Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Tanga(TangaUWASA) imeingia makubaliano maalum na taasisi ya ROTARY inayofanya kazi kwa kushirikiana na Mamlaka za Maji Nchini Uholanzi (VEi) ya kutekeleza mradi wa kuwezesha huduma za kijamii mashuleni kupitia ujenzi wa vyoo (SCHOOL WaSH) kwa shule za msingi katika Jiji la Tanga.

Akizungumza kwa niaba ya uwakilishi wa ROTARY Bi.Emma Lesterhuis ameainisha kuwa mradi huo utatekelezwa na TangaUWASA kwa kushirikiana na Halmashauri ya Jiji la Tanga na utajikita zaidi katika ujenzi wa vyoo kwa baadhi ya shule zenye idadi kubwa ya wanafunzi na uhaba wa matundu ya vyoo.

Nae kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa TangaUWASA, Mha. Geofrey Hilly amewashukuru ROTARY kwa kutambulisha mradi huo ambao unaenda kuwezesha jamii hususani wanafunzi kupata huduma muhimu na kuahidi kutoa ushirikiano wa kutosha wakati wote wa utekelezaji wa mradi na usimamizi wake.



Tanga unakuwa Mkoa wa tatu nchini kunufaika na mradi wa "SCHOOL WaSH" ukiungana na Mikoa ya Arusha na Mwanza ambayo utekelezaji wake unaendelea.

Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala wa Maendeleo ya Usimamizi wa Elimu (ADEM), Dkt. Maulid J. Maulid, anashiriki warsha ya uthibitishaji iliyoandaliwa na Kituo cha Afrika cha Uongozi wa Shule (ACSL) jijini Nairobi, Kenya, kuanzia tarehe 10 hadi 13 Februari 2026.

 


Na OWM - TAMISEMI, Dodoma

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo, Mhe Cecilia Daniel Paresso amesisitiza ushirikishwaji wa wananchi wakati wa utungaji na uhuishaji wa Sheria Ndogo za Mamlaka za Serikali za Mitaa, ili kuwajengea wananchi uelewa wa sheria hizo ambao utawezesha utekelezaji wake katika Mamlaka za Serikali za Mitaa.

Mhe. Paresso ametoa wito huo wa ushirikishwaji wa wananchi katika utungaji wa sheria ndogo leo  Februari 10, 2026 Jijini Dodoma, wakati akiongoza Kikao cha Mafunzo kwa kamati yake kuhusu Sheria Tatu za Mamlaka ya Serikali za Mitaa na uhusiano wake na sheria ndogo za Mamlaka hizo.

Mhe. Paresso na wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo wameishauri Ofisi ya Waziri Mkuu-TAMISEMI kufanya mapitio ya Sheria Ndogo ambazo zimepitwa na wakati ili kuzihuisha au kuziondoa sheria zitakazobainika kutotekelezeka.

Akimwakilisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu -TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe katika kikao hicho, Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Kaspar Mmuya amesema Ofisi ya Waziri Mkuu - TAMISEMI itawashirikisha wananchi wakati wa kutunga Sheria Ndogo za Mamlaka za Serikali za Mitaa kama kamati ilivyoelekeza, lengo likiwa ni kuwajengea uelewa wananchi na kuwezesha utekelezaji wake.

Aidha, Mhe. Mmuya ameiahidi kamati hiyo kuwa, Ofisi ya Waziri Mkuu -TAMISEMI itafanya mapitio ya Sheria Ndogo za Mamlaka za Mitaa ili kujiridhisha kama zinakwenda na wakati, na kuongeza kuwa itazihuisha na kuziondoa sheria ambazo zitakazobainika kupitwa na wakati.

Katika kikao kazi hicho cha mafunzo, wajumbe wa Kamati hiyo ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo wamepata fursa ya kupitia Sheria ya Serikali za Mitaa (Mamlaka za Miji) Sura ya 288, Sheria ya Serikali za Mitaa (Mamlaka za Wilaya) Sura ya 287, na Sheria ya Fedha za Serikali za Mitaa, Sura ya 290.












Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) leo, 10 Februari 2026, imetoa msaada wa mashuka 455 katika hospitali ya rufaa ya mkoa wa Iringa ili kuboresha huduma za kimatibabu hospitalini hapo, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa azimio la Baraza la Wafanyakazi wa Mamlaka hiyo, lililofanyika mkoani humo tarehe 9 hadi 10 Februari 2026.

Kaimu Katibu Tawala mkoa wa Iringa, Bi. Nuru Siyovelwa, alipokea msaada huo kwa niaba ya Katibu Tawala Mkoa, na kueleza kuwa, mashuka yamekuwa hayatoshelezi katika hospitali za mkoa huo, hivyo ameishukuru EWURA kwa kuguswa kwani yatasaidia kutoa huduma bora kwa wananchi.

Naye Mganga Mfawidhi wa hospitali hiyo, Dkt. Alfred Mwakalebela, alieleza kuwa mashuka hayo yatapunguza changamoto iliyokuwepo ya upungufu wa mashuka, kwani kwa siku, kila mgonjwa anatakiwa kutumia mashuka 6, ilhali kwa sasa huduma hiyo haitoshelezi kwa kila mgonjwa.

Akiwasilisha msaada huo kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, Meneja wa EWURA Kanda ya Kati, Mha. Hawa Lweno, alisema kuwa EWURA itaendelea na utaratibu wa kutoa mchango kwa jamii katika masuala mbalimbali ikiwemo afya.

Naibu Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Reuben Kwagilwa, amekagua maendeleo ya ujenzi wa jengo la Wagonjwa Mahututi (ICU) katika Hospitali ya Halmashauri ya Mji Handeni, mradi unaolenga kuondoa changamoto ya muda mrefu ya upatikanaji wa huduma hiyo kwa wananchi.

Mhe. Kwagilwa amefanya ukaguzi huo leo Februari 10, 2026, wakati wa ziara yake ya kikazi hospitalini hapo, ambapo alipata fursa ya kujionea hatua mbalimbali za utekelezaji wa mradi huo pamoja na maendeleo yaliyofikiwa hadi sasa.

Katika ziara hiyo, alipokea maelezo ya kitaalamu kutoka kwa wataalamu wa Halmashauri kuhusu maendeleo ya ujenzi, hali ya utekelezaji wa mradi pamoja na matarajio ya kukamilika kwake.

Ujenzi wa jengo hilo ni sehemu ya jitihada za Serikali za kuendelea kuboresha miundombinu ya sekta ya afya, kusogeza huduma muhimu karibu na wananchi pamoja na kuongeza uwezo wa hospitali kutoa huduma za dharura na kuokoa maisha ya wagonjwa.

Jengo hilo la kisasa linatarajiwa kuwa na mfumo wa hewa tiba (Oxygen) pamoja na vifaa maalum vya ufuatiliaji wa wagonjwa mahututi vitakavyowezesha uangalizi wa karibu wa hali zao.

 

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule, ameukaribisha Umoja wa Vyombo vya Habari vya Mitandao ya Kijamii Mkoa wa Dodoma (UMIKIDO) na kuutaka kuwa chachu ya kuimarisha mawasiliano kati ya Serikali na wananchi kupitia utoaji sahihi wa taarifa pamoja na ubunifu wa maudhui.

RC Senyamule ametoa kauli hiyo leo Februari 9, 2026, mara baada ya viongozi wa UMIKIDO kufika ofisini kwake kwa lengo la kujitambulisha na kuomba ushirikiano na Serikali ya Mkoa wa Dodoma.

“Hongereni kwa kuanzisha umoja huu. Nimefurahishwa sana kwani utarahisisha kazi na kuwa kiunganishi muhimu kati ya Serikali ya Mkoa na vyombo vya habari vya mitandaoni. Tulitamani kupata watu wanaozungumza lugha moja na Serikali, na tunaamini ninyi ni wazalendo,” amesema Mhe. Senyamule.

Ameeleza kuwa uwepo wa umoja huo utaisaidia Serikali kufikisha taarifa kwa wananchi kwa ufanisi zaidi, sambamba na kuongeza uelewa wa umma kuhusu shughuli na miradi mbalimbali inayotekelezwa na Serikali kwa ajili ya maendeleo ya Taifa.

“Ni muhimu Watanzania wakaendelea kufahamu kazi zinazofanywa na Serikali. Nina imani mtakuwa wabunifu katika kuandaa na kusambaza taarifa kwa njia zitakazowafikia wananchi kwa urahisi,” ameongeza.

Aidha, RC Senyamule amewataka wanachama wa UMIKIDO kuzingatia kutangaza miradi ya kimkakati na mipango ya maendeleo, ikiwemo uhifadhi wa mazingira, matumizi ya nishati safi ya kupikia, sekta ya utalii na michezo, pamoja na kuhamasisha matukio mbalimbali kuelekea mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2027.

Awali, viongozi wa UMIKIDO walieleza dhamira na malengo ya kuanzishwa kwa umoja huo, ikiwa ni pamoja na kuimarisha maadili ya uandishi wa habari za mitandaoni na kushirikiana kwa karibu na Serikali katika utoaji wa taarifa sahihi kwa umma. Pia waliomba ushirikiano kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa ili kutimiza malengo hayo.

Viongozi walioshiriki ziara hiyo ni (Mwenyekiti wa UMIKIDO Bw.Benny Majata,Katibu Emmanuel Charles, Zena Chitwanga (Mhasibu), Daniel Mkate (Afisa Mahusiano), Alex Sonna (Kamati ya Ufuatiliaji), Henry Masanja (Kamati ya Nidhamu) na Ronald Sonyo (Kamati ya Fedha na Mipango).



 


Na OWM – TAMISEMI, Dar es Salaam

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amekutana na Wakuu wa Mikoa wapya  wa Mkoa wa Kagera na Mtwara, Mhe. Kanali Yahya Ramadhani Kido na Mhe. Kanali Donald Wiliam Msengi ili kujipanga kiutendaji katika kutekeleza maelekezo ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan aliyoyatoa ili kuimarisha ufanisi na uwajibikaji katika kuwatumikia wananchi.

Prof. Shemdoe amekutana na Wakuu  hao leo Februari 09, 2026 katika Ofisi Ndogo ya TAMISEMI Jijini Dar es Salaam, mara baada ya viongozi hao kuapishwa na Mhe. Rais katika Ikulu ya Magogoni, ambapo Mhe. Rais amewataka viongozi hao kwenda kuimarisha uwajibikaji ili kukidhi matarajio ya wananchi hususani kwenye eneo la upatikanaji wa huduma za kijamii pamoja na ulinzi na usalama wa wananchi na mali zao.

Katika kuhakikisha viongozi hao wanatekeleza maelekezo ya Mhe. Rais kwa ufanisi, Prof. Shemdoe amewataka kuhakikisha, wanakwenda kuandikisha wakazi wote kwenye daftari la makazi, pamoja na  kusikikiliza na kutatua kero za wananchi kwa kushirikiana na viongozi na watumishi waliopo katika maeneo yao mapya ya Utawala.

Kikao kazi hicho cha Prof. Shemdoe na Wakuu wa hao ni hatua ya awali ya kujipanga na utekelezaji wa maelekezo ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan aliyoyatoa leo, wakati wa uapisho wa viongozi aliowateua Februari 06, 2026 kwa lengo la kuleta mabadiliko yatakayo imarisha ufanisi na uwajibikaji ili kuendana na kasi ya mahitaji ya wananchi.

 

Serikali yazindua Sera ya Taifa ya Kinga ya Jamii na ‘Hifadhi Scheme’ kwa Waliojiajiri

Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Mahusiano imezindua Sera ya Taifa ya Kinga ya Jamii pamoja na Mpango wa Hifadhi ya Jamii kwa Wananchi Waliojiajiri ‘Hifadhi Scheme’ hatua inayolenga kupanua wigo wa hifadhi ya jamii na kuongeza ushirikishwaji wa wananchi katika mifumo ya kinga ya kijamii.

Uzinduzi huo umefanyika Februari 9, 2026 katika mkutano wa wadau wa sekta ya kinga ya jamii uliofanyika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Arusha (AICC), ukiongozwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu kwa niaba ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Sangu alisema sera hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, inayolenga kuhakikisha wananchi wanapata huduma jumuishi za hifadhi ya jamii. Aliongeza kuwa tangu 2018, Serikali imefanya maboresho ikiwemo kuunganisha Mifuko ya Hifadhi ya Jamii na kubaki na NSSF na PSSSF ili kuongeza ufanisi wa huduma na ulipaji wa mafao.

Mhe. Sangu alisema maboresho hayo yameongeza idadi ya wanachama. NSSF imeongezeka kutoka wanachama 808,935 mwaka 2020 hadi zaidi ya wanachama 2,213,659 mwaka 2025, huku PSSSF ikiongezeka kutoka 697,677 hadi 899,948. Aidha, thamani ya uwekezaji wa Mifuko imeongezeka kutoka shilingi trilioni 9.36 hadi trilioni 20.14, na jumla ya thamani ya Mifuko kufikia trilioni 24.20.

Kuhusu mpango wa Hifadhi Scheme, alisema hadi Desemba 2025 zaidi ya wanachama 500,000 kutoka makundi mbalimbali yakiwemo wakulima, wafugaji, wavuvi na wajasiriamali wamejiunga, huku lengo likiwa kufikia wanachama milioni 5.5 ifikapo Juni 2031.

Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Mary Maganga, alisema Serikali imeipa NSSF jukumu la kupanua wigo wa hifadhi ya jamii kwa wananchi waliojiajiri ili kuhakikisha sera mpya inaleta matokeo yanayotarajiwa.

Awali, Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, Bw. Masha Mshomba, alisema Mfuko unaendelea kuboresha utoaji wa huduma, kuongeza uandikishaji wa wanachama wapya, na kupanua wigo wa uwekezaji ndani na nje ya nchi, ikiwemo nchi za SADC na Afrika Mashariki.

Bw. Mshomba alisema Mfuko umepata mafanikio makubwa katika Serikali ya awamu ya sita ambapo thamani ya NSSF imeongezeka kutoka trilioni 4.8 mwaka 2021 hadi trilioni 10.4 Desemba 2025, na kuwa imepata ziada kwa miaka minne mfululizo kuanzia 2021 hadi mwaka wa fedha 2024/25, ikivuka lengo la ziada ya shilingi trilioni moja.

Akizungumzia ukusanyaji wa michango, Bw. Mshomba alisema Mfuko umeendelea kuvuka malengo, ambapo mwaka wa fedha 2023/24 ulifikia zaidi ya shilingi trilioni mbili, huku mwaka 2024/25 makusanyo yakizidi trilioni 2.4 na kwamba katika kipindi cha miaka mitano mfululizo kuanzia 2020 hadi 2025, NSSF imefanikiwa kuvuka lengo la kukusanya angalau shilingi trilioni moja kwa mwaka. 

Bw. Mshomba aliongeza kuwa mafanikio hayo yamechangiwa na juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan. NSSF ina zaidi ya wanachama milioni 2.3 na imejikita kuboresha huduma kupitia TEHAMA na mpango wa miaka mitano unaolenga kufanikisha malengo ya Dira ya Taifa 2050 na Ilani ya Uchaguzi ya CCM.