Na Oscar Assenga,TANGA

Uzinduzi wa Kamati ya Ushauri wa Masuala ya Kisheria ngazi ya Mkoa itaanza Machi 9 hadi 15 katika viwanja vya Tangamano Jiji Tanga huku Jopo Mawakili wa Serikali 40 wanatarajiwa kusikiliza kero sugu za kisheria ambazo zitatolewa ufafanuzi wa kisheria na hatimaye kufungwa na hatimaye kuweza kuzimaliza.

Hayo yalisemwa na Mkuu wa Mkoa wa Tanga Balozi,Batilda Burian wakati akieleza kuhusu uzinduzi wa Kamati ya Ushauri wa Masuala ya Kisheria ngazi wa Mkoa Bila Malipo itakayofanyika kwenye viwanja vya Tangamano Jijini Tanga ikianza Machi 9 hadi 15 mwaka huu huku akiwataka wananchi wote .

Alisema kamati hizo zinalenga kutoka huduma kwa wananchi na watuumishi wa umma ,viongozi wa umma na wengine bila kubagua ili kutatua changamoto za kisheria zinazojitokeza huku akieleza itasadia kupunguza mashauri au migogoro dhidi ya Serikali katika ngazi ya mikoa na wilaya.

“Lakini kama mtakumbuka Rais Dkt Samia Suluhu alituma jopo la wanasheria kutoa Wizara ya sheria wakiongozwa na Waziri kwa ajili ya kuzindua kliniki za sheria mkoa lakini ofisi ya Mwanasheria mkuu wa Serikali alituma jopo la wanasheria kutoka ofisi yake na waliopo kwenye mikoa kushirikiana na wanasheria wengine wa kujitolea hapa Tanga”Alisema .

“Kama mtakumbuka hivi karibuni Waziri Mkuu alianza ziara ameenda Arusha na Manyara migiogoro ni mingi wenzetu hawa wamekuja kusaidia kutoa  suluhu za kisheria na kuwasaidia wananchi na zitakutanaisha mawakili wa serikali na taasisi mbalimbali kuwasaidia wananchi wenye changamoto mbalimbali”Alisema

Hata hivyo alisema kwamba huduma hiyo itawezesha kupunguza malalamiko kwa wananchi na hata jopo hilo likiondoka utaratibu huo utaendelea na zoezi hilo  litafanyika bila malipo kwa hiyo wananchi wajitokeze kwa wingi wenye malalamiko ikiwemo mabando yenye malalamiko yawabebe na yawe na vielelezo vya kutosha.

Alieleza kwamba hiyo yote ni ni muendelezo wa kazi nzuri anayoifanya Rais Dkt Samia Suluhu  na wanaendelea kumpongeza kuweza kulinda,kukuza na kutetea haki za wananchi wanyonge na kupinga vitendo vya uvunjifu wa haki za binadamu na misingi ya utawala bora na kuhakikisha ukatili wa kijinsia unatokomezwa.

Mkuu huyo wa mkoa alisema pia  lakini kuheshimu utawala wa sharia ambao ndio msingi wa maendeleo kwenye mkoa huo wanaendeela kupongeza Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kuhakikisha kamati ya ushauiri wa kisheria kwenye mkoa wa Tanga inazinduliwa na kuanza kutioa huduma kwa wananchi wote bila kujali uwezo wao wa kifedha .



Mwisho.

Mkutano Mkuu wa 12 wa Umoja wa Maafisa Elimu wa Mikoa na Halmashauri Tanzania Bara (REDEOA) umeendelea kufanyika jijini Arusha kwa siku saba tangu ulipofunguliwa rasmi Machi 2, 2026 na Waziri wa Ofisi ya Rais – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Profesa Riziki Shemdoe.
Wanawake wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC), Dar es Salam  wametembelea Gereza la Segerea na kutoa misaada mbalimbali kwa wafungwa, ikiwa ni sehemu ya kuelekea Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yanayoadhimishwa kila mwaka Machi 8.
Ziara hiyo pia imekuwa muendelezo wa maadhimisho ya miaka 25 ya chuo hicho, ambapo taasisi imekuwa ikitekeleza shughuli za kurejesha kwa jamii kupitia matendo ya kijamii na misaada kwa makundi yenye uhitaji.
Akizungumza wakati wa kukabidhi misaada hiyo, Zena Hussein, Meneja wa Sehemu ya Mafunzo kwa Njia ya Mtandao TPSC, aliyemwakilisha Mkuu wa Chuo, amesema wanamshukuru Mkuu wa  chuo kwa kuwawezesha kutekeleza jukumu hilo la kijamii, akieleza kuwa lengo ni kuonyesha upendo na mshikamano kwa wafungwa kama sehemu ya jamii.
Amesema kuwa, kama wanawake wafanyakazi wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania, wameona umuhimu wa kutambua kundi hilo na kujitoa kwa moyo wa huruma wakiamini kuwa si kila aliyepo gerezani ni mkosaji wa kukusudia, bali baadhi yao wamejikuta katika mazingira magumu yasiyotegemewa. Ameongeza kuwa misingi ya dini, kwa Waislamu na Wakristo, inahimiza kusaidia wahitaji na kuwa watoaji, hivyo wameamua kupeleka kile walichoweza kumudu.
Miongoni mwa misaada iliyotolewa ni sukari, mchele, unga, maharage, maji, dawa za usafi, khanga, mashuka ya watoto, ndala, mifagio, dawa za meno, mafuta ya kupaka, pedi za wanawake, nepi za watoto, maziwa ya watoto, vitabu vya dini ikiwemo Qur’an na Biblia pamoja na nguo.
Kwa upande wake, Mkuu wa Gereza la Wanawake Segerea, SSP Hamida Mussa Matimba, ameishukuru TPSC kwa msaada huo akisema vitabu vya dini vitakuwa nguzo muhimu katika kuwajenga wafungwa kiimani na kuwasaidia katika mchakato wa mabadiliko chanya.
Alieleza kuwa gereza hilo linaendesha programu mbalimbali za mafunzo ya ufundi stadi ikiwemo ushonaji, upishi, ufyatuaji wa matofali, ujenzi, ufundi magari na umeme, akisisitiza kuwa lengo ni kuhakikisha kila anayeingia gerezani anatoka akiwa na mabadiliko chanya ya kiimani, kimaadili na kiujuzi ili aweze kujitegemea anaporejea uraiani.
Aidha, aliwahimiza wanawake kuwa na moyo wa kusamehe ili kupunguza migogoro inayoweza kuishia kwenye vyombo vya sheria, akitolea mfano wa migogoro ya madeni katika vikundi vya mikopo. Pia alitoa wito kwa wazazi kuwalea vijana, hususan mabinti, katika misingi ya maadili na kuwajenga kuridhika ili kuepuka tamaa zinazoweza kuwaingiza katika matatizo ya kisheria.
Kaulimbiu ya Siku ya Wanawake Duniani mwaka 2026 inasema: “Haki na usawa kwa wanawake na wasichana ni msingi jumuishi kufikia Dira 2050.” Ziara hiyo imeakisi dhamira ya wanawake wa TPSC ya kuadhimisha siku hiyo kwa vitendo vinavyogusa jamii moja kwa moja
Meneja wa Sehemu ya Mafunzo kwa Njia ya Mtandao TPSC,Zena Hussein (kushoto) akikabidhi
Meneja wa Sehemu ya Mafunzo kwa Njia ya Mtandao TPSC,Zena Hussein akizungmza wakati kukabidhi misaada huo.
Mkuu wa Gereza la Wanawake Segerea, SSP Hamida Mussa Matimba akizungumza  wakati wa kukabidhi misaada huo. 
 
 

Kauli Mbiu ya Mwaka 2026:

“Medicinal and Aromatic Plants and Their Contribution to Human Welfare: The Way Forward for Sustainable Use”

(“Mimea ya Dawa na Harufu na Mchango Wake kwa Ustawi wa Binadamu: Njia ya Mbele ya Matumizi Endelevu”)

Kwa niaba ya Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira (TRAMEPRO), tunaungana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kupitia Tanzania Wildlife Management Authority (TAWA), pamoja na wadau wote wa uhifadhi wa mazingira, vyombo vya habari, na watabibu asili nchini kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Wanyamapori tarehe 03 Machi 2026. Aidha, tunaungana na mataifa mengine duniani kusherehekea siku hii muhimu inayotukumbusha wajibu wetu wa kulinda urithi wa asili kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Maadhimisho ya mwaka huu yanatukumbusha umuhimu wa kulinda na kutumia kwa busara rasilimali za asili, hususan mimea ya dawa na harufu, ambayo imekuwa nguzo muhimu katika afya ya jamii, ukuaji wa uchumi wa taifa, na ustawi wa binadamu kwa ujumla. Mimea hii si tu hazina ya tiba asilia bali pia ni rasilimali yenye mchango mkubwa katika tafiti za kisayansi, viwanda vya dawa, na maendeleo ya kijamii.

Tanzania imebarikiwa kuwa na bioanuwai adhimu ya wanyamapori, misitu, na vyanzo vya maji. Rasilimali hizi ni urithi wa taifa letu na msingi wa maendeleo endelevu. Hivyo basi, tunapaswa kushirikiana kwa dhati katika:

• Kulinda wanyamapori dhidi ya ujangili na uharibifu wa makazi yao.

• Kuhifadhi mimea ya tiba kwa matumizi endelevu yasiyoharibu mazingira.

• Kulinda vyanzo vya maji na mifumo ya ikolojia kwa manufaa ya sasa na vizazi vijavyo.

• Kuwezesha jamii kushiriki kikamilifu katika shughuli za uhifadhi na kunufaika nazo kiuchumi.

Tukiongozwa na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025–2050 inayolenga kujenga taifa lenye uchumi imara, amani, utulivu na maendeleo endelevu ya watu wake, tunasisitiza kuwa:

“Uhifadhi wa rasilimali za asili ni msingi wa ustawi wa taifa na kizazi kijacho.”

Kwa pamoja, tushikamane kulinda urithi wetu wa asili, kuenzi thamani ya mimea ya dawa, na kuhakikisha matumizi yake yanafanyika kwa njia endelevu kwa manufaa ya binadamu na mazingira.

TUSHIRIKIANE KWA UHIFADHI, USTAWI NA MAENDELEO ENDELEVU 

Imetolewa na: Boniventura Mwalongo

Katibu Mkuu Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira (TRAMEPRO)

Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA), yatakiwa kuongeza kasi ya urasimishaji wa biashara na kuimarisha mifumo ya kidijitali ili kuchochea ufanisi na ukuaji wa uchumi kwani BRELA ni lango kuu la uwekezaji nchini.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Judith Kapinga (Mb), Machi 04, 2026, wakati akifungua Baraza la wafanyakazi la BRELA na kuhimiza uwekezaji kwenye rasilimali watu, akitaka watumishi wapewe mafunzo na stahiki zao kwani ustawi wa wafanyakazi ndio siri ya mafanikio ya taasisi, na kuwataka watumishi kufanya kazi kwa uadilifu, weledi, na uzalendo.

Waziri Kapinga amebainisha kuwa kwa mujibu wa tafiti mbalimbali za wadau, zaidi ya 80% ya biashara nchini zipo sekta isiyo rasmi, hivyo BRELA lazima iwe kinara wa kuzirasimisha, hatua ambayo itawawezesha Wajasiriamali wadogo kupata mikopo, masoko, na ulinzi wa kisheria.

Aidha, ameagiza kuhuisha mifumo ya TEHAMA ili iwe rafiki itakayopunguza gharama pamoja na muda wa mteja kupata huduma na kusisitiza kuwa mifumo hiyo lazima iwe na usalama wa taarifa wa hali ya juu na itumike kupata mrejesho wa haraka kutoka kwa wateja ili kuboresha utendaji.

Aidha, ameipongeza BRELA kwa ongezeko la usajili na makusanyo, akisisitiza kuwa Serikali itaendelea kuweka mazingira wezeshi kwa wafanyakazi na kuitaka taasisi hiyo kugeukia mfumo wa uwezeshaji badala ya udhibiti pekee ili kukuza sekta binafsi nchini.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa BRELA Bw. Godfrey Nyaisa amebainisha kuwa BRELA imevuka lengo la mapato kwa asilimia 105 na kutekeleza malengo kwa asilimia 78 katika nusu mwaka wa 2025/26, ambapo taasisi hiyo imewasilisha Shilingi bilioni 3.1 kwa Msajili wa Hazina, na kusema mafanikio hayo yanayotokana na mshikamano, kujituma na bidii ya watumishi.

Vilevile, amewasilisha Mpango Mkakati wa 2026–2031 unaolenga kuboresha za usajili na miundombinu, ikiwemo ujenzi wa ofisi za Dodoma na Kinondoni na kubainisha kuwa uongozi unaendelea kuimarisha maslahi ya watumishi kupitia muundo mpya wa mishahara na motisha ili kutatua changamoto za uhaba wa wafanyakazi na kuongeza tija.

 

Wananchi wa Kata ya Oldonyosambu, wilayani Ngorongoro, wameishukuru Serikali kwa kuwajengea daraja la mawe lenye urefu wa mita 45 katika Mto Mbaga linalounganisha vijiji vya Jema na Oldonyosambu.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti wananchi hao walisema kukamilika kwa daraja hilo kumewaondolea changamoto ya muda mrefu ya usafirishaji wa mazao na upatikanaji wa huduma za kijamii hususan katika kipindi cha masika.

Diwani wa Kata ya Oldonyosambu, Mhe. Kabaney Mojah, amesema kabla ya ujenzi wa daraja hilo, wakazi wa eneo hilo walikumbwa na matatizo makubwa ya mawasiliano na usafirishaji wa mazao kutoka Kijiji cha Jema ambako kuna shughuli za kilimo.

“Kijiji cha Jema ni eneo letu kuu la uzalishaji mazao. Hapo awali tulikuwa na changamoto kubwa ya kusafirisha mazao kwenda soko la Arusha pamoja na mawasiliano kati ya vijiji hivi viwili. Tunaishukuru Serikali kwa kutatua tatizo hili,” alisema Mhe. Mojah.

Aliongeza kuwa Mto Mbaga ulikuwa kikwazo kikubwa, hasa nyakati za mvua, hali iliyosababisha usumbufu hata katika masuala ya dharura.

“Mto Mbaga ni mto korofi, zamani wakati wa masika wananchi hawakuweza kuvuka kabisa. Sasa tunaweza hata kuwasafirisha wanafunzi wanaougua kutoka Shule ya Sekondari Jema hadi Hospitali ya Wilaya iliyopo Wasso bila hofu,” amesisitiza.

Naye,  mkazi wa eneo hilo Bw. Likam Maroseck amesema  kabla ya daraja kujengwa, baadhi ya wananchi walikumbwa na hatari ya kusombwa na maji walipokuwa wakivuka kwenda kulima mashamba yao kijijini Jema.

“Ujenzi wa daraja hili umeleta ahueni kubwa. Kwa sasa shughuli zetu zinafanyika kwa urahisi na usalama zaidi,” amesema.

Kwa upande wake, Kaimu Meneja wa TARURA Wilaya ya Ngorongoro, Mhandisi Edwin Merdad, amesema kuwa katika mwaka wa fedha 2023/2024, walitenga bajeti ya shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa daraja hilo pamoja na uboreshaji wa barabara inayounganisha vijiji hivyo.

Amesema pamoja na mpango wa awali wa kuchonga na kuweka kifusi kwenye barabara yenye urefu wa kilomita tano, wamefanikiwa kujenga barabara yenye urefu wa kilomita 14 kati ya vijiji hivyo viwili.

“Daraja hili ni msaada mkubwa si tu kwa wakazi wa Oldonyosambu na Jema, bali pia kwa wafanyabiashara kutoka nchi jirani ya Kenya wanaoshiriki katika shughuli za minada. 

“Zamani wakati wa masika wananchi walishindwa kuvuka kwa takribani miezi miwili, lakini sasa hali hiyo imekuwa historia,” amesema Mhandisi Merdad.

Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro ina mtandao wa barabara wenye jumla ya kilomita 970.698, zikiwemo barabara za zege kilomita 0.224, barabara za changarawe kilomita 306.41 na barabara za udongo kilomita 664.064.











 


Anajulikana kwa jina la Utani Profesa kutokana na uwezo mkubwa wa kujua vitu vingi katika hifadhi ya Ngorongoro katika utumishi wake wa miaka 34, ni mwanamke shupavu kuelekea siku ya wanawake tarehe 8 Machi, 2026

Tukio la kusisimua na hatari katika maisha yake ni tarehe 6 Machi 2020 Kreta ya Ngorongoro kwenye utekelezaji wa majukumu yake, ghafla Faru akamkimbiza bila yeye kujua ambapo alijaribu kutumia mbinu za medani alizofundishwa jeshini kujinasua lakini bahati mbaya alishambuliwa ingawa baadaye aliweza kuokolewa na kukimbizwa hospitali kwa matibabu.

Kamanda huyu wa Uhifadhi anaadhimisha siku ya wanawake duniani akiendelea kuchapa kazi na mara nyingi utamkuta kreta akifanya shughuli za uhifadhi, utafiti, sensa za wanyamapori na kupambana na mimea vamizi bila woga.

Ngorongoro tunampa maua yake kwa kuwa uzoefu ni mama wa Maarifa hivyo yeye kama Chanda chema tunamvika Pete anapotimiza miaka 6 ya tukio la Faru.

 

Na Mwandishi Wetu

KATIKA kuelekea kilele cha maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani, Halmashauri ya Mji Handeni imejipanga kutekeleza shughuli mbalimbali ikiwamo uzinduzi wa Jukwaa la Uwezeshaji Wanawake Kiuchumi.

Akizungumza kuhusu maandalizi ya maadhimisho hayo, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Handeni, Maryam Ukwaju, amesema halmashauri hiyo inatambua na kuthamini mchango mkubwa wa wanawake katika maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla.

Amesema Machi 5, 2026 kutafanyika kongamano la wanawake litakaloenda sambamba na uzinduzi wa Jukwaa la Uwezeshaji Wanawake Kiuchumi la Halmashauri ya Mji Handeni, linalolenga kuwaunganisha wanawake ili kubadilishana uzoefu, kupata taarifa za fursa za kiuchumi na kuimarisha shughuli zao za ujasiriamali.

Ukwaju amesema kongamano hilo pia litaambatana na maonesho ya bidhaa mbalimbali zinazozalishwa na wanawake wajasiriamali, hatua inayolenga kuonesha ubunifu wao pamoja na juhudi wanazofanya katika kujikwamua kiuchumi.

Ameongeza kuwa katika kongamano hilo litakalofanyika katika ukumbi wa CCM Wilaya ya Handeni, washiriki watapatiwa elimu mbalimbali ikiwemo masuala ya umiliki wa ardhi na mirathi, malezi na makuzi ya watoto, ujasiriamali na biashara, elimu ya ushirika na SACCOS pamoja na kilimo bora na ufugaji wa kisasa.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi huyo, Machi 6, 2026 halmashauri itatoa msaada kwa baadhi ya kaya zinazoishi katika mazingira hatarishi ikiwa ni sehemu ya kuonesha mshikamano na kusaidia jamii zenye uhitaji.

Kadhalika amesema kilele cha maadhimisho hayo kwa ngazi ya Halmashauri kitafanyika Machi 7, 2026 katika viwanja vya Shule ya Msingi Kwenjugo, ambapo kutafanyika ugawaji wa taulo za kike kwa wanafunzi wa kike pamoja na utoaji wa vyeti kwa vikundi vinne vya wanawake vilivyotekeleza miradi yao kwa mafanikio na kurejesha mikopo ya asilimia 10 kwa wakati. Amesema mgeni rasmi katika shughuli hizo anatarajiwa kuwa Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese.

Ukwaju amesema maadhimisho hayo yanaongozwa na kaulimbiu isemayo “Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana; Msingi Jumuishi kufikia Dira 2050,” huku halmashauri ikiendelea kuhamasisha wananchi wote kushiriki kikamilifu katika kuimarisha usawa wa kijinsia na kuchochea maendeleo jumuishi kwa wanawake na wasichana.