Na Benny Mwaipaja, Dar es Salaam
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), amesema kuwa Tanzania ina dhamira ya kuimarisha zaidi ushirikiano wa kiuchumi na maendeleo na Serikali ya Jamhuri ya Comoro, ili kuleta manufaa ya pamoja kwa wananchi wa nchi hizo mbili.
Mhe. Balozi Omar, amesema hayo alipokutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Fedha, Bajeti na Sekta ya Benki wa Comoro, Mheshimiwa Moussa Abderemane, kilichofanyika katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha Jijini Dar es Salaam.
Alisema kuwa ushirikiano wa kiuchumi unapaswa kuwa kitovu cha juhudi za kuimarisha uhusiano kati ya Tanzania na Comoro na kuyataja maeneo yenye fursa kubwa za ushirikiano kuwa ni pamoja na biashara na uwekezaji, huduma za kifedha na kibenki, usimamizi wa fedha za umma, maendeleo ya miundombinu, nishati, utalii na kilimo.
Mhe. Balozi Omar alisisitiza umuhimu wa kuweka mazingira rafiki yatakayorahisisha usafirishaji wa bidhaa, huduma, mitaji na wafanyabiashara kati ya nchi hizo mbili na kwamba hatua hiyo inaweza kusaidia kuongeza biashara, uwekezaji na ajira.
Pia, alisema kuwa kikao hicho kilikuwa jukwaa muhimu la kubadilishana uzoefu na mbinu bora katika usimamizi wa uchumi, fedha za umma, ukusanyaji wa mapato ya ndani na ujenzi wa uchumi imara unaojumuisha wananchi wote.
Kwa upande wake, Waziri wa Fedha, Bajeti na Sekta ya Benki wa Comoro Mheshimiwa Moussa Abderemane, aliishukuru Tanzania kwa kuwa mshirika muhimu wa maendeleo ya nchi yake katika nyanja mbalimbali za kiuchumi, kijamii na kiutamaduni.
Alisema kuwa lengo la ziara yake nchini Tanzania, akiambatana na ujumbe wake, lilikuwa kujifunza namna Tanzania ilivyopiga hatua kubwa ya matumizi ya mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika ukusanyaji na usimamizi wa mapato ya Serikali.
Aliahidi kuwa watayatumia matokeo ya ziara yake hapa nchini kuboresha mifumo yao ya ukusanyaji mapato ya Serikali kwa kutumia TEHAMA na mifumo ya kodi hatua itakayochochea zaidi ukuaji wa uchumi wa nchi hiyo.
Kikao hicho kilihudhuriwa pia na Balozi wa Comoro nchini Tanzania,Mhe. Ahamada Elbadaoul Mohamed fakih, Mkurugenzi wa Masoko wa Kanda wa Kampuni ya SoftNet Technologies Bw. Maharage Chande, na viongozi wengine kutoka Tanzania na Comoro.































