MICHUANO ya Michezo ya Mei Mosi 2024 imefikia hatua ya nusu fainali katika michezo ya mpira wa miguu na netiboli ambapo kwa mwaka huu taasisi 54 zinashiriki mashindano hayo.

Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Michezo ya Mei Mosi Taifa Bi. Roselyne Massam wakati akiongea na waandishi wa Habari kuhusu michuano hiyo inayoendelea jijini Arusha ikiwa ni shamrashara za kuelekea maadhimisho ya sikukuu  ya Wafanyakazi Duniani

 “Tunategemea kilele cha michezo hii kufanyika Aprili 29, 2024 ambapo tutapata washindi wetu watakaopewa zawadi na Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani (Mei Mosi)" amesema Bi Massam.

Kwa upande wa mpira wa miguu, timu ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imeichapa Wizara ya Maliasili na Utalii magoli 2-0, huku timu ya Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) wamewafunga Wakala ya Barabara Tanzania (TANROADS) kwa magoli 4 -1, nayo Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) wamewaliza timu ya Wizara ya Maji kw bao 1 – 0 na timu ya  Wizara ya Mambo ya Ndani ya nchi imesonga mbele kwa kuwashinda Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa penalti 4–2. Timu hizo zilitoka suluhu katika dakika za kawaida.

Katika mchezo wa netiboli, timu ya Ofisi ya Rais Ikulu wameifunga  Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kwa jumla ya magoli 64 – 20, nayo Wizara ya Mambo ya Ndani ya nchi imewashinda TAMISEMI kwa magoli 46–22; huku  Wizara ya Ulizi na Jeshi la Kujenga Taifa wameichezesha kwata Wizara ya Uchukuzi kwa kuwafunga  magoli 63–18 na Wizara ya Afya wameifunga timu ya Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) kwa magoli 76 – 21.

Katika kuimarisha undugu na ushirikiano katika kutekeleza majukumu yao ya kila sekta binafsi, Bi Massam amewahimiza waajiri kuwaruhusu watumishi wao kufanya mazoezi wakati wote wanapokuwa kwenye vituo vyao vya kazi hatua itakayowafanya kuleta ushindani wakati wa mashindano ya Mei Mosi na mashindano ya mashirikisho ya SHIMIWI, BAMATA, SHIMISEMITA na SHIMMUTA.








 


Na Eleuteri Mangi, Arusha

Timu ya Viongozi wa vilabu vinavyoshiriki michuano ya Mei Mosi Taifa 2024 ambao ni mashabiki wa vilabu vya Simba na Yanga wametoa burudani kwa wakazi wa jiji la arusha katika mchezo wa mpira wa miguu na netiboli kuthibitisha umwamba wa vilabu vyao wanavyoshabikia hapa nchini.

Akizungumzia michezo hiyo iliyofanyika Aprili 26, 2024 katika Uwanja wa Sheikh Amri Abeid Arusha, Katibu wa Kamati ya Michezo ya Mei Mosi Taifa Bw. Alex Temba amesema kuwa wanamichezo hao ambao ni viongozi mashabiki wa timu ya Simba katika mpira wa miguu wameibuka kidedea kwa kuwafunga viongozi mashabiki wa Yanga kwa magoli 2 - 0 wakati kwa upande wa netibili viongozi wa timu ya Yanga wameibuka kidedea.

“Kwa kweli mechi ilikuwa nzuri imefurahisha, unaona mashabiki na wananchi wa jiji la Arusha walivyojitokeza kwa wingi, hizi timu zetu mbili zina mkusanyiko mkubwa sana wa watu. Tunawakaribisha wananchi wa Arusha waje kupata burudani ya michezo mbalimbali na kuwaona wanamichezo wa Rais Mama Samia wanavyojikinga na magonjwa na maradi yasiyoambukizwa kwa njia ya michezo” Bw. Temba. 

Kwa upande wake Mwenyekiti wa mashabiki wa Simba na Katibu wa Mawasiliano Sports Klab Bw. Aliko Mwaiteleke amesema wanaamini timu yao ya Simba bado ni imara na mengine ni ya kupita. 

“Sisi tumejiandaa kama Simba, ndiyo maana unaona tumejiandaa kama Simba na tumeshinda goli 2 – 0, watu wetu bado wana moyo sana na Simba sports Klab, angalia jezi zetu, ni lazima tuoneshe thamani ya timu yetu ndiyo maana tunasema Simba Nguvu Moja” Bw. Aliko.

Naye Mratibu wa mashabiki wa Yanga na Katibu wa Timu ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Bw. Kamna Shomary amesema viongozi wameamua na kupanga siku moja ya wao kucheza bonanza ambalo wamelitumia kama njia ya kufahamiana na kuimarisha udugu.

Kwa upande wa netiboli, viongozi mashabiki wa timu ya Sim ana Yanga na wakiongozwa na Jacqueline Sikozi shabiki wa timu ya Simba na Nyabuchwenza Metusela, Mwenyekiti wa timu ya Shirika la Viwango Tanzania (TBS) wamewasisitiza wachezaji na watumishi wa umma kuendelea kufanya mazoezi kwa kuwa michezo ni furaha, tiba, udugu n ani namna ya kuimarisha afya zao ili wanaporudi kazini wakafanye kazi kwa tija zaidi.


Na Mapuli Kitina Misalaba

Shirika la kuhudumia viwanda vidogo (SIDO) Mkoa wa Shinyanga leo Ijumaa Aprili 26,2024 limefunga mafunzo ya kutengeneza Vihenge ambapo jumla ya vijana 58 kutoka mikoa mbalimbali wakiwemo wa Shinyanga, Geita, Mwanza, Simiyu na Tabora wamenufaika na mafunzo hayo.

Mgeni rasmi katika hafla ya kufunga mafunzo hayo ni kaimu Meneja wa SIDO Mkoa wa shinyanga Bwana Joseph Taban ambaye amewapongeza vijana  kwa kuhitimu mafunzo huku akiwataka kuwa mabalozi wazuri katika jamii kwa kuhakikisha wanatumia ujuzi na maarifa waliyoyapata kuleta matokeo chanya katika jamii.

Mafunzo hayo yalianza Februari 26, 2024 kwa kundi la kwanza washiriki walikuwa 19, kundi la pili washiriki walikuwa 23 na kundi la tatu washiriki walikuwa 16 na kwamba yamefikia kilele leo Aprili26,2024 ikiwa jumla ya wahitimu 58 ambao wamehitimu na kuchukua vyeti vyao.

Bwana Taban amewasihi wahitimu hao kuendeleza umoja na ushirikiano katika kufanikisha ndoto zao kupitia ujuzi wa kutengeneza Vihenge ili kuinuka kiuchumi.

“Ni matumaini yangu kuwa mmepata dozi nzuri ya taaluma na mbinu mbalimbali za kutengeneza Vihenge, mmefundishwa masuala ya ujasiliamali, utengenezaji wa Vihenge kwa nadharia na vitendo, nadharia ya masoko, usimamizi wa fedha na urathimishaji wa biashara”.

“Ni matumaini yangu kuwa mafunzo mliyoyapata mtayatumia kwa vitendo kuhakikisha kuwa lengo la mafunzo haya linatimia, pia natarajia kuwa mafunzo haya yatawawezesha kuongeza kipato cha mtu mmoja mmoja, kaya na taifa kwa ujumla”.

“Mafunzo haya yametolewa kwa vijana wachache lakini wengi wangependa kupata mafunzo haya hivyo nitumie nafasi hii kuwaomba mkawe waalimu wa kufundisha vijana wenzenu kwenye maeneo yenu ya kazi ili kwa pamoja tuweze kupambana kwa vitendo kupunguza kama siyo kuondoa kabisa Sumukuvu”.

“Nitumie nafasi hii kuwapongeza kwa kuwa miongoni mwa vijana wachache waliopata bahati ya kupata mafunzo haya”.

Baadhi ya vijana ambao wamepata mafunzo hayo wamelishukuru na kulipongeza shirika la kuhudumia viwanda vidogo SIDO Mkoa wa Shinyanga kwa kutoa mafunzo hayo na kwamba wamesema yatawasaidia kwa kiasi kikuwa kuboresha utendaji wa kazi na kuzalisha bidhaa za Vihenge (Silos) na nyinginezo kwa tija ili kukidhi mahitaji ya soko la ndani na nje ya taifa la Tanzania.

Akisoma risala ambayo imeandaliwa na wahitimu wa mafunzo ya mradi wa kuthibiti Sumukuvu nchini kutoka kituo cha SIDO Mkoa wa Shinyanga Wanjala Daud amesema kwenye mafunzo hayo wamejifunza kwa nadharia na mada mbalimbali ikiwemo ujasiliamali, utengenezaji wa Vihenge kwa vitendo (Silos), nadharia ya masoko na huduma kwa wateja, usimamizi wa fedha pamoja na urasimishaji wa biashara.

“Tunapenda kushukuru uongozi wa SIDO na Wizara ya Kilimo kwa kutoa fursa ya mafunzo haya hakika yametujengea uwezo wa kujiamini na kuamsha ari ndani yetu ya kujiajiri na kuachana na kasumba ya kusubiri ajira”.

“Pamoja na ari na molari ya kujiajiri iliyojengeka ndani yetu tunakabiliwa na changamoto ya mitaji kwa ajili ya kununua vifaa au vitendea kazi vya kuanzisha shughuli mbalimbali kutoka na fani tulizojifunza hivyo tunaomba serikali ituangalie kwa jicho la kipekee ili tuweze kujikwamua na changamoto hii na hatimaye tuweze kujiajiri wenyewe hivyo kuchangia uchumi wetu na jamii huku tukitokomeza kabisa Sumukuvu kwa taifa letu hili la Tanzania”.

SIDO Mkoa wa Shinyanga imetekeleza mradi wa kuzuia Sumukuvu wa ‘Tanzania initiative for preventing aflatoxin contamination’ (TANIPAC) ambao upo chini ya Wizara ya Kilimo na kwamba mradi huo umelenga kuendelea kutoa elimu kwa wananchi ili kuimarisha usalama wa chakula na kuimarisha Afya ya jamii.

Mradi wa TANIPAC pia umelenga kuwezesha jamii kutumia njia sahihi na za kisasa za uhifadhi wa nafaka hususan Mahindi kutokana na Sumukuvu.

Serikali imeingia gharama kuhakikisha kuwa vijana wanapatiwa ujuzi wa kutengeneza vifaa vya kisasa na vinavyo dumu kwa muda mrefu (Vihenge) ili kutimiza adhima ya kupunguza Sumukuvu.

SIDO inawapatia wajasiliamali wadogo na wa kati huduma mbalimbali ikiwemo teknolojia na uendelezaji viwanda, mafunzo na usimamizi wa Mikoa, masoko na uwekezaji pamoja na huduma za fedha.

Kaimu Meneja wa SIDO Mkoa wa Shinyanga Bwana Joseph Taban akiwa katika zoezi la kukagua Vihenge vilivyotengenezwa na vijana ambao wamehitimu mafunzo ya kutengeneza Vihenge kupitia mradi wa kuthibiti Sumukuvu  wa ‘Tanzania initiative for preventing aflatoxin contamination’ (TANIPAC) ambao upo chini ya Wizara ya Kilimo.