Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Rosemary Senyamule ameitaka jamii kuzingatia haki na usawa kwa wanawake na wanaume ili kujenga jamii yenye maendeleo na mshikamano.

Amesema kuwa usawa wa kijinsia ni msingi muhimu katika kufanikisha maendeleo ya kijamii na kiuchumi, hivyo ni jukumu la kila mwananchi kuhakikisha wanawake wanapata fursa sawa katika elimu, uongozi na shughuli za kiuchumi.

Akizungumza Machi 8, 2026 wakati wa maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yaliyofanyika katika Wilaya ya Kongwa jijini Dodoma, Senyamule alisisitiza umuhimu wa kupinga vitendo vya ukatili wa kijinsia na mila potofu zinazowanyima wanawake haki zao. 

Alieleza kuwa wanawake wakipewa nafasi na kuaminiwa wana uwezo mkubwa wa kuchangia maendeleo ya familia, jamii na taifa kwa ujumla.

Aidha, aliwahimiza wanawake kuendelea kujitokeza katika shughuli za maendeleo, ujasiriamali na nafasi za uongozi kwa kuwa Serikali itaendelea kuweka mazingira rafiki yatakayowezesha wanawake kujikwamua kiuchumi na kushiriki kikamilifu katika kujenga taifa lenye usawa, haki na maendeleo kwa wote.

Mkurugunzi wa Mafunzo na Utafiti Grace Masambaji pamoja na Watumishi wanawake wa Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania (TCDC) ni kati ya watumishi waliohudhuria maadhimisho hayo yaliyoyobeba kauli mbiu ya Haki kwa wanawake na wasichana: Msingi wa Maendeleo jumuishi kufikia Dira 2050.





 


Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba amesema wananchi wa Mkoa wa Rukwa wataanza kupata umeme wa gridi kuanzia mwezi mei mwaka huu mara utakapokamilika mradi wa usafirishaji umeme wa msongo wa kV 400 kutokea mkoani Iringa.

Ameyasema hayo katika Mji wa Laela, Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga wakati wa ziara ya Waziri Mkuu, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba iliyoanza jana mkoani Rukwa.

“Kwa maelekezo ya Rais, Mhe.Dkt.Samia Suluhu Hassan na kwa maelekezo yako pia,, tunaendelea kuhakikisha inapofika mei 2026 tunawasha umeme kupitia mradi wa TAZA. Hali ya mradi inaenda vizuri na kama kila kitu kitakwenda kama kilivyo, itakapofika mwezi wa tano mwaka huu hatimaye Mkoa huu wa Rukwa utanufaika na umeme wa gridi.” Amesema Mhe.Salome

Ameeleza kuwa, kwa sasa mkoa wa Rukwa unapata umeme kutoka nchini Zambia kupitia mashirikiano ya biashara ya umeme katika nchi za Ukanda wa Kusini mwa Afrika (Southern Africa Power Pool) ambayo yanawezesha nchi wanachama kuuza au kununua umeme pale kunapokuwa na uhitaji ili kukidhi mahitaji ya wananchi.

Ameongeza kuwa, kutokana na nchi kuwa na umeme wa kutosha, kazi zinazoendelea ili kuweza kuutumia umeme huo ipasavyo ni ujenzi wa miundombinu imara ya usafirishaji na usambazaji umeme itakayowezesha kufikisha huduma hiyo kwa wananchi wengi.

Kuhusu Nishati Safi ya Kupikia, amesema jitihada mbalimbali zinaendelea ili kuweza kufikia asilimia 80 ya wananchi wanaotumia Nishati Safi ya Kupikia ifikapo 2034 ikiwemo ya kusambaza majiko banifu na mitungi ya gesi kwa bei ya ruzuku.







 

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Mwigulu Nchemba ameipongeza Wizara ya Ujenzi na Wakala wa Barabara nchini (TANROADS), Mkoa wa Rukwa kwa ujenzi wa kiwanja cha ndege cha Sumbawanga kwa ubora.

Amesema hayo leo alipokagua maendeleo ya ujenzi huo na kusisitiza kuwa kiwanja hicho kimejengwa kwa viwango vya kisasa.

" Hongereni wana Rukwa kwa kupata kiwanja cha ndege cha kisasa kitakachochochea fursa nyingi za kiuchumi", amesema Dkt. Nchemba.

Naibu Waziri wa Ujenzi Eng. Godfrey Kasekenya amesema ujenzi wa kiwanja cha ndege hicho unaotekelezwa na mkandarasi M/s Beijing Construction Engineering Group Co Ltd kutoka China umefikia asilimia 96 na utakamilika ifikapo April mosi mwaka huu.

" Tumejipanga kuhakikisha tunawakabidhi kiwanja hiki wenzetu wa Uchukuzi kiwanja hiki kikiwa kimekamilika ifikapo April mosi", amesisitiza Naibu Waziri Eng. Kasekenya.

Eng. Kasekenya amesema kazi ya ujenzi wa njia ya kuruka na kutua ndege, barabara za viungio, maegesho ya ndege na jengo la abiria imekamilika.

Nae Naibu Waziri wa Uchukuzi David Kihenzile amesema wako tayari kukipokea kiwanja hicho mapema mwezi ujao ili kuanza kutoa huduma za ndege mkoani humo.

Kiwanja cha ndege cha Sumbawanga ambacho kilijengwa mwaka 1945 na kukarabatiwa mwaka 1985 kimefanyiwa uboreshaji mkubwa na wa kisasa utakaowezesha ndege za saizi ya kati kutumia kiwanja hicho ambapo zaidi ya shilingi bilioni 60 zimetumika







 


Na Mwandishi Wetu - Pwani


Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) wameipongeza Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA), kusambaza miundombinu ya gesi asilia kwenye kaya takribani 1000 na shule moja ambapo mradi huo umefadhiliwa na Serikali kwa asilimia 100 kupitia REA.

Hayo yamezungumzwa leo Machi 8, 2026 na Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) Bw. Deodatus Balile wakati wa Ziara ya TEF Kutembelea mradi uliofadhiliwa na REA wa ujenzi wa miundombinu ya usambazaji wa gesi asilia kwenye nyumba za makazi mkoa wa Pwani

Bw. Balile amesema kupitia mradi huo Serikali imepunguza kwa kiasi kikubwa utegemezi wa Nishati nyingine kama mkaa wa kawaida, kuni, na mafuta ya taa na nishati gesi asilia sasa inakua ni chanzo cha nishati ya kupikia.

"REA imefanya kazi kubwa sana ya kufadhili mradi huu, hivyo basi mradi huu utaboresha kiwango cha maisha ya walengwa wa mradi kwa kuokoa gharama na muda wa kupika, mazingira safi afya bora na uwezeshaji wa wanawake kuongezeka, " Amesema Bw. Balile.

Kwa upande wake, Kaimu Meneja Usaidizi wa Kiufundi kwa Waendelezaji wa Mradi kutoka REA, Mha. Emmanuel Yessaya amesema kuwa Wakala ulitenga Fedha kwa ajili ya kufadhili mradi ya usambazaji wa gesi asilia kupitia Mfuko wa Nishati Vijijini (REF) ambapo takribani kaya 1000 pamoja na taasisi moja zimenufaika kwa kusambaziwa miundombinu ya gesi asilia kwa ajili ya kupikia majumbani katika mkoa wa Lindi na Pwani.

Mha.Yessaya ameongeza kuwa, Mradi huo ni wa kimkakati kwa ajili ya kupunguza gharama za nishati ya kupikia, kulinda afya za wananchi na kupunguza athari za kimazingira zitokanazo na ukataji wa misitu kwa ajili ya nishati ya kupikia kwa wananchi wanaoishi Vijijini na kwenye vijiji miji.

Kwa upande wake Mhandisi wa mradi huo kutoka Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) Mha. Anthony Karomba, amesema kuwa mradi huo wa kuunganisha wateja wa majumbani kwenye mtandao wa gesi asilia umegharamikiwa kwa fedha nyingi na Serikali kupitia REA na hivyo amewasihi wananchi kuendelea kuilinda miundombinu hiyo.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti wananchi wa Kata ya Kisemvule wameishukuru Serikali kupitia REA kwa kusambaza miundombinu ya gesi asilia ya kupikia katika miji yao. Wameeleza kuwa mradi umenufaisha kaya zao kwa kuokoa gharama, kuongeza muda wa kufanya shughuli za kuzalisha mali, imelinda mazingira, imeboresha afya zao na kuimarisha usawa wa kijinsia kwenye shughuli za kiuchumi.



 

Wakala wa Vipimo (WMA) wameshiriki katika maadhimisho ya Siku ya Wanawake Kimataifa, kwa kutoa elimu ya vipimo kwa wadau mbalimbali waliofika Kongwa, Dodoma mahali ambako sikukuu hiyo imefanyika ngazi ya Mkoa.

Akieleza kuhusu huduma zilizotolewa katika maonesho hayo, Meneja Mawasiliano wa WMA, Veronica Simba amesema ni pamoja na elimu kuhusu uandishi wa alama sahihi za vipimo katika bidhaa pamoja na kuhamasisha matumizi ya vipimo sahihi na kwa usahihi.

"Mahala hapa tumekutana na wanawake wengi ambao ni wajasiriamali na tumefanikiwa kuwapatia elimu ya matumizi sahihi ya vipimo kwa ajili ya biashara zao hivyo tumefanikiwa kama tulivyotarajia," amesema.

Vilevile, Simba ameongeza kuwa wamefanikiwa kutoa elimu ya vipimo kwa makundi mengine mbalimbali ya wanawake, wakiwemo watumishi wa umma, wawekezaji na hata kina mama wa nyumbani.

Amesema kuwa, makundi yote hayo yanahitaji elimu kuhusu umuhimu wa matumizi sahihi ya vipimo ili kila mmoja anufaike kulingana na uhitaji wake.

Awali, Mgeni Rasmi ambaye ni Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule alitembelea Banda la WMA na kuwasisitiza kuelekeza nguvu zaidi katika utoaji elimu ya vipimo kwa wanawake kulingana na shughuli zao za kila siku hususani malezi ya familia na hata biashara.

Katika kuenzi maadhimisho hayo, WMA iliwakilishwa na wafanyakazi wanawake ambao walitoa elimu ya vipimo na huduma nyingine mbalimbali.



Na Mwandishi Wetu
Wanawake wa Tume ya Ushindani (FCC ) wametakiwa kuwa na  upendo ambao utajenga mshikamano na kuleta ufanisi katika Taasisi.
Hayo ameyasema Mwakilishi wa Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, Bi. Magdarena Utouh katika  Maadhimisho  ya Siku ya  Wanawake Duniani ambayo hufanyika kila Machi 8 ya kila mwaka.
Magdelena amesema maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani ni ishara ya kufanya wanawake  kuwa na  nguvu ambayo inatoa mchango katika Taifa pamoja na kuchochea maendeleo.
Amesema kuwa maadhimisho hayo ni pamoja ya kupeleka ujumbe kwa Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan kuwa tuko nyuma yake na tunapiga kazi.
Aidha amesema.kuwa wanawake ni jeshi kubwa hivyo tunahitaji  kuendelea kujituma na kuleta matokeo  katika maeneo yetu ya kazi.
Kauli mbiu ya mwaka ya  Maadhimisho  ya Siku ya Wanawake Duniani  2026 ni Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana: Msingi Jumuishi kufikia Dira 2050.
 
 
 
 
 
 
 
 

Mnufaika wa Programu ya Taifa ya Ukuzaji Ujuzi, Mtawa Vestina Damian akizungumza kwa furaha mafanikio aliyopata kupitia Programu hiyo inayoratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano, tarehe 7 Machi, 2026 katika Chuo cha Laela, Sumbawanga Mkoani Rukwa.

Wanufaika wa Mafunzo ya Uanagenzi yanayotolewa kupitia Programu ya Taifa ya Ukuzaji Ujuzi wakisikiliza maelezo ya Mtawa Vestina Damian kuhusu manufaa aliyopata kupitia Programu hiyo inayoratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano, tarehe 7 Machi, 2026 katika Chuo cha Laela, Sumbawanga Mkoani Rukwa.

Wanufaika wa Mafunzo ya Uanagenzi yanayotolewa kupitia Programu ya Taifa ya Ukuzaji Ujuzi wakiwa katika picha ya pamoja na Wataalamu kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano, walipowatembelea katika Chuo cha Laela, tarehe 7 Machi, Sumbawanga Mkoani Rukwa.

Na: Mwandishi Wetu - Rukwa

Katika kuta za utulivu za Chuo cha Kilimo na Mifugo cha Kanisa Katoliki kilichopo Laela, mkoani Rukwa, sauti ya shukrani imesikika kutoka kwa mtawa mmoja aliyepata fursa ya kipekee ya kujinoa kupitia Programu ya Taifa ya Kukuza Ujuzi (Uanagenzi).

Mtawa Vestina Damian ambaye sasa amekuwa ishara ya matumaini na weledi, anasimulia jinsi mafunzo ya vitendo aliyoyapata yalivyomgeuza kutoka kuwa mwanafunzi wa nadharia na kuwa mtaalamu aliyepikwa vyema.

Maelezo hayo yalitolewa mbele ya Maofisa kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano wakiongozwa na Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini kutoka Ofisi hiyo Revocatus Kassimba walipofika chuoni hapo kufuatilia utekelezaji wa mafunzo ya Uanagenzi.

Sista Vestina Damian, akiwa mmoja wa wanufaika wa programu hiyo, alieleza kwa msisitizo namna mafunzo hayo ya uanagenzi yaliyochukua miezi minane yalivyomjengea weledi wa kitaalamu katika kilimo na ufugaji wa kisasa.

Alibainisha kuwa, kupitia mchanganyiko wa nadharia na vitendo, ameweza kujifunza mbinu za kisasa za kilimo cha umwagiliaji, matumizi sahihi ya mbolea, na mbegu bora zinazohimili mabadiliko ya tabianchi, maarifa ambayo sasa anayatumia kuifanya bustani na mashamba ya utawani kuwa mfano wa kuigwa katika eneo la Laela.

Upande wa mifugo, Sista huyo alieleza kuwa programu hiyo imemsaidia kuelewa kanuni za kitaalamu za ufugaji wa kisasa, ikiwemo ujenzi wa maboma bora, utayarishaji wa lishe mchanganyiko, na udhibiti wa magonjwa.

Aidha, amesema maarifa hayo aliyopata yamemwezesha kusaidia jamii inayomzunguka na hivyo kukuza tija katika kilimo na ufugaji, jambo ambalo linaendana na dhamira ya Serikali ya kuongeza tija na uzalishaji ili kuchochea mageuzi ya kiuchumi.

“Ujuzi huu umenipa heshima kubwa kwa jamii yanguj kwani umenipa uwezo wa kuhudumia watu wangu kwa weledi zaidi,” alieleza Sista Vestina Damian mbele ya maofisa hao na wanajamii wengine.

Vilevile, amesifu uamuzi wa Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano kwa kuweka mfumo unaoruhusu wananchi wa kada zote kupata ujuzi stahiki. Kwake, uanagenzi huo haukuwa tu mafunzo ya darasani, bali ulikuwa ni ukombozi wa fikra uliompa ujasiri wa kwenda kusimamia miradi ya uzalishaji inayolenga kuwasaidia wahitaji na jamii inayomzunguka.

"Naishukuru Serikali, namshukuru mama Samia kwa kutupa fursa hii sisi wananchi wake, bila kujali nafasi zetu," anasema Sista Vestina Damian huyo kwa unyenyekevu.

Alisisitiza katika shukurani zake kuwa ujuzi alioupata chuoni Laela ni hazina itakayotumika kuimarisha ustawi wa jamii kwa ujumla, huku akitoa rai kwa Serikali kuendelea kutanua wigo wa programu hiyo ili kuwafikia vijana na wahitaji wengi zaidi katika maeneo ya pembezoni.

Chini ya kaulimbiu isemayo “Nguvukazi yenye Ujuzi Stahiki kwa Ajira Endelevu". Serikali imeweka bayana dhamira yake ya kupunguza pengo la ujuzi linalowakabili vijana wengi nchini. Programu hii inalenga kuleta mabadiliko ya kifikra na kiuchumi kwa kutoa mafunzo yanayoakisi mahitaji halisi ya soko la ajira, yakijikita katika mchanganyiko wa nadharia na vitendo.

Uzinduzi wa awamu ya nane ya programu hii, umefanyika Machi 8 mwaka huu.Uendelevu wa programu unakuja wakati ambapo nchi inajipanga kuelekea Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050, ikihitaji nguvukazi yenye ushindani wa kimataifa. Katika awamu hii, Serikali imewekeza rasilimali nyingi kuwafikia vijana 5,746 nchi nzima.

Mafunzo yanatolewa kupitia vyuo 46 vilivyosambaa katika mikoa 25 ya Tanzania Bara, ambapo vyuo 29 ni vya Serikali na 17 ni vya sekta binafsi (ikiwemo Chuo cha Laela).

Programu hii ya uanagenzi ni sehemu ya mikakati ya Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano katika kuhakikisha kuwa nguvukazi ya Taifa inapata stadi muhimu za kuajirika au kujiajiri, hivyo kuchochea ukuaji jumuishi wa uchumi kuelekea mwaka 2050.

Na Mwandishi Wetu 
Mbunge wa Jimbo la Mkuranga na Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega, amewataka wananchi wa Wilaya ya Mkuranga kuendelea kuilinda na kuitunza amani ya nchi.Ulega ameyasema hayo wakati wa futari iliyoandaliwa  kwa wananchi  wa Mkuranga pamoja na Watoto Yatima wa Wilaya hiyo ,amesema   mbezi mtukufu wa Ramadhan unatengeneza upendo na mshikamano wa taifa kwa pamoja 

Amesema Kuwa kila mtanzania anatakiwa kuhubiri amani ikiwa ndio nguzo kuendelea  kuijenga nchi

“Tanzania ni nchi ya amani, hivyo ni jukumu la kila mwananchi kuilinda na kuitunza amani hiyo kwa manufaa ya taifa letu,” amesema Ulega.

Aidha, aliwataka wananchi kuendelea kumuombea Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan, ili aendelee kuwa na afya njema na kuiongoza nchi kwa mafanikio.“Tuendelee kumuombea Mheshimiwa Rais wetu awe na afya njema ili aendelee kuiongoza nchi kwa hekima na mafanikio,” ameongeza.

Ulega amesisitiza kuwa kudumisha amani ni jukumu la kila Mtanzania, na kwamba wananchi wanapaswa kushirikiana katika kulinda tunu hiyo muhimu kwa maendeleo ya taifa.