MBUNGE wa Singida Mashariki Miraji Mtaturu ametoa maombi mawili katika kuboresha sekta ya uvuvi na mifugo moja ikiwa ni kuwa na tume maalum itakayoratibu rasilimali za mifugo kwenye halmashauri.

Ombi la pili ni kwa wizara kukaribisha wawekezaji kwenye ranchi za Taifa watakaosimamiwa na watalaam waliyopo wizara ya mifugo na uvuvi ili kuleta mapinduzi ya ufugaji nchini.

Mtaturu ametoa maombi hayo Mei 2,2023,Bungeni Jijini Dodoma wakati akichangia mjadala wa bajeti ya wizara ya Mifugo na Uvuvi ya mwaka 2023/2024.

Amesema tume hiyo ikiundwa itasaidia kukarabati mabwawa ambayo mengi kwa sasa yamekufa lakini pia itasimamia fedha zinazopelekwa ili kuleta matokeo yanayotarajiwa.

“Mh Waziri kule kwenye halmashauri zetu unakuta kuna afisa mifugo yupo mmoja tu,wakiingia kwenye Kikao cha CMT vipaumbele vinakuwa kwenye sekta nyingine lakini sekta ya mifugo haiangaliwi,tumeona ufanisi kwenye mamlaka zilizoundwa mfano RUWASA,TANROADS ufanisi upo,sasa kwa nini tusifanye kwenye mifugo ili kuwe na ufuatiliaji,?”amehoji.

Amesema serikali imekuwa ikijenga majosho,mabwawa na miundombinu mbalimbali inayosaidia ufugaji lakini imekosekana utaratibu hivyo fedha imekuwa ikitupwa kwenye halmashauri na majosho mengi yanakufa kwak ukosa uwezo wa kuyakarabati. Akizungumzia kuhusu kuwakaribisha wawekezaji Mtaturu amesema wizara ya mifugo na uvuvi kama ilivyo wizara ya kilimo ina watalaam wengi hivyo ni vyema wakatumiwa ili waweze kuleta mapinduzi ya ufugaji nchini.

“Eneo hili la ranchi zetu ninajua mipango mmeshaiseti lakini mi naongezea fanyeni vizuri wakaribisheni wawekezaji wasimamieni ninaamini tutapata matokeo ambayo tunayatarajia,”amesema.

Amesema ranchi zilizopo ziliwekwa makusudi ili zisaidie mapinduzi ya ufugaji nchini lakini hazifanyi kazi ni kama hazipo yamebaki kuwa mapori tu

“Maeneo mengi ranchi zimebaki kuwa na walinzi tu mameneja wale wapo kulinda angalau msije mkaibiwa yale majengo ambayo yapo pale, hii sio sawa Mh waziri lakini hata ukiangalia leo umetuambia hapa ranchi ya NARCO umenunua vitu lakini vitu vyenyewe vinavyonunuliwa ni vichache yaani bado huwezi kujivunia kwamba kuna hatua mtapiga,”ameongeza.

“Ranchi zetu nyingine zipo grounded kabisa ,hoja yangu nataka kusema nini mh waziri huu mpango mnaokuja nao kuwasogeza wawekezaji ambao watakuja kufanya na sisi ili waweze kutumia miundombinu tunayoiweka kama serikali kuweza kunenepesha ng’ombe,kuweza kuongeza utalaam uhamilishaji na kutumia vituo wanafunzi kujifunza,”ameeleza.

Mtaturu amesisitiza kuwa ni lazima sekta ya mifugo na uvuvi ichangie pato la Taifa zaidi kwa kuwa kuna mifugo mingi hivyo asilimia 7 ya inayochangiwa katika pato la Taifa ni ndogo sana.

AKIZUNGUMZIA KUHUSU JIMBONI KWAKE.

Mtaturu ameomba kutengwa fedha kwa ajili ya kutoa tope lililopo kwenye bwawa la Muyanji lililopo Kijiji cha Kimbwi Mkoani Singida ambalo mbali na kutoa kitoweo pia linasaidia kupatikana kwa ajira kwa wananchi.

Amesema bwawa hilo lilijengwa enzi za ukoloni na walikuwa wanapata kitoweo lakini kipindi cha katikati hali imekuwa tofauti.

“Hapa katikati tumekuwa tukipata up and down,hatupati samaki wazuri sana,mwaka 2018 nikiwa Mkuu wa Wilaya ya Ikungi tulipeleka vifaranga 3,500 kupitia halmashauri yetu na tukapandikiza wananchi wakaendelea kupata kitoweo na vijana wakapata shughuli za uvuvi,

Kwa sasa bwawa lile limepungua kina,nikuombe tupate fedha tukatoe tope zilizoingia ndani tuliboreshe na kujenga miundombinu sehemu ya kunyweshea mifugo iwekwe ili isiendelee kutifua tifua udongo utakaoingia ndani ya bwawa lile,dhamira yetu ni bwawa lile la Muyanji liendelee kutoa samaki na kwa sababu wizara yako inatusaidia kwenye protini basi na samaki kule kwenye wilaya yetu ya Ikungi tuwapate,”ameongeza.

Ametaja kata za kimkakati ambazo zikiwekewa majosho mabadiliko yataonekana ambazo ni Siuyu,Mang’onyi,Issuna,Mkiwa na Misughaa.

“Katika wilaya yetu ya Ikungi wafugaji tunao tunahitaji majosho ,tunahitaji mabwawa,mh waziri kata hizo tano tukiwekewa miundombinu ya mabwawa na majosho tutaona mabadiliko ya ng’ombe wetu na utaalam,ni imani yangu itaenda kubadilisha ufugaji wetu,”ameleeza Mtaturu.

SHUKRANI KWA RAIS SAMIA NA SERIKALI KWA UJUMLA.

“Shukrani kwa Rais wetu Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anayoifanya ya kuwaongoza wananchi,nampongeza mh waziri kaka yangu na swahiba wangu Abdallah Bin Ulega na naibu wake na wizara nzima kwa hotuba nzuri yenye maono,uelekeo mzuri ambao unaonekana wazi tunapata mapinduzi makubwa kwenye sekta ya uvuvi na mifugo,

“Ninasema hivyo kwa sababu nimeipitia hii hotuba nimemsikiliza waziri nimesikiiza maoni pia ya kamati ambayo mengi yameipongeza wizara nasema kama haya mliyoyaandika ndani ya hii hotuba mtaenda kuyatengenezea mpango kazi mh waziri tutatoka kidedea na tutaona namna ambavyo sekta hii itafanya kazi vizuri ,”amesema.

Mtaturu katika mchango wake amegusia pia suala la ukusanyaji wa maziwa ambapo nchi za Afrika Mashariki wakenya wanakusanya lita 1,241,000,Uganda lita 707,560 lakini Tanzania wanakusanya lita 64,837.

“Mh waziri sisi tunasemwa tuna ng’ombe wengi sisi tunasemwa tunayo rasilimali nyingi ,tuna eneo kubwa la kufugia lakini bado tunaweza kukusanya maziwa kiasi hiki kidogo maana yake kuna kazi hatujafanya vizuri ,tunafanya ufugaji wa kienyeji ,ng’ombe wetu sio kwamba tunawaona kwa mazingira ng’ombe wetu ni wadogo hawana kilo nyingi nyama zao hazivutii kuliwa, “Tukienda kuchoma mnadani tukala tunaamini nyama nzuri lakini sio,ni lazima tupige hatua moja mbele,”ameongeza.

Share To:

Post A Comment: