Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Mhe. Nurdin Babu akifurahia jambo na washiriki wa Tamasha la Jinsia Kanda ya Kaskazini katika viwanja vya Kwasa Kwasa wilaya ya Same Mkoani Kilimanjaro.
Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Mhe. Nurdin Babu akifurahia baada ya kukata utepe ishara ya kuzindua Tamasha la Jinsia Kanda ya Kaskazini linalofanyika katika viwanja vya Kwasa Kwasa wilaya ya Same Mkoani Kilimanjaro.

Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Mhe. Nurdin Babu amezindua Tamasha la Jinsia Kanda ya Kaskazini linalofanyika katika viwanja vya Kwasa Kwasa wilaya ya Same Mkoani Kilimanjaro lililoandaliwa na Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) kwa kushirikiana na wadau wanaotetea haki za wanawake na usawa wa jinsia na wanaharakati binafsi kwa ufadhili wa Ubalozi wa Watu wa Canada, Sweeden, Coady Institute Canada na Seedchange.

Akizungumza wakati wa kuzindua Tamasha la Jinsia Kanda ya Kaskazini na Maonesho ya shughuli za wajariamali leo Jumatano Oktoba 5,2022 Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Mhe. Nurdin Babu amesema Rais wa Jamhuri ya Muungano Samia Suluhu Hassan anajitahidi kujenga jamii yenye usawa hivyo kuwataka wanawake kutembea kifua mbele.

“Rais Samia Suluhu Hassan anajitahidi kuleta usawa wa kijinsia, angalieni uteuzi mbalimbali wa viongozi anaofanya, wanawake ni wengi. Wanawake tembeeni kifua mbele, Imbeni Samia kwani anawapa kipaumbele wanawake, anatoa fursa mbalimbali kuwezesha wanawake. Rais Samia ni kinara wa kuwapa nguvu wanawake”,amesema Babu.


Mkuu huyo wa Mkoa amewataka wanawake kuchukua fursa kwenye kilimo na kuanza kuwa wakulima wakubwa kwani serikali imeongeza bajeti katika sekta ya kilimo na imeendelea kutoa mikopo ya asilimia 10 kwenye halmashauri za wilaya.

“Wanawake amkeni nendeni mkachukue mikopo, fanyieni kazi, rudisheni mikopo, ni lazima muwe waaminifu, mikopo hii inatolewa bila kwenye halmashauri za wilaya. Naziagiza halmashauri kuwapa fedha nyingi vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu, wapeni fedha nyingi ili wafanye mambo makubwa ikiwemo kulima mashamba makubwa. Ukimpa shilingi milioni 1 haimsaidii kitu, wapeni pesa nyingi”,amesema Babu.

Babu ametumia fursa hiyo kuwakumbusha wanaume kuacha kuwafanyia ukatili wanawake na badala yake wawapende na kuwathamini.

“Tusiwapige wanawake, tuwabembeleze wanawake, tuwasaidie wanawake. Mkeo kakupatia mtoto leo unakutana na mpita njia unachanganyikia.. Kwenye Mkoa wa Kilimanjaro haki ya nani nakwambia Mpige mwanamke uone. Mwanamke ukipigwa njoo kwa mkuu wa mkoa tukusaidie, nitamwambia nipige mimi halafu tuone”,amesema Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro.

“Mila na desturi potovu zinachangia ukatili wa kijinsia. Hakuna faida yoyote ya kukeketa mtoto wa kike zaidi ya hasara, kwanza vifaa wanavyotumia kukeketa siyo salama ni chanzo cha maambukizi ya Virusi vya Ukimwi”,amesema.

“Katika nchi ya Tanzania wanawake wengi wanakosa haki ya kumiliki ardhi. Naomba niwaambie kwamba Wanawake wana fursa sawa na wanaume, tumuogope Mungu na tuendelee kuheshimu sheria za nchi, tuwape fursa wananchi",amesema.

Katika hatua nyingine amewataka wananchi waendelee kuchukua tahadhari ya kutunza chakula. “Hali iliyopo, tutunze chakula, tupunguze sherehe”.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya TGNP, Gemma Akilimali amesema Tamasha la Jinsia Kanda ya Kaskazini ni tamasha la kwanza kufanyika na limekuwa la kipekee sana kwani washiriki zaidi ya 500 wanatoka katika mikoa mbalimbali nchini kwenye kanda mbalimbali.

“Hili ni tamasha la kwanza la kikanda kufanyika na la kipekee sana ambalo linafanyika wilayani Same kwa kipindi cha siku tatu (Oktoba 5-7,2022). Tamasha la Jinsia ni moja ya majukwaa ya TGNP katika ujenzi wa nguvu za Pamoja. Jukwaa hili ni la wazi kwa ajili ya wanawake na wadau wa haki za binadamu ambao hukutana pamoja kila baada ya mwaka mmoja kubadilishana uzoefu, kusherehekea, kutathmini na kupanga mipango ya kukabiliana na changamoto zinazowakabili.

“Sisi tunaamini katika nguvu ya pamoja ili kuleta mabadiliko makubwa katika jamii. Tumekwama kimaendeleo kwa sababu ya kuwaacha nyuma wanawake, tunataka watu wote wanawake kwa wanaume washiriki. Nchi yetu ni tajiri lakini tunashindwa kuona rasilimali na kutumia rasilimali zilizopo. Ni lazima tuwe na uchungu wa rasilimali zetu, ni lazima tuangalie namna bora ya kutumia rasilimali zilizopo ili zilete maendeleo endelevu”,amesema Akilimali.


“Tuangalie namna ya kushirikisha kundi la wanawake, tusiwaache nyuma wanawake. Kila mmoja alipo kuna rasilimali, kila mmoja aziangalie na kuzitumia ili kubadili maisha yetu. Matajiri mnaowaona walianza na vitu vidogo, tusiwaze vikubwa tu”,ameongeza Akilimali.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa TGNP, Lilian Liundi amesema Tamasha la Jinsia Kanda ya Kaskazini mwaka 2022 linaongozwa na mada kuu isemayo, ‘Haki ya Uchumi: Rasilimali Ziwanufaishe Wananchi Walioko Pembezoni kwa Maisha Endelevu’.

“Tumeamua kufanya Tamasha la Jinsia Kanda ya Kaskazini katika Wilaya ya Same kwa sababu Same inafanya vizuri katika masuala ya Jinsia ikiwemo kuingiza masuala ya kijinsia kwenye bajeti zao ikiwemo kujenga vyumba maalum kwa ajili ya watoto wa kike shuleni kujistiri, kuongeza matundu ya vyoo, kuweka huduma za maji katika zahanati. TGNP tuliwajengea uwezo lakini wao wakafanya kwa vitendo”,amesema Lilian.
Aidha amesema Tamasha hilo limewashirikisha wadau kutoka maeneo ya pembezoni kutokana na kwamba TGNP inafika kwenye maeneo ya pembezoni ambako wengine hawafiki.


“TGNP iliratibu tamasha la kwanza kabisa mwaka 1996 na hadi sasa takribani matamasha 14 yamekwishafanyika ambapo yameweza kuleta pamoja zaidi ya washiriki 25,000 (70% wanawake na 30%wanaume) katika viwanja vya TGNP.Kutokana na mafanikio ya Tamasha kubwa la Jinsia, mwaka 2010, TGNP na washirika wake walizindua tamasha la jinsia la kwanza ngazi ya wilaya ambapo hadi sasa matamasha sita ya Jinsia yamefanyika katika ngazi ya wilaya na kuleta pamoja zaidi ya washiriki 6000 (70% wanawake and 30% wanaume)”, amesema Lilian.

Amefafanua kuwa kama sehemu ya kuendelea kutanua harakati za ujenzi wa nguvu za pamoja nchini na kutoa fursa kwa watu wengi zaidi kushiriki, ilionekana kuna uhitaji wa kuanzisha Tamasha la Jinsia katika ngazi ya Kanda ambalo litaleta pamoja washiriki toka kanda mbalimbali hapa nchini

Naye Meneja Mradi wa Coady Institute Canada, Bw. Eric Smith amevishukuru Vituo vya taarifa na maarifa vinavyosimamiwa na TGNP kwa kazi nzuri wanazofanya katika masuala ya usawa wa kijinsia na kutokomeza ukatili wa kijinsia dhidi ya wanawake na watoto.

Mkuu wa wilaya ya Same, Edward Mpogolo ameishukuru TGNP kwa kupeleka Tamasha la Jinsia Kanda ya Kaskazini katika wilaya ya Same na kueleza kuwa tamasha hilo litaleta fursa kwa wananchi wa eneo hilo ambao wanajihusisha na kilimo na ufugaji.

“Kupitia tamasha hili pia tunatarajia kupata fursa za soko la zao la Tangawizi linalolimwa sana milimani hapa wilayani Same”,amesema.

Share To:

Post A Comment: