



Naibu Katibu Mkuu kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM- TAMISEMI) anayeshughulikia Miundombinu, Mhandisi Rogatus Mativila, amewataka wakandarasi wanaotekeleza miradi mbalimbali chini ya Mradi wa TACTIC kuzingatia viwango vya ubora vilivyoainishwa katika mikataba yao.
Mhandisi Mativila ametoa agizo hilo Mei 29,2026 wakati wa ziara ya ukaguzi wa miradi ya miundombinu inayotekelezwa na TACTIC katika mkoa wa Mara, ambapo amesisitiza kuwa ubora wa kazi ni jambo lisilopaswa kufanyiwa mzaha.
“Katika ziara hii, moja ya mambo muhimu tunayoyaangalia ni ubora wa miradi kwa kuzingatia maelezo yaliyopo kwenye mikataba, hivyo wakandarasi wote mnapaswa kuhakikisha mnatekeleza kazi kwa viwango vilivyokubaliwa,” amesema Mhandisi Mativila.
Ameeleza kuwa wakandarasi wanaposaini mikataba ya utekelezaji wa miradi, wanakuwa wamekubali kutekeleza kazi kwa ubora unaotakiwa, hivyo ni wajibu wao kujisimamia na kuhakikisha wanazingatia masharti yote ya mikataba bila kushurutishwa.
Aidha, Mhandisi Mativila amesema kuwa utekelezaji wa miradi kwa ubora ni sehemu ya kutekeleza maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye amekuwa akisisitiza umuhimu wa kujenga miradi yenye viwango bora ili iweze kudumu kwa muda mrefu na kutoa huduma stahiki kwa wananchi.
Katika ziara hiyo, Mhandisi Mativila amekagua miradi mbalimbali inayotekelezwa chini ya Mradi wa TACTIC, ikiwemo ujenzi wa soko, jengo la Ofisi ya TARURA pamoja na Stendi ya Bweli iliyopo mkoani humo.
Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi, amesema Serikali itaendelea kuweka kipaumbele katika ustawi wa wazee na uwezeshaji wa vijana kupitia utekelezaji wa programu mbalimbali zinazolenga kuboresha maisha yao na kuongeza ushiriki wao katika shughuli za maendeleo ya taifa.
Mhe. Mahundi ameyasema hayo tarehe 30 Mei, 2026 wakati akizungumza na wageni kutoka Taasisi isiyo ya Kiserikali ya Maryprisca Women Foundation wakiongozana na Machifu kutoka Mkoa wa Mbeya waliowasili mkoani Dodoma kwa ziara ya mafunzo na kujionea maendeleo yaliyofikiwa katika Mji wa Serikali Mtumba pamoja na shughuli zinazotekelezwa na Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum.
Amesema Serikali inaendelea kuhakikisha wazee wanapata huduma stahiki ikiwemo bima ya afya na kuishi katika mazingira salama na bora, huku ikiimarisha mikakati ya kuwawezesha vijana kiuchumi kupitia fursa za mikopo, mafunzo ya ujasiriamali na programu mbalimbali za maendeleo.
Katika ziara hiyo, wageni hao walipata fursa ya kutembelea Mji wa Serikali Mtumba na kujionea majengo ya kisasa ya Wizara na Taasisi mbalimbali yaliyojengwa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mMhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, hatua ambayo imeendelea kuifanya Dodoma kuwa kitovu cha shughuli za Serikali.
Aidha, walijifunza kuhusu majukumu na huduma zinazotolewa na Wizara katika kuimarisha ustawi wa jamii, hususan kwa makundi maalum yakiwemo wazee, wanawake, vijana na watu wenye ulemavu.
Kwa upande wao, baadhi ya machifu walioshiriki ziara hiyo wameipongeza Serikali kwa mafanikio makubwa yaliyofikiwa katika ujenzi wa Mji wa Serikali Mtumba na kwa kuendelea kutoa kipaumbele katika masuala ya maendeleo ya jamii.
Pia wamempongeza Mhe. Mahundi kwa juhudi zake katika kusimamia utekelezaji wa mipango inayolenga kuboresha maisha ya wananchi, hususan makundi maalum.
MWISHO










