FCC YAONGEZA NGUVU KATIKA KUDHIBITI BIDHAA BANDIA
Serikali imetoa wito kwa wazalishaji, waingizaji bidhaa, wasambazaji, wafanyabiashara, vyombo vya habari, vyombo vya dola, mamlaka za forodha, Taasisi za umma, asasi mbalimbali pamoja na wananchi kwa ujumla kuendelea kushirikiana kwa karibu na Tume ya Ushindani (FCC) katika kubaini na kudhibiti bidhaa bandia.
Vilevile, ameipongeza FCC kwa kuendelea kuimarisha juhudi katika kukabiliana na changamoto ya bidhaa bandia na kulipa uzito unaostahili katika mipango ya baadaye ili kuendelea kuboresha mazingira ya biashara Nchi
Hayo yamesemwa na Mkuu wa Wilaya ya Temeke, Mhe. Sixtus Mapunda, aliyemwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, katika kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Kudhibiti Bidhaa Bandia Duniani (WACD) 2026.
Aidha, amesema Serikali ya Awamu ya Sita itaendelea kuunga mkono FCC kupitia maboresho ya sera, sheria na mifumo ili kuhakikisha masoko salama na ushindani wa haki ili kukabiliana na athari zake kwa afya za wananchi na uchumi wa taifa.
Mapunda pia amesema FCC inapaswa kupanua matumizi ya teknolojia katika uchunguzi, ufuatiliaji na udhibiti wa bidhaa bandia, hususan katika masoko ya kidijitali na mipaka ya nchi ili kuziba mianya inayotumiwa na wahalifu wa kiuchumi.
Akizungumzia kaulimbiu isemayo, “Linda Maisha na Masoko Dhidi ya Pombe, Vilainishi na Sigara Bandia,” amesema bidhaa bandia zina madhara kwa afya, hupunguza mapato ya Serikali na kudhoofisha biashara halali.
Naye, Kamishna wa Tume Bw. Said Tunda ambaye alimwakilisha Mwenyekiti wa FCC Dkt. Aggrey Mlimuka amesema kampeni za elimu kwa umma na mijadala ya kitaalamu zimeendelea kuongeza uelewa kuhusu athari za bidhaa bandia kwa afya, uchumi na maendeleo ya biashara halali nchini.
Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, Bi. Khadija Ngasongwa, amesema maadhimisho yanalenga kuongeza uelewa wa umma kuhusu madhara ya bidhaa bandia na kuimarisha ushirikiano wa wadau.







.jpg)











