Na Munir Shemweta, KITETO
Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo ameahidi kupelewa kwa Mwenyekiti wa Baraza la Ardhi na Nyumba la wilaya ya Kiteto mkoani Manyara.
Dkt Akwilapo alitoa ahadi hiyo leo tarehe 26 Februari 2026 kufuatia kuwasilishwa kwa malalamiko na mwananchi mmoja aliyemueleza Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt Mwigulu Nchemba aliyeko katika ziara mkoani Manyara kuwa, katika wilaya ya kiteto wananchi wamekuwa wakipata shida ya kushughulikiwa mashauri yao ya ardhi kupitia Baraza la Ardhi kutokana na kukosekana kwa mwenyekiti wa Baraza.
Kwa sasa Baraza la Ardhi na Nyumba la Wilaya ya Kiteto linahudumiwa na Mwenyekiti wa Baraza la Ardhi na Nyumba kutoka Dodoma jambo lililoelezwa kuwa limechangia mashauri kuchukua muda mrefu.
Dkt Akwilapo amesema, suala la Mwenyekiti wa Baraza la Ardhi na Nyumba Wilaya katika wilaya ya Kiteto tayari limeshamfikia na analifanyia kazi na muda wowote mwenyeikiti atapatikana ndani ya muda mfupi.
‘’Nimemuagiza katibu mkuu aliyefanyie kazi na muda wowote tutapata mwenyekiti mahsusi kwa ajili ya eneo hili’’. Amesema Dkt Akwilapo
Akigeukia suala la migogoro ya ardhi katika wilaya ya Kiteto, Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi amesema, migogoro mingi katika wilaya ya Kiteto imesababishwa na ukosefu wa mipango ya matumizi ya ardhi.
Kwa mujibu wa Dkt Akwilapo, wilaya ya Kiteto ina jumla ya vijiji 63 na kati ya hivyo vijiji 33 ndivyo vilivyofanyiwa mpango wa matumizi ya ardhi huku vijiji 22 mpango wake ukiwa umeisha muda wake jambo alilolieleza kuwa, sasa jumla ya vijiji 52 vinahitaji kufanyiwa mpango wa matumizi ya ardhi.
Amesema, Wizara yake inalifanyia kazi suala hilo na katika mpango wa Bajeti ijayo ya 2026/2026 wameomba fedha na itakapofanikiwa Wizara yake itatekeleza mpango huo kwa kushirikiana na Jumuiya ya Hifadhi ya Wanyamapori (WMA).
📌Bilioni 7 kuwezesha maeneo 165 ya miji kupata huduma ya umeme Morogoro
Mkuu wa mkoa wa Morogoro Mhe. Adam Malima ameipongeza Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kwa utekekezaji wa miradi ya umeme maeneo ya Vijijini na Vitongoji hali iliyopelekea kuchochea uchumi wa wananchi na Taifa kwa ujumla.
RC Malima ametoa pongezi hizo leo Februari 26, 2026 mkoani humo wakati akizungumza na Bodi ya Nishati Vijijini (REB) pamona na Menejimenti ya Wakala wa Nishati Vijijini (REA) ilipomtembelea ofisini kwake kueleza utekelezaji wa miradi ya umeme vijijini inayoendelea na iliyokamilika mkoani humo.
"Nimeifahamu REA kwa mingi toka ilipoanzishwa rasmi. Hapa ilipofika leo hii lazima tujivunie sisi kama Watanzania kwa kuwa imeweza kufikisha umeme vijiji vyote na sasa utekekezaji unaendelea kwenye vitongoji vyote nchini," Amesema RC Malima.
Halikadhalika RC Malima ameipongeza Bodi ya REA na Menejimenti kwa kazi kubwa iliyofanyika kwa kusimamia miradi mbalimbali ya umeme katika mkoa huo ili Watanzania waweze kunufaika na nishati hiyo muhimu.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), Mhe. Balozi Meja Jenerali Mstaafu Jacob Kingu ameeleza kuwa REA itaendelea kutekekeza miradi ya umeme vijijini wa weledi huku ikiwasimamia wakandarasi wa miradi hiyo ili waweze kuikamilisha miradi hiyo kwa wakati.
"Sisi kama Bodi tunauhakika miradi inayoendelea tutaikamilisha kwa wakati kwa kuwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan tayari imetoa fedha nyingi ili kuwezesha na kukamilisha miradi hiyo, " Ameongeza Mhe. Balozi Kingu.
Naye, Mkurugenzi Mkuu wa REA Mha. Hassan Saidy ameeleza kuwa kwa mkoa huo Wakala ipo mbioni kuongeza miradi ya ziada katika maeneo ya miji ambayo bado hayajafikiwa na huduma ya umeme ambapo takribani maeneo 165 yatapatiwa huduma hiyo na wateja wa awali 1,750 watapatiwa huduma ya umeme ambapo Serikali imetoa takribani shilingi bilioni 7 kwa mkoa wa Morogoro kutekeleza miradi hiyo.
Mbunge wa Jimbo la Kisarawe mkoani Pwani, Selemani Jafo, ameonesha kuridhishwa na kasi ya utekelezaji wa mradi wa maji katika Kijiji cha Nyani, Kata ya Mafizi, akieleza kuwa hatua iliyofikiwa inaleta matumaini mapya kwa wananchi.
Mradi huo unaotekelezwa na kampuni ya BROADWAYS ENGINEERING CO LTD una thamani ya shilingi milioni 402.8 na hadi sasa umefikia asilimia 70 ya utekelezaji, jambo linaloashiria kuwa upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama kwa wakazi wa eneo hilo si wa muda mrefu tena.
Kwa mujibu wa taarifa ya utekelezaji, mradi unahusisha ujenzi wa mnara wa tanki la maji lenye urefu wa mita 12 na uwezo wa kuhifadhi lita 50,000, pamoja na ujenzi wa vituo vitano vya kuchotea maji na ulazaji wa mtandao wa mabomba wenye urefu wa kilometa 16.167.
Akizungumza wakati wa ukaguzi wa mradi huo, Dkt. Jafo alimpongeza mkandarasi kwa kufanya kazi kwa kasi na weledi mkubwa, akibainisha kuwa kampuni hiyo imeendelea na kazi hata kabla ya kupokea malipo yoyote, jambo alilolitaja kuwa ni uzalendo na kujitolea kwa maendeleo ya wananchi.
Kutokana na kasi hiyo, Jafo ameiiomba Wizara ya Maji kulipa kiasi cha shilingi milioni 279.1 kwa kazi zilizokamilika ili kumwezesha mkandarasi huyo kuendelea na hatua zilizobaki na kuhakikisha mradi unakamilika kwa wakati.
Mbali na mkandarasi, mbunge huyo pia amempongeza Meneja wa RUWASA Wilaya ya Kisarawe, Mhandisi Evangelista Kahwili, kwa usimamizi makini wa miradi ya maji ndani ya jimbo hilo, akisema nidhamu na ufuatiliaji wa karibu umechangia mafanikio yanayoonekana.
Wananchi wa Nyani na maeneo ya jirani wanatarajia kunufaika na mradi huo mara utakapokamilika, huku wakieleza kuwa utapunguza adha ya kutembea umbali mrefu kutafuta maji na kuboresha afya pamoja na shughuli za kiuchumi katika eneo hilo.

Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratous Ndejembi, ameitaka Mamlaka ya Udhibiti Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA) kuimarisha mipango yake katika ukusanyaji wa data sahihi, tathmini ya vitalu vya utafiti, na maandalizi ya Watanzania kushiriki kikamilifu katika miradi mikubwa ya kimkakati, ikiwemo mradi wa kuchakata gesi asilia kuwa kimiminika (LNG).
Mhe. Ndejembi ameyasema hayo wakati wa Kikao cha Tano cha Mkutano wa Pili wa Baraza la Wafanyakazi la PURA kilichofanyika mkoani Morogoro leo Februari 26, 2026.
Amesisitiza kwamba sekta ya nishati ina nafasi ya kipekee katika kufanikisha malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, hivyo PURA inatakiwa kuhakikisha mipango yake inaendana na maono hayo.
“Sekta ya Nishati imetambuliwa kama moja ya vichocheo muhimu vya uchumi wa taifa. Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Nishati zina wajibu mkubwa kuhakikisha upatikanaji endelevu, salama na wa uhakika wa rasilimali za mafuta na gesi asilia,” amesema Mhe. Ndejembi.
Aidha, Mhe. Ndejembi amewataka PURA kuongeza juhudi katika ukusanyaji na usimamizi wa data za kijiolojia na kufanya tafiti za awali, hasa ikizingatiwa kwamba maeneo makubwa ya nchi bado hayajafanyiwa utafiti wa kina.
“Takwimu sahihi ni msingi wa kuvutia uwekezaji na kuongeza ugunduzi wa rasilimali. Hatuwezi kuendeleza sekta bila taarifa za kutosha na tafiti madhubuti,” amesisitiza.
Waziri huyo pia ameagiza PURA kufanya tathmini ya kina katika vitalu vilivyopo, hususan katika ukanda wa Tanga, Ruvu, na maeneo mengine, ili kubaini iwapo wamiliki wa vitalu wanafanya shughuli za utafutaji kama inavyotakiwa.
Ameongeza kuwa si vyema kwa vitalu kukaa mikononi mwa wawekezaji wasioendeleza shughuli za utafutaji, na mamlaka za udhibiti zinapaswa kuchukua hatua pale inapobainika hakuna maendeleo yanayofanyika kwa manufaa ya Taifa.
Akizungumzia mradi wa LNG, Mhe. Ndejembi amewataka PURA kuanza mapema kuandaa mkakati wa kujenga uwezo wa kitaasisi katika kusimamia mradi huo.
Sambamba na hilo, amewahimiza kuandaa Watanzania kushiriki kikamilifu katika mnyororo wa thamani wa LNG, badala ya kusubiri utekelezaji wa mradi kuanza.
Awali katika kikao hicho, Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi Asilia, Dkt. James Mataragio, amewataka PURA kusimamia majukumu yake ya msingi kama yanavyoainishwa katika malengo ya kuanzishwa kwa taasisi hiyo.





.jpg)
.jpg)
.jpg)
.jpg)
.jpg)































