Na.Mwandishi Wetu
Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela ( NM- AIST) inatumia mbio za marathon kama moja ya mikakati ya kupata fedha za kutoa ufadhili wa masomo kwa wanawake na wasichana ili kuongeza ushiriki wao katika masomo ya Sayansi, Teknolojia, Hisabati na Ubunifu (STEM).
Hayo yamebainishwa Julai 19, 2026 Jijini Arusha wakati wa Maadhimisho ya Mbio za Taasisi hiyo na Katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha, Dkt. Toba Nguvila ambapo amesema kuwawezesha wanawake na wasichana katika masuala ya Sayansi si hisani bali ni uwekezaji wa kimkakati wa Maendeleo ya Taifa
Dkt. Nguvila ameeleza kuwa Dira ya Taifa 2050 inalenga kujenga uchumi wa maarifa unaotegemea ujuzi, utafiti na teknolojia hivyo ametoa wito kwa Taasisi za Elimu ya Juu hususan NM- AIST kuhakikisha tafiti zinazofanyika katika Taasisi hiyoziwe ni zile zizotatua changamoto za wananachi katika sekta za Kilimo, mifugo, madini na viwanda.
Akizungumza awali katika tukio hilo Makamu Mkuu wa Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela Prof. Maulilio Kipanyula amesema kuwa mbio hizo zilianzishwa mwaka 2024 kuhamasisha wasichana kusoma masomo ya sayansi na kutimiza ndoto zao za kuwa madaktari, wahandisi na watafiti.
"Kwa sasa, Mbio za Mandela zimekuwa alama ya mkoa wa Arusha kwa kuchangia ukuaji wa sekta za michezo, elimu, sayansi, afya na utalii. Tukio hili limeweka msingi imara wa kujenga taifa lenye ujumuishi, mshikamano, na kuandaa kizazi kipya cha wanasayansi na wabunifu wasichana na wanawake," amesema Prof Kipanyula
Mbio hizo zilizohusisha umbali wa kilomita 2.5, 5 10 na 21 zimevuta ushiriki mkubwa wa jamii kutoka ndani na nje ya nchi, na kufanya azma ya kuifanya Arusha kitovu cha sayansi na ubunifu barani Afrika kuwezekana.
Mbio za NM- AIST za Mwaka 2026 zina kauli mbiu isemayo Jitihada kwa Sayansi Hatua kwa Mafanikio.

















