Na James Mwanamyoto - Lushoto

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM–TAMISEMI) Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amemuelekeza Mkandarasi Namis Cooperate Limited aliyepewa kandarasi ya Ujenzi wa Mahakama ya Wilaya ya Lushoto, kuwapatia vijana wazawa na akina mama kazi zote ambazo hazihitaji utaalam ili kutengeneza ajira zitakazowapatia kipato ambacho kitainua uchumi wao.

Prof. Shemdoe ametoa maelekezo hayo leo  Disemba 31, 2025 wilayani Lushoto, wakati wa hafla ya kupokea eneo la Ujenzi wa Mahakama ya Wilaya ya Lushoto iliyohudhuriwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama, Prof. Elisante Ole Gabriel, viongozi wa mkoa na wilaya,  watumishi wa Mahakama  na wananchi wa Lushoto.

Prof. Shemdoe amemshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuridhia kutoa kiasi cha Shilingi Bilioni 4.272 kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama hiyo  ambapo ujenzi wake utawapatia kipato vijana watakaopewa kazi kwenye ujenzi wa jengo hilo.

“Mkandarasi ninakuomba huku nikikuelekeza kwamba, kazi zote ambazo hazihitaji expert wapewe vijana wetu wa hapa Lushoto ili tuweze kutengeneza ajira kwa vijana wetu wa hapa Lushoto,” Prof. Shemdoe amesisitiza.

Sanjari na hilo, Prof. amemtaka mkandarasi huyo kununua bidhaa za ujenzi zinazopatikana wilayani Lushoto ili kuongeza mzunguko wa fedha kwa wakazi wa wilaya hiyo ya Lushoto.

Pia, Prof. Shemdoe amemuelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto kuhakikisha anavikopesha fedha vikundi vya akina mama kupitia mikopo ya asilimia 10, ili vijishughulishe na biashara ya kuwauzia chakula vijana watakaoajiriwa kwenye mradi huo wa Ujenzi wa Jengo la Mahakama ya Wilaya ya Lushoto.

Aidha, Prof. Shemdoe ameushukuru ushirika wa kupanda kahawa Lushoto (coffee growers association) kwa uzalendo wao kwa kutoa bure eneo lenye ukubwa wa mita za mraba 6,269 kwa ajili ya Ujenzi wa jengo hilo la Mahakama. 

Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel amesema kuwa mkataba wa ujenzi wa Mahakama hiyo uliosaniwa leo hautakuwa na nyongeza ya muda wa mkataba wala nyongeza ya gharama, hivyo watasimamia ili kuhakikisha ujenzi unakamilika kwa wakati kwani wananchi wanashauku ya kuhudumiwa katika jengo jipya la Mahakama ya Wilaya. 

Mmoja wa wakazi wa Kata ya Magamba Wilayani Lushoto Bw. Salimu Omary amemshukuru Mbunge wa Jimbo la Lushoto ambaye ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu-TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe kwa kumuelekeza mkandarasi kuwapatia kazi vijana wazawa ili  kupata kipato kitakachoendesha maisha yao.

Naye mkazi mwingine wa Wilaya ya Lushoto Bw. Shaban Adam Mbwana amesema yeye binafsi atachangamkia fursa hiyo ya ajira kwenye mradi huo wa ujenzi wa jengo la Mahakama kwani ana watoto ambao wanahitaji kulipiwa ada shuleni hivyo atakuwa mnufaika wa mradi huo.

Kiasi cha Shilingi Bilioni 4,271,942,834.98 kitatumika kukamilisha mradi huo wa Ujenzi  wa Mahakama ya Wilaya ya Lushoto, ujenzi ambao unatarajiwa kutoa  ajira kwa vijana, akina mama lishe na wafanyabiashara wa wilayani Lushoto.










Mwenyekiti wa Klabu ya Waandishi wa Habari mkoani Dodoma (DPC) Bw.Musa Yusuf,akitoa neno la shukrani kwa Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) mara baada ya waandishi wa klabu hiyo kupatiwa mafunzo kuhusu udhibiti wa huduma za nishati na maji yaliyofanyika leo Disemba 31,2025 jijini Dodoma.

Na.Mwandishi Wetu-Dodoma

Wanachama wa Klabu ya Waandishi wa Habari mkoani Dodoma, leo 31 Desemba 2025, wameishukuru Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) kwa kuwapa mafunzo kuhusu udhibiti wa huduma za nishati na maji.

Mwenyekiti wa klabu hiyo, Musa Yusuf, ameipongeza EWURA kwa hatua ya kutoa mafunzo hayo, akibainisha umuhimu wa mkataba wa huduma kwa wateja, uvunaji wa maji ya mvua, na utekelezaji wa mkakati wa kitaifa wa matumizi ya nishati safi ya kupikia. Amesisitiza kuwa elimu waliyoipata wataitumia kwa kuelimisha umma.

“Asanteni sana EWURA kwa elimu hii, hakika imetufungua macho. Wenzangu wote ni mashahidi. Tunaomba mafunzo kama haya yaendelee,” amesema Bw. Yusuf.

Kwa upande wake Kaimu Meneja Mawasiliano na Uhusiano wa EWURA, Wilfred Mwakalosi, amesisitiza umuhimu wa waandishi wa habari kuelewa masuala yanayodhibitiwa na EWURA, kwani yanagusa huduma ambazo kila mwananchi kwa namna moja au nyingine anazitumia.

“Ninyi waandishi wa habari ni daraja kati ya EWURA na wananchi, tuendelee kushirikiana katika kuelimisha umma ili kila mtumiaji wa huduma tunazodhibiti ajue haki na wajibu wake”. Amesisitiza Mwakalosi.

 

   

 



Na Oscar Assenga, TANGA

MKUU wa Mkoa wa Tanga Balozi,Dkt Batilda Burian amewataka wananchi wa mkoa wa Tanga ambao wamepanga kutumia matairi kuchoma moto barabarani kama njia ya kusheherekea sikuuu ya mwaka mpya wasithubutu kufanya hivyo.

Dkt Batilda aliyasema hayo leo wakati akizungumza na waandishi wa habari kuelekea mkesha wa mwaka mpya ambao unatarajiwa kufanyika kwenye viwanja vya Urithi Jijini Tanga ambapo alisema kutokana huo ni uharibifu wa miundombinu ya barabara na hatari kwa Taifa.

Alisema kwamba ndio maana Ofisi ya Mkoa huo kwa kushirikiana na Uongozi wa Halmashauri ya Jiji la Tanga na Mbunge wa Jimbo la Tanga wameamua kufanya shughuli ya wana Tanga kwenye uwanja wa Burudani wa Uhuru Park.

Alisema kwamba kutakuwa na sanaa mbalimbali taarabu na miziki mbalimbali ikiwemo mashindano ya kupika maandazi ,vitumbua na watakaokuwa mabingwa wa kupika sambusa lakini watachoma samaki na mbuzi watu watakula bila gharama yoyote ili kuendeleza umoja,amani na ukarimu wa wana Tanga.

Aidha alisema kwamba baada ya hapo usiku watawasha mafataki watakayowashwa na wataalamu maalumu ya viwango maalumu hivyo kuliko kuchoma matairi waje kwenye uwanja wa uhuru ili kuona burudani mbalimbali ikiwemo mafataki.

Mkuu huyo wa mkoa aliwataka wana Tanga kwenda uwanja wa Urithi ili kuweza kuomba dua kumshukuru Mungu kuuona mwaka na baada ya hapo mtu kurudi nyumbani ni eneo ambalo litakuwa salama.

 

Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba, akikabidhiwa Jarida la “Hazina Yetu” Toleo la Tano, na Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Fedha, Bw. Benny Mwaipaja, katika ofisi ndogo za Wizara ya Fedha jijini Dar es Salaam, ambapo ameipongeza kitengo hicho kwa uandaaji mzuri wenye ubunifu, ubora na kwa kuendelea kuboresha mawasiliano na uelimishaji kwa umma katika masuala ya fedha na uchumi wa Taifa.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba, akimsikiliza Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Fedha, Bw. Benny Mwaipaja, baada ya kukabidhiwa Jarida la “Hazina Yetu” Toleo la Tano, katika ofisi ndogo za Wizara ya Fedha jijini Dar es Salaam, ambapo ameipongeza kitengo hicho kwa uandaaji mzuri wenye ubunifu, ubora na kwa kuendelea kuboresha mawasiliano na uelimishaji kwa umma katika masuala ya fedha na uchumi wa Taifa.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba, akisoma Jarida la “Hazina Yetu” Toleo la Tano, baada ya kukabidhiwa na Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Fedha, Bw. Benny Mwaipaja (hayupo pichani), katika ofisi ndogo za Wizara ya Fedha jijini Dar es Salaam, ambapo ameipongeza kitengo hicho kwa uandaaji mzuri wenye ubunifu, ubora na kwa kuendelea kuboresha mawasiliano na uelimishaji kwa umma katika masuala ya fedha na uchumi wa Taifa.

Katibu wa Waziri wa Fedha, Bw. Geoffrey Kesase na Katibu wa Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Bi. Fatma Shaaban, wakifurahia Jarida la “Hazina Yetu” Toleo la Tano, katika ofisi ndogo za Wizara ya Fedha jijini Dar es Salaam.

(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini,WF, Dar es Salaam)


Na. Joseph Mahumi, WF, Dar es Salaam


Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba, amepongeza ubunifu na ubora wa Jarida la Hazina Yetu Toleo la Tano ambalo limeandaliwa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini cha Wizara ya Fedha.

Ametoa pongezi hizo wakati akipokea Jarida hilo kutoka kwa Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Fedha, Bw. Benny Mwaipaja, katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha jijini Dar es Salaam.

Dkt. Mwamba alisema Jarida hilo ambalo limeendela kuwa bora na kufika kila mahali duniani kwa njia ya kidigitali ni nyenzo muhimu katika kuwasilisha taarifa sahihi, za wazi na kwa lugha inayoeleweka kuhusu shughuli, mafanikio na mipango ya Wizara ya Fedha.

Dkt. Mwamba alipongeza jitihada za Kitengo cha Mawasiliano Serikalini kwa kuendelea kuboresha mawasiliano na uelimishaji kwa umma pamoja na ubunifu na weledi unaooneshwa katika uandaaji wa Jarida hilo, akibainisha kuwa limeendelea kuwa chombo muhimu cha kuimarisha uwazi, uwajibikaji na ushirikishwaji wa wananchi katika masuala ya fedha na uchumi wa Taifa.

Kwa upande wake, Bw. Benny Mwaipaja alisema kuwa Jarida la Hazina Yetu linalenga kutoa taarifa kwa wananchi kuhusu utekelezaji wa majukumu ya Wizara ya Fedha pamoja na mchango wake katika maendeleo ya Taifa, akiahidi kuendelea kuliboresha ili liwe chombo chenye tija zaidi katika mawasiliano ya serikali.

Jarida la “Hazina Yetu Toleo la Tano” limesheheni maarifa mbalimbali kupitia Makala bora kabisa, habari, matukio ya picha na matangazo mbalimbali na linapatikana kwa njia ya nakala ngumu (hard copies) na nakala tete (soft copies) kupitia mitandao ya kijamii ya Wizara na wadau wengine wa habari pamoja na Tovuti ya Wizara ya Fedha www.mof.go.tz



Na Mwandishi wetu- KILIMANJARO

Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Uratibu na Watu wenye Ulemavu Mhe. Ummy Nderiananga ametoa wito kwa jamii kuwapenda, kuwajali na kuwahudumia makundi ya wenye mahitaji maalumu ili kukuza umoja na mshikamano katika Jamii.


Mhe. Nderiananga alisema hayo leo Disemba 31, 2025  akimuwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan katika utekelezaji wa utaratibu wa utoaji zawadi za sikukuu mbalimbali kuelekea Sikukuu ya Mwaka Mpya wa 2026, zawadi hizo  zimeenda kwa watoto 190 wakiwemo wenye ulemavu na wasio na ulemavu wanaolelewa na Shirika la The Creator Share Foundation lililopo Kata ya Kirua, Wilaya ya Moshi Vijijini mkoani  Kilimanjaro.

Alisema, ndani ya siku 100 za uongozi wake ameendelea kuleta faraja, upendo, tumaini na umoja kwa watanzania huku akisema kuwa kitendo hicho ni ishara ya upendo mkubwa kwa wananchi bila kujali hali zao.


“Naomba nitumie fursa hii kuwatakia kheri ya sikukuu ya mwaka mpya  wa  2026 twende tukasherehekee kwa amani  na tukiwa na faraja kwa sababu Mhe. Rais ametukumbuka sisi ni watoto wake hivyo tudumishe upendo huu miongoni mwetu kila mmoja amuone mwenzake ni wa muhimu katika jamii,” alisema Mhe. Nderiananga.

Akitaja vitu alivyovikabidhi kwa watoto hao alisema, ni pamoja na Mchele kilo 100, Ngano kilo 50, Mbuzi wawili, sabuni, mafuta ya kupikia, madaftari, sukari kilo 25 na vinywaji



" Nitoe wito kwa jamii kuwa, kila mmoja ana wajibu wa kuwahudumia watoto na watu wenye mahitaji maalum, siyo tu kwa siku za sikukuu, bali kwa muda wote ili kuwapa faraja na huo ndio upendo tunaotakiwa kuwaonesha," aliongeza.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Moshi Bw. Godfrey Mnzava  alibainisha kuwa,  ili kuwa na ustawi wa maisha ya kijamii ni lazima kuwajali watu wenye uhitaji  ili waweze kukidhi mahitaji muhimu ya kila siku.


Naye,Diwani wa Viti Maalum Tarafa ya Vunjo Magharaibi ambaye pia ana mtoto mwenye ulemavu anayelelewa katika Shirika hilo Bi. Pamela Chuwa alipongea hatua hiyo ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuwafikia watu wenye ulemavu hatua inayowaganya kujisikia kuwa ni sehemu ya jamii.



“Mimi kama mama mwenye mtoto wa mahitaji maalum nimejisikia furaha kwa kupewa kipaumbele na tumefurahi sana Naibu Waziri Ummy kutufikia ukizingatia baadhi yetu tumefukuzwa katika familia  tukionekana kama kuzaa watoto wenye ulemavu ni mkosi na laana katika familia,” alipongeza Bi. Diwani huyo.



Vilevile Afisa Rasilimali Watu katika Shirika hilo Bi. Judith Shio mara  baada ya kupokea zawadi hizo alimshukuru Mhe. Rais Dkt.  Samia  Suluhu Hassan kwa moyo wa upendo na kuwajali watu wenye mahitaji Maalum huku akitoa wito kwa wadau mbalimbali kujitolea ili kuendelezwa moyo wa upendo na faraja kwa makundi hayo.



“Kwa niaba ya Shirika tunatanguliza shukrani zetu za dhati kwa upendo huu na mwaka huu tunauanza kipekee sana na watoto wamefurahi hivyo kwetu imekuwa faraja kubwa na imegusa jamii,” alishukuru Bi. Judith.


 Nao baadhi ya watoto wanaolelewa katika Shirika hilo wameishukuru Serikali kwa kuwakumbuka wakisema ujio huo kwao umekuwa ni historia na furaha kubwa ya kuuanza mwaka mpya kwa matumaini huku wakimshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa upendo huo wa the kuwashika mkono watoto wenye mahitaji maalum.


MWISHO

 


Imeelezwa kuwa matumizi ya nishati safi ya kupikia yameendelea kufungua fursa nyingi za ajira kwa Watanzania, hususani katika uzalishaji wa mkaa mbadala na utengenezaji wa mashine za kuzalishia mkaa huo.

Mkurugenzi wa Nishati Safi ya Kupikia kutoka Wizara ya Nishati, Bw. Nolasco Mlay amesema hayo wakati wa ziara yake ya kutembelea Taasisi ya Wazalendo Movement inayojishughulisha na utengenezaji wa mashine za kuzalisha mkaa mbadala pamoja na uzalishaji wa mkaa huo wilayani Mkuranga mkoani Pwani.

Bw. Mlay amesema kuwa taasisi nyingi zinazohudumia watu kuanzia 100 na kuendelea zimeanza kuhamia katika matumizi ya nishati safi ya kupikia, jambo linaloongeza kwa kiasi kikubwa mahitaji ya mkaa mbadala na hivyo kuhitaji uzalishaji wa kasi zaidi.

“Niwapongeze kwa kazi nzuri mnayoifanya ya kuzalisha mkaa mbadala pamoja na mitambo ya kutengenezea mkaa huo. Hii ni fursa kubwa kwa Watanzania kwani mahitaji ni makubwa, lakini ni muhimu kuhakikisha mkaa huu unaozalishwa ni wa ubora wa hali ya juu na unaodumu hata ukisafirishwa kwa umbali mrefu,” amesisitiza Bw. Mlay

Kwa upande wake, Mhandisi Mwandamizi kutoka Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Deusdedit Malulu amesisitiza umuhimu wa kushirikisha Shirika la Viwango Tanzania (TBS) katika utengenezaji wa mkaa mbadala ili kuhakikisha bidhaa zinakidhi viwango vinavyotakiwa.

Aidha, amewahimiza wazalishaji kujisajili kwenye mfumo wa NEST ili kupata fursa mbalimbali na kubainisha kuwa REA ina mpango wa kutoa fursa kwa wananchi katika utengenezaji wa mashine kwa lengo la kuongeza upatikanaji wa vifaa vya kuzalisha mkaa mbadala.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Wazalendo Movement,Bw. Saidi Malema amesema kuwa taasisi hiyo, katika kuendelea kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia, imeanzisha kikundi cha nishati safi ya kupikia kinachojihusisha na uzalishaji wa mkaa mbadala unaotengenezwa kutokana na magunzi ya mahindi na nyasi kavu.

Amesema taasisi hiyo hutengeneza mashine za kuzalishia mkaa zinazotumia umeme na zisizotumia umeme.

Ameongeza kuwa taasisi hiyo pia imeanzisha kikundi cha Nishati Safi Sanaa Group, kinacholenga kutoa elimu kwa wananchi kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia kupitia sanaa ya maigizo na nyimbo.

Amesema Taasisi ya Wazalendo Movement imefanikiwa kuuza mashine zake kwa wadau katika mikoa ya Tabora, Singida na Pwani. Aidha, imekuwa ikigawa mashine ndogondogo kwa wananchi wa vijiji vya Wilaya ya Mkuranga ambako umeme bado haujafika ili kuwahamasisha kuhamia katika matumizi ya nishati safi ya kupikia.

Katika ziara hiyo, Bw. Nolasco Mlay pia alitembelea kampuni ya Matima Investment inayojishughulisha na utengenezaji wa majiko ya kuchomea nyama yanayotumia gesi, kwa lengo la kujionea namna majiko hayo yanavyosaidia kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini.






 


Na Angela Msimbira, Dar es Salaam


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, amewaagiza Wakuu wa Mikoa, Makatibu Tawala wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya pamoja na Wakurugenzi wa Halmashauri kuhakikisha hakuna mtoto anayezuiwa kuanza au kuendelea na masomo kwa sababu ya kukosa sare, wakati shule zote nchini zikitarajiwa kufunguliwa rasmi Januari 13, 2025.

Prof. Shemdoe amesema kuwa agizo hilo linapaswa kusimamiwa kikamilifu katika maeneo yote ya nchi ili kuhakikisha kila mtoto anapokelewa shuleni bila masharti yanayokiuka miongozo na sera za elimu.

Amesisitiza kuwa mara mtoto anapopokelewa shuleni, masuala mengine ikiwemo sare, yataendelea kushughulikiwa akiwa tayari anaendelea na masomo, hatua itakayosaidia kuondoa vikwazo vinavyowafanya baadhi ya watoto kukosa haki yao ya msingi ya elimu.

Aidha, Prof. Shemdoe amekemea tabia ya baadhi ya shule za Serikali kuweka michango mingi kwa wazazi, ikiwemo kuwalazimisha kununua sare shuleni, akieleza kuwa hatua hiyo ni kinyume na taratibu na miongozo ya Serikali.

Ameelekeza walimu wakuu, walimu na viongozi wa shule kusoma, kuelewa na kuzingatia miongozo ya elimu iliyopo, pamoja na kutoa elimu sahihi kwa wazazi na walezi ili kuondoa sintofahamu zisizo za lazima.

“Lengo la Serikali ni kuona watoto wote wanakwenda shule bila vikwazo vyovyote, na kuhakikisha hakuna mtoto anayenyimwa haki yake ya elimu kwa sababu ya changamoto za kiuchumi au maamuzi yasiyo sahihi,” amesisitiza Prof. Shemdoe.