Waandishi habari Vinara wa masuala ya Malezi, Makuzi na Maendeleo ya Awali ya Mtoto ( MMMAM)  kutoka mikoa 28 nchini wakiwa katika picha ya pamoja na Mgeni rasmi, Dk Dorothy Gwajima mara baada ya kufungua rasmi mafunzo hayo kwenye Ukumbi wa Mikutano wa St Gaspar jijini Dodoma mwanzoni mwa wiki hii.
Baadhi ya Waandishi habari Vinara wa masuala ya Malezi, Makuzi na Maendeleo ya Awali ya Mtoto ( MMMAM) wakiwa kwenye picha ya pamoja na nyuso za furahi tayari kwa ajili ya mafunzo hayo. 

 

Na Abby Nkungu, Dodoma

 

SERIKALI imesema itaendelea kuweka mifumo rafiki ya uwekezaji  kwa watoto kupitia programu mbalimbali; ikiwemo Programu Jumuishi ya Taifa juu ya Makuzi, Malezi na Maendeleo ya Awali ya Mtoto (PJT-MMMAM) ya miaka mitano iliyozinduliwa Desemba mwaka jana. 

Ahadi hiyo ilitolewa Jijini hapa na Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na  Makundi maalum, Dk Dorothy Gwajima wakati akizindua mafunzo ya Kitaifa ya Sayansi ya Malezi, Makuzi na Maendeleo ya Awali ya Mtoto (SECD).

Mafunzo hayo yaliyoandaliwa kwa pamoja na Taasisi ya Children in Crossfire (CiC), UTPC na Chuo Kikuu cha Aga Khan yanahudhuriwa na Waandishi habari vinara wa kuandika habari za Malezi, Makuzi na Maendeleo ya Awali ya Mtoto (MMMAM), Maofisa Maendeleo ya Jamii, Maofisa Ustawi wa Jamii, Mashirika yasiyokuwa ya Kiserikali (CSOs) na Mtandao wa Makuzi, Malezi  na Maendeleo ya Awali ya Mtoto Tanzania (TECDEN).

Alisema kuwa ili kufanikisha uwekezaji timilifu kwa mtoto nchini Serikali haina budi kuunga mkono juhudi zote zinazolenga kuboresha  kundi hilo kwa kuweka mifumo rafiki ya uwekezaji.

Aidha, alisema kuwa Serikali inataraji mapinduzi makubwa kwenye tasnia ya habari kitaifa na kimataifa katika kuhakikisha kuwa jamii inapata uelewa mzuri na taarifa sahihi kuhusu Sayansi ya Malezi na Makuzi ya Mtoto.(SECD) kutokana na idadi ya Waandishi habari kutoka kila mkoa nchini kushiriki mafunzo hayo.

Mkurugenzi wa  Shirika la Children in Crossfire (CiC), Craig Ferla alisema kuwa Programu Jumuishi ya Taifa kuhusu Makuzi, Malezi na Maendeleo ya Awali ya Mtoto inachochea kwa kiasi kikubwa utekelezaji wa mipango mbalimbali kwenye sekta za ECD.

Akitoa salamu za Muungano wa Klabu za Waandishi wa habari Nchini (UTPC) kwa niaba  ya Mkurugenzi Mtendaji, Victor Maleko alieleza kuwa tangu mwaka 2019 kupitia klabu 28 zilizopo, Waandishi habari wamekuwa wakihabarisha umma kuhusu Malezi, Makuzi  na Maendeleo ya Awali ya Mtoto  kupitia vyombo mbalimbali vya habari ambapo tangu kuzinduliwa kwa programu hiyo miezi 6  iliyopita, zaidi ya habari 400 zimeripotiwa.

Lengo la mafunzo hayo ya siku sita yanayoendelea Ukumbi wa St Gaspar jijini hapa ni kuongeza uelewa na uwajibikaji kwa wadau wote ili waone umuhimu wa kuwekeza kwenye huduma bora za Malezi, Makuzi na Maendeleo ya Awali ya Mtoto. 

Share To:

dotto mwaibale

Post A Comment: