Serikali ya India imeshatumia Dola za Kimarekani milioni 600 sawa na fedha za kitanzania Bilioni 1.4 katika kuwekeza miradi ya maendeleo hapa nchini ikiwa ni jitihada za kuiunga mkono serikali katika kuwaletea maendelea wananchi wake.

Fedha hizo ni kutoka na serikali ya India kutenga katika bajeti yake ya mwaka 2026/27 dola Bilioni 1.1 sawa na fedha za kitanzania  shilingi Trioni 2.7 kwa ajili ya miradi yote ya maendeleo hapa nchini.

Fedha hizo Dola milioni 600 ni kwa ajili ya  miradi ya maendeleo ikiwemo Afya,elimu,maji na barabara ikiwa ni njia mojawapo ya kuunga mkono utendaji kazi wa Rais Samia Suluhu Hassan katika kipindi cha uongozi wake.

Hayo yalisemwa na Balozi wa India hapa nchini ,Bishwadip Dey katika hafla ya uzinduzi wa mradi wa maji safi na salama toka chanzo cha chemchem ya tono,Kijiji cha Losirwa kata ya Iloirienito Tarafa ya Ketumbeine Wilayani Longido Mkoani Arusha ambapo serikali ya India ilitoa shilingi milioni 125 katika mradi huo na watu zaidi ya 2000 kunufaika.

Balozi Dey alisema yeye hakwenda Longido kama mtalii bali ameenda Longido kama mwanafamilia kwa kwenda kuangalia miradi iliyoanzishwa na kumalizwa na nchi ya India kupitia wawekezaji wa nchi hiyo.

Alisema serikali ya India inaunga mkono jitihada za serikali chini ya Rais Samia Suluhu Hassan katika kuwaletea wananchi wake maendeleo katika sekta zote na kwa kutambua hilo ndio maana serikali ya India imetenga fedha hizo ikiwa ni njia mojawapo ya  kumuunga mkono kazi ya Rais kwa kupeleka fedha katika miradi  sehemu mbalimbali kote nchini.

‘’Serikali ya India imepitisha bajeti kwa ajili ya miradi ya maendeleo kote nchini na tayari dola milioni 600 zimeshatumika katika miradi hiyo ikiwemo miradi iliyopo Longido hiyo ni kumsaidia Rais kwa kazi nzuri anayoifanya kwa wananchi wake’’ alisema Balozi Dey

Aidha ameishukuru kampuni ya Dar Solution inayomilikiwa na mwekezaji kutoka nchini India kwa kuchangia vifaa vya Tehama vyenye thamani ya shilingi milioni 15 na kuwezesha ukamilishaji wa majengo ya shule shikizi katika kata ya Engikaret,Noondoto na Ketumbeine vyneye thamani ya shilingi milioni 30 na kusema kuwa hayo yote ni matunda ya serikali yao katika kuwahimiza wawekezaji kushirikiana na serikali ya Tanzania.

Balozi alisema na kuwaeleza wananchi wa kata ya Iloirienito juu ya mahitajitaji ya shule ya katika Kata hiyo na kusema kuwa watakwenda kuyafanyia kazi  ili kata hiyo iwe na shule ya karibu kuondoa usumbufu kwa watoto kwenda umbali mrefu kusaka elimu huku wakikutwa na vikwazo vingi.

Naye Naibu Waziri wa Madini na Mbunge wa Jimbo la Longido ,Dkt Steven Kiruswa alisema mradi wa maji uliozinduliwa na Balozi Dey umewezeshwa kwa nguvu za wananchi wakishirikiana na yeye pamoja na wahisani toka kampuni ya kihindi ya Dar Solution ambayo ndio iliyonunuwa mabomba yote na matanki yaliyotumika kukusanya na kusambaza maji ya chemchem ya tono katika vitongoji vya Kisambi na Olomuki.

Kiruswa alisema na kuishukuru serikali ya India kwa ushirikiano mkubwa wanaoutoa kwa serikali na wananchi wa Longido na kusema kuwa wao kama serikali ya Tanzania na wananchi wa Longido watashirikiana kwa hali na mali katika kufanikisha miradi ya manedeleo katika Jimbo hilo iliyoanzishwa na nchi hiyo.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Longido,Salumu Kally pamoja na kumshukuru Balozi Dey pia aliwaomba wananchi wa Longido kutunza miradi hiyo ili iwajengee heshima kwa wahisani wawqeze kuendelea kusaidia miradi mingine wilayani huo.






















 


Na OWM - TAMISEMI, Lushoto

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba amesifu utendaji kazi wa Mbunge wa Lushoto ambaye ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu -TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe kwa namna anavyotumia uzoefu wake wa utendaji kazi Serikalini katika kuwahudumia na kuwaletea maendeleo wananchi wa Lushoto, ikiwa ni pamoja na kutekeleza jukumu la kusimamia Mamlaka za Serikali za Mitaa.

Dkt. Nchemba amempatia maua yake Prof. Shemdoe Februari 17, 2026 mbele ya wananchi wa Lushuto alipozungumza nao, mara baada ya kuzindua rasmi mtambo wa kuzalisha hewa tiba ya oksijeni katika Hospitali ya Wilaya ya Lushoto. 

“Nikiri mna Mbunge makini, mwenye hadhi, mzoefu wa utendaji kazi Serikalini, ameshaitumikia Serikali katika nyadhifa mbalimbali kwenye wizara kadhaa hivyo anafahamu jambo lolote linalohusu maendeleo ya Lushoto lishughulikiwaje na ni wizara ipi itahusika,” amesisitiza Prof. Shemdoe.

Mhe. Waziri Mkuu  amewaeleza wananchi wa Lushuto kuwa wamepata kiongozi jembe na mchapa kazi ambaye yuko tayari kuwaletea maendeleo wana Lushoto hivyo wamuunge mkono ili aweze kutimiza ndoto yake ya kuwatumikia wananchi wa Jimbo la lushoto.

Aidha, Dkt. Nchemba amemtaka Mwenyekiti wa Halmashauri na Madiwani kumsaidia Prof. Shemdoe kwa kuwatembelea wananchi, kusikiliza kero zao na kuziwasilisha kwa Prof. Shemdoe ili aweze kuzifanyia kazi kwani kutokana na majukumu ya kitaifa aliyonayo Prof. Shemdoe kuna wakati anakosa muda wa kuwatembelea wananchi na kupokea simu zao mara kwa mara.

“Kutokana na majukumu aliyonayo Prof. Shemdoe anapaswa kushughulika na mambo makubwa ya kimaendeleo kwa kuhakikisha fedha za utekelezaji zinafika kwa wakati, hivyo Mwenyekiti wa Halmashauri na Madiwani mkutane na wananchi na muwasilishe changamoto za wananchi hao kwa Prof. Shemdoe ili azifanyie kazi,” ameelekeza Dkt.  Nchemba. 

Dkt. Mwigulu Nchemba amewaeleza wananchi wa jimbo la Lushoto kuwa kitendo cha Prof. Shemdoe kuaminiwa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan na kumpatia dhamana ya kusimamia Tawala za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa wasitarajie atafanya ziara za kutembelea vitongoji kila mara na badala yake ziara hizo zitafanywa na madiwani.



Waziri Mkuu, Mwigulu Nchemba, ameielekeza kampuni ya Abanyambo Enterprises & General Supplies Ltd kuendelea na shughuli za uchimbaji wa madini ya bauxite katika Kata ya Magamba, Wilaya ya Lushoto, mkoani Tanga.


Hatua hiyo imekuja kufuatia utekelezaji wa agizo lililokuwa limetolewa awali na Waziri Mkuu mstaafu, Kassim Majaliwa, ambaye alisitisha uchimbaji huo hadi tathmini ya athari kwa mazingira na binadamu itakapofanyika na kukamilika.


Akizungumza wakati wa ziara yake mkoani humo, Waziri Mkuu alisema kampuni hiyo, ambayo inamiliki leseni nne halali, imeruhusiwa kuendelea na uzalishaji baada ya Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kujiridhisha na kutoa kibali rasmi cha tathmini ya athari kwa mazingira.

Alitoa kauli hiyo alipokuwa akijibu swali la aliyekuwa Mwenyekiti wa Kitongoji cha Magamba, Mahamud Kotti, ambaye alitaka kujua msimamo wa Serikali kuhusu mradi huo.  licha ya uchimbaji huo kuwa chanzo cha ajira na mapato kwa kijiji na halmashauri.



Hata hivyo Waziri Mkuu alisisitiza kuwa Serikali haitavumilia uvunjaji wa sheria katika sekta ya madini, akieleza kuwa wawekezaji wote wanapaswa kufuata taratibu zilizowekwa ili kulinda rasilimali za taifa pamoja na mazingira.

Katika hatua nyingine, alitangaza kusimamishwa kwa leseni 45 zilizokuwa zikitaka kufanya shughuli katika mgodi huo kinyume na sheria na masharti ya uchimbaji.


 Alifafanua kuwa uamuzi huo umefikiwa baada ya kubainika kuwepo kwa ukiukwaji wa taratibu ambao ungeweza kuhatarisha usalama wa mazingira na kusababisha upotevu wa mapato ya Serikali.


“Hatutakuwa tayari kuona rasilimali za nchi zinachimbwa bila kufuata sheria. Lazima kila mmoja aheshimu utaratibu,” alisisitiza Waziri Mkuu.

Aidha, amemuagiza Afisa Madini Mkoa wa Tanga kusimamia kikamilifu utekelezaji wa agizo hilo na kuhakikisha kuwa kampuni ya Abanyambo pekee ndiyo inayoendelea na shughuli za uchimbaji katika eneo hilo.


Ziara hiyo ni sehemu ya ukaguzi wa miradi ya maendeleo na shughuli za kiuchumi unaofanywa na Waziri Mkuu, kwa lengo la kuhakikisha sheria, uwazi na uwajibikaji vinazingatiwa katika usimamizi wa rasilimali za taifa.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda,akizungumza katika ufunguzi wa mafunzo elekezi ya Wathibiti Ubora wa Shule ngazi ya wilaya uliofanyika   wilayani Bagamoyo Mkoani Pwani.

......

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda, amesema kuwa jukumu kubwa la Wathibiti Ubora wa Shule ni kuhakikisha utekelezaji wa sera, sheria, miongozo na mikakati ya elimu unafanyika kwa ufanisi.

Akizungumza  wilayani Bagamoyo Mkoani Pwani katika ufunguzi wa mafunzo elekezi ya Wathibiti Ubora wa Shule ngazi ya wilaya, ameeleza kuwa watendaji wanapaswa kusaidia katika utekelezaji wa sera na kuhakikisha wanazielewa kikamilifu, hususani zinazohusu elimu ya amali na elimu ya lazima.

Profesa Mkenda amesema wathibiti Ubora wa Shule wanapaswa kutoa taarifa juu ya changamoto zinazojitokeza shuleni ikiwemo ukosefu wa vifaa au madarasa kwa Wakurugenzi na Wakuu wa Wilaya ili hatua za kutatua changamoto hizo zichukuliwe haraka.

Akizungumzia mageuzi makubwa ya Sekta ya Elimu, Waziri amesema kuwa kuanzia mwaka wa masomo 2027/2028, elimu ya msingi itaanza kutolewa kwa Miaka Sita badala ya Saba na elimu ya lazima itakuwa miaka kumi kuanzia darasa la kwanza hadi kidato cha nne.

"Mabadiliko haya yataleta “double cohort,” ambapo wanafunzi wa darasa la saba (mfumo wa zamani) na darasa la sita (mfumo mpya) wataingia kidato cha kwanza kwa wakati mmoja. Hata hivyo, hali hiyo ni ya mpito na mfumo utarejea katika “single cohort” baada ya muda,'amefafanua Waziri Mkenda.

Amesema Serikali inawekeza katika shue za ufundi, lakini bado kuna uhaba wa karakana, vifaa na walimu wenye sifa huku akisisitiza Halmashauri kupanga bajeti kwa umakini ili kuzuia shule kufungwa kutokana na ukosefu wa mahitaji ya msingi.

Mkurugenzi Msaidizi wa Uthibiti Ubora wa Shule, Monica Mpululu, amesema kuwa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imekuwa ikitekeleza majukumu yake kwa kasi na kwa ushirikiano wa karibu na Wathibiti Ubora wa shule nchini.

Mkurugenzi huyo ameeleza kuwa wizara imeendelea kuwawezesha wathibiti Ubora wa shule kwa kuwapatia rasilimali muhimu, ikiwemo fedha na vifaa vya kazi ambayo inasaidia kuboresha usimamizi na ufuatiliaji wa shule katika maeneo mbalimbali ya nchi na kuongeza ufanisi wa kazi za uthibiti ubora.

Mpululu amesema kuwa ushirikiano wa wadau wote wa elimu ni msingi wa mafanikio ya sekta, na kwamba juhudi zinazofanywa sasa ni matokeo ya kazi ya pamoja inayolenga kuinua kiwango cha elimu kwa manufaa ya taifa.

Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Dkt.Mosses Kusiluka amesema kuwa serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Raisi Daktari Samia Suluhu Hassan imeipa kipaumbele cha kwanza sekta ya TEHAMA nchini kwa kuendeleza mifumo mbalimbali na kuhakikisha huduma zinapatikana kirahisi.

Katika kufanikisha hilo pia serikali imeendelea kuwekeza katika sekta hiyo na kuhakikisha kuwa Tanzania inaendelea kuweka rekodi nzuri ya kutambuliwa kimataifa katika kutoa huduma nzuri ya serikali mtandao.

Ameyasema hayo leo wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha Sita cha Serikali Mtandao (eGA) kinachoendelea katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa (AICC) mkoani Arusha. 

"Kuwepo kwangu hapa leo ni kuonyesha  umuhimu wa serikali ya awamu ya Sita  ambayo imeipa umuhimu wa kipekee TEHAMA,Mheshimiwa Raisi wetu Daktari Samia  Suluhu Hassan  anaishi TEHAMA na anaitumia kwa kiasi ambacho watu wengi hawawezi kufahamu kwahiyo TEHAMA ni kipaumbele cha kwanza kwenye Utekelezaji wa Ajenda ya serikalimtandao"Alisisitiza Balozi  Kusiluka

Aidha amesema kuwa Tanzania ni nchi yenye mafanikio makubwa duniani kwenye matumizi ya TEHAMA,hatua kubwa imepigwa na mafanikio ya eGa ni kielelezo kizuri cha azma ya serikali  kutumia teknolojia  kurahisisha upatikanaji wa huduma kwa wananchi  hali ambayo inapelekea huduma kupatikana kwa wakati.

Nae Mhandisi Benedict  Ndomba  ni Mkurugenzi wa Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) amesema kuwa kikao hicho ni muhimu kwa kuwa kitakuja na maazimio ya pamoja ya kuboresha huduma ya serikali mtandao, kuongeza uwazi na uwajibikaji katika utendaji kazi na kujenga serikali mtandao.

Mhandisi Ndomba amewahikikishia washiriki eGA itaendelea kuwa mshirika wa karibu wa kuendelea kuijenga serikali Mtandao.

Kwa Upande wake Mwenyekiti wa Bodi  ya Wakurugenzi  Mamlaka  ya Serikali Mtandao (eGA), Daktari Mussa Kissaka amesema kuwa serikali ilianzisha mamlaka hiyo ili kuratibu  na kusimamia  jitihada za serikali mtandao pamoja na kuhakikisha kuwa uzingatiaji wa sera,sheria,kanuni na  miongozo na viwango ya serikali mtandao kupitia taasisi za umma huku  lengo likiwa ni kujenga  serikali mtandao kupitia teknolojia za kisasa kwa  ajili ya kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

Jumla ya washiriki 1400 wanashiriki mkutano huo ambao unajumuisha wadau mbali mbali kutoka serikalini na sekta binafsi kwa lengo la kuboresha serikali mtandao.











Na.Alex Sonna-DODOMA

WAZIRI  wa Madini na Mbunge wa Jimbo la Mtumba Mhe. Anthony Mavunde , amevitaka vikundi vilivyonufaika na mkopo wa shilingi bilioni mbili uliotolewa kwa wajasiriamali wa jimbo hilo, kutumia fedha hizo kama zilivyokusudiwa ili kujikwamua kiuchumi.

Akizungumza wakati wa hafla ya kukabidhi mikopo hiyo jijini Dodoma, Mhe.Mavunde amesema kuwa  azma ya serikali ni kuhakikisha wananchi wanapata nyenzo na mitaji ya kuwawezesha kupanua na kuendeleza shughuli zao za kiuchumi.

Amesema kuwa  Mkopo huo umefadhiliwa na CRDB Bank kupitia CRDB Bank Foundation katika programu ya imbeju inayolenga kuwawezesha wajasiriamali wadogo na wa kati.

"Tumieni vizuri  mikopo hiyo kwa kuanzisha na kuendeleza shughuli mbalimbali za ujasiriamali ili iweze kuleta tija, kuwaimarisha kiuchumi na hatimaye kurejeshwa kwa manufaa ya wengine."amesema Mhe.Mavunde

Mhe.Mavunde amesema kuwa  mikopo hiyo ni kama mbegu inayohitaji kutunzwa na kuendelezwa ili izae matunda yenye manufaa kwa mkopaji na jamii kwa ujumla.

“Mikopo hii ni mbegu. mkizitumia vizuri zitazaa matunda na kuwainua kiuchumi, lakini pia zitawawezesha wengine kupata fursa kama hii baada ya ninyi kurejesha kwa wakati,” amesisitiza 

Aidha ameongeza kuwa dhamira yake ni kuona wananchi wa mtumba wanaachana kabisa na mikopo umiza maarufu kama ‘mikopo ya kausha damu’ na badala yake wanatumia fursa rasmi za kifedha zenye masharti nafuu na rafiki kwa maendeleo yao.

“Wananchi wa mtumba wakae mkao wa kula. kuna mipango mingi ya kuwawezesha kiuchumi inaendelea kuja, na lengo letu ni kuhakikisha kila mmoja anapata fursa ya kujikwamua,” ameongeza

Hata hivyo amewataka wanufaika kuchangamkia fursa hizo kila zinapojitokeza na kuhakikisha wanarejesha mikopo kwa wakati ili wengine nao wapate kunufaika na mpango huo.

kwa upande wake, Mkurugenzi mtendaji wa CRDB Bank Foundation,Bi. Tully Esther Mwambapa, amesema kuwa  taasisi hiyo itaendelea kushirikiana na serikali kupitia programu mbalimbali zinazolenga kuyawezesha makundi tofauti ya wananchi kiuchumi.

Amesema kuwa  lengo la programu ya imbeju ni kuwajengea uwezo wajasiriamali kwa kuwapatia mitaji pamoja na elimu ya usimamizi wa biashara ili waweze kuendesha miradi yao kwa tija na ufanisi.

" Hadi sasa taasisi hiyo imetoa mikopo ya mitaji wezeshi yenye thamani ya shilingi bilioni 22.1, huku zaidi ya wajasiriamali milioni moja wakinufaika nchini kote."amesema 

Amesema kuwa  mikopo hiyo imekuwa chachu ya kuboresha ustawi wa kiuchumi wa jamii na kuchangia katika ukuaji wa pato la taifa kupitia shughuli za uzalishaji mali zinazofanywa na wanufaika.

Baadhi ya wanufaika wa mikopo hiyo wameishukuru CRDB  kwa kuwagusa moja kwa moja katika maisha yao na kuahidi kuitumia mikopo hiyo katika shughuli za uzalishaji mali pamoja na kuirejesha kwa wakati ili iweze kuwafikia watu wengi zaidi katika maeneo mbalimbali nchini.

hafla hiyo imeelezwa kuwa sehemu ya jitihada za kuimarisha uchumi wa wananchi wa mtumba na kuongeza mchango wao katika maendeleo ya taifa.