•Prof. Shemdoe atoa wito kwa sekta binafsi kuwekeza katika ujenzi wa nyumba za watumishi
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ameridhia ombi la wananchi wa mvomero la kujengewa shule mbili za Sekondari katika Halmashauri ya Mvomero, ombi ambalo liliwasilishwa kwa niaba yao na Mbunge wa Jimbo la Mvomero Mhe. Sara Msafiri pamoja na Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Morogoro Mhe. Josephine Kapoma wakilenga kuboresha mazingira ya ujifunzaji na ufundishaji katika Halmashauri hiyo.
Hayo yamesemwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM–TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, Julai 18, 2026 katika kijiji cha Mkindo, kata ya Mkindo, Halmashauri ya Mvomero Mkoa wa Morogoro, mara baada ya kukagua na kuweka jiwe la msingi katika miradi wa ujenzi wa Shule ya Sekondari Mkindo, ikiwa ni muendelezo wa ziara yake ya kikazi ya kukagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kuhimiza uwajibikaji kwa watumishi wa umma mkoani Morogoro.
"Mhe. Sara Msafiri akishirikiana na pacha wake Mhe. Josephine Kapoma waliniomba tujenge shule nne, nilipokea ombi hilo na kuliwasilisha kwa Mhe. Waziri Mkuu naye akaliwasilisha kwa Mhe. Rais ambaye ameridhia ombi hilo kwa kutoa Shilingi Bilioni 1.1 za kujenga shule mbili, na tayari fedha hizo zimeshaingizwa kwenye akaunti ya Halmashauri," amesema Prof. Shemdoe.
Katika kuhakikisha wananchi waliopo kwenye maeneo yenye uhitaji mkubwa wananufaika na shule hizo, Prof. Shemdoe ameelekeza zijengwe kwenye kata ya Dakawa na Mzumbe kama alivyoomba Mbunge wa Jimbo la hilo la Mvomero, Mhe. Msafiri, huku akitoa wito kwa sekta binafsi kuunga mkono jitihada za Serikali kwa kuwekeza katika ujenzi wa nyumba za walimu nchini.
Aidha, Prof. Shemdoe amesema kabla ya kufika shuleni hapo amekagua, ameweka jiwe la msingi na kuzindua huduma ya upasuaji katika jengo jipya la upasuaji la Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero lenye vifaa tiba vya kisasa, hatua itakayowawezesha wakazi wapatao 459,304 wa wilaya ya Mvomero na maeneo jirani kuwa na uhakika wa kupata huduma ya upasuaji katika hospitali hiyo.
Katika hatua ya kuboresha miundombinu ya elimu Mvomero, Prof. Shemdoe amesema pia ametembelea na kuzindua vyumba vinne vya madarasa katika Shule ya Msingi Miembeni yenye thamani ya Shilingi Milioni 115 ambayo imejengwa katika kijiji cha Mvomero, kata ya Mvomero wilayani Mvomero.
“Na sasa nipo hapa na nimeshiriki nanyi katika kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa Shule mpya ya Sekondari ya Mkindo katika kijiji hiki cha Mkindo kilichopo kata ya Mkindo, shule ambayo imejengwa baada ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kutoa Shilingi Milioni 528 za ujenzi wa shule hii,” ameeleza Prof. Shemdoe.
Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Mvomero, Mhe. Sara Msafiri, amemuomba Prof. Shemdoe kufikisha salamu za shukrani za wananchi wa Mvomero kwa Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha zilizowezesha ujenzi wa shule ya Sekondari ya Sayansi Mkindo, akisema shule hiyo itazalisha madaktari, wahandisi pamoja na walimu wa masomo ya sayansi.
Naye, Mbunge wa Viti Maalum, Mhe. Josephine Kapoma, amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutoa fedha za ujenzi wa miundombinu ya elimu katika maeneo ya vijijini hususani kwenye kijiji hicho cha Mkindo.