Wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi wa CRDB Bank Plc kutoka mataifa ya Burundi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Falme za Kiarabu na Rwanda wamerejea Nyumbani Ngorongoro kushuhudia asili ya mababu zao iliyosheheni vivutio vya utalii vya Wanyamapori, Malikale, Urithi wa Utamaduni na Jiolojia vilivyopo Ngorongoro ambayo ni Kivutio bora cha Utalii Afrika mwaka 2023 na 2025.

Wakiwa ndani ya hifadhi hiyo maarufu duniani, Wakurugenzi hao  wamefurahishwa na mandhari, uoto wa asili, wanyamapori pamoja na huduma bora za utalii zinazotolewa ndani ya hifadhi na kusisitiza kuwa uzoefu walioupata umeacha alama inayowafanya kurudi tena na familia zao.

Akizungumza kwa niaba ya ujumbe huo, Mwenyekiti wa Bodi ya CRDB Prof. Neema Mori amesema ujumbe huo umeichagua Ngorongoro kuwa sehemu yao ya mapumziko kutokana na upekee wake usiofananishwa na eneo lolote duniani  kwa kuwa Ngorongoro si tu kivutio cha Utalii bali ni hazina ya historia, utamaduni na asili inayoishi.

Akiwa na Ujumbe huo Kamishna Msaidizi Mwandamizi anayesimamia Utalii na Masoko Mariam Kobelo amesema kuwa  Ngorongoro ndio eneo lenye ushahidi wa kisayansi na Kimazingira kuwa binadamu wa kwanza alisimama kwa miguu yake miwili zaidi ya miaka Milioni 3.6 iliyopita huku hifadhi hiyo ikipambwa na wanyama wakubwa watano "Big Five", Spishi za Wanyama mbalimbali, Ndege, maua na mimea.




 


Mkuu wa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere (MNMA), Prof. Haruni Mapesa amewataka wanataaluma kuacha tabia ya kuchapisha makala zao kwenye Majarida yasiyotambulika ili kuzuia upotezaji wa nguvu na rasilimali za uchapishaji wa Tafiti.

Prof. Mapesa ameyasema hayo wakati akifungua Semina ya Uwasilishaji wa Makala Mijadala za a Kitaaluma iliyoandaliwa na Idara ya Lugha na Fasihii Chuoni hapo hafla iliyofanyika katika Kampasi ya Kivukoni jijini Dar es salaam.

Mkuu huyo wa Chuo amesema kuwa sasa Tasisi ipo katika hatua za ukuaji ikiwemo kuidhinishwa kwa Kitivo cha Uchumi na Biashara, ambapo chuo kimetenga kiasi cha shilingi milioni 120 kwa ajili ya tafiti na kuna mpango wa kuongeza fedha hizo ili kuwekeza zaidi kwa wahadhiri watakaofanya tafiti mbalimbali.

Naibu Mkuu wa Chuo anayesimamia Taaluma, Utafiti na Ushauri wa Kitaaluma Prof. Richard Kangalawe amekipongeza Kitivo cha Sanaa na Sayansi ya Jamii kupitia Idara ya Lugha na Fasihi kwa kuandaa semina hiyo na kuwahimiza washiriki kutumia fursa hiyo kuimarisha mawazo ya kitafiti, ikiwa ni pamoja na kuhakikisha tafiti zote zinasajiliwa rasmi na machapisho yawe yenye ubora wa hali. 

Kwa upande wake, Naibu Mkuu wa Chuo Mipango, Fedha na Utawala Prof. Evaristo Haulle amewataka Wanataaluma kubadilika na kuanza kufikiria namna ya kuchangia asilimia 30 ya mapato ya ndani kupitia Tafiti na Miradi wanayoifanya badala ya kutegemea rasilimali na fedha za ndani za chuo pekee.

Akiwasilisha taarifa ya Kitivo cha Sanaa na Sayansi ya Jamii, Mtiva wa Kitivo hicho Dkt. Luzabeth Kitali ameishukuru Menejimenti ya Chuo kwa Maelekezo na Ushauri na kuahidi kuwa idara yake imejipanga kikamilifu kusimamia ubora wa Tafiti, kuendeleza Uandishi ikiwa ni pamoja na kushiriki katika makongamano ya kitaaluma.


 

Imetolewa na;

Kitengo cha Mawasiliano na Masoko

CHUO CHA KUMBUKUMBU YA MWALIMU NYERERE

21.05.2026


Mwenyekiti wa Bodi ya Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere Mhe. Stephen Wasira ameipongeza Menejimenti ya Chuo hicho kwa Kujenga ofisi za Walimu na kumbi za Mihadhara kwa kutumia Makusanyo ya Mapato ya ndani, na hivyo kusaidia kupunguza changamoto ya Ofisi na Madarasa iliyokuwa inaikabili Taasisi hiyo.

Mhe. Wasira ameyasema hayo leo baada ya kuzindua jengo lenye ofisi zinazoweza kutumiwa na Walimu zaidi ya Sabini na kumbi mbili za Mihadhara zenye uwezo wa kuchukua wanafunzi Mia sita kwa mara moja kwa kila kumbi.

Kwa upande wake Mkuu wa Chuo Prof. Haruni Mapesa amesema kuzinduliwa kwa ofisi na kumbi za Mihadhara kutasaidia kupunguza changamoto ya uhaba wa vyumba vya kufundishia na ofisi ambazo zitatumiwa na Watumishi.

Mkuu huyo wa Taasisi amebanisha kuwa dhamira kuu ya ujenzi huo ni kuboresha ustawi na kutoa huduma bora kwa Wanafunzi na Wafanyakazi.

Ameongeza kuwa ujenzi huo utasaidia kuongeza mapato ndani ya Taasisi kwani chuo kitaongeza udahili wa Wanafunzi pamoja na kuendeleza mazingira bora, rafiki na safi kwa Ustawi wa jamii ya Chuo.


Mradi huo umegharimu kiasi cha Shilingi Bilioni Moja na Milioni Sitini na Saba.

 

Imetolewa na:

Kitengo cha Mawasiliano na Masoko

Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere

21.05.2026

Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga, akiwasilisha Hotuba ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 leo Mei 22,2026 bungeni Dodoma.

Na.Alex Sonn-DODOMA

WAZIRI wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga amesema Serikali inaendelea kuimarisha uzalishaji wa sukari nchini ili kupunguza utegemezi wa kuagiza sukari kutoka nje ya nchi kupitia upanuzi wa viwanda vya sukari.

Akiwasilisha Mpango wa bajeti ya Wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/2027 bungeni jijini Dodoma, Kapinga amesema viwanda viwili vya Mkulazi Holding Company Limited na Kilombero Sugar Company Limited vimefanya upanuzi mkubwa wa uzalishaji utakaoongeza upatikanaji wa sukari nchini.

Amesema baada ya upanuzi huo, Kiwanda cha Kilombero kitaongeza uwezo wa kuzalisha sukari kutoka tani 123,000 hadi tani 226,000 kwa mwaka, huku majaribio ya uzalishaji yakiwa yamekamilika na uzalishaji rasmi unatarajiwa kuanza mwezi Juni, 2026.

Kapinga amesema kwa upande wa Kiwanda cha Mkulazi, kimeongeza mtambo mpya utakaowezesha uzalishaji wa sukari ya viwandani (industrial sugar) kwa ajili ya matumizi ya viwanda mbalimbali nchini.

Amesema majaribio ya mitambo hiyo tayari yamefanyika kwa mafanikio na kiwanda kimefanikiwa kuzalisha tani 256 za sukari ya viwandani.

“Upanuzi huu utawezesha kuongeza uzalishaji wa sukari nchini, kupunguza uagizaji kutoka nje pamoja na kuchochea ukuaji wa sekta ya viwanda,” amesema Kapinga.

Aidha, amesema  kukamilika kwa miradi hiyo kutazalisha ajira za moja kwa moja 8,500 pamoja na ajira zisizo za moja kwa moja 25,000, hatua ambayo itaongeza kipato kwa wananchi na kuchochea maendeleo ya uchumi wa nchi.

Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga, akiwasilisha Hotuba ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 leo Mei 22,2026 bungeni Dodoma.

Na.Alex Sonna-DODOMA

WIZARA ya Viwanda na Biashara imeliomba Bunge kuidhinisha bajeti ya Shilingi bilioni 137.8 kwa mwaka wa fedha 2026/2027 kwa ajili ya kutekeleza majukumu mbalimbali ya maendeleo ya sekta ya viwanda na biashara nchini.

Kati ya fedha hizo, Shilingi bilioni 104.1 zimetengwa kwa matumizi ya kawaida, ambapo Shilingi bilioni 78.0 ni kwa ajili ya mishahara ya watumishi na Shilingi bilioni 26.0 kwa matumizi mengineyo ya uendeshaji.

Akiwasilisha bajeti hiyo Bungeni leo Mei 22, 2026 jijini Dodoma, Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga amesema Shilingi bilioni 33.6 zimetengwa kwa ajili ya miradi ya maendeleo, huku fedha zote za maendeleo zikitokana na vyanzo vya ndani vya Serikali.

Amesema bajeti hiyo inalenga kuendelea kuimarisha mazingira ya uwekezaji, kuongeza uzalishaji wa viwanda vya ndani, kukuza biashara na kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania katika masoko ya ndani na nje ya nchi.

Raia wa Iran, Jan Mohammed Millan, aliyekuwa nahodha wa jahazi la Al Arab, amehukumiwa kifungo cha jumla ya miaka 60 jela baada ya kupatilana na hatia ya kusafirisha dawa za Kulevya kilogramu 504.36 za heroin na kilogramu 355 za methamphetamine katika Bahari ya Hindi ndani ya eneo la kiuchumi la Tanzania.
Na Farida Mangube Morogoro

Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kimeanza utekelezaji wa miradi mipya 12 ya utafiti yenye thamani ya jumla ya shilingi bilioni 3.4 kwa lengo la kukuza maarifa na kutatua changamoto katika sekta za kilimo, mifugo, mazingira na maendeleo ya jamii kwa ujumla.
-Arusha

Wahasibu na wachumi wametakiwa kujijengea nidhamu ya kitaaluma kwa kufuata sheria, taratibu na kanuni zilizowekwa ili kujiepusha na vitendo vya udukuzi wa mifumo ya kielektroniki na kulinda taarifa za Serikali.
Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Hassan Abbasi leo Mei 21, 2026 amekagua maandalizi ya Maadhimisho ya Siku ya Nyuki Duniani yanayotarajiwa kufanyika Kitaifa katika Uwanja wa Vita mkoani Tabora.

Wakala wa Nishati Vijijini (REA) na Shirika la Mzinga leo Mei 21, 2026 wamesaini hati ya makubaliano ya ushirikiano yanayolenga kuimarisha ushirikiano katika Utafiti, Teknolojia, Uzalishaji na Usambazaji wa nishati safi ya kupikia.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo iliyofanyika Mkoani Morogoro, Mwenyekiti wa Bodi ya Shirika la Mzinga, Mhe. Balozi Luteni Jenerali (Mstaafu), Charles Lawrence Makakala, amesema utekelezaji wa mpango huo utakuwa msaada mkubwa kwa wanawake wa vijijini ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakikumbana na changamoto ya kutafuta nishati kwa ajili ya kupikia.

“Akina mama wa vijijini wanapata adha kubwa kutafuta nishati ya kupikia. Madhara ya kiafya wanayoyapata wao pamoja na watoto wao ni makubwa kwa sababu watoto pia hushiriki katika shughuli za maandalizi ya chakula. Hatua hii itasaidia utekelezaji wa sera ya nishati safi lakini pia kuinua ustawi wa jamii na uchumi endelevu,” amesema Makakala.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), Mhe. Balozi Meja Jenerali (Mstaafu), Jacob Kingu, amesema ushirikiano huo utaongeza uzalishaji wa mkaa mbadala utokanao na mabaki ya mimea pamoja na uzalishaji wa majiko banifu kwa bei nafuu zaidi na hivyo kuongeza matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini.

Mkurugenzi Mkuu wa REA, Mhandisi Hassan Saidy, amesema makubaliano hayo pia yanakwenda kuongeza aina za nishati safi za kutumika zenye gharama nafuu zaidi lengo likiwa kuongeza matumizi ya nishati safi ya kupikia.

Mhandisi Saidy amesema kuwa kati ya Watanzania wanne, ni mmmoja tu ndo anatumia nishati safi ya kupikia. Hivyo kupitia ushirikiano huo unaokwenda kuongeza uzalishaji wa mkaa mbadala pamoja na majiko banifu, idadi ya Watanzania wanaotumia nishati safi ya kupikia itakwenda kuongezeka.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Mzinga, Brigedia Jenerali Mhandisi Seif Athuman Hamisi, amesema makubaliano hayo yatahusisha maeneo mbalimbali ikiwemo kufanya tafiti za kuboresha matumizi ya majiko na mkaa safi ili kuhakikisha teknolojia hizo zinakidhi mahitaji ya wananchi.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amesema Serikali inatambua umuhimu mkubwa wa Waandishi Waendesha Ofisi kwa kuwa ni muhimili muhimu katika kuwawezesha Viongozi na watendaji kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.

Makamu wa Rais amesema hayo, wakati wa ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa 13 wa Kitaaluma wa Waandishi wa Waendesha Ofisi Tanzania (TAPSEA) unaofanyika katika Ukumbi wa Ngurdoto Mkoani Arusha. Amesema Serikali inaipa uzito Taasisi ya TAPSEA kwa kuwa inatambua ili kuwa na utulivu na mshikamano ni lazima Waandishi Waendesha ofisi kutimiza wajibu ipasavyo.

Amewapongeza Waandishi Waendesha Ofisi kwa kubeba sura za Taasisi wanazofanyia kazi kwa kuwa wakarimu na wenye kutoa msaada wa awali kwa wananchi wanaofika kutafuta huduma. Amewasihi kuendelea kutoa huduma kwa ukamilifu pamoja na kuwa na heshima na ukarimu ili kuwafariji wanaowahudumia.

 

Aidha Makamu wa Rais, amewasisitiza waandishi waendesha ofisi kuendelea kujitambua na kutunza siri wakati wa utekelezaji wa majukumu yao.

 

Makamu wa Rais amekipongeza Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania kwa kuimarisha elimu yao mpaka kufikia shahada ya uzamili ambayo imewawezesha Waandishi Waendesha Ofisi kuhama katika mfumo asili wa utekelezaji wa majukumu yao mpaka kufikia kuwa sehemu ya maamuzi ya kisera na upangaji wa mikakati na utekelezaji wake.

Amesisitiza kwamba Vyuo vinavyotoa mafunzo hayo, vinapaswa kuendelea kujiimarisha ili kuwa na Waandishi Waendesha Ofisi wanaoweza kusaidia vema Taifa. Makamu wa Rais ametoa wito kwa Taasisi mbalimbali kuhakikisha wanawawezesha Waandishi Waendesha Ofisi kushiriki mikutano ya kitaaluma.

Halikadhalika, Makamu wa Rais amewapongeza Viongozi wa Taasisi hiyo wanaomaliza muda wao kwa kufanya kazi nzuri iliyowaunganisha na kuwawezesha Waandishi Waendesha Ofisi nchini. Aidha amewataka kufanya uchaguzi wa haki ili kupata Viongozi sahihi wanataoiongoza vema Taasisi hiyo. Amewasihi kufanya uchaguzi kwa kuzingatia uhuru na haki ili kupata viongozi sahihi wa Taasisi hiyo pamoja na kuwataka wanachama kuchagua viongozi makini bila ubaguzi wa aina yeyote.

Kwa upande wake Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete, amesema Serikali kupitia ofisi hiyo, itaendelea kutoa ushirikiano kwa watumishi wote wa Umma ikiwemo uongozi wa TAPSEA ili kufanikisha masuala mbalimbali ya kiutumishi kwa wanachama wake.

Ameongeza kwamba, Ofisi hiyo itaendelea kuwaangalia na kuwalea wanaTAPSEA na kuwataka kuwa na imani na serikali inayoongozwa na Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwa wataendelea kuwaangalia katika hali zote kiwemo maslahi yao, kutoa mafunzo pamoja na kuwahakikisha kuwa salama muda wote.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Waandishi Waendesha Ofisi Tanzania (TAPSEA) Bi. Zuhura Maganga amesema Taasisi hiyo inajivunia mafanikio yaliyopatikana katika kuimarisha taaluma ya uandishi uendesha ofisi ikiwemo kuanzishwa kwa shahada ya utawala inayotolewa na Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania pamoja kuanzishwa kwa shahada ya uzamili ya Sanaa katika mawasiliano na usimamizi wa ofisi.

 

 

Imetolewa na

Ofisi ya Makamu wa Rais

21 Mei 2026

Arusha.



Jeshi la Polisi Kanda Maalum Dar es Salaam limeeleza kuwa linaendelea na uchunguzi wa tukio la kukamatwa kwa David Joseph Mghanja maarufu kama Djumbe, kufuatia taarifa zilizosambaa kupitia mitandao ya kijamii zikidai alichukuliwa na watu wasiojulikana maeneo ya Bunju.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo Mei 21, 2026 na Kaimu Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalum Dar es Salaam, Jeshi hilo lilianza kufuatilia tukio hilo tangu usiku wa Mei 20, 2026 baada ya taarifa mbalimbali kuanza kusambaa mtandaoni.

Katika ufuatiliaji huo, Polisi walifanikiwa kulipata gari lenye namba T 609 DTD aina ya Toyota Wish rangi nyeusi, linalomilikiwa na Allan Elisonguo Macha, ambalo inadaiwa Djumbe alikuwa akisafiria kama abiria wakati alipokamatwa na watu wanaodaiwa kutokujitambulisha.

Taarifa hiyo imeeleza kuwa asubuhi ya leo Mei 21, 2026, Jeshi la Polisi lilipokea taarifa zikidai kuwa Djumbe alikuwa katika Ofisi za Chadema zilizopo Mikocheni, jijini Dar es Salaam.

Amesema  Askari walifika katika eneo hilo lakini hawakumkuta, huku wakimkuta mtu anayedaiwa kuwa alikuwa pamoja naye wakati wa tukio la kukamatwa kwake.

Aidha, Jeshi la Polisi limethibitisha kuwa Djumbe tayari amepatikana salama na kwamba uchunguzi unaendelea ili kubaini watu waliomkamata pamoja na sababu za kufanya tukio hilo.

Polisi wameeleza kuwa hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi ya wahusika wote watakaobainika kuhusika na tukio hilo kwa mujibu wa sheria za nchi.



Na Mwandishi Wetu-Kigali, Rwanda


TUME ya Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC) imeshiriki Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali kuhusu Uvumbuzi wa Nishati ya Nyuklia Barani Afrika (NEISA 2026) uliofanyika Mei 19, 2026 mjini Kigali, Rwanda, ukiwakutanisha viongozi wa kitaifa, wataalamu wa nishati, wawekezaji pamoja na mashirika ya kimataifa kujadili mustakabali wa nishati ya nyuklia barani Afrika.

Mkutano huo ulilenga kujadili namna bora ya kuongeza upatikanaji wa nishati ya umeme, kupunguza uchafuzi wa mazingira, kusaidia maendeleo ya viwanda, kukuza ubunifu wa teknolojia za nyuklia pamoja na kuvutia uwekezaji katika miradi ya nishati kwa ajili ya kuimarisha uchumi endelevu.

Katika mkutano huo, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan alisema Tanzania inaendelea kutathmini matumizi ya nishati ya nyuklia kama sehemu ya mkakati wa muda mrefu wa kuongeza vyanzo vya nishati nchini.

Rais Samia alieleza kuwa teknolojia mpya za Small Modular Reactors (SMRs) na Micro Modular Reactors (MMRs) zinaweza kuwa suluhisho sahihi kwa nchi zinazoendelea kutokana na uwezo wake wa kuzalisha nishati kwa ufanisi na usalama zaidi.

Aidha, alitaja maeneo muhimu yanayopaswa kupewa kipaumbele katika maendeleo ya sayansi na teknolojia ya nyuklia kuwa ni pamoja na mifumo imara ya udhibiti, wataalamu wenye ujuzi pamoja na usimamizi madhubuti wa usalama kwa kuzingatia viwango vya kimataifa.

Alisisitiza kuwa matumizi ya teknolojia ya nyuklia katika uzalishaji wa nishati yanahitaji maandalizi ya mifumo ya udhibiti, uwezo wa taasisi, upatikanaji wa fedha, uelewa wa wananchi na ushirikiano wa kikanda.

Katika ushiriki wake, Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania, Profesa Najat Kassim Mohammed alihudhuria mkutano huo akiwa ameambatana na Mkurugenzi wa Teknolojia ya Nyuklia na Huduma za Ufundi, Dkt. Remigius Kawala.

Profesa Najat alipata fursa ya kushiriki kikao cha ndani kilichoongozwa na Rais Samia ambapo alitoa ufafanuzi kuhusu maendeleo ya nyuklia nchini pamoja na miradi inayotekelezwa na TAEC kwa kushirikiana na International Atomic Energy Agency.

Miongoni mwa mipango hiyo ni Rays of Hope unaolenga kuimarisha huduma za uchunguzi na matibabu ya saratani nchini, Atoms4Food unaohamasisha matumizi ya teknolojia ya nyuklia katika sekta ya kilimo pamoja na ushiriki wa TAEC katika mpango wa matumizi ya teknolojia ya nyuklia kwa uzalishaji wa umeme.

Profesa Najat alisisitiza umuhimu wa Tanzania kuendelea kuwekeza katika utafiti, usalama na mafunzo ya wataalamu ili kuhakikisha matumizi salama na endelevu ya teknolojia ya nyuklia katika sekta mbalimbali ikiwemo afya, kilimo, viwanda, utafiti wa madini na uzalishaji wa nishati.

Kupitia mkutano huo, TAEC ilipata nafasi ya kubadilishana uzoefu na wataalamu kutoka mataifa mbalimbali kuhusu usalama wa nyuklia, mifumo ya udhibiti wa teknolojia za nyuklia pamoja na uwekezaji katika miundombinu ya kisasa ya nishati.

Aidha, ushiriki wa Tanzania katika NEISA 2026 uliendana na maono ya serikali ya kukuza sekta ya nishati na kuimarisha ushirikiano wa kikanda ndani ya Afrika Mashariki.

Katika mkutano huo, viongozi mbalimbali wa Afrika walisisitiza umuhimu wa ushirikiano wa kikanda katika kuendeleza miradi ya nyuklia, kuongeza uwekezaji na kujenga uwezo wa wataalamu wa ndani.

Kwa ujumla, ushiriki wa TAEC katika NEISA 2026 umeiwezesha Tanzania kuendelea kujijengea nafasi katika mjadala wa kimataifa kuhusu mustakabali wa nishati ya nyuklia barani Afrika pamoja na kufungua fursa mpya za ushirikiano wa kitaalamu, kiteknolojia na kiuchumi kwa maendeleo endelevu ya taifa.

Mkutano wa NEISA 2026 uliandaliwa kwa ushirikiano wa International Atomic Energy Agency, United Nations Economic Commission for Africa, World Nuclear Association pamoja na Rwanda.

Na John Mapepele,Geneva, Uswisi

Waziri wa Afya wa Tanzania, Mheshimiwa Mohamed Mchengerwa, ametoa wito wa kuimarishwa kwa ushirikiano wa kikanda katika mapambano dhidi ya malaria na Magonjwa Yaliyokuwa Hayapewi Kipaumbele (NTDs), katika kikao maalum cha ngazi ya juu kilichofanyika sambamba na Mkutano wa 79 wa Shirika la Afya Duniani (WHA),akisisitiza kuwa udhibiti wa magonjwa hauwezi kufanikiwa bila hatua za pamoja zinazovuka mipaka ya mataifa.
Kibaha, Pwani

CCM leo imekuwa mwenyeji wa mkutano kati ya Chama cha Kikomunisti cha China (CPC) na Vyama Sita Rafiki vya Ukombozi Kusini mwa Afrika uliofanyika katika Shule ya Uongozi ya Mwalimu Julius Nyerere (MJNLS), Kibaha.
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

WAZIRI wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga, amewahimiza wawekezaji na wafanyabiashara nchini kuhakikisha wanalinda haki na usalama wa watumiaji kwa kuzingatia kanuni bora za uzalishaji kuanzia ununuzi wa malighafi, usafirishaji hadi uchakataji wa bidhaa ili kuzalisha bidhaa zenye viwango vya juu vya ubora vinavyokidhi matakwa ya walaji.
Na Mwandishi Wetu

Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Elimu Tanzania (TET), Dkt. Aneth Komba, amezitaka taasisi za elimu ya juu nchini kuhakikisha tafiti, ubunifu pamoja na matumizi ya teknolojia vinaelekezwa katika kutoa suluhisho la changamoto halisi zinazowakabili wananchi na kuchochea maendeleo ya taifa.

 

MONACO - Benki ya CRDB imeendelea kudhihirisha dhamira yake ya kuunga mkono maendeleo ya Taifa kupitia sekta mbalimbali kwa kushiriki katika Mkutano Mkuu wa 81 wa Michezo ya Majeshi Duniani (81st CISM General Assembly) uliofanyika nchini Monaco kuanzia tarehe 1 hadi 9 Mei 2026.

Mkutano huo wa kimataifa uliwakutanisha viongozi wa kijeshi na wadau wa michezo kutoka zaidi ya nchi 130 duniani kwa lengo la kuimarisha mshikamano, diplomasia ya michezo na amani kupitia kaulimbiu ya “Friendship Through Sport.”
Benki ya CRDB, ikiwa miongoni mwa wadau wakubwa wa maendeleo nchini, imeendelea kuunga mkono jitihada za vyombo vya ulinzi na usalama pamoja na michezo ya majeshi, hatua inayoimarisha ushirikiano wake na taasisi za Serikali katika kukuza ustawi wa askari na familia zao.

Ujumbe wa Tanzania katika mkutano huo uliongozwa na Brigedia Jenerali Saidi Hamisi Saidi, akisaidiana na Luteni Kanali Penina Anthony Igwe. Kutoka CRDB, ujumbe unajumuisha Meneja wa Kitengo cha Wateja Maalum, Crispin Sichalwe pamoja na Meneja Mawasiliano na Uhusiano kwa Umma, Emmanuel Tupeligwe.
Akizungumza kwenye mkutano huo, Sichalwe alisema CRDB imeendelea kutoa huduma maalum za kifedha kwa wanajeshi ndani na nje ya nchi, ikiwemo mikopo nafuu, bima na huduma za kifedha zinazowafikia popote walipo.

“Tunatambua mchango mkubwa wa majeshi katika usalama wa Taifa, hivyo tunahakikisha wanapata huduma bora na za haraka kupitia kitengo chetu maalum,” alisema.
Kwa upande wake, Tupeligwe alisisitiza kuwa CRDB itaendelea kushirikiana kwa karibu na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) kupitia elimu ya fedha na huduma zinazowafikia wanajeshi hata wakiwa katika maeneo ya mbali au majukumu ya kimataifa.

Aidha, benki hiyo imeendelea kuimarisha ushirikiano wake wa kimkakati na JWTZ ili kuhakikisha wanajeshi wanapata huduma bora za kifedha kwa urahisi, ikiwa ni sehemu ya mchango wake katika maendeleo na usalama wa Taifa.

 




NAIBU Spika wa Bunge, Daniel Sillo, ametoa wito kwa wananchi na wadau mbalimbali kushiriki katika kuchangia huduma za matibabu ya upandikizaji Uloto kwa Watoto wenye ugonjwa wa Sicle Cell na upandikizaji figo kwa wenye uhitaji hapa nchini.

Ameyasema hayo wakati wa hafla ya chakula cha jioni tarehe 19 Mei, 2026 katika ukumbi wa Domiya jijini Dodoma, ambapo hafla hiyo imewakutanisha viongozi waandamizi wa mkoa wa Dodoma, wabunge na wadau mbalimbali kwa lengo la kujadili namna ya kuimarisha mfuko wa kusaidia matibabu ya upandikizaji uloto na figo pamoja na huduma nyingine za kibingwa.

Amesema licha ya mafanikio yaliyopatikana ya huduma hizo za upandikizaji uloto na figo kutolewa hapa nchini na hivyo kuokoa fedha nyingi ambazo zingeweza kutumika endapo wananchi wangeenda kutibiwa nje ya nchi.

Alisema kila mwananchi anapaswa kutambua kuwa kuchangia huduma hizo si jukumu la serikali na taasisi pekee, bali ni wajibu wa pamoja kwa kuwa magonjwa ya figo na sickle cell hayachagui mtu kwa nafasi yake, dini wala hali ya maisha.

“Tunaposhiriki katika michango hii si kwa ajili ya taasisi moja, bali tunaunga mkono huduma za kitaifa zinazogusa maisha ya wananchi wengi wanaohitaji matibabu hayo,” alisema Mhe. Sillo.

Alitoa wito kwa wananchi, taasisi na wadau mbalimbali kuendelea kuunga mkono juhudi hizo za BMH ili kuwezesha wagonjwa wanaohitaji huduma za upandikizaji viungo na matibabu mengine maalumu kupata huduma kwa wakati.



Ameeleza kutegemea bajeti ya serikali pekee hakuwezi kukidhi mahitaji yote yanayoongezeka ya huduma za kibingwa, hivyo ushirikishwaji wa wadau ni njia muhimu ya kuimarisha sekta ya afya na kuokoa maisha ya Watanzania wengi.





Naibu Waziri, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Ndege Qwaray (Mb), amefanya ziara ya kikazi katika Kituo cha Utafiti, Ubunifu na Uendelezaji wa Serikali Mtandao (Research, Innovation and Development Centre – RIDC) kilichopo jijini Dodoma, ambapo amekagua miradi mbalimbali ya TEHAMA inayotekelezwa na kituo hicho kwa lengo la kuboresha utoaji wa huduma Serikalini.

Katika ziara hiyo iliyofanyika mapema wiki hii, Mhe. Qwaray alipata fursa ya kutembelea na kujionea miradi ya kiteknolojia inayolenga kutoa suluhisho kwa changamoto katika sekta mbalimbali ikiwemo elimu, afya na utawala.

Aidha, miradi hiyo inahusisha matumizi ya teknolojia zinazochipukia kama vile Internet of Things (IoT) na Akili Mnemba (AI), katika kurahisisha utendaji kazi Serikalini na kuongeza ufanisi wa huduma kwa wananchi.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mhe. Qwaray ameipongeza Mamlaka ya Serikali Mtandao (e-GA) kwa juhudi zake za kuibua na kuendeleza vipaji vya vijana, kupitia tafiti na ubunifu wa mifumo mbalimbali ya TEHAMA yenye mchango mkubwa katika maendeleo ya taifa.

“Niwapongeze e-GA kwa kazi kubwa mnayoifanya ya kukuza ubunifu na tafiti za teknolojia. Dunia ya sasa inabadilika kwa kasi kubwa kutokana na maendeleo ya teknolojia, hivyo ni muhimu kuendelea kujifunza, kufanya tafiti na kubuni mifumo mipya itakayokwenda sambamba na mabadiliko hayo,” amesema Mhe. Qwaray.

Amesisitiza kuwa, bunifu zote zinazotengenezwa zinapaswa kuwa na tija kwa jamii na kuchangia moja kwa moja katika kuboresha huduma zinazotolewa kwa wananchi pamoja na kuongeza ufanisi ndani ya taasisi za Serikali.

Sambamba na hilo, Mhe. Qwaray amesisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano kati ya e-GA, vyuo vikuu na sekta binafsi ili kuongeza uwekezaji katika tafiti, ubunifu na maendeleo ya teknolojia zinazoweza kusaidia kutatua changamoto mbalimbali za kijamii na kiuchumi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa e-GA, Mhandisi Benedict Ndomba, amesema kituo hicho kimeendelea kuwa chachu ya mageuzi ya kidijitali Serikalini kupitia ujenzi wa mifumo mbalimbali inayotumika katika taasisi za umma.

Ametaja baadhi ya mifumo hiyo kuwa ni Mfumo wa Uendeshaji wa Vikao vya Bodi na Menejimenti (e-Board) pamoja na Mfumo wa Uendeshaji wa Vikao Kidijitali (e-Mikutano), ambayo imekuwa ikisaidia kuongeza ufanisi katika shughuli za Serikali.

“Kituo hiki kimekuwa na manufaa makubwa kwa taifa kutokana na kazi zake za utafiti, ubunifu na maendeleo ya mifumo ya TEHAMA. Pia, kimefungua fursa kwa wanafunzi na vijana wenye taaluma ya TEHAMA kushiriki katika tafiti na bunifu mbalimbali kwa maslahi ya taifa,” amesema Mha.Ndomba.

Katika kuonesha dhamira ya Serikali kuendelea kuimarisha kituo hicho, Mhe. Qwaray ameahidi kuwa Wizara itaendelea kushirikiana na e-GA kutatua changamoto zinazoikabili RIDC ili kuongeza fursa kwa vijana wengi zaidi wa Kitanzania kupata nafasi ya kujifunza, kufanya tafiti na kushiriki katika ubunifu wa teknolojia mbalimbali za kisasa.