MCHIMBAJI na mnunuzi wa dhahabu mkazi wa Chunya mkoani Mbeya, Ezekia Luhwesha (31)anasbikiliwa na Jeshi la Polisi mkoani hapa akidaiwa kumuua kwa kumpiga risasi wakala wa maegesho ya magari aitwaye William Mgaya (58)mkazi wa John mkoani hapa.

Kamanda wa Polisi mkoani Mbeya, Benjamin Kuzaga amesema kuwa tukio hilo limetokea November 26 mwaka huu majira ya saa 4.30 asubuhi katika maeneo ya Mafiati ofisi za TARURA katika jengo la Tafisa lililopo kata ya Ruanda Jijini Mbeya.

Kamanda Kuzaga amesema kuwa Marehemu William Mgaya akiwa na mwenzake aitwaye Almas Shaban (32)ambao wote ni mawakala wa maegesho ya magari ya Halmashauri ya Jiji la Mbeya wakiwa katika kazi yao ya kukusanya ushuru unaotokana na kuegesha vyombo vya moto walimkamata Mtuhumiwa Ezekia luhwesha baada ya ya kuscan Namba yake ya gari T. 772 DVY Toyota Hilux na kugundua kuwa gari hilo lina deni la shs 7,500.

Amesema kuwa Mtuhumiwa alitakiwa kulipa deni hilo lakini alihitaji kuona hilo deni linatokana na maegesho gani hivyo kulazimika kuongozana naye hadi zilipo ofisi za TARURA kwa ajili kuangalia kwenye mfumo ili kupata taarifa za deni hilo.

Mtuhumiwa alionyeshwa taarifa za deni hilo na kuridhika kuahidi kulipa deni hilo lakini wakala mgaya alimtaka kulipa deni hilo papo hapo kutokana na deni hilo kuwa la muda mrefu ndipo yalitokea majibizano kati ya marehemu na mtuhumiwa hali iliyopelekea mtuhumiwa kutoa silaha yake Pistol na kufyatua risasi moja uelekeo alipokuwa marehemu na kumpiga sehemu ya kifuani upande wa kulia na kusababisha kifo chake muda mfupi baada ya kufikishwa Hospitali ya Rufaa Mbeya kwa matibabu.

Aidha amesema mtuhumiwa pamoja na Silaha Pistol aina ya Tisasi yenye namba T.0620-19J0037 ya mtuhumiwa ikiwa na risasi 09 ndani ya magazine anashikiliwa na Jeshi la Polisi.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya Kamishna Msaidizi wa Polisi Benjamin Kuzaga ACP ametoa rai kwa wananchi kuacha tabia ya kujichukulia sheria mkononi na badala yake watoe taarifa za malalamiko yao au kitendo chochote wanachofanyiwa kinyume cha sheria au taratibu zilizopo kwa viongozi wa mamlaka husika kwa ajili ya ufuatiliaji na hatua zaidi za kisheria.

Aidha Kamanda Kuzaga ametoa wito kwa wale wote wanaomiliki silaha kuzingatia masharti ya umilikishwaji wa silaha hizo pamoja na kuhakikisha silaha hizo wanazitumia kulingana na hitaji/mahitaji ya msingi waliyoombea silaha hizo na sio kutishia ama kuua watu jambo ambalo ni kinyume cha sheria za nchi na masharti ya umiliki wa silaha.

Share To:

Post A Comment: