Mbunge wa Jimbo la Dodoma Mjini  Anthony Mavunde amezindua jengo la wodi ya wazazi la Zahanati ya Kikuyu Kaskazini lililojengwa kwa pamoja kwa fedha za Mfuko wa Jimbo na Halmasauri ya Jiji la Dodoma na kulikabidhi kwa uongozi wa zahanati kwa ajili ya matumizi.

Mbunge Mavunde ameyafanya hayo jana katika Zahanati ya Kikuyu Kaskazini katika hafla fupi iliyojumuisha pia utoaji wa gari la wagonjwa(Ambulance) pamoja na vifaa tiba kwa ajili ya vituo vya Afya Dodoma Jiji.

“Tunamshukuru sana Mh. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa magari ya wagonjwa na vifaa tiba kwa vituo vya Afya Jijini Dodoma.

Ninawashukuru wadau wote kwa pamoja tuliokamilisha ahadi ya ujenzi wa wodi ya wazazi yenye thamani ya Tsh 84,000,000 na hivyo kuwaondolea adha wakina mama ambao walikuwa wanapata huduma katika jengo la awali.

Katika kuboresha mazingira ya zahanati hii nitahakikisha tunaanza ujenzi wa uzio mapema iwezekanavyo ili eneo letu liwe salama na lenye staha.

Moja ya jambo nitakalolifanya siku chache zijazo ni upatikanaji wa magari mawili ya wagonjwa(ambulance)”Alisema Mavunde

Wakiongea kwa nyakati tofauti Naibu Meya wa Jiji la Dodoma Asma Karama Diwani wa Kata ya Kikuyu Kaskazini  Israel Mwansasu na Mganga wa Zahanati ya Kikuyu Kaskazini Dkt. Azania Silliah Shekimweri wameshukuru Mbunge Mavunde kwa kuanzisha ujenzi wa jengo la wodi ya wazazi na kusaidia kutatua changamoto kubwa ya ufinyu wa eneo la kuwahudumia wakinama wakati wa kujifungua.

Akitoa salamu zake,Mkuu wa Wilaya Dodoma Alhaj Jabir Mussa Shekimweri amesema sekta ya Afya Dodoma Jiji inaendelea kuimarika kutokana na mchango mkubwa unaotolewa na Serikali chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan na Mbunge Mavunde na hivyo kuwataka wataalamu wa Afya kuboresha huduma za Afya kwa wananchi na kutunza vifaa vyote vilivyotolewa na kuhakikisha vinafanya kazi iliyokusudiwa.

Share To:

Post A Comment: