Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb), amefunga vikao vya majadiliano kati ya Serikali na Timu ya Wataalam kutoka Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) baada ya kukamilisha tathimini ya utekelezaji wa program ya Extended Credit Facility-(ECF), inayohusisha upatikanaji wa mkopo nafuu kwa ajili ya kuchachua uchumi kupitia sekta za uzalishaji na huduma za jamii.

Akifunga vikao hivyo katika Kikao cha majumuisho kilichofanyika Benki Kuu ya Tanzania, jijini Dar es Salaam, Dkt. Nchemba, alieleza kufurahishwa kwake na taarifa ya awali ya Timu hiyo iliyowasilishwa na Kiongozi wa Timu hiyo Bw. Harris Charambos Tsangarides, inayoonesha kuwa Tanzania imetekeleza ipasavyo vigezo vilivyowekwa na Shirika hilo la Fedha la Kimataifa IMF na kwamba itaendelea kusimamia ipasavyo program hiyo yenye thamani ya dola za Kimarekani bilioni 1.1 ambazo ni sawa na shilingi trilioni 2.4, ambayo itatekelezwa katika kipindi cha zaidi ya miaka mitatu.

Aidha, Dkt. Nchemba, alitumia nafasi kurejea maombi ya Tanzania kwa IMF, kuisaidia Serikali kupata fedha kupitia dirisha lake la Resilient and Sustainable Trust (RST), kwa ajili ya kutekeleza miradi mbalimbali ya kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Kwa upande wake Kiongozi wa Timu hiyo ya IMF Bw. Harris Charambos Tsangarides, amesema kuwa tathimini yao imeonesha kuwa Tanzania imetekeleza vizuri mpango wa ECF na kushauri hatua kadhaa zinazotakiwa kuchukuliwa ili nchi ipate fedha za kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi ikiwemo uzingatiwaji wa vigezo vya kuchachua uchumi kupitia sekta za uzalishaji na huduma za jamii kupitia Bajeti ya Serikali.

Tanzania inajiandaa kufanyiwa Tathimini ya awamu ya tatu ili iweze kupata fedha kutoka IMF kwa ajili ya kutekeleza miradi mbalimbali ya kiuchumi na kijamii ambapo hadi sasa nchi imepokea kiasi cha dola za Marekani milioni 455.3 kati ya dola za Marekani bilioni 1.1 ambazo Tanzania itanufaika katika kipindi cha kuanzia mwaka wa fedha 2023 hadi mwaka 2026.

Share To:

Post A Comment: