Wakala wa Nishati Vijijini (REA) na Shirika la Mzinga leo Mei 21, 2026 wamesaini hati ya makubaliano ya ushirikiano yanayolenga kuimarisha ushirikiano katika Utafiti, Teknolojia, Uzalishaji na Usambazaji wa nishati safi ya kupikia.
Akizungumza wakati wa hafla hiyo iliyofanyika Mkoani Morogoro, Mwenyekiti wa Bodi ya Shirika la Mzinga, Mhe. Balozi Luteni Jenerali (Mstaafu), Charles Lawrence Makakala, amesema utekelezaji wa mpango huo utakuwa msaada mkubwa kwa wanawake wa vijijini ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakikumbana na changamoto ya kutafuta nishati kwa ajili ya kupikia.
“Akina mama wa vijijini wanapata adha kubwa kutafuta nishati ya kupikia. Madhara ya kiafya wanayoyapata wao pamoja na watoto wao ni makubwa kwa sababu watoto pia hushiriki katika shughuli za maandalizi ya chakula. Hatua hii itasaidia utekelezaji wa sera ya nishati safi lakini pia kuinua ustawi wa jamii na uchumi endelevu,” amesema Makakala.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), Mhe. Balozi Meja Jenerali (Mstaafu), Jacob Kingu, amesema ushirikiano huo utaongeza uzalishaji wa mkaa mbadala utokanao na mabaki ya mimea pamoja na uzalishaji wa majiko banifu kwa bei nafuu zaidi na hivyo kuongeza matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini.
Mkurugenzi Mkuu wa REA, Mhandisi Hassan Saidy, amesema makubaliano hayo pia yanakwenda kuongeza aina za nishati safi za kutumika zenye gharama nafuu zaidi lengo likiwa kuongeza matumizi ya nishati safi ya kupikia.
Mhandisi Saidy amesema kuwa kati ya Watanzania wanne, ni mmmoja tu ndo anatumia nishati safi ya kupikia. Hivyo kupitia ushirikiano huo unaokwenda kuongeza uzalishaji wa mkaa mbadala pamoja na majiko banifu, idadi ya Watanzania wanaotumia nishati safi ya kupikia itakwenda kuongezeka.
Naye Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Mzinga, Brigedia Jenerali Mhandisi Seif Athuman Hamisi, amesema makubaliano hayo yatahusisha maeneo mbalimbali ikiwemo kufanya tafiti za kuboresha matumizi ya majiko na mkaa safi ili kuhakikisha teknolojia hizo zinakidhi mahitaji ya wananchi.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amesema Serikali inatambua umuhimu mkubwa wa Waandishi Waendesha Ofisi kwa kuwa ni muhimili muhimu katika kuwawezesha Viongozi na watendaji kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.
Makamu wa Rais amesema hayo, wakati wa ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa 13 wa Kitaaluma wa Waandishi wa Waendesha Ofisi Tanzania (TAPSEA) unaofanyika katika Ukumbi wa Ngurdoto Mkoani Arusha. Amesema Serikali inaipa uzito Taasisi ya TAPSEA kwa kuwa inatambua ili kuwa na utulivu na mshikamano ni lazima Waandishi Waendesha ofisi kutimiza wajibu ipasavyo.
Amewapongeza Waandishi Waendesha Ofisi kwa kubeba sura za Taasisi wanazofanyia kazi kwa kuwa wakarimu na wenye kutoa msaada wa awali kwa wananchi wanaofika kutafuta huduma. Amewasihi kuendelea kutoa huduma kwa ukamilifu pamoja na kuwa na heshima na ukarimu ili kuwafariji wanaowahudumia.
Aidha Makamu wa Rais, amewasisitiza waandishi waendesha ofisi kuendelea kujitambua na kutunza siri wakati wa utekelezaji wa majukumu yao.
Makamu wa Rais amekipongeza Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania kwa kuimarisha elimu yao mpaka kufikia shahada ya uzamili ambayo imewawezesha Waandishi Waendesha Ofisi kuhama katika mfumo asili wa utekelezaji wa majukumu yao mpaka kufikia kuwa sehemu ya maamuzi ya kisera na upangaji wa mikakati na utekelezaji wake.
Amesisitiza kwamba Vyuo vinavyotoa mafunzo hayo, vinapaswa kuendelea kujiimarisha ili kuwa na Waandishi Waendesha Ofisi wanaoweza kusaidia vema Taifa. Makamu wa Rais ametoa wito kwa Taasisi mbalimbali kuhakikisha wanawawezesha Waandishi Waendesha Ofisi kushiriki mikutano ya kitaaluma.
Halikadhalika, Makamu wa Rais amewapongeza Viongozi wa Taasisi hiyo wanaomaliza muda wao kwa kufanya kazi nzuri iliyowaunganisha na kuwawezesha Waandishi Waendesha Ofisi nchini. Aidha amewataka kufanya uchaguzi wa haki ili kupata Viongozi sahihi wanataoiongoza vema Taasisi hiyo. Amewasihi kufanya uchaguzi kwa kuzingatia uhuru na haki ili kupata viongozi sahihi wa Taasisi hiyo pamoja na kuwataka wanachama kuchagua viongozi makini bila ubaguzi wa aina yeyote.
Kwa upande wake Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete, amesema Serikali kupitia ofisi hiyo, itaendelea kutoa ushirikiano kwa watumishi wote wa Umma ikiwemo uongozi wa TAPSEA ili kufanikisha masuala mbalimbali ya kiutumishi kwa wanachama wake.
Ameongeza kwamba, Ofisi hiyo itaendelea kuwaangalia na kuwalea wanaTAPSEA na kuwataka kuwa na imani na serikali inayoongozwa na Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwa wataendelea kuwaangalia katika hali zote kiwemo maslahi yao, kutoa mafunzo pamoja na kuwahakikisha kuwa salama muda wote.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Waandishi Waendesha Ofisi Tanzania (TAPSEA) Bi. Zuhura Maganga amesema Taasisi hiyo inajivunia mafanikio yaliyopatikana katika kuimarisha taaluma ya uandishi uendesha ofisi ikiwemo kuanzishwa kwa shahada ya utawala inayotolewa na Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania pamoja kuanzishwa kwa shahada ya uzamili ya Sanaa katika mawasiliano na usimamizi wa ofisi.
Imetolewa na
Ofisi ya Makamu wa Rais
21 Mei 2026
Arusha.
Jeshi la Polisi Kanda Maalum Dar es Salaam limeeleza kuwa linaendelea na uchunguzi wa tukio la kukamatwa kwa David Joseph Mghanja maarufu kama Djumbe, kufuatia taarifa zilizosambaa kupitia mitandao ya kijamii zikidai alichukuliwa na watu wasiojulikana maeneo ya Bunju.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo Mei 21, 2026 na Kaimu Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalum Dar es Salaam, Jeshi hilo lilianza kufuatilia tukio hilo tangu usiku wa Mei 20, 2026 baada ya taarifa mbalimbali kuanza kusambaa mtandaoni.
Katika ufuatiliaji huo, Polisi walifanikiwa kulipata gari lenye namba T 609 DTD aina ya Toyota Wish rangi nyeusi, linalomilikiwa na Allan Elisonguo Macha, ambalo inadaiwa Djumbe alikuwa akisafiria kama abiria wakati alipokamatwa na watu wanaodaiwa kutokujitambulisha.
Taarifa hiyo imeeleza kuwa asubuhi ya leo Mei 21, 2026, Jeshi la Polisi lilipokea taarifa zikidai kuwa Djumbe alikuwa katika Ofisi za Chadema zilizopo Mikocheni, jijini Dar es Salaam.
Amesema Askari walifika katika eneo hilo lakini hawakumkuta, huku wakimkuta mtu anayedaiwa kuwa alikuwa pamoja naye wakati wa tukio la kukamatwa kwake.
Aidha, Jeshi la Polisi limethibitisha kuwa Djumbe tayari amepatikana salama na kwamba uchunguzi unaendelea ili kubaini watu waliomkamata pamoja na sababu za kufanya tukio hilo.
Polisi wameeleza kuwa hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi ya wahusika wote watakaobainika kuhusika na tukio hilo kwa mujibu wa sheria za nchi.

TUME ya Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC) imeshiriki Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali kuhusu Uvumbuzi wa Nishati ya Nyuklia Barani Afrika (NEISA 2026) uliofanyika Mei 19, 2026 mjini Kigali, Rwanda, ukiwakutanisha viongozi wa kitaifa, wataalamu wa nishati, wawekezaji pamoja na mashirika ya kimataifa kujadili mustakabali wa nishati ya nyuklia barani Afrika.
Mkutano huo ulilenga kujadili namna bora ya kuongeza upatikanaji wa nishati ya umeme, kupunguza uchafuzi wa mazingira, kusaidia maendeleo ya viwanda, kukuza ubunifu wa teknolojia za nyuklia pamoja na kuvutia uwekezaji katika miradi ya nishati kwa ajili ya kuimarisha uchumi endelevu.
Katika mkutano huo, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan alisema Tanzania inaendelea kutathmini matumizi ya nishati ya nyuklia kama sehemu ya mkakati wa muda mrefu wa kuongeza vyanzo vya nishati nchini.
Rais Samia alieleza kuwa teknolojia mpya za Small Modular Reactors (SMRs) na Micro Modular Reactors (MMRs) zinaweza kuwa suluhisho sahihi kwa nchi zinazoendelea kutokana na uwezo wake wa kuzalisha nishati kwa ufanisi na usalama zaidi.
Aidha, alitaja maeneo muhimu yanayopaswa kupewa kipaumbele katika maendeleo ya sayansi na teknolojia ya nyuklia kuwa ni pamoja na mifumo imara ya udhibiti, wataalamu wenye ujuzi pamoja na usimamizi madhubuti wa usalama kwa kuzingatia viwango vya kimataifa.
Alisisitiza kuwa matumizi ya teknolojia ya nyuklia katika uzalishaji wa nishati yanahitaji maandalizi ya mifumo ya udhibiti, uwezo wa taasisi, upatikanaji wa fedha, uelewa wa wananchi na ushirikiano wa kikanda.
Katika ushiriki wake, Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania, Profesa Najat Kassim Mohammed alihudhuria mkutano huo akiwa ameambatana na Mkurugenzi wa Teknolojia ya Nyuklia na Huduma za Ufundi, Dkt. Remigius Kawala.
Profesa Najat alipata fursa ya kushiriki kikao cha ndani kilichoongozwa na Rais Samia ambapo alitoa ufafanuzi kuhusu maendeleo ya nyuklia nchini pamoja na miradi inayotekelezwa na TAEC kwa kushirikiana na International Atomic Energy Agency.
Miongoni mwa mipango hiyo ni Rays of Hope unaolenga kuimarisha huduma za uchunguzi na matibabu ya saratani nchini, Atoms4Food unaohamasisha matumizi ya teknolojia ya nyuklia katika sekta ya kilimo pamoja na ushiriki wa TAEC katika mpango wa matumizi ya teknolojia ya nyuklia kwa uzalishaji wa umeme.
Profesa Najat alisisitiza umuhimu wa Tanzania kuendelea kuwekeza katika utafiti, usalama na mafunzo ya wataalamu ili kuhakikisha matumizi salama na endelevu ya teknolojia ya nyuklia katika sekta mbalimbali ikiwemo afya, kilimo, viwanda, utafiti wa madini na uzalishaji wa nishati.
Kupitia mkutano huo, TAEC ilipata nafasi ya kubadilishana uzoefu na wataalamu kutoka mataifa mbalimbali kuhusu usalama wa nyuklia, mifumo ya udhibiti wa teknolojia za nyuklia pamoja na uwekezaji katika miundombinu ya kisasa ya nishati.
Aidha, ushiriki wa Tanzania katika NEISA 2026 uliendana na maono ya serikali ya kukuza sekta ya nishati na kuimarisha ushirikiano wa kikanda ndani ya Afrika Mashariki.
Katika mkutano huo, viongozi mbalimbali wa Afrika walisisitiza umuhimu wa ushirikiano wa kikanda katika kuendeleza miradi ya nyuklia, kuongeza uwekezaji na kujenga uwezo wa wataalamu wa ndani.
Kwa ujumla, ushiriki wa TAEC katika NEISA 2026 umeiwezesha Tanzania kuendelea kujijengea nafasi katika mjadala wa kimataifa kuhusu mustakabali wa nishati ya nyuklia barani Afrika pamoja na kufungua fursa mpya za ushirikiano wa kitaalamu, kiteknolojia na kiuchumi kwa maendeleo endelevu ya taifa.
Mkutano wa NEISA 2026 uliandaliwa kwa ushirikiano wa International Atomic Energy Agency, United Nations Economic Commission for Africa, World Nuclear Association pamoja na Rwanda.


NAIBU Spika wa Bunge, Daniel Sillo, ametoa wito kwa wananchi na wadau mbalimbali kushiriki katika kuchangia huduma za matibabu ya upandikizaji Uloto kwa Watoto wenye ugonjwa wa Sicle Cell na upandikizaji figo kwa wenye uhitaji hapa nchini.
Ameyasema hayo wakati wa hafla ya chakula cha jioni tarehe 19 Mei, 2026 katika ukumbi wa Domiya jijini Dodoma, ambapo hafla hiyo imewakutanisha viongozi waandamizi wa mkoa wa Dodoma, wabunge na wadau mbalimbali kwa lengo la kujadili namna ya kuimarisha mfuko wa kusaidia matibabu ya upandikizaji uloto na figo pamoja na huduma nyingine za kibingwa.
.jpeg)
Amesema licha ya mafanikio yaliyopatikana ya huduma hizo za upandikizaji uloto na figo kutolewa hapa nchini na hivyo kuokoa fedha nyingi ambazo zingeweza kutumika endapo wananchi wangeenda kutibiwa nje ya nchi.
Alisema kila mwananchi anapaswa kutambua kuwa kuchangia huduma hizo si jukumu la serikali na taasisi pekee, bali ni wajibu wa pamoja kwa kuwa magonjwa ya figo na sickle cell hayachagui mtu kwa nafasi yake, dini wala hali ya maisha.
“Tunaposhiriki katika michango hii si kwa ajili ya taasisi moja, bali tunaunga mkono huduma za kitaifa zinazogusa maisha ya wananchi wengi wanaohitaji matibabu hayo,” alisema Mhe. Sillo.

Alitoa wito kwa wananchi, taasisi na wadau mbalimbali kuendelea kuunga mkono juhudi hizo za BMH ili kuwezesha wagonjwa wanaohitaji huduma za upandikizaji viungo na matibabu mengine maalumu kupata huduma kwa wakati.

Ameeleza kutegemea bajeti ya serikali pekee hakuwezi kukidhi mahitaji yote yanayoongezeka ya huduma za kibingwa, hivyo ushirikishwaji wa wadau ni njia muhimu ya kuimarisha sekta ya afya na kuokoa maisha ya Watanzania wengi.



Naibu Waziri, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Ndege Qwaray (Mb), amefanya ziara ya kikazi katika Kituo cha Utafiti, Ubunifu na Uendelezaji wa Serikali Mtandao (Research, Innovation and Development Centre – RIDC) kilichopo jijini Dodoma, ambapo amekagua miradi mbalimbali ya TEHAMA inayotekelezwa na kituo hicho kwa lengo la kuboresha utoaji wa huduma Serikalini.
Katika ziara hiyo iliyofanyika mapema wiki hii, Mhe. Qwaray alipata fursa ya kutembelea na kujionea miradi ya kiteknolojia inayolenga kutoa suluhisho kwa changamoto katika sekta mbalimbali ikiwemo elimu, afya na utawala.
Aidha, miradi hiyo inahusisha matumizi ya teknolojia zinazochipukia kama vile Internet of Things (IoT) na Akili Mnemba (AI), katika kurahisisha utendaji kazi Serikalini na kuongeza ufanisi wa huduma kwa wananchi.
Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mhe. Qwaray ameipongeza Mamlaka ya Serikali Mtandao (e-GA) kwa juhudi zake za kuibua na kuendeleza vipaji vya vijana, kupitia tafiti na ubunifu wa mifumo mbalimbali ya TEHAMA yenye mchango mkubwa katika maendeleo ya taifa.
“Niwapongeze e-GA kwa kazi kubwa mnayoifanya ya kukuza ubunifu na tafiti za teknolojia. Dunia ya sasa inabadilika kwa kasi kubwa kutokana na maendeleo ya teknolojia, hivyo ni muhimu kuendelea kujifunza, kufanya tafiti na kubuni mifumo mipya itakayokwenda sambamba na mabadiliko hayo,” amesema Mhe. Qwaray.
Amesisitiza kuwa, bunifu zote zinazotengenezwa zinapaswa kuwa na tija kwa jamii na kuchangia moja kwa moja katika kuboresha huduma zinazotolewa kwa wananchi pamoja na kuongeza ufanisi ndani ya taasisi za Serikali.
Sambamba na hilo, Mhe. Qwaray amesisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano kati ya e-GA, vyuo vikuu na sekta binafsi ili kuongeza uwekezaji katika tafiti, ubunifu na maendeleo ya teknolojia zinazoweza kusaidia kutatua changamoto mbalimbali za kijamii na kiuchumi.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa e-GA, Mhandisi Benedict Ndomba, amesema kituo hicho kimeendelea kuwa chachu ya mageuzi ya kidijitali Serikalini kupitia ujenzi wa mifumo mbalimbali inayotumika katika taasisi za umma.
Ametaja baadhi ya mifumo hiyo kuwa ni Mfumo wa Uendeshaji wa Vikao vya Bodi na Menejimenti (e-Board) pamoja na Mfumo wa Uendeshaji wa Vikao Kidijitali (e-Mikutano), ambayo imekuwa ikisaidia kuongeza ufanisi katika shughuli za Serikali.
“Kituo hiki kimekuwa na manufaa makubwa kwa taifa kutokana na kazi zake za utafiti, ubunifu na maendeleo ya mifumo ya TEHAMA. Pia, kimefungua fursa kwa wanafunzi na vijana wenye taaluma ya TEHAMA kushiriki katika tafiti na bunifu mbalimbali kwa maslahi ya taifa,” amesema Mha.Ndomba.
Katika kuonesha dhamira ya Serikali kuendelea kuimarisha kituo hicho, Mhe. Qwaray ameahidi kuwa Wizara itaendelea kushirikiana na e-GA kutatua changamoto zinazoikabili RIDC ili kuongeza fursa kwa vijana wengi zaidi wa Kitanzania kupata nafasi ya kujifunza, kufanya tafiti na kushiriki katika ubunifu wa teknolojia mbalimbali za kisasa.








Na OWM - TAMISEMI, Azerbaijan
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amesema Serikali inayoongozwa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imetoa kipaumbele katika maandalizi ya upanuzi wa haraka wa miji pembezoni ili kukabiliana na changamoto zinazotokana na fursa za ukuaji wa miji na majiji nchini Tanzania.
Prof. Shemdoe ameelezea hatua hiyo ya Serikali aliposhiriki mdahalo Mei 19, 2026 nchini Azerbaijan ambao ni sehemu ya Mkutano Mkubwa wa kidunia wa maswala ya Miji (World Urban Forum), baada ya kuulizwa ni hatua zipi zimechukuliwa na Serikali ya Tanzania katika kujiandaa kwa upanuzi wa haraka wa miji pembezoni ili kukabiliana na athari za kukua kwa miji na majiji ikiwepo changamoto kubwa ya ukosefu wa ajira.
Prof. Shemdoe amefafanua kuwa, hatua ya Serikali ya Awamu ya Sita kufanya maandalizi ya mapema ya upanuzi wa miji na majiji pembezoni ni muhimu kwani lango kuu la jiji la Dar es Salaam, pamoja na ya majiji ya Dodoma, Mwanza, Mbeya na Arusha yanakua kwa kasi isiyokuwa ya kawaida.
Prof. Shemdoe ameongeza kuwa, upanuzi wa miji na majiji pembezoni ukitokea bila kuwepo na mipango ya mapema unasababisha ukosefu wa ajira na makazi yasiyo rasmi ambayo hayana maji safi, umeme wa uhakika, na usafi wa mazingira unaostahili, hivyo kurekebisha miundombinu katika maeneo hayo kunaigharimu zaidi Serikali wakati maandalizi yangefanywa mapema gharama za ujenzi wa miundombinu zingekuwa nafuu.
Prof. Shemdoe ameanisha kuwa, changamoto zote tatu zilizojadiliwa katika mdahalo huo ikiwemo ya ukosefu wa ajira katika miji, kutojiandaa mapema kwa upanuzi wa haraka wa miji pembezoni na mwenendo hafifu wa maendeleo katika miji midogo zimeligusa taifa ndio maana Dira ya Taifa ya Maendeleo ya Mwaka 2050 imetoa kipaumbele katika utatuzi wa changamoto hizo.
Na OWM - TAMISEMI, Dodoma
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amewasisitiza washiriki wa Mkutano wa Mwaka wa Tathmini ya Afua ya Uthibiti wa Taka Ngumu na Usafi wa Miji, kuhakikisha suala usafi wa mazingira linakuwa ajenda ya kudumu katika vikao vyote vitakavyofanyika katika ngazi zote za Mamlaka za Serikali za Mitaa ili kuwezesha miji na majiji nchini kuwa masafi.
Prof. Shemdoe ametoa maelekezo hayo Mei 12, 2026 jijini Dodoma wakati akifungua mkutano wa kwanza wa Mwaka wa Tathmini ya Afua ya Uthibiti wa Taka Ngumu na Usafi wa Miji, unaofanyika katika Ukumbi wa Hoteli ya Jiji- Mtumba, unaohudhuriwa na Maafisa Afya wa Mikoa, Maafisa Afya wa Halmashauri na Maafisa Mazingira wa Halmashauri.
“Nasisitiza suala la usafi wa mazingira liwe ajenda ya vikao vyenu. Vikao vya Kamati za Ushauri za Mikoa, Kamati za Ushauri za Wilaya, Kamati za Maendeleo za Kata, Mabaraza ya Madiwani, Kamati za Kudumu za Halmashauri pamoja na vya ALAT ngazi ya mkoa na taifa,” amesema Prof. Shemdoe.
Prof. Shemdoe ameainisha kuwa, usafi wa mazingira ukizingatiwa katika ngazi zote za Mamlaka ya Serikali za Mitaa utapunguza milipuko ya magonjwa na matumizi ya fedha kwa ajili ya ununuzi wa madawa, na fedha zitakazookolewa zitaelekezwa katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo, hivyo amewataka maafisa hao kufanya kazi kwa bidii na weledi ili kupunguza milipuko ya magonjwa na matumizi ya ununuzi wa dawa.
“Namshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuona umuhimu wa kuanzisha vitengo vya udhibiti wa taka ngumu ambavyo vinasaidia kuboresha zoezi la usafi wa mazingira nchini,” Prof. Shemdoe ameeleza.
Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu - Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa anayeshughulikia afya Prof. Tumaini Nagu amesema uthibiti wa taka kwenye halmashauri ni jambo muhimu katika kuhakikisha kunakuwa na usafi wa mazingira na udhibiti wa magonjwa ya milipuko na kuongeza kuwa, takwimu za kisayansi zinaeleza kwamba uthibiti madhubuti wa taka ngumu unapelekea kupungua kwa asilimia 30 hadi 40 za magonjwa kama Malaria na mengineyo ambayo yanadhibitiwa kwa usafi wa mazingira.
Akizungumza kwa niaba ya washiriki, Mkuu wa Kitengo cha Udhibiti taka ngumu wa Halmashauri ya wilaya Bahi Bw. William Mpangala amesema kuwa Serikali kupitia Mamlaka za Serikali za Mitaa inaendelea kushirikisha sekta binafsi katika utekelezaji wa afua za udhibiti wa taka ngumu kama za ukusanyaji na uchakataji wa taka ngumu, na kuongeza kuwa ushirikishwaji huo umeongeza ufanisi katika udhibiti wa taka kwenye halmashauri nchini.
Mkutano wa Mwaka huu una kaulimbiu isemayo “Taka ngumu ni Mali; tumia, rejeleza na Weka Miji katika hali ya usafi”.
















