Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhandisi Maryprisca Mahundi amesema Serikali itaendelea kuwaunga mkono wafanyabiashara ndogondogo nchini wakiwemo wasusi, waendesha bodaboda, mama lishe na baba lishe kwa kuwawezesha kupata mikopo yenye masharti nafuu inayotolewa katika halmashauri mbalimbali.
Mahundi ameyasema hayo alipohudhuria tamasha la “Urembo na Ibada” lililoandaliwa na mjasiriamali na mmiliki wa saluni, Maria Wilson maarufu kama Chido Point, jijini Dar es Salaam na kukutanisha zaidi ya wanawake 300 Aprili 03, 2026.
Amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inaendelea kuweka mazingira rafiki kwa wafanyabiashara ndogondogo ili wajikwamue kiuchumi.
“Niwasihi mfike kwenye halmashauri zenu kufuata utaratibu wa mikopo hiyo na kuchangamkia fursa zilizopo. Aidha, nikiwa Mbunge wa Viti Maalum mkoa wa Mbeya, nitaendelea kushirikiana na Chido Point katika kuandaa na kuratibu tamasha hili, linalotarajiwa kufanyika mwezi Julai mwaka huu mkoani Mbeya,” amesema Mahundi.
Kwa upande wake muandaaji wa tamasha hilo, Maria Wilson amesema lengo la tamasha hilo ni kuwaunganisha wasusi kutoka mikoa mbalimbali ili kubadilishana uzoefu na kukuza taaluma ya ususi nchini na ameishukuru Serikali pamoja na Wizara ya Maendeleo ya Jamii kwa kuendelea kuwajali wasusi, huku akiomba wizara nyingine ikiwemo Wizara ya Afya kuangalia ustawi wao hasa katika masuala ya afya na usalama kazini.
“Tamasha hili linalenga kuwaunganisha wasusi na kuwahamasisha wazazi kuwapa kipaumbele watoto wao wenye vipaji vya ususi waweze kujiajiri na kuchangia maendeleo ya taifa” amesema Maria Wilson.
Baadhi ya washiriki wa tamasha hilo wameeleza kufurahishwa na jukwaa hilo pamoja na juhudi za Serikali, wakisema limewapa maarifa na motisha ya kukuza biashara zao na elimu waliyoipata imewapa mbinu mpya zitakazowasaidia kuboresha kazi zao.
Na Oscar Assenga
Kampuni ya Taifa Gesi imeendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa matumizi ya nishati safi, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuunga mkono sera ya Serikali ya kuhamasisha matumizi ya nishati rafiki kwa mazingira.
Akizungumza katika tamasha lililofanyika wilayani Handeni, Mkurugenzi wa Masoko wa Taifa Gesi, Oscar Shelukindo, alisema kampuni hiyo imekuwa ikishiriki katika matamasha ya kijamii tangu mwaka jana kwa lengo la kutoa elimu kwa wananchi kuhusu matumizi sahihi ya gesi safi.
Alisema kuwa katika tamasha hilo, wameelekeza nguvu zaidi kwa wakazi wa Handeni, hususan Kata ya Mdoe, ili kuwafikia wananchi wengi zaidi na kuwapa uelewa sahihi kuhusu faida za kutumia nishati hiyo.
“Tunafurahi kuwa hapa leo kutoa elimu ya matumizi ya gesi safi, kuondoa hofu kwa wananchi na kuwahamasisha kuachana na matumizi ya nishati zisizo rafiki kwa mazingira. Pia tunatoa gesi kwa bei nafuu ili kuwavutia zaidi kuitumia,” alisema Shelukindo.
Alifafanua kuwa bado kuna wananchi wengi ambao wana hofu au uelewa mdogo kuhusu matumizi ya gesi ya kupikia, hali inayowafanya kuendelea kutumia nishati kama kuni na mkaa, ambazo si rafiki kwa mazingira na pia zina madhara kiafya.
Kwa mujibu wa Shelukindo, utoaji wa elimu hiyo unalenga kubadili mtazamo wa jamii na kuwasaidia wananchi kuelewa kuwa gesi ni salama, nafuu kwa muda mrefu na rahisi kutumia.
Aidha, alisisitiza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya mchango wa sekta binafsi katika kusaidia juhudi za Serikali za kulinda mazingira, kupunguza ukataji wa miti na kuboresha afya za wananchi kupitia matumizi ya nishati safi.
Wananchi waliohudhuria tamasha hilo walipata fursa ya kuuliza maswali, kujifunza matumizi sahihi ya gesi pamoja na kununua bidhaa za gesi kwa bei iliyopunguzwa.
Kwa ujumla, jitihada za Taifa Gesi zinaonesha namna sekta binafsi inavyoweza kushirikiana na Serikali katika kuhamasisha matumizi ya nishati safi, hatua inayotarajiwa kuleta mabadiliko chanya katika jamii, hususan maeneo ya vijijini.

Wataalamu kutoka Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania (TAEC) wamehitimisha mafunzo maalum ya ulinzi na usalama dhidi ya mionzi kwa wafanyakazi wa Maweni Limestone Company. Mafunzo haya, yaliyofunguliwa na Meneja wa Idara ya Ubora wa kampuni hiyo, yalilenga kuwajengea uwezo wafanyakazi wanaoshughulika moja kwa moja na vifaa vya X-Ray Fluorescence (XRF) na nuclear gauges.
Kwa muda wa siku kadhaa, washiriki walipata nafasi ya kujifunza kwa kina kuhusu utambulisho wa mionzi ayonishi, kiasi cha mionzi na vipimo, matumizi ya mionzi, athari zake kiafya, kanuni za ulinzi, mfumo wa kisheria wa Tanzania, majukumu ya Afisa Usalama wa Mionzi (RSO), pamoja na usalama wa nyuklia na udhibiti wa usafirishaji haramu.
Katika hotuba ya kufunga mafunzo, wataalamu wa TAEC walisisitiza umuhimu wa kuimarisha utamaduni wa usalama kazini. “Tunataka kuona kila mfanyakazi akibeba jukumu la kulinda afya yake, wenzake na jamii kwa ujumla. Usalama wa mionzi si jambo la hiari, ni wajibu wa kitaifa,” alieleza Ndugu Mungubariki Nyaki, mkufunzi na msimamizi wa Ofisi ya TAEC Jijini Tanga.
Washiriki walionekana wenye shauku na ari ya kupeleka maarifa mapya kazini. Baadhi walikiri kuwa mafunzo haya yamewapa ujasiri wa kushughulika na vifaa vya mionzi kwa umakini zaidi, huku wengine wakisisitiza umuhimu wa kushirikiana na TAEC ili kuhakikisha viwango vya kitaifa na kimataifa vinazingatiwa.
Mafunzo haya pia yaligusia hatua za dharura endapo ajali za mionzi zitatokea, jambo lililowapa washiriki uelewa wa namna ya kukabiliana na changamoto kwa utulivu na ufanisi.
Kwa ujumla, kufungwa kwa mafunzo haya kumeacha taswira ya matumaini na uwajibikaji. Kampuni ya Maweni Limestone imeonyesha dhamira ya dhati ya kulinda wafanyakazi wake na jamii kwa kuhakikisha teknolojia za kisasa zinatumika kwa usalama na kwa manufaa ya Taifa.






Tamasha la Pasaka ‘Mtoko na Christina Shusho’
Na Mwandishi Wetu
WAZIRI Mkuu wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Nchemba, anatarajiwa kuwa mgeni rasmi Aprili 5, 2026, siku ya Jumapili ya Pasaka, katika tamasha la ‘Mtoko na Christina Shusho Pasaka’ litakalofanyika katika Ukumbi wa Mlimani City, jijini Dar es Salaam ambapo wananchi wataruhusiwa kuingia bure.
Kauli mbiu ya tamasha hilo ni “Ushindi wa Milele.”
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam Machi 30, 2026, Meneja wa msanii wa muziki wa injili Christina Shusho, Humphrey Gatimu, amesema maandalizi ya tamasha hilo yamekamilika kwa asilimia 100 na kusisitiza kuwa wananchi wote wanakaribishwa kushiriki bila malipo yoyote.
Na.Mwandishi Wetu
TUME ya Ushindani (FCC) Kanda ya Nyanda za Juu Kusini imeadhimisha Wiki ya Haki za Mlaji Duniani kwa kutoa msaada wa vifaa tiba katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya, ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za kuboresha huduma za afya kwa wananchi.
Shughuli hiyo imefanyika tarehe 31 Machi, 2026 ambapo FCC imekabidhi vifaa tiba vinne vya Oxygen Flow Meter vitakavyosaidia wagonjwa wanaohitaji huduma ya hewa tiba, hususan wale wanaopata changamoto ya kupumua.
Akizungumza wakati wa hafla ya makabidhiano hayo, Mkuu wa FCC Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, Bw.Dickson Mbanga, amesema kuwa tukio hilo ni sehemu ya kuadhimisha Wiki ya Haki za Mlaji Duniani pamoja na kutimiza miaka mitatu tangu kuanzishwa kwa ofisi hiyo katika ukanda huo.
Mbanga ameeleza kuwa FCC imeona ni vyema kutumia maadhimisho hayo kwa kutoa mchango wa kijamii utakaoleta tija moja kwa moja kwa wananchi, hasa katika sekta ya afya ambayo ni nyeti na muhimu kwa ustawi wa jamii.
"Vifaa hivyo vitasaidia kuongeza uwezo wa hospitali katika kuhudumia wagonjwa wanaohitaji msaada wa hewa tiba, hivyo kupunguza changamoto zinazoweza kujitokeza wakati wa utoaji wa huduma hizo."amesema Bw.Mbanga
Kwa upande wake, akipokea vifaa hivyo kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya, Muuguzi Kiongozi Ndg. Petro Seme ametoa shukrani za dhati kwa FCC kwa msaada huo muhimu.
Seme amesema kuwa vifaa hivyo ni vya kisasa na vina uwezo wa kuhudumia wagonjwa wawili kwa wakati mmoja, jambo ambalo litarahisisha upatikanaji wa huduma ya hewa tiba na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma kwa wagonjwa.


Katibu Mkuu-Mipango na Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango Dkt Tausi M. Kida ametoa wito kwa watendaji wa Tume hiyo kufanya kazi kwa weledi, ubunifu na ushirikiano ili kuishi dhana ya kufanya kazi isivyokawaida ili kuyafikia matarajio ya Taifa jumuishi, lenye ustawi, haki na linalojitegemea.
Dkt Kida ametoa wito huo leo jijini Dar es Salaam wakati akifungua Mkutano wa Baraza la Wafanyakazi wa Tume ya Taifa ya Mipango.
Aidha, amesisitiza kuwa Serikali ya awamu ya sita chini ya Mheshimiwa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan inayo matarajio makubwa kwa Tume ya kuhakikisha inatekeleza ipasavyo majukumu yake kwa weledi, ari na kuzingatia utu.
Mkutano huo, umeongozwa na kauli mbiu isemayo: Utumishi Imara ni Msingi wa Utekelezaji wa Dira 2050.






Mabadiliko ya bei za mafuta nchini kwa mwezi Aprili 2026 yamechangiwa kwa kiasi kikubwa na vita inayoendelea kati ya Marekani kwa kushirikiana na Israeli dhidi ya Irani iliyoanza tarehe 28 Februari 2026, mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) imesema jana.
“Kushambuliwa kwa visima vya mafuta, maghala ya kuhifadhi mafuta na viwanda vya kusafisha mafuta (refineries) pamoja na Irani kufunga Lango la Hormuz linalopitisha takriban asilimia 20 ya mafuta yanayosafirishwa kwenda kwenye masoko mbalimbali duniani, imeathiri hali ya uzalishaji mafuta kwenye nchi za Mashariki ya Kati ambako Tanzania inaagiza kwa kiasi kikubwa; imeongeza gharama za usafirishaji kutokana na kukosekana kwa meli za kusafirisha mizigo na imeongeza gharama za bima za meli za mizigo kutokana na vita,” imeeleza taarifa iliyosambazwa kwenye vyombo vya habari jana.
Kwa mwezi Aprili 2026, gharama za kuagiza mafuta (premiums) katika Bandari ya Dar es Salaam zimeongezeka kwa wastani wa asilimia 15.3 kwa mafuta ya petroli na asilimia 10.8 kwa mafuta ya dizeli na hakuna mabadiliko ya gharama kwa mafuta ya taa.
EWURA imesema ongezeko hilo ni janga la kidunia na Tanzania kama sehemu hiyo inachukua hatua mbalimbali kuhakikisha usalama wa upatikanaji wa mafuta nchini na bei himilivu ili kupunguza madhara ya kiuchumi na kijamii. Kutokana na hali hiyo, EWURA imewashauri wananchi kutumia mafuta kwa uangalifu na ufanisi mkubwa.
Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi, Hassan Saidy amewataka Watumishi wa Wakala kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi ili kuhakikisha ndani ya muda uliopangwa wanafikisha umeme kwenye vitongoji vyote vya Tanzania Bara.
Ametoa maelekezo hayo Machi 30, 2026 Makao Makuu ya REA, Jijini Dodoma wakati wa kikao kazi na Watumishi wote, ambapo amesema baada ya kusaini Mradi mkubwa wa HEP II (B); Mradi wa kusambaza umeme kwenye vitongoji 9,009 tarehe 17 Januari, 2026 na kuongeza kuwa kazi iliyombele ya kila Mtumishi ni kuhakikisha vitongoji hivyo vinafikishiwa umeme katika kipindi cha miaka mitatu yaani hadi 2029.
Awali ilielezwa kuwa Mradi huo wa HEP II (B) ni muendelezo wa jitihada za Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) za kuhakikisha upatikanaji wa huduma ya umeme kwa Wananchi wote wa Tanzania Bara.
Mhandisi Saidy amesema kukamilika kwa Mradi huo wa HEP II (B) pamoja na miradi mingine inayoendelea kutafanya jumla ya vitongoji ambavyo tayari vitakuwa vimefikishiwa umeme kuwa takriban 51,000 kufanya vitongoji vitakavyobakia bila umeme na bila kuwa katika mradi wowote kuwa taklibani 13,000 ambavyo vimepangwa kuanza kusambaziwa umeme ifikapo mwaka 2030 kama ilivyoelekezwa katika Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya Mwaka 2025 – 2030.
Mradi huo unatarajiwa kutoa manufaa ya moja kwa moja kwa Wananchi kwa kuongeza upatikanaji wa huduma ya umeme vitongojini; kuboresha huduma za kijamii hususan katika sekta za afya, elimu na maji; kuwezesha matumizi ya umeme katika shughuli za uzalishaji na kuongeza kipato cha Wananchi pamoja na kuchochea ukuaji wa uchumi wa maeneo ya vitogojini pamoja na kuimarisha ustawi wa jamii.
Aidha; Mhandisi, Saidy aliongoza Watumishi wa REA katika zoezi la kuchagua Viongozi wa TUGHE tawini hapo ambapo kwa kauli moja Watumishi waliwachagua Viongozi wao katika ngazi tofauti kama ifuatavyo: – Mwenyekiti wa Tawi ni Bwana Swalehe Kiloza, Katibu wa Tawi ni Mhandisi, Annet Malingumu; Mjumbe wa Halmashauri ya Tawi ni Bwana Issa Sabuni na Mwakilishi wa Kundi la Vijana, Mhandisi, Issac Sanga.
Viongozi wengine ni pamoja na Wajumbe wa Kamati ya Wanawake ya Tawi la TUGHE REA ni kama ifuatavyo: – Mwenyekiti ni Bi. Wilhelmina Cheyo; Katibu ni Bi. Ruth Emmanuel; Mweka Hazina ni Bi. Aveline Wilfred; Wajumbe Kamati ya Wanawake ni Bi. Happiness Ndunguru na Mhandisi, Bertha Mwaituka.
Vilevile Watumishi wa REA pia walichagua Viongozi kwa upande wa Klabu ya Michezo ya REA ambapo itaongozwa na Bwana Selemani Mtunzy kama Mwenyekiti na Mwenyekiti Msaidizi ni Bwana Samwel Sumwa; Katibu ni Bwana Praygod Ng’hunda; Mweka Hazina ni Bwana Daniel Kisaka wakati Wajumbe wa Kamati Tendaji kwa upande wa Wanaume atakuwa Mhandisi, Thomas Mmbaga na kwa upande wa Wanawake atakuwa Bi. Beatrice Shelukindo.
Wakati huo huo Watumishi wa REA walishiriki kwenye zoezi la kuchagua Viongozi wa Chama cha Kijamii cha Wafanyakazi (REA Social Club) chenye lengo la kusaidiana wakati wa raha na changamoto mbalimbali. Viongozi wa Chama hicho waliochaguliwa ni kama ifuatavyo: Mwenyekiti ni Bwana Elias Gunzer; Katibu ni Bi. Theresia Mang’ung’ula; Mweka Hazina ni Bwana Shukuru Malebeto; Wajumbe wa Kamati Tendaji ni Bwana Pastory Mwijage na Bi. Emmy Chali.
Na Carlos Claudio, Dodoma.
Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali imegawa vifaa vya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) vyenye thamani ya jumla ya Shilingi milioni 769 kwa shule za msingi na sekondari 19 zilizopo katika mikoa tisa nchini, ikiwemo Kusini Unguja (Zanzibar), Dodoma, Iringa, Ruvuma, Arusha, Geita, Kilimanjaro, Mbeya na Mtwara.
Akizungumza katika hafla ya ugawaji wa vifaa hivyo iliyofanyika jijini Dodoma, Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Wanu Hafidh Ameir, alisema hatua hiyo ni sehemu ya juhudi za Serikali za kuendelea kuimarisha sekta ya elimu kwa kuzingatia matumizi ya teknolojia za kisasa.
Alisema matumizi ya vifaa hivyo yataongeza uelewa kwa wanafunzi kwa kuwapa fursa ya kujifunza kwa vitendo na kuona, hasa katika masomo ya sayansi na teknolojia. Aidha, alieleza kuwa walimu watanufaika kwa kutumia mbinu bunifu za ufundishaji, kuandaa maudhui kwa ufanisi na kufuatilia maendeleo ya wanafunzi kwa urahisi kupitia mifumo ya kidijitali.
“Serikali inaendelea kutekeleza mageuzi makubwa katika sekta ya elimu kama yalivyoainishwa katika Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014 (Toleo la 2023) pamoja na mitaala iliyoboreshwa, kwa lengo la kuboresha ubora wa elimu na kuandaa rasilimali watu yenye ujuzi unaokidhi mahitaji ya sasa na ya baadaye,” alisema Ameir.
Alitaja baadhi ya hatua zinazoendelea kuchukuliwa kuwa ni pamoja na utekelezaji wa elimu ya lazima ya miaka 10, kuanzishwa kwa mkondo wa elimu ya amali unaolenga kuwapatia wanafunzi stadi za ufundi na ujasiriamali, pamoja na kuimarisha matumizi ya teknolojia za kidijitali katika ufundishaji, ujifunzaji na usimamizi wa elimu.
Aidha, aliongeza kuwa Serikali imeandaa na kuanza kutekeleza Mkakati wa Kitaifa wa Matumizi ya Teknolojia za Kidijitali katika Elimu, sambamba na miongozo mbalimbali ikiwemo mwongozo wa matumizi ya TEHAMA katika shule na vyuo vya ualimu pamoja na mwongozo wa matumizi ya Akili Unde (AI) katika elimu.
Kwa upande mwingine, alisema katika mwaka wa fedha 2025/2026, Serikali imeanzisha madarasa janja matano na kufunga mbao janja 422 katika shule za sekondari, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuboresha mazingira ya ujifunzaji nchini.
Naye Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Caroline Nombo, alisema Serikali inaendelea kuchukua hatua madhubuti za kuboresha elimu kwa kuzingatia mahitaji ya karne ya 21, hususan kwa kuimarisha matumizi ya teknolojia za kidijitali.
Alisema ugawaji wa vifaa hivyo ni sehemu ya utekelezaji wa sera ya elimu pamoja na mkakati wa TEHAMA katika sekta hiyo, na ni ushahidi wa dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha walimu na wanafunzi wanapata nyenzo bora za kufundishia na kujifunzia.
Profesa Nombo alisisitiza kuwa vifaa hivyo vitachangia kwa kiasi kikubwa kuboresha ubora wa elimu, kuongeza ufanisi wa ufundishaji na ujifunzaji, pamoja na kuwawezesha wanafunzi kupata ujuzi wa kidijitali unaohitajika katika dunia ya sasa.
Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais na Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) imeweka mikakati madhubuti ya kuimarisha mfumo wa usimamizi wa taka kwa kuandaa Mkakati wa Taifa wa usimamizi wa Taka (2025 - 2030) ambao unalenga kupunguza uzalishaji wa taka kwa kutumia dhana ya uchumi rejeshi.
Katika kuhakikisha mnyororo wa usimamizi wa taka unaimarika, Serikali inahamasisha wadau hususan sekta binafsi kuwekeza katika matumizi ya teknolojia za kisasa za kuchakata taka, uwekezaji katika viwanda vya urejelezaji na kuimarisha mifumo ya ukusanyaji wa taka ili kufikia malengo ya kupunguza au kuondoa taka katika Mazingira kwa kuigeuza kuwa malighafi ya uzalishaji wa bidhaa anuwai zinazofaa kwa matumizi mbalimbali.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni ameyasema hayo katika maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Taka Sifuri, Viwanja vya Mnazi Mmoja, jijini Dar es Salaam, Machi 30, 2026.
Amesema Siku ya Kimataifa ya Taka Sifuri huadhimishwa kila mwaka Machi 30 kwa lengo la kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa kupunguza matumizi ya bidhaa zinazopelekea kuzalisha taka, kutumia tena bidhaa kabla ya kugeuzwa taka na kuchakata taka kwa kurejeleza ili kuepuka uchafuzi wa mazingira.
“Kauli mbiu ya kimataifa kwa mwaka huu inatoa hamasa ya "KUWEZESHA TAKA SIFURI KWENYE SEKTA YA CHAKULA" ikiwa na lengo la kuhimiza matumizi endelevu ya vyakula na kupunguza taka zitokanazo na sekta hii. Kwa upande wa Tanzania, kauli mbiu ya Kitaifa inahimiza kutambua "TAKA NI FURSA" ikisisitiza kuwa taka si uchafu bali ni malighafi yenye thamani, endapo itasimamiwa na kuchakatwa vyema.”
“Uzalishaji wa taka umekuwa changamoto kubwa kwa nchi za Ugaibuni na Africa, hususani katika miji mikubwa kama Dar es Salaam, Mwanza na Arusha na takwimu zinaonesha takribani kiasi cha tani zaidi ya millioni 7 za taka ngumu huzalishwa nchini kwa mwaka ambapo wastani wa asilimia 45 hadi 50 tu hukusanywa na kutupwa dampo.
Aidha, amesema asilimia 50 hadi 55 hubaki kwenye mazingira na kuzagaa kwenye mito na mifereji ya maji taka na mitaro ya maji ya mvua. Hata hivyo, matokeo ya Sensa ya Taifa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022 yanaonesha kuwa, asilimia 40 ya kaya zinachoma taka ngumu na asilimia 22 ya kaya zinatumia njia ya ukusanyaji sahihi wa mara kwa mara.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Dkt. Immaculate Sware amesema ni wakati sasa wa kubadili mtazamo kuwa taka si uchafu tu bali ni rasilimali yenye thamani.
Amesema mabaki ya chakula yanaweza kuzalisha mbolea na nishati, plastiki inaweza kurejelezwa na kuwa bidhaa mpya, na chuma chakavu kinaweza kurejelezwa na kuzalisha bidhaa nyingine.
“Ninatoa wito kwa kila mmoja wetu kuanzia maeneo ya makazi, biashara na viwandani kuchukua hatua madhubuti za kupunguza uzalishaji wa taka, kuchambua taka katika vyanzo vyake na kuimarisha utamaduni wa kuchakata taka.”

Katika kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia, Wakala wa Vipimo (WMA) imetoa misaada ya vifaa vya ujenzi wa jiko la kisasa katika Kituo cha kulelea watoto wenye mahitaji maalumu Cha RAHMAN ORPHANAGE CENTER kilichopo Chang'ombe jijini Dodoma.

Akizungumza baada ya kutoa misaada hiyo Meneja wa WMA Mkoa wa Dodoma Said Ibrahimu amesema suala la mazingira safi ya kupikia ni haki ya kila mmoja ndio maana wameamua kama Wakala kutoa misaada hiyo itakayowezesha upishi wa kisasa katika mazingira safi na salama ikiwemo usalama wa chakula kwani kituo hicho wamekuwa wakipika kwa kutumia kuni na mazingira ya Nje ambayo sio salama kwa afya ya watoto hao.
"tunamuunga mkono Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha nishati safi ya kupikia inakuwa katika mazingira safi na salama ndio maana leo kwa niaba ya wafanyakazi wa WMA tumekabidhi Sementi, Marumaru na vifaa vingine vitakavyosaidia ujenzi wa jiko hilo, "amesema Meneja Said

Kadhalika, Mkurugenzi wa kituo hicho Bi. Rukia Abdallah ameishukuru WMA kwa misaada hiyo itakayokwenda kuboresha mazingira ya mapishi katika Kituo hicho chenye idadi ya watoto 120 huku akiomba wadau wengine kujitokeza kuchangia kituo hicho ikiwemo suala la usafiri ili watoto hao waweze kutembelea maeneo mbalimbali kwa ajili ya kujifunza zaidi.
Mmoja wa watoto wanaolelewa katika Kituo hicho Hazra Ramadhan ameipongeza Wakala wa Vipimo kwa kuona umuhimu wa kuwasaidia na kuwaomba kuendelea kuwakumbuka kila mara ili waweze kutimiza malengo yao.





















.jpeg)










.jpg)