Chuo cha Uhasibu Arusha (IAA) kimeendelea kutoa wahitimu mahiri wenye ujuzi wa kitaaluma, maadili na uwezo wa kiuongozi, wenye uwezo wa kuleta mabadiliko chanya katika taasisi na jamii wanazozihudumia.

Akizungumza Februari 6, 2026, wakati wa mahafali ya 27 ya wahitimu wa Shahada ya Uzamili ya mwaka 2025 yaliyofanyika katika Ukumbi wa Ngurdoto mkoani Arusha, Mkuu wa Chuo Profesa Eliamani Sedoyeka, amesema maboresho yanayoendelea katika huduma za ufundishaji na ujifunzaji yameiwezesha IAA kuandaa wataalamu wanaokidhi mahitaji ya taifa na soko la ajira.

Prof. Sedoyeka amewasisitiza wahitimu kuzingatia misingi ya uwajibikaji, uadilifu na uzalendo wanapotekeleza majukumu yao huku akiwataka kutumia ujuzi wa kisayansi, tafiti na maadili katika kufanya maamuzi katika maeneo watakayoaminiwa kuyahudumia.

“Mmeandaliwa kuwa viongozi wenye maarifa, maadili na uwezo wa kuongoza mabadiliko chanya katika taasisi na jamii mnazozihudumia, Ni wajibu wenu kuzingatia uwajibikaji, uadilifu na uzalendo katika kila jukumu mtakalotekeleza,” amesema Prof. Sedoyeka.

Akizungumzia mchango wa tafiti zilizofanywa na wahitimu, Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Chuo, Dkt. Mwamini Tulli, amesema tafiti hizo ni msingi muhimu katika kuongeza ufanisi wa utendaji kazi, kuboresha utoaji wa huduma na kuchochea ukuaji wa uchumi endelevu.

Dkt. Tulli amesisitiza kuwa matokeo ya tafiti zilizofanywa na wahitimu hazipaswi kubaki kwenye makabati bali yatumike kutatua changamoto halisi zinazolikabili taifa na taasisi zake.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula, ameupongeza uongozi wa IAA kwa kuendelea kuboresha miundombinu ya kisasa inayoendana na mabadiliko ya teknolojia duniani, hali iliyowawezesha kuzalisha wahitimu wenye uwezo wa kushindana katika soko la ajira ndani na nje ya nchi.

Naibu Waziri amethibitisha kuwa hatua hiyo ni ishara ya dhamira ya huo katika kuhakikisha mifumo ya ufundishaji na ujifunzaji inaendana na mahitaji ya dunia ya sasa na ya baadaye.












Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar(Mb), amekipongeza Chuo cha Uhasibu Arusha (IAA) kwa kufanya mageuzi ya kidigitali, ufanyaji wa tafiti, maendeleo pamoja na mipango na mikakati ya kuboresha na kuongeza ufanisi kwenye utoaji wa mafunzo, na ushauri wa kitaalam, ambazo ni miongoni mwa vichocheo vya kufikia Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2025-2050.


Hayo yasemwa na Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb), wakati akihutubia kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), katika Mahafali ya 27 (Duru ya Pili) ya Chuo hicho, yaliyofanyika katika Hoteli ya Ngurdoto, mkoani Arusha.

Mhe. Luswetula alisema kuwa mchango wa IAA katika uchumi wa Taifa ni mkubwa kwa kuwa kimeendelea kuzalisha wataalam wa fedha, uhasibu, uchumi, kodi, utalii, usimamizi biashara, benki, ununuzi na ugavi, masoko, bima, TEHAMA na nyingine nyingi.

 Alisema kuwa Wataalam hao wamekuwa mhimili muhimu katika ukusanyaji wa mapato ya Serikali, usimamizi wa fedha za umma, sekta binafsi, taasisi za kifedha na miradi ya maendeleo.

Aliongeza kuwa Kupitia wahitimu wake, Chuo kimechangia kwa vitendo katika kukuza uwajibikaji, uwazi na nidhamu ya kifedha nchini.

“Niwapongeze IAA mmeendelea kudhihirisha umahiri mkubwa katika kuandaa rasilimali watu mahiri, wanaokidhi mahitaji ya soko la ajira na kuchangia kikamilifu katika maendeleo ya uchumi wa Taifa letu” alisema Mhe. Luswetula.

Aidha, Mhe. Luswetula alikisifu Chuo cha IAA kwa kuwa kinara katika kuboresha mifumo ya ufundishaji na ujifunzaji kupitia matumizi ya teknolojia za kisasa sambamba na kuimarisha tafiti na ushauri wa kitaalam.

“Mageuzi ya kidigitali ni kichocheo muhimu cha maendeleo hususan katika kuboresha ukuaji wa uchumi na kuimarisha huduma za jamii ikiwemo elimu. Serikali inatambua na kupongeza juhudi za IAA katika kuwekeza kwenye mifumo ya kidigitali na katika kuimarisha ufanisi wa utoaji wa elimu kwa njia bunifu,” aliongeza Mhe. Luswetula.

Mhe. Luswetula alitumia fursa hiyo pia kuwasihi wanafunzi na wahitimu wa Shahada ya Uzamili kutumia tafiti zao kutoa majibu ya changamoto halisi zinazolikabili Taifa kama vile usimamizi wa fedha za umma, ukuaji wa uchumi jumuishi, ajira, ubunifu na matumizi sahihi ya teknolojia.

“Tafiti zenu ziwe chachu ya sera bora, maamuzi sahihi na maendeleo endelevu kwa wananchi na Taifa letu,” alisisitiza.

Aliongeza kuwa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, itaendelea kuweka mazingira wezeshi ya ukuaji wa uchumi na maendeleo jumuishi yanayomgusa kila Mtanzania, huku sekta za fedha, uhasibu, uchumi, benki, usimamizi wa biashara na miradi zikiwa nguzo muhimu katika kuhakikisha rasilimali za Taifa zinakusanywa, zinapangwa, zinatumika na zinadhibitiwa kwa ufanisi, uwazi na uwajibikaji.

Aidha, alisema kuwa Serikali kupitia Wizara ya Fedha, itaendelea kuhimiza na kuunga mkono Vyuo vya Elimu ya Juu vinavyoendana na dira ya Taifa ya kujenga uchumi wa kisasa unaotegemea maarifa na ujuzi.

“Wizara itaendelea kushirikiana na vyuo hivi katika kuweka mazingira wezeshi ya kifedha na kisera yatakayowezesha kuimarishwa kwa kozi za kimkakati, tafiti zenye tija, na maandalizi ya wataalam wanaokidhi viwango vya kitaifa na kimataifa.” Alisema Mhe. Luswetula

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Chuo cha Uhasibu Arusha (IAA), Dkt. Mwamini Tulli, alisema kuwa Chuo hicho kimejipanga kuendelea kutoa wahitimu mahiri kwa kuwekeza katika rasilimali watu, hususani wahadhiri wenye sifa, uzoefu wa kitaaluma na kitaalam, pamoja na kuimarisha mbinu shirikishi za ufundishaji na ujifunzaji.

Alisema kuwa IAA imejipambanua kama Taasisi inayozalisha wahitimu mahiri, wabunifu, na wenye uwezo wa kuchambua na kutatua changamoto za jamii inayowazunguka, maeneo wanayofanyia kazi zao na Taifa kwa ujumla.

Wahitimu wa Shahada ya Uzamili wa IAA wanatambulika kwa ubora wa taaluma, maadili, na weledi wa kitaaluma katika sekta mbalimbali.

“Ubora huu unatokana na mitaala inayozingatia mahitaji ya sasa ya soko la ajira, maendeleo ya teknolojia, na mabadiliko ya kiuchumi na kijamii. IAA imeendelea kuhakikisha kuwa programu zake za Uzamili zinawajengea wanafunzi ujuzi wa kina, fikra pevu, na uwezo wa uongozi” alisema Dkt. Tulli.

Aliongeza kuwa Baraza la Uongozi wa Chuo litaendelea kusimamia kwa karibu mipango na kimkakati ya Chuo, ili kuhakikisha IAA inaendelea kuwa Taasisi kinara katika elimu ya juu, tafiti, na ushauri wa kitaalamu nchini na nje ya nchi.

Naye Mkuu wa Chuo cha Uhasibu Arusha (IAA), Prof. Eliamani Sedoyeka, alisema kuwa kwa kutambua mabadiliko ya kasi katika mahitaji ya soko la ajira na uongozi wa kitaifa, Chuo hicho kinaendelea kuimarisha huduma za ufundishaji na ujifunzaji kwa kuboresha mitaala, mbinu za kufundishia, na mifumo ya tathmini ili kuendana na sera, mikakati, na dira ya maendeleo ya Taifa 2025-2050.

Alisema kuwa IAA imeweka mkakati mahususi wa kuwawezesha wahadhiri wengi zaidi kusomea Shahada ya Uzamivu ndani na nje ya nchi, ili kukidhi ongezeko la idadi ya wanafunzi wa Uzamili linaloendelea kushuhudiwa kila mwaka ambapo katika mwaka wa masomo 2025/2026 jumla ya wahadhiri 115 wamepelekwa kusoma Shahada ya Uzamivu (PhD) katika vyuo mbalimbali nchini na nje ya nchi.

“Mkakati huu unalenga kuhakikisha uwiano sahihi kati ya wanafunzi na wahadhiri, kuimarisha usimamizi wa tafiti, na kuongeza uwezo wa Chuo katika uzalishaji wa wataalam wanaokidhi mahitaji ya kitaifa na kimataifa” alisema Prof. Sedoyeka.

Mahafali ya 27 (Duru ya Pili) ya IAA, imewahusisha jumla ya wahitimu 2,250 kati yao wanaume wakiwa 1,369 sawa na asilimia 60.8 na wanawake 881 sawa na asilimia 39.2 ambao wametunukiwa Shahada ya Uzamili katika fani kumi na tano (15) .

Fani hizo ni (Accountancy), Uhasibu na Fedha (Accounting and Finance), Fedha na Benki (Finance and Banking), Fedha na Uwekezaji (Finance and Investment), Usimamizi wa Miradi (Project Planning Management), Usimamizi wa Taarifa (Information Management), Uchumi na Fedha (Economics and Finance), Usimamizi wa Elimu (Education Management), Usimamizi wa Rasilimali watu (Human Resource Management) na Amani na Usalama (Peace and Security ). Fani nyingine ni Usimamizi wa Biashara (Master of Business Administration in Corporate Management), Usimamizi wa Biashara katika Teknolojia ya Habari (MBA-Information Technology), Usimamizi wa Biashara katika Uandaaji na Utekelezaji wa Sera (MBA-Policy Development and Execution), Usimamizi wa Biashara katika Uongozi (MBA-Leadership and Governance), Usimamizi wa Biashara katika Ununuzi na Ugavi (MBA-Procurement and Supply Chain Management).














Mwenyekiti wa halmashauri ya Mji Handeni, Amiri Mwaliko,akizungumza katika mkutano wa kupokea na kujadili taarifa za kata za Halmashauri ya Mji Handeni uliofanyika leo Februari 7, 2026.

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Handeni, Maryam Ukwaju,akizungumza katika mkutano wa kupokea na kujadili taarifa za kata za Halmashauri ya Mji Handeni uliofanyika leo Februari 7, 2026.

Naibu Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Reuben Kwagilwa,akiteta jambo na Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese,wakati wa  mkutano wa kupokea na kujadili taarifa za kata za Halmashauri ya Mji Handeni uliofanyika leo Februari 7, 2026.

Sehemu ya Madiwani wakifuatilia mkutano wa kupokea na kujadili taarifa za kata za Halmashauri ya Mji Handeni uliofanyika leo Februari 7, 2026.

Na Augusta Njoji

MWENYEKITI wa Halmashauri ya Mji Handeni, Mhe. Amiri Mwaliko, amempongeza Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan, kwa kutoa kibali cha ajira kilichowezesha kupatikana kwa watumishi 82 wa kada mbalimbali na hivyo kupunguza uhaba wa watumishi katika halmashauri hiyo.

Akifungua mkutano wa kupokea na kujadili taarifa za kata wa Halmashauri hiyo uliofanyika Februari 7, 2026 mjini hapa, Mhe. Mwaliko amesema serikali imeendelea kuchukua hatua za kutatua changamoto ya upungufu wa watumishi.

“Tunaishukuru serikali kwa kuendelea kutatua changamoto ya watumishi. Tunafurahia hatua hii kwa kuwa lengo la serikali ni kuondoa uhaba wa watumishi na kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi,” amesema.

Aidha, amempongeza Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese, kwa kuhakikisha wilaya hiyo inaendelea kudumisha amani na utulivu.

Mhe. Mwaliko amewataka viongozi na watumishi kushirikiana katika kujenga halmashauri yenye mshikamano na kutatua changamoto zinazojitokeza.

Ameongeza kuwa ni muhimu kusimama pamoja na watumishi na kushughulikia changamoto kwa njia ya mazungumzo ili kujenga timu imara ya utendaji kwa maendeleo ya halmashauri.

Kadhalika, amesisitiza kuendelea kuchukuliwa hatua za kudhibiti utoro wa wanafunzi kwa kushirikiana na madiwani wa maeneo husika.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Handeni, Maryam Ukwaju, amesema katika mwaka wa fedha 2025/26 serikali imeajiri watumishi 82 wakiwemo walimu wa shule za msingi na sekondari pamoja na wauguzi.

Amesema changamoto ya upungufu wa watumishi inaendelea kupatiwa ufumbuzi kadri serikali inavyoendelea kutoa ajira, huku halmashauri ikiendelea kutenga bajeti kupitia mapato ya ndani kwa ajili ya kuchangia maendeleo ya kata, ikiwemo ununuzi wa madawati.

Naibu Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Reuben Kwagilwa,akizungumza katika mkutano wa kupokea na kujadili taarifa za kata za Halmashauri ya Mji Handeni uliofanyika leo Februari 7, 2026.

Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese,akizungumza katika mkutano wa kupokea na kujadili taarifa za kata za Halmashauri ya Mji Handeni uliofanyika leo Februari 7, 2026.

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Handeni, Maryam Ukwaju,akizungumza katika mkutano wa kupokea na kujadili taarifa za kata za Halmashauri ya Mji Handeni uliofanyika leo Februari 7, 2026.

Mwenyekiti wa halmashauri ya Mji Handeni, Amiri Mwaliko,akizungumza katika mkutano wa kupokea na kujadili taarifa za kata za Halmashauri ya Mji Handeni uliofanyika leo Februari 7, 2026.

Naibu Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Reuben Kwagilwa,akiteta jambo na Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese,wakati wa  mkutano wa kupokea na kujadili taarifa za kata za Halmashauri ya Mji Handeni uliofanyika leo Februari 7, 2026.

Sehemu ya washiriki wakifatilia hotuba ya Naibu Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Reuben Kwagilwa (hayupo pichani) wakati wa mkutano wa kupokea na kujadili taarifa za kata za Halmashauri ya Mji Handeni uliofanyika leo Februari 7, 2026.

Na Augusta Njoji

Naibu Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Reuben Kwagilwa, ameelekeza taasisi za serikali zinazohudumia wananchi wilayani Handeni kuwasilisha taarifa za utekelezaji wa majukumu yao katika Baraza la Madiwani ili kuongeza uwazi na kuwafanya wananchi kufahamu kazi zinazofanywa na serikali.

Akizungumza katika mkutano wa kupokea na kujadili taarifa za kata za Halmashauri ya Mji Handeni uliofanyika Februari 7, 2026, Mhe. Kwagilwa amesema ni muhimu kwa wakuu wa taasisi za serikali kuhudhuria vikao vya Baraza la Madiwani na kuwasilisha taarifa zao.

Amezitaja baadhi ya taasisi hizo kuwa ni pamoja na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA), Mamlaka ya Maji pamoja na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), akisisitiza kuwa taasisi hizo zinawajibika moja kwa moja kwa wananchi.

Pamoja na hayo, amempongeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Handeni, Maryam Ukwaju, pamoja na wataalamu wa halmashauri hiyo kwa mafanikio yaliyopatikana katika utekelezaji wa ilani ya uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) iliyopita na kuendelea kutekeleza ilani ya sasa.

Naye Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, Mhe. Amiri Mwaliko, amempongeza Naibu Waziri Kwagilwa kwa kuaminiwa na Rais Samia Suluhu Hassan kushika nafasi hiyo, akisema anaamini atatekeleza vyema majukumu yake katika kuisaidia TAMISEMI.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe.Salum Nyamwese ameahidi kuwapa ushirikiano Madiwani katika utekelezaji wa majukumu yao.

 


Na OWM- TAMISEMI, Dar es Salaam

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za  Mitaa (OWM- TAMISEMI), Prof. Riziki Shemdoe ameridhishwa na hatua iliyofikiwa ya maandalizi ya  ufunguzi Soko Kuu la Kariakoo lililopo Ilala Jijini Dar es Salaam.

Prof. Shemdoe ameyasema hayo leo Februari 07, 2026 alipotembelea soko hilo ili kujiridhisha na maandalizi ya hafla ya ufunguzi wa soko hilo litakalofunguliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Kesho Februari 08, 2026.

Prof. Shemdoe amemshukuru Mhe. Rais kwa uwekezaji uliofanyika katika soko hilo lililoungua mwaka 2021 ambalo limefanyiwa ukarabati na kujengwa soko lingine jipya lenye ghorofa sita (6)  katika eneo hilo.

"Ninamshukuru Mhe. Rais kwa Shilingi Bilioni 28 aliyoridhia itumike kwa ajili ya ukarabati na ujenzi huu, hii ni hatua kubwa sana ambayo tunapaswa kujivunia," amefafanua Prof. Shemdoe.

Soko kuu la Kariakoo liliungua Julai 10, 2021 na Mhe Rais alipotembelea soko hilo  kuwapa pole wafanyabiashara waliopatwa na kadhia hiyo, aliahidi   kuwa atafanya ukarabati na kuliboresha zaidi, ahadi ambayo ameitekeleza kwa vitendo.

Prof .Shemdoe amewasihi wananchi na wafanyabiashara wa Jiji la Dar es Salaam kujitokeza kwa wingi katika uzinduzi wa soko hilo huku akiwapongeza  viongozi wa mkoa wa Dar es Salaam, Jiji la Dar es Salaam pamoja na uongozi wa Shirika la Masoko ya Kariakoo kwa namna walivyoshirikiana na kufanikisha maandalizi hayo kwa kiwango cha juu.

Katika ziara hiyo Prof. Shemdoe ameambatana na Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, TAMISEMI,  Bw. Adolf Ndunguru, Naibu Katibu Mkuu-TAMISEMI, Bw. Sospeter Mtwale, Katibu Tawala,  Bw. Abdul Mhinte, Mkuu wa Wilaya ya Ilala Mhe. Edward Mpogolo, Mkurugenzi wa Jiji la Dar es Salaam  Bw. Elihuruma Mabehe na viongozi waandamizi wa Wizara hiyo.

 

Na.Mwandishi Wetu-Morogoro📍

Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Mhe. Adam Malima, tarehe 6 Februari, 2026 amewapokea wakandarasi wawili kutoka Wakala wa Nishati Vijijini (REA); watakaotekeleza Mradi mkubwa wa kusambaza umeme katika vitongoji 570 vya mkoa huo; ikielezwa kuwa Mradi huo una thamani ya shilingi bilioni 91.

Wakandarasi hao ni kampuni ya Sagemcom Energy & Telecom SAS (Italia) na China Railway No. 4 Engineering Group Co. Ltd (China) ambao watasambaza umeme katika vitongoji 570 katika Mradi huo mkubwa kwa gharama ya shilingi bilioni 91.

Akizungumza wakati wa hafla ya kuwatambulisha wakandarasi hao, Mhe. Malima alisema Mradi huo ni utekelezaji wa dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kuhakikisha Watanzania wote wanapata huduma ya umeme wa uhakika hususan maeneo ya vijijini.

Mhe. Malima alisema kuwa Serikali kupitia REA imeleta maendeleo makubwa kwenye Sekta ya Nishati hususan kwenye usambazaji wa umeme vijijini katika kipindi cha miaka 15; akitolea mfano wakati alipokuwa Naibu Waziri wa Nishati mwaka 2008 ambapo bajeti ya REA ilikuwa shilingi bilioni tano pekee.

“Leo hii baada ya miaka 15 mkoa wa Morogoro pekee yake, unatekeleza Miradi ya umeme yenye thamani ya shilingi bilioni 91. Hii inaonesha dhamira ya dhati ya Serikali katika kuhakikisha Wananchi wa vijijini wanapata umeme kwa maendeleo yao ya kiuchumi na kijamii.” alisema Mhe. Malima.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Umeme Vijijini, Mhandisi, Thomas Mmbaga kutoka REA alisema wamewatambulisha rasmi wakandarasi wawili watakaofanya kazi ya kusambaza umeme kwenye vitongoji 570 kwa mgawo wa kampuni ya Sagemcom Energy ambayo itasambaza umeme katika vitongoji 325 na kuunganisha wateja wa awali 11,399 katika wilaya ya Mvomero; Morogoro Vijijini na Gairo kwa gharama ya shilingi bilioni 48.4.

Mkandarasi wa pili ni kampuni ya China Railway No. 4 ambayo itasambaza umeme kwenye vitongoji 245 na kuunganisha wateja wa awali 8,649 katika wilaya ya Kilosa; Malinyi; Kilombero na Ulanga kwa gharama ya shilingi bilioni 42.5 ambapo kipindi cha utekelezaji kwa Mradi huo katika mkoa wa Morogoro ni miaka mitatu.

Naye Meneja wa TANESCO mkoa wa Morogoro, Mhandisi, Zawadi Macha alisema Shirika hilo limejipanga kikamilifu kusimamia utekelezaji wa Mradi huo kwa karibu ili kuhakikisha unatekelezwa kwa ubora unaotakiwa na kwa kuzingatia viwango vilivyowekwa.

Kwa upande wake, Meneja wa Mradi wa Kampuni ya Sagemcom Energy, Bwana Calvin Manase alisema kampuni hiyo ina uzoefu mkubwa katika utekelezaji wa miradi ya umeme na imejipanga kuhakikisha mradi unakamilika ndani ya miezi 34 licha mkataba kuwa miezi 36.

Manase aliongeza kuwa kampuni hiyo itatoa ajira kwa Wananchi (Wazawa) wa maeneo husika ili wanufaike moja kwa moja wakati wa utekelezaji wa Mradi huo. Aidha, ameipongeza REA kwa mpango wake wa kulipa malipo ya awali kwa wakandarasi akisema hatua hiyo itasaidia kupunguza changamoto ya upatikanaji wa vifaa vya ujenzi wa Mradi huo.