Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhe. Wanu Hafidh Ameir, amemtaka Mkandarasi wa COMFIX & ENGINEERING kuongeza kasi ya ujenzi wa miundombinu ya Mradi wa Kujenga Ujuzi na Ushirikiano Afika Mashariki (EASTRIP ) katika Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT) Kampasi ya Mwanza, ili ikamilike kwa wakati kulingana na maktaba.

Naibu Waziri huyo, ametoa maagizo hayo jijini Mwanza wakati akikagua maendeleo ya utekelezaji wa mradi huo. Pia amewataka wazabuni wote kuhakikisha vifaa na mitambo vinawasili na kufungwa kwa wakati ili kuwezesha utoaji wa mafunzo kwa wakati.

Mhe. Wanu Ameir amesema ucheleweshaji wa ujenzi unaweza kuathiri malengo ya Serikali ya kuhakikisha vijana wanapata ujuzi na umahiri unaohitajika katika soko la ajira la ndani na kimataifa, kama alivyoelekeza Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mhe. Ameir amewahakikishia wananchi na uongozi wa DIT kuwa Serikali itaendelea kuimarisha uwezo wa kampasi hiyo, ikiwemo kuongeza udahili wa wanafunzi kutoka 358 wa sasa hadi 2,000

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Daniel Mushi, amesema kuwa katika Kampasi ya DIT Mwanza kinajengwa Kituo cha Kikanda cha Umahiri cha uchakataji na utengenezaji wa bidhaa za Ngozi ambacho kinatekelezwa kupitia Mradi wa EASTRIP. Amesema kuwa ujenzi huo unahusisha majengo matano ambayo ni jengo la kufundishia, jengo la taaluma, hosteli mbili na karakana ya kisasa kwa ajili ya mafunzo ya utengenezaji wa bidhaa za ngozi.

Prof. Mushi ameongeza kuwa ujenzi wa majengo hayo unatekelezwa na Serikali kwa kushirikiana na Benki ya Dunia ambayo imetoa mkopo wa riba nafuu kufanikisha mradi huo. Ambapo gharama za utekelezaji wa mradi DIT Mwanza ni shilingi bilioni 37.

Mkurugenzi wa Taasisi ya Teknolojia ya Dar Es Salaam (DIT) Kampasi ya MWANZA Dkt. John Msumba amesema kuwa Kampasi hiyo imefufua Sekta ambayo ilikuwa imekufa nchini kutokana na kukosekana Kwa wataalamu na kwamba Viwanda Kwa sasa vinapata wataalamu tofauti na awali ambapo walikuwa wakilazimika kuwatoa nje ya nchi.

 

Na Mwandishi Wetu, Handeni TC

HALMASHAURI ya Jiji la Tanga imefanya ziara ya mafunzo katika Halmashauri ya Mji Handeni kwa lengo la kujifunza utekelezaji wa Mradi wa BOOST unaolenga kuboresha miundombinu ya elimu ya msingi na kupunguza msongamano wa wanafunzi darasani.

Katika ziara hiyo, Kamati ya Mradi wa BOOST kutoka Jiji la Tanga ilitembelea miradi miwili mikubwa ya ujenzi wa shule za msingi inayotekelezwa na Halmashauri ya Mji Handeni.

 Miradi hiyo ni ujenzi wa Shule ya Msingi Kwediziwa uliogharimu Sh milioni 540.3, ambapo madarasa 16 pamoja na matundu 28 ya vyoo yalijengwa, na Shule ya Msingi Mdoe, ambako Sh. milioni 543 zimetumika kujenga madarasa 14 na matundu 28 ya vyoo.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Ofisa Elimu wa Halmashauri ya Mji Handeni na Mratibu wa Mradi wa BOOST, Elizabeth Mwakalonge, amesema utekelezaji wa mradi huo umeleta mafanikio makubwa ikiwamo kupunguza msongamano wa wanafunzi darasani, kupunguza umbali wanaotembea wanafunzi kufuata shule pamoja na kuboresha mazingira ya ufundishaji na ujifunzaji.

Kwa upande wake, Katibu Msaidizi wa Tume ya Utumishi wa Walimu Jiji la Tanga na Mjumbe wa Kamati ya Mradi wa BOOST, Kurwa Mhoja, amesema lengo la ziara hiyo ni kujifunza uzoefu wa utekelezaji wa mradi wa BOOST katika Halmashauri ya Mji Handeni pamoja na kubadilishana uzoefu na maafisa elimu ili kuboresha utekelezaji wa miradi hiyo katika Jiji la Tanga.

Ameongeza kuwa ziara hiyo ni sehemu ya jitihada za Serikali katika kuimarisha sekta ya elimu kwa kuhakikisha miradi ya maendeleo inatekelezwa kwa ufanisi na kuleta matokeo chanya kwa wanafunzi na jamii kwa ujumla.

 


Na Munir Shemweta, WANMM MOROGORO

Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo amewaasa wahitimu wa Chuo cha Ardhi Morogoro (ARIMO) kujiepusha na matendo maovu na elimu na maarifa waliyopata yawe tunu na faida kwa Taifa.

Mhe. Dkt Akwilapo ametoa wito huo tarehe 12 Desemba 2025 wakati wa mahafali ya 44 ya Chuo cha Ardhi Morogoro (ARIMO) yaliyofanyika mkoani Morogoro ambapo jumla ya wahitimu 450 wa fani za Jiomatikia (Upimaji Ardhi), Upangaji Miji na Vijiji na Mifumo ya Taarifa za Kijiografia (GIS) walitunukiwa Astashada na Stashahada katika fani hizo.

Mhe. Dkt Akwilapo amewataka wahitimu hao kukumbuka kuwa utii, nidhamu na tabia njema ni silaha itakayowafanya wapendwe mahali popote.

‘’Tukiwa hapa Morogoro tunakumbuka maneno yaliyoimbwa na mwanamuziki wa hapa hayati Mbaraka Mwinshehe na bendi yake ya Okestra Volcano; alisema “Heshima Kijana tanguliza kwanza mbele, ujeuri mbaya; uzuri si hoja tabia njema ni silaha utapendwa popote” mwisho wa kunukuu, alisema Mhe. Dkt Akwilapo.

Amewataka vijana kutodanganyika na maneno ya eti kuna watu wanaitwa Gen Z ambapo alieleza kuwa, hizo ni propaganda za kujenga hofu na kufifisha juhudi za nchi maskini kujitafutia maendeleo.

“Msidanganywe kuwa eti nyie ni kizazi cha vijana wasio na nidhamu, wapenda fujo, wasiosikiliza wazee wao, viongozi wao, chenye kujiamulia mambo yao bila kufuata sheria, taratibu, miongozo na tamaduni zetu; na mambo mengine ya hovyo’’ amesisitiza Mhe. Dkt Akwilapo.

Kwa mujibu wa Waziri huyo wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, inasikitisha na kushangaza kuona vijana wa Kitanzania wanasikiliza maelekezo ya watu ambao hawaishi Tanzania na wala hawajawahi kuwaona na kupuuza  maelekezo ya Viongozi wao na hata wazazi wao ambao wamewalea mpaka hapo walipoifikia.

Amesema, kuhitimu masomo kunatakiwa kuendane na uzalendo waliojengewa wa kuipenda Tanzania na kusisitiza kuwa waithamini nchi yao.

Mhe. Dkt Akwilapo amewataka kutumia utaalamu walioupata kwa weledi, uadilifu na kufuata sheria, kanuni, taratibu na miongozo na kuepuka vitendo vinavyoenda kuhatarisha amani.

Vile vile amewataka kuendelea kujifunza kwani elimu ni bahari, haina mwisho na kuwataka wanaobaki chuoni kuongeza bidii katika masomo, nidhamu na kutunza amani na umoja kwani kesho yao inajengwa na maamuzi ya leo.

Kwa upande wake Mkuu wa wilaya ya Morogoro, Bw. Musa Ramadhani Kilakala akimuwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Bw. Adam Malima amesema, migogoro ya ardhi imepungua mkoani humo hasa pale wizara ya ardhi ilipoanzisha Kliniki za Ardhi ambazo amezieleza zimesaidia kwa kiasi kikubwa kuwafikia wananchi katika maeneo yao.

Akitoa taarifa kwa Mgeni Rasmi, Mkuu wa Chuo cha Ardhi Morogoro (ARIMO) Charles Saguda amesema chuo hicho kina Mpango Kabambe wa Miaka 20 (2023-2043) unaolenga kuboresha mazingira ya kujifunza na kujifunzia na utendaji wa chuo katika kuwaandaa wataalamu wa sekta ya ardhi.

“Mpango kabambe huu unalenga kuongeza udahili wa wana chuo kutoka 660 hadi 5000, kuongeza watumishi kutoka 58 hadi 310 kuongeza program za mafunzo ya wanafunzi kutoka 2 hadi 7 pamoja na kujenga kampasi mpya katika eneo Mlima Kola mkoani Morogoro’’. Amesema Bw. Saguda




Na Munir Shemweta, WANMM MOROGORO

 

Mkuu wa mkoa wa Morogoro Bw. Adam Malima ameipongeza Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa kuweka kumbukumbu za ardhi vizuri jambo alilolieleza kuwa linasaidia katika utatuzi wa migogoro ya ardhi.

 

‘’Mhe Waziri kwa kweli nitoe pongezi kwa wizara yako kwa kuwa na kumbukumbu nzuri za wamiliki wa ardhi jambo hili limetusaidia kama mkoa wa morogoro kutatua migogoro ya ardhi pale inapojitokeza’’ amesema Bw. Malima

 

Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi moja ya vipaumbele vyake ni katika mwaka wa fedha 2025/2026 ni kuongeza kasi ya upangaji, upimaji, umilikishaji na usajili wa ardhi mijini, vijijini na katika maeneo ya kimkakati.

 

Bw. Malima amesema hayo tarehe 12 Desemba 2025 ofisini kwake alipokutana na Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo aliyekuwa mkoani humo kwa ajili ya kuhudhuria mahafali ya 44 ya Chuo cha Ardhi Morogoro (ARIMO).

 

Amesema, migogoro ya ardhi katika mkoa wake wa Morogoro imepungua kwa kiasi kikubwa kutokana na juhudi kubwa za wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi kupitia ofisi ya Kamishna wa Ardhi Msaidizi mkoa ambapo imefanya kazi kubwa ya kufikia wananchi kupitia Kliniki ya Ardhi.

 

Kwa upande wake Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo alimueleza mkuu wa mkoa wa Morogoro kuwa, wizara yake kwa sasa inafanya juhudi kubwa kuhakikisha migogoro ya ardhi iliyopo inatatuliwa na hakuna migogoro mipya inayozalishwa kwenye maeneo mbalimbali nchini.

 

‘’Nikuhakikishe RC sisi ndani ya wizara tumejiwekea mikakati ya kuhakikisha migogoro iliyopo tunaimaliza lakini pia hakuna migogoro mipya inayozalishwa’’ amesema Mhe. Dkt Akwilapo.

 

Aidha, Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi amezihimiza taasisi za umma kuhakikisha zinalinda maeneo yao ili kuepuka uvamizi alioueleza kuwa ndiyo unaochangia kwa kikubwa migogoro ya ardhi katika maeneo ya umma.

 


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete amesema Wizara hiyo imefanya maboresho mbalimbali ya mifumo yake ikiwemo mfumo wa e- mrejesho, ili kutoa fursa zaidi kwa wananchi wa pembezoni kutoa maoni, malalamiko na pongezi kuhusu huduma zinazotolewa na serikali na Taasisi zake.

Mhe. Ridhiwani amebainisha hayo wakati akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dar Es Salaam, akisema mfumo huo unapatikana kwenye simu za mkononi kupitia nambari *152*00#, ukiwa na module ya sema na Kiongozi, sehemu inayomruhusu mwananchi kutoa maoni kwa Waziri, Mkuu wa Mkoa ama Kiongozi mwingine, akisema mfumo huo utakusanya maoni na kisha kuchakatwa na kufanyiwa kazi.

"Mfumo huu wa e- mrejesho ni kiunganishi cha moja kwa moja cha mwananchi na Kiongozi na hii itatusaidia pale tunapojadili namna ya kuboresha mifumo ya utumishi wa umma na ni mfumo wa kweli huu, hata kama kuna Kiongozi hatojibu sisi tutasimamia kuhakikisha majibu yanapatikana." Amesema Mhe. Ridhiwani.

Aidha Mhe. Ridhiwani amehimiza wananchi kuutumia mfumo huo katika kutoa maoni yao, akisisitiza kuwa maboresho hayo yanaenda sambamba na utengenezaji wa Aplikesheni itakayowezesha wananchi kutoa mrejesho wa haraka na wa uwazi ili kuimarisha uwajibikaji wa watumishi wa serikali.

 


✅️ _Akemea Jasi Kuuzwa na Kununuliwa Chini ya Bei Elekezi_

✅️ _Aingilia Kati Kero kwa Wachimbaji Wadogo, Wadau Kukutana Dodoma Kutafuta Suluhu ya Kudumu_

✅️ _Awahimiza Vijana Kuchangamkia Fursa Zilizopo Sekta ya Madini_ 

✅️ _Mining For A Brighter Tomorrow-MBT Kimbilio Jipya kwa Vijana na Wanawake_

Naibu Waziri wa Madini, Mhe. Dkt. Steven Kiruswa amesema kuwa Serikali kupitia Wizara ya Madini inatarajia kukutana jijini Dodoma katika siku za karibuni na wadau wa madini ya jasi (gypsum) wakiwemo wachimbaji wadogo, wasafirishaji, wamiliki wa viwanda vya saruji, Uongozi wa Wilaya na Halmashauri ya Wilaya ya Same ili kujadili na kutatua changamoto zinazoathiri shughuli za uchimbaji na biashara ya madini hayo ambazo zimechangia kusuasua kwa maendeleo ya wananchi wanaotegemea sekta hiyo.

Alitoa kauli hiyo jana, Desemba 12, 2025, wakati wa ziara yake ya kukagua shughuli za uchimbaji katika Kata za Makanye na Ruvu Jeungeni, wilayani Same, mkoani Kilimanjaro, ambako pia alizungumza na wachimbaji wadogo wa madini ya jasi.

Dkt. Kiruswa alisisitiza marufuku ya kununua madini ya jasi chini ya bei elekezi iliyotolewa na Tume ya Madini, akiwataka wote kuheshimu miongozo hiyo ili kulinda maslahi ya wachimbaji.

Kwa upande wa mazingira, alitoa wito kwa wachimbaji kuhakikisha utunzaji wa mazingira, kufukia mashimo mara baada ya shughuli za uchimbaji kukamilika, pamoja na kupongeza juhudi za uanzishwaji wa Mfuko Maalum wa kusaidia kurejesha mazingira mara baada ya kutamatika kwa shughuli za uchimbaji, ambao umeelezwa kuwa chachu ya kuimarisha uwajibikaji na uendelevu wa shughuli za madini wilayani humo.

Katika hatua nyingine, Dkt. Kiruswa aliendelea kusisitiza umuhimu wa mafunzo ya MBT kwa vijana na wanawake, utoaji wa leseni, pamoja na upatikanaji wa vifaa vya kisasa ili kuongeza ufanisi na usalama katika uchimbaji mdogo wa madini ya jasi na kuwahimiza vijana kuchangamkia fursa zilizopo katika mnyororo mzima wa Sekta ya Madini. 

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Same, Kasilda Mgeni alieleza kuwa uchimbaji wa jasi ni uti wa mgongo wa maendeleo ya wananchi na Halmashauri ya Wilaya ya Same, na kwamba kuibuka kwa mgogoro huo baina ya wachimbaji wadogo na wamiliki wa viwanda vya saruji unakwamisga maendeleo katika wilaya hiyo na kwamba Serikali imejipanga kuhakikisha sekta hiyo inakuwa na tija kwa wadau wote.

Naye, Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Kilimanjaro Mhandisi Abel Madaha alisema kuwa Tume ya Madini kwa kushirikiana na taasisi nyingine za Serikali pamoja na wadau wa madini wamekuwa wakikaa mara kwa mara kwa manufaa ya wachimbaji na watumiaji wa madini husika ikiwemo kutafuta ufumbuzi wa changamoto zinazowakumbuka wachimbaji kuanzia migodini hadi kwa watumiaji wa mwisho.











Shirika la Masoko ya Kariakoo limeanza rasmi maandalizi ya Mpango Mkakati mpya wa miaka mitano 2026-2031, hatua inayolenga kulifanya soko hilo la kimataifa kutoa huduma bora, kwa wakati na kuzingatia mabadiliko ya teknolojia yanayojitokeza duniani.

Meneja Mkuu wa Shirika la Masoko ya Kariakoo, CPA. Ashiraf Abdulkarim,akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya uchambuzi na uandaaji wa mpango Mkakati mpya wa miaka mitano 2026-2031 wa Shirika la Masoko ya Kariakoo.

....

Shirika la Masoko ya Kariakoo limeanza rasmi maandalizi ya Mpango Mkakati mpya wa miaka mitano 2026-2031, hatua inayolenga kulifanya soko hilo la kimataifa kutoa huduma bora, kwa wakati na kuzingatia mabadiliko ya teknolojia yanayojitokeza duniani.

Mpango huo unakuja baada ya baada ya mpango wa 2021-2025 kumaliza muda wake wa utekelezaji kwa mafanikio makubwa.

Akizungumza wakati wa ufunguzi mafunzo ya uchambuzi na uandaaji wa mpango huo, Meneja Mkuu wa Shirika la Masoko ya Kariakoo, CPA. Ashiraf Abdulkarim , amesema maandalizi ya mpango huo umeshirikisha wadau ikiwemo Ofisi Waziri Mkuu TAMISEMI, Wafanyabiashara wa Kariakoo, Wapangaji na wadau wengine ili kuwa na mpango mkakati bora, uliochukua mawazo ya wengi na unaojibu matamanio ya kila mmoja na hivyo kuwa rahisi katika utekelezaji wake.

CPA Abdulkarim ameongeza kuwa katika kuandaa mpango huo, Shirika litazingatia nyaraka mbalimbali ikiwemo Dira ya Maendeleo ya Taifa 2025-2050, hotuba ya Rais wakati akifungua Bunge la 13, Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa, Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2025-2030 pamoja na Sheria na miongozo mbalimbali iliyoanzisha Shirika la Kariakoo.

“Mafunzo haya yatafanyika kwa siku tano na yatakuwa endelevu. Lengo ni kuwa na mpango mkakati bora, unaotekelezeka na unaoweza kupimika kila mwaka kwa kipindi cha miaka mitano ambao utalifanya soko la kariakoo kuwa kinara na linalotoa huduma anuai na sio mazao pekee" amebainisha CPA Abdulkarim.

Amesema mpango huo ukikamilika utalibadilisha soko la Kariakoo kuwa kituo cha kisasa cha biashara, chenye mifumo ya kisasa ya uendeshaji na utoaji huduma.

CPA. Abdulkarim amesema kuwa Kariakoo mpya itakuwa na miundombinu ya kisasa kuanzia maeneo ya maegesho ya magari, mifumo ya kuzima moto, maeneo ya dharura, hewa ya kutosha na mifumo ya kiteknolojia ya uendeshaji. Tunataka kuwahudumia Watanzania katika mazingira bora na ya kisasa.

Kwa upande wake, Meneja wa Mipango na Biashara wa Shirika la Kariakoo, Bi. Mwinga Luhoyo amesema maandalizi ya mpango huo yanahusisha tathmini ya mpango uliopita wa 2021–2025 ili kubaini mafanikio, changamoto na maeneo yanayohitaji maboresho.

Meneja huyo ameongeza kuwa lengo ni kuhakikisha mpango huo unaendana na mikakati ya kitaifa na huku ukilenga kuongeza tija, kuimarisha biashara, na kukuza mchango wa Kariakoo katika uchumi wa taifa.