Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) Wilaya ya Moshi Vijijini umewaalika vijana na wananchi wote kushiriki katika Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani yatakayofanyika Agosti 12, 2026, katika Viwanja vya UVCCM Himo, kuanzia saa 4:00 kamili asubuhi.
Akizungumza na waandishi wa habari, Mwenyekiti wa UVCCM Wilaya ya Moshi Vijijini, Yuvenali Ole Rafaeli Shirima, amesema maadhimisho hayo yanalenga kuwaunganisha vijana, kuimarisha mshikamano, uzalendo na kuwahamasisha kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo ya Taifa.
Amesema maadhimisho hayo yatawakutanisha vijana kutoka maeneo mbalimbali pamoja na viongozi wa Serikali, Chama, taasisi na wadau wa maendeleo kwa ajili ya kujadili nafasi ya vijana katika ujenzi wa Taifa na kuhamasisha matumizi ya fursa mbalimbali za kiuchumi na kijamii.
Shirima ametoa wito kwa vijana wa Wilaya ya Moshi Vijijini, Mkoa wa Kilimanjaro na maeneo mengine kujitokeza kwa wingi kushiriki katika maadhimisho hayo, akisisitiza kuwa vijana ni nguvu muhimu katika kulinda amani na kuharakisha maendeleo ya nchi.
Maadhimisho ya mwaka huu yatafanyika chini ya kaulimbiu isemayo:
“Vijana ni Nguvu ya Taifa; Tushirikiane Kulinda Amani kwa Maendeleo ya Taifa Letu.”
#SikuYaVijanaDuniani2026 #UVCCMMoshiVijijini #VijanaNiNguvuYaTaifa #Kilimanjaro
Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) imeanza mazungumzo na wazalishaji wa parachichi katika wilaya za Mufindi na Njombe kwa lengo la kuanzisha mfumo wa ubunifu utakaoruhusu shamba kutumika kama ghala la bidhaa hai ili kuongeza ufanisi wa biashara ya zao hilo.
Mkurugenzi Mtendaji wa WRRB, Bw. Asangye Bangu, amesema hayo katika Maonesho ya Nanenane yanayoendelea kwenye Viwanja vya Dkt. John Malecela jijini Dodoma wakati akitoa maelezo kwa Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Denis Londo, aliyetembelea banda la WRRB.
Bw. Bangu amesema utaratibu huo utahakikisha matunda yanayovunwa ni yale tu yaliyofikia viwango vinavyohitajika na wanunuzi, jambo litakalopunguza upotevu wa mazao baada ya mavuno, kuhifadhi ubora wa bidhaa na kuongeza thamani ya biashara ya parachichi.
Aidha, amesema WRRB inatarajia kushirikiana na Shirika la Posta Tanzania ili kuunganisha Mfumo wa Stakabadhi za Ghala na huduma za kidijitali za biashara pamoja na usafirishaji wa bidhaa.
Amesema ushirikiano huo unatarajiwa kuongeza ufanisi wa biashara, kurahisisha miamala na kuimarisha imani ya wanunuzi katika soko.
Awali, Kaimu Mkurugenzi wa Uratibu Huduma wa WRRB, Bw. Mwita Thomas, amesema mfumo huo unaendelea kupanuliwa kutoka kwenye mazao ya kilimo pekee na sasa unahusisha pia bidhaa zisizo za kilimo, zikiwamo mifugo hai, mwani na samaki wanaofugwa kwenye vizimba.

Wakala wa Vipimo (WMA) umetakiwa kupanua mpango wa kuanzisha klabu za vipimo shuleni hadi katika shule za sekondari, ili kuongeza wigo wa elimu ya vipimo na kuhakikisha uelewa wa matumizi sahihi ya vipimo unafika hadi ngazi ya kaya.
Wito huo umetolewa na Mhadhiri wa Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE), Patroba Chaulo, ambaye amepongeza WMA kwa kuanzisha klabu hizo katika shule za msingi, akisema matumizi ya wanafunzi kama mabalozi wa elimu ya vipimo ni mkakati wenye tija kubwa kwa jamii.
Amesema mpango huo unatoa fursa ya kutumia mfumo wa elimu wa “mtoto kwa mtoto” (child-to-child), ambapo wanafunzi huweza kufikisha elimu na ujumbe kwa wenzao kwa urahisi zaidi, na hatimaye kuwafikishia wazazi na familia zao.
Kwa mujibu wa Chaulo, njia hiyo inaweza kuwa na ufanisi mkubwa kwa sababu wanafunzi wana nafasi kubwa ya kushirikiana na kuwasiliana na wenzao kwa lugha rahisi na inayoeleweka, jambo linalorahisisha uenezaji wa elimu ya vipimo.
“Mtoto anaweza kumwelewesha mtoto mwenzake kwa urahisi zaidi kuliko mtu mzima anapojaribu kumwelewesha mwanafunzi. Hii inafanya mfumo wa child-to-child kuwa fursa muhimu katika kueneza elimu ya vipimo,” amesema.
Ameeleza kuwa umuhimu wa mpango huo hauishii shuleni pekee, bali unaweza kusaidia elimu ya vipimo kufika hadi ngazi ya kaya, kwa kuwa wanafunzi wanaotoka katika klabu hizo wanaishi katika familia na jamii mbalimbali.
Amesema kupitia wanafunzi hao, WMA inaweza kuwa na mtandao mpana wa mabalozi ambao utasaidia kufikisha ujumbe kuhusu umuhimu wa vipimo sahihi katika maeneo ambayo ni vigumu kwa Wakala kufika moja kwa moja.
“WMA haiwezi kufika katika kila nyumba, lakini wanafunzi hawa wanatoka katika kaya mbalimbali. Hivyo, wanakuwa kiungo muhimu cha kufikisha elimu hii kutoka shuleni hadi katika familia na jamii kwa ujumla,” amesisitiza.
Chaulo amesema elimu hiyo ni muhimu katika kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu matumizi ya vipimo sahihi na vilivyothibitishwa, hususan katika shughuli za kila siku zinazohusisha biashara na miamala mbalimbali.
Amesema jamii yenye uelewa kuhusu vipimo inaweza kutambua umuhimu wa kuhakikisha bidhaa zinapimwa kwa vipimo sahihi na kulinda haki za watumiaji pamoja na wafanyabiashara.
Kwa msingi huo, amependekeza WMA kuendelea kuimarisha klabu hizo katika shule za msingi na kuzitanua hadi shule za sekondari ili kuwafikia vijana wengi zaidi na kujenga kizazi chenye uelewa mpana kuhusu viwango na vipimo.
Ameongeza kuwa uwekezaji katika elimu ya vipimo kupitia shule ni hatua muhimu ya kujenga utamaduni wa matumizi sahihi ya vipimo nchini, huku wanafunzi wakitumiwa kama sehemu ya suluhisho la kufikisha elimu hiyo katika jamii.
Mpango huo pia unatarajiwa kuongeza uelewa wa Watanzania kuhusu umuhimu wa kuwa na viwango na vipimo sahihi na vilivyothibitishwa (standards in measurements) katika maisha ya kila siku, hususan katika shughuli zinazohusisha biashara, ununuzi na uuzaji wa bidhaa.
Na OWM–TAMISEMI, Dar es Salaam
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM–TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, amemhakikishia Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kuwa Ofisi yake itatekeleza kikamilifu jukumu la kuisimamia Wakala wa Mabasi Yaendayo Haraka (DART), kwa lengo la kuhakikisha sera na mipango ya Serikali ya kuboresha usafiri wa umma jijini Dar es Salaam inafanikiwa.
Prof. Shemdoe ametoa kauli hiyo leo, Agosti 7, 2026, jijini Dar es Salaam, alipotoa salamu za OWM–TAMISEMI kwa Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan mbele ya wananchi, mara baada ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kufungua rasmi Mradi wa Mabasi Yaendayo Haraka, Awamu ya Pili (BRT II), unaohusisha barabara za Kilwa, Chang’ombe, Sokoine na Kawawa.
“Mheshimiwa Rais, kazi uliyotupa ya kuisimamia Wakala wa Mabasi Yaendayo Haraka (DART) tutaifanya kwa bidii, weledi na moyo wa uzalendo ili kufanikisha utekelezaji wa sera na mipango ya Serikali ya kuboresha usafiri wa umma,” amesema Prof. Shemdoe.
Akizungumzia mchango wa wadau katika kufanikisha mradi huo, Prof. Shemdoe amewashukuru wadau mbalimbali, wakiwemo Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), TANROADS, wakandarasi, washauri elekezi na watoa huduma, kwa ushirikiano wao uliowezesha kukamilika na kuzinduliwa kwa BRT II.
Amesema mradi huo unalenga kupunguza changamoto za usafiri kwa wakazi wa Dar es Salaam wanaotumia barabara za Kilwa, Chang’ombe, Sokoine na Kawawa, pamoja na kuboresha ufanisi wa usafiri wa umma jijini humo.
Akieleza faida za mabasi ya kisasa ya mwendokasi kwa wananchi na mazingira, Prof. Shemdoe amesema mabasi 60 yaliyoanza kutoa huduma katika njia ya Mbagala–Posta yamechangia kupunguza msongamano wa magari yanayoelekea katikati ya jiji, baada ya kuondoa daladala 400 kati ya daladala 1,627 zilizokuwa zikihudumia wakazi wa eneo hilo.
Amesema hatua hiyo si tu inaboresha usafiri kwa wananchi, bali pia inachangia kupunguza uzalishaji wa hewa yenye kiwango kikubwa cha gesi ya kaboni dioksidi (CO₂), inayozalishwa wakati injini za magari zinapochoma mafuta ya petroli na dizeli.
Kwa hatua hiyo, Serikali inaendelea kuimarisha usafiri wa umma wenye ufanisi na unaozingatia mahitaji ya wananchi, huku ikiweka mkazo katika kupunguza msongamano wa magari na athari za uzalishaji wa hewa ukaa jijini Dar es Salaam.
Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Dennis Londo,akizungumza na waandishi wa habari leo Agosti 7,2026 mara baada ya kutembelea mabanda ya Taasisi zilizochini ya Wizara ya Viwanda na Biashara wakati wa Maonesho ya 33 ya Wakulima Nane Nane yanayoendelea viwanja vya Dkt.John Malecela Nzuguni Jijini Dodoma.
Na Alex Sonna, Dodoma
Mkakati wa Serikali wa kuongeza thamani ya mazao ya kilimo, mifugo na uvuvi kupitia viwanda umeelezwa kuwa ndiyo nguzo ya kujenga uchumi shindani, kuongeza kipato cha wazalishaji na kufungua fursa zaidi za ajira kwa Watanzania.
Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Dennis Londo, amesema Serikali inaendelea kutekeleza mkakati huo kwa kushirikiana na taasisi zilizo chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara ili kuhakikisha mazao yanayozalishwa nchini yanachakatwa, yanaongezewa thamani na kuingia sokoni kama bidhaa zenye ubora na ushindani.
Akizungumza katika Maonesho ya Kimataifa ya Kilimo ya Nane Nane,Mhe. Londo amesema mazao ya kilimo, mifugo na uvuvi ni malighafi muhimu kwa maendeleo ya viwanda, hivyo Serikali imeweka mazingira yatakayowezesha mnyororo wa thamani kuanzia uzalishaji, uchakataji hadi masoko ya ndani na nje ya nchi kwa mujibu wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Amesema taasisi za wizara hiyo, zikiwemo BRELA, TBS, Tume ya Ushindani (FCC),Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB),SIDO na Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE), zinaendelea kusogeza huduma karibu na wananchi kwa kutoa elimu, usajili wa biashara, viwango vya ubora na huduma nyingine zinazolenga kuwajengea uwezo wazalishaji na wafanyabiashara kushiriki kikamilifu katika uchumi wa viwanda.
Aidha, amesema Serikali ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuboresha mazingira ya biashara kwa kuwekeza katika barabara, madaraja, vivuko, umeme wa REA na miundombinu ya mawasiliano ili kupunguza gharama za uzalishaji, kurahisisha usafirishaji wa bidhaa na kuwapa wananchi taarifa sahihi za masoko zinazowaongezea tija.
Mhe.Londo amewataka wananchi kutembelea banda la Wizara ya Viwanda na Biashara katika maonesho hayo ili kupata elimu na huduma mbalimbali zinazotolewa na taasisi zake, akisisitiza kuwa kuongeza thamani ya mazao ndiyo njia ya kuimarisha viwanda vya ndani, kuongeza mapato ya wananchi na kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha biashara na uzalishaji wa bidhaa zenye ushindani.

Mradi wa Kituo cha Kuongeza Msukumo wa Mafuta (Pump Station 3 – PS3) katika Mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP), kilichopo Wilaya ya Muleba mkoani Kagera, umefikia asilimia 88 ya utekelezaji na unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa Agosti au mwanzoni mwa Septemba mwaka huu.
Hayo yameelezwa Agosti 7, 2026 na Mkurugenzi wa Mipango na Uwekezaji wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), Bw. Derick Moshi, wakati wa ziara ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa kituo hicho.
Bw. Moshi amesema PS3 ni kituo cha tatu katika mradi wa EACOP kuanzia Uganda na cha kwanza upande wa Tanzania. Amefafanua kuwa kazi zote kuu za ujenzi zimekamilika na kinachoendelea ni kazi za ukamilishaji pamoja na majaribio ya mifumo kabla ya kituo kuanza kufanya kazi.
Aidha, amesema mradi huo umekuwa shamba darasa kutokana na ushirikiano mzuri kati ya Serikali na sekta binafsi katika utekelezaji wake, jambo lililowezesha kubadilishana ujuzi, kujenga uwezo wa wataalamu wa ndani na kuimarisha ushirikiano katika miradi mikubwa ya kimkakati.
Ameongeza kuwa mradi huo unaendana na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kwa kuimarisha ushiriki wa sekta binafsi katika maendeleo ya sekta ya nishati na kuendeleza miundombinu ya kisasa. Pia amesema kukamilika kwa PS3 kutachangia usafirishaji salama na wenye ufanisi wa mafuta ghafi kutoka Uganda kupitia Tanzania, hatua itakayochochea ukuaji wa uchumi na kuongeza nafasi ya Tanzania kama kitovu cha miundombinu ya nishati katika ukanda wa Afrika Mashariki.
Kwa upande wake, Kiongozi wa Timu ya Mkandarasi wa Kituo hicho, Dmitry Malyshev, amesema ameridhishwa na ziara ya wataalamu kutoka Wizara ya Nishati na TPDC kwani imewapa fursa ya kupokea maoni na maelekezo ya kitaalamu yatakayosaidia kukamilisha mradi kwa ubora, usalama na kwa kuzingatia viwango vinavyohitajika.
Yawataka wananchi kujiunga mapema kujikinga na gharama za matibabu
Na Grace Michael, Dodoma
MFUKO wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) umewahimiza wananchi nchini kujiunga na bima ya afya kabla ya kuugua, ukieleza kuwa ni njia salama ya kujikinga dhidi ya gharama kubwa za matibabu ambazo zinaweza kujitokeza wakati wowote.
Wito huo umetolewa leo Agosti 07, 2026 na Meneja Masoko na Huduma kwa Wateja wa NHIF, Angela Mziray, wakati akitoa elimu kwa wananchi waliotembelea banda la Mfuko katika Maonesho ya 49 ya Kilimo ya Nanenane yanayoendelea katika viwanja vya Nzuguni, mkoani Dodoma.
Bi. Mziray amesema maonesho hayo yameipa NHIF fursa ya kuwafikia wananchi wengi na kuwaelimisha kuhusu umuhimu wa kuwa na bima ya afya, sambamba na utekelezaji wa Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote inayolenga kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma za matibabu bila vikwazo vya kifedha.
Amesema changamoto za kiafya zinaweza kumpata mtu yeyote bila kutarajia, na mara nyingi husababisha familia nyingi kutumia akiba zao au hata kuuza mali ili kugharamia matibabu.
“Ugonjwa huja bila taarifa. Unaweza kuwa mzima leo lakini kesho ukahitaji matibabu ya gharama kubwa. Ndiyo maana tunawahimiza wananchi kujiunga na bima ya afya mapema ili wajenge kinga ya kifedha kwao na kwa familia zao," amesema Bi. Mziray.
Amefafanua kuwa mwananchi anapochangia bima ya afya kabla hajaugua, hupata uhakika wa matibabu bila kubeba mzigo mkubwa wa gharama wakati wa uhitaji.
“Ni muhimu wananchi wajidundulize kidogo kidogo na kuchangia bima ya afya. Hii ndiyo njia bora ya kuhakikisha familia inapata huduma za matibabu kwa wakati bila kuathiri mipango ya maendeleo," amesema.
Bi. Mziray amesema NHIF inaendelea kutoa elimu katika maeneo mbalimbali nchini ili kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu faida za bima ya afya na kuhamasisha matumizi ya mfumo wa bima badala ya kulipia matibabu moja kwa moja kutoka mfukoni.
Ameongeza kuwa wanachama wa NHIF wanapata huduma katika mtandao mpana wa vituo vya afya vya Serikali, binafsi na vya mashirika ya dini vilivyosajiliwa na Mfuko, jambo linalowapa urahisi wa kupata huduma popote wanapozihitaji.
Aidha, amesema kuwa na bima ya afya siyo tu kulinda afya ya mtu binafsi, bali pia ni kulinda uchumi wa familia kwa kupunguza matumizi yasiyotarajiwa yanayotokana na matibabu.
Katika Maonesho ya Nanenane, NHIF inaendelea kutoa huduma mbalimbali ikiwemo usajili wa wanachama wapya, elimu kuhusu vifurushi vya bima ya afya, ushauri kwa wanachama pamoja na ufafanuzi wa utekelezaji wa Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote.
Wananchi wanaotembelea banda la NHIF pia wanapata fursa ya kuuliza maswali, kupata majibu kuhusu huduma za Mfuko na kujiunga na bima ya afya papo hapo, hatua inayochangia kuongeza uelewa na ushiriki wa jamii katika kuhakikisha kila Mtanzania anakuwa na kinga ya kifedha dhidi ya gharama za matibabu.

Na.Mwandishi Wetu
Tume ya Ushindani (FCC) imetajwa kuwa mdau muhimu katika kuongeza thamani ya mazao ya Watanzania kupitia elimu ya ushindani wa haki na ulinzi wa mlaji, hatua inayowasaidia wazalishaji na wafanyabiashara kuboresha ubora wa bidhaa zao na kuzifanya zishindane katika masoko ya ndani na kimataifa.
Kauli hiyo imetolewa leo Agosti 7,2026 na Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Dennis Londo, alipotembelea banda la FCC katika Maonesho ya Kimataifa ya Kilimo ya Nanenane yanayoendelea katika viwanja vya Nzuguni jijini Dodoma. Amesema elimu inayotolewa na tume hiyo imeendelea kujenga uelewa kwa wananchi kuhusu umuhimu wa ushindani wa haki, ulinzi wa mlaji na kuongeza thamani ya bidhaa za Tanzania.
Ameipongeza FCC kwa kuendelea kushirikiana na wadau mbalimbali katika kuimarisha mazingira ya biashara, akieleza kuwa juhudi hizo zinaendana na dira ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kukuza sekta za uzalishaji kupitia soko lenye ushindani wa haki, uwazi na fursa sawa kwa wote.
Mhe. Londo ameihimiza FCC kuendelea kutumia Maonesho ya Nanenane na majukwaa mengine kuwafikia wananchi wengi zaidi ili kuongeza uelewa kuhusu sheria za ushindani na ulinzi wa mlaji, akisisitiza kuwa elimu hiyo ni nyenzo muhimu ya kuongeza thamani ya mazao, kuvutia masoko mapya na kuongeza kipato cha wazalishaji.
Aidha, ametoa wito kwa wakulima, wafugaji, wavuvi na wajasiriamali kwenda kuitumia vizuri elimu iliyotolewa na FCC kuboresha uzalishaji wao, kuzingatia sheria za ushindani na kuepuka vitendo vinavyovuruga soko, akieleza kuwa hatua hiyo itachangia kujenga uchumi shindani na kuongeza mchango wa sekta za uzalishaji katika maendeleo ya taifa.




























