Waziri wa Madini Anthony Mavunde amewakaribisha wawekezaji wa viwanda vya uzalishaji wa betri za magari ya umeme na vifaa vya kieletroniki kuwekeza nchini Tanzania kwa kuwa Tanzania imebarikiwa na madini mkakati ya kutosha ambayo ni malighafi kuu ya uzalishaji wa betri za magari ya umeme na vifaa vya kieletroniki.

Mh Mavunde ameyasema hayo leo Kwamsisi,Wilayani Handeni mkoani Tanga wakati akiweka jiwe la msingi la ujenzi wa kiwanda cha uchenjuaji madini mkakati ya kinywe(_Graphite_) kinachomilikiwa na Kampuni ya GODMWANGA GEMS LTD.

“Uwekezaji huu unatokana na mazingira mazuri na wezeshi yaliyowekwa na serikali ya awamu ya sita chini ya uongozi wa Mh. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Ninampongeza sana Mwekezaji Mtanzania Ndg. God Mwanga kwa kuwa mmoja kati ya wawekezaji wakubwa wa madini kinywe nchini Tanzania na hivyo kuchochea ukuaji wa sekta ya madini na upatikanaji wa nafasi za Ajira kwa watanzania.

Mkakati wa serikali ni kuhakikisha madini haya yanaongezwa thamani nchini Tanzania ili kutunza ajira za watanzania,kuwajengea uwezo na kukuza uchumi wa taifa kupitia kodi na mapato mbalimbali.Hivyo niwakaribishe wawekezaji wote wenye nia ya kuongeza thamani mkakati haya kuitumia fursa hii kwa kuwa Tanzania imebarikiwa madini mengi na ya kila aina.

Nitumie fursa hii kutoa rai kwa uongozi wa mikoa na wilaya kubainisha maeneo maalum ya ujenzi wa viwanda vya kuongeza thamani madini kama sehemu ya kuchochea uwekezaji katika eneo hili”Alisema Mavunde

Naye Mkuu wa Wilaya ya Handeni Wakili Alberto Msando amesema mkakati mkubwa wa Wilaya kwasasa ni kuhakikisha kunakuwepo na umeme wa kutosha ili kuongeza uzalishaji katika mgodi huu na kwasasa kuna mradi wa thamani ya shilingi 60bn wa ujenzi wa kituo kidogo cha kupoozea umeme ambao utaelekezwa katika maeneo ya uzalishaji ikiwemo viwanda vya uchenjuaji wa madini sambamba na ukarabati wa miundombinu ya Barabara.

Akitoa maelezo ya awali Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya GODMWANGA GEMS LTD God Mwanga amesema ujenzi wa kiwanda hicho ukikamilika utakuwa na uwezo wa uzalishaji wa Tani 800 za madini kinywe kwa usiku na utakuwa unauingizia serikali zaidi ya Tsh bilioni 1.8 kwa mwezi kama mapato yatokanayo na ada,tozo na mrahaba na hivyo kuwasilisha maombi rasmi serikalini juu ya upatikanaji wa umeme wa kutosha ili kufikia malengo makuu ya uzalishaji.

 

Share To:

Post A Comment: