Naibu Waziri wa Nishati Mhe. Salome Makamba amefanya ziara katika  Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) pamoja na Mamlaka ya Udhibiti wa Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA) kwa lengo la kuzungumza na Watendaji taasisi hizo mara baada ya kuteuliwa na Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kushika nyadhifa hiyo  ambapo amewataka watendaji kuhakikisha  Watanzania wananufaika moja kwa moja na uwepo wa rasilimali za mafuta na gesi.

Katika mazungumzo hayo yaliyofanyika jijini Dar es Salaam, Mhe. Salome ameweka mkazo kuhusu upatikanaji wa ajira kwa Watanzania, huduma za kijamii na upatikanaji wa nishati kwa gharama nafuu. 

Mhe. Salome pia ameielekeza Menejimenti ya TPDC kuongeza kasi ya usambazaji wa gesi asilia majumbani ili Watanzania waendelee kunufaika zaidi na rasilimali hiyo muhimu.

Vilevile  ameipongeza TPDC kwa jitihada wanazoendelea kufanya katika utafutaji na uendelezaji wa rasilimali za mafuta na gesi asilia nchini kwani uboreshaji huo umeanza kuleta matokeo chanya katika upatikanaji wa nishati hiyo katika maeneo mbalimbali nchini huku akiwataka kuhakikisha jitihada hizo zinawanufaisha wananchi wengi zaidi.

Katika hatua nyingine, Mhe. Salome amewapongeza PURA kwa kazi nzuri wanazozifanya katika kuhakikisha sekta ya mafuta inakua nchini huku akiwahimiza kuhakikisha mazingira ya uwekezaji yanakuwa rafiki kwa wawekezaji wapya ili kuongeza ajira na kuhakikisha wananchi wanapata manufaa ya moja kwa moja kutokana na rasilimali na uwekezaji uliopo nchini.  

Aidha, amesisitiza kuwa miradi ya utafiti na uendelezaji wa gesi asilia, ikiwemo mradi wa LNG, ipewe kipaumbele ili kuongeza tija katika uwekezaji na kuhakikisha nchi inanufaika kikamilifu na rasilimali zake huku akisisitiza kuwa taasisi zote zilizo chini ya Wizara lazima ziweke mbele maslahi ya wananchi wakati wa kusimamia miradi ya kimkakati ya nishati lakini pia kufuatilia utekelezaji wa maagizo ya Serikali kuhusu usimamizi, matumizi na faida za rasilimali za gesi asilia.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Dkt. James Mataragio amewasisitiza TPDC kuongeza kasi ya uzalishaji na upatikanaji wa  gesi ili nishati hiyo iwe ya kutosha na inawafikia wananchi huku akiisisitiza PURA kuhakikisha wanawapa wawekezaji kipaumbele katika kuwekeza katika fursa za mafuta na gesi kwa lengo la kuhakikisha Serikali inapata mapato na wananchi wananufaika na miradi hiyo.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa TPDC Mussa Makame amesema shirika linaendelea kuimarisha miundombinu ya kuhifadhi na kusafirisha nishati ya mafuta na gesi, huku likiandaa vizuri upande wa maboresho ya masoko ili kuongeza ufanisi na upatikanaji wa bidhaa hizo nchini na kueleza kuwa kampuni ipo kwenye hatua za kufanya upanuzi wa miradi ya gesi, ikiwemo utekelezaji wa miradi midogo ya LNG itakayowezesha kusafirisha gesi hiyo katika mikoa mbalimbali kwa gharama nafuu na kwa wakati.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa PURA, Eng. Charles Sangweni amesema PURA itaendelea kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi huku ikichangia kufanikisha malengo ya sekta kwa mujibu wa Dira ya Taifa 2050.

















Kampuni ya Noble Helium kutoka Australia imetangaza mpango wa kuajiri zaidi ya vijana 50 kupitia utafiti mpya wa Helium unaotarajiwa kuanza mwezi Desemba hadi Februari katika kijiji cha Kinambo, Wilayani Sumbawanga mkoani Rukwa.

Akizungumza kupitia mahojiano maalum hivi karibuni Mwakilishi wa Kampuni hiyo, Pius Simeon Mwita, alisema Noble Helium imefanikisha tafiti mbalimbali za awali na kubaini viashiria muhimu vya uwepo wa gesi ya Helium, huku ikichangia ajira na maendeleo kwa jamii zinazozunguka maeneo ya uchimbaji.

Mwita alisema katika tafiti zilizopita kampuni ilitoa ajira zisizo rasmi zipatazo 450, na pia ilishirikisha wananchi kwenye utoaji wa huduma kama ulinzi, usambazaji wa bidhaa, vilainishi kwa shughuli za uchorongaji, zabuni ndogo, ununuzi wa chakula pamoja na uboreshaji wa miundombinu ya barabara.

Aidha, alisema Noble Helium imekamilisha tathmini na ulipaji wa fidia kwa wananchi waliopo katika maeneo ya leseni ya utafiti wa Helium, ikiwa ni sehemu ya kuhakikisha shughuli za kampuni zinaendeshwa kwa kuzingatia maslahi ya jamii na sheria za nchi.

Kwa mujibu wa Mwita, utafiti mpya utakaofanyika Kinambo utaongeza nafasi nyingine zaidi 50 kwa vijana, na hivyo kuchochea maendeleo ya kiuchumi katika eneo hilo. 

“Tunawaomba vijana wajitokeze kwa wingi pindi fursa hizi zitakapotangazwa. Lengo letu ni kuhakikisha jamii inanufaika moja kwa moja na uwekezaji huu,” alisema.

Utafiti huo unatarajiwa kuongeza kasi ya maandalizi ya uwekezaji mkubwa wa Helium nchini, gesi ambayo imekuwa na mahitaji makubwa duniani kwa matumizi ya teknolojia za tiba, anga na vifaa vya sayansi.

 



Na Oscar Assenga, MUHEZA

VIKUNDI 29 vya Wanawake,Vijana na Watu Wenye ulemavu wamekabidhiwa Milioni 250 zinazotokana na mikopo asilimia 10 kutoka katika Halmashauri ya wilaya ya Muheza ikiwa ni kuwawezesha kujikwamua kiuchumi wao na jamii zao.

Makabidhiano ya Hundi ya Fedha hizo ilitolewa na Mkuu wa Mkoa wa Tanga Dkt,Balozi Batilda Burian na kushuhudiwa na viongozi mbalimbali wa wilaya ya Muheza akiwemo Mkuu wa wilaya,Mkurugenzi wa Halmashauri,Mwenyekiti wa Halamshauri na Madiwani wa Halmshauri hiyo.

Akizungumza baada ya kukabidhi mikopo hiyo ,Mkuu huyo wa Mkoa aliwaasa wanufaika wa mikopo ya asilimia 10 ya Halmashauri kuitumia kwa uangalifu ili kuweza kujikwamua kiuchumi pamoja na kuhakikisha wengine nao wananufaika na fursa hizo.

Alisema kwamba dhamira ya Rais Dkt Samia Suluhu ni kuona mikopo hiyo inawafikia wahitaji bila kuwepo kwa vikwazo vya aina yoyote kupitia mfumo wa mtandao bila kuhitaji kumjua mtu .

Aidha alitoa wito kwa vijana kujitokeza kwa wingi kuchangamkia fursa za uwepo wa mikopo hiyo ili waweze kujikwamua kiuchumi.

“Tumekubaliana kuandaa kongamano la vijana litakalowakutanisha maafisa maendeleo ya jamii na wadau wa mikopo kwa lengo la kuwaelimisha juu ya mchakato mzima wa kuipata na jinsi ya kuunda vikundi imara”Alisema

Mkuu huyo wa mkoa alisema lengo ni kuhakikisha kila kijana anakuwa na uelewa hatua za kuomba mikopo na kutumia fursa zilizopo.

Awali akizungumza Mkuu wa wilaya ya Muheza Ayoub Sebabili alisema kwamba mikopo iliyozinduliwa ya asilimia 10 ,wanawake asilimia 4,vijana 4 na walemavu 2 huku akimpongeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Muheza Dkt Jumaa Mhina na menejimentii ya halmshauri kwa kuratibu vizuri mikopo na kuwafikia walengwa.

Aliwaomba wanufaika wa mikopo hiyo watoa ushirikiano kwenye marejesho ili kuweza kutoa nafasi watu wengine kupata mikopo kwa lengo la kukuza kipato na kujikwamua kiuchumi.





“Tunaopokea mikopo hii tutoe ushirikiano wakati wa marejesho kwa sababu utapelekea mfuko wa mikopo uweze kuwa endelevu na kuwafikia watu wengine na hivyo kuondoa umaskini kwa mtu mmoja mmoja na wengine kunufika nayo”Alisisitiza



Naye kwa upande wake Mkurugenzi wa Halmshauri ya Muheza Dkt Jumaa Mhina alimpongeza Mkuu huyo wa wilaya akieleza kwamba ndio muhimili wa halmashauri kuhakikisha asilimia 10 inatoka na kufikia vikundi hivyo.


Dkt Jumaa alisema kwamba wameweka mkazo kwa vikundi vyote lakini hususani kwa vijana ambao siku za nyuma walikwa wanawatafuta kwa tochi hivyo sasa watawafuata vijana walipo ili kuwaibua waweze kuunda vikundi na hivyo kunufaika na mikopo asilimia 10 ikiwa ni sehemu ya kutengeneza ajira .



Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Mhe. Anthony Mtaka,akizungumza katika Ibada ya Jumamosi katika Kanisa la Waadventista Wasabato (SDA) Njombe Mjini.

Na Mwandishi Wetu, Njombe

Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Mhe. Anthony Mtaka, amewataka vijana wa kizazi kipya (Gen-Z) na wananchi kwa ujumla kuimarisha mshikamano na kuilinda amani ya Tanzania, akisisitiza kuwa ndiyo nguzo muhimu ya maendeleo ya taifa.

Akizungumza katika Ibada ya Jumamosi katika Kanisa la Waadventista Wasabato (SDA) Njombe Mjini, RC Mtaka amesema vijana wana nafasi kubwa katika kuhakikisha nchi inaendelea kuwa kisiwa cha amani.

“Vijana wetu wa Gen-Z wana wajibu wa kulinda amani ya Tanzania; ninyi ndiyo kizazi kinachobeba matumaini na sura ya taifa letu,"amesema.

Aidha, ameongeza kuwa amani ni matokeo ya haki na uwajibikaji wa kila mwananchi.

“Amani ni tunda la haki na wajibu, ni msingi thabiti wa maendeleo yetu kama jamii na kama taifa. Tuna wajibu wa kuilinda amani ya nchi yetu kwa wivu mkubwa… ni jukumu letu vijana wa leo kuitunza amani yetu kwa faida ya vizazi vilivyopo na vijavyo,"amesema.

Akizungumzia hali ya usalama mkoani Njombe, Mtaka amewahakikishia wananchi kuwa mazingira bado ni salama na hakuna viashiria vya kuvuruga utulivu.

“Mkoa wetu bado upo salama, hauna matishio ya kihalifu. Tunaendelea kujenga mazingira thabiti ya ulinzi wa watu na mali ili kutoa fursa kwa wananchi kuendelea na shughuli zao za uzalishaji. Usalama huu utaongeza imani kwa wawekezaji kuendelea kuchagua Njombe kama sehemu sahihi ya kuweka mitaji,” amesema.

Hata hivyo, amewataka wananchi kuendelea kushirikiana na vyombo vya dola kwa kutoa taarifa za mapema pale wanapohisi au kuona dalili za kuvunjika kwa amani.

“Wananchi wenzangu, mkiona au kuhisi dalili yoyote hata ndogo inayoashiria uvunjifu wa amani au kuhatarisha usalama wa eneo lenu au maisha ya mtu, basi mtoe taarifa mapema. Ulinzi shirikishi huanza na wanajamii mmoja mmoja,” amesisitiza.

Amehimiza umoja, uzalendo na uadilifu wa wananchi wote ili kuendelea kujenga Njombe yenye fursa, utulivu na maendeleo endelevu.

Makundi mbalimbali ya Vijana wanajishughulisha na shughuli mbalimbali za kajamii ikiwemo bodaboda wametakiwa kuacha kujihusisha na matukio yenye kuharibu amani ya nchi na badala yake wawe mstari wa mbele katika kuilinda na kuitunza amani iliyopo.

Hayo yamesemwa na mbunge wa jimbo la korogwe vijijini Mheshimiwa Timotheo Mnzava katika ziara yake ya kukutana na makundi mbalimbali ikiwemo vijana wanaojishughulisha na shughuli mbalimbali za kiuchumi ikiwemo madereva bodaboda.

Akizungumza na vijana wa jimbo hilo amesisitiza kuwa ni vyema kuilinda amani iliyopo kwa nguvu zote huku akisistiza vijana hao kutojihusisha katika maandamano yanayotajwa kufanyika desemba 9 ambayo si halali kisheria kwani wapo baadhi ya vijana walioweza kupata athari mbalimbali ikiwemo ulemavu katika maandamano ya oktoba 29.

Kwa upande wao baadhi ya vijana hao wameahidi kutojihusisha na matukio ya ukatili badala yake watakuwa mabalozi wazuri wa amani.

MKUU wa Wilaya ya Bagamoyo, Shaibu Ndemanga, amewapongeza Wakala wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu (ADEM) kwa kuratibu na kushiriki kikamilifu mbio za marathon zilizolenga kuhamasisha juhudi za kuboresha miundombinu ya elimu katika chuo hicho.
   

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda, amesema kuwa Serikali inawetegemea wanasayansi na wahandisi ili kufanikisha dhamira ya Tanzania ya kujenga uchumi wa viwanda, amesisitiza kuwa kundi hilo lina mchango katika kuendeleza ubunifu, kuongeza tija na kuleta maendeleo endelevu nchini.

Prof. Mkenda amesema hayo Disemba 5, 2025 jijini Dar es Salaam katika Mahafali ya 19 ya Taasisi ya Teknolojia ya Dar es Salaam (DIT), akisema katika kutimiza azma hiyo Serikali imeendelea kuongeza fursa za mafunzo na Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi ili kusimamia ubora wa elimu sambamba na utekelezaji wa Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014, Toleo la 2023.

"Mhe Dkt. Samia Suluhu Hassan amedhamiria kuleta mageuzi ya elimu, kwa kuwawezesha watanzania hususan vijana kupata maarifa, stadi na ujuzi ili kuchangia maendeleo ya kijamii na kiuchumi" Amesema Waziri Mkenda.

Amebainisha kuwa, Serikali kupitia mkopo nafuu wa Benki ya Dunia imewekeza jumla ya Dola za Marekani milioni tisini (90) ambapo kupitia fedha hizo Taasisi ya DIT, imeanzisha Kituo cha Umahiri cha Kikanda cha Mafunzo ya TEHAMA (RAFIC) katika Kampasi ya Dar es Salaam na Kituo cha Umahiri cha Uchakataji bidhaa za ngozi (CELPAT) kampasi ya Mwanza.

Ameipongeza DIT kwa kuendelea kutoa mafunzo bora, sambamba na kutambua, kujenga, kukuza na kuendeleza bunifu. Amesema kuwa Serikali inajivunia juhudi hizo na ameisisitiza kuendelea kusimamia majukumu yake kikamilifu.

Mkuu wa Taasisi ya DIT, Profesa Preksedis Ndomba, amesema kuwa Taasisi hiyo imejikita katika dhana ya ufundishaji inayotilia mkazo mafunzo kwa vitendo pamoja na ziara za mafunzo viwandani, ambayo imewasaidia wanafunzi kuwa wabunifu na kufikia viwango vya kuanzisha makampuni.

Naye, Mwenyekiti wa Baraza la Taasisi hiyo, Dtk. Richard Masika ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutenga zaidi ya Sh. Bilioni mbili katika mwaka wa fedha 2025/26, ili kuanzisha Kituo cha Ujasiriamali, Ubunifu na Uhawilishaji wa Teknolojia kupitia Mradi wa TELM II.

Kumbuka, Mradi huo wa miaka miaka mitano (2025/2030) unatekelezwa kwa bajeti ya Euro milioni 19.79 (sawa na Sh. Bilioni 54). Fedha hizo ni mkopo nafuu kutoka Serikali ya Italia kwa Serikali ya Tanzania kupitia makubaliano rasmi.

Taasisi zingine zinazonufaika na Mradi wa TELMS II, ni Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia Mbeya (MUST), Chuo cha Ufundi Arusha (ATC) na Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Karume (KIST).

Katika duru ya kwanza ya mahafali hayo, Waziri Mkenda amewatunuku vyeti jumla ya wahitimu 1,341 katika ngazi za Astashahada, Stashahada, Shahada na Shahada ya Uzamivu katika nyanja za Sayansi na Teknolojia. Kati ya hao, wanaume ni 1,003 na wanawake 338.



Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC) imefanikisha kuendesha mafunzo ya kitaifa ya siku nne kuhusu usalama wa mionzi ya mashine za X-Ray na vyanzo vingine vya mionzi vinavyotumika katika upigaji picha za kitabibu kwa binadamu.

Mafunzo hayo yalifanyika kuanzia Jumatatu, tarehe 1 hadi Alhamisi, tarehe 4 Desemba 2025, katika ofisi za TAEC Kanda ya Kaskazini jijini Arusha, na yalihusisha takribani washiriki 50 kutoka sekta mbalimbali muhimu nchini.

Mafunzo hayo yalifunguliwa rasmi na kufungwa na Dkt. Denis Mwalongo, Mkuu wa Kanda ya Kaskazini wa TAEC, aliyesimamia hafla hizo kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa TAEC, Prof. Najat Kassim Mohammed.

Katika hotuba yake ya ufunguzi, Dkt. Mwalongo alisisitiza umuhimu wa usalama wa mionzi katika kulinda wafanyakazi, wagonjwa, umma na mazingira.

Alibainisha kuwa mafunzo hayo ni kielelezo cha dhamira ya TAEC ya kuendelea kujenga uwezo wa kitaifa katika matumizi salama ya vifaa vya nyuklia.

“Mafunzo haya si suala la kufuata taratibu pekee; ni kuhusu kukuza utamaduni wa uwajibikaji na uelewa miongoni mwa wataalamu wanaofanya kazi na vifaa vinavyotoa mionzi,” alisema Dkt. Mwalongo.

Mafunzo yalilenga kuwapatia washiriki ujuzi wa nadharia na vitendo kuhusu usalama wa mionzi. Mada kuu zilizojadiliwa ni pamoja na: Utangulizi wa mionzi ayonisha, Vipimo na viwango vya mionzi, Matumizi ya mionzi ionizishi, Athari za kibaolojia za mionzi, Muhtasari wa mionzi isiyo ionizishi, Udhibiti wa kisheria wa vyanzo vya mionzi Tanzania, Mfumo wa kimataifa wa ulinzi wa mionzi, Vipengele vya udhibiti wa mionzi kazini, Hatua za ulinzi wa mionzi kwa wafanyakazi, Uboreshaji wa ulinzi wa mionzi katika ICT, Ubunifu wa majengo na vipengele vya usalama, Mpango wa uthibitisho wa ubora kwa mionzi ya kitabibu, Uboreshaji wa ulinzi wa mionzi kwa watoto, Uundaji wa programu za ulinzi wa mionzi, Upimaji na ufuatiliaji wa mionzi, Mionzi ya kitabibu na usimamizi wa dozi kwa wagonjwa, Uboreshaji wa ulinzi wa mionzi katika radiografia, Vipengele vya ulinzi wa mionzi katika radiografia ya kidigitali, Majukumu ya Maafisa Usalama wa Mionzi (RSOs)
Aidha, washiriki walitembelea Maabara ya Dosimetry na Maabara ya Secondary Standard Dosimetry Laboratory (SSDL) ya TAEC, ambapo walipata nafasi ya kutekeleza taratibu za usalama wa mionzi kwa vitendo.

Mafunzo haya yalilenga kuongeza uelewa, kuboresha ujuzi wa kiufundi, na kuhamasisha matumizi salama ya vyanzo vya mionzi katika sehemu za kazi. Kupitia mafunzo haya, TAEC inaendelea kuimarisha uwezo wa kitaifa katika usalama wa mionzi.

TAEC ina jukumu kubwa la kudhibiti na kuendeleza matumizi salama ya teknolojia ya nyuklia nchini Tanzania. Hatua zake zinaendana na viwango vya kimataifa na zinachangia katika malengo ya maendeleo ya taifa, kuhakikisha kuwa sayansi na teknolojia ya nyuklia zinatumika kwa uwajibikaji na usalama katika sekta ya afya.

Akitoa ujumbe wa Mkurugenzi Mkuu, Dkt. Mwalongo alieleza shukrani za Prof. Najat Kassim Mohammed kwa washiriki na kusisitiza maono ya TAEC kwa siku zijazo:

“Usalama wa mionzi ni kiini cha dhamira yetu ya kulinda maisha huku tukisonga mbele na teknolojia ya kitabibu. Kupitia uwekezaji katika mafunzo na ujenzi wa uwezo, TAEC inathibitisha upya kujitolea kwake kuhakikisha Tanzania inabaki mstari wa mbele katika matumizi salama na yenye uwajibikaji ya teknolojia ya nyuklia,” alisema Prof. Najat Kassim Mohammed.

Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania (TAEC) ndiyo mamlaka ya kitaifa yenye jukumu la kudhibiti, kuendeleza, na kuhakikisha matumizi salama ya teknolojia ya nyuklia nchini.


Kupitia mafunzo, utafiti, na udhibiti wa kisheria, TAEC inalinda afya, usalama na mazingira huku ikisaidia maendeleo ya kisayansi na kiteknolojia ya taifa.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete akizungumza na Watendaji na Menejimeti ya Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) wakati alipofanya ziara ya kikazi iliyolenga kuhimiza uwajibikaji katika ofisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam

Sehemu ya Watendaji na Menejimenti ya Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) wakimsikiliza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (hayupo pichani) wakati Waziri huyo alipofanya ziara ya kikazi iliyolenga kuhimiza uwajibikaji katika ofisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray akizungumza na Watendaji na Menejimeti ya Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) kabla ya kumkaribisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (aliyekaa) kuzungumza na Watendaji hao walipokuwa kwenye ziara ya kikazi iliyolenga kuhimiza uwajibikaji katika ofisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam

Mkurugenzi Mtendaji wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF), Bw. Shadrack Mziray akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa shughuli za TASAF kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (hayupo pichani) wakati wa ziara ya kikazi ya Waziri huyo iliyolenga kuhimiza uwajibikaji kwa watumishi wa ofisi hiyo jijini Dar es Salaam.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (kushoto) akifuatilia taarifa ya utekelezaji wa shughuli za Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) iliyokuwa ikiwasilishwa na Mkurugenzi Mtendaji wa TASAF, Bw. Shadrack Mziray (hayupo pichani) wakati wa ziara ya kikazi ya Waziri huyo iliyolenga kuhimiza uwajibikaji katika ofisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam. Kulia ni Naibu Waziri, Ofisi ya Rais-UTUMISHI na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (katikati) akifurahia jambo na Mkurugenzi Mtendaji wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF), Bw. Shadrack Mziray (wa kwanza kulia) wakati wa ziara ya kikazi ya Waziri huyo iliyolenga kuhimiza uwajibikaji kwa watumishi wa ofisi hiyo jijini Dar es Salaam. Wa kwanza kushoto ni Naibu Waziri, Ofisi ya Rais-UTUMISHI na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete akisaini kitabu cha wageni mara baada ya kuwasili katika ofisi za Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) wakati alipofanya ziara ya kikazi katika ofisi hiyo iliyolenga kuhimiza uwajibikaji kwa watumishi wa ofisi hiyo jijini Dar es Salaam.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (kushoto) akisalimiana na Naibu Waziri wa Ofisi yake, Mhe. Regina Qwaray mara baada ya kuwasili katika ofisi za Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) kwa lengo la kufanya ziara ya kikazi ili kuhimiza uwajibikaji kwa watumishi wa ofisi hiyo jijini Dar es Salaam.

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray (Wa kwanza kulia) akizungumza jambo na Viongozi na Watendaji wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) mara baada ya Naibu Waziri huyo kuwasili katika ofisi hizo kwenye ziara ya kikazi iliyolenga kuhimiza uwajibikaji kwa Watumishi wa ofisi hiyo jijini Dar es Salaam.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (meza kuu kushoto) na Naibu Waziri wa Ofisi yake, Mhe. Regina Qwaray wakifuatilia taarifa ya utekelezaji wa shughuli za Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) iliyokuwa ikiwasilishwa na Mkurugenzi Mtendaji wa TASAF, Bw. Shadrack Mziray (aliyesimama) wakati wa ziara ya kikazi ya Viongozi hao iliyolenga kuhimiza uwajibikaji katika ofisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam. Wengine ni Watendaji na Menejimenti ya TASAF.

Sehemu ya Watendaji na Menejimenti ya Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) wakimsikiliza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (hayupo pichani) wakati Waziri huyo alipofanya ziara ya kikazi iliyolenga kuhimiza uwajibikaji katika ofisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (waliokaa katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Menejimenti ya Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) jijini Dar es Salaam wakati wa ziara yake ya kikazi iliyolenga kuhimiza uwajibikaji wa Watumishi wa ofisi hiyo.


Na Veonica Mwafisi-Dar es Salaam


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete ameielekeza Menejimenti ya Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) kufanya tathmini na ufuatiliaji wa shughuli za Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini ili kuona ni kwa kiwango gani malengo ya Mpango huo yanafikiwa, kubainisha changamoto na kuzishughulikia ili kuboresha utendaji kazi na matokeo yanayotarajiwa.

Mhe. Kikwete ameyasema hayo leo tarehe 05 Disemba, 2025 alipokuwa akizungumza na Menejimenti ya TASAF wakati wa ziara yake ya kikazi iliyolenga kuhimiza uwajibikaji kwa watumishi wa TASAF jijini Dar es Salaam.

Amesema kufanya tathmini kutafichua mambo mengi ambayo yalikuwa hayajulikani katika utekelezaji ambapo itasaidia kuboresha awamu nyingine ya Mpango.

“Tufanye tathmini tuangalie kwanini kunakuwa na utofauti katika mafanikio ili tuone tunasaidiaje, je wasimamizi wa eneo fulani wana ubunifu zaidi kuliko wa eneo lingine? Amejiuliza, na kuongeza kuwa haya mambo ni vizuri yakawa shirikishi ili kuboresha zaidi tutakapoingia kwenye awamu nyingine ya Mpango,” Mhe. Kikwete ameongeza

Aidha, ameitaka TASAF kuzungumza mafanikio na changamoto za utekelezaji wa mradi huo kwa walengwa na wananchi. “Tutoke, tuseme mafanikio na changamoto kwanini wamekosa, watu waambiwe ukweli, TASAF imefanya mambo makubwa, tuwaonyeshe waliohitimu, wamefanya nini mpaka kufanikiwa na walioshindwa kufanikiwa wanatakiwa kufanya nini.” Mhe. Kikwete amesisitiza.

Mhe. Kikwete ameipongeza taasisi hiyo kwa kazi nzuri waliyoifanya kwa uendelea kuhawilisha ruzuku kwa kaya maskini zinazokidhi vigezo vya Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini pamoja na kutekeleza miradi ya maendeleo kwenye Sekta za Afya, Elimu, Maji, Mazingira na ujasiriamali.

Pamoja na pongezi hizo ameitaka TASAF kuendelea kuboresha shughuli za kuwezesha utekelezaji wa Miradi ya Jamii ya kutoa Ajira ya muda ili kupunguza changamoto ya ukosefu wa Ajira, kuwezesha jamii kutekeleza miradi ya kuendeleza miundombinu ya huduma za jamii katika Sekta za Afya, Elimu, Maji, Mazingira na ujasiriamali na uendelea kufungamanisha mikakati mbalimbali ya kuwezesha wananchi kiuchumi ili kuhakikisha matokeo yanayopatika kwenye kila mkakati yanaharakisha kasi ya kuondoa umaskini wa wananchi.

Vile vile ameitaka Taasisi hiyo kuimarisha miundombinu ya mifumo ili kulinda usalama wa taarifa za walengwa na kuungamanisha mifumo wa walengwa na mifumo mingine ya Serikali pamoja na kuongeza idadi ya walengwa wanaolipwa kwa njia za kielekitroniki ili kupunguza dosari za malipo ya ruzuku.

Mhe. Kikwete amesema malengo makubwa ya yeye na Naibu Waziri Mhe. Mhe. Regina Qwaray kutembelea TASAF leo ni kujitambulisha na kuendelea kufanya kazi kwa ushirikiano ili kufikia malengo ya TASAF yaliyokusudiwa.

“Mimi sio mgeni katika Ofisi hii, hivyo ninawaahidi tutaendelea kushirikiana kama ambavyo tulikuwa tukifanya siku zote nilipokuwa hapa kwa nafasi ya Naibu Waziri. Kuletwa kwangu katika Ofisi hii ni kuja kuongeza nguvu ili kupata matokeo chanya ikiwemo ubunifu katika maeneo mbalimbali. Tufanye kazi tuliyopangwa kufanya tukiongozwa na misingi yetu ya utendaji kazi. Lengo ni kujenga na kumsaidia Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kupunguza kaya masikini katika taifa letu.

Pia Mhe. Kikwete amesema dhana ya ushirikishwaji wa walengwa wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini ni nzuri kwani imewasaidia kubuni miradi mbalimbali na imepunguza changamoto nyingi ikiwemo za miundo mbinu, afya na elimu.

Amesisitiza kuwajengea uwezo wa kifikra walengwa, fedha ziwafikie kwa wakati, usimamizi mzuri huku wakitambua kuwa msingi mkubwa wa Mpango huo walengwa wake ni wananchi na si vinginevyo.

Kwa upande wake Naibu Waziri Mhe. Regina Qwaray ameipongeza TASAF kwa kazi nzuri wanayoifanya. “Mimi ni mgeni katika Ofisi hii, lakini napenda niwapongeze kwa kazi nzuri mnayoifanya, TASAF sio ngeni masikioni mwangu, hii inaonyesha ni kwa jinsi gani mnatekeleza majukumu yenu vizuri, naombeni ushirikiano ili tufanye kazi kwa pamoja na kuwa na matokeo chanya,” amesema Mhe. Qwaray.

Akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa shughuli za Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF), Mkurugenzi Mtendaji wa TASAF Bw. Shadrack Mziray amesema Mfuko huo ulianzishwa na Serikali mwaka 2000 kama mojawapo ya mikakati katika kupambana na umaskini kwa kutumia dhana ya ushirikishaji jamii na imetekelezwa kwa awamu tatu tangu kuanzishwa kwake.