Serikali imesaini mkataba  wa bilioni 27 kwaajili ya mradi wa maji katika vijiji 19 unaotarajiwa kutatua kero ya muda mrefu ya maji inayowakabili wananchi Wilayani Monduli mkoani Arusha.

Aidha Waziri wa Maji Jumaa Aweso amewaagiza wataalam wa maji na wahandisi kutokuwa kikwazo cha kukwamisha miradi ya maji inayotakiwa kuwafikia wananchi kwa lengo la kuwatua ndoo kichwani 

Akizungumza katika kata ya Lepurko eneo la Nanja wilayani Monduli,wakati wa kusaini mkataba wa mradi wa maji  toka Jiji la Arusha wenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 20 kwenda vijiji 13 na mkataba mradi wa maji kwenda vijiji vinne vya Makuyuni wenye thamani ya zaidi ya sh, bilioni 7, Waziri Aweso amesisitiza miradi kukamilika kwa wakati.

Alisema baadhi ya wakandarasi na  wataalamu wa maji wanakuwa ni kikwazo katika kukwamisha miradi ya maji hivyo alitoa rai kuhakikisha miradi ya maji haikwami ili kuwaondolea kero za maji  wananchi .

" Mimi Aweso sitakuwa kikwazo cha kukwamisha miradi ya maji kwa wananchi na nyie wataalamu wa maji hakikisheni maji yanawafikia wananchi kwa wakati"

Awali akizungumzia mradi huo ,Meneja wa Wakala wa Maji  na Usafi wa Mazingira Vijijini (Ruwasa)Mkoa wa Arusha, Joseph Makaidi  alisema mradi huo utatekelezwa kwa muda wa miaka miwili katika vijiji 19 ambapo utekelezaji wa mradi huo utabakiza vijiji sita ambavyo navyo vitapata  na vijiji 13 ndio vitaanza kutekelezwa katika mradi huo .

"Mradi huu utapunguza kero ya maji katika wilaya hii na sisi Ruwasa tutasimamia vema ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya maji"

Huku mmoja kati ya wananchi wanaoishi wilayani hapo,Jane Lowassa alishukuru mikataba hiyo kusainiwa kwani itaondoa kero ya maji wilayani hapo kwasababu awali walikuwa wakitumia maji ya bwawa ambayo si salama sana

Huku mbunge wa jimbo hilo ,Fredrick Lowassa na Mkuu wa wilaya  hiyo Joshua Nassari wakishukuru kusainiwa kwa mkataba huo ambao unatatua kero za maji kwa wananchi na kumshukuru Rais Samia Hassan Suluhu kwa kutatua kero ya maji kwa wananchi hao.

Ikumbukwe mwishoni mwa mwaka jana mtandao wetu uliripoti habari ya kukosekana kwa maji katika shule ya sekondari Nanja pampoja na vijiji vya jirani vunavyozunguka Kata hiyo.

unaweza kutazama makala yetu ya awali juu ya upatikanaji wa maji katika eneo la Nanja kwa kubonyeza hapa BONYEZA HAPA








Share To:

Post A Comment: