

Kauli Mbiu ya Mwaka 2026:
“Medicinal and Aromatic Plants and Their Contribution to Human Welfare: The Way Forward for Sustainable Use”
Kwa niaba ya Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira (TRAMEPRO), tunaungana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kupitia Tanzania Wildlife Management Authority (TAWA), pamoja na wadau wote wa uhifadhi wa mazingira, vyombo vya habari, na watabibu asili nchini kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Wanyamapori tarehe 03 Machi 2026. Aidha, tunaungana na mataifa mengine duniani kusherehekea siku hii muhimu inayotukumbusha wajibu wetu wa kulinda urithi wa asili kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.
Maadhimisho ya mwaka huu yanatukumbusha umuhimu wa kulinda na kutumia kwa busara rasilimali za asili, hususan mimea ya dawa na harufu, ambayo imekuwa nguzo muhimu katika afya ya jamii, ukuaji wa uchumi wa taifa, na ustawi wa binadamu kwa ujumla. Mimea hii si tu hazina ya tiba asilia bali pia ni rasilimali yenye mchango mkubwa katika tafiti za kisayansi, viwanda vya dawa, na maendeleo ya kijamii.
Tanzania imebarikiwa kuwa na bioanuwai adhimu ya wanyamapori, misitu, na vyanzo vya maji. Rasilimali hizi ni urithi wa taifa letu na msingi wa maendeleo endelevu. Hivyo basi, tunapaswa kushirikiana kwa dhati katika:
• Kulinda wanyamapori dhidi ya ujangili na uharibifu wa makazi yao.
• Kuhifadhi mimea ya tiba kwa matumizi endelevu yasiyoharibu mazingira.
• Kulinda vyanzo vya maji na mifumo ya ikolojia kwa manufaa ya sasa na vizazi vijavyo.
• Kuwezesha jamii kushiriki kikamilifu katika shughuli za uhifadhi na kunufaika nazo kiuchumi.
Tukiongozwa na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025–2050 inayolenga kujenga taifa lenye uchumi imara, amani, utulivu na maendeleo endelevu ya watu wake, tunasisitiza kuwa:
“Uhifadhi wa rasilimali za asili ni msingi wa ustawi wa taifa na kizazi kijacho.”
Kwa pamoja, tushikamane kulinda urithi wetu wa asili, kuenzi thamani ya mimea ya dawa, na kuhakikisha matumizi yake yanafanyika kwa njia endelevu kwa manufaa ya binadamu na mazingira.
TUSHIRIKIANE KWA UHIFADHI, USTAWI NA MAENDELEO ENDELEVU
Imetolewa na: Boniventura Mwalongo
Katibu Mkuu Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira (TRAMEPRO)
Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA), yatakiwa kuongeza kasi ya urasimishaji wa biashara na kuimarisha mifumo ya kidijitali ili kuchochea ufanisi na ukuaji wa uchumi kwani BRELA ni lango kuu la uwekezaji nchini.
Hayo yamesemwa na Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Judith Kapinga (Mb), Machi 04, 2026, wakati akifungua Baraza la wafanyakazi la BRELA na kuhimiza uwekezaji kwenye rasilimali watu, akitaka watumishi wapewe mafunzo na stahiki zao kwani ustawi wa wafanyakazi ndio siri ya mafanikio ya taasisi, na kuwataka watumishi kufanya kazi kwa uadilifu, weledi, na uzalendo.
Waziri Kapinga amebainisha kuwa kwa mujibu wa tafiti mbalimbali za wadau, zaidi ya 80% ya biashara nchini zipo sekta isiyo rasmi, hivyo BRELA lazima iwe kinara wa kuzirasimisha, hatua ambayo itawawezesha Wajasiriamali wadogo kupata mikopo, masoko, na ulinzi wa kisheria.
Aidha, ameagiza kuhuisha mifumo ya TEHAMA ili iwe rafiki itakayopunguza gharama pamoja na muda wa mteja kupata huduma na kusisitiza kuwa mifumo hiyo lazima iwe na usalama wa taarifa wa hali ya juu na itumike kupata mrejesho wa haraka kutoka kwa wateja ili kuboresha utendaji.
Aidha, ameipongeza BRELA kwa ongezeko la usajili na makusanyo, akisisitiza kuwa Serikali itaendelea kuweka mazingira wezeshi kwa wafanyakazi na kuitaka taasisi hiyo kugeukia mfumo wa uwezeshaji badala ya udhibiti pekee ili kukuza sekta binafsi nchini.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa BRELA Bw. Godfrey Nyaisa amebainisha kuwa BRELA imevuka lengo la mapato kwa asilimia 105 na kutekeleza malengo kwa asilimia 78 katika nusu mwaka wa 2025/26, ambapo taasisi hiyo imewasilisha Shilingi bilioni 3.1 kwa Msajili wa Hazina, na kusema mafanikio hayo yanayotokana na mshikamano, kujituma na bidii ya watumishi.
Vilevile, amewasilisha Mpango Mkakati wa 2026–2031 unaolenga kuboresha za usajili na miundombinu, ikiwemo ujenzi wa ofisi za Dodoma na Kinondoni na kubainisha kuwa uongozi unaendelea kuimarisha maslahi ya watumishi kupitia muundo mpya wa mishahara na motisha ili kutatua changamoto za uhaba wa wafanyakazi na kuongeza tija.




Wananchi wa Kata ya Oldonyosambu, wilayani Ngorongoro, wameishukuru Serikali kwa kuwajengea daraja la mawe lenye urefu wa mita 45 katika Mto Mbaga linalounganisha vijiji vya Jema na Oldonyosambu.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti wananchi hao walisema kukamilika kwa daraja hilo kumewaondolea changamoto ya muda mrefu ya usafirishaji wa mazao na upatikanaji wa huduma za kijamii hususan katika kipindi cha masika.
Diwani wa Kata ya Oldonyosambu, Mhe. Kabaney Mojah, amesema kabla ya ujenzi wa daraja hilo, wakazi wa eneo hilo walikumbwa na matatizo makubwa ya mawasiliano na usafirishaji wa mazao kutoka Kijiji cha Jema ambako kuna shughuli za kilimo.
“Kijiji cha Jema ni eneo letu kuu la uzalishaji mazao. Hapo awali tulikuwa na changamoto kubwa ya kusafirisha mazao kwenda soko la Arusha pamoja na mawasiliano kati ya vijiji hivi viwili. Tunaishukuru Serikali kwa kutatua tatizo hili,” alisema Mhe. Mojah.
Aliongeza kuwa Mto Mbaga ulikuwa kikwazo kikubwa, hasa nyakati za mvua, hali iliyosababisha usumbufu hata katika masuala ya dharura.
“Mto Mbaga ni mto korofi, zamani wakati wa masika wananchi hawakuweza kuvuka kabisa. Sasa tunaweza hata kuwasafirisha wanafunzi wanaougua kutoka Shule ya Sekondari Jema hadi Hospitali ya Wilaya iliyopo Wasso bila hofu,” amesisitiza.
Naye, mkazi wa eneo hilo Bw. Likam Maroseck amesema kabla ya daraja kujengwa, baadhi ya wananchi walikumbwa na hatari ya kusombwa na maji walipokuwa wakivuka kwenda kulima mashamba yao kijijini Jema.
“Ujenzi wa daraja hili umeleta ahueni kubwa. Kwa sasa shughuli zetu zinafanyika kwa urahisi na usalama zaidi,” amesema.
Kwa upande wake, Kaimu Meneja wa TARURA Wilaya ya Ngorongoro, Mhandisi Edwin Merdad, amesema kuwa katika mwaka wa fedha 2023/2024, walitenga bajeti ya shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa daraja hilo pamoja na uboreshaji wa barabara inayounganisha vijiji hivyo.
Amesema pamoja na mpango wa awali wa kuchonga na kuweka kifusi kwenye barabara yenye urefu wa kilomita tano, wamefanikiwa kujenga barabara yenye urefu wa kilomita 14 kati ya vijiji hivyo viwili.
“Daraja hili ni msaada mkubwa si tu kwa wakazi wa Oldonyosambu na Jema, bali pia kwa wafanyabiashara kutoka nchi jirani ya Kenya wanaoshiriki katika shughuli za minada.
“Zamani wakati wa masika wananchi walishindwa kuvuka kwa takribani miezi miwili, lakini sasa hali hiyo imekuwa historia,” amesema Mhandisi Merdad.
Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro ina mtandao wa barabara wenye jumla ya kilomita 970.698, zikiwemo barabara za zege kilomita 0.224, barabara za changarawe kilomita 306.41 na barabara za udongo kilomita 664.064.
Anajulikana kwa jina la Utani Profesa kutokana na uwezo mkubwa wa kujua vitu vingi katika hifadhi ya Ngorongoro katika utumishi wake wa miaka 34, ni mwanamke shupavu kuelekea siku ya wanawake tarehe 8 Machi, 2026
Tukio la kusisimua na hatari katika maisha yake ni tarehe 6 Machi 2020 Kreta ya Ngorongoro kwenye utekelezaji wa majukumu yake, ghafla Faru akamkimbiza bila yeye kujua ambapo alijaribu kutumia mbinu za medani alizofundishwa jeshini kujinasua lakini bahati mbaya alishambuliwa ingawa baadaye aliweza kuokolewa na kukimbizwa hospitali kwa matibabu.
Kamanda huyu wa Uhifadhi anaadhimisha siku ya wanawake duniani akiendelea kuchapa kazi na mara nyingi utamkuta kreta akifanya shughuli za uhifadhi, utafiti, sensa za wanyamapori na kupambana na mimea vamizi bila woga.
Ngorongoro tunampa maua yake kwa kuwa uzoefu ni mama wa Maarifa hivyo yeye kama Chanda chema tunamvika Pete anapotimiza miaka 6 ya tukio la Faru.
Na Mwandishi Wetu
KATIKA kuelekea kilele cha maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani, Halmashauri ya Mji Handeni imejipanga kutekeleza shughuli mbalimbali ikiwamo uzinduzi wa Jukwaa la Uwezeshaji Wanawake Kiuchumi.
Akizungumza kuhusu maandalizi ya maadhimisho hayo, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Handeni, Maryam Ukwaju, amesema halmashauri hiyo inatambua na kuthamini mchango mkubwa wa wanawake katika maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla.
Amesema Machi 5, 2026 kutafanyika kongamano la wanawake litakaloenda sambamba na uzinduzi wa Jukwaa la Uwezeshaji Wanawake Kiuchumi la Halmashauri ya Mji Handeni, linalolenga kuwaunganisha wanawake ili kubadilishana uzoefu, kupata taarifa za fursa za kiuchumi na kuimarisha shughuli zao za ujasiriamali.
Ukwaju amesema kongamano hilo pia litaambatana na maonesho ya bidhaa mbalimbali zinazozalishwa na wanawake wajasiriamali, hatua inayolenga kuonesha ubunifu wao pamoja na juhudi wanazofanya katika kujikwamua kiuchumi.
Ameongeza kuwa katika kongamano hilo litakalofanyika katika ukumbi wa CCM Wilaya ya Handeni, washiriki watapatiwa elimu mbalimbali ikiwemo masuala ya umiliki wa ardhi na mirathi, malezi na makuzi ya watoto, ujasiriamali na biashara, elimu ya ushirika na SACCOS pamoja na kilimo bora na ufugaji wa kisasa.
Kwa mujibu wa Mkurugenzi huyo, Machi 6, 2026 halmashauri itatoa msaada kwa baadhi ya kaya zinazoishi katika mazingira hatarishi ikiwa ni sehemu ya kuonesha mshikamano na kusaidia jamii zenye uhitaji.
Kadhalika amesema kilele cha maadhimisho hayo kwa ngazi ya Halmashauri kitafanyika Machi 7, 2026 katika viwanja vya Shule ya Msingi Kwenjugo, ambapo kutafanyika ugawaji wa taulo za kike kwa wanafunzi wa kike pamoja na utoaji wa vyeti kwa vikundi vinne vya wanawake vilivyotekeleza miradi yao kwa mafanikio na kurejesha mikopo ya asilimia 10 kwa wakati. Amesema mgeni rasmi katika shughuli hizo anatarajiwa kuwa Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese.
Ukwaju amesema maadhimisho hayo yanaongozwa na kaulimbiu isemayo “Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana; Msingi Jumuishi kufikia Dira 2050,” huku halmashauri ikiendelea kuhamasisha wananchi wote kushiriki kikamilifu katika kuimarisha usawa wa kijinsia na kuchochea maendeleo jumuishi kwa wanawake na wasichana.

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhe. Wanu Hafidh Ameir, ameutaka uongozi wa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Mzenga, kilichopo Kata ya Mzenga, Wilaya ya Kisarawe, kuhakikisha kinatoa mafunzo katika fani zinazoendana na shughuli za kiuchumi za eneo hilo.
Mhe. Wanu ametoa agizo hilo Machi 03, 2026, wilayani Kisarawe wakati wa ziara ya ufuatiliaji na ukaguzi wa miradi inayotekelezwa na Wizara katika wilaya hiyo.
Amewataka viongozi wa wilaya na wananchi wa eneo hilo kuona umuhimu wa mafunzo ya ujuzi na hivyo kuhamasisha vijana kujiunga na chuo hicho ili kupata ujuzi utakaowawezesha kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi.
Amesema chuo hicho, pamoja na vyuo vingine vya maendeleo ya wananchi, vinapaswa kuzingatia mahitaji halisi ya kiujuzi ili vijana waweze kujiunga kwa wingi.
“Mmesema hapa mnazalisha zao la korosho, ufuta na mihogo; kwa nini sasa msianzishe kozi ya kusindika mazao hayo? Hii itawamasisha vijana kujiunga na chuo kwa kuwa wanasoma kile wanachofanyia kazi,” amesema Mhe. Wanu.
Aidha, ameutaka uongozi wa chuo hicho kusimamia ipasavyo mifumo ya usimamizi wa watumishi ili kuimarisha uwajibikaji.
Akiwa wilayani humo, Mhe. Wanu pia amekagua ujenzi wa VETA Kisarawe na kusema kuwa Serikali inaendelea kujipanga kupata rasilimali fedha kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa chuo hicho ili malengo ya kutoa ujuzi kwa wananchi yafikiwe.
Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe, Mhe. Petro Magoti, amemuhakikishia Naibu Waziri Wanu ushirikiano katika kusimamia utekelezaji wa maagizo aliyoyatoa, ikiwemo kuhakikisha huduma za umeme na maji zinafika katika eneo la chuo ili kurahisisha hatua inayofuata ya ujenzi.




















