
IMEELEZWA kuwa uwepo wa Jukwaa la Wanawake na Kodi ni hatua muhimu inayodhihirisha dhamira ya kuendeleza usawa wa kijinsia na kukuza uchumi shirikishi nchini.
Akizungumza wakati akifungua Jukwaa hilo Meneja wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Tanga, CPA Castro John, alisema ni dhamira ya dhati ya kujenga mfumo wa kodi unaoshirikisha makundi yote ya jamii, hususan wanawake ambao ni nguzo muhimu ya uchumi wa Taifa.

Alisema takwimu zinaonesha wanawake wanachangia kwa kiwango kikubwa katika shughuli mbalimbali za kiuchumi zikiwemo biashara ndogondogo, kilimo, huduma, viwanda vidogo pamoja na biashara za kati na kubwa.
Kwa mujibu wa takwimu za mwaka 2024/2025, wanawake nchini, wakiwemo wa Mkoa wa Tanga, wanakadiriwa kushiriki katika nguvu kazi kwa asilimia 80, huku wakimiliki asilimia 54 ya biashara ndogo, za kati na kubwa.
“Bila ushiriki wa wanawake, juhudi za kuongeza wigo wa walipa kodi na kuongeza mapato ya ndani haziwezi kufikia malengo yaliyokusudiwa,” alisema CPA Castro John.
Alifafanua kuwa TRA imeanzisha Jukwaa hilo maalumu kwa lengo la kutoa elimu sahihi ya kodi, kusikiliza changamoto za wanawake wafanyabiashara, kujenga ushirikiano wa karibu pamoja na kuhamasisha ulipaji wa kodi kwa hiari na kwa wakati.
Aidha, alisema TRA imejikita katika kuboresha huduma kwa kuzingatia ushirikishwaji, uwazi, weledi na urahisi wa upatikanaji wa huduma. Aliongeza kuwa elimu ya kodi na mahusiano bora ni msingi muhimu wa kuongeza utii wa kodi.
Kupitia jukwaa hilo, wanawake watapata nafasi ya kupata ushauri kuhusu masuala ya kodi, kujifunza fursa mbalimbali pamoja na kuelewa wajibu wao wa kikodi.
“Tunataka mwanamke ajisikie salama, aheshimiwe na ashiriki kikamilifu katika mfumo wa kodi bila hofu wala kikwazo chochote,” alisema.
CPA Castro John alisisitiza kuwa kodi ndiyo injini ya maendeleo ya Taifa kwani mapato yake yanagharamia huduma muhimu kama elimu, afya, barabara, maji safi na miradi mingine ya kimkakati.
“Kila mwanamke anayelipa kodi anakuwa mshirika wa moja kwa moja wa Serikali katika kujenga Tanzania yenye uchumi imara na huduma bora kwa wananchi wake,” aliongeza.
Pia aliwataka wanawake kutumia jukwaa hilo kujifunza, kuuliza maswali na kuwa mabalozi wa utamaduni wa kulipa kodi katika jamii zao.
Aidha, aliwataka wadau wa sekta mbalimbali pamoja na taasisi za kifedha kuendelea kushirikiana na TRA katika kuwawezesha wanawake kukuza biashara zao kwa kuzingatia misingi ya kikodi.
Kwa upande mwingine, aliwahimiza wanawake wafanyabiashara kujisajili katika mfumo wa kodi na kutekeleza wajibu wao kwa hiari na kwa wakati.
“Kulipa kodi si wajibu wa kisheria tu, bali ni mchango wa moja kwa moja katika kujenga Taifa. Wanawake wakisimama kiuchumi, familia na jamii vinaimarika,” alisema.
Katika hatua nyingine, alisisitiza umuhimu wa kutumia mipaka rasmi ya biashara kwa wafanyabiashara wanaovuka mipaka kupitia maeneo ya Horohoro na Pangani, huku akiwataka kuachana na biashara za magendo na matumizi ya njia zisizo rasmi.
Naye Naibu Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Wafanyabiashara nchini, JW Ismail Masound, alisema jukwaa hilo lina umuhimu mkubwa kutokana na malengo ya Dira ya Taifa ya mwaka 2050 ambapo sekta binafsi inatarajiwa kuwa mhimili mkubwa wa ukuaji wa uchumi.
Alisema majukwaa hayo yanasaidia kuwawezesha wanawake na wafanyabiashara kufikia malengo ya maendeleo ya Taifa kwa kuongeza ushiriki wao katika shughuli za kiuchumi.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Jukwaa la Wanawake Mkoa wa Tanga (TWCC), Aziza Ramadhani, alisema jukwaa hilo litawasaidia wanawake kuelewa umuhimu wa kulipa kodi katika kukuza uchumi wa Mkoa wa Tanga na Taifa kwa ujumla.
“Hivyo ni wajibu wetu kuhakikisha Mkoa wa Tanga unalipa kodi kutokana na umuhimu wake kwa maendeleo ya jamii,” alisema.
Aliongeza kuwa jukumu la jukwaa hilo ni kuwaunganisha wanawake wa Mkoa wa Tanga ili kuwapa nafasi ya kujifunza, kushirikiana na kupata fursa mbalimbali za kiuchumi ndani na nje ya mkoa huo.
Aidha, alisema wamekuwa wakitoa mafunzo mbalimbali ikiwemo kuanzisha mashamba darasa kwa vijana wa kiume na wa kike, huku akiwakaribisha wanawake wajasiriamali kushiriki katika shughuli za maendeleo zinazochangia ukuaji wa uchumi wa Mkoa wa Tanga na Taifa kwa ujumla.
Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Mhe. Kanal Donald Msengi, amewashauri Viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuwahimiza wakulima kutumia Mfumo wa Stakabadhi za Ghala ili kuleta mabadiliko chanya kiuchumi na kuongeza tija katika uzalishaji wa mazao.
Akizungumza wakati wa Mafunzo ya Mfumo wa Stakabadhi za Ghala kwa Viongozi wa Chama na Serikali kutoka mkoa wa Dodoma yaliyofanyika mkoani Mtwara, Kanal Msengi amesema mfumo huo umeleta mafanikio makubwa kwa vyama vya ushirika mkoani humo kwa kuviwezesha kuwa imara kiuchumi. Ameeleza kuwa kupitia mfumo huo, vyama vimefanikiwa kufanya uwekezaji mbalimbali ikiwemo ujenzi wa maghala, ununuzi wa magari, uanzishaji wa viwanda pamoja na kuchangia huduma za kijamii kama elimu, afya na maji.
“Ni muhimu viongozi mkatumia nafasi zenu kuwahamasisha wakulima na wanaushirika kutumia mfumo huu, kwani umeleta manufaa makubwa na una uwezo wa kuleta mageuzi chanya kwa sekta ya kilimo,” amesema Kanal Msengi.
Naye Kaimu Mrajis Msaidizi wa Mkoa wa Mtwara, Robert Nzunza, amebainisha hatua muhimu za mchakato wa stakabadhi za ghala kuwa ni pamoja na maandalizi ya msimu wa mauzo, ukusanyaji wa mazao ghalani, usafirishaji wa mazao kwenda ghala kuu, mapokezi ya mazao, mauzo kupitia minada ya mtandao, malipo ya fedha kupitia vyama vikuu (Unions), malipo kwa wakulima na wadau, pamoja na utoaji wa mizigo ghalani.
Kwa upande wake Mkuu wa msafara huo ambaye pia ni Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa kutoka mkoa wa Dodoma, Donald Mejetii, amesema kuwa mafunzo hayo yatawasaidia kuwajengea uwezo viongozi hao ili waweze kuwahamasisha wakulima wa Dodoma kutumia mfumo huo kwa tija zaidi.
Viongozi wa Chama na Serikali kutoka mkoa wa Dodoma wapo mkoani Mtwara kwa ziara ya kujifunza Mfumo wa Stakabadhi za Ghala katika vyama vya ushirika na namna unavyoweza kuinua kipato cha mkulima. Katika ziara hiyo pia wametembelea Chama Kikuu cha Ushirika cha MAMCU LTD pamoja na Chama cha Msingi Mayanga AMCOS.

📌Mhandisi Mramba afanya mazungumzo na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Mafuta Kenya
Tanzania na Kenya zimekubaliana kuharakisha utekelezaji wa miradi mbalimbali ya njia za umeme zinazounganisha gridi za nchi hizo mbili pamoja na kuboresha mifumo ya usafirishaji wa umeme ili kuimarisha usalama wa nishati, kuongeza uhakika wa upatikanaji wa umeme na kukuza biashara ya umeme katika ukanda wa Afrika Mashariki.
Makubaliano hayo yamefikiwa baada ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Felchesmi Mramba, kufanya mazungumzo na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Mafuta wa Kenya, Bw. Alex Wachira, jijini Nairobi, Kenya.
Mazungumzo hayo yalijikita katika kuimarisha ushirikiano katika sekta ndogo ya umeme na nishati jadidifu, hususan biashara ya umeme, utekelezaji wa miradi ya uunganishaji wa gridi za umeme pamoja na maboresho ya mifumo ya usafirishaji na usambazaji wa umeme kati ya Tanzania na Kenya.
Viongozi hao pia walijadili hatua mbalimbali za kuimarisha biashara ya umeme katika ukanda wa Afrika Mashariki kupitia Umoja wa Soko la pamoja la Kuuziana Umeme na Kuimarisha Mifumo ya Gridi-Eastern Africa Power Pool (EAPP).
Sambamba na hilo, Makatibu Wakuu hao walisisitiza umuhimu wa kuongeza wigo wa njia za usafirishaji umeme zitakazounganisha nchi hizo mbili kupitia maeneo ya Namanga, Lungalunga, Loitoktok na Isibania/Sirari.
Aidha, kikao hicho kilijadili pendekezo la kuanzishwa kwa mfumo wa Ring Circuit utakaojumuisha njia za Ibadakuli – Masaka, Ibadakuli – Kilgoris na Kilgoris – Masaka kwa lengo la kuongeza uthabiti wa gridi za umeme na kuimarisha biashara ya umeme kati ya Tanzania na Kenya.
Katika hatua nyingine, Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Mafuta wa Kenya, Bw. Alex Wachira alieleza kuwa nchi hiyo imejipanga pia katika uwekezaji wa miundombinu ya gesi asilia kwa lengo la kuimarisha upatikanaji wa nishati hiyo nchini humo, pia kuongeza ushirikiano wa kikanda katika sekta ya nishati.
Aidha, Kenya ilieleza uzoefu wake katika biashara ya umeme wa kikanda, ikibainisha kuwa inaendelea kupokea umeme kutoka Ethiopia kupitia mikataba ya biashara ya umeme ya kikanda, ambapo kiwango cha umeme hupungua na kuongezeka kulingana na mahitaji, huku kikifikia takriban megawati 100 katika vipindi vya kawaida.
Hatua hiyo imeelezwa kusaidia kuimarisha uthabiti wa mfumo wa umeme nchini Kenya.
Kikao hicho kilihudhuriwa na viongozi na wataalam mbalimbali kutoka Wizara za Nishati za Tanzania na Kenya pamoja na taasisi za sekta ya umeme zikiwemo TANESCO, KETRACO na KPLC.
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo imeipongeza Wizara ya Viwanda na Biashara pamoja na taasisi zake kwa utekelezaji mzuri wa majukumu yake, huku ikizitaka kuongeza kasi ya utekelezaji wa mikakati ya kukuza uchumi wa taifa.
Pongezi hizo zimetolewa jijini Dodoma na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Deodatus Mwanyika (picha ya kwanza), wakati wa kikao cha tathmini ya utekelezaji wa shughuli za wizara kupitia taasisi zake ambazo ni Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Tume ya Ushindani Tanzania (FCC), Wakala wa Vipimo (WMA) na Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA). Mwanyika amesema juhudi zinazofanywa na wizara hiyo zimeanza kuleta matokeo chanya katika kuimarisha mazingira ya biashara na uzalishaji nchini. Aidha, ameielekeza wizara kuongeza nguvu katika mapambano dhidi ya bidhaa bandia na hafifu zinazoingia sokoni, akieleza kuwa bidhaa hizo husababisha hasara kwa wazalishaji wa ndani na kuhatarisha afya pamoja na usalama wa watumiaji. Pia ameagiza hatua kali kuchukuliwa dhidi ya matumizi ya vipimo visivyo sahihi katika biashara, hususan lumbesa, ambalo limekuwa likilalamikiwa na wananchi katika maeneo mbalimbali nchini kutokana na matumizi ya vipimo visivyo rasmi. Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Dennis Londo, amesema wizara imepokea maelekezo na ushauri uliotolewa na kamati hiyo na kuahidi kuyafanyia kazi kwa lengo la kuboresha huduma na kuongeza ufanisi katika sekta ya viwanda na biashara nchini. Naye Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Ashura Katunzi, pamoja na viongozi wengine wa taasisi zilizo chini ya wizara hiyo, wamesema wanaendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuimarisha usimamizi wa bidhaa na huduma nchini. Hatua hizo ni pamoja na kufanya operesheni maalumu za ukaguzi wa bidhaa bandia na kutoa elimu kwa wafanyabiashara kuhusu matumizi sahihi ya vipimo vinavyotambulika kisheria.

Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) kimeendelea kutoa mafunzo kupitia kozi ndefu 49 zinazolenga kuzalisha wataalam mahiri watakaosaidia utekelezaji wa miradi mikubwa ya maendeleo inayotekelezwa na Serikali nchini.
Serikali ya Tanzania ndani ya kipindi cha Miezi Mitatu ijayo inatarajiwa kuanza rasmi utekelezaji wa Mradi wa Kimkakati wa Liganga na Mchuchuma wenye uwekezaji wa Dola za Marekani Bilioni 2 hadi 3 baada ya mazungumzo kati ya Serikali na Mwekezaji kufikia zaidi ya asilimia 90.
Hayo yalibainishwa Mei 9, 2026 na Msemaji Mkuu wa Serikali ambaye pia ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Gerson Msigwa, wakati akizungumza na Waandishi wa Habari katika Shamba la Parachichi la Havira Farm Mkoani Njombe, pembeni mwa Kikao Kazi cha 21 cha Maafisa Habari, Mawasiliano, Itifaki na Uhusiano Serikalini, kinachotumika kama sehemu ya tathmini na kujipanga.
Alisema hatua hiyo inaashiria mwanzo wa utekelezaji wa mradi huo uliosubiriwa kwa miaka mingi ukitarajiwa kuongeza mapato ya Seikali, ajira kwa wananchi, kukuza sekta ya viwanda vya chuma na ustawi wa jamii inayozunguka mradi na taifa.
Aliongeza kwamba, mradi huo unatarajiwa kuzalisha tani milioni 2.9 za chuma ghafi kwa mwaka pamoja na tani milioni 1.1 za bidhaa za chuma kwa mwaka, huku ukitarajiwa kutoa zaidi ya ajira rasmi 6,500 na ajira zisizo rasmi zipatazo 26,000
‘’ Katika kipindi cha miaka 25 ya kwanza ya mradi, jumla ya mapato ya dola za Marekani 1,990,489,585,000 zinatarajiwa kupatikana ambapo kwenye miradi ya makaa ya mawe kiasi cha dola za Marekani 92,593,820; uchimbaji chuma kiasi cha dola za Marekani 910,781,519 na kiwanda cha chuma kiasi cha dola za Marekani 987,114,246,’’ alisema Msigwa.
Pia, aliongeza kwamba utekelezaji wa mradi huo utahusisha ujenzi wa msongo wa umeme wa Kilovoti 220 kati ya mchuchuma na na liganga na barabara kutoka Mchuchuma na Liganga ukiwemo mgodi wa makaa ya mawe mchuchuma wenye uwezo wa kuzalisha tani milioni 3 kwa mwaka na Kituo cha kufua umeme kwa megawati 600.
Msigwa alisema tayari Serikali imelipa zaidi ya shilingi bilioni 15 za fidia kwa wananchi ili kupisha utekelezaji wa mradi huo, hatua inayoonesha dhamira ya Serikali kuhakikisha mradi huo unaanza kwa vitendo baada ya kusubiriwa kwa muda mrefu.
Utekelezaji wa mradi wa Liganga na Mchuchuma unaashiria safari ya kuelekea Dira 2050 ambapo kupitia Sekta ya Madini imejipanga kufikia Uchumi wa Dola trilioni Moja ukiwa ni miongoni mwa miradi kielelezo iliyoanishwa kwenye mpango wa muda mrefu wa wa dira hiyo unaotarajiwa kuchochea sekta ya viwanda nchini.
Mbali na Sekta ya Madini, alisema Serikali inaendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo mkoani Njombe ikiwemo barabara, maji na umeme kwa lengo la kuufungua zaidi mkoa huo kiuchumi na kijamii.
#LigangaMchuchuma #Madini ni Maishana Utajiri #TanzaniaSteelHub
#NjombeMpya #SafariyaViwanda #InvestInTanzania #MiningSector
#Mining4Development #MineralForGrowth



