SERIKALI imeonya kuwa mtu au taasisi itakayobainika kuharibu au kutenda kosa dhidi ya Miundombinu Muhimu ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (CII) atakabiliwa na adhabu kali kwa mujibu wa Sheria ya Makosa ya Mtandao ya mwaka 2015.

Kaimu Mkurugenzi wa Udhibiti wa Bidhaa Bandia wa Tume ya Ushindani (FCC), Bw.Salvatory Chuwa, akiwasilisha mada  wakati wa Mkutano wa   Maafisa Biashara katika Kikao cha Tatu cha Wizara ya Viwanda na Biashara na Maafisa Biashara, kilichofanyika kwa siku mbili  jijini Dodoma.

Na Mwandishi Wetu

Tume ya Ushindani (FCC) imetoa elimu  kwa Maafisa Biashara kwa lengo la kuwaongezea uelewa kuhusu masuala ya ushindani katika biashara, udhibiti wa bidhaa bandia pamoja na umuhimu wa kumlinda mlaji dhidi ya bidhaa na huduma zisizokidhi viwango.

Semina hiyo imelenga kuwajengea uwezo Maafisa Biashara ambao wana nafasi muhimu katika kusimamia shughuli za biashara katika maeneo yao, ili waweze kutambua changamoto zinazohusiana na ushindani usio wa haki, bidhaa bandia na vitendo vinavyoweza kuwaathiri walaji.

Akitoa mada kuhusu udhibiti wa bidhaa bandia, wakati wa Mkutano wa  Maafisa Biashara nchini katika Kikao cha Tatu cha Wizara ya Viwanda na Biashara na Maafisa Biashara, kilichofanyika kwa siku mbili  jijini Dodoma.

Kaimu Mkurugenzi wa Udhibiti wa Bidhaa Bandia wa FCC, Bw. Salvatory Chuwa, ameeleza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano kati ya FCC na Maafisa Biashara katika kukabiliana na biashara ya bidhaa bandia.

"Bidhaa bandia zina madhara makubwa kwa uchumi, wafanyabiashara wanaofuata sheria na walaji, hivyo ni muhimu kwa Maafisa Biashara kuwa na uelewa wa kutosha kuhusu namna ya kubaini na kutoa taarifa kuhusu bidhaa zinazodhaniwa kuwa bandia."amesema Bw.Chuwa

Amesisitiza kuwa udhibiti wa bidhaa bandia unahitaji ushirikiano wa karibu kati ya taasisi za Serikali, wafanyabiashara na wananchi, huku akiwataka Maafisa Biashara kutumia nafasi zao kuelimisha wafanyabiashara na walaji kuhusu madhara ya bidhaa bandia.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Tafiti, Miungano ya Makampuni na Uraghibishi wa FCC, Bi. Zaytun Kikula, ametoa mada kuhusu masuala ya ushindani, akieleza umuhimu wa kuwepo kwa mazingira ya biashara yenye ushindani wa haki kwa ajili ya kukuza uchumi na kuwapa wafanyabiashara fursa sawa katika soko.

Bi.Kikula amebainisha kuwa ushindani wenye tija husaidia kuongeza ubunifu, kuboresha ubora wa bidhaa na huduma pamoja na kuwapa walaji fursa ya kupata bidhaa bora kwa bei shindani.

Aidha, amewataka Maafisa Biashara kushirikiana na FCC katika kutoa elimu kwa wafanyabiashara kuhusu sheria za ushindani na kuhakikisha kuwa vitendo vinavyoweza kuzuia au kupotosha ushindani vinatambuliwa na kuchukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria.

Semina hiyo ni sehemu ya jitihada za FCC za kuimarisha uelewa wa wadau kuhusu wajibu wa kulinda ushindani katika soko, kudhibiti bidhaa bandia na kuhakikisha haki za walaji zinalindwa.

FCC imeendelea kusisitiza kuwa ushirikiano wa wadau mbalimbali, hususan Maafisa Biashara, ni muhimu katika kujenga soko lenye ushindani wa haki, bidhaa salama na mazingira bora ya biashara kwa manufaa ya wafanyabiashara, walaji na uchumi kwa ujumla.

Kaimu Mkurugenzi wa Udhibiti wa Bidhaa Bandia wa Tume ya Ushindani (FCC), Bw.Salvatory Chuwa, akiwasilisha mada  wakati wa Mkutano wa   Maafisa Biashara katika Kikao cha Tatu cha Wizara ya Viwanda na Biashara na Maafisa Biashara, kilichofanyika kwa siku mbili  jijini Dodoma.

Mkurugenzi wa Tafiti, Miungano ya Makampuni na Uraghibishi wa FCC, Bi. Zaytun Kikula, akiwasilisha mada  wakati wa Mkutano wa   Maafisa Biashara katika Kikao cha Tatu cha Wizara ya Viwanda na Biashara na Maafisa Biashara, kilichofanyika kwa siku mbili  jijini Dodoma.

 Maafisa Biashara nchini wakifatilia mada mbalimbali kutoka kwa wataalamu wa Tume ya Ushindani (FCC) katika Kikao cha Tatu cha Wizara ya Viwanda na Biashara na Maafisa Biashara, kilichofanyika kwa siku mbili  jijini Dodoma.

 Maafisa Biashara nchini wakifatilia mada mbalimbali kutoka kwa wataalamu wa Tume ya Ushindani (FCC) katika Kikao cha Tatu cha Wizara ya Viwanda na Biashara na Maafisa Biashara, kilichofanyika kwa siku mbili  jijini Dodoma.

 



✅YAFUNGUA MILANGO YA UWEKEZAJI KWA SAUDI ARABIA


Shirika la Madini la Taifa( STAMICO) limefanya mazungumzo na ujumbe wa wafanyabiashara kutoka Serikali ya Saudi Arabia kuelezea fursa za uwekezaji zilizopo katika mnyororo wa rasilimali madini kwa manufaa ya watanzania.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO Dkt. Venance Mwasse katika Mkutano uliofanyika Agosti 18 2026 jijini Dar es Salam

Dkt Mwasse, amesema STAMICO inaendelea kufungua milango kwa wawekezaji kulingana na Sheria na taratibu za Serikali ili kuhakikisha inaleta manufaa kwa wote.

Amesema Shirika linazingatia misingi ya kujiendesha kibiashara na kwa uwazi ili kuzuia mianya ya urasimu na kuhakikisha inatoa matokeo yenye tija kwa haraka.

STAMICO, ni Shirika sahihi kuingia nalo ubia kwa kuwa lina wataalam wenye ujuzi na uzoefu wa kutosha, ushirika mzuri na jamii inayozunguka miradi na uwezo wa kushirikiana na taasisi zingine.

Naye, Abdulrahman Al Thobaity Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyabiashara wa Saudia Tanzania, ameshukuru kwa taarifa za fursa za uwekezaji na ushirikiano waliopata kutoka STAMICO.

Kwa upande wa wataalam meneja wa Utafiti Bw Frederick Mangasini Ametumia nafasi hiyo kuonesha fursa za uwekezaji katika miradi mbalimbali ikiwemo ya dhahabu, makaa ya mawe, shaba (copper) na uendelezaji wa wachimbaji wadogo

STAMICO inaendelea kujiimarisha na kuweka mazingira wezeshi ya uwekezaji kwa maslahi ya taifa.










 


Na Munir Shemweta, Tanga

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo, amesema Wizara yake iko tayari kutoa hati miliki za ardhi kwa maeneo yatakayotumika katika shughuli za utafiti, elimu ya ujuzi na ubunifu nchini.

Dkt. Akwilapo ameyasema hayo leo, Agosti 18, 2026, wakati wa uzinduzi wa Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu kwa mwaka 2026, inayoendelea viwanja vya Usagara jijini Tanga.

Amesema, Wizara ya Ardhi iko tayari kushirikiana na taasisi za elimu na utafiti kwa kuhakikisha maeneo yanayotumika katika shughuli hizo yanapatiwa hati miliki ili kuwezesha utekelezaji wa tafiti na ubunifu kwa ufanisi.

“Nichukue fursa hii kuipongeza Wizara ya Elimu, sambamba na kuwashukuru wahadhiri na wakufunzi wote kwa kazi nzuri ya kuandaa vijana katika kazi za ujuzi na ubunifu. Wizara yangu iko tayari kutoa hati miliki katika maeneo ya utafiti,” amesema Dkt. Akwilapo.

Akizungumzia Maonesho ya wiki ya kitaifa ya elimu, ujuzi na ubunifu nchini, Dkt. Akwilapo amepongeza kazi inayofanywa na taasisi za elimu, akisema Tanzania imepiga hatua kubwa katika matumizi ya teknolojia na ubunifu.

“Nipongeze ubunifu pamoja na maonesho. Kwa kweli yamefana sana, na ubunifu mliouonesha ni wa hali ya juu. Nawapongeza kwa yote mnayoyafanya katika taasisi zenu,” amesema.

Dkt. Akwilapo, ambaye aliwahi kuwa katika Wizara ya Elimu, ameeleza kuwa, mabadiliko yaliyofanyika katika sekta hiyo yanaonesha kuwa Tanzania imepiga hatua kubwa, hususan katika mabadiliko ya mitaala na kuibua vipaji vya vijana.

“Mimi nilikuwa Wizara ya Elimu na nilivyoiacha siyo ilivyo sasa. Mmepiga hatua kubwa, mmebadilisha. Tulivyoiacha siyo ilivyo leo. Mmerekebisha mtaala wa Amali na Sera, na matokeo yake tunayoyaona sasa, ambapo vijana wa kidato cha kwanza na cha pili wanaonesha uwezo wao,” amesema.

Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu kwa mwaka 2026 imezinduliwa rasmi na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Adolf Mkenda, ikiwa na lengo la kuendeleza ujuzi, ubunifu na matumizi ya teknolojia miongoni mwa vijana na jamii kwa ujumla.

Kaulimbiu ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu mwaka 2026 ni: “Elimu, Ujuzi na Ubunifu: Njia ya Kufikia Dira ya 2050.”





Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Queen Sendiga, amekabidhi wasanii hao T-shirt rasmi za Manyara Tanzanite Marathon, ikiwa ni sehemu ya maandalizi kuelekea tukio hilo ambalo limeendelea kupata mwitikio kutoka kwa wadau mbalimbali.


Na Mwandishi Wetu, Manyara


Manyara Tanzanite Marathon 2026 inatarajiwa kuwa na burudani ya aina yake baada ya wasanii maarufu nchini, Dully Sykes, Banana Zoro na Mr Blue, kuthibitisha kushiriki na kutumbuiza katika tukio hilo litakalofanyika Agosti 22, 2026 mjini Babati, mkoani Manyara.


Ushiriki wa wasanii hao umewezeshwa na kampuni ya Mati Super Brands Ltd kupitia kinywaji chake cha Tanzanite Royal Gin, hatua inayoongeza ushiriki wa sekta binafsi katika kufanikisha mbio hizo zinazolenga kuunganisha michezo, burudani na shughuli za kijamii.



Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Queen Sendiga, amekabidhi wasanii hao T-shirt rasmi za Manyara Tanzanite Marathon, ikiwa ni sehemu ya maandalizi kuelekea tukio hilo ambalo limeendelea kupata mwitikio kutoka kwa wadau mbalimbali.


Manyara Tanzanite Marathon 2026 imebeba kaulimbiu “Hatua Moja Okoa Maisha”, ikiwa na lengo la kukusanya Shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi wa wodi maalumu ya kuwahudumia watoto njiti wanaozaliwa kabla ya wakati.



Ujio wa Dully Sykes, Banana Zoro na Mr Blue unatarajiwa kuongeza hamasa kwa wanariadha, vikundi vya jogging na wananchi watakaoshiriki au kujitokeza kushuhudia mbio hizo. Burudani hiyo pia inalenga kuwapa washiriki na watazamaji uzoefu wa kipekee huku ikihamasisha jamii kuunga mkono kampeni ya kuokoa maisha ya watoto njiti..



Mchango wa Mati Super Brands Ltd kupitia Tanzanite Royal Gin unaendelea kuonesha nafasi ya sekta binafsi katika kusaidia shughuli zenye manufaa kwa jamii. Ushiriki huo unatarajiwa kuongeza mvuto wa marathon na kuwafikia watu wengi zaidi kupitia michezo na burudani.


Kwa ujumla, Manyara Tanzanite Marathon 2026 inatarajiwa kuwa jukwaa linalounganisha michezo, burudani, utalii na uwajibikaji kwa jamii, huku kila hatua ya washiriki ikilenga kuchangia upatikanaji wa huduma bora kwa watoto njiti mkoani Manyara.






Na Mwandishi Wetu.


Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Queen Sendiga, amezindua rasmi vifaa maalum (KIT) vitakavyotumiwa na washiriki wa Manyara Tanzanite Marathon 2026, huku idadi ya watu waliojiandikisha kushiriki mbio hizo za hisani ikifikia 2,200.


Uzinduzi wa KIT hiyo, inayojumuisha T-shirt, kofia na namba za washiriki, umefanyika Agosti 17, 2026, mjini Babati, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya mwisho kuelekea mbio hizo zinazotarajiwa kufanyika Agosti 22, 2026.


Manyara Tanzanite Marathon 2026 imeandaliwa ikiwa na lengo la kuchangisha fedha zitakazosaidia kuboresha huduma za afya kwa watoto njiti katika Mkoa wa Manyara, hususan katika maeneo yanayohitaji miundombinu na huduma bora zaidi kwa watoto wanaozaliwa kabla ya muda.






Kaulimbiu ya mbio hizo mwaka huu ni “Hatua Moja, Okoa Maisha ya Mtoto,” inayolenga kuhamasisha wananchi, taasisi, kampuni na wadau mbalimbali kushiriki katika tukio hilo huku wakitoa mchango wa moja kwa moja katika kuboresha maisha ya watoto njiti.


Akizungumza katika uzinduzi huo, RC Sendiga amehimiza wananchi na wadau mbalimbali kuendelea kujitokeza kwa wingi kushiriki mbio hizo, akieleza kuwa mwitikio wa watu 2,200 waliojisajili hadi sasa ni ishara ya namna jamii inavyoguswa na ajenda ya kuboresha afya na ustawi wa watoto.


Idadi hiyo ya washiriki inatarajiwa kuongezeka kadri siku ya mbio inavyokaribia, huku waandaaji wakiendelea kutoa wito kwa watu ambao bado hawajajisajili kutumia fursa hiyo kushiriki katika tukio lenye lengo la kuchangia ustawi wa watoto na maendeleo ya afya mkoani Manyara.





Mbali na kushiriki katika mbio hizo, tukio hilo limeandaliwa pia kwa namna inayolenga kukuza utalii wa ndani na kuifanya Manyara kuwa sehemu ya kuvutia kwa wageni kutoka ndani na nje ya Tanzania. Washiriki watakaokuwa wamechagua kifurushi kinachojumuisha ziara ya utalii watapata fursa ya kutembelea Hifadhi ya Taifa ya Tarangire baada ya kumalizika kwa mbio.


Uhusiano kati ya mbio hizo na utalii unalenga kuwapa washiriki uzoefu mpana zaidi, huku ukiendelea kutangaza vivutio vya utalii vilivyopo mkoani Manyara na kuchochea shughuli za kiuchumi zinazotokana na utalii.


Manyara Tanzanite Marathon imeendelea kujijenga kama moja ya matukio yanayounganisha michezo, afya, utalii na uwajibikaji kwa jamii. Kupitia mbio hizo, waandaaji wanatarajia kuhamasisha watu kutoka makundi mbalimbali kushiriki katika jitihada za kuchangia huduma za afya kwa watoto njiti.






Kwa mwaka 2026, msisitizo umewekwa katika kaulimbiu “Hatua Moja, Okoa Maisha ya Mtoto,” huku fedha zitakazopatikana kupitia mbio hizo zikilenga kusaidia ujenzi na uboreshaji wa huduma kwa watoto njiti katika Mkoa wa Manyara.


Uzinduzi wa KIT hiyo umeongeza hamasa kuelekea Agosti 22, ambapo Babati inatarajiwa kuwa kitovu cha tukio hilo litakalowakutanisha washiriki, wadau wa afya, taasisi, wafanyabiashara, watalii na wananchi kwa ujumla katika hatua ya pamoja ya kuokoa maisha ya watoto njiti.

 Mashindano ya 23 ya Shirikisho la Michezo ya Shule za Sekondari Afrika Mashariki (FEASSA) yamepata msukumo mkubwa baada ya Benki ya Maendeleo ya Afrika Mashariki (EADB) kutoa udhamini wa Dola za Marekani 90,000, (takribani mil 240) katika kuunga mkono maandalizi na uendeshaji wa mashindano ya shirikisho hilo yanayoendelea mkoani Morogoro.


Mashindano hayo makubwa zaidi ya michezo ya shule katika ukanda wa Afrika Mashariki yamezikutanisha timu 413 na washiriki 5,548 kutoka nchi mbalimbali za Afrika Mashariki, zinazoshindana katika aina 51 za michezo. Mashindano hayo yanatarajiwa kuhitimishwa Agosti 22, 2026.

Akizungumza katika hafla rasmi ya ufunguzi wa mashindano hayo, Meneja wa EADB nchini Tanzania, Bw. Stephen Wambura, alisema ushirikiano wa Benki hiyo na FEASSA unaakisi dhamira ya EADB ya kuwekeza kwa vijana na kuunga mkono mipango inayochangia maendeleo endelevu katika Afrika Mashariki.

“Ingawa jukumu letu kuu ni kufadhili miradi ya maendeleo katika sekta mbalimbali muhimu za uchumi, tunatambua kuwa maendeleo endelevu hayaishii kwenye miundombinu na shughuli za biashara. Pia yanahusisha kuwawezesha watu, hususan vijana, ambao ndio msingi wa mustakabali wa ukanda wetu,” alisema Bw. Wambura.

Alisema dhamira hiyo ndiyo iliyochochea uamuzi wa EADB kuwa mdhamini mkuu wa Mashindano ya 23 ya FEASSA, kwa kutoa mchango wa Dola za Marekani 90,000 kwa ajili ya kuwezesha mashindano hayo kufanyika kwa mafanikio.

“Udhamini wa michezo ni mojawapo ya nguzo muhimu katika ajenda yetu ya Mipango ya Uwajibikaji wa Kijamii wa Kampuni (CSI), kwa sababu tunaelewa uwezo mkubwa wa michezo katika kujenga tabia, kuhamasisha mtindo bora wa maisha na kufungua fursa kwa vijana katika ukanda wetu,” aliongeza.

“Kupitia udhamini huu, hatuwekezi tu katika mashindano haya, bali pia tunawekeza katika kuwaandaa kizazi kijacho cha viongozi wa Afrika Mashariki.”

Kwa mujibu wa makubaliano ya udhamini, EADB inasaidia utengenezaji wa medali na vikombe kwa ajili ya washindi, pamoja na upatikanaji wa sare za michezo kwa washiriki watakaoshiriki katika hatua za fainali.

Ikiwa mwenyeji wa mashindano ya mwaka huu, Tanzania imetuma moja ya vikosi vikubwa zaidi, ikiwa na timu 127 na washiriki 1,704 wanaoshiriki katika michezo mbalimbali.

Katika mpira wa miguu kwa wavulana, Tanzania inawakilishwa na Shule za Sekondari Nsumba, Mbeya Day, Morogoro na Urambo Day, ambazo zitakuwa na jukumu la kutetea heshima ya nchi katika mashindano hayo.

Kwa upande wa mpira wa miguu kwa wasichana, Tanzania inawakilishwa na Shule za Sekondari Ziba, Fountain Gate na Kilombero, ambazo zinatarajiwa kutumia vyema fursa ya kucheza mbele ya mashabiki wa nyumbani katika kuwania nafasi za juu.

Tanzania pia inalenga kufanya vizuri katika mpira wa wavu. Katika upande wa wavulana, Shule za Sekondari Lumala, Kaliua na Kajunjumele ndizo zinazobeba matumaini ya Tanzania, huku Mengele, Lumala na Mwanhuzi zikiiwakilisha nchi katika mashindano ya wasichana.

Mpira wa kikapu ni miongoni mwa michezo ambayo Tanzania inalenga kutumia vizuri fursa ya kucheza nyumbani. Katika mashindano ya wavulana ya 5x5, Tanzania inawakilishwa na Shule za Sekondari Nsumba, St Jude na Juhudi.

Kwa upande wa wasichana wa 5x5, Shule za Sekondari Orkeeswa, Uru Community na Rungwa ndizo zitakazobeba matumaini ya Tanzania.

Tanzania pia inatarajia kupata matokeo mazuri katika netiboli, mchezo ambao kwa muda mrefu umekuwa miongoni mwa michezo ambayo Tanzania imekuwa ikitoa timu zenye ushindani mkubwa. Shule za Sekondari Mkolani, Vwawa na Mbeya ni miongoni mwa timu zinazotarajiwa kuongoza kinyang’anyiro cha Tanzania katika mchezo huo.

Kwa kuwakutanisha maelfu ya vijana kutoka nchi mbalimbali za Afrika Mashariki, Michezo ya FEASSA haitoi tu jukwaa la ushindani wa kimichezo, bali pia inawapa vijana fursa ya kukuza vipaji, nidhamu, mshikamano, uwezo wa kufanya kazi kwa pamoja na uongozi, huku ikichangia kuimarisha mshikamano na ushirikiano wa kikanda kupitia michezo.

Kadiri mashindano yanavyoelekea kileleni kuelekea tarehe 22 Agosti, Tanzania inalenga kutumia vyema faida ya kuwa mwenyeji ili kujinyakulia medali katika michezo mbalimbali. Kwa upande wake, udhamini wa EADB unaendelea kusisitiza dhamira ya Benki hiyo ya kuunga mkono mipango inayowekeza katika vijana na kuchangia maendeleo ya muda mrefu ya Afrika Mashariki.

Meneja wa Benki ya Maendeleo ya Afrika Mashariki (EADB), Bw. Stephen Wambura (kulia), akikabidhi rasmi sare za michezo kwa Rais wa Shirikisho la Michezo ya Shule za Sekondari Afrika Mashariki (FEASSA), Bw. Justus Mugisha, kwa ajili ya kutumiwa na timu zinazoshiriki katika hatua za fainali za Michezo ya FEASSA zinazoendelea Morogoro, Tanzania. Sare hizo ni sehemu ya udhamini wa Dola za Marekani 90,000 ( takribani mil 240) kutoka EADB kwa ajili ya kufanikisha toleo la 23 la mashindano hayo ya michezo ya shule katika ukanda wa Afrika Mashariki, ambayo yamewakutanisha timu 413 na washiriki 5,548 kutoka nchi mbalimbali za Afrika Mashariki.

 


Dkt.Kiruswa Ataka Ujenzi Kuharakishwa, Asisitiza Uongezaji Thamani Nchini

Tayari WanaKigamboni 278 Wameajiriwa, Zaidi ya Asilimia 90 ni Watanzania

Mwezi Julai Pekee Mkoa wa Kimadini Dar/Pwani Umekusanya Bil 4.06

Tanzania imeingia katika Hatua Mpya ya Uendelezaji wa Madini Tembo (Heavy Mineral Sands), huku shughuli za uchimbaji zikiendelea kupitia Mradi wa Fungoni- Kigamboni na Tajiri sambamba na ujenzi wa Kiwanda cha Uchakataji wa Madini hayo Mkoani Tanga.

Uchimbaji na uchakataji wa Madini Tembo unatekelezwa kupitia Kampuni ya Ubia ya Nyati Mineral Sands Limited, ambapo Serikali inamiliki hisa zisizofifishwa za asilimia 16.

Akizungumza leo, Agosti 18, 2026, alipotembelea na kukagua shughuli za uzalishaji wa madini hayo katika Mradi wa Fungoni- Kigamboni, pamoja na kupata taarifa ya maendeleo ya ujenzi wa kiwanda cha uchakataji Tajiri- Tanga, Naibu Waziri wa Madini, Dkt. Steven Kiruswa, ameitaka kampuni hiyo kuharakisha ujenzi wa kiwanda hicho, akisisitiza dhamira ya Serikali ya kuongeza thamani ya madini nchini kabla ya kusafirishwa nje ya nchi.

Dkt. Kiruswa amesema Serikali imetoa kibali cha muda wa miaka miwili kwa kampuni hiyo kusafirisha madini ghafi nje ya nchi, hatua inayolenga kuipa kampuni nafasi ya kukamilisha ujenzi wa kiwanda na kukuza zaidi mtaji wa mradi.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa kampuni hiyo kuimarisha uhamishaji wa maarifa na ujuzi kwa Watanzania, kuongeza ushiriki wa Watanzania katika shughuli za mradi na kuendelea kuwajibika kwa jamii zinazozunguka maeneo ya mradi.

Vilevile,  Dkt. Kiruswa, amesisitiza kampuni kutekeleza Mpango wa Ufungaji wa Mgodi (Mine Closure Plan) kwa kurejesha maeneo yaliyotumika katika hali salama na yenye tija, huku athari kwa mazingira zikidhibitiwa.

Akielezea maendeleo ya Sekta ya Madini Mkoa wa Kimadini wa Dar es Salaam na Pwani, Dkt. Kiruswa amesema umeendelea kufanya vizuri katika ukusanyaji wa mapato ya Serikali ambapo katika mwaka wa Fedha 2025/26 ulikusanya Shilingi bilioni 27.07 dhidi ya lengo la Shilingi bilioni 24. Kwa mwaka wa fedha 2026/27, mkoa huo umepewa lengo la kukusanya Shilingi bilioni 33, huku tayari imekusanya Shilingi bilioni 4.06 kwa mwezi Julai pekee ambayo ni asilimia 147.50 ya lengo la mwezi ( bilioni 2.75).

Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa Nyati Mineral Sands Limited, Wei Huang, amesema kampuni mama, Shenghe Resources Holding Co. Ltd, imechagua Tanzania kuwa kitovu cha uchakataji wa Madini ya Tembo, ambapo madini yatakayozalishwa katika miradi yake nchi mbalimbali, ikiwemo Madagascar, yatachakatwa  Tanzania.

Amesema tangu mwaka 2024, jumla ya tani 85,000 za Madini Tembo zimezalishwa kupitia mradi wa Kigamboni, ambapo tani 14,793.35 tayari zimesafirishwa.

Akizungumzia thamani ya uwekezaji, Wei amesema miradi ya Kigamboni na Tajiri ina uwekezaji wa zaidi ya Dola za Marekani milioni 30, huku uwekezaji wa kampuni ya Shenghe nchini Tanzania ukifikia takribani Dola milioni 600, ukijumuisha mradi wa uchimbaji na uchakataji wa madini adimu (Rare Earth Elements) unaotekelezwa Mkoani Songwe.

Ameongeza kuwa zaidi ya asilimia 90 ya wafanyakazi katika miradi hiyo ni Watanzania, huku wakazi wa Kigamboni pekee wanaonufaika na ajira wakifikia 284. Kwa Mradi wa Kigamboni, uhai wa mgodi unakadiriwa kuwa miaka minne, huku mradi wa Tajiri, Tanga ukiwa na muda wa miaka 23 ya uwekezaji.

“Shenghe ina uzoefu wa kufanya shughuli hizi katika nchi mbalimbali duniani na tayari tumewekeza Australia, Canada, Nigeria, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na nchi nyingine. Tumeichagua Tanzania kutokana na mazingira ya uwekezaji na historia ya ushirikiano kati ya nchi hizi,” amesema Wei.

Naye, Afisa Tarafa wa Kigamboni, Augusta Safari, aliyemwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Kigamboni, amesema mradi huo umeanza kuleta manufaa kwa Wilaya hiyo kupitia mapato, ajira na utekelezaji wa shughuli za Uwajibikaji kwa Jamii (CSR). Amesema tayari fidia imelipwa kwa wakazi wote waliopisha mradi na Wilaya itaendelea kuhakikisha mazingira salama kwa uwekezaji.

Madini ya Tembo hutumika katika utengenezaji wa bidhaa mbalimbali, zikiwemo rangi za nyumba, vigae vya sakafu na ukutani pamoja na vipuri vya ndege, hivyo kuifanya Tanzania kuwa na fursa kubwa ya kuongeza thamani na kujenga mnyororo wa thamani wa madini hayo ndani ya nchi.