Na Mwandishi Wetu
Dar es Salaam, Machi 10, 2026. Tume ya Ushindani (FCC) imesema itaendelea kusimamia kwa karibu haki za walaji kwa taasisi na kampuni zinazotumia mikataba iliyoandaliwa kwa upande mmoja, ili kuhakikisha watumiaji wa huduma na bidhaa hawapati hasara kutokana na mikataba hiyo.
Kauli hiyo imetolewa leo na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, Khadija Ngasongwa, alipokuwa akizungumza katika semina ya wadau kutoka taasisi na kampuni zinazotumia mikataba ya upande mmoja, iliyofanyika jijini Dar es Salaam.
Ngasongwa alisema FCC inaendelea kufuatilia kwa karibu mikataba ya aina hiyo ili kuhakikisha haikiuki haki za walaji katika soko. Alifafanua kuwa mikataba ya upande mmoja hutumiwa sana na taasisi mbalimbali kwa lengo la kurahisisha utoaji wa huduma kwa wakati, lakini ni muhimu iwe chini ya uangalizi ili kuepuka matumizi yanayoweza kuwa kinyume na sheria za ushindani na ulinzi wa mlaji.
Alisema semina hiyo ni sehemu ya mwendelezo wa utoaji wa elimu kwa wadau kuelekea kilele cha maadhimisho ya Siku ya Mlaji Duniani, yanayolenga kuongeza uelewa kuhusu haki na wajibu wa walaji pamoja na watoa huduma.
“Ninatambua kuwa mikataba inayoandaliwa kwa upande mmoja ina faida katika kurahisisha utoaji wa huduma kwa wakati. Hata hivyo, FCC ina jukumu la kuifuatilia kwa karibu, kwani bila uangalizi kunaweza kuwa na mambo yanayofanyika kinyume na maslahi ya walaji katika soko,” alisema Ngasongwa.
Aliongeza kuwa hata pale taasisi zinapotaka kuunganisha huduma au mikataba yao, ni muhimu kufanya tathmini ya kina ili kubaini kama kuna vipengele vinavyoweza kukiuka masharti ya ushindani au kuathiri ubora wa huduma kwa walaji.
Ngasongwa alisisitiza kuwa kila mtu ni mlaji kwa namna moja au nyingine, hivyo ni muhimu kuhakikisha thamani ya fedha inayotolewa na mteja inaendana na ubora wa huduma au bidhaa anayopata. Alisema hali hiyo pia husaidia kujenga uaminifu kati ya watoa huduma na walaji.
Aidha, alisema FCC itaendelea kukutana na makundi mbalimbali ya wadau kwa lengo la kuwapa uelewa mpana kuhusu majukumu ya taasisi hiyo na umuhimu wa kuzingatia sheria za ushindani na ulinzi wa mlaji.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Umoja wa Mabenki Tanzania (TBA), Tusekelege Mwaikasu, alisema semina hiyo ni muhimu kwa taasisi za kifedha kwani itawasaidia kuboresha utoaji wa huduma kwa walaji kwa kuzingatia viwango vinavyokubalika.
Alisema benki, kupitia umoja wao, zimekuwa zikitekeleza kampeni ya “Niko Fiti”, inayolenga kuhakikisha huduma za kifedha zinatolewa kwa ubora na kwa kuzingatia mahitaji ya walaji.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindqni Ushindani Ushindani (FCC), Bi. Khadija Ngasongwa akizungumza wakati akifungua Semina kwa Taasisi na Kampuni zenye mikataba iliyoandaliwa upande mmoja jijini Dar es Salaam. Mkurugenzi wa Udhibiti wa Mienendo ya Bidhaa inayokatazwa na Sheria ya Ushindani FCC, Bi.Magdalena Utouh  akizunguza wakati wa kuhitimisha semina ya wadau wa Taasisi na Kampuni zenye mikataba iliyoandaliwa na upande mmoja jijini Dar es Salaam.
Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini wa FCC,Bi. Roberta Feruzi akitoa maelezo kuhusiana na Semina ya wadau wa Taasisi na Kampuni zenye mikataba iliyoandaliwa upande mmoja jijini Dar es Salaam. Mkurugenzi Mtendaji wa Umoja wa Mabenki Tanzania (TBA ) Bi.Tusekelege Mwaikasu akitoa neno kwa niaba ya wadau katika mkutano na FCC ,jijini Dar es Salaam. Mkutano ukiendelea Kaimu Mkurugenzi Mkurugenzi Mkuu wa FCC Khadija Ngasongwa akiwa katika matukio picha za za pamoja makundi mbalimbali.
Mafunzo ya siku tano kwa Maafisa Elimu kutoka mikoa 26 ya Tanzania Bara yameanza rasmi jijini Arusha, yakilenga kuwajengea uwezo viongozi hao katika utekelezaji wa majukumu yao ya kiutendaji.

 


Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba, amesema asilimia 89 ya vitongoji 724 wilayani Nkasi Mkoa wa Rukwa  vimesambaziwa umeme, na vitongoji vilivyosalia  vitakuwa vimesambaziwa nishati hiyo ifikapo 2030.

Mhe. Salome amesema hayo katika Mji wa Namanyere, Wilaya ya Nkasi, Mkoa wa Rukwa wakati wa ziara ya Waziri Mkuu, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba.

“Sisi Sekta ya Nishati jukumu letu ni kuhakikisha Watanzania wote wanapata umeme wa uhakika wakati wote. Hapa Nkasi kwa sasa wanatumia umeme kutoka nchini Zambia kupitia makubaliano ya kikanda ya kuuza na kununua umeme ili kuweka mfumo imara wa upatikanaji wa umeme. Hata hivyo, tunatarajia kama kila kitu kitakwenda sawa, Nkasi itapata umeme wa gridi ifikapo mwezi Mei mwaka huu,” amesema Mhe. Salome

Ameongeza kuwa, mradi wa kupeleka umeme wa gridi mkoani Rukwa unaendelea vizuri na mara umeme huo utakapofika mkoani humo,  wananchi watanufaika na umeme wa uhakika  huku pia wakiwa na nafasi ya kupata umeme wa ziada kutoka nchini Zambia. Aidha, kituo cha umeme cha Sumbawanga kinatarajiwa kutumika pia katika biashara ya umeme kwa nchi jirani, ikiwemo Zambia.

Akizungumza na wananchi katika Mji wa Namanyere, Mhe.Salome amewahamasisha kuachana na matumizi ya nishati isiyo safi kama kuni na mkaa na badala yake watumie nishati safi ya kupikia.

Amesema Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan anaendelea kuchukua hatua mbalimbali kuhakikisha wananchi wanatumia nishati safi ya kupikia, ikiwemo kutoa ruzuku ya hadi asilimia 85 kwa majiko banifu na ruzuku ya asilimia 50 kwa mitungi ya gesi ya kilo sita.






 


Na Oscar Assenga,TANGA


MKUU wa Mkoa wa Tanga Balozi,Dkt Batilda Burian amezindua Kamati za Ushauri wa Kisheria ngazi ya mkoa na wilaya na kliniki ya Sheria bila malipo huku akieleza kwamba zitasaidia kupunguza mashauri au migogoro dhidi ya Serikali kutokana na kukutanisha mawakili wa Serikali.

Aliyasema hayo leo kwenye viwanja vya Tangamano Jijini Tanga ambako kilifanyika uzinduzi wa Kamati hizo ambapo alisema pia wale wa taasisi mbalimbali na kuwasaidia wananchi wenye changamoto mbalimbali kupata ufumbuzi.

Alisema uwepo wa huduma hizo utawawezesha mawakili wa Serikali kusimamia utawala wa Sheria katika kushirikiana na wadau wengine katika kutatua kero za wananchi na kupunguza malalamikko ya kisheria kutoka kwa wananchi.

“Lakini pia kutoa elimu ya Sheria kwa umma katika kushughulikia changamoto mbalimbali katika maeneo yao pamoja na kutoa elimu kwa viongozi na maafisa wa Serikali waweze kutoa maamuzi kwa mujibu wa Sheria”Alisema






Aidha alisema pia itapunguza vitendo vya uonevu na vinavyovunja sheria na taratibu za nchi nah ii itawezesha mimi na wakuu wa wilaya kushughulikia masuala ya miradi ya maendeleo badala ya kuhangaika na migogoro ya wananchi .

“Lakini nanukuu katika kitabu cha Mathayo 5:9 Yesu anasema “Heri wapatanishi ,maana hao wataitwa wana wa Mungu”.Hii inaonyesha kuwa kazi ya kupatanisha ni ya Kiungu na inampendeza Mungu”

“Pia kwenye Qur’an inasititiza sana kutenda haki (Uadilifu)kama wajibu Mkuu wa kidini na kijami,ikiamrisha kusimamia haki hata kama ni dhidi ya nafsi zenu waziazi ,au jamaa (Quran 4:1:35,5.8).Uadilifu ni msingi wa imani,ukihimiza kulinda haki za wengine ,kuondoa chuki na kutoa fidia kwa wahasiriwa”Alisema

Aidha aliwataka wadau waelewe kuwa jukumu la kutatua migogoro katika maisha ya watanzania sio la Serikali pekee bali ni la wote wa maendeleo huku akieleza kazi kubwa Serikali iliyonayo ni pamoja na kutengeneza mazingira mamzuri yanayoweza kusaidia kamati hizo.

Alisema hilo linatokana na uwepo wa migogoro mingi katika jamii hasa migogoro ya ardhi na mirathi hivyo kamati hizo zinatakiwa kukaa kila mara kwa ajili ya kutekeleza majukumu yake ya kusikiliza malalamiko ya ksiheria na kutoa elimu kwa umma kwa kushirikiana na ofisi za wakuu wa wilaya.

Hata hivyo alitoa rai kwamba kuna haja ya kuhakikisha kuwa kamati za mkoa na wilaya zinafanya mambo mbalimbali ili kukabiliana na migogoro ikiwemo kuendelea kuboresha kiwango cha utoaji wa huduma ya ushauri wa kisheria na kuongeza wigo na upatikanaji katika maeneo ambayo hayajafanikiwa kufikiwa hasa maeneo ya nje ya jiji.

Mkuu huyo wa mkoa alizitaka kujiwekea utaratibu wa kuandaa kliniki za kisheria bila malipo kwa utaratibu wa kuwafuata wananchi katika maeneo yaona hiyo inatokana na wapo wananchi wengine ambao wanaogopa kuingia kwenye ofisi za Serikali pamoja na wengine hawana uwezo wa kusafiri na kwenda kwenye ofisi hizo.

“Lakini hakikisheni mnapopokea malalamiko au migogoro mnaifuatilia mpaka mwisho ili kujiridhisha namna gani imemalizika na kuweka kumbukumbu ya kufungua na kufunga migogoro hii lengo likiwa kuzuia walalamikaji kurudi kuwasilisha malalamiko yaliyopita hasa pale anapoona uongozi umebadilika “Alisema

Hata hivyo nitoa wito kwa wananchi wote wa mkoa wa Tanga wenye migogoro kutumia nafasi hii kuwasilisha migogoro yenu katika kliniki ya Sheria bila malipo iliyoanza leo kwenye viwanja vya Tangamano mpaka Machi 15 mwaka huu .

Awali akzungumza akizungumza Mkurugenzi wa Uratibu na Huduma za Ushauri kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali Neema Ringo alisema kwamba wamekuja mkoani Tanga kutoa huduma kwa wananchi za kisheria kwa maana yake kutekeleza wajibu wake katika kuwahudumia wananchi ambao ndio wanaipa mamlaka Serikali.

Alisema wakiwa mkoani Tanga watapata fursa ya kusikiliza kero mbalimbali za wananchi na kuweza kuzipatia ufumbuzi huku akiwataka wananchi kuchangamkia fursa hiyo kwa kujitokeza kwa wingi kuweza kupata huduma






Balozi wa Ireland nchini Tanzania, Mhe. Nicola Brennan na uongozi wa Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela (NM-AIST) wamejadiliana namna ya kuimarisha utekelezaji wa mpango wa Samia Scholarship Extended DS/AI+ unaolenga kujenga wataalamu wa Akili Bandia (AI) na Sayansi ya Takwimu (Data Science) nchini.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo iliyofanyika tarehe 9 Machi 2026 katika Taasisi hiyo jijini Arusha, Makamu Mkuu wa NM-AIST, Prof. Maulilio Kipanyula, amesema katika awamu ya kwanza ya mpango huo wanafunzi 34 wa Kitanzania wamepata nafasi ya kusoma katika vyuo vikuu vya Ireland.

Ameongeza kuwa Serikali kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) pamoja na NM-AIST inapanga kuandaa *bootcamp* maalum kwa ajili ya kuwaandaa wanafunzi watakaofuata kunufaika na mpango huo.

Kwa upande wake, Balozi Brennan ameipongeza Serikali ya Tanzania chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa dhamira ya kuwekeza katika elimu ya juu katika fani za AI, Data Science na Sayansi shirikishi, akibainisha kuwa wanafunzi wa Kitanzania watapata elimu yenye viwango vya kimataifa katika vyuo vikuu vya Ireland.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa kuongeza ushiriki wa wanawake katika masomo ya STEM na kuhimiza taasisi na wabunifu kuhakikisha matokeo ya tafiti yanafika sokoni ili kuchangia maendeleo ya uchumi, usalama wa chakula na ajira.

Katika ziara hiyo, Balozi Brennan pia alitembelea maabara, kituo cha kompyuta chenye uwezo mkubwa (HPC), Data Driven Institute (DDI) pamoja na vituo vya ubunifu vya NM-AIST ili kujionea mchango wa taasisi hiyo katika maendeleo ya sayansi na teknolojia nchini.