📌 Vijana maeneo ya mradi wa umeme kwenye vitongoji kupewa kipaumbele kwenye ajira

Bodi ya Nishati Vijijini (REB) imetoa wito kwa wananchi kuwa walinzi wa kwanza wa miundombinu ya miradi ya kufikisha umeme vijijini inayotekelezwa na serikali, huku ikieleza kusikitishwa na matukio ya wizi wa vifaa vya umeme ikiwemo waya za mashine umba (transfoma) katika baadhi ya maeneo.

Wito huo umetolewa leo Mei 11, 2026 Mkoani Manyara na Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini, Mhe. Balozi Meja Jenerali (Mstaafu), Jacob Kingu wakati akihitimisha ziara ya Bodi hiyo katika mikoa ya Tanga, Kilimanjaro, Arusha na Manyara ya kukagua utekelezaji wa miradi ya Wakala wa Nishati Vijijini (REA) ikiwa ni miradi ya nishati safi ya kupikia pamoja na miradi ya kusambaza umeme katika vitongoji.

Balozi Kingu amesema serikali imetumia fedha nyingi kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya umeme, hivyo ni jukumu la kila mwananchi kushiriki kikamilifu katika kulinda miundombinu hiyo dhidi ya vitendo vya hujuma na wizi vinavyoweza kuchelewesha maendeleo ya wananchi.

Katika ziara hiyo mkoani Manyara, Bodi ya REB imefanya kikao na Wakandarasi wanaotekeleza mradi wa kupeleka umeme katika vitongoji ambao ni kampuni ya Sagemcom Energy & Telecom Tanzania pamoja na China Railway Seventh Group.

Awali akitoa taarifa ya utekelezaji wa miradi hiyo, Msimamizi wa Miradi wa REA Mkoa wa Manyara, Mhandisi Geofrey Mkeni, amesema serikali kupitia REA imetenga zaidi ya shilingi bilioni 45.8 kwa ajili ya miradi ya kusambaza umeme katika vitongoji 267 vya mkoa wa Manyara.

Mhandisi Mkeni amesema miradi hiyo inalenga kuongeza upatikanaji wa huduma ya umeme kwa wananchi wa vijijini ili kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

Pia ametoa wito kwa wananchi wanaoishi katika maeneo yanayofikiwa na miradi hiyo kuanza kufanya maandalizi ya miundombinu ya ndani ya nyumba ikiwemo wiring ili wawe tayari kuunganishiwa huduma ya umeme mara baada ya miradi hiyo kukamilika.

Kwa upande wao, wakandarasi wanaotekeleza miradi hiyo wameahidi kuhakikisha kazi zinakamilika kwa wakati huku wananchi wakinufaika kupitia ajira zinazotokana na utekelezaji wa miradi hiyo.

Akizungumza kwa niaba ya kampuni ya Sagemcom Energy & Telecom Tanzania, Afisa Mahusiano ya Jamii na Mazingira, Oliver Charles, amesema miradi hiyo imefungua fursa mbalimbali za ajira kwa vijana wanaoishi katika maeneo yenye miradi ili wawe sehemu ya maendeleo yanayoletwa na serikali.

Naye Mhandisi wa Miradi kutoka kampuni ya China Railway Seventh Group, Estheria Fumbuka, amesema kampuni hiyo itaendelea kufanya kazi kwa bidii kuhakikisha miradi yote inakamilika kwa wakati ili malengo ya serikali ya kuwafikishia wananchi huduma ya umeme vijijini yaweze kutimia.

 


Serikali kupitia Bohari ya Dawa (MSD) itaendelea kununua dawa zinazozalishwa na wawekezaji wa ndani ili kuimarisha uzalishaji wa ndani wa bidhaa za afya na kupunguza utegemezi wa bidhaa kutoka nje ya nchi.

Hayo yamesemwa Waziri wa Afya, Mohammed Mchengerwa leo Mei 11 2026 akiwasilisha Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Afya kwa mwaka wa fedha 2026/27 Bungeni, Jijini Dodoma.

“Serikali imejipanga kuhakikisha MSD inanunua kwanza dawa zinazozalishwa ndani ya nchi zilizokidhi viwango vya Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA) kabla ya kwenda kununua kutoka nje ya nchi, hatua inalenga kukuza viwanda vya ndani, kuongeza ajira na kuimarisha uchumi wa Taifa” amesema Waziri Mchengerwa

Amesema Serikali itaendelea kuweka mazingira rafiki na wezeshi kwa wawekezaji wa ndani na nje ya nchi, ikiwemo kuboresha upatikanaji wa ardhi, miundombinu muhimu pamoja na kuratibu uwekezaji katika sekta ya dawa na bidhaa za afya ili kuvutia uwekezaji zaidi nchini.

Waziri Mchengerwa amesema Serikali imeendelea kuimarisha upatikanaji wa bidhaa za afya nchini kwa kutoa Shilingi trilioni 1.4 kupitia MSD ili kuhakikisha wananchi wanapata dawa na bidhaa muhimu za afya kwa wakati.

“Upatikanaji wa bidhaa muhimu za afya umeongezeka kutoka asilimia 58 mwaka 2021/22 hadi asilimia 88 mwezi Machi 2026” amesema Waziri Mchengerwa.

Amesema kuwa Wizara ya Afya itaendelea kuhamasisha wawekezaji wa ndani na nje ya nchi pamoja na kuwawekea mazingira rafiki na wezeshi, ikiwemo upatikanaji wa ardhi na miundombinu muhimu, ili kuwavutia kuwekeza katika ujenzi wa viwanda vya bidhaa za afya na kupunguza utegemezi.

Waziri Mchengerwa amesisitiza kuwa dhamira ya Serikali ni kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma bora za afya, dawa salama na huduma zenye ubora bila kuachwa nyuma.

 -Wanufaika 463,228 waanza kupata huduma za matibabu.



Na Grace Michael, NHIF-Dodoma

Serikali imeanza rasmi utekelezaji wa Mpango wa Bima ya Afya kwa Wote kwa kaya zisizo na uwezo kwa kutoa Shilingi bilioni 48.8 kwa ajili ya kuwawezesha wananchi wa makundi maalum kupata huduma za afya kwa uhakika.

Kupitia utekelezaji huo, jumla ya kaya 172,297 tayari zimefikiwa na kuingizwa kwenye mpango huo, huku wanufaika 463,228 wakianza kupata huduma mbalimbali za matibabu katika vituo vilivyosajiliwa nchini.

Akiwasilisha Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Afya Fungu 52 kwa mwaka 2026/27 Waziri wa Afya Mhe. Omary Mchengerwa amesema kuwa, utekelezaji huu unaonesha dhamira ya Serikali ya kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma bora za afya bila kujali hali yake ya kiuchumi, ikiwa ni sehemu ya safari ya kuelekea huduma jumuishi za afya kwa wananchi wote.

Katika kuimarisha sekta ya afya sambamba na utekelezaji wa mpango huo, mabaraza na bodi za kitaaluma yameendelea kusimamia ubora wa huduma kwa kusajili wataalam wa afya 14,310, hatua inayoongeza nguvu kazi muhimu kwa utoaji wa huduma nchini.

Amesema kuwa kuhusu upatikanaji wa huduma za matibabu, jumla ya maduka ya dawa 330 yamesajiliwa pamoja na watarajali 3,004, huku vituo vya kutolea huduma za afya 3,643 vikisajiliwa ili kuongeza upatikanaji wa huduma karibu na wananchi.

Katika kuhakikisha taaluma na maadili yanaendelea kuzingatiwa hususan wakati huu wa kuhudumia wananchi wengi zaidi kupitia mfumo wa Bima ya Afya, vituo binafsi vya afya 654 vimekaguliwa ili kuhakikisha vinakidhi viwango na kutoa huduma salama kwa wananchi.

Mafanikio hayo yanaakisi hatua kubwa ya Serikali katika kujenga mfumo imara wa afya unaojali usawa, ubora na upatikanaji wa huduma kwa wote, huku Bima ya Afya kwa Wote ikiendelea kuwa nguzo muhimu ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

 Na Hassan Kimweri, WAF - Dodoma


Sekta ya afya nchini imepata mafanikio makubwa katika kipindi cha awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan yaliyoongeza upatikanaji wa huduma za afya kwa wananchi kupitia ujenzi wa miundombinu, ununuzi wa vifaa tiba, uoatikanaji wa dawa pamoja na huduma za kibingwa na za dharura nchini.

Waziri wa Afya Mhe. Mohamed Mchengerwa amesema hayo leo Mei 11, 2026 wakati akiwasilisha Bajeti ya Wizara ya Afya kwa mwaka wa fedha 2026/27 katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya Spika wa Bunge Mhe. Mussa Azan Zungu.

"Eneo la vituo vya kutolea huduma za afya vimeongezeka kutoka elfu 10,153 mwaka 2021/22 hadi elfu 13,683 kufikia Machi 2026, sawa na ongezeko la vituo 3,530, Zahanati zimeongezeka kutoka elfu 7,189 hadi elfu 8,706 huku hospitali zikiongezeka kutoka mia 404 hadi mia 475 mwaka 2026," amesema Waziri Mchengerwa

Aidha, Waziri Mchengerwa amesema Serikali imeongeza majengo mapya katika hospitali mbalimbali zikiwemo Hospitali ya Muhimbili, KCMC, BMH, Bugando, Mirembe, pamoja na Kibong'oto huku ikiwa imejenga hospitali mpya 10 za rufaa za mikoa, kukarabati hospitali kongwe 50, kukamilisha maboma 980 ya zahanati na kujenga vituo vya afya 390.

Amesema, katika huduma za afya ya uzazi, mama na mtoto, Serikali imeongeza wodi za watoto wachanga kutoka 80 hadi 438 pamoja na vituo vya upasuaji wa dharura kutoka 445 hadi 630 ambayo ni mafanikio yaliyochangia kupungua kwa vifo vitokanavyo na uzazi kutoka vifo 556 mwaka 2016 hadi vifo 104 mwaka 2022 kwa kila vizazi hai 100,000.

"Katika huduma za uchunguzi na matibabu ya kibingwa, Serikali imenunua na kusimika vifaa tiba vyenye thamani ya Shilingi bilioni 241.6 ambapo mashine za MRI zimeongezeka kutoka 7 hadi 13, CT Scan kutoka 12 hadi 45 pamoja na Digital X-ray kutoka 147 hadi 559," amesema Waziri Mchengerea

Kwa upande wa chanjo, amesema watoto waliopata chanjo ya Pentavalent dozi ya tatu wameongezeka kutoka watoto milioni 2,093,412 hadi milioni 3,186,979 huku kiwango cha chanjo kikiongezeka kutoka asilimia 93 hadi 96, juu ya lengo la kimataifa la asilimia 90.

"Upatikanaji wa dawa na bidhaa za afya umeimarika, Serikali imetoa Shilingi trilioni 1.4 kwa ajili ya ununuzi wa dawa na vifaa tiba, viwanda vipya 11 vya dawa na vifaa tiba vimeanzishwa huku 'Tanzania Pharmaceutical Industries kikifufuliwa kwa ajili ya uzalishaji wa dawa za VVU nchini," amesema Waziri Mchengerea

 Waziri wa Afya, Omary Mchenjgerwa amesema Serikali imeendelea kuimarisha mapambano dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza kwa kuongeza huduma za matibabu, kinga na elimu kwa jamii, hatua iliyochangia kuongezeka kwa kliniki za kisukari na shinikizo la damu nchini.

Akizungumza leo Mei 11, 2026 bungeni jijini Dodoma wakati akiwasilisha hotuba ya makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Afya kwa mwaka wa fedha 2026/2027, Mchenjgerwa amesema wizara imeendelea kuimarisha uratibu na utekelezaji wa afua za magonjwa ya kisukari, shinikizo la damu pamoja na magonjwa sugu ya mfumo wa upumuaji.

Amesema katika kipindi cha Julai 2025 hadi Machi 2026, Serikali imeanzisha kliniki mpya 130 za huduma za kisukari na shinikizo la damu, na kufanya idadi ya kliniki hizo kufikia 168 kutoka kliniki 38 zilizokuwepo katika kipindi kama hicho mwaka 2025.

Kwa mujibu wa Waziri huyo, kliniki hizo zimepatiwa dawa muhimu, vifaa tiba pamoja na mafunzo kwa watumishi wa afya ili kuboresha upatikanaji na ubora wa huduma kwa wananchi wenye magonjwa yasiyoambukiza.

Aidha, amesema Serikali imeendelea kuboresha huduma za kinga na uchunguzi wa magonjwa hayo kupitia kampeni mbalimbali za afya ikiwemo upimaji wa magonjwa yasiyoambukiza katika maeneo ya kazi, utoaji wa elimu kwa jamii pamoja na matembezi ya Kitaifa yanayohamasisha wananchi kufanya mazoezi.

Mchenjgerwa ameongeza kuwa Wizara pia imeendelea kutumia vyombo mbalimbali vya habari kutoa elimu ya uhamasishaji kwa wananchi kuhusu namna ya kujikinga na kudhibiti magonjwa yasiyoambukiza, hatua inayolenga kupunguza ongezeko la wagonjwa na madhara yatokanayo na magonjwa hayo nchini.


Bodi ya Nishati Vijijini (REB) leo Mei 10, 2026 imefanya ziara katika Kampuni zinazozalisha, kusambaza bidhaa za nishati safi ya kupikia katika Mkoa wa Arusha.

Bodi hiyo ikiwa imeongozwa na Mwenyekiti wake, Mhe. Balozi Meja Jenerali (mstaafu), Jacob Kingu pamoja na Wajumbe wa Bodi hiyo, Mhe. Radhia Msuya na Mhandisi Sophia Mgonja waliweza kutembelea kampuni ya Ignate Energy Access yenye bidhaa za My Sol pamoja na kampuni ya HannyG Investment.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mwenyekiti Kingu, amezipongeza kampuni hizo kwa kuunga mkono kampeni ya Serikali ya Nishati Safi ya Kupikia kwa kuanza kutengeneza pamoja na kusambaza bidhaa za nishati safi ya kupikia huku akitoa wito kwa makampuni mengine kuendelea kuunga mkono kampeni hiyo ili malengo yaliyowekwa ya ifikapo 2034, Asilimia 80 ya Watanzania wawe wanatumia nishati safi ya kupikia.

Awali akitoa taarifa ya utendaji wa kampuni ya My Sol, Meneja Uendeshaji wa Mitambo, Joe Chambua, amesema kuwa pamoja na huduma zingine zinatolewa na kampuni hiyo ikiwamo huduma ya ufungaji wa umeme jua, kampuni hiyo imeanza kutekeleza mradi wa nishati safi ya kupikia kwa kuja na teknolojia rahisi na ya gharama nafuu ya mtambo wa biogasi.

Amesema kuwa wamefanikiwa kufunga mitambo ya biogasi katika taasisi mbalimbali nchini ikiwemo Magereza.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Msaidizi wa kampuni ya Hanny G Investment, Hanny Mbaria, ambao wanajishughulisha na utengenezaji wa majiko banifu pamoja na mkaa mbadala ameishukuru Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kwa kuipa kampuni hiyo kazi ya kusambaza majiko banifu na mkaa mbadala katika shule 53 Tanzania Bara.

Mbaria amesema licha ya mradi wa nishati safi ya kupikia kulinda mazingira lakini pia mradi huo umetoa ajira kwa vijana wengi.

“Kwa sasa kampuni yetu imekua zaidi na tumeajiri vijana wengi zaidi tofauti na hapo awali. Kwa sasa tuna wafanyakazi zaidi ya 120 wenye ajira za kudumu na wasio na ajira za moja kwa moja ni 1000,” amesema Mbaria.

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kwa kushirikiana na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya, Halmashauri za Miji, Halmashauri za Wilaya, Shule za msingi, wadau wa mazingira pamoja na Mabalozi wa Mazingira, limepanda miche ya miti elfu arobaini katika maeneo mbalimbali nchini ikiwa ni sehemu ya kuelekea maadhimisho ya miaka 40 tangu kuanzishwa kwa Baraza hilo.



NAIBU Waziri wa Madini na Mbunge wa Jimbo la Longido Mkoani Arusha,Dkt Steven Kiruswa  amesema katika kipindi cha miaka mitano ijayo cha uongozi wake anawiwa na kuhakikisha anatekeleza vipaumbele 16 katika kukamilisha miradi ya maendeleo katika Jimbo hilo.

Dkt Kiruswa alisema hayo katika mkutano wa hadhara wenye lengo la kuwashukuru wananchi wa Jimbo la Longido kwa kukichagua chama chake cha Chama Cha Mapinduzi{CCM},Mgombea Urasi wa chama hicho Rais Samia Suluhu Hassan na Makamu wake Dkt Emmanuel Nchimbi,Mbunge na Madiwani wote wa chama hicho katika mkutano uliohudhuriwa na viongozi mbalimbali wa chama na serikali katika ngazi ya tawi,kata na wilaya uliofanyika katika uwanja wa Longido Polisi.

Alisema moja ya vipaumbe ambavyo anataka kuvifanyia kazi katika kipindi miaka mitano ya ubunge wake ni pamoja na kukamilisha ujenzi wa shule za msingi na sekondari katika kata zote za Jimbo hilo,kubuni miradi ya ajira kwa vijana,kukamilisha mradi wa maji wa chanzo cha Loormokerian Kijiji cha Oltepesi,kuchimba visima vya maji Kiseriani na Orkesumet.

Waziri Kiruswa alitaja kipaumbe kingine ni pamoja na ukarabati na ufunguaji wa barabara zilizo chini ya Wakala wa Barabara Mjini na Vijijni{TARURA} kwenye maeneo ynye vipaumbele,uendelezaji wa shule shikizi katika kata ambazo hazina ikiwa ni njia ya kupunguza umbali mrefu kwa watoto kwenda na kurudi shule na kujikinga na wanyama wakali.

Alisema ana uhakika ndani ya muda huo vipaumbele alivyovioanisha vitakuwa vimekamilika kwa kushirikiana na wananchini,serikali kuu,wadau wa maendeleo na wafadhili wa ndani na nje lengo kuu ni kutaka kuwapelekea huduma wananchi.

Aidha alitumia nafasi hiyo kuwashukuru wananchi kwa kumpa kura nyingi Rais Samia Suluhu Hassan na kuwa Rais awamu ya sita na kusema kuwa uamuzi walioufanya umeiheshimisha Longido kwani imekuwa wilaya ya kwanza kwa kutoa kura Nyingi Mkoani Arusha.

Waziri Kiruswa alisema kutokana na hali hiyo aliwaomba wananchi wa Longido kuwa wamoja na watulivu katika kuiletea maendeleo Longido na kumwombea afya njema Rais ili aweze kuendelea kuiongoza nchi kwa amani na upendo.

''Nawaomba wananchi wa Longido tuiombe nchi amani na tumwombee Rais wetu Samia Suluhu Hassan afya njema kwani amekuwa mstari wa mbele kuiendeleza Longido hivyo kila mmoja kwa imani yake ya kiislamu na kikrusto anapaswa kufanya hivyo''alisema Kiruswa

Naye Mkuu wa wilaya ya Longido,Salumu Kally amesema ni wakati wa wana Longido kushirikiana na Mbunge katika kuiletea maendeleo Jimbo hilo na kusema kuwa mifarakano mara nyingi hurudisha nyumba maendeleo hivyo hataki kuliona hilo likitokea.

Naye Mbunge wa Monduli,Joseph Isack na Mbunge wa Ngorongoro Yannick Ndoinyo wote waliwaomba wananchi wa Longido kushirikiana na Mbunge wao Kiruswa kwani mbunge huyo ni mpenda watu na mpenda maendeleo hivyo wasidhubutu kuipoteza lulu hiyo kwa namna yoyote ile kwani watakuwa wamefanya maksa makubwa sana,

 

Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga, amewashauri Wamiliki wa Viwanda vipya Kutoa kipaumbele kwa wazawa katika ajira ili kukuza uchumi na mapato ya Taifa kwa ujumla.

Akizungumza Mei 09, 2026, wakati wa akifungua wa Kiwanda kipya cha kutengeneza tambi za papo hapo (Instant) cha Kura Food mkoani Pwani, amesema kuwa Serikali inaendelea kuboresha mazingira ya Biashara ikiwemo sera, miundombinu, na mifumo ili kuvutia Wawekezaji na wafanyabiashara na kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania kimataifa.

Aidha, Wizara imefanya mapitio ya sheria na kanuni ili kuhakikisha zinajielekeza katika kuwezesha biashara na kuondoa vikwazo badala ya kudhibiti pekee. Lengo ni kushirikiana na wadau wa mnyororo wa thamani, kutumia teknolojia za kisasa zinazoongeza tija, uzalishaji, na ufanisi wa biashara nchini.

Naye, Mwenyekiti wa Kura Food, Bw. Wu Yeping, ameipongeza Serikali kwa kuweka mazingira rafiki yanayorahisisha uwekezaji,

Huku Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mhe. Abubakar Kunenge, akibainisha kuanza kwa uboreshaji wa miundombinu ya barabara na Reli ya Kisasa (SGR) kuanzia mwaka ujao ili kufungua zaidi fursa za kibiashara mkoani humo.

Naye Mbunge wa Kisarawe, Mhe. Selemani Jafo, amemshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa sera zake thabiti ambazo zimekuwa chachu ya kuvutia wawekezaji. Sera hizi zimesaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza changamoto ya ukosefu wa ajira kwa wananchi wa jimbo hilo kupitia kuanzishwa kwa viwanda vipya.

            
Na Mwandishi Wetu

Benki ya Ushirika (Coop Bank) mwishoni mwa wiki ilizindua rasmi tawi lake jipya Mtwara mjini ikiwa ni hatua muhimu katika utekelezaji wa mkakati wa benki hiyo wa kupanua huduma za kifedha na kuimarisha uchumi jumuishi.

Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), Mhe. Balozi Meja Jenerali (Mstaafu), Jacob Kingu amelipongeza Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) kwa utekelezaji wa mradi wa nishati safi ya kupikia katika kambi zake, huku akiwahamasisha kuelimisha jamii zinazozunguka kambi hizo nazo kutumia nishatia nishati safi ya kupikia.

Pongezi hizo zimetolewa leo Mei 9, 2026 wakati wa ziara ya Bodi hiyo iliyolenga kukagua utekelezaji wa miradi ya nishati safi ya kupikia inaayotekelezwa na Wakala wa Nishati Vijijini (REA) katika Kambi ya JKT ya Oljoro Jijini Arusha.

Mradi huo unahusisha uzalishaji wa bayogesi kupitia mbolea ya ng’ombe, matumizi ya majiko ya gesi, majiko banifu na mashine za kutengenezea mkaa mbadala.

Mwenyekiti Kingu pia, amesisitiza juu ya vijana waliopo kwenye kambi hizo za JKT kupatiwa mafunzo ya namna ya kutengeneza mkaa mbadala ili waweze kutumia ujuzi huo kujiajiri na kuwa mawakala wa kutengeneza mkaa mbadala pindi watakapomaliza mafunzo yao.

Kwa upande wake, akimwakilisha Mkuu wa JKT, Kanali Projest Rutaihwa aliishukuru Bodi hiyo pamoja na Menejimenti ya REA kwa utekelezaji wa miradi nishati safi ya kupikia ambapo kambi 22 zimepata fedha kutoka REA za utekelezaji wa mradi huo ili kulinda mazingira pamoja na afya za wanaoandaa chakula.

Naye Kamanda wa Kikosi cha 833 KJ Oljoro, Kanali Victor Rutayuga Faustine, amesema mradi huo wa nishati safi ya kupikia umeleta mafanikio makubwa katika utunzaji wa mazingira na kupunguza matumizi ya kuni kambini hapo pamoja na kutumia muda mdogo kwenye kuandaa chakula cha vijana wanaopata mafunzo kambini hapo.

“Kabla ya mradi huu tulikuwa tunaagiza lori la kuni kutoka Mbeya kwa ajili ya kupikia chakula cha vijana wetu wa mafunzo hapa kambini. Lakini sasa matumizi ya nishati safi yamesaidia kupunguza utegemezi huo na kulinda mazingira,” amesema Kanali Faustine.

REA imetoa ruzuku ya zaidi ya shilingi bilioni 5.2 kwa ajili ya kuwezesha matumizi ya nishati safi ya kupikia katika kambi za JKT ambapo fedha hizo pamoja na mambo mengine, zimewezesha kufungwa kwa mifumo ya nishati safi ya kupikia pamoja na ununuzi wa mashine za kutengenezea mkaa mbadala.