Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalumu, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi amewaomba Wakristo na Waislamu mkoani Mbeya kuendelea kutenda mema, kuishi kwa upendo, umoja na amani hata baada ya kumalizika kwa vipindi vya mfungo wa Kwaresma na Ramadhani. 

Ameyasema hayo  katika futari (Iftari)  iliyoandaliwa na Taasisi ya Maryprisca Women Foundation iliyowakutanisha viongozi wa serikali, Jeshi la Polisi, vyama vya siasa, taasisi za kidini pamoja na wananchi wa Kata ya Iwambi na kata jirani, Mahundi amesema waumini wanapaswa kuyaishi mafundisho ya vitabu vitakatifu hata baada ya kumaliza ibada za mfungo na kuendelea kuiombea nchi. 

“Ni wajibu wetu kuyaishi yale yote tunayofundishwa katika vitabu vitakatifu vya dini zetu. Tusiache kuiombea nchi yetu ya Tanzania ili iendelee kuwa na amani na upendo kwa sababu hiyo ndiyo lugha yetu na utamaduni wetu kama taifa,ni wasihi tuendelee kuiamini serikali na kuendelea kudumisha mshikamano maana hii ni tunu yetu watanzania wote ” amesema Mahundi.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Kyela, Josephine Manase, alimpongeza Mhe. Mahundi kwa moyo wake wa upendo kwa jamii na kuwataka viongozi wa dini kuendelea kuwajali watoto yatima pamoja na watu wasiojiweza katika jamii maana hiyo ndio ibada kuu katika maisha ya mwanadamu.

“Katika ibada mnazozifanya msisahau kuwahudumia watoto yatima na wale wasiojiweza kwa sababu kuwahudumia wao ni sehemu ya ibada kubwa na kumbukumbu isiyofutika mbele za Mwenyezi Mungu lakini pia tuendelee kumuombea Rais wetu ili aweze kuendelea kufanya kazi ya kutuletea maendeleo” amesema Manase.

Salamu za Serikali ya Wilaya ya Mbeya zilizowasilishwa na Afisa Tawala wa Wilaya hiyo kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya, Devotha Chacha, zimemhakikishia Mhe. Mahundi ushirikiano wa kutosha katika shughuli zake za kijamii. ambapo Serikali ya Wilaya ya Mbeya itaendelea kushirikiana  kwa karibu na taasisi hiyo kwani kazi wanazozifanya  ni huduma kwa jamii na ni wito kutoka kwa Mwenyezi Mungu"amesema Devotha

Kwa upande wao viongozi mbalimbali wa dini waliohudhuria iftari hiyo wamempongeza Mhe. Mahundi kwa kuendelea kudumisha utaratibu wa kuwakutanisha wananchi wa dini tofauti katika futari hiyo wakisema hatua hiyo inaimarisha upendo, mshikamano na amani katika jamii. 

"Utaratibu huu wa kuwakutanisha watu wa dini mbalimbali ni jambo jema linaloendelea kuimarisha upendo na umoja katika jamii, na tunaona mabadiliko kila mwaka kwa kuwa wananchi wanaendelea kuungana zaidi,” wamesema viongozi hao wa dini.

 

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba leo Machi 15, 2026 ameweka jiwe la msingi la Shule ya Sekondari Mgombe yenye mkondo wa Amali ya Kihandisi iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Mlele, mkoani Katavi, ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kikazi ya kukagua na kufuatilia utekelezaji wa miradi ya maendeleo mkoani humo.

Ujenzi wa shule hiyo unatekelezwa kupitia Mradi wa Kuimarisha Ubora wa Elimu ya Sekondari (SEQUIP) kwa gharama ya shilingi bilioni 1.694 na hadi sasa umefikia asilimia 99 ya utekelezaji.

Shule hiyo itatoa mafunzo ya amali katika fani mbalimbali zikiwemo ufundi magari, ufundi bomba, mifumo ya umeme wa jua pamoja na ufundi umeme wa magari. Mafunzo hayo yanalenga kuwajengea wanafunzi ujuzi wa vitendo utakaowawezesha kujiajiri, kuajiriwa au kuendelea na masomo ya elimu ya juu.



 


Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imefanya ziara ya ukaguzi katika Kituo cha Kupokea na Kupoza Umeme cha Mpomvu kilichopo mkoani Geita tarehe 15 Machi 2026, ikiwa ni sehemu ya ufuatiliaji wa utekelezaji wa miradi ya kimkakati ya Nishati inayolenga kuimarisha upatikanaji wa umeme nchini.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Subira Mgallu amesema ziara hiyo imelenga kukagua maendeleo ya miradi ya nishati pamoja na kuhakikisha uwekezaji unaofanywa na Serikali unaleta matokeo yaliyokusudiwa kwa wananchi.

“Kama Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini tuna jukumu la kuisimamia Wizara ya Nishati ili kuhakikisha inatekeleza majukumu yake kikamilifu. Tumeridhishwa na uwekezaji uliofanywa katika kituo hiki ambacho kina mchango mkubwa katika kuhakikisha upatikanaji wa umeme wa uhakika kwa wananchi na shughuli za kiuchumi,” amesema Mhe. Mgallu.

Ameongeza kuwa Kituo hicho kina uwezo wa kupokea na kusambaza takribani megawati 90, huku jitihada zikiendelea kuboresha miundombinu ya usambazaji wa umeme ikiwemo mpango wa kuongeza laini maalum kwa ajili ya Mgodi wa dhahabu wa Geita (GGM).

“Mahitaji ya umeme ya mgodi wa GGM yanatarajiwa kufikia takribani megawati 70 ifikapo mwaka 2035 kutoka megawati 36 zinazotumika kwa sasa, hivyo ni muhimu kuendelea kuimarisha miundombinu ya usambazaji wa umeme ili kukidhi mahitaji hayo,” ameongeza.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Nishati Mhe. Salome Makamba amesema Serikali inaendelea kuimarisha miundombinu ya umeme katika Mkoa wa Geita kutokana na ukuaji mkubwa wa shughuli za kiuchumi na kijamii hususan katika sekta ya madini.

“Kituo hiki kina mchango mkubwa katika kuimarisha upatikanaji wa umeme katika Mkoa wa Geita pamoja na maeneo ya jirani ikiwemo Biharamulo na Ngara mkoani Kagera, Sengerema mkoani Mwanza na Kakonko mkoani Kigoma,” amesema Mhe. Salome.

Naibu Waziri wa Nishati ameongeza kuwa Kituo cha Mpomvu kimegharimu takribani shilingi bilioni 50, uwekezaji ambao umeongeza uwezo wa usambazaji wa umeme katika eneo hilo linalokua kwa kasi kiuchumi ambapo mahitaji ya sasa ya umeme yamefikia Megawati 73.64.

Awali, Mkoa wa Geita ulikuwa ukipokea umeme kutoka Mkoa wa Shinyanga wenye uwezo wa takribani megawati 4 pekee, kiwango ambacho hakikukidhi mahitaji ya umeme yaliyokuwa yakiongezeka kutokana na shughuli za kiuchumi hususan uchimbaji wa madini.

Kituo cha Kupokea na Kupoza umeme cha Mpomvu kilianza kujengwa mwaka 2019 na kukamilika mwaka 2020, kabla ya kuzinduliwa rasmi mwaka 2022 na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.







 -Akemea watumishi wanaowaelekeza wananchi kununua dawa nje ya hospitali

-Aonya utapeli wa ardhi za vijiji

-Akemea wakandarasi wanaolipwa fedha za miradi lakini hawawalipi mafundi


WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba ameagiza kufanyika kwa uchunguzi kuhusu mfumo wa upatikanaji wa dawa katika hospitali na vituo vya kutolea huduma za afya nchini.

Ametoa agizo hilo leo Jumapili (Machi 15, 2026) alipokuwa akizungumza na wananchi wa Wilaya ya Nsimbo katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika viwanja vya Shule ya Msingi Songambele mkoani Katavi, ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kikazi mkoani humo.

Amesema Serikali imekuwa ikipeleka fedha kwa ajili ya ununuzi wa dawa katika hospitali na vituo vya afya, lakini bado baadhi ya wananchi wanapofika kutafuta huduma wanaelekezwa kwenda kununua dawa katika maduka binafsi nje ya hospitali.

“Takwimu zinaonesha tuna utoshelevu wa dawa lakini mwananchi akienda hospitalini anaelekezwa mtaani kwenda kununua dawa. Huu mchezo haukubaliki. Duka la mtaani linapata wapi dawa ambayo Serikali haiwezi ikapata?” amesema.

Kutokana na hali hiyo, Waziri Mkuu amesema ni muhimu kufanya uchunguzi wa kina ili kubaini namna fedha za ununuzi wa dawa zinavyotumika pamoja na mfumo wa upatikanaji wa dawa katika vituo vya kutolea huduma za afya.

Katika hatua nyingine, Dkt. Mwigulu ameonya tabia ya baadhi ya viongozi kuuza ardhi ya vijiji kwa njia zisizo halali na kusababisha migogoro ya ardhi katika jamii.

“Hata tukigombana ardhi haiongezeki. Binadamu tunaongezeka lakini ardhi haiongezeki. Hata tukipigana ardhi haiongezeki, kwa hiyo tuepuke kuchukiana kwa misingi hiyo,” amesema.

Amesema Serikali haitavumilia vitendo vya utapeli wa ardhi vinavyofanywa na baadhi ya viongozi wasiowaadilifu.

“Watu wa aina hii wakishagundulika wasidunde mtaani lazima wafike kwenye mkono wa sheria. Wanataka kuvunja undugu wetu kwa tamaa na ubinafsi,” amesema.

Kadhalika, Waziri Mkuu ameonya wakandarasi wanaolipwa fedha za miradi ya Serikali lakini wanashindwa kuwalipa mafundi na wakandarasi wadogo waliotekeleza kazi hizo.

“Mkandarasi anapewa kazi anaajiri mafundi, anatoa subcontract kwa wengine, yeye analipwa fedha yote ya mradi lakini hawalipi wale waliofanya kazi. Watu wa aina hiyo wasakwe popote pale walipo na wasiwe huru mpaka wawalipe watu ambao wameshafanya kazi,” amesema.

Amesema vitendo hivyo vinawanyima haki wananchi waliotekeleza kazi kwa uaminifu na vinaweza kuifanya jamii kuilaumu Serikali wakati fedha za miradi tayari zimeshalipwa kwa wakandarasi.

“Hii kuchukua fedha Serikali imeshalipa halafu wananchi wetu ambao wamefanya kazi hawajalipwa ni kuwasababishia umaskini watu ambao wamefanya kazi kwa uaminifu,” amesema.

Katika mkutano huo, Waziri Mkuu amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuwekeza katika miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo sekta za afya, elimu na miundombinu.

Amesema katika kipindi cha miaka minne iliyopita Serikali imejenga hospitali za wilaya 119, vituo vya afya 649 pamoja na zahanati zaidi ya 2,700 nchini kote kwa lengo la kuboresha huduma za afya kwa wananchi.

Aidha, amesema Serikali imejenga zaidi ya shule za sekondari 1,300 pamoja na shule za ufundi zaidi ya 103 ili kuwawezesha vijana kupata elimu na ujuzi unaowawezesha kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo.






 

 

















Na Oscar Assenga,Muheza, Tanga

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais anayeshughulikia Maendeleo ya Vijana, Joel Nanauka amesema serikali itaendelea kuvipa kipaumbele vikundi vya vijana vinavyoonyesha uwajibikaji kwa kurejesha mikopo wanayopewa ili viweze kukuza shughuli zao za kiuchumi.

Nanauka aliyasema hayo leo wakati wa ziara ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii iliyotembelea kikundi cha Vijana cha Mali Hai kilichopo wilayani Muheza mkoani Tanga kwa lengo la kukagua shughuli zao za uzalishaji pamoja na miradi iliyopata fedha kupitia mikopo ya halmashauri.

Akiwa kwenye kikundi hicho alionyesha kuridhishwa na juhudi na nidhamu ya kikundio hicho kurejesha mikopo baada ya kufanikiwa kukuza mtaji wake kutoka shilingi milioni 20 hadi kufikia zaidi ya shilingi milioni 50, hatua inayotajwa kuwa mfano bora kwa vikundi vingine vya vijana nchini.

Nanauka alisema kikundi cha Mali Hali ni miongoni mwa vikundi vichache nchini vilivyofanikiwa kurejesha mikopo kwa wakati, jambo ambalo limekifanya kupata nafasi ya kuangaliwa kwa karibu zaidi katika mipango ya kusaidiwa kuongeza mtaji na kupanua shughuli zake.

Alisema katika mchakato unaoendelea wa kusaidia wajasiriamali wadogo na kurasimisha shughuli zao, serikali itaangalia namna ya kukiweka kikundi hicho kwenye orodha ya vikundi vitakavyosaidiwa ili kuimarisha shughuli zao za uzalishaji.

Aidha, alieleza kuwa serikali inatekeleza maelekezo ya Rais ya kuhakikisha vijana wanaochukua hatua ya kufanya kazi na kuonyesha juhudi wanapatiwa mikopo na serikali ili waweze kujikwamua kiuchumi na pia kutoa ajira kwa wengine.

“Vijana hawa wameonyesha mfano mzuri kwa watanzania wengine wameanza na mtaji mdogo mwaka 2008,wakapata msaada wa shilingi milioni tano mwaka 2018 na baadaye mkopo wa shilingi milioni 20 mwaka wa fedha 2020/2021. Leo hii wameongeza mtaji wao hadi kufikia zaidi ya milioni 50. Huu ni ushahidi kwamba ndoto kubwa zinaweza kuanza na mwanzo mdogo,” alisema Nanauka.

Aliongeza kuwa serikali itahakikisha vijana wenye juhudi kama hao wanapata fursa zaidi, ikiwemo mikopo mingine, pamoja na kushirikishwa katika zabuni za serikali ili waweze kukuza biashara zao.

Nanauka pia aliwashauri vijana nchini kutokudharau mwanzo mdogo na kuwa na uvumilivu wanapotekeleza ndoto zao za kimaendeleo.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii, Hawa Mchafu, alisema kamati hiyo ipo katika ziara ya kawaida ya kukagua miradi ya maendeleo kabla ya kuanza kwa Bunge la Bajeti, ambapo wamepita katika maeneo mbalimbali kutathmini miradi iliyopata fedha za serikali.

Alisema kamati hiyo imevutiwa na kazi nzuri inayofanywa na kikundi hicho cha vijana, lakini imebaini changamoto ya eneo la uzalishaji kuwa dogo na huenda lisiweze kukidhi mahitaji yao iwapo wataongeza mtaji zaidi.

Kutokana na hali hiyo, kamati imeitaka wizara husika kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Tanga kuhakikisha vijana hao wanapatiwa eneo kubwa zaidi la kufanyia shughuli zao za uzalishaji ili waweze kupanua biashara zao.

“Eneo walilonalo sasa ni dogo ukilinganisha na malengo yao ya kupanua uzalishaji hivyo tunashauri wapatiwe eneo kubwa zaidi na lililopo sasa likibaki kama sehemu ya maonesho ya bidhaa wanazozalisha,” alisema Mchafu.

Pia aliishauri serikali kuangalia uwezekano wa kukipa kikundi hicho mkopo mwingine wa kifedha ili kiweze kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazokikabili, ikiwemo kununua gari kwa ajili ya shughuli za uzalishaji na usafirishaji wa bidhaa.

Aidha, alitumia nafasi hiyo kuwakumbusha vijana nchini kutumia fursa zilizotolewa na serikali kupitia mifuko mbalimbali ya maendeleo ya vijana badala ya kujikita kwenye mfuko mmoja pekee.

Mchafu alisema kuwa Rais ametoa zaidi ya shilingi bilioni 200 kwa ajili ya kusaidia maendeleo ya vijana kupitia wizara na taasisi mbalimbali, hivyo vijana wanapaswa kuzitumia fursa hizo kujikwamua kiuchumi.

Kamati hiyo pia imeishauri serikali kuhakikisha sheria ya manunuzi ya umma inayotaka asilimia 30 ya zabuni za serikali zitolewe kwa vijana, wanawake na watu wenye ulemavu inatekelezwa kikamilifu ili kuwapatia vijana nafasi ya kukua kiuchumi.

Kwa sasa kikundi cha Mali Hali kinadaiwa kuajiri vijana zaidi ya 20 katika shughuli zake za uzalishaji, jambo ambalo limeelezwa kuwa linaunga mkono dhamira ya serikali ya kukuza ajira kwa vijana na kuimarisha uchumi wa wananchi.

Vijana wa kikundi hicho pia wamemshukuru Rais kwa kuendelea kutoa fursa na kuahidi kuendelea kufanya kazi kwa bidii ili kufikia ndoto zao za kuanzisha kampuni kubwa inayoweza kutoa ajira kwa vijana wengi zaidi katika Mkoa wa Tanga na maeneo mengine nchini.

Mwisho.

Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum na Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Mbeya kupitia kundi la wanawake, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi, amewataka wanawake kuchangamkia fursa za mikopo inayotolewa na Serikali ili kujiinua kiuchumi na kujenga jamii imara yenye wanawake wanaojitegemea.

Akizungumza akiwa mgeni rasmi katika hafla ya utoaji wa Tuzo za Mwanamke Shujaa mkoa wa Mbeya, Mhe. Mahundi amesema Serikali imeendelea kuweka mazingira bora ya upatikanaji wa mikopo kwa makundi mbalimbali hususan wanawake wanaojishughulisha na biashara ndogo ndogo, ili kuwafikia wanawake wengi zaidi na kuwasaidia kujenga uchumi imara. 

 “Serikali imeweka utaratibu wa mikopo kwa ajili ya kuwainua wanawake kiuchumi. Nawahimiza wanawake kuitumia ipasavyo ili kujenga uchumi imara na kuondokana na utegemezi  Wanawake tukisimama kiuchumi tutaimarisha familia zetu na kuchangia maendeleo ya Taifa kwa ujumla, hivyo ni muhimu kila mwanamke kuona fursa hizi na kuzitumia kwa bidii na uaminifu,” amesema Mahundi.

Kwa upande wake Mkuu wa wilaya ya Kyela, Mhe. Josephine Manase, amewataka wanawake kuzingatia malezi bora ya watoto, kusimamia haki za watoto pamoja na kushirikiana kupunguza vitendo vya ukatili wa kijinsia katika jamii ambapo jukumu la malezi na ulinzi wa watoto linahitaji mshikamano wa jamii nzima hususan wanawake ambao mara nyingi ndio walezi wakuu katika familia.

 “Wanawake tunapaswa kushirikiana na kupeana fursa badala ya kubaguana tukishikamana ndipo uimara wa mwanamke utaonekana na hapo tutakuwa na nguvu kubwa ya kuleta mabadiliko chanya katika jamii ili kujenga nguvu ya pamoja katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi na tukiwa na Uchumi imara hata malezi ya familia zetu yanakuwa bora kwa kuwa tunakuwa na uimara wa akili hivyo na wasihi tuzingatie malezi bora ” amesema Josephine.

Naye mwanzilishi wa tuzo hizo, Sara Nyambura Ndambo, amewashukuru wanawake wote waliojitokeza kushiriki na kuunga mkono shughuli mbalimbali za kijamii pamoja na kuwapongeza wanawake waliotunukiwa tuzo hizo kwa juhudi zao katika jamii.

“Lengo la tuzo za Mwanamke Shujaa ni kutoa motisha kwa wanawake wanaojitoa katika shughuli za kijamii na maendeleo ili waendelee kufanya kazi zao kwa bidii zaidi huku wakihamasisha wengine kufuata nyayo zao na tutaendelea kuboresha tuzo hizi kila mwaka ili ziwe chachu ya kuwahamasisha wanawake wengi zaidi kufanya mambo makubwa katika jamii” amesema Sara.

Hafla hiyo ya utoaji wa Tuzo za Mwanamke Shujaa imewakutanisha wanawake kutoka maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Mbeya na imekuwa jukwaa la kuhamasisha ushiriki wa wanawake katika shughuli za maendeleo, kuimarisha mshikamano wao pamoja na kutambua mchango wa wanawake wanaofanya kazi kubwa katika jamii.

Maafisa wa kulinda walaji kutoka Tume ya Ushindani (FCC) wametoa elimu kwa wananchi wa Halmashauri ya Chalinze mkoani Pwani kuhusu haki na wajibu wa mlaji, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya maadhimisho ya Siku ya Kumlinda Mlaji duniani yanayotarajiwa kufanyika Machi 31, 2026.
Elimu hiyo imelenga kuwajengea wananchi uelewa kuhusu namna ya kutambua bidhaa na huduma zenye ubora, pamoja na hatua wanazopaswa kuchukua pale wanapokutana na udanganyifu au ukiukwaji wa haki zao kama walaji. Wananchi pia wamehimizwa kuhifadhi risiti za manunuzi na kutoa taarifa kwa mamlaka husika wanapobaini vitendo vya biashara visivyozingatia sheria.
Maafisa hao wameeleza kuwa lengo la utoaji wa elimu hiyo ni kuhakikisha walaji wanakuwa na uelewa wa kutosha ili kujilinda dhidi ya bidhaa bandia, bei zisizo halali na huduma zisizokidhi viwango. Aidha, wamesisitiza umuhimu wa wananchi kushiriki kikamilifu katika kulinda maslahi yao kwa kufahamu haki na wajibu wao wanapofanya manunuzi au kutumia huduma mbalimbali.
Maadhimisho ya Siku ya Kumlinda Mlaji hufanyika kila mwaka duniani kote kwa lengo la kuongeza uelewa kuhusu haki za walaji na kuhamasisha biashara kufuata misingi ya haki, uwazi na uwajibikaji katika utoaji wa bidhaa na huduma. Serikali na taasisi mbalimbali nchini huendelea kutumia maadhimisho hayo kutoa elimu kwa jamii ili kujenga mazingira salama na yenye ushindani wa haki sokoni.
 
 
 



Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum na Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Mbeya kupitia kundi la wanawake, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi, ametembelea ofisi za BAKWATA Mkoa wa Mbeya na kukabidhi shilingi milioni tano, kuchangia ujenzi wa Shule ya Sekondari ya BAKWATA Mkoani humo.

Kati ya fedha hizo, shilingi milioni mbili zimetolewa kwa ajili ya ununuzi wa vifaa vya ujenzi ikiwemo nondo na saruji, huku shilingi milioni tatu zikitolewa taslimu kusaidia kuendeleza ujenzi wa shule hiyo.

Akizungumza wakati wa kukabidhi msaada huo, Mhe. Mahundi amesema ataendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kutafuta rasilimali zaidi ili kuharakisha ujenzi wa shule hiyo muhimu kwa jamii.

“Elimu ni msingi wa maendeleo ya jamii. Nitaendelea kutafuta wadau na washirika ili tuongeze nguvu katika kukamilisha ujenzi wa shule hii ambayo itawanufaisha vijana wengi wa Mkoa wa Mbeya,” amesema Mhe. Mahundi.

Kwa upande wake, Sheikh Mkuu wa BAKWATA Mkoa wa Mbeya Ndg.Ayas Njalambaah  amesema shule hiyo haitawahudumia Waislamu pekee bali itakuwa wazi kwa wanafunzi wa dini zote, kwa lengo la kuimarisha elimu na mshikamano wa jamii.

Aidha, amempongeza Mhe. Mahundi kwa moyo wake wa kujitolea katika maendeleo ya taasisi hiyo, akibainisha kuwa hata katika ujenzi wa ofisi za BAKWATA mkoa wa Mbeya, fedha za kuweka jiwe la kwanza zilitolewa na Mhe. Mahundi mwenyewe.

“Tunamshukuru sana Mheshimiwa Mahundi kwa moyo wake wa kujitoa. Ameendelea kuwa sehemu ya maendeleo ya taasisi yetu tangu mwanzo, ikiwemo kufanikisha hatua za awali za ujenzi wa ofisi hizi,” amesema Sheikh huyo.

Ujenzi wa Shule ya Sekondari ya BAKWATA Mkoa wa Mbeya unatarajiwa kusaidia kuongeza fursa za elimu kwa vijana na kuchochea maendeleo ya elimu katika eneo hilo.

 


๐Ÿ“Œ Yasema utekelezaji wa mradi huo umeboresha upatikanaji wa umeme vijijini.

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imeipongeza Wizara ya Nishati kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kasi ya utekelezaji wa mradi wa kusambaza umeme katika vitongoji 15 kwa kila jimbo nchini ili kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi kwa wananchi wa maeneo ya vijijini.

 Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe.Subira Mgalu ametoa kauli hiyo katika ziara ya Kamati hiyo walioambatana na Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba, kukagua utekelezaji wa miradi ya umeme katika vitongoji vya Wilaya ya Kahama mkoani Shinyanga.

Akizungumza katika ziara hiyo, Mhe. Mgalu amesema kuwa Bunge liliidhinisha bajeti ya Wizara ya Nishati kwa mwaka wa fedha 2025/2026 kwa ajili ya kupeleka umeme katika vitongoji 15 kwa kila jimbo Tanzania Bara kupitia REA, mpango ambao umeanza kuonyesha matokeo chanya katika maeneo mbalimbali ya nchi.

Amesema katika Mkoa wa Shinyanga pekee, umeme tayari umefika katika vitongoji 90, jambo linaloonyesha juhudi kubwa za Serikali katika kuhakikisha wananchi wa vijijini wanapata huduma muhimu ya nishati.

“Tunaipongeza Wizara ya Nishati kwa kazi nzuri ya kusimamia mradi huu kupitia REA. Kasi ya usambazaji wa umeme vitongojini inaendelea kuleta matumaini makubwa kwa wananchi na kuboresha maisha yao,” amesema Mhe. Mgalu.

Aidha, ameihimiza REA kuendelea kuongeza juhudi katika kupeleka umeme kwenye taasisi muhimu za umma kama zahanati, vituo vya afya, shule za msingi na sekondari, miradi ya maji pamoja na taasisi za dini ili kuhakikisha wananchi wengi zaidi wananufaika na huduma hiyo.

Amesisitiza Wizara hiyo kusimamia wananchi kuunganishiwa huduma ya umeme katika vitongoji kwa gharama ya Sh.27,000 ili kutimiza maono ya Mhe.Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kuhakikisha umeme unafika katika vitongoji vyote nchini ifikapo mwaka 2030.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome amesema utekelezaji wa miradi ya kupeleka umeme katika vitongoji mkoani Shinyanga unaendelea vizuri na tayari umeanza kuleta manufaa kwa wananchi, hususan katika shughuli za uzalishaji na huduma za kijamii, hali inayoleta tabasamu kwa wananchi.

Amesema ataendelea kushirikiana na Waziri wa Nishati, Mhe.Deogratius Ndejembi, kusimamia maelekezo ya Rais kuhakikisha umeme unawashwa katika vitongoji vyote, sambamba na kauli mbiu ya wananchi wa Mkoa wa Shinyanga ya 'Salome Makamba, Washa umeme'.

Katika ziara hiyo, Kamati ya Bunge pia ilikagua na kuwasha umeme katika Zahanati ya Mine iliyopo Jimbo la Msalala, pamoja na kuwasha huduma ya umeme katika mashine ya kusaga na kukoboa katika Jimbo la Kahama Mjini, huduma zilizopatikana kupitia mradi wa kusambaza umeme vitongoji 15 kwa kila jimbo (HEP IIA).

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo imeiagiza Wakala wa Vipimo (WMA) kuhakikisha mita za umeme zinahakikiwa kikamilifu kabla ya kufungwa kwa ajili ya matumizi, kwa kuzingatia sheria zilizopo ili kulinda haki za watumiaji.

Aidha, Kamati hiyo imeipongeza WMA kwa jitihada za uhakiki na ukaguzi wa vipimo mbalimbali, ikiwemo mita za maji, huku ikiitaka Wakala hiyo kuendelea kusimamia kwa ukaribu vipimo katika sekta ya ujenzi ili kupunguza malalamiko ya wananchi yanayotokana na bidhaa hizo.

Hayo yameelezwa leo Machi 14, 2026, na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Deodatus Mwanyika, wakati wa ziara ya kikazi katika Kituo cha WMA cha Uhakiki wa Vipimo Misugusugu mkoani Pwani kwa lengo la kukagua miradi ya maendeleo na kujionea shughuli za uhakiki wa vipimo zinavyotekelezwa kituoni hapo.

Akizungumza katika ziara hiyo, Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Dennis Londo, aliihakikishia Kamati kuwa wizara itatekeleza maelekezo yote yaliyotolewa.

Alisisitiza kuwa azma ya Serikali ni kuhakikisha WMA inasimamia matumizi ya vipimo sahihi katika uzalishaji na uuzaji wa bidhaa mbalimbali, pamoja na Uhakiki wa mita za umeme na maji, ili kutatua changamoto zinazowakabili wananchi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Kibaha, Mhe. Nickson Simon, akitoa salamu kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani, alibainisha kuwa uhakiki wa vipimo ni uti wa mgongo wa uchumi wa mkoa huo. Alieleza kuwa kwa sasa Mkoa wa Pwani una jumla ya viwanda 1,688, vikiwemo viwanda vikubwa 199 na vidogo sana 1,017, hivyo uhakiki wa usahihi wa Vipimo ni nyenzo muhimu katika kuvutia uwekezaji zaidi.

Naye Ofisa Mtendaji Mkuu wa WMA, Bw. Alban Kihulla, alisema kuwa ukaguzi na uhakiki wa vipimo una nafasi kubwa katika kuhakikisha haki na usawa baina ya pande mbili zinazofanya biashara.

Pia, aliwahimiza wananchi kuhakikisha wanatumia vipimo vilivyohakikiwa, huku akiwasihi watoa huduma kuzingatia uadilifu kwa kutoa huduma kupitia vipimo sahihi ili kuleta usawa na kuhakikisha bidhaa zinazonunuliwa zinaendana na thamani halisi ya fedha.