Na Mapuli Kitina Misalaba

Shirika la kuhudumia viwanda vidogo (SIDO) Mkoa wa Shinyanga leo Ijumaa Aprili 26,2024 limefunga mafunzo ya kutengeneza Vihenge ambapo jumla ya vijana 58 kutoka mikoa mbalimbali wakiwemo wa Shinyanga, Geita, Mwanza, Simiyu na Tabora wamenufaika na mafunzo hayo.

Mgeni rasmi katika hafla ya kufunga mafunzo hayo ni kaimu Meneja wa SIDO Mkoa wa shinyanga Bwana Joseph Taban ambaye amewapongeza vijana  kwa kuhitimu mafunzo huku akiwataka kuwa mabalozi wazuri katika jamii kwa kuhakikisha wanatumia ujuzi na maarifa waliyoyapata kuleta matokeo chanya katika jamii.

Mafunzo hayo yalianza Februari 26, 2024 kwa kundi la kwanza washiriki walikuwa 19, kundi la pili washiriki walikuwa 23 na kundi la tatu washiriki walikuwa 16 na kwamba yamefikia kilele leo Aprili26,2024 ikiwa jumla ya wahitimu 58 ambao wamehitimu na kuchukua vyeti vyao.

Bwana Taban amewasihi wahitimu hao kuendeleza umoja na ushirikiano katika kufanikisha ndoto zao kupitia ujuzi wa kutengeneza Vihenge ili kuinuka kiuchumi.

“Ni matumaini yangu kuwa mmepata dozi nzuri ya taaluma na mbinu mbalimbali za kutengeneza Vihenge, mmefundishwa masuala ya ujasiliamali, utengenezaji wa Vihenge kwa nadharia na vitendo, nadharia ya masoko, usimamizi wa fedha na urathimishaji wa biashara”.

“Ni matumaini yangu kuwa mafunzo mliyoyapata mtayatumia kwa vitendo kuhakikisha kuwa lengo la mafunzo haya linatimia, pia natarajia kuwa mafunzo haya yatawawezesha kuongeza kipato cha mtu mmoja mmoja, kaya na taifa kwa ujumla”.

“Mafunzo haya yametolewa kwa vijana wachache lakini wengi wangependa kupata mafunzo haya hivyo nitumie nafasi hii kuwaomba mkawe waalimu wa kufundisha vijana wenzenu kwenye maeneo yenu ya kazi ili kwa pamoja tuweze kupambana kwa vitendo kupunguza kama siyo kuondoa kabisa Sumukuvu”.

“Nitumie nafasi hii kuwapongeza kwa kuwa miongoni mwa vijana wachache waliopata bahati ya kupata mafunzo haya”.

Baadhi ya vijana ambao wamepata mafunzo hayo wamelishukuru na kulipongeza shirika la kuhudumia viwanda vidogo SIDO Mkoa wa Shinyanga kwa kutoa mafunzo hayo na kwamba wamesema yatawasaidia kwa kiasi kikuwa kuboresha utendaji wa kazi na kuzalisha bidhaa za Vihenge (Silos) na nyinginezo kwa tija ili kukidhi mahitaji ya soko la ndani na nje ya taifa la Tanzania.

Akisoma risala ambayo imeandaliwa na wahitimu wa mafunzo ya mradi wa kuthibiti Sumukuvu nchini kutoka kituo cha SIDO Mkoa wa Shinyanga Wanjala Daud amesema kwenye mafunzo hayo wamejifunza kwa nadharia na mada mbalimbali ikiwemo ujasiliamali, utengenezaji wa Vihenge kwa vitendo (Silos), nadharia ya masoko na huduma kwa wateja, usimamizi wa fedha pamoja na urasimishaji wa biashara.

“Tunapenda kushukuru uongozi wa SIDO na Wizara ya Kilimo kwa kutoa fursa ya mafunzo haya hakika yametujengea uwezo wa kujiamini na kuamsha ari ndani yetu ya kujiajiri na kuachana na kasumba ya kusubiri ajira”.

“Pamoja na ari na molari ya kujiajiri iliyojengeka ndani yetu tunakabiliwa na changamoto ya mitaji kwa ajili ya kununua vifaa au vitendea kazi vya kuanzisha shughuli mbalimbali kutoka na fani tulizojifunza hivyo tunaomba serikali ituangalie kwa jicho la kipekee ili tuweze kujikwamua na changamoto hii na hatimaye tuweze kujiajiri wenyewe hivyo kuchangia uchumi wetu na jamii huku tukitokomeza kabisa Sumukuvu kwa taifa letu hili la Tanzania”.

SIDO Mkoa wa Shinyanga imetekeleza mradi wa kuzuia Sumukuvu wa ‘Tanzania initiative for preventing aflatoxin contamination’ (TANIPAC) ambao upo chini ya Wizara ya Kilimo na kwamba mradi huo umelenga kuendelea kutoa elimu kwa wananchi ili kuimarisha usalama wa chakula na kuimarisha Afya ya jamii.

Mradi wa TANIPAC pia umelenga kuwezesha jamii kutumia njia sahihi na za kisasa za uhifadhi wa nafaka hususan Mahindi kutokana na Sumukuvu.

Serikali imeingia gharama kuhakikisha kuwa vijana wanapatiwa ujuzi wa kutengeneza vifaa vya kisasa na vinavyo dumu kwa muda mrefu (Vihenge) ili kutimiza adhima ya kupunguza Sumukuvu.

SIDO inawapatia wajasiliamali wadogo na wa kati huduma mbalimbali ikiwemo teknolojia na uendelezaji viwanda, mafunzo na usimamizi wa Mikoa, masoko na uwekezaji pamoja na huduma za fedha.

Kaimu Meneja wa SIDO Mkoa wa Shinyanga Bwana Joseph Taban akiwa katika zoezi la kukagua Vihenge vilivyotengenezwa na vijana ambao wamehitimu mafunzo ya kutengeneza Vihenge kupitia mradi wa kuthibiti Sumukuvu  wa ‘Tanzania initiative for preventing aflatoxin contamination’ (TANIPAC) ambao upo chini ya Wizara ya Kilimo.



 

Share To:

Misalaba

Post A Comment: