NA EMMANUEL MBATILO, BAGAMOYO

WAHITIMU wa Wakala wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu (ADEM) wametakiwa kuwa mstari wa mbele katika kusimamia masuala mtambuko ikiwemo kupinga vitendo vya rushwa, ukatili wa kijinsia, utoaji wa elimu jumuishi, lishe shuleni, na mapambano dhidi ya dawa za kulevya pamoja na maambukizi mapya ya VVU.

Wito huo umetolewa leo Desemba 5, 2025 wilayani Bagamoyo, Mkoa wa Pwani, na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Hussein Omary, wakati wa mahafali ya 33 ya ADEM ambapo jumla ya wahitimu 785 wa kozi zaStashahada ya Uongozi, Usimamizi na Utawala katika Elimu -DELMA, Stashahada ya Uthibiti Ubora wa Shule - DSQA na Astashahada ya Uongozi, Usimamizi na Utawala katika Elimu -CELMA wamehitimu.

Dkt. Omary amesema masuala hayo yakiwa hayapatiwi uzito unaostahili yanaweza kuathiri kwa kiasi kikubwa sekta ya elimu na maendeleo ya taifa kwa ujumla. Ameongeza kuwa serikali inawategemea wahitimu hao kwa kuwa ujuzi walioupata ni muhimu kwa mustakabali wa elimu nchini.

“Mtakaporudi katika vituo vyenu vya kazi, hakikisheni mnashirikiana na uongozi wa ngazi zote pamoja na jumuiya za shule ili kuhakikisha shule zinafanya vizuri kitaaluma na katika nidhamu,” alisema.

Akizungumzia changamoto ya ukosefu wa rasilimali fedha za kutosha kwa ajili ya ujenzi na utoaji wa mafunzo, Dkt. Omary alisema Serikali kupitia wizara itaendelea kushirikiana na ADEM kupunguza changamoto hizo na, inapowezekana, kuondoa kabisa.

Kwa upande wake Mtendaji Mkuu wa ADEM, Dkt. Maulid Maulid, alisema wahitimu wote wa ngazi mbalimbali ni wataalam mahiri wanaohitajika katika sekta ya elimu, na mchango wao ni muhimu katika kukuza rasilimali watu.

“Hii inaonesha kuwa chuo kinaendelea kuchangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya taifa kupitia uzalishaji wa wataalam wa uongozi na usimamizi wa elimu,” alisema.

Aidha, Dkt. Maulid alibainisha changamoto ya kukosekana kwa bajeti ya kuendesha mafunzo ya muda mfupi kwa viongozi wa elimu, wakiwemo walimu wakuu, wakuu wa shule, maafisa elimu ngazi ya kata hadi mkoa, wathibiti wa shule na viongozi waandamizi wa wizara.

Amesema ili kukabiliana na changamoto hizo, chuo kitaimarisha ushirikiano na taasisi binafsi pamoja na mashirika ya kimataifa ili kuongeza rasilimali fedha na kuendeleza mafunzo.

“Tutaongeza nguvu kupitia ushirikiano wa ‘Public Private Partnership’ na ‘Tanzania Investment Centre’ ili kubainisha wadau wanaoweza kuwekeza katika maeneo ya ardhi tunayomiliki,” alieleza.

Aidha, aliwasihi wahitimu kutumia maarifa waliyopata kuelimisha jamii kuhusu athari za uvunjifu wa amani, mmomonyoko wa maadili na ukosefu wa uzalendo.

“Wahitimu wakasimamie ipasavyo maeneo yao kwa kutoa maarifa kwa walimu na wanafunzi ili watambue thamani ya amani, uzalendo na maadili,” alisema Dkt. Maulid.
 

Na, Ruth Kyelula, Manyara RS.

Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe Queen Sendiga, amefanya ziara ya ukaguzi wa muradi, kusikiliza kero za wananchi na kuzitatua, ambapo ameanza ziara yake hiyo ya Kata kwa Kata, yenye kauli mbiu "tunavua buti ama hatuvui, tukutane site".

Ziara hiyo imefanyika Desemba 04, 2025, katika Halmashauri ya Wilaya ya Hanang', ambapo ameambatana na Wakuu wa Taasisi zote za Umma na binafsi za Mkoa wa Manyara.

Katika ziara yake hiyo ya siku tatu, amefanya ukaguzi wa mradi wa jengo la Utawala la Halmashauri ya Wilaya ya Hanang',ameweka jiwe la msingi shule ya awali na msingi Semonyan iliyopo Kata ya Mogitu, amekagua ujenzi wa mradi wa shule mpya ya Sekondari Waret, amekabidhi nyumba kwa mwathirika wa maporomoko ya tope la Desemba 03,2023, amefanya mkutano wa hadhara Waret, amekagua madarasa mawili shule ya msingi Gisamjanga, amekagua ujenzi wa mradi wa bweni la wavulana shule ya sekondari Mwahu,na amefanya mkutano wa hadhara kijiji cha Gehandu.

Aidha RC Sendiga, katika ziara yake hiyo ya ukaguzi wa miradi na kusikiliza kero, ametoa wito kwa wananchi kupanda miti ya kivuli na miti ya matunda maeneo yote ya miradi na miradi ya ujenzi wa shule, ikamilike kwa wakati ili mwezi Januari watoto waingie shule.

Na WMJJWM - Morogoro

Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum kwa kushirikiana na Wizara za kisekta pamoja na Baraza la Taifa la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NaCoNGO) imeanza zoezi la kufanya tathmini ya utendajii kazi wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NGOs) kwa kipindi cha miaka mitano 2020/2021 - 2024/2025.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi akikabidhi Tuzo maalumu Meneja Mkazi wa Kampuni ya Emirates Leisure Retail Zanzibar, Paul Atallah (wa pili kushoto), kwa niaba ya kampuni hiyo na Qatar Foundation kwa kutambua mchango wao mkubwa katika kusaidia watu wenye uhitaji.

...............................

 Na Dotto Mwaibale, Zanzibar

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi ametoa Tuzo maalum kwa Kampuni ya Emirates Leisure Retail Zanzibar na Qatar Foundation kwa kutambua mchango wao mkubwa katika kusaidia watu wenye uhitaji.

Dkt. Mwinyi alitoa tuzo hizo katika kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Watu Wenye Ulemavu yaliyofanyika Desemba 4, 2025 kwenye Ukumbi wa Dr. Shein – Tunguu, Chuo Kikuu cha SUZA, Mkoa wa Kusini Unguja tukio lililohudhuriwa na viongozi wa Serikali, wadau wa maendeleo, mashirika ya kijamii, na wananchi kutoka sehemu mbalimbali za Zanzibar.

Akihutubia katika maadhimisho hayo Rais Mwinyi aliwataka wadau kuendelea kuunga mkono jitihada za Serikali za kuwawezesha watu wenye ulemavu na alisisitiza kuwa maendeleo ya kweli ni yale yanayowahusisha watu wote bila kuacha kundi lolote nyuma.

Aidha, Dkt. Mwinyi alitumia nafasi hiyo kuwapongeza wadau na wahisani kwa kujitolea kwao kuchangia maendeleo ya jamii zenye watu wenye ulemavu na kueleza kuwa Serikali itayafanyia kazi maoni na ushauri uliotolewa ili kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata fursa kamili za kutimiza malengo yao.

Kwa upande wake Meneja Mkazi wa Kampuni ya Emirates Leisure Retail Zanzibar, Paul Atallah, alilishukuru Baraza la Watu Wenye Ulemavu Zanzibar kwa kutambua mchango wa Emirates Leisure Retail na kueleza kwamba kampuni hiyo itaendelea kuwa mshirika wa karibu wa Serikali na jamii katika kuleta maendeleo chanya kwa watu wenye ulemavu.

Utambuzi wa Wadau Maalumu

Katibu Mtendaji wa Baraza la Watu Wenye Ulemavu Zanzibar, Ussi Khamis Debe, akizungumza kwenye maadhimisho hayo  alitoa shukrani kwa wadau wote wanaounga mkono juhudi za Serikali katika kusaidia watu wenye ulemavu.

Aidha, kwa nafasi ya kipekee alimshukuru Afisa Utawala Msaidizi wa Kampuni ya Emirates Leisure Retail Zanzibar, Ramadhan Hussein Layya (Maarufu Msokolo),kwa mchango wake mkubwa na wa muda mrefu, hususan katika kusaidia watu wenye ulemavu wa ngozi kupitia misaada, ushiriki, na michango inayobadilisha maisha ya wanufaika.

Kaulimbiu ya Maadhimisho:

"Uwezeshaji na Ushirikishwaji wa Watu Wenye Ulemavu kwa Maendeleo Jumuishi."

Misaada Iliyotolewa katika maadhimisho hayo kwa ajili ya makundi mbalimbali ya wahitaji ni

Vyerehani kwa ajili ya kujiajiri, kofia maalumu (round hats) kwa ulinzi wa ngozi, miwani ya kinga na vifaa vya kurekebisha uoni, baiskeli za mwendo kwa watu wenye ulemavu wa viungo, fedha za mikopo kwa kuanzisha au kuendeleza biashara.

Vifaa vingine vilivyotolewa ni vya kuongeza uwezo wa kujitegemea mashine za kusaga nafaka.

Misaada hiyo imeleta furaha, matumaini, na thamani kubwa kwa wanufaika na familia zao, ambayo inakwenda kuwasaidia kutimiza ndoto zao na kuimarisha ustawi wa familia zenye watu wenye uhitaji maalumu.

Kauli ya Emirates Leisure Retail Zanzibar na Qatar Foundation:

Uongozi wa kampuni hizo umeeleza dhamira zao za kuendelea kushirikiana na Serikali na wadau wengine kuhakikisha watu wenye ulemavu Zanzibar wanapata fursa sawa za ustawi na maendeleo, na kuendelea kuwekeza katika miradi ya kijamii inayobadilisha maisha ya watu wenye uhitaji maalumu.

Viongozi wa Kampuni hizo na wadau mbalimbali wakiwa kwenye maadhimisho hayo.
 

Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) imekuwa mshindi wa kwanza na kupewa tuzo ya umahiri katika utayarishaji bora wa taarifa za hesabu kwa mwaka 2024 kwa kufuata viwango vya Kimataifa vya Uandaaji wa Hesabu International Public Sectors Accounting Standards (IPSAS) katika kundi la Taasisi za Serikali zinazojitegemea.

MAMLAKA ya Mapato tanzania (TRA), imeibuka Mshindi wa kwanza wa jumla katika tuzo ya Uandaaji wa Hesabu za Kifedha zinazozingatia viwango vya Kimataifa vya Uhasibu katika Sekta ya Umma (IPSAS), zinazotolewa na Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu (NBAA).

Pia imeibuka mshindi wa kwanza katika tuzo ya kipengele cha Taasisi za Serikali (Government Agency Categories).

Akizungumza jana jijini Dar es Salaam katika hafla ya kukabidhi tuzo hizo, Naibu Waziri wa Fedha Laurent Luswetula, alizipongeza taasisi zilizoibuka na ushindi, huku akisema wizara hiyo itaendelea kutoa ushirikiano kwa NBAA, ili kuendelea kuzalisha wahasibu na wakaguzi bora.

Pia alisema serikali itahakikisha NBAA inasimama imara ili iendelee kuzalisha watendaji bora kwa maslahi mapana ya taifa.

"Wizara ya fedha itaendelea kuhakikisha inatoa ushirikiano kwa NBAA ili kuzalisha wahasibu na wakaguzi bora kwa mslahi mapana ya taifa letu."alisema

Vilevile Naibu Waziri huyo alipongeza NBAA kwa kuendelea kupanua wigo wa kuongeza washiriki kila mwaka.

Naye Naibu Kamishina Mkuu wa TRA Mcha Hassan Mcha lisema, tuzo waliyopata ina umuhimu mkubwa, kwani inachangia kuonesha utendaji wao unakubalika Kimataifa.

Pia alisema tuzo hiyo inaonesha umahiri na ubunifu uliyopo kwa watumishi wa mamlaka hiyo.

"Tuzo hii ina umuhimu sana kwetu, inachangia kuonesha utendaji wetu unakubalika Kimataifa na ina waonesha Walipa Kodi kwamba kila shilingi inayokusanywa inafika katika mfuko Mkuu wa Serikali."alisema

Vilevile Mcha aliwashukuru Walipa Kodi kwa kuendelea kulipa kwasababu TRA imeendelea kuvuka malengo ya ukusanyaji mapato kila mwaka.

Kwamujibu wa Mwenyekiti wa Bodi ya NBAA Profesa Slyivia Temu, katika hafla hiyo jumla ya taasisi 86 za Umma na binafsi zimeshiriki katika kujipima ubora wa kuwasilisha taarifa za fedha kwa mwaka 2024.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa NBAA Pius Maneno, lengo la tuzo hizo ni kuhakikisha taarifa za hesabu zinazotolewa zinakuwa na uwazi na uwajibikaji.

Alifafanua kuwa, tuzo hizo ni taarifa za hesabu za kuanzia Januari mwaka 2024 hadi Desemba, ambazo zimezalishwa kwa kufuata hesabu za Kimataifa na zilizopata hati safi.

Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese,akizungumza wakati akifungua Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Mji Handeni lililofanyika katika ukumbi wa Halmashauri.

Na Mwandishi Wetu, Handeni TC

Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese, ametoa wito kwa Madiwani wa Halmashauri ya Mji Handeni kushirikiana na Ofisi ya Mkurugenzi katika kubuni vyanzo vipya vya mapato, sambamba na kuimarisha umoja, amani na uzalendo katika maeneo yao ya utawala.

Wito huo umetolewa katika ufunguzi wa Baraza la Madiwani lililofanyika katika ukumbi wa Halmashauri, muda mfupi baada ya madiwani hao kuapishwa rasmi kuanza kutekeleza majukumu yao.

Akizungumza wakati wa kikao hicho, Mhe. Nyamwese amewataka madiwani kuhakikisha wanakuwa chachu ya amani na utulivu, akisisitiza kuwa misingi hiyo ni nguzo muhimu kwa ustawi wa jamii na utekelezaji wa shughuli za maendeleo.

Amebainisha kuwa madiwani wana wajibu mkubwa wa kushirikiana kikamilifu na Mkurugenzi wa Halmashauri katika kubuni vyanzo vipya na endelevu vya mapato vitakavyoongeza uwezo wa Serikali ya Mtaa kusimamia na kutekeleza miradi ya wananchi.

Aidha, ameeleza kuwa kuimarisha ukusanyaji mapato na kusimamia miradi ya kimkakati kutasaidia kupunguza utegemezi na kuongeza kasi ya maendeleo ya Halmashauri.

“Madiwani mna wajibu wa kuhakikisha ushirikiano baina ya watendaji na wananchi unaongezeka ili kufanikisha malengo ya pamoja ya maendeleo,” amesisitiza.