
Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga, akiwasilisha Hotuba ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 leo Mei 22,2026 bungeni Dodoma.
Na.Alex Sonna-DODOMA
Serikali imefikia hatua muhimu katika utekelezaji wa Mradi mkubwa wa Chuma wa Liganga na Makaa ya Mawe wa Mchuchuma baada ya kukamilisha majadiliano na mwekezaji mpya wa mradi huo, hatua inayotajwa kuwa ya kihistoria katika safari ya Tanzania kuelekea uchumi wa viwanda.
Akiwasilisha bajeti ya Wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026-2027,bungeni Waziri wa Viwanda na Biashara,Judith Kapinga,amesema Serikali imekamilisha mazungumzo na kampuni ya Shudao Investment Group Company Limited (SDIG), kampuni inayomilikiwa na Serikali ya China, kwa ajili ya kuendeleza mradi huo kwa kushirikiana na Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC).
Kampuni hiyo imechukua nafasi ya kampuni ya awali ya Sichuan Hongda Group Company Limited (SHG), iliyokuwa imeanza majadiliano ya utekelezaji wa mradi huo miaka iliyopita.
Amesema kuwa pande zote zimefikia mwafaka katika maeneo muhimu ya uwekezaji ikiwemo mgawanyo wa hisa, kiwango cha mtaji wa mradi, muundo wa usimamizi, muda wa mikataba pamoja na namna ya kuongeza thamani ya madini hapa nchini.
Madini yatakayoongezwa thamani nchini ni pamoja na chuma, vanadium na titanium, hatua inayotarajiwa kuongeza mchango wa sekta ya madini katika uchumi wa Taifa pamoja na kuchochea maendeleo ya viwanda vya ndani.
Aidha, rasimu za mikataba ya ubia na wanahisa kwa ajili ya shughuli za uchimbaji na ujenzi wa kiwanda cha kuzalisha bidhaa za chuma tayari zimekamilika, huku hatua za mwisho za idhini kutoka mamlaka husika zikiendelea.
Serikali imeeleza kuwa mikataba hiyo inatarajiwa kusainiwa katika nusu ya kwanza ya mwaka wa fedha 2026/2027, kabla ya kuanza rasmi kwa ujenzi wa mradi ambao unatarajiwa kuchukua miaka mitatu kukamilika.
Mradi huo unatajwa kuwa miongoni mwa miradi mikubwa ya kimkakati kuwahi kutekelezwa nchini kutokana na manufaa yake makubwa kiuchumi.
Taarifa zinaonesha kuwa utekelezaji wake utawezesha Tanzania kuokoa zaidi ya dola za Marekani bilioni 1.22, sawa na shilingi trilioni 3.2, ambazo kwa sasa hutumika kuagiza bidhaa za chuma kutoka nje ya nchi.
Bidhaa za chuma zimeendelea kuwa miongoni mwa bidhaa zinazoongoza kwa matumizi makubwa ya fedha za kigeni baada ya mafuta ya petroli.
Mbali na kupunguza utegemezi wa bidhaa za nje, mradi huo pia unatarajiwa kufungua mlolongo mkubwa wa viwanda vitakavyotumia malighafi za chuma, makaa ya mawe na madini mengine yatakayozalishwa ndani ya nchi.
Vilevile, Serikali inaamini kuwa kuanza kwa uzalishaji wa chuma nchini kutasaidia kupunguza matumizi ya chuma chakavu kinachochangia uharibifu wa miundombinu katika maeneo mbalimbali.
Amesema tathmini ya awali ya kifedha iliyofanywa kwa pamoja na wataalamu wa Serikali na mwekezaji, Serikali inatarajia kupata mapato makubwa kupitia kodi na mirahaba ndani ya kipindi cha miaka 25 ya utekelezaji wa mradi huo.
Makadirio yanaonesha kuwa Serikali inaweza kukusanya hadi dola za Marekani trilioni 1.99 kupitia kodi mbalimbali na malipo ya mrahaba yatakayotokana na mauzo ya umeme, makaa ya mawe, bidhaa za chuma, titanium, vanadium pamoja na aluminium sulphate.
Aidha, utekelezaji wa mradi huo unatarajiwa kuzalisha ajira za moja kwa moja zipatazo 6,500 na nyingine zaidi ya 26,000 zisizo za moja kwa moja, hatua inayotarajiwa kuongeza kipato kwa wananchi na kukuza uchumi wa maeneo ya mradi.
Wakati huo huo, Serikali kupitia Shirika la Taifa la Maendeleo imeendelea kusimamia utekelezaji wa Mradi wa Magadi Soda katika bonde la Engaruka wilayani Monduli.
Hatua zilizofikiwa hadi sasa ni pamoja na ulipaji wa fidia kwa wananchi wanaopisha mradi pamoja na upatikanaji wa mwekezaji wa mradi huo.
Ameeleza kuwa hadi Aprili 2026, Serikali ilikuwa imelipa shilingi bilioni 5.82 sawa na asilimia 98.7 ya fedha za fidia kwa wananchi 513 kati ya 594 waliotakiwa kulipwa.
Zoezi la kukamilisha malipo linaendelea kwa wananchi waliobaki huku Serikali ikieleza kuwa baadhi yao bado wanakamilisha nyaraka muhimu za mirathi na umiliki.
Aidha, Timu ya Serikali ya Majadiliano inaendelea na mazungumzo ya mwisho ya mkataba wa ubia na kampuni iliyoshinda zabuni ya kuendeleza mradi huo.
Mradi wa Magadi Soda unatarajiwa kuokoa zaidi ya dola za Marekani milioni 121 zinazotumika kila mwaka kuagiza malighafi ya magadi soda pamoja na bidhaa zake kutoka nje ya nchi.

Post A Comment: