
Baraza la Ushindani (FCT) limeendesha mafunzo ya uwezeshaji kwa wadau mbalimbali jijini Moshi, mkoani Kilimanjaro,katika ukumbi wa Kiringe. Mafunzo hayo yaliwahusisha wafanyabiashara na wananchi kwa lengo la kuongeza uelewa kuhusu masuala ya ushindani, haki za kibiashara na mifumo ya kisasa ya utoaji wa haki.
Mafunzo hayo yalijibiwa kwa mwitikio mkubwa, ishara kuwa kuna mahitaji makubwa ya elimu kuhusu taratibu za kisheria na huduma zinazotolewa na Baraza la Ushindani.
Akizungumza katika mafunzo hayo, Msajili wa Baraza, Mhe. Mbegu Kaskasi, amewashukuru wadau wa Moshi kwa kujitokeza kwa wingi na kuonesha hamasa ya kujifunza, akisema hatua hiyo inaonyesha utayari wa jamii kuimarisha mazingira ya biashara yenye ushindani wa haki.
Mhe. Kaskasi amebainisha kuwa Baraza linaendelea kuboresha mifumo yake ili kurahisisha upatikanaji wa haki, ikiwemo mfumo wa kielektroniki wa uwasilishaji wa mashauri ya rufaa (e-filing), ambao umepunguza gharama na kuondoa usumbufu wa kusafiri kwa wale waliokuwa wakilazimika kufika ofisini moja kwa moja.
Baadhi ya washiriki wa mafunzo hayo walieleza kunufaika na elimu waliyoipata, wakisema imewasaidia kuelewa haki zao, wajibu wao na hatua za kufuata wanapohitaji kuwasilisha mashauri yao.

Wakala wa Nishati Vijijini (REA) pamoja na Mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP) zimeingia makubaliano yaliyolenga kufikisha umeme katika vitongoji na jamii ambazo zimepitiwa na bomba hilo la mafuta kwa upande wa Tanzania.
Mkataba huo wa ushirikiano ambao utatekelezwa kwa miaka mitano, umesainiwa leo Januari 23, 2026 Jijini Dar es Salaam kati ya Mkurugenzi Mkuu wa REA, Mhandisi Hassan Saidy pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa EACOP, Guillaume Dulout.
Akizungumza baada ya kusainiwa kwa mkataba huo, Mkurugenzi Mkuu wa REA, Mhandisi Saidy amesema kuwa makubaliano hayo yatahakikisha jamii zinazoishi pembezoni mwa mradi wa bomba la mafuta kutoka Mkoa wa Kagera mpaka Mkoa wa Tanga zinafikiwa na kunufaika na mradi huo kwa kufikishiwa huduma ya umeme.
Mhandisi Saidy ameongeza kuwa ushirikiano huo pamoja na manufaa mengine unalenga kuimarisha huduma za kijamii kama shule, vituo vya afya na miradi ya maji, pamoja na kuchochea matumizi ya umeme kwa shughuli za uzalishaji mali na kukuza biashara maeneo ya vijijini.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa EACOP, Dulout amesema kuwa utekelezwaji wa mradi huo ni muendelezo wa EACOP kuboresha maisha ya jamii zinazopitiwa na mradi wa bomba la mafuta.
Kwa Tanzania, mradi wa bomba la mafuta linapita katika mikoa 8, halmashauri 27 na vijiji 231, hivyo kugusa moja kwa moja maisha ya jamii nyingi za vijijini na utekelezwaji wa makubaliano kati ya REA na EACOP, ni hatua muhimu katika kuhakikisha kuwa jamii zilizo kando kando ya na mradi wa bomba la mafuta zinanufaika moja kwa moja na upatikanaji wa umeme.


Msajili wa Baraza la Ushindani (FCT), Mhe. Mbegu Kaskasi,akizungumza wakati akifungua mafunzo kwa wadau na wafanyabiashara mkoani Arusha ya kuwajengea uwezo kuhusu matumizi ya mfumo wa usajili wa mashauri kwa njia ya kielektroniki (e-filing).
ARUSHA:
Baraza la Ushindani (FCT) limewahimiza wadau na wafanyabiashara mkoani Arusha kutumia kikamilifu mfumo wa usajili wa mashauri kwa njia ya kielektroniki (e-filing), lengo likiwa ni kuongeza ufanisi na kupunguza gharama katika uwasilishaji wa mashauri.
Akizungumza katika mafunzo hayo Msajili wa Baraza hilo, Mhe. Mbegu Kaskasi, alisema mfumo huo wa kisasa umeundwa ili kurahisisha usajili wa mashauri na rufaa bila wadau kulazimika kufika katika ofisi za FCT, hatua ambayo itaokoa muda na kuongeza ufanisi.
“Mfumo huu utaimarisha uwazi, kasi ya utoaji haki na kupunguza usumbufu kwa wadau,” alisema Mhe. Kaskasi, akibainisha kuwa hatua hiyo inakwenda sambamba na msukumo wa Serikali ya Awamu ya Sita wa kuimarisha matumizi ya TEHAMA katika utoaji wa huduma."amesema Mhe.Kaskasi
Kwa upande wake, Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha, Bw. Moses Pesha, amelipongeza Baraza kwa kuendelea kutoa elimu kwa wanaohusika na wananchi kwa ujumla, akisema hatua hiyo imeongeza uelewa na kuimarisha imani ya wananchi katika mifumo ya utoaji haki.
Naye Afisa TEHAMA wa FCT, Ndg. Athumani Kanyegezi, amesema mfumo wa e-filing unaimarisha usalama wa taarifa na kuongeza urahisi wa kuzifikia ndani ya muda mfupi, tofauti na mfumo wa zamani wa kuhifadhi mafaili kwa mikono.
Katika upande wa wadau, mfanyabiashara wa jijini Arusha, Bi. Jonia Karumuna, ameipongeza Serikali inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kupitia Wizara ya Viwanda na Biashara, kwa kuwezesha taasisi kama Baraza la Ushindani kuendelea kulinda haki za wafanyabiashara na kusikiliza rufaa zinazotokana na migogoro kutoka Tume ya Ushindani (FCC) na mamlaka mbalimbali za udhibiti ikiwemo EWURA, LATRA, TCRA, TCAA na PURA.
Amesema uwepo wa Baraza hilo umeongeza imani kwa wafanyabiashara kutokana na mchango wake katika kuhakikisha haki inatolewa kwa wakati na kwa kuzingatia misingi ya ushindani wa haki nchini.

Na OWM - TAMISEMI, Dodoma
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM–TAMISEMI), Prof. Riziki Shemdoe, leo amepokea mpango mkakati wa ukamilishaji wa ujenzi wa jengo la Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Morogoro kutoka kwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Morogoro, Dkt. Mussa Ali Mussa (Mshitiri), Msanifu Majengo Justine Katabalo wa Kampuni ya MCB Company Ltd (Mkandarasi) pamoja na Mhandisi Khamadu Kitunzi kutoka Wakala wa Majengo Tanzania (Mshauri Elekezi), ikiwa ni utekelezaji wa maelekezo yake aliyoyatoa Januari 17, 2026 mjini Morogoro wakati wa ziara yake ya kikazi ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa jengo hilo.
Prof, shemdoe ameridhishwa na mpango mkakati uliowasilishwa ambao utawezesha jengo la Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Morogoro kukamilia ifikapo Juni 07, 2026 tofauti na maelekezo ya awali ambapo ilipaswa jengo hilo kukamilika mwezi Julai 2026.
Awali, Prof. Shemdoe alielekeza ndani ya wiki moja Katibu Tawala Mkoa wa Morogoro, Mkandarasi kampuni ya MCB Company LTD na Mshauri Elekezi Wakala wa Majengo (TBA) kukutana na kuandaa mpango mkakati wa kukamilisha ujenzi wa jengo hilo na kuuwasilisha ofisini kwake leo.
Prof. Shemdoe alilazimika kutoa maelekezo hayo baada ya kutoridhishwa na maendeleo ya ujenzi wa jengo hilo, licha ya kutokuwa na changamoto ya fedha. Ujenzi wa jengo hilo ulianza kutekelezwa Mei 27, 2022 na ulitakiwa kukamilika Mei 26, 2024.









