Na Mwandishi Wetu.

Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela  inashiriki kikamilifu katika kuleta hamasa na chachu ya Wasichana na Wanawake  kupenda na kujiunga na masomo ya Sayansi, Hisabati, Teknolojia, Uhandisi na Ubunifu katika kuongeza wataalam wa fani hizo nchini.

Hayo yamesemwa  Februari 11, 2024 Jijini Arusha  na Naibu Makamu Mkuu wa Taasisi Mipango,Fedha na Utawala wa Taasisi hiyo,  Prof. Suzana Augustino wakati wa Maadhimisho ya Kimataifa ya Siku ya Wanawake na Watoto katika
Sayansi iliyofanyika  ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa AICC jjini hapo.

“Katika kulitekeleza hili mbali na kutoa mafunzo ya Shahada ya Uzamili na Uzamivu pia tunatoa hamasa kwa wanafunzi wa elimu ya Msingi na Sekondari ili wapenda masomo ya sayansi, Hisabati, Teknolojia, Uhandisi na Ubunifu kupitia klabu na vikundi vinavyofanya kazi na watafiti wetu.” amesisitiza Prof. Suzana
Augustino.

Ameongeza kuwa,  taasisi imekuwa ikifanya kazi kwa kushirikiana na shule za msingi na sekondari kwa kutoa utaalamu kupitia wabunifu wake katika kuwafundisha wanafunzi kwa vitendo kupitia nyanja mbalimbali.

“Kuna shule ambayo watoto wanajifunza mambo ya nishati mbadala ambapo taasisi yetu inatoa utaalamu lakini wao wanafanya kwa vitendo, kwa kufanya hivyo miaka mitano ijayo tutakuwa na watoto wanaopenda masomo ya sayansi na hivyo kuchangia katika adhma  ya serikali ya kuongeza idadi na ushiriki wa wanawake na wasichana katika sayansi” ameeleza Prof. Suzana Augustino.

Naye Mhadhiri kutoka Taasisi hiyo Prof. Neema Kassim ametoa wito kwa jamii kuwapa nafasi watoto ya kushiriki masomo ya vitendo ili kuweza kupenda wanachofanya kwa kuwashirikisha katika midahalo mbalimbali ili kuwa na uwezo wa kujiamini.

Maadhimisho ya siku  ya wanawake na wasichana katika sayansi mwaka huu yameongonzwa na  Kauli Mbiu  “Wanawake na wasichana katika Uongozi wa Sayansi, Enzi Mpya ya Maendeleo Endelevu”.

Share To:

Post A Comment: