Na Alex Sonna– Dodoma
Kampuni ya Mbolea Tanzania (TFC) imeanza utekelezaji wa mpango mkubwa wa kuongeza upatikanaji wa mbolea nchini kwa kuagiza tani 200,000 za mbolea kwa msimu wa kilimo wa mwaka huu, sambamba na uwekezaji katika viwanda vya kuchanganya mbolea na uchakataji wa chokaa ili kuongeza tija ya uzalishaji wa mazao.
Mkurugenzi Mkuu wa TFC, Samuel Ahadi Mshote, amesema hatua hiyo inalenga kuhakikisha wakulima wanapata mbolea bora kwa wakati, kuongeza matumizi ya pembejeo na kuimarisha usalama wa chakula pamoja na uchumi wa kilimo nchini.
Akizungumza leo Agosti 1,2026 kwenye Maonesho ya 49 ya Kilimo ya Nane Nane yanayoendelea kitaifa katika viwanja vya Dkt.John Samuel Malecela jijini Dodoma, Mshote amesema TFC ina jukumu la kuhakikisha upatikanaji wa mbolea zenye ubora unaokidhi mahitaji ya wakulima, huku ikijiandaa kuanza uzalishaji wa mbolea zinazochanganywa kulingana na afya ya udongo na mahitaji ya mazao mbalimbali.
Amesema katika awamu ya kwanza kampuni imeagiza tani 70,000 za mbolea, ambapo tani 35,000 za mbolea aina ya DAP tayari zimewasili nchini na zinafungashwa katika Bandari ya Dar es Salaam kwa ajili ya kusambazwa kwa wakulima kupitia utaratibu wa pembejeo zenye ruzuku ya Serikali.
Aidha, amesema tani nyingine 40,000 za mbolea aina ya Urea zinatarajiwa kuwasili ndani ya muda mfupi ili kuendelea kukidhi mahitaji ya msimu wa kilimo unaoanza.
"Tunataka kuhakikisha hakuna mkulima anayekosa mbolea kwa sababu ya upungufu wa usambazaji. Ndiyo maana tumejipanga kuongeza uagizaji na kuimarisha mtandao wa usambazaji nchini kote," amesema Mshote.
Amesema TFC imepanua mtandao wake wa huduma kwa kuongeza vituo vya mauzo kutoka nane hadi 26 vilivyopo katika mikoa 22 ya Tanzania Bara, hatua iliyorahisisha wakulima kupata mbolea karibu na maeneo yao.
Mbali na vituo hivyo, kampuni hiyo inashirikiana na zaidi ya mawakala 600 wa pembejeo za kilimo, vyama vya ushirika 29 (AMCOS) pamoja na halmashauri mbalimbali ili kuhakikisha mbolea zinawafikia wakulima hadi ngazi ya vijiji.
Kwa mujibu wa Mshote, tangu TFC ilipoanza kusambaza mbolea mwaka 2022, tayari zaidi ya tani 350,000 za mbolea za ruzuku zimesambazwa kwa wakulima wanaojihusisha na uzalishaji wa mpunga, mahindi, mboga mboga, vitunguu na mazao mengine ya biashara.
Katika hatua nyingine, amesema kampuni hiyo inakamilisha ufungaji wa mtambo wa kisasa wa kuchanganya mbolea katika jiji la Dar es Salaam, ambao utakuwa na uwezo wa kuzalisha tani 300,000 za mbolea kwa mwaka kulingana na mahitaji ya udongo na mazao husika.
Amesema uwekezaji huo utapunguza utegemezi wa uagizaji wa mbolea kutoka nje ya nchi na kuongeza upatikanaji wa mbolea maalumu kwa mazao ya kimkakati kama vitunguu, ufuta, parachichi na mazao mengine yenye thamani kubwa kiuchumi.
Sambamba na hilo,amesema TFC imeanza kutekeleza mradi wa uchimbaji na uchakataji wa chokaa mkoani Tanga baada ya kupatiwa eneo na Halmashauri ya Jiji la Tanga. Chokaa hicho kitatumika kurekebisha tindikali kwenye udongo pamoja na kuwa malighafi muhimu katika uzalishaji wa mbolea.
Mshote amesema mafanikio ya utekelezaji wa mpango wa ruzuku ya mbolea yameongeza matumizi ya pembejeo nchini kutoka tani 300,000 hadi zaidi ya tani milioni 1.2 kwa mwaka, huku takribani asilimia 80 ya wanufaika wakiwa ni wakulima wadogo.
Amesema ongezeko hilo limechangia kuimarika kwa uzalishaji wa mazao na kuiwezesha Tanzania kufikia kiwango cha zaidi ya asilimia 130 cha kujitosheleza kwa chakula.
Aidha, matumizi ya mbolea kwa hekta yameongezeka kutoka kilo 16 hadi kilo 24, huku Serikali na wadau wa sekta hiyo wakilenga kufikia kiwango cha kilo 30 kwa hekta kama kinavyoelekezwa na Azimio la Abuja kuhusu matumizi ya mbolea barani Afrika.
Amesema utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 unahitaji ushirikiano wa karibu kati ya Serikali, sekta binafsi, taasisi za umma na wananchi ili kuhakikisha malengo yaliyowekwa yanafikiwa kwa wakati na kwa ufanisi.
Ameeleza kuwa dhamira ya Serikali ni kuona Tanzania inafikia uchumi shindani, wenye tija na jumuishi ifikapo mwaka 2050, huku akiahidi kuwa wataendelea kusimamia kwa dhati utekelezaji wa mipango na vipaumbele vilivyowekwa ili kuhakikisha maono hayo yanageuka kuwa matokeo yanayoonekana kwa manufaa ya Watanzania wote.
Mshote amewataka wakulima kutembelea banda la TFC katika Maonesho ya Nane Nane ili kupata elimu kuhusu matumizi sahihi ya mbolea na kufahamu aina zinazofaa kwa mazao na mazingira yao, akisisitiza kuwa matumizi ya pembejeo bora ndiyo msingi wa kuongeza tija, kipato cha mkulima na ukuaji wa sekta ya kilimo nchini.
















Na. Mtemi Sona

Na Mwandishi Wetu, Dodoma
Takribani watoto 10,000 nchini wanahusishwa na shughuli za uchimbaji mdogo wa dhahabu zinazotumia zebaki hali inayowaweka katika hatari ya kupata madhara ya kiafya kutokana na sumu ya kemikali hiyo.
Mbali na watoto, wanawake kati ya asilimia 20 hadi 30 katika sekta ya uchimbaji mdogo wa madini pia wanakabiliwa na athari kubwa za kiafya zinazotokana na matumizi ya zebaki, ikiwemo madhara ya mfumo wa fahamu na afya ya uzazi.
Hali hiyo imechochea wadau wa mazingira kutaka biashara ya zebaki duniani ikomeshwe na matumizi yake katika uchimbaji mdogo kusitishwa ifikapo mwaka 2032.
Akizungumza leo Julai 30, 2026 jijini Dodoma katika Warsha ya Mradi wa Marekebisho ya Mkataba wa Minamata kuhusu Zebaki unaotekelezwa na AGENDA kwa kushirikiana na IPEN,Afisa Programu wa AGENDA, Angel Shaniva amesema mbali na kuhusisha watoto, sekta ya uchimbaji mdogo wa dhahabu (ASGM) inakadiriwa kuajiri moja kwa moja zaidi ya watu milioni 1.2 huku zaidi ya watu milioni 7.2 wakitegemea shughuli zake kwa njia zisizo za moja kwa moja.
Shaniva amesema jamii inapaswa kuachana na matumizi ya zebaki (mercury) ili kuwalinda wanawake na watoto dhidi ya athari za kiafya na kimazingira.
Amesema mradi huo unalenga kuongeza uelewa na kujenga ushirikiano kati ya wadau wote ili kuharakisha utekelezaji wa Mkataba wa Minamata na kuunga mkono marekebisho yanayolenga kukomesha biashara ya zebaki duniani pamoja na kuweka tarehe rasmi ya kusitisha matumizi yake katika uchimbaji mdogo wa dhahabu.
Amesema AGENDA imekuwa ikifanya kazi katika maeneo ya mazingira, mabadiliko ya tabianchi, elimu na jinsia, ambapo kupitia zaidi ya miradi 140 iliyotekelezwa imeendelea kukuza ushirikiano na kuongeza uelewa kuhusu masuala ya maendeleo endelevu.
Kwa upande wake Afisa Program wa AGENDA, Clara Benjamin, amesema Tanzania ni miongoni mwa nchi 153 wanachama wa Mkataba wa Minamata unaolenga kulinda afya ya binadamu na mazingira dhidi ya madhara ya zebaki, lakini bado biashara ya kemikali hiyo inaendelea huku kukiwa hakuna tarehe rasmi ya kusitisha matumizi yake katika uchimbaji mdogo wa dhahabu.
Amesema takwimu zinaonyesha biashara ya zebaki duniani imeongezeka kutoka tani 1,200 mwaka 2017 hadi tani 1,700 mwaka 2022, sawa na ongezeko la asilimia 40, huku sekta ya uchimbaji mdogo wa dhahabu ikiendelea kutumia zaidi ya tani 2,000 za zebaki kila mwaka bila dalili za kupungua.
Kwa mujibu wake, maeneo yenye matumizi makubwa ya zebaki nchini ni Geita, Shinyanga, Mbeya na Mara ambako kemikali hiyo hutumika kutenganisha dhahabu, lakini matumizi hayo yameendelea kusababisha uchafuzi wa ardhi, mito na samaki pamoja na madhara makubwa ya kiafya ikiwemo uharibifu wa mfumo wa fahamu na kuhatarisha usalama wa chakula.
Amesema matumizi ya zebaki pia yanahusishwa na biashara haramu ya dhahabu, kuikosesha Serikali mapato na kudhoofisha usimamizi wa sekta ya madini.
Amesema marekebisho yanayopendekezwa katika Mkataba wa Minamata yanataka biashara ya kimataifa ya zebaki ipigwe marufuku isipokuwa kwa matumizi yanayokubalika kimazingira pamoja na kuweka mwaka 2032 kuwa mwisho wa matumizi ya zebaki katika uchimbaji mdogo wa dhahabu.
Kwa upande wake, Afisa Mazingira Mkuu wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), Ahmad Hassan Mbwana, amesema Serikali kwa kushirikiana na Wizara ya Afya na wadau wengine imeendelea kutekeleza miradi ya kupunguza matumizi yasiyo salama ya zebaki kupitia utoaji wa elimu katika mikoa saba ikiwemo Mwanza na Geita.
Amesema wachimbaji wadogo wameendelea kuelimishwa kuhusu madhara ya zebaki, matumizi ya teknolojia salama na umuhimu wa kufanya tathmini za athari kwa mazingira kabla na wakati wa shughuli za uchimbaji.
Mbwana amesema elimu hiyo imechangia kuongeza uelewa kuhusu uhifadhi wa mazingira na pia kuongeza tija ya uzalishaji kwa wachimbaji wanaotumia teknolojia salama, huku uratibu wa wadau na mapitio ya sheria mbalimbali ukiendelea kuboreshwa.
Hata hivyo amesema bado ipo changamoto ya baadhi ya wachimbaji kutokuwa na anuani rasmi za maeneo yao ya kazi, hali inayofanya kuwa vigumu kuwafikia kwa ajili ya ukaguzi wa usalama, utoaji wa elimu na ufuatiliaji wa matumizi ya kemikali hatarishi.
Naye Mkaguzi wa Usalama Mahali pa Kazi (OSHA), Thadei Mwasamila, amesema ni muhimu kuimarisha ukaguzi wa mara kwa mara katika migodi midogo, kubaini vihatarishi na kuhakikisha wachimbaji pamoja na waajiri wanazingatia viwango vya afya na usalama kazini.
Amesema OSHA itaendelea kusisitiza matumizi sahihi ya vifaa vya kinga binafsi, uhifadhi salama wa kemikali na usimamizi wa taka zenye zebaki ili kupunguza madhara ya muda mrefu kwa wachimbaji na jamii zinazozunguka maeneo ya migodi.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa NESODO, Alfred Lugela, amesema kupanda kwa bei ya dhahabu duniani kumeongeza matumizi ya zebaki katika uchimbaji mdogo, huku akieleza kuwa udhibiti wa biashara ya kemikali hiyo unaweza kuhamasisha matumizi ya teknolojia mbadala zilizo salama.
Kutokana na hayo Mhandisi wa Migodi kutoka Wizara ya Madini, Yusuf Yusufu, amesema usimamizi madhubuti wa shughuli za uchimbaji mdogo pamoja na matumizi ya teknolojia mbadala kama gravity concentration na borax ni muhimu katika kulinda afya za wananchi, mazingira na kuongeza tija katika sekta ya madini.
Afisa Mazingira kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais, Tawfiq Halfan, amesema mafanikio ya kupunguza matumizi ya zebaki yatategemea ushirikiano wa Serikali, wadau wa mazingira, wachimbaji na jamii kwa ujumla ili kuhakikisha rasilimali za madini zinatumika bila kuhatarisha afya za wananchi na mazingira.
Kwa mujibu wa wadau hao, kuungwa mkono kwa marekebisho ya Mkataba wa Minamata kutaiwezesha Tanzania kupunguza matumizi ya zebaki, kuimarisha usimamizi wa sekta ya madini na kulinda afya za wachimbaji, wanawake, watoto na vizazi vijavyo.

