SAME. 

MAKAMU wa Rais na Waziri Mkuu mstaafu, John Samuel Malecela amesema kuwa, swala la Utalii kokote Duniani linaenda sambamba na swala la Amani na Utulivu na kuwaomba wananchi kuhakikisha wanalinda Amani ili kukuza Utalii nchi na kuendelea kujinufaisha kupitia sekta hiyo. 

Malecela alitoa kauli hiyo jana wakati wa Uzinduzi wa tamasha la Same Utalii festival lililofanyika katika viwanja vya stendi wilayani Same mkoani Kilimanjaro ambapo alisema kuwa, utalii ni kite ambacho huchangia kuleta fedha za kigeni. 

Alisema kuwa, baadhi ya nchi ulimwenguni serikali zinaendeshwa kwa fedha za Utalii na kuwataka kulichukulia swala hilo kwa umakini mkubwa. 

Kiongozi huyo alidai kuwa, misingi ya Utalii ni ukarimu kwa wageni na kuwataka wananchi wa wilaya ya Same kuwa mfano katika ukarimu ili kukuza Utalii wa wilaya ya Same. 

"Hata sehemu kukiwa na njiwa 10,000  wamejaa lakini jiwe likigonga tu wote wanakimbia kwa hiyo na sisi utalii wetu uanze na sisi wenyewe Watanzania kuwa na Amani ni jambo la msingi sana kwani Amani ndio italeta na kuwakaribisha watalii na ndio itatufanya tuendelee kukua kiuchumi" Alisema Malecela. 

Na kuongeza "Swala la ukarimu kwa wageni ni kitu muhimu sana mahali pengine watu hawaendi kwa sababu hakuna moyo wa kuwapokea wageni lakini kwetu same tuwe na moyo wa kuwapokea wageni ili kukuza utalii wetu".

Alisema kuwa, kinachotuunga pamoja ni Amani na kuwasihi Watanzania kuendelea kuitunga na mambo mengine yatafuata. 

"Ili Utalii wa same uweze kukua ni lazima uanze na sisi wenyewe wanasama kuwa na moyo dhabiti wa ukarimu ili wanapokuja na kurudi wakatoe sifa ni kweli wataenda kuona wanyama lakini mkiwakaribisha kwa moyo upande hawatarudi tena" Alisema Malecela.






 


Na OWM - TAMISEMI, Dodoma


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu -TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amesema kuwa, zoezi la kubadilisha tahasusi na kozi za vyuo vya kati kwa wanafunzi waliohitimu kidato cha nne mwaka 2025 limeanza rasmi leo Aprili 11, 2026 na litahitimishwa  Mei 10, 2026. 

Prof. Shemdoe amesema hayo leo Aprili 11, 2026 jijini Dodoma, wakati akitoa taarifa kwa umma kuhusu wahitimu wa kidato cha nne mwaka 2025 kufanya mabadiliko ya Tahasusi za kidato cha tano na kozi za vyuo vya kati kwa njia ya mtandao kwenye mfumo wa kielektroniki wa uchaguzi wa wanafunzi wa kidato cha tano na Vyuo mwaka 2026.

“Ninawahimiza wanafunzi, wazazi na walezi kushauriana kikamilifu ikiwa ni pamoja na kupata ushauri wa kitaalam na kitaaluma kabla ya kufanya mabadiliko ya tahasusi au kozi,” amesisitiza Prof. Shemdoe.

Sanjari na hilo, Prof. Shemdoe amewataka wahitimu kufanya marekebisho ya machaguo ya tahasusi na kozi kulingana na ufaulu wao, kwa kuingia kwenye Mfumo wa Uchaguzi wa Wanafunzi (Student Selection MIS) unaopatikana kupitia kiunganishi cha selform.tamisemi.go.tz. 

Aidha, Prof. Shemdoe amewataka wahitimu kuzingatia muda uliotolewa wa kufanya marekebisho ili ratiba ya kuwachagua na kuwapangia shule na vyuo iweze kuendelea kwa muda uliopangwa, kwani mara baada ya kutangazwa kwa matokeo ya kujiunga na Kidato cha Tano na Vyuo hakutakuwa na fursa ya kufanya mabadiliko tahasusi na kozi.

Prof. Shemdoe amefafanua kuwa, huduma ya kubadilisha tahasusi ni bure na endapo wanafunzi watapata changamoto, wawasiliane na dawati la huduma la kwa mteja kupitia barua pepe: huduma@tamisemi.go.tz au kuwasiliana moja kwa moja na kituo cha huduma kwa wateja kwa simu +255 262 160 210 na +255 735 160 210 na kuongeza kuwa, mwanafunzi, mzazi au mlezi atakayekuwa na suala linalohitaji maelezo au ufafanuzi zaidi aende katika Ofisi za Elimu za Mikoa na Halmashauri.





Na Oscar Assenga, Tanga

Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Tanga kimeeleza kuwa suluhisho la kudumu la kuboresha eneo la kuchezea katika Uwanja wa CCM Mkwakwani ni uwekaji wa nyasi bandia, huku wakipanga kushirikiana na wadau wa soka kufanikisha mpango huo.

Akizungumza wakati wa ziara ya kukagua uwanja huo, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Tanga, Rajab Abdurahman, alisema uwekaji wa nyasi bandia unakadiriwa kugharimu kati ya shilingi milioni 400 hadi 500.

Ziara hiyo ni sehemu ya ukaguzi wa miradi mbalimbali ya maendeleo mkoani humo, ikiwemo ile inayotekelezwa kwa fedha zinazotolewa na Serikali chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa lengo la kupunguza kero kwa wananchi.

Abdurahman aliwataka viongozi wa CCM, ambao ni wamiliki wa uwanja huo, kutumia ubunifu na kushirikiana na wadau wa soka ili kuhakikisha wanapata fedha za kuweka nyasi bandia.

“Tutawaomba wadau wa soka nchini watakapohitajika kutusaidia, kwani dhamira yetu ni njema. Kama ambavyo wamekuwa wakitusaidia hapo awali, tunaamini watashiriki nasi kuhakikisha tunakuwa na uwanja wa kisasa zaidi,” alisema.

Alieleza kuwa maboresho ya uwanja huo yatasaidia kuinua uchumi wa Mkoa wa Tanga, kwani utaweza kutumika kwa mashindano ya kitaifa na kimataifa, ikiwemo CECAFA na michuano mingine ya Afrika.

“Tunapokuwa na uwanja mzuri, hata timu za nje zitakuja kucheza hapa Tanga. Hii itaongeza mzunguko wa fedha na kukuza uchumi wa mkoa wetu,” aliongeza.

Aidha, alikumbusha kuwa uwanja huo uliwahi kufungiwa kutokana na kutokidhi vigezo, hasa ubora wa eneo la kuchezea, akisisitiza kuwa hatua zinazochukuliwa sasa zinalenga kuhakikisha viwango vinazingatiwa kwa usalama wa wachezaji na ubora wa mchezo.

“Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) linapofungia uwanja si kwa kupenda, bali kuhakikisha viwango vinazingatiwa. Ndiyo maana tumekuwa wepesi kuchukua hatua za maboresho,” alisema.

Katika hatua nyingine, Abdurahman alieleza kuridhishwa na maendeleo ya ufungaji wa viti 6,500 vilivyotolewa na TFF chini ya Rais wake, Wallace Karia, licha ya kuwepo kwa ucheleweshaji mwanzoni.

Amesema tayari ameagiza kazi hiyo ikamilike ndani ya mwezi mmoja, na kwa sasa inaendelea vizuri chini ya usimamizi wa Mjumbe wa Kamati ya Siasa ya Mkoa, Nasoro Makau.

Kwa mujibu wa mpango huo, maeneo ya kipaumbele ni jukwaa kuu pamoja na sehemu za mashabiki wa klabu za Coastal Union na African Sports. Pia wameomba viti vingine 2,500 ili kukamilisha uwanja mzima.

Abdurahman aliishukuru Serikali kupitia Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, inayoongozwa na Waziri Paul Makonda na Naibu wake Hamisi Mwinjuma, pamoja na Rais wa TFF Wallace Karia, kwa ushirikiano wao katika kuboresha uwanja huo.

Alisisitiza kuwa maboresho hayo yanalenga kuhakikisha klabu za Coastal Union na African Sports zinaendelea kucheza mechi zao za nyumbani mkoani Tanga badala ya kuhamishiwa maeneo mengine.

Aidha, aliwataka mashabiki wa soka kujitokeza kwa wingi uwanjani kuunga mkono timu zao.

“Haileti maana kuwa na uwanja mzuri halafu mashabiki wanabaki nyumbani kuangalia mechi,” alisisitiza.

Kwa upande wake, Meneja wa Uwanja wa Mkwakwani, Nasoro Makau, alisema hadi sasa wamefikia asilimia 40 ya ufungaji wa viti na wana uhakika wa kukamilisha kazi hiyo ndani ya mwezi mmoja.

 

TAMASHA la Utalii la Same festival linalofanyika kila mwaka wilayani Same mkoani Kilimanjaro limetajwa kuwa chanzo cha kuchochea idadi ya wageni wanaotembelea hifadhi ya Taifa ya Mkomazi.

Hayo yamebainishwa na Kaimu Mhifadhi wa hifadhi hiyo, Kamishna Emmanuel Sisiya katika uzinduzi wa tamasha hilo uliofanyika wilayani Same, ambapo alisema kuwa hapo nyuma wageni waliokuwa wakitembelea hifadhi hiyo walikuwa wachache.

Alisema kuwa, tamasha hilo limekuwa chachu na hamasa kubwa ya kutangaza hifadhi ya Taifa ya Mkomazi ambapo kabla ya kuanzishwa tamasha hilo idadi ya wageni waliokuwa wakitembelea hifadhi walikuwa wachache lakini kwa sasa wameongezeka ambapo kwa mwaka wa fedha uliopita walipokea wageni 7700 na katika wageni hao 4000 ni Watanzania.

"Wageni wengi wamechangiwa na hamasa kubwa inayofanywa kupitia tamasha hili la Same Utalii festival na kila anayekuja anakiri kuwa yeye ameifahamu Mkomazi kupitia matamasha mbalimbali ambayo yamekuwa yakifanyika kuitangaza Mkomazi hivyo nirudishe pongezi kwa Mkuu wa wilaya Kasilda Mgeni kwa kuanzisha tamasha hili " Alisema Kumishna Sisiya.

Aliongeza kuwa, kwa sasa hifadhi hiyo ina fursa ya uwekezaji ambapo yapo maeneo kwa wageni kuja kuwekeza maeneo ya malazi na hoteli kwani wageni wengi wanaofika Same hudai eneo la malazi hayatoshi.

Alisema kuwa, ndani ya hifadhi maeneo ya malazi yaliyopo hayatoshi hivyo sasa ni fursa kwa Watanzania kuwekeza ndani ya hifadhi hiyo.

"Hifadhi ya Mkomazi katika Kanda ya Kaskazini ni ya pili ambapo ukifika utaweza kuwaona wale wanyama wakubwa watano tofauti na hapo katika Kanda ya Kaskazini utaweza kuwaona Serengeti na Ngorongoro lakini kwa urahisi na kwa ukaribu ukitaka kumwona faru mweusi utamwona ndani ya hifadhi ya Mkomazi" alisema.








Katibu Wakuu wa Ofisi ya Makamu wa Rais, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Wizara za Fedha, Afya na Maji, wamekutana jijini Dodoma mahsusi kuhusu utekelezaji wa agizo la Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba kuhakikisha huduma ya majisafi na salama inafika katika shule na vituo vya afya nchini.

Hatua hiyo inafanyika ikiwa ni maandalizi ya Mpango wa Kuboresha Huduma za Maji, Usafi wa Mazingira na Usafi wa Mtu Binafsi (Presidential WASH Compact).

Mpango unalenga kuhakikisha huduma za majisafi, usafi wa mazingira na usafi wa mtu binafsi zinapatikana kwa uhakika, usawa na ubora nchini ifikapo 2030.

WASH Compact ni mkataba unaobeba ahadi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, unaolenga kuimarisha usalama wa maji na utoaji endelevu wa huduma za maji, usafi wa mazingira na usafi wa mtu binafsi. 

Mkataba huo unaainisha matokeo yanayotarajiwa, mageuzi ya kisekta, uwekezaji unaohitajika pamoja na misingi ya uwajibikaji.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Mhandisi Mwajuma Waziri akiongoza kikao amesema lengo kuu la kikao hicho ni kujenga uelewa wa pamoja miongoni mwa sekta mtambuka zinazotekeleza WASH kabla ya kuanza rasmi kwa utekelezaji.

“Ni muhimu kwa sekta zote kushirikiana na kuwa na uelewa wa pamoja ili kuhakikisha mpango huu unatekelezwa kwa ufanisi na kuleta matokeo chanya,” Mhandisi Mwajuma amesema.

Ameongeza, licha ya Sekta ya Maji kuwa mhimili muhimu wa maendeleo, mafanikio ya mpango huo yanategemea ushirikiano madhubuti kati ya sekta zote husika.

Kikao kimewahusisha wataalamu kutoka wizara mbalimbali pamoja na wataalamu washauri wa mpango huo, ambao wamesisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano wa kisekta ili kufanikisha utekelezaji wake.

Miongoni mwa mambo yaliyojadiliwa ni pamoja na kuongeza uwekezaji katika miundombinu ya huduma ya maji, hususan maeneo ya vijijini na yenye uhitaji mkubwa, pamoja na kuimarisha matumizi ya mifumo ya kidigitali katika utoaji wa huduma.

Viongozi hao wamejadili mbinu za kuhakikisha upatikanaji endelevu wa rasilimali fedha, ikiwemo ushirikishwaji wa sekta binafsi na washirika wa maendeleo katika utekelezaji wa mpango huo.

Mpango katika utekelezaji utajikita katika nguzo kuu tatu ; kuongeza upatikanaji wa huduma za WASH katika maeneo mbalimbali kama kaya, shule na vituo vya afya, kuimarisha mifumo ya utoaji huduma pamoja na kuboresha mbinu za upatikanaji wa rasilimali fedha.

Mpango wa WASH Compact ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuharakisha maendeleo ya jamii na uchumi, ukitarajiwa kuleta mageuzi makubwa katika ustawi wa maisha ya wananchi.














Shirika la Maendeleo ya Viwanda Vidogo (SIDO) limetangaza kuwa Maonesho yake ya Tano ya Kitaifa yanatarajiwa kufanyika Oktoba 21 hadi 30, 2026 katika Uwanja wa Magufuli uliopo Manispaa ya Kahama, mkoani Shinyanga, yakilenga kuinua uchumi wa wajasiriamali wadogo nchini.

 


📌Bilioni 12.1 yatumika kusambaza umeme vitongojini

📌Dkt. Homera awasha Umeme kwenye vitongoji

📌Aipongeza REA kwa utekelezaji miradi ya nishati vitongojini

Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA), imewekeza jumla ya shilingi bilioni 12.1 katika miradi ya kupeleka umeme kwenye vitongoji katika wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma.

Hayo yamezungumzwa na Mbunge wa Jimbo la Namtumbo ambaye pia ni Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Juma Homera mara baada ya kuwasha umeme rasmi katika kitongoji cha Ujamaa na Kisutu vilivyopo wilaya ya Namtumbo mkoani humo.

Dkt. Homera amesema, uwashaji wa umeme katika vitongoji hivyo ni sehemu ya utekelezaji wa dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha upatikanaji wa umeme vijijini unawafikia wananchi wote ifikapo mwaka 2030

"Nampongeza sana Mkurugenzi Mkuu wa REA, Mha. Hassan Saidy na timu yake kwa kuwezesha vijiji vyote 66 vya jimbo langu kupata huduma ya umeme na kama mnavyoona kasi bado inaendelea ya kupeleka umeme katika vitongoji 79 vilivyobakia vya jimbo hili," Amesema Dkt. Homera.

Halikadhalika Dkt. Homera ametumia fursa hiyo kuwataka wananchi wa vitongoji hivyo kuchangamkia fursa kwa kufanya wiring ya umeme katika nyumba zao ili waweze kunufaika na huduma ya umeme ambayo imeletwa kwao kwa bei ya ruzuku ya shilingi 27,000 tu.

Kwa upande wake, Meneja wa Usimamizi wa Miradi ya Kusambaza Umeme kutoka REA, Mha. Deogratius Nagu amesema kuwa Serikali imeweka jumla ya shilingi bilioni 12.1 katika miradi ya umeme wilayani Namtumbo kupitia miradi ya Ujazilizi na upanuzi wa miundombinu ya umeme ikiwemo miradi ya Densificationi 2C, HEP 2A na HEP 2B.

Ameongeza kuwa, Serikali  kupitia REA imeendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya umeme kwa mafanikio makubwa ambapo vijiji vyote 66 vimefikiwa na huduma ya umeme wilayani Namtumbo.

"Kati ya vitongoji 424 vilivyopo, vitongoji 307 tayari vina umeme, na vitongoji 79 vipo katika hatua mbalimbali za utekelezaji na vinapatiwa umeme pindi miradi hii itakapokamilika, hali itakayofikisha upatikanaji wa umeme hadi takribani asilimia 91 ya vitongoji vyote, " Amesema Mha. Nagu.

Naye, Msimamizi wa Miradi Mkoa wa Ruvuma Mha. Hamis Mrope amesema kuwa umeme huo utachochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii kwa kuongeza fursa za biashara, kuimarisha huduma za afya na elimu pamoja na kuboresha maisha ya wananchi.

 


Na OWM - TAMISEMI, Dar es Salaam

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (OWM-TAMISEMI) Mhe. Prof. Riziki Shemdoe ameelekeza hatua za haraka zichukuliwe kuwarejesha wafanyabiashara wa Soko la Mawasiliano (Simu 2000) ili kuendelea na shughuli za biashara katika soko hilo ambalo lilipata ajali ya moto iliyoteketeza soko hilo Aprili 04, 2026.

Prof. Shemdoe ametoa maelekezo hayo Aprili 10, 2026 alipolitembelea soko hilo na kuridhishwa na utekelezaji wa Maelekezo ya Waziri Mkuu Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba aliyoyatoa Aprili 6, 2026, alipofika kukagua madhara ya tukio hilo la moto na kuelekeza soko hilo kusafishwa mara moja ili kuruhusu wafanyabiashara kuanza taratibu za kurejesha shughuli zao.

“Nimeridhishwa na utekelezaji wa maelekezo aliyotupatia Mhe. Rais na Mhe. Waziri Mkuu, hivyo naelekeza haraka iwezekanavyo wafanyabiashara warejeshwe kuendelea na shughuli zao lakini wasijenge vibanda na badala yake waweke meza pamoja na miamvuli ili kujikinga dhidi ya jua na mvua,” amesisitiza Prof. Shemdoe.

Prof. Shemdoe amemtaka Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe. Albert Chalamila kusimamia kikamilifu maelekezo aliyoyatoa, huku akimtaka Mkuu wa Wilaya ya Ubungo Mhe. Albert Msando kufanya ufuatiliaji wa kila siku ili wafanyabiashara wa soko hilo warejee haraka kuendelea na shughuli zao.

Aidha, katika hatua nyingine Prof. Shemdoe ameilekeza DART na Mkandarasi anayejenga soko jipya la Mawasiliano kuhakikisha ujenzi unakamilika kwa viwango ndani ya miezi minne badala ya sita ili wafanyabiashara hao wanaorejeshwa kwa kutumia meza wapate vibanda vya kufanyia biashara.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe. Albert Chalamila amempongeza Mkuu wa Wilaya ya Ubungo Mhe. Albert Msando kwa usimamizi mzuri wa utekelezaji wa maelekezo ya Mhe. Waziri Mkuu ambayo yanayowezesha urejeshwaji wa haraka wa wafanyabiashara hao walioathirika na ajali ya moto katika soko hilo la mawasiliano (simu 2000). 

Naye, Mkuu wa Wilaya ya Ubungo Mhe. Albert Msando amesema, ameelekeza ndani ya siku tatu kuanzia leo kufanyike zoezi la utambuzi wa wafanyabishara wote kwa majina matatu na vitambulisho ili kuepuka changamoto ya watu kuchukua vibanda na kuwapangisha wafanyabiasharana kuongeza kuwa atahakikisha wafanyabiashara watakaopata mikopo ni wale waliothirika na janga la moto na wenye sifa na stahiri ya  kupata mikopo.









 


Na Mwandishi wetu ..Arusha

Baada ya kupita miaka 42 tangu kufariki kwa aliyekuwa Waziri Mkuu wa zamani, Hayati Edward Moringe Sokoine, wananchi mkoani Arusha wameendelea kukumbuka na kuthamini mchango wake, wakisisitiza umuhimu wa uwajibikaji, mapambano dhidi ya rushwa na kilimo cha kufa na kupona.

Wakizungumza wakati wa maandalizi ya misa ya kumbukizi itakayofanyika Aprili 12 katika eneo la Monduli Juu, wananchi hao walisema Sokoine alijitofautisha kwa uongozi wa vitendo ulioweka mbele maslahi ya taifa.

Baadhi ya viongozi wa chama cha wazee wanaume Tanzania Joseph Laitatei makamu wa Rais wa chama hicho alisema Sokoine alikuwa kiongozi aliyesimamia haki bila kuyumba na hakuvumilia vitendo vya rushwa. Kwa upande wake, Cloud Gwangu alieleza kuwa kiongozi huyo alihamasisha kwa nguvu sera ya kilimo cha kufa na kupona, akilenga kujenga taifa linalojitegemea kwa uzalishaji.

Naye Abel Mollel Mwenyekiti  wa wilaya wa chama hicho alisisitiza kuwa uwajibikaji wa Sokoine unapaswa kuwa somo kwa viongozi wa sasa, huku Geoge Mwakalukwa akimtaja kama mfano wa uongozi wa uadilifu usio na hofu.

Aidha viongozi wa Chama cha Wazee Wanaume Tanzania wameipongeza familia ya Sokoine kwa kuendelea kuuenzi na kuudumisha kumbukumbu ya kiongozi huyo kila mwaka, wakieleza kuwa hatua hiyo inasaidia kizazi cha sasa na kijacho kujifunza misingi ya uongozi bora.

Katika kuenzi uzalendo wa Hayati Edward Moringe Sokoine, baadhi ya wananchi wameeleza namna walivyoguswa na uongozi wake wa kujitolea kwa taifa.

Akizungumza, Cloud Gwandu, mkazi wa Arusha, amesema Sokoine alikuwa kiongozi wa vitendo aliyethamini maslahi ya wananchi kuliko yake binafsi.

“Uzalendo wake ulikuwa wa kweli, alipambana na rushwa bila kuogopa na alihakikisha rasilimali za taifa zinawanufaisha wananchi wote. Viongozi wa sasa wanapaswa kujifunza kutoka kwake,” amesema Gwandu.

Ameongeza kuwa msisitizo wa Sokoine kwenye kilimo cha kufa na kupona ulikuwa sehemu ya uzalendo wake, kwani aliamini taifa lenye chakula cha kutosha lina uhuru wa kweli.

Kwa mujibu wa Gwandu, mfano wa Sokoine unaendelea kuwa somo muhimu kwa kizazi cha sasa katika kujenga uongozi wenye uwajibikaji na uadilifu.

Hayati Sokoine alifariki dunia Aprili 12 mwaka 1984 kufuatia ajali ya gari iliyotokea Dumila mkoani Morogoro.

Wananchi hao wameeleza kuwa licha ya kupita kwa muda mrefu, bado taifa lina kila sababu ya kuuenzi na kuutumia urithi wa Sokoine kama mwongozo wa kujenga uongozi bora, unaozingatia uwajibikaji, kupinga rushwa na kukuza kilimo kwa maendeleo endelevu.