



Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Hamad Chande, ameipongeza Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) kwa mchango wake katika kuwawezesha wakulima kupata masoko yenye ushindani kupitia Mfumo wa Stakabadhi za Ghala.
Mhe. Chande ameyasema hayo leo Agosti 6, 2026, baada ya kutembelea banda la WRRB katika Maonesho ya 88 yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Malecela, jijini Dodoma.
Amesema WRRB imeendelea kuwa nyenzo muhimu katika kuimarisha biashara ya mazao kwa kuwawezesha wakulima kupata masoko yenye ushindani, kuongeza thamani ya mazao yao na kuchangia ukuaji wa uchumi wa taifa.
Aidha, ameipongeza WRRB kwa kuendelea kutoa elimu kwa wananchi na kutoa wito kwa wadau wa sekta ya kilimo kuendelea kutekeleza kwa vitendo kauli mbiu ya Maonesho ya Nane Nane ya mwaka 2026 isemayo, "Tambua Soko, Ongeza Tija, Tekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050," kwa kuimarisha mifumo ya masoko, kuongeza tija katika uzalishaji na kuhakikisha wakulima wananufaika na fursa zilizopo katika mnyororo wa thamani wa mazao.
Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Uratibu Huduma ,Bw. Mwita Thomas ameeleza kuwa WRRB itaendelea kuboresha huduma zake, kuimarisha usimamizi wa mfumo huo kwa kushirikiana na wadau ili kuhakikisha sekta ya kilimo inakuwa chachu ya maendeleo ya uchumi na ustawi wa wananchi.


Mkurugenzi wa Uthibiti Ubora wa Shule, Dkt. Ephraim Simbeye,akizungumza wakati akifungua kikao kazi cha Wakuu wa Vyuo vya Ualimu vya Serikali na visivyo vya Serikali pamoja na Waratibu wa Taaluma jijini Dodoma, leo Agosti 6, 2026, kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia,
Na.Mwandishi wetu-
Serikali imesisitiza kuwa ubora wa walimu wanaoandaliwa katika vyuo vya ualimu ndio utakaoamua mustakabali wa elimu nchini katika miaka ijayo.
Akifungua kikaokazi cha Wakuu wa Vyuo vya Ualimu vya Serikali na visivyo vya Serikali pamoja na Waratibu wa Taaluma jijini Dodoma, Agosti 6, 2026, kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mkurugenzi wa Uthibiti Ubora wa Shule, Dkt. Ephraim Simbeye, amewataka Wakuu wa vyuo kuimarisha usimamizi wa mafunzo ili kuhakikisha wahitimu wanakuwa na umahiri, maadili na stadi zinazokidhi mahitaji ya Taifa.
Ameongeza kuwa vyuo vya Ualimu vina jukumu kubwa katika utekelezaji wa mtaala kwa kuhakikisha walimu wanaohitimu wanakidhi viwango hitajika.
Dkt. Simbeye ameeleza kuwa kikaokazi hicho kimefanyika katika kipindi muafaka baada ya kukamilika kwa mzunguko wa kwanza wa wahitimu wa Mtaala Ulioboreshwa wa Elimu ya Ualimu ulioanza kutekelezwa mwaka 2023 na kusema kuwa hatua hiyo inatoa nafasi ya kutathmini mafanikio, changamoto na maeneo yanayohitaji maboresho.
Kiongozi huyo amesema kuwa Wakuu wa Vyuo wanapaswa kuwa wabunifu katika matumizi ya rasilimali. Ushirikiano na sekta binafsi pamoja na kuanzisha miradi ya uzalishaji mali bila kuathiri utoaji wa elimu.
Aidha, amesisitiza umuhimu wa kuzingatia miongozo ya Serikali katika utekelezaji wa mtaala, mafunzo kwa vitendo na utoaji wa mafunzo kwa njia ya masafa, ili kuhakikisha nchi inapata walimu wenye viwango vinavyofanana vya umahiri, maadili na uzalendo.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Elimu ya Ualimu na Mafunzo, Mathias Mvula, amesema lengo la kikao kazi hicho ni kubadilishana uzoefu uliopatikana katika utekelezaji wa mtaala ulioboreshwa wa Elimu ya Ualimu.


Serikali imewataka wakulima, wafugaji, wavuvi na wajasiriamali nchini kutumia elimu ya ushindani wa haki na ulinzi wa mlaji kama nyenzo ya kuongeza thamani ya bidhaa zao, kupanua masoko na kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa.
Wito huo umetolewa na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Hamad Chande, alipotembelea banda la Tume ya Ushindani (FCC) katika Maonesho ya 33 ya Kilimo ya Nanenane yanayoendelea jijini Nzuguni Dodoma.
Mhe Chande amesema elimu inayotolewa na FCC imekuwa na mchango mkubwa katika kuwajengea uwezo wazalishaji na wafanyabiashara kuzalisha bidhaa zenye ubora unaoweza kushindana katika soko la ndani na la kimataifa.
"Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inaendelea kujenga mazingira rafiki ya biashara yanayozingatia ushindani wa haki, fursa sawa kwa washiriki wa soko na ulinzi wa maslahi ya walaji. Msingi huo unachochea uwekezaji, huongeza tija katika uzalishaji na kuimarisha mchango wa sekta mbalimbali katika kukuza uchumi wa Taifa."amesema Mhe.Chande
Hata hivyo amewahimiza wakulima, wafugaji, wavuvi na wajasiriamali kutumia kikamilifu elimu inayotolewa na FCC kwa kuzingatia sheria za ushindani, kuepuka vitendo vinavyopotosha soko na kujikita katika uzalishaji wa bidhaa bora zenye kukidhi mahitaji ya walaji.
"Hatua hiyo itaongeza thamani ya mazao, kuinua kipato cha wazalishaji na kufungua fursa zaidi za biashara ndani na nje ya nchi."amesema
Aidha, Naibu Waziri huyo ameipongeza FCC kwa kuendelea kushirikiana na taasisi mbalimbali katika kutoa elimu kwa umma kuhusu haki za walaji na ushindani wa haki, akieleza kuwa juhudi hizo zinaimarisha mazingira ya biashara yenye uwazi na usawa kwa manufaa ya wazalishaji na watumiaji wa bidhaa na huduma.
Amesisitiza kuwa Maonesho ya Nanenane yameendelea kuwa jukwaa muhimu la kuwafikia wananchi moja kwa moja na kuwapa maarifa yatakayowawezesha kuongeza ubora wa mazao na bidhaa zao.
Ametoa rai kwa FCC kuendeleza kampeni za elimu nchini kote ili Watanzania wengi zaidi wanufaike na fursa zinazotokana na soko lenye ushindani wa haki na hivyo kuchangia kwa kiwango kikubwa maendeleo ya uchumi wa Taifa.
