📌PPRA Yatambua Ubora na Usimamizi .

Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) Mkoa wa Tanga imeibuka miongoni mwa taasisi zilizofanya vizuri zaidi nchini katika usimamizi wa ununuzi wa umma baada ya kutwaa tuzo mbili katika Kongamano la 10 la Ununuzi wa Umma la mwaka 2026 linaloendelea jijini Arusha.

Tuzo hizo zilizotolewa na Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA) zinatokana na mafanikio ya TARURA Tanga katika kuzingatia kikamilifu matakwa ya Sheria ya Ununuzi wa Umma pamoja na kuonyesha ufanisi mkubwa katika utoaji wa mikataba.

Katika tuzo ya kwanza TARURA Tanga ilitambuliwa kwa kutekeleza kwa kiwango cha juu matakwa ya sheria yanayotaka asilimia 30 ya bajeti ya ununuzi kutengwa kwa ajili ya vikundi vya kijamii hatua iliyotajwa kuwa mfano bora wa utekelezaji wa sera za Serikali za kuwainua makundi yenye mahitaji maalum kiuchumi.

Tuzo ya pili ilitokana na mafanikio ya Wakala huo katika usimamizi wa mikataba baada ya kufanikisha utoaji wa mikataba 106 katika mwaka wa fedha 2025/2026, jambo lililoiweka miongoni mwa taasisi zilizofanya vizuri zaidi nchini.

Mafanikio hayo yanaendelea kuithibitisha TARURA kuwa miongoni mwa taasisi zinazosimamia kwa ufanisi matumizi ya fedha za umma kupitia uzingatiaji wa sheria, uwazi na uwajibikaji katika mchakato wa ununuzi nchini.







 

Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA) imeshiriki Kongamano la 10 la Ununuzi wa Umma mwaka 2026 linaloendelea jijini Arusha, limewakutanisha wadau wa ununuzi pamoja na viongozi wa Serikali kwa lengo la kujadili na kuweka mikakati ya kuimarisha Sekta ya ununuzi na ugavi nchini.

Akizungumza kwa niaba ya Katibu Mtendaji wa PPAA, Bw. James Sando, Mkuu wa Sehemu ya Huduma za Sheria PPAA, Bi. Agnes Sayi amewahimiza wadau wa ununuzi wa umma kutembelea banda la Mamlaka ya Rufani kupata uelewa juu ya majukumu na huduma mbalimbali zinazotolewa na taasisi hiyo hususan matumizi ya Moduli ya kupokea na kushughulikia malalamiko na rufaa katika mfumo wa NeST.

PPAA imeshiriki maonesho yanayofanyika pembezoni mwa Kongamano hilo kwa lengo la kutoa elimu kuhusu uamuzi juu ya rufaa zinazotokana na mchakato wa ununuzi wa umma, uamuzi juu ya rufaa zinazotokana na kufungiwa kushiriki katika michakato ya ununuzi wa umma pamoja na uamuzi juu ya malalamiko yanayotokana na kushindwa kwa Afisa Masuuli kutoa uamuzi ndani ya muda uliowekwa.

Awali, akifungua Kongamano hilo kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar, (Mb.), Katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha, Dkt. Toba Nguvila amesema sekta ya ununuzi wa umma inahusisha sehemu kubwa ya matumizi ya fedha za serikali, hivyo kuna ulazima wa kuhakikisha fedha zote zinazotengwa zinasimamiwa kwa umakini mkubwa ili kuleta matokeo yaliyokusudiwa.

Dkt. Nguvila amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuimarisha matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika mfumo wa ununuzi wa umma ili kuongeza uwazi, kupunguza gharama za ununuzi, kuharakisha mchakato na kurahisisha ufuatiliaji wa matumizi ya fedha za umma.

"Ununuzi wa umma na ugavi ni nyenzo ya kisera na kimkakati ya Serikali katika kuchochea uzalishaji, ukuaji wa viwanda, kuongeza ajira, kuimarisha kampuni za ndani, kukuza ubunifu, na kuhakikisha maendeleo yanayopatikana yanawanufaisha Watanzania wengi zaidi," amesema Dkt. Nguvila.

Kongamano hilo la siku tatu limeanza tarehe 29 - 31 Julai, 2026 limewakutanisha wadau wa ununuzi zaidi ya 1,500. Aidha, limewakutanisha Wakuu wa Taasisi, Maafisa Masuuli, Maafisa Ununuzi, Idara Tumizi, Maafisa Sheria, Wazabuni na Taasisi binafsi.





Mlezi wa APSP na Kamishna Mstaafu wa Sera za Ununuzi wa Umma, Dkt. Fredrick Asumile Mwakimbinga,

 Mkutano Mkuu wa Tano wa Chama cha Wataalamu wa Ununuzi na Ugavi Tanzania (APSP) umefanyika jijini Arusha ukiwa na lengo la kupokea taarifa za uongozi, kujadili utekelezaji wa maazimio, fedha na bajeti, pamoja na kuweka mikakati ya kuongeza ushiriki wa makundi maalum na biashara ndogo na za kati (SMEs) katika fursa za ununuzi wa umma.


Akifungua mkutano huo, Mlezi wa APSP na Kamishna Mstaafu wa Sera za Ununuzi wa Umma, Dkt. Fredrick Asumile Mwakimbinga, alisema zaidi ya asilimia 70 ya fedha za Serikali hupitia katika shughuli za ununuzi, hivyo aliwataka wataalamu wa sekta hiyo kufanya kazi kwa uadilifu, kuzingatia maadili ya taaluma na kulinda heshima ya taasisi zao.

Dkt. Mwakimbinga pia aliwahimiza wanachama kuendelea kuimarisha taaluma ya ununuzi na ugavi kwa kuzingatia sheria na matumizi ya teknolojia, kushiriki kutoa elimu kwa umma, kusimamia migogoro ya mikataba, kufanya ukaguzi wa bidhaa na kuzuia bidhaa bandia ili kuhakikisha fedha za umma zinatumika kwa ufanisi na miradi ya maendeleo inatekelezwa kwa wakati.

Alisema kaulimbiu ya mkutano huo, inayohusu kuimarisha ushiriki wa kitaaluma na kuwezesha makundi maalum pamoja na SMEs kunufaika na fursa za ununuzi wa umma, inalenga kuwafanya wataalamu kuwa kiungo muhimu kati ya sheria, urasimishaji wa biashara na utekelezaji wa maendeleo nchini.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya APSP, Dkt. Emmanuel Urembo, alisema mustakabali wa taaluma hiyo unategemea uwezo wa wataalamu kuendana na maendeleo ya teknolojia, kuzingatia maadili na kutoa ushauri wa kimkakati. Alibainisha kuwa chama kina wanachama zaidi ya 2,200 na kimepata mafanikio ikiwemo kusaini mikataba ya ushirikiano, kulipa deni la kiwanja la shilingi milioni 134 na kusajili nembo ya chama kupitia BRELA.

Naye Mkuu wa Kitengo cha Huduma za Sheria na Uzingatiaji kutoka BRELA, Wakili Lamecky Nyangi Samson, alisema wataalamu wa ununuzi wana mchango mkubwa katika kuhamasisha urasimishaji wa biashara kwa kuzingatia sheria na kuunganisha wafanyabiashara na fursa zinazotokana na ununuzi wa umma.

Akifunga mkutano huo, Mkurugenzi Mkuu wa PPRA, Bw. Denis Kwame Simba, aliwataka washiriki kutumia mifumo ya kielektroniki kwa ufanisi, kuzingatia uwazi, ushindani na thamani ya fedha, kutenga asilimia 30 ya zabuni kwa makundi maalum, kusimamia vihatarishi, kujibu hoja za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa wakati na kuzingatia masuala ya mabadiliko ya tabianchi katika utekelezaji wa shughuli za ununuzi wa umma.

 




Tanga, Julai 28, 2026


Katika kuendeleza dhamira yake ya kuchangia maendeleo ya jamii kupitia mpango wa Uwajibikaji kwa Jamii (CSI) chini ya kampeni yake ya #PSSSFKaribuNaJamii, Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) umekabidhi rasmi mradi wa miundombinu wenye thamani ya Shilingi milioni 25 katika Shule ya Msingi Majani Mapana iliyopo mkoani Tanga.


Mradi huo unahusisha ujenzi wa chumba cha darasa, chumba cha mapumziko pamoja na vifaa mbalimbali vya michezo kwa ajili ya watoto wenye mahitaji maalum.

Akizungumza wakati wa makabidhiano hayo, Bw. Kwame Temu alieleza kuwa msaada huo unalenga kuunga mkono juhudi za Serikali kwa kuhakikisha watoto wenye mahitaji maalum wanapata haki yao ya msingi ya elimu. Alisisitiza kuwa hatua hiyo itawasaidia wanafunzi hao kujifunza katika mazingira yanayowawezesha kujifunza kwa ufanisi, kushiriki katika michezo na kukuza vipaji vyao mbalimbali.

Kwa upande wake, Afisa Elimu Kata ya Nguvumali, Bi. Lilian Shetui, aliishukuru PSSSF kwa mchango huo akieleza kuwa miundombinu hiyo itaongeza ubora wa huduma za elimu shuleni hapo. Kwa niaba ya Afisa Elimu Shule za Awali na Msingi wa mkoa huo, Bi. Lilian alipongeza PSSSF kwa kuona umuhimu wa kundi hilo na kutoa msaada utakaokuwa na tija kubwa kwa watoto hao.

Kupitia mchango huo, jumla ya wanafunzi 71 wenye mahitaji maalum na usonji katika Shule ya Majani Mapana wanatarajiwa kunufaika na mazingira rafiki ya kujifunzia, kupumzika na kucheza, hatua inayochochea elimu jumuishi na kuwajengea msingi bora wa maisha ya baadaye.




 


Na OWM – TAMISEMI, Dodoma

Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM–TAMISEMI), Bw. Sospeter Mtwale, ameongoza kikao kazi kati ya ofisi yake na Shirika lisilo la Kiserikali la World Vision Tanzania, kilicholenga kujadili Mkakati wa Jubilee 2026–2030 uliowasilishwa na World Vision Tanzania wa kuboresha ustawi wa watoto nchini.

Mkakati huo uliofanyika leo Julai 29, 2026 unalenga kuwafikia watoto moja kwa moja kupitia programu za afya, lishe, elimu, ulinzi wa mtoto, huduma za maji safi na usafi wa mazingira (WASH), pamoja na kuimarisha kipato cha kaya. 

Akifafanua kuhusu lengo la mkakati huo, Mkurugenzi wa Ubora na Mikakati wa World Vision Tanzania Bw. Simon Moikan amesema, mpango huo  unakusudia kushughulikia changamoto tatu zinazoendelea kuathiri mamilioni ya watoto nchini ambazo ni utapiamlo, utoro wa shule na ukatili dhidi ya watoto.

Mara baada ya Mkakati huo kuwasilishwa, Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu –TAMISEMI Bw. Sospeter Mtwale alitoa fursa kwa wataalamu kutoka idara mbalimbali za Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI zinazoshughulikia masuala ya ustawi wa watoto pamoja na wataalamu kutoka World Vision Tanzania, kujadiliana kuhusu namna bora ya kuratibu ushirikiano katika utekelezaji wa mkakati huo iwapo mamlaka itaridhia, pindi utakapowasilishwa Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI kwa hatua za uidhinishaji.

Majadiliano hayo  yanaakisi dhamira ya kuimarisha ushirikiano kati ya Serikali na wadau wa maendeleo katika kuhakikisha watoto wa Tanzania wanapata huduma bora na mazingira salama yanayowezesha ukuaji, maendeleo na ustawi wao.
















 


Na. Ramadhani Kissimba, Durban.

 

Nchi wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) zimeshauriwa kuwekeza zaidi katika maendeleo ya viwanda na miundombinu ili kuwawezesha wanawake na vijana kushiriki kikamilifu katika shughuli za uzalishaji na kuongeza mchango wao katika ukuaji wa uchumi wa ukanda wa SADC.

 

Ushauri huo umetolewa jijini Durban nchini Afrika Kusini na Meneja wa Utafiti na Biashara wa Benki ya Maendeleo Tanzania (TIB), Dkt. Hilderbrand Shayo, kando ya Mkutano wa Wiki ya Viwanda wa SADC unaoendelea nchini humo.

 

Alisema kuwa uwekezaji katika viwanda vya kuongeza thamani ya bidhaa utasaidia kuwainua wanawake na vijana kiuchumi, kupanua masoko ya bidhaa za Tanzania na kuongeza mapato yatokanayo na mauzo ya bidhaa nje ya nchi.

 

Akizungumzia kuhusu ushiriki wa Tanzania katika mkutano na maonesho hayo, Dkt. Shayo alisema matukio hayo yanaendana na vipaumbele vya maendeleo vya Tanzania, hususan katika sekta za madini, kilimo, bidhaa za afya pamoja na maendeleo ya miundombinu na ubunifu, ambazo ni maeneo yanayopewa kipaumbele katika kufikia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

 

"Ushiriki wa Tanzania katika Wiki ya Viwanda ya SADC una umuhimu mkubwa kwa sababu mkutano huu umejikita katika kuimarisha mnyororo wa thamani wa sekta za madini, kilimo na bidhaa za afya, sambamba na maendeleo ya miundombinu na ubunifu na ni maeneo muhimu katika safari ya Tanzania kuelekea uchumi wa viwanda na maendeleo endelevu," alisema Dkt. Shayo.

 

Aidha, alisema kuwa maonesho hayo yamefungua fursa mpya za uwekezaji, ambapo wawekezaji kutoka nchi mbalimbali wameonesha nia ya kuwekeza nchini Tanzania kutokana na mazingira mazuri ya biashara pamoja na nafasi ya kimkakati ya nchi hiyo kama lango la biashara kupitia Bandari ya Dar es Salaam inayohudumia nchi nyingi wanachama wa SADC.

 

Dkt. Shayo, aliongeza kuwa ushiriki wa Tanzania katika maonesho hayo umeiwezesha nchi kuzitangaza fursa zake za uwekezaji na kuimarisha ushirikiano wa kibiashara na wadau mbalimbali wa maendeleo kutoka ndani na nje ya ukanda wa SADC.

 

Sambamba na hilo, Dkt. Shayo alizishauri taasisi za fedha zilizoshiriki katika mkutano huo, ikiwemo Benki ya Maendeleo Tanzania (TIB), Benki ya Exim, BADEA, Nedbank na taasisi nyingine za kifedha, kuimarisha ushirikiano katika kutafuta mitaji na fedha za kugharamia miradi ya maendeleo na uwekezaji nchini Tanzania.

 

"Taasisi za fedha zilizoshiriki katika maonesho haya zina nafasi kubwa ya kushirikiana katika kuhamasisha upatikanaji wa fedha kwa ajili ya miradi ya maendeleo na uwekezaji ambayo itachochea ukuaji wa uchumi wa Tanzania," alisema Dkt. Shayo

 

Akizungumzia sekta ya madini, Dkt. Shayo alisema Tanzania imebarikiwa kuwa na madini mengi ya kimkakati yanayohitajika duniani, hususan katika kipindi hiki cha maendeleo ya teknolojia.

 

Alisisitiza umuhimu wa kuyachakata madini hayo ndani ya nchi badala ya kuuza malighafi pekee, hatua ambayo itaongeza thamani ya bidhaa, kuzalisha ajira zaidi, kuongeza mapato ya fedha za kigeni na kuchochea ukuaji wa viwanda vya ndani.

 

Mkutano wa Wiki ya Viwanda wa SADC umeendelea kuwa jukwaa muhimu la kuimarisha ushirikiano wa kikanda katika biashara, uwekezaji na maendeleo ya viwanda. Kwa Tanzania, ushiriki katika mkutano huo unaendelea kufungua fursa mpya za uwekezaji, masoko na ubia wa kifedha, huku ukiunga mkono juhudi za Serikali za kujenga uchumi wa viwanda, kuongeza thamani ya rasilimali za ndani na kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.



Na. Peter Haule, WF, Arusha

 

Serikali imesema matumizi ya Mfumo wa Kielektroniki wa Ununuzi wa Umma (NeST) yameendelea kuongezeka nchini, hatua iliyochangia kuimarika kwa uwazi, ushindani, uwajibikaji na matumizi yenye tija ya fedha za umma katika shughuli za ununuzi na ugavi.

 

Hayo yalielezwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), katika hotuba iliyosomwa kwa niaba yake na Katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha, Dkt. Toba Nguvila, wakati wa Kongamano la 10 la Ununuzi wa Umma 2026 lililofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC).

 

Alisema kuwa hadi Juni 30, 2026, jumla ya wazabuni 45,270 walikuwa wameidhinishwa na kusajiliwa katika Mfumo huo, ambapo asilimia 95 kati yao walikuwa wazabuni wa ndani.

 

“Katika mwaka wa fedha 2025/2026, hadi Juni 30, 2026, jumla ya tuzo za zabuni 181,057 zenye thamani ya shilingi trilioni 14.5 zilitolewa kupitia mfumo wa NeST, hatua inayoonesha kuongezeka kwa matumizi ya Mfumo huo katika utekelezaji wa shughuli za ununuzi wa umma”, alisema Dkt. Nguvila.

 

Dkt. Nguvila alisema mafanikio hayo yanaonesha kuwa NeST imeendelea kuwa nyenzo muhimu katika kuimarisha usimamizi wa shughuli za ununuzi wa umma na ugavi, pamoja na kuongeza uwazi, ushindani na thamani ya fedha za umma.

 

Alisema Mfumo huo pia umeipa Tanzania heshima kimataifa baada ya kuchaguliwa kuwa miongoni mwa Mifumo 20 bora ya Serikali duniani katika Tuzo za World Summit on the Information Society, mafanikio yanayoakisi hatua kubwa iliyopigwa katika mageuzi ya kidijitali kwenye sekta ya ununuzi wa umma na ununuzi endelevu.

 

Dkt. Nguvila alifafanua kuwa, ujenzi wa Mfumo wa NeST umekamilika kwa asilimia 100 na kwa sasa shughuli zote muhimu za ununuzi wa umma, kuanzia usajili wa wazabuni, uandaaji wa zabuni, usimamizi wa mikataba hadi malipo, zinafanyika kupitia Mfumo huo.

 

Alisisitiza kuwa taasisi zote za umma zina wajibu wa kutekeleza shughuli za ununuzi kupitia Mfumo wa NeST, akionya kuwa taasisi yoyote itakayofanya ununuzi nje ya Mfumo huo itakuwa imekiuka matakwa ya Sheria ya Ununuzi wa Umma.

 

"Serikali itaendelea kusimamia matumizi ya Mfumo wa NeST ili kuhakikisha taasisi zote za umma zinafuata sheria na taratibu zilizowekwa," alisema Dkt. Nguvila.

 

Aidha, Dkt. Nguvila aliipongeza Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA) kwa kuendelea kusimamia utekelezaji wa Sheria ya Ununuzi wa Umma na kuimarisha matumizi ya Mfumo wa NeST, ambapo aliitaka Mamlaka hiyo kuendelea kuuboresha Mfumo huo na kuuunganisha na mifumo mingine ya Serikali ili kuongeza ufanisi, kurahisisha ubadilishanaji wa taarifa na kuimarisha usimamizi wa matumizi ya fedha za umma.

 

Aliongeza kuwa Serikali inaendelea kutambua ununuzi wa umma kama nyenzo muhimu ya sera ya uchumi inayochochea maendeleo ya viwanda vya ndani, kukuza ushiriki wa wazabuni wazawa, kuongeza ajira na kuchangia ukuaji wa uchumi wa Taifa pamoja na kufanikisha malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

 

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA), Bw. Dennis Simba, alisema taasisi zote za Serikali zinapaswa kuzingatia kikamilifu Sheria ya Ununuzi wa Umma, akisisitiza kuwa taasisi zitakazoshindwa kutekeleza matakwa ya sheria hiyo zitawekwa hadharani, ikiwa ni utekelezaji wa maelekezo ya, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

 

Bw. Simba pia aliwapongeza wadau walioshiriki Kongamano la 10 la Ununuzi wa Umma 2026 na kuwataka kutumia fursa hiyo kuongeza uelewa na uwezo wa kitaalamu ili kuendelea kuboresha utekelezaji wa shughuli za ununuzi wa umma nchini.

 


Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Taifa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Akiongoza Kikao Maalum cha Halmashauri  Kuu ya CCM Taifa  kilichofanyika Zanzibar Jumatano tarehe 29 Julai, 2026.











Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam


Dar es Salaam imeandika historia mpya katika harakati za kuboresha huduma za afya baada ya Mkoa wa Manyara kufanikisha zoezi kubwa la kuchangisha fedha lililowezesha kupatikana kwa zaidi ya Shilingi bilioni 1.3 kwa ajili ya kuokoa maisha ya watoto wanaozaliwa njiti na kuimarisha huduma za afya katika mkoa huo.


Fedha hizo zilikusanywa kupitia hafla maalumu ya chakula cha jioni cha hisani (Manyara Tanzanite Marathon Dinner Gala) iliyofanyika Julai 24, 2026 katika Hoteli ya Serena, Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya kampeni ya Hatua Moja Okoa Maisha ya Mtoto, ambayo inalenga kuongeza upatikanaji wa vifaa tiba vya kisasa, kuboresha huduma za watoto wachanga na kupunguza vifo vinavyotokana na kuzaliwa njiti.


Jumla ya Shilingi 1,356,900,000 zilipatikana kupitia ahadi za michango na fedha taslimu kutoka kwa wadau mbalimbali wa maendeleo, taasisi za fedha, makampuni binafsi, viongozi wa Serikali, wabunge, wafanyabiashara na wananchi waliojitokeza kuunga mkono kampeni hiyo.



Hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi wa kitaifa na kikanda pamoja na wadau wa sekta ya afya, ambapo mshikamano mkubwa ulionekana katika jitihada za kuhakikisha watoto wanaozaliwa njiti wanapata huduma bora na salama.


Akizungumza baada ya harambee hiyo, Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mbunge wa Babati Vijijini, Mhe. Daniel Baran Sillo, aliyekuwa mgeni rasmi, alisema mafanikio hayo yanaonesha moyo wa uzalendo na mshikamano wa Watanzania katika kusaidia sekta ya afya.


Alisema lengo la kampeni hiyo ni kufikisha zaidi ya Shilingi bilioni 1.5, huku akiwakaribisha Watanzania kushiriki Manyara Tanzanite Marathon itakayofanyika Agosti 22, 2026 mkoani Manyara.





“Tunawashukuru wadau wote waliojitokeza na kuchangia. Kila mchango una maana kubwa katika kuokoa maisha ya watoto wetu. Tunataka kuhakikisha hospitali zetu zinakuwa na vifaa vinavyohitajika kuwahudumia watoto njiti kwa kiwango cha kisasa,” alisema Mhe. Sillo.


Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Sendiga, alisema kampeni hiyo imeibuka kuwa jukwaa muhimu la kuunganisha nguvu za Serikali na sekta binafsi katika kuboresha huduma za afya kwa mama na mtoto.


Aliwataka wananchi, taasisi na wadau mbalimbali kuendelea kujitokeza kuchangia ili kufanikisha lengo lililowekwa, akisisitiza kuwa uwekezaji katika afya ya watoto ni uwekezaji katika mustakabali wa taifa.







“Kila mtoto ana haki ya kuishi. Tunapowekeza katika vifaa tiba na huduma za watoto njiti, tunaokoa familia, tunaimarisha jamii na tunajenga taifa lenye nguvu,” alisema Mhe. Sendiga.


Naye Mganga Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Dkt. Andrew Method, alieleza kuwa mkoa huo unakabiliwa na changamoto kubwa ya watoto wanaozaliwa njiti, ambapo kati ya watoto 3,000 hadi 3,200 huzaliwa njiti kila mwaka.


Alisema idadi hiyo inaweka shinikizo kubwa katika vituo vya kutolea huduma za afya, hasa katika upatikanaji wa mashine za kusaidia watoto kupumua, incubators, vifaa vya ufuatiliaji wa afya za watoto wachanga na miundombinu ya huduma maalumu.



“Watoto njiti wanahitaji uangalizi wa karibu na vifaa maalumu. Bila uwekezaji wa kutosha, tunakuwa katika hatari ya kupoteza maisha ambayo yangeweza kuokolewa,” alisema Dkt. Method.


Kwa mujibu wa wataalamu wa afya, kuzaliwa njiti ni miongoni mwa sababu kuu zinazochangia vifo vya watoto wachanga duniani, na huduma bora katika saa na siku za mwanzo baada ya kuzaliwa ndiyo huamua kwa kiasi kikubwa uwezekano wa mtoto kuendelea kuishi.


Wadau waliohudhuria hafla hiyo walieleza kuwa kampeni hiyo imeonesha mfano wa namna matukio ya michezo yanaweza kutumika kama nyenzo ya kuchangisha fedha kwa ajili ya miradi ya kijamii na maendeleo.



Mbio za Manyara Tanzanite Marathon zimekuwa zikikua kwa kasi na sasa zinatajwa kuwa moja ya matukio makubwa ya michezo na hisani nchini Tanzania, yakilenga kuhamasisha afya, utalii na maendeleo ya jamii kwa wakati mmoja.


Waandaaji wa marathon hiyo walisema fedha zitakazopatikana zitaelekezwa katika ununuzi wa vifaa tiba, uboreshaji wa huduma za watoto wachanga na kuimarisha uwezo wa hospitali za Mkoa wa Manyara kuhudumia watoto njiti kwa ufanisi zaidi.


Kampeni hiyo pia inaunga mkono juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambazo zimekuwa zikilenga kuboresha huduma za afya, kupunguza vifo vya mama na mtoto, kuimarisha ustawi wa jamii na kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora katika maeneo yote ya nchi.




Waandaaji wameendelea kutoa wito kwa Watanzania kushiriki mbio hizo au kuchangia kupitia akaunti maalumu za kampeni, wakisisitiza kuwa kila mchango ni hatua muhimu katika kuokoa maisha ya mtoto mmoja au zaidi.


Michango inaendelea kupokelewa kupitia CRDB Lipa Namba 113069180 na CRDB Account No. 10401215064 (Manyara Tanzania Marathon).


Kwa mafanikio yaliyopatikana katika usiku huo wa kihistoria, Mkoa wa Manyara umeonesha kuwa mshikamano wa jamii unaweza kuwa nguvu kubwa ya kuokoa maisha, huku kampeni ya Hatua Moja Okoa Maisha ya Mtoto ikiendelea kuwa mwanga wa matumaini kwa maelfu ya watoto wanaozaliwa njiti kila mwaka nchini Tanzania.