Mwenge wa Uhuru umeanza mbio zake mkoani Singida ambapo utatembelea, kukagua, kuweka mawe ya msingi na kuzindua miradi ya maendeleo 47 yenye thamani zaidi ya shilingi Bilioni 100. 

Kati ya fedha hizo wananchi wamechangia zaidi ya Milioni 287, Wahisani Bilioni Moja na Serikali Kuu imetoa zaidi ya shilingi Bilioni 30. Makabidhiano ya Mwenge wa Uhuru yamefanyika katika viwanja vya shule ya msingi Chikuyu wilayani Manyoni kati ya Mkuu wa mkoa wa Singida Halima Dendego na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Rozimary Senyamule. 

Rc Dendego amesema kwa mkoa wa Singida Mwenge wa Uhuru utakimbizwa kilomita 800 kwenye Wilaya Tano na Halmashauri Saba za Mkoa huo Aidha, Mkuu huyo wa Mkoa wa Singida amewasisitiza wananchi wa mkoa wa Singida kujitokeza kwa wingi kwa ajili ya kuushangilia Mwenge wa Uhuru pamoja na kusikiliza ujumbe wa mbio za Mwenge wa Uhuru wa Mwaka huu pindi utakapopita kwenye maeneo yao. 

Kwa upande wake, Mkimbiza Mwenge wa Uhuru Kitaifa Godfrey Mnzava, amewaagiza Viongozi wa mkoa wa Singida wahakikishe taarifa zote za utekelezaji wa miradi ya maendeleo kuwepo kwenye maeneo ya miradi yote ili kujua ubora na thamani halisi ya fedha zilizotumika kwenye miradi hiyo ili kujua ubora kuhusu miradi hiyo. 

Mnzava pia amesisitiza nyaraka zote zinazohusiana na miradi kuwepo eneo la miradi pamoja na Wataalamu wote waliosimamia utekelezaji wa miradi itakayopitiwa na Mbio hizo za Mwenge wa Uhuru kuwepo kwenye miradi hiyo ili waweze kutoa ufafanuzi kwa maswali watakaoulizwa na wakimbiza Mwenge wa Uhuru Kitaifa lengo likiwa ni kujua kama miradi hiyo imetekelezwa kwa viwango vinavyotakiwa kulingana na thamani ya fedha. 

Mwenge wa Uhuru ukiwa wilayani Manyoni umetembelea, kukagua, kuweka mawe ya msingi na kuzindua miradi ya maendeleo Saba yenye thamani ya Shilingi Bilioni 2. 

Kauli mbinu ya Mwenge wa Uhuru mwaka huu “Tunza Mazingira na Shiriki Uchaguzi wa Serikali za Mitaa kwa Ujenzi wa Taifa Endelevu”.

Share To:

Post A Comment: