Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Kimataifa ya Viongozi Wanawake (WPL) Mhe. Neema Lugangira ameendelea kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia inayolenga kulinda afya na kutunza mazingira miongoni mwa Watanzania.

Lugangira ameyasema hayo wakati akikabidhi mitungi ya gesi katika makundi mbalimbali wakiwemo Viongozi wa chama cha bodaboda,madereva taxi sambamba na vijana waliojiari katika migahawa (wauzachipsi) katika Manispaa ya Bukoba.

“Moja ya changamoto zinazoleta athari ya afya na kusababisha vifo kwa akina mama ni matumizi ya nishati isiyo safi mfano kuni na mkaa ambavyo vinatoa hewa isiyofaa naakina mama wa Tanzaniawamekuwa wakiathirika kwa kuvuta hewa hiyo lakini pia ukataji miti unaharibu mazingira yetu,” amesema Lugangira

Kwa upande wake Danstan ambaye ni mwakilishi wa kundi la vijana waliojiajiri katika migahawa amempongeza Neema Lugangira kwa kuwakumbuka na kuwapatia nishati safi ya kupikia.

"Tunamshukuru sana Lugangira kwa kutuletea mitungi hii ambayo ni rafiki kwa mazingira, sasa tutapika kwa wakati mfupi,tunakushukuru kwa kuwajali wananchi wa Bukoba kwa sasa tunakwenda kutumia mitungi ya kisasa" Amesema Danstan

Hata hivyo wananchi wa Bukoba wamempongeza Neema Lugangira kwa kuaminiwa na kuteuliwa kuwa Katibu Mkuu wa WPL kwani alifanya kazi nzuri sana wakati akiwa Mbunge aliyewakilisha Kundi la NGO’s kwa kuwa kinara katika kuchangia maendeleo katika jamii.















 Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Deus Sangu, amekutana na kufanya mazungumzo na ujumbe kutoka Japan kuhusu kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na Japan katika maendeleo ya rasilimali watu hususan kwenye sekta ya ujenzi.


Katika mazungumzo hayo, pande zote mbili zimejadili fursa za kuboresha ujuzi wa wataalam wa sekta ya ujenzi kupitia mafunzo, kubadilishana uzoefu na programu maalumu za kukuza uwezo. 

Aidha, Ujumbe wa Japan umeonesha utayari wa kuendelea kushirikiana na Serikali ya Tanzania katika kuhakikisha nguvu kazi ya Kitanzania inakuwa na weledi unaokidhi mahitaji ya soko la kimataifa.


Mazungumzo hayo yamefanyika leo Novemba 24, 2025 Jijini Dar es salaam ambapo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Mohmoud Thabit na Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano Bi. Zuhura Yunus wamehudhuria mazungumzo hayo.





 


Magesa Magesa ,Arusha .

WIZARA  ya maji imesema kwamba itahakikisha idadi kubwa ya watanzania walioko mjini na vijijini wanapata maji safi salama na ya uhakika .

Waziri wa maji Jumaa Aweso ameyasema hayo leo jijini Arusha wakati akifungua kongamano la maji la mwaka 2025 lililoandaliwa na Taasisi ya huduma za maji (ATAWAS )  linaloendelea mjini hapa .

Aweso amesema kuwa, amewataka watwndaji na watumishi wote wa sekta ya maji nchini kuhakikisha kuwa wanafanya kazi kwa bidii na kujituma ili kuondoa  changamoto ya upatikanaji wa maji kwa watanzania hususani maeneo ya vijijini.

"Katika kongamano hili nataka mhakikishe mnaweka mikakati kwa kushirikisha sekta binafsi na za umma ili kupunguza mbalimbali zinazoikabili sekta ya maji hapa nchini "amesema Aweso.

Amesema kuwa, katika utendaji kazi wao hawawezi kufanya kazi wenyewe bali ni lazima washirikiane na sekta binafsi katika kuweka mikakati madhubuti  namna ya utendaji kazi wao na hatimaye kwa pamoja kuweza kufikia malengo yaliyowekwa .

 Akimkaribisha Waziri wa maji ,Katibu mkuu wa wizara hiyo Mwajuma Waziri amewataka watumishi wa wizara hiyo kuhakikisha kuwa wanasimamia kikamilifu mikakati na mipango iliyowekwa na wizara hiyo ya kuhakikisha wananchi wote wanapata huduma ya maji safi na salama .

"Dira ya Taifa ya mwaka 2025 inasema kwamba ifikapo mwaka 2050 nchi yetu iwe na uhakika wa upatikanaji wa maji safi na salama kwa asilimia mia moja ,hivyo ni jukumu la kila mmoja kuhakikisha anawajibika kikamilifu katika eneo lake."amesema .

Kadhalika amewataka wataalamu kuhakikisha wanaweka mipango mikakati ikiwemo kutoa elimu ya uvunaji wa maji ya mvua kwa kutengeneza miundombinu ya kuhifadhia maji hayo hali itakayosaidia kutatua changamoto ya upungufu wa maji hususani katika taasisi mbalimbali za kiserikali ikiwemo mashule,mahospitali nk.

Mwenyekiti wa bodi ya ATAWAS, Geofrey Hilly amesema kuwa mkutano huu ni  mwendelezo wa mikutano yote ambayo wamekuwa wakifanya kila mwaka ambapo Atawas  inashirikisha watu wa sekta ya maji kwa ujumla wake.

Hilly amesema kuwa ,lengo la kukutana leo ni kuangalia namna gani sekta binafsi itashiriki katika kuhakikisha huduma za maji zinasambaa kwa kasi .

Ameongeza  kuwa ,Atawas ni taasisi ambazo karibu kila nchi inakuwa na taasisi kama hii ikiwemo Malawi,Kenya na dunia nzima  na kwamba mkutano huu umeshirikisha taasisi za serikali na binafsi zinazojishughulisha ja shughuli za utafutaji na usambazaji wa maji pamoja na vifaa vyake

Mwonekano wa jengo la mradi wa makazi ya Watumishi wa Umma lililopo katika Kijiji cha Makunda, Halmashauri ya Wilaya ya Iramba, mkoani Singida.

Kaimu Mkurugenzi wa Kitengo cha Ufuatiliaji na Tathmini, Ofisi ya Rais-UTUMISHI na Utawala Bora, Bw. Patrick Allute (aliyenyanyua mkono) akizungumza jambo wakati Timu ya wataalam kutoka Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Wizara ya Fedha na Watumishi Housing Investments ikikagua na kufanya tathmini ya mwisho ya kukamilika kwa mradi wa ujenzi wa makazi ya Watumishi wa Umma katika Kijiji cha Makunda, Halmashauri ya Wilaya ya Iramba, mkoani Singida. Wengine ni Watumishi wa Zahanati ya Makunda.

Katibu wa Afya, Halmashauri ya Wilaya ya Iramba, Bw. Sunday Mbonigaba (wakwanza kushoto) akifafanua jambo kwa Timu ya wataalam kutoka Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Wizara ya Fedha na Watumishi Housing Investments mara baada ya timu hiyo kukagua na kufanya tathmini ya mwisho ya kukamilika kwa mradi wa ujenzi wa makazi ya Watumishi wa Umma katika Halmashauri hiyo Kijiji cha Makunda mkoani Singida.

Kaimu Mkurugenzi wa Kitengo cha Ufuatiliaji na Tathmini, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bw. Patrick Allute (wanne kutoka kulia) akielekea kukagua na kufanya tathmini ya mwisho ya kukamilika kwa mradi wa ujenzi wa makazi ya Watumishi wa Umma katika Kijiji cha Makunda, Halmashauri ya Wilaya ya Iramba, mkoani Singida. Wengine ni Wakurugenzi na Maafisa kutoka Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Wizara ya Fedha na Watumishi Housing Investments.

Mwonekano wa jengo la mradi wa makazi ya Watumishi wa Umma lililopo katika Kijiji cha Maluga, Halmashauri ya Wilaya ya Iramba, mkoani Singida.

Kaimu Mkurugenzi wa Kitengo cha Ufuatiliaji na Tathmini, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bw. Patrick Allute (aliyenyoosha mkono) akisisitiza jambo mara baada ya kukagua na kufanya tathmini ya mwisho ya kukamilika kwa mradi wa ujenzi wa makazi ya Watumishi wa Umma katika Kijiji cha Maluga, Halmashauri ya Wilaya ya Iramba, mkoani Singida. Wengine ni Wakurugenzi na Maafisa kutoka Ofisi ya Rais-UTUMISHI, Wizara ya Fedha na Watumishi Housing Investments.

Timu ya wataalam kutoka Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Wizara ya Fedha na Watumishi Housing Investments ikitazama makazi ya Watumishi wa Umma katika Kijiji cha Maluga, Halmashauri ya Wilaya ya Iramba, wakati ikikagua na kufanya tathmini ya mwisho ya kukamilika kwa mradi wa ujenzi wa makazi ya Watumishi wa Umma mkoani Singida.

Kaimu Mkurugenzi wa Kitengo cha Ufuatiliaji na Tathmini, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bw. Patrick Allute (wakwanza kulia) akifurahia jambo na Mkurugenzi wa Fedha na Uwekezaji, Watumishi Housing Investments, Bw. Paskali Massawe (kulia kwake) mara baada ya kukagua na kufanya tathmini ya mwisho ya kukamilika kwa mradi wa ujenzi wa makazi ya Watumishi wa Umma katika Kijiji cha Maluga, Halmashauri ya Wilaya ya Iramba, mkoani Singida.

Na. Veronica Mwafisi-Singida

Timu ya wataalam kutoka Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Wizara ya Fedha na Watumishi Housing Investments ikiongozwa na Kaimu Mkurugenzi wa Kitengo cha Ufuatiliaji na Tathmini, Ofisi ya Rais-UTUMISHI na Utawala Bora, Bw. Patrick Allute imefanya ziara ya kikazi iliyolenga kukagua na kufanya tathmini ya mwisho ya kukamilika kwa mradi wa ujenzi wa makazi ya Watumishi wa Umma wa Shule ya Sekondari Maluga yanayojengwa katika Kijiji cha Maluga, Halmashauri ya Wilaya ya Iramba na Zahanati ya Makunda, Kijiji cha Makunda Halmashauri ya Wilaya ya Iramba, mkoani Singida ambapo kukamilika kwa mradi huo kutasaidia kuongeza tija Serikalini.

Akizungumza kwa niaba ya timu hiyo mara baada ya kukagua mradi huo, Kaimu Mkurugenzi Allute amesema, makazi ya watumishi wa umma yanapokuwa karibu na maeneo ya kazi huongeza ufanisi na uwajibikaji hivyo, utekelezaji wa mradi huo kwa awamu ya kwanza katika mikoa ya Dodoma, Singida, Lindi, Pwani na Ruvuma utamkomboa mtumishi wa umma katika utendaji kazi.

“Maeneo ya pembezoni yamekuwa na changamoto ya makazi na kusababisha baadhi ya watumishi wa umma kutokutekeleza majukumu yao kwa ufanisi, kupitia mradi huu unaotekelezwa kwa awamu ya kwanza katika mikoa ya Dodoma, Singida, Lindi, Pwani na Ruvuma unatarajiwa kuongeza ufanisi na uwajibikaji kwa watumishi wa umma kwenye maeneo hayo,” amesema Mkurugenzi Allute

Naye, Mkurugenzi Msaidizi Sehemu ya Mipango na Bajeti, Bi. Julieth Magambo amesema ili makazi hayo yawe na ubora wa kudumu ni vema Watumishi watakaoishi katika makazi hayo wakazingatia utunzaji wa miundombinu.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Fedha na Uwekezaji kutoka Watumishi Housing Investments, Bw. Paskali Massawe, amesema makazi hayo yamejengwa kwa kuzingatia ubora ili kuendana na malengo ya Serikali katika kuwatengenezea mazingira bora watumishi wa umma.

Kadhalika, Afisa Usimamizi wa Fedha kutoka Wizara ya fedha, Bw. Ezekiel Odipo ameeleza kuwa, ili kutimiza malengo ya Serikali ya kuongeza tija kwa watumishi wa umma fedha nyingi imetolewa kwa lengo la kuboresha makazi ya watumishi hao ili waweze kutoa huduma bora kwa ustawi wa taifa.


Kwa mujibu wa maelekezo ya Mtendaji Mkuu wa TANROADS, Mhandisi Mohamed Besta, kwa Mameneja wa Mikoa yote kuhakikisha barabara zinabaki salama na kupitika kipindi hiki cha mvua, TANROADS Mkoa wa Njombe imeongeza kasi ya usimamizi na matengenezo katika maeneo yaliyoathiriwa na mvua.

Barabara ya Itoni–Ludewa–Manda (km 211.4), hususan Sehemu ya Pili ya Itoni–Lusitu (km 50) inayojengwa kwa kiwango cha zege, imefanyiwa matengenezo ya haraka baada ya changamoto za mvua ili kuhakikisha watumiaji wanaendelea kusafiri kwa usalama na uhakika.

Kazi zinaendelea mchana na usiku, kuhakikisha magari yanapita bila kukwama na shughuli za kiuchumi zinaendelea vyema katika mkoa wa Njombe.

Kwa kushirikiana, TANROADS Makao Makuu, ofisi ya TANROADS Mkoa wa Njombe, pamoja na mkandarasi, wamehamia barabarani kuhakikisha kila eneo linalohitaji uingiliaji linafanyiwa kazi mara moja.

Ujumbe kwa wananchi:
Serikali kupitia TANROADS inaendelea kuhakikisha barabara zote zinapitika msimu mzima wa mvua ili kuimarisha usafiri, usafirishaji na uchumi wa wananchi.







 


Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, amesema kuwa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) limeendelea kufanya mageuzi makubwa katika kuboresha upatikanaji wa  huduma ya umeme nchini hatua ambayo imeongeza imani na fursa mbalimbali za kiuchumi kwa wananchi.

Mhe. Ndejembi ameyasema hayo Novemba 22, 2025, mkoani Dodoma katika kikao chake na viongozi wa TANESCO chenye lengo la kufanya tathmini na kukumbushana majukumu muhimu ya kuwahudumia wananchi. Ameutumia mkutano huo kuwataka watendaji wa TANESCO kuongeza kasi na ubunifu katika kuwaunganishia wananchi umeme kama sehemu ya utekelezaji wa Mpango Mkakati wa Misheni 300.

Amesema kuwa ili mpango huo utekelezeke ipasavyo, ni lazima kuwachukulia  hatuaza kisheria  wakandarasi wote watakaobainika kuwa wazembe au kushindwa kuendana na kasi ya serikali ya kuhakikisha kila Mtanzania ananufaika na huduma ya umeme.

“Nawapongeza TANESCO kwa kazi kubwa na nzuri ya kuwafikishia wananchi huduma ya umeme, lakini bado tuna kazi kubwa mbele yetu. Ongezeni ubunifu na mbinu bora za kuwaunganishia wananchi umeme kwa haraka. Ninaamini tukishirikiana na wadau wetu, tutafikia lengo la kuwaunganishia wateja milioni 1.7 kwa mwaka,” alisema Mhe. Ndejembi.

Naye Naibu Waziri wa Nishati Mhe. Salome Makamba amemshukuru Rais.  Dkt.  Samia Suluhu Hassan kwa kuwekeza katika miradi ya umeme ambayo imekuwa na dhamira ya dhati ya  kuhakikisha wananchi wote mijini na vijijini wanafikiwa na huduma ya umeme.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mhe. Felchesmi Mramba, amesema TANESCO imekuwa ikitekeleza miradi yake kwa viwango vya kimataifa, hatua inayofanya Tanzania kuwa kielelezo kwa mataifa mengine katika ujenzi na usimamizi wa miradi ya umeme.

Naye Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa TANESCO, Mhe. Balozi Zuhura Bundala, amesema  Shirika hilo lina watendaji wazalendo na wenye kujituma, ambao wanaendelea kufanya kazi kwa bidii  ambapo amesisitiza bodi hiyo itaendelea kushirikiana na Shirika ili kufikia malengo yaliyowekwa.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Bw. Lazaro Twange, amesema  katika kipindi cha siku 100 za utendaji wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, Shirika litakamilisha miradi ya umeme  kwa kasi zaidi, ukiwemo mradi wa kuzalisha umeme wa jua wa Kishapu ambao kwa sasa umefikia asilimia 83 ya utekelezaji.

“Katika kipindi cha siku 100 za Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, tumejipanga kuhakikisha baadhi ya miradi ya umeme inakamilika, ukiwemo mradi wa umeme wa jua wa Kishapu. Pia tunaendelea na mkakati wa kuwaunganishia wananchi umeme  lengo ni kuwafikia wateja milioni 1.7 kwa mwaka,” alieleza Bw. Twange.

Kikao kazi hicho  kimehusisha viongozi wa ngazi ya juu wa TANESCO, wakurugenzi wa kanda, mameneja wa mikoa na wilaya, na kilifunguliwa rasmi na Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius  Ndejembi ambaye aliambatana na Naibu waziri wa nishati Mhe. Salome Makamba