Waziri wa  Nishati Mhe. Deogratius Ndejembi  amewaagiza Watumishi wa Wizara hiyo kufanya kazi kwa bidii ili kutimiza Vipaumbele vya Serikali katika Sekta ya Nishati ikiwemo kufikia Megawati 8000 ifikapo 2030.

Mhe. Ndejembi ameyasema hayo tarehe 18 Novemba 2025 wakati akizungumza na watumishi wa Wizara mara baada ya kuwasili Katika Wizara  Mji  wa Serikali Mtumba Jijini Dodoma. 

Amesema watumishi wa Wizara ya Nishati ndio watendaji wakuu na wenye dhamana ya kuhakikisha kwamba malengo ya Serikali yaliyowekwa yanatimia kwa kufanya kazi kwa bidii , kuwataka watumishi kuchambua kwa kina  hotuba ya Mhe   Rais ili kuweza kufikia vipaumbele kwa wakati  na kuyoa huduma bora kwa wananchi wa Tanzania.

Pia amesisitiza watumishi kutumia siku mia moja za Mhe. Rais kama kipimo na  kielelezo cha kutathmini uelekeo wa malengo ya Serikali.

“Sisi kama viongozi wenu tunategemea zaidi ushirikano kutoka kwenu ninyi wataalamu wa hapa Wizara ya Nishati  ili tuweze kukamilisha Vipaumbele vya Mhe. Rais alivyoviweka katika sekta yetu  kwasababu tunatakiwa tuanze kwa kukimbia na sio kutembea“ amesema Mhe. Ndejembi.

Nae Naibu Waziri wa  Nishati Mhe. Salome Makamba amewataka watumishi kushirikiana kwa pamoja na viongozi wa Wizara hiyo ili kuendesha Sekta ya Nishati kwa pamoja, na kuongeza kuwa anatambua kwamba maswala mengi ya sekta ya Nishati yameshafanyika tayari mpaka sasa.

Amesema  Serikali imeshafikisha Megawat 4000 za kiwango cha kuzalisha Umeme, hivyo ni jukumu letu kukamilisha miradi iliyokuwa inaendelea na kuongeza vyanzo vingine vya uzalishaji umeme ili kufikia megawati 8,000 ifikapo 2030.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati Mha. Felchesmi Mramba amewashukuru viongozi hao na amewataka watumishi wa Wizara ya Nishati kutoa ushirikiano kwa viongozi hao sambamba na kutekeleza majukumu yao kwa wakati ili kuweza kutekeleza Vipaumbele vya Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan ifikapo mwaka 2030.












 


Waziri wa Madini Anthony Mavunde amewataka Watumishi wa Wizara ya Madini  na Taasisi zake kutambua kwamba maelekezo yaliyotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Hassan kuhusu kutumia fedha za ndani zinazotokana  na rasilimali kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maendeleo  ni agizo  linaloigusa  Wizara ya Madini moja kwa moja.

Ameyasema hayo Novemba 18, 2025 wakati akizungumza na Watumishi wa Wizara ya madini na taasisi zake Makao Makuu ya Wizara Mtumba, mapema baada ya kuapishwa Ikulu ya Chamwino Dodoma na Rais  Dkt. Samia Hassan.

‘’Mapato ya ndani aliyoyaelekeza Mhe.  Rais yanatugusa sisi Sekta ya Madini moja kwa moja. Dkt. Samia anataka uongozi unaogusa watu hivyo tuendelee kuongeza kasi. Lakini Katibu Mkuu nitapenda maelekezo aliyoyasema wakati akihutubia Bunge, haya ya leo na yale yaliyoahidiwa kwenye Ilani ya Uchaguzi yamfikie kila mtumishi,’’ amesisitiza Mavunde.

Mhe. Mavunde ameeleza kuwa Rais. Dkt.Samia Suluhu Hassan amekuwa na imani kubwa na Wizara ya Madini hususan kutokana na mapato yanayotokana na  rasilimali madini kuendesha uchumi wa nchi  na hivyo kumtaka kila mtumishi kutumia nafasi yake kuhakikisha sekta ya madini inagusa maisha ya kila mwananchi kwa manufaa ya jamii na taifa.

Akielezea kuhusu programu ya Mining for A Brighter Tommorrow (MBT), Mhe. Mavunde amesema kuwa mradi huo utatekelezwa kikamilifu kama ulivyopangwa kwa lengo la kuwawezesha wachimbaji vijana na wanawake kuchimba kwa tija. Kupitia mradi wa MBT Wizara imepanga kuwawezesha vijana na wanawake kwa kuwapatia maeneo ya kuchimba na teknolojia ili kuwarahisishia shughuli zao.

Pia, ametumia fursa hiyo kumshukuru Dkt. Samia kwa kumuamini na kumrejesha tena kuitumika wizara hiyo pamoja na kuwashukuru watumishi wote na wadau wote wa Sekta ya madini  kwa ushirikiano mkubwa waliompatia katika kipindi cha miaka miwili aliyohudumu katika wizara hiyo na kueleza kwamba, kwake mlango uko wazi kwa  ajili ya kupokea maoni na mapendekezo yanayojenga kwa lengo la kuendelea kuboresha Sekta ya Madini.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Madini Dkt. Steven Kiruswa Dkt. Kiruswa ameshukuru Rais Samia kwa kumuamini kuendelea kuhudumu katika Wizara ya Madini na kuwashukuru watendaji wote kwa ushirikiano waliompatia na kuwapongeza watumishi kwa kazi wanayofanya hususan kuendelea na ukusanyaji wa maduhuli ya Serikali.

‘’Mhe. Rais ametoa mwelekeo, hivyo tunapaswa  kutekeleza yale  tuliyoagizwa,  tuliwaacha na mchango wa asilimia 10.1 matamanio ni kufikia  asilimia 15 – 20  ifikapo mwaka 2030’’ amesema Dkt. Kiruswa.

Naye, Katibu Mkuu Wizara ya Madini Eng. Yahya Samamba amewapongeza viongozi hao kwa kuchaguliwa tena katika Wizara ya Madini na kuahidi kuendelea kuwapa ushirikiano wa utendaji kazi  kuanzia ngazi ya chini mpaka juu.

Pamoja na mambo Kamishna wa Madini Dkt.AbdulRahman Mwanga kwa pamoja  amewapongeza  hao  kwa kuchaguliwa tena na kuahidi  ushirikiano

*#Vision 2030: Madini ni Maisha na Utajiri*

 


Na WAF, Dodoma

Waziri wa Afya, Mhe. Mohamed Mchengerwa, amewataka watendaji wa Wizara ya Afya kufanya kazi kwa bidii, weledi na uadilifu  na kuacha kufanya kazi kwa mazoea ili kuleta tija na ufanisi kwa wananchi.

Mhe. Mchengerwa ametoa wito huo leo, Novemba 18, 2025, alipokutana na Menejimenti ya Wizara mara baada ya kuwasili rasmi kuanza majukumu yake mapya ya kazi kwenye wizara hiyo.

Amesema huu ni wakati wa watumishi kuongeza juhudi na kuto bweteka, ili kuendelea kusukuma maendeleo ya Sekta ya  Afya mbele.

“Nawasisitiza watumishi wote kuacha kufanya kazi kwa mazoea Tubadilike na kutekeleza majukumu kwa ufanisi ili kuhakikisha Taifa letu linasonga mbele katika Sekta ya Afya,” amesema Mhe. Mchengerwa.

Aidha, Waziri Mchengerwa amewataka watumishi wote kufuata maadili ya kazi na kusimamia kwa umakini maelekezo yanayotolewa, ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora za afya.







Wajumbe wa Kamati Kuu ya Kitaifa ya Tuzo za Uhifadhi na Utalii 2025 wakiongozwa na Mkurugenzi Msaidizi Utalii Richie Wandwi wameendelea na zoezi la uhamasishaji na utoaji elimu kwa wadau wa utalii na uhifadhi juu ya tuzo za Serengeti zinazotarajiwa kufanyika mwezi Desemba 2025.

Zoezi hilo linalolenga kuwajengea uelewa wadau juu mambo muhimu ikiwemo, kategoria za tuzo na namna ya kujisajili na kuwa mshiriki wa tuzo hizo limefanyika Jumatatu Novemba 17 Jijini Arusha kwa Kanda ya Kaskazini.










 


Na: OWM (KVAU) – Nairobi

Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeibuka mshindi wa jumla kwenye maonesho ya 25 ya Wajasiliamali Wadogo na wa Kati wa Jumuiya ya Afrika Mashariki baada ya kampuni ya utengenezaji magari ya KAYPEE Motors kushinda kipengele cha mjasiliamali bora wa Afrika Mashariki (Best Exhibitor - EAC) mwenye uwezo wa kutunza mazingira.

Mjasiriamali huyo kutoka kampuni ya KAYPEE Motors inayojishughulisha na ubunifu na uzalishaji wa magari yanayoendeshwa kwa kutumia nishati ya safi ya umeme ambapo imetambuliwa kwenye kundi maalum la wajasiliamali wanaotunza hifadhi ya mazingira.

Tuzo hiyo imetolewa katika Maonesho ya Wajasiliamali maarufu Jua kali ambayo yamehitimishwa tarehe 16 Novemba 2025 katika viwanja vya Uhuru Gardens jijini Nairobi, nchini Kenya ambapo tarehe hiyo ilikuwa pia ni siku maalumu ya Tanzania katika maonesho hayo yalioshirikisha zaidi wajasiliamali zaidi ya 3000 toka nchi nane zinazounda Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Akifunga maonesho haya Waziri wa Viwanda na Biashara wa Kenya, Mhe. Wycliffe Oparanya alisema maonesho haya yamefanyika kwa mafanikio makubwa ikiwa ni miaka 25 tangu yalipoasisiwa mwaka 1999 na kwamba yanasaidia kujenga mshikamano baina ya nchi wanachama.

Waziri huyo alitoa wito kwa nchi wanachama uongeza bajeti za kusaidia shughuli za wajasiliamali ili wabuni na kuzalisha bidhaa bora zinazokidhi mahitaji ya soko la Afrika Mashari na dunia kote na kwamba Serikali zote zinahimizwa kutafuta suluhu ya kuondoa vikwazo vya kibiashara.

Vile vile alisisitiza kuhusu umuhimu wa matumizi ya teknolojia ya habari na mawasiliano, Waziri huyo aliwasihi wajasiliamali kutumia mifumo ya kidijitali kukuza biashara zao na kuongeza masoko nje ya mipaka yao.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki anayeshughulikia masuala ya Fedha na Biashara, Annette Mutaawe aliwapongeza wanachama wote kwa kujitokeza kwa wingi kwenye maonesho ya mwaka huu ambapo alitaja nchi wananchama kuwa ni kutoka Kenya, Uganda, Tanzania, Sudan Kusini, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Rwanda, Burundi na Somalia.

Awali Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Vijana,Ajira na Wenye Ulemavu Zuhura Yunus aliyeongoza ujumbe wa Tanzania nchini Kenya alisema Serikali ya Awamu ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan itaendelea kuwaratibu na kuwasaidia wajasiliamali ili waongeze tija na ubora wa bidhaa.

Kwa upande wake, Balozi wa Tanzania nchini Kenya Dkt. Bernard Kibesse akizungumza wakati wa hafla hiyo amewapongeza wajasiriamali wa Tanzania kwa kujitokeza kwa wingi katika maonesho hayo.

Akizungumzia ushindi huo mjasiriamali kutoka kampuni ya KAYPEE Motors, Mkurugenzi wa Uzalishaji, Bw. Rajab Hassan alisema ushindi waliopata umetokana na uzalishaji wa bidhaa bora ambapo mwaka huu ni wa kumi tangu walipoanza uzalishaji wa magari hayo na kwamba ushindi huu ni wa wajasiliamali wote wa Tanzania.

Hassan aliongeza kusema miongoni mwa mafanikio waliyoyapata hadi sasa kwenye maonesho ya mwaka huu ni kupata oda ya magari nane  ahadi ya Rais William Ruto wa Kenya aliyagiza magari mawili na mengine sita ni oda toka wananchi wa Kenya.

Katika maonesho ya mwaka huu Tanzania iliwakilishwa na wajasiliamali 375 waliotoka Tanzania Bara na Zanzibar ambapo serikali imeratibu ushiriki wa Wajasiliamali.

 


Na Oscar Assenga, PANGANI.

MJUMBE wa Kamati Kuu ya CCM Taifa Rajab Abdurhaman amekabidhi kiasi cha Milioni 13.4 kwa vijana wa Kikundi cha Bodaboda cha Hatupoi Group chenye maskani yao Kivukoni wilayani Pangani ikiwa ni hatua ya kuunga mkono hotuba ya Rais Dkt Samia Suluhu kwa vitendo kuwakwamua kiuchumi.


Akizungumza wakati akikabidhi hundi ya fedha hizo kwa Mwenyekiti wa Bodaboda wilaya ya Pangani alisema kwamba ameamua kuwaunga mkono kuwalipia deni la mkopo la Milioni 13.4 ambalo walipaswa kulilipa katika marejesho yao yaliyobakia baada ya kupata mkopo wa asilimia 10 kutoka Halmashauri.

Alisema kwamba wamekwenda kumuunga mkono Rais Dkt Samia Suluhu na kumshukuru kwa vitendo kwa hotuba yake aliyoitoa wakati anazindua Bunge la aliongeza mambo mengi kwa mustakabali wa mzima wa maendeleo ya Tanzania.

“Kwa niaba ya wana CCM na Wananchi mkoa wa Tanga nichukue nafasi hii kumpongeza Rais Samia kwa hotuba yake iliyosheheni mwelekezo mpya wa Taifa la wakati akizundua Bunge la 13 kama alivyosema hotuba hiyo ilishehena mambo mengi amezungumzia amani,umoja wa kitaifa wa nchi na maridhiano katika nchi yetu ili amani iendelee kuwepo ”Alisema



Rajabu ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Tanga alisema kwamba kiongozi huyo mkuu wa nchi amezungumzia mambo mengi na kila mtanzania na mwana Tanga ameisikia na amefarijika na kufurahisha wa hotuba hiyo.


Aidha alisema kwamba wao watu wa Tanga wanampongeza na kumshuruku kama alivyosema kwenye hotuba kuna mambo mengi na moja wapo ambalo mkuu huyo wa nchi amezungumzia ni suala la kuwanyanyua kiuchumi vijana na wakina mama katika Taifa hili.

“Lakini akaenda mbali zaidi kusema ataunda wizara maalumu itakayohusiana na vijana na wanaposema vijana wapo vijana wa kiume na wakike tunampongeza kwa kiliona hilo tunaamini kupitia wizara hiyo atakayoiunda changamto za vijana zinazowakabili zitapatiwa majawabu kwa wakati”Alisema

Aliongeza kwamba wanamatumaini makubwa kwamba changamoto za vijana kwenye ajira serikalini na ajira za kujiajiri wenyewe na ajira za sekta binafasi zinakwenda kupatiwa majawapo kwa kwa muda mfupi.

Rajabu alisema kwamba ameamua kuwaunga mkono kama walivyosema walichukua mkopo halmashauri kwa mujibu wa mkataba miezi 16 mwaka mmoja na miezi minne na wanatakiwa kila tarahe 16 kila mwezi wawe wanarudisha kila walichoelekezwa na wameshalipa miezi 8 hivyo wamekwenda kuunga mkono hotuba ya rais kuhusu vijana na uchumi kwa vitendo

Akisoma Risala ya Kikundi cha Hatupoi Bodaboda Group alisema kwamba kilianzishwa mwaka 2020 wakiwa na wanachama na wanachama 10 na walipata cheti cha utambuzi kutoka wilaya ya Pangani .

Alisema baada ya kupata cheti hicho waliomba mkopo halmashauri kutoka fedha za asilimia 10 na hivyo kuweza kukopeshwa kiasi cha milioni 27,592,000 kwa ajili ya kununua pikipiki kwa ajili ya kuendesha mradi wa bodaboda.

Alieleza baada ya kupokea mkopo huo walikuwa wakirejesha kwa miezi 16 na ukomo wake ukiwa ni mwakani 2026 na kila mwezi rejesho ni 1,724,500 ambapo kupitia fedha hizo waliweza walinunua pikipiki 8 na mafuta ya kuanzia kazi na nauli za wajumbe kwenda kununua .



Hata hivyo alieleza baada ya kuanza kazi kwa muda wa miezi nane walifanikiwa kurejesha Milioni 14,152,000 na kubaki deni la Milioni 13,540,000 huku akieleza mafanikio mbalimbali walioyapata ikiwemo kutoa ajira za vijana 8,usimamizi wa fedha na kufanikiwa kurejesha fedha hizo .

“Tunamshukuru Rais Dkt Samia Suluhu katika hotuba yake ya kulizundua Bunge baada ya kueleza kutakuwa na idara itakayosimamia vijana hivyo itawasaidia sana hivyo tunampongeza”Alisema





Kwa upande wake Mkuu wa dara ya Maendeleo ya Jamii Pangani Sekela Mwalukasa alisema kwamba wanajivunia uwepo wa kikundi hicho ambacho kimekuwa cha mfano huku akieleza Serikali ni sikivu imeweza kuja na mkakati wa kuwatoa vijana ili waweze kujikwamua kichumi kwa kutoa mikopo hiyo ya asilimia 10 ambayo haina riba inayotolewa kwa vijana na watu wenye ulemavu.



Hata hivyo Mwenyekiti wa Bodaboda Mkoa wa Tanga Mohamed Chande alimpongeza Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Rajabu Abdurhamn kwa juhudi kubwa na Serikali ya Rais Dkt Samia Suluhu kwa kazi nzuri ya kutenga wizara ya vijana na fedha zinazotoka za mikopo sio za bure lazima zirejeshwe na vijana wapo tayari na kumpongeza mwenyekiti wa Bodaboda kwa kusimamia wilaya yake vizuri.

Mwisho.

 

AIRTEL Africa inaendelea kuandika historia katika ukuaji wa sekta ya mawasiliano barani Afrika, Matokeo yake ya nusu mwaka yanaonyesha namna Airtel ilivyopiga hatua kubwa. Kwa miezi sita iliyomalizika tarehe 30 Septemba 2025, kampuni ya mawasiliano na huduma za fedha kwa njia ya simu, Airtel imerekodi ongezeko kubwa la mapato, wateja, na matumizi ya huduma za kidijitali ikiakisi dhamira yake ya kuwaunganisha watu na kupanua ujumuishaji wa kifedha barani.

Airtel inafanya biashra katiak nchi 14, ambapo mapato ya Airtel Africa yaliongezeka kwa 24.5% na kufikia dola bilioni 2.98. Ongezeko hili limetokana kuongezeka kwa na matumizi ya huduma za data, pesa kwa njia ya mtandano yaani Airtel Money, na huduma za sauti. Kwa mara ya kwanza, data imekuwa chanzo kikubwa cha mapato, ikikua kwa 37%. Airtel Money pia imeongezeka kwa 30%, ikionyesha jinsi watu wengi sasa wanatumia simu kufanya miamala ya kifedha.

Idadi ya wateja wa Airtel Africa imefikia takribani milioni 174, ikiwa ni ongezeko la 11%. Wateja wa data wameongezeka kwa 20% hadi milioni 69.5, na watumiaji wa Airtel Money sasa ni milioni 49.8. Hii ni kutokana na kuongezeka kwa matumizi ya simu janja, ambayo sasa yanafikia 46.8%, ikichochewa na mipango ya Airtel kusaidia watu kumiliki simu janja kwa njia ya mkopo na kuendelea kulipa kidogo kidogo. kupitia

Airtel Africa inaendelea kupanua mtandao wake. Katika kipindi hiki, imeshaongeza minara mipya zaidi ya 2,350 na kuongeza kilomita 4,000 za nyaya za fibre. Hii imeiwezesha mtandao wake kuwafikia watu kwa 81.5% katika masoko yake, huku 98.5% ya minara yake ikiwa ina teknolojia ya kisasa ya 4G. Kampuni pia inatazama uwezekano wa kuleta 5G katika maeneo yenye mahitaji makubwa ya data.

Kwa upande wa uendeshaji, kampuni inaendelea kufanya vizuri. Faida kabla ya makato (EBITDA) imeongezeka kwa 33.2% hadi dola bilioni 1.45, na faida baada ya kodi imepanda hadi dola milioni 376, kutoka milioni 79 mwaka uliopita. Hii inaonyesha usimamizi bora wa gharama na faida zilizopatikana baada ya kufanya marekebisho ya madeni.

Airtel Money imeendelea kuwa huduma muhimu sana kwa kampuni na kwa watumiaji. Katika kipindi hiki, huduma hiyo imepitisha miamala yenye thamani ya dola bilioni 193, ongezeko la karibu 36% ikilinganishwa na mwaka uliopita. Kwa watu wengi barani Afrika, Airtel Money imekuwa njia rahisi na salama ya kutuma na kupokea pesa, kufanya malipo, kuweka akiba na hata kupata mikopo isiyoukuwa na masharti.

Mkurugenzi Mtendaji wa Airtel Africa, Sunil Taldar, anasema matokeo haya yanaonyesha matarajio makubwa ya soko la Afrika. “Ukuaji tunaouona katika matumizi ya data na simu janja pamoja na Airtel Money unaonyesha jinsi Afrika ina fursa kubwa ya kukua kidijitali,” alisema. “Tutaendelea kuboresha huduma, kuwekeza katika mtandao na kuhakikisha wateja wanapata huduma zinazokidhi mahitaji yao .”

Mafanikio ya Airtel Africa pia yanaonyesha mabadiliko mapya katika sekta ya mawasiliano. Watu wanahamia zaidi kwenye huduma za kidijitali kuliko simu za sauti pekee. Data sasa inatumika kufanya biashara, kwenye utoaji wa elimu kwa mtandao , na kuboresha maisha ya kila siku.

Airtel Africa imeongeza bajeti ya uwekezaji hadi dola milioni 900 kwa mwaka mzima. Kampuni pia inaendelea kutoa mgao na kununua baadhi ya hisa zake kama njia ya kuwapa thamani zaidi wawekezaji.

Kwa ujumla, matokeo haya ya nusu mwaka yanaonyesha jinsi Airtel Africa ilivyo sehemu muhimu ya safari ya Afrika ya kuwa bara lililounganishwa zaidi. Kila simu janja inayotumika, kila kifurushi cha data, na kila muamala wa Airtel Money ni hatua moja kuelekea mustakabali bora kwa watu wa Afrika.