



Na.Ashura Mohamed - Arusha
Katika kuhakikisha kuwa Uchumi wa wakazi wa mkoa wa Arusha unaimarika wananchi wa mkoa huo hususani Vijana wametakiwa kuhakikisha kuwa wanachangamkia fursa mbali mbali za kiuchumi ili kunufaika na ujio wa mashindano ya kimataifa ya Afcon 2027.
Akizungumza kwa niaba ya mkuu wa Wilaya ya Arusha Mjini bw.Jospeh Mkude,wakati wa Kongamano la Vijana la Engutoto Youth Summit kuhusu Mashindano ya AFCON 2027,Wakili Irene Ndosi ambaye ni Katibu Tarafa Suye amesema kuwa ujio wa Afcon ni neema kubwa kwa wakazi wa mkoa wa Arusha ambapo mbali na kupata burudani ya mpira wa miguu lakini pia ni fursa kwa makundi yote kuongeza uchumi wao.
"Fursa zitaanzia kuanzia watu wa chini kabisa boda boda,watu wa usafirishaji mpaka wanawake watengeneza shanga,kila mtu achukue nafasi hiyo kuleta mabadiliko chanya kwenye uchumi wake binafsi na familia yake na mkoa kwa ujumla,pia tuwe tayari kujaza eneo la uwanja wa Afcon kwasababu mashindano haya ni yakipekee na yanashirika nchi tatu ambazo ni Tanzania,Kenya na Uganda."Amesitiza Ndosi
Aidha Hamza Juma Njiku ni Diwani wa Kata ya Engutoto amesema kuwa kongamano hilo ni muhimu kwa kuwa limewakutananisha vijana na wadau mbal8 mbali katika kuonyesha fursa zilizopo kuelekea mashindano hayo ya Afcon.
"Sisi katika kata yetu fursa za Afcon zimetugusa moja kwa moja kwa kuwa tunajengewa Uwanja mkubwa mzuri wa Mazoezi kwaajili ya mashindano hayo ambapo utakuwa na uwezo wa kuchukuwa watu 5000 waliokaa,maegesho ya magari 500 na mabasi mawili kwaajili ya zile timu ambazo zitaingia kufanya mazoezi,ila uwanja ukikamilika na mashindano kumalizika utatumika kwaajili ya ligi kuu na michuano mbali mbali."Amesema Diwani Njiku
Kwa Upande wake Mwenyekiti wa Umoja wa Chama cha Mapinduzi (UVCCM),Kata ya Engutoto ambaye ndio muandaaji wa Kongamano Engutoto Youth Summit,bw.Ibzan Michael Ruheta amesema kuwa kongamano hili si jukwaa la kisiasa bali ni jukwaa linalokutanisha watu wote kujadili fursa za AFCON kuelekea mwaka 2027.
Bw.Ruheta amesema kuwa Mashindano ya AFCON hayatahuishwa na Tanzania peke yake bali ushirikiano na mataifa mengine wakiwemo Kenya pamoja na Uganda,hivyo kama Watanzania ni wajibu wao kuamka na kuhakikisha tunaitumia nafasi hiyo ipasavyo.
"Ndugu mgeni rasmi, kama unavyojua nchi yetu imepata fursa ya kuandaa mashindano haya ya AFCON,hivyo kama viongozi mliopo katika nafasi za maamuzi, ni vizuri kujipanga kwa kushirikiana na wadau mbalimbali na taasisi mbalimbali zilizopo nchi yetu kwa kikisha fursa hizi tunazipata kwa wakati, vijana waheshimiwe, wasikilizwe na kero zao zitatuliwe ili nchi yetu inufaike."Amefafanua Mwenyekiti huyo
Kongamano la Engutoto Youth Summit lenye kauli mbiu ya "Unlocking 2027 AFCON Opportunity" limeandaliwa na Vijana wa Chama Cha Mapinduzi Kata ya Engutoto,na limekusudia kuwajengea vijana uwezo wa kunufaika na fursa za michezo hiyo kubwa ya kimataifa ambapo limefanyika katika Chuo cha Uhasibu Arusha(IAA) na kukutanisha Vijana Zaidi ya 1000 ili kuonesha nyanja mbali mbali ambazo vijana wanaweza kunuifa nazo.
Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba amemuagiza Waziri wa Maji kwenda Mkoa wa Mwanza kushughulikia mara moja changamoto ya upatikanaji wa maji inayowakabili wananchi wa mkoa huo na kuhakikisha huduma hiyo inarejea kwa haraka.

Na Mwandishi Wetu, Muheza
Mkuu wa Wilaya ya Muheza mkoani Tanga, Ayoub Sebabili, amewahimiza wananchi kujitokeza kwa wingi katika shughuli za mapokezi ya Mwenge wa Uhuru 2026, akisema ushiriki mkubwa wa wananchi utasaidia wilaya hiyo kufanya vizuri katika mashindano ya Kitaifa ya Mwenge wa Uhuru.
Sebabili ametoa wito huo wakati wa zoezi la Jogging lililoandaliwa kama sehemu ya maandalizi ya mapokezi ya Mwenge wa Uhuru, ambapo aliwashukuru wananchi kwa kujitokeza kwa wingi na kushiriki shughuli hiyo.
Alisema Mwenge wa Uhuru unatarajiwa kuwasili wilayani Muheza Juni 23, 2026 ukitokea Wilaya ya Mkinga na kupokewa katika eneo la Kilapura, huku ukitarajiwa kulala katika Uwanja wa Jitegemee.
"Niwashukuru kwa namna mlivyojitokeza leo. Ushiriki wenu unaonyesha dhamira ya kuhakikisha Muheza inafanya vizuri katika mapokezi ya Mwenge wa Uhuru. Kila mmoja wetu awe balozi wa kuhamasisha wananchi wengine kujitokeza kwa wingi," alisema Sebabili..
Kwa upande wake, Mratibu wa Mwenge wa Uhuru Wilaya ya Muheza alisema maandalizi yanaendelea vizuri na kuwa viongozi katika ngazi zote wamepewa jukumu la kuhamasisha wananchi wa makundi mbalimbali, wakiwemo vijana, wanawake, wazee na watu wenye ulemavu kushiriki kikamilifu katika shughuli hizo.
Alisema Mwenge wa Uhuru utapitia maeneo mbalimbali ya wilaya hiyo kwa ajili ya kuzindua na kukagua miradi ya maendeleo pamoja na kutoa ujumbe wa umoja, uzalendo na mshikamano wa kitaifa.
Kwa mujibu wa ratiba iliyopangwa, Mwenge wa Uhuru utaanzia Kata ya Mlingano kabla ya kuelekea Machemba kwa uzinduzi wa mradi na ukaguzi wa banda la lishe litakaloonyesha juhudi za Halmashauri ya Muheza katika kupambana na utapiamlo, malaria na maambukizi ya Virusi vya Ukimwi.
Baadaye utaelekea katika Shule ya Venance Mabeyo na Kata ya Mpapayu kwa ajili ya uzinduzi wa miradi mbalimbali ya maendeleo.
Katika Kata ya Genge, Mwenge wa Uhuru utazindua maabara katika Shule ya Sekondari Chief Mang'enya iliyojengwa kwa nguvu za wananchi na kuweka jiwe la msingi katika mradi wa madarasa mapya kwa ajili ya maandalizi ya wanafunzi wa Kidato cha Kwanza mwaka 2027.
Mratibu huyo alisema pia kutakuwa na shughuli za Klabu ya Wapinga Rushwa pamoja na programu mbalimbali za elimu kwa jamii.
Katika Kata za Magila na Majengo, Mwenge wa Uhuru utatembelea kikundi kilichonufaika na mkopo wa asilimia 10 wa Halmashauri unaotolewa kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu, ambapo kikundi hicho kimepata Sh25 milioni kwa ajili ya shughuli za maendeleo ya kiuchumi.
Aidha, katika eneo la Mikwamba kutakuwa na maonesho ya fursa za zabuni kupitia PPRA, yakilenga kuhamasisha vikundi maalumu kushiriki katika zabuni zinazotengwa kwa makundi hayo.
Ratiba hiyo itahitimishwa kwa shughuli mbalimbali katika Kata ya Tongwe na eneo la Mpaa, ikiwemo uzinduzi wa daraja la karavati, uzinduzi wa Jengo la Havest Inn na mkesha wa Mwenge wa Uhuru katika Uwanja wa Jitegemee.
Viongozi hao wamewataka wananchi kuzingatia amani, utulivu na usalama katika kipindi chote cha shughuli hizo, huku wakisisitiza kuwa vitendo vya uhalifu na uvunjifu wa amani havitavumiliwa.
Akizungumza katika hafla hiyo, Katibu Tawala wa Wilaya (DAS) wa Muheza, Mohamed Mfaki, aliwashukuru wananchi kwa ushirikiano wao katika maandalizi ya mapokezi ya Mwenge wa Uhuru na kuwataka kuendelea kushiriki kikamilifu.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Muheza, Dk Juma Mhina, alisema wilaya hiyo imejipanga kufanya vizuri zaidi mwaka huu na inalenga kushika nafasi ya kwanza kitaifa katika mapokezi ya Mwenge wa Uhuru
"Malengo yetu ni kuona wananchi wanajitokeza kwa wingi katika shughuli zote za Mwenge wa Uhuru. Tunataka Muheza iwe mfano wa mafanikio na ushirikiano katika mapokezi ya Mwenge wa Uhuru 2026," alisema Dk Mhina.
Na OWM - TAMISEMI, Dar es Salaam
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) Mhe. Prof. Riziki Shemdoe ametaka Mkandarasi kampuni ya China Railways and Bridges Corporation (CRBC) inayojenga barabara tisa (9) za lami zenye urefu wa kilometa 5.42 kukamilisha ujenzi wa barabara saba (7) zilizosalia ifikapo Agosti 14, 2026, barabara hizo zinajengwa kupitia Mradi wa Uboreshaji wa Jiji la Dar es Salaam Awamu ya Pili (DMDP II) katika kata za Sinza, Mburahati, Mabibo na Makurumla wilayani Ubungo.
Prof. Shemdoe ametoa maelekezo hayo Juni 13, 2026 Katika Manispaa ya Ubungo jijini Dar es Salaam wakati wa ziara yake ya kikazi ya kukagua ujenzi wa barabara 23 zenye urefu wa kilometa 52.37 zinazojengwa wilayani Ubungo katika kata 11 kupitia utekelezaji wa Mradi wa Uboreshaji wa Jiji la Dar es Salaam Awamu ya Pili (DMDP II).
Prof. Shemdoe amesitiza kuwa, mkandarasi huyo anayesuasua katika ujenzi wa barabara hizo kwa kisingizio cha lami kuchelewa kufika kutokana na vita ya Mashariki ya Kati, hatopewa muda wa nyongeza wa kukamilisha ujenzi wa barabara hizo iwapo atashindwa kukamilisha ifikapo Agosti 14, 2026 kwa mujibu wa mkataba.
“TARURA hakuna kumuongezea muda mkandarasi huyu, atafute lami popote atakapoipata na afanye kazi usiku na mchana kukamilisha barabara hizi 7 zilizosalia ili kuwaondolea adha wananchi,” amesisitiza Prof. Shemdoe.
Katika kuhakikisha barabara zinakamilika kwa wakati, Prof. Shemdoe ameitaka TARURA na Mshauri Elekekezi (NIMETA Consult (T) kumshauri mkandarasi CRBC kwa kuangalia uwezekano wa kukabidhi baadhi ya barabara hizo kwa mkandarasi mwingine (sub contract) ili ujenzi ukamilike kwa wakati.
Aidha, Prof. Shemdoe amemuelekeza Mtendaji Mkuu wa TARURA Mhandisi Victor Seff kumuondoa Mkuu wa Kitengo cha Fedha na Uhasibu Bw. Evans Mgeusa anayesimamia Fedha za Miradi ya Benki ya Dunia kwa kitendo cha kuchelewesha malipo na kumleta mwingine ambaye atafanya kazi kwa weledi na wakati.
Sanjari na hilo, Prof. Shemdoe amemuelekeza Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu - TAMISEMI Bw. Adolf Ndunguru kuwaondoa Wahasibu Bw. Julius Bashuta na Mbwana Mkembe wa kitengo hicho cha Fedha na Uhasibu kinachosimamia fedha za miradi ya Benki ya Dunia, na kuwaleta wengine ambao watafanya kazi vizuri na kwa uaminifu.
Akizungumzia jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita, Prof. Shemdoe amempongeza Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwezesha utiaji saini wa mikataba minne ya ujenzi wa barabara za wilaya ya Ubungo yenye thamani ya shilingi bilioni 77, 457,169,172.73 kupitia Mradi wa Uboreshaji wa Jiji la Dar es Salaam Awamu ya Pili (DMDP II).
Kwa upande wake Mkazi wa Sinza Bw. Jawa Waziri amemshukuru Prof. Shemdoe kwa kufanya ziara ya ukaguzi wa barabara ya mtaa wake wa Sinza Lion na kumpongeza kwa kumuelekeza mkandarasi CRBC kukamilisha kwa wakati barabara hiyo ambayo imekuwa ni kero kwa wakazi wa eneo hilo.