NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

Baraza la Famasi limeanzisha mkakati wa kuimarisha ushirikiano na wahariri na waandishi wa habari nchini kwa kuwajengea uelewa kuhusu majukumu yake, hatua inayolenga kuhakikisha wananchi wanapata taarifa sahihi kuhusu huduma za dawa na usimamizi wa taaluma ya famasi ili kulinda afya ya jamii.
Wananchi, wanafunzi, wataalamu, wawekezaji na wadau mbalimbali wa maendeleo wanatarajiwa kukutana jijini Mbeya Julai 3, 2026, katika mhadhara maalum wa hadhara utakaolenga kujadili nafasi ya ubia kati ya sekta ya umma na sekta binafsi (PPP) katika kufanikisha utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

 


Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi, amesisitiza umuhimu wa malezi na makuzi bora kwa watoto, akieleza kuwa ndiyo msingi wa kujenga kizazi chenye maadili, afya njema, elimu na uwezo wa kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya jamii na Taifa.

Akizungumza katika nyakati tofauti tarehe 1Julai, 2026 mkoani Mtwara, Naibu Waziri Mahundi amesema malezi ya mtoto ni jukumu la wazazi wote wawili, hivyo akawataka akina baba na akina mama kushirikiana kwa karibu katika kuwalea watoto wao badala ya kumwachia mzazi mmoja jukumu hilo.

"Malezi ya mtoto si jukumu la mama pekee, Baba na mama wanapaswa kushirikiana kwa upendo, uwajibikaji na mshikamano ili kuwajengea watoto msingi imara wa maisha kwa kuwa watoto wa leo ndiyo viongozi na nguvu kazi ya kesho, hivyo wanahitaji kulelewa katika mazingira salama na yenye maadili mema," amesema Naibu Waziri Mahundi.

Aidha, Naibu Waziri Mahundi amesema Serikali inaendelea kuweka mazingira wezeshi yanayowainua wananchi kiuchumi kupitia fursa mbalimbali za uwezeshaji, hivyo amewahimiza wajasiriamali kutumia kikamilifu mikopo inayotolewa kupitia mabenki na taasisi za kifedha ili kukuza biashara zao, kuongeza kipato na kuboresha ustawi wa familia.

"Mikopo inayotolewa na Serikali ni fursa ya kujiletea maendeleo nawahimiza wajasiriamali kuitumia kwa malengo yaliyokusudiwa ili biashara zikue, kipato kiongezeke na hatimaye familia ziwe na uwezo wa kuwapatia watoto huduma bora za elimu, afya na lishe." amesema Naibu Waziri Mahundi.

Katika ziara hiyo, Naibu Waziri Mahundi amempongeza Mbunge wa Jimbo la Mtwara Mjini na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Maendeleo ya Vijana, Joel Nanauka, kwa kuanzisha kituo cha kulelea watoto katika Soko la Chuno, akieleza kuwa kituo hicho ni mfano wa ubunifu unaowasaidia wazazi, hususan wajasiriamali, kutekeleza shughuli zao za kiuchumi huku watoto wao wakipata huduma ya uangalizi katika mazingira salama.

Naibu Waziri Mahundi amesema uwepo wa kituo hicho umeleta nafuu kwa wazazi wanaofanya shughuli za biashara sokoni hapo, huku ukiwa sehemu ya jitihada za kuhakikisha watoto wanapata malezi na ulinzi stahiki wakati wazazi wao wakitafuta kipato cha kuendesha maisha ya familia.

Kwa upande wake, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Maendeleo ya Vijana na Mbunge wa Jimbo la Mtwara Mjini, Joel Nanauka, amesema elimu hiyo itaongeza uelewa wa jamii na kuwahamasisha wananchi kushiriki kikamilifu katika kujenga familia imara na Taifa lenye maendeleo endelevu.



Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, leo Jumatano, Julai 1, 2026, amekagua maendeleo ya ujenzi wa Jengo la Utawala la Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti, lililopo mjini Mugumu, mkoani Mara, ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kikazi ya siku tano mkoani humo.

Akiwasilisha taarifa ya ujenzi huo, Msanifu Majengo wa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) Mkoa wa Mara, Bw. Nicholas Jeje, alisema mradi huo unagharimu shilingi bilioni 4.5 zinazotolewa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Alisema ujenzi ulianza Aprili 10, 2025 na unatarajiwa kukamilika Aprili 9, 2028, huku utekelezaji wake ukiwa umefikia asilimia 42.

Alieleza kuwa jengo hilo litakuwa na ofisi 62, zikiwemo ofisi za Mkurugenzi wa Halmashauri na Mwenyekiti wa Halmashauri, pamoja na kumbi mbili za mikutano zenye uwezo wa kuchukua watu 50 na 110 mtawalia, hatua inayolenga kuboresha mazingira ya utoaji wa huduma kwa wananchi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Mara, Kanali Evans Mtambi, alimkaribisha Waziri Mkuu mkoani humo na kusema ziara hiyo itamwezesha kutembelea wilaya zote sita, halmashauri zote tisa na majimbo yote 10 ya uchaguzi yaliyopo mkoani Mara, ambapo pamoja na mambo mengine atakagua miradi ya maendeleo na kuzungumza na wananchi.








 

 

 Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Ndugu Asha-Rose Migiro, amefanya mazungumzo na Mheshimiwa Christine Grau, Balozi wa Umoja wa Ulaya nchini Tanzania, katika Ofisi ya Katibu Mkuu wa CCM, Lumumba, Dar es Salaam.

Mazungumzo hayo yamefanyika jana Juni 30,2026, ikiwa ni sehemu ya ziara ya kumuaga Balozi Grau anayehitimisha kipindi chake cha uwakilishi nchini Tanzania. Viongozi hao walitathmini ushirikiano wa muda mrefu kati ya Tanzania na Umoja wa Ulaya na kujadili namna ya kuuendeleza kwa manufaa ya pande zote mbili.

Katika mazungumzo hayo, viongozi hao walibadilishana mawazo kuhusu umuhimu wa kuimarisha misingi ya utawala bora, amani, utulivu na mshikamano wa kitaifa kama nguzo ya maendeleo endelevu ya Taifa. Katika muktadha huo, CCM ilisisitiza dhamira yake ya kuendelea kujenga Taifa linaloongozwa kwa misingi ya haki, uwajibikaji na utulivu wa kisiasa.

Pia, ilitambua changamoto zilizojitokeza nchini katika kipindi cha Uchaguzi Mkuu uliopita na umuhimu wa hatua ambazo Serikali inaendelea kuzichukua katika kuimarisha imani ya wananchi, ikiwemo kuundwa kwa Tume ya Uchunguzi, Tume ya Upelelezi wa Jinai na hatua nyingine za kisheria zinazolenga kuhakikisha ukweli, uwajibikaji na haki vinaendelea kutawala katika kulinda amani na mshikamano wa Taifa.

Aidha, ilielezwa kuwa ajenda ya kuendelea kuimarisha demokrasia nchini, ikiwemo mchakato wa Katiba Mpya ambao umeainishwa katika Ilani ya CCM ya Uchaguzi ya mwaka 2025–2030, inabaki kuwa sehemu muhimu ya maono ya muda mrefu ya kuimarisha utawala bora na mshikamano wa Taifa.

Viongozi hao pia walitambua nafasi ya vijana katika mustakabali wa maendeleo ya Tanzania na umuhimu wa kuhakikisha kizazi hicho kinaendelea kuwa sehemu ya safari ya Taifa kuelekea utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 na ujenzi wa uchumi wenye ushindani na maendeleo jumuishi.

CCM inathamini ushirikiano wake na Umoja wa Ulaya na inaamini kuwa ushirikiano huo utaendelea kuimarika kwa kuzingatia misingi ya kuheshimiana, maslahi ya pamoja na dhamira ya pamoja ya kuendeleza maendeleo endelevu ya Tanzania.







 

 


HALMASHAURI za Wilaya, Miji na Jiji mkoani Tanga, zimeagizwa kuzuia vyanzo vinavyosababisha hoja zinazoibuliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG). 

Agizo hilo limetoa leo Juni 30, 2026 na Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe. Balozi Dkt Batilda Burian, alipozungumza kwenye vikao maalum vya kujadili hoja za CAG katika Baraza la Madiwani wa Halmashauri za Lushoto na Bumbuli.

Amesema, taarifa za CAG kwa kipindi cha miaka mitano iliyopita, inaonesha halmashauri hizo zimefanikiwa kupata hati inayoridhisha, ikiwa ni Ishara ya ufanisi, weledi na kujituma kwa watumishi na watendaji.

Amesema, hali hiyo inapaswa kuendelezwa ili kufikia malengo msingi ya Serikali katika kutoa huduma bora kwa wananchi.


Hata hivyo, Mhe. Balozi Dkt Batilda amesema, pamoja na mafanikio hayo, halmashauri hizo zinatakiwa kudhibiti vitendo vinavyosababisha hoja za ukaguzi.

Awali, taarifa ya Mkaguzi Mkuu wa Nje, Mkoa wa Tanga, Hamu Mwakasola, ilieleza kuwa kutolewa hati inayoridhisha haimaanishi kuwepo mifumo mizuri ya udhibiti wa ndani, bali kutokuwepo dosari kubwa wakati wa ukaguzi.

“Inamaanisha hapakuwa dosari kubwa zilizobainika wakati wa ukaguzi ambazo zingemzua Mkaguzi kutoa maoni, au kumlazimu kutoa hati yenye mashaka au hati mbaya,” amesema

Naye Katibu Tawala Mkoa (RAS) wa Tanga, Rashid Mchatta, pamoja na mambo mengine, amewahimiza watumishi na umma, kuendeleza mahusiano mema ili kuongeza ufanisi na tija mahali pa kazi.

Amesema, viongozi, watendaji na watumishi katika Mamlaka za Serikali za Mitaa wanapaswa kutambua ‘uzito’ wa hadhi ya Ofisi ya CAG katika ukaguzi wa hesabu uliopo katika ngazi za kimataifa.

Mchatta amesema utambuzi wa ubora huo utachangia kuboresha utendaji kazi na kupunguza kwa kiasi kikubwa hoja za ukaguzi, hali itakayoifanya CAG kutekeleza vema wajibu wake wa ushauri wa kitaalamu kwa taasisi husika.  


 


📌 Waziri Ndejembi asema mradi utaimarisha Gridi ya Taifa na kuongeza uwezo wa kusafirisha umeme

📌 Mradi unatarajiwa kukamilika Agosti 21, 2026

📌 MD TANESCO asema Shirika limevunja rekodi kwa kuunganisha wateja zaidi ya laki nane mwaka 2025/26


Mradi wa ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme ya msongo wa kilovoti 400 kutoka Chalinze hadi Dodoma wenye urefu wa kilometa 345 umefikia asilimia 89 ya utekelezaji na unatarajiwa kukamilika Agosti 21, 2026, hatua itakayoongeza uwezo wa kusafirisha umeme na kuimarisha uthabiti wa Gridi ya Taifa.

Akikagua maendeleo ya Mradi huo Julai 1, 2026, Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi (Mb), amesema mradi huo ni miongoni mwa uwekezaji wa kimkakati wa Serikali unaolenga kuimarisha miundombinu ya usafirishaji wa umeme nchini na kuongeza uwezo wa Gridi ya Taifa kuhudumia mahitaji yanayoendelea kuongezeka.

Amesema njia hiyo ya kusafirisha umeme ina umuhimu mkubwa kutokana na kuwezesha usafirishaji wa umeme unaozalishwa na Kituo cha Kufua Umeme cha Julius Nyerere chenye uwezo wa kuzalisha megawati 2,115.

Aidha, Waziri Ndejembi amesema Serikali itaendelea kuwekeza katika miradi ya umeme ili kuhakikisha huduma ya umeme wa uhakika inaendelea kuwafikia Watanzania na kukidhi mahitaji ya sekta mbalimbali za uzalishaji.

“Serikali imeona mahitaji ya umeme nchini yanazidi kuongezeka, hivyo ujenzi wa njia hii ya umeme ni muhimu sana kwani utaleta uthabiti katika Gridi ya Taifa,” amesema Mhe. Ndejembi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Bw. Razalo Twange, amesema ongezeko la uwekezaji katika miundombinu ya umeme limechangia kuongezeka kwa idadi ya wateja wanaounganishiwa huduma, ambapo katika mwaka wa fedha 2025/26 Shirika limeandika historia kwa kuwaunganishia umeme zaidi ya wateja laki nane.

“Haijawahi kutokea tangu Tanzania ipate uhuru. Hii inaonesha mahitaji ya umeme yameongezeka, na hivyo sisi tunaendelea kuongeza miundombinu ya umeme,” amesisitiza Bw. Twange.

Awali, akitoa taarifa ya utekelezaji wa mradi huo, Meneja wa Mradi, Mha. Newton Mwakifamba, amesema kazi zinaendelea vizuri na zinatarajiwa kukamilika Agosti 21, 2026, kwa mujibu wa ratiba ya mkataba.
















Na Mwandishi Wetu- Dodoma

Kaimu Mkurugenzi wa Taasisi ya Chakula na Lishe Tanzania (TFNC) Bi. Debora Charwe amesema, Serikali ipo katika mchakato wa kuandaa Mpango wa Muda Mrefu wa Lishe wa Taifa (NN-LTP) ili kuongeza jitihada za sekta mtambuka katika kuboresha utekelezaji wa lishe kwa kipindi cha miaka 25 ijayo

Bi. Debora ameyasema hayo leo tarehe 30 Juni, 2026 wakati akifungua Warsha ya mafunzo kuhusu kuandaa mpango wa muda mrefu wa lishe wa Taifa (National Nutrition Long Term Plan 2026-2050) ambayo inafanyika jijini Dodoma kwa siku tatu kuanzia Juni 30 hadi Julai 02, 2026



Amesema, mafunzo hayo yanatolewa kwa Wataalam kutoka ngazi ya Wizara mbalimbali kwa lengo la kuwajengea uwezo kuhusu uandaaji wa mipango ya muda mrefu wa lishe inayojumuisha sekta mtambuka pamoja na kubadilishana uzoefu kusaidia katika usanifu, muundo na taratibu za utekelezaji wa Mpango wa muda mrefu wa Lishe wa Taifa.




















Vilevile Bi. Debora amefafanua kuwa, mpango huo unaandaliwa chini ya usimamaizi wa Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kushirikiana na Taasisi ya Chakula na Lishe Tanzania (TFNC) na wadau wengine wa maendeleo kwa kuzingatia haja ya kuifanya lishe kuwa moja ya kichocheo na kipimo katika kufikiwa kwa malengo ya Dira ya Maendeleo ya Tanzania kufikia 2050.

Aidha, warsha hiyo imehusisha Afisa viungo wa lishe kutoka Wizara mbalimbali zikiwemo Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Ofisi ya Rais Maendeleo ya Vijana, Ofisi ya Waziri Mkuu TAMISEMI, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano) pamoja na Wizara ya Kilimo, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Wizara ya Viwanda, Wizara ya Maji na Wizara ya Mambo na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.


Baada ya Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kuzindua Dira 2050, Julai 17, 2025 jijini Dodoma, hatimaye leo tarehe 1 Julai, 2026, Tanzania imeanza rasmi utekelezaji wa Dira hiyo.

Kuanza kwa utekelezaji wa Dira 2050 kunahitimisha safari ndefu ya utekelezaji wa DIRA 2025 na kuanza kwa safari nyingine ya robo karne (miaka 25) inayolenga kubadilisha sura ya kiuchumi, kijamii, na kiteknolojia ya taifa letu.

Kwa mujibu wa Katibu Mkuu Ofisi ya Rais-Mipango na Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango Dkt. Tausi M. Kida, Dira ya 2050 imejengwa juu ya misingi ya ushiriki wa moja kwa moja wa mwananchi. Kuanzia kwa mkulima wa kijijini hadi kwa mbunifu wa teknolojia mjini, kila mmoja leo anaanza kuhesabiwa kama injini ya mabadiliko haya.

"Huu ni wakati wa kuangalia jinsi kila sekta, (binafsi na ya umma) inavyoingiza vipaumbele vya Dira 2050 kwenye utendaji wake wa kila siku, kwa kuwa mafanikio ya utekelezaji wake yanategemea ushiriki wa kila mmoja wetu" amesema Dkt. Kida.

Dira hiyo, inatarajiwa kujenga Taifa jumuishi lenye ustawi, haki na linalojitagemea, Taifa litakalokuwa na uchumi imara, jumuishi na wenye Pato la thamani ya dola za Marekani trilioni moja ifikapo 2050.

Naibu Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya EWURA, Mha. Ngosi Mwihava (kushoto) na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, Ndg. Gerald Maganga (Kulia) wakimkabidhi Mh. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan mfano wa hundi kama ishara ya kukabidhi Hazina mchango wa kisheria wa taasisi hiyo wa Sh. 10.6 bilioni, kwa mwaka wa Fedha 2025/26, kwenye hafla iliyofanyika Ikulu jana.

 

 


● Yaligunduliwa kwa mara ya kwanza duniani mwaka 1959 katika Wilaya ya Kongwa, Mkoa wa Dodoma.

● Yana thamani kubwa katika elimu, utafiti wa kisayansi na utalii wa jiolojia.

● Ni sehemu ya urithi wa asili wa Tanzania.


Imeelezwa kuwa kuna umuhimu wa kuchukua hatua madhubuti za kuhifadhi na kulinda madini adimu aina ya Yoderite yanayopatikana katika eneo la Mlima wa Mautia, Wilaya ya Kongwa, Mkoa wa Dodoma, ili kuhakikisha urithi huo wa kipekee wa kijiolojia unabaki salama kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.

Hayo yalisemwa Juni 30, 2026 na Meneja wa Jiolojia kutoka Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST), Solomon Maswi, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari waliotembelea eneo hilo kwa ziara maalumu.

Maswi alisema kuwa uhifadhi wa Yoderite unaweza kuiwezesha Tanzania kuwa kitovu cha kimataifa cha tafiti kuhusu madini adimu, sambamba na kuongeza idadi ya watalii wanaotembelea maeneo yenye urithi wa jiolojia.

Aliongeza kuwa Yoderite ni miongoni mwa madini adimu yanayoifanya Tanzania kutambulika duniani kutokana na historia yake ya kugunduliwa kwa mara ya kwanza katika Mlima wa Mautia.

Aidha, alifafanua kuwa madini hayo yana mchango mkubwa katika tafiti za kisayansi kwa kusaidia kuelewa mchakato wa uundaji wa miamba na mazingira yenye shinikizo na joto la juu ndani ya ganda la dunia. Pia yana umuhimu mkubwa katika elimu ya jiolojia, maendeleo ya utalii wa jiolojia na uhifadhi wa urithi wa asili duniani.

Maswi alibainisha kuwa, kutokana na uchache wake na kupatikana katika maeneo machache sana duniani, madini ya Yoderite hayachimbwi kwa matumizi ya viwandani wala biashara. Badala yake, yanahifadhiwa kama urithi wa kipekee wa kijiolojia unaovutia watafiti, wanafunzi, wataalamu wa sayansi na watalii kutoka ndani na nje ya nchi. Hali hiyo inaipa Tanzania fursa ya kujijengea hadhi kama kitovu cha tafiti za kimataifa na utalii wa jiolojia unaotegemea urithi wa asili.

Taasisi za utafiti wa madini na vyuo vya Madini vimeshauriwa kutumia eneo hilo kwa mafunzo endelevu ya utafiti wa madini.

Madini ya Yoderite yaligunduliwa kwa mara ya kwanza duniani mwaka 1959 katika Milima ya Mautia, Wilaya ya Kongwa, Mkoa wa Dodoma.

Kutokana na kuendelea kwa tafiti baada ya miaka 35 watafiti wa miamba na madini walifanikiwa kugundua aina hiyo ya madini nchini Zimbambwe.

Jina la Yoderite lilipewa kwa heshima ya mwanajiolojia mashuhuri wa Marekani, Hatten Yoder Jr., kutokana na mchango wake mkubwa katika tafiti za miamba na madini.