Serikali mkoani Kilimanjaro imeanza utekelezaji wa mkakati maalum wa kuwawezesha maafisa ugani kupitia mafunzo ya kitaalamu, ikiwa ni jitihada za kuleta mapinduzi katika sekta ya kilimo na kuongeza tija kwa wakulima.


Hatua hiyo inalenga pia kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi pamoja na kuinua kipato cha wakulima katika mkoa huo.

Akizungumza kwa niaba ya Katibu Tawala wa Mkoa wakati wa ufunguzi wa mafunzo yaliyoandaliwa na Mamlaka ya Udhibiti wa Nafaka na Mazao Mchanganyiko (COPRA), yaliyofanyika Machi 17, 2026 katika ukumbi wa Manispaa ya Moshi, Katibu Tawala Msaidizi wa Kilimo na Ufugaji, Dkt. Emmanuel Lema alisema maafisa ugani wanapaswa kutumia mbinu za kisasa na ubunifu ili kuwahudumia wakulima kwa ufanisi zaidi.

Alisema mafunzo hayo yanalenga kuwajengea uwezo maafisa hao ili waweze kushauri matumizi sahihi ya mbegu bora, teknolojia za kisasa za kilimo pamoja na mbinu za kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi.


Aidha, Dkt. Lema alibainisha kuwa Serikali inaendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuboresha sekta ya kilimo, ikiwa ni pamoja na kuimarisha miundombinu ya umwagiliaji, kusambaza pembejeo na kuwapatia maafisa ugani vitendea kazi vinavyohitajika. Pia aliwataka maafisa hao kushiriki kikamilifu katika kudhibiti migogoro kati ya wakulima na wafugaji.


Kwa mujibu wa takwimu za mkoa, Kilimanjaro imezalisha tani 1,259,115 za mazao ya chakula katika mwaka wa kilimo 2024/2025, kiwango kinachozidi mahitaji ya tani 773,115.


Naye Afisa Kilimo kutoka COPRA, Bi. Paskalia Sitembela alisema taasisi hiyo itaendelea kushirikiana na Serikali katika kutoa mafunzo yatakayochochea uzalishaji wa mazao yenye ubora unaokidhi mahitaji ya soko.


Maafisa ugani walioshiriki mafunzo hayo wameahidi kuyatumia ipasavyo ili kuwafikia wakulima katika maeneo yao na kuwapatia elimu sahihi ya kilimo, hatua itakayosaidia kuongeza uzalishaji wenye tija katika mkoa na taifa kwa ujumla.

 


Babati, Manyara: Sherehe ya kumbukizi ya kuzaliwa ya Mkurugenzi wa Mati Super Brands Ltd, Bilionea David Mulokozi, imegeuka kuwa somo la upendo na kuthaminiana baada ya mkewe, Doreen Mulokozi, kumuandalia tukio la kushtukiza lililogusa wengi.

Katika sherehe hiyo iliyofanyika Babati Mjini na kuhudhuriwa na wageni mbalimbali waalikwa, Doreen alimzawadia mumewe zawadi mbili kubwa—ikiwa ni pamoja na kumualika mwanamuziki anayempenda, Banana Zoro, ambaye aling’ara jukwaani kwa burudani ya hali ya juu na kukonga nyoyo za mwenyeji wa hafla pamoja na wageni wote.


Mbali na burudani hiyo iliyoongeza shamrashamra katika tukio hilo, Doreen alimkabidhi mumewe gari kama zawadi maalum ya kumbukumbu ya siku yake ya kuzaliwa, hatua iliyodhihirisha mapenzi ya dhati na kuthamini mchango wake ndani ya familia.

Kwa upande wake, Banana Zoro alitoa shukrani zake za pekee kwa mwaliko huo, akieleza kuwa kushiriki katika hafla hiyo kumekuwa na maana kubwa kwake binafsi na kitaaluma.

Akizungumza kwa hisia na furaha, David Mulokozi alimshukuru mkewe kwa maandalizi hayo pamoja na zawadi ya kushtukiza, akieleza kuwa tukio hilo limekuwa moja ya kumbukumbu muhimu zaidi katika maisha yake.
“Kumbukizi yangu ya kuzaliwa alinifanyia mke wangu Doreen… kwangu vilikuwa vitu vya kipekee sana katika maisha yangu,” alisema Mulokozi.

Kwa utani, Mulokozi aliwataka pia wanawake wengine kuiga mfano huo kwa kuwapatia waume zao zawadi zenye thamani, badala ya zawadi ndogo ndogo za kawaida, jambo lililozua vicheko na furaha miongoni mwa wageni waliohudhuria.
Naye Doreen alimtakia mumewe baraka na mafanikio zaidi katika shughuli zake, huku akimuomba aitunze zawadi hiyo kama kumbukumbu muhimu ya upendo wao ili waendelee kuikumbuka hata watakapokuwa wazee.
Sherehe hiyo ilifanyika kwa mafanikio makubwa, ikijumuisha burudani, furaha na mshikamano wa kifamilia pamoja na marafiki, huku ikiakisi ujumbe mzito wa kuthaminiana, upendo wa kweli na umuhimu wa kusherehekea maisha pamoja.
Katika kuendeleza dhamira ya uwajibikaji kwa jamii, Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) limetembelea Kituo cha Watoto Yatima cha Umra Orphanage jijini Dar es Salaam, na kutoa msaada wa mahitaji muhimu sambamba na kuwapa faraja watoto wanaolelewa kituoni hapo, kuelekea sikukuu ya Idd.
NA EMMANUEL MBATILO, BAGAMOYO

WIZARA ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kupitia Wakala wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu (ADEM) itaendelea kutoa fursa za mafunzo endelevu ya viongozi wa elimu wa ngazi mbalimbali na wadau wengine wa elimu ili waweze kuimarisha uongozi, usimamizi na uendeshaji wa shule kwa ajili ya utoaji wa elimu bora nchini. 

 




Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria imetembelea na kukagua mradi wa ujenzi wa Kituo cha Utengamao cha Taifa unaotekelezwa na Mamlaka ya Kudhibiti na kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) katika eneo la Itega, jijini Dodoma.

Ziara hiyo imefanyika leo tarehe 18 Machi 2026 na kuongozwa na Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Edwin Swale ikiwa ni sehemu ya majukumu ya kamati ya kusimamia na kukagua utekelezaji wa miradi mbalimbali.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mhe. Swale amesema kuwa kamati imeridhishwa na hatua ya utekelezaji ambayo mradi umefikia kwani unaenda kutimiza dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kujali Utu na Ustawi wa Watanzania.

Sambamba na hilo, ameipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu kupitia Mamlaka ya kudhibiti na kupambana na dawa za Kulevya kwa kubuni mbinu ya jinsi ya kusaidia waraibu watokanao na matumizi ya madawa za kulevya.

Awali,Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Mhe. Ummy Nderiananga amesema kuwa Mradi huo ni endelevu ikiwa ni juhudi ya Serikali katika mapambano dhidi ya Dawa za kulevya na kuahidi kuendelea kushirikiana na Taasisi binafsi katika mapambano dhidi ya matumizi ya Dawa za kulevya Nchini.

Kwa upande wake Kamishna Jenerali wa Mamlaka ya Kudhibiti na kupambana na Dawa za kulevya Bw. Aretas Lymo ameongeza kuwa kituo hiko kinatarajia kutoa huduma za matibabu, urekebishaji wa kitabia pamoja programu za kuwawezesha waathirika kurejea katika jamii wakiwa na uwezo wa kujitegemea.

Wakati huo huo, Makamu Mwenyekiti Mhe. Swale ameelekeza kuwa Ujenzi wa kituo hicho cha utengamao uzingatie Uwepo wa Miundombinu ya watu wenye mahitaji maalum na kutilia maanani malengo ya kituo ya kuwasaidia kiujuzi waraibu wa madawa ya kulevya .



 Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) umeingia katika mpango wa ushirikiano na kampuni ya Land Africa Safaris ili kukuza utalii wa ikolojia kupitia tukio la Cape to Cairo Arusha International Marathon linalotarajiwa kufanyika Mei 28 hadi 30, 2026 mkoani Arusha.

Makubaliano hayo yamefikiwa katika kikao kilichofanyika Machi 17, 2026 katika Ofisi ya Mhifadhi Mkuu wa Ziwa Duluti, Arumeru.

Akizungumza baada ya kikao hicho, Mhifadhi Mkuu wa Ziwa Duluti, Peter A. Myonga, alisema ushirikiano huo ni fursa muhimu kwa TFS kutumia michezo kutangaza vivutio vya misitu na kuongeza idadi ya watalii wanaotembelea maeneo hayo.

Alisema tukio hilo linatarajiwa kuvutia zaidi ya washiriki 5,000 kutoka ndani na nje ya nchi, hatua itakayochochea ongezeko la wageni, muda wa kukaa kwa watalii jijini Arusha na mapato yatokanayo na utalii.

Kwa mujibu wa Myonga, TFS imejipanga kushiriki kikamilifu katika mbio hizo ambapo vivutio vyake vya Napuru na Ziwa Duluti vitatembelewa na washiriki wa mbio hizo kwa ajili ya kutangaza utalii wa misitu na nyuki (api-tourism).

Aidha, alisema washiriki wa mbio hizo watapata fursa ya kutembelea vivutio vya misitu ikiwemo Shamba la Miti Meru na Ziwa Duluti kabla na baada ya tukio, huku mipango ikiwekwa kuhakikisha katika msimu ujao wa 2027 njia ya mbio inapita ndani ya hifadhi hizo ili kuongeza mvuto wa utalii.

Aliongeza kuwa TFS itanufaika pia kwa kuanzisha mabanda ya maonyesho, kutengeneza vifurushi vya utalii, huduma za kambi katika eneo la Napuru na kushiriki katika hafla ya Gala Dinner itakayotoa jukwaa la kuitangaza sekta ya misitu na nyuki.

Kwa upande wake, Haffy Mohamed  kutoka Land Africa Safaris alisema wataendelea kushirikiana na TFS kuhakikisha tukio hilo linakuwa chachu ya kukuza utalii wa michezo nchini.

Hatua hiyo ni sehemu ya jitihada za kuunganisha sekta ya michezo na utalii ili kuongeza mchango wa rasilimali za asili katika uchumi wa Taifa.





Shirika la Umeme Tanzania, TANESCO, limezindua rasmi matumizi ya ndege nyuki (drones) kwa ajili ya kufanya ukaguzi wa njia za kusafirisha na kusambaza umeme ikiwa ni hatua inayolenga kuongeza ufanisi wa utoaji huduma na kupunguza muda wa kutatua changamoto za kukatika kwa umeme.

Uzinduzi huo umefanyika tarehe 17 Machi 2026 katika Ofisi za TANESCO, Ubungo jijini Dar es Salaam, ukiongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika hilo, Bw. Lazaro Twange.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Bw. Twange amesema TANESCO inasimamia mtandao mkubwa wa miundombinu ya umeme nchini unaohitaji ufuatiliaji wa karibu kwa kutumia teknolojia za kisasa.

“Tuna njia za kusafirisha umeme ambazo zimetembea urefu wa takribani kilomita 8,500, na tuna njia za kusambaza umeme ambazo zimetembea karibu kilomita 200,000. Njia hizi zimepita ardhini kwenye mapori, pembezoni mwa barabara na maeneo yetu,” amesema Bw. Twange.

Ameeleza kuwa jukumu la msingi la Shirika hilo ni kuhakikisha wateja wanapunguziwa muda wa utatuzi wa pale changamoto za umeme zinapojitokeza na kuhakikisha huduma inarejea kwa wakati wote.

“Kazi yetu ya kuhudumia wateja, moja ya kitu tunachopambana nacho zaidi ni kuhakikisha wateja wanapata umeme. Leo tumeanza safari ya mapinduzi ya teknolojia ya kuturahisishia kufanya kazi zetu,” alisisitiza.

Kwa mujibu wa Bw. Twange, pamoja na uwepo wa mifumo ya kubaini hitilafu, bado kulikuwa na changamoto ya kutambua eneo halisi la tatizo kwa haraka.

Amebainisha kuwa ndege nyuki (drones) zitasaidia kufanya ukaguzi wa haraka na wa kina kabla ya hitilafu kutokea.

“Leo tunazindua utaratibu huu mpya wa kutumia vifaa hivi aina ya ndege nyuki (drones) ambazo zimewekwa mifumo maalum ya kufuatilia miundombinu yetu ya umeme ili kugundua hali ya njia zetu kabla madhara hayajatokea,” ameeleza Bw. Twange

Aliongeza kuwa hatua hiyo pia itapunguza gharama na muda uliokuwa ukitumika awali katika ukaguzi wa kawaida.

“Hiki kitu kilikuwa kinatumia muda mrefu sana na kinatumia gharama kubwa kiasi.Timu zetu zilikuwa zinazunguka na magari, lakini sasa tutatumia muda mfupi kufanya ukaguzi kabla tatizo halijatokea,” alisema.

Kwa upande wake, Meneja wa TANESCO Wilaya ya Kibamba Salma Yahaya alisema matumizi ya ndege nyuki (drones) yatakuwa suluhisho la changamoto za muda na ugumu wa kufikia baadhi ya maeneo wakati wa ukaguzi.

“Ni mfumo utakaoturahisishia kuwapa wateja huduma kwa haraka. Tulikuwa tunatumia muda mwingi kufanya ukaguzi. Tulikuwa tunaenda kwa miguu kila nguzo, lakini kwa mfumo huu tutaweza kuona matatizo kwa urahisi na kupanga mpango kazi wa kuyatatua ili wateja wetu wasikose umeme,” amesema.

Uzinduzi wa matumizi ya ndege nyuki (drones) unaashiria mwendelezo wa hatua muhimu za mageuzi ya Shirika kutumia njia za kidijitali katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya umeme  iliyo bora ndani ya wakati na endelevu.

 


Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga amewataka Watumishi wa Wizara ya Nishati kuendelea kukuza matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini ili kufanikisha ajenda hiyo  ambayo kinara wake ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Ameeleza kuwa ajenda ya nishati safi ya kupikia tayari imeanza kuonesha mafanikio nchini na hivyo kupelekea Tanzania kutambuliwa katika maeneo mbalimbali duniani ikiwemo katika nchi zilizo katika Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC).

Kamishna Luoga amesema hayo tarehe 18 Machi 2026 jijini Dodoma wakati akifungua kikao cha Tatu cha Mkutano wa Pili wa Baraza la Wafanyakazi la Wizara ya Nishati kwa niaba ya Ma-Katibu Wakuu wa Wizara ya Nishati.

“Katika Mkutano wa SADC ambao Tanzania ilishiriki hivi karibuni, kupitia hotuba mbalimbali zilizotolewa katika mkutano huo ikiwemo ya mgeni rasmi ambaye ni Rais wa Zimbabwe, Mhe. Emmerson Mnangagwa aliitambua na kuipongeza Tanzania kwa kupiga hatua kwenye matumizi ya nishati safi ya kupikia, lakini pia katika maazimio ya mwisho yaliyoandaliwa na sekretarieti ya SADC, nchi zote za SADC zilitakiwa kuunga mkono juhudi hizo za Tanzania.” Amesema Kamishna Luoga

Kutokana na hilo, amempongeza Rais, Mhe.Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa juhudi anazochukua kufanikisha ajenda ya nishati safi ya kupikia, pia amewapongeza Watumishi Wizara ya Nishati kwa kufanikisha juhudi hizo ambazo zinalenga kuimarisha afya za watanzania na kupunguza uharibifu wa mazingira.

Aidha, katika kikao hicho cha Baraza la Wafanyakazi kilicholenga kujadili, kutoa maoni, ushauri na kupitisha mapendekezo ya Bajeti ya Wizara ya Nishati kwa mwaka 2026/2027, Mhandisi Luoga amewataka wajumbe wa Baraza kujiridhisha kuhusu maeneo yote muhimu ya vipaumbele vya Wizara kama yametengewa fedha ili kuwezesha Wizara kuhudumia watanzania kwa ufanisi.

Vilevile, amewataka Watumishi kuzingatia maadili ya utumishi wa umma katika utekelezaji wa majukumu yao na kujiepusha na utoro, rushwa na kutanguliza uzalendo katika kuwahudumia watanzania.

Mkutano wa Baraza la Wafanyakazi Wizara ya Nishati umehudhuriwa pia na Viongozi wa TUGHE Mkoa na Tawi la Nishati, pamoja wawakilishi kutoka Taasisi zilizo chini ya Wizara


 




Na Oscar Assenga,TANGA


MBUNGE wa Viti Maalumu (CCM) Mkoa wa Tanga Mhandisi Mwanaisha Ulenge  amekabidhi mchele kilo 200 na Mbuzi katika Kituo cha Kulea Watoto Yatima cha Goodwil Humanity Foundation cha Jijini Tanga ili kuwawezesha kusheherekea kwa amani na upendo sikukuu ya Eid El Firi itakapotangazwa.

Mhandisi Ulenge alikabidhi vitu hivyo katika kituo hicho baada ya kumalizika kwa Iftari iliyoandaliwa na Mbunge huyo ambapo imekuwa ikifanyika kila mwaka kwa lengo la kuileta jamii pamoja iliyokutanisha wadau mbalimbali.

Alisema katika kuelekea kumalizika kwa mwezi mtukufu wa ramadhani ameona aunge mkono kufuturisha jamii ikiwemo kutoa sadaka hiyo ili kuwawezesha watoto hao kusheherekea sikuuu ya Eid El Fitri kwa amani na upendo wakati itakapotangazwa.

“Nimeona nitoe ili watoto waweze kusherehekea sikuuu ya Eid El Fitri kwa kupata chakula kile bora ambacho mwana Mtume amesema kiliwe siku ya Eid Pilau na Birian name kimekabidhi Mbuzi huyu na kilo 200 za Mchele kwa ajili ya kituo hiki hapo itapotangazwa”Alisema Mhe Ulenge

Awali akizungumza katika Iftari hiyo Mkurugenzi wa Goodwil and Humanity Foundation Sayyed Muhdhari Idarus alimshukuru Mbunge Ulenge kwa kuweza kuandaa futari hiyo katika kituo hicho huku akimuomba Mwenyezi Mungu amfalie afya njema na mafanikio.

Hata hivyo aliwashukuru mashehe waliojitokeza katika futari hiyo kwa lengo la kuimarisha amani na upendo ikiwemo kuzishukuru asasi zote zilizoendelea kuunga mkono juhudi za taasisi hiyo ikiwemo  ndugu zao wa nyumba ya furaha iliyopo Bombo wamekuwa wakishirikiana nao kulea watoto.

 Mwisho        

 

 

MWANZA

Wadau wa Sekta ya Milki mkoani Mwanza wamesisitizwa kufanya kazi kwa weledi kwa kuzingatia sheria, taratibu na misingi ya taaluma ya milki ili kuhakikisha sekta hiyo inaendelea kutoa huduma bora na zenye kuaminika kwa wananchi.

Msisitizo huo umetolewa leo Machi 17, 2026 mkoani Mwanza na Kamishna wa Ardhi Msaidizi wa Mkoa huo, Bw. Wilson Luge, wakati akifunga kikao kazi cha wadau wa Sekta ya Milki kilichoandaliwa na Kitengo cha Milki kutoka Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.

Amesema mafunzo na semina zinazotolewa kwa wadau wa Sekta ya Milki yana mchango mkubwa katika kuongeza uelewa wa kitaalamu pamoja na kuimarisha utendaji kazi katika kutoa huduma bora kwa wananchi, hususan katika masuala yanayohusu tathmini ya mali na usimamizi wa milki.

“Tunapenda kuishukuru Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kupitia Kitengo cha Milki kwa kutoa semina na mafunzo kwa wadau wetu wa Sekta ya Milki. Mafunzo haya yatawasaidia kuongeza ujuzi na kuimarisha weledi katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku,” amesema Luge.

Aidha, amewasisitiza wadau hao wa sekta ya milki kufanya kazi kwa kuzingatia maadili ya taaluma yao na kujiepusha na vitendo vinavyokiuka sheria ikiwemo kujihusisha na masuala ya utakatishaji fedha, huku akielezea umuhimu wa kufuata taratibu zote za kisheria na kitaaluma katika kutoaji huduma za tathmini ya mali.

Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kupitia Kitengo cha Milki (Real Estate) inaendesha mijadala ya pamoja na wadau kwa lengo la kupata maoni kuhusu utambuzi na usajili wa Wadau wa Sekta ya Milki ili kuboresha na kukuza sekta ya milki nchini.

Mijadala hiyo inalenga kutoa elimu, kubadilishana uzoefu na kujadili changamoto zinazoikabili sekta ya milki nchini ambapo tayari kitengo hicho kimefanya vikao vya mijadala katika mkoa wa Dar es Salaam, Arusha, Dodoma, Tanga, Mwanza na Morogoro.