NA DENIS CHAMBI, TANGA.
WASHINDI kupitia maonesho ya Elimu ujuzi na ubunifu yanayoendelea kufanyika kitaifa mkoani Tanga wanatarajiwa kuiwakilisha Tanzania katika maonesho ya kidunia kwenda kuonesha ujuzi ,ubunifu na maarifa yao.
Hayo yameelezwa na katibu mtendaji kutoka baraza la Taifa la elimu ya ufundi na mafunzo ya ufundi stadi (NACTVET) Mwajuma Lingwanda wakati akizungumza na waandishi wa habari katika maonesho hayo ambapo amesema jumla ya washiriki 49 waliopatikana kwenye mchujo uliofanyika katika ngazi ya Kanda watashindanishwa kwenye vipengele 9 ambapo kila mshidi atakata tiketi ya kwenda kuiwakilisha Tanzania kimataifa.
"Mashindano haya yalianza katika ngazi ya Kanda ambapo tulikiwa na washiriki katika maeneo 9 ya ujuzi na baada ya hapo tumefikia kwenye maonesho ya kitaifa na tuna washiriki 49 kutoka kwenye taasisi mbalimbali waamuzi wako tayari wale watakaofanikiwa kufaulu na kuwa washindi wa kwanza watapata nafasi ya kushiriki kwenye mashindano ya kimataifa mwaka huu"amesema Lingwanda.
Fani hizo zitakazoshindaniwa ni pamoja na mapishi , mekatroniksi, ujenzi, ujuzi wa mitandao, uchomeleaji wa vyuma , uhandisi, ushonaji wa nguo, na urembo.
Akizungumza Mkurugenzi mdhibiti ubora kutoka NACTVET Geoffrey Oleke amesema kuwa ujuzi katika nyanja mbalimbali ni una umuhimu husasani kwa rika la vijana ambao ndio tegemeo na Taifa la kesho hivyo Taifa linapaswa kuwekeza katika elimu ya sayansi.
Amesema mchakato wa kuwapata washiriki wa maonesho hayo ulianza juni 2026 ambapo vyuo vyote vya sayansi vilishiriki katika mchakato katika fani 15 ambapo kati ya hizo fani 9 zilipata washiriki wengi hivyo kupewa kipaumbele kwa washiriki wa mwaka huu kitaifa ambapo kila fani ina washiriki watano watakaochuana kuonyesha maarifa na ujuzi wao.
"Bila ujuzi kwa Hakika hakuna nchi inaweza ikaendelea kwahiyo na sisi kama nchi tunashiriki kwa lengo la kuhakikisha kwamba tunakuza ujuzi wa vijana wetu katika shule za sekondari na vyuo ili tupate nguvu kazi iliyo imara ambayo itaisaidia nchi yetu katika kuchochea maendeleo yake" amesema Oleke.
Maonesho hayo ambayo kwa mwaka huu wa 2026 yamebebwa na kauli mbiu isemayo Elimu ujuzi na ubunifu , njia ya kufikia dira 2050 yameanza kufanyika August 16 yakifunguliwa rasmi na waziri wa elimu Prof. Adolfu Mkenda huku yakitarajiwa kufungwa August 24 na waziri mkuu wa jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt Mwigulu Nchemba




Post A Comment: