Kibaha, Pwani

CCM leo imekuwa mwenyeji wa mkutano kati ya Chama cha Kikomunisti cha China (CPC) na Vyama Sita Rafiki vya Ukombozi Kusini mwa Afrika uliofanyika katika Shule ya Uongozi ya Mwalimu Julius Nyerere (MJNLS), Kibaha.
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

WAZIRI wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga, amewahimiza wawekezaji na wafanyabiashara nchini kuhakikisha wanalinda haki na usalama wa watumiaji kwa kuzingatia kanuni bora za uzalishaji kuanzia ununuzi wa malighafi, usafirishaji hadi uchakataji wa bidhaa ili kuzalisha bidhaa zenye viwango vya juu vya ubora vinavyokidhi matakwa ya walaji.
Na Mwandishi Wetu

Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Elimu Tanzania (TET), Dkt. Aneth Komba, amezitaka taasisi za elimu ya juu nchini kuhakikisha tafiti, ubunifu pamoja na matumizi ya teknolojia vinaelekezwa katika kutoa suluhisho la changamoto halisi zinazowakabili wananchi na kuchochea maendeleo ya taifa.

 

MONACO - Benki ya CRDB imeendelea kudhihirisha dhamira yake ya kuunga mkono maendeleo ya Taifa kupitia sekta mbalimbali kwa kushiriki katika Mkutano Mkuu wa 81 wa Michezo ya Majeshi Duniani (81st CISM General Assembly) uliofanyika nchini Monaco kuanzia tarehe 1 hadi 9 Mei 2026.

Mkutano huo wa kimataifa uliwakutanisha viongozi wa kijeshi na wadau wa michezo kutoka zaidi ya nchi 130 duniani kwa lengo la kuimarisha mshikamano, diplomasia ya michezo na amani kupitia kaulimbiu ya “Friendship Through Sport.”
Benki ya CRDB, ikiwa miongoni mwa wadau wakubwa wa maendeleo nchini, imeendelea kuunga mkono jitihada za vyombo vya ulinzi na usalama pamoja na michezo ya majeshi, hatua inayoimarisha ushirikiano wake na taasisi za Serikali katika kukuza ustawi wa askari na familia zao.

Ujumbe wa Tanzania katika mkutano huo uliongozwa na Brigedia Jenerali Saidi Hamisi Saidi, akisaidiana na Luteni Kanali Penina Anthony Igwe. Kutoka CRDB, ujumbe unajumuisha Meneja wa Kitengo cha Wateja Maalum, Crispin Sichalwe pamoja na Meneja Mawasiliano na Uhusiano kwa Umma, Emmanuel Tupeligwe.
Akizungumza kwenye mkutano huo, Sichalwe alisema CRDB imeendelea kutoa huduma maalum za kifedha kwa wanajeshi ndani na nje ya nchi, ikiwemo mikopo nafuu, bima na huduma za kifedha zinazowafikia popote walipo.

“Tunatambua mchango mkubwa wa majeshi katika usalama wa Taifa, hivyo tunahakikisha wanapata huduma bora na za haraka kupitia kitengo chetu maalum,” alisema.
Kwa upande wake, Tupeligwe alisisitiza kuwa CRDB itaendelea kushirikiana kwa karibu na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) kupitia elimu ya fedha na huduma zinazowafikia wanajeshi hata wakiwa katika maeneo ya mbali au majukumu ya kimataifa.

Aidha, benki hiyo imeendelea kuimarisha ushirikiano wake wa kimkakati na JWTZ ili kuhakikisha wanajeshi wanapata huduma bora za kifedha kwa urahisi, ikiwa ni sehemu ya mchango wake katika maendeleo na usalama wa Taifa.

 




NAIBU Spika wa Bunge, Daniel Sillo, ametoa wito kwa wananchi na wadau mbalimbali kushiriki katika kuchangia huduma za matibabu ya upandikizaji Uloto kwa Watoto wenye ugonjwa wa Sicle Cell na upandikizaji figo kwa wenye uhitaji hapa nchini.

Ameyasema hayo wakati wa hafla ya chakula cha jioni tarehe 19 Mei, 2026 katika ukumbi wa Domiya jijini Dodoma, ambapo hafla hiyo imewakutanisha viongozi waandamizi wa mkoa wa Dodoma, wabunge na wadau mbalimbali kwa lengo la kujadili namna ya kuimarisha mfuko wa kusaidia matibabu ya upandikizaji uloto na figo pamoja na huduma nyingine za kibingwa.

Amesema licha ya mafanikio yaliyopatikana ya huduma hizo za upandikizaji uloto na figo kutolewa hapa nchini na hivyo kuokoa fedha nyingi ambazo zingeweza kutumika endapo wananchi wangeenda kutibiwa nje ya nchi.

Alisema kila mwananchi anapaswa kutambua kuwa kuchangia huduma hizo si jukumu la serikali na taasisi pekee, bali ni wajibu wa pamoja kwa kuwa magonjwa ya figo na sickle cell hayachagui mtu kwa nafasi yake, dini wala hali ya maisha.

“Tunaposhiriki katika michango hii si kwa ajili ya taasisi moja, bali tunaunga mkono huduma za kitaifa zinazogusa maisha ya wananchi wengi wanaohitaji matibabu hayo,” alisema Mhe. Sillo.

Alitoa wito kwa wananchi, taasisi na wadau mbalimbali kuendelea kuunga mkono juhudi hizo za BMH ili kuwezesha wagonjwa wanaohitaji huduma za upandikizaji viungo na matibabu mengine maalumu kupata huduma kwa wakati.



Ameeleza kutegemea bajeti ya serikali pekee hakuwezi kukidhi mahitaji yote yanayoongezeka ya huduma za kibingwa, hivyo ushirikishwaji wa wadau ni njia muhimu ya kuimarisha sekta ya afya na kuokoa maisha ya Watanzania wengi.





Naibu Waziri, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Ndege Qwaray (Mb), amefanya ziara ya kikazi katika Kituo cha Utafiti, Ubunifu na Uendelezaji wa Serikali Mtandao (Research, Innovation and Development Centre – RIDC) kilichopo jijini Dodoma, ambapo amekagua miradi mbalimbali ya TEHAMA inayotekelezwa na kituo hicho kwa lengo la kuboresha utoaji wa huduma Serikalini.

Katika ziara hiyo iliyofanyika mapema wiki hii, Mhe. Qwaray alipata fursa ya kutembelea na kujionea miradi ya kiteknolojia inayolenga kutoa suluhisho kwa changamoto katika sekta mbalimbali ikiwemo elimu, afya na utawala.

Aidha, miradi hiyo inahusisha matumizi ya teknolojia zinazochipukia kama vile Internet of Things (IoT) na Akili Mnemba (AI), katika kurahisisha utendaji kazi Serikalini na kuongeza ufanisi wa huduma kwa wananchi.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mhe. Qwaray ameipongeza Mamlaka ya Serikali Mtandao (e-GA) kwa juhudi zake za kuibua na kuendeleza vipaji vya vijana, kupitia tafiti na ubunifu wa mifumo mbalimbali ya TEHAMA yenye mchango mkubwa katika maendeleo ya taifa.

“Niwapongeze e-GA kwa kazi kubwa mnayoifanya ya kukuza ubunifu na tafiti za teknolojia. Dunia ya sasa inabadilika kwa kasi kubwa kutokana na maendeleo ya teknolojia, hivyo ni muhimu kuendelea kujifunza, kufanya tafiti na kubuni mifumo mipya itakayokwenda sambamba na mabadiliko hayo,” amesema Mhe. Qwaray.

Amesisitiza kuwa, bunifu zote zinazotengenezwa zinapaswa kuwa na tija kwa jamii na kuchangia moja kwa moja katika kuboresha huduma zinazotolewa kwa wananchi pamoja na kuongeza ufanisi ndani ya taasisi za Serikali.

Sambamba na hilo, Mhe. Qwaray amesisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano kati ya e-GA, vyuo vikuu na sekta binafsi ili kuongeza uwekezaji katika tafiti, ubunifu na maendeleo ya teknolojia zinazoweza kusaidia kutatua changamoto mbalimbali za kijamii na kiuchumi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa e-GA, Mhandisi Benedict Ndomba, amesema kituo hicho kimeendelea kuwa chachu ya mageuzi ya kidijitali Serikalini kupitia ujenzi wa mifumo mbalimbali inayotumika katika taasisi za umma.

Ametaja baadhi ya mifumo hiyo kuwa ni Mfumo wa Uendeshaji wa Vikao vya Bodi na Menejimenti (e-Board) pamoja na Mfumo wa Uendeshaji wa Vikao Kidijitali (e-Mikutano), ambayo imekuwa ikisaidia kuongeza ufanisi katika shughuli za Serikali.

“Kituo hiki kimekuwa na manufaa makubwa kwa taifa kutokana na kazi zake za utafiti, ubunifu na maendeleo ya mifumo ya TEHAMA. Pia, kimefungua fursa kwa wanafunzi na vijana wenye taaluma ya TEHAMA kushiriki katika tafiti na bunifu mbalimbali kwa maslahi ya taifa,” amesema Mha.Ndomba.

Katika kuonesha dhamira ya Serikali kuendelea kuimarisha kituo hicho, Mhe. Qwaray ameahidi kuwa Wizara itaendelea kushirikiana na e-GA kutatua changamoto zinazoikabili RIDC ili kuongeza fursa kwa vijana wengi zaidi wa Kitanzania kupata nafasi ya kujifunza, kufanya tafiti na kushiriki katika ubunifu wa teknolojia mbalimbali za kisasa.







 


Na OWM - TAMISEMI, Azerbaijan

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amesema Serikali inayoongozwa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imetoa kipaumbele katika maandalizi ya upanuzi wa haraka wa miji pembezoni ili kukabiliana na  changamoto zinazotokana na fursa za ukuaji wa miji na majiji nchini Tanzania.

Prof. Shemdoe ameelezea hatua hiyo ya Serikali aliposhiriki mdahalo Mei 19, 2026  nchini Azerbaijan ambao ni sehemu ya Mkutano Mkubwa wa  kidunia wa maswala ya Miji (World Urban Forum), baada ya kuulizwa ni hatua zipi zimechukuliwa na Serikali ya Tanzania katika kujiandaa kwa upanuzi wa haraka wa miji pembezoni ili kukabiliana na athari za kukua kwa miji na majiji ikiwepo changamoto kubwa ya ukosefu wa ajira.

Prof. Shemdoe amefafanua kuwa, hatua ya Serikali ya Awamu ya Sita  kufanya maandalizi ya mapema ya upanuzi  wa miji na majiji pembezoni ni muhimu kwani lango kuu la jiji la Dar es Salaam, pamoja na ya majiji ya Dodoma, Mwanza, Mbeya na Arusha yanakua kwa kasi isiyokuwa ya kawaida.

Prof. Shemdoe ameongeza kuwa, upanuzi wa miji na majiji pembezoni ukitokea bila kuwepo na mipango ya mapema unasababisha ukosefu wa ajira na makazi yasiyo rasmi ambayo hayana maji safi, umeme wa uhakika, na usafi wa mazingira unaostahili, hivyo kurekebisha miundombinu katika maeneo hayo kunaigharimu zaidi Serikali  wakati  maandalizi yangefanywa mapema  gharama za ujenzi wa miundombinu zingekuwa nafuu. 

Prof. Shemdoe ameanisha kuwa, changamoto zote tatu zilizojadiliwa katika mdahalo huo ikiwemo ya ukosefu wa ajira  katika miji, kutojiandaa mapema kwa upanuzi wa haraka wa miji pembezoni na mwenendo hafifu wa maendeleo katika miji midogo  zimeligusa  taifa  ndio maana Dira ya Taifa ya Maendeleo ya Mwaka  2050 imetoa kipaumbele katika utatuzi wa changamoto hizo.

 Na OWM - TAMISEMI, Dodoma


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amewasisitiza washiriki wa Mkutano wa Mwaka wa Tathmini ya Afua ya Uthibiti wa Taka Ngumu na Usafi wa Miji, kuhakikisha suala usafi wa mazingira linakuwa ajenda ya kudumu katika vikao vyote vitakavyofanyika katika ngazi zote za Mamlaka za Serikali za Mitaa ili kuwezesha miji na majiji nchini kuwa masafi.

Prof. Shemdoe ametoa maelekezo hayo Mei 12, 2026 jijini Dodoma wakati akifungua mkutano wa kwanza wa Mwaka wa Tathmini ya Afua ya Uthibiti wa Taka Ngumu na Usafi wa Miji, unaofanyika katika Ukumbi wa Hoteli ya Jiji- Mtumba, unaohudhuriwa na Maafisa Afya wa Mikoa, Maafisa Afya wa Halmashauri na Maafisa Mazingira wa Halmashauri.

“Nasisitiza suala la usafi wa mazingira liwe ajenda ya vikao vyenu. Vikao vya Kamati za Ushauri za Mikoa, Kamati za Ushauri za Wilaya, Kamati za Maendeleo za Kata, Mabaraza ya Madiwani, Kamati za Kudumu za Halmashauri pamoja na vya ALAT ngazi ya mkoa na taifa,” amesema Prof. Shemdoe.

Prof. Shemdoe ameainisha kuwa, usafi wa mazingira ukizingatiwa katika ngazi zote za Mamlaka ya Serikali za Mitaa utapunguza milipuko ya magonjwa na matumizi ya fedha kwa ajili ya ununuzi wa madawa, na fedha zitakazookolewa zitaelekezwa katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo, hivyo amewataka maafisa hao kufanya kazi kwa bidii na weledi ili kupunguza milipuko ya magonjwa na matumizi ya ununuzi wa dawa.

“Namshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuona umuhimu wa kuanzisha vitengo vya udhibiti wa taka ngumu ambavyo vinasaidia kuboresha zoezi la usafi wa mazingira nchini,” Prof. Shemdoe ameeleza.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu - Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa anayeshughulikia afya Prof. Tumaini Nagu amesema uthibiti wa taka kwenye halmashauri ni jambo muhimu katika kuhakikisha kunakuwa na usafi wa mazingira na udhibiti wa magonjwa ya milipuko na kuongeza kuwa, takwimu za kisayansi zinaeleza kwamba uthibiti madhubuti wa taka ngumu unapelekea kupungua kwa asilimia 30 hadi 40 za magonjwa kama Malaria na mengineyo ambayo yanadhibitiwa kwa usafi wa mazingira.

Akizungumza kwa niaba ya washiriki, Mkuu wa Kitengo cha Udhibiti taka ngumu wa Halmashauri ya wilaya Bahi Bw. William Mpangala amesema kuwa Serikali kupitia Mamlaka za Serikali za Mitaa inaendelea kushirikisha sekta binafsi katika utekelezaji wa afua za udhibiti wa taka ngumu kama za ukusanyaji na uchakataji wa taka ngumu, na kuongeza kuwa ushirikishwaji huo umeongeza ufanisi katika udhibiti wa taka kwenye halmashauri nchini.

Mkutano wa Mwaka huu una kaulimbiu isemayo “Taka ngumu ni Mali; tumia, rejeleza na Weka Miji katika hali ya usafi”.









NA NOEL RUKANUGA, DAR ES SALAAM

Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Elimu Tanzania (TET), Dkt. Aneth Komba, amefungua maonesho ya Wiki ya Utafiti na Ubunifu ya Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu Dar es Salaam (DUCE), huku akiahidi kushirikiana na chuo hicho katika kutumia matokeo ya tafiti kuimarisha ufundishaji nchini.
ARUSHA

Tume ya Madini imeendelea kuonesha mafanikio makubwa katika usimamizi wa rasilimali za umma baada ya kupata hati safi ya ukaguzi kwa Hesabu za Mwaka wa Fedha 2024/2025 sambamba na kukusanya maduhuli yaliyofikia Shilingi Trilioni 1.192, sawa na asilimia 99 ya lengo la mwaka.

 -Magereza 12 Morogoro Yanufaika na Mradi wa Nishati Safi ya Kupikia kutoka REA     

Jeshi la Magereza Mkoa wa Morogoro limeendelea kuhamasishwa matumizi ya nishati safi ya kupikia ikiwa ni sehemu ya Mkakati wa Serikali kuhakikisha Asilimia 80 ya wanatumia wahamie kutumia nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034.

Akizungumza wakati wa ziara ya kukagua miradi ya nishati safi ya kupikia kwa Jeshi la Magereza mkoani Morogoro, Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), Mhe. Balozi Meja Jenerali (Mstaafu), Jacob Kingu amesema kuwa lengo la taifa la kufikia matumizi makubwa ya nishati safi ya kupikia linawezekana kutokana na uwepo wa vyanzo mbalimbali vya nishati hiyo.

Amesema wananchi wana nafasi ya kuchagua aina ya nishati safi kulingana na mazingira wanayoishi, ikiwemo gesi, mkaa mbadala pamoja na matumizi ya umeme kwa ajili ya kupikia.

“Inawezekana ifikapo mwaka 2034 asilimia 80 ya watanzania wanatumia nishati safi za kupikia maana zipo nyingi" amesema Mwenyekiti Kingu.

Aidha, ameeleza kuwa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) unaendelea kupeleka huduma ya umeme katika Vijiji na Vitongoji jambo litakalowezesha wananchi wengi zaidi kutumia umeme kama chanzo cha nishati safi ya kupikia.

Kwa upande wake, Mkuu wa Magereza Mkoa wa Morogoro, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Magereza (SACP), Peter Anatory amesema mradi wa majiko ya nishati safi ya kupikia unaotekelezwa na Wakala wa Nishati Vijijini (REA) umewezesha magereza 12 ya Mkoa wa Morogoro kunufaika na huduma hiyo.

Amesema kupitia mradi huo, magereza hayo yamepata majiko 15 yanayotumia mkaa rafiki kwa mazingira pamoja na tani 236 za mkaa huo, hali iliyosaidia kuongeza matumizi ya nishati safi katika taasisi za magereza.

“Mradi huu umekuwa kichocheo kikubwa kwa magereza katika kuhakikisha tunatumia nishati safi ya kupikia,” amesema Anatory.

Naye Kamishna Msaidizi wa Magereza (ACP) Samuel Aron Mwakatika amesema matumizi ya nishati safi yana mchango mkubwa katika kuboresha maisha ya wananchi, kulinda mazingira pamoja na kukuza uchumi wa taifa.

Amesema katika Chuo cha Udereva KPF Kingolwira, matumizi ya nishati safi yamesaidia kuokoa muda uliokuwa unapotea kwa wanafunzi kwenda kutafuta kuni.

“Katika chuo hiki tuna wanafunzi 381, hivyo zamani ilikuwa lazima kuwe na kundi la wanafunzi wanaokwenda kutafuta kuni jambo lililokuwa linapunguza muda wa kujifunza. Nishati safi imesaidia kuondoa changamoto hiyo,” amesema Mwakatika.

Aidha, Mrakibu Mwandamizi wa Magereza (SSP), Nicostatus Magori amesema gereza hilo liliacha kutumia kuni kwa ajili ya kupikia chakula cha wafungwa tangu Desemba mwaka 2024 baada ya kuanza kutekelezwa kwa mradi huo wa kufungiwa mifumo ya nishati safi ya kupikia katika magereza. 





 

WAKALA wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) unatarajia kujenga kiwanda kipya na uwekaji mitambo ya kisasa kwa ajili ya kuchakata mazao ya nyuki ili kuwezesha kukidhi mahitaji ya soko la ndani na nje ya nchi la asali.

Kiwanda hicho kipya kitajengwa wilayani Manyoni, Mkoa wa  Singida ambako kuna kiwanda kidogo cha uchakataji kinachohudumia Kanda ya Kati inayojumisha mikoa ya Singida, Manyara na Dodoma ambacho kinatarajiwa kugharimu zaidi ya Sh milioni 200 .

Mhifadhi Mkuu Daraja la Pili wa TFS , Claudia Kinabo amesema hayo alipozungumzia mikakati ya uzalishaji wa mazao ya nyuki ikiwemo asali katika kanda hiyo na namna ilivyojioanga kwenye maadhimisho ya Siku ya Nyuki Duniani Mei 20 mwaka huu ambapo kitaifa ya kifanyika mkoani Tabora.

Kinabo ambaye ni msimamizi wa kitengo cha Ufugaji Nyuki Kanda ya Kati alisema Wakala huo umetenga bajeti kwa ajili ya kujenga kiwanda kikubwa zaidi ya ukataji wa mazao ya nyuki ambapo kwa sasa kipo kiwanda kidogo katika kituo cha Wilaya ya Manyoni.

“Ujenzi kwa maana ya upanuzi huu wa kiwanda cha Manyoni utakuwa na mchango mkubwa katika kukuza sekta ya asali na kuongeza uzalishaji katika eneo hili,” amesema Kinabo.

Kinabo amesema Kanda  yaKati unaendelea kuwa miongoni mwa maeneo yanayoongoza kwa uzalishaji wa asali chini ya TFS kwa sababu ina mazingira mazuri ya misitu yanayofaa kwa ufugaji nyuki.

Amesema kuwa Kanda hiyo una mashamba makubwa matano ya nyuki yaliyopo katika wilaya za Singida na Kondoa, maeneo yanayojulikana kwa mazingira mazuri ya ufugaji nyuki na uzalishaji wa asali bora.

Naye, Mhifadhi Nyuki Shamba la Nyuki Manyoni, Mrina Robert amesema kiwanda cha kuchakata mazao ya nyuki kimekuwa kikichakata mazao hayo kutoka wilaya mbalimbali za Kanda ya Kati pamoja na asali za wadau mbalimbali .

Mrina amesema kiwanda cha sasa licha ya kuendelea kuchakata mazao ya nyuki  kikiwa na uwezo wa kuchakata kilo 500 kwa saa nane  kwa siku.

Amesema kutokana na mahitaji makubwa na mtambo uliopo  ni mdogo pamoja na jengo, wakala katika bajeti yake umejipanga kujenga jengo kubwa la kiwanda na kuweka mitambo mikubwa nay a kisasa zaidi  ya kuchakata mazao ya nyuki kwa maana ya asali, nta na mengine.

Mrina amesema kiwanda hicho kipya kitachangia kuongeza kasi ya uchakataji wa asali  na kutoa ushawishi kwa wadau wenye mashamba ya nyuki kuleta mazao yao kuchakatwa.

Kwa upande wake, Mhifadhi Mkuu na Msaidizi wa Kamanda wa TFS Kanda ya Kati anayeshughulikia Dawati la Mipango na Masoko, Ignas Lupala alisema kwa mwaka wa fedha wa 2024/2025 lengo lilikuwa kuzalisha tani 20 za mazao ya nyuki na hadi kufikia msimu ulipomalizika zilizalishwa tani 16.5 za asali.

Lupala amesema kwa mwaka wa fedha 2025/2026 Kanda hiyo imeweka lengo la kuvuna jumla ya tani 21 za asali na  bado msimu wa uvunaji unaendelea na mikakati mbalimbali imewekwa ya uzalishaji  mazao ya nyuki kwa wingi yanafikiwa kila mwaka.

Wataalam wa Tasnia ya Maziwa nchini wameonya juu ya matumizi holela ya dawa kwa mifugo ambayo husababisha uwepo wa masalia ya dawa katika maziwa, hali inayoweza kuhatarisha afya za walaji na kuathiri ubora wa bidhaa za maziwa.
Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) linaendelea kuimarisha ushirikiano na jamii kwa kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kulinda na kuhakikisha usalama wa miundombinu ya bomba la gesi asilia katika vijiji vya Mkwalia Kitumbo na Sunguvuni, wilayani Mkuranga mkoani Pwani.

 


📌 Afungua Mkutano Mkuu wa Mwaka 2026 wa Maafisa Uhusiano na Huduma kwa Wateja TANESCO


📌 Asisitiza utoaji wa taarifa sahihi kwa wateja 


📌 Aagiza kuboreshwa kwa maslahi ya watoa huduma kuongeza ufanisi wa utendaji kazi 



Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba, amewataka Maafisa Uhusiano na Huduma kwa Wateja wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kutumia kwa ufanisi mifumo ya kidigitali na akili mnemba ili kuendana na kasi ya ukuaji wa teknolojia na kuongeza ufanisi wa huduma na mawasiliano kwa wateja.

Mhe. Makamba amesema hayo Mei 18, 2026 wakati akifungua Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Maafisa hao unaofanyika kwa siku tano katika Ukumbi wa Lavenda Hotel jijini Dodoma ukilenga kutathmini utendaji kazi, kutambua changamoto, kujadili mikakati ya kuboresha huduma kwa wateja na kuimarisha mawasiliano ya kimkakati ndani ya Shirika kwa mwaka ujao wa fedha.

“ Sote tunatambua, teknolojia ndiyo msingi wa utoaji huduma wa kisasa hivyo ni wajibu wenu Maafisa Huduma kwa Wateja kuhakikisha mifumo ya kidigitali ikiwemo akili mnemba inatumika kwa ufanisi ili wananchi wapate huduma bora na taarifa sahihi kwa wakati.” amesisita , Mhe. Salome Makamba

Katika hotuba yake, amesema Serikali inatambua jitihada za dhati zinazofanywa na TANESCO katika maboresho yaliyofanyika katika huduma kwa wateja na  mawasiliano ya kimkakati kupitia matumizi ya mitandao ya kijamii, makundi ya WhatsApp pamoja na utoaji wa elimu kuhusu matumizi salama ya umeme na Nishati Safi ya kupikia.

Aidha, ameitaka Menejimenti ya TANESCO kuboresha motisha kwa watoa huduma kwa wateja ili kuongeza ari na ufanisi wao kazini kwa kuzingatia kuwa wao ni watendaji wa mstari wa mbele katika kujenga taswira ya Shirika kwa wateja .

“ Kwa niaba ya Uongozi wa Wizara, nawapongeza watoa huduma kwa kujituma kwenu. Nimuombe Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO kusimamia uboreshaji wa maslahi yao ili waweze kutoa huduma bora na yenye uhakika kwa wateja,” amesema Mhe. Makamba.

Akizungumza kuhusu maboresho ya huduma kwa wateja, amesisitiza umuhimu wa kuongeza ufanisi katika vituo vya huduma kwa wateja (Call Centers) ili kuhakikisha changamoto za wateja zinatatuliwa kwa wakati. 

“Nahimiza ushirikiano madhubuti kati ya TANESCO na wadau mbalimbali ili wateja waweze kupata taarifa sahihi kwa wakati. Aidha, kuna umuhimu mkubwa wa kuimarisha ushirikiano wa ndani kati ya Idara za TEHAMA na Huduma kwa Wateja kwa lengo la kufikia viwango bora zaidi vya utoaji huduma,” ameongeza .

Awali akizungumza kwa niaba ya Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa TANESCO, Dkt. Lucy-Mary Mboma, amesema Bodi inaendelea kuthamini mchango wa Maafisa Huduma kwa Wateja na inatarajia kuona Shirika likiendelea kuimarisha taswira yake kupitia huduma bora na mawasiliano yenye tija.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Bw. Lazaro Twange, amesema Shirika limewekeza katika mifumo rasmi itakayowezesha kuhudumia zaidi ya wateja milioni sita kwa ufanisi mkubwa mara itakapoanza kufanya kazi hivi karibuni. Amesema hatua hiyo pia itasaidia kuokoa takribani shilingi milioni 400 zilizokuwa zikitumika kwenye mifumo ya nje.

“ TANESCO itaendelea kuwekeza katika mifumo ya kisasa ya utoaji huduma ili kuongeza ufanisi, kuhudumia kwa uhakika zaidi ya wateja milioni sita na kupunguza gharama za uendeshaji wa mifumo ya nje.” amebainisha, Bw. Twange. 

Mkutano huu wa mwaka wa Maafisa Uhusiano na Huduma kwa Wateja ni muendelezo wa utamaduni wa taratibu za Shirika wenye tija katika kuboresha utendaji kazi kwa maslahi ya Shirika, wateja na nchi kwa ujumla.

 

WAZIRI wa Katiba na Sheria, Dk Juma Homera amesema watu wanaoitukana Serikali, kufanya uchochezi na  vitendo visivyo vya maadili mitandaoni, majina yao yameshakabidhiwa kwa Wizara ya Mambo ya Ndani ili Jeshi la Polisi ili wachukuliwe hatua za kisheria.

Aliyasema hayo jana wakati akifungua mkutano wa siku wa mafunzo kwa mawakili wa serikali yaliyoandaliwa na Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali jijini Arusha.

Dk. Homera alitoa kauli hiyo akijibu ombi la Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Dk. Damas Ndumbaro aliyetaka mawakili wa serikali kuisaidia Serikali dhidi mashambulizi na upotoshaji unaofanywa mitandaoni.

Dk. Homera alisema majina ya wahusika wa uhalifu huo tayari yamekabidhiwa Wizara ya Mambo ya Ndani kwa hatua za kisheria.

Alisema kuna Sheria ya Mitandao, sheria za Jeshi la Polisi na sheria ya Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) ambazo zinadhibiti upotoshaji, uchochezi na uvunjifu wa maadili, hivyo serikali itahakikisha inazisimamia ili kukomesha uhali huo nchini.

"Serikali haikatai kukosolewa, lakini ikoselewa kwa jambo la haki na kweli na si jambo la uongo, na kutumia lugha ya matusi au uchochezi, hivyo wahusika watachukuliwa hatua za kisheria ili kuimarisha amani na usalama,"alisisitiza Dk Homera.

Aliongeza"Jeshi la Polisi limeanza kuchukua hatua dhidi ya wanaoitukana serikali, kufanya uchochezi na vitendo visivyo vya maadili mitandaoni."

Kuhusu mafunzo hayo, alisema yatawasaidia mawakili wa serikali kuishauri serikali ipasavyo na kwa weledi, kuwa na uelewa mpana wa masuala mbalimbali, kujengewa uelewa kuhusu miradi ya ubia kati ya sekta ya umma na sekta binafsi (PPP) na masuala mengine mbalimbali.

Alisema Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali inafanya kazi nzuri ya kuitetea serikali katika mashauri mbalimbali na kufanikiwa kuisadia serikali kuokoa zaidi ya shilingi trilioni moja kwa kushinda kesi hizo.

Naye Wakili Mkuu wa Serikali, Dk Ally Possi alisema katika kipindi cha Julai 2025 hadi Machi 2026, kati ya mashauri 641, serikali ilishinda mashauri 595 sawa na asilimia 88.1 na kuokoa Sh bilioni 316.3 ambayo serikali ingelipa kama ingeshindwa mashauri hayo.

Kuhusu mashauri ya usuluhishi, alisema mashauri 18 yamekamilika na serikali kuokoa Sh bilioni 6.8 katika kipindi hicho.

"Kwa hiyo katika mashauri yote ya madai na usuluhishi kuanziaJulai 2025 hadi Aprili 2026, Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali tumeisadia Serikali kuokoa shilingi trilioni 1.35,"alisema Dk Possi.

Aliongeza"Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali ilianzishwa mwaka 2018, na moja ya mafanikio makubwa tuliyoyapata ni kuitetea serikali katika kesi ya kukamatwa kwa ndege yetu na kushinda."

Pia alisema mafunzo hayo kwa mawakili wa serikali yanalenga kulinda kila senti ya mlipakodi, kutetea rasilimali za serikali, kuongeza uwezo wa mawakili katika nyanja mbalimbali, kujinoa kitaaluma, na kuendesha mashauri kwa weledi na umahiri.

Naye Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Dk. Damas Ndumbaro alisema kuna haja kwa mawakili wa serikali kuja na mpango wa namna ya kuitetea serikali dhidi ya mashambulizi na upotoshaji mkubwa dhidi ya serikali.

"Nini nafasi ya mawakili wa Serikali katika jambo hili? Nashauri kupitia mafunzo haya jadilianeni nini cha kufanya ili kuihudumia nchi na jamii yetu kwa weledi,"alisema Dk. Ndumbaro

Pia alisema kwa kuwa asilimia 36 ya migogoro yote iliyoibuliwa na  timu ya Msaada wa Kisheria ya Samia imetokana na ardhi, hivyo alimuomba Wizara ya Katiba na Sheria kulifanyia utafiti jambo hilo ili kujua chanzo na kuja na suluhu ya kuikomesha migogoro hiyo.

Dk Ndumbaro aliwataka mawakili hao wa serikali kujifunza kwa vitendo kupitia mashauri mbalimbali wanayoshinda na kushindwa ili kufanya mabadiliko ya kisheria yanayohitajika kwa maslshi ya taifa na kuleta ufanisi katika sekta ya sheria.

Kwa mujibu wake, Februari 2018, Tanzania ilifanya mageuzi makubwa katika sekta ya sheria nchini kwa kupangilia upya nafasi tatu ikiwemo Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali na Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP).

Alisema mageuzi hayo yamesaidia kuleta ufanisi katika sekta ya sheria nchini.

Naye Naibu Wakili Mkuu wa Serikali, Alice Mtulo alisema mafunzo hayo yanalenga kuwajengea uwezo Mawakili wa serikali kuhusu uendedhaji wa mashauri ya madai na usuluhishi.

Alisema jumla ya washiriki 600 wanahudhuria mafunzo hayo wakiwemo mawakili kutoka Wizara ya Katiba na Sheria, taasisi za serikali na Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali

Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Samwel Maneno alisema mawakili wa serikali wanawajibu wa kuisaidia serikali kwa kutoa ushauri mzuri wa kisheria pale serikali inapoingia mikataba na sekta binafsi ambayo ni injini ya uchumi wa taifa.

Maneno alisema Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali imeshasajili mawakili zaidi ya 30 katika kitengo cha ushirikiano kati ya sekta ya umma na binafsi (PPP) katika kutekeleza miradi ya ubia.

Naye Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali Zanzibar, Shaaban Abdalla aliwataka mawakili hao wa serikali kusimamia mashauri ya madai na usuluhishi kwa weledi na uzalendo kupitia mafunzo wanayopewa.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama Tanzania, Profesa Elisante Ole Gabriel alisema kwa kuwa Mahakama ni chombo cha juu na cha mwisho katika kutoa haki, hivyo Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali ni mdau muhimu katika jambo hilo.








NAIBU Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Ngwaru Jumanne Maghembe amesisitiza umuhimu wa vijana katika kuleta maendeleo endelevu na mabadiliko chanya kupitia teknolojia, diplomasia na ubunifu katika ngazi ya taifa na kimataifa.

 


Mbunge mstaafu na mdau wa masuala ya teknolojia na maendeleo ya kidijitali, Neema Lugangira, amepata heshima ya kuteuliwa tena na Katibu Mkuu wa United Nations kuhudumu katika Kamati ya Ushauri kuhusu masuala ya utawala wa mtandao duniani pamoja na maendeleo ya kidijitali.

Kamati hiyo ya kimataifa ina jukumu la kumshauri Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kuhusu namna bora ya kuimarisha ushirikiano wa kidijitali, usalama wa mtandao, upatikanaji wa teknolojia, pamoja na kuhakikisha maendeleo ya kidijitali yanawanufaisha watu wote duniani kwa usawa.

Akizungumzia uteuzi huo, wachambuzi wa masuala ya teknolojia wameeleza kuwa nafasi hiyo ni ishara ya kuongezeka kwa ushawishi wa Watanzania katika majukwaa ya kimataifa yanayojadili mustakabali wa dunia ya kidijitali.

Neema Lugangira amekuwa mmoja wa viongozi wanaosukuma ajenda ya matumizi ya teknolojia, ubunifu wa kidijitali pamoja na ujumuishaji wa wananchi katika uchumi wa kidijitali nchini Tanzania na Afrika kwa ujumla.

Uteuzi huo pia unatajwa kuwa fursa muhimu kwa Tanzania kuendelea kushiriki katika maamuzi na mijadala ya kimataifa kuhusu sera za teknolojia, mtandao na maendeleo ya kidijitali katika dunia inayobadilika kwa kasi.