Na Oscar Assenga,LUSHOTO

Benki ya CRDB imeendelea kudhihirisha dhamira yake ya kuchangia maendeleo ya jamii kwa kutoa zaidi ya shilingi bilioni 2.7 katika mwaka uliopita, fedha ambazo zimeelekezwa kwa kiasi kikubwa katika sekta ya elimu na uwezeshaji wa wananchi kiuchumi.

Akizungumza katika hafla ya kukabidhi vyumba viwili vya madarasa pamoja na ofisi ya walimu katika Shule ya Msingi Kwendoghohi, iliyopo Kata ya Usambara wilayani Lushoto, Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi Taasisi ya CRDB Bank Foundation, Marian Balampama, alisema kati ya fedha hizo, shilingi bilioni 1 zimetumika kuboresha elimu.

Alieleza kuwa uwekezaji huo umejumuisha ujenzi wa madarasa, ununuzi wa madawati, pamoja na upatikanaji wa vifaa vya kufundishia na kujifunzia, ikiwemo maabara. Alisisitiza kuwa benki hiyo haijikita tu katika miundombinu, bali pia inahakikisha mwanafunzi anapata mazingira salama na bora ya kujifunzia.

Mbali na elimu, CRDB pia imewekeza katika kuwawezesha wananchi kiuchumi kupitia programu mbalimbali. Balampana alisema benki hiyo inaamini kuwa kumwezesha mtu mmoja ni sawa na kuinua familia na jamii kwa ujumla.

Kupitia kampuni tanzu ya CRDB Bank Foundation na programu ya Embeju, zaidi ya wanufaika 500,000 pamoja na vikundi mbalimbali wamenufaika. Alifafanua kuwa uwezeshaji huo hauishii kwenye utoaji wa fedha pekee, bali pia unahusisha mafunzo ya ujuzi na mbinu za kutambua masoko ili kuongeza tija na faida.

Aidha, alibainisha kuwa benki hiyo imekuwa ikiangalia pia changamoto nyingine za kijamii, ikiwemo upatikanaji wa huduma za afya, kwa lengo la kuboresha ustawi wa wananchi kwa ujumla.

“Sisi tunajisikia fahari kushirikiana na Serikali, hususan katika kusimamia mikopo ya asilimia 10 katika baadhi ya mikoa, ili kuhakikisha fedha zinawafikia walengwa na kuleta matokeo chanya,” alisema Balampana.

Aliongeza kuwa CRDB inaendelea kushirikiana kwa karibu na viongozi wa Wilaya ya Lushoto pamoja na Mkoa wa Tanga katika kutekeleza miradi ya maendeleo.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Lushoto, Zephania Sumaye, aliishukuru benki hiyo kwa mchango huo, akisema ujenzi wa madarasa hayo utasaidia kupunguza msongamano wa wanafunzi na kuboresha mazingira ya kujifunzia.

Alieleza kuwa shule hiyo, iliyoanzishwa mwaka 1965, ilikuwa na miundombinu iliyochakaa, hivyo msaada huo unaleta matumaini mapya katika kuinua ubora wa elimu katika eneo hilo.

Kwa ujumla, hatua ya CRDB inaonesha namna taasisi za kifedha zinavyoweza kuwa chachu ya maendeleo kwa kurejesha kwa jamii sehemu ya mapato yao, sambamba na kuunga mkono juhudi za Serikali kufikia dira ya maendeleo ya Taifa ya mwaka 2050.







Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi amesema Serikali inachukua hatua katika kuimarisha uwezeshaji wanawake kiuchumi pamoja na kuongeza uelewa kuhusu mifuko ya maendeleo inayowanufaisha wanawake.

Akizungumza Mei 6, 2026 bungeni jijini Dodoma, Mhe. Mahundi amesema Serikali imeweka mikakati mbalimbali ya kuhakikisha wanawake wengi zaidi wanapata taarifa na kunufaika na Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake (WDF), ikiwa ni pamoja na kushirikiana na taasisi za fedha na wadau wa maendeleo kutoa mafunzo ya ujasiriamali na uendeshaji wa biashara kupitia makongamano ya kikanda.

 “Serikali itaendelea kushirikiana na Wizara ya Fedha, TAMISEMI pamoja na Baraza la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi kuhakikisha makundi ya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu yanapatiwa mafunzo na fursa za mikopo nafuu.” amesema Mhe. Mahundi

Katika swali lingine, ameeleza kuwa Serikali inaendelea kuimarisha mifuko iliyopo badala ya kuanzisha mipya, ikiwemo Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake unaotoa mikopo yenye masharti nafuu kwa wanawake wajasiriamali. 

"Kupitia ushirikiano na Benki ya Dunia, Serikali ipo katika hatua za mwisho za kuanza utoaji wa mikopo kupitia mradi wa PAMOJA, hatua itakayopanua wigo wa wanawake kunufaika na fursa za kiuchumi". amesema Mhe. Mahundi

Ameeleza kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na sekta binafsi, taasisi za fedha na wadau wa maendeleo ili kuhakikisha wanawake wanajengewa uwezo wa kiuchumi na kuchangia kikamilifu katika maendeleo ya taifa.

Dar es Salaam, Mei 5, 2026

Kampuni changa (startups) nchini waaswa kuongeza juhudi katika kukuza ubunifu na kuugeuza kuwa bidhaa ama huduma zenye ushindani, hatua iliyotajwa kuwa mhimili muhimu wa kukuza uchumi wa taifa na kuimarisha ajira kwa vijana.

 


Maadhimisho ya siku ya Urithi wa Dunia Afrika yaliyofanyika katika Makumbusho ya Urithi Jiopaki mjini Karatu tarehe 5 Mei, 2026 yameyakutanisha  wanafunzi wa shule za msingi na sekondari ikiwa na lengo la kuwarithisha kizazi kipya historia na elimu ya urithi na utamaduni.

Mkuu wa wilaya ya Karatu Mhe. Dkt Lameck Karanga amesema uwepo wa makabila hayo, historia yao pamoja na kuenzi tamaduni zao ni utajiri mkubwa kwa Tanzania na kutoa wito kwa wadau na jamii kwa ujumla kuendelea kulinda maeneo ya urithi wa dunia na kuibua maeneo mapya yatakayoingizwa katika orodha ya Urithi wa Dunia ili kuongeza thamani ya ubora wa kipekee ulimwenguni (Outstanding Universal Value) na kuvutia wageni wengi zaidi.

Naibu Kamishna wa Uhifadhi, Utalii na Maendeleo ya Jamii Ngorongoro Joas Makwati ameeleza kuwa mamlaka itaendelea kuongeza juhudi za kulihifadhi eneo la Ngorongoro ambalo ni urithi wa dunia na  kultangazia zaidi kama eneo pekee lenye Ushahidi wa kisayansi  kuhusu historia ya binadamu unaoeleza kuwa binadamu kwa kuthibitishwa na ugunduzi wa masalia ya binadamu wa kale na zana za mawe zilizopatikana katika bonde la Olduvai. 

Kwa upande wake Naibu Katibu wa Tume ya Taifa ya UNESCO Tanzania Dkt. Khamis Said ameeleza kuwa tangu Tanzania ijiunge na UNESCO imepata mafanikio mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuridhia mikataba kumi (10) ya  UNESCO,Kuwepo kwa Hifadhi Hai za Mwanadamu na Mazingira  sita (6)  na Kuwepo kwa maeneo saba (7) ya urithi wa Dunia.

Kauli mbiu ya siku ya urithi wa dunia kwa mwaka huu ni “Kusherekea siku ya Urithi wa Dunia na kukuza Viongozi wa baadaye”. (Celebrating Africa’s Heritage, Mentoring the Leaders of Tomorrow).

Chuo Kikuu Mzumbe kupitia Shule yake ya Biashara kimeandaa tukio la Siku ya Mzumbe na Kambi ya Wajasiriamali, litakalofanyika kwa mara ya kumi mfululizo katika Kampasi Kuu Morogoro, kuanzia Mei 6 hadi 8, 2026.

 



Na OWM - TAMISEMI, Dodoma


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) Mhe. Prof. Riziki Shemdoe na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof.  Adolf Mkenda wamewapokea walimu wapatao 150 wa amali waliokwenda kwenye ziara ya mafunzo ya mwezi mmoja nchini India, ambayo yatawawezesha kutoa elimu ya ufundi na mafunzo ya stadi za kazi nchini ili kukuza uchumi wa viwanda, kupunguza ukosefu wa ajira kwa vijana, na kuwajengea uwezo wa kushindana katika soko la ajira.

Walimu hao mara baada ya kurejea nchini, walipata mwaliko wa Mhe. Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba kuhudhuria shughuli za Bunge Mei 04, 2026 jijini Dodoma na kupokelewa kwa pamoja na Waziri wa TAMISEMI Mhe. Prof Shemdoe na Waziri wa Elimu Mhe. Prof. Mkenda ambao ofisi zao ziliratibu ziara ya mafunzo ya walimu hao  nchini India.

Akizunguza na walimu hao katika viwanja vya Bunge, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu -TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe ameshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuidhinisha fedha kiasi cha Shilingi Bilioni 3 na kutoa kibali cha walimu hao kwenda kwenye ziara ya mafunzo nchini India ili kujifunza na kupata ujuzi utakaowawezesha kuleta athari chanya zaidi katika mfumo wa elimu ya ufundi.

Sanjari na hilo, Prof. Shemdoe amewataka walimu hao kuhakikisha yote waliyojifunza nchini India wanaenda kuwafundisha wanafunzi madarasani na kwa vitendo ili wapate ujuzi utakaowawezesha kuwa wabunifu, wajasiriamali na uwezo wa kushindana katika ajira za ndani na nje ya nchi ikiwa ni pamoja na kujiajiri.

“Vijana wetu wanahitaji kupata maarifa na ujuzi mlioupata kwenye ziara yenu ya mafunzo nchini India, hivyo nendeni mkawafundishe kwa umahiri ili waje kutoa mchango katika maendeleo ya taifa,” amesisitiza Prof. Shemdoe.

Naye, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof.  Adolf Mkenda amesema kuwa Serikali iliwapeleka walimu hao wapatao 150 nchini India kwenda kujifunza namna wanavyoendesha shule za amali na kutekeleza mtaala wao wa elimu ili wakirejea nchini waweze kuwa chachu ya kutekeleza vema mtaala mpya wa elimu kwa kutumia vema teknolojia iliyopo katika kuwafundisha vijana wa kitanzania elimu ya ufundi stadi.

“Sisi tulichukua walimu 150 na kuwapeleka India ili waende kujifunza namna masomo ya elimu ya amali yanavyofundishwa ili wakirejea waje kuwa chachu ya kuboresha namna ya kufundisha masomo ya amali, hatua hii ni sehemu ya utekelezaji wa maelekezo ya mapema ya Mhe. Rais kwa wizara ya Elimu na yale aliyoyatoa wakati akizindua sera yetu ya elimu,” amesema Prof. Mkenda.

Tanzania imepiga hatua muhimu katika kuboresha afya na ustawi wa vijana kwa uzinduzi rasmiwa Kozi Mtandao ya Elimu ya Stadi za Maisha na Afya ya Uzazi (CSE) chini ya mradi wa“Maisha yetu, Haki Zetu, Mustakabali wetu”- (O3 Plus). 

*Watoto wanaolazwa wapungua kutoka 32 hadi 7 kwa robo mwaka

Na Augusta Njoji

IDADI ya watoto wanaokabiliwa na utapiamlo mkali katika Halmashauri ya Mji Handeni imepungua kwa kiasi kikubwa, kutoka watoto 32 waliokuwa wakilazwa hospitalini kwa robo mwaka 2024/25 hadi wastani wa watoto watano hadi saba kwa robo mwaka 2025/26.

Mafanikio hayo yanatajwa kuchangiwa na mikakati madhubuti ya utoaji elimu ya lishe kwa jamii inayotekelezwa na Hospitali ya Halmashauri hiyo, ikilenga kupunguza lishe duni hususan kwa watoto.

Akizungumza Mei 5, 2026 katika kikao cha tathmini ya shughuli za lishe kwa kipindi cha Januari hadi Machi 2025/26, Afisa Tarafa ya Chanika, Julieth Mushi, akimwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese, amepongeza juhudi hizo na mafanikio yaliyopatikana katika utekelezaji wa mkataba wa lishe.

Amesisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya Idara ya Afya, Ustawi wa Jamii na Lishe pamoja na Idara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi katika kuhamasisha jamii kuanzisha bustani za mboga majumbani na kufuga wanyama ili kukabiliana na tatizo la utapiamlo kwa watoto.

Kwa upande wake, Mganga Mkuu wa Halmashauri hiyo, Dkt.Hudi Shehdadi, amesema mikakati inayoendelea kutekelezwa ni pamoja na kushirikiana na Idara za Elimu ya Msingi na Sekondari pamoja na kamati za lishe za kata kuhamasisha upandaji wa miti ya matunda na uanzishaji wa bustani za mboga, huku kila shule ikitakiwa kutenga angalau hekari mbili kwa ajili ya kilimo cha mahindi.

Aidha, amebainisha kuwa juhudi zimeongezwa katika kuhamasisha wajawazito kuhudhuria huduma za afya mapema ili kupata elimu ya lishe pamoja na virutubisho vya madini chuma, hatua inayolenga kupunguza idadi ya watoto wanaozaliwa na uzito pungufu.

Awali, akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa shughuli za lishe kwa kipindi cha Januari hadi Machi 2025/26, Kaimu Afisa Lishe wa Halmashauri hiyo, Getruda Kasabaja, amesema jumla ya wazazi na walezi 9,571 wamefikiwa na elimu ya lishe, huku watoto 17,390 wakifanyiwa tathmini ya hali ya lishe.

Ameeleza kuwa kati ya watoto hao, watoto 221 walikuwa na uzito pungufu sawa na asilimia 1.27, watoto 80 walikuwa na udumavu (asilimia 0.4), na watoto 96 walikuwa na ukondefu (asilimia 0.55). Aidha, watoto saba walipatiwa matibabu ya utapiamlo mkali katika kipindi hicho.

 

Na OWM - TAMISEMI, Dodoma


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, amewataka walimu wapatao 150 wa shule za amali waliopatiwa mafunzo nchini India kwenda kuwapatia ujuzi  vijana wa kitanzania katika shule wanazofundisha ambao utawawezesha kuwa wabunifu, wajasiriamali  na washindani katika ajira za ndani na nje ya nchi ili  kutoa mchango katika maendeleo ya taifa.

Prof. Shemdoe ametoa wito huo Mei 04, 2026 wakati wa kikao chake na walimu hao wapatao 150 wa Shule za Amali ambao wamerejea nchini kutoka nchini India walihudhuria mafunzo ya kuwajengea uwezo wa kutoa elimu ya ufundi na mafunzo ya stadi za kazi kama nyenzo muhimu ya kukuza uchumi wa viwanda, kupunguza ukosefu wa ajira kwa vijana, na kuongeza ushindani katika soko la ajira.

“Tunategemea vijana watakaotoka katika shule za amali wawe na uwezo wa kushindana katika ajira za ndani na nje ya nchi, waweze kujiajiri na kuwa wajasiriamali wenye mchango kwa taifa, hivyo muwapatie ujuzi na maarifa yote mliyoyapata nchini india,” amesisitiza Prof. Shemdoe.

Aidha, Prof. Shemdoe amewataka walimu hao kwenda kuwafundisha walimu ambao hawakupata fursa  kupata mafunzo nchini India na kuongeza kuwa, Ofisi ya Waziri Mkuu-TAMISEMI kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu watawasilisha ombi kwa Mhe. Rais la kupatiwa fedha za kwenda kuwajengea uwezo walimu wa amali 601 waliosalia ili wawe na tija katika Taifa.

Prof. Shemdoe amempongeza Waziri wa Elimu na timu yake pamoja na Katibu Mkuu-TAMISEMI na timu yake kwa kushirikiana na Washauri Elekezi Global Education Link kuratibu zoezi la walimu hao wapatao 150 wa amali kwenda nchini India kupatiwa mafunzo yatakayowezesha utekelezaji wa mtaala mpya wa elimu.

Mmoja wa walimu walionufaika na mafunzo hayo, Mwalimu Paul Maziku wa Shule ya Sekondari Chato amesema wamefundishwa namna ya kuwawezesha wanafunzi kufikia ndoto zao na malengo yaliyokusudiwa na Serikali ya kuwa na elimu ya amali na kuongeza kuwa, walimu wote wapatao 150 waliopatiwa mafunzo wana ari ya kufundisha ili kuleta mabadiliko katika elimu.

Naye mnufaika mwingine wa mafunzo, Mwalimu Sungura Mollel wa Shule ya Sekondari ya Amali Ruvuma amesema kuwa wakiwa nchini India, wamejifunza namna  ya kuandaa mitaala kulingana na uhitaji wa viwanda hivyo anaamini kwamba ujuzi walioupata utawawezesha kuwaandaa vijana wa kitanzania kuwa na ujuzi wenye tija kwa taifa ikizingatiwa kwamba wao  ni walezi.








 


>Agawa vifaa vya michezo kwa timu zote zinazoshiriki Ligi ya wilaya ya Mkinga

Na Oscar Assenga, MKINGA

Mbunge wa Jimbo la Mkinga mkoani Tanga, Twaha Mwakioja, ameahidi kushirikiana na wadau mbalimbali wa michezo kuinua kiwango cha soka wilayani humo kwa kuwekeza katika elimu na maendeleo ya waamuzi pamoja na makocha.

Akizungumza wakati wa mchezo wa Ngao ya Jamii uliokwenda sambamba na uzinduzi wa Ligi ya Wilaya ya Mkinga, uliofanyika katika Uwanja wa Chamazi, Kata ya Matamba, Mwakioja alisema lengo lao ni kuwekeza katika michezo kwa vijana ili kuwapatia ajira, kuboresha afya zao, pamoja na kuimarisha amani, mahusiano mema na ushirikiano miongoni mwao.

Alieleza kuwa dhamira yao ni kuwashika mkono vijana ili waweze kupiga hatua kutoka ngazi ya wilaya, kwenda mkoa, kanda na hatimaye ligi za juu, huku yeye akiwa bega kwa bega nao kuhakikisha wanafikia malengo yao.

Mbunge huyo alibainisha kuwa wamepata taarifa ya kuwepo kwa changamoto mbalimbali, ikiwemo uhaba wa makocha na waamuzi wenye sifa. Hivyo, wamejipanga kuwekeza katika mafunzo ya makocha ili kila kata iwe na angalau kocha mmoja mwenye ujuzi na mafunzo rasmi, pamoja na kuandaa waamuzi wenye vyeti ili kuboresha usimamizi wa michezo.

Alisisitiza kuwa uwekezaji huo utaenda sambamba na ushirikiano na Chama cha Soka Wilaya ya Mkinga katika kukuza na kuendeleza vipaji vya vijana.

Aidha, alisema mpango wao ni kuhakikisha kila kata na kijiji kinakuwa na timu ya mpira wa miguu inayoshiriki ligi ya wilaya. Aliongeza kuwa watawekeza zaidi ili kuibua timu imara zitakazoweza kushiriki ligi za ngazi ya mkoa, kanda na hatimaye Ligi Kuu, hatua itakayosaidia kuitangaza Mkinga katika ramani ya soka nchini.

Katika kuonyesha dhamira hiyo, Mwakioja alikabidhi jezi na mipira kwa timu zinazoshiriki ligi hiyo, ikiwa ni sehemu ya kuhamasisha na kusaidia maendeleo ya michezo wilayani humo.

Kwa upande wake, Katibu wa Chama cha Soka Wilaya ya Mkinga, Fadhili Habibu, alisema ratiba ya ligi hiyo imeanza Mei 4 katika kituo cha Mkinga, huku kituo cha Maramba kikitarajiwa kuanza Mei 6 (Jumatano), ambapo kutakuwa na vituo vinne vitakavyochezwa katika Kijiji cha Maramba, ikiwa ni pamoja na mechi kati ya Viva Dynamo na Maramba FC.

Habibu alisema lengo la ligi hiyo ni kusimamia na kuibua vipaji vya vijana, pamoja na kuwapa mwelekeo wa maendeleo yao kisoka. Alimshukuru mbunge kwa kujitoa na kushirikiana nao katika kufanikisha malengo hayo.

Naye Mwenyekiti wa Chama cha Soka Wilaya ya Mkinga, Hassan Zumo, alimpongeza mbunge kwa juhudi zake za kuendeleza michezo wilayani humo, akieleza kuwa hatua hiyo imeongeza hamasa na matarajio ya ushindani mkubwa katika ligi hiyo, hasa baada ya timu kukabidhiwa vifaa.

Zumo aliongeza kuwa tangu kuanzishwa kwa chama hicho mwaka 2008, wamekuwa wakipeleka vilabu katika mashindano ya ngazi ya mkoa lakini wamekuwa wakikwama kutokana na changamoto za kifedha. Hata hivyo, alisema kupitia uongozi wa Mbunge Mwakioja, wana matumaini ya kupata timu itakayoweza kufika hadi Ligi Kuu.

Aidha, timu zinazoshiriki mashindano hayo zimeahidi kujituma na kupambana kwa juhudi zote ili kuhakikisha ligi hiyo inaleta mafanikio na tija kwa vijana wa Wilaya ya Mkinga.




Na Mwandishi Wetu, Kibaha-Pwani.


Imeelezwa kuwa Tume ya Taifa ya Mipango imekamilisha nyenzo zote za utekelezaji wa Dira 2050 ambazo ni Mpango Elekezi wa Maendeleo wa Muda Mrefu 2026/2027–2050/2051 (LTPP 2050), Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Miaka Mitano 2026/27 – 2030/31 (FYDP IV) na Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2026/2027 kuelekea Julai 1, 2026 ambapo utekelezaji wa Dira hiyo utaanza rasmi.

Hayo yameelezwa leo Mei 4, 2026 na Katibu Mkuu Ofisi ya Rais-Mipango na Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango Dkt. Tausi Kida alipofungua mafunzo kwa Wakurugenzi wa Sera na Mipango, Wakurugenzi wa Ufuatiliaji na Tathmini, na Wakuu wa Idara na Vitengo vya Ufuatiliaji na Tathmini kutoka Wizara na Taasisi mbalimbali za Serikali yanayofanyika katika Chuo cha Uongozi Mwalimu Julius Nyerere, Kibaha - Pwani.

Dkt. Kida amewaambia washiriki wa mafunzo hayo kuwa, baada ya kukamilisha Dira 2050 na nyenzo zake, mafunzo hayo ni utekelezaji wa mkakati mahususi wa Serikali wa kujipanga kufanya utekelezaji wa Dira hiyo kwa kuhakikisha kunakuwepo na uelewa wa pamoja na utekelezaji unaolingana katika ngazi zote za Wizara, Taasisi za Serikali, Sekretarieti za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa katika kuhakikisha mipango ya Kitaifa inatekelezwa kwa tija.

“ Serikali kupitia Tume ya Taifa ya Mipango inakamilisha Miongozo ya Upangaji (NPGs), Mfumo wa Ufuatiliaji na Tathmini wa Programu na mirado ya Maendeleo (NF-MEDeP) na Mfumo wa Kidigitali uitwao E-Delivery. Mfumo huu na miongozo hiyo italetwa kwenu na mafunzo stahiki yanaandaliwa kwa ajili yenu” Amesisitiza Dkt. Kida.

Aidha, Dkt. Kida amesema kupitia mafunzo hayo, washiriki watapata fursa ya kujifunza kwa vitendo (i.e. case studies), kubadilishana uzoefu, na kujenga uwezo katika hatua zote za mzunguko wa miradi ya maendeleo kuanzia uibuaji, upangaji, uchambuzi, uidhinishaji hadi utekelezaji na ufuatiliaji.








Kutoka Pemba, Unguja, Mji mkongwe, Bagamoyo, Kondoa, Magofu ya kilwa, paa la mlima kilimanjaro na maeneo mengine ya Tanzania, wadau wa urithi wa dunia wamekutana katika Makumbusho ya Urithi Geopark Karatu Mkoani Arusha yanayosimamiwa na Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro  kwa lengo la kuadhimisha   Urithi wa Dunia Afrika yaliyoanza leo tarehe 04/05/2026 hadi tarehe 05/05/2026.

Wakiwa katika jengo la makumbusho ya Urithi Geopark Wadau hao wameelezwa jinsi Ngorongoro ilivyo ni utajiri wa urithi wa dunia kutokana na uumbwaji wake uliotokana na mlipuko wa volcano zaidi ya miaka milioni mbili iliyopita na kutengeneza kasoko iliyokusanya asili, uhai wa binadamu, mifumo ya ikolojia, na ustawi wa viumbe mbalimbali.

Katika  taarifa yake kwa vyombo vya habari Kamishna wa Uhifadhi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro Bw. Abdul-Razaq Badru amewashukuru wadau wote hasa Shirika la Umoja wa Mataifa la  Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO)   kwa kuipa fursa Ngorongoro kuandaa na kuwa mwenyeji wa maadhimisho hayo kwa mwaka huu.

Wadau wa urithi wa duania wakiwa katika Makumbusho ya Urithi Geopark walipata fursa ya kuelezewa kuhusu uthibitisho wa wasomi unaoeleza wazi historia ya chimbuko la binadamu wa kale aliyepatikana katika bonde la olduvai  takribani milioni  2 iliyopita na ushahidi wa Nyanyo za binadamu wa kale  katika eneo la Laetoli takribani miaka  3.6 iliyopiTa ambapo binadamu hao walitembea kwa miguu miwili.

Taasisi zinazoshiriki maadhimisho hayo ambazo zinasimamia maeneo ya urithi wa dunia ni pamoja na Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro (NCAA), Shirika la hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) Mamlaka ya Uzimamizi wa Wanyamapori (TAWA), Wakala wa Huduma za misitu Tanzania (TFS), pamoja na wawakilishi wa maeneo ya urithi wa dunia kutoka Zanzibar.

NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

WAHITIMU wa Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE) (alumni) wametakiwa kutumia nafasi zao kuchangia maendeleo ya taifa kupitia taaluma, uzoefu na rasilimali walizonazo.
Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania (TCDC) imemtangaza Irene Luoga, Afisa Ushirika Mwandamizi kutoka Ofisi ya Mrajis Msaidizi wa Vyama vya Ushirika mkoa wa Mbeya, kuwa mfanyakazi hodari kwa mwaka 2025/2026.
Tuzo hiyo imetolewa kufuatia mchango wake mkubwa katika kusimamia na kuendeleza shughuli za ushirika, ikiwa ni pamoja na kuhamasisha uwajibikaji, uwazi na ufanisi katika Sekta ya ushirika.
Katika kipindi hicho, Irene ameonyesha weledi wa hali ya juu katika utekelezaji wa majukumu yake, akisimamia vyema shughuli mbalimbali za maendeleo ya Ushirika na kutoa msaada wa kitaalamu kwa wanachama na viongozi wa vyama. Juhudi zake zimechangia kuimarika kwa utendaji wa vyama vingi pamoja na kuongeza imani ya wanachama katika sekta ya ushirika nchini.
Akizungumza mara baada ya kupokea tuzo hiyo, Irene alieleza shukrani zake kwa Uongozi wa TCDC kwa kutambua mchango wake, akiahidi kuendelea kufanya kazi kwa bidii zaidi.
 “Ninawashukuru sana TCDC kwa kunichagua kuwa mfanyakazi hodari wa mwaka huu.Hii ni heshima kubwa kwangu na inanipa motisha ya kuendelea kufanya kazi kwa bidii, uadilifu na ufanisi zaidi ili kuleta maendeleo chanya katika sekta ya ushirika nchini na Taifa kwa ujumla,” alisema Irene.