Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi, Hassan Saidy amewataka Watumishi wa Wakala kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi ili kuhakikisha ndani ya muda uliopangwa wanafikisha umeme kwenye vitongoji vyote vya Tanzania Bara.
Ametoa maelekezo hayo Machi 30, 2026 Makao Makuu ya REA, Jijini Dodoma wakati wa kikao kazi na Watumishi wote, ambapo amesema baada ya kusaini Mradi mkubwa wa HEP II (B); Mradi wa kusambaza umeme kwenye vitongoji 9,009 tarehe 17 Januari, 2026 na kuongeza kuwa kazi iliyombele ya kila Mtumishi ni kuhakikisha vitongoji hivyo vinafikishiwa umeme katika kipindi cha miaka mitatu yaani hadi 2029.
Awali ilielezwa kuwa Mradi huo wa HEP II (B) ni muendelezo wa jitihada za Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) za kuhakikisha upatikanaji wa huduma ya umeme kwa Wananchi wote wa Tanzania Bara.
Mhandisi Saidy amesema kukamilika kwa Mradi huo wa HEP II (B) pamoja na miradi mingine inayoendelea kutafanya jumla ya vitongoji ambavyo tayari vitakuwa vimefikishiwa umeme kuwa takriban 51,000 kufanya vitongoji vitakavyobakia bila umeme na bila kuwa katika mradi wowote kuwa taklibani 13,000 ambavyo vimepangwa kuanza kusambaziwa umeme ifikapo mwaka 2030 kama ilivyoelekezwa katika Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya Mwaka 2025 – 2030.
Mradi huo unatarajiwa kutoa manufaa ya moja kwa moja kwa Wananchi kwa kuongeza upatikanaji wa huduma ya umeme vitongojini; kuboresha huduma za kijamii hususan katika sekta za afya, elimu na maji; kuwezesha matumizi ya umeme katika shughuli za uzalishaji na kuongeza kipato cha Wananchi pamoja na kuchochea ukuaji wa uchumi wa maeneo ya vitogojini pamoja na kuimarisha ustawi wa jamii.
Aidha; Mhandisi, Saidy aliongoza Watumishi wa REA katika zoezi la kuchagua Viongozi wa TUGHE tawini hapo ambapo kwa kauli moja Watumishi waliwachagua Viongozi wao katika ngazi tofauti kama ifuatavyo: – Mwenyekiti wa Tawi ni Bwana Swalehe Kiloza, Katibu wa Tawi ni Mhandisi, Annet Malingumu; Mjumbe wa Halmashauri ya Tawi ni Bwana Issa Sabuni na Mwakilishi wa Kundi la Vijana, Mhandisi, Issac Sanga.
Viongozi wengine ni pamoja na Wajumbe wa Kamati ya Wanawake ya Tawi la TUGHE REA ni kama ifuatavyo: – Mwenyekiti ni Bi. Wilhelmina Cheyo; Katibu ni Bi. Ruth Emmanuel; Mweka Hazina ni Bi. Aveline Wilfred; Wajumbe Kamati ya Wanawake ni Bi. Happiness Ndunguru na Mhandisi, Bertha Mwaituka.
Vilevile Watumishi wa REA pia walichagua Viongozi kwa upande wa Klabu ya Michezo ya REA ambapo itaongozwa na Bwana Selemani Mtunzy kama Mwenyekiti na Mwenyekiti Msaidizi ni Bwana Samwel Sumwa; Katibu ni Bwana Praygod Ng’hunda; Mweka Hazina ni Bwana Daniel Kisaka wakati Wajumbe wa Kamati Tendaji kwa upande wa Wanaume atakuwa Mhandisi, Thomas Mmbaga na kwa upande wa Wanawake atakuwa Bi. Beatrice Shelukindo.
Wakati huo huo Watumishi wa REA walishiriki kwenye zoezi la kuchagua Viongozi wa Chama cha Kijamii cha Wafanyakazi (REA Social Club) chenye lengo la kusaidiana wakati wa raha na changamoto mbalimbali. Viongozi wa Chama hicho waliochaguliwa ni kama ifuatavyo: Mwenyekiti ni Bwana Elias Gunzer; Katibu ni Bi. Theresia Mang’ung’ula; Mweka Hazina ni Bwana Shukuru Malebeto; Wajumbe wa Kamati Tendaji ni Bwana Pastory Mwijage na Bi. Emmy Chali.
Na Carlos Claudio, Dodoma.
Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali imegawa vifaa vya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) vyenye thamani ya jumla ya Shilingi milioni 769 kwa shule za msingi na sekondari 19 zilizopo katika mikoa tisa nchini, ikiwemo Kusini Unguja (Zanzibar), Dodoma, Iringa, Ruvuma, Arusha, Geita, Kilimanjaro, Mbeya na Mtwara.
Akizungumza katika hafla ya ugawaji wa vifaa hivyo iliyofanyika jijini Dodoma, Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Wanu Hafidh Ameir, alisema hatua hiyo ni sehemu ya juhudi za Serikali za kuendelea kuimarisha sekta ya elimu kwa kuzingatia matumizi ya teknolojia za kisasa.
Alisema matumizi ya vifaa hivyo yataongeza uelewa kwa wanafunzi kwa kuwapa fursa ya kujifunza kwa vitendo na kuona, hasa katika masomo ya sayansi na teknolojia. Aidha, alieleza kuwa walimu watanufaika kwa kutumia mbinu bunifu za ufundishaji, kuandaa maudhui kwa ufanisi na kufuatilia maendeleo ya wanafunzi kwa urahisi kupitia mifumo ya kidijitali.
“Serikali inaendelea kutekeleza mageuzi makubwa katika sekta ya elimu kama yalivyoainishwa katika Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014 (Toleo la 2023) pamoja na mitaala iliyoboreshwa, kwa lengo la kuboresha ubora wa elimu na kuandaa rasilimali watu yenye ujuzi unaokidhi mahitaji ya sasa na ya baadaye,” alisema Ameir.
Alitaja baadhi ya hatua zinazoendelea kuchukuliwa kuwa ni pamoja na utekelezaji wa elimu ya lazima ya miaka 10, kuanzishwa kwa mkondo wa elimu ya amali unaolenga kuwapatia wanafunzi stadi za ufundi na ujasiriamali, pamoja na kuimarisha matumizi ya teknolojia za kidijitali katika ufundishaji, ujifunzaji na usimamizi wa elimu.
Aidha, aliongeza kuwa Serikali imeandaa na kuanza kutekeleza Mkakati wa Kitaifa wa Matumizi ya Teknolojia za Kidijitali katika Elimu, sambamba na miongozo mbalimbali ikiwemo mwongozo wa matumizi ya TEHAMA katika shule na vyuo vya ualimu pamoja na mwongozo wa matumizi ya Akili Unde (AI) katika elimu.
Kwa upande mwingine, alisema katika mwaka wa fedha 2025/2026, Serikali imeanzisha madarasa janja matano na kufunga mbao janja 422 katika shule za sekondari, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuboresha mazingira ya ujifunzaji nchini.
Naye Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Caroline Nombo, alisema Serikali inaendelea kuchukua hatua madhubuti za kuboresha elimu kwa kuzingatia mahitaji ya karne ya 21, hususan kwa kuimarisha matumizi ya teknolojia za kidijitali.
Alisema ugawaji wa vifaa hivyo ni sehemu ya utekelezaji wa sera ya elimu pamoja na mkakati wa TEHAMA katika sekta hiyo, na ni ushahidi wa dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha walimu na wanafunzi wanapata nyenzo bora za kufundishia na kujifunzia.
Profesa Nombo alisisitiza kuwa vifaa hivyo vitachangia kwa kiasi kikubwa kuboresha ubora wa elimu, kuongeza ufanisi wa ufundishaji na ujifunzaji, pamoja na kuwawezesha wanafunzi kupata ujuzi wa kidijitali unaohitajika katika dunia ya sasa.
Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais na Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) imeweka mikakati madhubuti ya kuimarisha mfumo wa usimamizi wa taka kwa kuandaa Mkakati wa Taifa wa usimamizi wa Taka (2025 - 2030) ambao unalenga kupunguza uzalishaji wa taka kwa kutumia dhana ya uchumi rejeshi.
Katika kuhakikisha mnyororo wa usimamizi wa taka unaimarika, Serikali inahamasisha wadau hususan sekta binafsi kuwekeza katika matumizi ya teknolojia za kisasa za kuchakata taka, uwekezaji katika viwanda vya urejelezaji na kuimarisha mifumo ya ukusanyaji wa taka ili kufikia malengo ya kupunguza au kuondoa taka katika Mazingira kwa kuigeuza kuwa malighafi ya uzalishaji wa bidhaa anuwai zinazofaa kwa matumizi mbalimbali.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni ameyasema hayo katika maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Taka Sifuri, Viwanja vya Mnazi Mmoja, jijini Dar es Salaam, Machi 30, 2026.
Amesema Siku ya Kimataifa ya Taka Sifuri huadhimishwa kila mwaka Machi 30 kwa lengo la kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa kupunguza matumizi ya bidhaa zinazopelekea kuzalisha taka, kutumia tena bidhaa kabla ya kugeuzwa taka na kuchakata taka kwa kurejeleza ili kuepuka uchafuzi wa mazingira.
“Kauli mbiu ya kimataifa kwa mwaka huu inatoa hamasa ya "KUWEZESHA TAKA SIFURI KWENYE SEKTA YA CHAKULA" ikiwa na lengo la kuhimiza matumizi endelevu ya vyakula na kupunguza taka zitokanazo na sekta hii. Kwa upande wa Tanzania, kauli mbiu ya Kitaifa inahimiza kutambua "TAKA NI FURSA" ikisisitiza kuwa taka si uchafu bali ni malighafi yenye thamani, endapo itasimamiwa na kuchakatwa vyema.”
“Uzalishaji wa taka umekuwa changamoto kubwa kwa nchi za Ugaibuni na Africa, hususani katika miji mikubwa kama Dar es Salaam, Mwanza na Arusha na takwimu zinaonesha takribani kiasi cha tani zaidi ya millioni 7 za taka ngumu huzalishwa nchini kwa mwaka ambapo wastani wa asilimia 45 hadi 50 tu hukusanywa na kutupwa dampo.
Aidha, amesema asilimia 50 hadi 55 hubaki kwenye mazingira na kuzagaa kwenye mito na mifereji ya maji taka na mitaro ya maji ya mvua. Hata hivyo, matokeo ya Sensa ya Taifa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022 yanaonesha kuwa, asilimia 40 ya kaya zinachoma taka ngumu na asilimia 22 ya kaya zinatumia njia ya ukusanyaji sahihi wa mara kwa mara.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Dkt. Immaculate Sware amesema ni wakati sasa wa kubadili mtazamo kuwa taka si uchafu tu bali ni rasilimali yenye thamani.
Amesema mabaki ya chakula yanaweza kuzalisha mbolea na nishati, plastiki inaweza kurejelezwa na kuwa bidhaa mpya, na chuma chakavu kinaweza kurejelezwa na kuzalisha bidhaa nyingine.
“Ninatoa wito kwa kila mmoja wetu kuanzia maeneo ya makazi, biashara na viwandani kuchukua hatua madhubuti za kupunguza uzalishaji wa taka, kuchambua taka katika vyanzo vyake na kuimarisha utamaduni wa kuchakata taka.”

Katika kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia, Wakala wa Vipimo (WMA) imetoa misaada ya vifaa vya ujenzi wa jiko la kisasa katika Kituo cha kulelea watoto wenye mahitaji maalumu Cha RAHMAN ORPHANAGE CENTER kilichopo Chang'ombe jijini Dodoma.

Akizungumza baada ya kutoa misaada hiyo Meneja wa WMA Mkoa wa Dodoma Said Ibrahimu amesema suala la mazingira safi ya kupikia ni haki ya kila mmoja ndio maana wameamua kama Wakala kutoa misaada hiyo itakayowezesha upishi wa kisasa katika mazingira safi na salama ikiwemo usalama wa chakula kwani kituo hicho wamekuwa wakipika kwa kutumia kuni na mazingira ya Nje ambayo sio salama kwa afya ya watoto hao.
"tunamuunga mkono Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha nishati safi ya kupikia inakuwa katika mazingira safi na salama ndio maana leo kwa niaba ya wafanyakazi wa WMA tumekabidhi Sementi, Marumaru na vifaa vingine vitakavyosaidia ujenzi wa jiko hilo, "amesema Meneja Said

Kadhalika, Mkurugenzi wa kituo hicho Bi. Rukia Abdallah ameishukuru WMA kwa misaada hiyo itakayokwenda kuboresha mazingira ya mapishi katika Kituo hicho chenye idadi ya watoto 120 huku akiomba wadau wengine kujitokeza kuchangia kituo hicho ikiwemo suala la usafiri ili watoto hao waweze kutembelea maeneo mbalimbali kwa ajili ya kujifunza zaidi.
Mmoja wa watoto wanaolelewa katika Kituo hicho Hazra Ramadhan ameipongeza Wakala wa Vipimo kwa kuona umuhimu wa kuwasaidia na kuwaomba kuendelea kuwakumbuka kila mara ili waweze kutimiza malengo yao.








Na Joseph Mahumi, WF
Kampuni ya tathmini ya nchi kukopa na kulipa mikopo ya Fitch Ratings, imeithibitisha Tanzania kuendelea kuwa ‘B+’ huku likidumisha mtazamo wa “Stable Outlook”. Hatua hiyo inaashiria imani ya Kampuni hiyo katika mwenendo wa uchumi wa nchi pamoja na uthabiti wake wa kifedha katika kipindi cha kati.
Kwa mujibu wa tathmini hiyo, Tanzania inaendelea kunufaika na ukuaji mzuri wa pato la taifa (GDP) , kiwango cha chini cha mfumuko wa bei, deni kuendelea kuwa himilivu ikilinganishwa na nchi nyingine zinazofanana.
Mwenendo mzuri wa uchumi umepelekea upatikanaji wa fedha za nje kupitia programu za Shirika la Fedha la Kimataifa - IMF ikiwemo Extended Credit Facility (ECF) inayohusisha upatikanaji wa mkopo nafuu kwa ajili ya kuimarisha uchumi wa nchi kupitia sekta za uzalishaji na huduma za jamii na Resilience Sustainability Facility (RSF) ya kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.
Ripoti hiyo pia imeeleza kuwa ushindi wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika uchaguzi wa Oktoba 2025 unatarajiwa kuendeleza sera za kiuchumi, jambo litakalosaidia utekelezaji wa mipango ya mageuzi ya uchumi na kuendelea kuweka mazingira wezeshi kwa wawekezaji.
Kwa upande wa ukuaji wa uchumi, Fitch inatarajia Tanzania kuendelea kuwa na kasi ya ukuaji wa asilimia 6 mwaka 2026 na 2027, juu ya wastani wa nchi zilizo katika kundi la ‘B’ ambapo Ukuaji huo utachangiwa na sekta za kilimo na madini pamoja na uwekezaji mkubwa katika miundombinu, ikiwemo mradi wa reli ya kisasa ya Standard Gauge Railway na bomba la mafuta ghafi la Afrika Mashariki (EACOP).
Kwa upande wa sera za fedha za umma, Fitch inakadiria nakisi ya bajeti kubaki karibu asilimia 3 ya Pato la Taifa katika miaka ya fedha 2026 na 2027, huku ukusanyaji wa mapato ukiendelea kuimarika kutoka asilimia 14.2 ya Pato la Taifa mwaka wa fedha 2021 hadi asilimia 15.9 mwaka wa fedha 2025.
Ripoti hiyo inaonesha kuwa Mapato ya utalii (travel exports) yalifikia dola za Marekani bilioni 4.4 mwaka 2025, sawa na asilimia 25 ya mauzo yote ya bidhaa na huduma nje ya nchi.
Hata hivyo, hali hii itafidiwa kwa kiasi na kuongezeka kwa thamani ya mauzo ya dhahabu ya Tanzania nje ya nchi, ambayo yalifikia dola za Marekani bilioni 4.7 mwaka 2025 (sawa na asilimia 27 ya jumla ya mauzo ya bidhaa na huduma nje ya nchi).
Aidha, deni la serikali linatarajiwa kushuka hadi asilimia 47 ya Pato la Taifa ifikapo mwaka 2027, likisaidiwa na ukuaji wa uchumi na nidhamu ya matumizi ya Serikali.
Tathmini hiyo pia imepongeza jitihada za Serikali katika kuboresha usimamizi wa fedha za umma, ikiwemo kupunguza madeni ya wazabuni na marejesho ya VAT katika miaka ya karibuni ambapo Kufikia Desemba 2025, kiasi kilichothibitishwa cha madeni hayo kilipungua hadi asilimia 0.2 ya Pato la Taifa (GDP), kutoka asilimia 1.2 mwishoni mwa Desemba 2022, hatua inayochangia kuongeza uwazi na ufanisi wa kifedha.
“Ninawapongeza Viongozi wa Wizara Taasisi zake zote waliofanikisha kazi ya kusimamia sekta hii ya uchumi na fedha, tunafarijika kuona matokeo haya ambayo ni muhimu kwa maendeleo ya nchi yetu kwani tutaendelea kuaminika katika masoko ya fedha na dhamana ya Kimataifa” alisema Dkt. Natu El-maamry Mwamba, Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha
Kwa ujumla, uthibitisho wa daraja la ‘B+’ na mtazamo thabiti unaashiria kuwa Tanzania inaendelea kujenga msingi imara wa uchumi, huku ikiongeza imani ya wawekezaji wa ndani na kimataifa katika uwezo wa nchi kusimamia uchumi wake na kukabiliana na mishtuko ya nje.
Mradi wa Uendelezaji Jiji la Dar es Salaam Awamu ya Pili (DMDP II) unatekeleza ujenzi wa barabara zenye urefu wa Kilomita 51.2 kwa kiwango cha lami na zege katika Kata zaidi ya nane (8) na mitaa isiyopungua 20 katika halmashauri ya Manispaa ya Temeke.
Hayo yamebainishwa na Meneja wa TARURA wilaya ya Temeke, Mhandisi Paul Mhere ambapo ameeleza kuwa wameingia mikataba ya ujenzi wa barabara kwa gharama ya shilingi Bilioni 97.176.
"TARURA wilaya ya Temeke tuna mtandao wa barabara Kilomita 648.45, tuna majimbo matatu (3) ambayo ni Temeke, Chamazi na Mbagala na kote miradi inaendelea utekelezaji wake upo zaidi ya asilimia 75 isipokuwa Mbagala na Yombo mikataba ilisainiwa mwezi wa Aprili 2025 utekelezaji wake upo asilimia 32", amesema.
Ameongeza kuwa zaidi ya Kilomita 166 za barabara wilayani humo ni lami na zege, barabara za zege zinahimili uzito wa aina yoyote na zinadumu muda mrefu huku zikipunguza matengenezo ya mara kwa mara na kuondolea gharama serikali.
"Wilaya yetu ina bandari kavu na pia tuna bandari ambayo inahudumia nchi za Afrika Mashariki na Kati, hivyo malori yanayopita katika barabara zetu ni mengi, barabara hizi za zege zitadumu kwa muda mrefu na wananchi wameanza kufurahia maboresho ya miundombinu hii", amesema.
Naye, Diwani wa Kata ya Chang'ombe Mhe. Caroline Henrich amesema wamepata barabara sita (6) ambazo ni Igombe-Yemen, Songambele, Majimaji, Basra, Diwani na Mwakalinga ambapo hapo awali kipindi cha mvua maji yalijaa kwenye makazi ya watu na kusababisha kero lakini kukamilika kwa ujenzi wa mitaro sasa maji hayatuami na kero imeondoka pia thamani ya nyumba imepanda.
"Namshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa mradi huu, awali barabara zilikuwa korofi Kata yetu ni mtambuka barabara kubwa ya VETA na ile inayoelekea Uwanja wa Taifa zikiwa zina foleni hakuna njia nyingine ya kupita zaidi ya barabara zetu, lakini sasa barabara zimejengwa imara kwa kiwango cha zege wageni wengi wanakuja kwa ajili ya biashara", amesema.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa mtaa wa Bora, Bw. Pius Kapungu ameeleza kuwa awali kulikuwa na mashimo na kipindi cha mvua maji yalikuwa yanaingia mpaka kwenye makazi ya watu lakini sasa wanashukuru mitaro iliyowekwa imesaidia hakuna maji na taa zikiwekwa kutakuwa salama mitaa itapendeza na ulinzi utaimarika.
Aidha, Bi. Saada Salim mkazi wa mtaa wa Majimaji ameipongeza serikali kwa ujenzi wa barabara na mifereji kwani kipindi cha mvua watu walishindwa kupata wateja wa kupangisha lakini sasa wanapata wateja wengi uchumi unakua, mazingira yamekuwa mazuri, maduka yamekuwa mengi na magari yanafika.
Naye, Bw. Jimmy Mwakipesile mkazi wa Chang'ombe maduka mawili amesema barabara imewarahisishia kusafirisha abiria kwa usalama tofauti na awali walikuwa wanadondoka kwenye maji na matope, pia sasa abiria wameongezeka kwa siku walikuwa wanapata shilingi 15,000 hadi 20,000 lakini sasa wanaweza kupata hadi shilingi 40,000 mpaka 50,000 kwa siku.
Naibu Waziri wa Nishati Mh. Salome Makamba amekabidhi vitendea kazi vya usafiri kwa TANESCO Mkoa wa Shinyanga kwa lengo la kuimarisha utoaji wa huduma kwa wananchi na kutatua changamoto zao kwa haraka.
Akizungumza leo tarehe 27, Machi 2026 wakati wa hafla ya kukakabidhi vitendea kazi hivyo iliyofanyika katika Manispaa ya Kahama Mkaoni Shinyaga Mhe. Salome amesema hatua hiyo ya kukabidhi vitendea kazi hivyo ni kuyaishi maono ya Mhe Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha wananchi wanapata huduma za Umeme wa uhakika.
Amesema vitendea kazi hivyo vinakwenda kuongeza ufanisi katika utendaji kazi kwa watumishi wa TANESCO Mkoa wa Shinyanga na kuwawezesha kutatua changamoto za wateja kwa wakati.
“Kupitia vyombo hivi vya usafiri vitakwenda kuleta mabadiliko makubwa katika kumfikia mteja kwa haraka na kumhudumia, niwaombe mvitumie kutatua changamoto zao kwa wakati “ amesema Salome.
Aidha Mhe. Salome ametumia nafasi hiyo kuwataka wakazi wa Manispaa ya Kahama kuchangamkia matumizi ya Nishati safi ya umeme kupikia kwani Nishati ya umeme ni nafuu salama na rafiki kwa mazingira.
“Niwaombe wakina mama wa Kahama tuchangamkie matumizi ya nishati safi ya kupikia ya umeme, TANESCO wameleta majiko hapa unapika kwa urahisi na haraka zaidi”.
Hata hivyo Mhe. Salome amesema Serikali kupitia Shirika la Umeme TANESCO inaendelea kwa kasi kuimarisha hali ya upatikanaji wa umeme katika Manispaa ya Kahama kutokana na kuendelea kukua kwa Mji huo ambapo mpaka sasa tayari zaidi ya Shilingi milioni 600 zimetengwa kwa ajili ya kujenga laini mpya ya umeme itakayo wahudumia wakazi wa Manispaa ya Kahama.
Kwa upande wake Kaimu Meneja wa TANESCO Mkoa wa Shinyanga Mhandisi Benson Mbigili amesema wamepokea vitendea kazi mbalimbali ikiwemo Magari manne (4), Bajaji moja (1) pamoja na Pikipiki nne (4).
Mha. Benson ameipongeza Serikali kupitia Shirika la Umeme Tanzania TANESCO kwa kuwezesha vitendea kazi hivyo ambavyo kwa sasa wanakwenda kuvitumia kufikisha huduma kwa wananchi kwa haraka zaidi.
Amesema kupitia Magari hayo sasa yatawasaidia kuwafikia wateja wapya katika maeneo yote hasa yale korofi ambapo kabla ya Magari hayo ilikuwa changamoto kuwafikia na kuwaahidi wananchi kuendelea kutoa huduma bora na ya uhakika kila wakati.
“Tunaishukuru Serikali kupitia Shirika la umeme Tanzania TANESCO kwa kutupa vitendea kazi hivi ambavyo kwa sasa tunakwenda kuvitumia kufikisha huduma kwa wananchi kwa haraka zaidi.
Aidha amesema TANESCO Mkoa wa Shinyanga inaendelea kwa kasi kubwa kuhamasisha matumizi ya Nishati safi ya kupikia kwa umeme ili wananchi waweze kuelewa umuhimu wa kutumia nishati hiyo kupikia.












.jpeg)










.jpg)

.jpeg)
.jpeg)


.jpeg)













