Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Mwigulu Nchemba ameipongeza Wizara ya Ujenzi na Wakala wa Barabara nchini (TANROADS), Mkoa wa Rukwa kwa ujenzi wa kiwanja cha ndege cha Sumbawanga kwa ubora.

Amesema hayo leo alipokagua maendeleo ya ujenzi huo na kusisitiza kuwa kiwanja hicho kimejengwa kwa viwango vya kisasa.

" Hongereni wana Rukwa kwa kupata kiwanja cha ndege cha kisasa kitakachochochea fursa nyingi za kiuchumi", amesema Dkt. Nchemba.

Naibu Waziri wa Ujenzi Eng. Godfrey Kasekenya amesema ujenzi wa kiwanja cha ndege hicho unaotekelezwa na mkandarasi M/s Beijing Construction Engineering Group Co Ltd kutoka China umefikia asilimia 96 na utakamilika ifikapo April mosi mwaka huu.

" Tumejipanga kuhakikisha tunawakabidhi kiwanja hiki wenzetu wa Uchukuzi kiwanja hiki kikiwa kimekamilika ifikapo April mosi", amesisitiza Naibu Waziri Eng. Kasekenya.

Eng. Kasekenya amesema kazi ya ujenzi wa njia ya kuruka na kutua ndege, barabara za viungio, maegesho ya ndege na jengo la abiria imekamilika.

Nae Naibu Waziri wa Uchukuzi David Kihenzile amesema wako tayari kukipokea kiwanja hicho mapema mwezi ujao ili kuanza kutoa huduma za ndege mkoani humo.

Kiwanja cha ndege cha Sumbawanga ambacho kilijengwa mwaka 1945 na kukarabatiwa mwaka 1985 kimefanyiwa uboreshaji mkubwa na wa kisasa utakaowezesha ndege za saizi ya kati kutumia kiwanja hicho ambapo zaidi ya shilingi bilioni 60 zimetumika







 


Na Mwandishi Wetu - Pwani


Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) wameipongeza Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA), kusambaza miundombinu ya gesi asilia kwenye kaya takribani 1000 na shule moja ambapo mradi huo umefadhiliwa na Serikali kwa asilimia 100 kupitia REA.

Hayo yamezungumzwa leo Machi 8, 2026 na Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) Bw. Deodatus Balile wakati wa Ziara ya TEF Kutembelea mradi uliofadhiliwa na REA wa ujenzi wa miundombinu ya usambazaji wa gesi asilia kwenye nyumba za makazi mkoa wa Pwani

Bw. Balile amesema kupitia mradi huo Serikali imepunguza kwa kiasi kikubwa utegemezi wa Nishati nyingine kama mkaa wa kawaida, kuni, na mafuta ya taa na nishati gesi asilia sasa inakua ni chanzo cha nishati ya kupikia.

"REA imefanya kazi kubwa sana ya kufadhili mradi huu, hivyo basi mradi huu utaboresha kiwango cha maisha ya walengwa wa mradi kwa kuokoa gharama na muda wa kupika, mazingira safi afya bora na uwezeshaji wa wanawake kuongezeka, " Amesema Bw. Balile.

Kwa upande wake, Kaimu Meneja Usaidizi wa Kiufundi kwa Waendelezaji wa Mradi kutoka REA, Mha. Emmanuel Yessaya amesema kuwa Wakala ulitenga Fedha kwa ajili ya kufadhili mradi ya usambazaji wa gesi asilia kupitia Mfuko wa Nishati Vijijini (REF) ambapo takribani kaya 1000 pamoja na taasisi moja zimenufaika kwa kusambaziwa miundombinu ya gesi asilia kwa ajili ya kupikia majumbani katika mkoa wa Lindi na Pwani.

Mha.Yessaya ameongeza kuwa, Mradi huo ni wa kimkakati kwa ajili ya kupunguza gharama za nishati ya kupikia, kulinda afya za wananchi na kupunguza athari za kimazingira zitokanazo na ukataji wa misitu kwa ajili ya nishati ya kupikia kwa wananchi wanaoishi Vijijini na kwenye vijiji miji.

Kwa upande wake Mhandisi wa mradi huo kutoka Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) Mha. Anthony Karomba, amesema kuwa mradi huo wa kuunganisha wateja wa majumbani kwenye mtandao wa gesi asilia umegharamikiwa kwa fedha nyingi na Serikali kupitia REA na hivyo amewasihi wananchi kuendelea kuilinda miundombinu hiyo.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti wananchi wa Kata ya Kisemvule wameishukuru Serikali kupitia REA kwa kusambaza miundombinu ya gesi asilia ya kupikia katika miji yao. Wameeleza kuwa mradi umenufaisha kaya zao kwa kuokoa gharama, kuongeza muda wa kufanya shughuli za kuzalisha mali, imelinda mazingira, imeboresha afya zao na kuimarisha usawa wa kijinsia kwenye shughuli za kiuchumi.



 

Wakala wa Vipimo (WMA) wameshiriki katika maadhimisho ya Siku ya Wanawake Kimataifa, kwa kutoa elimu ya vipimo kwa wadau mbalimbali waliofika Kongwa, Dodoma mahali ambako sikukuu hiyo imefanyika ngazi ya Mkoa.

Akieleza kuhusu huduma zilizotolewa katika maonesho hayo, Meneja Mawasiliano wa WMA, Veronica Simba amesema ni pamoja na elimu kuhusu uandishi wa alama sahihi za vipimo katika bidhaa pamoja na kuhamasisha matumizi ya vipimo sahihi na kwa usahihi.

"Mahala hapa tumekutana na wanawake wengi ambao ni wajasiriamali na tumefanikiwa kuwapatia elimu ya matumizi sahihi ya vipimo kwa ajili ya biashara zao hivyo tumefanikiwa kama tulivyotarajia," amesema.

Vilevile, Simba ameongeza kuwa wamefanikiwa kutoa elimu ya vipimo kwa makundi mengine mbalimbali ya wanawake, wakiwemo watumishi wa umma, wawekezaji na hata kina mama wa nyumbani.

Amesema kuwa, makundi yote hayo yanahitaji elimu kuhusu umuhimu wa matumizi sahihi ya vipimo ili kila mmoja anufaike kulingana na uhitaji wake.

Awali, Mgeni Rasmi ambaye ni Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule alitembelea Banda la WMA na kuwasisitiza kuelekeza nguvu zaidi katika utoaji elimu ya vipimo kwa wanawake kulingana na shughuli zao za kila siku hususani malezi ya familia na hata biashara.

Katika kuenzi maadhimisho hayo, WMA iliwakilishwa na wafanyakazi wanawake ambao walitoa elimu ya vipimo na huduma nyingine mbalimbali.



Na Mwandishi Wetu
Wanawake wa Tume ya Ushindani (FCC ) wametakiwa kuwa na  upendo ambao utajenga mshikamano na kuleta ufanisi katika Taasisi.
Hayo ameyasema Mwakilishi wa Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, Bi. Magdarena Utouh katika  Maadhimisho  ya Siku ya  Wanawake Duniani ambayo hufanyika kila Machi 8 ya kila mwaka.
Magdelena amesema maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani ni ishara ya kufanya wanawake  kuwa na  nguvu ambayo inatoa mchango katika Taifa pamoja na kuchochea maendeleo.
Amesema kuwa maadhimisho hayo ni pamoja ya kupeleka ujumbe kwa Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan kuwa tuko nyuma yake na tunapiga kazi.
Aidha amesema.kuwa wanawake ni jeshi kubwa hivyo tunahitaji  kuendelea kujituma na kuleta matokeo  katika maeneo yetu ya kazi.
Kauli mbiu ya mwaka ya  Maadhimisho  ya Siku ya Wanawake Duniani  2026 ni Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana: Msingi Jumuishi kufikia Dira 2050.
 
 
 
 
 
 
 
 

Mnufaika wa Programu ya Taifa ya Ukuzaji Ujuzi, Mtawa Vestina Damian akizungumza kwa furaha mafanikio aliyopata kupitia Programu hiyo inayoratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano, tarehe 7 Machi, 2026 katika Chuo cha Laela, Sumbawanga Mkoani Rukwa.

Wanufaika wa Mafunzo ya Uanagenzi yanayotolewa kupitia Programu ya Taifa ya Ukuzaji Ujuzi wakisikiliza maelezo ya Mtawa Vestina Damian kuhusu manufaa aliyopata kupitia Programu hiyo inayoratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano, tarehe 7 Machi, 2026 katika Chuo cha Laela, Sumbawanga Mkoani Rukwa.

Wanufaika wa Mafunzo ya Uanagenzi yanayotolewa kupitia Programu ya Taifa ya Ukuzaji Ujuzi wakiwa katika picha ya pamoja na Wataalamu kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano, walipowatembelea katika Chuo cha Laela, tarehe 7 Machi, Sumbawanga Mkoani Rukwa.

Na: Mwandishi Wetu - Rukwa

Katika kuta za utulivu za Chuo cha Kilimo na Mifugo cha Kanisa Katoliki kilichopo Laela, mkoani Rukwa, sauti ya shukrani imesikika kutoka kwa mtawa mmoja aliyepata fursa ya kipekee ya kujinoa kupitia Programu ya Taifa ya Kukuza Ujuzi (Uanagenzi).

Mtawa Vestina Damian ambaye sasa amekuwa ishara ya matumaini na weledi, anasimulia jinsi mafunzo ya vitendo aliyoyapata yalivyomgeuza kutoka kuwa mwanafunzi wa nadharia na kuwa mtaalamu aliyepikwa vyema.

Maelezo hayo yalitolewa mbele ya Maofisa kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano wakiongozwa na Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini kutoka Ofisi hiyo Revocatus Kassimba walipofika chuoni hapo kufuatilia utekelezaji wa mafunzo ya Uanagenzi.

Sista Vestina Damian, akiwa mmoja wa wanufaika wa programu hiyo, alieleza kwa msisitizo namna mafunzo hayo ya uanagenzi yaliyochukua miezi minane yalivyomjengea weledi wa kitaalamu katika kilimo na ufugaji wa kisasa.

Alibainisha kuwa, kupitia mchanganyiko wa nadharia na vitendo, ameweza kujifunza mbinu za kisasa za kilimo cha umwagiliaji, matumizi sahihi ya mbolea, na mbegu bora zinazohimili mabadiliko ya tabianchi, maarifa ambayo sasa anayatumia kuifanya bustani na mashamba ya utawani kuwa mfano wa kuigwa katika eneo la Laela.

Upande wa mifugo, Sista huyo alieleza kuwa programu hiyo imemsaidia kuelewa kanuni za kitaalamu za ufugaji wa kisasa, ikiwemo ujenzi wa maboma bora, utayarishaji wa lishe mchanganyiko, na udhibiti wa magonjwa.

Aidha, amesema maarifa hayo aliyopata yamemwezesha kusaidia jamii inayomzunguka na hivyo kukuza tija katika kilimo na ufugaji, jambo ambalo linaendana na dhamira ya Serikali ya kuongeza tija na uzalishaji ili kuchochea mageuzi ya kiuchumi.

“Ujuzi huu umenipa heshima kubwa kwa jamii yanguj kwani umenipa uwezo wa kuhudumia watu wangu kwa weledi zaidi,” alieleza Sista Vestina Damian mbele ya maofisa hao na wanajamii wengine.

Vilevile, amesifu uamuzi wa Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano kwa kuweka mfumo unaoruhusu wananchi wa kada zote kupata ujuzi stahiki. Kwake, uanagenzi huo haukuwa tu mafunzo ya darasani, bali ulikuwa ni ukombozi wa fikra uliompa ujasiri wa kwenda kusimamia miradi ya uzalishaji inayolenga kuwasaidia wahitaji na jamii inayomzunguka.

"Naishukuru Serikali, namshukuru mama Samia kwa kutupa fursa hii sisi wananchi wake, bila kujali nafasi zetu," anasema Sista Vestina Damian huyo kwa unyenyekevu.

Alisisitiza katika shukurani zake kuwa ujuzi alioupata chuoni Laela ni hazina itakayotumika kuimarisha ustawi wa jamii kwa ujumla, huku akitoa rai kwa Serikali kuendelea kutanua wigo wa programu hiyo ili kuwafikia vijana na wahitaji wengi zaidi katika maeneo ya pembezoni.

Chini ya kaulimbiu isemayo “Nguvukazi yenye Ujuzi Stahiki kwa Ajira Endelevu". Serikali imeweka bayana dhamira yake ya kupunguza pengo la ujuzi linalowakabili vijana wengi nchini. Programu hii inalenga kuleta mabadiliko ya kifikra na kiuchumi kwa kutoa mafunzo yanayoakisi mahitaji halisi ya soko la ajira, yakijikita katika mchanganyiko wa nadharia na vitendo.

Uzinduzi wa awamu ya nane ya programu hii, umefanyika Machi 8 mwaka huu.Uendelevu wa programu unakuja wakati ambapo nchi inajipanga kuelekea Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050, ikihitaji nguvukazi yenye ushindani wa kimataifa. Katika awamu hii, Serikali imewekeza rasilimali nyingi kuwafikia vijana 5,746 nchi nzima.

Mafunzo yanatolewa kupitia vyuo 46 vilivyosambaa katika mikoa 25 ya Tanzania Bara, ambapo vyuo 29 ni vya Serikali na 17 ni vya sekta binafsi (ikiwemo Chuo cha Laela).

Programu hii ya uanagenzi ni sehemu ya mikakati ya Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano katika kuhakikisha kuwa nguvukazi ya Taifa inapata stadi muhimu za kuajirika au kujiajiri, hivyo kuchochea ukuaji jumuishi wa uchumi kuelekea mwaka 2050.

Na Mwandishi Wetu 
Mbunge wa Jimbo la Mkuranga na Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega, amewataka wananchi wa Wilaya ya Mkuranga kuendelea kuilinda na kuitunza amani ya nchi.Ulega ameyasema hayo wakati wa futari iliyoandaliwa  kwa wananchi  wa Mkuranga pamoja na Watoto Yatima wa Wilaya hiyo ,amesema   mbezi mtukufu wa Ramadhan unatengeneza upendo na mshikamano wa taifa kwa pamoja 

Amesema Kuwa kila mtanzania anatakiwa kuhubiri amani ikiwa ndio nguzo kuendelea  kuijenga nchi

“Tanzania ni nchi ya amani, hivyo ni jukumu la kila mwananchi kuilinda na kuitunza amani hiyo kwa manufaa ya taifa letu,” amesema Ulega.

Aidha, aliwataka wananchi kuendelea kumuombea Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan, ili aendelee kuwa na afya njema na kuiongoza nchi kwa mafanikio.“Tuendelee kumuombea Mheshimiwa Rais wetu awe na afya njema ili aendelee kuiongoza nchi kwa hekima na mafanikio,” ameongeza.

Ulega amesisitiza kuwa kudumisha amani ni jukumu la kila Mtanzania, na kwamba wananchi wanapaswa kushirikiana katika kulinda tunu hiyo muhimu kwa maendeleo ya taifa.

 
 
 
 
 
 
 
Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) Kampasi ya Tanga leo tarehe 7 Machi 2026 kimetekeleza shughuli ya kutoa huduma kwa jamii kwa kutembelea Kituo cha Afya Ngamiani kilichopo jijini Tanga. Katika ziara hiyo, chuo kimetoa msaada wa vifaa tiba pamoja na mahitaji mbalimbali ya msingi kwa watoto waliopo katika wodi ya wazazi.
Sambamba na hilo, watumishi na wanafunzi wa kampasi hiyo wakiongozwa na Mkurugenzi wa Kampasi, Bi. Zawadi Rashidi, walifanya usafi katika maeneo mbalimbali ya kituo hicho ikiwa ni sehemu ya maandalizi kuelekea kilele cha maadhimisho ya miaka 25 ya chuo hicho.
Akizungumza wakati wa kukabidhi misaada hiyo, Bi. Zawadi Rashidi alisema kuwa chuo kina historia na wajibu wa kurudisha kwa jamii inayokizunguka. Alisisitiza kuwa kusaidia jamii ni sehemu ya dhima ya chuo kwa mujibu wa sera zake.
“Msaada huu unaonyesha mapenzi ya dhati kwa jamii inayotuzunguka. Pamoja na wajibu wa kutoa elimu, pia tuna jukumu la kuhudumia jamii inayotuzunguka, hasa katika kipindi hiki ambacho chuo kinasherehekea miaka ishirini na tano tangu kuanzishwa kwake,” alisema.
Aliongeza kuwa msaada uliotolewa unatarajiwa kusaidia kuboresha huduma zinazotolewa katika wodi ya wazazi pamoja na vitengo vingine ndani ya kituo hicho, ambacho kinaendelea kuhudumia wananchi wengi wa jiji la Tanga na maeneo jirani.
Kwa upande wake, Mfamasia wa Kituo cha Afya Ngamiani, Michael Mrosho, aliyepokea misaada hiyo kwa niaba ya Mganga Mfawidhi wa kituo hicho, alishukuru kwa niaba ya uongozi na watumishi wote wa kituo hicho. Alisema msaada huo unaonyesha mapenzi ya dhati ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania kwa jamii inayokizunguka.
“Tunawashukuru kwa msaada huu unaoonyesha upendo wenu kwa jamii, hususan wananchi wa Ngamiani. Kupitia vifaa hivi, utoaji wa huduma kwa wagonjwa utaimarika zaidi,” alisema Mrosho.
Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania kinaendelea na mfululizo wa shughuli mbalimbali za kijamii nchini kote kuelekea kilele cha maadhimisho ya miaka 25 tangu kuanzishwa kwake, kwa lengo la kuimarisha uhusiano kati ya chuo na jamii pamoja na kuendeleza utamaduni wa uwajibikaji kwa jamii.
 
 
 

Wanawake wa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) mkoa wa Dodoma leo Machi 8, 2026 wameungana na wanawake wenzao wa mkoa wa Dodoma, Tanzania na ulimwenguni kuadhimisha Siku ya Mwanamke Duniani, ambapo maadhimisho ya kimkoa yamefanyika katika wilaya ya Kongwa.

Maadhimisho hayo yalipambwa na shamrashamra mbalimbali zikiwemo burudani za ngoma za asili, matarumbeta pamoja na Brass Band ya JKT Makutupora. Mgeni rasmi katika hafla hiyo alikuwa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule.

Mapema asubuhi ya leo, wanawake walikusanyika katika viwanja vya maadhimisho kabla ya kuanza kwa maandamano rasmi. Walionekana kuwa na uchangamfu na kujiamini, hali iliyoonesha ari kubwa ya kushiriki katika maadhimisho hayo muhimu.

Baadhi ya wanawake wa TBA waliozungumza katika maadhimisho hayo wamesema kuwa maadhimisho ya mwaka huu yamekuwa ya kuvutia na yenye kuhamasisha ushiriki wa wanawake katika nyanja mbalimbali za maendeleo.

Akizungumzia maendeleo ya wanawake ndani ya TBA, Afisa Rasilimali Watu wa TBA, Bi. Nashila Iddi amesema kuwa wanawake ndani ya taasisi wamepiga hatua kubwa kitaaluma na kiutendaji.

Amesema kuwa idadi ya wanawake wataalamu kama wahandisi, wakadiriaji majengo (QS) pamoja na wabunifu wa majengo inaendelea kuongezeka kila mwaka, jambo linaloonesha maendeleo chanya katika ushiriki wa wanawake katika taaluma za ujenzi.

“Ndani ya TBA tuna wanawake wengi katika nafasi za uongozi. Yupo Mkurugenzi, wapo mameneja wa mikoa, wakuu wa vitengo pamoja na wasimamizi wa miradi, na wote wanafanya kazi zao kwa ufanisi mkubwa,” amesema Bi. Nashila.

Kwa upande wake, Afisa Manunuzi wa TBA, Bi. Ruth Mwakalinga amesema wanawake wanazidi kujiamini kadri wanavyopata fursa katika maeneo mbalimbali ya kazi.

“Wanawake wanazidi kujiamini kila mwaka, na kila wanapopata nafasi wanaonyesha uwezo mkubwa walionao katika kuleta maendeleo,” amesema.

Naye Maria Paulo, ambaye anafanya kazi katika mradi wa ujenzi wa nyumba 3,500 unaotekelezwa na TBA katika eneo la Nzuguni, amesema wanawake kwa sasa wanajituma zaidi katika utekelezaji wa miradi.

“Wanawake kwa sasa wanajituma sana. Hata hapa kwenye mradi wetu tunaona namna wanavyofanya kazi kwa bidii na kujituma,” amesema.

Siku ya Mwanamke Duniani huadhimishwa kila mwaka Machi 8 ikiwa na ujumbe maalum wa kuhamasisha haki, usawa na maendeleo ya wanawake. Kaulimbiu ya mwaka huu inasema: “Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana ni Msingi Jumuishi wa Kufikia Dira ya Maendeleo 2050.”