Tume ya Ushindani Tanzania (FCC) imeendelea kuimarisha kampeni ya utoaji elimu kwa umma kuhusu madhara ya biashara ya bidhaa bandia, ikisisitiza kuwa utengenezaji, usambazaji na uuzaji wa bidhaa hizo ni kosa la jinai linaloadhibiwa kwa mujibu wa sheria za nchi.

Akizungumza leo Juni 22, 2026, katika eneo la Kariakoo Jijini Dar es Salaam, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Uhusiano kwa Umma wa FCC, Bi. Roberta Feruzi, amesema bidhaa bandia zina athari kubwa kwa uchumi, afya na usalama wa wananchi, huku zikidhoofisha ushindani wa haki katika biashara.

Amesema watu watakaobainika kujihusisha na biashara ya bidhaa bandia wanaweza kukabiliwa na adhabu ya kifungo cha kati ya miaka minne hadi 15 jela pamoja na faini inayofikia kati ya Shilingi milioni 10 na milioni 50, kulingana na masharti ya sheria husika.

Bi. Feruzi ameeleza kuwa FCC inaendelea kushirikiana na taasisi mbalimbali za ndani na kimataifa katika kudhibiti bidhaa bandia ili kuhakikisha haziingii nchini, hazisambazwi katika soko la ndani, wala kutumiwa kama njia ya kupitishwa kwenda mataifa mengine kupitia mifumo ya usafirishaji.

Amebainisha kuwa nafasi ya Tanzania kama lango muhimu la biashara na usafirishaji katika ukanda wa Afrika Mashariki inaifanya nchi kuwa miongoni mwa maeneo yanayoweza kutumiwa na wahalifu kusafirisha bidhaa bandia, hali inayohitaji ushirikiano wa karibu kati ya serikali, sekta binafsi na wananchi katika kupambana na tatizo hilo.

Kwa mujibu wa Bi. Feruzi, biashara ya bidhaa bandia si changamoto ya Tanzania pekee, bali ni tatizo la kimataifa linalosababishwa na watu wasio waaminifu wanaotafuta faida kwa kutumia kazi, ubunifu na alama za biashara za wengine kinyume cha sheria.

Ametoa wito kwa wananchi na wafanyabiashara kuwa makini wanaponunua au kuuza bidhaa, huku akiwahimiza kutoa taarifa kwa mamlaka husika wanapobaini uwepo wa bidhaa zinazohisiwa kuwa bandia.

Vilevile, amesema Tanzania itaadhimisha Siku ya Kitaifa ya Udhibiti wa Bidhaa Bandia Juni 25, 2026, yakiwa na  kauli mbiu isemayo: "Linda Maisha na Masoko Dhidi ya Pombe, Vilainishi na Sigara Bandia" ambapo maadhimisho hayo yatatumika kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu athari za bidhaa bandia na kuimarisha juhudi za kitaifa na kimataifa za kupambana na biashara hiyo haramu.

Amesisitiza kuwa mafanikio ya vita dhidi ya bidhaa bandia yanategemea ushirikiano wa wadau wote, ikiwemo Serikali, wafanyabiashara , wazalishaji na wananchi, ili kulinda uchumi wa taifa, afya za watumiaji na mazingira ya biashara yenye ushindani wa haki.



Na Benny Mwaipaja, Dodoma

Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, limepitisha kwa kishindo Bajeti Kuu ya Serikali ya Mwaka wa Fedha 2026/27 kwa asilimia 97.66 baada ya wabunge 385 kupiga kura ya ndio kuunga mkono Bajeti hiyo.

Akitangaza matokeo ya kura ya wazi iliyopigwa bungeni jijini Dodoma, Spika wa Bunge Mhe. Mussa Azzan Zungu alisema kuwa kati ya kura hizo 393 zilizopigwa, kura 8 zimekataa kuunga mkono bajeti hiyo na wabunge wengine nane 8 hawakupiga kura kwa sababu hawakuwepo bungeni.

Akihitimisha hoja baada ya Bunge kupitisha Muswada wa Sheria kwa ajili ya kuidhinisha Serikali kuanza kutekeleza Bajeti Kuu ya Serikali ya Mwaka wa Fedha 2026/2026 (zaidi ya shilingi trlilioni 62.33) kutoka katika Mfuko Mkuu wa Hazina, Mhe. Spika Zungu alimpongeza Waziri wa Fedha, Mhe. Ballozi Khamis Mussa Omar (Mb) wasaidizi wake, watendaji wa Wizara kwa kazi kubwa na nzuri waliyoifanya na Wabunge wote kwa michango yao yenye tija kwa Taifa.

“Kura zimepigwa na Serikali imeruhusiwa kuzitumia pesa kuanzia sasa, mkazitumie pesa hizi kama Kamati za Bunge zilivyoelekeza, kuhakikisha maslahi ya watu kwanza yanazingatiwa kabla ya mambo mengine. Bunge hili litaendelea kufuatilia utekelezaji wake na kuhakikisha kuwa miradi yote iliyoainishwa inazingatiwa na kuleta furaha kwa wananchi” alisisitiza Mhe. Zungu.

Kupitia kwa Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), Serikali ililiomba Bunge lipitishe Bajeti ya shilingi trilioni 62.33 kwa ajili ya matumizi ya kawaida na maendeleo katika Mwaka wa Fedha 2026/2027, ikiwa ni ongezeko la asilimia 10.3 ikilinganishwa na bajeti ya mwaka 2025/26. 

Mhe. Balozi Omar alisema kuwa, mapato yalitarajiwa kuwa shilingi trilioni 46.79 ambapo mapato ya kodi ni shilingi trilioni 36.99, mapato mengine ni shilingi trilioni 9.24 (ikijumuisha mapato ya Mamlaka za Serikali za Mitaa shilingi trilioni 1.977) na misaada kutoka kwa washirika wa maendeleo shilingi bilioni 563.1.

Aidha aliongeza kuwa ili kuendana na dhamira ya kujitegemea katika uendeshaji wa Serikali na maendeleo, takribani robo tatu ya bajeti yote ya mwaka 2026/27, sawa na asilimia 74.2 itagharamiwa na mapato ya ndani.

Matumizi na uwekezaji katika mali zisizo za kifedha yalikadiriwa kuwa shilingi trilioni 54.50 pasipo kujumuisha malipo ya mtaji wa deni la Serikali ambapo kati ya kiasi hicho, stahiki za watumishi ikijumuisha michango ya pensheni ni shilingi trilioni 10.13.

“Gharama za bidhaa na huduma itakuwa shilingi trilioni 5.22, malipo ya riba ni shilingi trilioni 6.86, ruzuku shilingi trilioni 25.32, mafao na misaada ya kijamii shilingi trilioni 1.01, uwekezaji katika mali zisizo za kifedha shilingi trilioni 2.33 na gharama nyingine shilingi trilioni 3.63.” alisema Mhe. Balozi Omar

Aliongeza kuwa kulingana na makadirio ya mapato na matumizi hayo, kunajitokeza nakisi kwenye bajeti ya shilingi trilioni 7.71 na Serikali itaendelea kugharamia nakisi ya bajeti hiyo kwa kutumia mikopo kutoka vyanzo vya ndani na nje kwa kuzingatia Mkakati wa Muda wa Kati wa Kusimamia Deni la Serikali (2025/26 – 2027/28).

Mhe. Balozi Omar alisema kuwa, katika mwaka 2026/27, Serikali inatarajia kukopa jumla ya shilingi trilioni 15.54 ambapo kati ya kiasi hicho, mikopo ya ndani itakuwa shilingi trilioni 6.56, mikopo ya nje yenye masharti nafuu shilingi trilioni 6.55 na mikopo ya nje yenye masharti ya kibiashara shilingi trilioni 2.43.
Aidha, Serikali inakadiria kulipa malipo ya mtaji kwa mikopo iliyoiva shilingi trilioni 7.84.

Baada ya kupitishwa kwa bajeti hiyo, Bunge linatarajia kupokea, kujadili na kupitisha Muswada wa Sheria ya Fedha wa Mwaka 2026 ( The Finance Bill,2026) tarehe 24 Juni, 2026

Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) imeendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu haki na wajibu wao katika sekta za nishati na maji, sambamba na kuhamasisha uwekezaji wa vituo vya mafuta vijijini ili kuongeza upatikanaji wa huduma salama na kukomesha biashara holela ya mafuta.

Hatua hiyo ni sehemu ya mafanikio ya ushiriki wa EWURA katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali, jijini Dodoma, ambapo maelfu ya wananchi wamefika katika banda la mamlaka hiyo kupata elimu na ufafanuzi kuhusu huduma mbalimbali zinazodhibitiwa na EWURA.

Akizungumza katika maonesho hayo, Kaimu Meneja wa Mawasiliano na Uhusiano wa EWURA, Wilfred Mwakalosi, amesema kwa siku nane mfululizo mamlaka hiyo imekuwa ikitoa elimu kwa wananchi kuhusu sekta za mafuta, umeme, gesi asilia na maji, pamoja na kupokea na kushughulikia maswali na changamoto mbalimbali zinazowakabili watumiaji wa huduma hizo.

Amesema wananchi wengi walitumia fursa hiyo kupata ufahamu kuhusu namna ya kuwasilisha malalamiko wanapokumbana na changamoto za huduma, huku mada ya uwekezaji katika vituo vya mafuta vijijini ikiwa miongoni mwa masuala yaliyoibua maswali mengi zaidi.

“Wananchi wengi walitaka kufahamu taratibu na fursa zilizopo za kuanzisha vituo vya kisasa vya mafuta vijijini ili kuondokana na biashara ya mafuta inayofanyika kwa kutumia chupa, ndoo na magaloni, ambayo mara nyingi huhatarisha usalama wa watu na mali,” amesema Mwakalosi.

Ameeleza kuwa Serikali kupitia EWURA imeweka mazingira rafiki ya uwekezaji kwa kupunguza kwa kiasi kikubwa gharama za vibali na leseni kwa wawekezaji wa vituo vya mafuta vijijini.

Kwa mujibu wa EWURA, ada ya kibali cha ujenzi wa kituo cha mafuta katika maeneo ya vijijini imepunguzwa kutoka Shilingi 500,000 zinazotozwa maeneo ya mijini hadi Shilingi 50,000, huku ada ya leseni ikishushwa kutoka Shilingi milioni moja hadi Shilingi 100,000.

Mbali na punguzo hilo, EWURA imepunguza baadhi ya masharti ya uwekezaji kwa kuruhusu matumizi ya nyaraka za uthibitisho wa umiliki wa ardhi zinazotolewa na serikali za vijiji badala ya hati kamili za ardhi zinazohitajika katika maeneo ya mijini.

Hatua hiyo inalenga kuvutia wawekezaji wengi zaidi katika maeneo ya vijijini na kuongeza upatikanaji wa mafuta kwa njia salama, nafuu na inayozingatia viwango vya usalama.

Katika maonesho hayo, wananchi pia walipata ufafanuzi kuhusu namna EWURA inavyosimamia ukokotoaji wa bei za mafuta, viwango vya huduma za maji na umeme, pamoja na taratibu za kuwasilisha malalamiko pale wanaporidhika au kutoridhika na huduma zinazotolewa na watoa huduma.

Aidha, Mwakalosi amewahimiza wananchi kusoma na kuelewa mikataba ya huduma kwa wateja inayotolewa na taasisi za maji, umeme na nishati, akieleza kuwa mikataba hiyo inaainisha kwa uwazi haki, wajibu na viwango vya huduma vinavyopaswa kutolewa kwa mteja.

Amesisitiza kuwa wananchi wenye uelewa wa mikataba hiyo wanakuwa na uwezo mkubwa wa kudai huduma bora, kufuatilia utekelezaji wa haki zao na hata kudai fidia pale ambapo watoa huduma watashindwa kutekeleza viwango walivyoahidi.

Vilevile, EWURA imewahakikishia wananchi kuwa nchi inaendelea kuwa na hali nzuri ya upatikanaji wa umeme, gesi na maji kutokana na uwekezaji mkubwa unaoendelea kufanywa na Serikali katika sekta hizo.

Mwakalosi ametaja ongezeko la uzalishaji wa umeme kupitia Bwawa la Mwalimu Nyerere kuwa miongoni mwa hatua zilizochangia kuimarika kwa huduma za nishati nchini, huku EWURA ikiendelea kusimamia upatikanaji endelevu wa huduma za maji na nishati kwa manufaa ya wananchi wa sasa na vizazi vijavyo.




Na Mwandishi Wetu - Dodoma


Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC) imehitimisha kwa mafanikio ushiriki wake katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yaliyofanyika katika Viwanja vya Chinangali jijini Dodoma, ambapo ilitoa elimu kwa wananchi kuhusu matumizi salama ya mionzi na mchango wa teknolojia ya nyuklia katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi nchini.

Katika kipindi chote cha maonesho hayo, banda la TAEC lilitembelewa na wananchi, wanafunzi, wataalamu na wadau mbalimbali waliopata fursa ya kujifunza kuhusu majukumu ya Tume katika kusimamia matumizi ya mionzi nchini pamoja na kuhakikisha teknolojia ya nyuklia inatumika kwa kuzingatia viwango vya usalama vinavyolinda afya za binadamu na mazingira.

Wataalamu wa TAEC walitoa elimu kuhusu usimamizi na udhibiti wa matumizi ya vyanzo vya mionzi, utoaji wa vibali kwa watumiaji wa teknolojia hiyo pamoja na ukaguzi wa mara kwa mara unaofanyika katika taasisi na maeneo mbalimbali yanayotumia vifaa vya mionzi ili kuhakikisha usalama unaendelea kuzingatiwa wakati wote.

Aidha, wananchi walipata uelewa kuhusu matumizi ya teknolojia ya nyuklia katika sekta mbalimbali zikiwemo afya, kilimo, mifugo, viwanda, migodi, maji na utafiti wa kisayansi. Elimu hiyo ilibainisha mchango mkubwa wa teknolojia hiyo katika kuboresha huduma za uchunguzi na matibabu ya magonjwa, kuongeza uzalishaji katika sekta za uzalishaji na kusaidia matumizi endelevu ya rasilimali za taifa.

Vilevile, TAEC ilitoa ufafanuzi kuhusu nafasi ya teknolojia ya nyuklia katika uzalishaji wa nishati ya umeme, ikieleza namna teknolojia hiyo inavyoweza kuchangia upatikanaji wa nishati ya uhakika kwa ajili ya kuendeleza shughuli za viwanda, biashara na ukuaji wa uchumi wa taifa.

Katika sekta ya afya, wananchi walielimishwa kuhusu matumizi ya mionzi katika uchunguzi na matibabu ya magonjwa mbalimbali, huku katika sekta ya chakula wakipata maelezo kuhusu matumizi ya teknolojia ya mionzi katika uhifadhi wa mazao na bidhaa za chakula kwa kuzuia uharibifu unaosababishwa na wadudu na vimelea, hivyo kuongeza muda wa matumizi na kupunguza upotevu wa mazao baada ya kuvunwa.

Mbali na kupata elimu, washiriki wa maonesho hayo walipata fursa ya kuuliza maswali na kufanya majadiliano ya moja kwa moja na wataalamu wa TAEC kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu usalama wa mionzi, hatua za tahadhari zinazopaswa kuzingatiwa pamoja na mchango wa Tume katika kulinda jamii dhidi ya madhara yanayoweza kusababishwa na matumizi yasiyo salama ya mionzi.

TAEC imeeleza kuwa ushiriki wake katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma umeendelea kuwa jukwaa muhimu la kuwafikia wananchi, kutoa taarifa sahihi kuhusu huduma zake na kuongeza uelewa wa umma kuhusu matumizi salama ya teknolojia ya nyuklia kwa maendeleo endelevu ya taifa.

Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yaliyohitimishwa leo yameendelea kutoa fursa kwa taasisi za umma kuwasilisha huduma zao kwa wananchi, kuimarisha uwajibikaji, kujenga imani ya umma na kuongeza uelewa wa jamii kuhusu mchango wa taasisi hizo katika maendeleo ya Tanzania.











 

Dodoma

Katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha, Dkt. Toba Nguvila, amepongeza matumizi ya mfumo wa kisasa wa Supervisory Control and Data Acquisition (SCADA) unaotumiwa na Wakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (PBPA), akisema umeongeza uwazi na ufanisi katika usimamizi wa mafuta nchini.

Dkt. Nguvila alitoa pongezi hizo Juni 23, 2026, alipotembelea banda la PBPA katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali jijini Dodoma na kupata maelezo kuhusu namna mfumo huo unavyofanya kazi.

Alisema matumizi ya teknolojia za kisasa katika sekta ya mafuta yanaisaidia Serikali kufuatilia kwa karibu mwenendo wa mafuta yanayoingia nchini na kuhifadhiwa katika maghala mbalimbali, hivyo kudhibiti upotevu na kuongeza uwajibikaji.

“Ni jambo la kutia moyo kuona taasisi za umma zinatumia teknolojia za kisasa katika kuboresha usimamizi wa rasilimali za taifa. Mfumo huu unasaidia kuongeza uwazi na kuhakikisha mafuta yanayopokelewa yanafika katika maeneo yaliyokusudiwa,” alisema Dkt. Nguvila.

Akitoa maelezo kwa mgeni huyo, Mkaguzi wa Mafuta wa PBPA, Bw. Issa Khamis Mwitazy, alisema mfumo wa SCADA umechangia kwa kiasi kikubwa kudhibiti upotevu wa mafuta ambao kwa muda mrefu ulikuwa changamoto katika sekta hiyo.

Bw. Mwitazy alisema mfumo huo hulinganisha kiwango cha mafuta kilichopokelewa kutoka melini na kiwango kilichofika kwenye maghala, ambapo taarifa hutolewa mara moja endapo kutabainika tofauti yoyote ili hatua za haraka zichukuliwe.

Aidha, alisema mfumo huo unasoma na kufuatilia kwa wakati halisi ujazo wa mafuta kupitia mita za Serikali zilizopo katika bandari za Dar es Salaam, Tanga na Mtwara, pamoja na kusoma kiwango cha mafuta kilichopo katika maghala ya kampuni za mafuta.

Kwa mujibu wa PBPA, matumizi ya mfumo wa SCADA ni sehemu ya jitihada za Serikali za kuimarisha usimamizi wa mafuta nchini na kuhakikisha sekta hiyo inaendeshwa kwa uwazi, ufanisi na tija zaidi.

 

Wataalamu wa afya, watafiti, viongozi wa vijana na wadau mbalimbali wa maendeleo kutoka ndani na nje ya Afrika wamekutana jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kujadili namna ya kuimarisha huduma na sera za afya kwa vijana balehe barani Afrika.

Kwa mujibu wa taarifa kwa umma iliyotolewa na Mtandao wa ARISE kupitia Mkurugenzi Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Afrika ya Afya ya Umma, Dkt. Mary Mwanyika Sando, Juni 22, 2026, inaeleza kuwa Mkutano wa 2026 wa Afya ya Vijana Balehe Kusini mwa Jangwa la Sahara (CAH-SSA) pamoja na Mikutano ya Mwaka ya Mtandao wa Utafiti, Sayansi ya Utekelezaji na Elimu Afrika (ARISE), unafanyika kuanzia Juni 22 hadi 25, 2026 Jijini Dar es Salaam.


Mkutano huo unafanyika chini ya kaulimbiu “Kuonesha Mafanikio ya Afua Endelevu za Afya ya Vijana Balehe Zinazoongozwa na Jamii”, ukiwa na lengo la kuonesha matokeo ya tafiti na kujadili mbinu bora za kuboresha afya ya vijana.

Mgeni rasmi katika mkutano huo ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya Tanzania, Dkt. Seif Abdallah Shekalaghe, ambaye amezungumzia namna matokeo ya tafiti yanavyoweza kutumika kuboresha sera za afya, kuimarisha huduma kwa vijana na kuongeza ushiriki wa vijana katika ubunifu na utekelezaji wa afua zinazowahusu.

Mkutano huo umewakutanisha wadau mbalimbali wakiwemo Serikali, washirika wa maendeleo, viongozi wa vijana, watafiti, taasisi za utafiti na sekta binafsi kwa lengo la kujenga ushirikiano wa kuongeza matokeo chanya katika afya ya vijana barani Afrika.

Katika mkutano huo, vijana pia wamepewa nafasi kupitia Wawakilishi wa Bodi ya Ushauri ya Vijana Balehe na Vijana kwa ujumla (AYAB), akiwemo Mtanzania Bi. Mariam Surve na Bi. Mariam Yusuff kutoka Nigeria, ambao wanawakilisha sauti na mahitaji ya vijana katika uundaji na utekelezaji wa programu za afya.

Miongoni mwa maeneo yatakayojadiliwa ni matokeo ya miradi ya DASH na ARISE-NUTRINT inayolenga kuboresha afya ya vijana katika maeneo ya lishe, mazoezi, afya ya uzazi na afya ya akili. Miradi hiyo imefadhiliwa na Serikali ya Ujerumani pamoja na Umoja wa Ulaya.

Aidha, mkutano huo unalenga kuimarisha mipango ya Mtandao wa ARISE kwa kipindi cha mwaka 2026–2027 kwa kuweka mikakati itakayowezesha afua za afya kwa vijana kuwa endelevu kifedha na kutekelezwa kwa upana katika ngazi za jamii, kitaifa na kikanda.

Wakizungumza kuhusu umuhimu wa mkutano huo, viongozi wa ARISE wamesema jukwaa hilo ni muhimu katika kuunganisha tafiti, matokeo yake, sera na utekelezaji wa programu zinazolenga kuboresha maisha ya vijana barani Afrika.

Mtandao wa ARISE ni ushirikiano wa taasisi za Afrika na mabara mengine unaolenga kuimarisha uwezo wa utafiti wa afya ya umma na kuendeleza utekelezaji wa afua zenye msingi wa ushahidi, ukiwa na zaidi ya taasisi 22 kutoka nchi mbalimbali Kusini mwa Jangwa la Sahara.








 


Na Oscar Assenga, Muheza

WANANCHI 6,258 wa Kijiji cha Muungano, Wilaya ya Muheza, wanatarajiwa kunufaika na huduma bora za afya kufuatia kukamilika kwa ujenzi wa Zahanati ya Muungano, mradi ambao umepokelewa na kuridhiwa na Mwenge wa Uhuru 2026 baada ya kukaguliwa na kupokea taarifa ya utekelezaji wake.

Akizungumza wakati wa ukaguzi wa mradi huo, Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2026 alisema kukamilika kwa zahanati hiyo kutasaidia kusogeza huduma za matibabu karibu na wananchi na kupunguza changamoto ya kusafiri umbali mrefu kufuata huduma za afya.

Alisema Serikali tayari imepeleka vifaa tiba pamoja na watumishi wa afya watakaotoa huduma katika zahanati hiyo, hatua inayoonesha dhamira ya kuboresha upatikanaji wa huduma za afya, hususan katika maeneo ya vijijini.

“Mradi huu ni muhimu kwa wananchi wa Muungano na maeneo jirani kwa sababu unasaidia kuboresha upatikanaji wa huduma za afya na kuongeza ustawi wa jamii,” alisema.

Kiongozi huyo aliongeza kuwa mafanikio ya mradi huo yametokana na ushirikiano kati ya Serikali na wadau wa maendeleo, hususan Taasisi ya Islamic Help, iliyochangia ujenzi wa zahanati hiyo, huku Serikali ikigharamia vifaa tiba na watumishi wa afya.

Aliwashukuru wadau wa maendeleo kwa kuendelea kushirikiana na Serikali katika utekelezaji wa miradi ya kijamii, na kuwataka kuendeleza ushirikiano huo ili kusaidia kuboresha huduma muhimu kwa wananchi.

Aidha, aliwahimiza wananchi kuendelea kulinda amani na utulivu wa nchi, akisema kuwa mazingira hayo yanawezesha utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kuvutia wadau zaidi kushirikiana na Serikali.

Kwa upande wake, akitoa taarifa ya mradi huo, Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Wilaya ya Muheza, Dk. Fani Mussa, alisema ujenzi wa Zahanati ya Muungano ulianza Machi 2, 2025 na kukamilika kwa gharama ya Shilingi milioni 165.94.

Alieleza kuwa kati ya fedha hizo, Shilingi milioni 141.55 zilitumika kwa ujenzi, huku Shilingi milioni 24.39 zikitumika kununua vifaa tiba.

Kwa mujibu wa Dk. Mussa, zahanati hiyo itahudumia wakazi 6,258 wa Kijiji cha Muungano, wakiwemo wanaume 3,089 na wanawake 3,169, na inatarajiwa kwa kiasi kikubwa kuboresha upatikanaji wa huduma za afya katika eneo hilo.

Baada ya ukaguzi huo, Mwenge wa Uhuru 2026 ulieleza kuridhishwa na ubora wa utekelezaji wa mradi huo, ukibainisha kuwa ni hatua muhimu katika kusogeza huduma za afya karibu na wananchi na kuunga mkono jitihada za Serikali za kuimarisha sekta ya afya nchini.