

📌 Jumla ya Megawati 50 kuingizwa kwenye Gridi ya Taifa ifikapo Machi 1, 2026
📌 Shilingi bilioni 118.6 zatumika katika ujenzi kwa awamu ya kwanza
📌 Maandalizi ya awamu ya pili (MW 100) yaanza.
Tanzania imeandika historia mpya katika sekta ya nishati baada ya kukamilika kwa ujenzi wa Mradi wa Kuzalisha Umeme kwa nishati ya jua ulioko Kishapu, mkoani Shinyanga mradi ambao ni mkubwa na wa kwanza wa aina yake nchini.
Akizungumza Februari 21, 2026 mara baada ya kukagua maendeleo ya mradi huo, Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Bw. Lazaro Twange, amesema kukamilika kwa mradi huo ni ushahidi wa dhamira thabiti ya Serikali ya Awamu ya Sita katika kuimarisha upatikanaji wa huduma ya umeme ya uhakika kwa Watanzania.
“Hii ni historia mpya imeandikwa kwa nchi yetu. Tangu tupate uhuru, hatujawahi kuwa na mradi mkubwa wa aina hii ya umeme wa jua. Serikali kupitia Wizara ya Nishati na TANESCO imeandika historia, na leo mmeshuhudia hapa umeme ukizalishwa. Mpaka kufikia Machi 1, 2026 jumla ya Megawati 50 zitakuwa zimeunganishwa kwenye Gridi ya umeme ya Taifa,” alisisitiza Bw. Twange.
Bw. Twange ametumia fursa hiyo kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuwezesha upatikanaji wa jumla ya Shilingi bilioni 118.6 kwa ushirikiano na Benki ya Maendeleo ya Ufaransa (AFD), fedha zilizowezesha utekelezaji wa awamu ya kwanza ya mradi huo.
Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Kishapu, Mhe. Peter Masindi, amesema mradi huo ni kichocheo muhimu cha ukuaji wa uchumi wa eneo hilo, hasa kwa vijana wanaojishughulisha na uchimbaji wa madini na shughuli za kilimo.
“Mradi huu umeleta ajira kwa wananchi wetu na umefungua ukurasa mpya wa maendeleo. Umeme wa uhakika utaongeza tija katika sekta za madini na kilimo, na kuchochea shughuli za kiuchumi na kijamii kwa wakazi wa Kishapu,” alisema Mhe. Masindi.
Naye Kaimu Meneja wa Kituo cha Kuzalisha Umeme Kishapu, Mhandisi Mariana Mrosso, alieleza kuwa kituo hicho kitaimarisha uthabiti wa Gridi ya Taifa na kuboresha ubora wa upatikanaji wa umeme, hususan kwa wateja wa maeneo ya mikoa ya Kanda ya Ziwa.
“Umeme unaozalishwa hapa utaongeza uwezo wa uzalishaji kwenye Gridi ya Taifa na kuboresha ufanisi wa huduma kwa wateja wetu hasa katika mikoa ya Kanda ya Ziwa,” alifafanua Mhandisi Mrosso.
Imeelezwa kuwa ifikapo Machi 1, 2026, megawati zote 50 zitakuwa zimeunganishwa kwenye Gridi ya Taifa.
Wakati huo huo, TANESCO ipo katika hatua za mwisho za kumpata mkandarasi kwa ajili ya utekelezaji wa awamu ya pili ya mradi huo, itakayozalisha megawati 100 kwa gharama ya Shilingi bilioni 200.4 za kitanzania.
Mradi wa Umeme wa Jua Kishapu unatajwa kuwa alama ya mabadiliko makubwa na hatua muhimu katika mwelekeo wa Tanzania kutumia matumizi ya nishati jadidifu katika uzalishaji wa umeme, hatua inayolenga kuimarisha usalama wa nishati zinazozalishwa nchini na kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii kwa Taifa.
Naibu Mrajis - Uhamasishaji, Consolata Kiluma, amekipongeza chama kikuu cha Ushirika SIMCU (2018) LTD, kwa usimamizi wa ujenzi wa ujenzi na ukarabati wa kiwanda cha kuchakata pamba kilichopo wilayani Maswa mkoa wa Simiyu ambacho kinatarajiwa kuanza kazi musimu huu wa 2026/2027.
Ametoa pongezi hizo leo Februari 21, 2026 alipofanya ziara katika chama hicho kwa lengo kukagua na kuona hatua zilizofikiwa za ujenzi kuelekea uzinduzi wake.
Aidha amewataka viongozi wa SIMCU (2018) LTD, kuendelea kufufua viwanda vingine vinavyomilikiwa na chama ambavyo havifafanyi kazi kwa sasa ikiwa ni sehemu ya kuimarisha ushirika wa viwanda ili kuongeza thamani ya mazao ya wakulima.
Naye, Mwenyekiti wa SIMCU (2018) LTD, Ramadhani Matani, amesema juhudi mbalimbali zinaendelea kuhakikisha kiwanda kinaanza kufanya kazi haraka iwezekanavyo ambapo mpaka sasa wamefikia zaidi ya asilimia 75 ya ujenzi wa kiwanda hicho.

Na OWM - TAMISEMI, Dar es Salaam
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu -TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amewaelekeza Mameneja na waratibu wa Mradi wa Uendelezaji Miundombinu ya Miji Tanzania (TACTIC) kuhakikisha magari 14 aliyoyakabidhi yanakwenda kufanya kazi iliyokusudiwa ya usimamizi wa mradi huo ili wananchi wanufaike na barabara, masoko na stendi zinazojengwa kupitia mradi huo.
Prof. Shemdoe ametoa maelelezo hayo leo Februari 21, 2026, wakati wa hafla ya kukabidhi magari hayo kwa Mameneja wa TARURA wa Miji 12 ya kundi la kwanza la Mradi wa TACTIC, iliyofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Millenium Tower Kijitonyama, Dar es Salaam.
“Magari haya yamenunuliwa kwa fedha za umma, hivyo yatunzwe na yakatumike kwa kazi za usimamizi wa mradi wa TACTIC na si nyinginezo,” amesisitiza Prof. Shemdoe.
Aidha, Prof. Shemdoe amewata wakandarasi walio kwenye maeneo ya utekelezaji wa miradi ya TACTIC, kuhakikisha wanafanya kazi kwa ufanisi kwa kuzingatia mikataba waliosaini ili miradi hiyo ikamilike kwa wakati, na kuongeza kuwa Serikali haitosita kusitisha mikataba inayosuasua kwa mujibu wa sheria na vipengele vya mikataba husika.
Prof. Shemdoe amesema Serikali haina changamoto ya kukosa fedha za utekelezaji miradi, kwani pindi mkandarasi akiwasilisha hati ya maombi ya malipo analipwa kwa wakati, hivyo hakuna sababu ya wakandarasi kushindwa kukamilisha na kukabidhi miradi kwa wakati.
Kwa upande wake, Meneja wa TARURA Wilaya ya Sumbawanga Mhandisi Albert Kyando ameishukuru Serikali kwa kuwakabidhi magari yatakayowawezesha kusimamia miradi ya TACTIC kwa karibu na kuahidi kuwa watayatunza kama Prof. Shemdoe alivyoelekeza kwa maslahi ya umma na taifa.
Naye, Mmoja wa Madereva waliokabidhiwa magari hayo kutoka Jiji la Arusha Bw. Joshua Magati, amesema watayatunza magari hayo kama alivyoelekeza Prof. Shemdoe, na kuongeza kuwa watazingatia muda wa kuyafanyia ukaguzi na matengenezo pamoja na kuyatumia kwa kazi iliyokusudiwa ya usimamizi wa miradi ya TACTIC.
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba anatarajiwa kuanza ziara ya kikazi ya siku tatu Mkoani Arusha kuanzia Februari 22-24, 2026,akitokea mkoa wa Kilimanjaro.
Akizungumza na waandishi wa habari Ofisini kwake leo Jumamosi Februari 21, 2026, Mkuu wa Mkoa wa Arusha CPA Amos Gabriel Makalla amesema Mhe. Waziri Mkuu kesho Jumapili ataweka jiwe la msingi kwenye mradi wa ujenzi wa bweni la kisasa la Chuo kikuu cha Kimataifa cha sayansi cha Nelson Mandela,kisha kukagua upanuzi wa Miundo mbinu ya Hospitali ya Oltrumet pamoja na kuzungumza na wananchi eneo la Ngaramtoni.
"Tarehe 23, Mhe. Waziri Mkuu atakuwa Wilaya ya Longido na atatembelea na kupokea taarifa ya mradi mkubwa wa maji Kata ya Sinya, atazindua mradi wa Upanuzi wa shule ya Sekondari Sinya iliyopanuliwa na kuwa na Kidato cha tano na sita na baadae kutembelea kituo cha utoaji wa huduma za Pamoja (One stop Border Post), Namanga na kisha kuzungumza na wananchi kwenye Viwanja vya shule ya msingi Namanga." Amesema CPA Makalla.
Mhe. Makalla ametumia fursa hiyo kuwaalika wananchi wote kushiriki katika ziara hiyo,ambapo amesema kwa siku ya tatu Mhe. Waziri Mkuu atafanya ziara yake Wilaya ya Arusha akitarajiwa kukagua maendeleo ya Ujenzi wa kituo Kikuu cha mabasi Jiji la Arusha eneo la Bondeni City, na kisha kuweka jiwe la msingi kwenye ujenzi wa soko la Kilombero pamoja na kuzungumza na wananchi kupitia Mkutano wa hadhara kwenye eneo hilo la soko Jijini Arusha.
"Naomba niwaalike waananchi wote wa mkoa wa Arusha kuhudhuria kwa wingi katika ziara hiyo na ambaye anahisi anaweza kutumia fursa hiyo kutoa kero yake anakaribishwa sana sisi kazi yetu ni kusimamia wananchi na kuwasaidia."Amesisitiza CPA Makala
Aidha mkuu huyo wa mkoa amesema kuwa mheshimiwa Waziri Mkuu atatembelea wilaya tatu tu na kisha kuelekea mkoani Dodoma kwa ajili ya Vikao vya Chama kisha baadae atarejea kuendelea na ziara hiyo katika wilaya ya Karatu,Monduli na Ngorongoro.
Miradi hiyo sita ina thamani ya shilingi Bilioni 194.2 kwenye Wilaya za Arumeru, Arusha na Longido ambapo pia atazungumza na wananchi eneo la ngaramtoni Mkoani Arusha.
📌Kuhusisha Mifumo ya umeme jua 20,000 katika visiwa 120
📌Rais Samia awawekea wananchi ruzuku hadi ya asilimia 75 kuunganisha umeme
📌Mhe.Salome asema Serikali itafikisha umeme kwa wananchi bila kujali umbali na mtawanyiko wa makazi
Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba amezindua mradi wa kusambaza mifumo ya umeme jua visiwani unaolenga kuweka mifumo 20,000 ya umeme jua katika visiwa 120 kwa gharama ya Shilingi Bilioni 8 ambapo Rais, Dkt.Samia Suluhu Hassan ameweka ruzuku hadi ya asilimia 75 katika gharama za uunganishaji umeme.
Mhe. Salome Makamba amezindua mradi huo katika kisiwa cha Bezi wilayani Ilemela mkoani Mwanza ambapo mradi huo unatekelezwa chini ya Wakala wa Nishati Vijijini (REA).
"Maeneo ya visiwani na delta yana changamoto za kipekee, zikiwemo umbali kutoka Gridi ya Taifa, gharama kubwa za usafirishaji wa vifaa na mtawanyiko wa makazi unaoongeza gharama za usambazaji wa nishati ya umeme. Hata hivyo, changamoto hizi haziwanyimi wananchi haki ya kupata huduma ndio maana Serikali imekuja na mpango huu mahsusi wa matumizi ya mifumo ya umeme jua pamoja na gridi ndogo kama suluhisho la haraka la kuwafikia wananchi wa visiwa na maeneo ya pembezoni." Amesema Mhe.Salome
Ameeleza kuwa hatua nyingine iliyochukuliwa na Serikali ili kurahisisha upatikanaji wa umeme katika maeneo kama hayo ya visiwa ni pamoja na kutoa ruzuku kwa mifumo ya umeme jua ili kuharakisha upatikanaji wa nishati safi, kupunguza utegemezi wa vyanzo visivyo endelevu kama dizeli, na kuhakikisha gharama za nishati zinakuwa nafuu.
Amesema mradi huo aliouzindua una mchango wa moja kwa moja katika kukuza Uchumi wa Buluu, ambao ni kipaumbele cha Taifa katika maeneo ya pwani na visiwa kwani mifumo ya umeme jua inayofungwa itawawezesha wavuvi kuongeza thamani ya samaki na dagaa kabla ya kupelekwa sokoni, jambo litakaloongeza mapato ya wananchi, Halmashauri pamoja na nchi, kuimarisha shughuli za ufugaji wa samaki (aquaculture), kilimo cha mwani, na huduma za utalii wa fukwe na visiwa, ambazo zote ni sehemu ya Uchumi wa Buluu.
Mhe. Salome amemshukuru Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutoa fedha za utekelezaji wa miradi mbalimbali ya nishati na kueleza kuwa Wizara itaendelea kusimamia kwa ukaribu utekelezaji wa miradi hiyo ili kuhakikisha ubora, uwazi na uwajibikaji vinazingatiwa katika kila hatua.
Aidha, ameiagiza REA na TANESCO kuweka mifumo ya umeme kwa taasisi zinazotoa huduma muhimu kwa jamii kama vituo vya afya, mashule, vituo vya polisi ambavyo hadi sasa bado havijapata huduma hiyo.
Vilevile ameiagiza REA kuchochea matumizi ya nishati safi ya kupikia katika maeneo ya minada, stendi na masoko.Na katika kisiwa hicho cha Bezi wafanye tathmini ya matumizi ya nishati safi katika soko la samaki na kuweka miundombinu ya nishati safi ya kupikia ili kuwalinda wakaangaji na wateja dhidi ya moshi wa kuni na mkaa ambao una athari kwa afya ya binadamu na mazingira.
Kwa upande wake, Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati (Umeme na Nishati Jadidifu), Mhandisi Edson Ngabo amewaasa wananchi kutumia miradi ya umeme kama sehemu ya mabadiliko ya maisha kwa kuhakikisha unatumika pia katika shughuli za kiuchumi.
Amesema Serikali inaendelea kuhakikisha miradi ya nishati jadidifu ikiwemo ya jua inakuwa na mchango mkubwa katika gridi ya taifa na nje ya gridi huku moja ya mifano ukiwa ni mradi huo wa umeme jua wa bei ya ruzuku uliozinduliwa pamoja na mradi wa Kishapu wa megawati 150.
Ameeleza kuwa, Serikali itaendelea kuhusisha sekta binafsi katika utekelezaji wa miradi ya nishati lengo likiwa ni kufikisha megawati 8000 ifikapo 2030.
Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa REA , Mhandisi Jones Olotu amesema mradi huo utakaotekelezwa katika mikoa nane kwa miaka miwili ni sehemu ya utekelezaji wa mpango wa nishati (Energy Compact) ambao moja ya azimio lake ni kufikisha huduma ya umeme kwa wananchi wote ifikapo 2030 na hii ukijumuisha kuunga wateja wapya takriban milioni 8.
Kwa Mkoa wa Mwanza amesema mradi utagusa visiwa 65 kwa gharama ya shilingi bilioni 4.8 ambapo Serikali tayari imetoa shilingi bilioni 3.3 na pesa iliyobaki wananchi watalipia kwa mfumo wa ruzuku.
Mikoa itakayonufaika na mradi wa kusambaza mifumo ya umeme jua visiwani unaolenga kuweka mifumo 20,000 ya umeme jua katika visiwa 120 ni Mwanza, Geita, Kagera, Mara, Rukwa, Lindi, Mtwara na Pwani.










































