Na.Ashura Mohamed - Arusha

 Maonyesho ya kimataifa ya utalii,ya Karibu Kilifair 2026 yanatarajiwa kuwakutanisha  wageni zaidi ya 1000  na waoneshaji wasiopungua 546 katika sekta ya Utalii hali ambayo itapelekea kuongeza Idadi ya Watalii nchini na Kipato kwa mkoa wa Arusha na Taifa kwa Ujumla.

Maonesho hayo yanatarajuiwa kufanyika  Juni 4 hadi 7, 2026 katika viwanja vya Magereza jijini Arusha,ambapo yatafunguliwa na Waziri wa Mali asili na Utalii Dkt.Ashatu Kijaji.

Akizungumza na Vyombo vya habari jijini Arusha Mkurugenzi wa Kilifair Promotion Ltd, Dominic Shoo,amesema maandalizi yamekamilika kwa asilimia kubwa  na lengo ni kutengeneza jukwaa la biashara linalouza vivutio vya Tanzania duniani,ambapo mwaka huu maonyesho yamevutia ushiriki kutoka  nchi 40, huku  kwa mara ya kwanza  Nigeria na Ghana zimejiunga na nchi nyingine kushiriki maonesho hayo.

‘’Mwaka huu tuna mtandao mkubwa sana wa kibiashara,tumeongeza vivutio vipya ikiwemo kupanda Mlima Kilimanjaro kwa njia ya kidijitali ndani ya viwanja, ambapo mshindi atapata safari halisi ya kupanda Kilimanjaro au Tsh. Milioni 1,” alisema Shoo.

Kwa Upande wake  mdau wa utalii  Timothy Mdinka  amesema kufanyika kwa maonyesho haya nchini kunapunguza gharama kwa Watanzania na kuwapa fursa ya kushindana kimataifa bila kusafiri nje.

“Kilifair wamerahisishia mambo mengi sana, mwaka huu wameongeza utalii wa michezo na utamaduni,Sisi kama wadau tunashukuru kwa kuwa wanatuwezesha kutengeneza bidhaa mpya za utalii pia siku zimeongezwa tofauti na awali hivyo tunatarajia yatakuwa na tija kubwa tofauti na miaka mingine,”alisema Mdinka.

Shoo alihitimisha kwa kusema kuwa maonyesho haya yanainua uchumi wa Arusha kwa kiwango kikubwa, kuanzia mama ntilie hadi hoteli kubwa, na yanaiweka mji huo kwenye ramani ya utalii duniani,ambapo lengo  ni kuwakutanisha wadau wa utalii chini ya mwavuli mmoja na kutengeneza jukwaa la biashara linalouza vivutio vya Tanzania duniani.

 


Na Jackline Minja, Dodoma

Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi, amesema Serikali itaendelea kuthamini mchango wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali katika kusaidia utekelezaji wa shughuli za Maendeleo na Ustawi wa Jamii nchini.

Akizungumza leo tarehe 15 Mei, 2026 wakati wa uwasilishaji wa shughuli za Mashirika Yasiyo ya Kiserikali kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii, Mhe. Mahundi amesema mashirika hayo yamekuwa yakisaidia wananchi kupitia afua mbalimbali za kijamii na kiuchumi ambapo mchango wao mkubwa katika kusaidia juhudi za Serikali kuwafikia wananchi kupitia miradi ya maendeleo inayogusa maisha yao ya kila siku.

“Shirika la Hand in Hand Eastern Tanzania (TZ) ni Shirika la Kimataifa lenye Makao yake makuu jijini Arusha ambalo linajishughulisha na afua za kuwawezesha wananchi kiuchumi katika Mikoa saba (7) nchini ambayo ni Dodoma, Simiyu, Arusha, Singida, Manyara, Kilimanjaro na Iringa na Shirika hili linalenga kuinua jamii na kuiwezesha kupitia biashara na ajira endelevu.” amesema Mhe. Mahundi

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Hand in Hand Eastern Africa Tanzania, Jane Richard Sabuni, amesema shirika hilo linaendelea kuweka nguvu katika kuwawezesha wananchi kujitegemea kupitia mafunzo ya ujasiriamali na ukuzaji wa biashara ndogondogo.

“Lengo letu ni kuona jamii inakuwa na uwezo wa kujitegemea kiuchumi kwa kuwapa wananchi maarifa, ujuzi na fursa za maendeleo zitakazoboresha maisha yao hivyo tutazidi kushirikiana na Serikali pamoja na wadau mbalimbali kuhakikisha wanawake, vijana na makundi maalum wanapata nafasi ya kushiriki kikamilifu katika shughuli za uzalishaji mali” amesema Jane.

Nao baadhi ya wabunge waliohudhuria semina hiyo wamepongeza mashirika hayo kwa kazi kubwa wanayoifanya katika kuongeza ufanisi wa maendeleo ya jamii pamoja na kusaidia wananchi katika maeneo mbalimbali nchini.

 


Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Hassan Saidy amewanasihi watumishi wa wakala kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa kufuata miongozo ya utumishi wa umma kwa kuzingatia sheria, taratibu na kanuni zilizopo.

Ametoa rai hiyo Jijini Dodoma Mei 15, 2026 katika kikao kazi na watumishi wote wa Wakala ambapo amewanasihi kuimarisha usimamizi wa miradi na kuwa sehemu ya miradi sambamba na kuimarisha mawasiliano na viongozi wa Serikali maeneo ya mradi.

“Tusirudi nyuma, tusilewe sifa tufikirie mambo makubwa zaidi. Tuwe wabunifu, tuchape kazi kwa weledi na ushirikiano na hii ndiyo nguzo itakayofanya tuendelee kusonga mbele,” amesema Mha. Saidy.

Mha. Saidy amesema Wakala umejipanga kuhakikisha miradi yote ya kusambaza nishati vijijini inakamilika kwa wakati na kwa ubora unaotakikana.

Katika kikao kazi hicho, watumishi walipata fursa ya kujadili masuala mbalimbali yanayolenga kuimarisha utendaji wa kazi, kukumbushana kuhusu miongozo mbalimbali ya utumishi wa umma pamoja na kupima afya zao kwa kuwa afya ni msingi wa ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao.

Wakati huohuo; Madaktari kutoka Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete kwa mwaliko maalum wa Menejimenti ya REA wameendesha zoezi la upimaji wa magonjwa yasiyoambukiza (moyo; homa ya ini na ugonjwa wa kisukari).

Zoezi hilo lilienda sambamba na utoaji wa chanjo ya kujikinga na ugonjwa wa homa ya ini ambapo Zaidi ya Watumishi 100 walipata huduma hiyo ya kinga.

NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Dkt. Ashura Katunzi, amesema katika kipindi cha miaka 50 Shirika hilo limefanikiwa kujenga na kusimamia mifumo ya udhibiti ubora na usalama wa bidhaa nchini hatua iliyosaidia kuongeza tija katika uchumi na sekta ya Viwanda na Biashara kwa ujumla.

 



Na Mwandishi Wetu, Arusha.

Serikali imeipongeza Benki ya CRDB Bank Plc kwa juhudi zake za kuhamasisha uwekezaji nchini kupitia elimu ya fedha, uwekezaji wa hisa na uwezeshaji wa kiuchumi unaolenga kuwajenga vijana kuwa wawekezaji wa baadaye.

Pongezi hizo zimetolewa jana jijini Arusha na Waziri wa Fedha, Khamis Mussa Omar wakati akifungua Semina ya Wanahisa wa Benki ya CRDB iliyofanyika sambamba na Mkutano Mkuu wa 31 wa mwaka wa benki hiyo katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC).

Semina hiyo ilikuwa na kaulimbiu isemayo “Vijana na Uwekezaji kwenye Hisa” na iliwakutanisha viongozi wa serikali, wanahisa, wataalamu wa masoko ya mitaji pamoja na vijana kutoka maeneo mbalimbali nchini.

Akizungumza katika semina hiyo, Waziri Omar alisema vijana wanapaswa kushiriki kikamilifu katika umiliki wa uchumi kupitia uwekezaji badala ya kutegemea ajira pekee.

“Kaulimbiu ya mwaka huu imebeba ujumbe mkubwa wa kimkakati kwa taifa letu. Vijana hawapaswi kuishia kutafuta ajira pekee, bali wanastahili kushiriki katika umiliki wa uchumi kupitia uwekezaji,” alisema Waziri Omar.

Aidha, aliipongeza benki hiyo kwa hatua ya kufungua Ofisi ya Uwakilishi Dubai, akisema hatua hiyo imeongeza hadhi ya Tanzania katika sekta ya fedha na uwekezaji kimataifa.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela alisema benki hiyo itaendelea kuwawezesha vijana kupitia huduma za kifedha, ubunifu na programu za maendeleo ya ujasiriamali.

Alisema kupitia CRDB Bank Foundation na programu ya IMBEJU, maelfu ya vijana na wafanyabiashara wadogo wamefikiwa kwa mafunzo, mitaji na ushauri wa biashara.

“Tunaamini vijana wa leo si wateja tu wa benki yetu, bali ni wawekezaji, wabunifu na viongozi wa uchumi wa kesho,” alisema Dkt. Nsekela.

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Benki ya CRDB, Neema Mori alisema uwekezaji katika hisa ni njia muhimu ya kujenga ustawi wa kifedha wa muda mrefu kwa vijana na familia za Kitanzania.

Profesa Mori alisema mafanikio ya Benki ya CRDB yanaonyesha namna uwekezaji wa muda mrefu unavyoweza kuleta matokeo chanya kwa wanahisa.

Alibainisha kuwa ndani ya miaka mitatu iliyopita thamani ya hisa za benki hiyo imeongezeka kwa zaidi ya asilimia 253, huku bei ya hisa ikifikia wastani wa Sh2,800 kutoka Sh460 mwaka 2023.

Aidha, alisema bodi ya wakurugenzi inapendekeza gawio la Sh90 kwa kila hisa kutokana na matokeo mazuri ya kifedha ya mwaka 2025, ikiwa ni ongezeko la asilimia 38 ikilinganishwa na mwaka uliopita.

Profesa Mori aliwahamasisha wazazi kuanza kuwawekezea watoto wao hisa mapema ili kuwajengea msingi imara wa maisha ya kifedha ya baadaye.

Benki ya CRDB ni miongoni mwa taasisi kubwa za kifedha Afrika Mashariki na Kati, ikiwa na zaidi ya wateja milioni sita katika nchi za Tanzania, Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo pamoja na ofisi ya uwakilishi Dubai, Falme za Kiarabu.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akizungumza wakati akifungua Semina ya Wanahisa wa Benki ya CRDB katika Mkutano Mkuu wa 31 wa Wanahisa, uliobeba kauli mbiu ya “Vijana na Uwekezaji kwenye Hisa”, semina inayofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC), ambapo alitoa wito kwa Taasisi za Fedha nchini kupunguza riba na gharama nyingine za mikopo ili kuwawezesha wananchi wakiwemo vijana kupata mitaji ya kuwekeza kwenye shughuli zao za kiuchumi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Dkt. Abdulmajid Nsekela, akizungumza wakati wa hafla ya ufunguzi wa Semina ya Wanahisa wa Benki ya CRDB katika Mkutano Mkuu wa 31 wa Wanahisa hao, uliobeba kauli mbiu ya “Vijana na Uwekezaji kwenye Hisa”, uliofunguliwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (hayupo pichani), uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC).
Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Benki ya CRDB, Prof. Neema Mori, akizungumza wakati wa hafla ya ufunguzi wa Semina ya Wanahisa wa Benki ya CRDB katika Mkutano Mkuu wa 31 wa Wanahisa hao, uliobeba kauli mbiu ya “Vijana na Uwekezaji kwenye Hisa”, uliofunguliwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (hayupo pichani), uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC).









Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) imetoa gawio la shilingi Bilioni 8.38 kwa serikali ikiwa ni ongezeko la Asilimia 50 kutoka shilingi Bilioni 5.58 ya mwaka 2024, katika Mkutano Mkuu wa wanahisa kwa mwaka ulioishia 31 Desemba 2025.
Shirika la Viwango Tanzania (TBS) limeshiriki Mkutano wa 28 wa Kamati ya Viwango Afrika Mashariki (EASC) uliofanyika Makao Makuu ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) jijini Arusha kuanzia Mei 12 hadi 14, 2026, kwa lengo la kutekeleza mpango kazi wa viwango, upimaji, metrolojia na ubora wa bidhaa (SQMT).



Na Mwandishi wetu- MBEYA

Mkurugenzi msaidizi wa Kituo cha Taifa cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Bi. Jane Kikunya amewataka Wajumbe wa Timu ya kukabiliana na Dharura na Uendeshaji wa Kitio cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura ya Mkoa wa Mbeya kufanya kazi kwa ushirikiano, mshikamano na mawasiliano ya karibu ili kutekeleza wajibu wao kwa weledi na ufanisi unaotakiwa.



Mkurugenzi huyo, ameyasema hayo wakati akifungua mafunzo ya siku tano yanayolenga kuziandaa timu za kukabiliana na Maafa za Mkoa huo.


Aidha, mafunzo hayo ambayo yaliyoandaliwa na Ofisi ya Waziri Mkuu yanatolewa kwa Wajumbe wa Kamati ya Wataalamu ya Usimamizi wa Maafa, Wajumbe wateule wa Timu ya kukabiliana na Dharura ya Mkoa na wataalamu wa Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura, Waratibu wa Maafa Mkoa na Halmashauri.




Vilevile, Bi. Jane amesema mafunzo hayo yatakuwa mhimili muhimu katika kuhakikisha Mkoa unajiandaa vyema ili kukabiliana na matukio ya dharura kwa haraka hivyo ni lazima timu lengwa ifanye kazi kwa mshikamano ili kuleta ufanisi unaohitajika.


Kwa upande wao wanufaika wa mafunzo hayo wameishukuru Serikali kwa namna inavyofanya jitihada kuhakikisha wananchi wanaishi katika mazingira salama.



Hivyo, wameahidi kutumia elimu hiyo ya kukabiliana na maafa pindi yanapotokea kuokoa maisha ya watu, mali zao na kurejesha hali.




 


Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora (OR- MUUUB) imetoa mafunzo kwa viongozi na watumishi wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM – TAMISEMI) yaliyolenga kuwajengea uwezo katika eneo la usimamizi wa utendaji kazi, ufungamanifu wa Mipango ya Maendeleo ya Kitaifa, Mpango Mkakati wa TAMISEMI na Shughuli za kila siku za Watumishi wa Makao Makuu, Mikoa, Halmashauri na Wadau wote ili  kutoa huduma bora kwa wananchi.

Mafunzo hayo yametolewa leo jijini Dodoma Mei 14, 2026 na Bw. Oswin Mkinga na Paulo Jorojick wa  OR- MUUB ikiwa ni utekelezaji wa maelekezo ya Mhe. Rais  Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kutoa huduma bora kwa wananchi.

“Mheshimiwa Rais, kwa nyakati tofauti ametuagiza watumishi wa umma viongozi na wasio viongozi kuhakikisha tunawahudumia Watanzania, hivyo Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Bw. Juma Selemani Mkomi ametulekeza tuje kuwapa mafunzo yatakayowajengea uwezo kiutendaji ili kuongeza ufanisi na tija katika kuwahudumia wananchi," amesema Bw. Mkinga.

Akiendelea kutoa mafunzo hayo, Bw. Mkinga amesema kuwa kwa mujibu wa Ibara ya 35 (1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Watumishi wa Serikali wanatekeleza majukumu ya Serikali kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, hivyo mafunzo hayo yamelenga kukuza utendaji kazi unaojali wananchi na maslahi ya taifa kwa jumla.

Aidha, Bw. Mkinga ameongeza kuwa  baadhi ya watumishi wa umma katika taasisi zao wanafanya kazi ambazo hazina mchango katika utekelezaji wa malengo ya taasisi zao na taifa, hivyo Mfumo wa e-Utendaji (PEPMIS) unasaidia kubaini mipango isiyofungamana, isiyopimika na ambayo haijibu matarajio ya wananchi.

Akizungumza kwa niaba ya Katibu Mkuu OWM-TAMISEMI, Mkurugenzi wa Idara ya Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu Bi. Emma Lyimo amesema mafunzo ya mfumo wa e-Utendaji (PEPMIS) ni muhimu katika kutimiza malengo ya Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, hivyo amewataka watumishi na viongozi waliohudhuria mafunzo hayo kuyazingatia kikamilifu na kwenda kutekeleza majukumu yao kwa ufasaha.









Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA), Mhandisi Charles Sangweni, amesema kuwa sekta ya mafuta na gesi asilia nchini Tanzania ina fursa kubwa na zenye mvuto kwa uwekezaji, hivyo kuwahimiza wadau mbalimbali wa sekta hiyo kuchangamkia fursa zilizopo.
SHIRIKA la Viwango Tanzania (TBS) limezindua huduma za Maabara ya Metrolojia katika Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, hatua inayotarajiwa kuongeza upatikanaji wa huduma za ugezi kwa haraka, kwa ufanisi na kwa gharama nafuu zaidi kwa wadau wa ukanda huo.

 




Na Oscar Assenga Tanga

IMEELEZWA kuwa uwepo wa Jukwaa la Wanawake na Kodi ni  hatua muhimu inayodhihirisha dhamira ya kuendeleza usawa wa kijinsia na kukuza uchumi shirikishi nchini.

Akizungumza wakati akifungua Jukwaa hilo Meneja wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Tanga, CPA Castro John, alisema ni dhamira ya dhati ya kujenga mfumo wa kodi unaoshirikisha makundi yote ya jamii, hususan wanawake ambao ni nguzo muhimu ya uchumi wa Taifa.



Alisema takwimu zinaonesha wanawake wanachangia kwa kiwango kikubwa katika shughuli mbalimbali za kiuchumi zikiwemo biashara ndogondogo, kilimo, huduma, viwanda vidogo pamoja na biashara za kati na kubwa.

Kwa mujibu wa takwimu za mwaka 2024/2025, wanawake nchini, wakiwemo wa Mkoa wa Tanga, wanakadiriwa kushiriki katika nguvu kazi kwa asilimia 80, huku wakimiliki asilimia 54 ya biashara ndogo, za kati na kubwa.

“Bila ushiriki wa wanawake, juhudi za kuongeza wigo wa walipa kodi na kuongeza mapato ya ndani haziwezi kufikia malengo yaliyokusudiwa,” alisema CPA Castro John.



Alifafanua kuwa TRA imeanzisha Jukwaa hilo maalumu kwa lengo la kutoa elimu sahihi ya kodi, kusikiliza changamoto za wanawake wafanyabiashara, kujenga ushirikiano wa karibu pamoja na kuhamasisha ulipaji wa kodi kwa hiari na kwa wakati.

Aidha, alisema TRA imejikita katika kuboresha huduma kwa kuzingatia ushirikishwaji, uwazi, weledi na urahisi wa upatikanaji wa huduma. Aliongeza kuwa elimu ya kodi na mahusiano bora ni msingi muhimu wa kuongeza utii wa kodi.

Kupitia jukwaa hilo, wanawake watapata nafasi ya kupata ushauri kuhusu masuala ya kodi, kujifunza fursa mbalimbali pamoja na kuelewa wajibu wao wa kikodi.



“Tunataka mwanamke ajisikie salama, aheshimiwe na ashiriki kikamilifu katika mfumo wa kodi bila hofu wala kikwazo chochote,” alisema.

CPA Castro John alisisitiza kuwa kodi ndiyo injini ya maendeleo ya Taifa kwani mapato yake yanagharamia huduma muhimu kama elimu, afya, barabara, maji safi na miradi mingine ya kimkakati.

“Kila mwanamke anayelipa kodi anakuwa mshirika wa moja kwa moja wa Serikali katika kujenga Tanzania yenye uchumi imara na huduma bora kwa wananchi wake,” aliongeza.

Pia aliwataka wanawake kutumia jukwaa hilo kujifunza, kuuliza maswali na kuwa mabalozi wa utamaduni wa kulipa kodi katika jamii zao.



Aidha, aliwataka wadau wa sekta mbalimbali pamoja na taasisi za kifedha kuendelea kushirikiana na TRA katika kuwawezesha wanawake kukuza biashara zao kwa kuzingatia misingi ya kikodi.

Kwa upande mwingine, aliwahimiza wanawake wafanyabiashara kujisajili katika mfumo wa kodi na kutekeleza wajibu wao kwa hiari na kwa wakati.



“Kulipa kodi si wajibu wa kisheria tu, bali ni mchango wa moja kwa moja katika kujenga Taifa. Wanawake wakisimama kiuchumi, familia na jamii vinaimarika,” alisema.

Katika hatua nyingine, alisisitiza umuhimu wa kutumia mipaka rasmi ya biashara kwa wafanyabiashara wanaovuka mipaka kupitia maeneo ya Horohoro na Pangani, huku akiwataka kuachana na biashara za magendo na matumizi ya njia zisizo rasmi.



Naye Naibu Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Wafanyabiashara nchini, JW Ismail Masound, alisema jukwaa hilo lina umuhimu mkubwa kutokana na malengo ya Dira ya Taifa ya mwaka 2050 ambapo sekta binafsi inatarajiwa kuwa mhimili mkubwa wa ukuaji wa uchumi.

Alisema majukwaa hayo yanasaidia kuwawezesha wanawake na wafanyabiashara kufikia malengo ya maendeleo ya Taifa kwa kuongeza ushiriki wao katika shughuli za kiuchumi.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Jukwaa la Wanawake Mkoa wa Tanga (TWCC), Aziza Ramadhani, alisema jukwaa hilo litawasaidia wanawake kuelewa umuhimu wa kulipa kodi katika kukuza uchumi wa Mkoa wa Tanga na Taifa kwa ujumla.

“Hivyo ni wajibu wetu kuhakikisha Mkoa wa Tanga unalipa kodi kutokana na umuhimu wake kwa maendeleo ya jamii,” alisema.

Aliongeza kuwa jukumu la jukwaa hilo ni kuwaunganisha wanawake wa Mkoa wa Tanga ili kuwapa nafasi ya kujifunza, kushirikiana na kupata fursa mbalimbali za kiuchumi ndani na nje ya mkoa huo.

Aidha, alisema wamekuwa wakitoa mafunzo mbalimbali ikiwemo kuanzisha mashamba darasa kwa vijana wa kiume na wa kike, huku akiwakaribisha wanawake wajasiriamali kushiriki katika shughuli za maendeleo zinazochangia ukuaji wa uchumi wa Mkoa wa Tanga na Taifa kwa ujumla.