Awataka wakuu wa mikoa kuendeleza kampeni za usafi


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) Mhe. Prof. Riziki amewapongeza Maafisa Afya wa Mikoa na Halmashauri nchini kwa kupunguza mlipuko wa kipindupindu kutoka maambukizi ya watu 12,000 hadi 700 kwa mwaka 2025/26, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa malengo waliyojiwekea mwaka jana.

Prof. Shemdoe ametoa pongezi hizo Juni 01, 2026 jijini Arusha, wakati  akifungua mkutano wa mwaka wa tathmini ya utekelezaji wa afua za afya na usafi wa mazingira nchini, unaofanyika katika Ukumbi wa Mkutano wa Kimataifa (AICC).

“Niwapongeze kwa utekelezaji wa lengo la kupunguza mlipuko wa ugonjwa wa kipindupindu mlilojiwekea mwaka jana, mmefanikiwa kupunguza kiwango cha mlipuko kutoka kesi 12,000 hadi 700, sasa niwaombe mwaka huu muweke lengo la kuendelea kutokomeza mlipuko wa ugonjwa huu,” amesema Prof. Shemdoe.

Sanjari na hilo, Prof. Shemdoe amewasisitiza Wakuu wa Mikoa, Maafisa Afya wa Mikoa na Halmashauri kuwahimiza wananchi kufanya mazoezi ili kuepukana na magonjwa yasiyoambukizwa kama shinikizo la damu, kisukari, magonjwa ya moyo, kiharusi, pumu, ambayo yanasababisha vifo na kuathiri nguvu kazi ya taifa.

Aidha, Prof. Shemdoe amewataka Wakuu wa Mikoa nchini kuendelea na kampeni ya kufanya usafi kila jumamosi ya mwisho wa mwezi kwani kampeni hiyo itaendelea kuimarisha hali ya usafi, kupunguza na kuondoa kabisa changamoto uwepo ya magonjwa ya milipuko ikiwepo kipindupindu.

Prof. Shemdoe ametumia fursa hiyo, kumshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uongozi wake na namna anavyowekeza katika sekta ya afya na mazingira, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa maono yake ya kutaka kila mtanzania awe na afya bora.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mhe. CPA Amos Makalla amemhakikishia Prof. Shemdoe kuwa, mkoa wake umejipanga ipasavyo katika utekelezaji wa miradi ya afya, na kuongeza kuwa ofisi yake itaendelea kushirikiana na wataalam wa afya katika kukabiliana na magonjwa ya milipuko.

Naye, Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu - TAMISEMI anayeshughulikia Afya Prof. Tumaini Nagu amesema mkutano huo umelenga kutathmini mpango kazi wa mwaka 2025/26 waliojiwekea maafisa afisa afya kuanzia ngazi ya mikoa hadi Mamlaka za Serikali za Mitaa, pamoja na kuandaa mpango kazi wa mwaka wa fedha 2026/27. 

Akifafanua malengo la mkutano huo, Mkurugenzi wa Afya,Ustawi wa Jamii na Lishe wa Ofisi ya Waziri Mkuu -TAMISEMI Dkt. Rashid Mfaume amesema kuwa, malengo ya mkutano huo ni kutathmini maendeleo ya utekelezaji wa afua ya afya na usafi wa mazingira katika ngazi ya Mikoa na Halmashauri kwa kuzingatia viashiria vya kitaifa na malengo ya kisekta.

Akizungumza kwa niaba ya washiriki wa mkutano huo, Mwenyekiti wa Maafisa Afya wa Halmashauri Bw. Fanuel Nyadwike amemuahaidi Prof. Shemdoe kuwa, watatumia mkutano huo kutathmini utekelezaji wa shughuli za mwaka uliopita wa 2025/26, kubadilishana uzoefu na kujifunza mbinu bora za kuboresha huduma za afya na usafi wa mazingira kwa mwaka 2026/27. 

Mkutano huo wa mwaka huu wa 2026 umebeba kaulimbiu isemayo “Kuimarisha Mifumo Jumuishi na Endelevu ya Afya na Usafi wa Mazingira ili Kujenga Jamii Stahimilivu yenye Afya Bora”.












Mkurugenzi wa Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB), Bw. Asangye Bangu, amewataka waendesha maghala kuzingatia uadilifu, uwajibikaji na utoaji wa huduma bora ili kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala.

Akifungua kikao maalumu cha waendesha maghala kilichofanyika mjini Morogoro Julai 1, 2026, Bangu, amesema waendesha ghala wanapaswa kuendana na wakati kwa kuwa waadilifu, kutoa huduma zenye viwango vya juu na kuhakikisha mfumo wa stakabadhi za ghala unaendelea kuwa na tija kwa wakulima, wafanyabiashara na wananchi kwa ujumla.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Waendesha ghala Tanzania, Abdulikarim amesema kikao hicho kimeandaliwa kwa lengo la kuongeza uelewa kuhusu masuala mbalimbali ya kiutendaji, kujadili changamoto zinazowakabili pamoja na kutafuta suluhisho la kuboresha maslahi ya waendesha ghala kutokana na kupanda kwa gharama za maisha na uendeshaji wa shughuli zao.

Ameongeza kuwa maazimio na maelekezo yaliyotolewa katika kikao hicho yatawasaidia waendesha ghala kuongeza ufanisi wa kazi zao na kuendelea kutoa huduma bora kwa wadau wote wa sekta ya kilimo.



Standard Chartered Tanzania kwa kushirikiana na Nipe Fagio imeadhimisha miaka 20 ya programu ya kujitolea kwa jamii ya Standard Chartered duniani kwa kufanya zoezi la kila mwaka la usafi wa fukwe katika Ufukwe wa Silversand, Kunduchi.

Jumla ya washiriki 74, wakiwemo watoto 20, walishiriki katika zoezi hilo lililolenga kuchangia uhifadhi wa mazingira na kuhamasisha ushiriki wa wafanyakazi katika shughuli za maendeleo ya jamii.

Akizungumza kuhusu shughuli hiyo, Afisa Mtendaji Mkuu na Mkuu wa Kitengo cha Coverage wa Standard Chartered Bank Tanzania, Geofrey Mchangila, alisema:

"Zoezi la mwaka huu lina umuhimu wa pekee kwetu kwani linafanyika wakati Standard Chartered inaadhimisha miaka 20 ya kujitolea kwa jamii duniani kote. Tunaamini kuwa mabadiliko ya kweli huanza pale watu wanapounganisha nguvu zao. 

Kupitia ushirikiano wetu na wafanyakazi, familia zao pamoja na Nipe Fagio, tunaendelea kuchangia kulinda ukanda wa pwani wa Tanzania na kujenga jamii zenye afya bora na mazingira endelevu kwa vizazi vijavyo."

Katika zoezi hilo, washiriki walisafisha eneo lenye ukubwa wa takribani mita za mraba 4,000 za ufukwe na kukusanya kilo 506 za taka zilizohifadhiwa katika mifuko 55. 

Uchambuzi wa taka zilizokusanywa ulionyesha kuwa plastiki, hususan povu la polystyrene na chupa za plastiki za vinywaji, ndizo zilikuwa taka zilizopatikana kwa wingi, hali inayodhihirisha umuhimu wa kuendelea kuchukua hatua za kudhibiti uchafuzi wa mazingira ya bahari.

Kwa kipindi cha miaka mitatu iliyopita, kupitia ushirikiano wake na Nipe Fagio, Standard Chartered Tanzania imefanikisha jumla ya kampeni tano za usafi wa fukwe, ikihusisha washiriki 594, kusafisha zaidi ya mita za mraba 32,000 za ukanda wa pwani na kukusanya karibu tani tano za taka.

Mpango huu ni sehemu ya mkakati mpana wa Standard Chartered wa kuendeleza uhimilivu wa mazingira na maendeleo endelevu, huku ukiunga mkono Malengo ya Maendeleo Endelevu ya Umoja wa Mataifa (SDGs), hususan Lengo la 13 la Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi, Lengo la 14 la Kuhifadhi Maisha ya Chini ya Maji na Lengo la 17 la Kuimarisha Ushirikiano kwa Ajili ya Kufanikisha Malengo.

Standard Chartered inapoendelea kuadhimisha miaka 20 ya programu yake ya kujitolea kwa jamii, inaendelea kuwahamasisha wafanyakazi wake kutumia muda, ujuzi na utaalamu wao kuleta mabadiliko chanya na endelevu katika jamii na mazingira.










 


Serikali imetangaza kuanza kutoa vibali vya ujenzi na kufanya majadiliano na wamiliki wa ardhi na nyumba ambao wapo tayari kushiriki kwenye Mpango wa Uendelezaji Upya eneo la Sinza, huku ikisisitiza kuwa mchakato uliopita umefutwa ili kutoa nafasi ya kuanza upya kwa misingi ya uwazi, ushirikishwaji na kujenga maridhiano.

Kauli hiyo ilitolewa Julai 1, 2026 jijini Dar es Salaam na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dkt. Leonard Akwilapo, alipokutana na wamiliki wa ardhi na nyumba wa Sinza kwa lengo la kuwafafanulia hatua za utekelezaji wa mpango huo na kusikiliza maoni yao.

Dkt. Akwilapo alisema Serikali imeamua kufungua ukurasa mpya baada ya kubaini kuwa mchakato uliopita uliacha malalamiko kutoka kwa baadhi ya wananchi, hivyo vikao vyote vya awali vimefutwa na sasa mazungumzo yanaanza upya kwa ushirikiano na wananchi.

Alieleza kuwa ukuaji wa miji ni jambo lisiloepukika kutokana na ongezeko la watu na mahitaji ya makazi, hivyo Serikali ina wajibu wa kupanga matumizi ya ardhi kwa kuzingatia mahitaji ya sasa na ya baadaye.

Waziri huyo alisema Sinza ya sasa imebadilika kwa kiwango kikubwa ikilinganishwa na ilivyokuwa miaka ya nyuma, jambo ambalo linahitaji mpango mpya wa maendeleo utakaoendana na hadhi yake kama eneo muhimu la makazi na biashara ndani ya Jiji la Dar es Salaam.

"Kama mwananchi anaona mpango huu haufai, hiyo ni haki yake, lakini ipo siku ataona umuhimu wake. Tusiporatibu maendeleo ya miji, tutakuwa na maeneo yasiyo na mpangilio na yenye miundombinu isiyokidhi mahitaji ya wananchi," alisema.

Dkt. Akwilapo alibainisha kuwa uendelezaji upya wa maeneo ya makazi si jambo geni nchini, kwani maeneo kama Posta, Kariakoo, Upanga, Oysterbay na Masaki yamepitia hatua kama hizo na yameendelea kuwa na thamani kubwa zaidi kutokana na upangaji mzuri wa matumizi ya ardhi.

Waziri huyo aliwataka wananchi kuwa makini na watu wasio waaminifu wanaoweza kutumia mchakato huo kuwahadaa au kuwasambazia taarifa zisizo sahihi kwa manufaa binafsi.

Kwa upande wake, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo, alisema mafanikio ya mpango huo yatategemea kiwango cha ushirikishwaji wa wananchi na kuzingatia maoni yao.

Alipendekeza muda wa ukusanyaji wa maoni uongezwe kwa miezi mitatu ili wananchi wengi zaidi wapate nafasi ya kuelewa mpango huo na kutoa maoni yao kabla ya hatua za utekelezaji kuanza.

"Wananchi wasikilizwe, maoni yao yazingatiwe na rasimu iboreshwe ili iakisi matakwa yao. Serikali ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan haiwezi kupora haki za wananchi bali itafuata sheria, kanuni na taratibu zote zinazotambuliwa," alisema Profesa Mkumbo.

Naye Katibu Mkuu wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhandisi Anthony Sanga aliwataka wamiliki wa ardhi na nyumba wa Sinza kuwa watulivu na kutochukua maamuzi ya haraka ya kuuza maeneo yao kutokana na taarifa zisizo rasmi.

Alisema thamani ya ardhi katika eneo la Sinza imeongezeka maradufu hivyo wananchi wanapaswa kutambua fursa iliyopo badala ya kufanya maamuzi yatakayowagharimu baadaye.

Akizungumza kwa niaba ya Kamati ya Wamiliki wa Ardhi na Nyumba wa Sinza, Mwenyekiti wa kamati hiyo, Bw. Asibwene Lumuli, alisema ushirikiano kati ya Serikali na wananchi ndio utakaohakikisha mpango huo unatekelezwa kwa mafanikio na kwa manufaa ya pande zote.






Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga, leo Julai 1, ametembelea banda la Wakala wa Ufundi na Umeme Tanzania (TEMESA) katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Sabasaba, yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, Barabara ya Kilwa, jijini Dar es Salaam.

Akizungumza bandani hapo, Mhe. Kapinga ameipongeza TEMESA kwa kasi ya mabadiliko inayoenda nayo katika matengenezo ya magari na mabadiliko ya mifumo ya utoaji huduma.



“Nawapongeza sana kwa kazi nzuri mnazozifanya katika matengenezo ya magari na pia matumizi yenu ya mifumo katika utoaji huduma. Hongareni sana.” Amesema Mhe. Kapinga.

Waziri wa Viwanda na Biashara alipotembelea banda la TEMESA alipata fursa ya kujionea huduma mbalimbali zinazotolewa na TEMESA, ikiwemo huduma za vivuko, umeme na elektroniki, matengenezo ya magari na mitambo, ushauri wa kihandisi pamoja na mifumo ya kidijitali na ubunifu unaolenga kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.



Maonesho hayo ya biashara yamebebwa na kauli mbiu isemayo “Hii ni Kubwa Kuliko” na yanatarajiwa kuzinduliwa rasmi siku ya ijumaa tarehe 3 Juni, 2026



TEMESA inaendelea kuwakaribisha wananchi, wadau na wageni wote kutembelea banda lake ili kujifunza kuhusu huduma zake, kupata ushauri wa kitaalamu na kufahamu mchango wa Wakala katika maendeleo ya sekta ya ufundi na umeme nchini.