JUHUDI za wananchi wa kitongoji cha Lailupa katika Kijiji cha Meirugoi Kata ya Gelai-Meirugoi wilayani Longido Mkoani Arusha za kujitoa na kujenga darasa la shule ya awali {chekechea} kwa gharama ya shilingi milioni 12 kumemuibua Mbunge wa Jimbo hilo Dkt Steven Kiruswa kuamua kumalizia ujenzi wa darasa hilo kwa gharama zake binafsi za kiasi cha shilingi milioni 6.
Akizungumza nasi ,Mwenyekiti wa Kitongoji cha Nailupa Ndung’anak Mepukor alisema wananchi wa Kitongoji hicho walimsimamisha Kiruswa ambaye pia ni Naibu Waziri wa Madini aliyekuwa akielekea kata nyingine kukagua miradi ya maendeleo kutembelea darasa hilo na kujionea mwenye watoto wakipata elimu chini ya mti bila kujali jua wala mvua.
Mepukor alisema jitihada za ushawishi wa akina mama ,vijana ,viongozi wa Milla maarufu kwa jina la Laigwanani ulimfanya Mbunge kwenda kutembelea darasa hilo ambalo bado lilikuwa halijakamilika kwa kukosekana mlango mmoja,madirisha sita ,bati 60 ,madawati 20,mbao,madawati 20 na umaliziaji wa kupiga Plasta hatua iliyomfanya mbunge kubeba gharama hiyo kwa gharama ya kiasi hicho cha fedha cha shilingi milioni 6
Mwenyekiti alisema ujenzi wa darasa hilo uliofanywa na wananchi hao umetokana na michango ya kila kaya kwa fedha taslimu na uuzwaji wa mifugo kwa kila kaya na kujitoa kwa uchimbaji wa msingi na ujenzi wa darasa sambamba na ubebaji wa matofali kwa kila mwananchi wa kitongoji hicho ili watoto waweze kusoma ndani ya darasa hilo wakiwa wameketi kwenye madawati.
‘’Tulijitahidi hadi kufikia hatua hiyo na Mbunge Kiruswa kukubali tu kufika kuona hali halisi ya watoto kusomea chini ya mti na kuona jitihada za wananchi katika ujenzi wa darasa hilo ameamua kumalizia kila kitu kwa gharama zake’’alisema Mepukor
Akizungumza katika mara baada ya kuahidi kumalizia hatua iliyobaki ,Kiruswa alisema kwa kuwashukuru wananchi hao kwa kujitoa na kufanikisha ujenzi wa darasa hilo na kusema kuwa hatua hiyo imempa faraja kubwa sana na yeye kuamua kuchangia na kumamilisha ujenzi wa darasa ili watoto waweze kusoma karibu na makazi na kuondoka na kutembea umbalim mrefu kufuata elimu.
Kiruswa alisema jukumu la kutaka watoto kusoma na kupata elimu bora ni la kila mwananchi wa Jimbo la Longido na sehemu kubwa inayofanywa na serikali inapaswa kuungwa mkono na wananchi na kilichofanyika katika kitongoji cha Lailupa ni kitendo kinachopaswa kupongezwa na kuungwa mkono na yeye na Halmashauri ya wilaya ya Longido.
Alisema jukumu lake la pili ni kuhakikisha shule hiyo ya awali inasajiliwa na kupata mwalimu mwenye sifa tofauti na sasa mwalimu anayewafundisha ni wa kujitolea na asiyekuwa na sifa na jukumu hilo linabebwa na yeye na hadi mwakani januari kila kitu kinapaswa kukamilika ili watoto wasomeshwe na mwalimu mwenye sifa shule kutambuliwa na serikali.
Naye Diwani wa Kata ya Gelai Meirugoi,Daniel Nasinda alisema kuwa watoto wa Kitongoji cha Lailupa hutembea umbali wa zaidi ya km 10 kwenda na kurudi kusaka elimu hatua ambayo ni hatari kwao kwa kuwa na eneo hilo lina wanyama wakali na ndio maana wazazi walijitoa kujenga darasa ili iwe salama kwa watoto wao kwenda shule.

























