Na Oscar Assenga, Pangani

SERIKALI imeanza rasmi kulipa fidia kwa wananchi 474 wa vijiji vya Mseko na Kigurusimba, Kata ya Masaika, Wilaya ya Pangani mkoani Tanga, kupisha utekelezaji wa mradi mkubwa wa kilimo cha miwa na ujenzi wa kiwanda cha sukari wenye thamani ya dola za Marekani milioni 350.

Hatua hiyo inaashiria mwanzo wa utekelezaji wa moja ya miradi mikubwa ya uwekezaji nchini inayotarajiwa kuzalisha maelfu ya ajira, kuongeza uzalishaji wa sukari na kuchochea ukuaji wa uchumi wa Wilaya ya Pangani na taifa kwa ujumla.

Akizindua rasmi zoezi la ulipaji fidia, Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Dkt. Batilda Burian, alisema Serikali imeanza kuwalipa wananchi wote waliokamilisha taratibu zinazohitajika ili kuondoa vikwazo vya utekelezaji wa mradi huo.

Alisema zaidi ya wananchi 400 tayari wamekamilisha kusaini nyaraka zinazowaruhusu kupokea malipo yao, huku akibainisha kuwa waliojitokeza mapema watapewa kipaumbele na wengine wataendelea kuhudumiwa kadri watakavyokamilisha taratibu.

"Tunataka zoezi hili lifanyike kwa uwazi, haki na kwa wakati. Serikali imejipanga kuhakikisha kila mwananchi aliyestahili analipwa fidia yake bila kuchelewa," alisema Dkt. Burian.

Aidha, aliwataka wananchi kuendelea kushirikiana na mamlaka zinazoratibu zoezi hilo ili kuhakikisha mradi unaanza kwa wakati na kuleta manufaa yaliyokusudiwa kwa jamii na taifa.

Awali, akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalumu ya Kiuchumi Tanzania (TISEZA), Remigius Reverius alisema malipo yanafanyika moja kwa moja kupitia akaunti za benki za wanufaika waliokamilisha uhakiki wa nyaraka zao.

Alisema zoezi hilo limeanza katika Kijiji cha Kigurusimba na litaendelea kwa awamu hadi wananchi wote waliothibitishwa kulipwa fidia watakapopokea stahiki zao.

"Tunawashukuru wananchi kwa ushirikiano wao. Serikali kupitia TISEZA imejipanga kuhakikisha kila aliyefanyiwa tathmini analipwa haki yake. Zoezi hili litaendelea hadi Juni 30 mwaka huu," alisema Reverius.

Aliongeza kuwa wataalamu wanaendelea kuhakiki taarifa za akaunti za benki pamoja na nyaraka mbalimbali ili kuhakikisha malipo yote yanafanyika kwa usahihi na bila dosari.

Mwakilishi wa wakulima wa Kigurusimba, Biligita Batilimeo, alisema kuanza kwa ulipaji wa fidia ni hatua muhimu inayoonyesha dhamira ya Serikali ya kutekeleza mradi huo huku ikilinda maslahi ya wananchi.

Alisema pamoja na fidia, mradi huo unatarajiwa kufungua fursa nyingi za ajira na biashara ambazo zitainua uchumi wa wakazi wa Pangani.

Naye mkazi wa Kigurusimba, Benard Mhagama, aliwasihi wananchi watakaopokea fidia kutumia fedha hizo kwa busara kwa kuwekeza katika shughuli za maendeleo zitakazowanufaisha wao na familia zao kwa muda mrefu.

Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Masaika, George Mariano, alisema uwekezaji huo utabadilisha sura ya uchumi wa Pangani kwa kuongeza ajira, kuchochea shughuli za biashara na kuongeza mapato ya Serikali.

Mradi huo wa kilimo cha miwa na ujenzi wa kiwanda cha sukari unatekelezwa na TISEZA katika eneo la ekari 22,000 kwa gharama ya dola za Marekani milioni 350, na unatarajiwa kuwa miongoni mwa miradi mikubwa itakayochangia kuongeza uzalishaji wa sukari nchini pamoja na kuharakisha maendeleo ya kiuchumi katika Mkoa wa Tanga.

Mwisho.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Deus Sangu akizungumza katika Mkutano Mkuu wa 67 wa Chama cha Waajiri Tanzania (ATE) uliofanyika leo Juni 25, 2026 katika hoteli ta Serena Jijini Dar es Salaam.
Kariakoo, 25 Juni, 2026

Kuelekea maadhimisho ya Tuzo za Rais kwa Walipakodi Bora, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Kariakoo imewapongeza walipakodi kwa mchango wao mkubwa katika ulipaji wa kodi na uzingatiaji wa sheria za kodi, hali iliyowezesha baadhi yao kutambuliwa kama walipakodi bora wa mwaka.

Serikali itaendelea kushirikiana kwa karibu na wawekezaji wa sekta ya viwanda ili kutatua changamoto zinazokwamisha uzalishaji na kuweka mazingira bora yatakayochochea ukuaji wa uchumi wa viwanda nchini.

Kauli hiyo imetolewa  na  Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe.Judith Kapinga mara baada ya kufanya ziara katika kiwanda kikubwa cha kuchakata na kuzalisha mafuta ya kula cha Mainland Group Agro Process Tanzania  jijini Dodoma, ambapo amejionea shughuli mbalimbali za uzalishaji na kiwango cha uwekezaji kilichofanyika katika kiwanda hicho.

Akizungumza baada ya kutembelea mitambo ya uzalishaji, Waziri Kapinga amesema   Serikali inatambua mchango mkubwa wa sekta binafsi katika kukuza uchumi, kuongeza ajira na kuimarisha mapato ya Taifa, hivyo itaendelea kuhakikisha changamoto zinazowakabili wawekezaji zinapatiwa ufumbuzi kwa wakati.

Amesema ameoneshwa kuvutiwa na uwekezaji mkubwa uliofanyika katika kiwanda hicho na kusisitiza kuwa viwanda vya kuongeza thamani ya mazao ya ndani vina nafasi muhimu katika kufanikisha malengo ya maendeleo ya Taifa pamoja na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

“Tunataka kuona mazao yanayozalishwa na wakulima wetu yanaongezewa thamani hapa hapa nchini. Hii ndiyo njia sahihi ya kuongeza tija kwa mkulima, mfanyabiashara, mwekezaji na Serikali kwa ujumla,” amesema Kapinga

Amebainisha kuwa licha ya Tanzania kuwa miongoni mwa wazalishaji wakubwa wa mazao ya mafuta, bado uzalishaji wa mafuta ya kula haujakidhi mahitaji ya ndani, hali inayolazimu nchi kuagiza sehemu ya mafuta kutoka nje.

Kutokana na hali hiyo, amesema Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali ikiwemo maboresho ya sera, sheria na mifumo ya kodi ili kuvutia uwekezaji zaidi katika viwanda vya mafuta ya kula na kuongeza uzalishaji wa ndani.

Waziri huyo amesema Serikali inalenga kuona nchi inafikia kujitosheleza kwa mafuta ya kula katika miaka ijayo kwa kuongeza uzalishaji wa malighafi na kuimarisha uwezo wa viwanda vilivyopo.

Katika mazungumzo yake na viongozi wa kiwanda hicho, ameelezwa kuwa changamoto kubwa inayokikabili ni upatikanaji mdogo wa malighafi, hususan mbegu za mazao ya mafuta, jambo linalofanya kiwanda kufanya kazi chini ya uwezo wake licha ya uwekezaji mkubwa uliowekwa.

Aidha, Serikali imeanza kushirikiana na Wizara ya Kilimo pamoja na taasisi zake kuweka mikakati ya kuongeza uzalishaji wa mazao ya mafuta ili kuhakikisha viwanda vinapata malighafi za kutosha na kutumia uwezo wake kikamilifu.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa kiwanda hicho, Bw. Jiaweli Chen, ameipongeza Serikali ya Tanzania kwa kuendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji na kutoa ushirikiano unaowezesha viwanda kufanya kazi kwa ufanisi na kuchangia maendeleo ya uchumi wa nchi.

Amesema kuwa sera na hatua mbalimbali zinazochukuliwa na Serikali zimeongeza imani kwa wawekezaji, jambo ambalo limechangia ukuaji wa shughuli za uzalishaji na kuongeza ajira kwa wananchi katika maeneo mbalimbali nchini.

Bw. Chen pia ameishukuru Serikali kwa kutembelea mradi huo na kusikiliza changamoto zinazowakabili, akieleza kuwa hatua hiyo inaonesha utayari wa viongozi kushirikiana na sekta binafsi katika kutafuta suluhisho la changamoto zinazojitokeza wakati wa utekelezaji wa shughuli za uzalishaji.

Hatahivyo amesema kuwa kiwanda hicho kitaendelea kushirikiana na Serikali katika kuongeza uzalishaji, kuimarisha ubora wa bidhaa na kuchangia jitihada za taifa za kukuza sekta ya viwanda, huku akieleza matumaini yake kuwa changamoto zilizowasilishwa zitapatiwa ufumbuzi kwa manufaa ya wawekezaji na wananchi kwa ujumla.

 



Na. Josephine Majura, WF, Dodoma

Wizara ya Fedha imezitaka kampuni na taasisi zinazotoa bidhaa na huduma kwa Wizara kuendelea kuzingatia viwango vya ubora, uaminifu, uwazi na masharti ya mikataba ili kuhakikisha Serikali inapata thamani halisi ya fedha katika matumizi ya rasilimali za umma.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa Kikao cha Tathmini ya Mwaka 2025/26 cha Utendaji wa Wazabuni na Watoa Huduma kwa Wizara ya Fedha kilichofanyika katika Ukumbi wa Kambarage, Treasury Square, jijini Dodoma, Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu wa Wizara ya Fedha, Bw. Lusius Mwenda, alisema kuwa Wizara inatarajia kuona maboresho makubwa katika utoaji wa bidhaa na huduma, hususan katika maeneo ya ubora, ufanisi na matumizi ya teknolojia za kidijitali.

Alisema kuwa pamoja na mafanikio yaliyopatikana katika utekelezaji wa mikataba mbalimbali, bado kuna umuhimu wa kuimarisha ushirikiano kati ya Wizara na watoa huduma ili kukabiliana na changamoto zinazojitokeza na kuongeza tija katika utekelezaji wa majukumu ya Serikali.

“Tunatarajia wazabuni na watoa huduma kuendelea kuzingatia viwango vya ubora vilivyokubalika, kuwasilisha bidhaa na huduma kwa wakati, pamoja na kuzingatia maadili ya kitaaluma na taratibu zote za ununuzi wa umma,” alisema Bw. Mwenda.

Aidha, alisisitiza umuhimu wa kujenga na kudumisha uhusiano wa kikazi unaozingatia uaminifu na uwazi, akieleza kuwa misingi hiyo ndiyo msingi wa mafanikio katika utekelezaji wa mikataba ya Serikali.

Wizara pia imeeleza kuwa itaendelea kuweka mazingira rafiki kwa wazabuni na watoa huduma ili kuhakikisha mikataba inatekelezwa kwa ufanisi na changamoto zinazojitokeza zinapatiwa ufumbuzi kwa wakati.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Kitengo cha Ununuzi na Ugavi, Wizara ya Fedha, Bw. Boaz Ntembanda, alisema lengo la kikao hicho ni kufanya tathmini ya utekelezaji wa mikataba ya wazabuni na watoa huduma, kubaini changamoto zilizojitokeza na kuweka mikakati ya pamoja ya kuboresha utoaji wa bidhaa na huduma kwa wakati, kwa ubora unaotakiwa na kwa kuzingatia masharti yaliyokubaliwa.

 

Naye mmoja wa wwaakilishi wa wazabuni wanaotoa huduma Wizara ya Fedha, Bi. Happiness Kategile, aliipongeza Wizara kwa kuwakutanisha pamoja wazabuni na watoa huduma, akisema hatua hiyo imefungua fursa ya kujadiliana kwa uwazi, kubadilishana uzoefu na kuimarisha ushirikiano katika utekelezaji wa mikataba.

Katika kikao hicho, washiriki walipata fursa ya kujadili utekelezaji wa mikataba, ubora wa huduma zilizotolewa, matumizi ya TEHAMA katika mifumo ya ununuzi na ugavi, pamoja na masuala ya mazingira, jamii na utawala bora katika shughuli za ununuzi wa umma.










 

Na: OWM – KAM, Dar es Salaam

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu amewataka waajiri nchini kuzingatia viwango vya kima cha chini cha mshahara vilivyowekwa na Serikali ili kuhakikisha wafanyakazi katika sekta binafsi wanapata stahiki zao kwa mujibu wa sheria hatua itakayosaidia utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050.

Mhe. Sangu ametoa wito huo Juni 25, 2026, wakati akifungua Mkutano Mkuu wa 67 wa Chama cha Waajiri Tanzania (ATE) uliofanyika katika Hoteli ya Serena, jijini Dar es Salaam ambapo amesema ulipaji wa mishahara inayokidhi viwango vya chini vilivyowekwa kisheria ni wajibu wa kila mwajiri ambapo inaongeza motisha kwa wafanyakazi na kuimarisha uzalishaji katika maeneo ya kazi.

Waziri Sangu amesema ili sekta ya kazi kuendelea kuwa na mafanikio ni jambo muhimu kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ili kuhakikisha nguvu kazi ya wafanyakazi inalindwa na wakati huo huo kuhakikisha kuwa mazingira ya biashara yanabaki rafiki, shindani na endelevu.

Amesema Serikali haitasita kuchukua hatua za kisheria dhidi ya waajiri watakaobainika kukiuka masharti ya mishahara kwa kuwalipa wafanyakazi kiwango cha chini ya kile kilichoainishwa katika sheria na kanuni za kazi.

Sambamba na hilo, Waziri Sangu amewataka waajiri wote kuendelea kuzingatia sheria za kazi kwa kuwasilisha kwa wakati michango ya wafanyakazi katika mifuko ya hifadhi ya jamii ikiwemo NSSF, PSSSF pamoja na Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) bila kuchelewa au kukiuka taratibu zilizowekwa.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa kuendeleza mahusiano mazuri kazini kupitia majadiliano na ushirikiano kati ya waajiri na wafanyakazi ili kuimarisha tija, amani na maendeleo katika maeneo ya kazi.

Katika hatua nyingine, Mhe. Sangu amepongeza Chama cha Waajiri Tanzania (ATE) kwa kuingia makubaliano na NSSF akieleza kuwa hatua hiyo itasaidia kuongeza uelewa na uzingatiaji wa sheria za kazi, hususan katika masuala ya kinga ya jamii, mishahara na utoaji wa ajira zenye staha.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama cha Waajiri Tanzania (ATE), Bw. Oscar Mgaya amesema mkakati mpya wa miaka mitano wa chama hicho unalenga kuimarisha uwezo wa waajiri kuboresha huduma kwa wanachama na kuongeza mchango wa sekta binafsi katika maendeleo ya taifa ili kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

“Waajiri ni nguzo muhimu katika kukuza uchumi, kuongeza ajira zenye staha na kuchangia mapato ya Serikali, hivyo ushirikiano kati ya Serikali, Waajiri na Wafanyakazi utaendelea kuimarishwa kupitia majadiliano ya kijamii yenye tija ili kutatua changamoto za maeneo ya kazi kwa wakati,” amesema Mgaya.

Naye Katibu Mkuu wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA), Bw. Hery Mkunda amesema TUCTA na ATE zimeendelea kushirikiana katika kutekeleza miradi mbalimbali yenye lengo la kuongeza tija kwa wafanyakazi na waajiri.

Miongoni mwa miradi hiyo ni programu za ukuzaji ujuzi na uanzishwaji wa kituo kinachotoa taarifa sahihi na huduma kwa Watanzania wanaokwenda kufanya kazi nje ya nchi pamoja na raia wa kigeni wanaokuja kufanya kazi nchini.

Mkunda amewakumbusha waajiri kuendelea kuimarisha ushirikiano na wafanyakazi kwa kuwashirikisha katika masuala ya maeneo ya kazi na kuondoa dhana kwamba wafanyakazi ni wapinzani wa waajiri.

Katika hatua nyingine Mkurugenzi wa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) Bw. Masha Mshomba akizungumza mara baada ya kusaini hati ya makubaliano ya ushirikiano wa taasisi yake na ATE amesema utaongeza wigo mpana wa kufanikisha shughuli za NSSF ikiwa ni mkakati wa kuanza kutekeleza Dira ya 2050 kupitia wigo wa hifadhi ya jamii.