Na OWM - TAMISEMI, Arusha

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya TAMISEMI, Mhe. Florent Kyombo ameipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mkoa na Serikali za Mitaa (OWM- TAMISEMI), kwa usimamizi mzuri wa utekelezaji wa miradi ya TACTIC katika Jiji la Arusha, miradi ambayo imeweka kiwango bora cha utekelezaji wa miradi ya aina hiyo ambayo inatekelezwa katika miji na majiji 45 nchini.

Mhe.  Kyombo ametoa pongezi hizo leo Machi 17, 2026 mara baada ya kamati yake kutembelea, kukagua na kuridhishwa na usimamizi wa utekelezaji wa miradi ya ujenzi wa Kituo Kikuu cha Mabasi yaendayo mikoani (Bondeni City Bus Terminal), ujenzi wa soko la Mrombo, ujenzi wa soko la Kilombero pamoja na ujenzi wa mradi wa uboreshaji wa bustani ya mapumziko Themi.

“Naungana na wajumbe wenzangu kutoa pongezi za dhati kwa utekelezaji mzuri wa miradi ya TACTIC katika jiji la Arusha, hakika utekelezaji wa miradi hii umeweka kiwango bora cha namna ya kutekeleza miradi ya aina hii nchini,” amesistiza Prof. Shemdoe.

Aidha, Mhe. Kyombo amempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuleta fedha za utekelezaji wa miradi pamoja na kumpa dhamana ya usimamizi wa miradi hiyo Prof. Shemdoe na watendaji wanaomsaidia, ambao wanaitendea haki dhamana waliyopewa na Mheshimiwa Rais.

Sanjari na hilo, Mhe. Kyombo amempongeza Mkandarasi wa Kampuni ya M/S MOHAMMEDI BUILDERS LIMITED kwa kiwango kizuri cha utekelezaji wa miradi yote minne ya TACTIC inayotekelezwa katika jiji la Arusha, ambayo itachochea ukuaji wa uchumi ndani ya jiji hilo.

Akizungumzia suala la ushirikishaji wa wadau katika miradi hiyo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu-TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amesema kuwa kabla ya kuanza kutekelezwa miradi hiyo,  timu ya kuandaa mazingira ya utekelezaji wa mradi hupita ikiwa na fomu maaluum ya kupokea maoni ya wadau kuhusiana na mradi husika, na kuongeza kuwa maoni ya wadau yalizingatiwa kwani hicho ni kigezo muhimu cha miradi yote inayotekelezwa na Benki ya Dunia.

Naye mmoja wa Wajumbe wa Kamati hiyo ya Bunge ya Kudumu ya TAMISEMI Mhe. Hawa Mwaifunga, amesema amefarijika kuona hatua nzuri iliyofikiwa ya Ujenzi wa Kituo Kikuu cha Mabasi yaendayo mikoani  na kuongeza kuwa kituo hicho kitakapokamilika kitakuwa na manufaa kwa wananchi wa Jiji la Arusha.

Kwa upande wake, Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya TAMISEMI Mhe. Jafari Chege ameupongeza uongozi wa mkoa na Jiji la Arusha kwa kutekeleza vizuri miradi ya TACTIC ambayo imelenga kuboresha utoaji wa huduma za kijamii na kukuza uchumi wa wananchi wa Jiji la Arusha.

Akizungumza kwa niaba ya wananchi, Diwani wa Kata ya Themi Mhe. Melance Kinabo, amemshukuru na kumpongeza Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kulijali Jiji la Arusha kwa kuliletea fedha za utekelezaji wa miradi minne ya TACTIC, ambayo ikikamilika itaongeza wigo wa wananchi kupata ajira zitakazowaingizia kipato.

 



Na Mwandishi Wetu, Tanga.


Wananchi wa Wilaya ya Mkinga mkoani Tanga wanatarajiwa kunufaika zaidi kiuchumi kupitia uwekezaji wa Serikali katika sekta ya kilimo cha mwani, hatua inayolenga kuongeza thamani ya mazao ya bahari na kuboresha maisha ya jamii za pwani.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa kaushio jipya na mashine mbili za kisasa za kusaga mwani uliofanyika tarehe 16 Machi 2026 katika Kijiji cha Kichaka Miba, Wilaya ya Mkinga, Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Mhe. Ummy H. Nderiananga, amesema mradi huo ni sehemu ya jitihada za Serikali kuimarisha uchumi wa wananchi wa maeneo ya pwani.

Mradi wa Kuimarisha Usalama wa Bahari unaratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Idara ya Menejimenti ya Maafa kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), na unatekelezwa na Chuo cha Mipango na Maendeleo Vijijini (IRDP) Tawi la Mwanza kwa ushirikiano na Halmashauri ya Wilaya ya Mkinga ambapo Lengo lake ni kuimarisha ufuatiliaji na ulinzi wa bahari pamoja na kuongeza thamani ya rasilimali za baharini kwa manufaa ya jamii.

Mhe. Nderiananga amesema kupitia mradi huo, Serikali imenunua boti mbili za doria, kujenga kaushio la kisasa la mwani, kusimika mashine za kusaga mwani na kutoa mafunzo kwa vikundi vya wakulima. Ameongeza kuwa hatua hizo zitaboresha ubora wa mwani, kupanua masoko, kuongeza kipato cha wakulima na kusaidia kuzuia vitendo vya kihalifu baharini.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Chuo cha Mipango na Maendeleo Vijijini (IRDP), Dkt. Guvenail Mkonoko, amesema kabla ya utekelezaji wa mradi huo wataalamu walifanya tathmini iliyobaini changamoto za mbinu duni za kilimo, ukaushaji usio salama na ukosefu wa miundombinu ya kisasa ya uchakataji. 





Naye mwakilishi wa wakulima wa mwani, Bi. Mwamvua Bwebwe, Ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwawezesha kuongeza uzalishaji, kupunguza upotevu wa mazao na kuboresha kipato chao.


Morogoro:

Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) leo imeongoza kampeni ya kupanda miti mkoani Morogoro ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Wiki ya Maji Duniani, inayofikia kilele chake kila mwaka tarehe 22 Machi, kwa lengo la kulinda vyanzo vya maji na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Akizungumza wakati zoezi hilo, Wilfred Mwakalosi, aliyemwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, alisema taasisi hiyo kwa kushirikiana na Ofisi ya Bonde la Maji la Wami Ruvu na Wakala wa Huduma za Misitu ( TFS) wamefanikiwa kupanda miti zaidi ya 5,000 katika eneo linalozunguka mto Lukulunge, Kata ya Mzumbe, mkoani Morogoro.

Mwakalosi alibainisha kuwa hatua hiyo ni sehemu ya mkakati wa muda mrefu wa kuhifadhi mazingira, vyanzo vya maji na kuhakikisha upatikanaji endelevu wa maji kqtika maeneo mbalimbali nchini. “Morogoro ni miongoni mwa maeneo yaliyokuwa na vyanzo vingi vya maji hapo awali, lakini kwa sasa hali imebadilika kwa kiasi kikubwa kutokana na uharibifu wa mazingira na mabadiliko ya tabianchi, hivyo kutishia upatikanaji wa maji kwa wakazi wake” alieleza.

Mhifadhi wa Wakala wa Huduma za Misitu (TFS) wa Wilaya ya Morogoro, Stanley Kweka, alisema uharibifu wa misitu umechangia kupungua kwa kina cha maji katika Bwawa la Mindu, huku mmomonyoko wa udongo ukiendelea kuwa tatizo kubwa hivyo upandaji wa miti ni suluhisho muhimu katika kulinda kingo za mito na kuhakikisha vyanzo vya maji vinabaki salama kwa matumizi ya sasa na baadaye.

Naye  Meneja wa Uratibu wa Mazingira na Jumuiya za Watumia Maji kutoka Bodi ya Bonde la ya Maji la Wami/Ruvu Janeth Kisoma,alisema mto Lukulunge ni chanzo muhimu kinachochangia maji katika Bwawa la Mindu, ambalo linahudumia zaidi ya asilimia 75 ya wakazi wa Manispaa ya Morogoro, hivyo uhifadhi wake unahitaji ushirikiano wa wadau mbalimbali.

 


Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge Tawala wa Mikoa na  Serikali wa Mitaa - TAMISEMI,  wameridhishwa na kupongeza utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa shule mpya ya sekondari ya wasichana Longido Samia Girl's, wilaya ya Longido Mkoa wa Arusha, mradi uliotekelezwa na Serikali kwa gharama ya shilingu Bilioni 4.4, kupitia programu ya SEQUIP.

Akizungumza mara baada ya kukagua mradi huo mapema leo machi 17,2026, Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Florent Kyombo (Mb), licha ya kuridhishwa na ubora wa mradi huo, ameipongeza Serikali ya awamu ya sita chini ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha nyingi za kuboresha miundonu ya elimu nchini huku Mkoa wa Arusha ukiwa ni miongoni mwa wanufaika. 

Ameweka wazi kuwa, lengo la serikali ni kuhakisha watoto wa kitanzania wanapata elimu kwenye mazingira rafiki na dhamira ya dhati Dkt.Samia ni kuwahamasisha watoto wa kike nchini kusoma masomo ya Sayansi ili kuzalisha watalamu wengi katika fani za Sayansi.

Hata hivyo wajumbe hao, wameshauri mkoa kuwa na msimamizi wa majengo 'Estate Manager' atakayekuwa na dhamani ya kusimami majengo yote ya serikali yaliyokamilika, ili kuhakikisha yanaendelea kutunzwa na kuendelea kuwa bora pamija na kushugulikia masuala ya ukarabati wa majengo hayo. 

Naye mkuu wa wilaya ya Longido Mhe.  Ally Kali, amewashukuru wajumbe wa kamati hiyo kwa niaba ya wananchi wake, kwa kuwatembelea na kukagua mradi huo wa shule, mradi ambao amekiri ni muhimu kwa watoto wa jamii ya Kimaasai, jamii ambao hapo awali wasichana wengi walikosa nafasi ya kupata elimu.

Mhe. Kali, amesisitiza kufanyia kazi maelekezo na ushauri ulmntolewa na wajumbe ikiwa ni pamoja na kupeleka maombi ya mahitaji ya shule hiyo kwenye Kamati ya Bajetii ili yaingizwe kwenye bajeti ya mwaka ujao wa fedha

Awali shule ya wasichana Longdo Samia Girl ni miongoni mwa shule 26 za kimkoa,ukiwa na lengo la kuongeza idadi ya shule na kuboresha mazingira ya ujifunzaji na ufundishaji nchini, iliyoanza kupokea wanafunzi mwaka 2024 ina wanafunzi 681 wa kidato cha 1-6 kwa mchepuo wa Sayansi.











 

Na Mwandishi wetu- Dodoma

 Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu imeendelea na hatua ya tatu ya kujengewa uwezo  wa namna ya kufanya tathmini za programu na miradi kupitia programu ya Kuendeleza  Sekta ya Kilimo Awamu ya Pili (ASDP II)  ili kuwawezesha watalaam wa ufuatiliaji na tathmini kupata uelewa na namna ya kutathmini miradi na programu mbalimbali zinazotekelezwa katika taasisi za umma.


Hayo yamesemwa leo tarehe 16 Machi 2026, jijini Dodoma na Mkurugenzi wa Ufuatiliaji na Tathmini ya Utendaji wa Serikali, Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Bi. Sakina Mwinyimkuu   wakati akifungua mafunzo yanayofanyika kwa siku nne Jijini Dodoma yakihusisha washiriki kutoka wizara zinazotekeleza  program ya ASDP II na washiriki kutoka nchini Zimbabwe na Malawi kwa lengo la kujifunza chini ya Twendembele Initiative ambapo Tanzania ni mshirika.



Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalumu, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi amewaomba Wakristo na Waislamu mkoani Mbeya kuendelea kutenda mema, kuishi kwa upendo, umoja na amani hata baada ya kumalizika kwa vipindi vya mfungo wa Kwaresma na Ramadhani. 

Ameyasema hayo  katika futari (Iftari)  iliyoandaliwa na Taasisi ya Maryprisca Women Foundation iliyowakutanisha viongozi wa serikali, Jeshi la Polisi, vyama vya siasa, taasisi za kidini pamoja na wananchi wa Kata ya Iwambi na kata jirani, Mahundi amesema waumini wanapaswa kuyaishi mafundisho ya vitabu vitakatifu hata baada ya kumaliza ibada za mfungo na kuendelea kuiombea nchi. 

“Ni wajibu wetu kuyaishi yale yote tunayofundishwa katika vitabu vitakatifu vya dini zetu. Tusiache kuiombea nchi yetu ya Tanzania ili iendelee kuwa na amani na upendo kwa sababu hiyo ndiyo lugha yetu na utamaduni wetu kama taifa,ni wasihi tuendelee kuiamini serikali na kuendelea kudumisha mshikamano maana hii ni tunu yetu watanzania wote ” amesema Mahundi.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Kyela, Josephine Manase, alimpongeza Mhe. Mahundi kwa moyo wake wa upendo kwa jamii na kuwataka viongozi wa dini kuendelea kuwajali watoto yatima pamoja na watu wasiojiweza katika jamii maana hiyo ndio ibada kuu katika maisha ya mwanadamu.

“Katika ibada mnazozifanya msisahau kuwahudumia watoto yatima na wale wasiojiweza kwa sababu kuwahudumia wao ni sehemu ya ibada kubwa na kumbukumbu isiyofutika mbele za Mwenyezi Mungu lakini pia tuendelee kumuombea Rais wetu ili aweze kuendelea kufanya kazi ya kutuletea maendeleo” amesema Manase.

Salamu za Serikali ya Wilaya ya Mbeya zilizowasilishwa na Afisa Tawala wa Wilaya hiyo kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya, Devotha Chacha, zimemhakikishia Mhe. Mahundi ushirikiano wa kutosha katika shughuli zake za kijamii. ambapo Serikali ya Wilaya ya Mbeya itaendelea kushirikiana  kwa karibu na taasisi hiyo kwani kazi wanazozifanya  ni huduma kwa jamii na ni wito kutoka kwa Mwenyezi Mungu"amesema Devotha

Kwa upande wao viongozi mbalimbali wa dini waliohudhuria iftari hiyo wamempongeza Mhe. Mahundi kwa kuendelea kudumisha utaratibu wa kuwakutanisha wananchi wa dini tofauti katika futari hiyo wakisema hatua hiyo inaimarisha upendo, mshikamano na amani katika jamii. 

"Utaratibu huu wa kuwakutanisha watu wa dini mbalimbali ni jambo jema linaloendelea kuimarisha upendo na umoja katika jamii, na tunaona mabadiliko kila mwaka kwa kuwa wananchi wanaendelea kuungana zaidi,” wamesema viongozi hao wa dini.

 

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba leo Machi 15, 2026 ameweka jiwe la msingi la Shule ya Sekondari Mgombe yenye mkondo wa Amali ya Kihandisi iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Mlele, mkoani Katavi, ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kikazi ya kukagua na kufuatilia utekelezaji wa miradi ya maendeleo mkoani humo.

Ujenzi wa shule hiyo unatekelezwa kupitia Mradi wa Kuimarisha Ubora wa Elimu ya Sekondari (SEQUIP) kwa gharama ya shilingi bilioni 1.694 na hadi sasa umefikia asilimia 99 ya utekelezaji.

Shule hiyo itatoa mafunzo ya amali katika fani mbalimbali zikiwemo ufundi magari, ufundi bomba, mifumo ya umeme wa jua pamoja na ufundi umeme wa magari. Mafunzo hayo yanalenga kuwajengea wanafunzi ujuzi wa vitendo utakaowawezesha kujiajiri, kuajiriwa au kuendelea na masomo ya elimu ya juu.



 


Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imefanya ziara ya ukaguzi katika Kituo cha Kupokea na Kupoza Umeme cha Mpomvu kilichopo mkoani Geita tarehe 15 Machi 2026, ikiwa ni sehemu ya ufuatiliaji wa utekelezaji wa miradi ya kimkakati ya Nishati inayolenga kuimarisha upatikanaji wa umeme nchini.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Subira Mgallu amesema ziara hiyo imelenga kukagua maendeleo ya miradi ya nishati pamoja na kuhakikisha uwekezaji unaofanywa na Serikali unaleta matokeo yaliyokusudiwa kwa wananchi.

“Kama Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini tuna jukumu la kuisimamia Wizara ya Nishati ili kuhakikisha inatekeleza majukumu yake kikamilifu. Tumeridhishwa na uwekezaji uliofanywa katika kituo hiki ambacho kina mchango mkubwa katika kuhakikisha upatikanaji wa umeme wa uhakika kwa wananchi na shughuli za kiuchumi,” amesema Mhe. Mgallu.

Ameongeza kuwa Kituo hicho kina uwezo wa kupokea na kusambaza takribani megawati 90, huku jitihada zikiendelea kuboresha miundombinu ya usambazaji wa umeme ikiwemo mpango wa kuongeza laini maalum kwa ajili ya Mgodi wa dhahabu wa Geita (GGM).

“Mahitaji ya umeme ya mgodi wa GGM yanatarajiwa kufikia takribani megawati 70 ifikapo mwaka 2035 kutoka megawati 36 zinazotumika kwa sasa, hivyo ni muhimu kuendelea kuimarisha miundombinu ya usambazaji wa umeme ili kukidhi mahitaji hayo,” ameongeza.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Nishati Mhe. Salome Makamba amesema Serikali inaendelea kuimarisha miundombinu ya umeme katika Mkoa wa Geita kutokana na ukuaji mkubwa wa shughuli za kiuchumi na kijamii hususan katika sekta ya madini.

“Kituo hiki kina mchango mkubwa katika kuimarisha upatikanaji wa umeme katika Mkoa wa Geita pamoja na maeneo ya jirani ikiwemo Biharamulo na Ngara mkoani Kagera, Sengerema mkoani Mwanza na Kakonko mkoani Kigoma,” amesema Mhe. Salome.

Naibu Waziri wa Nishati ameongeza kuwa Kituo cha Mpomvu kimegharimu takribani shilingi bilioni 50, uwekezaji ambao umeongeza uwezo wa usambazaji wa umeme katika eneo hilo linalokua kwa kasi kiuchumi ambapo mahitaji ya sasa ya umeme yamefikia Megawati 73.64.

Awali, Mkoa wa Geita ulikuwa ukipokea umeme kutoka Mkoa wa Shinyanga wenye uwezo wa takribani megawati 4 pekee, kiwango ambacho hakikukidhi mahitaji ya umeme yaliyokuwa yakiongezeka kutokana na shughuli za kiuchumi hususan uchimbaji wa madini.

Kituo cha Kupokea na Kupoza umeme cha Mpomvu kilianza kujengwa mwaka 2019 na kukamilika mwaka 2020, kabla ya kuzinduliwa rasmi mwaka 2022 na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.