Waziri Mkuu, Mwigulu Nchemba, ameielekeza kampuni ya Abanyambo Enterprises & General Supplies Ltd kuendelea na shughuli za uchimbaji wa madini ya bauxite katika Kata ya Magamba, Wilaya ya Lushoto, mkoani Tanga.


Hatua hiyo imekuja kufuatia utekelezaji wa agizo lililokuwa limetolewa awali na Waziri Mkuu mstaafu, Kassim Majaliwa, ambaye alisitisha uchimbaji huo hadi tathmini ya athari kwa mazingira na binadamu itakapofanyika na kukamilika.


Akizungumza wakati wa ziara yake mkoani humo, Waziri Mkuu alisema kampuni hiyo, ambayo inamiliki leseni nne halali, imeruhusiwa kuendelea na uzalishaji baada ya Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kujiridhisha na kutoa kibali rasmi cha tathmini ya athari kwa mazingira.

Alitoa kauli hiyo alipokuwa akijibu swali la aliyekuwa Mwenyekiti wa Kitongoji cha Magamba, Mahamud Kotti, ambaye alitaka kujua msimamo wa Serikali kuhusu mradi huo.  licha ya uchimbaji huo kuwa chanzo cha ajira na mapato kwa kijiji na halmashauri.



Hata hivyo Waziri Mkuu alisisitiza kuwa Serikali haitavumilia uvunjaji wa sheria katika sekta ya madini, akieleza kuwa wawekezaji wote wanapaswa kufuata taratibu zilizowekwa ili kulinda rasilimali za taifa pamoja na mazingira.

Katika hatua nyingine, alitangaza kusimamishwa kwa leseni 45 zilizokuwa zikitaka kufanya shughuli katika mgodi huo kinyume na sheria na masharti ya uchimbaji.


 Alifafanua kuwa uamuzi huo umefikiwa baada ya kubainika kuwepo kwa ukiukwaji wa taratibu ambao ungeweza kuhatarisha usalama wa mazingira na kusababisha upotevu wa mapato ya Serikali.


“Hatutakuwa tayari kuona rasilimali za nchi zinachimbwa bila kufuata sheria. Lazima kila mmoja aheshimu utaratibu,” alisisitiza Waziri Mkuu.

Aidha, amemuagiza Afisa Madini Mkoa wa Tanga kusimamia kikamilifu utekelezaji wa agizo hilo na kuhakikisha kuwa kampuni ya Abanyambo pekee ndiyo inayoendelea na shughuli za uchimbaji katika eneo hilo.


Ziara hiyo ni sehemu ya ukaguzi wa miradi ya maendeleo na shughuli za kiuchumi unaofanywa na Waziri Mkuu, kwa lengo la kuhakikisha sheria, uwazi na uwajibikaji vinazingatiwa katika usimamizi wa rasilimali za taifa.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda,akizungumza katika ufunguzi wa mafunzo elekezi ya Wathibiti Ubora wa Shule ngazi ya wilaya uliofanyika   wilayani Bagamoyo Mkoani Pwani.

......

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda, amesema kuwa jukumu kubwa la Wathibiti Ubora wa Shule ni kuhakikisha utekelezaji wa sera, sheria, miongozo na mikakati ya elimu unafanyika kwa ufanisi.

Akizungumza  wilayani Bagamoyo Mkoani Pwani katika ufunguzi wa mafunzo elekezi ya Wathibiti Ubora wa Shule ngazi ya wilaya, ameeleza kuwa watendaji wanapaswa kusaidia katika utekelezaji wa sera na kuhakikisha wanazielewa kikamilifu, hususani zinazohusu elimu ya amali na elimu ya lazima.

Profesa Mkenda amesema wathibiti Ubora wa Shule wanapaswa kutoa taarifa juu ya changamoto zinazojitokeza shuleni ikiwemo ukosefu wa vifaa au madarasa kwa Wakurugenzi na Wakuu wa Wilaya ili hatua za kutatua changamoto hizo zichukuliwe haraka.

Akizungumzia mageuzi makubwa ya Sekta ya Elimu, Waziri amesema kuwa kuanzia mwaka wa masomo 2027/2028, elimu ya msingi itaanza kutolewa kwa Miaka Sita badala ya Saba na elimu ya lazima itakuwa miaka kumi kuanzia darasa la kwanza hadi kidato cha nne.

"Mabadiliko haya yataleta “double cohort,” ambapo wanafunzi wa darasa la saba (mfumo wa zamani) na darasa la sita (mfumo mpya) wataingia kidato cha kwanza kwa wakati mmoja. Hata hivyo, hali hiyo ni ya mpito na mfumo utarejea katika “single cohort” baada ya muda,'amefafanua Waziri Mkenda.

Amesema Serikali inawekeza katika shue za ufundi, lakini bado kuna uhaba wa karakana, vifaa na walimu wenye sifa huku akisisitiza Halmashauri kupanga bajeti kwa umakini ili kuzuia shule kufungwa kutokana na ukosefu wa mahitaji ya msingi.

Mkurugenzi Msaidizi wa Uthibiti Ubora wa Shule, Monica Mpululu, amesema kuwa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imekuwa ikitekeleza majukumu yake kwa kasi na kwa ushirikiano wa karibu na Wathibiti Ubora wa shule nchini.

Mkurugenzi huyo ameeleza kuwa wizara imeendelea kuwawezesha wathibiti Ubora wa shule kwa kuwapatia rasilimali muhimu, ikiwemo fedha na vifaa vya kazi ambayo inasaidia kuboresha usimamizi na ufuatiliaji wa shule katika maeneo mbalimbali ya nchi na kuongeza ufanisi wa kazi za uthibiti ubora.

Mpululu amesema kuwa ushirikiano wa wadau wote wa elimu ni msingi wa mafanikio ya sekta, na kwamba juhudi zinazofanywa sasa ni matokeo ya kazi ya pamoja inayolenga kuinua kiwango cha elimu kwa manufaa ya taifa.

Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Dkt.Mosses Kusiluka amesema kuwa serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Raisi Daktari Samia Suluhu Hassan imeipa kipaumbele cha kwanza sekta ya TEHAMA nchini kwa kuendeleza mifumo mbalimbali na kuhakikisha huduma zinapatikana kirahisi.

Katika kufanikisha hilo pia serikali imeendelea kuwekeza katika sekta hiyo na kuhakikisha kuwa Tanzania inaendelea kuweka rekodi nzuri ya kutambuliwa kimataifa katika kutoa huduma nzuri ya serikali mtandao.

Ameyasema hayo leo wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha Sita cha Serikali Mtandao (eGA) kinachoendelea katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa (AICC) mkoani Arusha. 

"Kuwepo kwangu hapa leo ni kuonyesha  umuhimu wa serikali ya awamu ya Sita  ambayo imeipa umuhimu wa kipekee TEHAMA,Mheshimiwa Raisi wetu Daktari Samia  Suluhu Hassan  anaishi TEHAMA na anaitumia kwa kiasi ambacho watu wengi hawawezi kufahamu kwahiyo TEHAMA ni kipaumbele cha kwanza kwenye Utekelezaji wa Ajenda ya serikalimtandao"Alisisitiza Balozi  Kusiluka

Aidha amesema kuwa Tanzania ni nchi yenye mafanikio makubwa duniani kwenye matumizi ya TEHAMA,hatua kubwa imepigwa na mafanikio ya eGa ni kielelezo kizuri cha azma ya serikali  kutumia teknolojia  kurahisisha upatikanaji wa huduma kwa wananchi  hali ambayo inapelekea huduma kupatikana kwa wakati.

Nae Mhandisi Benedict  Ndomba  ni Mkurugenzi wa Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) amesema kuwa kikao hicho ni muhimu kwa kuwa kitakuja na maazimio ya pamoja ya kuboresha huduma ya serikali mtandao, kuongeza uwazi na uwajibikaji katika utendaji kazi na kujenga serikali mtandao.

Mhandisi Ndomba amewahikikishia washiriki eGA itaendelea kuwa mshirika wa karibu wa kuendelea kuijenga serikali Mtandao.

Kwa Upande wake Mwenyekiti wa Bodi  ya Wakurugenzi  Mamlaka  ya Serikali Mtandao (eGA), Daktari Mussa Kissaka amesema kuwa serikali ilianzisha mamlaka hiyo ili kuratibu  na kusimamia  jitihada za serikali mtandao pamoja na kuhakikisha kuwa uzingatiaji wa sera,sheria,kanuni na  miongozo na viwango ya serikali mtandao kupitia taasisi za umma huku  lengo likiwa ni kujenga  serikali mtandao kupitia teknolojia za kisasa kwa  ajili ya kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

Jumla ya washiriki 1400 wanashiriki mkutano huo ambao unajumuisha wadau mbali mbali kutoka serikalini na sekta binafsi kwa lengo la kuboresha serikali mtandao.











Na.Alex Sonna-DODOMA

WAZIRI  wa Madini na Mbunge wa Jimbo la Mtumba Mhe. Anthony Mavunde , amevitaka vikundi vilivyonufaika na mkopo wa shilingi bilioni mbili uliotolewa kwa wajasiriamali wa jimbo hilo, kutumia fedha hizo kama zilivyokusudiwa ili kujikwamua kiuchumi.

Akizungumza wakati wa hafla ya kukabidhi mikopo hiyo jijini Dodoma, Mhe.Mavunde amesema kuwa  azma ya serikali ni kuhakikisha wananchi wanapata nyenzo na mitaji ya kuwawezesha kupanua na kuendeleza shughuli zao za kiuchumi.

Amesema kuwa  Mkopo huo umefadhiliwa na CRDB Bank kupitia CRDB Bank Foundation katika programu ya imbeju inayolenga kuwawezesha wajasiriamali wadogo na wa kati.

"Tumieni vizuri  mikopo hiyo kwa kuanzisha na kuendeleza shughuli mbalimbali za ujasiriamali ili iweze kuleta tija, kuwaimarisha kiuchumi na hatimaye kurejeshwa kwa manufaa ya wengine."amesema Mhe.Mavunde

Mhe.Mavunde amesema kuwa  mikopo hiyo ni kama mbegu inayohitaji kutunzwa na kuendelezwa ili izae matunda yenye manufaa kwa mkopaji na jamii kwa ujumla.

“Mikopo hii ni mbegu. mkizitumia vizuri zitazaa matunda na kuwainua kiuchumi, lakini pia zitawawezesha wengine kupata fursa kama hii baada ya ninyi kurejesha kwa wakati,” amesisitiza 

Aidha ameongeza kuwa dhamira yake ni kuona wananchi wa mtumba wanaachana kabisa na mikopo umiza maarufu kama ‘mikopo ya kausha damu’ na badala yake wanatumia fursa rasmi za kifedha zenye masharti nafuu na rafiki kwa maendeleo yao.

“Wananchi wa mtumba wakae mkao wa kula. kuna mipango mingi ya kuwawezesha kiuchumi inaendelea kuja, na lengo letu ni kuhakikisha kila mmoja anapata fursa ya kujikwamua,” ameongeza

Hata hivyo amewataka wanufaika kuchangamkia fursa hizo kila zinapojitokeza na kuhakikisha wanarejesha mikopo kwa wakati ili wengine nao wapate kunufaika na mpango huo.

kwa upande wake, Mkurugenzi mtendaji wa CRDB Bank Foundation,Bi. Tully Esther Mwambapa, amesema kuwa  taasisi hiyo itaendelea kushirikiana na serikali kupitia programu mbalimbali zinazolenga kuyawezesha makundi tofauti ya wananchi kiuchumi.

Amesema kuwa  lengo la programu ya imbeju ni kuwajengea uwezo wajasiriamali kwa kuwapatia mitaji pamoja na elimu ya usimamizi wa biashara ili waweze kuendesha miradi yao kwa tija na ufanisi.

" Hadi sasa taasisi hiyo imetoa mikopo ya mitaji wezeshi yenye thamani ya shilingi bilioni 22.1, huku zaidi ya wajasiriamali milioni moja wakinufaika nchini kote."amesema 

Amesema kuwa  mikopo hiyo imekuwa chachu ya kuboresha ustawi wa kiuchumi wa jamii na kuchangia katika ukuaji wa pato la taifa kupitia shughuli za uzalishaji mali zinazofanywa na wanufaika.

Baadhi ya wanufaika wa mikopo hiyo wameishukuru CRDB  kwa kuwagusa moja kwa moja katika maisha yao na kuahidi kuitumia mikopo hiyo katika shughuli za uzalishaji mali pamoja na kuirejesha kwa wakati ili iweze kuwafikia watu wengi zaidi katika maeneo mbalimbali nchini.

hafla hiyo imeelezwa kuwa sehemu ya jitihada za kuimarisha uchumi wa wananchi wa mtumba na kuongeza mchango wao katika maendeleo ya taifa.



Na Mwandishi Wetu - Dar es Salaam


Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais (Uwekezaji) Dkt. Fred Msemwa ametoa wito kwa vijana hususani walioko vyuo vikuu kujenga utamaduni wa kujifunza kuhusu uwekezaji, kwa kuwa wana faida ya kuwa na uwezo wa kiutendaji na utimamu wa kimwili.

Dkt. Msemwa, ametoa wito huo leo katika hafla ya uzinduzi wa Klabu ya Uwekezaji kwa Vijana (YIC) katika Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE), Dar es Salaam, ambapo amesisitiza kuwa Dira 2050 imewapatia vijana umuhimu mkubwa kwa kuwaona wao kama rasilimaliwatu Muhimu.

“Dira inawatambua nyinyi kama rasilimali muhimu ya Taifa, inasisitiza kuwaandaa kuwa na ujuzi wa hali ya juu ili muiwezasha nchi kushindana kimataifa.” Alisema Dkt. Msemwa.

Katika mazungumzo yake na vijana hao, aliwapa changamoto ya kujiwekea msingi imara wa kiuchumi, akawafundisha nguzo nne muhimu zilizohusisha; kuwa na malengo, kujenga mtizamo sahihi, kujifunza kuweka akiba na kuwekeza, na kujifunza tabia ya kufanya zaidi.

Vile vile, Katibu Mkuu amewakumbusha kuwa Elimu ya Fedha, Ujasiriamali, Uwekezaji kwenye mifuko ya kijamii, na ujuzi wa Kuanzisha na Kusimamia Biashara, iliyokuwa ikitolewa katika hafla hiyo ilikuwa muhimu kwa kuwa inajibu changamoto zao binafsi na za jamii.

Ufunguzi wa Klabu hiyo, ni sehemu ya utekelezaji wa program ya uwajibikaji kwa jamii (CSR) wa Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalumu ya Kiuchumi Tanzania (TISEZA) unaolenga kukuza elimu ya fedha, ujasiriamali na utamaduni wa uwekezaji miongoni mwa vijana na wanafunzi wa vyuo vya elimu ya juu nchini.













Na Oscar Assenga, TANGA

WAZIRI Mkuu Dkt Mwigulu Nchemba amefanya ziara ya kutembelea utekelezaji wa mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki unaotekelzwa eneo la Chongoleani Jijini Tanga huku akiridhishwa na kasi ya utekelezaji wake unaoendelea kwa kuzingatiwa viwango vilivyowekwa.

Nchemba aliyasema hayo wakati akizungumza katika ziara yake eneo la Chongoleani Jijini Tanga linapoishia Bomba la Mafuta ambalo litasafirisha mafuta kutoka Hoima nchini Uganda hadi eneo la Chongoleani licha ya kuwepo kwa changamoto zilizojitokeza wakati wa utekelezaji wake.

Alisema kwamba kwamba mradi huo wa kimkakati ambao utagharimu Dola za Marekani Bilioni 5.65 ni kielelezo cha Undugu Kati ya Tanzania na Uganda ambapo mradi huo umefikia asilimia 81 ya utekelezaji wake

Ambapo alisema changamoto hizo ni pamoja na mlipuko wa ugonjwa wa Uviko 19 pamoja na mtikisiko wa uchumi wa dunia lakini akabainisha kuwa hatua zilizochukuliwa zimewezesha mradi huo kuendelea bila kuathiri ubora na malengo yake.
"Mradi umepiga hatua lakini wakati wa utekelezaji wa mradi huu kulikuwepo na changamoto ikiwemo dunia kupita kwenye misikusuko ya kiuchumi na mabadilio ya sera za kiuchumi lakini umeendelea kutekelezwa kwa kasi jambo ambalo linaendelea kuipa heshima nchi yetu pamoja na ndugu zetu tunaotekeleza mradi huo kwa pamoja "Alisema

Mradi huo wa EACOP una urefu wa takribani Kilomita 1,444 ukianzia Hoima nchini Uganda hadi Chongoleani Tanzania na unatarajiwa kusafirisha mafuta ghafi kutoka maeneo ya uzalishaji ya Uganda hadi kwenye Kituo cha Kuhifadhi na Kusafirisha mafuta eneo la Chongoleani Jijini Tanga.

Alisema kwamba mradi huo unatajwa kuwa miongoni mwa miradi mikubwa ya kimkakati katika ukanda wa Afrika Mashariki ukilenga kuchochea ukuaji wa uchumi na kuongeza ajira kwa wananchi pamoja na

Aidha Waziri Mkuu huyo aliwatahadharisha watu wanaoanzisha makampuni na kuyaita ya wazawa huku yakiwa yanamilikiwa na wageni ili kunufaika na fursa ya “Loal Content” ya ushirikishwaji wa watanzania mradi kwamba watakapogundulika watafungiwa na hawatafanya kazi tena hapa nchini kwani hivyo ni kuwatapeli watanzania na kuwaibia fursa

Awali akizungumza katika ziara hiyo,Naibu Waziri wa Nishati Salome Makamba alisema kwamba katika mradi huo ulianza mwaka 2022 na unatarajiwa kukamilika Julai 2026 huku akieleza Serikali kwa kushirikiana na EACOP imekamilisha zoezi la kuthamini na utwaaji wa ardhi ya mradi.

Alisema kwamba hadi kufikia Januari 2026 Jumla ya Sh. Bilioni 35.06 zimetumika kulipa stahiki ya fidia kwa wananchi 9,869 kati ya wananchi 9,927 sawa na asilimia 96.4 kwa wanaopisha eneo la mradi na mkoani Tanga wananchi 1,688 wamefidiwa na kulipwa Jumla ya Bilioni 10.49.

Aidha alisema wananchi 294 wamenufaika kwa kujengewa nyumba 340 za makazi mbadala na wameshakabidhiwa nyumba zao hapa Tanga walionufaika ni wananchi 43.

Alisema kwamba wananchi wa Mkoa wa Tanga waliopatiwa udhamani wa chakula ni 1,200 huku wananchi 191 wameshiriki mafunzo ya ufugaji wa kuku,nyuki na ujasiriamali ili kuongeza kipato.

Makamba alisema katika mkoa huo miundombinu iliyojengwa ni pamoja na kituo kimoja cha Afya na kituo kimoja cha kupunguza mgandamizi wa mafuta ghafi kilichopo Handeni,Matenki Mawili ya Kuhifadhia Mafuta yaliyopo Tanga na Gati ya kupakia mafuta na kituo kikuu cha kuongeza ulinzi wa bomba la mafuta.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Tanga Balozi,Dkt Batilda Burian alisema wana Tanga wanamshukruu Rais kwa jinsi ambavyo maono yake na Rais wa Uganda Yoweri Museveni kwamba mradi umekuwa mzuri na shughuli zimekwenda vizuri na wananchi wa Tanga wamepata ajira.

Alisema pia kwa waliopitiwa na mradi waliweza kupata fidia bila kuwepo kwa changamoto yoyote lakini waliweza kusaidiwa na mashamba yaliyoguswa waliweza kulimiwa huku akiwashukuru EACOP kuna maeneo walikwenda kwa sababu walikwenda na utaalamu wakarudi kumueleza kuna changamoto ya uharibifu wa panya wa mazao iliwasaidia nao kuwaeleza wizara na hivyo kuondosha changamoto hiyo.

Mkuu wa Mkoa alisema kwamba zaidi vijana wa Tanga wameweza kushirikiana na wahandisi na wanashukuru mradi upo salama na hawajapata changamoto yoyote ya watu kupata madhara na suala la mazingira kwa sababu mradi umekwenda kwenye bahari wamehakikisha maeneo yenye uoto asili waliweza kuzingatia na hata kuchepusha ili wasiharibu na wanazingatia mazingira ya bahari.