WAKAZI wa Kijiji cha Utiga halmashauri ya Wanging'ombe mkoani Njombe wameushukuru Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) kwa kuchangia fedha za ujenzi wa zahanati, vyumba vya madarasa, nyumba ya mwalimu na kisima hivyo, kupunguza adha zilizokuwa zinawakabili.


Kabla ya ujenzi huo, wananchi hao wamesema walikuwa wakitembea umbali wa Kilometa tano kwenda kituo cha afya Wanging'ombe hali iliyochangia wanawake kujifungulia njiani na hata wengine kupoteza maisha.

Akizungumza na wahariri wa vyombo mbalimbali vya habari nchini, waliotembelea miradi inayofanywa na TASAF mkoani Njombe hivi karibuni, Upendo Kalesi amesema moja ya changamoto waliyokabiliana nayo ni ktembea umbali wa Kilometa tano kutoka kijiji hicho hadi Wanging'ombe hivyo hali iliyokuwa inawapelekea kupoteza mgonjwa iwapo akizidiwa njiani.

"Tunaishukuru sana serikali ya awamu ya sita kusaidia Kijiji chetu kupata huduma karibu. Tunaomba serikali ituwezeshe vifaa vya kujifungulia kwani tunapata shida wanapopata uchungu," amesema

Ameeleza kuwa baadhi ya wanawake hujifungua njiani kwa kushindwa kufika kwa wakati hospitalini kutokana na miundombinu mibovu na umbali.

Amesema kijiji hicho kinawatu wengi na kwamba wanaojifungulia njiani, hukimbizwa Wanging'ombe ili kuwasaidia kukabiliana na hatari.

Mwananchi mmoja, Edson Wigenge anasema, awali walikuwa wanapata usafiri wa shida wanatumia pikipiki na kutokana na umbali, wanashindwa kufika kwenye vituo vya afya kwa wakati hivyo kusababisha wanawake kujifungua njiani.

"Tunaomba kulingana na miundombinu iliyopo watupatie usafiri wa magari yawe yanapita ili kurahisisha huduma kwani kwa siku gari lipo moja," amesema.

Mganga Mfawidhi wa Zahanati ya Utiga, Dkt. Peter Sumuni amesema zahanati hiyo imeanza kutoa huduma mwaka 2023 kutokana na juhudi za TASAF na wanakijiji.

Amesema kwa pamoja waliamua kusogeza huduma za afya karibu na wananchi na kwamba kwa wastani wa watu 8 huhudumiwa kwa siku.

Dkt. Sumuni amesema kabla ya kujengwa kwa zahanati hiyo wananchi wengi walikuwa wanapata matibabu katika hospitali ya Wanging'ombe.

"Tangu kuanza kwa zahanati yetu imepunguza msongamano wa wagonjwa waliokuwa wanapata matibabu katika kituo cha Wanging'ombe Huduma tunazotoa ni matibabu ya nje," amesisitiza.

Mwenyekiti wa kijiji cha Utiga, Sadick Kisakanyike amesema walikuwa wanatumia zahanati ya Wang'ing'ombe na baada ya kuona wanapata huduma mbali, walikaa kikao na wananchi ili kujenga Zahanati hiyo.

Amesema TASAF iliwapatia zaidi ya Sh milioni 300 kwa ajili ya ujenzi wa zahanati, nyumba ya mganga, nyumba za walimu, madarasa na kisima.

"Tuligawa vitongoji kwa ajili ya wananchi kuchangia ujenzi huu. Tunaishukuru TASAF kutusaidia kupunguza adha ya wagonjwa kutembea umbali mrefu," amesema

Mwalimu wa Shule ya Msingi Utiga, Athuman Kindole amesema shule hiyo ina wanafunzi wengi katika halmashauri ya Wang'ing'ombe kwani ina jumla ya wanafunzi 667.

Amesema TASAF iliwapatia fedha kwa ajili ujenzi wa madarasa mawili, ofisi, nyumba ya mwalimu na matundu sita ya vyoo.

"Kulikuwa na mrundikano wa wanafunzi darasani, sasa madarasa mapya yanaingiza wanafunzi 80 hivyo kupunguza changamoto ya mrundikano wa watoto na kutusaidia madawati 80," amesema Mwalimu Kindole.

Amefafanua kuwa walikuwa na mahitaji ya nyumba za walimu 16; zilizokuwepo zilikuwa tatu na ni nyumba moja iliyokuwa na unafuu kwani zilizobaki ni chakavu.

Mwalimu Kindole amesema kwa sasa upungufu ni wa nyumba 12 hivyo walishukuru serikali kuboresha miundombinu katika shule hiyo ikiwemo ujenzi wa matundu sita ya vyoo.

"Kulikuwa na upungufu wa matundu 10 ya vyoo vya wasichana na sasa imebaki matundu manne na hivyo shule nzima ina jumla ya matundu 24 ya vyoo.

Amesema "kabla ya TASAF mahudhurio ya wanafunzi hayakuwa mazuri lakini kwa sasa wanamahudhurio mazuri."


Pia wamesema .TASAF imeongeza madarasa mawili na kwamba kabla ya kujenga nyumba za walimu, walikuwa wanakaa vijijini.

Amesema kwa sasa kuna unafuu kwani watoto wakipata shida wanaweza kuhudumiwa kwa karibu na walimu.

"Kuna bomba za maji ambayo hutoa maji kwa mwezi mara moja au mbili, tuna kisima ambacho kina umbali wa Kilometa moja.
 

Nyumba ya watumishi wa Zahanati ya Kijiji cha Utiga, iliyopo Halmashauri ya Wang'ing'ombe mkoani Njombe
 

Mwenyekiti wa Kijiji cha Utiga, Sadick Kisakanyike akitoa maelezo ya miradi mitano iliyotekelezwa na fedha za TASAF katika kijiji chake
 

Mganga Mfawidhi wa Zahanati ya Utiga, Dkt. Peter Sumuni akielezea mradi wa jengo la zahanati na nyumba ya watumishi zilizojengwa kw afedha za TASAF
 

Baadhi ya wanakijiji cha Kijii cha Utiga, kilichopo katika Halmashauri ya Wanging'ombe mkoani Njombe, wakifuatilia maelezo ya Mwenyekiti wa kijiji hicho, Sadick Kisakanyike (hayupo pichani)

Share To:

Post A Comment: