Nilianza kuchoka kihisia. Watu wengine walinicheka, wengine wakasema labda si majaliwa yangu. Nilijikuta nikiumia kimya kimya.
Nilianza kuchoka kihisia. Watu wengine walinicheka, wengine wakasema labda si majaliwa yangu. Nilijikuta nikiumia kimya kimya.
Nilianza kuwa na hofu na kukosa amani. Hata usingizi haukuwa mzuri. Nilijikuta nikijiuliza maswali mengi bila kupata majibu. Siku moja nilimweleza rafiki yangu hali yangu. SOMA ZAIDI.

Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC), kwa kushirikiana na Wakala wa Kimataifa wa Nguvu za Atomu (IAEA), imeanza kuimarisha maandalizi ya usalama wa nyuklia na mionzi kuelekea Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2027, ambazo Tanzania itakuwa mwenyeji kwa pamoja na Kenya na Uganda.
Maandalizi hayo yanalenga kujenga uwezo wa kitaifa wa kuzuia, kubaini na kukabiliana na vitisho vinavyoweza kuhusisha nyenzo za nyuklia au vyanzo vingine vya mionzi wakati wa mashindano hayo, ambayo yanatarajiwa kuvutia wachezaji, viongozi, mashabiki, waandishi wa habari na wageni kutoka mataifa mbalimbali.
Akifungua rasmi jijini Arusha warsha ya siku tano kuhusu uandaaji na utekelezaji wa hatua za usalama wa nyuklia katika matukio makubwa ya umma, Mkurugenzi Mkuu wa TAEC, Profesa Najat Kassim Mohammed, amesema ukubwa na hadhi ya AFCON 2027 vinahitaji maandalizi ya kina na ushirikiano wa taasisi mbalimbali ili kuhakikisha mashindano hayo yanafanyika katika mazingira salama.
Warsha hiyo, inayofanyika kuanzia Agosti 31 hadi Septemba 4, 2026, inawakutanisha wataalamu na maofisa kutoka Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Jeshi la Polisi Tanzania, vyombo vya usalama, mamlaka zinazohusika na forodha na uhamiaji, wasimamizi wa viwanja vya michezo pamoja na taasisi nyingine zenye majukumu katika ulinzi na usalama.
Profesa Najat amesema maandalizi ya mashindano yenye hadhi ya AFCON hayaishii katika ujenzi na uboreshaji wa viwanja na miundombinu mingine pekee, bali yanapaswa kwenda sambamba na kuimarisha mifumo ya usalama kwa ajili ya kulinda wananchi na wageni watakaokuwa nchini wakati wa mashindano hayo.
Amesema mikusanyiko mikubwa ya kimataifa inahitaji maandalizi yanayozingatia aina mbalimbali za vitisho na hatari zinazoweza kujitokeza, hivyo ni muhimu kwa taasisi zinazohusika kuwa na uwezo wa kubaini mapema jambo lolote lisilo la kawaida na kuchukua hatua stahiki kwa wakati.
“Ni lazima kuhakikisha kuwa vifaa vya mionzi na nyenzo nyingine zinazohusiana na nyuklia hazitumiki kwa madhumuni ya uhalifu, uharibifu au matumizi mengine yasiyoruhusiwa wakati wa AFCON 2027,” amesema Profesa Najat.
Amesisitiza kuwa usalama wa nyuklia katika matukio makubwa ya umma hauwezi kusimamiwa na taasisi moja pekee, bali unahitaji ushirikiano wa karibu, uratibu na ubadilishanaji wa taarifa kati ya taasisi zote zenye wajibu katika mfumo wa kitaifa wa ulinzi na usalama.
Kwa mujibu wa Profesa Najat, mafanikio katika eneo hilo yatategemea kwa kiasi kikubwa uwezo wa taasisi zinazohusika kufanya kazi kwa pamoja, kila moja ikifahamu wajibu wake na namna ya kushirikiana na taasisi nyingine kabla, wakati na baada ya tukio.
Amesema warsha hiyo ni sehemu ya maandalizi yanayolenga kujenga uelewa wa pamoja miongoni mwa taasisi zinazohusika, kuimarisha uwezo wa wataalamu na kuhakikisha mifumo ya uratibu inafanya kazi kwa ufanisi endapo kutatokea tukio linalohitaji hatua za kiusalama.
Tanzania tayari imeendelea kuchukua hatua za kuimarisha uwezo wake katika eneo la usalama wa nyuklia na mionzi, ikiwemo matumizi ya vifaa vya kugundua mionzi katika baadhi ya maeneo muhimu na mipakani, pamoja na kuwajengea uwezo maofisa walio mstari wa mbele katika kubaini na kukabiliana na matukio yanayoweza kuhusisha vyanzo vya mionzi.
Profesa Najat amesema pamoja na uwepo wa vifaa hivyo, jambo la msingi ni kuhakikisha wataalamu wana uwezo wa kuvitumia kwa usahihi na taasisi zinazohusika zinafahamu hatua zinazopaswa kuchukuliwa baada ya kubainika kwa tukio linalohitaji uchunguzi zaidi.
Katika kipindi cha siku tano, washiriki watapatiwa mafunzo ya nadharia na vitendo kuhusu hatua za kuzuia vitisho kabla ya tukio, namna ya kuendesha operesheni za usalama katika matukio makubwa, utambuzi wa mionzi, tathmini ya tahadhari, taratibu za upekuzi na matumizi ya vifaa mbalimbali vya kugundua mionzi.
Miongoni mwa vifaa vitakavyotumika katika mafunzo hayo ni Personal Radiation Detectors (PRDs), Radioisotope Identification Devices (RIDs) pamoja na vifaa vya kugundua mionzi vinavyobebwa mgongoni. Washiriki watafundishwa namna ya kutumia vifaa hivyo, kutambua tahadhari zinazotolewa na kufanya tathmini kabla ya hatua nyingine kuchukuliwa.
Mafunzo pia yatahusisha taratibu za kufanya uchunguzi kwa watu na magari, namna ya kuthibitisha tahadhari inayotolewa na vifaa vya kugundua mionzi, pamoja na taratibu za kushughulikia vifurushi vinavyotiliwa shaka.
Profesa Najat amesema sehemu muhimu ya warsha hiyo itakuwa mazoezi ya vitendo yatakayowawezesha washiriki kutumia maarifa watakayopata darasani katika mazingira yanayofanana na hali halisi ya tukio kubwa la umma.
Washiriki watagawa majukumu katika timu mbalimbali, zikiwemo timu ya uongozi wa operesheni, timu za utafutaji na timu ya msaada wa kitaalamu wa masuala ya mionzi. Timu hizo zitafanya maandalizi ya uchunguzi wa eneo kabla ya tukio, kuandaa namna ya kukabiliana na hali mbalimbali na kugawana majukumu kulingana na wajibu wa kila upande.
Mazoezi hayo yatahusisha pia uchunguzi wa kimionzi katika mazingira ya uwanja wa michezo, ikiwemo eneo la uwanja na sehemu za kukaa watazamaji. Lengo ni kuwajengea washiriki uzoefu wa kufanya uchunguzi kabla ya tukio na kutambua mapema hali yoyote inayohitaji hatua zaidi.
Profesa Najat amesema mazoezi hayo yatasaidia kutathmini uwezo uliopo na kubaini maeneo yanayohitaji kuendelea kuimarishwa katika kipindi kilichobaki kuelekea AFCON 2027.
Amesema, hata hivyo, maandalizi hayo hayaishii katika AFCON pekee kwa sababu utaalamu, vifaa na mifumo ya ushirikiano inayojengwa sasa itabaki kuwa sehemu ya uwezo wa Taifa katika kusimamia usalama wa matukio mengine makubwa yatakayofanyika nchini.
“Uwezo tunaoujenga kupitia warsha hii utakuwa rasilimali ya kudumu kwa Taifa letu na utatumika katika kulinda mikutano ya kimataifa, mashindano ya michezo, ziara za viongozi, mikusanyiko mikubwa ya kitaifa na matukio mengine yenye umuhimu mkubwa kwa nchi,” amesema Profesa Najat.
Ameongeza kuwa moja ya mambo yanayotarajiwa baada ya warsha hiyo ni kuwa na mwelekeo wa pamoja kuhusu hatua zinazopaswa kuchukuliwa katika kipindi kilichobaki kuelekea AFCON 2027, huku kila taasisi ikifahamu eneo lake la wajibu na namna ya kushirikiana na taasisi nyingine.
Profesa Najat ameishukuru IAEA kwa kuendelea kushirikiana na Tanzania katika kujenga uwezo wa wataalamu na kuimarisha mifumo ya usalama wa nyuklia, akisema ushirikiano huo umekuwa muhimu katika kupata utaalamu, mafunzo na uzoefu unaohitajika katika kukabiliana na changamoto zinazoweza kujitokeza.

Kwa upande wake, Kiongozi wa Timu ya Wataalamu kutoka IAEA, Lacina Saro, amepongeza Tanzania kwa kuanza mapema maandalizi ya usalama wa nyuklia kuelekea AFCON 2027, akisema tukio kubwa la aina hiyo linahitaji mipango ya kina, mafunzo na mazoezi ya kutosha kabla ya kuanza kwa mashindano.
“Uchaguzi wa Tanzania kuwa miongoni mwa wenyeji wa AFCON 2027 ni jambo la kujivunia, lakini pia unaambatana na wajibu. Mpangilio wa usalama wa nyuklia wa kiwango hiki unapaswa kuandaliwa mapema, kufanyiwa majaribio kwa kina na kutekelezwa kwa ufanisi na timu za kitaifa zilizopewa mafunzo,” amesema Saro.
Amesema IAEA itaendelea kushirikiana na Tanzania kupitia utoaji wa miongozo, mafunzo na msaada wa kiufundi unaolenga kuimarisha uwezo wa nchi katika usalama wa nyuklia.
“Tuko hapa kufanya kazi pamoja nanyi na kuunga mkono Tanzania katika kujenga uwezo wa usalama wa nyuklia ambao mnaweza kuutegemea wakati wa AFCON 2027 na hata baada ya mashindano hayo,” amesema Saro.
Naye Mkurugenzi wa Teknolojia na Huduma za Ufundi wa TAEC, Dkt. Remigius Kawala, amesema Tanzania inaendelea kujiandaa katika eneo la usalama wa nyuklia na mionzi huku Serikali ikiendelea kuwekeza katika wataalamu, vifaa na mifumo inayohitajika kuhakikisha mashindano hayo yanafanyika katika mazingira salama.
Dkt. Kawala amesema Tanzania ina wataalamu wenye ujuzi pamoja na vifaa vinavyoweza kutumika katika kubaini na kukabiliana na vitisho vinavyoweza kuhusisha mionzi, huku mafunzo yanayoendelea yakilenga kuongeza uwezo wa taasisi mbalimbali kufanya kazi kwa pamoja.
Amesema maandalizi hayo yanalenga pia kujenga uwezo wa muda mrefu utakaotumika kulinda wananchi na miundombinu muhimu wakati wa matukio mengine makubwa yatakayofanyika nchini.
Dkt. Kawala amewataka washiriki kutumia kikamilifu fursa ya mafunzo hayo kuongeza ujuzi, kubadilishana uzoefu na kuimarisha uratibu baina ya taasisi zao, hatua ambayo itasaidia kuongeza utayari wa nchi kuelekea mashindano hayo.
Warsha hiyo itahitimishwa Septemba 4, 2026, baada ya washiriki kupitia mafunzo ya darasani na mazoezi ya vitendo yatakayohusisha maandalizi ya eneo, uchunguzi wa kimionzi, tathmini ya tahadhari na namna ya kuchukua hatua pale tukio lisilo la kawaida linapobainika.
TAEC itaendelea kushirikiana na taasisi za kitaifa na washirika wa kimataifa katika kuimarisha usalama wa nyuklia na mionzi nchini, huku maandalizi ya AFCON 2027 yakitumika pia kama fursa ya kuongeza uwezo wa wataalamu na kuimarisha mifumo itakayoendelea kutumika hata baada ya mashindano hayo.
Hatua hiyo ni sehemu ya jitihada za kuhakikisha Tanzania inaingia katika AFCON 2027 ikiwa imejiandaa si katika viwanja na miundombinu pekee, bali pia katika eneo la usalama, ili wananchi na wageni watakaofika nchini waweze kushiriki na kufurahia mashindano hayo katika mazingira salama.










Benki Kuu ya Tanzania (BoT) imewataka wasanii na wadau wengine wenye ushawishi kwa jamii kuwa mabalozi wa elimu ya matumizi sahihi ya fedha, ikiwemo umuhimu wa kutunza noti na sarafu kwa usahihi.
Na Munir Shemweta, MOROGORO
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii, Mhe. Timotheo Mzava, ameitaka Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi kuongeza nguvu katika kuboresha na kupanua Chuo cha Ardhi Morogoro (ARIMO) ili kuongeza uwezo wa kuzalisha wataalamu wengi zaidi katika sekta ya ardhi.
Aidha, Mhe. Mzava ameitaka Wizara ya Ardhi kwa kushirikiana na Mamlaka za Serikali za Mitaa (Mamlaka za Upangaji) katika kuweka utaratibu wa kutumia wataalamu wanaozalishwa na vyuo vya ardhi kusaidia wananchi kutatua changamoto za ardhi na hivyo kupunguza migogoro inayojitokeza katika maeneo mbalimbali nchini.
Mhe. Mzava ametoa kauli hiyo, Agosti 30, 2026, wakati wa ziara ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii katika Chuo cha Ardhi Morogoro (ARIMO), mkoani Morogoro.
Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mhe. Mzava amekipongeza Chuo cha Ardhi Morogoro kwa kazi kinayoifanya ya kuwaandaa vijana kitaaluma licha ya kukabiliwa na changamoto mbalimbali.
“Nikipongeze Chuo cha Ardhi Morogoro. Pamoja na changamoto zake, kinafanya kazi nzuri ya kuwaandaa vijana ili watumikie Taifa lao.”
Amesema, chuo hicho ni taasisi muhimu katika uzalishaji wa wataalamu wa sekta ya ardhi na kwamba ni muhimu kuendelea kuboresha mipango yake ya maendeleo, ikiwemo kutekeleza mpango kabambe wa chuo.
Amebainisha kuwa, anatamani kuona mabadiliko makubwa katika vyuo vya Ardhi vya Morogoro na Tabora, ikiwa ni pamoja na kuboreshwa kwa miundombinu, mazingira ya kujifunzia na uwezo wa vyuo hivyo kuzalisha wataalamu wenye ujuzi unaoendana na mahitaji ya soko.
Kwa upande wake, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo, ameishukuru Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa kutembelea Chuo cha ARIMO na kujionea shughuli zinazofanyika katika chuo hicho.
Waziri Akwilapo ameihakikishia Kamati ya Kudumu ya Bunge kuwa Wizara yake itakiangalia kwa karibu Chuo cha Ardhi Morogoro ili kuhakikisha wanafunzi wanapata mazingira bora ya kusomea na kujifunzia.
Nao wajumbe wa Kamati wamekipongeza Chuo cha Ardhi Morogoro na Wizara kwa ujumla kwa kazi nzuri inayofanyika katika kuendeleza elimu ya ardhi nchini.
Hata hivyo, wamependekeza chuo kuangalia uwezekano wa kuongeza na kuanzisha kozi mbalimbali tofauti na zile zinazotolewa kwa sasa, ili kukidhi mahitaji ya soko la ajira na kuongeza fursa kwa vijana.
Wajumbe hao pia wamekishauri chuo kuanza mapema kutafuta maeneo ya ardhi kwa ajili ya upanuzi wa shughuli zake katika miaka ijayo, wakieleza kuwa si jambo baya kwa chuo kutafuta eneo katika mikoa mingine, ikiwemo Iringa, kwa ajili ya shughuli za kitaaluma na maendeleo ya chuo.
Vile vile wamesisitiza umuhimu wa upatikanaji wa vifaa vya kisasa kwa lengo la kusaidia wanafunzi kupata mafunzo yanayozingatia teknolojia za kisasa na kuwawezesha kushindana katika soko la ajira ndani na nje ya nchi.
Katika ziara yake ya siku moja katika Chuo cha Ardhi Morogoro Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi Maliasili na Utalii ilipata taarifa maendeleo ya chuo Pamoja na kukagua mradi wa ujenzi wa madarasa Pamoja mpango wa uendelezaji chuo katika eneo la Mlimakola mkoani Morogoro.
>AWATAKA WATUMISHI KUACHA KUFANYA KAZI KWA MAZOEA
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Deogratius Ndejembi, amewataka watumishi wa Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira kuongeza bidii, uwajibikaji na kuachana na utendaji wa kazi kwa mazoea ili kuhakikisha majukumu ya Serikali yanatekelezwa kwa ufanisi na kwa wakati.
Makamu wa Rais ametoa wito huo leo, alipofanya ziara yake ya kwanza katika Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), iliyopo Mtumba, jijini Dodoma, ambako alipokelewa na wafanyakazi pamoja na Menejimenti ya Wizara hiyo.
Amesisitiza umuhimu wa watumishi kubadili mitazamo na namna ya kufanya kazi, akitaka kila mmoja kuwa mbunifu na kuweka mipango inayolenga kuleta matokeo yanayoonekana kwa wananchi na Taifa kwa ujumla.
Makamu wa Rais amewasihi watumishi kutumia nafasi zao kutoa huduma yenye thamani kwa watanzania na kutambua dhamana waliyonayo katika kuwahudumia wananchi. Pia amewataka kubadili mitazamo na namna ya kufikiri, kuwa wabunifu na kuhakikisha mipango inayowekwa inaleta tija na matokeo chanya katika shughuli mbalimbali zinazotekelezwa kwa maslahi mapana ya Taifa.
Halikadhalika, amewataka kuongeza jitihada katika kudumisha Muungano kwa kuwa na mipango endelevu inayolenga kutatua changamoto mbalimbali pamoja na kutoa elimu ya fursa zilizopo katika Muungano.
Amewasihi Viongozi na Watumishi wa Wizara hiyo, kuwa na mipango endelevu katika utekelezaji wa ajenda ya ulinzi na uhifadhi wa mazingira kwa kutumia vema kampeni za upandaji miti, usafi wa majiji na miji kwa kuweka nyenzo zitakazosaidia kufanya hali hiyo kuwa endelevu. Vile vile amesisitiza umuhimu wa kuwa na Mpango maalum utakao saidia wananchi kuhama katika shughuli za kila siku zinazoharibu mazingira.
Awali, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhandisi Hamad Masauni, amempongeza Makamu wa Rais kwa kuaminiwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika nafasi hiyo na kumhakikishia ushirikiano katika kutekeleza majukumu mbalimbali yanayohusu Ofisi ya Makamu wa Rais.
Akiwasilisha taarifa kuhusu shughuli zinazotekelezwa na idara mbalimbali zilizo chini ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Katibu Mkuu, Ofisi ya Makamu wa Rais Dkt. Richard Muyungi, amesema wizara hiyo ina Idara nne, Vitengo nane na Taasisi mbili zinazotekeleza majukumu mbalimbali, ikiwemo utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 katika masuala ya Muungano na Mazingira.
Na WMA - MWANZA
Meneja wa Wakala wa Vipimo (WMA) Mkoa wa Geita, Bi. Eva Ikula amesema usimamizi wa matumizi sahihi ya vipimo unaofanywa na WMA umewezesha bidhaa za Tanzania kuaminiwa na kukubalika zaidi katika soko la kimataifa.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Agosti 31, 2026 katika banda la WMA wakati wa Maonesho ya Biashara ya Afrika Mashariki yanayoendelea katika Viwanja vya Furahisha jijini Mwanza, Bi. Ikula amesema mojawapo ya sababu kubwa ya bidhaa za Tanzania kukubalika katika soko la kimataifa ni uhakika wa vipimo.
"Kilo yetu ni kilo ya Kenya, ya India, na ya Ujerumani pia. Hiyo ndiyo nguvu ya matumizi ya vipimo sahihi."
Amesema WMA inaendelea kutoa elimu kupitia kampeni mbalimbali ili kujenga uelewa kuwa "Kipimo sahihi ni pasipoti ya bidhaa yako kuingia soko lolote duniani."
Amebainisha kuwa wanunuzi wa kimataifa wanaiamini Tanzania kwa sababu WMA inatumia mfumo mmoja wa kimataifa wa vipimo - SI Units.
"Matokeo yake ni rahisi. Mkataba unapotiwa saini London, Beijing au Johannesburg, wanajua kilo ya Tanzania ni sawa na kilo yao," amesema.
Amehitimisha kwa kusema WMA haijali tu kilo na lita bali inajenga imani.
" Tunapouza kwa kipimo sahihi, tunauza kwa heshima. Na dunia inaheshimu wale wanaouza kwa heshima."
Maonesho ya Biashara ya Afrika Mashariki yalianza Agosti 28 na yanatarajiwa kuhitimishwa Septemba 6, 2026 yakiongozwa na kaulimbiu isemayo "Usalama na Amani ni Kichocheo cha Biashara na Uwekezaji".
▪️Azindua na Zoezi la Urushaji wa Helikopta ya Utafiti wa Madini ya Barrick
▪️Maeneo ya Leseni za Vijana,Wanawake na Wenye Ulemavu Kufanyiwa Utafiti kwa Helikopta
▪️Rais Dkt. Samia Apongezwa kwa Maelekezo na Maono Yake Sekta ya Madini
▪️Baraza la Dhahabu Duniani Lavutiwa na Programu ya MBT
▪️Waziri Mavunde Aagiza Mitambo ya Uchorongaji ya STAMICO Kufika Mara Baada ya Utafiti Kukamilika
Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde, amezindua rasmi Programu ya Mining for a Brighter Tomorrow (MBT), maarufu kama “Kesho Iliyo Njema,” na kueleza kuwa programu hiyo ni hatua ya kimkakati ya Serikali katika kufungua milango mipya ya fursa na uwezeshaji kwa vijana, wanawake na watu wenye mahitaji maalum kushiriki kikamilifu katika Sekta ya Madini na kwamba programu inalenga kuwasaidia walengwa kuondokana na uchimbaji wa kubahatisha na kuelekea kwenye uchimbaji wenye tija, unaotumia maarifa, teknolojia na taarifa sahihi za kijiolojia, huku Serikali ikiendelea kuweka mazingira wezeshi ya upatikanaji wa maeneo ya uchimbaji, leseni na fursa za kiuchumi zinazotokana na rasilimali madini.
Waziri Mavunde amebainisha hayo, leo Agosti 31, 2026, katika eneo la Nyamongo, Wilaya ya Tarime, Mkoani Mara, wakati akizungumza katika hafla hiyo iliyokwenda sambamba na uzinduzi wa utafiti wa kina wa madini unaofanywa na Barrick Gold Corporation,
Mhe. Mavunde ametumia nafasi hiyo kumpogeza na kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa maelekezo na maono yake ya kuweka mazingira wezeshi kwa makundi hayo na kuongeza kuwa Rais Dkt. Samia ameagiza asilimia 10 ya mapato yatokanayo na makusanyo ya Sekta ya Madini kutengwa kwa ajili ya utafiti wa kina wa madini, hatua ambayo inalenga kuongeza taarifa za rasilimali madini nchini na kufungua fursa zaidi kwa wananchi.
Waziri Mavunde pia ameishukuru Barrick kwa kukubali kufanya utafiti katika maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya wachimbaji wadogo Nyamongo, akieleza kuwa ndani ya wiki mbili utafiti huo unaweza kufanyika katika eneo lenye ukubwa wa takribani kilomita za mraba 6,000 na kusisitiza kuwa dhamira ya Serikali kuhakikisha matokeo ya utafiti yanageuka kuwa fursa halisi kwa wananchi, sambamba na kumuelekeza Kamishna wa Madini, kwa kushirikiana na GST na STAMICO, kukaa na Barrick na kuhakikisha mara utafiti utakapokamilika, mitambo ya uchorongaji inafika Nyamongo kwa ajili ya hatua inayofuata ya utafiti.
Aidha, Waziri Mavunde amesema uzinduzi huo unaashiria mwanzo wa safari ya kujenga “Kesho Iliyo Njema” katika Sekta ya Madini, huku akieleza kuwa Rais wa Baraza la Dhahabu Duniani (World Gold Council) amevutiwa na programu ya MBT na kwamba vijana wa Nyamongo ndio watakaokuwa miongoni mwa vijana wa kwanza kunufaika na mpango huo.
“Tunaenda kupanda mbegu, tunaanza safari; leo mnaianza safari ya kwenda kubadilisha maisha yenu na mimi nitasimamia programu hii ili tufikie lengo,” amesema Mavunde.
Kwa upande mwingine, Waziri Mavunde amesema kuwa amedhamiria kuipima Maafisa Madini Wakazi wa Mikoa ya Kimadini kwa kuhakikisha maeneo maalum yanatengwa kwa ajili ya makundi ya vijana na wanawake, huku leseni zikitolewa kwa kasi ili kuwawezesha kushiriki katika shughuli za uchimbaji, amesema lengo ni kuona programu ya MBT ikienda sambamba na ukusanyaji wa maduhuli na kwamba angependa kuona kila siku fursa mpya za leseni zikitolewa kwa vijana kupitia programu hiyo. Aidha, ametoa wito kwa viongozi wa vijana wachimbaji kuweka pembeni tofauti zao, kushirikiana na kuepuka kuwagawa vijana, akisisitiza kuwa Serikali haitakubali migogoro ya makundi iwe kikwazo cha utekelezaji wa programu hiyo.
Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Mara, Brigedia Jenerali Evans Mtambi amesema kuwa, Kupitia programu hiyo na tafiti zinazofanyika, tunaamini vijana wataweza kuchimba kisayansi zaidi, kwa kutumia taarifa na teknolojia badala ya kuchimba kwa kubahatisha na kwamba hatua hiyo itasaidia kupunguza gharama na hasara zisizo za lazima, kuongeza tija na hatimaye kuwawezesha wachimbaji wetu kupata matokeo makubwa zaidi kutokana na juhudi wanazoweka katika shughuli zao na kwamba ukosefu wa taarifa sahihi zinazoweza kuwaongoza wachimbaji kujua madini yapo wapi kwa kiwango gani na namna bora ya kuyafikia ndiyo ilikuwa changamoto kubwa.
Awali, Meneja Mkazi (Country Manager) wa Kampuni ya Barrick Gold nchini Tanzania, Dkt. Melkiory Ngido ameeleza kuwa kama Barrick wanajivunia kuwa miongoni mwa wadau walioshiriki katika programu tangu mwanzo.
“Tulichukua hatua ya kimkakati ya kurudisha leseni ya eneo ambalo tayari tulikuwa tumelifanyia utafiti na kubaini kuwa lina uwezo wa kutoa fursa kwa makundi ya wachimbaji wadogo. Tuliona ni muhimu eneo hilo lisibaki chini ya umiliki wetu wakati linaweza kuwa chanzo cha ajira, kipato na fursa za kiuchumi kwa Watanzania wanaojihusisha na uchimbaji mdogo. Hatua hii inaakisi dhamira yetu ya kushirikiana na Serikali katika kuhakikisha rasilimali za madini zinawanufaisha wananchi na zinachangia maendeleo ya jamii zinazozunguka maeneo ya migodi.” Amesema Ngido
Makamu Rais wa FEMATA, Victor Tesha ameeleza kuwa wao kama wachimbaji wadogo wa madini nchini Tanzania wanayo furaha kubwa kwa hatua hii iliyofikiwa na wanaiona programu ya Mining for a Brighter Tomorrow (MBT) kama hatua muhimu sana katika kutatua changamoto ambazo zimekuwa zikituathiri kwa muda mrefu, ameongeza kuwa wana imani kubwa na Serikali na wanaamini kupitia programu hiyo, maisha ya wachimbaji wadogo na familia zinazotegemea shughuli za madinj yanaenda kubadilika kwa kiwango kikubwa.



































