Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria imetembelea na kukagua mradi wa ujenzi wa Kituo cha Utengamao cha Taifa unaotekelezwa na Mamlaka ya Kudhibiti na kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) katika eneo la Itega, jijini Dodoma.
Ziara hiyo imefanyika leo tarehe 18 Machi 2026 na kuongozwa na Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Edwin Swale ikiwa ni sehemu ya majukumu ya kamati ya kusimamia na kukagua utekelezaji wa miradi mbalimbali.
Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mhe. Swale amesema kuwa kamati imeridhishwa na hatua ya utekelezaji ambayo mradi umefikia kwani unaenda kutimiza dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kujali Utu na Ustawi wa Watanzania.
Sambamba na hilo, ameipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu kupitia Mamlaka ya kudhibiti na kupambana na dawa za Kulevya kwa kubuni mbinu ya jinsi ya kusaidia waraibu watokanao na matumizi ya madawa za kulevya.

Awali,Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Mhe. Ummy Nderiananga amesema kuwa Mradi huo ni endelevu ikiwa ni juhudi ya Serikali katika mapambano dhidi ya Dawa za kulevya na kuahidi kuendelea kushirikiana na Taasisi binafsi katika mapambano dhidi ya matumizi ya Dawa za kulevya Nchini.

Kwa upande wake Kamishna Jenerali wa Mamlaka ya Kudhibiti na kupambana na Dawa za kulevya Bw. Aretas Lymo ameongeza kuwa kituo hiko kinatarajia kutoa huduma za matibabu, urekebishaji wa kitabia pamoja programu za kuwawezesha waathirika kurejea katika jamii wakiwa na uwezo wa kujitegemea.
Wakati huo huo, Makamu Mwenyekiti Mhe. Swale ameelekeza kuwa Ujenzi wa kituo hicho cha utengamao uzingatie Uwepo wa Miundombinu ya watu wenye mahitaji maalum na kutilia maanani malengo ya kituo ya kuwasaidia kiujuzi waraibu wa madawa ya kulevya .




Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) umeingia katika mpango wa ushirikiano na kampuni ya Land Africa Safaris ili kukuza utalii wa ikolojia kupitia tukio la Cape to Cairo Arusha International Marathon linalotarajiwa kufanyika Mei 28 hadi 30, 2026 mkoani Arusha.
Makubaliano hayo yamefikiwa katika kikao kilichofanyika Machi 17, 2026 katika Ofisi ya Mhifadhi Mkuu wa Ziwa Duluti, Arumeru.
Akizungumza baada ya kikao hicho, Mhifadhi Mkuu wa Ziwa Duluti, Peter A. Myonga, alisema ushirikiano huo ni fursa muhimu kwa TFS kutumia michezo kutangaza vivutio vya misitu na kuongeza idadi ya watalii wanaotembelea maeneo hayo.
Alisema tukio hilo linatarajiwa kuvutia zaidi ya washiriki 5,000 kutoka ndani na nje ya nchi, hatua itakayochochea ongezeko la wageni, muda wa kukaa kwa watalii jijini Arusha na mapato yatokanayo na utalii.
Kwa mujibu wa Myonga, TFS imejipanga kushiriki kikamilifu katika mbio hizo ambapo vivutio vyake vya Napuru na Ziwa Duluti vitatembelewa na washiriki wa mbio hizo kwa ajili ya kutangaza utalii wa misitu na nyuki (api-tourism).
Aidha, alisema washiriki wa mbio hizo watapata fursa ya kutembelea vivutio vya misitu ikiwemo Shamba la Miti Meru na Ziwa Duluti kabla na baada ya tukio, huku mipango ikiwekwa kuhakikisha katika msimu ujao wa 2027 njia ya mbio inapita ndani ya hifadhi hizo ili kuongeza mvuto wa utalii.
Aliongeza kuwa TFS itanufaika pia kwa kuanzisha mabanda ya maonyesho, kutengeneza vifurushi vya utalii, huduma za kambi katika eneo la Napuru na kushiriki katika hafla ya Gala Dinner itakayotoa jukwaa la kuitangaza sekta ya misitu na nyuki.
Kwa upande wake, Haffy Mohamed kutoka Land Africa Safaris alisema wataendelea kushirikiana na TFS kuhakikisha tukio hilo linakuwa chachu ya kukuza utalii wa michezo nchini.
Hatua hiyo ni sehemu ya jitihada za kuunganisha sekta ya michezo na utalii ili kuongeza mchango wa rasilimali za asili katika uchumi wa Taifa.
Shirika la Umeme Tanzania, TANESCO, limezindua rasmi matumizi ya ndege nyuki (drones) kwa ajili ya kufanya ukaguzi wa njia za kusafirisha na kusambaza umeme ikiwa ni hatua inayolenga kuongeza ufanisi wa utoaji huduma na kupunguza muda wa kutatua changamoto za kukatika kwa umeme.
Uzinduzi huo umefanyika tarehe 17 Machi 2026 katika Ofisi za TANESCO, Ubungo jijini Dar es Salaam, ukiongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika hilo, Bw. Lazaro Twange.
Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Bw. Twange amesema TANESCO inasimamia mtandao mkubwa wa miundombinu ya umeme nchini unaohitaji ufuatiliaji wa karibu kwa kutumia teknolojia za kisasa.
“Tuna njia za kusafirisha umeme ambazo zimetembea urefu wa takribani kilomita 8,500, na tuna njia za kusambaza umeme ambazo zimetembea karibu kilomita 200,000. Njia hizi zimepita ardhini kwenye mapori, pembezoni mwa barabara na maeneo yetu,” amesema Bw. Twange.
Ameeleza kuwa jukumu la msingi la Shirika hilo ni kuhakikisha wateja wanapunguziwa muda wa utatuzi wa pale changamoto za umeme zinapojitokeza na kuhakikisha huduma inarejea kwa wakati wote.
“Kazi yetu ya kuhudumia wateja, moja ya kitu tunachopambana nacho zaidi ni kuhakikisha wateja wanapata umeme. Leo tumeanza safari ya mapinduzi ya teknolojia ya kuturahisishia kufanya kazi zetu,” alisisitiza.
Kwa mujibu wa Bw. Twange, pamoja na uwepo wa mifumo ya kubaini hitilafu, bado kulikuwa na changamoto ya kutambua eneo halisi la tatizo kwa haraka.
Amebainisha kuwa ndege nyuki (drones) zitasaidia kufanya ukaguzi wa haraka na wa kina kabla ya hitilafu kutokea.
“Leo tunazindua utaratibu huu mpya wa kutumia vifaa hivi aina ya ndege nyuki (drones) ambazo zimewekwa mifumo maalum ya kufuatilia miundombinu yetu ya umeme ili kugundua hali ya njia zetu kabla madhara hayajatokea,” ameeleza Bw. Twange
Aliongeza kuwa hatua hiyo pia itapunguza gharama na muda uliokuwa ukitumika awali katika ukaguzi wa kawaida.
“Hiki kitu kilikuwa kinatumia muda mrefu sana na kinatumia gharama kubwa kiasi.Timu zetu zilikuwa zinazunguka na magari, lakini sasa tutatumia muda mfupi kufanya ukaguzi kabla tatizo halijatokea,” alisema.
Kwa upande wake, Meneja wa TANESCO Wilaya ya Kibamba Salma Yahaya alisema matumizi ya ndege nyuki (drones) yatakuwa suluhisho la changamoto za muda na ugumu wa kufikia baadhi ya maeneo wakati wa ukaguzi.
“Ni mfumo utakaoturahisishia kuwapa wateja huduma kwa haraka. Tulikuwa tunatumia muda mwingi kufanya ukaguzi. Tulikuwa tunaenda kwa miguu kila nguzo, lakini kwa mfumo huu tutaweza kuona matatizo kwa urahisi na kupanga mpango kazi wa kuyatatua ili wateja wetu wasikose umeme,” amesema.
Uzinduzi wa matumizi ya ndege nyuki (drones) unaashiria mwendelezo wa hatua muhimu za mageuzi ya Shirika kutumia njia za kidijitali katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya umeme iliyo bora ndani ya wakati na endelevu.
Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga amewataka Watumishi wa Wizara ya Nishati kuendelea kukuza matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini ili kufanikisha ajenda hiyo ambayo kinara wake ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Ameeleza kuwa ajenda ya nishati safi ya kupikia tayari imeanza kuonesha mafanikio nchini na hivyo kupelekea Tanzania kutambuliwa katika maeneo mbalimbali duniani ikiwemo katika nchi zilizo katika Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC).
Kamishna Luoga amesema hayo tarehe 18 Machi 2026 jijini Dodoma wakati akifungua kikao cha Tatu cha Mkutano wa Pili wa Baraza la Wafanyakazi la Wizara ya Nishati kwa niaba ya Ma-Katibu Wakuu wa Wizara ya Nishati.
“Katika Mkutano wa SADC ambao Tanzania ilishiriki hivi karibuni, kupitia hotuba mbalimbali zilizotolewa katika mkutano huo ikiwemo ya mgeni rasmi ambaye ni Rais wa Zimbabwe, Mhe. Emmerson Mnangagwa aliitambua na kuipongeza Tanzania kwa kupiga hatua kwenye matumizi ya nishati safi ya kupikia, lakini pia katika maazimio ya mwisho yaliyoandaliwa na sekretarieti ya SADC, nchi zote za SADC zilitakiwa kuunga mkono juhudi hizo za Tanzania.” Amesema Kamishna Luoga
Kutokana na hilo, amempongeza Rais, Mhe.Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa juhudi anazochukua kufanikisha ajenda ya nishati safi ya kupikia, pia amewapongeza Watumishi Wizara ya Nishati kwa kufanikisha juhudi hizo ambazo zinalenga kuimarisha afya za watanzania na kupunguza uharibifu wa mazingira.
Aidha, katika kikao hicho cha Baraza la Wafanyakazi kilicholenga kujadili, kutoa maoni, ushauri na kupitisha mapendekezo ya Bajeti ya Wizara ya Nishati kwa mwaka 2026/2027, Mhandisi Luoga amewataka wajumbe wa Baraza kujiridhisha kuhusu maeneo yote muhimu ya vipaumbele vya Wizara kama yametengewa fedha ili kuwezesha Wizara kuhudumia watanzania kwa ufanisi.
Vilevile, amewataka Watumishi kuzingatia maadili ya utumishi wa umma katika utekelezaji wa majukumu yao na kujiepusha na utoro, rushwa na kutanguliza uzalendo katika kuwahudumia watanzania.
Mkutano wa Baraza la Wafanyakazi Wizara ya Nishati umehudhuriwa pia na Viongozi wa TUGHE Mkoa na Tawi la Nishati, pamoja wawakilishi kutoka Taasisi zilizo chini ya Wizara
Na Oscar Assenga,TANGA
MBUNGE wa Viti Maalumu (CCM) Mkoa wa Tanga Mhandisi Mwanaisha Ulenge amekabidhi mchele kilo 200 na Mbuzi katika Kituo cha Kulea Watoto Yatima cha Goodwil Humanity Foundation cha Jijini Tanga ili kuwawezesha kusheherekea kwa amani na upendo sikukuu ya Eid El Firi itakapotangazwa.
Mhandisi Ulenge alikabidhi vitu
hivyo katika kituo hicho baada ya kumalizika kwa Iftari iliyoandaliwa na Mbunge
huyo ambapo imekuwa ikifanyika kila mwaka kwa lengo la kuileta jamii pamoja iliyokutanisha
wadau mbalimbali.
Alisema katika kuelekea kumalizika
kwa mwezi mtukufu wa ramadhani ameona aunge mkono kufuturisha jamii ikiwemo
kutoa sadaka hiyo ili kuwawezesha watoto hao kusheherekea sikuuu ya Eid El
Fitri kwa amani na upendo wakati itakapotangazwa.
“Nimeona nitoe ili watoto waweze
kusherehekea sikuuu ya Eid El Fitri kwa kupata chakula kile bora ambacho mwana
Mtume amesema kiliwe siku ya Eid Pilau na Birian name kimekabidhi Mbuzi huyu na
kilo 200 za Mchele kwa ajili ya kituo hiki hapo itapotangazwa”Alisema Mhe
Ulenge
Awali akizungumza katika Iftari hiyo Mkurugenzi wa Goodwil and Humanity Foundation Sayyed Muhdhari Idarus alimshukuru Mbunge Ulenge kwa kuweza kuandaa futari hiyo katika kituo hicho huku akimuomba Mwenyezi Mungu amfalie afya njema na mafanikio.
Hata hivyo aliwashukuru mashehe waliojitokeza katika futari hiyo kwa lengo la kuimarisha amani na upendo ikiwemo kuzishukuru asasi zote zilizoendelea kuunga mkono juhudi za taasisi hiyo ikiwemo ndugu zao wa nyumba ya furaha iliyopo Bombo wamekuwa wakishirikiana
nao kulea watoto.
MWANZA
Wadau wa Sekta ya Milki mkoani Mwanza wamesisitizwa kufanya kazi kwa weledi kwa kuzingatia sheria, taratibu na misingi ya taaluma ya milki ili kuhakikisha sekta hiyo inaendelea kutoa huduma bora na zenye kuaminika kwa wananchi.
Msisitizo huo umetolewa leo Machi 17, 2026 mkoani Mwanza na Kamishna wa Ardhi Msaidizi wa Mkoa huo, Bw. Wilson Luge, wakati akifunga kikao kazi cha wadau wa Sekta ya Milki kilichoandaliwa na Kitengo cha Milki kutoka Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.
Amesema mafunzo na semina zinazotolewa kwa wadau wa Sekta ya Milki yana mchango mkubwa katika kuongeza uelewa wa kitaalamu pamoja na kuimarisha utendaji kazi katika kutoa huduma bora kwa wananchi, hususan katika masuala yanayohusu tathmini ya mali na usimamizi wa milki.
“Tunapenda kuishukuru Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kupitia Kitengo cha Milki kwa kutoa semina na mafunzo kwa wadau wetu wa Sekta ya Milki. Mafunzo haya yatawasaidia kuongeza ujuzi na kuimarisha weledi katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku,” amesema Luge.
Aidha, amewasisitiza wadau hao wa sekta ya milki kufanya kazi kwa kuzingatia maadili ya taaluma yao na kujiepusha na vitendo vinavyokiuka sheria ikiwemo kujihusisha na masuala ya utakatishaji fedha, huku akielezea umuhimu wa kufuata taratibu zote za kisheria na kitaaluma katika kutoaji huduma za tathmini ya mali.
Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kupitia Kitengo cha Milki (Real Estate) inaendesha mijadala ya pamoja na wadau kwa lengo la kupata maoni kuhusu utambuzi na usajili wa Wadau wa Sekta ya Milki ili kuboresha na kukuza sekta ya milki nchini.
Mijadala hiyo inalenga kutoa elimu, kubadilishana uzoefu na kujadili changamoto zinazoikabili sekta ya milki nchini ambapo tayari kitengo hicho kimefanya vikao vya mijadala katika mkoa wa Dar es Salaam, Arusha, Dodoma, Tanga, Mwanza na Morogoro.


Zaidi ya wakazi 57,000 wilayani Mkinga mkoa wa Tanga wanatarajiwa kunufaika na mradi mkubwa wa maji wa Mkinga-Horohoro uliofikia asilimia 65 ya utekelezaji wake huku kijiji kimoja cha Mtimbwani kikiwa tayari kinapata huduma hiyo.
Mradi huo unatekelezwa na mkandarasi mzawa STC kwa gharama ya shilingi bilioni 35 ambapo utakapokamilika utaongeza huduma ya majisafi wilayani Mkinga kufikia asilimia 88.
Hayo yamebainishwa na Meneja wa RUWASA mkoa wa Tanga Mha. Upendo Lugongo wakati akitoa taarifa ya mradi kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira iliyofanya ziara ya kukagua maendeleo ya mradi huo Machi 17, 2026 ambapo alisema jumla ya vijiji 37 vinatarajiwa kunufaika baada ya mradi kukamilika.
Alisema katika awamu ya kwanza jumla ya vijiji 27 vitanufaika na tayari wakazi wa kijiji kimoja cha Mtimbwani wameshaanza kufurahia huduma ya maji ikiwemo shule na zahanati za kijiji hicho ambazo nazo zimeunganishiwa majisafi ya bomba.





Furaha imetanda kwa kinamama wa taasisi ya JAI baada ya kupokea sadaka ya Iftar kutoka kwa taasisi ya Ramadhani Charity Program 2026, ikiwa ni sehemu ya kuendelea kusaidia jamii katika mwezi mtukufu wa Ramadhani.
Na Mwandishi Wetu.
Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imesisitiza kuwa uhuru wa vyombo vya habari nchini upo, unalindwa kisheria na unatambuliwa katika Katiba pamoja na Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, huku ikitoa wito kwa wanahabari kuzingatia maadili na uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu yao.
Kauli hiyo ya JAB imetolewa na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi hiyo, Wakili Patrick Kipangula, alipokuwa akizungumza katika kipindi cha moja kwa moja cha Hatua za Ushindi kinachorushwa na Kituo cha Televisheni cha Hope Channel Tanzania, leo Machi 17, 2026 jijini Dar es Salaam.
Ameeleza kuwa kifungu cha 7 cha Sheria ya Huduma za Habari kinaweka bayana haki na uhuru wa vyombo vya habari, ikiwa ni pamoja na haki ya mwandishi wa habari kutafuta, kuchakata na kusambaza taarifa, huku wananchi wakiwa na haki ya kupata taarifa sahihi kuhusu maendeleo yanayowazunguka.
“Uhuru wa vyombo vya habari upo na unalindwa kisheria. Mwandishi ana haki ya kutafuta na kusambaza taarifa, na mwananchi ana haki ya kupata taarifa. Huu ndio msingi wa uwazi na uwajibikaji katika jamii,” amesema Wakili Kipangula.
Hata hivyo, amesisitiza kuwa uhuru huo unaambatana na wajibu wa kuzingatia maadili ya taaluma, akibainisha kuwa dhana ya uwajibikaji haipaswi kuchanganywa na kile kinachoitwa ukandamizaji wa vyombo vya habari.
Amebainisha kuwa baadhi ya malalamiko ya ukandamizaji yanatokana na kutokuzingatia misingi ya kitaaluma, hususan pale ambapo taarifa zinapotolewa bila uthibitisho, uwiano au kwa lugha isiyozingatia maadili.

“Ni muhimu kutofautisha kati ya uwajibikaji na ukandamizaji. Usipozingatia maadili ya taaluma, usiseme unakandamizwa. Uwajibikaji ni sehemu ya taaluma, na haupaswi kutafsiriwa kama kubanwa kwa uhuru wa habari,” amesisitiza Kipangula.
Katika hatua nyingine, Wakili Kipangula ameeleza kuwa Serikali imeendelea kuboresha mazingira ya sekta ya habari kupitia mageuzi ya kisheria na kisera, ikiwemo kufutwa kwa Sheria ya Magazeti iliyokuwa ikitajwa kuwa kandamizi na kuanzishwa kwa Sheria ya Huduma za Habari inayolenga kuimarisha uhuru, uwajibikaji na weledi katika tasnia hiyo.
Amesema maboresho hayo yameleta mwelekeo mpya unaowezesha vyombo vya habari na wanahabari kufanya kazi zao kwa uhuru zaidi, huku wakizingatia viwango vinavyokubalika kitaaluma na kisheria.
Aidha, ametoa wito kwa wanahabari kuendelea kuilinda taaluma yao kwa kuzingatia ukweli, usahihi na uwiano katika utoaji wa taarifa, sambamba na kuheshimu haki za wananchi za kupata taarifa sahihi na kwa wakati kwa mujibu wa Sheria ya Kupata Taarifa.
Amesisitiza umuhimu kwa waajiri kote nchini kuhakikisha wanapata wataalamu wenye sifa stahiki kuingia katika menejimenti zao, sanjari na kuwatumia waandishi wenye ithibati, katika kazi zote za kihabari ili kulinda na kuipa thamani taaluma ya uandishi wa habari.
Na OWM - TAMISEMI, Arusha
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya TAMISEMI, Mhe. Florent Kyombo ameipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mkoa na Serikali za Mitaa (OWM- TAMISEMI), kwa usimamizi mzuri wa utekelezaji wa miradi ya TACTIC katika Jiji la Arusha, miradi ambayo imeweka kiwango bora cha utekelezaji wa miradi ya aina hiyo ambayo inatekelezwa katika miji na majiji 45 nchini.
Mhe. Kyombo ametoa pongezi hizo leo Machi 17, 2026 mara baada ya kamati yake kutembelea, kukagua na kuridhishwa na usimamizi wa utekelezaji wa miradi ya ujenzi wa Kituo Kikuu cha Mabasi yaendayo mikoani (Bondeni City Bus Terminal), ujenzi wa soko la Mrombo, ujenzi wa soko la Kilombero pamoja na ujenzi wa mradi wa uboreshaji wa bustani ya mapumziko Themi.
“Naungana na wajumbe wenzangu kutoa pongezi za dhati kwa utekelezaji mzuri wa miradi ya TACTIC katika jiji la Arusha, hakika utekelezaji wa miradi hii umeweka kiwango bora cha namna ya kutekeleza miradi ya aina hii nchini,” amesistiza Prof. Shemdoe.
Aidha, Mhe. Kyombo amempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuleta fedha za utekelezaji wa miradi pamoja na kumpa dhamana ya usimamizi wa miradi hiyo Prof. Shemdoe na watendaji wanaomsaidia, ambao wanaitendea haki dhamana waliyopewa na Mheshimiwa Rais.
Sanjari na hilo, Mhe. Kyombo amempongeza Mkandarasi wa Kampuni ya M/S MOHAMMEDI BUILDERS LIMITED kwa kiwango kizuri cha utekelezaji wa miradi yote minne ya TACTIC inayotekelezwa katika jiji la Arusha, ambayo itachochea ukuaji wa uchumi ndani ya jiji hilo.
Akizungumzia suala la ushirikishaji wa wadau katika miradi hiyo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu-TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amesema kuwa kabla ya kuanza kutekelezwa miradi hiyo, timu ya kuandaa mazingira ya utekelezaji wa mradi hupita ikiwa na fomu maaluum ya kupokea maoni ya wadau kuhusiana na mradi husika, na kuongeza kuwa maoni ya wadau yalizingatiwa kwani hicho ni kigezo muhimu cha miradi yote inayotekelezwa na Benki ya Dunia.
Naye mmoja wa Wajumbe wa Kamati hiyo ya Bunge ya Kudumu ya TAMISEMI Mhe. Hawa Mwaifunga, amesema amefarijika kuona hatua nzuri iliyofikiwa ya Ujenzi wa Kituo Kikuu cha Mabasi yaendayo mikoani na kuongeza kuwa kituo hicho kitakapokamilika kitakuwa na manufaa kwa wananchi wa Jiji la Arusha.
Kwa upande wake, Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya TAMISEMI Mhe. Jafari Chege ameupongeza uongozi wa mkoa na Jiji la Arusha kwa kutekeleza vizuri miradi ya TACTIC ambayo imelenga kuboresha utoaji wa huduma za kijamii na kukuza uchumi wa wananchi wa Jiji la Arusha.
Akizungumza kwa niaba ya wananchi, Diwani wa Kata ya Themi Mhe. Melance Kinabo, amemshukuru na kumpongeza Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kulijali Jiji la Arusha kwa kuliletea fedha za utekelezaji wa miradi minne ya TACTIC, ambayo ikikamilika itaongeza wigo wa wananchi kupata ajira zitakazowaingizia kipato.
Na Mwandishi Wetu, Tanga.
Wananchi wa Wilaya ya Mkinga mkoani Tanga wanatarajiwa kunufaika zaidi kiuchumi kupitia uwekezaji wa Serikali katika sekta ya kilimo cha mwani, hatua inayolenga kuongeza thamani ya mazao ya bahari na kuboresha maisha ya jamii za pwani.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa kaushio jipya na mashine mbili za kisasa za kusaga mwani uliofanyika tarehe 16 Machi 2026 katika Kijiji cha Kichaka Miba, Wilaya ya Mkinga, Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Mhe. Ummy H. Nderiananga, amesema mradi huo ni sehemu ya jitihada za Serikali kuimarisha uchumi wa wananchi wa maeneo ya pwani.
Mradi wa Kuimarisha Usalama wa Bahari unaratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Idara ya Menejimenti ya Maafa kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), na unatekelezwa na Chuo cha Mipango na Maendeleo Vijijini (IRDP) Tawi la Mwanza kwa ushirikiano na Halmashauri ya Wilaya ya Mkinga ambapo Lengo lake ni kuimarisha ufuatiliaji na ulinzi wa bahari pamoja na kuongeza thamani ya rasilimali za baharini kwa manufaa ya jamii.
Mhe. Nderiananga amesema kupitia mradi huo, Serikali imenunua boti mbili za doria, kujenga kaushio la kisasa la mwani, kusimika mashine za kusaga mwani na kutoa mafunzo kwa vikundi vya wakulima. Ameongeza kuwa hatua hizo zitaboresha ubora wa mwani, kupanua masoko, kuongeza kipato cha wakulima na kusaidia kuzuia vitendo vya kihalifu baharini.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Chuo cha Mipango na Maendeleo Vijijini (IRDP), Dkt. Guvenail Mkonoko, amesema kabla ya utekelezaji wa mradi huo wataalamu walifanya tathmini iliyobaini changamoto za mbinu duni za kilimo, ukaushaji usio salama na ukosefu wa miundombinu ya kisasa ya uchakataji. 
Naye mwakilishi wa wakulima wa mwani, Bi. Mwamvua Bwebwe, Ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwawezesha kuongeza uzalishaji, kupunguza upotevu wa mazao na kuboresha kipato chao.








.jpeg)
.jpeg)





.jpg)




