Dar es Salaam.

Wananchi wa Jiji la Dar es Salaam wanatarajiwa kushuhudia uzinduzi wa kampeni maalum ya kitaifa ijulikanayo kama Muungano Caravan, yenye lengo la kuelimisha jamii kuhusu umuhimu wa Muungano wa Tanzania pamoja na kuhamasisha uzalendo, mshikamano wa kitaifa na ushiriki wa wananchi katika maendeleo ya nchi.

Uzinduzi huo unatarajiwa kufanyika katika maeneo mbalimbali ya Dar es Salaam, huku mamia ya wananchi, vijana, viongozi wa serikali, wadau wa maendeleo, wanafunzi pamoja na makundi mbalimbali ya kijamii wakitarajiwa kushiriki kwa wingi katika shughuli hiyo muhimu ya kitaifa.

Kwa mujibu wa waandaaji wa kampeni hiyo, Muungano Caravan ni jukwaa maalum litakalowakutanisha wananchi kutoka makundi tofauti ili kupata elimu kuhusu historia ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, mafanikio yaliyopatikana tangu kuanzishwa kwake, pamoja na nafasi ya wananchi katika kuuenzi na kuulinda Muungano huo kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Wadau hao wameeleza kuwa vijana ndio walengwa wakuu wa kampeni hiyo kutokana na umuhimu wa kuwajengea uelewa mpana kuhusu tunu za taifa, historia ya nchi na wajibu wao katika kudumisha amani na umoja wa Watanzania.

Kupitia maonesho mbalimbali, mijadala ya wazi, semina za elimu ya uraia na vipindi vya maswali na majibu, wananchi watapata nafasi ya kujifunza kwa kina kuhusu hatua zilizopigwa katika sekta mbalimbali kutokana na Muungano ikiwemo elimu, biashara, uwekezaji, michezo, utamaduni na maendeleo ya kijamii.

Aidha, waandaaji wamebainisha kuwa vijana wengi wamekuwa wakihitaji elimu ya kina kuhusu Muungano ili waweze kuelewa chimbuko lake, faida zake na changamoto zinazoweza kujitokeza. Kupitia kampeni hiyo, vijana watapata nafasi ya kuuliza maswali moja kwa moja kwa wataalamu na viongozi wanaohusika na masuala ya Muungano.

Mbali na elimu hiyo, washiriki watapata nafasi ya kushiriki katika Muungano Challenge, shindano maalum litakalotoa zawadi mbalimbali kwa washiriki watakaofanya vizuri katika maswali yanayohusu Muungano, uzalendo, historia ya Tanzania na masuala ya maendeleo ya taifa.

Tamasha hilo pia linatarajiwa kupambwa na burudani kutoka kwa wasanii mbalimbali maarufu nchini, vikundi vya ngoma za asili, muziki wa kizazi kipya pamoja na sanaa za maonesho zitakazobeba ujumbe wa umoja, amani na uzalendo.

Katika kuhakikisha ujumbe unawafikia wananchi wengi zaidi, msafara wa Muungano Caravan utaendelea katika wilaya mbalimbali za Dar es Salaam zikiwemo Ilala, Temeke, Kinondoni, Kigamboni na Ubungo. Kila eneo litakuwa na programu maalum za elimu, burudani na ushiriki wa wananchi ili kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa Muungano katika maendeleo ya taifa.

Akizungumza kuhusu kampeni hiyo, mmoja wa waratibu alisema kuwa dhamira kuu ni kujenga kizazi chenye uelewa wa historia ya taifa lao na kinachothamini amani, umoja na mshikamano uliopo nchini.

“Tunataka vijana wawe mstari wa mbele katika kuujua na kuuenzi Muungano wetu. Elimu hii ni muhimu kwa sababu vijana ndio viongozi wa kesho, hivyo wanapaswa kuelewa mchango wa Muungano katika kulinda amani na kuleta maendeleo ya taifa letu,” alisema.

Aidha, viongozi mbalimbali wa kijamii na wadau wa maendeleo wamepongeza kuanzishwa kwa kampeni hiyo wakisema kuwa itasaidia kuimarisha mshikamano wa kitaifa na kuongeza uelewa kwa wananchi kuhusu masuala ya Muungano ambayo kwa muda mrefu yamekuwa yakihitaji elimu zaidi hasa kwa kizazi cha vijana.

Kaulimbiu ya kampeni hiyo ni:
*“Safari ya Umoja – Tudumishe Muungano Wetu kwa Maendeleo Endelevu.”*

Wananchi wametakiwa kujitokeza kwa wingi kushiriki katika uzinduzi huo ambao unatarajiwa kuwa mwanzo wa harakati mpya za kuendeleza uzalendo, elimu ya uraia na mshikamano wa kitaifa nchini Tanzania.




 



Naibu Waziri wa Nishati, Salome Makamba amesema hadi Aprili 2026, jumla ya nyumba 2,512 zimeunganishwa na miundombinu ya gesi asilia katika mikoa ya Mtwara, Lindi, Pwani na Dar es Salaam.

Mhe. Salome ametoa taarifa hiyo Mei 8, 2026 bungeni jijini Dodoma alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Asha Omar Rashid, aliyetaka kujua mpango wa Serikali wa kuboresha upatikanaji wa nishati ya gesi vijijini.

Akijibu swali hilo, Mhe.Salome amesema Serikali kupitia Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) inaendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya usambazaji wa gesi asilia, ambapo hadi Aprili 2026 nyumba 425 zimeunganishwa katika Mkoa wa Mtwara, 677 Mkoa wa Lindi, 530 Mkoa wa Pwani na 880 Mkoa wa Dar es Salaam.

Aidha, amesema katika kuhakikisha nishati ya gesi inawafikia Watanzania wengi zaidi, Wakala wa Nishati Vijijini (REA) unaendelea kutekeleza mradi wa kusambaza mitungi 452,445 ya Gesi Oevu ya Petroli (LPG) yenye ujazo wa kilogramu sita kwa ruzuku ya asilimia 50 ili kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia katika maeneo ya vijijini na vijiji-miji.

Vilevile, Serikali inaendelea kuhamasisha sekta binafsi kuwekeza katika miundombinu ya usambazaji wa gesi ya LPG katika maeneo ya vijijini na vijiji-miji.

Mhe. Salome amesema Serikali pia inaendelea kufanya tafiti katika maeneo ya mijini na vijijini ili kubaini aina sahihi ya miundombinu inayohitajika kwa ajili ya kufikisha na kusambaza gesi asilia kwa ufanisi zaidi.

Amefafanua kuwa matokeo ya tafiti hizo yatawezesha kubainisha njia bora za usambazaji wa gesi asilia kulingana na mahitaji ya maeneo husika, sambamba na kuibua fursa za kuanzishwa kwa miradi mingine ya usambazaji wa gesi asilia itakayotekelezwa kwa ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi ili kuhakikisha wananchi wengi zaidi mijini na vijijini wananufaika na nishati hiyo safi.

 


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete amesema Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameendelea kupeleka furaha na neema kwa watumishi wa umma nchini, kutokana na uamuzi wake wa hivi karibuni wa kuridhia kuwapandisha madaraja watumishi 219,042 ikiwa ni hatua ya kihistoria katika kuimarisha Utumishi wa Umma nchini.

Mhe. Kikwete amesema hayo wakati akizungumza na Maafisa Tawala na RasilimaliWatu , katika mkutano uliofanyika Ukumbi wa AICC, Arusha na kuwakumbusha kutekeleza wajibu wa kuwahudumia watumishi wa umma wenzao ili kuleta furaha miongoni mwao na hatimae wapeleke tabasamu kwa watanzania, kama Mheshimiwa Rais alivyoelekeza.

“Ninawaelekeza mkatimize wajibu wa kuwahudumia watumishi wa umma wenzenu ili wawe na ari na morali ya kuwatumikia wananchi, na kwa kufanya hivyo mtakuwa mnaunga mkono kwa vitendo jitihada na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan za kuhakikisha maslahi ya Watumishi wa umma nchini yanaendelea kuboreka,” alisisitiza Mhe. Kikwete.

Mhe. Kikwete amefafanua kuwa, upandishaji wa madaraja watumishi 219,042 uliotokana na ridhaa ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, pamoja na ongezeko la mishahara ya watumishi wa umma (2025): +35.1% , Ongezeko la kima cha chini sekta binafsi (2025/26): +33.4%, utapelekea Sekta mbalimbali kuathiriwa na maboresho haya ikiwemo afya, elimu, kilimo, mawasiliano, usafirishaji, nishati, viwanda, biashara, hoteli, michezo, uvuvi, baharini, madini na utamaduni. 

Mhe. Kikwete ameanisha kuwa, Matokeo haya kitakwimu yanaonyesha kasi ya mageuzi ya kiutumishi chini ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ambayo imekuwa kinara katika uongozi wa kimkakati, ambao umejipambanua kuweka mbele ustawi wa watumishi wa umma na ufanisi wa utendaji kazi wa taasisi za umma nchini.

Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Jamhuri ya Zambia zimeazimia kuendelea kuchukua hatua katika kuondoa vikwazo vya biashara ili kurahisisha usafirishaji wa bidhaa, huduma na watu, hatua inayolenga kuimarisha zaidi ushirikiano wa kiuchumi, biashara na uwekezaji kati ya mataifa hayo mawili.
Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii Dkt. Hassan Abbasi leo Mei 7, 2026, ameongoza ujumbe wa Tanzania kushiriki Mkutano wa Kimataifa unaowakutanisha Wadau wa Utalii Duniani chini ya Baraza la Usafiri na Utalii Duniani (WTTC) unaofanyika ndani ya meli ya Crystal Serenity inayosafiri kutoka bandari ya Sokhna kuelekea Alexandria nchini Misri.



Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda,  akiwasilisha Hotuba ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 leo Mei 7,2026  bungeni Dodoma.


Serikali imeendelea kuimarisha ushirikiano wa kitaifa, kikanda na kimataifa katika sekta ya elimu ya juu kwa lengo la kukuza ubora wa elimu, kubadilishana maarifa na kuendeleza lugha ya Kiswahili pamoja na taaluma mbalimbali nchini.

Hayo yameelezwa leo bungeni na Waziri wa Wizara hiyo,Prof Adolf Mkenda wakati akiwasilisha mapato na matumizi ya Wizara hiyo Kwa mwaka wa fedha 2026-2027.

Amesema kuwa Serikali itaendelea kutoa ufadhili kwa wanafunzi wa kimataifa wanaosoma katika vyuo vikuu vya Tanzania kama sehemu ya mkakati wa kuimarisha diplomasia ya elimu na kukuza nafasi ya nchi katika ramani ya elimu duniani.

“Serikali itaendelea kuwafadhili wanafunzi 15 raia wa China wanaosoma Lugha ya Kiswahili katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, hatua inayolenga kukuza na kubiasharisha Kiswahili kimataifa. Aidha, wanafunzi wawili raia wa Oman pamoja na wanafunzi watano raia wa Hungaria wataendelea kusoma katika vyuo vikuu vya Tanzania kwa kuzingatia mikataba na taratibu za ushirikiano wa elimu ya juu.”amesema 

Hatua hiyo inalenga kuimarisha ushirikiano wa kielimu na kitamaduni kati ya Tanzania na mataifa mengine, sambamba na kuongeza mvuto wa vyuo vikuu vya nchini kama kituo cha kimataifa cha elimu.

Katika upande mwingine, Serikali itaendelea kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia katika vyuo vikuu na taasisi za sayansi na teknolojia kwa kuwekeza katika miundombinu muhimu ya elimu. Hii ni pamoja na ujenzi na ukarabati wa vyumba vya semina, kumbi za mihadhara, madarasa, ofisi, maabara, maktaba pamoja na miundombinu mingine ya kitaaluma.

Utekelezaji wa maboresho hayo unafanyika katika taasisi 21 za elimu ya juu kupitia Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi, hatua inayolenga kuongeza ubora wa elimu, utafiti na ubunifu ili kuchochea maendeleo ya taifa.

Serikali imeeleza kuwa jitihada hizo ni sehemu ya mkakati mpana wa kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha elimu ya juu na utafiti barani Afrika, huku ikituza matumizi ya Kiswahili na kuongeza ushindani wa wahitimu wake katika soko la ajira la kimataifa.

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu TAMISEMI, Profesa Riziki Shemdoe, ameipongeza Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma kwa kuandaa mpango wa kuwapeleka walimu 40 kwenda kusoma Korea Kusini, akieleza kuwa ni hatua muhimu ya kuimarisha ubora wa elimu nchini.




Waziri wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (Mb), leo tarehe 6 Mei, 2026 amefungua rasmi Mkutano Mkuu wa Pili wa Mwaka wa Jumuiya ya Wataalamu wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu katika Utumishi wa Umma (AAPAM), unaowakutanisha wadau mbalimbali wa sekta hiyo.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mkutano huo uliofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC), Waziri Ridhiwani alisisitiza umuhimu wa wataalamu wa Rasilimali watu katika kuimarisha utendaji na ufanisi wa taasisi za umma ambapo alibainisha kuwa mchango wao ni muhimu katika kufanikisha utoaji wa huduma bora ili kuendana na kasi ya mabadiliko ya kiutawala na kiteknolojia.

Aidha, alieleza kuwa Serikali inaendelea kuweka mazingira rafiki kwa wataalamu hao ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa weledi.


Katika ziara yake katika mabanda ya maonesho yanayoambatana na mkutano huo, Mhe. Ridhiwani alitembelea banda la Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA), ambapo alipata fursa ya kujionea shughuli mbalimbali zinazotekelezwa na taasisi hiyo pamoja na maboresho ya huduma zake.

Meneja Masoko na Uhusiano kwa Umma TEMESA Bi Martha Joachim akimkabidhi zawadi Waziri
wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (Mb)

Akiwa katika banda hilo, aliipongeza TEMESA kwa kumpata Mtendaji Mkuu mpya, nakusema hatua hiyo imeashiria fursa ya kuimarisha zaidi uongozi, kuongeza ubunifu na kuleta matokeo chanya katika utoaji wa huduma kwa umma.


“TEMESA kwanza nawapongeza kwa kupata mtendaji mpya naamini mabadiliko haya yataleta chachu ya kiutendaji na utoaji wa huduma bora hongereni sana.” Amesema Mhe. Ridhiwani.


Mkutano huo wa siku nne umebeba kaulimbiu isemayo: “Kufikiri upya utoaji wa huduma kwa umma: Jinsi Serikali inavyoweza kutumia teknolojia kuanzisha huduma bora na zinazomlenga mwananchi, kukabiliana na ukosefu wa ajira kwa vijana pamoja na changamoto za mazingira.”
Wafanyabiashara Wa Kijiwe cha Raha Square Wamepata Fursa Ya Kukutana Na Kaimu Meneja Wa Kariakoo Bw.Edson Issanya, ambapo waliwasilisha changamoto mbalimbali wanazokutana nazo katika utekelezaji wa majukumu yao ya kikodi, ikiwemo uelewa mdogo wa masuala ya kodi.
Uongozi wa Taasisi ya LALJI FOUNDATION ukiwa katika picha ya pamoja na wanachama wa Chama cha Wanawake Wajane Tanzania (CCWWT) mkoani Kigoma mara baada ya kukabidhi mizinga 50 ya nyuki, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuwawezesha wajane kiuchumi kupitia ufugaji nyuki.
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

Hatua ya Benki ya Biashara ya Mwalimu (MCB) kuuza hisa stahiki imeelezwa kuwa chachu ya kuimarisha mtaji na kupanua wigo wa utoaji wa mikopo nafuu kwa walimu pamoja na wafanyabiashara wadogo nchini.

 


Na Oscar Assenga,LUSHOTO

Benki ya CRDB imeendelea kudhihirisha dhamira yake ya kuchangia maendeleo ya jamii kwa kutoa zaidi ya shilingi bilioni 2.7 katika mwaka uliopita, fedha ambazo zimeelekezwa kwa kiasi kikubwa katika sekta ya elimu na uwezeshaji wa wananchi kiuchumi.

Akizungumza katika hafla ya kukabidhi vyumba viwili vya madarasa pamoja na ofisi ya walimu katika Shule ya Msingi Kwendoghohi, iliyopo Kata ya Usambara wilayani Lushoto, Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi Taasisi ya CRDB Bank Foundation, Marian Balampama, alisema kati ya fedha hizo, shilingi bilioni 1 zimetumika kuboresha elimu.

Alieleza kuwa uwekezaji huo umejumuisha ujenzi wa madarasa, ununuzi wa madawati, pamoja na upatikanaji wa vifaa vya kufundishia na kujifunzia, ikiwemo maabara. Alisisitiza kuwa benki hiyo haijikita tu katika miundombinu, bali pia inahakikisha mwanafunzi anapata mazingira salama na bora ya kujifunzia.

Mbali na elimu, CRDB pia imewekeza katika kuwawezesha wananchi kiuchumi kupitia programu mbalimbali. Balampana alisema benki hiyo inaamini kuwa kumwezesha mtu mmoja ni sawa na kuinua familia na jamii kwa ujumla.

Kupitia kampuni tanzu ya CRDB Bank Foundation na programu ya Embeju, zaidi ya wanufaika 500,000 pamoja na vikundi mbalimbali wamenufaika. Alifafanua kuwa uwezeshaji huo hauishii kwenye utoaji wa fedha pekee, bali pia unahusisha mafunzo ya ujuzi na mbinu za kutambua masoko ili kuongeza tija na faida.

Aidha, alibainisha kuwa benki hiyo imekuwa ikiangalia pia changamoto nyingine za kijamii, ikiwemo upatikanaji wa huduma za afya, kwa lengo la kuboresha ustawi wa wananchi kwa ujumla.

“Sisi tunajisikia fahari kushirikiana na Serikali, hususan katika kusimamia mikopo ya asilimia 10 katika baadhi ya mikoa, ili kuhakikisha fedha zinawafikia walengwa na kuleta matokeo chanya,” alisema Balampana.

Aliongeza kuwa CRDB inaendelea kushirikiana kwa karibu na viongozi wa Wilaya ya Lushoto pamoja na Mkoa wa Tanga katika kutekeleza miradi ya maendeleo.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Lushoto, Zephania Sumaye, aliishukuru benki hiyo kwa mchango huo, akisema ujenzi wa madarasa hayo utasaidia kupunguza msongamano wa wanafunzi na kuboresha mazingira ya kujifunzia.

Alieleza kuwa shule hiyo, iliyoanzishwa mwaka 1965, ilikuwa na miundombinu iliyochakaa, hivyo msaada huo unaleta matumaini mapya katika kuinua ubora wa elimu katika eneo hilo.

Kwa ujumla, hatua ya CRDB inaonesha namna taasisi za kifedha zinavyoweza kuwa chachu ya maendeleo kwa kurejesha kwa jamii sehemu ya mapato yao, sambamba na kuunga mkono juhudi za Serikali kufikia dira ya maendeleo ya Taifa ya mwaka 2050.







Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi amesema Serikali inachukua hatua katika kuimarisha uwezeshaji wanawake kiuchumi pamoja na kuongeza uelewa kuhusu mifuko ya maendeleo inayowanufaisha wanawake.

Akizungumza Mei 6, 2026 bungeni jijini Dodoma, Mhe. Mahundi amesema Serikali imeweka mikakati mbalimbali ya kuhakikisha wanawake wengi zaidi wanapata taarifa na kunufaika na Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake (WDF), ikiwa ni pamoja na kushirikiana na taasisi za fedha na wadau wa maendeleo kutoa mafunzo ya ujasiriamali na uendeshaji wa biashara kupitia makongamano ya kikanda.

 “Serikali itaendelea kushirikiana na Wizara ya Fedha, TAMISEMI pamoja na Baraza la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi kuhakikisha makundi ya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu yanapatiwa mafunzo na fursa za mikopo nafuu.” amesema Mhe. Mahundi

Katika swali lingine, ameeleza kuwa Serikali inaendelea kuimarisha mifuko iliyopo badala ya kuanzisha mipya, ikiwemo Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake unaotoa mikopo yenye masharti nafuu kwa wanawake wajasiriamali. 

"Kupitia ushirikiano na Benki ya Dunia, Serikali ipo katika hatua za mwisho za kuanza utoaji wa mikopo kupitia mradi wa PAMOJA, hatua itakayopanua wigo wa wanawake kunufaika na fursa za kiuchumi". amesema Mhe. Mahundi

Ameeleza kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na sekta binafsi, taasisi za fedha na wadau wa maendeleo ili kuhakikisha wanawake wanajengewa uwezo wa kiuchumi na kuchangia kikamilifu katika maendeleo ya taifa.

Dar es Salaam, Mei 5, 2026

Kampuni changa (startups) nchini waaswa kuongeza juhudi katika kukuza ubunifu na kuugeuza kuwa bidhaa ama huduma zenye ushindani, hatua iliyotajwa kuwa mhimili muhimu wa kukuza uchumi wa taifa na kuimarisha ajira kwa vijana.

 


Maadhimisho ya siku ya Urithi wa Dunia Afrika yaliyofanyika katika Makumbusho ya Urithi Jiopaki mjini Karatu tarehe 5 Mei, 2026 yameyakutanisha  wanafunzi wa shule za msingi na sekondari ikiwa na lengo la kuwarithisha kizazi kipya historia na elimu ya urithi na utamaduni.

Mkuu wa wilaya ya Karatu Mhe. Dkt Lameck Karanga amesema uwepo wa makabila hayo, historia yao pamoja na kuenzi tamaduni zao ni utajiri mkubwa kwa Tanzania na kutoa wito kwa wadau na jamii kwa ujumla kuendelea kulinda maeneo ya urithi wa dunia na kuibua maeneo mapya yatakayoingizwa katika orodha ya Urithi wa Dunia ili kuongeza thamani ya ubora wa kipekee ulimwenguni (Outstanding Universal Value) na kuvutia wageni wengi zaidi.

Naibu Kamishna wa Uhifadhi, Utalii na Maendeleo ya Jamii Ngorongoro Joas Makwati ameeleza kuwa mamlaka itaendelea kuongeza juhudi za kulihifadhi eneo la Ngorongoro ambalo ni urithi wa dunia na  kultangazia zaidi kama eneo pekee lenye Ushahidi wa kisayansi  kuhusu historia ya binadamu unaoeleza kuwa binadamu kwa kuthibitishwa na ugunduzi wa masalia ya binadamu wa kale na zana za mawe zilizopatikana katika bonde la Olduvai. 

Kwa upande wake Naibu Katibu wa Tume ya Taifa ya UNESCO Tanzania Dkt. Khamis Said ameeleza kuwa tangu Tanzania ijiunge na UNESCO imepata mafanikio mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuridhia mikataba kumi (10) ya  UNESCO,Kuwepo kwa Hifadhi Hai za Mwanadamu na Mazingira  sita (6)  na Kuwepo kwa maeneo saba (7) ya urithi wa Dunia.

Kauli mbiu ya siku ya urithi wa dunia kwa mwaka huu ni “Kusherekea siku ya Urithi wa Dunia na kukuza Viongozi wa baadaye”. (Celebrating Africa’s Heritage, Mentoring the Leaders of Tomorrow).

Chuo Kikuu Mzumbe kupitia Shule yake ya Biashara kimeandaa tukio la Siku ya Mzumbe na Kambi ya Wajasiriamali, litakalofanyika kwa mara ya kumi mfululizo katika Kampasi Kuu Morogoro, kuanzia Mei 6 hadi 8, 2026.

 



Na OWM - TAMISEMI, Dodoma


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) Mhe. Prof. Riziki Shemdoe na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof.  Adolf Mkenda wamewapokea walimu wapatao 150 wa amali waliokwenda kwenye ziara ya mafunzo ya mwezi mmoja nchini India, ambayo yatawawezesha kutoa elimu ya ufundi na mafunzo ya stadi za kazi nchini ili kukuza uchumi wa viwanda, kupunguza ukosefu wa ajira kwa vijana, na kuwajengea uwezo wa kushindana katika soko la ajira.

Walimu hao mara baada ya kurejea nchini, walipata mwaliko wa Mhe. Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba kuhudhuria shughuli za Bunge Mei 04, 2026 jijini Dodoma na kupokelewa kwa pamoja na Waziri wa TAMISEMI Mhe. Prof Shemdoe na Waziri wa Elimu Mhe. Prof. Mkenda ambao ofisi zao ziliratibu ziara ya mafunzo ya walimu hao  nchini India.

Akizunguza na walimu hao katika viwanja vya Bunge, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu -TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe ameshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuidhinisha fedha kiasi cha Shilingi Bilioni 3 na kutoa kibali cha walimu hao kwenda kwenye ziara ya mafunzo nchini India ili kujifunza na kupata ujuzi utakaowawezesha kuleta athari chanya zaidi katika mfumo wa elimu ya ufundi.

Sanjari na hilo, Prof. Shemdoe amewataka walimu hao kuhakikisha yote waliyojifunza nchini India wanaenda kuwafundisha wanafunzi madarasani na kwa vitendo ili wapate ujuzi utakaowawezesha kuwa wabunifu, wajasiriamali na uwezo wa kushindana katika ajira za ndani na nje ya nchi ikiwa ni pamoja na kujiajiri.

“Vijana wetu wanahitaji kupata maarifa na ujuzi mlioupata kwenye ziara yenu ya mafunzo nchini India, hivyo nendeni mkawafundishe kwa umahiri ili waje kutoa mchango katika maendeleo ya taifa,” amesisitiza Prof. Shemdoe.

Naye, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof.  Adolf Mkenda amesema kuwa Serikali iliwapeleka walimu hao wapatao 150 nchini India kwenda kujifunza namna wanavyoendesha shule za amali na kutekeleza mtaala wao wa elimu ili wakirejea nchini waweze kuwa chachu ya kutekeleza vema mtaala mpya wa elimu kwa kutumia vema teknolojia iliyopo katika kuwafundisha vijana wa kitanzania elimu ya ufundi stadi.

“Sisi tulichukua walimu 150 na kuwapeleka India ili waende kujifunza namna masomo ya elimu ya amali yanavyofundishwa ili wakirejea waje kuwa chachu ya kuboresha namna ya kufundisha masomo ya amali, hatua hii ni sehemu ya utekelezaji wa maelekezo ya mapema ya Mhe. Rais kwa wizara ya Elimu na yale aliyoyatoa wakati akizindua sera yetu ya elimu,” amesema Prof. Mkenda.

Tanzania imepiga hatua muhimu katika kuboresha afya na ustawi wa vijana kwa uzinduzi rasmiwa Kozi Mtandao ya Elimu ya Stadi za Maisha na Afya ya Uzazi (CSE) chini ya mradi wa“Maisha yetu, Haki Zetu, Mustakabali wetu”- (O3 Plus). 

*Watoto wanaolazwa wapungua kutoka 32 hadi 7 kwa robo mwaka

Na Augusta Njoji

IDADI ya watoto wanaokabiliwa na utapiamlo mkali katika Halmashauri ya Mji Handeni imepungua kwa kiasi kikubwa, kutoka watoto 32 waliokuwa wakilazwa hospitalini kwa robo mwaka 2024/25 hadi wastani wa watoto watano hadi saba kwa robo mwaka 2025/26.

Mafanikio hayo yanatajwa kuchangiwa na mikakati madhubuti ya utoaji elimu ya lishe kwa jamii inayotekelezwa na Hospitali ya Halmashauri hiyo, ikilenga kupunguza lishe duni hususan kwa watoto.

Akizungumza Mei 5, 2026 katika kikao cha tathmini ya shughuli za lishe kwa kipindi cha Januari hadi Machi 2025/26, Afisa Tarafa ya Chanika, Julieth Mushi, akimwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese, amepongeza juhudi hizo na mafanikio yaliyopatikana katika utekelezaji wa mkataba wa lishe.

Amesisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya Idara ya Afya, Ustawi wa Jamii na Lishe pamoja na Idara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi katika kuhamasisha jamii kuanzisha bustani za mboga majumbani na kufuga wanyama ili kukabiliana na tatizo la utapiamlo kwa watoto.

Kwa upande wake, Mganga Mkuu wa Halmashauri hiyo, Dkt.Hudi Shehdadi, amesema mikakati inayoendelea kutekelezwa ni pamoja na kushirikiana na Idara za Elimu ya Msingi na Sekondari pamoja na kamati za lishe za kata kuhamasisha upandaji wa miti ya matunda na uanzishaji wa bustani za mboga, huku kila shule ikitakiwa kutenga angalau hekari mbili kwa ajili ya kilimo cha mahindi.

Aidha, amebainisha kuwa juhudi zimeongezwa katika kuhamasisha wajawazito kuhudhuria huduma za afya mapema ili kupata elimu ya lishe pamoja na virutubisho vya madini chuma, hatua inayolenga kupunguza idadi ya watoto wanaozaliwa na uzito pungufu.

Awali, akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa shughuli za lishe kwa kipindi cha Januari hadi Machi 2025/26, Kaimu Afisa Lishe wa Halmashauri hiyo, Getruda Kasabaja, amesema jumla ya wazazi na walezi 9,571 wamefikiwa na elimu ya lishe, huku watoto 17,390 wakifanyiwa tathmini ya hali ya lishe.

Ameeleza kuwa kati ya watoto hao, watoto 221 walikuwa na uzito pungufu sawa na asilimia 1.27, watoto 80 walikuwa na udumavu (asilimia 0.4), na watoto 96 walikuwa na ukondefu (asilimia 0.55). Aidha, watoto saba walipatiwa matibabu ya utapiamlo mkali katika kipindi hicho.