Na OWM - TAMISEMI, Colombia

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu - TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, amesema ili mageuzi ya uchumi wa vijijini yawe na tija na manufaa kwa wananchi yanapaswa kuhusisha  uchumi wa buluu, ufugaji pamoja na misitu na mazao yake.

Prof. Shemdoe amesema hayo  Februari 26, 2026 wakati akichangia mada juu ya mageuzi ya uchumi na maendeleo vijijini kwenye mkutano wa pili wa Kimataifa wa Mageuzi ya Uchumi na Maendeleo Vijijini unaoendelea katika mji wa Cartagena, nchini Colombia, akimwakilisha Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika mkutano huo.

Mchango huo wa Prof. Shemdoe umelenga kutimiza azma ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kukifanya kilimo na ufugaji kuwa na faida kwa wananchi na sio shughuli za kujikimu, kukuza uchumi wa bluu kwa kutumia rasilimali za maji kuongeza kipato cha jamii za Pwani, ikiwa ni pamoja na kuhifadhi na kutumia misitu kwa njia endelevu ili kuongeza thamani ya mazao yake na kulinda mazingira.

Katika kikao cha kujadili maazimio ya Mkutano huo, Prof. Shemdoe amesisitiza kutambua   shughuli za ufugaji na uvuvi kama sehemu kubwa inayochangia maendeleo vijijini na kuongeza kuwa, kuwe na mkakati  kutathmini  utekelezaji wa maazimio kwa wakati ili tathmini isifanyike baada ya mikaka 20 kama ilivyofanyika ya mkutano wa kwanza wa mwaka 2006  katika mkutano huu wa pili wa mwaka 2026.

Katika hatua nyingine, Prof. Shemdoe ameongoza ujumbe wa Tanzania kufanya kikao cha pembeni cha uwili kati ya Tanzania na Indonesia ambapo ujumbe wa Indonesia uliongozwa na Naibu Waziri wa Kilimo Dkt. Ir. Sam Herodian.

Katika kikao hicho, Tanzania na Indonesia zimejadiliana kufufua ushirikiano wao kwenye njanja za kilimo cha mpunga na ufadhili wa masomo kwa Watanzania nchini Indonesia kama ilivyokuwa miaka ya nyuma.

“Majadiliano yetu yamepelekea tuanze maandalizi ya rasimu ya hati ya makubaliano kupitia Wizara ya Mambo ya Nje na Ubalozi wa Indonesia nchini Tanzania,” amesema Prof. Shemdoe.

Vile vile, Prof. Shemdoe amekutana na kufanya mazungumzo na Amy Regas, Mwakilishi wa Shirika la Land Facility ambalo limeonesha nia ya kuifadhili TAMISEMI kuandaa mradi mkubwa wa kujengea uwezo Mamlaka za Serikali za Mitaa kuhusu masuala ya mabadiliko ya tabia nchi, biashara ya kaboni kupitia Mkutano wa Wadau wa Maendeleo (Donor Roundtable meeting) utakaofanyika mwezi Mei, 2026.









 


Katika jitihada za kuendelea kuboresha utoaji wa huduma bora kwa wateja wake, Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) limepokea magari mapya 12 katika awamu ya pili kati ya magari 205 yanayotarajiwa kuwasili ifikapo mwishoni mwa mwezi Aprili.

Hatua hii ambayo ni sehemu ya mkakati wa muda mfupi uliotekelezwa na Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO Bw. Lazaro Twange inalenga kuongeza kasi na ufanisi wa utoaji wa huduma kwa wananchi katika maeneo mbalimbali nchini.

Hayo yamebainishwa Februari 21, 2026 na Meneja wa Huduma za Usalama wa TANESCO, Bw. Lenin Kiobya, wakati akizungumza katika zoezi la kupokea magari hayo lililofanyika katika Ofisi za TANESCO, Ubungo, Jijini Dar es Salaam.

Bw. Kiobya amesema kwamba magari hayo yatakuwa na mchango mkubwa katika kuwafikishia wananchi huduma ya umeme kwa wakati, hususan katika maeneo yenye changamoto za kimazingira na ambayo awali hayakuwa rahisi kufikika.

“Magari haya yatasaidia sana kufanikisha malengo makubwa ya shirika, ikiwemo mpango wa Mission 300 unaolenga kuongeza idadi ya wananchi wanaotumia umeme nchini. Tunawaomba madereva watakao kabidhiwa magari haya kuyatunza vyema ili yaendelee kusaidia kikamilifu katika shughuli za kila siku,” alisema Bw. Kiobya.

Kwa upande wake, Bw. Thomas Gowele, Msimamizi wa Kitengo cha Usafiri TANESCO, amesema kwamba magari hayo ni ya kisasa yakiwa na mfumo wa kamera mbele na nyuma ili kurahisisha dereva kuona vizuri wakati wa majukumu yake. Aidha, magari hayo yameambatanishwa na mashine ya kuinua mizigo (crane) yenye uwezo wa kuzunguka nyuzi 360°, ambayo itarahisisha kupandisha na kushusha nguzo pamoja na vifaa vingine.

“Magari haya ni ya kisasa, yamebuniwa kuboresha utoaji wa huduma zetu huku yakiweka kipaumbele cha usalama wa wafanyakazi,” alisema Bw. Gowele.

TANESCO inaendelea kuwekeza katika ununuzi wa vitendea kazi vya usafiri, ikiwa ni pamoja na magari madogo, malori, bajaji na pikipiki, ili kuhakikisha maeneo yote yanayohitaji huduma ya umeme yanafikiwa kwa urahisi na ufanisi zaidi.

 


Na Munir Shemweta, KITETO

Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo ameahidi kupelewa kwa Mwenyekiti wa Baraza la Ardhi na Nyumba la wilaya ya Kiteto mkoani Manyara.

Dkt Akwilapo alitoa ahadi hiyo leo tarehe 26 Februari 2026 kufuatia kuwasilishwa kwa malalamiko na mwananchi mmoja aliyemueleza Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt Mwigulu Nchemba aliyeko katika ziara mkoani Manyara kuwa, katika wilaya ya kiteto wananchi wamekuwa wakipata shida ya kushughulikiwa mashauri yao ya ardhi kupitia Baraza la Ardhi kutokana na kukosekana kwa mwenyekiti wa Baraza.

Kwa sasa Baraza la Ardhi na Nyumba la Wilaya ya Kiteto linahudumiwa na Mwenyekiti wa Baraza la Ardhi na Nyumba kutoka Dodoma jambo lililoelezwa kuwa limechangia mashauri kuchukua muda mrefu.

Dkt Akwilapo amesema, suala la Mwenyekiti wa Baraza la Ardhi na Nyumba Wilaya katika wilaya ya Kiteto tayari limeshamfikia na analifanyia kazi na muda wowote mwenyeikiti atapatikana ndani ya muda mfupi.

‘’Nimemuagiza katibu mkuu aliyefanyie kazi na muda wowote tutapata mwenyekiti mahsusi kwa ajili ya eneo hili’’. Amesema Dkt Akwilapo

Akigeukia suala la migogoro ya ardhi katika wilaya ya Kiteto, Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi amesema, migogoro mingi katika wilaya ya Kiteto  imesababishwa na ukosefu wa mipango ya matumizi ya ardhi.

Kwa mujibu wa Dkt Akwilapo, wilaya ya Kiteto ina jumla ya vijiji 63 na kati ya hivyo vijiji 33 ndivyo vilivyofanyiwa mpango wa matumizi ya ardhi huku vijiji 22 mpango wake ukiwa umeisha muda wake jambo alilolieleza kuwa, sasa jumla ya vijiji 52 vinahitaji  kufanyiwa mpango wa matumizi ya ardhi.

Amesema, Wizara yake inalifanyia kazi suala hilo na katika mpango wa Bajeti ijayo ya 2026/2026 wameomba fedha na itakapofanikiwa Wizara yake itatekeleza mpango huo kwa kushirikiana na Jumuiya ya Hifadhi ya Wanyamapori (WMA).






 

Mganga Mkuu wa Serikali Dkt. Grace Magembe amewataka wanataaluma wa lishe nchini kutoa elimu sahihi kwa wananchi kwa viwango vinavyokubalika kupitia kwa makundi mbalimbali ikiwemo wana-habari, mama lishe, baba lishe ili jamii ione faida ya uwepo wa wanataaluma hao. 

Dkt. Magembe amesema hayo leo Februari 26, 2026 alipokua anafungua Mkutano Mkuu wa Nne wa Chama cha Wataalamu wa Lishe Tanzania 2026 uliofanyika katika ukumbi wa Mabeyo Mkoani Dodoma. 

"Sasa hivi, huko kwenye mitandao ya kijamii kuna watu wengi ambao hata hawajui chochote kuhusu lishe, lakini wako bize kila siku kutoa elimu ya lishe kwenye mitandao ya kijamii, mtaani, tusiwaache wale waongee kwa sababu wakati mwengine wanapotosha," amesema Dkt. Magembe 

Amesema, jamii inatakiwa kupata elimu sahihi, ujumbe sahihi, kujua nini na kwa wakati gani chakula kipi kinafaa kuliwa, vitu gani visiliwe na kwa wakati gani, hii itapelekea kupata taifa lenye afya bora. 

Aidha, Dkt. Magembe amewataka wanataaluma hao kufanya tafiti ili kujua tatizo la lishe nchini katika baadhi ya Mikoa na kujua kwa nini matatizo ya lishe yanayofautiana kati ya mkoa mmoja na mwengine. 

"Hakuna taaluma yoyote katika Sekta ya Afya ambayo inaweza kwenda bila tafiti, tunakazi ya kufanya ili tujue tatizo ni nini, kwa nini mikoa yenye uzalishaji wa chakula ndio kuna udumavu," amesema Dkt. Magembe 

katika hatua nyingine Dkt. Magembe ametumia fursa hiyo kuiasa jamii juu ya kupanda miti ya matunda pamoja na bustani za mbogamboga majumbani na hata katika vituo vya afya nchini






 


📌Bilioni 7 kuwezesha maeneo 165 ya miji kupata huduma ya umeme Morogoro


Mkuu wa mkoa wa Morogoro Mhe. Adam Malima ameipongeza Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kwa utekekezaji wa miradi ya umeme maeneo ya Vijijini na Vitongoji hali iliyopelekea kuchochea uchumi wa wananchi na Taifa kwa ujumla.

RC Malima ametoa pongezi hizo leo Februari 26, 2026 mkoani humo wakati akizungumza na Bodi ya Nishati Vijijini (REB) pamona na Menejimenti ya Wakala wa Nishati Vijijini (REA) ilipomtembelea ofisini kwake kueleza utekelezaji wa miradi ya umeme vijijini inayoendelea na iliyokamilika mkoani humo. 

"Nimeifahamu REA kwa mingi toka ilipoanzishwa rasmi. Hapa ilipofika leo hii lazima tujivunie sisi kama Watanzania kwa kuwa imeweza kufikisha umeme vijiji vyote na sasa utekekezaji unaendelea kwenye vitongoji vyote nchini," Amesema RC Malima.

Halikadhalika RC Malima ameipongeza Bodi ya REA na Menejimenti kwa kazi kubwa iliyofanyika kwa kusimamia miradi mbalimbali ya umeme katika mkoa huo ili Watanzania waweze kunufaika na nishati hiyo muhimu. 

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), Mhe. Balozi Meja Jenerali Mstaafu Jacob Kingu ameeleza kuwa REA itaendelea kutekekeza miradi ya umeme vijijini wa weledi huku ikiwasimamia wakandarasi wa miradi hiyo ili waweze kuikamilisha miradi hiyo kwa wakati. 

"Sisi kama Bodi tunauhakika miradi inayoendelea tutaikamilisha kwa wakati kwa kuwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan tayari imetoa fedha nyingi ili kuwezesha na kukamilisha miradi hiyo, " Ameongeza Mhe. Balozi Kingu. 

Naye, Mkurugenzi Mkuu wa REA Mha. Hassan Saidy ameeleza kuwa kwa mkoa huo Wakala ipo mbioni kuongeza miradi ya ziada katika maeneo ya miji ambayo bado hayajafikiwa na huduma ya umeme ambapo takribani  maeneo 165 yatapatiwa huduma hiyo na wateja wa awali 1,750 watapatiwa huduma ya umeme ambapo Serikali imetoa takribani shilingi bilioni 7 kwa mkoa wa Morogoro kutekeleza miradi hiyo. 








 

Mbunge wa Jimbo la Kisarawe mkoani Pwani, Selemani Jafo, ameonesha kuridhishwa na kasi ya utekelezaji wa mradi wa maji katika Kijiji cha Nyani, Kata ya Mafizi, akieleza kuwa hatua iliyofikiwa inaleta matumaini mapya kwa wananchi.

Mradi huo unaotekelezwa na kampuni ya BROADWAYS ENGINEERING CO LTD una thamani ya shilingi milioni 402.8 na hadi sasa umefikia asilimia 70 ya utekelezaji, jambo linaloashiria kuwa upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama kwa wakazi wa eneo hilo si wa muda mrefu tena.

Kwa mujibu wa taarifa ya utekelezaji, mradi unahusisha ujenzi wa mnara wa tanki la maji lenye urefu wa mita 12 na uwezo wa kuhifadhi lita 50,000, pamoja na ujenzi wa vituo vitano vya kuchotea maji na ulazaji wa mtandao wa mabomba wenye urefu wa kilometa 16.167.

Akizungumza wakati wa ukaguzi wa mradi huo, Dkt. Jafo alimpongeza mkandarasi kwa kufanya kazi kwa kasi na weledi mkubwa, akibainisha kuwa kampuni hiyo imeendelea na kazi hata kabla ya kupokea malipo yoyote, jambo alilolitaja kuwa ni uzalendo na kujitolea kwa maendeleo ya wananchi.

Kutokana na kasi hiyo, Jafo ameiiomba Wizara ya Maji kulipa kiasi cha shilingi milioni 279.1 kwa kazi zilizokamilika ili kumwezesha mkandarasi huyo kuendelea na hatua zilizobaki na kuhakikisha mradi unakamilika kwa wakati.

Mbali na mkandarasi, mbunge huyo pia amempongeza Meneja wa RUWASA Wilaya ya Kisarawe, Mhandisi Evangelista Kahwili, kwa usimamizi makini wa miradi ya maji ndani ya jimbo hilo, akisema nidhamu na ufuatiliaji wa karibu umechangia mafanikio yanayoonekana.

Wananchi wa Nyani na maeneo ya jirani wanatarajia kunufaika na mradi huo mara utakapokamilika, huku wakieleza kuwa utapunguza adha ya kutembea umbali mrefu kutafuta maji na kuboresha afya pamoja na shughuli za kiuchumi katika eneo hilo.


Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratous Ndejembi, ameitaka Mamlaka ya Udhibiti Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA) kuimarisha mipango yake katika ukusanyaji wa data sahihi, tathmini ya vitalu vya utafiti, na maandalizi ya Watanzania kushiriki kikamilifu katika miradi mikubwa ya kimkakati, ikiwemo mradi wa kuchakata gesi asilia kuwa kimiminika (LNG).

Mhe. Ndejembi ameyasema hayo wakati wa Kikao cha Tano cha Mkutano wa Pili wa Baraza la Wafanyakazi la PURA kilichofanyika mkoani Morogoro leo Februari 26, 2026.

 Amesisitiza kwamba sekta ya nishati ina nafasi ya kipekee katika kufanikisha malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, hivyo PURA inatakiwa kuhakikisha mipango yake inaendana na maono hayo.

“Sekta ya Nishati imetambuliwa kama moja ya vichocheo muhimu vya uchumi wa taifa. Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Nishati zina wajibu mkubwa kuhakikisha upatikanaji endelevu, salama na wa uhakika wa rasilimali za mafuta na gesi asilia,” amesema Mhe. Ndejembi.

Aidha, Mhe. Ndejembi amewataka PURA kuongeza juhudi katika ukusanyaji na usimamizi wa data za kijiolojia na kufanya tafiti za awali, hasa ikizingatiwa kwamba maeneo makubwa ya nchi bado hayajafanyiwa utafiti wa kina.

“Takwimu sahihi ni msingi wa kuvutia uwekezaji na kuongeza ugunduzi wa rasilimali. Hatuwezi kuendeleza sekta bila taarifa za kutosha na tafiti madhubuti,” amesisitiza.

Waziri huyo pia ameagiza PURA kufanya tathmini ya kina katika vitalu vilivyopo, hususan katika ukanda wa Tanga, Ruvu, na maeneo mengine, ili kubaini iwapo wamiliki wa vitalu wanafanya shughuli za utafutaji kama inavyotakiwa.

 Ameongeza kuwa si vyema kwa vitalu kukaa mikononi mwa wawekezaji wasioendeleza shughuli za utafutaji, na mamlaka za udhibiti zinapaswa kuchukua hatua pale inapobainika hakuna maendeleo yanayofanyika kwa manufaa ya Taifa.

Akizungumzia mradi wa LNG, Mhe. Ndejembi amewataka PURA kuanza mapema kuandaa mkakati wa kujenga uwezo wa kitaasisi katika kusimamia mradi huo. 

Sambamba na hilo, amewahimiza kuandaa Watanzania kushiriki kikamilifu katika mnyororo wa thamani wa LNG, badala ya kusubiri utekelezaji wa mradi kuanza.

Awali katika kikao hicho, Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi Asilia, Dkt. James Mataragio, amewataka PURA kusimamia majukumu yake ya msingi kama yanavyoainishwa katika malengo ya kuanzishwa kwa taasisi hiyo.