Na Mwandishi Wetu, Lindi na Mtwara
Katika jitihada za kuongeza uelewa wa matumizi ya Moduli ya kupokea na kushughulikia Malalamiko na Rufaa kupitia Mfumo wa Kielektroniki wa Ununuzi ya Umma (NeST), Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA) imetoa mafunzo kwa wazabuni, wajasiriamali na watumishi wa Umma waliopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa, Mikoa ya Lindi na Mtwara. 
Akielezea kuhusu mafunzo hayo ya siku tano (kuanzia tarehe 16 - 20 Februari, 2026), Meneja wa Usimamizi wa Rufaa na Sheria (PPAA), Bi. Florida Mapunda amesema kuwa mafunzo hayo yamelenga kutoa elimu kwa wadau wa ununuzi wa Umma kuhusu taratibu za uwasilishaji na ushughulikiaji wa malalamiko na rufaa katika mfumo wa NeST kama ilivyoelekezwa katika Sheria ya Ununuzi wa Umma. 
“Sheria ya Ununuzi wa Umma imeweka sharti la lazima kwa ununuzi wa umma kufanyika katika mfumo wa NeST. Kutokana na sharti hilo, PPAA kwa kushirikiana na PPRA tumejenga moduli ya kupokea na kushughulikia malalamiko katika mfumo wa NeST ili kuwasaidia wadau wa ununuzi wa umma (Wazabuni na Taasisi za Umma) kuwasilisha malalamiko na rufaa kieletroniki,” amesema Bi. Mapunda.
Pamoja na mambo mengine, Bi. Mapunda ameongeza kuwa Moduli ya kupokea na kushughulikia malalamiko na rufaa katika mfumo wa NeST ina manufaa makubwa kwa wazabuni kwani inarahisisha uwasilishaji wa malalamiko ya zabuni kwa njia ya mtandao bila kufika ofisini, jambo linalochangia kuokoa muda, gharama na kuongeza uwazi na uwajibikaji katika ununuzi wa Umma.
Kwa upande wake Mkuu wa Sehemu ya Rufaa kutoka PPAA, Bi. Violet Limilabo ameeleza kuwa PPAA ina mchango mkubwa katika kulinda haki za wazabuni kwa kuwapa fursa ya kusikilizwa wanapoona hawakutendewa haki katika michakato ya Ununuzi wa Umma. 
Aidha, PPAA imeendelea kuimarisha uwazi na usawa kwa kuhakikisha taratibu za ununuzi wa umma zinafuatwa kwa mujibu wa sheria na kupunguza migogoro kwa kutoa suluhisho la kisheria.
Naye Afisa Ununuzi kutoka ofisi za PPRA Kanda ya Kusini, Bw. Aziz Njovu alitoa mafunzo kuhusu moduli mpya za majadiliano (negotiations) na uandaaji, upekuzi na utiaji saini wa Mkataba (Contract preparation, vetting and signing kwenye mfumo wa NeST, alisema kwa sasa mchakato wa majadiliano na utiaji saini wa mkataba unahitimishwa kwa njia ya mtandao.
“Matumizi ya mfumo wa NeST yameendelea kuimarisha uwajibikaji na kurahisisha ufuatiliaji wa mikataba ya ununuzio wa umma,” amesema Bw. Njovu.
Mafunzo hayo yamewahusisha jumla ya washiriki 322 ambao ni  wataalamu wa sheria, Tehama na ununuzi pamoja na wazabuni, makundi maalum yakiwemo wanawake, vijana, wazee na watu wenye mahitaji maalum pamoja na mafundi wa ndani.
Mafunzo kuhusu Matumizi ya Moduli ya kupokea na Kushughulikia Malalamiko na Rufaa katika Mfumo wa NeST yaligawanyika katika makundi matatu ambapo Kundi la kwanza ni Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa (tarehe 16 Februari, 2026), Mkoa wa Lindi (tarehe 17 na 18 Februari, 2026) na Mkoa wa Mtwara (tarehe 19 na 20 Februari, 2026)
Mafunzo hayo ni mwendelezo wa mafunzo ya awali yaliyofanyika katika Kanda ya Pwani, Kanda ya Ziwa, Kanda ya Kaskazini, Kanda ya Nyanda za Juu Kusini pamoja na Kanda ya Kati.
 
 
 
 

Katika nchi inayokumbwa na changamoto za kiafya, mazingira na umasikini, nishati safi ya kupikia si tu hitaji la msingi bali ni kichocheo cha maendeleo ya kweli kwa watu na Taifa kwa ujumla.

Katika kukabiliana na ukataji miti ambapo takribani asilimia 16 ya eneo la nchi tayari limegeuka kuwa janga, Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ilizindua mkakati wa kitaifa wa nishati safi ya kupikia unaolenga kuhakikisha asilimia 80 ya watu wanaachana na matumizi ya kuni na mkaa ifikapo mwaka 2034.

Akizungumza ofisini kwake leo tarehe 23 Februari 2026 mara baada ya kupokea ujumbe wa wataalamu kutoka Wakala wa Nishati Vijijini - REA waliopo mkoani Singida kwa ajili ya kuutambulisha mradi wa uuzwaji wa majiko banifu kwa bei ya ruzuku, Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe. Halima Dendego amempongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwa kinara katika utekelezaji wa mkakati wa nishati safi ya kupikia.

Vilevile Mhe Dendego amesema kuwa Rais Samia ni kinara wa utekelezaji wa Nishati safi Afrika hivyo mkoa wa Singida upo tayari na utaanza kugawa majiko hayo banifu katika wilaya zote za mkoa wa Singida ili mpaka kufikia mwaka 2030 mkoa huo uwe umetengeneza alama kubwa kwa wananchi wake kabla hata ya kufikia mwaka 2034.

Pia, amesema kuwa mkoa wa Singida umepokea mitungi ya gesi zaidi ya 18,000 ambayo imesambazwa kwa wananchi ili kutokomeza kabisa nishati chafu ya kupikia.

Kwa upande wake Mhandisi Raya Majallah kutoka REA-Idara ya Nishati Jadidifu na Teknolojia Mbadala akizungumza mbele ya Mkuu wa Mkoa wa Singida ameutambulisha mradi wa uuzwaji wa majiko banifu kwa bei ya ruzuku katika mkoa huo ambapo amesema kuwa Wakala wa Nishati Vijijini umeandaa mpango huo wa uuzaji wa majiko banifu 200,000 kwa bei ya ruzuku yenye ufanisi mkubwa katika utumiaji wake.

Mradi huo unahusisha usambazaji wa majiko banifu yanayotumia kuni na mkaa kidogo ili kupunguza matumizi ya vyanzo hivyo vya nishati Pamoja na athari za moshi zitokanazo na matumizi katika majiko ya kawaida.

Mhandisi Majallah amesema kuwa mikataba hiyo ilisainiwa Mei 9, 2025 na itatekelezwa ndani ya miezi 15 ambapo gharama ya mradi huo ni Shilingi Milioni 340,288,200 kwa mkoa wa Singida na ruzuku inayotolewa na wakala wa nishati vijijini-REA ni shilingi milioni 289,230,504.47 sawa na asilimia 85 ya gharama ya mradi huku wananchi wakichangia Shilingi 51,057,691.53 sawa na asilimia 15 ya gharama ya mradi.

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, ametoa wito kwa Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela kuhakikisha inakuwa kitovu cha ubora wa kitaaluma, utafiti na ubunifu unaolenga kutatua changamoto halisi za dunia ya leo.

Wito huo umetolewa wakati wa hafla ya uwekaji wa jiwe la msingi la ujenzi wa bweni la wanafunzi katika taasisi hiyo.

Waziri Mkuu amesema ujenzi wa bweni hilo ni kielelezo cha dhamira ya dhati ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kuimarisha miundombinu ya elimu ya juu pamoja na kukuza maendeleo ya sayansi na teknolojia nchini. Alisisitiza kuwa miundombinu bora ya elimu ni msingi muhimu wa kuboresha mazingira ya kujifunzia, hasa katika kipindi ambacho idadi ya wanafunzi inaendelea kuongezeka mwaka hadi mwaka.

 "Nitoa wito kwa mkandarasi na uongozi wa taasisi kuhakikisha kunakuwa na usimamizi madhubuti wa rasilimali na utekelezaji wa mradi kwa ufanisi na kwa wakati, ili bweni hilo likamilike mapema na kuanza kutumika kwa manufaa ya wanafunzi."amesema Dkt.Nchemba

Kwa upande wake, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda, amesema Taasisi ya Nelson Mandela inaendana kikamilifu na maelekezo ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuwekeza katika sayansi na teknolojia. Ameeleza kuwa tayari Serikali imeanzisha shule za wasichana za sayansi katika mikoa yote 26 ya Tanzania, hatua inayolenga kuongeza idadi ya wanafunzi wa sayansi watakaokuja kujiunga na taasisi hiyo.

Naye  Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Taasisi ya Nelson Mandela Balozi Maimuna Tarishi, amesema bweni hilo linajengwa kwa kuzingatia viwango vya ubora ili kuhakikisha wanafunzi wanapata makazi salama na yanayowezesha kujifunza, kufanya utafiti na ubunifu kwa utulivu.

Balozi Tarishi ameongeza kuwa bweni hilo litakuwa na vyumba 184, ambapo vyumba 160 vitakuwa vya kujitegemea (self-contained), na vyumba 20 vitakuwa maalumu kwa wanafunzi wenye watoto wadogo na wenye mahitaji maalumu (apartment).

Katika kuelekea kilele cha maadhimisho ya miaka 25 ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC), Kampasi ya Tabora imefanya ziara ya kijamii katika Kituo cha Kulelea Wazee wenye Mahitaji Maalum kilichopo Ipuli, Manispaa ya Tabora. Ziara hiyo ilikuwa ni sehemu ya mikakati ya chuo kuimarisha ushirikiano na jamii.
Katibu Tawala wa Wilaya ya Tabora, Bi. Asha Churu, kwa kushirikiana na Mkurugenzi wa Kampasi ya Tabora, Dkt. Joseph Mbwillo, wameongoza timu  ya watumishi na wanachuo wa Kampasi ya Tabora kutembelea kituo hicho katika kujali na kusaidia wazee wenye mahitaji maalum.
Lengo kuu la ziara lilikuwa ni kuwapelekea misaada mbalimbali kwa wahitaji hao, ikiwa ni pamoja na mchele, maharage, mafuta ya kupikia na mafuta ya kujipaka, sabuni za kuogea na kufulia, nguo, sukari, mashuka pamoja na nguo katika kuboresha maisha ya wazee hao.
Pamoja na kutoa misaada hiyo, timu hiyo pia ilifanya kazi ya usafi wa mazingira ya makazi ya wazee pamoja na  zoezi la upandaji miti katika eneo hilo kwa lengo la kuimarisha ustawi wao na kuhifadhi mazingira kwa ujumla.
Ziara hii ni sehemu kuelekea kilele cha maadhimisho ya mika 25 ya chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania kwa kuonyesha mfano wa jamii inayojali na kuendeleza mazingira kwa manufaa ya wote.
 
 
 
 
 
 

 


📌 Jumla ya Megawati 50 kuingizwa kwenye Gridi ya Taifa ifikapo Machi 1, 2026

📌 Shilingi bilioni 118.6 zatumika katika ujenzi kwa awamu ya kwanza

📌 Maandalizi ya awamu ya pili (MW 100) yaanza.

Tanzania imeandika historia mpya katika sekta ya nishati baada ya kukamilika kwa ujenzi wa Mradi wa Kuzalisha Umeme kwa nishati ya jua ulioko Kishapu, mkoani Shinyanga mradi ambao ni mkubwa na wa kwanza wa aina yake nchini.

Akizungumza Februari 21, 2026 mara baada ya kukagua maendeleo ya mradi huo, Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Bw. Lazaro Twange, amesema kukamilika kwa mradi huo ni ushahidi wa dhamira thabiti ya Serikali ya Awamu ya Sita katika kuimarisha upatikanaji wa huduma ya umeme ya uhakika kwa Watanzania.

“Hii ni historia mpya imeandikwa kwa nchi yetu. Tangu tupate uhuru, hatujawahi kuwa na mradi mkubwa wa aina hii ya umeme wa jua. Serikali kupitia Wizara ya Nishati na TANESCO imeandika historia, na leo mmeshuhudia hapa umeme ukizalishwa. Mpaka kufikia Machi 1, 2026 jumla ya Megawati 50 zitakuwa zimeunganishwa kwenye Gridi ya umeme ya Taifa,” alisisitiza Bw. Twange.

Bw. Twange ametumia fursa hiyo kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuwezesha upatikanaji wa jumla ya Shilingi bilioni 118.6 kwa ushirikiano na Benki ya Maendeleo ya Ufaransa (AFD), fedha zilizowezesha utekelezaji wa awamu ya kwanza ya mradi huo.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Kishapu, Mhe. Peter Masindi, amesema mradi huo ni kichocheo muhimu cha ukuaji wa uchumi wa eneo hilo, hasa kwa vijana wanaojishughulisha na uchimbaji wa madini na shughuli za kilimo.

“Mradi huu umeleta ajira kwa wananchi wetu na umefungua ukurasa mpya wa maendeleo. Umeme wa uhakika utaongeza tija katika sekta za madini na kilimo, na kuchochea shughuli za kiuchumi na kijamii kwa wakazi wa Kishapu,” alisema Mhe. Masindi.

Naye Kaimu Meneja wa Kituo cha Kuzalisha Umeme Kishapu, Mhandisi Mariana Mrosso, alieleza kuwa kituo hicho kitaimarisha uthabiti wa Gridi ya Taifa na kuboresha ubora wa upatikanaji wa umeme, hususan kwa wateja wa maeneo ya mikoa ya Kanda ya Ziwa.

“Umeme unaozalishwa hapa utaongeza uwezo wa uzalishaji kwenye Gridi ya Taifa na kuboresha ufanisi wa huduma kwa wateja wetu hasa katika mikoa ya Kanda ya Ziwa,” alifafanua Mhandisi Mrosso.

Imeelezwa kuwa ifikapo Machi 1, 2026, megawati zote 50 zitakuwa zimeunganishwa kwenye Gridi ya Taifa. 

Wakati huo huo, TANESCO ipo katika hatua za mwisho za kumpata mkandarasi kwa ajili ya utekelezaji wa awamu ya pili ya mradi huo, itakayozalisha megawati 100 kwa gharama ya Shilingi bilioni 200.4 za kitanzania.

Mradi wa Umeme wa Jua Kishapu unatajwa kuwa alama ya mabadiliko makubwa na hatua muhimu katika mwelekeo wa Tanzania kutumia matumizi ya nishati jadidifu katika uzalishaji wa umeme, hatua inayolenga kuimarisha usalama wa nishati zinazozalishwa nchini na kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii kwa Taifa.














Naibu Mrajis - Uhamasishaji, Consolata Kiluma, amekipongeza chama kikuu cha Ushirika SIMCU (2018) LTD, kwa usimamizi wa ujenzi wa ujenzi na ukarabati wa kiwanda cha kuchakata pamba kilichopo wilayani Maswa mkoa wa Simiyu ambacho kinatarajiwa kuanza kazi musimu huu wa 2026/2027.

Ametoa pongezi hizo leo Februari 21, 2026 alipofanya ziara katika chama hicho kwa lengo kukagua na kuona hatua zilizofikiwa za ujenzi kuelekea uzinduzi wake.

Aidha amewataka viongozi wa SIMCU (2018) LTD, kuendelea kufufua viwanda vingine vinavyomilikiwa na chama ambavyo havifafanyi kazi kwa sasa ikiwa ni sehemu ya kuimarisha ushirika wa viwanda ili kuongeza thamani ya mazao ya wakulima.

Naye, Mwenyekiti wa SIMCU (2018) LTD, Ramadhani Matani, amesema juhudi mbalimbali zinaendelea kuhakikisha kiwanda kinaanza kufanya kazi haraka iwezekanavyo ambapo mpaka sasa wamefikia zaidi ya asilimia 75 ya ujenzi wa kiwanda hicho.

 


Na OWM - TAMISEMI, Dar es Salaam

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu -TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amewaelekeza Mameneja na waratibu wa Mradi wa Uendelezaji Miundombinu ya Miji Tanzania (TACTIC) kuhakikisha magari 14 aliyoyakabidhi yanakwenda kufanya kazi iliyokusudiwa ya usimamizi wa mradi huo ili wananchi wanufaike na barabara, masoko na stendi zinazojengwa kupitia mradi huo.

Prof. Shemdoe ametoa maelelezo hayo leo Februari 21, 2026, wakati wa hafla ya kukabidhi magari hayo kwa Mameneja wa TARURA wa Miji 12 ya kundi la kwanza la Mradi  wa TACTIC, iliyofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Millenium Tower  Kijitonyama, Dar es Salaam.

“Magari haya yamenunuliwa kwa fedha za umma, hivyo yatunzwe na yakatumike kwa kazi za usimamizi wa mradi wa TACTIC na si nyinginezo,” amesisitiza Prof. Shemdoe.

Aidha, Prof. Shemdoe amewata wakandarasi  walio kwenye maeneo ya utekelezaji wa miradi ya TACTIC, kuhakikisha  wanafanya kazi kwa ufanisi kwa kuzingatia mikataba waliosaini  ili miradi hiyo ikamilike kwa wakati, na kuongeza kuwa Serikali haitosita kusitisha mikataba inayosuasua kwa mujibu wa sheria na vipengele vya mikataba husika.

Prof. Shemdoe amesema Serikali haina changamoto ya kukosa fedha za utekelezaji miradi, kwani pindi mkandarasi akiwasilisha hati ya maombi ya malipo analipwa kwa wakati, hivyo hakuna sababu ya wakandarasi kushindwa kukamilisha na kukabidhi miradi kwa wakati.

Kwa upande wake, Meneja wa TARURA Wilaya ya Sumbawanga Mhandisi Albert Kyando ameishukuru Serikali kwa kuwakabidhi magari  yatakayowawezesha kusimamia miradi ya TACTIC kwa karibu   na kuahidi kuwa watayatunza kama Prof. Shemdoe alivyoelekeza kwa maslahi ya umma na taifa.

Naye, Mmoja wa Madereva waliokabidhiwa magari hayo kutoka Jiji la Arusha Bw. Joshua Magati, amesema watayatunza magari hayo kama alivyoelekeza Prof. Shemdoe, na kuongeza kuwa watazingatia muda wa kuyafanyia ukaguzi na matengenezo  pamoja na kuyatumia kwa kazi iliyokusudiwa ya usimamizi wa miradi ya TACTIC.