Benki ya Absa Tanzania, kwa ushirikiano na Microsoft na Women in Tech, imezindua rasmi Mpango wa ElevateHer AI nchini Tanzania, ambao unalenga kuwawezesha wasichana 5,000 wa Kitanzania kupata ujuzi na cheti cha Akili Mnemba (AI).

Mpango huu ni sehemu ya juhudi pana za kiafrika zinazolenga kutoa mafunzo kwa wanawake 50,000 barani Afrika ili waweze kushiriki kikamilifu katika uchumi wa kidijitali unaokua kwa kasi.

Kupitia mpango wa ElevateHer, washiriki watapata fursa ya kujifunza mtandaoni kwa njia ya kujitegemea bila malipo, ambapo watapata maarifa ya msingi ya AI, matumizi ya AI katika biashara, na maendeleo ya taaluma katika mazingira ya kazi yanayoendeshwa na teknolojia ya AI. Mpango huu utakuwa wazi kwa mwaka mzima.

Ofisa Mkuu wa Uendeshaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Oscar Mwamfwagasi, amesema mpango huu unaakisi dhamira ya benki kuhakikisha wasichana wanapata ujuzi wa kidijitali unaohitajika kwa siku za usoni. “Artificial intelligence inabadilisha jinsi uchumi unavyofanya kazi na jinsi watu wanavyofanya kazi. 

Kupitia Mpango wa ElevateHer AI, Benki ya Absa Tanzania inalenga kuhakikisha wasichana wa Kitanzania wanapata ujuzi na kujiamini kushiriki kikamilifu katika uchumi wa kidijitali na kuchangia ubunifu na ukuaji.”

Juhudi hii inaendeleza michango ya Absa Tanzania ya kukuza ushiriki wa wanawake katika teknolojia, ikiwa ni pamoja na GirlCode Hackathon ya mwaka jana, ambapo wasichana wabunifu walikusanyika ili kutengeneza suluhisho za kiteknolojia.

Mpango wa ElevateHer unatoa njia tatu za kujifunza: AI kwa Wote, AI kwa Biashara, na AI kwa Ukuaji wa Kitaaluma, na kutoa fursa kwa washiriki kujenga maarifa ya vitendo na kutumia zana za AI katika safari zao za kitaaluma au za ujasiriamali.

Bi. Tiara Pathon, Mkurugenzi wa Ujuzi wa AI katika Microsoft Elevate, Microsoft Afrika Kusini, amesema upatikanaji wa ujuzi wa kidijitali kwa kila mmoja ni muhimu kwa ushiriki wa Afrika katika uchumi wa AI duniani. “Ukuaji wa uchumi jumuishi katika zama za AI unahitaji kujenga ujuzi kwa wingi katika masoko yanayokua. Kwa Afrika, hii inamaanisha kuwekeza kwa makusudi katika ujuzi wa kidijitali na AI kwa wanawake. Kupitia ushirikiano wetu na Absa na Women in Tech, mpango wa ElevateHer unawawezesha wanawake barani kote kupata ujuzi wa vitendo unaohitajika kazini na kuimarisha nafasi ya Afrika katika ajira za baadaye.”

Mpango huu pia unasaidiwa na Women in Tech Global, shirika linalojitolea kuwawezesha wanawake na wasichana milioni tano katika Sayansi, Teknolojia, Uhandisi, na Hisabati (STEM) kufikia mwaka 2030.

Wanawake wanaopenda kushiriki wanaweza kujisajili mtandaoni kupitia: https://elevateher-in-africa.org/⁠ 

Kwa niaba ya Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira (TRAMEPRO), napenda kuungana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na jumuiya ya kimataifa katika kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Figo. Siku hii ni muhimu katika kuongeza uelewa wa jamii kuhusu umuhimu wa kulinda na kutunza afya ya figo.

Takwimu za kimataifa zinaonesha kuwa zaidi ya watu milioni 850 duniani wanaishi na aina fulani ya ugonjwa wa figo, huku takribani asilimia 10 ya watu wazima duniani wakiwa na dalili za ugonjwa huo. Aidha, mamilioni ya watu hulazimika kutegemea matibabu ya gharama kubwa kama dialysis au upandikizaji wa figo (kidney transplant) ili kuendelea kuishi.

Barani Afrika, tafiti zinaonesha kuwa kati ya asilimia 13 hadi 15 ya watu wazima wanaweza kuwa na dalili za ugonjwa wa figo. Nchini Tanzania, tafiti mbalimbali zinaonesha kuwa takribani asilimia 10 hadi 12 ya watu wazima wanaweza kuwa katika hatari au tayari wana dalili za ugonjwa wa figo, huku wengi wakigundulika katika hatua za mwisho za ugonjwa.

Gharama za matibabu ya magonjwa ya figo ni kubwa sana. Mgonjwa anayehitaji dialysis hulazimika kufanya matibabu hayo mara mbili hadi tatu kwa wiki, ambapo gharama ya kikao kimoja inaweza kufikia wastani wa dola za Marekani 80 hadi 200. Hii ina maana kuwa kwa mwaka mmoja, gharama za matibabu zinaweza kufikia dola 10,000 hadi 25,000 au zaidi kwa mgonjwa mmoja.

Aidha, matibabu ya upandikizaji wa figo (kidney transplant) yanaweza kugharimu kati ya dola 15,000 hadi 30,000, bila kujumuisha gharama za dawa za kudhibiti kinga ya mwili ambazo mgonjwa hulazimika kutumia maisha yote.

Kutokana na hali hii, ni wazi kuwa kinga ni bora zaidi kuliko tiba, na jamii inapaswa kuhamasishwa kuchukua hatua za kulinda afya ya figo mapema.

Katika muktadha huu, tiba asilia ina nafasi muhimu katika kusaidia kuimarisha kinga ya mwili na afya kwa ujumla. Hata hivyo, bado kuna changamoto ya uhaba wa ushahidi wa kisayansi unaothibitisha kwa kina baadhi ya dawa na mbinu za tiba asilia. Kwa sababu hiyo, TRAMEPRO inaendelea kusisitiza umuhimu wa tafiti za kisayansi, uthibitishaji wa dawa za asili, na ushirikiano kati ya wataalamu wa afya na taasisi za utafiti.

Kwa sasa, nikiwa katika ziara ya kitaaluma mjini New Delhi, India, ninapata uzoefu na kujifunza kuhusu matibabu mtambuka (Integrative Medicine) katika taasisi mbalimbali ikiwemo Max Super Speciality Hospital pamoja na taasisi za tiba asilia chini ya mfumo wa AYUSH. Uzoefu huu unalenga kuimarisha uelewa na ushirikiano katika kuunganisha tiba asilia na tiba za kisasa kwa manufaa ya afya ya jamii.

TRAMEPRO itaendelea kushirikiana na taasisi za utafiti, hospitali, na wataalamu wa magonjwa ya figo ili kuendeleza tafiti, kutoa elimu kwa jamii, na kuhakikisha matumizi salama na yenye tija ya tiba asilia.

Katika maadhimisho haya, ninatoa wito kwa:

Watabibu wa tiba asilia kuzingatia viwango vya usalama, maadili ya kitaaluma na uthibitisho wa kisayansi katika huduma wanazotoa.

Wananchi kuchukua hatua za kinga dhidi ya magonjwa ya figo ikiwa ni pamoja na kudhibiti shinikizo la damu na kisukari, kunywa maji ya kutosha, kutumia dawa kwa usahihi, na kufanya uchunguzi wa afya mara kwa mara.

Serikali na taasisi za utafiti kuendelea kuwekeza katika tafiti za dawa za asili na kuimarisha mfumo wa huduma za afya jumuishi.

Kwa pamoja tunaweza kujenga mfumo wa afya unaounganisha hekima ya tiba asilia na sayansi ya tiba ya kisasa kwa manufaa ya binadamu na mazingira yetu.

Mungu aibariki Tanzania na awajalie wananchi wake afya njema.

Boniventura Mwalongo Katibu Mkuu – TRAMEPRONew Delhi, India 12 Machi 2026

Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Mambo ya Ndani ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Bw. Shaibu Mmari, amesema ushirikiano kati ya TRA na mawakala wa forodha ni nguzo muhimu katika kuimarisha usimamizi wa maadili na uwajibikaji kwa watumishi wa Mamlaka.

Bw. Mmari amesema hayo jijini Dar es Salaam wakati wa kikao cha mazungumzo kati ya TRA na viongozi wa Chama cha Waondoshaji na Wapelekaji Shehena Bandarini na Mipakani Tanzania (TAFFA), kilicholenga kuimarisha mahusiano ya kikazi na kubadilishana taarifa kuhusu uvunjifu wa maadili unaoweza kujitokeza katika shughuli za forodha.

Amesema kuwa ushirikiano wa karibu kati ya TRA na wadau wa sekta ya forodha ni muhimu katika kusaidia kubaini na kudhibiti vitendo vinavyokiuka maadili, pamoja na kuimarisha uwazi na uwajibikaji katika utoaji wa huduma.

“TRA ina jukumu la kukusanya mapato ya Serikali, kusimamia shughuli za forodha, na kuhakikisha sheria na taratibu za ushuru zinafuatwa ipasavyo. Ushirikiano na wadau kama TAFFA unatusaidia kuimarisha uadilifu na kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu haya,” amesema Bw. Mmari.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa wadau kuendelea kushirikiana na TRA katika kutoa taarifa pale wanapoona dalili za uvunjifu wa maadili au vitendo vinavyoweza kuathiri uadilifu wa huduma za forodha.

Kwa upande wake, Mhasibu Mkuu wa TAFFA, Bw. Anthony Mukyamuzi, ameipongeza TRA kwa juhudi inazoendelea kufanya katika kuboresha mifumo ya forodha na utoaji wa huduma kwa wadau.

Amesema maboresho hayo yameongeza ufanisi katika shughuli za uondoshaji na uingizaji wa mizigo bandarini na mipakani, na kuimarisha mazingira ya biashara kwa wadau wa sekta ya usafirishaji na uondoshaji shehena.

Mwisho, pande hizo mbili zimeahidi kuendelea kuimarisha ushirikiano katika kubadilishana taarifa, kuhamasisha maadili mema kwa watumishi, na kujenga mfumo wa uwajibikaji utakaosaidia kulinda uadilifu wa shughuli za forodha nchini.

 

Ofisi ya BAKWATA Mkoa wa Singida, kupitia Sheikh wa Mkoa huo Issa Bin Nassoro, imezipongeza taasisi za Ramadhan Charity Programme2026, inayoongozwa na Ndugu Ahmed Misanga pamoja na Taasisi ya JAI Tanzania kwa kutoa sadaka katika Gereza la Manispaa ya Singida, misikiti pamoja na vituo vya watoto yatima.
Sheikh Issa amesema hayo leo wakati wa ziara yake ya kutembelea wafungwa katika Gereza la Manispaa ya Singida, ambapo pia walitoa sadaka ya Iftar kwa wafungwa ili waweze kupata futari pamoja na daku katika kipindi hiki cha mwezi mtukufu wa Ramadhani. Sadaka hizo zimetolewa na taasisi za Ramadhan Charity Programme 2026 pamoja na JAI Tanzania.
Katika hotuba yake, Sheikh Issa aliwaomba watu mbalimbali katika jamii kuwajali watu wenye mahitaji na masikini, akisisitiza kuwa kufanya hivyo ni jambo linalompendeza Mungu. Aliongeza kuwa hata mitume waliwahudumia na kuwasaidia watu masikini na wenye uhitaji.
Aidha, Sheikh wa Mkoa alitoa salamu kutoka kwa Mufti na Sheikh Mkuu wa Tanzania, Dkt. Abubakar Zubeir bin Ally, akisisitiza umuhimu wa kuendelea kuwajali watu wenye mahitaji maalum, wakiwemo wafungwa na makundi mengine yenye uhitaji katika jamii.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Ramadhan Charity Programme 2026, Ndugu Ahmed Misanga, amesema kuwa utoaji wa sadaka ya Iftar kwa watu wenye mahitaji ni utaratibu wao wa kila mwaka, hususan katika magereza na makundi mengine ya jamii. Amesema kuwa wamekuwa wakifanya shughuli hiyo kwa zaidi ya miaka mitano sasa.
Misanga alisisitiza kuwa watu waliopo magerezani wanahitaji huruma na faraja kutoka kwa jamii ili kuwapa moyo na kuwasaidia kumkaribia Mungu, ili wanaporudi uraiani wawe watu wema wenye hofu ya Mungu na mchango chanya kwa jamii.
Katika msaada huo, Ramadhan Charity Programme 2026 kwa kushirikiana na JAI Tanzania walitoa sadaka ya Iftar iliyojumuisha boksi la tende, sukari, tambi, mchele, ngano, juisi pamoja na taulo za kike kwa ajili ya wafungwa wanawake katika gereza hilo.
Naye Kaimu Mkuu wa Gereza la Wilaya ya Singida, Ndugu Amini Mjenza, amesema amefurahishwa na taasisi ya Ramadhan Charity chini ya uongozi wa Ahmed Misanga kwa kuwapatia sadaka ya Iftar, akieleza kuwa msaada huo utawasaidia sana wafungwa waliopo gerezani.
“Tutaitumia sadaka hii ya Iftar kama mlivyokusudia, na tunamuomba Mungu awalipie pale mlipotoa kwa ajili ya wafungwa wote, wanawake na wanaume,” amesema.
Katika tukio hilo, washiriki pia walipata nafasi ya kuliombea Taifa pamoja na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Taasisi ya Ramadhan Charity Programme 2026 imewataka Watanzania kutumia mwezi huu mtukufu wa Ramadhani kuwa wamoja, kusaidiana na kufanya kazi kwa pamoja katika kuwasaidia wenye mahitaji katika jamii.
 
 

Wakala wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu (ADEM) leo imepokea ujumbe wa wadau wa maendeleo kutoka taasisi mbalimbali ikiwemo Mastercard Foundation, Education for Sub-Saharan Africa (ESSA), Tanzania Education Network (TEN/MET), African Centre for School Leadership (ACSL), Teach United na Educate kwa ajili ya kujadili ushirikiano wa kuimarisha uongozi wa shule za sekondari nchini.
Wakala wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu - ADEM umeendesha mafunzo maalumu ya siku tano kwa Maafisa Elimu wa Mikoa 26 kutoka Tanzania Bara kuanzia tarehe 8-12 Machi, 2026 jijini Arusha.

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo, Mhe. Deodatus Mwanyika (Mb), ameeleza kuridhishwa kwake na hatua ya ujenzi wa jengo la kisasa la Vipimo na Viwango katika Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE) jijini Dar es Salaam.

Akizungumza Machi 12, 2026, Mhe. Mwanyika amebainisha kuwa mradi huo wa ghorofa 10 umefikia asilimia 93 ya utekelezaji wake, jambo linaloashiria usimamizi madhubuti na weledi katika ukamilishaji wa Jengo Jengo hilo ili kukidhi ongezeko la wanafunzi wanaodahiliwa kila mwaka.

Vilevile, Mwenyekiti huyo ametoa rai kwa uongozi wa chuo kuendelea kutoa na kuimarisha elimu ya kati (middle-level education) katika fani za biashara hususani ujasiliamali kwa kuwa ni nyenzo adhimu kwa wahitimu wanaojiandaa kuingia kwenye soko la ajira binafsi na

Kutasaidia kuongeza hadhi ya chuo na kuchochea ari ya wanafunzi wengi zaidi kujiunga na taasisi hiyo.

Amesema kuwa uimara wa chuo unategemea ubora wa mafunzo unayoyatoa na uwezo wake wa kuzalisha wataalamu wenye ushindani katika soko la ndani na nje ya nchi.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Dennis Londo (Mb), amefafanua kuwa mradi huo unatekelezwa kupitia bajeti ya Serikali ya mwaka wa fedha 2025/26 na unatarajiwa kuwa na uwezo wa kubeba zaidi ya wanafunzi 4,000 kwa wakati mmoja.

Aidha amebainisha kuwa Jengo hilo la Vipimo na Viwango litakuwa kitovu cha mafunzo ya masoko na nyanja mbalimbali za kibiashara ambazo zinahitajika kwa kiasi kikubwa kulingana na mwelekeo wa sasa wa uchumi wa viwanda.

Naye Mkuu wa Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE), Prof. Edda Lwoga, ameeleza kuwa mradi huo ulioanza Mei 25, 2023, umekuwa mhimili wa mabadiliko makubwa ya kitaaluma chuoni hapo. Alibainisha kuwa kukamilika kwa jengo hilo kutaongeza fursa za udahili kwa wanafunzi wengi wanaohitaji masomo ya biashara na ujasiriamali, ikiwemo kozi fupi ambazo zimekuwa na mahitaji makubwa kwa wadau wa sekta binafsi.

๐Ÿ“*Geita.*

Mwenyekiti wa Kamati ya TEITI, Balozi Wilson Masilingi, ametembelea Mgodi wa Dhahabu wa Geita Gold Mining Limited akiambatana na Menejimenti ya TEITI, kwa lengo la kujitambulisha na kufanya mazungumzo na menejimenti ya mgodi huo.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Balozi Masilingi alisema ziara hiyo imelenga kujenga na kuimarisha ushirikiano kati ya TEITI na wadau wa sekta ya uziduaji, hususan migodi mikubwa inayochangia maendeleo ya taifa.

Alisema kuwa aliteuliwa kusimamia taasisi hiyo muhimu na Mhe.Dkt.Samia Suluhu Hassan, Rais wa Tanzania, mwezi Januari mwaka huu, hivyo anaona ni muhimu kujitambulisha kwa wadau wakuu wa sekta hiyo ili kuimarisha ushirikiano katika utekelezaji wa majukumu ya TEITI.

“Utekelezaji wa shughuli za EITI nchini ni wa ushirikiano, hivyo nitashirikiana kikamilifu na wadau wote ili kuendeleza gurudumu la uwazi na uwajibikaji katika sekta ya uziduaji,” alisema Balozi Masilingi.

Katika ziara hiyo, menejimenti ya mgodi ilitoa maelezo kuhusu maendeleo yaliyofikiwa tangu kuanzishwa kwa mgodi huo, ikiwemo namna wanavyotekeleza sheria, kanuni na miongozo ya sekta ya madini pamoja na masharti ya leseni ya uchimbaji.

Aidha, ilielezwa kuwa mgodi huo umeendelea kutenga fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya Uwajibikaji kwa Jamii (CSR) katika halmashauri mbalimbali za Mkoa wa Geita, hatua inayochangia maendeleo ya jamii zinazouzunguka mgodi.

Pia ilibainishwa kuwa kwa sasa mgodi huo unaendeshwa kwa kiasi kikubwa na Watanzania na umeendelea kuongeza ajira kwa wananchi wa ndani ikilinganishwa na miaka ya awali ya uendeshaji wake.

Balozi Masilingi aliishukuru menejimenti ya mgodi kwa mapokezi mazuri waliompatia pamoja na utayari wao wa kuendeleza ushirikiano kwa manufaa ya sekta ya uziduaji na maendeleo ya taifa.

Kwa upande wake, Katibu Mtendaji wa TEITI, Bi. Mariam Mgaya, aliishukuru menejimenti ya mgodi kwa kuendelea kushirikiana na TEITI katika utekelezaji wa matakwa ya EITI pamoja na Sheria ya TEITA ya mwaka 2015, inayolenga kuimarisha uwazi na uwajibikaji katika sekta ya uziduaji.

Alisisitiza kuwa ushirikiano huo unapaswa kuendelezwa ili kuongeza uwazi na uwajibikaji katika usimamizi wa rasilimali za madini, mafuta na gesi asilia nchini.

Naye Meneja wa mgodi huo, Bw. Ashraf Suryaningrat, alisema Geita Gold Mining Limited itaendelea kushirikiana kikamilifu na TEITI katika kufanikisha lengo la uwazi na uwajibikaji katika sekta ya uziduaji, akibainisha kuwa mgodi huo ni miongoni mwa wadau wakubwa wa TEITI nchini.

 


Naibu Waziri wa Ujenzi Eng. Godfrey Kasekenya amemtaka mkandarasi JASCO anaejenga daraja la Kabalisi mita 40 na GEMEN anaejenga daraja la Sange mita 40 wilayani Ileje kuhakikisha ujenzi huo unakamilika ifikapo machi 30 mwaka huu.

Eng. Kasekenya amezungumzia umuhimu wa ujenzi huo kuendana na uwekaji wa taa katika madaraja hayo na kuhakikisha mitaro karibu na madaraja hayo inasakafiwa vizuri.

" Hakikisheni ujenzi wa madaraja haya unakidhi ubora uliosanifiwa ili kuwiana na barabara za lami zitakapojengwa", amesema Eng. Kasekenya.

Msimamizi wa ujenzi huo Eng. Jonas Matete kutoka Kitengo cha Usimamizi wa Barabara cha TANROADS (TECU), amesema atawasimamia Wakandarasi hao ili madaraja hayo yayojengwa sehemu zenye miinuko yakamilike kwa wakati na ubora na hivyo kuchochea fursa za kijamii na kiuchumi kwa wananchi

Madaraja ya Kabalisi na Sange yako katika barabara ya mkoa itokayo Ibungu- Kalembo-Kafwafwa hadi Kimo yenye urefu wa km 46.1 na inaunganisha wilaya ya Ileje mkoani Songwe na Rungwe mkoani Mbeya.

Zaidi ya shilingi bilioni 7.9 zimetumika katika ujenzi wa daraja la Kabalisi wakati shilingi bilioni 7 zikitumika kujenga daraja la Sange.



Na WMJJWM Dar Es Salaam 

Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi, amezindua kamati maalum ya kuratibu na kuhamasisha michango kwa ajili ya kuwasaidia wanafunzi  wenye mahitaji maalum.

Akizungumza baada ya kuzindua kamati hiyo Machi 11, 2026, Mkoani Dar Es salaam, Mahundi amesema uanzishwaji wa Kamati hiyo ni sehemu ya juhudi za serikali na wadau kuhakikisha wanafunzi wenye mahitaji maalum wanapata huduma na kuwa na mazingira bora ya kujifunzia na kuendeleza ndoto zao.

“Watoto wenye mahitaji maalum ni sehemu muhimu ya jamii yetu hivyo Serikali itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha wanapata fursa sawa za elimu, huduma na msaada unaowawezesha kufikia ndoto zao pia kamati hii itakuwa na jukumu la kuhamasisha jamii, taasisi na wadau mbalimbali kuchangia rasilimali zitakazosaidia kuboresha mahitaji ya wanafunzi hao ikiwemo vifaa vya kujifunzia, huduma za kijamii na mazingira rafiki ya elimu.,” amesema Mhe. Mahundi.

Naye Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Dar Es Salaam Lawrence Malangwa amesema ni muhimu ushirikiano wa jamii katika kuwasaidia watoto wenye uhitaji ili kuhakikisha hakuna mtoto anayekosa haki ya elimu kutokana na changamoto za maisha hiivyo tutasimamia vyema upatikananji wa vifaa na mtumizi kwa Watoto hao.

Kwa upande wake Mhazini wa Kamati ya Elimu Mama Tunu Pinda ameipongeza Wizara kwa kuendelea kuonesha dhamira ya dhati katika kutetea na kuimarisha ustawi wa makundi maalum nchini, akieleza kuwa hatua hiyo itachochea ari ya wadau wengi zaidi kujitokeza kusaidia wanafunzi wenye mahitaji.

Uzinduzi huo unatarajiwa kuwa chachu ya kuimarisha ushirikiano kati ya Serikali, wadau na jamii katika kuhakikisha wanafunzi wenye uhitaji wanapata msaada unaohitajika ili waweze kusoma na kufanikiwa kama watoto wengine.