Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango amesema upo umuhimu wa kupitia upya vipengele katika nyaraka zinazoandaliwa na Taasisi ya Kidunia ya  Mikataba ya Ujenzi na Ununuzi (FIDIC) ili kuhakikisha kunakuwa na uwajibikaji katika makosa na madhaifu ya wahandisi washauri.

Makamu wa Rais amesema hayo wakati akifungua Mkutano wa 30 wa Kimataifa wa Wahandisi Washauri Afrika unaofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere Dar es Salaam. Amesema yapo mapungufu yanayosababisha uzembe na kushindwa kukamilisha miradi kwa ubora na muda uliopangwa na hivyo kusababisha hasara kubwa kwa mteja ikiwa ni pamoja na Serikali.

Aidha Makamu wa Rais amesema ni wakati sasa, uandaaji wa nyaraka za mikataba ya ujenzi na ununuzi za FIDIC kuweka kipaumbele matumizi ya wazawa katika miradi husika ili kukuza wahandisi washauri wa ndani kujiongezea maarifa ya kiteknolojia na uzoefu. Amesema Wahandisi washauri wa ndani wanakabiliwa na ukosefu wa ufadhili ikiwemo katika tafiti na maendeleo pamoja na ukosefu wa vifaa vya kisasa tofauti na wahandisi washauri wa kigeni

Halikadhalika Makamu wa Rais amesema kuna tofauti kubwa katika ubora wa ushauri wa uhandisi na elimu ya ufundi shirikishi kote barani Afrika ambayo ubora wake mara nyingi haukidhi mahitaji ya soko la ajira. Amesema jambo hilo linasababisha ugumu katika kubakiza wahandisi washauri wenye talanta barani Afrika ambapo Idadi kubwa ya wahandisi washauri wa juu wamehama bara hilo ili kutafuta fursa zaidi nje ya Afrika.

Makamu wa Rais amewaasa kutumia mkutano huo kutambua umuhimu wa vituo vya ubunifu katika nchi nyingi za Afrika kama jukwaa la wahandisi washauri kushirikiana na kubadilishana mawazo ya kibunifu ili kupata ufumbuzi wa changamoto mbalimbali katika mataifa husika.

Kwa upande wake Prof. Patrick Lumumba ambaye ni mtoa mada katika Mkutano huo ametoa rai kwa Wahandisi barani Afrika kushiriki kikamilifu katika ujenzi wa miundombinu ya Bara hili ili lengo la ufanyaji biashara baina ya mataifa ikiwemo kutumia Ukanda huru wa Biashara Barani Afrika (AfCFTA) liweze kutimia.

Amesema miundombinu barani Afrika imeendelea kuwa changamoto inayokwamisha shughuli mbalimbali za kiuchumi zinazorudisha nyuma maono yaliyokuwepo wakati wa uanzishwaji wa mataifa mengi barani Afrika. Pia Prof. Lumumba amesema bado mataifa mengi yameendelea kutumia wahandisi wa kigeni licha ya mataifa hayo kuwa na wahandisi wazawa waliopata elimu ya katika vyuo vikuu mbalimbali.

Ametoa wito kwa vyuo vya elimu ya juu barani Afrika kuwekeza katika tafiti zitakazosaidia upatikanaji wa nishati kama vile nishati ya jua na nishati ya upepo ili Mataifa yenyewe ya Afrika yaweze kujitegemea katika kuzalisha na kusambaza nishati hiyo.

 

Imetolewa na

Ofisi ya Makamu wa Rais

27 Mei 2024

Dar es Salaam.

Share To:

Post A Comment: