Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Dennis Londo,akizungumza na waandishi wa habari leo Agosti 7,2026 mara baada ya kutembelea mabanda ya Taasisi zilizochini ya Wizara ya Viwanda na Biashara wakati wa  Maonesho ya 33 ya Wakulima Nane Nane yanayoendelea viwanja vya Dkt.John Malecela Nzuguni Jijini Dodoma.

Na Alex Sonna, Dodoma

Mkakati wa Serikali wa kuongeza thamani ya mazao ya kilimo, mifugo na uvuvi kupitia viwanda umeelezwa kuwa ndiyo nguzo ya kujenga uchumi shindani, kuongeza kipato cha wazalishaji na kufungua fursa zaidi za ajira kwa Watanzania.

Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Dennis Londo, amesema Serikali inaendelea kutekeleza mkakati huo kwa kushirikiana na taasisi zilizo chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara ili kuhakikisha mazao yanayozalishwa nchini yanachakatwa, yanaongezewa thamani na kuingia sokoni kama bidhaa zenye ubora na ushindani.

Akizungumza katika Maonesho ya Kimataifa ya Kilimo ya Nane Nane,Mhe. Londo amesema mazao ya kilimo, mifugo na uvuvi ni malighafi muhimu kwa maendeleo ya viwanda, hivyo Serikali imeweka mazingira yatakayowezesha mnyororo wa thamani kuanzia uzalishaji, uchakataji hadi masoko ya ndani na nje ya nchi kwa mujibu wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Amesema taasisi za wizara hiyo, zikiwemo BRELA, TBS, Tume ya Ushindani (FCC),Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB),SIDO na Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE), zinaendelea kusogeza huduma karibu na wananchi kwa kutoa elimu, usajili wa biashara, viwango vya ubora na huduma nyingine zinazolenga kuwajengea uwezo wazalishaji na wafanyabiashara kushiriki kikamilifu katika uchumi wa viwanda.

Aidha, amesema Serikali ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuboresha mazingira ya biashara kwa kuwekeza katika barabara, madaraja, vivuko, umeme wa REA na miundombinu ya mawasiliano ili kupunguza gharama za uzalishaji, kurahisisha usafirishaji wa bidhaa na kuwapa wananchi taarifa sahihi za masoko zinazowaongezea tija.

Mhe.Londo amewataka wananchi kutembelea banda la Wizara ya Viwanda na Biashara katika maonesho hayo ili kupata elimu na huduma mbalimbali zinazotolewa na taasisi zake, akisisitiza kuwa kuongeza thamani ya mazao ndiyo njia ya kuimarisha viwanda vya ndani, kuongeza mapato ya wananchi na kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha biashara na uzalishaji wa bidhaa zenye ushindani.

 


Mradi wa Kituo cha Kuongeza Msukumo wa Mafuta (Pump Station 3 – PS3) katika Mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP), kilichopo Wilaya ya Muleba mkoani Kagera, umefikia asilimia 88 ya utekelezaji na unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa Agosti au mwanzoni mwa Septemba mwaka huu.

Hayo yameelezwa Agosti 7, 2026 na Mkurugenzi wa Mipango na Uwekezaji wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), Bw. Derick Moshi, wakati wa ziara ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa kituo hicho.

Bw. Moshi amesema PS3 ni kituo cha tatu katika mradi wa EACOP kuanzia Uganda na cha kwanza upande wa Tanzania. Amefafanua kuwa kazi zote kuu za ujenzi zimekamilika na kinachoendelea ni kazi za ukamilishaji pamoja na majaribio ya mifumo kabla ya kituo kuanza kufanya kazi.

Aidha, amesema mradi huo umekuwa shamba darasa kutokana na ushirikiano mzuri kati ya Serikali na sekta binafsi katika utekelezaji wake, jambo lililowezesha kubadilishana ujuzi, kujenga uwezo wa wataalamu wa ndani na kuimarisha ushirikiano katika miradi mikubwa ya kimkakati.

Ameongeza kuwa mradi huo unaendana na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kwa kuimarisha ushiriki wa sekta binafsi katika maendeleo ya sekta ya nishati na kuendeleza miundombinu ya kisasa. Pia amesema kukamilika kwa PS3 kutachangia usafirishaji salama na wenye ufanisi wa mafuta ghafi kutoka Uganda kupitia Tanzania, hatua itakayochochea ukuaji wa uchumi na kuongeza nafasi ya Tanzania kama kitovu cha miundombinu ya nishati katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Kwa upande wake, Kiongozi wa Timu ya Mkandarasi wa Kituo hicho, Dmitry Malyshev, amesema ameridhishwa na ziara ya wataalamu kutoka Wizara ya Nishati na TPDC kwani imewapa fursa ya kupokea maoni na maelekezo ya kitaalamu yatakayosaidia kukamilisha mradi kwa ubora, usalama na kwa kuzingatia viwango vinavyohitajika.











 

Yawataka wananchi kujiunga mapema kujikinga na gharama za matibabu

Na Grace Michael, Dodoma

MFUKO wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) umewahimiza wananchi nchini kujiunga na bima ya afya kabla ya kuugua, ukieleza kuwa ni njia salama ya kujikinga dhidi ya gharama kubwa za matibabu ambazo zinaweza kujitokeza wakati wowote.

Wito huo umetolewa leo Agosti 07, 2026 na Meneja Masoko na Huduma kwa Wateja wa NHIF, Angela Mziray, wakati akitoa elimu kwa wananchi waliotembelea banda la Mfuko katika Maonesho ya 49 ya Kilimo ya Nanenane yanayoendelea katika viwanja vya Nzuguni, mkoani Dodoma.

Bi. Mziray amesema maonesho hayo yameipa NHIF fursa ya kuwafikia wananchi wengi na kuwaelimisha kuhusu umuhimu wa kuwa na bima ya afya, sambamba na utekelezaji wa Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote inayolenga kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma za matibabu bila vikwazo vya kifedha.

Amesema changamoto za kiafya zinaweza kumpata mtu yeyote bila kutarajia, na mara nyingi husababisha familia nyingi kutumia akiba zao au hata kuuza mali ili kugharamia matibabu.

“Ugonjwa huja bila taarifa. Unaweza kuwa mzima leo lakini kesho ukahitaji matibabu ya gharama kubwa. Ndiyo maana tunawahimiza wananchi kujiunga na bima ya afya mapema ili wajenge kinga ya kifedha kwao na kwa familia zao," amesema Bi. Mziray.

Amefafanua kuwa mwananchi anapochangia bima ya afya kabla hajaugua, hupata uhakika wa matibabu bila kubeba mzigo mkubwa wa gharama wakati wa uhitaji.

“Ni muhimu wananchi wajidundulize kidogo kidogo na kuchangia bima ya afya. Hii ndiyo njia bora ya kuhakikisha familia inapata huduma za matibabu kwa wakati bila kuathiri mipango ya maendeleo," amesema.

Bi. Mziray amesema NHIF inaendelea kutoa elimu katika maeneo mbalimbali nchini ili kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu faida za bima ya afya na kuhamasisha matumizi ya mfumo wa bima badala ya kulipia matibabu moja kwa moja kutoka mfukoni.

Ameongeza kuwa wanachama wa NHIF wanapata huduma katika mtandao mpana wa vituo vya afya vya Serikali, binafsi na vya mashirika ya dini vilivyosajiliwa na Mfuko, jambo linalowapa urahisi wa kupata huduma popote wanapozihitaji.

Aidha, amesema kuwa na bima ya afya siyo tu kulinda afya ya mtu binafsi, bali pia ni kulinda uchumi wa familia kwa kupunguza matumizi yasiyotarajiwa yanayotokana na matibabu.

Katika Maonesho ya Nanenane, NHIF inaendelea kutoa huduma mbalimbali ikiwemo usajili wa wanachama wapya, elimu kuhusu vifurushi vya bima ya afya, ushauri kwa wanachama pamoja na ufafanuzi wa utekelezaji wa Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote.

Wananchi wanaotembelea banda la NHIF pia wanapata fursa ya kuuliza maswali, kupata majibu kuhusu huduma za Mfuko na kujiunga na bima ya afya papo hapo, hatua inayochangia kuongeza uelewa na ushiriki wa jamii katika kuhakikisha kila Mtanzania anakuwa na kinga ya kifedha dhidi ya gharama za matibabu.

 

Na.Mwandishi Wetu

Tume ya Ushindani (FCC) imetajwa kuwa mdau muhimu katika kuongeza thamani ya mazao ya Watanzania kupitia elimu ya ushindani wa haki na ulinzi wa mlaji, hatua inayowasaidia wazalishaji na wafanyabiashara kuboresha ubora wa bidhaa zao na kuzifanya zishindane katika masoko ya ndani na kimataifa.

Kauli hiyo imetolewa leo Agosti 7,2026 na Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Dennis Londo, alipotembelea banda la FCC katika Maonesho ya Kimataifa ya Kilimo ya Nanenane yanayoendelea katika viwanja vya Nzuguni jijini Dodoma. Amesema elimu inayotolewa na tume hiyo imeendelea kujenga uelewa kwa wananchi kuhusu umuhimu wa ushindani wa haki, ulinzi wa mlaji na kuongeza thamani ya bidhaa za Tanzania.

Ameipongeza FCC kwa kuendelea kushirikiana na wadau mbalimbali katika kuimarisha mazingira ya biashara, akieleza kuwa juhudi hizo zinaendana na dira ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kukuza sekta za uzalishaji kupitia soko lenye ushindani wa haki, uwazi na fursa sawa kwa wote.

Mhe. Londo ameihimiza FCC kuendelea kutumia Maonesho ya Nanenane na majukwaa mengine kuwafikia wananchi wengi zaidi ili kuongeza uelewa kuhusu sheria za ushindani na ulinzi wa mlaji, akisisitiza kuwa elimu hiyo ni nyenzo muhimu ya kuongeza thamani ya mazao, kuvutia masoko mapya na kuongeza kipato cha wazalishaji.

Aidha, ametoa wito kwa wakulima, wafugaji, wavuvi na wajasiriamali kwenda kuitumia vizuri  elimu iliyotolewa na FCC kuboresha uzalishaji wao, kuzingatia sheria za ushindani na kuepuka vitendo vinavyovuruga soko, akieleza kuwa hatua hiyo itachangia kujenga uchumi shindani na kuongeza mchango wa sekta za uzalishaji katika maendeleo ya taifa.

Benki Kuu ya Tanzania (BoT) imezindua rasmi Kielelezo cha Faida Rejea ya Dhamana za Serikali (Tanzania Sovereign Yield Curve), hatua inayotarajiwa kuongeza uwazi, ushindani na ufanisi katika soko la Dhamana za Serikali na kuimarisha mazingira ya uwekezaji nchini.
 

Meneja wa Kanda ya Kaskazini (TBS),Mhandisi Yona Afrika akitoa elimu ya Viwango kwa wajasiriamali katika maonesho ya Nanenane Kanda ya Kaskazini yanayoendelea jijini Arusha.

Na.Mwandishi Wetu.

SHIRIKA la Viwango Tanzania (TBS) limehimiza wajasiriamali kuchangamkia fursa ya kuthibitisha ubora wa bidhaa wanaozalisha bure kwa gharama za Serikali, hatua ambayo itawasaidia kuondokana na vikwazo vya kiabiashara.

Mbali na wito huo kwa wajasiriamali, shirika hilo limewataka wananchi kuhakikisha wananunua na kutumia bidhaa zilizothibishwa ubora na shirika hilo kwa kujenga utamaduni wa kusoma taarifa zilizopo kwenye vifungashio.

Wito huo umetolewa na Meneja wa TBS Kanda ya Kaskazini,, Yona Afrika,. wakati akizungumza kwenye Maonesho ya Nanenane yanayoendelea jijini Arusha.

Alisema Serikali inatambua mchango mkubwa wa wajasiriamali katika kukuza uchumi wa Taifa na wao binafsi, ndiyo maana imebeba dhamana ya kuthibitisha ubora wa bidhaa zao bure.

"Kwa hiyo tumeshiriki katika maonesho haya kwa sababu ni fursa ya kukutana na wadau mbalimbali na kuwaelezea shughuli zinazofanywa na TBS na fursa nyingine ambazo zinapatikana kama kuthibitisha bidhaa za wajasiriamali bure," alisema.

Alisema bidhaa zikishathibitishwa na TBS zinaingia masoko ya Nchi za Afrika Mashariki (EAC) na ya kikanda bila vikwanzo vya biashara.

Alisema nchi za EAC zimeingia makubaliano, ambapo bidhaa zikishathitishwa na shirika la viwango la nchi husika,hazitakiwi kupimwa tena zinapopelekwa kwenye soko la nchi nyingine.

"Kwa hiyo TBS tumeshiriki maonesho haya kusudi kukutana na wadau mbalimbali, ambao tunawafikia na kuwapa taratibu za kufuata kuthibitisha ubora.

"Kwa kweli tunaishukuru Serikali kwa kuendelea kuandaa Maonesho haya ya Nanenane, kwani fursa muhimu ya kukutana na kutoa elimu kwa wadau.

Mfano tunawaambia kuwa wakipata barua ya utambulisho kutoka SIDO wakija kwetu utaratibu wa kuthibitisha ubora wa bidhaa unaanza mara moja, kwa wajasiriamali" alisema Afrika.

Kwa upande wa wananchi waliotembelea banda la TBS, walitakiwa kuhakikisha wanatumia bidhaa zilizothibitishwa ubora ili kulinda afya zao na kuona thamani ya fedha zao.

Alisema ni muhimu kusoma taarifa zilizopo kwenye vigungashio ili kujua kama zina ubora uliothititishwa na shirika pamoja na muda wake wa mwisho wa matumizi.



‎Waziri Ofisi ya Rais, Maendeleo ya Vijana, Mhe. Joel Nanauka ameipongeza Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) kwa utekelezaji wa Mpango wa Matengenezo ya Barabara kwa Kutumia Vikundi vya Kijamii (CBRM) akieleza kuwa ni fursa muhimu ya kuwawezesha wananchi hususan vijana kushiriki katika shughuli za matengenezo ya barabara na kujiongezea kipato.
‎Mhe. Nanauka ametoa pongezi hizo alipotembelea banda la TARURA katika Maonesho ya Kitaifa na Kimataifa ya Kilimo Nanenane yanayoendelea katika uwanja wa Dkt. John Malecela mkoani Dodoma.
‎Amesema kuna umuhimu wa kuwafikia wananchi kwa kuwapa elimu ya kutosha kuhusu fursa zinazotolewa kupitia mpango wa CBRM ili waweze kushiriki kikamilifu. Aidha, amependekeza kuwepo kwa ushirikiano wa karibu kati ya Wizara ya Maendeleo ya Vijana na TARURA katika utekelezaji wa mpango huo.
‎"Ni muhimu kuongeza kasi ya utoaji wa elimu kwa wananchi kuhusu fursa zilizopo katika mpango wa CBRM. Pia napendekeza kuwepo kwa vikao vya mara kwa mara kati ya Wizara ya Maendeleo ya Vijana na TARURA ili kuimarisha ushirikiano na kuhakikisha malengo ya mpango huu yanafikiwa", amesema Mhe. Nanauka.
‎Kwa upande wake, Mratibu wa mpango wa CBRM TARURA Makao Makuu, Mhandisi Richard Missa amemueleza Waziri huyo kuwa Wakala umeanza utekelezaji katika mkoa wa Tanga, Morogoro,Dodoma na Pwani ambapo barabara zaidi ya kilomita 1500 zinahudumiwa na vikundi 302 kwa mwaka wa fedha 2025/2026.
‎Aidha, amesema Wakala umejipanga kutekeleza mpango wa CBRM katika mikoa yote 25 ya Tanzania Bara kwa mwaka wa fedha 2026/2027 ambapo zaidi ya kilomita 7000 za barabara zitafanyiwa matengenezo na vikundi 1100 vitapata fursa katika kazi hizo. 
‎Mhandisi Missa amesema mpango huo unalenga kuongeza ushiriki wa wananchi katika matengenezo ya kawaida ya barabara sambamba na kuchochea ajira na maendeleo ya kiuchumi katika jamii.
‎TARURA itaendelea kutoa elimu kwa umma kuhusu utekelezaji na mafanikio ya mpango wa CBRM ili wananchi waendelee kunufaika na fursa zinazotokana na mpango huo.
‎Wakati huo huo, TARURA imewahimiza wananchi kuendelea kutembelea banda lake katika Maonesho ya Nanenane ili kupata elimu kuhusu majukumu ya Wakala, ufafanuzi wa masuala mbalimbali yanayohusu miundombinu ya barabara pamoja na kujionea mafanikio ya miradi inayotekelezwa nchini kwa lengo la kuimarisha maendeleo endelevu.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano), Deus Sangu,akiwahutubia washiriki wa mafunzo ya usalama na afya mahali pa kazi yaliyotolewa na OSHA katika Mgodi wa Namungo uliopo Wilaya ya Ruangwa Mkoani Lindi.
 

Na Mwandishi Wetu

Meneja Kanda ya Kati wa Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA), Bi. Hawa Lweno, ametoa wito kwa mafundi umeme kutembelea banda la Mamlaka hiyo katika Maonesho ya Nanenane yanayoendelea katika Viwanja vya John Malecela jijini Dodoma, ili kupata elimu kuhusu umuhimu wa kupata leseni za ufundi umeme zinazotolewa na EWURA, pamoja na utaratibu wa kuomba leseni hizo.

Amesema kuwa leseni za ufundi umeme ni muhimu katika kuhakikisha huduma za ufungaji, ukarabati na matengenezo ya mifumo ya umeme zinafanywa na mafundi wenye sifa na wanaozingatia viwango vya ubora na usalama, hivyo kupunguza ajali zinazoweza kusababishwa na kazi za umeme zisizokidhi matakwa ya kitaalamu.

“Hili linaendana sambamba na wito kwa wananchi kuhakikisha wanafanya ukaguzi wa mifumo yao ya umeme kila baada ya miaka mitano tangu mfumo huo ulipofungwa,” ameeleza.

Bi. Lweno amesema EWURA pia inatumia Maonesho ya Nanenane kutoa elimu kwa wananchi kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa Mkakati wa Taifa wa Nishati Safi ya Kupikia unaolenga kuongeza matumizi ya nishati safi kwa Watanzania.

Aidha, maeneo mengine yanayotolewa elimu ni pamoja na fursa za uwekezaji wa vituo vya mafuta katika maeneo ya vijijini, taratibu za kuwasilisha na kushughulikia malalamiko yanayohusu huduma zinazodhibitiwa na EWURA, pamoja na matumizi salama ya huduma za mafuta, umeme na gesi.