Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM–TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, amesema Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuweka mazingira bora ya uwekezaji na usimamizi wa rasilimali madini, kwa lengo la kuhakikisha utajiri wa madini unatumika kikamilifu katika kujenga uchumi wa taifa na kuongeza fursa za ajira kwa wananchi.

Prof. Shemdoe amesema hayo Septemba 16, 2026, akiwa Ruangwa mkoani Lindi, wakati akifungua Maonesho ya Madini na Fursa za Uwekezaji mkoani humo.

“Lengo la Serikali ni kuhakikisha kuwa sekta ya madini haibaki kuwa ya uchimbaji pekee, bali inakuwa kichocheo cha viwanda, teknolojia, ajira, biashara, ubunifu na maendeleo ya jamii,” amesisitiza Prof. Shemdoe.

Katika kuhakikisha lengo hilo linatimia, Prof. Shemdoe ameyataka makampuni makubwa yaliyowekeza katika sekta ya madini kuangalia namna bora ya kuwekeza katika ujenzi wa viwanda vya uchenjuaji wa madini mkoani Lindi, hususan katika maeneo yenye rasilimali hizo, ili wananchi wanaozunguka maeneo hayo wanufaike zaidi kupitia fursa za ajira.

Prof. Shemdoe amesema maonesho hayo ni jukwaa muhimu linalowaunganisha Serikali, wananchi, wawekezaji katika sekta mbalimbali za uchumi, wataalam pamoja na taasisi za kifedha, kwa ajili ya kujenga uelewa mpana kuhusu rasilimali zilizopo na fursa za uwekezaji, pamoja na namna sekta mbalimbali za uchumi, ikiwemo madini, zinavyoweza kuongeza ajira, mapato na kukuza uchumi wa mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla.

“Nilipofika hapa nilitembelea mabanda mbalimbali yaliyowakutanisha wachimbaji wakubwa, wadogo, wanaoleta teknolojia, akina mama, vijana na taasisi za kifedha, ili wakitoka hapa watoke na fursa mbalimbali zinazotokana na uwekezaji katika sekta ya madini,” ameeleza Prof. Shemdoe.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Mhe. Adam Kighoma Malima, amesema mkoa huo si maskini, bali changamoto ni wananchi wake kuwa maskini, kwani mkoa hauwezi kuitwa maskini wakati una utajiri wa madini mbalimbali, jambo aliloliona kupitia maonesho hayo.

Mhe. Malima ameahidi kuwa ofisi yake itaendelea kusimamia maonesho kama hayo ya madini ili yaendelee kuibua fursa na kuvutia uwekezaji utakaowanufaisha wananchi.

Aidha, Mhe. Malima amesema anatarajia kuwa ndani ya kipindi cha uongozi wa miaka mitano wa Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, mkoa wa Lindi utakuwa umetambua fursa zake, kuzipa kipaumbele na hatimaye kuwa miongoni mwa mikoa yenye mapato makubwa nchini.

Naye Mbunge wa Ruangwa ambaye pia ni Naibu Waziri, Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Kaspar Mmuya, amesema Ruangwa ina kiwanda kikubwa cha graphite, huku akieleza kuwa madini yaliyopo wilayani humo si graphite, dhahabu na kopa pekee, bali yapo madini mengine mengi.

Mhe. Mmuya amesema kutokana na uwepo wa rasilimali hizo, Ruangwa imeendelea kunufaika na mapato yatokanayo na sekta ya madini, ambapo mwaka jana wilaya hiyo ilichangia kiasi cha shilingi bilioni 2.9.














 


Na: OWM – TAMISEMI, Ruangwa

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM–TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, ameitaka Halmashauri ya Manispaa ya Lindi kukamilisha mchakato wa kushughulikia upatikanaji wa hati ya umiliki wa ardhi kwa ajili ya Kampasi ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) mkoani Lindi.

Prof. Shemdoe ametoa agizo hilo wakati wa kikao kazi chake na viongozi wa Halmashauri ya Manispaa ya Lindi na Chuo Kikuu cha Dar es salaaam (UDSM), kilicholenga kupata ufumbuzi wa changamoto zinazohusu maendeleo ya kampasi hiyo, ikiwa ni utekelezaji wa agizo la Waziri Mkuu Mhe. Dkt. Lameck Mwigulu Nchemba alilolitoa wakati wa ziara yake mkoani Lindi akielekeza hatua zichukuliwe kuhakikisha kampasi hiyo ya UDSM Lindi inapata hati ya umiliki wa ardhi.

Katika kikao hicho kilichofanyika Septemba 16, 2026 Ruangwa mkoani Lindi, Prof. Shemdoe amemsisitiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Lindi, Bw. Juma Mnwele, kuhakikisha suala la hati ya umiliki wa ardhi la Kampasi hiyo ya UDSM Lindi linashughulikiwa kwa haraka na apatiwe mrejesho wa utekelezaji wake.

Aidha, Prof. Shemdoe ameiagiza Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) mkoani Lindi kukamilisha maandalizi ya ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami yenye urefu wa kilomita 1.5, itakayounganisha Kampasi hiyo ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Lindi na barabara kuu ya Lindi.

Kikao hicho cha Prof. Shemdoe kwa upande wa Serikali kilihudhuriwa na Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Mhe. Adam Kighoma Malima, Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Kaspar Mmuya,    Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Lindi Bw. Juma Mnwele, Meneja wa TARURA Mkoa wa Lindi Mhandisi Alberto Kindole, pamoja wataalam na viongozi wengine wa Mkoa.

Kwa upande wa Chuo Kikuu cha Dar es salaam (UDSM), kikao kazi hicho kiliudhuriwa na ujumbe uliongozwa na Naibu Makamu Mkuu wa Chuo anayeshughulikia Mipango, Fedha na Utawala (DVC-PFA), Prof. Bernadeta Killian.












 


🔶 WAAHIDI UTENDAJI MAHIRI ZAIDI


Na WMA  - DODOMA.


Baadhi ya madereva kutoka Wakala wa Vipimo (WMA) wanashiriki Kongamano la Tano la Chama cha Madereva wa Serikali Tanzania (MST-TGDU) linaloendelea katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete jijini Dodoma.

Kongamano hilo la kitaifa lililoanza Septemba 12 limewakutanisha mamia ya madereva wa Serikali kutoka mikoa yote nchini, ambapo pamoja na mambo mengine wanajadili mustakabali wa taaluma yao, changamoto wanazokutana nazo barabarani na namna ya kuimarisha nidhamu na weledi kazini.

Kwa mujibu wa waandaaji, kongamano hili ni zaidi ya mkutano wa kawaida; ni darasa huru la kubadilishana uzoefu, kujifunza mbinu mpya za uendeshaji salama, matunzo ya vyombo vya moto vya Serikali na umuhimu wa uwajibikaji katika kulinda mali za umma.

Akizungumza kwa niaba ya madereva wa WMA, Dereva Mkuu kutoka WMA Mkoa wa Dodoma, Bw. John Jumbe amesema ushiriki wao umewapa fursa ya kipekee kujifunza na kuona thamani ya taaluma yao.

 "Tumefurahi sana kushiriki kongamano hili. Tumebadilishana uzoefu na wenzetu kutoka taasisi nyingine na tumejifunza mengi kuhusu uwajibikaji, usalama barabarani na namna ya kuwa mabalozi wazuri wa WMA na Serikali kwa ujumla. Tutaenda kuyafanyia kazi tuliyojifunza," amesema Bw. Mhando.

Ushiriki wa WMA katika kongamano hilo unaakisi dhamira ya Wakala inayoongozwa na Afisa Mtendaji Mkuu Bw. Alban Mark Kihulla, ya kuendelea kuwawezesha watumishi wake katika ngazi zote ili kuhakikisha wanatoa huduma bora na yenye tija kwa wananchi.

Kaulimbiu ya Kongamano hilo linalotarajiwa kuhitimishwa Septemba 19, 2026 ni 'Dereva wa Serikali, Nguvu Moja, Sauti Moja, Kulinda Amani ya Nchi ni Jukumu letu pia.'







WANANCHI 1,560 na mifugo 3,480 katika Kitongoji cha Katikati, Kijiji cha Njoroi, Kata ya Ololosokwan, Wilaya ya Ngorongoro, mkoani Arusha, wanatarajia kuondokana na adha ya kutembea zaidi ya kilomita saba kusaka maji kufuatia uzinduzi wa mradi wa maji wa Sh milioni 65.

Kabla ya kukamilika kwa mradi huo, wananchi walilazimika kutembea umbali mrefu kutafuta huduma hiyo muhimu,huku wengine wakivuka mpaka kwenda nchini Kenya, hali iliyokuwa ikiongeza mzigo kwa wanawake na watoto.

Mradi huo uliozinduliwa na Mkuu wa Wilaya ya Ngorongoro, Brigedia Jenerali Wilson Sakulo, unatarajiwa kuboresha upatikanaji wa maji kwa matumizi ya wananchi na mifugo, pamoja na kupunguza changamoto za kiusalama zinazohusiana na safari za kutafuta maji.

Naye Kaimu Meneja wa RUWASA, wilayani hapo, Jumbe Mollel, amesema Kitongoji cha Katikati kilikuwa na changamoto kubwa ya upatikanaji wa maji, ambapo RUWASA iliwahi kujaribu kupeleka mitambo kwa ajili ya kuchimba kisima, lakini juhudi hizo hazikufanikiwa.

Wakati huo huo, Mjumbe wa Bodi ya PWC, Kooya Timan, amewataka wanawake wanaonufaika na mradi huo kuutunza na kuhakikisha miundombinu yake inabaki katika hali nzuri ili huduma hiyo iendelee kutolewa kwa muda mrefu.



 


Sheria kuanzisha Bodi ya Wajiolojia kusimamia na kuratibu taaluma nchini

Serikali kutenga asilimia 10 ya mapato ya madini kwa utafiti wa jiosayansi

Taarifa sahihi za jiolojia kuimarisha uwekezaji na kuwalinda wadau wa madini


Wizara ya Madini imewasilisha pendekezo la kuanzishwa kwa Sheria ya Usimamizi wa Wajiolojia nchini katika Sekretarieti ya Baraza la Mawaziri, hatua inayolenga kuweka mfumo madhubuti wa kusimamia taaluma hiyo na kuhakikisha taarifa za jiosayansi zinazotolewa nchini zinakuwa sahihi na zenye kuaminika.

Hayo yamebainishwa leo, Septemba 16, 2026, jijini Mwanza na Naibu Waziri wa Madini, Dkt. Steven Kiruswa, wakati akifunga Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Jumuiya ya Wajiolojia Tanzania (TGS).

Dkt. Kiruswa amesema endapo Sheria hiyo itapitishwa, itaanzishwa Bodi ya Wajiolojia itakayokuwa na jukumu la kusimamia, kuratibu na kuimarisha taaluma hiyo, ikiwemo kuweka viwango vya kitaaluma na kuhakikisha wataalamu wanaohusika na shughuli za jiosayansi wanatambulika na kuwajibika ipasavyo.

Amesema hatua hiyo ni muhimu kutokana na umuhimu wa taarifa za jiosayansi katika shughuli za utafutaji, uchimbaji na uwekezaji katika sekta ya madini, huku akieleza kuwa kumekuwa na baadhi ya taarifa zisizo sahihi zinazotolewa na watu wasio waaminifu au wasiokuwa na weledi na ujuzi unaohitajika, hali ambayo imekuwa ikisababisha hasara kwa baadhi ya wadau wa sekta hiyo.

“Ni muhimu kuwa na chombo kitakachosimamia taaluma hii ili kuhakikisha taarifa za jiosayansi zinazotokana na tafiti zinazofanywa nchini zinakuwa za uhakika na zinatolewa na wataalamu wenye sifa, weledi na uwajibikaji,” amesema Dkt. Kiruswa.

Katika hatua nyingine, Dkt. Kiruswa amesema Serikali imefanya uamuzi wa kutenga asilimia 10 ya makusanyo yatokanayo na mapato yasiyo ya kodi katika sekta ya madini kwa ajili ya shughuli za utafiti wa madini nchini, ambapo fedha hizo zinakadiriwa kufikia takribani Sh bilioni 140.

Amesema fedha hizo zitawezesha Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) kuongeza kasi ya tafiti za jiosayansi na kuzalisha taarifa nyingi na sahihi zitakazosaidia kubainisha rasilimali zilizopo nchini na kuweka msingi imara wa uwekezaji katika sekta ya madini.

Dkt. Kiruswa amesema Wizara ya Madini itaendelea kushirikiana na Jumuiya ya Wajiolojia Tanzania katika kuimarisha taaluma hiyo na kuhakikisha wataalamu wa ndani wanashiriki kikamilifu katika tafiti na shughuli za jiosayansi zinazolenga kuongeza manufaa ya rasilimali za madini kwa Taifa.

Ameeleza kuwa hatua hiyo inakwenda sambamba na vipaumbele vya Wizara vinavyotokana na Dira ya Maendeleo ya Tanzania 2050 na Sera ya Madini, ambavyo ni pamoja na kuongeza utafiti na upatikanaji wa taarifa sahihi za jiolojia, kuongeza thamani madini, kuunganisha sekta ya madini na sekta nyingine za uchumi, kurasimisha na kuboresha uchimbaji mdogo, pamoja na kuimarisha usimamizi wa mazingira na kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

Kwa upande wake, Rais wa Jumuiya ya Wajiolojia Tanzania, Prof. Alisante Mshiu, amesema Mkutano Mkuu wa Mwaka ulianza Septemba 14, 2026, ukiwa na dhima ya “Matumizi ya Suluhisho za Jiosayansi kwa Ukuaji wa Viwanda, Uhakika wa Upatikanaji wa Nishati, Kuelekea Matumizi ya Nishati Safi na Maendeleo Stahimilivu Tanzania.”

Amesema mkutano huo umelenga kutoa fursa kwa wataalamu kubadilishana uzoefu na maarifa katika nyanja mbalimbali za jiosayansi, kwa lengo la kuongeza matumizi ya taaluma hiyo katika kutatua changamoto za maendeleo, kukuza uchumi na kuongeza manufaa yatokanayo na rasilimali zilizopo nchini.


















Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM–TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, amesema hajaridhishwa na kasi ya utekelezaji wa miradi inayotekelezwa na Mkandarasi KIKIM Contractors Limited kwa kushirikiana na mbia wake AMACO Enterprises katika Manispaa ya Lindi.

Miradi hiyo inahusisha ujenzi wa barabara zenye urefu wa kilomita 5.3, Stendi ya Mabasi Mitwero, Soko Kuu la Matopeni na Ofisi ya Mradi, inayotekelezwa na Serikali kupitia Mradi wa Ustawishaji Miji Tanzania (TACTIC).

Prof. Shemdoe ameeleza kutoridhishwa kwake na kasi ya utekelezaji wa miradi hiyo Septemba 15, 2026, mara baada ya kutembelea na kukagua ujenzi wa Stendi ya Mabasi ya Mitwero na Soko Kuu la Matopeni, ambapo alibaini kuwa utekelezaji wake umefikia asilimia 23, huku ikiwa imesalia miezi mitano kabla ya muda wa kukamilisha na kukabidhi miradi hiyo.

Akizungumza baada ya kukagua miradi hiyo, Prof. Shemdoe amemtaka Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Mhe. Adam Kighoma Malima, kuhakikisha suala la utekelezaji wa mikataba hiyo linashughulikiwa kwa mujibu wa masharti ya mikataba, ili kuharakisha utekelezaji na kuhakikisha miradi hiyo inakamilika kwa wakati.

“Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa, hawa wanaotukwamisha ni wakandarasi wazawa ambao usipowapa kazi wanalalamika. Hivyo, Mheshimiwa RC, hawa wana mikataba, shughulikia suala hili kwa mujibu wa mkataba, kwani wakandarasi hawa wanaonekana ni wababaishaji,” amesema Prof. Shemdoe.

Aidha, Prof. Shemdoe amemtaka Mkuu wa Mkoa wa Lindi kukutana na wakandarasi hao ili wampe mpango mkakati wa kukamilisha miradi hiyo haraka iwezekanavyo, na kuwasilisha kwake mpango kazi huo ifikapo Septemba 23, 2026.Vilevile, ameelekeza kuwa kila baada ya wiki mbili apatiwe mrejesho wa utekelezaji wa mpango huo, ili kufahamu hatua zinazochukuliwa na maendeleo ya miradi hiyo.

Akieleza chanzo cha kasi ndogo ya utekelezaji wa miradi hiyo, Mwakilishi wa Mhandisi Mshauri kutoka kampuni ya Interconsult Ltd, ambaye pia ni Mhandisi Mkazi, Mhandisi Rashidi Abdallah, amesema changamoto hiyo imetokana na mkandarasi kutokuwa amejipanga vyema kiutendaji, kutokuwa na rasilimaliwatu ya kutosha na kutumia vibaya fedha za awali alizolipwa kwa ajili ya utekelezaji wa mradi.

Naye mmoja wa Wakurugenzi wa kampuni zilizopewa kandarasi hizo, John Daniel, amekiri kuwa wamechelewa kutekeleza miradi hiyo kutokana na uzembe, huku akieleza kuwa wamejipanga kufanya kazi usiku na mchana baada ya kuzifanyia kazi changamoto zilizokuwa zikikwamisha utekelezaji. 

Bw. Daniel ameomba kukutana na Mkuu wa Mkoa wa Lindi ili kuwasilisha mpango kazi wao, huku akimuomba Mkuu wa Mkoa kuwawekea malengo ya muda mfupi yatakayowawezesha kukamilisha kandarasi yao kwa wakati.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Mhe. Adam Kighoma Malima, amesema atakutana na wakandarasi hao ili wamueleze mkakati wanaokuja nao wa kukamilisha miradi yote ndani ya miezi mitano iliyobaki.

Mhe. Malima amewataka wakandarasi hao, wakati wa kikao hicho, kuwa tayari kuridhia kutoa mkataba mdogo (sub-contract) kwa mkandarasi mwingine kutekeleza sehemu ya mradi endapo wataona hawana uwezo wa kuikamilisha kwa wakati.

Katika ziara yake ya Septemba 15, 2026, Prof. Shemdoe alitembelea na kukagua pia utekelezaji wa miradi ya ujenzi wa Daraja la Ng’uni katika Kata ya Nanganga, ujenzi wa shule mpya ya msingi eneo la Shule ya Sekondari Kitandi, ujenzi wa Kituo cha Afya Chiola Nachingwea, pamoja na kufanya mkutano wa hadhara katika Kijiji cha Mtuha, Nachingwea DC.