Na, Ruth Kyelula, Manyara RS.
Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe Queen Sendiga, amefanya ziara ya ukaguzi wa muradi, kusikiliza kero za wananchi na kuzitatua, ambapo ameanza ziara yake hiyo ya Kata kwa Kata, yenye kauli mbiu "tunavua buti ama hatuvui, tukutane site".
Ziara hiyo imefanyika Desemba 04, 2025, katika Halmashauri ya Wilaya ya Hanang', ambapo ameambatana na Wakuu wa Taasisi zote za Umma na binafsi za Mkoa wa Manyara.
Katika ziara yake hiyo ya siku tatu, amefanya ukaguzi wa mradi wa jengo la Utawala la Halmashauri ya Wilaya ya Hanang',ameweka jiwe la msingi shule ya awali na msingi Semonyan iliyopo Kata ya Mogitu, amekagua ujenzi wa mradi wa shule mpya ya Sekondari Waret, amekabidhi nyumba kwa mwathirika wa maporomoko ya tope la Desemba 03,2023, amefanya mkutano wa hadhara Waret, amekagua madarasa mawili shule ya msingi Gisamjanga, amekagua ujenzi wa mradi wa bweni la wavulana shule ya sekondari Mwahu,na amefanya mkutano wa hadhara kijiji cha Gehandu.
Aidha RC Sendiga, katika ziara yake hiyo ya ukaguzi wa miradi na kusikiliza kero, ametoa wito kwa wananchi kupanda miti ya kivuli na miti ya matunda maeneo yote ya miradi na miradi ya ujenzi wa shule, ikamilike kwa wakati ili mwezi Januari watoto waingie shule.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi akikabidhi Tuzo maalumu Meneja Mkazi wa Kampuni ya Emirates Leisure Retail Zanzibar, Paul Atallah (wa pili kushoto), kwa niaba ya kampuni hiyo na Qatar Foundation kwa kutambua mchango wao mkubwa katika kusaidia watu wenye uhitaji.
...............................
Na Dotto Mwaibale, Zanzibar
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt.
Hussein Ali Mwinyi ametoa Tuzo maalum kwa Kampuni ya Emirates Leisure Retail
Zanzibar na Qatar Foundation kwa kutambua mchango wao mkubwa katika kusaidia
watu wenye uhitaji.
Dkt. Mwinyi alitoa tuzo hizo katika kilele cha Maadhimisho
ya Siku ya Watu Wenye Ulemavu yaliyofanyika Desemba 4, 2025 kwenye Ukumbi wa
Dr. Shein – Tunguu, Chuo Kikuu cha SUZA, Mkoa wa Kusini Unguja tukio
lililohudhuriwa na viongozi wa Serikali, wadau wa maendeleo, mashirika ya
kijamii, na wananchi kutoka sehemu mbalimbali za Zanzibar.
Akihutubia katika maadhimisho hayo Rais Mwinyi aliwataka
wadau kuendelea kuunga mkono jitihada za Serikali za kuwawezesha watu wenye
ulemavu na alisisitiza kuwa maendeleo ya kweli ni yale yanayowahusisha watu
wote bila kuacha kundi lolote nyuma.
Aidha, Dkt. Mwinyi alitumia nafasi hiyo kuwapongeza wadau na
wahisani kwa kujitolea kwao kuchangia maendeleo ya jamii zenye watu wenye
ulemavu na kueleza kuwa Serikali itayafanyia kazi maoni na ushauri uliotolewa
ili kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata fursa kamili za kutimiza malengo
yao.
Kwa upande wake Meneja Mkazi wa Kampuni ya Emirates Leisure Retail Zanzibar, Paul Atallah, alilishukuru Baraza la Watu Wenye Ulemavu Zanzibar kwa kutambua mchango wa Emirates Leisure Retail na kueleza kwamba kampuni hiyo itaendelea kuwa mshirika wa karibu wa Serikali na jamii katika kuleta maendeleo chanya kwa watu wenye ulemavu.
Utambuzi wa Wadau Maalumu
Katibu Mtendaji wa Baraza la Watu Wenye Ulemavu Zanzibar,
Ussi Khamis Debe, akizungumza kwenye maadhimisho hayo alitoa shukrani kwa wadau wote wanaounga mkono
juhudi za Serikali katika kusaidia watu wenye ulemavu.
Aidha, kwa nafasi ya kipekee alimshukuru Afisa Utawala Msaidizi wa Kampuni ya Emirates
Leisure Retail Zanzibar, Ramadhan Hussein Layya (Maarufu Msokolo),kwa
mchango wake mkubwa na wa muda mrefu, hususan katika kusaidia watu wenye
ulemavu wa ngozi kupitia misaada, ushiriki, na michango inayobadilisha maisha
ya wanufaika.
Kaulimbiu ya Maadhimisho:
"Uwezeshaji na Ushirikishwaji wa Watu Wenye Ulemavu kwa
Maendeleo Jumuishi."
Misaada Iliyotolewa katika maadhimisho hayo kwa ajili ya
makundi mbalimbali ya wahitaji ni
Vyerehani kwa ajili ya kujiajiri, kofia maalumu (round hats)
kwa ulinzi wa ngozi, miwani ya kinga na vifaa vya kurekebisha uoni, baiskeli za
mwendo kwa watu wenye ulemavu wa viungo, fedha za mikopo kwa kuanzisha au
kuendeleza biashara.
Vifaa vingine vilivyotolewa ni vya kuongeza uwezo wa kujitegemea
mashine za kusaga nafaka.
Misaada hiyo imeleta furaha, matumaini, na thamani kubwa kwa
wanufaika na familia zao, ambayo inakwenda kuwasaidia kutimiza ndoto zao na
kuimarisha ustawi wa familia zenye watu wenye uhitaji maalumu.
Kauli ya Emirates Leisure Retail Zanzibar na Qatar
Foundation:
Uongozi wa kampuni hizo umeeleza dhamira zao za kuendelea
kushirikiana na Serikali na wadau wengine kuhakikisha watu wenye ulemavu
Zanzibar wanapata fursa sawa za ustawi na maendeleo, na kuendelea kuwekeza katika
miradi ya kijamii inayobadilisha maisha ya watu wenye uhitaji maalumu.
Viongozi wa Kampuni hizo na wadau mbalimbali wakiwa kwenye maadhimisho hayo.
MAMLAKA ya Mapato tanzania (TRA), imeibuka Mshindi wa kwanza wa jumla katika tuzo ya Uandaaji wa Hesabu za Kifedha zinazozingatia viwango vya Kimataifa vya Uhasibu katika Sekta ya Umma (IPSAS), zinazotolewa na Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu (NBAA).
Pia imeibuka mshindi wa kwanza katika tuzo ya kipengele cha Taasisi za Serikali (Government Agency Categories).
Akizungumza jana jijini Dar es Salaam katika hafla ya kukabidhi tuzo hizo, Naibu Waziri wa Fedha Laurent Luswetula, alizipongeza taasisi zilizoibuka na ushindi, huku akisema wizara hiyo itaendelea kutoa ushirikiano kwa NBAA, ili kuendelea kuzalisha wahasibu na wakaguzi bora.
Pia alisema serikali itahakikisha NBAA inasimama imara ili iendelee kuzalisha watendaji bora kwa maslahi mapana ya taifa.
"Wizara ya fedha itaendelea kuhakikisha inatoa ushirikiano kwa NBAA ili kuzalisha wahasibu na wakaguzi bora kwa mslahi mapana ya taifa letu."alisema
Vilevile Naibu Waziri huyo alipongeza NBAA kwa kuendelea kupanua wigo wa kuongeza washiriki kila mwaka.
Naye Naibu Kamishina Mkuu wa TRA Mcha Hassan Mcha lisema, tuzo waliyopata ina umuhimu mkubwa, kwani inachangia kuonesha utendaji wao unakubalika Kimataifa.
Pia alisema tuzo hiyo inaonesha umahiri na ubunifu uliyopo kwa watumishi wa mamlaka hiyo.
"Tuzo hii ina umuhimu sana kwetu, inachangia kuonesha utendaji wetu unakubalika Kimataifa na ina waonesha Walipa Kodi kwamba kila shilingi inayokusanywa inafika katika mfuko Mkuu wa Serikali."alisema
Vilevile Mcha aliwashukuru Walipa Kodi kwa kuendelea kulipa kwasababu TRA imeendelea kuvuka malengo ya ukusanyaji mapato kila mwaka.
Kwamujibu wa Mwenyekiti wa Bodi ya NBAA Profesa Slyivia Temu, katika hafla hiyo jumla ya taasisi 86 za Umma na binafsi zimeshiriki katika kujipima ubora wa kuwasilisha taarifa za fedha kwa mwaka 2024.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa NBAA Pius Maneno, lengo la tuzo hizo ni kuhakikisha taarifa za hesabu zinazotolewa zinakuwa na uwazi na uwajibikaji.
Alifafanua kuwa, tuzo hizo ni taarifa za hesabu za kuanzia Januari mwaka 2024 hadi Desemba, ambazo zimezalishwa kwa kufuata hesabu za Kimataifa na zilizopata hati safi.

Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese,akizungumza wakati akifungua Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Mji Handeni lililofanyika katika ukumbi wa Halmashauri.
Na Mwandishi Wetu, Handeni TC
Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese, ametoa wito kwa Madiwani wa Halmashauri ya Mji Handeni kushirikiana na Ofisi ya Mkurugenzi katika kubuni vyanzo vipya vya mapato, sambamba na kuimarisha umoja, amani na uzalendo katika maeneo yao ya utawala.
Wito huo umetolewa katika ufunguzi wa Baraza la Madiwani lililofanyika katika ukumbi wa Halmashauri, muda mfupi baada ya madiwani hao kuapishwa rasmi kuanza kutekeleza majukumu yao.
Akizungumza wakati wa kikao hicho, Mhe. Nyamwese amewataka madiwani kuhakikisha wanakuwa chachu ya amani na utulivu, akisisitiza kuwa misingi hiyo ni nguzo muhimu kwa ustawi wa jamii na utekelezaji wa shughuli za maendeleo.
Amebainisha kuwa madiwani wana wajibu mkubwa wa kushirikiana kikamilifu na Mkurugenzi wa Halmashauri katika kubuni vyanzo vipya na endelevu vya mapato vitakavyoongeza uwezo wa Serikali ya Mtaa kusimamia na kutekeleza miradi ya wananchi.
Aidha, ameeleza kuwa kuimarisha ukusanyaji mapato na kusimamia miradi ya kimkakati kutasaidia kupunguza utegemezi na kuongeza kasi ya maendeleo ya Halmashauri.
“Madiwani mna wajibu wa kuhakikisha ushirikiano baina ya watendaji na wananchi unaongezeka ili kufanikisha malengo ya pamoja ya maendeleo,” amesisitiza.


















