Mkuu wa Mkoa wa Geita Mhe.Rosemary Senyamule akifungua mafunzo kwa Wajasiriamali-Wachakataji wa Mbegu za Mafuta ya Alizeti mkoani Geita ambapo Mafunzo hayo hutolewa na TBS. Baadhi ya Wajasiriamali-Wachakataji wa Mbegu za Mafuta ya Alizeti mkoani Geita wakiwa kwenye mafunzo ambayo yanatolewa na Shirika la Viwango Tanzania (TBS).

*************************

NA MWANDISHI WETU

SHIRIKA la Viwango Tanzania (TBS) limetoa Mafunzo kwa wasindikaji wa mbegu za mafuta ya alizeti wasiopungua 40, ambao tayari wanafanya shughuli ya usindikaji na ufungashaji na kwamba tayari bidhaa zao zipo kwenye soko ila hazijathibitishwa ubora na TBS.

Akizungumza wakati akifungua mafunzo hayo leo Juni 02,2022 mkoani Geita, Mkuu wa Mkoa wa Geita Mhe.Rosemary Senyamule amesema kuwa Mkoa wa Geita ni moja ya Mkoa ambao unakua katika sekta ya kilimo na biashara na kwa hivyo basi usindikaji wa mbegu za mafuta ya alizeti ni sehemu ya shughuli kuu za uzalishaji kwa wajasiriamali na wafanyabiashara wakubwa na wadogo kwenye Mkoa huo.

Amesema azma ya Serikali ni kuhakikisha kuwa nchi yetu tunajitosheleza katika uzalishaji wa mafuta ya kula ili kupunguza matumizi makubwa ya fedha za kigeni kuagiza mafuta kutoka nje.

"Takwimu za hivi karibuni zinaonesha kwamba, mahitaji yetu halisi ya mafuta ya kula kwa mwaka ni takribani tani 570,000, ukilinganisha na uzalishaji wa ndani wa tani 205,000 tunakuwa na upungufu wa tani 365,000 (TARI 2020) ambazo serikali inalazimika kuagiza kutoka nje ya nchi ili kufidia pengo hilo". Amesema RC Senyamule

Aidha amesema tuwe na uelewa wa pamoja kwamba, kujitosheleza huko ni pamoja na kwenda sambamba na uzalishaji wa mafuta yanayozingatia viwango, ubora na usalama ili kulinda afya ya mlaji.

Share To:

emmanuel mbatilo

Post A Comment: