Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum na Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Mbeya kupitia kundi la wanawake, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi, amewataka wanawake kuchangamkia fursa za mikopo inayotolewa na Serikali ili kujiinua kiuchumi na kujenga jamii imara yenye wanawake wanaojitegemea.
Akizungumza akiwa mgeni rasmi katika hafla ya utoaji wa Tuzo za Mwanamke Shujaa mkoa wa Mbeya, Mhe. Mahundi amesema Serikali imeendelea kuweka mazingira bora ya upatikanaji wa mikopo kwa makundi mbalimbali hususan wanawake wanaojishughulisha na biashara ndogo ndogo, ili kuwafikia wanawake wengi zaidi na kuwasaidia kujenga uchumi imara.
“Serikali imeweka utaratibu wa mikopo kwa ajili ya kuwainua wanawake kiuchumi. Nawahimiza wanawake kuitumia ipasavyo ili kujenga uchumi imara na kuondokana na utegemezi Wanawake tukisimama kiuchumi tutaimarisha familia zetu na kuchangia maendeleo ya Taifa kwa ujumla, hivyo ni muhimu kila mwanamke kuona fursa hizi na kuzitumia kwa bidii na uaminifu,” amesema Mahundi.
Kwa upande wake Mkuu wa wilaya ya Kyela, Mhe. Josephine Manase, amewataka wanawake kuzingatia malezi bora ya watoto, kusimamia haki za watoto pamoja na kushirikiana kupunguza vitendo vya ukatili wa kijinsia katika jamii ambapo jukumu la malezi na ulinzi wa watoto linahitaji mshikamano wa jamii nzima hususan wanawake ambao mara nyingi ndio walezi wakuu katika familia.
“Wanawake tunapaswa kushirikiana na kupeana fursa badala ya kubaguana tukishikamana ndipo uimara wa mwanamke utaonekana na hapo tutakuwa na nguvu kubwa ya kuleta mabadiliko chanya katika jamii ili kujenga nguvu ya pamoja katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi na tukiwa na Uchumi imara hata malezi ya familia zetu yanakuwa bora kwa kuwa tunakuwa na uimara wa akili hivyo na wasihi tuzingatie malezi bora ” amesema Josephine.
Naye mwanzilishi wa tuzo hizo, Sara Nyambura Ndambo, amewashukuru wanawake wote waliojitokeza kushiriki na kuunga mkono shughuli mbalimbali za kijamii pamoja na kuwapongeza wanawake waliotunukiwa tuzo hizo kwa juhudi zao katika jamii.
“Lengo la tuzo za Mwanamke Shujaa ni kutoa motisha kwa wanawake wanaojitoa katika shughuli za kijamii na maendeleo ili waendelee kufanya kazi zao kwa bidii zaidi huku wakihamasisha wengine kufuata nyayo zao na tutaendelea kuboresha tuzo hizi kila mwaka ili ziwe chachu ya kuwahamasisha wanawake wengi zaidi kufanya mambo makubwa katika jamii” amesema Sara.
Hafla hiyo ya utoaji wa Tuzo za Mwanamke Shujaa imewakutanisha wanawake kutoka maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Mbeya na imekuwa jukwaa la kuhamasisha ushiriki wa wanawake katika shughuli za maendeleo, kuimarisha mshikamano wao pamoja na kutambua mchango wa wanawake wanaofanya kazi kubwa katika jamii.

.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)























