Airtel Tanzania imezindua minara miwili mipya ya mawasiliano ya 4G inayotumia umeme wa gridi ya taifa katika mikoa ya Geita na Dodoma, hatua inayotarajiwa kuboresha upatikanaji wa simu na intaneti kwa maelfu ya wananchi wa maeneo ambayo kwa muda mrefu yamekosa mawasiliano ya uhakika.
Minara hiyo imejengwa katika Kata ya Nyaruyeye, Wilaya ya Geita, na Kijiji cha Chinagali, Kata ya Zoissa, Wilaya ya Kongwa, Mkoa wa Dodoma, ikiwa na lengo la kuboresha mawasiliano, huduma za intaneti na huduma za kifedha kupitia simu kwa jamii zilizokuwa zikikabiliwa na changamoto za mtandao kwa miaka mingi.
Tofauti na minara mingine ya vijijini inayotegemea majenereta, minara hiyo imeunganishwa na umeme wa gridi ya taifa huku ikiwa na majenereta ya akiba, hatua inayopunguza gharama za uendeshaji na kuchangia uhifadhi wa mazingira kupitia kupunguza matumizi ya mafuta.
Katika Kata ya Nyaruyeye, zaidi ya wananchi 15,000 pamoja na wakazi wa Kata ya Nyarugusu na maeneo jirani wanatarajiwa kunufaika na maboresho hayo.
Uwekezaji huo unafuatia tathmini iliyofanywa na Airtel baada ya kupokea malalamiko ya wananchi kuhusu changamoto za upatikanaji wa huduma za mawasiliano katika maeneo hayo.
Hatua hiyo inalenga kuimarisha mawasiliano, kuongeza ujumuishaji wa kifedha na kufungua fursa za kidijitali kwa jamii.
Viongozi wa maeneo husika wamesema minara hiyo itasaidia shughuli za elimu, biashara na utoaji wa huduma za umma, pamoja na kuchochea shughuli za kiuchumi, hususan katika maeneo yanayojishughulisha na kilimo na ufugaji kama Wilaya ya Kongwa.
Airtel imesema uwekezaji huo ni sehemu ya mkakati wake wa kuhakikisha wananchi wa vijijini wanapata fursa sawa katika uchumi wa kidijitali kupitia upatikanaji wa miundombinu ya mawasiliano ya uhakika
Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limesisitiza ushirikiano wa wadau wote wakiwemo Serikali, Sekta binafsi, taasisi za umma, jamii na wananchi katika kusimamia na kuhifadhi mazingira kwa maendeleo endelevu.
Akizungumza na waandishi wa habari tarehe 17 Juni, 2026 katika ukumbi wa mikutano wa NEMC Jijini Dar es salaam, Kaimu Meneja Uhusiano na Mawasiliano kwa Umma NEMC, Bi. Martha Kawishe, amesema mazingira ni suala mtambuka linalohitaji kila mdau kutimiza wajibu wake kwa kuzingatia Sheria na Miongozo ya Mazingira iliyowekwa.
Ameeleza kuwa NEMC inaendelea kusimamia utekelezaji wa Sheria kupitia ukaguzi wa miradi, utoaji wa elimu kwa umma katika masuala mazima ya udhibiti wa kelele chafuzi za mazingira, uharibifu wa vyanzo vya maji, utupaji holela wa taka, kutiririsha maji taka msimu wa mvua, ukataji hovyo wa miti na kuhakikisha miradi yote inazingatia Tathmini ya Athari kwa Mazingira (TAM) kabla ya kuanza.
Aidha, amewataka wananchi kuwa makini na watu wanaojifanya maafisa wa NEMC kwa lengo la udanganyifu, akisisitiza kuwa malipo yote hufanyika kwa utaratibu wa kiserakili na ukaguzi hufanywa na maafisa kisheria wakiwa na vithibitsho vifuatavyo: vitambulisho vya ukaguzi, vitambulisho vya kazi pamoja na nyaraka zinazompa mamlaka kisheria ya kufanya ukaguzi, na hasa ikizingatiwa ukaguzi hufanywa kidigitali ambapo mteja hupokea ujumbe mara baada ya ukaguzi.
NEMC pia imehimiza wananchi kutumia huduma rasmi ya kituo cha huduma kwa mteja kwa kupiga namba ya bure 0800110115 na kutumia mfumo wa e-mrejesho kwa kufuata menyu ya *152*00# na kufuata maelekezo ili kutoa ushauri, taarifa au changamoto za kimazingira.
DAR ES SALAAM:
Mabadiliko yanayoendelea kufanyika katika mpango wa Marekani wa Food for Peace yameibua mjadala muhimu ambao Afrika haiwezi tena kuupuuza: utegemezi wa muda mrefu wa misaada ya chakula kutoka nje ya bara.
Kwa zaidi ya miongo saba, mpango huo umekuwa miongoni mwa vyanzo vikubwa vya msaada wa chakula kwa mataifa yanayokabiliwa na njaa, migogoro na majanga ya kibinadamu. Hata hivyo, taarifa za hivi karibuni zinaonyesha kuwa mwelekeo wa mpango huo unabadilika, huku ukihusishwa zaidi na maslahi ya kilimo na biashara ya Marekani kuliko malengo ya kibinadamu pekee.
Kwa Afrika, suala hili linapaswa kutazamwa kama tahadhari badala ya mgogoro. Linaonesha jinsi usalama wa chakula wa bara unavyoweza kuathiriwa na maamuzi yanayofanyika nje ya mipaka yake.
Kwa miaka mingi, mataifa mengi ya Afrika yamekuwa yakitegemea misaada ya chakula wakati wa ukame, migogoro au misukosuko ya kiuchumi. Ingawa misaada hiyo imeokoa maisha ya mamilioni ya watu, imeacha swali muhimu: Je, usalama wa chakula wa Afrika unaweza kuendelea kutegemea sera zinazobadilika kulingana na vipaumbele vya mataifa wafadhili?
Jibu linaonekana kuwa hapana.
Hoja hii inaendana na mjadala mpana unaoendelea kuhusu uhuru wa kiuchumi wa Afrika. Wanasiasa, wachambuzi na wanazuoni wengi wa Kiafrika wamekuwa wakisisitiza kuwa uhuru wa kisiasa hauwezi kuwa kamili bila uwezo wa bara kujitegemea kiuchumi.
Mgombea urais wa Tanzania kupitia chama cha ADC, Doyo Hassan Doyo, hivi karibuni alieleza kuwa Afrika inapaswa kuimarisha mifumo yake ya ndani badala ya kutegemea sana taasisi za kimataifa. Akizungumzia nafasi ya bara katika mfumo wa dunia, alisema lengo si kujitenga na mataifa mengine bali kuhakikisha usawa katika mahusiano ya kimataifa.
“Lengo si kujitenga, bali ni kuwa na uwiano,” alisema.
Kauli hiyo inaweza kutumika pia katika mjadala wa usalama wa chakula. Kadri nchi za wafadhili zinavyobadilisha sera zao kulingana na mahitaji ya ndani, ndivyo hatari ya Afrika kubaki katika mazingira ya kutegemea maamuzi ya wengine inavyoongezeka.
Wakati huo huo, Afrika ina rasilimali nyingi zinazoweza kuiwezesha kujitosheleza kwa chakula. Bara lina sehemu kubwa ya ardhi inayofaa kwa kilimo ambayo bado haijatumika kikamilifu, vyanzo vikubwa vya maji pamoja na nguvu kazi inayoongezeka kwa kasi.
Hata hivyo, changamoto zinaendelea kujitokeza katika maeneo ya umwagiliaji, uhifadhi wa mazao, usafirishaji na uchakataji wa bidhaa za kilimo. Kiasi kikubwa cha mazao hupotea baada ya kuvunwa huku baadhi ya nchi zikiendelea kuagiza chakula kutoka nje.
Hali hii inaonesha kuwa tatizo si ukosefu wa rasilimali, bali ni namna ya kuzitumia kwa ufanisi.
Eneo la Biashara Huria la Afrika (AfCFTA) linaweza kuwa sehemu ya suluhisho. Kupitia ushirikiano wa kikanda, nchi za Afrika zinaweza kurahisisha biashara ya mazao ya kilimo na kuhakikisha maeneo yenye ziada ya chakula yanasaidia yale yanayokabiliwa na upungufu.
Lakini mafanikio hayo hayawezi kupatikana bila taasisi imara za ndani.
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk. Lupa Ramadhani, anaamini kuwa uimara wa mifumo ya utawala ni msingi muhimu wa kujenga uhuru wa kweli wa Afrika.
“Kushindwa kuchukua hatua ndani ya nchi kunakaribisha uangalizi kutoka nje,” amesema.
Kauli hiyo inaakisi hali ilivyo katika sekta ya chakula. Pale ambapo sera za kilimo hazitekelezwi ipasavyo, uwekezaji ni mdogo au taasisi zinashindwa kutimiza wajibu wake, utegemezi wa misaada kutoka nje huongezeka.
Katika kipindi ambacho dunia inashuhudia mabadiliko ya kisiasa na kiuchumi, pamoja na kuongezeka kwa ushindani wa kijiografia kati ya mataifa makubwa, Afrika inalazimika kufikiria upya mkakati wake wa maendeleo.
Hii haimaanishi kukataa ushirikiano wa kimataifa. Misaada ya kibinadamu itaendelea kuwa muhimu wakati wa majanga na dharura. Hata hivyo, ushirikiano huo unapaswa kuimarisha vipaumbele vya Afrika badala ya kuvibadilisha.
Mustakabali wa usalama wa chakula wa bara hautaamuliwa Washington, Brussels au katika miji mingine ya dunia. Utaamuliwa na maamuzi yatakayofanywa katika miji mikuu ya Afrika kuhusu uwekezaji katika kilimo, miundombinu, biashara ya kikanda na taasisi za umma.
Mjadala kuhusu Food for Peace ni zaidi ya mjadala wa misaada. Ni ukumbusho kwamba uhuru wa kweli unahitaji uwezo wa kulisha wananchi wako mwenyewe. Kwa Afrika, huo si uchaguzi wa kisera pekee, bali ni hitaji la kimkakati kwa mustakabali wa bara.
Mwenza wa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama Neema Mwigulu Nchemba, amehimiza Taasisi za umma na binafsi kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuboresha huduma za kijamii kupitia utekelezaji wa programu za uwajibikaji kwa jamii (CSR).
Ameyasema hayo, Juni 16, 2026 katika hafla ya kukabidhi vifaa vya hospitali vilivyotolewa na Shirika la Viwango Tanzania (TBS) katika Hospitali ya Wilaya ya Chamwino, Mkoa wa Dodoma, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 50 ya Shirika hill.
Aisha, Mama Neema ameishukuru, Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uwekezaji mkubwa katika sekta ya afya hususani katika ujenzi wa Hospitali, utoaji wa ajira kwa wataalamu wa atya, upatikanaji wa dawa na vifaa tiba pamoja na kuimarisha huduma za kibingwa na ubingwa bobezi ziliOrahisisha upatikanaji wa huduma bora za afya nchini.
Amesema vifaa hivyo vilivyotolewa vinajumuisha vitimwendo 20, vitanda vya kujifungulia vitano, vitanda vya kufanyia uchunguzi vitano, vitanda vitano vya kulaza wagonjwa, machela moja ya kisasa, makabati matatu ya kuhitadhia vitaa tiba pamoja na mabeseni yenye vifaa mbalimbali kwa ajili ya akinamama 30 waliojifungua vitasaidia vitasaidia kuboresha utoaji wa huduma katika Hospitali ya Wilaya ya Chamwino na kuongeza ustawi wa mama na mtoto.
Awali, akimkaribisha mgeni rasmi kuzungumza katika hafla hiyo, Waziri wa Viwanda na Blashara, Judith Kapinga amesema Serikali itaendelea kuhimiza taasisi zake kutekeleza kwa vitendo sera ya uwajibikaji kwa jamii ili kuchangia kuboresha huduma za kijamii na maisha ya wananchi.
Naye Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule, amesema Mkoa wake uko tayari katika kushirikiana na Wizara Pamoja na TBS kwa ujumla katika kuendeleza Sekta ya Viwanda na Biashara na jitihada za uwajibikaji kwa Jamii katika Mkoa wake.
Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya (TBS) Profesa Othman Chande na Mkurugenzi Mkuu wa TBS, Dkt. Ashura Katunzi wamesema TBS itaendelea kutekeleza sera yake ya kuwajibika kwa jamii (CSR Policy) ili kuendelea kuwa karibu na jamii katika kuleta tija na maendeleo.

Katika jamii ya Kimaasai, maisha ya mwanaume hupitia hatua mbalimbali za kimila zinazoonyesha ukuaji, Miongoni mwa hatua hizo muhimu ni kufanyiwa sherehe inayojulikana kwa jina la Orkiteng le Sirit ikimaanisha ni mwisho wa ujana na kuingia uzeeni.
Katika hatua hii ambapo mtu anatawazwa kuingia rika la uzee, wazee wa jamii hiyo huchagua Dume la rika ambalo lina afya njema na lililohasiwa tangu utoto wake, dume hili siku ya shughuli ndio hutolewa mwanzo kwenye boma lenye Ng’ombe wengi na kumwagiwa maziwa kisha hunyongwa hadi kufa.
Sherehe ya Orkiteng le Sirit , si sherehe ya kawaida bali ni tukio la heshima kubwa linalofanyika kwa kufuata mila na desturi za kale zilizorithishwa kutoka kizazi hadi kizazi. Kwa jamii ya Kimaasai, ni hatua ya ukamilifu wa mwanaume na uthibitisho kwamba ametimiza majukumu yake ya kifamilia na kijamii, kufanyiwa sherehe hii hakuangalii umri ila inazingatia jinsia kwa kuwa anayefanyiwa sherehe hii ni mwanaume pekee, vigezo vinavyoangaliwa ili mwanaume afanyiwe sherehe hii, ni lazima awe ameoa, awe na watoto wa kike na kiume na awe mtu mwema na maadili katika jamii.
Akizungumza wakati wa sherehe hiyo, Alaigwanani wa kabila la kimasai Maningo Rinjo amesema viongozi wa mila wa ukoo kama (Laizer, Mollel, Laitayo, Ngidong’i) ndio wenye jukumu la kumchagua dume atakayechinjwa baada ya kujiridhisha kuwa ana sifa zote zinazotakiwa kwa mujibu wa mila na desturi za Kimaasai ili kutekeleza jukumu hilo la kijamii ambalo linahudhuriwa na ndugu wote wa familia na jamii yote ya wamasai inayozunguka Kijiji hicho.
“Si kila dume anaruhusiwa kutumika katika sherehe hii, sisi viongozi wa mila hukagua na kuthibitisha sifa zake kabla ya kutoa ruhusa ya kuchinjwa, dume wa kutekeleza sherehe hii lazima awe amehasiwa tangu utotoni, hajawahi kumpanda dume jike, pembe zake ziwe zimenyooka bila kupinda mithili ya pembe za mbogo, asiwe mgonjwa na sifa zingine za ndani ambazo viongozi wa kimila ndio huzichunguza kwa undani,” alisema Alaigwanani Maningo Rinjo.
Alaigwanani Olonyori Lemoyan kutoka Ukoo wa Laizer Kata ya Nainokanoka Ngorongoro alisisitiza kuwa si kila mwanaume anastahili kufanya sherehe ya Orkiteng le Sirit, moja wa masharti muhimu ili mwanaume afanyiwe tukio hilo kuwa
na familia yenye watoto wa kike na kiume, awe na mali na uelekeo wa maisha, mtu anayejali watu na awe ni rafiki wa ukoo wake na jamii inayomzunguka pamoja na kupata ridhaa ya ukoo wake kufanya sherehe hiyo.
“Orkiteng le Sirit ni heshima kubwa katika jamii ya Kimaasai. Mwanaume lazima awe ametimiza wajibu wake wa kifamilia kwa kupata watoto wa kike na wa kiume. Bila kutimiza sharti hilo, hawezi kufikia hatua hii muhimu ya maisha,” alisema Alaigwanani Olonyori Lemoyan.
Wakati wa sherehe hizo baada ya dume kunyongwa na kutolewa nyama zake, mwanaume anayehitimu (anayepandishwa rika) pamoja na mke wake na mama yake mzazi wanatakiwa hukalia utumbo wa dume hilo kama ishara ya kuaga rasmi ujana na kuingia katika hatua ya uzee. Kitendo hicho hubeba maana kubwa ya kiutamaduni na kuashiria mwanzo wa jukumu jipya ndani ya jamii na kuachana na usharobaro na mambo yote ya ujana.
Baada ya taratibu hizo kukamilika, rika la Korianga huungana na mwenzao aliyeingia hatua ya uzee timilifu huimba nyimbo za furaha na heshima huku wakielekea bomani, wakimpongeza mwenzao kwa kufikia hatua hiyo adhimu. Nyimbo hizo huashiria kukubalika kwake rasmi katika kundi la wazee na kupewa nafasi ya kushiriki kikamilifu katika mila, desturi na maamuzi yanayohusu ustawi wa jamii.
Orkiteng le Sirit si tu sherehe ya kuchinja dume laa hasha, ni alama ya mafanikio ya maisha, uwajibikaji wa kifamilia na heshima ya kuwa mzee katika jamii ya Kimaasai. Hatua hii ni urithi wa kipekee unaoendelea kuunganisha vizazi na kuhifadhi utamaduni wenye thamani kubwa kwa jamii hiyo.
Waziri wa Nishati, Deogratius Ndejembi, amesema serikali imechukua hatua madhubuti kumaliza changamoto za kukatika kwa umeme zilizokuwa zikiathiri baadhi ya maeneo ya Wilaya ya Kongwa mkoani Dodoma, hali iliyokuwa ikisababisha wilaya nzima kukosa umeme pindi hitilafu zinapotokea kwenye baadhi ya sehemu za mtandao.
Ndejembi amebainisha hayo leo wakati wa uzinduzi wa Kituo cha Usambazaji Umeme (Switching Station) pamoja na transfoma mpya zilizojengwa kwa lengo la kuimarisha na kudhibiti mfumo wa usambazaji umeme katika wilaya hiyo.
Amesema uwepo wa miundombinu hiyo utasaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza changamoto ya mgao wa umeme wa ghafla, ambao hapo awali ulikuwa ukisababisha maeneo mengi ya Kongwa na wilaya jirani kuathirika pindi hitilafu inapotokea sehemu moja ya mfumo.
“Kwa muda mrefu, changamoto ya voltage ndogo na kukatika kwa umeme mara kwa mara ilikuwa kikwazo kikubwa kwa wananchi na wajasiriamali wadogo, hususan waliokuwa wakishindwa kuendesha shughuli za uzalishaji kama kusaga nafaka na kukamua mafuta kutokana na uhaba wa umeme wa uhakika,” amesema Ndejembi.
Ameongeza kuwa serikali, chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan, imeendelea kuliweka sekta ya nishati katika kipaumbele cha juu, hali iliyowezesha utekelezaji wa miradi mikubwa ya kimkakati inayolenga kuboresha maisha ya wananchi na kuchochea maendeleo ya kiuchumi.
Amesema zaidi ya shilingi bilioni 10 zimewekezwa katika eneo la Mbande kwa ajili ya ujenzi wa Switching Station hiyo, hatua ambayo itanufaisha wakazi wa wilaya za Kongwa, Kiteto, Gairo, Chamwino na Mpwapwa kwa kupata umeme wa uhakika na wa kutosha.
“Lengo letu siyo tu kuhakikisha wananchi wanapata umeme wa kuwasha taa, bali ni umeme wa kuendesha viwanda na shughuli za uzalishaji. Hii itasaidia kukuza uchumi wa maeneo haya na kuongeza fursa za ajira,” ameongeza.
Uzinduzi wa mradi huo unatajwa kuwa sehemu ya jitihada za serikali kuboresha miundombinu ya nishati nchini na kuhakikisha upatikanaji wa umeme wa uhakika unafika kwa wananchi wengi zaidi, hususan maeneo ya vijijini na pembezoni.
Na: OWM (KAM) – Dar es Salaam
Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kutoa fursa za ajira zenye tija kwa wananchi na suala hilo limekuwa kipaumbele cha kitaifa.
Hayo yamesemwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano ya Kazi, Mheshimiwa Deus Sangu, wakati akizindua Maonesho ya Ajira ya Tano (5) kati ya Tanzania na China yaliyofanyika katika viwanja vya Maktaba ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, leo Juni 16, 2026.
Aidha, Mheshimiwa Sangu amesema Serikali inatekeleza sera na programu zinazohamasisha viwanda, mafunzo ya ujuzi, ujasiriamali, ufanisi wa soko la ajira na kazi zenye staha kwa wote. Pia, amesema kupitia Dira ya Tanzania 2050, imewekwa wazi kuwa kila kijana nchini anapaswa kupata nafasi ya kujipatia ujuzi, kupata ajira yenye staha na kushiriki kikamilifu katika mabadiliko ya kiuchumi ya Taifa.
“Tanzania ni Taifa lenye vijana wengi, wameelimika, wana ndoto, wabunifu na wako tayari kuchangia katika maendeleo ya taifa,” amesema Waziri Sangu.
Ameongeza kuwa kupitia maonesho haya ya ajira, vijana wa Kitanzania wameunganishwa na waajiri, wameanzisha kazi zenye mafanikio na kupata uzoefu muhimu kupitia fursa zilizoundwa na jukwaa hilo.
Kadhalika, Waziri Sangu amesema makampuni ya Kichina yanayofanya kazi nchini Tanzania yamekuwa washirika muhimu kupitia uwekezaji katika miundombinu, viwanda, sekta ya madini, teknolojia ya habari, usafirishaji, nishati na sekta nyingine za kimkakati. Makampuni hayo yamechangia kwa kiasi kikubwa katika ukuaji wa uchumi na kutoa fursa za ajira kwa Watanzania.
Kwa upande mwingine, Mhe. Sangu amesema Serikali ya Tanzania itaendelea kuimarisha ushirikiano na Serikali ya China katika uhamishaji wa ujuzi, teknolojia, ubunifu na utaalamu ili kuongeza ushindani wa taifa katika uchumi wa dunia unaobadilika kwa kasi.
Naye, Balozi wa China nchini Tanzania, Mheshimiwa Chen Mingjian, amesema Maonesho ya Ajira yaliyoandaliwa na Chama cha Makampuni ya China yanayofanya shughuli nchini Tanzania yamekuwa jukwaa muhimu kwa makampuni hayo na wahitimu wa Kitanzania kukutana na kujadili kwa pamoja kuhusu fursa za ajira. Aidha, amezitaka kampuni hizo kuendelea kuwa daraja la ushirikiano kwa kutoa nafasi zaidi za ajira kwa Watanzania.
Zaidi ya kampuni 60 zinashiriki katika maonesho hayo kutoka sekta mbalimbali ikiwemo Uhandisi, Viwanda, Biashara, Teknolojia ya Habari na Mawasiliano, Fedha pamoja na Huduma.
Maonesho ya Ajira ya Tano (5) kati ya China na Tanzania yamelenga kutangaza na kuwaunganisha vijana wahitimu na wenye ujuzi wa Kitanzania na makampuni ya Kichina, ili kuimarisha ajira, ubunifu na ushirikiano wa kiuchumi kwa manufaa ya pande zote mbili.


















.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)



.jpeg)


.jpeg)