Awataka kuwa na nidhamu na kusoma kwa bidii

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amewaasa wanafunzi walioshiriki mashindano ya UMISSETA mwaka 2026 kuendeleza vipaji vya michezo na Sanaa walivyonavyo kwani vitawasaidia katika maisha yao ya baadaye, huku akiwataka kuzingatia nidhamu na kusoma kwa bidii ili  kufikia ndoto zao na kutoa mchango katika maendeleo ya taifa.

Prof. Shemdoe ametoa wito huo kwa wanafunzi leo Juni 28, 2026 mjini Iringa katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Lugalo, wakati akifunga mashindano ya UMISSETA kwa mwaka wa 2026.

“Nina wasihi muendelee kuwa na nidhamu, kujituma katika masomo yenu na kuendeleza vipaji vyenu vya michezo na sanaa, msiviache vipaji vyenu kwani hata mimi juzi tulipokuwa tunapokea Mwenge wa Uhuru Lushoto nilijikuta nikikumbushia kipaji changu cha kupiga ngoma za utamaduni na kuimba kwa umahiri,” amesisitiza Prof. Shemdoe.

Prof. Shemdoe amewahakikishia wanafunzi hao kuwa, Serikali itaendelea kuweka mazingira bora ya kuhakikisha vipaji vya wanafunzi vinaibuliwa, vinatambuliwa, vinakuzwa ili kuwanufaisha na kulinufaisha taifa kupitia ushiriki wao katika kuliwakilisha taifa kwenye mashindano ya michezo na Sanaa ndani na nje ya nchi.

Aidha, Prof. Shemdoe ametumia fursa hiyo kumpongeza Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuipa kipaumbele sekta ya elimu, michezo, sanaa na maendeleo ya vijana kwenye ajenda kuu ya taifa na kuongeza kuwa, uwekezaji huo unaendelea kuweka msingi imara wa kuibua na kuendeleza vipaji vya watoto na vijana wa Tanzania.

 Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu - TAMISEMI anayeshughulikia Elimu Bw. Atupele Mwambene amesema kuwa, ushiriki wa wanafunzi katika michezo mbalimbali ya UMITASHUMTA na UMISSETA umeendelea kuwa jukwaa muhimu la kitaifa la kuibua vipaji, kuimarisha afya, kujenga urafiki na kuendeleza umoja wa kitaifa miongoni mwa wanafunzi. 

Naye Mwakilishi wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Bi. Leah Kihimbi amemuhakikishia Prof. Shemdoe kuwa wizara yake itatekeleza ipasavyo jukumu la kuibua kuendeleza vipaji na vipawa vinavyotokana na mashindano hayo ya sanaa na michezo shuleni. 

Mwakilishi wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar ambaye ni Afisa Mdhamini Bw. Mohamed Nassoro Salimu amesema Zanzibar inakwenda kujipanga ili kuleta ushindani mkubwa katika mashindano ya mwakani, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa maelekezo ya Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi ya kufanya mageuzi katika sekta ya michezo.

Akitoa neno la shukrani, Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu - TAMISEMI Bw. Adolf Ndunguru amewashukuru maafisa elimu, wakuu wa shule, walimu, waratibu wa michezo na walezi wa wanafunzi, kwa kazi kubwa walioifanya ya kuwaandaa na kuwaleta wanafunzi katika mashindano ambayo yamewawezesha kujifunza thamani ya nidhamu, ushindani wa haki, uvumilivu, uzalendo na mshikamano wa kitaifa.















NAIBU Waziri wa Madini ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Longido Mkoani Arusha, Dkt Steven Kiruswa amewataka wananchi wa jimbo hilo kujenga umoja  na wananchi wa nchi jirani ya Kenya kwani viongozi wa juu ya nchi hizo wanamahusiano mazuri na hivyo nao wanapaswa kufuata nyayo hizo. 

Kiruswa alisema hayo juzi katika kijiji cha Kimwat kilichopo kata ya Sinonik wilayani Longido ambacho kipo mpakani mwa Kenya wakati akizindua miradi miwili ya maendeleo ikiwemo mradi wa Zahanati na mradi wa maji vyote vikiwa na gharama ya zaidi ya shilingi milioni 188.3 miradi hiyo imetekelezwa kwa mchango wa Mbunge Kiruswa , nguvu za wananchi,shirika lisilo la kiserikali la Pingo's na fedha kutoka serikali kuu.

Alisema kijiji hicho na kata kwa ujumla walikuwa wakipata huduma ya maji ,elimu na afya katika nchi jirani ya Kenya kutokana na mahusiano mazuri waliyajenga na wananchi wa nchi hizo lakini awamu ya sita ya uongozi wa serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan huduma hiyo inapatikana nchini na sasa wananchi wa Kenya wanakuja kupata huduma hizo hapa nchini.

Kiruswa alisema kutokana na uhusiano mzuri na wananchi wa Kenya na Tanzania ndio màana Uzinduzi wa miradi hiyo umehudhuriwa wananchi wa nchini humo wakiongozwa na viongozi wao akiwemo  Afisa Mtendaji Kijiji cha Meto,Peter Milia na Joseph Kink Afisa Mtendaji wa Kata ya Meto.

Alisema mradi wa Zahanati ulianza kujengwa june 2023 na kukamilika mwaka huu yeye binafsi amechangia kiasi cha shilingi milioni 5,michango ya wananchi sh milioni 11 na fedha toka serikali kuu zilipelekwa shilingi milioni 80 na sasa Zahanati hiyo inahudumia wananchi wa Kijiji cha Kimwat na wananchi wa nchi jirani.

Naibu Waziri kiruswa aliipongeza Pingo’s kwa kusimamia na kutoa fedha shilingi milioni 70 ,michango ya wananchi shilingi milioni 2.3 na Mbunge shilingi milioni 20 na kusema kuwa mradi huo utasaidia wananchi na wananchi na mifugo na utekelezaji huo ni kutekeleza ilani ya Chama Cha Mapinduzi(CCM) kufikisha huduma karibu na wananchi.

Naye Mkuu wa wilaya ya Longido ,Salumu Kally amewaomba wananchi wa Longido kumpa ushirikiano Mbunge Kiruswa kwani kiongozi mwenye upendo na wananchi wake na amekuwa mstari wa mbele kuhakikisha huduma zote muhimu ikiwemo miradi ya Maji ,Afya ,elimu ,umeme na Barabara inakamilika kwa maslahi ya wananchi wake hivyo hapasŵi kupotezwa katika uongozi wake.

Naye Afisa Mtendaji wa Kijiji cha Kimwat Rosemary Mbogho wakati akisoma risala kwa mgeni rasmi Kiruswa alisema kijiji kinakabiliwa na changamoto ikiwemo upungufu wa watumishi wa Zahanati,nyumba za watumishi ,madarasa ,barabara na umeme katika vitongoji na Mbunge Kiruswa aliahidi yeye na marafiki zake kujenga nyumba ya watumishi na suala la barabara alimwagiza Meneja wa Wakala wa Barabara Mjini na Vijijini(TARURA) kutekeleza hilo kwani bajeti fedha hizo zipo.