Na: OWM (KAM) - Mwanza

Serikali imehimiza wananchi kujiunga katika na Hifadhi Skimu ili kujihakikishia usalama wa maisha yao ya sasa na baadaye ikiwemo kunufaika na mafao yanayotolewa na Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF).
Akizungumza katika hafla ya uhamasishaji wa kujiunga na hifadhi hiyo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Deus Sangu amewasihi wananchi kutumia fursa hiyo kujiunga kwa wingi na kuchangia kikamilifu ili wanufaike na mafao mbalimbali yakiwemo ya matibabu pamoja na mafao ya uzeeni.
Aidha, amesema kuwa Serikali kupitia Mfuko wa NSSF imeanzisha Skimu ya Taifa ya Hifadhi ya Jamii kwa wananchi waliojiajiri kwa ajili ya kuhudumia Wananchi waliojiajiri kwenye shughuli za kiuchumi.
Waziri Sangu amebainisha kuwa Hifadhi Skimu ni mpango wa uchangiaji wa hiari unaolenga kuwafikia wananchi waliojiajiri wakiwemo wavuvi, wafanyabiashara, machinga, bodaboda, wakulima, wachimbaji wadogo, wasanii pamoja na makundi mengine  yanayounda sehemu kubwa ya nguvu kazi ya Taifa.
Vilevile, amesema Serikali ya Awamu ya Sita itaendelea kuweka mazingira rafiki ya ajira na kujiajiri sambamba na kuimarisha mifumo ya hifadhi ya jamii ili kuhakikisha hakuna Mtanzania anayebaki nyuma katika kunufaika na huduma hizo muhimu.
“Hifadhi ya jamii ni haki ya msingi inayosaidia wananchi kuwa na maisha yenye heshima hasa wanapofikia umri wa uzee au wanapokumbana na changamoto zisizotarajiwa kama vile maradhi” amesema.
Awali akizungumza Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe. Said Mtanda amewahimiza wananchi wa Mkoa wa huo kuchangamkia fursa ya kujiunga na Hifadhi Skimu, akieleza kuwa ni hatua muhimu ya kuilinda familia dhidi ya majanga ya maisha pamoja na kujihakikishia kipato cha baadaye.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii Masha Mshomba amesema Hifadhi Skimu itawasaidia wananchi kuboresha maisha yao kwa kuondokana na utegemezi, hivyo kuwawezesha kujitegemea kiuchumi na kupata usalama wa maisha yao si tu kwa sasa bali pia wanapofikia umri wa uzee.
 
 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni akizungumza wakati akizindua Bodi ya Kituo Taifa cha Kuratibu Kaboni (NCMC), Machi 6, 2026 jijini Dar es Salaam.

Na; Mwandishi Wetu,Dar es Salaam.

Waziri wa nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni ametoa maagizo matano kwa Bodi ya Kituo Taifa cha Kuratibu Kaboni (NCMC) kilichopo Morogoro mara baada ya kuizindua bodi hiyo.

Waziri Masauni ametoa maagizo hayo Machi 6, 2026 wakati wa uzinduzi wa Bodi hiyo jijini Dar es Salaam akieleza imepaswa kuimarisha mifumo ya kitaifa ya Upimaji, Utoaji Taarifa na Uhakiki wa gesijoto (MRV) ili kuhakikisha kuwa taarifa za kaboni nchini zinakuwa sahihi, za kuaminika na zinazokubalika kimataifa.

Pia ameielekeza Bodi hiyo kuhakikisha Miradi yote ya kaboni inayotekelezwa nchini inasimamiwa kwa ufanisi, uwazi na kwa kuzingatia viwango vya kitaifa na kimataifa pamoja na maslahi mapana ya Taifa. 

Mhe. Masauni ameongeza kuwa bodi inapaswa kuweka Mazingira wezeshi yatakayovutia uwekezaji wa ndani wa kimataifa katika Sekta ya Kaboni huku ikihakikisha kuwa uwekezaji huo unalinda rasilimali za Taifa na kuleta manufaa ya kweli kwa wananchi, kuhakikisha kunakuwepo mfumo wa haki na uwazi wa mgawanyiko wa manufaa ili jamii zinazohifadhi rasilimali za asili zinufaike moja kwa moja na Miradi ya Kaboni inayotekelezwa katika maeneo yao.

“Kuimarisha ushiriki wa Tanzania katika mifumo ya kimataifa ya biashara ya Kaboni hususan chini ya Ibara ya 6 ya Mkataba wa Paris, ikiwemo mifumo ya soko la Kaboni ili kuongeza fursa za kiuchumi kwa Taifa letu.

Aidha, ameisisitiza Bodi hiyo kufanya kazi kwa bidii na kuhakikisha Kituo hicho kinaendeshwa kwa uwajibikaji, uadilifu na weledi wa hali ya juu ili kuhakikisha mifumo ya Usimamizi wa Sekta ya Kaboni inalinda kikamilifu maslahi ya Taifa.

"Ni matarajio ya Serikali kuona kituo hiki kinakuwa kitovu cha ubora katika maswala ya ufuatiliaji wa Kaboni, biadhara ya Kaboni na Tafiti za mabadiliko ya tabianchi katika ukanda wa Afrika. Haya ni matarajio makubwa kwa taifa letu na yanahitaji Usimamizi madhubuti wa taasisi, mifumo imara ya ufuatiliaji pamoja na ushirikiano wa wadau wote.” Amesema Mhe. Masauni.

Ameongeza kuwa matarajio ya Serikali yaliyoainishwa katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, na Mpango wa muda mrefu wa Utekelezaji wake, sekta ya Kaboni inauwezo wa kuchangia takribani Dola za kimarekani bilioni mbili kwa Mwaka katika uchumi wa Taifa.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi, Dkt. Albina Chuwa amesema ushirikiano ndio jambo la msingi katika kufikisha lengo na ndoto za watanzania, hivyo watajitahidi kutafuta fursa ili kupata matokeo mazuri.

“Ushirikiano wa kutosha ndio naomba kutoka kwa kila mmoja wetu kwani haya yote tunayoyazungumza tutakuwa tunafanya kazi nyepesi katika kuhakikisha kituo chetu cha Kaboni kinafanya vizuri,” amesema Dkt. Albina.

Amesema Uzinduzi wa Bodi unakuja katika kipindi muhimu ambacho sekta ya biashara ya kaboni inaendelea kukua kwa kasi duniani na hapa nchini, NCMC ina jukumu muhimu la kuhakikisha kuwa rasilimali za kaboni za nchi yetu zinasimamiwa kwa uwazi, weledi na kwa kuzingatia mifumo na viwango vinavyokubalika kimataifa.

Wajumbe wanaounda Bodi hiyo ni Bw. Khamis Hamza Khamis, Bi. Amne Sued Kagasheki, Bi. Farhat Mabrouk, Dkt. Ladislaus Kyaruzi, Bw. Rishad Bade pamoja na Dkt.Philipina Fenest Shayo.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni akizungumza wakati akizindua Bodi ya Kituo Taifa cha Kuratibu Kaboni (NCMC), Machi 6, 2026 jijini Dar es Salaam.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Mwenyekiti wa Bodi ya NCMC, Dkt. Albina Chuwa (kushoto kwake), Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt, Festo Dugange, Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Dkt. Richard Muyungi (kulia kwake) na Naibu Katibu Mkuu (Mazingira) Ofisi ya Makamu wa Rais, Balozi Baraka Luvanda, mara baada ya uzinduzi wa Bodi ya Kituo Taifa cha Kuratibu Kaboni (NCMC), Machi 6, 2026 jijini Dar es Salaam.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni akimpongeza Mwenyekiti wa Bodi ya Kituo Taifa cha Kuratibu Kaboni (NCMC, Dkt. Albina Chuwa mara baada ya uzinduzi wa Bodi hiyo, Machi 6, 2026 jijini Dar es Salaam

Naibu Waziri, Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Festo Dugange akizungumza wakati wa uzinduzi wa Bodi ya Kituo Taifa cha Kuratibu Kaboni (NCMC), Machi 6, 2026 jijini Dar es Salaam.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Wajumbe wa Bodi ya Kituo Taifa cha Kuratibu Kaboni (NCMC), mara baada ya uzinduzi wa Bodi hiyo, Machi 6, 2026 jijini Dar es Salaam.

PICHA NA OFISI YA MAKAMU WA RAIS

 " NINA IMANI KUBWA NA UTENDAJI KAZI WA OFISI YA MWANDISHI MKUU WA SHERIA".  MWANASHERIA MKUU 



Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Hamza S. Johari amewataka  Watumishi wa Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria kufanya kazi kwa Weledi na Ufanisi ili kufikia malengo ya Ofisi kwani ana Imani kubwa na utendaji kazi wa OFISI ya Mwandishi Mkuu wa Sheria.


Mhe. Johari amesema hayo alipofungua kikao cha kwanza cha Baraza la Wafanyakazi la Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria tarehe 6 Machi, 2026 jijini Dar es Salaam.


*"Niwaombe muendelee kutekeleza majukumu ya Ofisi hii kwa Weledi na Ufanisi ili kufikia malengo ya Ofisi na nina imani kubwa na utendaji kazi wa Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria”* amesema Mhe. Johari 

Aidha Mhe. Johari ameendelea kwa kuwataka watumishi wa  Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria kuzingatia kanuni na Sheria za Utumishi wa Umma ili kutoathiri utendaji kazi wa Serikali.


*"Utumishi wa Umma unaongozwa na Sheria pamoja na Kanuni, hivyo natoa rai kwa watumishi wote tuzingatie Miongozo ya Utumishi wa Umma ili tusiathiri utendaji kazi wa Serikali,"* ameongeza Mhe. Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Vilevile Mhe. Johari ameitaka Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria kuboresha matumizi ya mifumo ya TEHAMA ili kufanya kazi kwa ufanisi zaidi.


*"Naomba nisisitize matumizi ya mifumo ya TEHAMA ili kurahisisha utendaji kazi na kutoa kazi zenye ufanisi kwa matumizi ya Serikali na jamii kwa ujumla,"* ameeleza Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. Hamza Johari.

Awali, akimkaribisha Mgeni Rasmi, Mwandishi Mkuu wa Sheria, Bw. Onorius Njole, amesema Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria imewekeza nguvu kubwa kwenye mifumo ya TEHAMA ili kuendelea kuimarisha utendaji kazi.


*"Katika kuendelea kuimarisha  utekelezaji wa Uandishi wa Sheria tumeamua kuweka nguvu kubwa kwenye mifumo ya Tehama kwa kuanzisha e-drafting, e-translation na e-revision na kwa usaidizi wako Mwanasheria Mkuu wa Serikali tutaweza kufanikisha hili.* amesema.


Pia, Mwandishi Mkuu wa Sheria Bw. Njole amemshukuru Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kuendelea kuwa kiongozi bora na mwenye msaada mkubwa kwa Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria.



*"Kwa niaba ya menejimenti ya Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria na Wafanyakazi wote, tunamshukuru Sana Mhe. Johari kwa kuwa kiongozi bora kwa Ofisi yetu, na kutupa ushirikiano kila tunapohitaji”* Amesema.


Miongoni mwa Wageni waalikwa katika Baraza la Wafanyakazi wa Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria ni Mkurugenzi wa Mashtaka, Bw. Sylvester Mwakitalu. 


Baraza la kwanza la Wafanyakazi wa Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria, limefanyika tarehe 6 Machi, 2026 katika ukumbi wa Mikutano wa Julius Nyerere (JNICC) jijini, Dar es salaam.

 

Na Mwandishi Wetu

Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) imetangaza kufuta leseni ya rejareja ya bidhaa za mafuta ya petroli ya kampuni ya Iyan Energy Limited na kusitisha kwa muda wa miezi sita leseni ya kampuni ya Crescent Energy Tanzania Limited, baada ya kubaini ukiukwaji wa sheria na masharti ya leseni.

Kwa mujibu wa taarifa ya EWURA, uamuzi huo umefanyika kufuatia maamuzi yaliyotolewa na Bodi ya Wakurugenzi wakati wa vikao vyake vya hivi karibuni.

EWURA imesema leseni iliyofutwa ni Petroleum Retail Licence Na. PRL-2018-269, iliyokuwa ikimilikiwa na Iyan Energy Limited kwa ajili ya kuendesha biashara ya rejareja ya mafuta katika Kiwanja Na. 26 na 27, Barabara ya Pangani, Jiji la Tanga.

Wakati huohuo, Bodi imesitisha kwa muda wa miezi sita leseni ya rejareja ya bidhaa za mafuta ya petroli Namba PRL-2022-296 ya Crescent Energy Tanzania Limited, iliyotolewa kwa ajili ya kuendesha biashara ya rejareja katika Kiwanja Na. 5, Kitalu “N”, Eneo la Chamakweza, Wilaya ya Chalinze, Mkoa wa Pwani.

Taarifa hiyo imeeleza kuwa maamuzi hayo yamefanyika baada ya EWURA kujiridhisha kuwa kampuni hizo zilikuwa zikijihusisha na shughuli zinazofanana na biashara ya uuzaji wa bidhaa za mafuta kwa jumla, hali ambayo haikuruhusiwa chini ya leseni za rejareja walizokuwa nazo.

EWURA imeeleza kuwa hatua hizo zinakiuka Kifungu Na. 131 cha Sheria ya Petroli, Sura ya 392, pamoja na Kanuni ya 9 na 11 za Kanuni za Mafuta (Biashara ya Jumla, Uhifadhi, Rejareja na Matumizi Binafsi), Tangazo la Serikali Na. 150/2022.

Onyo kwa umma

Katika taarifa yake, EWURA imeutaarifu umma kuwa kujihusisha kwa namna yoyote na kampuni hizo katika biashara ya usambazaji wa bidhaa za mafuta ya petroli kutakuwa kinyume cha sheria, na kwamba hatua stahiki za kisheria zitachukuliwa dhidi ya watakaokiuka.

Mamlaka hiyo imeongeza kuwa itaendelea kusimamia sekta ya mafuta kwa kuhakikisha kunakuwa na mazingira ya ushindani wa haki na upatikanaji wa uhakika wa bidhaa za mafuta nchini, kwa kudumisha “uwanja ulio sawa” kwa wadau wote.

 

Na Mwandishi Wetu, Handeni

Wanawake katika Halmashauri ya Mji Handeni wametakiwa kutumia simu janja na teknolojia ya kidijitali kwa kuwa ni nyenzo muhimu ya kukuza biashara na kujikwamua kiuchumi kupitia fursa mbalimbali zinazopatikana mtandaoni.

 Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese ameyasema hayo wakati akizindua Jukwaa la Uwezeshaji Wanawake Kiuchumi katika kongamano la wanawake lililofanyika mjini Handeni.

Amesema matumizi sahihi ya simu janja yanaweza kuwasaidia wanawake kupanua masoko ya biashara zao kupitia mitandao ya kijamii pamoja na kupata taarifa muhimu za fursa za kiuchumi zinazotolewa na serikali.

Nyamwese amesema jukwaa hilo limekuja wakati muafaka kutokana na juhudi za serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan katika kuwawezesha kiuchumi wanawake na wasichana.

“Jukwaa hili litawawezesha kupata fursa na kujadiliana namna ya kujikwamua. Mtapata mbinu mbalimbali za kuongeza thamani ya biashara zenu na namna ya kuzifikia fursa zinazotolewa na serikali ikiwamo mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na halmashauri,” amesema.

Aidha, amewasisitiza wanawake kuwa wabunifu katika biashara zao na kutumia kikamilifu teknolojia pamoja na mikopo inayotolewa na halmashauri ili kujiongezea kipato.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Handeni, Maryam Ukwaju amesema halmashauri imeandaa mkakati wa kusaidia vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu kujiunga kwenye mfumo wa ununuzi wa umma wa NeST ili viweze kunufaika na fursa ya asilimia 30 ya zabuni zinazotolewa kwa makundi hayo.

Amesema kupitia mfumo huo vikundi vitapata nafasi ya kushiriki kikamilifu katika zabuni zinazotangazwa na halmashauri na hivyo kuongeza kipato na kukuza uchumi wao.

Akizungumza kuhusu kongamano hilo, Mkurugenzi huyo amesema katika kongamano hilo wanawake walipata elimu mbalimbali ikiwamo masuala ya fedha, msaada wa kisheria, umiliki wa ardhi pamoja na masuala ya ndoa ili kuwajengea uelewa na kuwasaidia kuwa chachu ya maendeleo ya Handeni.

Aliongeza kuwa elimu hiyo pia inalenga kuwawezesha wanawake kushiriki kikamilifu katika kufikia malengo ya maendeleo ya Taifa yaliyowekwa katika Dira ya Maendeleo ya mwaka 2050.

Akisoma taarifa ya uendeshaji wa shughuli za majukwaa ya uwezeshaji wananchi kiuchumi, Mratibu wa majukwaa hayo, Carin Umwambe amesema jukwaa hilo linalenga kuwaunganisha wanawake wajasiriamali na watoa huduma katika sekta za umma na binafsi ili waweze kupata fursa mbalimbali za kiuchumi na kibiashara.

Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) Mkoa wa Dodoma unashiriki katika Kliniki maalum ya kutatua kero na changamoto mbalimbali za wananchi iliyoandaliwa na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, inayofanyika tarehe 3 hadi 6 Machi, 2026 katika viwanja vya Nyerere Square jijini Dodoma.

Kupitia kliniki hiyo, TBA inakutana na wateja wake ambao ni wapangaji wa nyumba zake kwa lengo la kusikiliza na kutatua changamoto pamoja na kero mbalimbali zinazojitokeza katika maeneo wanayoishi.

Aidha, kliniki hiyo imekuwa fursa kwa taasisi mbalimbali za Serikali kutoa elimu kwa wananchi pamoja na kueleza mafanikio yaliyopatikana katika utekelezaji wa majukumu yao ndani ya siku 100 za Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan tangu kuingia madarakani.

Katika kliniki hiyo, TBA kama zilivyo taasisi nyingine za Serikali imeweka banda maalum kwa ajili ya kutoa elimu kwa wananchi kuhusu majukumu yake pamoja na kueleza miradi mbalimbali iliyotekelezwa na wakala huo katika kipindi hicho.

Akitembelea mabanda ya taasisi mbalimbali katika viwanja hivyo leo Machi 5, 2026, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule, ameipongeza TBA kwa kutekeleza miradi mikubwa ya Serikali katika mkoa wa Dodoma, ikiwemo ujenzi wa Mji wa Serikali Mtumba pamoja na mradi wa ujenzi wa nyumba 3,500 za makazi ya watumishi wa umma katika eneo la Nzuguni.

Kwa upande wao, wananchi waliotembelea banda la TBA wamepongeza utekelezaji wa mradi wa nyumba za makazi katika eneo la Nzuguni, wakisema umechangia kusogeza huduma za kijamii na biashara karibu na wananchi pamoja na kuimarisha hali ya ulinzi na usalama katika eneo hilo.

Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) kupitia Kanda ya Kaskazini, leo tarehe 5 Machi 2026 imetoa elimu kwa viongozi wa Wilaya ya Korogwe katika semina iliyofanyika katika ukumbi wa GMCC.

Akimkaribisha Mgeni Rasmi, Meneja wa EWURA Kanda ya Kaskazini, George Mhina, alisema lengo ni kuwajengea viongozi uelewa kuhusu majukumu ya EWURA na maeneo inayoyadhibiti ili kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.

Katika semina hiyo, washiriki walipatiwa elimu kuhusu umuhimu wa uvunaji wa maji ya mvua, matumizi ya nishati safi ya kupikia, leseni za mafundi umeme, ujenzi wa vituo vya mafuta vijijini pamoja na namna ya kutatua migogoro katika sekta za maji na nishati.

Akizungumza katika kikao hicho, Mkuu wa Wilaya ya Korogwe Mhe. William Mwakilema amewasisitiza viongozi hao kuwa mabalozi wa elimu waliyoipata kwa kuhakikisha wanaifikisha kwa wananchi ili kuongeza uelewa na matumizi sahihi ya huduma za maji na nishati.

 

Dar es salaam –
Mufti na Sheikh Mkuu wa Tanzania, Abubakar Zubeir, ametoa wito kwa Watanzania kujitokeza kwa wingi kutumia fursa ya huduma za ardhi zinazotolewa kupitia Samia Ardhi Kliniki, akisisitiza umuhimu wa wanawake kumiliki ardhi kama njia ya kujikomboa kiuchumi.
Mufti Zubeir alitoa kauli hiyo baada ya kufika katika Kliniki ya Ardhi inayofanyika katika Ofisi za Ardhi za Mkoa wa Dar es Salaam, ambapo alipata hati ya ardhi huku akishuhudia namna wananchi wanavyohudumiwa katika kliniki hiyo ambayo inaendelea nchi nzima.
Akizungumza mara baada ya kupata huduma hiyo, Mufti Zubeir alisema hatua ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kuandaa Samia Ardhi Kliniki yenye kulenga kuwapa kipaumbele wanawake ni jambo muhimu linalosaidia kuongeza usawa katika umiliki wa rasilimali muhimu kama ardhi.
Alisema wanawake wanapaswa kutumia kikamilifu fursa hiyo ili waweze kupata hati za ardhi na kujiimarisha kiuchumi.
“Wanawake wana haki ya kumiliki mali mbalimbali ikiwemo magari na mali nyingine, hivyo hakuna sababu ya kuwanyima nafasi ya kumiliki ardhi. Ni muhimu jamii, hususan wanaume, kuachana na mila kandamizi zinazowazuia wanawake kumiliki rasilimali,” alisema Mufti Zubeir.
Aidha, aliwataka wanaume kuwapa nafasi wanawake kumiliki ardhi ili kuongeza idadi ya wanawake wenye umiliki rasmi wa ardhi nchini, jambo ambalo litasaidia kuimarisha ustawi wa familia na jamii kwa ujumla.
Katika hatua nyingine, Mufti Zubeir alipongeza maandalizi mazuri yaliyofanywa na Ofisi ya Mkoa wa Dar es Salaam katika uendeshaji wa kliniki hiyo, kuanzia mapokezi hadi utoaji wa huduma kwa wananchi.
Alisema namna wateja wanavyohudumiwa kwa ufanisi ni jambo jema lenye manufaa kwa jamii na lina thawabu kubwa mbele za Mwenyezi Mungu, hususan katika kipindi hiki cha mwezi mtukufu wa Ramadhani.
Mufti Zubeir pia aliwaombea heri watumishi wanaotoa huduma katika kliniki hiyo ili waendelee kuwahudumia wananchi kwa uadilifu na bidii.
Samia Ardhi Kliniki zinaendelea kufanyika katika maeneo mbalimbali nchini kwa lengo la kurahisisha upatikanaji wa huduma za ardhi, hususan kwa wanawake, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kuelekea Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yanayoadhimishwa Machi 8 kila mwaka.
 
 
 

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule ameipongeza Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa kuendesha zoezi la Samia Ardhi Kliniki linalofanyika nchi nzima.

Mhe. Senyamule ametoa pongezi hizo leo Machi 5, 2026 alipotembelea kliniki hiyo inayoendelea katika viwanja vya Ofisi ya Kamishna wa Ardhi Msaidizi Mkoa wa Dodoma.

“Nimekaa sijawahi kuona ubunifu wa jambo hili, na nimeambiwa linafanyika nchi nzima ya Tanzania. Hiki ni kitu cha pekee sana,” amesema Senyamule.

Kwa mujibu wa Mkuu huyo wa mkoa wa Dodoma, awali aliposikia kuhusu kliniki hiyo alijiuliza kama kutapatikana wanawake wa kutosha kwenda kutatuliwa kero zao za ardhi, lakini hali imekuwa tofauti.

“Nilijiuliza kama wanawake watapatikana kwa wingi, lakini leo nimeshangaa kuona na kushuhudia kuwa sasa wanawake wengi wanamiliki ardhi,” amesema Senyamule.

Aidha, amesema kuwa kama jambo hilo lingefanyika miaka kumi au ishirini iliyopita, isingekuwa rahisi kupata wanawake wengi kwa sababu wengi hawakuwa na uelewa wa haki yao ya kumiliki ardhi.

“Kama ungelifanya jambo hili miaka kumi au ishirini iliyopita na kusema wanawake waje washughulikie kero zao za ardhi na kupata hati, usingewapata wengi kwa sababu wakati huo hatukuwa na uelewa kuwa sisi pia tunastahili kumiliki ardhi,” ameongeza.

Katika hatua nyingine, Mhe. Senyamule amewaasa wanawake kutunza vizuri hati zao za ardhi, akieleza kuwa ardhi ya Dodoma ina thamani kubwa inayoongezeka kila siku.

“Ukishapata hati yako, itunze vizuri kwa sababu ardhi ya Dodoma ina thamani kubwa na thamani yake inaendelea kuongezeka kila siku,” amesema.

Sambamba na hilo, Mhe. Senyamule pia amekabidhi hati miliki kwa baadhi ya wanawake waliofika katika kliniki hiyo iliyofanyika katika viwanja vya Ofisi ya Kamishna Msaidizi wa Ardhi Mkoa wa Dodoma.

Samia Ardhi Kliniki ilianza rasmi tarehe 2 Machi 2026 katika mikoa yote nchini na inatarajiwa kuhitimishwa tarehe 7 Machi 2026 yenye Kauli Mbiu, Mwanamke; Haki Yako, Miliki Ardhi sasa.

 


๐Ÿ“ŒUmegharimu bilioni 11 na kuingiza umeme gridi ya Taifa.

Katibu wa Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa, Kenan Kihongosi ameipongeza Wizara ya Nishati kwa utekelezaji wa mradi wa umeme jua wenye thamani ya shilingi bilioni 11 unaoingiza megawati tano (5) katika Gridi ya Taifa.

Kihongosi ametoa pongezi hizo mara baada ya kutembelea mradi huo uliopo katika Kijiji cha Kayenze, Jimbo la Ushetu wilayani Kahama, akiwa katika ziara yake ya kikazi mkoani Shinyanga.

“Naipongeza Wizara ya Nishati kwa mradi huu wenye tija ambao ni sehemu ya vielelezo vya utekelezaji wa miradi ya nishati safi kwa ajili ya wananchi. Kupitia mradi huu tunaendelea kuona dhamira ya Serikali ya kupeleka maendeleo katika maeneo mbalimbali nchini,” amesema Kihongosi

Aidha, amemshukuru na kumpongeza Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa maono yake yaliyowezesha kukamilika kwa miradi mbalimbali ya kimkakati ikiwemo mradi wa Julius Nyerere unaozalisha megawati 2,115 pamoja na mradi wa umeme jua wa Kishapu ambapo awamu ya kwanza imekamilika na kuanza kuzalisha megawati 50.

Kihongosi pia amempongeza Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba pamoja na viongozi wengine  kwa usimamizi madhubuti unaoifanya sekta ya nishati kuwa imara na yenye utulivu, huku akisisitiza kasi ya utekelezaji wa miradi kuendelea.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Nishati na Mbunge wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Salome Makamba amesema umeme unaozalishwa katika mradi huo unaingizwa kwenye Gridi ya Taifa kupitia njia ya msongo wa kilovolti 33 (33kV). Ameongeza kuwa mradi huo ulikamilika mwezi Mei 2025 na kuanza kufanya kazi mara moja.

Ameeleza pia kuwa pamoja na kusaidia kuimarisha hali ya upatikanaji wa umeme, mradi huo umechangia maendeleo ya jamii kwa kujenga jengo la zahanati katika Kijiji cha Kayenze kwa gharama ya shilingi milioni 130.

Kuhusu usambazaji wa umeme katika Jimbo la Ushetu, Mhe. Salome amesema Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ametoa fedha kwa ajili ya kusambaza umeme katika vitongoji 136 jimboni humo, huku vitongoji takriban 100 vilivyosalia vitakuwa vimefikiwa na huduma hiyo ifikapo mwaka 2030.