Na OWM - TAMISEMI, Lushoto
Mhe. Alhaji Dkt. Hussein Mwinyi, Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Zanzibar, amekubali ombi la Mbunge wa Jimbo la Lushoto Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, kwa kutoa mchango wa Shilingi Milioni 200 kwa ajili ya kuendeleza Kituo cha Elimu ya Kiislamu Irshaad (Irshaad Islamic Centre) kilichopo Lushoto, mkoani Tanga.
Fedha hizo zinatarajiwa kuwezesha utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo katika kituo hicho, ikiwemo kuboresha Chuo cha Ufundi, kuanzisha bustani ya kisasa, kujenga madrasa yenye kukidhi mahitaji ya wanafunzi, kujenga nyumba za walimu, jengo la kupokelea wageni, hospitali pamoja na ukumbi wa kisasa wa kufanyia shughuli mbalimbali za kielimu na kijamii.
Prof. Shemdoe alitoa ombi hilo Julai 5, 2026 wakati wa Sherehe ya Maulidi ya Kumswalia Mtume Muhammad S.A.W iliyoandaliwa na Sheikh Sharrif Hussein Ahmad Badawiyy wa Kituo cha Irshaad Islamic Centre Lushoto, ambapo Mgeni Rasmi alikuwa Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi.
Katika hatua nyingine, Mhe. Rais Dkt. Hussein Mwinyi amekubali ombi la Rais wa Kituo cha Irshaad Islamic Centre Lushoto Sheikh Sharrif Hussein Ahmad Badawiyy la kumwomba awe mlezi wa kituo hicho, ambapo Mhe. Dkt. Dkt. Hussein Mwinyi ameahidi kuendelea kushirikiana na viongozi pamoja na wadau mbalimbali katika kukiendeleza ili kiwe kitovu cha utoaji wa elimu bora na maadili mema.
Sanjari na hilo, Mhe. Rais Dkt. Mwinyi ameridhia pia ombi la Rais wa Kituo hicho cha Irshaad Islamic Centre la kumtaka kuridhia jina la Hayati Alhaji Ali Hassan Mwinyi, litumike katika eneo la bustani linalotarajiwa kujengwa katika Chuo cha Ufundi kilichopo ndani ya kituo hicho, ikiwa ni sehemu ya kumuenzi na kutambua mchango wa maendeleo alioutoa Hayati Alhaji Ali Hassan Mwinyi akiwa ni mlezi wa kituo hicho.
Mhe. Prof. Shemdoe alimuunga mkono Mhe. Rais Dkt. Hussein Mwinyi kwa kuchangia Shilingi Milioni 20, Mkuu wa Mkoa wa Tanga Dkt. Batilda Burian Milioni 5, Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mhe. Adam Malima Milioni 5, Mbunge wa Bumbuli Mhe. Mhandisi Ramadhani Hamza Milioni 5, Mwenyekiti wa CCM Mkoa Bw. Rajab Abdallah Milioni 3 na Mbunge wa Afrika Mashariki Mhe. Dkt. Abdullah Makame amechanga Milioni 5 na kufanya jumla ya fedha zilichangwa kuwa Milioni 248, hatua iliyoonyesha mshikamano wa viongozi hao katika kuunga mkono maendeleo ya elimu na ustawi wa jamii.
Akizungumza mara baada ya hafla hiyo, Mhe. Prof. Shemdoe amemshukuru Mhe. Rais Dkt. Mwinyi kwa kukubali ombi hilo, akieleza kuwa msaada huo utakuwa chachu ya kuinua viwango vya elimu, ustawi wa jamii na huduma zinazotolewa katika kituo hicho, ambacho kimeendelea kuwa nguzo muhimu ya malezi na elimu kwa vijana wa Lushoto na maeneo jirani.
Aidha, Wananchi na viongozi waliohudhuria hafla hiyo wamempongeza Mhe. Rais Dkt. Mwinyi kwa kukubali maombi yaliyowasilishwa na Mhe. Prof. Shemdoe, wakieleza kuwa uamuzi huo utaacha alama ya kudumu katika maendeleo ya Kituo cha Elimu ya Kiislamu Irshad Lushoto na kuongeza fursa za elimu, ujuzi na huduma za kijamii kwa vizazi vya sasa na vijavyo.






















































