Na OWM - TAMISEMI, Dar es Salaam

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu -TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amewaelekeza Mameneja na waratibu wa Mradi wa Uendelezaji Miundombinu ya Miji Tanzania (TACTIC) kuhakikisha magari 14 aliyoyakabidhi yanakwenda kufanya kazi iliyokusudiwa ya usimamizi wa mradi huo ili wananchi wanufaike na barabara, masoko na stendi zinazojengwa kupitia mradi huo.

Prof. Shemdoe ametoa maelelezo hayo leo Februari 21, 2026, wakati wa hafla ya kukabidhi magari hayo kwa Mameneja wa TARURA wa Miji 12 ya kundi la kwanza la Mradi  wa TACTIC, iliyofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Millenium Tower  Kijitonyama, Dar es Salaam.

“Magari haya yamenunuliwa kwa fedha za umma, hivyo yatunzwe na yakatumike kwa kazi za usimamizi wa mradi wa TACTIC na si nyinginezo,” amesisitiza Prof. Shemdoe.

Aidha, Prof. Shemdoe amewata wakandarasi  walio kwenye maeneo ya utekelezaji wa miradi ya TACTIC, kuhakikisha  wanafanya kazi kwa ufanisi kwa kuzingatia mikataba waliosaini  ili miradi hiyo ikamilike kwa wakati, na kuongeza kuwa Serikali haitosita kusitisha mikataba inayosuasua kwa mujibu wa sheria na vipengele vya mikataba husika.

Prof. Shemdoe amesema Serikali haina changamoto ya kukosa fedha za utekelezaji miradi, kwani pindi mkandarasi akiwasilisha hati ya maombi ya malipo analipwa kwa wakati, hivyo hakuna sababu ya wakandarasi kushindwa kukamilisha na kukabidhi miradi kwa wakati.

Kwa upande wake, Meneja wa TARURA Wilaya ya Sumbawanga Mhandisi Albert Kyando ameishukuru Serikali kwa kuwakabidhi magari  yatakayowawezesha kusimamia miradi ya TACTIC kwa karibu   na kuahidi kuwa watayatunza kama Prof. Shemdoe alivyoelekeza kwa maslahi ya umma na taifa.

Naye, Mmoja wa Madereva waliokabidhiwa magari hayo kutoka Jiji la Arusha Bw. Joshua Magati, amesema watayatunza magari hayo kama alivyoelekeza Prof. Shemdoe, na kuongeza kuwa watazingatia muda wa kuyafanyia ukaguzi na matengenezo  pamoja na kuyatumia kwa kazi iliyokusudiwa ya usimamizi wa miradi ya TACTIC.






 


Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba anatarajiwa kuanza ziara ya kikazi ya siku tatu  Mkoani Arusha kuanzia Februari 22-24, 2026,akitokea mkoa wa Kilimanjaro.

Akizungumza na waandishi wa habari Ofisini kwake leo Jumamosi Februari 21, 2026, Mkuu wa Mkoa wa Arusha CPA Amos Gabriel Makalla amesema Mhe. Waziri Mkuu kesho Jumapili ataweka jiwe la msingi kwenye mradi wa ujenzi wa bweni la kisasa la Chuo kikuu cha Kimataifa cha sayansi cha Nelson Mandela,kisha  kukagua upanuzi wa Miundo mbinu ya Hospitali ya Oltrumet pamoja na kuzungumza na wananchi eneo la Ngaramtoni.

"Tarehe 23, Mhe. Waziri Mkuu atakuwa Wilaya ya Longido na atatembelea na kupokea taarifa ya mradi mkubwa wa maji Kata ya Sinya, atazindua mradi wa Upanuzi wa shule ya Sekondari Sinya iliyopanuliwa na kuwa na Kidato cha tano na sita na baadae kutembelea kituo cha utoaji wa huduma za Pamoja (One stop Border Post), Namanga na kisha kuzungumza na wananchi kwenye Viwanja vya shule ya msingi Namanga." Amesema CPA Makalla.

Mhe. Makalla  ametumia fursa hiyo kuwaalika wananchi wote kushiriki katika ziara hiyo,ambapo  amesema kwa siku ya tatu Mhe. Waziri Mkuu atafanya ziara yake Wilaya ya Arusha akitarajiwa kukagua maendeleo ya Ujenzi wa kituo Kikuu cha mabasi Jiji la Arusha eneo la Bondeni City, na kisha kuweka jiwe la msingi kwenye ujenzi wa soko la Kilombero pamoja na kuzungumza na wananchi kupitia Mkutano wa hadhara kwenye eneo hilo la soko Jijini Arusha.

"Naomba niwaalike waananchi wote wa mkoa wa Arusha kuhudhuria kwa wingi katika ziara hiyo na ambaye anahisi anaweza kutumia fursa hiyo kutoa kero yake anakaribishwa sana sisi kazi yetu ni kusimamia wananchi na kuwasaidia."Amesisitiza CPA Makala

Aidha mkuu huyo wa mkoa amesema kuwa mheshimiwa Waziri Mkuu atatembelea wilaya tatu tu na kisha kuelekea mkoani Dodoma kwa ajili ya Vikao vya Chama kisha baadae atarejea kuendelea na ziara hiyo katika wilaya ya Karatu,Monduli na Ngorongoro.

Miradi hiyo  sita  ina  thamani ya shilingi Bilioni 194.2 kwenye Wilaya  za Arumeru, Arusha na Longido ambapo pia atazungumza na wananchi eneo la ngaramtoni Mkoani Arusha.





 


📌Kuhusisha Mifumo ya umeme jua 20,000 katika visiwa 120

📌Rais Samia awawekea wananchi ruzuku hadi ya asilimia 75 kuunganisha umeme

📌Mhe.Salome asema Serikali itafikisha umeme kwa wananchi bila kujali umbali na mtawanyiko wa makazi

Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba amezindua mradi wa kusambaza mifumo ya umeme jua visiwani unaolenga kuweka mifumo 20,000 ya umeme jua katika visiwa 120 kwa gharama ya Shilingi Bilioni 8 ambapo Rais, Dkt.Samia Suluhu Hassan ameweka ruzuku hadi ya asilimia 75 katika gharama za uunganishaji umeme.

Mhe. Salome Makamba amezindua mradi huo katika kisiwa cha Bezi wilayani Ilemela mkoani Mwanza ambapo  mradi huo unatekelezwa chini ya Wakala wa Nishati Vijijini (REA).

"Maeneo ya visiwani na delta yana changamoto za kipekee, zikiwemo umbali kutoka Gridi ya Taifa, gharama kubwa za usafirishaji wa vifaa na mtawanyiko wa makazi unaoongeza gharama za usambazaji wa nishati ya umeme. Hata hivyo, changamoto hizi haziwanyimi wananchi haki ya kupata huduma ndio maana Serikali imekuja na mpango huu mahsusi wa matumizi ya mifumo ya umeme jua pamoja na gridi ndogo kama suluhisho la haraka la  kuwafikia wananchi wa visiwa na maeneo ya pembezoni." Amesema Mhe.Salome

Ameeleza kuwa hatua nyingine iliyochukuliwa na Serikali ili kurahisisha upatikanaji wa umeme katika maeneo kama hayo ya visiwa ni pamoja na kutoa ruzuku kwa mifumo ya umeme jua ili kuharakisha upatikanaji wa nishati safi, kupunguza utegemezi wa vyanzo visivyo endelevu kama dizeli, na kuhakikisha gharama za nishati zinakuwa nafuu.

Amesema mradi huo aliouzindua una mchango wa moja kwa moja katika kukuza Uchumi wa Buluu, ambao ni kipaumbele cha Taifa katika maeneo ya pwani na visiwa kwani mifumo ya umeme jua inayofungwa itawawezesha wavuvi kuongeza thamani ya samaki na dagaa kabla ya kupelekwa sokoni, jambo litakaloongeza mapato ya wananchi, Halmashauri pamoja na nchi, kuimarisha shughuli za ufugaji wa samaki (aquaculture), kilimo cha mwani, na huduma za utalii wa fukwe na visiwa, ambazo zote ni sehemu ya Uchumi wa Buluu. 

Mhe. Salome amemshukuru Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutoa fedha za utekelezaji wa miradi mbalimbali ya nishati na kueleza kuwa Wizara itaendelea kusimamia kwa ukaribu utekelezaji wa miradi hiyo ili kuhakikisha ubora, uwazi na uwajibikaji vinazingatiwa katika kila hatua. 

Aidha, ameiagiza REA na TANESCO kuweka mifumo ya umeme kwa taasisi zinazotoa huduma muhimu kwa jamii kama vituo vya afya, mashule, vituo vya polisi ambavyo hadi sasa bado havijapata huduma hiyo.

Vilevile ameiagiza REA kuchochea matumizi ya nishati safi ya kupikia katika maeneo ya minada, stendi na masoko.Na katika kisiwa hicho cha Bezi wafanye  tathmini ya matumizi ya nishati safi katika soko la samaki na kuweka miundombinu ya nishati safi ya kupikia ili kuwalinda wakaangaji na wateja dhidi ya moshi wa kuni na mkaa ambao una athari kwa afya ya binadamu na mazingira. 

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati (Umeme na Nishati Jadidifu), Mhandisi Edson Ngabo amewaasa wananchi kutumia miradi ya umeme kama sehemu ya mabadiliko ya maisha  kwa kuhakikisha unatumika pia katika shughuli za kiuchumi.

Amesema Serikali inaendelea kuhakikisha miradi ya nishati jadidifu ikiwemo ya jua inakuwa na mchango mkubwa  katika gridi ya taifa na nje ya gridi huku moja ya mifano ukiwa ni mradi huo wa umeme  jua wa bei ya ruzuku uliozinduliwa pamoja na mradi wa Kishapu wa megawati 150.

Ameeleza kuwa, Serikali itaendelea kuhusisha sekta binafsi katika utekelezaji wa miradi ya nishati lengo likiwa ni kufikisha megawati 8000 ifikapo 2030.

Kwa upande wake, Kaimu  Mkurugenzi Mkuu wa REA , Mhandisi Jones Olotu amesema mradi huo utakaotekelezwa katika mikoa nane kwa miaka miwili ni sehemu ya utekelezaji wa mpango wa nishati  (Energy Compact)  ambao moja ya azimio lake ni kufikisha huduma ya umeme kwa wananchi wote ifikapo 2030 na hii ukijumuisha kuunga wateja wapya takriban milioni 8.

Kwa Mkoa wa Mwanza amesema mradi utagusa visiwa 65 kwa gharama ya shilingi bilioni 4.8 ambapo Serikali tayari imetoa shilingi bilioni 3.3 na pesa iliyobaki wananchi watalipia kwa mfumo wa ruzuku.

Mikoa itakayonufaika na mradi wa kusambaza mifumo ya umeme jua visiwani unaolenga kuweka mifumo 20,000 ya umeme jua katika visiwa 120 ni Mwanza, Geita, Kagera, Mara, Rukwa, Lindi, Mtwara na Pwani.

















Na Mwandishi Wetu Wetu - DODOMA


Wakala wa Vipimo Tanzania (WMA) imetoa mafunzo ya vipimo kwa wanafunzi wa Dr. Samia Dodoma Secondary School, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa vipimo sahihi katika biashara na maisha ya kila siku.

Katika zoezi hilo, wanafunzi walipata fursa ya kujifunza kuhusu dhima na majukumu ya Wakala huo, pamoja na namna unavyolinda maslahi ya watumiaji na wafanyabiashara kwa kuhakikisha vipimo vinakuwa sahihi na vya kuaminika.

Akizungumza baada ya mafunzo hayo, Meneja Mawasiliano na Uhusiano wa WMA, Veronica Simba, amesema elimu ya vipimo itatolewa katika mikoa yote ya Tanzania Bara ili kuhakikisha wanafunzi wengi zaidi wanapata uelewa wa matumizi sahihi ya vipimo.

Amesema mpango huo unalenga kukuza uelewa wa masuala ya vipimo kwa vijana, sambamba na kuimarisha utamaduni wa uadilifu na uwajibikaji katika sekta ya biashara nchini.

Kwa upande wake, Meneja wa Wakala wa Vipimo Mkoa wa Dodoma, Said Ibrahim, amesema mafunzo hayo yanaenda sambamba na uanzishwaji wa Klabu za Vipimo mashuleni ili kuendelea kuandaa mabalozi mahiri watakaotoa elimu ya vipimo shuleni na katika jamii kwa ujumla.

“Kwa Dodoma tayari tumeshatoa mafunzo katika shule mbili ambazo ni Shule ya Msingi Mtemi Mazengo na leo tumetoa hapa katika Shule ya Sekondari ya Dkt. Samia Dodoma. Tunaamini mabadiliko katika matumizi ya vipimo sahihi yataongezeka,” amesema Said.

Naye , Mwalimu Mussa Madandi, ambaye pia ni mlezi wa Klabu ya Vipimo shuleni hapo, amesema elimu hiyo wamekuwa wakiifundisha darasani, lakini mafunzo yaliyotolewa na WMA yamewapa wanafunzi nafasi ya kujifunza kwa vitendo, jambo litakalosaidia kuongeza uelewa na kuimarisha matumizi ya vipimo sahihi.

“Vipimo ni somo tunalolifundisha karibu kila darasa, lakini leo wanafunzi wamepata mafunzo kwa vitendo kutoka kwa wataalamu wenyewe. Naamini hali hii itaongeza hamasa ya kuzingatia usahihi katika matumizi ya vipimo na kuwafanya wawe mabalozi wazuri kwa wazazi wao na jamii inayowazunguka,” amesema Mwalimu Madandi.

Mwanafunzi Itabangola Elias amesema elimu hiyo imewasaidia kuelewa namna ya kutambua vipimo sahihi na kujikinga dhidi ya udanganyifu unaoweza kujitokeza katika biashara.

Baada ya mafunzo hayo, wanafunzi walishiriki kujibu maswali mbalimbali kuhusiana na vipimo na shughuli za Wakala huo, ambapo waliofanya vizuri walipatiwa zawadi mbalimbali kama sehemu ya kuwahamasisha kuendelea kujifunza na kuwa mabalozi wa matumizi sahihi ya vipimo katika jamii.




Na Mwandishi Wetu

MBUNGE wa Jimbo la Kisarawe mkoani Pwani, Dkt. Selemani Jafo, ametangaza mpango wa kuweka kambi maalum katika eneo la ujenzi wa Daraja la Kitomondo lililopo katika barabara ya Mzenga–Gwata, akilenga kuharakisha ukamilishaji wa mradi huo na kuondoa adha wanazokumbana nazo wananchi hasa nyakati za mvua.

Dkt. Jafo alitoa kauli hiyo wakati wa ziara yake ya kikazi katika Kata za Mzenga na Mafizi ndani ya Jimbo la Kisarawe, ambapo alikagua maendeleo ya mradi huo na kusikiliza changamoto za wananchi wanaotegemea daraja hilo kwa shughuli za kila siku.

Daraja la Kitomondo linajengwa na kampuni ya Neloyt Tanzania Limited kwa gharama ya shilingi milioni 359.67 chini ya usimamizi wa Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini (TARURA), hata hivyo ujenzi wake umechelewa kukamilika hali inayosababisha usumbufu mkubwa kwa wakazi wa Mzenga na Mafizi.

Mbunge huyo amesema daraja hilo ni kiungo muhimu kwa wakazi wa kata hizo na vijiji vya Mafizi, Nyani, Gwata na Ving’andi, akieleza kuwa kuchelewa kwake kumeathiri shughuli za kiuchumi na kijamii ikiwemo usafiri wa wanafunzi, wagonjwa na wafanyabiashara.

Amesisitiza kuwa kukamilika kwa daraja hilo kutarahisisha usafiri na usafirishaji wa mazao na bidhaa, hivyo kuchochea maendeleo katika Jimbo la Kisarawe.

Kwa upande wake, Meneja wa TARURA Wilaya ya Kisarawe, Eng. Africano Orota, amemhakikishia Dkt. Jafo kuwa wataongeza usimamizi na kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa maelekezo yaliyotolewa ili kuhakikisha mradi huo unakamilika kwa wakati na kwa viwango vinavyotakiwa.

Na.Mwandishi Wetu

Taasisi ya Jafo Education Foundation imefadhili jumla ya vijana 51 kusoma katika Chuo cha FDC Kisarawe - Mzenga, kwa lengo la kuwawezesha kupata ujuzi wa fani mbalimbali za ufundi.

Akizungumza wakati wa ziara yake ya kukagua miradi na kuzungumza na wananchi katika Kata ya Mzenga, Mbunge wa Jimbo la Kisarawe Mhe.Dkt. Selemani Jafo, amesema vijana hao 51 watatoka katika kata zote 17 za wilaya hiyo na taasisi hiyo itagharamia ada zao za masomo.

 "Hii ni fursa muhimu kwa vijana wa Kisarawe kujipatia ujuzi utakaowawezesha kujiajiri na kuajiriwa, hasa katika kipindi hiki ambacho soko la ajira linahitaji wataalamu wenye ujuzi wa vitendo."amesema Dkt. Jafo

Dkt.Jafo amesema kuwa Chuo cha FDC Kisarawe – Mzenga ni chuo kipya kilichojengwa wilayani humo na tayari kinatoa mafunzo katika fani mbalimbali zikiwemo ufundi magari, ushonaji, ujenzi, mapishi, umeme, kompyuta pamoja na mafunzo ya muda mfupi.

Aidha, Dkt. Jafo ameeleza kuwa tangu mwaka 2010 amefanikiwa kusaidia zaidi ya vijana 500 kutoka familia zenye changamoto kusoma katika ngazi mbalimbali, ikiwemo kidato cha tano, astashahada, stashahada na shahada.

Katika kuendeleza juhudi za kukuza elimu ya ufundi, tarehe 20 Februari, Dkt. Jafo kupitia taasisi yake amekabidhi msaada wa vyerehani vinne vya umeme katika chuo hicho, ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Samia Suluhu Hassan.

Amesema kuwa dhamira kuu ni kuwawezesha vijana katika fani za ufundi ili kujenga msingi imara wa ajira rasmi na zisizo rasmi, pamoja na kuongeza kasi ya maendeleo katika Wilaya ya Kisarawe.

 


Serikali imeendelea kuimarisha huduma na mazingira katika Makazi ya Wazee na Wasiojiweza kwa lengo la kuhakikisha wazee wanaishi kwa heshima, usalama na kupata huduma stahiki za kijamii na afya.

Hayo yamesema na Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi tarehe 20, Februari 2026 wakati alipotembelea Makazi ya wazee Nunge  yaliyopo Kigamboni, mkoani Dar Es Salaam kwa lengo la kujionea hali ya utoaji wa huduma na kusikiliza changamoto zinazowakabili wazee wanaoishi katika kituo hicho. 

Mhandisi Mahundi amesema Serikali inawatambua Wazee kama tunu, hazina ya hekima na msingi wa maadili ya Taifa hivyo Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya uongozi wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuchukua hatua madhubuti za kuboresha mazingira ya kuishi kwa Wazee, hususan wale walio katika mazingira hatarishi na wasiokuwa na msaada wa familia.

“Ndugu zangu nipende kusema Serikali inawatambua Wazee kama tunu, hazina ya hekima na msingi wa maadili ya Taifa letu, Tunathamini mchango wenu mkubwa walioutoa katika ujenzi wa familia, jamii na Taifa na tutaendelea kuhakikisha wanaishi kwa heshima, usalama na utu wanaostahili ni ukweli usiopingika kuwa kuzeeka ni hatua ya maisha ambayo kila mmoja wetu anaelekea kuifikia na kufikia uzee ni neema kubwa ya Mwenyezi Mungu,” amesema Mhandisi Mahundi. 

Kwa upande wake, Mfawidhi wa Makazi ya Wazee Nunge, Jacklina Kanyamwenge, amesema kituo hicho kinaendelea kutoa huduma mbalimbali kwa wazee ikiwemo malazi, lishe na huduma za afya kwa lengo la kuhakikisha ustawi wao unaimarika.

“Tunawahudumia wazee hawa kwa kuwapatia mahitaji yao muhimu ya kila siku na tunaendelea kushirikiana na Serikali na wadau mbalimbali kuboresha zaidi huduma na mazingira ya makazi haya ili yaendane na mahitaji yao,” amesema Jacklina.

Nao Baadhi ya wazee wanaoishi katika makazi hayo wameishukuru Serikali kwa kuendelea kuwapatia matunzo na huduma muhimu, wakisema hatua hiyo imewapa faraja na kuwafanya waishi kwa matumaini na amani.









 


Baraza la Ardhi na Nyumba la Wilaya, Mkoa wa Dodoma limewasikiliza wananchi wa jamii ya Kiiraqw waliofika katika Baraza hilo kuwasilisha hoja na ushahidi wao katika mgogoro wa ardhi, wakidai kumiliki kihalali shamba lenye ukubwa wa ekari nane lililopo Wilaya ya Chamwino, Mkoa wa Dodoma.

Hatua hiyo imekuja kufuatia maombi ya wadaawa hao ambao ni pande mbili zinazohusika katika shauri hilo, kubainisha kuwa wanakabiliwa na changamoto ya lugha, hali iliyokuwa ikiathiri uwezo wao wa kujitetea na kueleza kwa uwazi hoja zao mbele ya Mwenyekiti wa Baraza hilo, Mhe. Omary Mbega.

Kutokana na hilo, Baraza lilitoa huduma ya ukalimani kupitia mkalimani, Ndg. Simon Tlatlaa Emmay, ambaye alitafsiri maelezo yao na kuwawezesha wadaawa hao kufafanua kwa kina madai yao, kuwasilisha ushahidi pamoja na vielelezo muhimu bila kikwazo cha lugha.

Shauri hilo ni Shauri la Ardhi Na. 92 la mwaka 2025, linalomhusu Ekaristi Ngu’nda kama Mleta Maombi dhidi ya Lolote Nanacha na Martin Lolo Nanacha, ambao ni Wajibu Maombi. Mgogoro huo unahusu umiliki wa shamba lenye ukubwa wa ekari nane lililopo Kitongoji cha Msunjirire, Kijiji cha Zajilwa, Kata ya Zajilwa, Wilaya ya Chamwino, Mkoa wa Dodoma.

Katika madai yake, Mleta Maombi anadai kuwa ndiye mmiliki halali wa eneo hilo la ardhi, akieleza kuwa ekari hizo ziliuzwa na Wajibu Maombi kwa utaratibu unaozua mgogoro wa kisheria.

Akizungumza mara baada ya kusikilizwa kwa shauri hilo, mmoja wa Wajibu Maombi, Ndg. Lolo Nanacha, alisema uwepo wa mkalimani umeimarisha imani yake katika mfumo wa utoaji haki.

“Leo nimejisikia huru kueleza ukweli wangu. Nimeeleweka vizuri, na ninaamini haki itatendeka,” alisema.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Baraza hilo, Mhe. Omary Mbega, alisisitiza kuwa huduma ya ukalimani ni sehemu muhimu ya kuhakikisha kila mwananchi anapata haki sawa bila kujali tofauti ya lugha au asili yake.

Shauri hilo limeahirishwa hadi tarehe 15 Aprili 2026, ambapo mashahidi zaidi watasikilizwa kabla ya kutolewa uamuzi wa mwisho.