Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi, Dkt. James Mataragio amesema Tanzania sasa itakuwa na jumla ya vitalu vitatu vinavyozalisha gesi asilia kufuatia uzinduzi wa uchimbaji wa visima vya kuongeza uzalishaji pamoja na bomba la kusafirisha gesi asilia kutoka Ntorya hadi Kiwanda cha Kuchakata Gesi Asilia cha Madimba.
Dkt. Mataragio ameyasema hayo leo, Februari 27, 2026, wakati wa ziara ya kikazi ya Waziri wa Nishati Mhe. Deogratius Ndejembi, mkoani Mtwara katika maeneo ya vitalu vya uchimbaji wa gesi asilia.
Dkt. Mataragio amemshkuru Waziri wa Nishati kwa kuzindua mradi huo wa kimkakati katika maendeleo ya sekta ya mafuta na gesi asilia nchini na kusema hatua hiyo itaongeza uzalishaji wa gesi na kuimarisha usalama wa upatikanaji wa nishati nchini.
Akizungumzia umuhimu wa mradi wa Ntorya, amesema kuwa ukikamilika utaongeza upatikanaji wa gesi asilia na kufungua fursa kwa miradi mingine inayohitaji nishati hiyo, ikiwemo miradi ya uzalishaji wa mbolea ambayo kwa sasa inakabiliwa na changamoto ya upatikanaji wa gesi.
‘Ongezeko la uzalishaji wa gesi unatarajiwa kuchochea matumizi yake katika uzalishaji wa umeme, viwanda, taasisi mbalimbali, vyombo vya usafiri pamoja na matumizi ya majumbani, na hivyo kuimarisha utekelezaji wa agenda ya matumizi ya nishati safi nchini’ amesisitiza Dkt. Mataragio.
Mradi wa uchimbaji wa visima vya kuongeza gesi asilia pamoja na ujenzi wa bomba la kusafirisha gesi kutoka Ntorya hadi Madimba unasimamiwa kwa karibu na Shirika la Maendeleo ya Petrolu Tanzania (TPDC) kwa kutumia wataalamu wake wa ndani, hali inayoonesha mafanikio ya uwekezaji wa Serikali katika kuandaa wataalamu wa sekta ya mafuta na gesi nchini.













































