Na OWM - TAMISEMI, Colombia

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu -TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, ameongoza ujumbe wa Tanzania katika Mkutano wa Pili wa Kimataifa wa wa nchi zinazoshughulika  na masuala Kilimo, Ardhi na Maendeleo vijijini,  ulioanza  Februari 24, 2026 nchini Colombia kwenye jiji la Cartegina.

Prof. Shemdoe amemuwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika mkutano huo, baada ya Mhe. Rais kupokea mwaliko wa kuudhuria mkutano huo kutoka kwa Rais Gustavo Petro Urrego wa Colombia. 

Lengo kuu la mkutano huo uliohudhuriwa na nchi zaidi 100 duniani, ni kutoka na mwafaka wa namna gani matumizi bora ya ardhi katika kilimo yanaweza kupunguza migogoro ya ardhi na kuharakisha maendeleo vijijini.

Aidha nchi hizo zaidi ya 100 zilizoshiriki mkutano huo, ambazo zinashughulika na masuala ya Kilimo, Ardhi na Maendeleo ya Vijijini, zimepata fursa ya kubadilishana uzoefu katika masuala ya kilimo, Ardhi na Maendeleo Vijijini pamoja na matumizi ya teknolojia katika shughuli hizo, ambapo wananchi katika mataifa hayo watanufaika

Katika Mkutano huo wa siku tano unaotarajiwa kufikia tamati Februari 28, 2026 Prof. Shemdoe ameambatana na Naibu Waziri wa Kilimo Mhe. David Silinde, wataalam kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu TAMISEMI na  Wizara ya Kilimo, lengo likiwa ni kutimiza ndoto za  Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan za kuleta mapinduzi ya kilimo nchini ili kuwanufaisha watanzania na kuwapatia tabasamu la kudumu.







.


 TUME ya Kuchunguza Matukio ya Uvunjifu wa Amani yaliyojitokeza Wakati na Baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, Leo Februari 24 imekutana na aliyewahi kuwa mkuu wa Wilaya ya Hai, Lengai Ole Sabaya.


Mahojiano hayo ya Tume na Sabaya yamefanyika katika Ofisi za Tume hiyo zilizopo Benki Kuu ya Tanzania (BoT) mkoani hapa, ikiwa ni sehemu ya juhudi za Tume kukusanya taarifa, maoni na ushauri kutoka kwa watu mbalimbali wakiwemo viongozi wa sasa, wastaafu.

Katika mkutano huo wa Tume na Sabaya yamejadiliwa kwa kina namna matukio ya uvunjifu wa amani yalivyoanza, athari zake kwa wananchi, mali zao na miundombinu, pamoja na ushauri na mapendekezo ya namna ya kudhibiti na kuzuia matukio kama hayo yasijirudie siku zijazo.

Hivi karibuni Mamlaka ya Uteuzi imeiongezea Tume muda wa siku arobaini na mbili (42) kuanzia tarehe 20 Februari, 2026 ili Tume iweze kukamilisha uchunguzi wa matukio ya uvunjifu wa amani ya wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa tarehe 29 Oktoba, 2025 na kuitaka ikamilishe kazi na kuwasilisha Taarifa yake kabla au ifikapo tarehe 3 Aprili, 2026.

Kwa sasa Tume inaendelea na mahojiano na waathirika wa Matukio hayo kwa ajili ya hatua zaidi kama Taifa ili Matukio kama hayo yasijirudie tena.




 Ikiwa ni majira ya Masika na kiubaridi, Bustani ya Eden ya Ngorongoro ikizungukwa na kingo zenye urefu wa Mita 610  huku wanyama na ndege wakichagiza kwa sauti murua zinazoashiria kuwa Ngorongoro ni mwamba wa miamba usiotikisika  na kusheheni msingi imara wa vivutio vya asili, urithi wa utamanuni na maajabu saba katika eneo moja.

Miamba inayounda Bodi ya Wakurugenzi ikiongozwa na makamu mwenyekiti  Dkt Harrieth Mtae inatembelea hifadhi ya Ngorongoro kuanzia ofisi za makao makuu hadi Kreta ya Ngorongoro na kujionea Eden hiyo ikiwa imesheheni kila aina ya ufahari unaoweza kuelezeka  kidunia.

Bodi hii ni sawa na miamba ndani ya Mwamba kwani imejaa wabobezi katika masuala  mengi ikiwemo ulinzi,uhifadhi, uchumi, ikolojia, maendeleo ya jamii, ukaguzi, sheria, utawala na diplomasia

Kubwa wanalilosisitiza kwa menejimenti  “mnafanya kazi nzuri endeleeni kuchapa kazi na tangazeni kitaifa na kimataifa fahari ya Ngorongoro ambayo ni kivutio bora  cha Utalii Afrika mwaka 2025.




 Serikali kupitia Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) imetia saini mkataba wa uwekezaji katika sekta ya madini kwa ajili ya kuendeleza leseni ya uchimbaji wa dhahabu katika eneo la Kigosi, mkoani Geita.


Hatua hiyo inaelezwa kuwa chachu mpya ya kukuza uchumi wa eneo hilo na taifa kwa ujumla.

Hafla ya utiaji saini imefanyika Februari 24, wilayani Bukombe mbele ya Naibu Waziri wa Madini, Steven Kiruswa, aliyekuwa mgeni rasmi.

Mkataba huo umehusisha pande mbili ambazo ni STAMICO na kampuni ya Plantcor Mining and Plant Hire PTY Ltd ya Afrika Kusini, ambayo itawekeza katika uendelezaji wa mradi huo wa dhahabu.

Kiruswa ametoa maagizo kwa STAMICO pamoja na mwekezaji kuhakikisha kuwa uwekezaji huo unatekelezwa kwa vitendo na kuanza kazi mara moja bila kupoteza muda, ili uweze kuleta manufaa kwa wananchi wa Kigosi na maeneo jirani.

Aidha, amesisitiza kuwa mradi huo unapaswa kupanua wigo wa shughuli za uchimbaji katika eneo la Kigosi ili kuwapa nafasi wachimbaji kupata maeneo halali ya kuendelea na shughuli zao.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa STAMICO, Simon Sirro, amewaomba wananchi waliokuwa wakifanya shughuli katika pori la Kigosi kushirikiana na uwekezaji huo mpya na kuepuka kuwa chanzo cha vikwazo, hasa kutokana na mazoea yaliyokuwepo kabla ya mradi kuanza rasmi.

Sambamba na hilo, Naibu Waziri Kiruswa amesisitiza umuhimu wa kampuni mwekezaji kuzingatia masuala ya Uwajibikaji kwa Jamii (CSR), ili kuhakikisha kuwa jamii zinazozunguka eneo la Kigosi na wilaya ya Bukombe zinanufaika moja kwa moja kupitia miradi ya maendeleo kama vile elimu, afya na miundombinu.

Mkataba huo unatarajiwa kuleta manufaa makubwa kwa Watanzania, ikiwa ni pamoja na Kuongeza ajira kwa vijana, Kuongeza mapato ya serikali,Kuchochea ukuaji wa uchumi wa vijiji vinavyozunguka Kigosi pamoja na Kukuza sekta ya madini nchini

Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO Venance Mwasse, amesema kuwa mradi huo utaanza kwa kufanya utafiti wa kina wa kijiolojia, uchorongaji na uthibitishaji wa rasilimali.

Aidha, hatua zitakazofuata ni pamoja na upembuzi yakinifu wa kiuchumi, maendeleo ya mgodi, ujenzi wa miundombinu muhimu na usimikaji wa mtambo wa uchenjuaji wa dhahabu.

Uwekezaji huu wa dhahabu katika eneo la Kigosi unaonekana kuwa fursa muhimu kwa maendeleo ya mkoa wa Geita na taifa kwa ujumla. Ushirikiano kati ya serikali, mwekezaji na wananchi utakuwa nguzo kuu ya kuhakikisha mradi huu unaleta matokeo chanya na endelevu kwa kizazi cha sasa na kijacho.







 


Na OWM - TAMISEMI, Muheza

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu -TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, amewaelekeza Makatibu Tawala wa Mikoa na Wakurugenzi wa Halmashauri kutowahamisha au kuwaombea uhamisho watumishi wanaobainika kuwa na changamoto za kinidhamu katika Mamlaka za Mikoa na Serikali za Mitaa, na badala yake kuchukua hatua kwa kuwafungulia mashauri ya kinidhamu. 

Prof. Shemdoe ametoa maelekezo hayo hivi karibuni akiwa katika kikao kazi na watumishi wa Muheza kilicholenga kuhimiza uwajibikaji katika usimamizi na matumizi ya fedha za miradi ya maendeleo, ikiwa ni utekelezaji wa maelekezo ya Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba, ambaye wakati wa ziara yake wilayani Muheza alibaini ubadhirifu wa fedha katika Mradi wa Jengo la Utawala na kumuelekeza Prof. Shemdoe na Waziri wa Ofisi ya Rais UTUMISHI na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete kuchukua hatua.

Aidha, Prof. Shemdoe amewaeleleza viongozi hao, kutotumia fedha au vifungu vya bajeti ya maendeleo kufanya malipo ya stahiki za watumishi, na kwamba fedha za mapato ya ndani zinazotengwa na Halmashauri kwa ajili ya miradi ya maendeleo zitumike kwenye shughuli zilizopangwa na si vinginevyo.

Sanjali na hayo, Prof. Shemdoe amewataka Wakurugenzi wa Halmashauri kuendelea kusimamia kikamilifu upatikanaji wa rasilimali fedha na matumizi sahihi ya rasilimali hizo ili kuwaletea wananchi maendeleo endelevu na tabasamu la kudumu.

Vivile, amewataka Makatibu Tawala wa Mikoa kufanya uchambuzi wa matumizi wa fedha za miradi ya maendeleo, pamoja na zinazotoka Serikali kuu na za mapato ya ndani katika kipindi cha kuanzia mwaka wa fedha 2024/25 hadi sasa, “Kama ikibainika kuna Halmashauri yoyote ina ubadhilifu na kuna watuhumiwa wa ubadhirifu huo mimi na Mhe. Ridhiwani Kikwete tutachukua hatua,” amesisitiza Prof. Shemdoe.

Hatua hiyo ya Prof. Shemdoe  ni sehemu ya jitihada za kuunga mkono kwa vitendo azma ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kutaka fedha za miradi ya maendeleo kutumika katika kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi kupitia ujenzi wa miundombinu bora afya, elimu na barabara.

Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) Kanda ya Mashariki imewakumbusha wafanyabiashara na wadau wa gesi ya kupikia (LPG) kuzingatia usalama, afya na utunzaji wa mazingira, wakati wa kusafirisha, kuhifadhi na kuuza bidhaa hizo kwa wateja.

Meneja wa EWURA Kanda ya Mashariki, Mhandisi Lorivii Long’idu, akizungumza wakati wa semina ya wadau hao iliyofanyika mkoani Pwani, 24 Februari 2026 aliwasisitiza wafanyabiashara wa jumla wa LPG kuwa na mikataba na wasambazaji wao na wauzaji wa rejareja wa bidhaa hiyo ili kukidhi matakwa ya kisheria na kiusalama.

Mhandisi Long’idu aliwahimiza pia wadau hao kuwaelimisha wasambazji na wauzaji wa rejareja wa LPG kuhusu usalama na umuhimu wa kutumka mizani iliyohakikiwa na Wakala wa Vipimo wakati wa kutoa huduma ili wananchi wapate huduma bora.

Waziri wa Maji Mhe. Jumaa Aweso (Mb) ameipatia tuzo Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) kwa kutambua mchango wake na unaotolewa na Mamlaka hiyo katika usimamizi wa Mamlaka za Majisafi na Usafi wa Mazingira nchini.

Tuzo hiyo iliyotolewa wakati wa Usiku wa Tuzo za Umahiri katika Sekta ya Maji, tarehe 23 Februari jijini Arusha, ilipokelewa na Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, Dkt. James Andilile.

Akizungumza baada ya kukabidhi tuzo hiyo, Mhe. Aweso alieleza kuwa, lengo ni kutambua utendaji bora wa mamlaka za maji, wasimamizi na watendaji katika maeneo waliofanya vizuri kwa kipindi cha miaka mitatu (2021/22, 2022/23 na 2023/24).

Akizungumza baada ya kupokea tuzo, Dkt. Andilile, alisema kuwa EWURA itaendelea kushirikiana na Wizara ya Maji pamoja na kuzisimamia kwa uthabiti ili ziendelee kufanya vizuri katika utoaji wa huduma.

Na Mwandishi Wetu, Lindi na Mtwara
Katika jitihada za kuongeza uelewa wa matumizi ya Moduli ya kupokea na kushughulikia Malalamiko na Rufaa kupitia Mfumo wa Kielektroniki wa Ununuzi ya Umma (NeST), Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA) imetoa mafunzo kwa wazabuni, wajasiriamali na watumishi wa Umma waliopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa, Mikoa ya Lindi na Mtwara. 
Akielezea kuhusu mafunzo hayo ya siku tano (kuanzia tarehe 16 - 20 Februari, 2026), Meneja wa Usimamizi wa Rufaa na Sheria (PPAA), Bi. Florida Mapunda amesema kuwa mafunzo hayo yamelenga kutoa elimu kwa wadau wa ununuzi wa Umma kuhusu taratibu za uwasilishaji na ushughulikiaji wa malalamiko na rufaa katika mfumo wa NeST kama ilivyoelekezwa katika Sheria ya Ununuzi wa Umma. 
“Sheria ya Ununuzi wa Umma imeweka sharti la lazima kwa ununuzi wa umma kufanyika katika mfumo wa NeST. Kutokana na sharti hilo, PPAA kwa kushirikiana na PPRA tumejenga moduli ya kupokea na kushughulikia malalamiko katika mfumo wa NeST ili kuwasaidia wadau wa ununuzi wa umma (Wazabuni na Taasisi za Umma) kuwasilisha malalamiko na rufaa kieletroniki,” amesema Bi. Mapunda.
Pamoja na mambo mengine, Bi. Mapunda ameongeza kuwa Moduli ya kupokea na kushughulikia malalamiko na rufaa katika mfumo wa NeST ina manufaa makubwa kwa wazabuni kwani inarahisisha uwasilishaji wa malalamiko ya zabuni kwa njia ya mtandao bila kufika ofisini, jambo linalochangia kuokoa muda, gharama na kuongeza uwazi na uwajibikaji katika ununuzi wa Umma.
Kwa upande wake Mkuu wa Sehemu ya Rufaa kutoka PPAA, Bi. Violet Limilabo ameeleza kuwa PPAA ina mchango mkubwa katika kulinda haki za wazabuni kwa kuwapa fursa ya kusikilizwa wanapoona hawakutendewa haki katika michakato ya Ununuzi wa Umma. 
Aidha, PPAA imeendelea kuimarisha uwazi na usawa kwa kuhakikisha taratibu za ununuzi wa umma zinafuatwa kwa mujibu wa sheria na kupunguza migogoro kwa kutoa suluhisho la kisheria.
Naye Afisa Ununuzi kutoka ofisi za PPRA Kanda ya Kusini, Bw. Aziz Njovu alitoa mafunzo kuhusu moduli mpya za majadiliano (negotiations) na uandaaji, upekuzi na utiaji saini wa Mkataba (Contract preparation, vetting and signing kwenye mfumo wa NeST, alisema kwa sasa mchakato wa majadiliano na utiaji saini wa mkataba unahitimishwa kwa njia ya mtandao.
“Matumizi ya mfumo wa NeST yameendelea kuimarisha uwajibikaji na kurahisisha ufuatiliaji wa mikataba ya ununuzio wa umma,” amesema Bw. Njovu.
Mafunzo hayo yamewahusisha jumla ya washiriki 322 ambao ni  wataalamu wa sheria, Tehama na ununuzi pamoja na wazabuni, makundi maalum yakiwemo wanawake, vijana, wazee na watu wenye mahitaji maalum pamoja na mafundi wa ndani.
Mafunzo kuhusu Matumizi ya Moduli ya kupokea na Kushughulikia Malalamiko na Rufaa katika Mfumo wa NeST yaligawanyika katika makundi matatu ambapo Kundi la kwanza ni Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa (tarehe 16 Februari, 2026), Mkoa wa Lindi (tarehe 17 na 18 Februari, 2026) na Mkoa wa Mtwara (tarehe 19 na 20 Februari, 2026)
Mafunzo hayo ni mwendelezo wa mafunzo ya awali yaliyofanyika katika Kanda ya Pwani, Kanda ya Ziwa, Kanda ya Kaskazini, Kanda ya Nyanda za Juu Kusini pamoja na Kanda ya Kati.
 
 
 
 

Katika nchi inayokumbwa na changamoto za kiafya, mazingira na umasikini, nishati safi ya kupikia si tu hitaji la msingi bali ni kichocheo cha maendeleo ya kweli kwa watu na Taifa kwa ujumla.

Katika kukabiliana na ukataji miti ambapo takribani asilimia 16 ya eneo la nchi tayari limegeuka kuwa janga, Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ilizindua mkakati wa kitaifa wa nishati safi ya kupikia unaolenga kuhakikisha asilimia 80 ya watu wanaachana na matumizi ya kuni na mkaa ifikapo mwaka 2034.

Akizungumza ofisini kwake leo tarehe 23 Februari 2026 mara baada ya kupokea ujumbe wa wataalamu kutoka Wakala wa Nishati Vijijini - REA waliopo mkoani Singida kwa ajili ya kuutambulisha mradi wa uuzwaji wa majiko banifu kwa bei ya ruzuku, Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe. Halima Dendego amempongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwa kinara katika utekelezaji wa mkakati wa nishati safi ya kupikia.

Vilevile Mhe Dendego amesema kuwa Rais Samia ni kinara wa utekelezaji wa Nishati safi Afrika hivyo mkoa wa Singida upo tayari na utaanza kugawa majiko hayo banifu katika wilaya zote za mkoa wa Singida ili mpaka kufikia mwaka 2030 mkoa huo uwe umetengeneza alama kubwa kwa wananchi wake kabla hata ya kufikia mwaka 2034.

Pia, amesema kuwa mkoa wa Singida umepokea mitungi ya gesi zaidi ya 18,000 ambayo imesambazwa kwa wananchi ili kutokomeza kabisa nishati chafu ya kupikia.

Kwa upande wake Mhandisi Raya Majallah kutoka REA-Idara ya Nishati Jadidifu na Teknolojia Mbadala akizungumza mbele ya Mkuu wa Mkoa wa Singida ameutambulisha mradi wa uuzwaji wa majiko banifu kwa bei ya ruzuku katika mkoa huo ambapo amesema kuwa Wakala wa Nishati Vijijini umeandaa mpango huo wa uuzaji wa majiko banifu 200,000 kwa bei ya ruzuku yenye ufanisi mkubwa katika utumiaji wake.

Mradi huo unahusisha usambazaji wa majiko banifu yanayotumia kuni na mkaa kidogo ili kupunguza matumizi ya vyanzo hivyo vya nishati Pamoja na athari za moshi zitokanazo na matumizi katika majiko ya kawaida.

Mhandisi Majallah amesema kuwa mikataba hiyo ilisainiwa Mei 9, 2025 na itatekelezwa ndani ya miezi 15 ambapo gharama ya mradi huo ni Shilingi Milioni 340,288,200 kwa mkoa wa Singida na ruzuku inayotolewa na wakala wa nishati vijijini-REA ni shilingi milioni 289,230,504.47 sawa na asilimia 85 ya gharama ya mradi huku wananchi wakichangia Shilingi 51,057,691.53 sawa na asilimia 15 ya gharama ya mradi.

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, ametoa wito kwa Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela kuhakikisha inakuwa kitovu cha ubora wa kitaaluma, utafiti na ubunifu unaolenga kutatua changamoto halisi za dunia ya leo.

Wito huo umetolewa wakati wa hafla ya uwekaji wa jiwe la msingi la ujenzi wa bweni la wanafunzi katika taasisi hiyo.

Waziri Mkuu amesema ujenzi wa bweni hilo ni kielelezo cha dhamira ya dhati ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kuimarisha miundombinu ya elimu ya juu pamoja na kukuza maendeleo ya sayansi na teknolojia nchini. Alisisitiza kuwa miundombinu bora ya elimu ni msingi muhimu wa kuboresha mazingira ya kujifunzia, hasa katika kipindi ambacho idadi ya wanafunzi inaendelea kuongezeka mwaka hadi mwaka.

 "Nitoa wito kwa mkandarasi na uongozi wa taasisi kuhakikisha kunakuwa na usimamizi madhubuti wa rasilimali na utekelezaji wa mradi kwa ufanisi na kwa wakati, ili bweni hilo likamilike mapema na kuanza kutumika kwa manufaa ya wanafunzi."amesema Dkt.Nchemba

Kwa upande wake, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda, amesema Taasisi ya Nelson Mandela inaendana kikamilifu na maelekezo ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuwekeza katika sayansi na teknolojia. Ameeleza kuwa tayari Serikali imeanzisha shule za wasichana za sayansi katika mikoa yote 26 ya Tanzania, hatua inayolenga kuongeza idadi ya wanafunzi wa sayansi watakaokuja kujiunga na taasisi hiyo.

Naye  Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Taasisi ya Nelson Mandela Balozi Maimuna Tarishi, amesema bweni hilo linajengwa kwa kuzingatia viwango vya ubora ili kuhakikisha wanafunzi wanapata makazi salama na yanayowezesha kujifunza, kufanya utafiti na ubunifu kwa utulivu.

Balozi Tarishi ameongeza kuwa bweni hilo litakuwa na vyumba 184, ambapo vyumba 160 vitakuwa vya kujitegemea (self-contained), na vyumba 20 vitakuwa maalumu kwa wanafunzi wenye watoto wadogo na wenye mahitaji maalumu (apartment).