasha fedha zote zikalipwa kwenye halamashari itakuwa na manufaa makubwa sana”alisema Profesa Shemdoe.
Kwa upande wake Makamo Mkurugenzi Chuo cha Mipango Kanda ya Ziwa Profesa Jvenal Nkwazoki alisema kuwa ipo haja ya kupeleka mafunzo hao kwa watoa maamuzi ili kuweka uelewa wa pamoja katika kupanga na kuamua miradi yenye manufaa kwa halmashauri husika.
Naye muwezeshaji wa mafunzo hayo ambaye pia ni Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Songea Dokta Frederick Sagamiko alisema kuwa faida zaidi zitakazo patikana kwenye mfumo ni halmashau kuanzisha miradi ya uwekezaji ni kwamba miradi hiyo itasimamiwa na wataalamu na kuongeza ajira kwa maafisa masoko ambao hata hivyo kwa sasa hakuna halmashauri iliyoajiri afisa masoko.
Dokta Bonimass Mbasa mhadhiri mwandamizi chuo cha mipango ya maendeleo vijijini alisema kuwa mafunzo hayo yatapelekwa kwenye halmashauri zonte nchini na kwa maafisa mipango nchi nzima pamoja na wakurugenzi wote wa ahalamashauri ili kuwajengea uwezo wa namna bora ya uanzishaji wa kampuni ili waweze kukopa na kupata fedha za uendeshaji wa kampuni hizo.
Serikali imesema hadi kufika mwaka 2025 huduma ya maji safi na salama katika mkoa wa Manyara inatarajiwa kuwafikia wananchi kwa asilimia 85.
Hayo yamesema na mkuu wa mkoa wa Manyara Charles Makongoro Nyerere wakati akishuhudia utiaji saini wa mikataba ya miradi ya maji katika maeneo mbalimbali ya mkoa wa Manyara kati ya Wakala wa maji safi na usafi wa mazingira (RUWASA) na wazabuni waliopata tenda ya kutekeleza miradi hiyo ya maji uliofanyika katika ofisi za mkuu wa mkoa wa Manyara.
Makongoro amesema mpango wa kuhakikisha changamoto ya maji unatatuliwa Mkoa wa Manyara ni mpango wa serikali hadi kufikia mwaka 2025 hivyo amewaasa wazabuni pamoja na makampuni ya usambazaji waliosaini m ikataba ya kutekeleza miradi mbalimbali ya maji mkoani manyara kufanya bidii ili ikamilike kwa wakati.
Aidha kutokana na changamoto ya ununuzi wa mabomba ya miradi ya mwaka 2022 Makongoro amesema zoezi hilo litafanywa na RUWASA na kazi ya wakandarasi itakuwa ni kutekeleza ujenzi wa miradi hiyo ili kuepusha usumbufu na changamoto zisizokuwa za lazima.
Miradi inayotarajiwa kutekelezwa na wakandarasi waliosaini mikataba ni miradi 28 ambapo miradi 7 ni mipya, miradi 8 ya kuongeza mitandao, visima 26 na usanifu wa miradi 53 kwa ujumla utekelezaji wa miradi hiyo utagharimu kiasi cha shilingi bilioni 15 na milioni 406 ambazo tayari zimetolewa na serikali ya jamhuri ya muungano wa Tanzania.
Kulingana na mikataba miradi hiyo inatarajiwa kukamilika mwezi desemba mwaka 2023 na itapunguza changamoto ya maji kutoka vijiji 91 hadi kufikia vijiji 51 na kukamilisha jumla idadi ya vijiji 40 vitakavyonufaika na miradi ya maji kwa mwaka huu ndani ya mkoa wa Manyara.
Baadhi ya vijiji hivyo ni Madunga, Utwari, Enoth, Lusinyai, Kiperesa, Esuguta, Aicho, Titiwi, Naberera, Losokonoi, Lobeno, Orkesmet, Luremo, Komolo, Olembere, Mogitu Gehandu..
Akizungumza kwenye hafla ya kusaini mikataba ya miradi hiyo, Meneja wa RUWASA mkoa wa Manyara Mhandisi Walter Kirita amesema kwa sasa wanahudumia asilimia 80 ya wakazi wa mkoa wa manyara hasa waliopo vijijini na huduma ya maji imefikia asilimia 64.3 sawa na ongezeko la asilimia 3.3 kutoka asilimia 61 mwezi juni mwaka 2022.
Akizungumzia Takwimu za utoaji wa huduma ya maji Mkoa wa Manyara, Kirita amesema wilaya ya Hanang ni asilimia 64, Babati asilimia 76, Kiteto asilimia 60.9, Mbulu asilimia 65.2 na Simanjiro ni asilimia 51.6.
Akizungumza kwa niaba ya wakuu wa wilaya, mkuu wa wilaya ya Babati Lazaro Twange amesema watasimamia miradi hiyo ikamilike kama ilivyopangwa na kumpongeza Raisi Samia kwa kuendelea kutekeleza miradi mbalimbali inayogusa wananchi wote kama miradi ya maji pia amewasisitiza viongozi wengine wote watoe ushirikiano kwa wakandarasi ili kuwasaidia panapotokea changamoto.
Nao wakandarasi na wazabuni wamesema wapo tayari kufanya kazi kwa bidii kama mikataba inavyoeleza kuhakikisha miradi hiyo inakamilika kwa wakati ili wananchi waweze kupata huduma ya maji safi na salama.