Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhe. Wanu Hafadh Ameir, amesisitiza nafasi muhimu ya wanawake wanataaluma katika kufanikisha Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Akizungumza jijini Dar es Salaam katika hafla ya Inclusive Mwalimu Gala 2026, Naibu Waziri amesema kuwa kauli mbiu ya hafla hiyo, “The Contribution of Women Professionals to the Implementation of Tanzania Development Vision 2050”, imeakisi mchango wa wanawake katika kujenga uchumi wa maarifa, ubunifu na teknolojia.

Ameeleza kuwa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuwekeza kwa kiwango kikubwa katika sekta ya elimu. Hatua zilizotekelezwa ni pamoja na maboresho ya sera na sheria, ujenzi wa miundombinu ya kufundishia na kujifunzia, pamoja na kuimarisha matumizi ya teknolojia katika ufundishaji na ujifunzaji.

Aidha, amesisitiza kuwa mchango wa wanawake hauwezi kupuuzwa na kwamba Serikali ikiendelea kuimarisha usawa wa kijinsia, kuongeza ushiriki wa wanawake katika fani za STEM, kuzuia ukatili wa kijinsia na kuwekeza katika maendeleo ya kitaaluma ya walimu na wahadhiri kupitia mafunzo endelevu na tafiti.

Naibu Waziri ametoa wito kwa walimu, wakufunzi na wahadhiri kuendelea kuwa chachu ya mabadiliko ya Taifa kwa kuandaa kizazi chenye maadili, maarifa na ubunifu.

“Mustakabali wa Taifa upo mikononi mwa vijana na wanafunzi,” amesisitiza, akiwataka kutumia kikamilifu fursa za elimu zinazotolewa na Serikali ili kuleta suluhisho kwa changamoto za kijamii na kiuchumi." amesema Naibu Waziri

Naye Mbunge Viti Maalum Mwakilishi wa Vyuo Vikuu, Mhe. Asha Feruzi, amesema kuwa hafla ya Inclusive Mwalimu Gala 2026 ni jukwaa la kujadili mustakabali wa elimu, ubunifu na teknolojia katika kufanikisha Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Mhe. Feruzi amebainisha kuwa matokeo yanayotarajiwa kupitia ushirikiano huo ni kuimarika kwa tafiti, ubunifu na matumizi ya teknolojia za kisasa, hususan akili unde (Artificial Intelligence). Ameongeza kuwa vyuo vikuu na sekta binafsi vitaunganishwa ili kuzalisha suluhisho, bidhaa na huduma zinazochochea ukuaji wa uchumi shindani na endelevu.

 

Baraza la Michezo la Taifa (BMT) limetangaza fursa 12 zitakazotokana na Tanzania kuwa mwenyeji mwenza wa Mashindano ya Mataifa ya Afrika AFCON 2027 ambazo zitafungua zaidi milango ya maendeleo ya uchumi, ajira, biashara, utalii na uwekezaji nchini.

Akizungumza kuhusu fursa hizo, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Uhusiano kwa Umma wa BMT, Bw. Aminiel Aligaesha, amesema AFCON 2027 ni tukio la kihistoria litakalofanyika kwa mara ya kwanza Ukanda wa Afrika Mashariki na likiwa linatimiza miaka 70 mwakani tangu kuanzishwa kwake.

Kwa mujibu wa Bw. Aligaesha, fursa ya kwanza ni kuongezeka kwa biashara na shughuli za kiuchumi, ambapo hoteli, nyumba za kulala wageni, migahawa, maduka pamoja na wauzaji wa bidhaa zenye nembo za mashindano watanufaika kutokana na ongezeko la wageni na mashabiki.

Aidha, amesema sekta ya benki na huduma za kifedha itanufaika kupitia ongezeko la miamala ya kifedha, huduma za kubadilisha fedha za kigeni, udhamini wa matukio na utoaji wa bidhaa maalum za kifedha kwa wafanyabiashara watakaohudumia wageni.

Katika upande wa ajira, Bw. Aligaesha amesema vijana watapata nafasi za kazi katika sekta za ukarimu, usafiri, utalii, teknolojia, uandishi wa habari, uzalishaji wa maudhui na huduma nyingine, hali itakayowaongezea uzoefu wa kufanya kazi katika mazingira ya kimataifa.

Pia ametaja sekta ya usafiri kuwa miongoni mwa zitakazonufaika kutokana na kuongezeka kwa mahitaji ya usafiri wa anga, nchi kavu na majini, ikiwemo safari za ndani, huduma za teksi, mabasi, usafiri wa mtandaoni na vifurushi maalum vya safari za AFCON vinavyoweza kujumuisha utalii na malazi.

Kwa mujibu wa Bw. Aligaesha, AFCON 2027 pia itachochea maendeleo ya soka nchini kwa kuhamasisha uwekezaji katika akademi za vijana, ukocha, urefa na ukuzaji wa vipaji, huku sekta ya afya ikitarajiwa kunufaika kupitia utoaji wa huduma kwa wageni na kukuza utalii wa afya kutokana na uwekezaji mkubwa uliofanywa na Serikali.

Amesema mashindano hayo yatatoa jukwaa la kutangaza utamaduni wa Tanzania kupitia muziki, vyakula, sanaa, mavazi na lugha ya Kiswahili, sambamba na kuitangaza Tanzania (national branding) kwa mamilioni ya watazamaji duniani kupitia televisheni, mitandao ya kijamii na vyombo vya habari vya kimataifa.

Kuhusu sekta ya utalii, Bw. Aligaesha alisema wageni watakaokuja kushuhudia mashindano hayo watapata nafasi ya kutembelea vivutio mbalimbali ikiwemo Serengeti, Ngorongoro, Mlima Kilimanjaro na Zanzibar, jambo litakaloongeza mapato ya sekta hiyo.

Ameongeza kuwa maandalizi ya AFCON tayari yamechochea maboresho makubwa ya miundombinu ikiwamo ukarabati wa Uwanja wa Benjamin Mkapa, ujenzi wa viwanja vipya Arusha na kule Zanzibar, pamoja na uboreshaji wa barabara, viwanja vya mazoezi na mifumo ya huduma za kidijitali ambayo itaendelea kutumika hata baada ya mashindano hayo kumalizika.

Kwa mujibu wa Bw. Aligaesha, mafanikio ya maandalizi na uendeshaji wa AFCON 2027 yataifanya Tanzania kuwa kitovu cha michezo barani Afrika, huku yakifungua milango ya kuandaa mashindano mengine ya kimataifa, kuvutia wawekezaji na kukuza uchumi wa michezo.

Aidha, amesema mashindano hayo yataimarisha diplomasia ya michezo na ushirikiano wa Afrika Mashariki pamoja na kuimarisha uhusiano wa kikanda katika biashara, utalii, utamaduni na uwekezaji.

Akihitimisha, Bw. Aligaesha amewataka Watanzania kuendelea kufuatilia taarifa za BMT, akieleza kuwa utaratibu rasmi wa namna wananchi na wadau watakavyoweza kushiriki na kunufaika kupitia fursa hizo utatangazwa baadaye mwaka huu.

"Tunatoa wito kwa wananchi, wafanyabiashara na wadau wote kuanza kujiandaa mapema. AFCON 2027 ni mwanzo wa ukurasa mpya wa maendeleo ya michezo na uchumi wa michezo nchini, na muda si mrefu tutatangaza utaratibu wa namna fursa hizi zitakavyopatikana," amesisitiza Bw. Aligaesha

 

MC Mzungu Mweusi na Neema Naftari


Mwandishi wa habari na mshereheshaji maarufu nchini, Amos John, maarufu kama MC Mzungu Mweusi, ameanza rasmi maisha mapya ya ndoa baada ya kufunga ndoa takatifu na mpenzi wake, Neema Naftari, katika Kanisa Katoliki Parokia ya Buhangija, Manispaa ya Shinyanga.

Ibada ya ndoa iliyofanyika Jumamosi, Agosti 1, 2026, ilihudhuriwa na ndugu, jamaa, marafiki, viongozi wa dini, Washereheshaji, waandishi wa habari pamoja na wadau mbalimbali waliofika kushuhudia tukio hilo muhimu na kuwaombea wanandoa hao baraka katika maisha yao mapya.

Baada ya ibada hiyo, sherehe ya awali ilifanyika nyumbani kwa bwana harusi katika eneo la Kizumbi, Manispaa ya Shinyanga, kabla ya wageni kuelekea kwenye hafla ya mapokezi iliyofanyika katika Ukumbi wa Makindo Hotel, ambapo kulikuwa na burudani, pongezi na shamrashamra zilizoakisi furaha ya siku hiyo ya kipekee.

MC Mzungu Mweusi amejizolea heshima kubwa kupitia taaluma yake ya uandishi wa habari na umahiri wake wa kusherehesha matukio mbalimbali ya kitaifa na kijamii. 

Umahiri wake wa kuwasiliana na watu, uchangamfu na weledi wake vimemfanya kuwa miongoni mwa washereheshaji wanaoheshimika na kupendwa na wengi, hususan katika Kanda ya Ziwa na maeneo mengine nchini.

Mbali na taaluma yake, Amos John amekuwa akishiriki kikamilifu katika shughuli za kijamii na maendeleo, jambo lililomjengea taswira ya kiongozi mwenye moyo wa kujitolea na kuigusa jamii kupitia kazi zake.

Siku hiyo imebaki kuwa kumbukumbu muhimu kwa familia, marafiki na wadau wake, waliotumia nafasi hiyo kuwapongeza wanandoa hao na kuwatakia maisha marefu ya ndoa yenye upendo, amani, umoja na mafanikio.

Hongera Amos John (MC Mzungu Mweusi) na Neema Nasari kwa hatua hii muhimu ya maisha. Mungu awabariki na kuwaongoza katika safari yenu mpya ya ndoa.