Asilimia 10 ya mapato ya sekta ya madini kuelekezwa kwenye utafiti
MBT kuwanufaisha wachimbaji Mundarara
Naibu Waziri wa Madini, Dkt. Steven Kiruswa, amesimamisha kwa muda uchaguzi wa Viongozi wa Mabroka wa Madini katika Wilaya ya Longido, Mkoa wa Arusha, akisisitiza kuwa uchaguzi huo hautafanyika hadi pale wapiga kura watakapopatiwa elimu ya kutosha kuhusu haki, wajibu na taratibu za uchaguzi kwa mujibu wa Katiba ya Mabroka.
Hatua hiyo inalenga kuhakikisha uchaguzi unafanyika kwa uwazi, haki na ushirikishwaji wa wadau wote, huku ukiepusha migogoro inayoweza kujitokeza kutokana na kutokuelewa taratibu za uchaguzi.
Akizungumza leo Juni 10, 2026 na wachimbaji, wafanyabiashara wa madini na viongozi wa Serikali wakati wa ziara yake wilayani humo, Dkt. Kiruswa amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imejidhatiti kujenga sekta ya madini yenye uwazi, uwajibikaji na ushiriki mpana wa Watanzania katika shughuli zote za mnyororo wa thamani wa madini.
"Nataka uchaguzi huu ufanyike kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zote. Kwanza tutoe elimu kwa wapiga kura ili kila mshiriki ajue haki na wajibu wake. Tukifanya hivyo tutapata viongozi wenye uhalali, wanaokubalika na watakaoweza kuwatumikia wadau wa sekta ya madini kwa ufanisi," amesema Dkt. Kiruswa.
Ameelekeza Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyabiashara wa Madini Tanzania (CHAMMATA), Jeremiah Kituyo, kwa kushirikiana na viongozi wa kitaifa wa chama hicho, kuhakikisha elimu hiyo inatolewa kwa wakati na uchaguzi mpya unaratibiwa mara baada ya zoezi hilo kukamilika bila kucheleweshwa.
Naibu Waziri huyo amewakumbusha mabroka wote wa madini kuzingatia matakwa ya Sheria ya Madini kwa kuhakikisha wanakuwa na leseni halali za ubroka pamoja na vitambulisho vinavyoonesha namba za leseni zao wakati wote wanapotekeleza shughuli zao.
Amesema Serikali haitamvumilia mtu yeyote atakayejihusisha na ubroka wa madini bila leseni halali, akibainisha kuwa hatua hiyo inalenga kulinda maslahi ya wafanyabiashara, kuongeza uwajibikaji na kuhakikisha Serikali inakusanya mapato yote yanayostahili.
Aidha, amewataka viongozi wa vijiji, viongozi wa sekta ya madini na wananchi kushirikiana kwa karibu katika kulinda rasilimali za madini na kuhakikisha shughuli za uchimbaji zinafanyika kwa mujibu wa sheria na zinawanufaisha wananchi wa maeneo husika.
Katika kuimarisha sekta ya madini, Dkt. Kiruswa amesema Serikali imeanza kutekeleza maelekezo ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kurejesha sehemu ya mapato yanayotokana na sekta ya madini katika maendeleo ya sekta hiyo, ambapo asilimia 10 ya makusanyo ya sekta itaelekezwa kwenye shughuli za utafiti wa madini.
Amesema hatua hiyo itaiwezesha Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) kufanya tafiti zaidi za kijiolojia, kuongeza upatikanaji wa taarifa za kisayansi kuhusu maeneo yenye madini na kuwasaidia wachimbaji wadogo kufanya uwekezaji wenye tija.
"Utafiti ni msingi wa mafanikio ya sekta ya madini. Tunataka wachimbaji wetu waondokane na uchimbaji wa kubahatisha na badala yake watumie taarifa sahihi za kijiolojia zitakazoongeza uzalishaji, kupunguza hasara na kuongeza kipato chao," amesema.
Ameongeza kuwa uwekezaji katika tafiti za madini utaongeza ugunduzi wa maeneo mapya yenye rasilimali, kuchochea uwekezaji, kuongeza ajira na kuimarisha mchango wa sekta ya madini katika Pato la Taifa.
Dkt. Kiruswa amesema Serikali kupitia Wizara ya Madini inatekeleza Programu ya Mining For A Brighter Tomorrow (MBT), inayowalenga wachimbaji wadogo, wanawake, vijana na watu wenye mahitaji maalum ili washiriki kikamilifu katika shughuli za utafiti, uchimbaji, uchakataji, uongezaji thamani na biashara ya madini.
Kutokana na fursa hizo, amewahamasisha wananchi wa Kijiji cha Mundarara kuunda vikundi na kujiandikisha katika programu hiyo ili kunufaika na mafunzo, teknolojia, mitaji na fursa mbalimbali zinazotolewa na Serikali kwa ajili ya kukuza shughuli za madini.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyabiashara wa Madini Tanzania (CHAMMATA), Jeremiah Kituyo, amesema uchaguzi wa mabroka katika ngazi ya wilaya utasimamiwa na viongozi wa mkoa kwa mujibu wa Katiba na mwongozo wa chama.
Amesema mwanachama atakayeshiriki uchaguzi atalazimika kuwa na kitambulisho hai cha chama pamoja na leseni halali ya biashara ya madini, huku akibainisha kuwa viongozi wa masoko ya madini na vituo vya ununuzi huchaguliwa kila mwaka ili kuimarisha uwajibikaji, uwazi na uwakilishi wa wadau wa sekta hiyo.
Kituyo amesema chama kitaendelea kushirikiana na Wizara ya Madini kuhakikisha uchaguzi huo unafanyika kwa amani, uwazi na kuzingatia sheria, hatua itakayochangia kuimarisha mazingira ya biashara ya madini nchini.