Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Ridhiwani Kikwete ameagiza ofisi ya Kamishna wa Ardhi Msaidizi mkoa wa Dar es Salaam kuitisha mimala ya wananchi wa kata ya kivule wasiopatiwa hati katika zoezi la urasimishaji makazi holela ili waweze kutatuliwa changamoto katika zoezi hilo.

 

Ridhiwani ametoa kauli hiyo tarehe 23 Desemba 2022 wakati akizungumza na wananchi wa kivule Manispaa ya Ilala alipokwenda kutoa Hati ikiwa ni juhudi za Wizara ya Ardhi kuwapelekea wananchi  hatimiliki za ardhi katika maeneo yao.

 

"Kwa kuwa wananchi waliorasimishiwa makazi yao waliacha namba zao za simu basi Kamishna itisha miamala ya wale waliolipa na kuwaelekeza ni kitu gani cha kufanya ili waweze kupata hati’’. Alisema Ridhiwani

 

Katika mkutano huo, wananchi wa kata ya Kivule Manispaa ya Ilala walimueleza Naibu Waziri wa Ardhi kuwa, pamoja na wao kulipa 160,000 lakini wameshindwa kupatiwa hati na kueleza kuwa kumekuwepo mawasiliano hafifu baina ya wananchi na kamati zinazosimamia zoezi hilo. Wananchi hao wa Kivule pia walishusha lawama kwa Chuo cha Ardhi Morogoro (ARIMO) kuwa kinachelewesha kukamilisha zoezi la urasimishaji katika mitaa ya Kivule.

 

Hata hivyo, kwa mujibu wa Kamishna wa Ardhi Msaidizi mkoa wa Dar es Salaam Shukran Kyando, Chuo cha Ardhi Morogoro kimefanya kazi kwa zaidi ya asilimia 80 lakini fedha zilizotolewa na wananchi katika zoezi hilo ni asilimia 11 pekee.

 

"Kata ya Kivuke ina mitaa minne na Chuo cha Ardhi Morogoro kimeingia mkataba wa kufanya kazi katika mitaa hiyo kwa ajili ya kumalizia kazi ya urasimishaji lakini zipo changamoto mbili yaani upande wa kampuni na ule wa wananchi kutolipia viwanja zaidi ya 7000 ambavyo vimeidhinidhwa" alisema Kyando.

 

Naibu Waziri wa Ardhi Mhe. Ridhiwani kupitia mkutano huo amekitaka Chuo cha Ardhi Morogoro kupeleka miamala yote iliyofanyia kazi kwa Kamishna wa Ardhi Msaidizi mkoa wa Dar es Salaam na kusisitiza kuwa, taarifa zote zinazokusanywa kuhusiana na zoezi la urasimishaji mwenye mamlaka nazo ni kamishna na siyo kampuni.

 

"Kama kuna maeneo yamekwama basi makampuni yaongee na kamishna ili kujua namna ya kutatua kero ili kwenda mbele na naelekeza hadi  kufikia tarehe 1 februari 2022 suala la wananchi wa Kivule kuhusiana na uasimishaji makazi tuwe tumemalizana nalo." Alisema Ridhiwani.

Share To:

Post A Comment: