📌Washiriki Nishati Safi expo wafurahishwa na miradi ya REA

Wakala wa Nishati Vijijini (REA) umeshiriki Maonesho na Kongamano la Nishati Safi expo 2026 yanayofanyika katika ukumbi wa Ubungo EACLC jijini Dar es Salaam ambapo mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba. 

Akizungumza katika kongamano hilo leo Juni 24, 2026, Msimamizi wa miradi ya REA, Mha. Francis Manyama amesema kuwa, upatikanaji wa umeme vijijini umechangia kwa kiasi kikubwa kupunguza matumizi ya nishati zinazochafua mazingira na kuongeza matumizi ya nishati safi.

Ameongeza kuwa, miradi ya usambazaji wa umeme vijijini imewezesha wananchi kuachana na matumizi ya majenereta na vyanzo vingine vya nishati vinavyotumia mafuta, hali inayosaidia kupunguza uzalishaji wa hewa chafuzi.

Halikadhalika, REA inaendelea na mradi wa kufunga mifumo ya umeme jua katika visiwa mbalimbali nchini, ambapo mifumo 20,000 inatarajiwa kufungwa ili kuongeza upatikanaji wa nishati safi katika maeneo yasiyofikika kirahisi na gridi ya taifa.

Mbali na hilo, amesema wakala unasaidia wazalishaji wadogo wa umeme wanaotumia maporomoko ya maji ili kuongeza matumizi ya nishati jadidifu na kupunguza utegemezi wa vyanzo vya nishati vinavyoharibu mazingira.

Katika kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia, REA inaendelea kufunga miundombinu ya majiko ya kisasa katika taasisi mbalimbali za umma na binafsi zikiwemo shule, vyuo na taasisi za huduma za jamii.

Amesema katika awamu ya kwanza, pili na tatu za utekelezaji wa mradi huo, taasisi 454 zinazohudumia zaidi ya watu 100 zitafikiwa na miundombinu hiyo ambayo inafungwa bila gharama kwa taasisi husika.

Aidha, amesema REA inatoa ruzuku ya asilimia 50 kwa mitungi ya gesi ya kilo sita pamoja na ruzuku ya asilimia 80 hadi 85 kwa majiko banifu ili kuwezesha wananchi wa vijijini kupata nishati safi kwa gharama nafuu.

Mha. Manyama amesema wakala umefunga mifumo ya nishati safi ya kupikia katika magereza nchini na kambi 22 za Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) zilizopo katika mikoa 14, hatua inayochangia kupunguza matumizi ya kuni na mkaa pamoja na kulinda mazingira kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.











 


Aelekeza kijana mlemavu Joseph kupewa ajira ya kudumu


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amemuelekeza Katibu Mkuu - UTUMISHI Bw. Juma Selemani Mkomi kufanya tathmini ya kubaini Maafisa Utumishi waliozembea kukamilisha mchakato wa Watumishi wa Umma kupandishwa madaraja kwa mwaka wa fedha 2025/26 na kuwachukulia hatua stahiki kwa mujibu wa Sheria, Taratibu, Kanuni na  Miongozo ya Utumishi wa Umma. 

Prof. Shemdoe ametoa maelekezo hayo Juni 23, 2026 kwa niaba ya Katibu Mkuu Kiongozi Mhe. Balozi Dkt. Moses Kusiluka, wakati wa Kilele cha Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma mwaka 2026 katika Viwanja vya Chinangali Park, jijini Dodoma.

“Kuna Maafisa Utumishi kwa uzembe wamesababisha watumishi kutopandishwa madaraja mwaka 2025/26, Katibu Mkuu UTUMISHI kwa niaba ya Katibu Mkuu Kiongozi nakuelekeza kufanya tathmini ya kubaini maafisa waliokwamisha upandishaji wa madaraja na kuchukua hatua ya kuwaondoa katika nafasi zao,” amesisitiza Prof. Shemdoe. 

Prof. Shemdoe amewataka Wakuu wa Taasisi za Umma na Maafisa Utumishi nchini kushughulikia kwa wakati kero na malalamiko ya watumishi wanaowaongoza, kwani nafasi walizonazo ni kwa ajili ya kuwatumikia watumishi hao ili nao waweze kutoa huduma bora kwa wananchi.

Pia, Prof. Shemdoe amemuelekeza Katibu Mkuu UTUMISHI kumpatia ajira ya kudumu kijana mlemavu aliyemkuta kwenye banda la VETA ambaye hana mikono lakini ana ujuzi wa kusanifu majengo na samani kwa kutumia miguu yake kupitia kompyuta mpakato.

Aidha, Prof. Shemdoe kwa niaba ya watumishi wa umma nchini amemshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwapandisha madaraja watumishi wa umma, kulipa madai ya muda mrefu ya watumishi wa umma, ikiwa ni pamoja na kuajiri watumishi wengi wa kada mbalimbali wakiwemo walimu na wa sekta ya afya.  

Sanjari na hilo, Prof. Shemdoe amezipongeza taasisi za kifedha zikiwemo CRDB, NMB, AZANIA, NBC na nyinginezo zilizoshiriki maonesho ya Wiki ya Wiki ya Utumishi wa Umma kutokana na kuhitajika kwa taasisi hizo kwa watumishi wa umma, ambako kunawapa wigo watumishi kuchagua benki wanayoona inafaa kuchukua mkopo wa kuwezesha shughuli zao binafsi za kiuchumi na kijamii.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma Bw. Juma Selemani Mkomi amesema kupitia maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma mwaka huu, wananchi wamepata huduma za moja kwa moja kutoka katika taasisi za umma na kuongeza kuwa, taasisi za umma zimepata fursa ya kubadilishana uzoefu kiutendaji ikiwa ni pamoja na kuiwezesha Serikali kupata mrejesho utakaoiwezesha kuborsha utoaji wa huduma.

Katika maadhimisho ya mwaka huu, jumla ya Taasisi za Umma 226 zimetoa elimu na huduma mbalimbali kwa watumishi wa umma na wananchi ikiwemo matumizi ya mifumo ya utoaji wa huduma katika Utumishi wa Umma, hati za viwanja, vyeti vya kuzaliwa, vitambulisho vya taifa na huduma za kitabibu za kibingwa kutoka Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Benjamini Mkapa, Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete, Taasisi ya Mifupa (MOI) na Hospitali ya Bugando.











Tume ya Ushindani Tanzania (FCC) imeendelea kuimarisha kampeni ya utoaji elimu kwa umma kuhusu madhara ya biashara ya bidhaa bandia, ikisisitiza kuwa utengenezaji, usambazaji na uuzaji wa bidhaa hizo ni kosa la jinai linaloadhibiwa kwa mujibu wa sheria za nchi.

Akizungumza leo Juni 22, 2026, katika eneo la Kariakoo Jijini Dar es Salaam, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Uhusiano kwa Umma wa FCC, Bi. Roberta Feruzi, amesema bidhaa bandia zina athari kubwa kwa uchumi, afya na usalama wa wananchi, huku zikidhoofisha ushindani wa haki katika biashara.

Amesema watu watakaobainika kujihusisha na biashara ya bidhaa bandia wanaweza kukabiliwa na adhabu ya kifungo cha kati ya miaka minne hadi 15 jela pamoja na faini inayofikia kati ya Shilingi milioni 10 na milioni 50, kulingana na masharti ya sheria husika.

Bi. Feruzi ameeleza kuwa FCC inaendelea kushirikiana na taasisi mbalimbali za ndani na kimataifa katika kudhibiti bidhaa bandia ili kuhakikisha haziingii nchini, hazisambazwi katika soko la ndani, wala kutumiwa kama njia ya kupitishwa kwenda mataifa mengine kupitia mifumo ya usafirishaji.

Amebainisha kuwa nafasi ya Tanzania kama lango muhimu la biashara na usafirishaji katika ukanda wa Afrika Mashariki inaifanya nchi kuwa miongoni mwa maeneo yanayoweza kutumiwa na wahalifu kusafirisha bidhaa bandia, hali inayohitaji ushirikiano wa karibu kati ya serikali, sekta binafsi na wananchi katika kupambana na tatizo hilo.

Kwa mujibu wa Bi. Feruzi, biashara ya bidhaa bandia si changamoto ya Tanzania pekee, bali ni tatizo la kimataifa linalosababishwa na watu wasio waaminifu wanaotafuta faida kwa kutumia kazi, ubunifu na alama za biashara za wengine kinyume cha sheria.

Ametoa wito kwa wananchi na wafanyabiashara kuwa makini wanaponunua au kuuza bidhaa, huku akiwahimiza kutoa taarifa kwa mamlaka husika wanapobaini uwepo wa bidhaa zinazohisiwa kuwa bandia.

Vilevile, amesema Tanzania itaadhimisha Siku ya Kitaifa ya Udhibiti wa Bidhaa Bandia Juni 25, 2026, yakiwa na  kauli mbiu isemayo: "Linda Maisha na Masoko Dhidi ya Pombe, Vilainishi na Sigara Bandia" ambapo maadhimisho hayo yatatumika kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu athari za bidhaa bandia na kuimarisha juhudi za kitaifa na kimataifa za kupambana na biashara hiyo haramu.

Amesisitiza kuwa mafanikio ya vita dhidi ya bidhaa bandia yanategemea ushirikiano wa wadau wote, ikiwemo Serikali, wafanyabiashara , wazalishaji na wananchi, ili kulinda uchumi wa taifa, afya za watumiaji na mazingira ya biashara yenye ushindani wa haki.



Na Benny Mwaipaja, Dodoma

Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, limepitisha kwa kishindo Bajeti Kuu ya Serikali ya Mwaka wa Fedha 2026/27 kwa asilimia 97.66 baada ya wabunge 385 kupiga kura ya ndio kuunga mkono Bajeti hiyo.

Akitangaza matokeo ya kura ya wazi iliyopigwa bungeni jijini Dodoma, Spika wa Bunge Mhe. Mussa Azzan Zungu alisema kuwa kati ya kura hizo 393 zilizopigwa, kura 8 zimekataa kuunga mkono bajeti hiyo na wabunge wengine nane 8 hawakupiga kura kwa sababu hawakuwepo bungeni.

Akihitimisha hoja baada ya Bunge kupitisha Muswada wa Sheria kwa ajili ya kuidhinisha Serikali kuanza kutekeleza Bajeti Kuu ya Serikali ya Mwaka wa Fedha 2026/2026 (zaidi ya shilingi trlilioni 62.33) kutoka katika Mfuko Mkuu wa Hazina, Mhe. Spika Zungu alimpongeza Waziri wa Fedha, Mhe. Ballozi Khamis Mussa Omar (Mb) wasaidizi wake, watendaji wa Wizara kwa kazi kubwa na nzuri waliyoifanya na Wabunge wote kwa michango yao yenye tija kwa Taifa.

“Kura zimepigwa na Serikali imeruhusiwa kuzitumia pesa kuanzia sasa, mkazitumie pesa hizi kama Kamati za Bunge zilivyoelekeza, kuhakikisha maslahi ya watu kwanza yanazingatiwa kabla ya mambo mengine. Bunge hili litaendelea kufuatilia utekelezaji wake na kuhakikisha kuwa miradi yote iliyoainishwa inazingatiwa na kuleta furaha kwa wananchi” alisisitiza Mhe. Zungu.

Kupitia kwa Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), Serikali ililiomba Bunge lipitishe Bajeti ya shilingi trilioni 62.33 kwa ajili ya matumizi ya kawaida na maendeleo katika Mwaka wa Fedha 2026/2027, ikiwa ni ongezeko la asilimia 10.3 ikilinganishwa na bajeti ya mwaka 2025/26. 

Mhe. Balozi Omar alisema kuwa, mapato yalitarajiwa kuwa shilingi trilioni 46.79 ambapo mapato ya kodi ni shilingi trilioni 36.99, mapato mengine ni shilingi trilioni 9.24 (ikijumuisha mapato ya Mamlaka za Serikali za Mitaa shilingi trilioni 1.977) na misaada kutoka kwa washirika wa maendeleo shilingi bilioni 563.1.

Aidha aliongeza kuwa ili kuendana na dhamira ya kujitegemea katika uendeshaji wa Serikali na maendeleo, takribani robo tatu ya bajeti yote ya mwaka 2026/27, sawa na asilimia 74.2 itagharamiwa na mapato ya ndani.

Matumizi na uwekezaji katika mali zisizo za kifedha yalikadiriwa kuwa shilingi trilioni 54.50 pasipo kujumuisha malipo ya mtaji wa deni la Serikali ambapo kati ya kiasi hicho, stahiki za watumishi ikijumuisha michango ya pensheni ni shilingi trilioni 10.13.

“Gharama za bidhaa na huduma itakuwa shilingi trilioni 5.22, malipo ya riba ni shilingi trilioni 6.86, ruzuku shilingi trilioni 25.32, mafao na misaada ya kijamii shilingi trilioni 1.01, uwekezaji katika mali zisizo za kifedha shilingi trilioni 2.33 na gharama nyingine shilingi trilioni 3.63.” alisema Mhe. Balozi Omar

Aliongeza kuwa kulingana na makadirio ya mapato na matumizi hayo, kunajitokeza nakisi kwenye bajeti ya shilingi trilioni 7.71 na Serikali itaendelea kugharamia nakisi ya bajeti hiyo kwa kutumia mikopo kutoka vyanzo vya ndani na nje kwa kuzingatia Mkakati wa Muda wa Kati wa Kusimamia Deni la Serikali (2025/26 – 2027/28).

Mhe. Balozi Omar alisema kuwa, katika mwaka 2026/27, Serikali inatarajia kukopa jumla ya shilingi trilioni 15.54 ambapo kati ya kiasi hicho, mikopo ya ndani itakuwa shilingi trilioni 6.56, mikopo ya nje yenye masharti nafuu shilingi trilioni 6.55 na mikopo ya nje yenye masharti ya kibiashara shilingi trilioni 2.43.
Aidha, Serikali inakadiria kulipa malipo ya mtaji kwa mikopo iliyoiva shilingi trilioni 7.84.

Baada ya kupitishwa kwa bajeti hiyo, Bunge linatarajia kupokea, kujadili na kupitisha Muswada wa Sheria ya Fedha wa Mwaka 2026 ( The Finance Bill,2026) tarehe 24 Juni, 2026

Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) imeendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu haki na wajibu wao katika sekta za nishati na maji, sambamba na kuhamasisha uwekezaji wa vituo vya mafuta vijijini ili kuongeza upatikanaji wa huduma salama na kukomesha biashara holela ya mafuta.

Hatua hiyo ni sehemu ya mafanikio ya ushiriki wa EWURA katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali, jijini Dodoma, ambapo maelfu ya wananchi wamefika katika banda la mamlaka hiyo kupata elimu na ufafanuzi kuhusu huduma mbalimbali zinazodhibitiwa na EWURA.

Akizungumza katika maonesho hayo, Kaimu Meneja wa Mawasiliano na Uhusiano wa EWURA, Wilfred Mwakalosi, amesema kwa siku nane mfululizo mamlaka hiyo imekuwa ikitoa elimu kwa wananchi kuhusu sekta za mafuta, umeme, gesi asilia na maji, pamoja na kupokea na kushughulikia maswali na changamoto mbalimbali zinazowakabili watumiaji wa huduma hizo.

Amesema wananchi wengi walitumia fursa hiyo kupata ufahamu kuhusu namna ya kuwasilisha malalamiko wanapokumbana na changamoto za huduma, huku mada ya uwekezaji katika vituo vya mafuta vijijini ikiwa miongoni mwa masuala yaliyoibua maswali mengi zaidi.

“Wananchi wengi walitaka kufahamu taratibu na fursa zilizopo za kuanzisha vituo vya kisasa vya mafuta vijijini ili kuondokana na biashara ya mafuta inayofanyika kwa kutumia chupa, ndoo na magaloni, ambayo mara nyingi huhatarisha usalama wa watu na mali,” amesema Mwakalosi.

Ameeleza kuwa Serikali kupitia EWURA imeweka mazingira rafiki ya uwekezaji kwa kupunguza kwa kiasi kikubwa gharama za vibali na leseni kwa wawekezaji wa vituo vya mafuta vijijini.

Kwa mujibu wa EWURA, ada ya kibali cha ujenzi wa kituo cha mafuta katika maeneo ya vijijini imepunguzwa kutoka Shilingi 500,000 zinazotozwa maeneo ya mijini hadi Shilingi 50,000, huku ada ya leseni ikishushwa kutoka Shilingi milioni moja hadi Shilingi 100,000.

Mbali na punguzo hilo, EWURA imepunguza baadhi ya masharti ya uwekezaji kwa kuruhusu matumizi ya nyaraka za uthibitisho wa umiliki wa ardhi zinazotolewa na serikali za vijiji badala ya hati kamili za ardhi zinazohitajika katika maeneo ya mijini.

Hatua hiyo inalenga kuvutia wawekezaji wengi zaidi katika maeneo ya vijijini na kuongeza upatikanaji wa mafuta kwa njia salama, nafuu na inayozingatia viwango vya usalama.

Katika maonesho hayo, wananchi pia walipata ufafanuzi kuhusu namna EWURA inavyosimamia ukokotoaji wa bei za mafuta, viwango vya huduma za maji na umeme, pamoja na taratibu za kuwasilisha malalamiko pale wanaporidhika au kutoridhika na huduma zinazotolewa na watoa huduma.

Aidha, Mwakalosi amewahimiza wananchi kusoma na kuelewa mikataba ya huduma kwa wateja inayotolewa na taasisi za maji, umeme na nishati, akieleza kuwa mikataba hiyo inaainisha kwa uwazi haki, wajibu na viwango vya huduma vinavyopaswa kutolewa kwa mteja.

Amesisitiza kuwa wananchi wenye uelewa wa mikataba hiyo wanakuwa na uwezo mkubwa wa kudai huduma bora, kufuatilia utekelezaji wa haki zao na hata kudai fidia pale ambapo watoa huduma watashindwa kutekeleza viwango walivyoahidi.

Vilevile, EWURA imewahakikishia wananchi kuwa nchi inaendelea kuwa na hali nzuri ya upatikanaji wa umeme, gesi na maji kutokana na uwekezaji mkubwa unaoendelea kufanywa na Serikali katika sekta hizo.

Mwakalosi ametaja ongezeko la uzalishaji wa umeme kupitia Bwawa la Mwalimu Nyerere kuwa miongoni mwa hatua zilizochangia kuimarika kwa huduma za nishati nchini, huku EWURA ikiendelea kusimamia upatikanaji endelevu wa huduma za maji na nishati kwa manufaa ya wananchi wa sasa na vizazi vijavyo.




Na Mwandishi Wetu - Dodoma


Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC) imehitimisha kwa mafanikio ushiriki wake katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yaliyofanyika katika Viwanja vya Chinangali jijini Dodoma, ambapo ilitoa elimu kwa wananchi kuhusu matumizi salama ya mionzi na mchango wa teknolojia ya nyuklia katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi nchini.

Katika kipindi chote cha maonesho hayo, banda la TAEC lilitembelewa na wananchi, wanafunzi, wataalamu na wadau mbalimbali waliopata fursa ya kujifunza kuhusu majukumu ya Tume katika kusimamia matumizi ya mionzi nchini pamoja na kuhakikisha teknolojia ya nyuklia inatumika kwa kuzingatia viwango vya usalama vinavyolinda afya za binadamu na mazingira.

Wataalamu wa TAEC walitoa elimu kuhusu usimamizi na udhibiti wa matumizi ya vyanzo vya mionzi, utoaji wa vibali kwa watumiaji wa teknolojia hiyo pamoja na ukaguzi wa mara kwa mara unaofanyika katika taasisi na maeneo mbalimbali yanayotumia vifaa vya mionzi ili kuhakikisha usalama unaendelea kuzingatiwa wakati wote.

Aidha, wananchi walipata uelewa kuhusu matumizi ya teknolojia ya nyuklia katika sekta mbalimbali zikiwemo afya, kilimo, mifugo, viwanda, migodi, maji na utafiti wa kisayansi. Elimu hiyo ilibainisha mchango mkubwa wa teknolojia hiyo katika kuboresha huduma za uchunguzi na matibabu ya magonjwa, kuongeza uzalishaji katika sekta za uzalishaji na kusaidia matumizi endelevu ya rasilimali za taifa.

Vilevile, TAEC ilitoa ufafanuzi kuhusu nafasi ya teknolojia ya nyuklia katika uzalishaji wa nishati ya umeme, ikieleza namna teknolojia hiyo inavyoweza kuchangia upatikanaji wa nishati ya uhakika kwa ajili ya kuendeleza shughuli za viwanda, biashara na ukuaji wa uchumi wa taifa.

Katika sekta ya afya, wananchi walielimishwa kuhusu matumizi ya mionzi katika uchunguzi na matibabu ya magonjwa mbalimbali, huku katika sekta ya chakula wakipata maelezo kuhusu matumizi ya teknolojia ya mionzi katika uhifadhi wa mazao na bidhaa za chakula kwa kuzuia uharibifu unaosababishwa na wadudu na vimelea, hivyo kuongeza muda wa matumizi na kupunguza upotevu wa mazao baada ya kuvunwa.

Mbali na kupata elimu, washiriki wa maonesho hayo walipata fursa ya kuuliza maswali na kufanya majadiliano ya moja kwa moja na wataalamu wa TAEC kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu usalama wa mionzi, hatua za tahadhari zinazopaswa kuzingatiwa pamoja na mchango wa Tume katika kulinda jamii dhidi ya madhara yanayoweza kusababishwa na matumizi yasiyo salama ya mionzi.

TAEC imeeleza kuwa ushiriki wake katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma umeendelea kuwa jukwaa muhimu la kuwafikia wananchi, kutoa taarifa sahihi kuhusu huduma zake na kuongeza uelewa wa umma kuhusu matumizi salama ya teknolojia ya nyuklia kwa maendeleo endelevu ya taifa.

Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yaliyohitimishwa leo yameendelea kutoa fursa kwa taasisi za umma kuwasilisha huduma zao kwa wananchi, kuimarisha uwajibikaji, kujenga imani ya umma na kuongeza uelewa wa jamii kuhusu mchango wa taasisi hizo katika maendeleo ya Tanzania.