Morogoro:

Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) leo imeongoza kampeni ya kupanda miti mkoani Morogoro ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Wiki ya Maji Duniani, inayofikia kilele chake kila mwaka tarehe 22 Machi, kwa lengo la kulinda vyanzo vya maji na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Akizungumza wakati zoezi hilo, Wilfred Mwakalosi, aliyemwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, alisema taasisi hiyo kwa kushirikiana na Ofisi ya Bonde la Maji la Wami Ruvu na Wakala wa Huduma za Misitu ( TFS) wamefanikiwa kupanda miti zaidi ya 5,000 katika eneo linalozunguka mto Lukulunge, Kata ya Mzumbe, mkoani Morogoro.

Mwakalosi alibainisha kuwa hatua hiyo ni sehemu ya mkakati wa muda mrefu wa kuhifadhi mazingira, vyanzo vya maji na kuhakikisha upatikanaji endelevu wa maji kqtika maeneo mbalimbali nchini. “Morogoro ni miongoni mwa maeneo yaliyokuwa na vyanzo vingi vya maji hapo awali, lakini kwa sasa hali imebadilika kwa kiasi kikubwa kutokana na uharibifu wa mazingira na mabadiliko ya tabianchi, hivyo kutishia upatikanaji wa maji kwa wakazi wake” alieleza.

Mhifadhi wa Wakala wa Huduma za Misitu (TFS) wa Wilaya ya Morogoro, Stanley Kweka, alisema uharibifu wa misitu umechangia kupungua kwa kina cha maji katika Bwawa la Mindu, huku mmomonyoko wa udongo ukiendelea kuwa tatizo kubwa hivyo upandaji wa miti ni suluhisho muhimu katika kulinda kingo za mito na kuhakikisha vyanzo vya maji vinabaki salama kwa matumizi ya sasa na baadaye.

Naye  Meneja wa Uratibu wa Mazingira na Jumuiya za Watumia Maji kutoka Bodi ya Bonde la ya Maji la Wami/Ruvu Janeth Kisoma,alisema mto Lukulunge ni chanzo muhimu kinachochangia maji katika Bwawa la Mindu, ambalo linahudumia zaidi ya asilimia 75 ya wakazi wa Manispaa ya Morogoro, hivyo uhifadhi wake unahitaji ushirikiano wa wadau mbalimbali.

 


Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge Tawala wa Mikoa na  Serikali wa Mitaa - TAMISEMI,  wameridhishwa na kupongeza utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa shule mpya ya sekondari ya wasichana Longido Samia Girl's, wilaya ya Longido Mkoa wa Arusha, mradi uliotekelezwa na Serikali kwa gharama ya shilingu Bilioni 4.4, kupitia programu ya SEQUIP.

Akizungumza mara baada ya kukagua mradi huo mapema leo machi 17,2026, Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Florent Kyombo (Mb), licha ya kuridhishwa na ubora wa mradi huo, ameipongeza Serikali ya awamu ya sita chini ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha nyingi za kuboresha miundonu ya elimu nchini huku Mkoa wa Arusha ukiwa ni miongoni mwa wanufaika. 

Ameweka wazi kuwa, lengo la serikali ni kuhakisha watoto wa kitanzania wanapata elimu kwenye mazingira rafiki na dhamira ya dhati Dkt.Samia ni kuwahamasisha watoto wa kike nchini kusoma masomo ya Sayansi ili kuzalisha watalamu wengi katika fani za Sayansi.

Hata hivyo wajumbe hao, wameshauri mkoa kuwa na msimamizi wa majengo 'Estate Manager' atakayekuwa na dhamani ya kusimami majengo yote ya serikali yaliyokamilika, ili kuhakikisha yanaendelea kutunzwa na kuendelea kuwa bora pamija na kushugulikia masuala ya ukarabati wa majengo hayo. 

Naye mkuu wa wilaya ya Longido Mhe.  Ally Kali, amewashukuru wajumbe wa kamati hiyo kwa niaba ya wananchi wake, kwa kuwatembelea na kukagua mradi huo wa shule, mradi ambao amekiri ni muhimu kwa watoto wa jamii ya Kimaasai, jamii ambao hapo awali wasichana wengi walikosa nafasi ya kupata elimu.

Mhe. Kali, amesisitiza kufanyia kazi maelekezo na ushauri ulmntolewa na wajumbe ikiwa ni pamoja na kupeleka maombi ya mahitaji ya shule hiyo kwenye Kamati ya Bajetii ili yaingizwe kwenye bajeti ya mwaka ujao wa fedha

Awali shule ya wasichana Longdo Samia Girl ni miongoni mwa shule 26 za kimkoa,ukiwa na lengo la kuongeza idadi ya shule na kuboresha mazingira ya ujifunzaji na ufundishaji nchini, iliyoanza kupokea wanafunzi mwaka 2024 ina wanafunzi 681 wa kidato cha 1-6 kwa mchepuo wa Sayansi.











 

Na Mwandishi wetu- Dodoma

 Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu imeendelea na hatua ya tatu ya kujengewa uwezo  wa namna ya kufanya tathmini za programu na miradi kupitia programu ya Kuendeleza  Sekta ya Kilimo Awamu ya Pili (ASDP II)  ili kuwawezesha watalaam wa ufuatiliaji na tathmini kupata uelewa na namna ya kutathmini miradi na programu mbalimbali zinazotekelezwa katika taasisi za umma.


Hayo yamesemwa leo tarehe 16 Machi 2026, jijini Dodoma na Mkurugenzi wa Ufuatiliaji na Tathmini ya Utendaji wa Serikali, Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Bi. Sakina Mwinyimkuu   wakati akifungua mafunzo yanayofanyika kwa siku nne Jijini Dodoma yakihusisha washiriki kutoka wizara zinazotekeleza  program ya ASDP II na washiriki kutoka nchini Zimbabwe na Malawi kwa lengo la kujifunza chini ya Twendembele Initiative ambapo Tanzania ni mshirika.



Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalumu, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi amewaomba Wakristo na Waislamu mkoani Mbeya kuendelea kutenda mema, kuishi kwa upendo, umoja na amani hata baada ya kumalizika kwa vipindi vya mfungo wa Kwaresma na Ramadhani. 

Ameyasema hayo  katika futari (Iftari)  iliyoandaliwa na Taasisi ya Maryprisca Women Foundation iliyowakutanisha viongozi wa serikali, Jeshi la Polisi, vyama vya siasa, taasisi za kidini pamoja na wananchi wa Kata ya Iwambi na kata jirani, Mahundi amesema waumini wanapaswa kuyaishi mafundisho ya vitabu vitakatifu hata baada ya kumaliza ibada za mfungo na kuendelea kuiombea nchi. 

“Ni wajibu wetu kuyaishi yale yote tunayofundishwa katika vitabu vitakatifu vya dini zetu. Tusiache kuiombea nchi yetu ya Tanzania ili iendelee kuwa na amani na upendo kwa sababu hiyo ndiyo lugha yetu na utamaduni wetu kama taifa,ni wasihi tuendelee kuiamini serikali na kuendelea kudumisha mshikamano maana hii ni tunu yetu watanzania wote ” amesema Mahundi.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Kyela, Josephine Manase, alimpongeza Mhe. Mahundi kwa moyo wake wa upendo kwa jamii na kuwataka viongozi wa dini kuendelea kuwajali watoto yatima pamoja na watu wasiojiweza katika jamii maana hiyo ndio ibada kuu katika maisha ya mwanadamu.

“Katika ibada mnazozifanya msisahau kuwahudumia watoto yatima na wale wasiojiweza kwa sababu kuwahudumia wao ni sehemu ya ibada kubwa na kumbukumbu isiyofutika mbele za Mwenyezi Mungu lakini pia tuendelee kumuombea Rais wetu ili aweze kuendelea kufanya kazi ya kutuletea maendeleo” amesema Manase.

Salamu za Serikali ya Wilaya ya Mbeya zilizowasilishwa na Afisa Tawala wa Wilaya hiyo kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya, Devotha Chacha, zimemhakikishia Mhe. Mahundi ushirikiano wa kutosha katika shughuli zake za kijamii. ambapo Serikali ya Wilaya ya Mbeya itaendelea kushirikiana  kwa karibu na taasisi hiyo kwani kazi wanazozifanya  ni huduma kwa jamii na ni wito kutoka kwa Mwenyezi Mungu"amesema Devotha

Kwa upande wao viongozi mbalimbali wa dini waliohudhuria iftari hiyo wamempongeza Mhe. Mahundi kwa kuendelea kudumisha utaratibu wa kuwakutanisha wananchi wa dini tofauti katika futari hiyo wakisema hatua hiyo inaimarisha upendo, mshikamano na amani katika jamii. 

"Utaratibu huu wa kuwakutanisha watu wa dini mbalimbali ni jambo jema linaloendelea kuimarisha upendo na umoja katika jamii, na tunaona mabadiliko kila mwaka kwa kuwa wananchi wanaendelea kuungana zaidi,” wamesema viongozi hao wa dini.

 

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba leo Machi 15, 2026 ameweka jiwe la msingi la Shule ya Sekondari Mgombe yenye mkondo wa Amali ya Kihandisi iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Mlele, mkoani Katavi, ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kikazi ya kukagua na kufuatilia utekelezaji wa miradi ya maendeleo mkoani humo.

Ujenzi wa shule hiyo unatekelezwa kupitia Mradi wa Kuimarisha Ubora wa Elimu ya Sekondari (SEQUIP) kwa gharama ya shilingi bilioni 1.694 na hadi sasa umefikia asilimia 99 ya utekelezaji.

Shule hiyo itatoa mafunzo ya amali katika fani mbalimbali zikiwemo ufundi magari, ufundi bomba, mifumo ya umeme wa jua pamoja na ufundi umeme wa magari. Mafunzo hayo yanalenga kuwajengea wanafunzi ujuzi wa vitendo utakaowawezesha kujiajiri, kuajiriwa au kuendelea na masomo ya elimu ya juu.



 


Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imefanya ziara ya ukaguzi katika Kituo cha Kupokea na Kupoza Umeme cha Mpomvu kilichopo mkoani Geita tarehe 15 Machi 2026, ikiwa ni sehemu ya ufuatiliaji wa utekelezaji wa miradi ya kimkakati ya Nishati inayolenga kuimarisha upatikanaji wa umeme nchini.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Subira Mgallu amesema ziara hiyo imelenga kukagua maendeleo ya miradi ya nishati pamoja na kuhakikisha uwekezaji unaofanywa na Serikali unaleta matokeo yaliyokusudiwa kwa wananchi.

“Kama Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini tuna jukumu la kuisimamia Wizara ya Nishati ili kuhakikisha inatekeleza majukumu yake kikamilifu. Tumeridhishwa na uwekezaji uliofanywa katika kituo hiki ambacho kina mchango mkubwa katika kuhakikisha upatikanaji wa umeme wa uhakika kwa wananchi na shughuli za kiuchumi,” amesema Mhe. Mgallu.

Ameongeza kuwa Kituo hicho kina uwezo wa kupokea na kusambaza takribani megawati 90, huku jitihada zikiendelea kuboresha miundombinu ya usambazaji wa umeme ikiwemo mpango wa kuongeza laini maalum kwa ajili ya Mgodi wa dhahabu wa Geita (GGM).

“Mahitaji ya umeme ya mgodi wa GGM yanatarajiwa kufikia takribani megawati 70 ifikapo mwaka 2035 kutoka megawati 36 zinazotumika kwa sasa, hivyo ni muhimu kuendelea kuimarisha miundombinu ya usambazaji wa umeme ili kukidhi mahitaji hayo,” ameongeza.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Nishati Mhe. Salome Makamba amesema Serikali inaendelea kuimarisha miundombinu ya umeme katika Mkoa wa Geita kutokana na ukuaji mkubwa wa shughuli za kiuchumi na kijamii hususan katika sekta ya madini.

“Kituo hiki kina mchango mkubwa katika kuimarisha upatikanaji wa umeme katika Mkoa wa Geita pamoja na maeneo ya jirani ikiwemo Biharamulo na Ngara mkoani Kagera, Sengerema mkoani Mwanza na Kakonko mkoani Kigoma,” amesema Mhe. Salome.

Naibu Waziri wa Nishati ameongeza kuwa Kituo cha Mpomvu kimegharimu takribani shilingi bilioni 50, uwekezaji ambao umeongeza uwezo wa usambazaji wa umeme katika eneo hilo linalokua kwa kasi kiuchumi ambapo mahitaji ya sasa ya umeme yamefikia Megawati 73.64.

Awali, Mkoa wa Geita ulikuwa ukipokea umeme kutoka Mkoa wa Shinyanga wenye uwezo wa takribani megawati 4 pekee, kiwango ambacho hakikukidhi mahitaji ya umeme yaliyokuwa yakiongezeka kutokana na shughuli za kiuchumi hususan uchimbaji wa madini.

Kituo cha Kupokea na Kupoza umeme cha Mpomvu kilianza kujengwa mwaka 2019 na kukamilika mwaka 2020, kabla ya kuzinduliwa rasmi mwaka 2022 na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.







 -Akemea watumishi wanaowaelekeza wananchi kununua dawa nje ya hospitali

-Aonya utapeli wa ardhi za vijiji

-Akemea wakandarasi wanaolipwa fedha za miradi lakini hawawalipi mafundi


WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba ameagiza kufanyika kwa uchunguzi kuhusu mfumo wa upatikanaji wa dawa katika hospitali na vituo vya kutolea huduma za afya nchini.

Ametoa agizo hilo leo Jumapili (Machi 15, 2026) alipokuwa akizungumza na wananchi wa Wilaya ya Nsimbo katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika viwanja vya Shule ya Msingi Songambele mkoani Katavi, ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kikazi mkoani humo.

Amesema Serikali imekuwa ikipeleka fedha kwa ajili ya ununuzi wa dawa katika hospitali na vituo vya afya, lakini bado baadhi ya wananchi wanapofika kutafuta huduma wanaelekezwa kwenda kununua dawa katika maduka binafsi nje ya hospitali.

“Takwimu zinaonesha tuna utoshelevu wa dawa lakini mwananchi akienda hospitalini anaelekezwa mtaani kwenda kununua dawa. Huu mchezo haukubaliki. Duka la mtaani linapata wapi dawa ambayo Serikali haiwezi ikapata?” amesema.

Kutokana na hali hiyo, Waziri Mkuu amesema ni muhimu kufanya uchunguzi wa kina ili kubaini namna fedha za ununuzi wa dawa zinavyotumika pamoja na mfumo wa upatikanaji wa dawa katika vituo vya kutolea huduma za afya.

Katika hatua nyingine, Dkt. Mwigulu ameonya tabia ya baadhi ya viongozi kuuza ardhi ya vijiji kwa njia zisizo halali na kusababisha migogoro ya ardhi katika jamii.

“Hata tukigombana ardhi haiongezeki. Binadamu tunaongezeka lakini ardhi haiongezeki. Hata tukipigana ardhi haiongezeki, kwa hiyo tuepuke kuchukiana kwa misingi hiyo,” amesema.

Amesema Serikali haitavumilia vitendo vya utapeli wa ardhi vinavyofanywa na baadhi ya viongozi wasiowaadilifu.

“Watu wa aina hii wakishagundulika wasidunde mtaani lazima wafike kwenye mkono wa sheria. Wanataka kuvunja undugu wetu kwa tamaa na ubinafsi,” amesema.

Kadhalika, Waziri Mkuu ameonya wakandarasi wanaolipwa fedha za miradi ya Serikali lakini wanashindwa kuwalipa mafundi na wakandarasi wadogo waliotekeleza kazi hizo.

“Mkandarasi anapewa kazi anaajiri mafundi, anatoa subcontract kwa wengine, yeye analipwa fedha yote ya mradi lakini hawalipi wale waliofanya kazi. Watu wa aina hiyo wasakwe popote pale walipo na wasiwe huru mpaka wawalipe watu ambao wameshafanya kazi,” amesema.

Amesema vitendo hivyo vinawanyima haki wananchi waliotekeleza kazi kwa uaminifu na vinaweza kuifanya jamii kuilaumu Serikali wakati fedha za miradi tayari zimeshalipwa kwa wakandarasi.

“Hii kuchukua fedha Serikali imeshalipa halafu wananchi wetu ambao wamefanya kazi hawajalipwa ni kuwasababishia umaskini watu ambao wamefanya kazi kwa uaminifu,” amesema.

Katika mkutano huo, Waziri Mkuu amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuwekeza katika miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo sekta za afya, elimu na miundombinu.

Amesema katika kipindi cha miaka minne iliyopita Serikali imejenga hospitali za wilaya 119, vituo vya afya 649 pamoja na zahanati zaidi ya 2,700 nchini kote kwa lengo la kuboresha huduma za afya kwa wananchi.

Aidha, amesema Serikali imejenga zaidi ya shule za sekondari 1,300 pamoja na shule za ufundi zaidi ya 103 ili kuwawezesha vijana kupata elimu na ujuzi unaowawezesha kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo.






 

 

















Na Oscar Assenga,Muheza, Tanga

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais anayeshughulikia Maendeleo ya Vijana, Joel Nanauka amesema serikali itaendelea kuvipa kipaumbele vikundi vya vijana vinavyoonyesha uwajibikaji kwa kurejesha mikopo wanayopewa ili viweze kukuza shughuli zao za kiuchumi.

Nanauka aliyasema hayo leo wakati wa ziara ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii iliyotembelea kikundi cha Vijana cha Mali Hai kilichopo wilayani Muheza mkoani Tanga kwa lengo la kukagua shughuli zao za uzalishaji pamoja na miradi iliyopata fedha kupitia mikopo ya halmashauri.

Akiwa kwenye kikundi hicho alionyesha kuridhishwa na juhudi na nidhamu ya kikundio hicho kurejesha mikopo baada ya kufanikiwa kukuza mtaji wake kutoka shilingi milioni 20 hadi kufikia zaidi ya shilingi milioni 50, hatua inayotajwa kuwa mfano bora kwa vikundi vingine vya vijana nchini.

Nanauka alisema kikundi cha Mali Hali ni miongoni mwa vikundi vichache nchini vilivyofanikiwa kurejesha mikopo kwa wakati, jambo ambalo limekifanya kupata nafasi ya kuangaliwa kwa karibu zaidi katika mipango ya kusaidiwa kuongeza mtaji na kupanua shughuli zake.

Alisema katika mchakato unaoendelea wa kusaidia wajasiriamali wadogo na kurasimisha shughuli zao, serikali itaangalia namna ya kukiweka kikundi hicho kwenye orodha ya vikundi vitakavyosaidiwa ili kuimarisha shughuli zao za uzalishaji.

Aidha, alieleza kuwa serikali inatekeleza maelekezo ya Rais ya kuhakikisha vijana wanaochukua hatua ya kufanya kazi na kuonyesha juhudi wanapatiwa mikopo na serikali ili waweze kujikwamua kiuchumi na pia kutoa ajira kwa wengine.

“Vijana hawa wameonyesha mfano mzuri kwa watanzania wengine wameanza na mtaji mdogo mwaka 2008,wakapata msaada wa shilingi milioni tano mwaka 2018 na baadaye mkopo wa shilingi milioni 20 mwaka wa fedha 2020/2021. Leo hii wameongeza mtaji wao hadi kufikia zaidi ya milioni 50. Huu ni ushahidi kwamba ndoto kubwa zinaweza kuanza na mwanzo mdogo,” alisema Nanauka.

Aliongeza kuwa serikali itahakikisha vijana wenye juhudi kama hao wanapata fursa zaidi, ikiwemo mikopo mingine, pamoja na kushirikishwa katika zabuni za serikali ili waweze kukuza biashara zao.

Nanauka pia aliwashauri vijana nchini kutokudharau mwanzo mdogo na kuwa na uvumilivu wanapotekeleza ndoto zao za kimaendeleo.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii, Hawa Mchafu, alisema kamati hiyo ipo katika ziara ya kawaida ya kukagua miradi ya maendeleo kabla ya kuanza kwa Bunge la Bajeti, ambapo wamepita katika maeneo mbalimbali kutathmini miradi iliyopata fedha za serikali.

Alisema kamati hiyo imevutiwa na kazi nzuri inayofanywa na kikundi hicho cha vijana, lakini imebaini changamoto ya eneo la uzalishaji kuwa dogo na huenda lisiweze kukidhi mahitaji yao iwapo wataongeza mtaji zaidi.

Kutokana na hali hiyo, kamati imeitaka wizara husika kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Tanga kuhakikisha vijana hao wanapatiwa eneo kubwa zaidi la kufanyia shughuli zao za uzalishaji ili waweze kupanua biashara zao.

“Eneo walilonalo sasa ni dogo ukilinganisha na malengo yao ya kupanua uzalishaji hivyo tunashauri wapatiwe eneo kubwa zaidi na lililopo sasa likibaki kama sehemu ya maonesho ya bidhaa wanazozalisha,” alisema Mchafu.

Pia aliishauri serikali kuangalia uwezekano wa kukipa kikundi hicho mkopo mwingine wa kifedha ili kiweze kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazokikabili, ikiwemo kununua gari kwa ajili ya shughuli za uzalishaji na usafirishaji wa bidhaa.

Aidha, alitumia nafasi hiyo kuwakumbusha vijana nchini kutumia fursa zilizotolewa na serikali kupitia mifuko mbalimbali ya maendeleo ya vijana badala ya kujikita kwenye mfuko mmoja pekee.

Mchafu alisema kuwa Rais ametoa zaidi ya shilingi bilioni 200 kwa ajili ya kusaidia maendeleo ya vijana kupitia wizara na taasisi mbalimbali, hivyo vijana wanapaswa kuzitumia fursa hizo kujikwamua kiuchumi.

Kamati hiyo pia imeishauri serikali kuhakikisha sheria ya manunuzi ya umma inayotaka asilimia 30 ya zabuni za serikali zitolewe kwa vijana, wanawake na watu wenye ulemavu inatekelezwa kikamilifu ili kuwapatia vijana nafasi ya kukua kiuchumi.

Kwa sasa kikundi cha Mali Hali kinadaiwa kuajiri vijana zaidi ya 20 katika shughuli zake za uzalishaji, jambo ambalo limeelezwa kuwa linaunga mkono dhamira ya serikali ya kukuza ajira kwa vijana na kuimarisha uchumi wa wananchi.

Vijana wa kikundi hicho pia wamemshukuru Rais kwa kuendelea kutoa fursa na kuahidi kuendelea kufanya kazi kwa bidii ili kufikia ndoto zao za kuanzisha kampuni kubwa inayoweza kutoa ajira kwa vijana wengi zaidi katika Mkoa wa Tanga na maeneo mengine nchini.

Mwisho.