Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi, Dkt. James Mataragio amesema Tanzania sasa itakuwa na jumla ya vitalu vitatu vinavyozalisha gesi asilia kufuatia uzinduzi wa uchimbaji wa visima vya kuongeza uzalishaji pamoja na bomba la kusafirisha gesi asilia kutoka Ntorya hadi Kiwanda cha Kuchakata Gesi Asilia cha Madimba.

Dkt. Mataragio ameyasema hayo leo, Februari 27, 2026, wakati wa ziara ya kikazi ya Waziri wa Nishati Mhe. Deogratius Ndejembi, mkoani Mtwara katika maeneo ya vitalu vya uchimbaji wa gesi asilia.

Dkt. Mataragio amemshkuru Waziri wa Nishati kwa kuzindua mradi huo wa kimkakati katika maendeleo ya sekta ya mafuta na gesi asilia nchini na kusema hatua hiyo itaongeza uzalishaji wa gesi na kuimarisha usalama wa upatikanaji wa nishati nchini.

Akizungumzia umuhimu wa mradi wa Ntorya, amesema kuwa ukikamilika utaongeza upatikanaji wa gesi asilia na kufungua fursa kwa miradi mingine inayohitaji nishati hiyo, ikiwemo miradi ya uzalishaji wa mbolea ambayo kwa sasa inakabiliwa na changamoto ya upatikanaji wa gesi.

‘Ongezeko la uzalishaji wa gesi unatarajiwa kuchochea matumizi yake katika uzalishaji wa umeme, viwanda, taasisi mbalimbali, vyombo vya usafiri pamoja na matumizi ya majumbani, na hivyo kuimarisha utekelezaji wa agenda ya matumizi ya nishati safi nchini’ amesisitiza Dkt. Mataragio.

Mradi wa uchimbaji wa visima vya kuongeza gesi asilia pamoja na ujenzi wa bomba la kusafirisha gesi kutoka Ntorya hadi Madimba unasimamiwa kwa karibu na Shirika la Maendeleo ya Petrolu Tanzania (TPDC) kwa kutumia wataalamu wake wa ndani, hali inayoonesha mafanikio ya uwekezaji wa Serikali katika kuandaa wataalamu wa sekta ya mafuta na gesi nchini.











Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu (ADEM), Dkt. Maulid J. Maulid, akimkabidhi cheti cha ushiriki wa Mafunzo ya Usimamizi wa Kimkakati wa Elimu Mwalimu Dennis John Otieno, ambaye ni Mwenyekiti wa Umoja wa Wakuu wa Shule za Sekondari Tanzania (TAHOSSA) na pia Mkuu wa Shule ya Sekondari Ilboru mkoani Arusha.

 


Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi amelitaka Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) kumsimamia kikamilifu Mkandarasi anayetekeleza mradi wa ujenzi wa bomba la kusafirisha gesi asilia kutoka eneo la ugunduzi la Ntorya hadi Kiwanda cha Kuchakata Gesi Asilia cha Madimba ili kuhakikisha unakamilika ifikapo Septemba 2026

Amesema hayo, leo tarehe 27 Februari 2026 mkoani Mtwara mara baada ya kuweka jiwe la msingi la mradi wa bomba la gesi asilia Ntorya–Madimba ambao utekelezaji wake umefikia asilimia 35 akieleza kuwa mradi huo utachangia kuongeza matumizi ya gesi asilia na kuchochea ukuaji wa uchumi

“Tumeweka ‘taget’ ya mwezi wa tisa kuhakikisha visima hivi vinazalisha gesi na kuunga kwenye bomba kuu la Madimba, ikifika muda huo kusiwe na hadisi nyingine, ili haya yasitokee tunahitaji usimamizi wa hali ya juu kuhakikisha TPDC mnakuwa site muda wote, Watanzania wanataka wanataka kuona maendeleo,” amesisitiza Ndejembi

Aidha, Ndejembi amewataka wataalamu wa TPDC kuhakikisha shughuli zote zinafanyika kwa ubora na kwa kuzingatia muda uliokubaliwa kwenye mkataba huku akibainisha kuwa mradi huo utachochea ukuaji wa sekta ya gesi kwa kuongeza uzalishaji wa umeme kuvutia uwekezaji na kukuza viwanda vitakavyozalisha ajira kwa Watanzania

Ameihimiza TPDC kuongeza kasi ya utafutaji na uendelezaji wa visima vipya ili kuhakikisha upatikanaji wa gesi ya kutosha hususan ikizingatiwa kuwa miundombinu ya usafirishaji tayari ipo nchini pamoja na kutekeleza kikamilifu miradi ya uwajibikaji kwa jamii katika maeneo ya mradi kwa kushirikiana na wananchi kutatua changamoto kama ujenzi wa vyumba vya madarasa uchimbaji wa visima vya maji na miradi mingine kulingana na mahitaji ya eneo husika

Vilevile, Waziri Ndejembi amesema Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kupitia Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 imelenga kuongeza upatikanaji na matumizi ya gesi asilia hatua itakayowezesha kufikiwa kwa lengo la kuzalisha megawati 8000 za umeme ifikapo mwaka 2030

Awali, Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi Dkt. James Mataragio amesema kitalu cha Ntorya kitaongeza upatikanaji wa gesi asilia huku akibainisha kuwa mahitaji ya gesi hiyo yanaongezeka kila siku na wawekezaji wa viwanda wamekuwa wakiwasilisha maombi ya gesi hiyo

Mradi wa bomba la kusafirisha gesi asilia ghafi kutoka kitalu cha Ntorya ulisainiwa tarehe 3 Julai 2025 kati ya TPDC na mkandarasi wa kampuni za China Petroleum Pipeline Engineering Co. Ltd. na China Petroleum Technology & Development Corporation kwa thamani ya Dola za Marekani Milioni 46.8 na unatarajiwa kukamilika ifikapo tarehe 30 Septemba 2026.












Mbunge wa Jimbo la Kisarawe,Mhe.Dkt. Selemani Jafo, ameendelea kuonesha dhamira yake ya dhati katika kuboresha huduma za afya kupitia kampeni yake ya “Kila Mtu Atibiwe Kwao”, inayolenga kuhakikisha kila kijiji kinakuwa na zahanati ili kusogeza huduma karibu na wananchi.

Akiwa katika ziara ya kuwashukuru wananchi wa Kitongoji cha Kola, Jafo amechangia tofali 1,500 kwa ajili ya ujenzi wa zahanati mpya itakayohudumia wakazi wa eneo hilo.

"Mchango huo ni sehemu ya mkakati mpana wa kupunguza adha ya wananchi kusafiri umbali mrefu kufuata matibabu, hususan wajawazito, watoto na wazee ambao kwa muda mrefu wamekumbana na changamoto ya kukosa huduma za afya karibu na makazi yao."amesema Dkt.Jafo

Akizungumza na wananchi, Dkt.Jafo amesisitiza kuwa afya ni haki ya msingi kwa kila mwananchi na kwamba ni wajibu wa viongozi kuhakikisha huduma hizo zinapatikana kwa urahisi bila usumbufu.

Ameeleza kuwa kampeni ya “Kila Mtu Atibiwe Kwao” inalenga kukamilisha ujenzi wa zahanati katika kila kijiji ndani ya jimbo hilo, ili kuimarisha ustawi wa jamii na kupunguza vifo vinavyoweza kuzuilika.

Aidha amebainisha kuwa katika kipindi cha miaka mitano kuanzia 2020 hadi 2025, aliweza kuhamasisha ujenzi wa zahanati 27 kupitia ushirikiano wa Mfuko wa Jimbo, Halmashauri, Serikali Kuu pamoja na wadau wa maendeleo.

Amesema mafanikio hayo yanatoa msingi imara wa kuendeleza juhudi zaidi katika awamu ijayo.

Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Masaki, Pili Kondo Chamgui, amempongeza Dkt.Jafo kwa juhudi zake za kuwajali wananchi. Ameeleza kuwa kwa sasa vijiji vyote vya kata hiyo vina zahanati, huku Kituo cha Afya cha Masaki kikiwa kinatoa pia huduma za upasuaji, hatua iliyopunguza kwa kiasi kikubwa rufaa zisizo za lazima.

Ameongeza kuwa ujenzi wa zahanati katika Kitongoji cha Kola utakuwa mkombozi mkubwa kwa wakazi wa eneo hilo ambao hulazimika kusafiri zaidi ya kilometa sita kufuata huduma za afya katika kijiji mama cha Kisanga.

Nao,Wananchi wa Kitongoji cha Kola, wameeleza shukrani zao kwa mbunge huyo, wakisema amesikia kilio chao cha muda mrefu cha ukosefu wa huduma za afya karibu na makazi yao. Walisema changamoto hiyo ilikuwa ikiweka maisha yao hatarini hasa wakati wa dharura za kiafya.

Kwa ujumla, kampeni ya “Kila Mtu Atibiwe Kwao” inaendelea kuleta matumaini mapya kwa wananchi wa Kisarawe, huku ushirikiano kati ya viongozi na jamii ukiwa chachu muhimu ya kusogeza huduma bora za afya karibu zaidi na wananchi.

Eneo la Hifadhi ya Ngorongoro jana tarehe 26 Februari 2026 limepokea ugeni mzito uliongozwa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi wa Tanzania, Mhe. Patrobas Paschal Katambi na Waziri wa Mambo ya Ndani na Usalama wa Jamhuri ya Zambia Mhe. Jacob Jack Mwiimbu pamoja na ujumbe wa wageni 70  wa majeshi ya ulinzi na usalama waliopo nchini kwa majukumu mbalimbali na kufanya utalii hifadhi ya Ngorongoro.

Waheshimiwa mawaziri na Ujumbe wao waliopata fursa ya kutembelea vivutio vilivyopo Ngorongoro na kushuhudia Wanyama wakubwa watano (Simba, Chui, Nyati, faru na Tembo), makundi ya Pofu, pundamilia, swala, Nyumbu, Ngiri, Viboko, ndege, mimea ya asili, kasoko ya Ngorongoro na kupata simulizi mbalimbali kuhusu utalii wa miamba na hadhi tatu za kitamaifa zilizopo Ngorongoro.  

Mhe. Katambi ameipongeza Ngorongoro kwa uhifadhi unaozingatia usalama wa mazingira, kulinda fahari ya Ngorongoro kama kivutio bora cha utalii Afrika.







 Mtendaji Mkuu Dkt. Maulid J. Maulid amefunga mafunzo ya uongozi na usimamizi wa shule yaliyoendeshwa kwa Wakuu wa Shule za Sekondari za Wilaya ya Arusha pamoja na viongozi wa elimu kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Arusha. 


Mafunzo hayo yameendeshwa na ADEM kwa muda wa siku tatu kuanzia tarehe 24-26 Februari, 2026 ADEM Bagamoyo.

Akifunga mafunzo hayo amewasisitiza viongozi hao wa elimu kwenda kuweka mkazo kwenye uongozi bunifu wa kimkakati unaoleta mabadiliko kama msingi wa maendeleo katika taasisi za elimu.

Pia amesisitiza juu ya uongozi jumuishi ambapo wanapaswa kushirikisha wadau, kusikiliza maoni ya jamii na kujenga mazingira ya uaminifu na uwajibikaji wa pamoja katika kufikia mafanikio ya usimamizi wa taasisi za elimu wanazozisimamia.

“Nawasihi mwende kuwa viongozi wenye maono, wenye uwezo wa kufanya maamuzi ya kimkakati, na ujuzi wa kusimamia mabadiliko ya taasisi mnazosimamia kwa ufanisi kwani ninyi ndio mtachochea mabadiliko hayo”. Ameeleza Dkt. Maulid.

Aidha, Makamu Mkuu wa Chuo Taaluma, Tafiti na Ushauri Elekezi Dkt. Lucas Mzelela amesema, mafunzo ya ADEM yamelenga kuwawezesha viongozi wa elimu kwa ujuzi wa vitendo, fikra za kimkakati na uwezo wa kusimamia taasisi za elimu kwa ufanisi ili kuleta mabadiliko ya kweli katika sekta ya elimu.

Nae Mwenyekiti wa TAHOSSA Mkoa wa Arusha, Mwalimu Omari Nyangu ameipongeza ADEM kwa namna ilivyoendesha mafunzo hayo kwa umahiri na weledi mkubwa na kutanabaisha kuwa maendeleo ya sekta ya elimu hayawezi kupatikana bila uwekezaji katika kuwajengea uwezo viongozi na wasimamizi wa taasisi za elimu na mafunzo waliyopatiwa ni dira katika usimamizi wa taasisi za elimu wanazozisimamia.

Wakuu hao wa shule wamejengewa uwezo kuhusu utawala bora wa elimu, Mpango wa Jumla wa Maendeleo ya Shule, usimamizi wa utekelezaji wa Mtaala, ustawi na usalama wa wanafunzi shuleni, ushirikishwaji wa jamii katika kuleta maendeleo ya shule, usimamizi wa rasilimali za shule, kuzingatia itifaki na huduma kwa wateja pamoja na ufuatiliaji na tathmini wa shughuli za elimu shuleni.