Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule, ameukaribisha Umoja wa Vyombo vya Habari vya Mitandao ya Kijamii Mkoa wa Dodoma (UMIKIDO) na kuutaka kuwa chachu ya kuimarisha mawasiliano kati ya Serikali na wananchi kupitia utoaji sahihi wa taarifa pamoja na ubunifu wa maudhui.

RC Senyamule ametoa kauli hiyo leo Februari 9, 2026, mara baada ya viongozi wa UMIKIDO kufika ofisini kwake kwa lengo la kujitambulisha na kuomba ushirikiano na Serikali ya Mkoa wa Dodoma.

“Hongereni kwa kuanzisha umoja huu. Nimefurahishwa sana kwani utarahisisha kazi na kuwa kiunganishi muhimu kati ya Serikali ya Mkoa na vyombo vya habari vya mitandaoni. Tulitamani kupata watu wanaozungumza lugha moja na Serikali, na tunaamini ninyi ni wazalendo,” amesema Mhe. Senyamule.

Ameeleza kuwa uwepo wa umoja huo utaisaidia Serikali kufikisha taarifa kwa wananchi kwa ufanisi zaidi, sambamba na kuongeza uelewa wa umma kuhusu shughuli na miradi mbalimbali inayotekelezwa na Serikali kwa ajili ya maendeleo ya Taifa.

“Ni muhimu Watanzania wakaendelea kufahamu kazi zinazofanywa na Serikali. Nina imani mtakuwa wabunifu katika kuandaa na kusambaza taarifa kwa njia zitakazowafikia wananchi kwa urahisi,” ameongeza.

Aidha, RC Senyamule amewataka wanachama wa UMIKIDO kuzingatia kutangaza miradi ya kimkakati na mipango ya maendeleo, ikiwemo uhifadhi wa mazingira, matumizi ya nishati safi ya kupikia, sekta ya utalii na michezo, pamoja na kuhamasisha matukio mbalimbali kuelekea mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2027.

Awali, viongozi wa UMIKIDO walieleza dhamira na malengo ya kuanzishwa kwa umoja huo, ikiwa ni pamoja na kuimarisha maadili ya uandishi wa habari za mitandaoni na kushirikiana kwa karibu na Serikali katika utoaji wa taarifa sahihi kwa umma. Pia waliomba ushirikiano kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa ili kutimiza malengo hayo.

Viongozi walioshiriki ziara hiyo ni (Mwenyekiti wa UMIKIDO Bw.Benny Majata,Katibu Emmanuel Charles, Zena Chitwanga (Mhasibu), Daniel Mkate (Afisa Mahusiano), Alex Sonna (Kamati ya Ufuatiliaji), Henry Masanja (Kamati ya Nidhamu) na Ronald Sonyo (Kamati ya Fedha na Mipango).



 


Na OWM – TAMISEMI, Dar es Salaam

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amekutana na Wakuu wa Mikoa wapya  wa Mkoa wa Kagera na Mtwara, Mhe. Kanali Yahya Ramadhani Kido na Mhe. Kanali Donald Wiliam Msengi ili kujipanga kiutendaji katika kutekeleza maelekezo ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan aliyoyatoa ili kuimarisha ufanisi na uwajibikaji katika kuwatumikia wananchi.

Prof. Shemdoe amekutana na Wakuu  hao leo Februari 09, 2026 katika Ofisi Ndogo ya TAMISEMI Jijini Dar es Salaam, mara baada ya viongozi hao kuapishwa na Mhe. Rais katika Ikulu ya Magogoni, ambapo Mhe. Rais amewataka viongozi hao kwenda kuimarisha uwajibikaji ili kukidhi matarajio ya wananchi hususani kwenye eneo la upatikanaji wa huduma za kijamii pamoja na ulinzi na usalama wa wananchi na mali zao.

Katika kuhakikisha viongozi hao wanatekeleza maelekezo ya Mhe. Rais kwa ufanisi, Prof. Shemdoe amewataka kuhakikisha, wanakwenda kuandikisha wakazi wote kwenye daftari la makazi, pamoja na  kusikikiliza na kutatua kero za wananchi kwa kushirikiana na viongozi na watumishi waliopo katika maeneo yao mapya ya Utawala.

Kikao kazi hicho cha Prof. Shemdoe na Wakuu wa hao ni hatua ya awali ya kujipanga na utekelezaji wa maelekezo ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan aliyoyatoa leo, wakati wa uapisho wa viongozi aliowateua Februari 06, 2026 kwa lengo la kuleta mabadiliko yatakayo imarisha ufanisi na uwajibikaji ili kuendana na kasi ya mahitaji ya wananchi.

 

Serikali yazindua Sera ya Taifa ya Kinga ya Jamii na ‘Hifadhi Scheme’ kwa Waliojiajiri

Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Mahusiano imezindua Sera ya Taifa ya Kinga ya Jamii pamoja na Mpango wa Hifadhi ya Jamii kwa Wananchi Waliojiajiri ‘Hifadhi Scheme’ hatua inayolenga kupanua wigo wa hifadhi ya jamii na kuongeza ushirikishwaji wa wananchi katika mifumo ya kinga ya kijamii.

Uzinduzi huo umefanyika Februari 9, 2026 katika mkutano wa wadau wa sekta ya kinga ya jamii uliofanyika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Arusha (AICC), ukiongozwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu kwa niaba ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Sangu alisema sera hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, inayolenga kuhakikisha wananchi wanapata huduma jumuishi za hifadhi ya jamii. Aliongeza kuwa tangu 2018, Serikali imefanya maboresho ikiwemo kuunganisha Mifuko ya Hifadhi ya Jamii na kubaki na NSSF na PSSSF ili kuongeza ufanisi wa huduma na ulipaji wa mafao.

Mhe. Sangu alisema maboresho hayo yameongeza idadi ya wanachama. NSSF imeongezeka kutoka wanachama 808,935 mwaka 2020 hadi zaidi ya wanachama 2,213,659 mwaka 2025, huku PSSSF ikiongezeka kutoka 697,677 hadi 899,948. Aidha, thamani ya uwekezaji wa Mifuko imeongezeka kutoka shilingi trilioni 9.36 hadi trilioni 20.14, na jumla ya thamani ya Mifuko kufikia trilioni 24.20.

Kuhusu mpango wa Hifadhi Scheme, alisema hadi Desemba 2025 zaidi ya wanachama 500,000 kutoka makundi mbalimbali yakiwemo wakulima, wafugaji, wavuvi na wajasiriamali wamejiunga, huku lengo likiwa kufikia wanachama milioni 5.5 ifikapo Juni 2031.

Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Mary Maganga, alisema Serikali imeipa NSSF jukumu la kupanua wigo wa hifadhi ya jamii kwa wananchi waliojiajiri ili kuhakikisha sera mpya inaleta matokeo yanayotarajiwa.

Awali, Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, Bw. Masha Mshomba, alisema Mfuko unaendelea kuboresha utoaji wa huduma, kuongeza uandikishaji wa wanachama wapya, na kupanua wigo wa uwekezaji ndani na nje ya nchi, ikiwemo nchi za SADC na Afrika Mashariki.

Bw. Mshomba alisema Mfuko umepata mafanikio makubwa katika Serikali ya awamu ya sita ambapo thamani ya NSSF imeongezeka kutoka trilioni 4.8 mwaka 2021 hadi trilioni 10.4 Desemba 2025, na kuwa imepata ziada kwa miaka minne mfululizo kuanzia 2021 hadi mwaka wa fedha 2024/25, ikivuka lengo la ziada ya shilingi trilioni moja.

Akizungumzia ukusanyaji wa michango, Bw. Mshomba alisema Mfuko umeendelea kuvuka malengo, ambapo mwaka wa fedha 2023/24 ulifikia zaidi ya shilingi trilioni mbili, huku mwaka 2024/25 makusanyo yakizidi trilioni 2.4 na kwamba katika kipindi cha miaka mitano mfululizo kuanzia 2020 hadi 2025, NSSF imefanikiwa kuvuka lengo la kukusanya angalau shilingi trilioni moja kwa mwaka. 

Bw. Mshomba aliongeza kuwa mafanikio hayo yamechangiwa na juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan. NSSF ina zaidi ya wanachama milioni 2.3 na imejikita kuboresha huduma kupitia TEHAMA na mpango wa miaka mitano unaolenga kufanikisha malengo ya Dira ya Taifa 2050 na Ilani ya Uchaguzi ya CCM. 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Ajira na Mahusiano, Deus Sangu, amewataka wadau wa mifuko ya hifadhi ya jamii kuimarisha utoaji wa huduma kwa kuhakikisha taarifa za wanachama zinakuwa sahihi na waajiri wote wanawasilisha michango kwa wakati.

Akizungumza leo Februari 9, 2026, wakati wa Mkutano wa Wadau wa Sekta ya Kinga ya Jamii unaofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC), Waziri Sangu amesema utekelezaji wa wajibu wa kila muajiri ni hatua muhimu ya kupunguza usumbufu unaowakabili wanachama wanapohitaji huduma.

“Mifuko iimarishe utoaji wa huduma kwa kuhakikisha taarifa za wanachama zipo sahihi na waajiri wote wanawasilisha michango kwa wakati. Katika hili, kila muajiri atekeleze wajibu wake, hii itasaidia kuwaondolea wanachama usumbufu,” amesema Sangu.

Mkutano huo umewakutanisha wadau mbalimbali wakiwemo Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF), Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF), Mfuko wa Maendeleo ya Jamii Tanzania (TASAF) pamoja na Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF).

Mkutano unaongozwa na kauli mbiu “Kinga ya jamii kwa maendeleo”, na umeambatana na uzinduzi wa Sera ya Kinga ya Jamii ya mwaka 2023, inayolenga kuimarisha mifumo ya kinga ya jamii ili kuchochea ustawi wa wananchi na maendeleo endelevu ya taifa.














 

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akiwa na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe. Prof. Adolf Mkenda (kulia) pamoja na Viongozi mbalimbali, wakionesha Mpango wa Ushirikiano kati ya Taasisi za Elimu na Viwanda mara baada ya kuuzindua katika hafla iliyofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) Jijini Dar es Salaam, leo tarehe 09 Februari 2026.



Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akizindua Mpango wa Ushirikiano kati ya Taasisi za Elimu na Viwanda katika hafla iliyofanyika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) Jijini Dar es Salaam, leo tarehe 09 Februari 2026.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akihutubia wakati wa Uzinduzi wa Mpango wa Ushirikiano kati ya Taasisi za Elimu na Viwanda uliyofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) Jijini Dar es Salaam, leo tarehe 09 Februari 2026.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, akiwa na Viongozi mbalimbali katika picha ya pamoja na baadhi ya Waajiri, mara baada ya kuzindua Mpango wa Ushirikiano kati ya Taasisi za Elimu na Viwanda katika hafla iliyofanyika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) Jijini Dar es Salaam, leo tarehe 09 Februari 2026.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akiwasili katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) Jijini Dar es Salaam kwaajili ya Uzinduzi wa Mpango wa Ushirikiano kati ya Taasisi za Elimu na Viwanda, leo tarehe 09 Februari 2026.


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akiwa na Viongozi mbalimbali wakati akishiriki Uzinduzi wa Mpango wa Ushirikiano kati ya Taasisi za Elimu na Viwanda uliyofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) Jijini Dar es Salaam, leo tarehe 09 Februari 2026.