Wamiliki wa shule zisizo za serikali nchini wamezitaka mamlaka za serikali za mitaa kuacha kutoza ushuru na tozo ambazo wanadai tayari zilisamehewa na Serikali Kuu, wakisema hali hiyo inaongeza gharama za uendeshaji na kuhatarisha utoaji wa huduma za elimu.
Wakizungumza na waandishi wa habari jijini Arusha, viongozi wa Shirikisho la Wamiliki na Mameneja wa Shule na Vyuo Visivyo vya Serikali Tanzania (TAMONGSCO) wamesema shule zisizo za serikali zinakabiliwa na zaidi ya tozo na makato mbalimbali, ikiwemo ushuru wa huduma unaotozwa na halmashauri kwa taasisi zinazotoa huduma, ada za mitihani, leseni za mabango ya shule pamoja na michango ya michezo na taaluma.
Mtendaji Mkuu wa TAMONGSCO, Benjamin Nkonya, alisema pamoja na mzigo wa makusanyo hayo, kinachowasumbua zaidi ni namna baadhi ya halmashauri zinavyotekeleza ukusanyaji wake.
Alidai kuwa katika baadhi ya matukio, askari mgambo huingia shuleni kufuatilia madeni ya ushuru na tozo, jambo ambalo kwa mujibu wake huathiri mazingira ya kufundishia na kujifunzia.
“Tunachohoji si suala la kulipa wajibu wa kisheria pekee, bali ni matumizi ya nguvu katika ukusanyaji wa fedha hizo na kuendelea kudai baadhi ya tozo ambazo tunaamini tayari ziliondolewa au kutolewa mwongozo wake na Serikali Kuu,” alisema Nkonya.
Amesema shirikisho hilo limekuwa na mahusiano mazuri na mamlaka ya Mapato nchini TRA wakati wote wanapohitaji ushirikiano wao tofauti na halmashauri ambao wamekuwa wakitumia ubabe kukusanya tozo hizo wakati taasisi hizo zikiwa zimesamehewa ushuru huo.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa TAMONGSCO Kanda ya Kaskazini, Leonard Mao, Malalamiko hayo yameelekezwa zaidi kwa baadhi ya halmashauri, hususan, ambazo zinadaiwa kuendelea kukusanya ushuru na tozo mbalimbali kutoka kwa shule zisizo za serikali licha ya kuwepo kwa maelekezo ya serikali kuhusu baadhi ya makusanyo hayo.
“Tunaamini mwongozo wa wazi utasaidia kuondoa migogoro isiyo ya lazima na kuweka mazingira bora ya uwekezaji katika sekta ya elimu,” alisema Mao.
Naye Wakili Mshauri wa TAMONGSCO, Pascal Temba, alisema iwapo kuna ushuru au tozo zinazodaiwa baada ya kufutwa na Serikali Kuu, mamlaka husika zinapaswa kuweka wazi msingi wa kisheria unaoruhusu makusanyo hayo.
Kutokana na hali hiyo, TAMONGSCO imesema tayari imewasilisha barua kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali ikiomba ufafanuzi wa kisheria kuhusu mamlaka ya halmashauri kuendelea kukusanya baadhi ya ushuru na tozo zinazolalamikiwa.
Shirikisho hilo linaeleza kuwa majibu yatakayopatikana yatasaidia kutoa mwongozo kwa wadau wote na kuondoa mkanganyiko uliopo.
Wakati wakisubiri ufafanuzi huo, wamiliki wa shule zisizo za serikali wanaonya kuwa endapo changamoto hiyo haitapatiwa ufumbuzi, gharama za uendeshaji wa shule zinaweza kuongezeka na hatimaye kuathiri upatikanaji wa elimu kwa wazazi na wanafunzi.
Kwa wadau wa elimu, mjadala huu unafungua swali muhimu: Je, mazingira yaliyopo yanasaidia kukuza uwekezaji katika sekta ya elimu au yanaongeza mzigo ambao mwisho wake hubebwa na mzazi na mwanafunzi.















