MKUU wa Wilaya ya Handeni, Salum Nyamwese,akizungumza wakati wa maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yaliyofanyika katika Halmashauri ya Mji Handeni chini ya kaulimbiu isemayo “Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana; Msingi Jumuishi kufikia Dira 2050.”

Na Mwandishi Wetu

MKUU wa Wilaya ya Handeni, Salum Nyamwese, amesema Rais Samia Suluhu Hassan amedhamiria kuwatua ndoo kichwani wanawake wa Handeni kupitia utekelezaji wa mradi wa maji wa miji 28 ambao umefikia zaidi ya asilimia 75 ya utekelezaji.

Mradi huo unaogharimu Dola za Marekani 81,142,931 unatekelezwa na mkandarasi M/s Jwil Infra Limited kutoka India na unatarajiwa kuhudumia zaidi ya wakazi 870,629 kutoka vijiji 161 vya wilaya za Handeni, Korogwe, Muheza na Pangani.

Nyamwese ametoa kauli hiyo wakati wa maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yaliyofanyika katika Halmashauri ya Mji Handeni chini ya kaulimbiu isemayo “Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana; Msingi Jumuishi kufikia Dira 2050.”

Amesema mradi huo utakuwa mkombozi kwa wanawake ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakitumia muda mwingi kutafuta maji.

“Niwahakikishie msikae kinyonge mkajiona nyie ni dhaifu. Serikali imewasikia na tatizo hili la maji litatatuliwa hivi karibuni… hata yale mnayosema kina mama wanashindwa kusuka nywele vizuri kwa sababu ya maji, watasuka na tutawaona,” amesema.

Nyamwese amesema serikali chini ya uongozi wa Rais Samia imeendelea kuweka mazingira rafiki ya kumuwezesha mwanamke kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo kupitia sera, sheria na mipango mbalimbali.

Amebainisha kuwa Rais Samia pia alitoa maelekezo ya kuboreshwa kwa utoaji wa mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na halmashauri kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu baada ya kubaini awali kulikuwa na changamoto katika utoaji wake.

“Mheshimiwa Rais alielekeza halmashauri kuweka utaratibu mzuri wa utoaji wa mikopo hii ili kuhakikisha makundi haya yanapata fursa ya kujikwamua kiuchumi,” amesema.

Ameongeza kuwa Wilaya ya Handeni imeendelea kushuhudia maendeleo ya wanawake katika shughuli za kiuchumi zikiwamo ujasiriamali, kilimo na ufugaji.

Kuhusu kupambana na ukatili wa kijinsia, Nyamwese amesema serikali inaendelea kutoa elimu kwa jamii ili kuheshimu utu wa mwanamke na kumpa mtoto wa kike nafasi sawa katika fursa mbalimbali.

“Changamoto ya ndoa za utotoni, mimba za utotoni na mila potofu zinazokwamisha maendeleo ya mwanamke, ikiwamo umiliki wa ardhi, serikali imeendelea kuzishughulikia,” amesema.

Amewataka viongozi wa Jukwaa la Uwezeshaji Wanawake Kiuchumi la Halmashauri ya Mji Handeni kuandaa mpango maalum wa kutoa elimu kwa wanawake ili kuwajengea uwezo wa kutumia fursa zilizopo.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Handeni, Maryam Ukwaju, amesema halmashauri imejipanga kuhakikisha wanawake wanashiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi ili kufikia malengo ya Dira 2050.

Amesema hadi mwisho wa Machi 2026 halmashauri inalenga kusajili angalau vikundi 50 vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu katika mfumo wa NEST ili vinufaike na miradi inayotekelezwa katika eneo hilo.

Awali akisoma risala ya wanawake wa halmashauri hiyo, Carin Umwambe, amesema ukosefu wa maji umekuwa ukisababisha wanawake kutumia muda mwingi kutafuta maji badala ya kujishughulisha na shughuli za maendeleo na kuiomba serikali kuharakisha upatikanaji wa huduma hiyo.



Na Mwandishi Wetu - Dar es Salaam


Wanawake wa Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL) wameonesha moyo wa kujitolea kwa kutoa msaada wa vifaa mbalimbali kwa watoto wenye matatizo ya moyo wanaopatiwa matibabu katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) jijini Dar es Salaam.

Msaada huo umetolewa ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani ambayo huadhimishwa kila mwaka Machi 8.

Akizungumza katika hafla ya kukabidhi msaada huo, kwa niaba ya MWENYEKITI wa Kamati ya wanawake TTCL, Afisa Uhusiano Mwandamizi, Bi. Adeline Berchimance,amesema wanawake wa shirika hilo wameguswa na changamoto zinazowakabili watoto wenye matatizo ya moyo pamoja na wazazi na walezi wao.

Amesema wameona umuhimu wa kufika katika taasisi hiyo ili kuwafariji na kuwapa matumaini watoto pamoja na familia zao katika kipindi wanachopitia cha matibabu.

“Watoto hawa ni sehemu ya jamii yetu na wana haki ya kupata upendo, faraja na msaada kutoka kwa watu wanaowazunguka. Hivyo tumeona ni muhimu kuwafikia na kuwapa msaada huu mdogo kama ishara ya upendo wetu,” amesema Bi. Adeline.

Ameeleza kuwa msaada uliotolewa umejumuisha pampas kwa watoto, maziwa kwa watoto wachanga pamoja na pedi kwa wazazi na walezi wanaokaa hospitalini kwa muda mrefu wakihudumia watoto wao.

Amesema wanawake wa TTCL wanaamini kuwa pamoja na msaada wa vifaa, uwepo wao hospitalini hapo unatoa faraja na kuongeza matumaini kwa watoto pamoja na wazazi wao.




📌Atoa maelekezo mahsusi kwa Mkandarasi na Wasimamizi wa mradi


Naibu Waziri wa Nishati, Mhe.Salome Makamba leo amekagua utekelezaji wa mradi wa kuzalisha umeme wa Malagarasi (MW 49.5) unaotekelezwa katika Wilaya ya Uvinza mkoani Kigoma ambapo ameeleza kutoridhishwa kwake na kasi ya utekelezaji.

Akiwa katika Kijiji cha Mazungwe wilayani Uvinza Mhe Salome amekagua sehemu mbalimbali za mradi ikiwemo ujenzi wa tuta na uchepushaji mto, ujenzi wa jengo la kuendeshea  mitambo na kambi za wafanyakazi ambapo hakukuta wafanyakazi wa kutosha kama ambavyo mkataba unaelekeza.

Kutokana na hilo, Naibu Waziri wa Nishati amemuagiza mkandarasi kampuni ya Dongfang ya China kuhakikisha kuwa anaongeza wafanyakazi,  vifaa vya kazi na ndani ya mwezi mmoia awe amejenga kambi ya wafanyakazi.

Aidha,  amemtaka Mkandarasi kuwasilisha ratiba mpya  ya utekelezaji wa kazi.

Vilevile, ameagiza wasimamizi wa mradi wa Malagarasi kutoka Kampuni ya Mkandarasi  Mshaurii na TANESCO kuhamia katika eneo la mradi ndani ya mwezi  mmoja ili kuweza kuusimamia mradi huo kwa ukaribu.

"Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ameiagiza Wizara ya Nishati kuzalisha megawati 8000 za umeme ifikapo 2030, hatutakubali mtu atukwamishe katika kufikia malengo haya. Mkandarasi hakikisha unakamilisha kazi ifikapo Oktoba 2027 kama mkataba unavyoelekeza." Amesisitiza Mhe.Salome

Aidha, amemtaka Mkandarasi  Mshauri kampuni ya Multiconsult Norge AS ya Norway na Norplan kutoka Tanzania kuhakikisha kuwa wanamsimamia mkandarasi ipasavyo ili mradi ukamilike kwa wakati na kwa viwango stahiki.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Uvinza, Dinah Mathamani ameeleza kuwa uongozi wa wilaya hiyo utasimamia kwa karibu maelekezo yanayotolewa na Wizara ili mkandarasi atekeleze kazi kulingana na.mkataba.

Naye, Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati (Umeme na Nishati Jadidifu), Mhandisi Edson Ngabo amesema utekelezaji wa mradi wa Malagarasi kwa saaa ulipaswa kuwa kwenye asilimia 28 ila  umefikia asilimia 23.

Amesema Wizara ya Nishati itaendelea  kumsimamia kwa karibu mkandarasi  ili amalize kazi kwa wakati.

Sehemu nyingne zinazohusisha mradi wa Malagarasi ni upelekaji umeme katika vijiji saba vyenye vitongoji 18 ambapo mradi huo umekamilika kwa asilimia 100.

Pia ujenzi wa njia ya msongo wa kV 132 kutoka eneo la mradi hadi Kidahwe ambao umekamilika kwa asilimia 100.




















 


Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, amempa siku 14 mkandarasi anayetekeleza mradi wa kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 220 kutoka Songea hadi Mahumbika kupitia Tunduru na Masasi kurejea eneo la mradi na kuendelea na kazi mara moja.

Hatua hiyo imechukuliwa kufuatia kutoridhishwa na kasi ya utekelezaji wa mradi huo unaotekelezwa na kampuni ya Kalpataru Projects International Limited, ambayo ina jukumu la kujenga vituo vya kupoza umeme katika wilaya za Tunduru, Masasi na Mahumbika.

Akitoa agizo hilo Machi 7, 2026 wilayani Tunduru mkoani Ruvuma, Ndejembi amesema mkandarasi huyo hapaswi kupewa kazi nyingine yoyote ya serikali hadi atakapokamilisha mradi huo ambao utekelezaji wake umechelewa kinyume na masharti ya mkataba.

Aidha, Waziri huyo amemuagiza Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati kumuandikia barua ya onyo mkandarasi huyo, akieleza kuwa tayari walikutana na uongozi wa kampuni hiyo jijini Dodoma na kukubaliana kuwa wangeanza kazi ndani ya siku 25 baada ya kulipwa fedha walizokuwa wanadai tangu Desemba 2025.

Hata hivyo, amesema hadi sasa mkandarasi huyo hajarejea katika eneo la mradi wala kuanza kazi.

“Huyu mkandarasi anafanya kazi kwa kusuasua sana. Walilipwa fedha mwezi Desemba na tukakubaliana ndani ya siku 25 wawe wamerudi site na kazi ianze, lakini muda wote umeisha na hakuna kinachoendelea,” amesema Ndejembi.

Kwa mujibu wa Waziri huyo, mradi huo ulipaswa kukamilika ndani ya kipindi cha miaka miwili na kukabidhiwa mwishoni mwa mwaka huu, lakini hadi sasa utekelezaji umefikia takribani asilimia 50 pekee.

Amesema mradi huo ni sehemu ya mpango wa serikali wa kuunganisha mikoa ya kanda ya kusini ambayo ni Ruvuma, Lindi na Mtwara kwenye gridi ya taifa ili kuboresha upatikanaji wa umeme wa uhakika.

“Wananchi wa Kusini wanahitaji umeme wa uhakika na serikali imeweka kipaumbele katika kutatua changamoto hiyo kwa kutoa fedha za kutekeleza mradi huu. Haiwezekani mkandarasi akachelewesha kazi hii,” amesema.

Ameongeza kuwa “Baada ya onyo tutakalompa, endapo ataendelea kusuasua tutachukua hatua zaidi.”











 


Na Oscar Assenga,TANGA

Watumishi Wanawake  Bandari ya Tanga imesheherekea maadhimisho ya siku ya wanawake Duniani kwa kutoa msaada wa Mashine ya Kuwasaidia watoto wachanga kupumua na Oyxgen Flowmeter  katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Tanga-Bombo vyenye  thamani ya zaidi ya Milioni 5.

Akizungumza wakati akikabidhi msaada huo,Afisa Rasimali Watu wa Bandari ya Tanga  Bi. Sharifa  Konshuma Nuhu  alisema wamekuwa wakitumia siku hiyo kufanya matendo ya huduma kwa jamii zinazowazunguka na mwaka huu wameamua kwenda Bombo Hospitali kwa ajili ya kutoa msaada

Alisema kwamba msaada huo ni kuchangia nguvu zao kwa juhudi za Serikali kuhakikisha wanaboresha afya za watoto na raia wa nchi na wao walichagua kutoa mashine hizo kwa  wodi ya watoto wachanga wanaozaliwa kutokana na changamoto mbalimbali na kutambua umuhimu wa watoto .


Alisema kwamba watoto ni Taifa la kesho ambalo linatakiwa lijengwe  hivyo wanahitaji watoto wenye nguvu,watu wenye nguvu ambao wataleta mchango mkubwa kuhakikisha nchi inasonga mbele.

“Tulifika hapa tukafahamu mahitaji na Mkuu wa Idara ya Watoto wanachangamoto hizo za watoto hivyo tukaona tuwashike mkono bombo kutokana na Hospitali ya Rufaa ya  Bombo ndio hospitali zote wagonjwa wanapewa rufaa kutoka wilayani kufika hapa kwa kiasi kidogo ambacho tumekifanya kitakuwa kimeongeza huduma”Alisema

Hata hivyo alisema kwamba vifaa vyenye thamani ya zaidi ya milioni 5 waliona wachangie ili kuweza kufikisha malengo na wanajisikia furaha na faraja kutokana na furaha ya mama ambao wanapata watoto salama na huzuni kwa wale wanaowazaa wenye changamoto .

Awali akizungumza baada ya kupokea msaada huo ,Kaimu Mganga Mfawidhi wa Hosptali ya Rufaa ya Mkoa wa Tanga-Bombo Dkt Abdi Msangi aliwashukuru kwa msaada huo ambao wameutoa kutokana na kufika wakati muafaka kutokana na uwepo wa upungufu mkubwa wa vifaa vya kuwahudumia watoto na watoto wachanga wenye matatizo ya upumuaji

Alisema hasa ukizingatia kumekuwa na ongezeko kubwa kwa watoto wanaozaliwa na wanaopewa rufaa kwenda kwenye hospitali hiyo kupata huduma hizo ambao wanakuwa na changamoto za kupumua kwa hiyo wanashukruu kwa msaada huo ambao utaendelea kuboresha huduma wanazotoa kwenye Hospitali hiyo.

Alisema huduma hizo zitaendelea kuboreshwa hasa katika idara ya watoto na watoto wachanga huku akiwahimiza wadau wengine waliopo Tanga na nje kuendelea kuwasapoti kwenye nyanja mbalimbali za utoaji huduma na hiyo itasaidia kuboresha huduma na kukava ile gepu.

Naye kwa upande wake Daktari Bingwa wa Watoto katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Tanga-Bombo Dkt Mohamed Salehe alisema kwamba wanawashukuru TPA Tanga kwenda na  kutembelela wodi ya watoto na kuwapelekea zawadi kati yao mashine ya Simpapu kuwawezesha hasa watoto waliozaliwa kabla ya siku zao (watoto  ) kuweza kupumua.

Alisema na  mashine ya  Suction ambayo inasidia kuvuta katika njia ya hewa ikiwa  kuna uchafu kwa mtoto na mashine nyengine ambazo ni msaada mkubwa kwenye wodi yao pamoja na hayo wameweza kutoa zawadi kwa wakina mama na watoto na wamefarijika kwa ujio wao na wameona hispitali yao imeweza kuonwa na uhitaji ni mkubwa.

Aidha alisema kwamba changamoto za hospitali hazikoesekana kutokana na hospitali ya mkoa wanapata watoto wengi wanaolazwa na kupelekea mahitaji waliokuwa nayo yanavuka uwezo hospitali walionao.

Aliongeza kwamba vifaa vimefika wakati muafaka kwa maana idadi ya watoto wanaolazwa inaongezeka kadri siku zinavyokwenda kuonekana umuhimu wa hiyo huduma kutokana nawali walipokuwa wakizaa watoto njiti walikuwa wanaona hawana uwezo  wa kuweza kuishi.

“Lakini baada ya kuona huduma zipo watu wanaona umuhimu wa kuwapeleka Hospitali watoto kupata huduma huku akieleza hizo mashine zitakuwa msaada mkubwa na tunawaomba na wadau wengine waone umuhimu wa kujitokeza kuwasaidia kuokoa maisha na kuwasaidia “Alisema