Waziri wa Madini, Anthony Mavunde (Mb), ametembelea na kushuhudia utekelezaji wa utafiti wa kina wa madini kwa kutumia teknolojia ya ndege nyuki (drone) katika Kata ya Basotu, Wilaya Hanang, mkoani Manyara. Utafiti huo wa jiofizikia unalenga kubainisha maeneo yenye hifadhi ya madini utakaopelekea kuanzishwa kwa mgodi mkubwa wa dhahabu wilayani humo.

Ziara hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan aliyoyatoa wakati akihutubia Bunge Oktoba 13, 2025 ambapo alitaja utafiti wa madini kama kipaumbele kwa mwaka 2025 - 2030 utakaopelekea kufikia angalau asilimia 50 ya utafiti wa kina wa madini nchini ifikapo mwaka 2030.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Waziri Mavunde amesema utafiti huo ni hatua muhimu kwa maendeleo ya wananchi wa Hanang na Mkoa wa Manyara kwa ujumla, kwani matokeo yake yanatarajiwa kuongeza ajira, kuvutia uwekezaji na kuchochea utekelezaji wa miradi ya kijamii kupitia leseni za uchimbaji madini.

“Tunatarajia utafiti huu utaleta matokeo chanya yatakayobadilisha maisha ya wananchi. Serikali itaendelea kusimamia sekta hii ili iwe chachu ya maendeleo kwa wote,” amesema Mavunde.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Hanang, Mhe. Almish Hazal, amemshukuru Waziri Mavunde kwa kutembelea eneo la mradi huo na kuendelea kusisitiza umuhimu wa tafiti za madini katika wilaya yake pia, ameiomba Wizara ya Madini kuendeleza kasi hiyo katika maeneo mengine ya Hanang yenye uwezekano wa kuwa na madini.

Naye, Mkurugenzi Mtendaji wa Cobra Resources Ltd, Bw. Amos Nzungu amempongeza Waziri Mavunde kwa ushirikiano na uzalendo anaouonesha kwa kufuatilia utekelezaji wa miradi ya utafiti wa madini na kuahidi kukabidhi matokeo ya utafiti mara tu yatakapokamilika.

Kwa upande wa Meneja wa Kampuni ya SkyPM Solution inayofanya utafiti huo, Bw. Paul Madata amesema matumizi ya teknolojia ya ndege nyuki yamerahisisha na kuongeza ufanisi wa utafiti wa awali, kwani inaweza kupima hadi zaidi ya kilomita tatu chini ya uso wa ardhi kwa muda mfupi.

Awali, Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Manyara, Mhandisi Godfrey Nyanda ametoa taarifa ya maendeleo ya sekta ya madini mkoani hapo, akibainisha kuwa hadi kufikia robo ya kwanza ya mwaka wa fedha 2025/26 (Julai–Oktoba), wamekusanya asilimia 35.21 ya lengo la makusanyo ya Shilingi Bilioni 2.2 lililopangwa kwa mwaka mzima.

“Tutaendelea kusimamia kikamilifu maagizo ya Mhe. Rais na ya Waziri wetu Mhe. Mavunde ili kuhakikisha sekta ya madini inaendelea kukua na kuimarika hapa Manyara,” amesema Mha. Nyanda.



Na Mwandishi wetu -Dodoma


Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania  kupitia  Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) imeendelea kuiishi kauli mbiu ya "Kazi na Utu" kwa kufanya ziara maalum ya kuwatembelea wanafunzi wenye mahitaji maalum waliopo vyuo vikuu Nchini kwa lengo la kusikiliza changamoto zinazowakabili na kuzitafutia ufumbuzi ili kuwasaidia wanafunzi hao kutimiza malengo yao.

Hayo yalisemwa na  Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Mhe. Ummy Nderiananga kwenye ziara yake alipotembelea wanafunzi wenye ulemavu katika Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), jijini Dodoma.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo Mhe. Nderiananga amesema kuwa Serikali ipo tayari kushirikiana na wanafunzi wenye ulemavu kutatua changamoto zinazowakabili ili kuhakikisha wanafikia malengo yao ikiwa ni utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi itakayowezesha kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya 2025-2050.


Aidha, Nderiananga ametoa wito kwa vijana wenye ulemavu kuwaelimisha watu wengine juu ya dhima ya kutunza amani, kwa sababu amani ikikosekana watu wenye ulemavu wanaathirika zaidi kutoka na kukosa uwezo wa kujiokoa.

Awali, Mkurugenzi wa Elimu Maalum Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Magreth Matonya aliwaambia wanafunzi wenye ulemavu kuwa kupata mkopo asilimia 100 ni haki yao hivyo watashirikiana na Bodi ya Mikopo (HESLB) ili kuhakikisha wanafunzi wenye ulemavu ambao hawajapata mikopo wanapata kwa wakati.


"Serikali imekuwa ikitoa fedha kila mwaka kwa ajili ya kununulia vifaa vya wanafunzi wenye mahitaji maalum, uhitaji bado upo lakini si mkubwa kama ilivyokuwa hapo awali kutokana na juhudi zinazofanywa na Serikali. Ameongeza Dkt. Matonya



Kwa upande wake Bi. Grace Daniel mwanafunzi mwenye ulemavu wa Ngozi  katika Chuo Kikuu cha DODOMA ameiomba Serikali na Sekta binafsi kuendelea kutoa kipaumbele cha ajira kwa watu wenye ulemavu wenye sifa.


Naye Bw. Jackson James mwanafunzi mwenye ulemavu wa viungo katika Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita kwa kuendelea kutoa vifaa kama vile Viti mwendo  vinavyowawezesha kuhudhuria vipindi kwa urahisi huku akiiomba Seriklai kuwafiki wanafunzi wenyeulemavu Vijijini.


 


= MWISHO=


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete akizungumza na Menejimenti ya Ofisi ya Rais Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma (hawapo pichani) wakati wa ziara yake ya kikazi katika Ofisi hiyo, tarehe 24 Novemba, 2025 jijini Dodoma.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (wa tatu kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Menejimenti Ofisi ya Rais Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma wakati wa ziara yake ya kikazi katika Ofisi hiyo tarehe 24. Novemba, 2025 jijini Dodoma. kulia kwake ni Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray na Kushoto kwake ni Katibu wa Sekretarieti ya Ajira Katika Utumishi wa Umma, Bwana Mick Kiliba.

Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray akitoa neno kabla ya kumkaribisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete kuzungumza na Watumishi wa Ofisi ya Rais Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma wakati wa ziara ya kikazi ya viongozi hao katika Ofisi hiyo tarehe 24. Novemba,2025 jijini Dodoma.

Katibu wa Sekretarieti ya Ajira Katika Utumishi wa Umma, Bwana Mick Kiliba akitambulisha Menejimenti ya Ofisi yake wakati wa ziara ya kikazi ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, tarehe 24. Novemba, 2025 jijini Dodoma

Naibu katibu Mkuu Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bw. Xavery Daudi akifurahia jambo alipokuwa akimsikiliza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (hayupo pichani) alipokuwa akizungumza na Menejimenti ya Ofisi ya Rais Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma (hawapo pichani) wakati wa ziara yake ya kikazi katika Ofisi hiyo, tarehe 24 Novemba, 2025 jijini Dodoma.

Katibu mkuu Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma,Bw. Juma Mkomi akitaka ufafanuzi juu ya utendaji kazi wa kituo cha huduma kwa Mteja wakati wa ziara ya kikazi ya Waziri wa Ofisi hiyo Mhe. Ridhiwani Kikwete, tarehe 24. Novemba, 2025 jijini Dodoma


Na Antonia Mbwambo-Dodoma


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete ameitaka Menejimenti ya Ofisi ya Rais Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma kuharakisha na kuweka wazi mchakato wa ajira 12,000 zilizotangazwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan wakati akifungua rasmi Bunge la 13 la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tarehe 14 Novemba, 2025 jijini Dodoma.

Mhe. Kikwete ameyasema hayo leo tarehe 24.11.2025 ikiwa ni ziara yake ya kwanza katika taasisi hiyo tangu alipoapishwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan tarehe 18 Novemba, 2025 kuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora.

Amesema moja ya ahadi za Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ni kuhakikisha Utumishi wa Umma unakuwa bora katika kutekeleza majukumu ya utoaji wa huduma bora kwa wananchi na kuongeza kuwa ili kuhakikisha hili linaanza kutekelezwa aliahidi kutoa vibali vya ajira 12,000 kwa Kada ya Elimu watumishi 7,000 na Kada ya Afya, watumishi 5,000.

“Kibali cha ajira kimeshatolewa, nawashukuru kwa kuanza kufanyia kazi, ni jambo zuri, ni mategemeo yangu kuwa majawabu ya maelekezo ya Mhe. Rais tutayaona hivi karibuni, hakikisheni mnasimamia kwa ukamilifu, mchakato wote wa ajira hizi uwekwe wazi ili kuondoa dhana potofu ya kuwa kuna upendeleo katika kutoa ajira.” Mhe. Kikwete amesisitiza.

Ameitaka Menejimenti hiyo kuongeza kasi ya kuratibu mchakato wa ajira “Tuangalie changamoto zinazokwamisha uharakishaji wa mchakato wa ajira ili tuweze kutatua na kuendelea na kukamilisha kwa wakati.” Ameongeza.

Pia, ameielekeza Menejimenti hiyo kuzingatia maadili katika kusimamia mchakato huo wa ajira ili kuhakikisha wanapatikana watumishi sahihi na wenye vigezo. kwa maendeleo ya taifa.

Aidha, ameisisitiza Menejimenti hiyo kutoonea watumishi walio chini yao bali wawaelekeze kwa upendo. “Tusimamie maadili katika utekelezaji wa majukumu yetu, tusionee watumishi walio chini yetu, tuzingatie taratibu za utendaji kazi.” Ameongeza

Pamoja na maelekezo aliyoyatoa kwa Menejimenti hiyo, Mhe. Kikwete ameomba ushirikiano katika utekelekezaji wa majukumu ya Serikali ili kufikia malengo ya Serikali ya utoaji wa huduma bora kwa ustawi wa taifa

Amewapongeza kwa kutekeleza maelekezo ya Wabunge katika kuendesha usaili ngazi ya mkoa na wanaopangiwa kazi kupokelea barua za ajira katika mikoa yao.

“Nawashukuru, pamoja na kuwa nilikuwa katika Ofisi nyingine lakini mmefanya kazi nzuri, tuendelee tusirudi nyuma, suala la kufanya mahojiano mikoani na kuchukua barua za ajira mikoani limeweza kupunguza kadhia.” Amesema.

Katika hatua nyingine, amewapongeza kwa kuanzisha Kituo cha Huduma kwa Mteja (call centre) kwani itapunguza adha kwa wenye uhitaji wa huduma na kuwasisitiza kuwaweka watumishi wenye kauli nzuri.

Naye Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray amesisitiza ushirikiano toka kwa Menejimenti hiyo. “Tumekuja kujitambulisha, ninaomba ushirikiano wenu, tufanye kazi kwa pamoja, tutatue kero za wananchi kama ambayo Rais wetu anatamani iwe.

Aidha amepongeza kazi inayofanyika katika taasisi hiyo. “Ni mara yangu ya kwanza kufika katika jengo hili, ni masaa machache nimetembelea katika jengo hili lakini napenda niwapongeze nimeona kazi zinavyofanyika, hongereni sana.

Kwa upande wake, Katibu wa Sekretarieti ya Ajira Katika Utumishi wa Umma, Bwana Mick Kiliba akielezea majukumu ya Taasisi hiyo, amemshukuru Mhe. Waziri na Viongozi wa Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora aliombatana nao kwa kuona umuhimu wa kutembelea katika Ofisi hiyo na kuwahimiza uwajibikaji kwa maslahi mapana ya taifa.

Akiainisha mafanikio mbalimbali ya Taasisi hiyo, Bw. Kiliba amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwawezesha kumiliki jengo lao ambapo sasa watumishi wote wako katika jengo moja na kuwaongezea bajeti ya utekelezaji wa majukumu yao ya masuala ya ajira.

 


Na James K. Mwanamyoto, OWM TAMISEMI

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM–TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amewataka Walimu Wakuu wa Shule za Msingi na Sekondari, viongozi katika Sekretarieti za Mikoa na Serikali za Mitaa kutenga muda wa kusikiliza kero na malalamiko ya watumishi wa umma pamoja na wananchi kwa lugha ya staha.

Prof. Shemdoe ametoa maelekezo hayo leo, wakati akifungua Mkutano Mkuu wa Chama cha Walimu Wakuu wa Shule za Msingi uliohudhuriwa na Wenyeviti wa Wakuu wa Shule za Msingi Tanzania Bara, unafanyika katika Ukumbi wa Sephile Sapphire Pride uliopo jijini Dodoma.

“Tuwasikilize watumishi wenzetu pamoja na wananchi kwa lugha ya staha, tutachukua hatua ya kumuondoa yeyote atakayeshindwa kuwasikiliza watumishi na wananchi,” amesisitiza Prof. Shemdoe.

Prof. Shemdoe amefafanua kuwa, suala hili la kuwasikiliza watumishi na wananchi lizingatiwe na  Wakurugenzi, Wakuu wa Idara na  Wakuu wa Vitengo katika Halmashauri zote nchini ili waweze kutatua kero na changamoto zinazowakabili watumishi wa umma na wananchi katika maeneo yao ya kazi.

Prof. Shemdoe amehimiza kuwa, moja ya jukumu la viongozi walio chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu-TAMISEMI ni kuwatumikia watanzania hivyo kila aliyebahatika kupata nafasi ya uongozi ahakikishe anawatumikia watanzania kwa ufanisi na uzalendo.

“Sisi watumishi wa Ofisi ya Waziri Mkuu-TAMISEMI tunao wajibu wa kipekee wa kuleta tabasamu kwa wananchi, tukitimiza kikamilifu jukumu la kutoa huduma bora,” amesema Prof. Shemdoe.

Naye, Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu-TAMISEMI anayeshughulikia Elimu Bw. Atupele Mwambene amesema, Walimu Wakuu walioudhuria mkutano huo ndio wenye jukumu la kupeleka tabasamu kupitia malezi watakayoyatoa kwa walimu wanaowasimamia na hatimaye wanafunzi watapata uelewa na ufaulu mzuri.

Akizungumza kwa niaba ya washiriki wa mkutano huo, Katibu Mkuu wa Chama cha Walimu Wakuu wa Shule za Msingi, Bw. Didas Bambaza amemuahidi Prof. Shemdoe kuwa, Walimu Wakuu watakwenda kutekeleza kwa vitendo maelekezo yote aliyoyatoa ili huduma zitakazotolewa katika shule zote zilete tabasamu kwa wanafunzi na wananchi.

Kaulimbiu ya Mkutano Mkuu huo wa Saba wa Mwaka wa Chama cha Walimu Wakuu wa Shule za Msingi (TAPSHA) ni Mtaala Ulioboreshwa kwa Elimu Bora; Ujuzi na Ubunifu kwa Maendeleo endelevu ya Taifa.










 

Imeelezwa kuwa matumizi ya Nishati safi ya kupikia sio anasa bali ni muhimu kwa kutunza mazingira na afya za wananchi,na pia inasaidia kupunguza muda wa uzalishaji  ambapo kwa sasa wananchi wanatakiwa kuhama katika tamaduni za kubaki kutumia nishati isiyo safi na kutumia nishati safi ya kupikia.

hayo yameelezwa na Naibu Waziri wa Nishati Mhe. Salome Makamba alipokutana na Bodi ya Wakala wa Nishati Vijini (REA),katika Ofisi za REA zilizopo jijini Dodoma,Novemba 25, 2025 ikiwa ni mwendelezo wa ziara zake kwenye taasisi zilizoko chini ya Nishati.

"Natoa rai kwa watanzania kuwa matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia sio anasa bali kwanza yanasaidia kutunza mazingira , pili yanasaidia kupunguza muda wa uzalishaji ambao mwanamke anakaa jikoni muda mrefu kupika wakati ukitumia nishati safi na inaokoa zaidi ya asilimia 70% ya muda ambao unatumia kupika".

Aidha, amesisitiza kwa wananchi wote kubadilika na kwenda na wakati sambamba na kwenda na kasi ya Dunia inavyoenda,ambapo kwa sasa matumizi ya kuni na matumizi ya Mkaa  kwa sehemu kubwa ya dunia hawatumii kabisa,  hivyo tunatakiwa kwenda kwa kasi hiyo ili watu wote  watumie nishati safi ya kupikia.

Nishati safi ya kupikia ni kapaumbele cha Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan, hivyo kama serikali inaendelea kutoa ruzuku ili kuhakikisha wananchi wanapoenda kujaza au kunua mitungi gesi  bei inakua pungufu,  pia Serikali inaweka juhudi kubwa kuhakikisha vituo vya ujazaji wa gesi katika mitungi inakua karibu na  wananchi walipo.

Aidha, Mhe. Makamba ameongeza kuwa mipango mingi ambayo Serikali imejiwekea ipo ile mingi ambayo ni ya muda mfupi na michache ya muda mrefu,  lengo likiwa ni kuendelea kutekeleza ahadi ya Mhe. Rais ya  kuwafikishia wananchi umeme kwenye vitongoji.

Ameongeza kuwa Wizara ya Nishati kupitia  REA inaendelea kutekeleza mpango wa kuvifikia vitongoji 9000 kwa kipindi hiki kifupi na kuhakikisha wananchi wanapata umeme wa uhakika.

Sambamba na hilo Mh. Rais amekua kinara wa Nishati safi ya kupikia na amezungumzia sana juu ya suala hili katika majukwaa mbalimbali , hivyo basi kwa upande wa nishati safi ya kupikia Wizara kupitia REA ndani ya muda huu mfupi imeandaa mradi wa muhsusi kuhakikisha taasisi zaidi ya hamsini (50) zinapata nishati safi ya kupikia na hizi ni taasisi ambazo zina idadi ya watu kuanzia 100 na zadi, ili kuweza kupunguza uharibifu wa mazingira pamoja na kuokoa muda ambao taasisi zinatumia kwa ajili ya kutengeneza chakula.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya wakala wa nishati vijijini- REA Mha.Hassan Said amesema kuwa mpango wa serikali  ni kuhakikisha kasi ya kuwaunganishia umeme wananchi katika vitongoji unakua endelevu na kuongeza kuwa hali ya upatikanaji wa umeme inaongezeka.

Amesema jumla ya vitongoji vilivyopo nchini ni  64,359 kati ya hivyo vitongoji 39,000 tayari vimepatiwa umeme ikiwa ni sawa na  asilimia 60%  vilivobakia ni vitongoji 25,400 kati ya hivyo vitongoji 2,500 miradi inaendelea wakati vitongoji 9,000 Wakala upo katika hatua ya mwisho ya utiaji saini ili vifikishiwe umeme.

Aidha Mhe. Naibu waziri alifanya ziara ya kufanya ziara kutembelea Kituo cha kupoza na kusafirisha umeme cha Zuzu kwenda kujionea hali ya kituo,kazi inayofanyika sambamba na hatua za ujenzi iliyofikiwa kwa baadhi ya maeneo ya kituo hicho zinavyoendelea.













 


Mkurugenzi wa Mipango Ofisi ya Rais UTUMISHI Bw. Cosmas Ngangaji amemshukuru Mkurugenzi wa Usimamizi wa Rasilimaliwatu na Utawala Bw. Musa Magufuli kwa ubunifu wake na kuweka utaratibu wa kuwapongeza na kuwatakia kila la kheri watumishi wake kwa kuzingatia mwezi waliozaliwa.

“Kwa niaba ya watumishi wenzangu tuliozaliwa mwezi Novemba ikiwa ni pamoja na Katibu Mkuu wetu Bw. Juma Mkomi, tunashukuru kwa motisha hii ya kufanya tukio la kumbukizi ya kuzaliwa kwetu kwa pamoja na kufurahi na watumishi wenzetu” alisema Bw. Ngangaji.

Aliongeza kuwa tabia njema huonekana kama ni ya kawaida, lakini kwa tukio hili haina budi kupongeza wote waliofanikisha jitihada hizi zenye kufurahisha jamii.

Naye Mkurugenzi Msaidizi wa Sehemu ya Anuai za Jamii kutoka Ofisi ya Rais- UTUMISHI, Bi. Mwanaamani Mtoo amewasisitiza wazaliwa wote wa mwezi Novemba kuzingatia mafunzo waliyopata leo kuhusu usimamizi wa fedha binafsi na uwekezaji kwa kuwa ni kipimo cha utu ambacho kinatakiwa kufikiwa na kila mmoja.

Aidha, amewapongeza wote waliozaliwa mwezi Novemba na kuwatakia kila la kheri katika kumbukizi ya kuzaliwa kwao na kuwaomba waendelee kutumikia familia zao na taifa kwa ufanisi.

 


Na. Benny Mwaipaja, Accra, Ghana

Rais wa Ghana, Mhe. John Dramani Mahama, amewataka Wahasibu Barani Afrika kuhakikisha kuwa wanazishauri na kuzisimamia nchi zao kuwa na matumizi sahihi ya fedha za umma ili kuharakisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii ya nchi hizo kwa kutumia mifumo thabiti ya kidigitali na akili unde (artificial Intelligence).

Mhe. Mahama ametoa wito huo Mjini Accra nchini Ghana, wakati akifungua Mkutano wa Tatu wa Jumuiya ya Wahasibu wa Serikali barani Afrika (African Association of Accountants General Meeting (AAAG), unaofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Accra (AICC), unaolenga kujadili namna kada hiyo ya wahasibu inavyoweza kuchangia maendeleo ya nchi zao kwa kuhakikisha kuwa kunakuwa na uwazi na uwajibikaji katika matumizi ya fedha za umma na rasilimali nyingine.

Alisema kuwa Afrika imebarikiwa kuwa na rasilimali nyingi, yakiwemo madini, gesi ardhi na rasilimali nyingine, lakini Bara hilo limeendelea kuwa katika hali ya umasikini kutokana na kukosekana kwa uwajibikaji na uadilifu wa matumizi ya rasilimali hizo hali inayokwaza maendeleo ya wananchi.

Alitolea mfano wa sekta ya ununuzi ambayo alisema kuwa imekuwa ikitumika kupoteza fedha nyingi za Serikali kutokana na gharama kubwa za kandarasi za utekelezaji wa miradi ya Serikali ambazo haziendani na hali halisi ya bei katika soko.

Alitoa rai kwa Wahasibu wa Serikali katika nchi za Afrika kuwa jicho la umma kwa kuhakikisha kuwa wanaweka na kutumia mifumo thabiti ya kuzuia upotevu wa fedha na kuwashauri watawala kujali maslahi ya wananchi.

Kwa upande wake, Mhasibu Mkuu wa Serikali ya Tanzania, CPA Leonard Mkude, alisema kuwa mkutano huo utaweka maazimio ya namna ya kuongeza uwazi na uwajibikaji wa matumizi ya fedha za umma yatakayowasilishwa kwa Wakuu wa Nchi za Afrika kwa ajili ya kuzipatia ufumbuzi changamoto mbalimbali zinazotokana na matumizi ya fedha za umma.

Alisema kuwa Kada ya Wahasibu ni Kada muhimu inayotakiwa kuweka misingi mizuri ya matumizi sahihi ya fedha za umma kwa kuwa ndiyo inayohusika na malipo ya kila siku ya huduma na utekelezaji wa miradi ya wananchi inayofanywa na Serikali.

Naye, Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Wahasibu wa Serikali Barani Afrika, Bw. Fredrick Riaga, alisema kuwa Mkutano huo uliobeba Kaulimbiu isemayo “Afrika ya Kesho: Kuimarisha Usimamizi wa Fedha za Umma kwa ajili ya Ustawi wa Kiuchumi", umewahusisha washiriki zaidi ya 2,000 kutoka nchi 55 za Afrika, umelenga kuweka mikakati ya pamoja ya namna ya kusimamia matumizi sahihi ya fedha za umma.

Mkutano huo ambao pia ulizikutanisha Jumuiya za wafanyabiashara na wadau wengine, umehudhuriwa na viongozi wengine mashuhuri akiwemo Mwanzilishi wa Mfuko wa P.L.O Lumumba, Profesa Patrick Loch Otieno Lumumba, mabaye alikuwa miongoni wa watoa mada walioalikwa.







Wizara ya Madini imezifutia leseni 73 za madini baada ya wamiliki wake kushindwa kurekebisha makosa yaliyobainishwa na Tume ya Madini katika ukaguzi wake wa hivi karibuni.

Akizungumza mbele ya wanahabari leo Waziri wa Madini, Antony Mavunde, alisema hatua hiyo ni sehemu ya msimamo wa serikali kuhakikisha rasilimali za madini zinatumika ipasavyo kwa manufaa ya taifa.


"Ninaiagiza Tume ya Madini kufuta jumla ya leseni 73 ambazo wamiliki wake wameshindwa kurekebisha makosa. Sitawavumilia watu wanaochukua leseni na kukaa nazo bila kuziendeleza," alisema Waziri Mavunde.


Kwa mujibu wa Waziri, Tume ya Madini ilitoa Hati za Makosa kwa leseni 205, ikijumuisha leseni 110 za utafiti wa madini na leseni 95 za uchimbaji mkubwa na wa kati. Baada ya kutakiwa kurekebisha dosari hizo, baadhi ya wamiliki walikidhi matakwa, huku wengine wakishindwa kufanya hivyo.

 

Miongoni mwa waliotelekezwa na hatua za marekebisho ni wamiliki wa leseni 44 za utafiti wa madini pamoja na wamiliki wa leseni 29 za uchimbaji wa kati, ambao wote walishindwa kurekebisha makosa yao kwa mujibu wa masharti ya sheria.


Waziri Mavunde aliwataka wamiliki wote wa leseni za madini kuhakikisha wanazingatia masharti na wajibu wa umiliki wa leseni zao, akisisitiza kuwa Serikali haitasita kuchukua hatua kali kwa yeyote anayekiuka sheria.


Aidha, amewaalika wawekezaji wenye nia ya dhati—wadogo kwa wakubwa—kuwasilisha maombi ya leseni katika maeneo ya wazi, akiahidi kuwa Wizara itaharakisha mchakato wa upatikanaji wa leseni kwa wakati.


Mavunde ametoa wito kwa wawekezaji wote kutekeleza matakwa ya Sheria ya Madini, Sura ya 123, huku Wizara ikiendelea kutoa ushirikiano kwa wote wanaotaka kufanya uwekezaji wenye tija katika sekta hiyo muhimu kwa uchumi wa taifa.






 


Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Nishati, Bi. Neema Mbuja amesema kuwa Serikali itaendelea kuunga mkono ajenda ya matumizi ya nishati safi ya kupikia kwa vitendo ili kufikia malengo ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kuhakikisha ifikapo mwaka 2034, asilimia 80% ya wananchi wanatumia nishati safi katika shughuli za upishi.

Akizungumza leo Novemba 25, 2024 katika kipindi cha Jambo Tanzania cha TBC1, katika kipengele cha Jikoni na Chigo, Bi. Mbuja amesema kuwa mahojiano hayo ni sehemu ya muendelezo wa ziara ya Wizara ya Nishati katika vyombo mbalimbali vya habari kwa lengo la kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu faida na umuhimu wa kutumia nishati safi ya kupikia.

Aidha, amesisitiza kuwa Wizara ya Nishati itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali pamoja na jamii katika kuhakikisha elimu kuhusu matumizi ya nishati safi inawafikia wananchi wengi zaidi, hivyo kuchochea utekelezaji wa mkakati wa kitaifa wa kuimarisha afya, mazingira na ustawi wa jamii kupitia matumizi ya nishati rafiki.