Na Mwandishi Wetu, Dodoma
Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA) umewataka vijana wanaoshiriki mpango wa Kujenga kesho bora (Building a Better Tomorrow (BBT) kutumia fursa ya urasimishaji wa biashara ili kuongeza thamani ya shughuli zao za kilimo na ufugaji, hatua itakayowawezesha kushindana katika masoko ya ndani na nje ya nchini.
Wito huo umetolewa leo Agosti 6,2026 jijini Dodoma na Afisa Usajili wa BRELA, Bw. Yusuph Mwasakafyuka,wakati akitoa mafunzo kwa vijana wa BBT, wanaoshiriki katika Maonesho ya 33 ya Kimataifa ya Kilimo (nanenane) Nzuguni jijini Dodoma. “Urasimishaji wa biashara ni nguzo muhimu ya kuwajengea uwezo wa kufanya kilimo cha kisasa kinachozalisha tija, badala ya kuendelea na mifumo ya jadi isiyo na ushindani wa kibiashara”. Amesema Mwasakafyuka.
Aidha amewaeleza vijana hao kuwa; wanapaswa kutambua kuwa mradi wa BBT hauwalengi tu kuwapa ujuzi wa uzalishaji wa mazao na mifugo, bali pia kuwajengea msingi wa kuwa wajasiriamali wenye biashara rasmi zinazotambulika kisheria. Alieleza kuwa kuongeza thamani ya mazao huanza kwa kusajili biashara au kampuni ili kuwapa nafasi ya kupanua shughuli zao na kuvutia masoko pamoja na wawekezaji.
Amefafanua kuwa BRELA imewapatia washiriki hao elimu kuhusu huduma mbalimbali zinazotolewa na taasisi hiyo, ikiwemo usajili wa majina ya biashara, usajili wa makampuni, upatikanaji wa leseni pamoja na usajili wa alama za biashara, hatua ambazo zitawawezesha kulinda bidhaa na huduma zao dhidi ya matumizi yasiyo halali.
Aongeza kuwa elimu hiyo inalenga kuwahamasisha vijana kuanza mapema urasimishaji wa biashara wanazotaka kushughulika nazozao ili wanapohitimu mafunzo na kuanza uzalishaji wa kibiashara wawe tayari kushiriki kikamilifu katika uchumi rasmi, kupata fursa za mikopo, masoko na ushirikiano na taasisi mbalimbali za kifedha. Kwa upande wake Afisa Usajili Mkuu wa Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA) Bw. Nassoro Mtavu, amewahimiza vijana wajasiriamali kutambua umuhimu wa kusajili alama za biashara na huduma ili kulinda bidhaa na huduma zao dhidi ya matumizi yasiyo halali.
Amesema usajili wa alama za biashara pamoja na ulinzi wa hataza ni nyenzo muhimu zinazowezesha wabunifu na wajasiriamali kunufaika na kazi zao, kuongeza ushindani sokoni na kujenga chapa zenye kuaminika ndani na nje ya nchi.
Aidha, amewasisitiza vijana hao kutumia huduma zinazotolewa na BRELA mapema ili kuhakikisha bunifu na biashara zao zinalindwa kisheria, hatua itakayochochea ukuaji wa biashara, kuvutia uwekezaji na kuongeza thamani ya bidhaa za Kitanzania. Aidha, BRELA imeeleza itaendelea kushirikiana na wadau wa maendeleo na programu mbalimbali za kuwawezesha vijana ili kuhakikisha elimu ya urasimishaji wa biashara inawafikia wananchi wengi zaidi, ikiwa ni sehemu ya jitihada za Serikali za kujenga uchumi shindani unaochochewa na biashara rasmi, ubunifu na ongezeko la thamani katika sekta ya kilimo.


















.jpg)








