Na John Walter-Babati

Kamati ya Siasa wilaya ya Babati imeridhishwa na ujenzi wa mradi wa kituo cha afya cha kata ya Gidas ambapo mpaka sasa ujenzi wake umefikia asilimia 75.

Kituo hicho cha afya cha Gidas kimepokea shilingi milioni 250,000,000 kutoka serikali kuu,  huku wananchi wakitakiwa kuchangia milioni 27,000,000 ambapo hadi sasa wamechangia milioni 17,160,000.

Kamati hiyo imeongozwa na Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi wilaya ya Babati Jackson Hhaibey ambaye amewataka wasimamizi wa mradi kukamilisha kwa wakati ili wananchi wapate huduma bora za afya kwa karibu zaidi.

Hhaibey alisema pesa zinazotumika katika miradi mbalimbali ya maendeleo zinatokana na kodi za wananchi na kuagiza zitumike kama zilivyo kusudiwa.

Aidha kituo hicho cha Afya cha Gidas kimepata mradi wa ujenzi wa choo cha wateja, kichomea taka na tenki la kuvunia maji huku kiasi cha shilingi milioni sitini na nne na laki tano (64,500,000) kikiwa tayari kimepokelewa kwa ajili ya kutekeleza.

Mkuu wa wilaya ya Babati Lazaro Twange amesema atahakikisha maagizo yote yaliyotolewa na kamati hiyo yanasimamiwa vyema na kutekelezwa hadi mradio utakapokamilika Oktoba 13,2023.

Share To:

Post A Comment: