Na OWM - TAMISEMI, Dodoma
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) Mhe. Prof. Riziki Shemdoe na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Adolf Mkenda wamewapokea walimu wapatao 150 wa amali waliokwenda kwenye ziara ya mafunzo ya mwezi mmoja nchini India, ambayo yatawawezesha kutoa elimu ya ufundi na mafunzo ya stadi za kazi nchini ili kukuza uchumi wa viwanda, kupunguza ukosefu wa ajira kwa vijana, na kuwajengea uwezo wa kushindana katika soko la ajira.
Walimu hao mara baada ya kurejea nchini, walipata mwaliko wa Mhe. Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba kuhudhuria shughuli za Bunge Mei 04, 2026 jijini Dodoma na kupokelewa kwa pamoja na Waziri wa TAMISEMI Mhe. Prof Shemdoe na Waziri wa Elimu Mhe. Prof. Mkenda ambao ofisi zao ziliratibu ziara ya mafunzo ya walimu hao nchini India.
Akizunguza na walimu hao katika viwanja vya Bunge, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu -TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe ameshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuidhinisha fedha kiasi cha Shilingi Bilioni 3 na kutoa kibali cha walimu hao kwenda kwenye ziara ya mafunzo nchini India ili kujifunza na kupata ujuzi utakaowawezesha kuleta athari chanya zaidi katika mfumo wa elimu ya ufundi.
Sanjari na hilo, Prof. Shemdoe amewataka walimu hao kuhakikisha yote waliyojifunza nchini India wanaenda kuwafundisha wanafunzi madarasani na kwa vitendo ili wapate ujuzi utakaowawezesha kuwa wabunifu, wajasiriamali na uwezo wa kushindana katika ajira za ndani na nje ya nchi ikiwa ni pamoja na kujiajiri.
“Vijana wetu wanahitaji kupata maarifa na ujuzi mlioupata kwenye ziara yenu ya mafunzo nchini India, hivyo nendeni mkawafundishe kwa umahiri ili waje kutoa mchango katika maendeleo ya taifa,” amesisitiza Prof. Shemdoe.
Naye, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Adolf Mkenda amesema kuwa Serikali iliwapeleka walimu hao wapatao 150 nchini India kwenda kujifunza namna wanavyoendesha shule za amali na kutekeleza mtaala wao wa elimu ili wakirejea nchini waweze kuwa chachu ya kutekeleza vema mtaala mpya wa elimu kwa kutumia vema teknolojia iliyopo katika kuwafundisha vijana wa kitanzania elimu ya ufundi stadi.
“Sisi tulichukua walimu 150 na kuwapeleka India ili waende kujifunza namna masomo ya elimu ya amali yanavyofundishwa ili wakirejea waje kuwa chachu ya kuboresha namna ya kufundisha masomo ya amali, hatua hii ni sehemu ya utekelezaji wa maelekezo ya mapema ya Mhe. Rais kwa wizara ya Elimu na yale aliyoyatoa wakati akizindua sera yetu ya elimu,” amesema Prof. Mkenda.
*Watoto wanaolazwa wapungua kutoka 32 hadi 7 kwa robo mwaka
Na Augusta Njoji
IDADI ya watoto wanaokabiliwa na utapiamlo mkali katika Halmashauri ya Mji Handeni imepungua kwa kiasi kikubwa, kutoka watoto 32 waliokuwa wakilazwa hospitalini kwa robo mwaka 2024/25 hadi wastani wa watoto watano hadi saba kwa robo mwaka 2025/26.
Mafanikio hayo yanatajwa kuchangiwa na mikakati madhubuti ya utoaji elimu ya lishe kwa jamii inayotekelezwa na Hospitali ya Halmashauri hiyo, ikilenga kupunguza lishe duni hususan kwa watoto.
Akizungumza Mei 5, 2026 katika kikao cha tathmini ya shughuli za lishe kwa kipindi cha Januari hadi Machi 2025/26, Afisa Tarafa ya Chanika, Julieth Mushi, akimwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese, amepongeza juhudi hizo na mafanikio yaliyopatikana katika utekelezaji wa mkataba wa lishe.
Amesisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya Idara ya Afya, Ustawi wa Jamii na Lishe pamoja na Idara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi katika kuhamasisha jamii kuanzisha bustani za mboga majumbani na kufuga wanyama ili kukabiliana na tatizo la utapiamlo kwa watoto.
Kwa upande wake, Mganga Mkuu wa Halmashauri hiyo, Dkt.Hudi Shehdadi, amesema mikakati inayoendelea kutekelezwa ni pamoja na kushirikiana na Idara za Elimu ya Msingi na Sekondari pamoja na kamati za lishe za kata kuhamasisha upandaji wa miti ya matunda na uanzishaji wa bustani za mboga, huku kila shule ikitakiwa kutenga angalau hekari mbili kwa ajili ya kilimo cha mahindi.
Aidha, amebainisha kuwa juhudi zimeongezwa katika kuhamasisha wajawazito kuhudhuria huduma za afya mapema ili kupata elimu ya lishe pamoja na virutubisho vya madini chuma, hatua inayolenga kupunguza idadi ya watoto wanaozaliwa na uzito pungufu.
Awali, akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa shughuli za lishe kwa kipindi cha Januari hadi Machi 2025/26, Kaimu Afisa Lishe wa Halmashauri hiyo, Getruda Kasabaja, amesema jumla ya wazazi na walezi 9,571 wamefikiwa na elimu ya lishe, huku watoto 17,390 wakifanyiwa tathmini ya hali ya lishe.
Ameeleza kuwa kati ya watoto hao, watoto 221 walikuwa na uzito pungufu sawa na asilimia 1.27, watoto 80 walikuwa na udumavu (asilimia 0.4), na watoto 96 walikuwa na ukondefu (asilimia 0.55). Aidha, watoto saba walipatiwa matibabu ya utapiamlo mkali katika kipindi hicho.

Na OWM - TAMISEMI, Dodoma
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, amewataka walimu wapatao 150 wa shule za amali waliopatiwa mafunzo nchini India kwenda kuwapatia ujuzi vijana wa kitanzania katika shule wanazofundisha ambao utawawezesha kuwa wabunifu, wajasiriamali na washindani katika ajira za ndani na nje ya nchi ili kutoa mchango katika maendeleo ya taifa.
Prof. Shemdoe ametoa wito huo Mei 04, 2026 wakati wa kikao chake na walimu hao wapatao 150 wa Shule za Amali ambao wamerejea nchini kutoka nchini India walihudhuria mafunzo ya kuwajengea uwezo wa kutoa elimu ya ufundi na mafunzo ya stadi za kazi kama nyenzo muhimu ya kukuza uchumi wa viwanda, kupunguza ukosefu wa ajira kwa vijana, na kuongeza ushindani katika soko la ajira.
“Tunategemea vijana watakaotoka katika shule za amali wawe na uwezo wa kushindana katika ajira za ndani na nje ya nchi, waweze kujiajiri na kuwa wajasiriamali wenye mchango kwa taifa, hivyo muwapatie ujuzi na maarifa yote mliyoyapata nchini india,” amesisitiza Prof. Shemdoe.
Aidha, Prof. Shemdoe amewataka walimu hao kwenda kuwafundisha walimu ambao hawakupata fursa kupata mafunzo nchini India na kuongeza kuwa, Ofisi ya Waziri Mkuu-TAMISEMI kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu watawasilisha ombi kwa Mhe. Rais la kupatiwa fedha za kwenda kuwajengea uwezo walimu wa amali 601 waliosalia ili wawe na tija katika Taifa.
Prof. Shemdoe amempongeza Waziri wa Elimu na timu yake pamoja na Katibu Mkuu-TAMISEMI na timu yake kwa kushirikiana na Washauri Elekezi Global Education Link kuratibu zoezi la walimu hao wapatao 150 wa amali kwenda nchini India kupatiwa mafunzo yatakayowezesha utekelezaji wa mtaala mpya wa elimu.
Mmoja wa walimu walionufaika na mafunzo hayo, Mwalimu Paul Maziku wa Shule ya Sekondari Chato amesema wamefundishwa namna ya kuwawezesha wanafunzi kufikia ndoto zao na malengo yaliyokusudiwa na Serikali ya kuwa na elimu ya amali na kuongeza kuwa, walimu wote wapatao 150 waliopatiwa mafunzo wana ari ya kufundisha ili kuleta mabadiliko katika elimu.
Naye mnufaika mwingine wa mafunzo, Mwalimu Sungura Mollel wa Shule ya Sekondari ya Amali Ruvuma amesema kuwa wakiwa nchini India, wamejifunza namna ya kuandaa mitaala kulingana na uhitaji wa viwanda hivyo anaamini kwamba ujuzi walioupata utawawezesha kuwaandaa vijana wa kitanzania kuwa na ujuzi wenye tija kwa taifa ikizingatiwa kwamba wao ni walezi.
>Agawa vifaa vya michezo kwa timu zote zinazoshiriki Ligi ya wilaya ya Mkinga
Mbunge wa Jimbo la Mkinga mkoani Tanga, Twaha Mwakioja, ameahidi kushirikiana na wadau mbalimbali wa michezo kuinua kiwango cha soka wilayani humo kwa kuwekeza katika elimu na maendeleo ya waamuzi pamoja na makocha.
Akizungumza wakati wa mchezo wa Ngao ya Jamii uliokwenda sambamba na uzinduzi wa Ligi ya Wilaya ya Mkinga, uliofanyika katika Uwanja wa Chamazi, Kata ya Matamba, Mwakioja alisema lengo lao ni kuwekeza katika michezo kwa vijana ili kuwapatia ajira, kuboresha afya zao, pamoja na kuimarisha amani, mahusiano mema na ushirikiano miongoni mwao.
Alieleza kuwa dhamira yao ni kuwashika mkono vijana ili waweze kupiga hatua kutoka ngazi ya wilaya, kwenda mkoa, kanda na hatimaye ligi za juu, huku yeye akiwa bega kwa bega nao kuhakikisha wanafikia malengo yao.
Mbunge huyo alibainisha kuwa wamepata taarifa ya kuwepo kwa changamoto mbalimbali, ikiwemo uhaba wa makocha na waamuzi wenye sifa. Hivyo, wamejipanga kuwekeza katika mafunzo ya makocha ili kila kata iwe na angalau kocha mmoja mwenye ujuzi na mafunzo rasmi, pamoja na kuandaa waamuzi wenye vyeti ili kuboresha usimamizi wa michezo.
Alisisitiza kuwa uwekezaji huo utaenda sambamba na ushirikiano na Chama cha Soka Wilaya ya Mkinga katika kukuza na kuendeleza vipaji vya vijana.
Aidha, alisema mpango wao ni kuhakikisha kila kata na kijiji kinakuwa na timu ya mpira wa miguu inayoshiriki ligi ya wilaya. Aliongeza kuwa watawekeza zaidi ili kuibua timu imara zitakazoweza kushiriki ligi za ngazi ya mkoa, kanda na hatimaye Ligi Kuu, hatua itakayosaidia kuitangaza Mkinga katika ramani ya soka nchini.
Katika kuonyesha dhamira hiyo, Mwakioja alikabidhi jezi na mipira kwa timu zinazoshiriki ligi hiyo, ikiwa ni sehemu ya kuhamasisha na kusaidia maendeleo ya michezo wilayani humo.
Kwa upande wake, Katibu wa Chama cha Soka Wilaya ya Mkinga, Fadhili Habibu, alisema ratiba ya ligi hiyo imeanza Mei 4 katika kituo cha Mkinga, huku kituo cha Maramba kikitarajiwa kuanza Mei 6 (Jumatano), ambapo kutakuwa na vituo vinne vitakavyochezwa katika Kijiji cha Maramba, ikiwa ni pamoja na mechi kati ya Viva Dynamo na Maramba FC.
Habibu alisema lengo la ligi hiyo ni kusimamia na kuibua vipaji vya vijana, pamoja na kuwapa mwelekeo wa maendeleo yao kisoka. Alimshukuru mbunge kwa kujitoa na kushirikiana nao katika kufanikisha malengo hayo.
Naye Mwenyekiti wa Chama cha Soka Wilaya ya Mkinga, Hassan Zumo, alimpongeza mbunge kwa juhudi zake za kuendeleza michezo wilayani humo, akieleza kuwa hatua hiyo imeongeza hamasa na matarajio ya ushindani mkubwa katika ligi hiyo, hasa baada ya timu kukabidhiwa vifaa.
Zumo aliongeza kuwa tangu kuanzishwa kwa chama hicho mwaka 2008, wamekuwa wakipeleka vilabu katika mashindano ya ngazi ya mkoa lakini wamekuwa wakikwama kutokana na changamoto za kifedha. Hata hivyo, alisema kupitia uongozi wa Mbunge Mwakioja, wana matumaini ya kupata timu itakayoweza kufika hadi Ligi Kuu.
Aidha, timu zinazoshiriki mashindano hayo zimeahidi kujituma na kupambana kwa juhudi zote ili kuhakikisha ligi hiyo inaleta mafanikio na tija kwa vijana wa Wilaya ya Mkinga.

Na Mwandishi Wetu, Kibaha-Pwani.
Imeelezwa kuwa Tume ya Taifa ya Mipango imekamilisha nyenzo zote za utekelezaji wa Dira 2050 ambazo ni Mpango Elekezi wa Maendeleo wa Muda Mrefu 2026/2027–2050/2051 (LTPP 2050), Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Miaka Mitano 2026/27 – 2030/31 (FYDP IV) na Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2026/2027 kuelekea Julai 1, 2026 ambapo utekelezaji wa Dira hiyo utaanza rasmi.
Hayo yameelezwa leo Mei 4, 2026 na Katibu Mkuu Ofisi ya Rais-Mipango na Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango Dkt. Tausi Kida alipofungua mafunzo kwa Wakurugenzi wa Sera na Mipango, Wakurugenzi wa Ufuatiliaji na Tathmini, na Wakuu wa Idara na Vitengo vya Ufuatiliaji na Tathmini kutoka Wizara na Taasisi mbalimbali za Serikali yanayofanyika katika Chuo cha Uongozi Mwalimu Julius Nyerere, Kibaha - Pwani.
Dkt. Kida amewaambia washiriki wa mafunzo hayo kuwa, baada ya kukamilisha Dira 2050 na nyenzo zake, mafunzo hayo ni utekelezaji wa mkakati mahususi wa Serikali wa kujipanga kufanya utekelezaji wa Dira hiyo kwa kuhakikisha kunakuwepo na uelewa wa pamoja na utekelezaji unaolingana katika ngazi zote za Wizara, Taasisi za Serikali, Sekretarieti za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa katika kuhakikisha mipango ya Kitaifa inatekelezwa kwa tija.
“ Serikali kupitia Tume ya Taifa ya Mipango inakamilisha Miongozo ya Upangaji (NPGs), Mfumo wa Ufuatiliaji na Tathmini wa Programu na mirado ya Maendeleo (NF-MEDeP) na Mfumo wa Kidigitali uitwao E-Delivery. Mfumo huu na miongozo hiyo italetwa kwenu na mafunzo stahiki yanaandaliwa kwa ajili yenu” Amesisitiza Dkt. Kida.
Aidha, Dkt. Kida amesema kupitia mafunzo hayo, washiriki watapata fursa ya kujifunza kwa vitendo (i.e. case studies), kubadilishana uzoefu, na kujenga uwezo katika hatua zote za mzunguko wa miradi ya maendeleo kuanzia uibuaji, upangaji, uchambuzi, uidhinishaji hadi utekelezaji na ufuatiliaji.







Kutoka Pemba, Unguja, Mji mkongwe, Bagamoyo, Kondoa, Magofu ya kilwa, paa la mlima kilimanjaro na maeneo mengine ya Tanzania, wadau wa urithi wa dunia wamekutana katika Makumbusho ya Urithi Geopark Karatu Mkoani Arusha yanayosimamiwa na Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro kwa lengo la kuadhimisha Urithi wa Dunia Afrika yaliyoanza leo tarehe 04/05/2026 hadi tarehe 05/05/2026.
Wakiwa katika jengo la makumbusho ya Urithi Geopark Wadau hao wameelezwa jinsi Ngorongoro ilivyo ni utajiri wa urithi wa dunia kutokana na uumbwaji wake uliotokana na mlipuko wa volcano zaidi ya miaka milioni mbili iliyopita na kutengeneza kasoko iliyokusanya asili, uhai wa binadamu, mifumo ya ikolojia, na ustawi wa viumbe mbalimbali.
Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari Kamishna wa Uhifadhi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro Bw. Abdul-Razaq Badru amewashukuru wadau wote hasa Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) kwa kuipa fursa Ngorongoro kuandaa na kuwa mwenyeji wa maadhimisho hayo kwa mwaka huu.
Wadau wa urithi wa duania wakiwa katika Makumbusho ya Urithi Geopark walipata fursa ya kuelezewa kuhusu uthibitisho wa wasomi unaoeleza wazi historia ya chimbuko la binadamu wa kale aliyepatikana katika bonde la olduvai takribani milioni 2 iliyopita na ushahidi wa Nyanyo za binadamu wa kale katika eneo la Laetoli takribani miaka 3.6 iliyopiTa ambapo binadamu hao walitembea kwa miguu miwili.
Taasisi zinazoshiriki maadhimisho hayo ambazo zinasimamia maeneo ya urithi wa dunia ni pamoja na Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro (NCAA), Shirika la hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) Mamlaka ya Uzimamizi wa Wanyamapori (TAWA), Wakala wa Huduma za misitu Tanzania (TFS), pamoja na wawakilishi wa maeneo ya urithi wa dunia kutoka Zanzibar.
Ripoti ya Tume iliyoongozwa na Jaji Mohamed Chande Othman ya kuchunguza matukio ya uvunjifu wa amani wakati na baada ya uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025 imeendelea kuzua mjadala mkubwa nchini, huku mchambuzi wa masuala ya uongozi, uchumi na siasa Tanzania, Dk Netho Ndilito (PhD), akiitaja kama nyaraka muhimu iliyofichua mambo makubwa matano yenye maslahi kwa taifa.
Akizungumza kuhusu ripoti hiyo, Dk Ndilito amesema baada ya kupitia maoni ya Watanzania, wanamitandao na wachambuzi mbalimbali, amebaini kuwa taarifa hiyo imeleta mwanga mpya kuhusu hali halisi ya taifa na changamoto zilizokuwa zikijadiliwa kwa muda mrefu.
Kwa mujibu wa Dk Ndilito, jambo la kwanza ni kwamba ripoti hiyo imeliponya taifa kwa kueleza ukweli ambao kwa muda mrefu haukupata nafasi ya kujadiliwa waziwazi, ikifichuliwa pia kwa nia na dhamira ovu za baadhi ya watu waliotamani vurugu kabla, wakati na baada ya uchaguzi, jambo ambalo sasa limewekwa wazi kupitia uchunguzi huo.
Aidha, ameeleza kuwa ripoti hiyo imeweka bayana upotoshaji na taarifa zisizo sahihi zilizokuwa zikisambazwa na baadhi ya watu wasiolitakia mema taifa, huku wakitamani kuona nchi ikiingia kwenye machafuko.
Katika hoja ya nne, Dk Ndilito amesema ripoti hiyo imeonesha namna Watanzania wengi wanavyoipenda nchi yao, kuiamini serikali yao na kutokuwa tayari kushawishika kuivuruga amani, umoja na mshikamano wa taifa, huku pia ripoti hiyo ikionesha uimara wa serikali pamoja na ukomavu wa vyombo vya ulinzi na usalama katika kushughulikia masuala ya ndani kwa weledi na utulivu.
Dk Ndilito alitumia nafasi hiyo kuwapongeza Watanzania kwa kuendelea kudumisha umoja, upendo, mshikamano na amani, akisisitiza kuwa huo ndiyo utamaduni uliojenga heshima ya taifa kwa miaka mingi.
“Watanzania wameendelea kuonesha ukomavu mkubwa wa kisiasa na uzalendo. Hii ndiyo desturi yetu kama taifa,” alisema.
Yajipanga Kubeba Suluhu ya Uhaba wa Gesi hiyo Duniani
Helium One Global Yasema Akiba ya Songwe ina Thamani Kubwa Kijiolojia
Mradi Kuanza Kutekelezwa baada ya Miezi 18, Zaidi ya Dola Milioni 60 tayari Zimewekezwa
Serikali Kumiliki Asilimia 17 ya Hisa kupitia Kampuni ya Ubia ya Songwe Helium Limited
Tanzania imeanza rasmi Safari Mpya ya Kihistoria ikiingia kwenye ramani ya dunia kama Mzalishaji na Msambazaji wa kimkakati wa Gesi ya Helium. Hatua hiyo inafuatia baada ya kusainiwa kwa Mkataba wa Uchimbaji wa gesi hiyo baina ya Serikali na kampuni ya Helium One Global Limited kupitia Kampuni ya Ubia ya Songwe Helium Limited, katika hafla iliyofanyika Mei 2, 2026 Mkoani Songwe.
Hayo yamebainishwa na Naibu Waziri wa Madini Dkt. Steven Kiruswa wakati akizungumza katika hafla hiyo na kueleza kuwa, uzalishaji wa helium duniani kwa sasa unatawaliwa na nchi chache, hususan Marekani na Qatar, zinazochangia zaidi ya asilimia 75 ya uzalishaji wote, huku Urusi, Algeria, Canada, China na Poland zikichangia kwa kiwango kidogo. Ameongeza kuwa mahitaji ya gesi hiyo tayari yamevuka futi za ujazo bilioni 6 kwa mwaka na yanatarajiwa kuongezeka hadi zaidi ya bilioni 8.5 ifikapo mwaka 2030 ambapo kwa Tanzania kampuni za Helium One Global Limited na Noble Helium zimepiga hatua kubwa katika shughuli za utafiti wa gesi hiyo.
Ameeleza kuwa, mradi wa Southern Rukwa ni wa kimkakati unaoiwezesha Tanzania kuingia kwenye soko lenye thamani kubwa na ushindani mdogo na kuiweka katika nafasi ya kuathiri mwelekeo wa soko la helium duniani, huku ikitarajiwa kuwa sehemu ya suluhisho la uhaba wa gesi hiyo duniani na kueleza kwamba, uchimbaji wa helium utakwenda sambamba na gesi ambata kama hydrogen ambapo manufaa yake kimapato yatatenganishwa.
Aidha, Dkt. Kiruswa amefafanua kwamba kupitia mkataba huo, Serikali itamiliki asilimia 17 ya hisa katika kampuni ya ubia ya Songwe Helium Limited, hatua inayoiwezesha kushiriki moja kwa moja katika maamuzi ya kimkakati na kunufaika na mapato ya mradi kwa manufaa ya Taifa na wananchi.
‘’Huu ni utekelezaji halisi wa falsafa ya Serikali ya Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa rasilimali za nchi lazima ziwe chanzo cha ustawi wa taifa,’’ amesema Dkt. Kiruswa.
Akizungumzia manufaa mengine ya mradi huo amesema utachangia ajira kwa vijana wa eneo husika na taifa kwa ujumla, fursa za kibiashara kwa wazawa kupitia huduma za ugavi, uboreshaji wa miundombinu, mapato kwa Serikali na fedha za kigeni na uboreshaji wa miundombinu muhimu kama barabara na huduma za kijamii.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Helium One Global Limited, Lorna Blaisse amesema utiaji saini huo ni hatua muhimu kwa Tanzania na soko la helium duniani, akibainisha kuwa mradi una akiba yenye thamani kubwa na unaelekea kwenye uzalishaji wa kibiashara baada ya mafanikio ya uchimbaji kisima mwaka 2024 ambacho kilipelekea ugunduzi wa helium katika kisima cha Itambula West-1.
‘’Katika upimaji wa kisima uliopanuliwa robo ya tatu ya 2024, kisima cha ITW-1 kilirekodi helium yenye mkusanyiko wa asilimia 5.5 hadi juu ya ardhi, na hadi asilimia 7.6 kutoka miamba ya Karoo iliyovunjika na miamba ya Basement iliyopasuka,’’ amesema
Amesema baada ya utiaji saini wa leseni ya uchimbaji, kampuni ya Songwe Helium Ltd itaendelea na hatua za uendeshaji kuelekea uzalishaji wa kwanza wa kibiashara wa heliamu. Amezitaja hatua hizo kuwa ni pamoja na kukamilisha mipango ya maendeleo; mfumo wa usimamizi wa tathmini ya athari za mazingira na jamii; kubuni miundombinu, na kununua vifaa vya uchakataji na usafirishaji wa bidhaa.
Pia, ameishukuru Serikali ya Tanzania kwa ushirikiano wake na kuridhia muundo wa ubia unaohakikisha nchi inanufaika na rasilimali zake, akibainisha dhamira ya kuzalisha helium ya Tanzania kwa uwajibikaji na ubora wa juu kwa soko la dunia.
Awali, akizungumza katika hafla hiyo, Mwenyekiti wa Kamati ya Majadiliano ya Wizara ya Madini Prof. Sifuni Mchome amesema kupitia utaratibu wa Serikali kumiliki hisa huru zisizohafifishwa thamani, Serikali inashiriki moja kwa moja katika miradi ya madini, inapata faida kupitia gawio, mrabaha,kodi na tozo mbalimbali, inashiriki maamuzi ya kimkakati, kulinda mapato na maslahi ya wananchi kwa uwazi na uwajibikaji.
" Tulijadiliana kwa utaratibu mzuri bila kugombana na tumefika kwenye hatua ya kila mmoja apate, na leo tuko hapa kuweka wazi na kila mmoja ashuhudie," amesema Prof. Mchome.
Naye, Mkuu wa Mkoa wa Songwe Mhe. Jabiri Makame amesema Mkoa huo ni wa kimkakati ukiwa na utajiri wa Madini mbalimbali yakiwemo ya rare earth elements ambao utafiti wake unaendelea.
" Tunaipongeza Wizara ya Madini kwa kutafsiri kwa vitendo. Kwetu sisi suala la kuwasaidia wawekezaji kutekeleza mradi Kwa mafanikio ni kipaumbele cha kwanza," amesema Mhe. Makame.
Helium ni gesi ya kipekee sana duniani kwa sababu haina mbadala wake na matumizi yake ni ya kimkakati kwa maisha ya kisasa ya binadamu; inatumika katika vifaa vya tiba kama MRI, uzalishaji wa vifaa vya kielektroniki na teknolojia za kidigitali; sekta ya anga; ulinzi na tafiti za kisayansi, teknolojia za kisasa kama fibre optics na quantum computing.
Mradi huo unatekelezwa katika eneo la kilomita za mraba 480 ukiwa zaidi katika Mkoa wa Songwe Wilaya ya Momba na sehemu ndogo ikiingia Mkoa wa Rukwa.





















