Dkt.Kiruswa Ataka Ujenzi Kuharakishwa, Asisitiza Uongezaji Thamani Nchini

Tayari WanaKigamboni 278 Wameajiriwa, Zaidi ya Asilimia 90 ni Watanzania

Mwezi Julai Pekee Mkoa wa Kimadini Dar/Pwani Umekusanya Bil 4.06

Tanzania imeingia katika Hatua Mpya ya Uendelezaji wa Madini Tembo (Heavy Mineral Sands), huku shughuli za uchimbaji zikiendelea kupitia Mradi wa Fungoni- Kigamboni na Tajiri sambamba na ujenzi wa Kiwanda cha Uchakataji wa Madini hayo Mkoani Tanga.

Uchimbaji na uchakataji wa Madini Tembo unatekelezwa kupitia Kampuni ya Ubia ya Nyati Mineral Sands Limited, ambapo Serikali inamiliki hisa zisizofifishwa za asilimia 16.

Akizungumza leo, Agosti 18, 2026, alipotembelea na kukagua shughuli za uzalishaji wa madini hayo katika Mradi wa Fungoni- Kigamboni, pamoja na kupata taarifa ya maendeleo ya ujenzi wa kiwanda cha uchakataji Tajiri- Tanga, Naibu Waziri wa Madini, Dkt. Steven Kiruswa, ameitaka kampuni hiyo kuharakisha ujenzi wa kiwanda hicho, akisisitiza dhamira ya Serikali ya kuongeza thamani ya madini nchini kabla ya kusafirishwa nje ya nchi.

Dkt. Kiruswa amesema Serikali imetoa kibali cha muda wa miaka miwili kwa kampuni hiyo kusafirisha madini ghafi nje ya nchi, hatua inayolenga kuipa kampuni nafasi ya kukamilisha ujenzi wa kiwanda na kukuza zaidi mtaji wa mradi.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa kampuni hiyo kuimarisha uhamishaji wa maarifa na ujuzi kwa Watanzania, kuongeza ushiriki wa Watanzania katika shughuli za mradi na kuendelea kuwajibika kwa jamii zinazozunguka maeneo ya mradi.

Vilevile,  Dkt. Kiruswa, amesisitiza kampuni kutekeleza Mpango wa Ufungaji wa Mgodi (Mine Closure Plan) kwa kurejesha maeneo yaliyotumika katika hali salama na yenye tija, huku athari kwa mazingira zikidhibitiwa.

Akielezea maendeleo ya Sekta ya Madini Mkoa wa Kimadini wa Dar es Salaam na Pwani, Dkt. Kiruswa amesema umeendelea kufanya vizuri katika ukusanyaji wa mapato ya Serikali ambapo katika mwaka wa Fedha 2025/26 ulikusanya Shilingi bilioni 27.07 dhidi ya lengo la Shilingi bilioni 24. Kwa mwaka wa fedha 2026/27, mkoa huo umepewa lengo la kukusanya Shilingi bilioni 33, huku tayari imekusanya Shilingi bilioni 4.06 kwa mwezi Julai pekee ambayo ni asilimia 147.50 ya lengo la mwezi ( bilioni 2.75).

Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa Nyati Mineral Sands Limited, Wei Huang, amesema kampuni mama, Shenghe Resources Holding Co. Ltd, imechagua Tanzania kuwa kitovu cha uchakataji wa Madini ya Tembo, ambapo madini yatakayozalishwa katika miradi yake nchi mbalimbali, ikiwemo Madagascar, yatachakatwa  Tanzania.

Amesema tangu mwaka 2024, jumla ya tani 85,000 za Madini Tembo zimezalishwa kupitia mradi wa Kigamboni, ambapo tani 14,793.35 tayari zimesafirishwa.

Akizungumzia thamani ya uwekezaji, Wei amesema miradi ya Kigamboni na Tajiri ina uwekezaji wa zaidi ya Dola za Marekani milioni 30, huku uwekezaji wa kampuni ya Shenghe nchini Tanzania ukifikia takribani Dola milioni 600, ukijumuisha mradi wa uchimbaji na uchakataji wa madini adimu (Rare Earth Elements) unaotekelezwa Mkoani Songwe.

Ameongeza kuwa zaidi ya asilimia 90 ya wafanyakazi katika miradi hiyo ni Watanzania, huku wakazi wa Kigamboni pekee wanaonufaika na ajira wakifikia 284. Kwa Mradi wa Kigamboni, uhai wa mgodi unakadiriwa kuwa miaka minne, huku mradi wa Tajiri, Tanga ukiwa na muda wa miaka 23 ya uwekezaji.

“Shenghe ina uzoefu wa kufanya shughuli hizi katika nchi mbalimbali duniani na tayari tumewekeza Australia, Canada, Nigeria, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na nchi nyingine. Tumeichagua Tanzania kutokana na mazingira ya uwekezaji na historia ya ushirikiano kati ya nchi hizi,” amesema Wei.

Naye, Afisa Tarafa wa Kigamboni, Augusta Safari, aliyemwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Kigamboni, amesema mradi huo umeanza kuleta manufaa kwa Wilaya hiyo kupitia mapato, ajira na utekelezaji wa shughuli za Uwajibikaji kwa Jamii (CSR). Amesema tayari fidia imelipwa kwa wakazi wote waliopisha mradi na Wilaya itaendelea kuhakikisha mazingira salama kwa uwekezaji.

Madini ya Tembo hutumika katika utengenezaji wa bidhaa mbalimbali, zikiwemo rangi za nyumba, vigae vya sakafu na ukutani pamoja na vipuri vya ndege, hivyo kuifanya Tanzania kuwa na fursa kubwa ya kuongeza thamani na kujenga mnyororo wa thamani wa madini hayo ndani ya nchi.







 


Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii leo Agosti 18, 2026 Bungeni Jijini Dodoma, imeipongeza Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia Taasisi yake ya Utafiti wa Wanyamapori Tanzania(TAWIRI)

Kwa namna inavyofanya jitihada za kugundua mbinu mbalimbali za kupambana na kudhibiti wanyamapori wakali na waharibifu.

Pongezi hizo zimetolewa wakati kamati hiyo ikipokea  na kujadili taarifa ya Wizara ya Maliasili na Utalii ya utendaji wa Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori Tanzania (TAWIRI). 

“ tunaona na kuthamini kazi nzuri ya Wizara kupitia TAWIRI kwa kufanya tafiti zilizosaidia kupata njia bora zinazoonesha matokeo chanya katika kudhibiti wanyama wakali na waharibifu” amesema Mwenyekiti wa kamati hiyo Mhe. Timotheo Mnzava

Kwa upande wake Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji ameihakikishia Kamati kuwa , Wizara hiyo itaendelea kuziwezesha taasisi zake ili ziendelee kufanya kazi kwa  ufanisi na kufikia malengo yanayotarajiwa, 

“ Wizara na wataalamu wake wapo kazini kila wakati kuhakikisha changamoto zinazojitokeza zinapatiwa ufumbuzi wa haraka ili kuifanya Sekta ya Maliasili na Utalii kuendelea kuwa na mchango mkubwa katika ustawi wa wananchi na taifa kwa ujumla” amebainisha Dkt. Kijaji

Ikumbukwe mbali na jukumu la Kufanya, Kuratibu na Kusimamia tafiti za wanyamapori hapa nchini, TAWIRI inajukumu la kuishauri serikali juu ya masuala yote ya sayansi ya wanyamapori kwa uhifadhi endelevu, ustawi wa jamii na kukuza utalii.







Mkurugenzi Mtendaji wa BODI ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) , Bw. Asangye Bangu, akizungumza wakati wa Mkutano wa   Maafisa Biashara katika Kikao cha Tatu cha Wizara ya Viwanda na Biashara na Maafisa Biashara, kilichofanyika kwa siku mbili  jijini Dodoma.

Na.Mwandishi Wetu-DODOMA

BODI ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) imesema itaendelea kushirikiana kwa karibu na Sekretarieti za Mikoa na Halmashauri nchini ili kuimarisha utekelezaji wa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala (WRS), kuongeza tija kwa wakulima na kuchangia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Mkurugenzi Mtendaji wa WRRB, Bw. Asangye Bangu, ameyasema hayo leo Agosti 18, 2026, wakati akizungumza na Maafisa Biashara katika Kikao cha Tatu cha Wizara ya Viwanda na Biashara na Maafisa Biashara, kilichofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete, jijini Dodoma.

Bw. Bangu amesema utekelezaji wenye tija wa mfumo huo katika mikoa na halmashauri unahitaji ushiriki wa karibu wa Maafisa Biashara, hususan katika usimamizi wa shughuli zinazohusiana na maghala pamoja na minada ya mazao inayofanyika katika maeneo yao.

Amesema Maafisa Biashara wana nafasi muhimu katika kuhakikisha taarifa sahihi kuhusu mahitaji ya maghala katika maeneo yao zinapatikana, sambamba na kufuatilia hali, matumizi na uhitaji wa maghala katika halmashauri na mikoa ili kuwezesha Mfumo wa Stakabadhi za Ghala kutekelezwa kwa ufanisi.

Kwa upande wake, Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Mahusiano kwa Umma na Mawasiliano wa WRRB, Bw. Dionis Musseru, amesema utoaji wa elimu kwa umma umeendelea kuongeza uelewa na ushiriki wa wadau katika mfumo huo, ambapo hadi sasa mazao 11 yanauzwa kupitia WRS.

 


📌 Umeme wa JNHPP kufika Dodoma kupitia Chalinze

📌 SGR kupata njia yake maalum ya umeme, kuimarisha uhakika wa huduma


Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Felchesmi Mramba, amesema Njia ya Kusafirisha Umeme ya Msongo wa Kilovolti 400 kutoka Chalinze hadi Dodoma imekamilika hatua itakayowezesha umeme unaozalishwa katika Bwawa la Julius Nyerere (JNHPP) kufika Dodoma kupitia Chalinze.

Mramba ameyasema hayo leo, Agosti 18, 2026, wakati akikagua hatua za mwisho za utekelezaji wa Mradi wa Ujenzi wa Njia ya Kusafirisha Umeme ya Chalinze–Dodoma yenye urefu wa kilomita 345, pamoja na upanuzi wa Vituo vya Kupoza na Kusambaza Umeme vya Chalinze mkoani Pwani na Zuzu jijini Dodoma.

Amesema ujenzi wa njia hiyo umefikia asilimia 99, huku upanuzi wa Kituo cha Zuzu ukiwa umefikia asilimia 98 na kwamba wataalamu wamekamilisha maandalizi ya kuanza kuwasha njia hiyo.

“Kituo cha Zuzu kipo tayari katika hatua za mwisho kabisa. Wataalamu wamenieleza waatanza kuwasha kwa majaribio katika kituo. Umeme utaanza kufika Dodoma kutoka Bwawa la Julius Nyerere kupitia Chalinze hadi kufika Dodoma,” amesema Mramba.

Amesema kukamilika kwa njia hiyo ya kV 400 ni hatua muhimu katika kuimarisha mfumo wa usafirishaji wa umeme nchini, kwa kuwa itapokea umeme unaozalishwa katika Bwawa la Julius Nyerere na kuusafirisha kutoka Chalinze hadi Dodoma, ambako utaingizwa kwenye Gridi ya Taifa na kusambazwa kwenda maeneo mbalimbali nchini.

Aidha, Mramba amesema wanufaika wakubwa wa mradi huo ni Reli ya SGR, akifafanua kuwa njia ya umeme inayotumika kwa ajili ya SGR ilikuwa ikitumika pia kwa matumizi ya watumiaji wengine ambapo kukamilika kwa njia hiyo kutawezesha watumiaji wengine kuondolewa kwenye njia inayotumiwa na SGR, hivyo reli hiyo kuwa na njia yake ya umeme kwa matumizi yake.

Aidha, Mramba amesema utatuzi wa changamoto kama iliyotokea hivi karibuni ya kuzimika kwa Gridi ya Taifa ni kukamilika kwa Njia ya Kusafirisha Umeme ya Chalinze hadi Dodoma, ambayo itawezesha kuwepo kwa utulivu na kuimarisha ubora wa umeme katika Gridi ya Taifa kwa kuwepo kwa umeme wa kutosha.

Amesema kwa sasa mradi huo ni miongoni mwa miradi muhimu kwa nchi, ambapo unagharamiwa na Serikali ya Tanzania kwa asilimia 100 kwa takribani Shilingi bilioni 600, ukiwa ni miongoni mwa miradi mikubwa ya kusafirisha umeme inayotekelezwa nchini.

Mramba ameeleza kuwa maeneo yatakayonufaika na njia hiyo ya umeme ni pamoja na mikoa ya Kanda ya Ziwa, ikiwemo Mwanza, Shinyanga, Tabora na Kigoma, pamoja na Singida upande wa magharibi. upande wa kaskazini, mikoa ya Manyara, Arusha na Kilimanjaro itanufaika na umeme utakaosafirishwa kupitia njia hiyo.

Mramba amemshukuru Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwezesha utekelezaji wa mradi huo pamoja na usimamizi wa Waziri wa Nishati, Deogratius Ndejembi akieleza kuwa kukamilika kwake kutaongeza uwezo wa mfumo wa usafirishaji wa umeme nchini na kuimarisha upatikanaji wa huduma ya umeme yenye ubora na uhakika kwa wananchi.















NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

SHIRIKA la Viwango Tanzania (TBS) limeweka Viwango vya Chini vya Ufanisi wa Nishati (MEPS) kwa vifaa vinavyotumia umeme, hatua inayolenga kupunguza matumizi yasiyo ya lazima ya nishati na kuwasaidia wananchi kupata vifaa bora na vyenye ufanisi mkubwa.

 




 Na Mwandishi wetu- IRINGA

Naibu  Waziri  Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Mhe. Ummy Nderiananga amewataka watu wenye ulemavu kutumia mikopo inayotolewa na Serikali kama fursa ya kujikwamua kiuchumi na kubadili maisha yao, badala ya kuichukulia kama msaada au hisani.


Naibu Waziri aliyasema  hayo katika Ofisi za Mkoa wa Iringa, wakati wa ziara yake ya kutoa elimu kwa watu wenye ulemavu kuhusu fursa mbalimbali zinazopatikana kwa lengo la kuwawezesha kiuchumi na kijamii.

Amesemalisema  Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan  imeendelea kuweka mazingira wezeshi kwa watu wenye ulemavu kupata mikopo na fursa nyingine za kiuchumi, huku akibainisha kuwa kiasi kikubwa cha fedha tayari kimetolewa kwa wanufaika nchini.



“Hadi sasa watu wenye ulemavu Nchi nzima  wameshakopa shilingi Bilioni 26.8 huvyo tunapaswa kushukuru na kuipongeza Serikali kwa mikakati mizuri kuhakikisha Kundi hili linafikiwa na sisi kama watu wenye ulemavu tuchangamkie fursa hihi ya mikopo tujiinue kiuchumi na tuwe waaminifu kurejesha ili kuwawezesha na wengine,”Alieleza Mhe. Ummy.

Mhe. Ummy Alieleza kwamba  ongezeko hilo ni ishara kuwa watu wenye ulemavu wameanza kutambua na kutumia fursa zinazotolewa kwa ajili ya kuanzisha na kuendeleza shughuli za kiuchumi, hivyo kuwataka kuendelea kujitokeza na kutumia fursa hizo .

"Mafanikio ya baadhi ya watu wenye ulemavu waliopata mikopo yanapaswa kutumika kama mfano na kuwahamasisha  wengine kuchangamkia fursa hii ya mikopo kwani wapo wenye ulemavu wengi wamenufaika hatimaye kupungua wimbi la utegemezi katika familia hata Taifa," Alisisitiza.


Aidha Waziri Ummy aliitaka  Halmashauri ya Manispaa ya Iringa kujitathmini katika utoaji wa mikopo kwa watu wenye ulemavu akibainisha kuwa kiwango kilichotolewa katika manispaa hiyo

bado ni kidogo ikilinganishwa na mahitaji yaliyopo huku akiwapongeza watu wenye ulemavu wanaofanya shughuli zao kama vile kiwanda cha kufyatua matofali Kata ya Nduli, duka la jumla la mahitaji ya nyumbani, mnufaika wa mikopo aliyenunua bajaji ya baishara na wafanyabiashara wadogo katika Halmashauri ya Manispaa ya Iringa.

“Serikali za mitaa zinapaswa kuhakikisha fursa za mikopo zinawafikia walengwa, huku wakitenga pia maeneo maalumu ambayo watu wenye ulemavu watafanya  shughuli za uzalishaji na biashara biashara zao bila kusumbuliwa,” Alibainisha.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Iringa, Mhe. Benjamini Sitta alisema Serikali imefanya jitihada kubwa kuhakikisha inatatua changamoto ya mikopo kwa wenye ulemavu kutoka utaratibu wa kukopa kwa vikundi wa awali  hadi mtu mmoja mmoja.

Awali akitoa taarifa ya Halmashauri ya Manispaa ya Iringa ya Utoaji wa mikopo kwa vijana, wanawake na wenye ulemavu  kwa kipindi cha mwaka 2024/2025 hadi 2025/2026, Afisa Maendeleo ya Jamii ambaye ni Mratibu wa mikopo Bi. Sunday Mtamakaya alieleza kuwa vikundi 183 vimepatiwa mikopo wakiwemo wanawake, vijana na wenye ulemavu.

“ Halmashauri imefanikiwa kuwawezesha wenye ulemavu mitaji, wana vikundi kuboresha hali za maisha yao na baadhi ya wanavikundi kuwaajiri watu wengine katika biashara zao. Licha ya mafanikio hayo bada ya kurejeshwa utaratibu wa mikopo bado kuna changamoto ya baadhi yao kushindwa kuejesha mikopo hiyo kwa uaminifu,” Alisema Afisa Maendeleo huyo.


Naye  Mnufaika wa mikopo hiyo mwenye ualbino  Bwa. Issa Iddi Sogoi ambaye anamiliki duka la jumla la mahitaji ya nyumbani  katika Halmashauri hiyo alimshukuru Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa namna anavyoonyesha upendo, kujali na kuwaunga mkono watu wenye ulemavu kupitia mikopo hatua inayomsaidia kumudu mahitaji ya familia na kujiongezea kipato ambapo pia ametoa ajira kwa vijana wengine.






NA DENIS CHAMBI, TANGA.


WASHINDI  kupitia maonesho ya  Elimu ujuzi na ubunifu yanayoendelea kufanyika  kitaifa mkoani Tanga  wanatarajiwa kuiwakilisha Tanzania katika maonesho ya kidunia  kwenda kuonesha ujuzi ,ubunifu na maarifa yao.


Hayo yameelezwa na  katibu mtendaji kutoka baraza la Taifa la elimu  ya ufundi na mafunzo ya ufundi stadi (NACTVET) Mwajuma Lingwanda wakati akizungumza na waandishi wa habari katika maonesho hayo ambapo amesema jumla ya washiriki 49  waliopatikana kwenye mchujo uliofanyika katika ngazi ya Kanda watashindanishwa  kwenye vipengele 9 ambapo kila  mshidi atakata tiketi ya kwenda kuiwakilisha Tanzania kimataifa.

"Mashindano haya yalianza katika ngazi ya Kanda ambapo tulikiwa na washiriki  katika maeneo 9 ya ujuzi  na baada ya hapo tumefikia kwenye maonesho ya kitaifa na tuna washiriki 49 kutoka kwenye taasisi mbalimbali waamuzi wako tayari  wale watakaofanikiwa kufaulu na kuwa washindi wa kwanza  watapata nafasi ya kushiriki kwenye mashindano ya kimataifa  mwaka huu"amesema Lingwanda.


Fani hizo zitakazoshindaniwa ni pamoja na mapishi , mekatroniksi, ujenzi, ujuzi wa mitandao,  uchomeleaji wa vyuma , uhandisi, ushonaji wa nguo, na urembo.

Akizungumza Mkurugenzi  mdhibiti ubora kutoka NACTVET Geoffrey Oleke amesema kuwa  ujuzi katika nyanja mbalimbali ni una umuhimu husasani kwa rika la vijana ambao ndio tegemeo na Taifa la kesho hivyo Taifa linapaswa kuwekeza katika elimu ya sayansi.


Amesema mchakato wa kuwapata washiriki wa maonesho hayo ulianza juni 2026 ambapo vyuo vyote vya sayansi vilishiriki katika mchakato katika fani 15 ambapo kati ya hizo  fani 9 zilipata washiriki wengi hivyo kupewa kipaumbele kwa washiriki wa mwaka huu kitaifa ambapo kila fani ina washiriki watano watakaochuana kuonyesha maarifa na ujuzi wao.


"Bila ujuzi kwa Hakika hakuna nchi inaweza ikaendelea kwahiyo na sisi kama nchi tunashiriki kwa lengo la kuhakikisha kwamba tunakuza ujuzi wa vijana wetu katika shule za sekondari na vyuo ili tupate nguvu kazi iliyo imara ambayo itaisaidia nchi yetu katika kuchochea maendeleo yake" amesema  Oleke.


Maonesho hayo ambayo kwa mwaka huu wa 2026 yamebebwa na kauli mbiu isemayo Elimu ujuzi na ubunifu , njia ya kufikia dira 2050 yameanza kufanyika August 16 yakifunguliwa  rasmi na waziri wa elimu Prof. Adolfu Mkenda huku yakitarajiwa kufungwa August 24 na waziri mkuu wa jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt Mwigulu Nchemba




NA DENIS CHAMBI, TANGA.


TAASISI za elimu zilizopo hapa nchini zimetakiwa kuendana na  dira ya Taifa ya 2050  katika kupitia masomo tafiti na ujuzi mbalimbali wanaoutoa kwa wanafunzi  wanaosoma ngazi mbalimbali ili kuendana na maendeleo ya teknolojia..


Wito huo umetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Tanga Balozi Dkt Batilda Buriani wakati alipotembelea na kukagua maandalizi ya maonesho ya wiki ya kitaifa ya Elimu ujuzi na ubunifu yanayoendelea katika viwanja ya shule ya sekondari Usagara ambapo yanayotarajiwa kuzinduliwa rasmi na waziri wa elimu Prof Adolfu Mkenda  17 august 2026.


Dkt.Buriani amesema kuwa Kila taasisi  za elimu Zina wajibu wa kuwaelimisha wananchi juu ya mwelekeo wa kitaifa wa dira ya 2050 ili kutoa ufahamu juu ya malengo ya serikali katika maendeleo  kupitia nyanja mbalimbali ikiwemo za kielimu.


kaimu mkuu wa kitengo Cha mawasiliano na masoko kutoka katika chuo cha maji  kilichopo mkoani Dar es salaam chini ya wizara ya maji Godfrey Kituli wakati akizungumza na Msumba Blog katika maonesho ya Elimu , sayansi na ubunifu yanayoendelea kufanyika kitaifa mkoani Tanga ambapo ameeleza kuwa katika kuunga mkono jitihada za serikali juu ya umuhimu wa utunzaji wa vyanzo vya maji wameweza kupanda miti zaidi ya 1500 katika chuo hicho.


"Kumekuwa na uharibifu wa vyanzo mbalimbali vya maji  kutokana na shughuli za kibinadamu  tunaendelea kufanya tafiti na kutoa elimu kwa jamii ili kuhakikisha vyanzo vya maji  vinalindwa na kutunzwa, tunaiunga mkono moja kwa moja  serikali katika kuhakikisha wananchi wanapata elimu juu ya utunzaji wa mazingira hususani vyanzo vya maji vinavyowazunguka katika maeneo yao". Amesema Kituli.


Maonesho hayo ambayo yanajumuiaha zaidi ya taasisi 300  kwa mwaka 2026 yamebebwa na kauli mbiu isemayo Elimu , ujuzi na ubunifu njia  ya kufikia dira ya 2050 yanatarajiwa kufungwa rasmi august 24 na waziri mkuu wa jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt Mwigulu Nchemba.

Meneja wa Usajili wa Bidhaa na Majengo wa TBS, Bw.Habakuki Kalebo,akiwasilisha mada wakati wa kikao kilichoandaliwa na BRELA cha Maafisa Biashara pamoja na Wakuu wa Idara za Viwanda na Biashara kinachofanyika kwa siku mbili jijini Dodoma.

Na.Mwandishi Wetu-DODOMA 

Shirika la Viwango Tanzania (TBS) limesisitiza umuhimu wa kusajili maeneo yote yanayohusika na uuzaji, usambazaji na uhifadhi wa bidhaa za chakula na vipodozi, likieleza kuwa hatua hiyo ni muhimu katika kuhakikisha wananchi wanapata bidhaa salama na bora, kulinda afya zao.

Meneja wa Usajili wa Bidhaa na Majengo wa TBS, Bw.Habakuki Kalebo, amesema hayo wakati wa kikao kilichoandaliwa na BRELA cha Maafisa Biashara pamoja na Wakuu wa Idara za Viwanda na Biashara, akieleza kuwa TBS inashirikiana na Ofisi ya Rais–TAMISEMI kupitia mamlaka za serikali za mitaa katika kusimamia usajili wa maeneo hayo.

Kalebo amesema usajili huo unalenga kuhakikisha bidhaa zinazouzwa, kusambazwa au kuhifadhiwa ni salama, bora na zimethibitishwa na TBS, huku mazingira yanayotumika kuhifadhi na kuuza bidhaa yamekidhi masharti ya usalama na usafi. Amesema kwa bidhaa za chakula, hatua hiyo inasaidia kuzuia uchafuzi kwa kuhakikisha chakula hakihifadhiwi au kuchanganywa na bidhaa nyingine zinazoweza kuhatarisha ubora wake.

Aidha, amesema usajili huo unasaidia kudhibiti usalama wa vipodozi vinavyoingizwa sokoni, kwa kuhakikisha havina viambata vyenye madhara kwa watumiaji. Ameongeza kuwa ukaguzi katika maeneo hayo pia husaidia kubaini na kuondoa bidhaa zilizomaliza muda wake kabla hazijawafikia wananchi, hivyo kupunguza hatari zinazoweza kujitokeza kutokana na matumizi ya bidhaa zisizofaa.

 "Mfumo wa usajili pia una umuhimu katika ufuatiliaji wa bidhaa sokoni, kwani pale changamoto inapojitokeza, TBS inaweza kubaini bidhaa husika zilipo, kiasi kilichopo na kuchukua hatua za haraka za kuziondoa sokoni. Amesema utaratibu huo unaimarisha udhibiti wa bidhaa na kuongeza uwezo wa Serikali kulinda afya na usalama wa wananchi."amesema Bw.Kalebo 

Amesema ushirikiano kati ya TBS, Maafisa Biashara na Mamlaka za serikali za mitaa ni muhimu katika kuhakikisha wafanyabiashara wanaelewa na kutekeleza matakwa ya Sheria na Viwango vya bidhaa. 

Kalebo amesisitiza kuwa ulinzi wa afya ya wananchi unapaswa kuwa sehemu muhimu ya usimamizi wa biashara, akieleza kuwa mtu mwenye afya njema ana uwezo mkubwa wa kushiriki katika shughuli za uzalishaji na kuchangia uchumi wa taifa.

Amesema matumizi ya bidhaa salama hupunguza hatari za magonjwa na gharama za matibabu, hivyo usajili na udhibiti wa maeneo ya biashara ya chakula na vipodozi ni hatua muhimu katika kulinda afya ya jamii na kuongeza tija ya Taifa.


Katibu Mkuu Ofisi ya Rais – Mipango na Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango, Dkt. Tausi M. Kida, amesema ushirikiano kati ya Serikali, Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) Tanzania na wadau mbalimbali ni muhimu katika kugeuza ubunifu, teknolojia na utafiti kuwa chachu ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.


Dkt. Kida amesema hayo kuelekea Wiki ya Ubunifu Tanzania 2026, inayotarajiwa kufanyika Agosti 31 hadi Septemba 4, 2026 katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere (JNICC), Dar es Salaam.



Amesema jukwaa hilo litasaidia kuunganisha mawazo bunifu, utafiti, teknolojia, sera, mitaji, masoko na uwekezaji, ili kuchochea suluhisho zenye kuongeza tija, kuzalisha ajira na kuboresha maisha ya wananchi.

“Hatuhitaji ubunifu unaobaki katika mawazo au maabara. Tunahitaji kuugeuza kuwa bidhaa, huduma na suluhisho zinazoongeza tija, kuzalisha ajira, kuvutia uwekezaji na kuboresha maisha ya wananchi,” amesema Dkt. Kida.

Aidha, Amesema ushirikiano wa Serikali, sekta binafsi, taasisi za elimu na utafiti, wabunifu, wajasiriamali, wawekezaji na washirika wa maendeleo utakuwa muhimu katika kujenga mazingira yatakayowezesha mawazo bunifu kufikia hatua ya utekelezaji na soko.

Wiki ya Ubunifu Tanzania 2026, yenye kaulimbiu “Kutoka Kwenye Matarajio hadi Mabadiliko; Kutumia Ubunifu katika Kuelekea Tanzania yenye Ustawi wa Pamoja,” itajumuisha mijadala ya kisera, maonesho ya ubunifu, shughuli za vijana na majadiliano ya uwekezaji.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Mhe. Prof. Kitila Alexander Mkumbo anatarajiwa kuzindua Jukwaa hilo, litakalohusisha mjadala wa Mawaziri kuhusu Ubunifu na Utekelezaji, utakaojadili namna ubunifu na teknolojia vinavyoweza kuimarishwa katika mipango na utekelezaji wa maendeleo ya Taifa.

Unaweza kujisajili sasa kupitia https://summitpoint.co.tz/events/iwtz-2026