Na OWM–TAMISEMI, Lilongwe, Malawi

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM–TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, ameongoza kikao cha Baraza la Mawaziri wa Kamisheni ya Pamoja ya Bonde la Mto Songwe (SONGWECOM) kilichofanyika Julai 10, 2026 jijini Lilongwe, Malawi, kwa lengo la kujadili kuharakisha utekelezaji wa Mradi wa Maendeleo wa Bonde la Mto Songwe.

Mradi huo unatarajiwa kujengwa kwa pamoja na Serikali za Tanzania na Malawi na kuzalisha umeme wa megawati 180.2, huku ukiwa na manufaa makubwa katika sekta za umwagiliaji, usambazaji wa maji, uvuvi, utalii pamoja na kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii kwa wananchi wa nchi hizo mbili.

Kikao hicho kilijadili hatua mbalimbali za utekelezaji wa mradi, ikiwemo kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na Malawi ili kuhakikisha mradi unatekelezwa kwa ufanisi na kwa wakati, kwa manufaa ya wananchi wa pande zote za Bonde la Mto Songwe.

Miongoni mwa viongozi waliohudhuria kikao hicho ni Naibu Waziri wa Maji, Mhandisi Kundo Andrea Mathew, Naibu Waziri wa Kilimo, Mhe. David Silinde, Balozi wa Tanzania nchini Malawi, Mhe. Agnes Kayola, pamoja na Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Mhandisi Kasper Kasper Mmuya, na wataalamu mbalimbali kutoka Serikali za Tanzania na Malawi.

Baraza la Mawaziri la Kamisheni ya Pamoja ya Bonde la Mto Songwe (The Joint Songwe River Basin Commission – SONGWECOM) linaundwa na Mawaziri kumi kutoka Tanzania na Malawi wanaowakilisha sekta tano muhimu ambazo ni Maji, Nishati, Kilimo cha Umwagiliaji, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), pamoja na Ardhi, ndilo chombo cha juu cha maamuzi kinachosimamia shughuli za Kamisheni hiyo. 

Kupitia kikao hicho, Tanzania na Malawi zimeendelea kudhihirisha dhamira ya kuimarisha ushirikiano wa kikanda katika usimamizi endelevu wa rasilimali za Bonde la Mto Songwe, kwa lengo la kuongeza upatikanaji wa nishati, kuimarisha usalama wa maji na chakula, na kuchochea maendeleo endelevu ya wananchi wa mataifa hayo mawili.











 


Mawaziri wa Nishati kutoka nchi wanachama wa Soko la Pamoja la Nishati Mashariki mwa Afrika (Eastern Africa Power Pool – EAPP) wameazimia kuharakisha utekelezaji wa soko la pamoja la umeme ili kuimarisha upatikanaji wa nishati, kuongeza biashara ya umeme kati ya nchi wanachama na kukabiliana na changamoto za upatikanaji wa umeme katika ukanda huo.

Azimio hilo limefikiwa wakati wa Mkutano wa 22 wa Baraza la Mawaziri wa EAPP uliofanyika Julai 9 hadi 10, 2026 jijini Addis Ababa, Ethiopia ambapo Tanzania iliwakilishwa na Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba (Mb), kwa niaba ya Waziri wa Nishati.

Mkutano huo uliwakutanisha Mawaziri wa Nishati, wakuu wa taasisi za umeme na wawakilishi wa sekta ya nishati kutoka nchi wanachama wa EAPP kujadili hatua za kuimarisha ushirikiano wa kikanda kupitia biashara ya umeme, uunganishaji wa gridi za taifa na matumizi bora ya rasilimali za nishati.

Maazimio yaliyofikiwa yanatarajiwa kuweka mfumo madhubuti utakaowezesha nchi wanachama kuuziana umeme kwa ufanisi, kuimarisha uhakika wa upatikanaji wa nishati, kuchochea ukuaji wa uchumi, kuvutia uwekezaji na kuimarisha maendeleo ya kijamii katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Akizungumza baada ya mkutano huo, Mhe. Salome Makamba amesema maazimio hayo yatachangia kuongeza uhakika wa upatikanaji wa umeme, kupunguza changamoto za upungufu na kukatika kwa umeme katika nchi wanachama, pamoja na kuimarisha ushindani na ufanisi wa taasisi za umeme kupitia kubadilishana uzoefu na teknolojia.

Amesema upatikanaji wa umeme wa uhakika utaongeza kasi ya ukuaji wa viwanda vidogo, vya kati na vikubwa, hali itakayochochea uzalishaji, kuvutia uwekezaji na kuzalisha ajira zaidi kwa vijana, ikiwemo kuwapa Watanzania fursa za kushiriki katika shughuli mbalimbali za kitaalamu ndani ya EAPP.

Akihitimisha mkutano huo, Mwenyekiti wa Baraza la Mawaziri la EAPP ambaye pia ni Waziri wa Maji na Nishati wa Ethiopia, Mhe. Dkt. Habtamu Itefa, amesema ushirikiano na mshikamano wa kikanda ni msingi muhimu katika kufanikisha uunganishaji wa mifumo ya umeme na kuhakikisha wananchi wa nchi wanachama wanapata huduma ya umeme salama, ya uhakika na endelevu.











 



 Asilimia 10 ya mapato ya sekta ya madini kuelekezwa kwenye utafiti

MBT kuwanufaisha wachimbaji Mundarara


Naibu Waziri wa Madini, Dkt. Steven Kiruswa, amesimamisha kwa muda uchaguzi wa Viongozi wa Mabroka wa Madini katika Wilaya ya Longido, Mkoa wa Arusha, akisisitiza kuwa uchaguzi huo hautafanyika hadi pale wapiga kura watakapopatiwa elimu ya kutosha kuhusu haki, wajibu na taratibu za uchaguzi kwa mujibu wa  Katiba ya Mabroka.

Hatua hiyo inalenga kuhakikisha uchaguzi unafanyika kwa uwazi, haki na ushirikishwaji wa wadau wote, huku ukiepusha migogoro inayoweza kujitokeza kutokana na kutokuelewa taratibu za uchaguzi.

Akizungumza leo Juni 10, 2026 na wachimbaji, wafanyabiashara wa madini na viongozi wa Serikali wakati wa ziara yake wilayani humo, Dkt. Kiruswa amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imejidhatiti kujenga sekta ya madini yenye uwazi, uwajibikaji na ushiriki mpana wa Watanzania katika shughuli zote za mnyororo wa thamani wa madini.

"Nataka uchaguzi huu ufanyike kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zote. Kwanza tutoe elimu kwa wapiga kura ili kila mshiriki ajue haki na wajibu wake. Tukifanya hivyo tutapata viongozi wenye uhalali, wanaokubalika na watakaoweza kuwatumikia wadau wa sekta ya madini kwa ufanisi," amesema Dkt. Kiruswa.

Ameelekeza Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyabiashara wa Madini Tanzania (CHAMMATA), Jeremiah Kituyo, kwa kushirikiana na viongozi wa kitaifa wa chama hicho, kuhakikisha elimu hiyo inatolewa kwa wakati na uchaguzi mpya unaratibiwa mara baada ya zoezi hilo kukamilika bila kucheleweshwa.

Naibu Waziri huyo amewakumbusha mabroka wote wa madini kuzingatia matakwa ya Sheria ya Madini kwa kuhakikisha wanakuwa na leseni halali za ubroka pamoja na vitambulisho vinavyoonesha namba za leseni zao wakati wote wanapotekeleza shughuli zao.

Amesema Serikali haitamvumilia mtu yeyote atakayejihusisha na ubroka wa madini bila leseni halali, akibainisha kuwa hatua hiyo inalenga kulinda maslahi ya wafanyabiashara, kuongeza uwajibikaji na kuhakikisha Serikali inakusanya mapato yote yanayostahili.

Aidha, amewataka viongozi wa vijiji, viongozi wa sekta ya madini na wananchi kushirikiana kwa karibu katika kulinda rasilimali za madini na kuhakikisha shughuli za uchimbaji zinafanyika kwa mujibu wa sheria na zinawanufaisha wananchi wa maeneo husika.

Katika kuimarisha sekta ya madini, Dkt. Kiruswa amesema Serikali imeanza kutekeleza maelekezo ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kurejesha sehemu ya mapato yanayotokana na sekta ya madini katika maendeleo ya sekta hiyo, ambapo asilimia 10 ya makusanyo ya sekta itaelekezwa kwenye shughuli za utafiti wa madini.

Amesema hatua hiyo itaiwezesha Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) kufanya tafiti zaidi za kijiolojia, kuongeza upatikanaji wa taarifa za kisayansi kuhusu maeneo yenye madini na kuwasaidia wachimbaji wadogo kufanya uwekezaji wenye tija.

"Utafiti ni msingi wa mafanikio ya sekta ya madini. Tunataka wachimbaji wetu waondokane na uchimbaji wa kubahatisha na badala yake watumie taarifa sahihi za kijiolojia zitakazoongeza uzalishaji, kupunguza hasara na kuongeza kipato chao," amesema.

Ameongeza kuwa uwekezaji katika tafiti za madini utaongeza ugunduzi wa maeneo mapya yenye rasilimali, kuchochea uwekezaji, kuongeza ajira na kuimarisha mchango wa sekta ya madini katika Pato la Taifa.

Dkt. Kiruswa amesema Serikali kupitia Wizara ya Madini inatekeleza Programu ya Mining For A Brighter Tomorrow (MBT), inayowalenga wachimbaji wadogo, wanawake, vijana na watu wenye mahitaji maalum ili washiriki kikamilifu katika shughuli za utafiti, uchimbaji, uchakataji, uongezaji thamani na biashara ya madini.

Kutokana na fursa hizo, amewahamasisha wananchi wa Kijiji cha Mundarara kuunda vikundi na kujiandikisha katika programu hiyo ili kunufaika na mafunzo, teknolojia, mitaji na fursa mbalimbali zinazotolewa na Serikali kwa ajili ya kukuza shughuli za madini.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyabiashara wa Madini Tanzania (CHAMMATA), Jeremiah Kituyo, amesema uchaguzi wa mabroka katika ngazi ya wilaya utasimamiwa na viongozi wa mkoa kwa mujibu wa Katiba na mwongozo wa chama.

Amesema mwanachama atakayeshiriki uchaguzi atalazimika kuwa na kitambulisho hai cha chama pamoja na leseni halali ya biashara ya madini, huku akibainisha kuwa viongozi wa masoko ya madini na vituo vya ununuzi huchaguliwa kila mwaka ili kuimarisha uwajibikaji, uwazi na uwakilishi wa wadau wa sekta hiyo.

Kituyo amesema chama kitaendelea kushirikiana na Wizara ya Madini kuhakikisha uchaguzi huo unafanyika kwa amani, uwazi na kuzingatia sheria, hatua itakayochangia kuimarisha mazingira ya biashara ya madini nchini.














Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba, ametembelea Ubalozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania jijini Addis Ababa, Ethiopia, na kufanya mazungumzo na Mhe. Balozi. Innocent Shiyo.

Ziara hiyo imefanyika wakati Mhe. Salome akiwa nchini humo kushiriki Mkutano wa 22 wa Baraza la Mawaziri la Soko la Pamoja la Nishati Mashariki mwa Afrika (Eastern African Power Pool – EAPP), mkutano unaotarajiwa kuhitimishwa leo kwa kupitisha maamuzi muhimu kuhusu biashara ya pamoja ya umeme na uimarishaji wa gridi za taifa kati ya nchi wanachama.

Katika ziara hiyo, Mhe. Salome aliambatana na Kaimu Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa Mipango, Utafiti na Uwekezaji wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), Mha. HenryFried Byabato, aliyemuwakilisha Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, pamoja na wataalam kutoka Wizara ya Nishati.












 


Uwekezaji katika miundombinu ya sekta ya nishati unahitaji ushirikiano wa karibu kati ya Serikali, sekta binafsi na taasisi za fedha ili kuhakikisha miradi mikubwa inapata rasilimali zinazohitajika na kutekelezwa kwa ufanisi.

Akizungumza katika Kongamano la Siku ya Nishati (Energy Day) linaloendelea wakati wa Maonesho ya Sabasaba jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi wa Sera na Mipango wa Wizara ya Nishati, Bw. Petro Lyatuu, amesema uwekezaji katika miradi mikubwa ya nishati unahitaji mifumo imara ya ufadhili pamoja na ushirikiano wa wadau mbalimbali.

Bw. Lyatuu amesema miradi ya uzalishaji, usafirishaji na usambazaji wa umeme inahitaji uwekezaji mkubwa wa kifedha ambao hauwezi kutegemea chanzo kimoja pekee, hivyo kuna umuhimu wa kuendelea kuvutia wawekezaji na kushirikiana na taasisi za fedha katika kuwezesha utekelezaji wa miradi hiyo.

Ameeleza kuwa Serikali ina nafasi muhimu katika kuweka mazingira wezeshi, kuandaa sera na mikakati inayosaidia kuvutia uwekezaji, huku taasisi za fedha zikiwa na jukumu la kusaidia upatikanaji wa mitaji kwa ajili ya miradi ya kimkakati ya sekta ya nishati.

Aidha, amesema kwa miradi mikubwa inayohusisha uzalishaji wa umeme, njia za kusafirisha umeme na miundombinu ya usambazaji, kunahitajika rasilimali fedha za kutosha pamoja na ushirikiano wa muda mrefu kati ya Serikali, sekta binafsi na washirika wa maendeleo.

Ameongeza kuwa Tanzania ina fursa kubwa ya kuendeleza sekta ya nishati, hivyo ni muhimu kuimarisha mifumo ya kifedha, kuondoa vikwazo vya uwekezaji na kuhakikisha miradi ya nishati inatekelezwa kwa manufaa ya maendeleo ya Taifa.

Meneja wa Miradi ya Nishati wa Umoja wa Ulaya (European Union – EU), Massimiliano Pedretti, amesema ushirikiano wa karibu kati ya Serikali, sekta binafsi, taasisi za fedha na washirika wa maendeleo ni msingi muhimu wa kufanikisha utekelezaji wa miradi mikubwa ya nishati nchini.

Akizungumza katika Kongamano la Siku ya Nishati (Energy Day) lililofanyika wakati wa Maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), Pedretti amesema miradi ya uzalishaji, usafirishaji na usambazaji wa umeme inahitaji uwekezaji mkubwa wa kifedha ambao hauwezi kutegemea Serikali pekee, hivyo ni muhimu wadau wote kushirikiana katika kuhamasisha na kuwezesha upatikanaji wa rasilimali fedha.

Amesema Umoja wa Ulaya unaendelea kuunga mkono maendeleo ya sekta ya nishati nchini kupitia utoaji wa ruzuku za mitaji (capital grants) kwa miradi midogo ya nishati pamoja na kusaidia kutafuta na kuwezesha masuluhisho ya kifedha kwa miradi mikubwa ya kimkakati inayohitaji uwekezaji mkubwa.

Pedretti ametoa wito kwa sekta binafsi kutumia fursa hizo kwa kuandaa na kuwasilisha mapendekezo ya miradi (proposals) yenye ubora na yenye lengo la kutatua changamoto za nishati nchini, ili yaweze kufanyiwa tathmini na kuangaliwa namna bora ya kuyawezesha kupata ufadhili.

Aidha, amesema Serikali ina jukumu la kuendelea kuweka sera na mazingira wezeshi yanayovutia uwekezaji, huku taasisi za fedha zikihimizwa kubuni bidhaa na huduma za kifedha zitakazorahisisha upatikanaji wa mitaji kwa wawekezaji wa sekta ya nishati.

Ameeleza kuwa taasisi za kimataifa za fedha na washirika wa maendeleo zipo tayari kuendelea kushirikiana na Tanzania katika kufadhili miradi ya nishati, lakini mafanikio yake yanategemea uwepo wa miradi iliyoandaliwa kwa viwango vinavyokubalika kimataifa, mifumo madhubuti ya usimamizi pamoja na mazingira yanayojenga imani kwa wawekezaji.

Kwa mujibu wa Pedretti, kuimarisha ushirikiano kati ya Serikali, sekta binafsi, taasisi za fedha na washirika wa maendeleo kutachochea uwekezaji zaidi katika sekta ya nishati, kuharakisha utekelezaji wa miradi ya kimkakati na kuchangia ukuaji endelevu wa uchumi wa Taifa.

 


Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Emmanuel Tutuba, ameipongeza Chuo cha Uhasibu Arusha (IAA) kwa juhudi zake za kuwawezesha vijana kujiajiri kupitia Kituo chake cha Kiatamizi cha IAA Business Start Up Centre, kinachowasaidia kubadili mawazo ya kibunifu kuwa biashara zenye mafanikio.

Tutuba alitoa pongezi hizo alipotembelea banda la IAA katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.

Alisema anafurahishwa na maendeleo ya kituo hicho, akieleza kuwa anakumbuka hatua za mwanzo za kuanzishwa kwake na sasa anashuhudia matokeo chanya kupitia vijana wanaobuni na kuanzisha biashara zinazochangia maendeleo ya uchumi.

"Ninakumbuka tulipoanzisha kituo hiki. Leo ninafurahi kuona kinaendelea kuzalisha vijana wenye ubunifu na kuwageuza mawazo yao kuwa fursa za kiuchumi," alisema Tutuba.

Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha Ushirikiano wa Kimataifa, Uhusiano na Masoko wa IAA, Sarah Goroi, alisema taasisi hiyo imeendelea kuwekeza katika kuwaandaa vijana kwa kujiajiri kupitia Kituo cha Kiatamizi, sambamba na kutoa elimu inayokidhi mahitaji ya soko la ajira.

Alisema mbali na mafunzo ya darasani, IAA imeweka mazingira rafiki yanayowezesha wanafunzi kuanzisha biashara zao huku wakipata ushauri wa kitaalamu, mafunzo ya ujasiriamali na ufuatiliaji wa karibu ili kuhakikisha mawazo yao yanakua na kuwa biashara endelevu.

Sarah alisema katika mwaka  wa masomo 2024/2025  zaidi  ya vijana 8,600 walinufaika na programu za ujasiriamali, huku vijana 1,520 wakiwasilisha mawazo mbalimbali ya biashara kupitia kituo hicho.

Aliongeza kuwa kati ya mawazo hayo, zaidi ya biashara 50 zilianzishwa na kampuni 12 zikafanikiwa kusajiliwa rasmi, zikijikita katika sekta mbalimbali zikiwemo biashara, teknolojia, sanaa, uhifadhi wa mazingira na shughuli nyingine za kiuchumi.

Alisema kupitia Kituo cha Kiatamizi, wahitimu wengi wamefanikiwa kujiajiri na wengine kuanzisha kampuni zinazowaajiri vijana wenzao, hatua inayochangia kupunguza tatizo la ukosefu wa ajira na kuchochea ukuaji wa uchumi kupitia ubunifu na ujasiriamali.