Na Munir Shemweta, WANMM ARUSHA

 

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo amewasisitiza wananchi wenye maeneo ya ardhi, kuhakikisha wanayaendeleza kabla serikali haijaanza kuchukua hatua.

 

Dkt. Akwilapo ametoa kauli hiyo leo tarehe 11 Februari 2026 wakati akifungua Kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) kinachoendelea jijini Arusha.

 

Akwilapo amesema kumekuwa na tabia kwa baadhi ya wananchi kununua maeneo ya ardhi na kuyahifadhi kwa muda mrefu kama mtaji kwa lengo la kupata faida baadaye.

 

"Bado natafakari  nifanye nini maana sheria ipo, usipoendeleza eneo lako ndani ya miaka mitatu unaweza kunyang'anywa na wengi wanafanya ardhi kama mtaji. Nadhani kuna taasisi maalum za kukuza mitaji, kama vile Soko la Hisa la Dar es Salaa na UTT-AMIS, tumieni hizo taasisi. Huku ardhi tutapishana maneno". Amesema Dkt Akwilapo.

 

Sheria ya Ardhi Sura Namba 113 kifungu cha 49 inaeleza wazi kuwa mmiliki wa ardhi asiyeendeleza eneo lake katika kipindi cha miaka mitatu serikali inaweza kulichukua eneo lake kutokana na kushindwa kuliendeleza.

 

Kupitia kikao hicho cha Baraza la wafanyakazi, Mhe. Dkt Akwilapo amewataka waendelezaji milki nchini  likiwemo Shirika la Nyumba la Taifa, kuhakikisha wananchi wanapata nyumba bora na za gharama nafuu ili watanzania waweze kuwa na tabasamu.

 

Amewaasa watumishi wa NHC kuzingatia utu, maadili, uwazi na uaminifu wakati wote wa kutekeleza majukumu yao huku wakiachana na ile dhana ya kuuliza watapata kitu gani ndani ya shirika na badala yake wajiulize watalifanyia nini shirika hilo.

 

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Baraza la wafanyakazi la NHC ambaye pia ndiye Mkurugenzi Mkuu wa Shirika hilo, Bw. Hamad Abdallah amesema shirika lake limekuwa likifanya jitihada mbalimbali za kuhakikisha linaboresha maslahi ya watumishi. 

 

Kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi cha Shirika la Nyumba la Taifa kilichoanza leo tarehe 11 Februari 2026 kinatarajiwa kuhitimishwa Alhamisi tarehe 12 Februari 2026. Kikao hicho pamoja na mambo mengine kinajadili Mizania na Bajeti ya NHC kwa mwaka wa fedha 2026/2027.










Katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha, Dk. Toba Alnason Nguvila, amewasistiza watumishi wa Umma kufanya kazi kwa kufuata Sheria, taratibu na kanuni kwa kuzingatia kiwango cha juu cha Maadili ya Utumishi wa Umma, ili kufikia lengo la Serikali la kuwahudumia wananchi.

Dkt.Nguvila ametoa wito huo, wakati akizungumza na baadhi ya watumishi wa Umma mkoa wa Arusha, kwenye hafla fupi ya mapokezi yake, iliyofanyika kwenye ukumbi wa Mikutano Ofisi ya Mkuu wa Mkoa huo, leo Februari 10, 2026, muda mfupi baada ya kupokelewa ofisini hapo, tayari kwa kuanza kutekeleza majukumu yake kwa washifa huo.

Amewasisitiza watumishi hao, kila mmoja kwa nafasi yake kuzingatia kuwa, mkoa huo ni mkoa wa Utalii hivyo wanalo jukumu la kuhakikisha wadau wa utalii wanafanya kazi kwenye mazingira rafiki, yasiyo na vikwazo vya aina yoyote huku akisisitiza kuto kuvumilia vikwazo vya kiutendaji wala urasimu unaokwamisha wawekezaji katika sekta ya utalii. 

"Sisi watalamu tunapaswa kuwa kichocheo cha kuiimarisha sekta ya utalii, kwa kuwa kila wilaya ina vivutio vyake, hivyo si busara kwa baadhi ya watendaji kuweka urasimu usio wa lazima unaoweza kudhoofisha sekta hiyo, sitavumilia urasimu wala migogoro inayokwamisha wawekezaji katika sekta ya utalii". Amesema Dkt.Nguvila

Aidha, amewaagiza Wakurugenzi wa Halmashauri zote, kutenga bajeti ya kutekeleza shughuli za utalii kwenye maeneo yao, kubuni vyanzo vya mapato pamoja na kusimamia ukusanyaji wa mapato, ikiwa ni pamoja na kutoka maofisini na kuwafuata wananchi ili kubaini changamoto zao na kuzitatua kwa haraka.

Katika kutekeleza maelekezo ya Serikali, Dkt.Nguvila ameataka viongozi hao, kuwa na kampeni maalumu ya kutoa elimu na usajili sambamba na kuhamasisha wananchi kujiunga na mpango wa Bima ya Afya kwa wote, ili ili kufikia lengo la Serikali ya awamu ya sita ya kila mwananchi kujiunga na Bima hiyo, itakayowawezesha kupata huduma za matibabu wanapougua.

Awali, Dkt.Nguvila amemshukuru Mhe.Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kumuanini na kumteua kuwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha na ameahidi kushirikiana na watalamu wa ngazi zote katika kuwahudumi wananchi.

















Na Oscar Assenga,MUHEZA

MKURUGENZI Bonde la Maji la Pangani Segule Segule amewaonya watu ambao wanao kuchukua maji chini ya ardhi,juu ya ardhi bila kufuata utaratibu uliowekwa kisheria ikiwemo kuwa vibali kuacha mara moja kwani wakiwafikia watawakamata.

Segule aliyasema hayo wakati wa Mkutano Mkuu wa Uchaguzi wa Jumuiya ya Maji Mto Zigi uliofanyika mjini Muheza ambapo alisema iwe mtu binafasi au taasisi huku akiwashauri wafuate utaratibu na kuchukua vibali na vibali vyao vinawaeleza kitu gani wanapaswa kufanya.

Aliwaeleza wadau wa Jumuiya hiyo kuwa Bonde la Mto Pangani linasimamia vyanzo vilivyopo chini ya ardhi kupitia visima na katika eneo hilo watu wengi hawana ufahamu au wengine wanaelewa lakini hawafuati utaratibu uliowekwa

Aidha alisema watu hawana ufahamu wa kutosha katika eneo la visima kwamba ukipewa ridhaa na Mkurugenzi wa Halmshauri ukipewa hatia na Wizara ya Ardhi juu ya kutumia ardhi na unaporaka kutumia rasilimali maji lazima upate kibali kutoka kwenye Bonde husika na katika Kanda ya Kaskazini anayetaka kutimia maji kutoka chini ya ardhi lazima apate kibali kuyoka Bonde la Pangani.

Aidha alisema kwamba Serikali imefanya kwa nia njema na sio kuweka ugumu watu wasitumie lakini wasiposimamiana katika hilo ipo siku maji yote yatachafuliwa na yanaweza yasiwepo.

Alieleza kwamba wao hawatoi vibali pekee bali wanaratibu wachimbaji kujua wana utaalamu wa kutosha wanaanza kuratibu kwenye utafiti huyo anayefanya utafiti je ana taaluma hiyo mpaka wanapotoa kibali cha kuchimbiwa visima wanauhakika wanakuwa ni watu sahihi wanaotumia utaalamu sahihi hivyo uchimbahji wake hauwezi kuleta madhara kwenye jmii husika,

Awali akizungumza wakati akifungua mkutano huo kwa niaba ya Mkuu wa wilaya ya Muheza, Katibu Tawala wa wilaya hiyo serikali inatambua ushirikishwaji wa wadau mbalimbali katika usimamizi na uhifadhi na uendelezaji wa rasimali za maji na mazingira.

Alisema lengo kuu katika juhudi hizo ni kuhakikisha rasilimali za maji zinazopatikana kwa wingi ikiwemo ubora unaokubalika na kwa uendelevu wa matumizi ya maji kwa sasa na vizazi vijavyo.

“Niwapongeze viongozi mliomaliza muda wenu kwa kazi nzuri na kubwa mlioifanya na kusimamia uendeshaji wa jumuiya ikiwemo usimamizi wa vyanzo vya maji”Alisema

Aliongeza kwa athari za mabadiliko ya tabia ya nchi na hali ya hewa hapa nchini ikiwemo Muheza joto kali mvua hazinyeshi hayo yote yamebadilika kutokana na uharibifu wa mazingira unaoendelea.

Alisisitiza utunzaji wa mazingira ni jambo muhimu ambalo limeendelewa kupewa kipaumbele na Rais na hata alipoazimisha siku ya kuzaliwa alipanda miti hivyo kupitia jumuya hiyo waendelee kuwahamasisha watu wapande miti katika kila sikukuu zao muhimu ikiwemo kuzaliwa.

Hata hivyo alieleza kwamba kuna umuhimu wa Jumuiya hizo kuendelea kujengewa uwezo ili kuweza kutunza mazingira ikiwemo mafunzo ya mara kwa mara ili waweze kuendana na kazi na mazingira kipindi cha sasa.









 

Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Tanga(TangaUWASA) imeingia makubaliano maalum na taasisi ya ROTARY inayofanya kazi kwa kushirikiana na Mamlaka za Maji Nchini Uholanzi (VEi) ya kutekeleza mradi wa kuwezesha huduma za kijamii mashuleni kupitia ujenzi wa vyoo (SCHOOL WaSH) kwa shule za msingi katika Jiji la Tanga.

Akizungumza kwa niaba ya uwakilishi wa ROTARY Bi.Emma Lesterhuis ameainisha kuwa mradi huo utatekelezwa na TangaUWASA kwa kushirikiana na Halmashauri ya Jiji la Tanga na utajikita zaidi katika ujenzi wa vyoo kwa baadhi ya shule zenye idadi kubwa ya wanafunzi na uhaba wa matundu ya vyoo.

Nae kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa TangaUWASA, Mha. Geofrey Hilly amewashukuru ROTARY kwa kutambulisha mradi huo ambao unaenda kuwezesha jamii hususani wanafunzi kupata huduma muhimu na kuahidi kutoa ushirikiano wa kutosha wakati wote wa utekelezaji wa mradi na usimamizi wake.



Tanga unakuwa Mkoa wa tatu nchini kunufaika na mradi wa "SCHOOL WaSH" ukiungana na Mikoa ya Arusha na Mwanza ambayo utekelezaji wake unaendelea.

Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala wa Maendeleo ya Usimamizi wa Elimu (ADEM), Dkt. Maulid J. Maulid, anashiriki warsha ya uthibitishaji iliyoandaliwa na Kituo cha Afrika cha Uongozi wa Shule (ACSL) jijini Nairobi, Kenya, kuanzia tarehe 10 hadi 13 Februari 2026.

 


Na OWM - TAMISEMI, Dodoma

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo, Mhe Cecilia Daniel Paresso amesisitiza ushirikishwaji wa wananchi wakati wa utungaji na uhuishaji wa Sheria Ndogo za Mamlaka za Serikali za Mitaa, ili kuwajengea wananchi uelewa wa sheria hizo ambao utawezesha utekelezaji wake katika Mamlaka za Serikali za Mitaa.

Mhe. Paresso ametoa wito huo wa ushirikishwaji wa wananchi katika utungaji wa sheria ndogo leo  Februari 10, 2026 Jijini Dodoma, wakati akiongoza Kikao cha Mafunzo kwa kamati yake kuhusu Sheria Tatu za Mamlaka ya Serikali za Mitaa na uhusiano wake na sheria ndogo za Mamlaka hizo.

Mhe. Paresso na wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo wameishauri Ofisi ya Waziri Mkuu-TAMISEMI kufanya mapitio ya Sheria Ndogo ambazo zimepitwa na wakati ili kuzihuisha au kuziondoa sheria zitakazobainika kutotekelezeka.

Akimwakilisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu -TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe katika kikao hicho, Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Kaspar Mmuya amesema Ofisi ya Waziri Mkuu - TAMISEMI itawashirikisha wananchi wakati wa kutunga Sheria Ndogo za Mamlaka za Serikali za Mitaa kama kamati ilivyoelekeza, lengo likiwa ni kuwajengea uelewa wananchi na kuwezesha utekelezaji wake.

Aidha, Mhe. Mmuya ameiahidi kamati hiyo kuwa, Ofisi ya Waziri Mkuu -TAMISEMI itafanya mapitio ya Sheria Ndogo za Mamlaka za Mitaa ili kujiridhisha kama zinakwenda na wakati, na kuongeza kuwa itazihuisha na kuziondoa sheria ambazo zitakazobainika kupitwa na wakati.

Katika kikao kazi hicho cha mafunzo, wajumbe wa Kamati hiyo ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo wamepata fursa ya kupitia Sheria ya Serikali za Mitaa (Mamlaka za Miji) Sura ya 288, Sheria ya Serikali za Mitaa (Mamlaka za Wilaya) Sura ya 287, na Sheria ya Fedha za Serikali za Mitaa, Sura ya 290.