Serikali kupitia Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC) imeendelea kuimarisha usimamizi wa matumizi salama ya mionzi nchini kwa kufanya ziara maalum katika Kanda ya Ziwa. Ziara hiyo, iliyohusisha Bodi na Menejimenti ya TAEC, ililenga kukagua na kujionea utendaji kazi wa ofisi zake zilizopo Uwanja wa Ndege wa Mwanza, Bandari ya Mwanza, Ofisi ya TAEC Nyegezi pamoja na Ofisi ya TAEC Sirari.

Katika hatua ya kwanza, wajumbe wa Bodi na Menejimenti walitembelea Uwanja wa Ndege wa Mwanza na kufanya mazungumzo na Meneja wa Uwanja wa Ndege Kanda ya Ziwa, Bi. Rose Comino. Alieleza namna TAEC inavyoshirikiana na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege katika ukaguzi wa mashine za kukagulia mizigo (Baggage Scanners) na kutoa elimu juu ya matumizi sahihi ya mashine hizo. Bi. Comino alibainisha kuwa mashine zote zinazotumika kwa ukaguzi wa mizigo zimekidhi matakwa ya kisheria kwa kupata vibali kutoka TAEC. Aidha, alieleza kuwa ujenzi mkubwa unaoendelea kiwanjani utakapokamilika, mashine za ziada za ukaguzi wa mizigo zitafungwa ili kuboresha zaidi huduma kwa abiria.

Mwenyekiti wa Bodi ya TAEC, Profesa Joseph Msambishaka, alisisitiza kuwa lengo la ziara hiyo ni kuimarisha ushirikiano na kuboresha utekelezaji wa majukumu ya pamoja. Mkurugenzi Mkuu wa TAEC, Profesa Najat Kassim Mohammed, alitoa shukrani kwa mapokezi mazuri na kusisitiza kuwa ushirikiano mzuri uliopo ni chachu ya mafanikio ya utekelezaji wa majukumu ya kisheria ya TAEC.

Afisa Ukaguzi wa Mionzi wa TAEC, Bw. Stephani Kapama, alieleza kuwa ofisi hiyo hukusanya wastani wa sampuli 30 kila mwezi kutoka shehena za mizigo na kuzifanyia vipimo ili kubaini uwepo wa mionzi. Pia hufanya ukaguzi wa mionzi kila siku katika maeneo yenye shughuli nyingi za binadamu: eneo la kuhifadhia mizigo, eneo la abiria wanaowasili na eneo la abiria wanaoondoka. Aliongeza kuwa muda wa kuchakata vibali vya mionzi umepungua kutoka siku saba hadi siku moja pekee, hatua iliyoongeza ufanisi wa usafirishaji wa bidhaa na huduma.

Bodi na Menejimenti waliendelea na ziara kwa kuonana na Meneja wa Bandari Kanda ya Ziwa, Bi. Rosemary Ndesamburo. Alieleza namna bandari inavyoshirikiana na TAEC hususani katika ukaguzi wa mashine za midaki zinazotumika kukagua mizigo. TAEC hukagua mashine hizo na kutoa vibali vya matumizi yake kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu za matumizi salama ya mionzi. Mamlaka ya Bandari Kanda ya Ziwa inasimamia jumla ya bandari saba ambazo ni Mwanza South, Mwanza North, Nansio (Ukerewe), Kemondo Bay, Bukoba, Musoma na Kisorya.

Bandari hizi ni kiungo muhimu cha usafirishaji wa abiria na mizigo ndani ya Ziwa Victoria na zinashirikiana kwa karibu na TAEC kuhakikisha usalama wa matumizi ya teknolojia ya mionzi.

Bodi na Menejimenti walitembelea pia ofisi ya TAEC iliyopo Nyegezi na kujionea utekelezaji wa kazi mbalimbali zinazotolewa na ofisi ya kanda katika kuhudumia wananchi wa Kanda ya Ziwa. Msimamizi wa Ofisi ya Kanda, Dkt. Suleiman Ameir Suleiman, alieleza kuwa ofisi hiyo hufanya kazi za kila siku ikiwemo utoaji wa elimu kwa shule na jamii juu ya matumizi salama ya teknolojia ya nyuklia, ukaguzi wa vituo vinavyomiliki vyanzo vya mionzi, upimaji wa mionzi kwenye bidhaa za vyakula vinavyoingia na kutoka ndani ya kanda, upimaji wa viasili vya mionzi kwenye mazingira pamoja na utafutaji wa vyanzo vya mionzi vilivyopotea.

Ziara ya Bodi na Menejimenti ya TAEC katika Kanda ya Ziwa ilihitimishwa kwa kutembelea mpaka wa Sirari, ambapo wajumbe walikutana na viongozi kutoka taasisi mbalimbali za serikali zinazoshirikiana katika kutoa huduma kwa ufanisi mpakani hapo. Afisa Mkuu wa Forodha wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Bw. Godfrey Leonard, aliyemuwakilisha Meneja Msaidizi wa TRA Sirari, alieleza namna taasisi zote zilizopo mpakani zinavyoshirikiana kwa karibu kuhakikisha huduma zinatolewa kwa haraka na kwa ufanisi.

Taasisi zinazoshirikiana Sirari ni pamoja na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Jeshi la Polisi Tanzania, Jeshi la Wananchi wa Tanzania (TPDF), Ofisi ya Rais, Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC), Wakala wa Vipimo, Wizara ya Madini, Jeshi la Wanyamapori, Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Mamlaka ya Afya ya Mimea na Viuatilifu Tanzania (TPHPA), Mamlaka ya Usafirishaji wa Nchi Kavu (SUMATRA), Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA), Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania (TAEC), Idara ya Uhamiaji Tanzania na Tanzania Bureau of Standards (TBS).

Mwenyekiti wa Bodi ya TAEC, Profesa Joseph Msambishaka, alieleza kuwa ziara hiyo ililenga kufika mpaka wa Sirari ili wajumbe wapya wa Bodi waweze kufahamu kwa undani namna TAEC inavyotekeleza majukumu yake katika eneo hilo. Alisisitiza kuwa ni busara Bodi kujionea kwa macho yake jinsi kazi za ukaguzi wa mionzi zinavyofanyika mpakani, hususan katika shehena za mizigo, ili kubaini uwepo wa uchafuzi wa mionzi au kuzuia usafirishaji holela wa vyanzo vya mionzi.

Bodi ilipata maelezo kutoka kwa Mkaguzi wa Mionzi wa TAEC, Bw. Kasoga, ambaye alieleza namna ofisi ya TAEC mpakani hapo inavyotekeleza majukumu yake ya kila siku katika kuhakikisha taratibu zote zinafuatwa kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu za matumizi salama ya mionzi. Aidha, wajumbe walitembelea maabara ya TAEC Sirari na kupata maelezo juu ya namna inavyotumika katika ukaguzi wa sampuli za bidhaa mbalimbali, na kujionea vifaa na teknolojia zinazotumika kupima viwango vya mionzi.

Ziara hii imekuwa chachu ya mafanikio kwa wajumbe wa Bodi ya TAEC kujionea kwa karibu utekelezaji wa majukumu ya Tume katika maeneo nyeti ya mipaka, viwanja vya ndege na bandari. Hatua hii imeimarisha ushirikiano wa taasisi za serikali katika kuhakikisha usalama wa wananchi dhidi ya mionzi na kuendeleza matumizi salama ya teknolojia ya nyuklia nchini. Mafanikio haya ni kielelezo cha dira ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye ameendelea kusimamia kwa maono makubwa na uongozi thabiti juhudi za kulinda afya na usalama wa Watanzania. Kupitia msisitizo wake wa kuimarisha taasisi za kitaifa na kuhimiza matumizi ya sayansi na teknolojia kwa maendeleo endelevu, taifa linaendelea kujengeka katika misingi imara ya usalama, uchumi na ustawi wa wananchi.



 


Na OWM - TAMISEMI, Dodoma

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu Mhe. Selemani Kakoso ameipongeza Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini (TARURA) kwa kujenga miundombinu ya barabara iliyookoa maisha ya wananchi katika maeneo mbalimbali ambayo awali kuharibika kwa miundombinu hiyo kulisababisha vifo vya wananchi.

Mhe. Kakoso amesema hayo leo Februari 11, 2026 wakati wa kikao cha mafunzo kwa wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu, yaliyohusu uboreshaji wa Mtandao wa Barabara za Wilaya, Mikakati, Changamoto na Fursa kwa Maendeleo ya Taifa yaliyofanyika katika Ukumbi wa Anne Makinda Bungeni Jijini Dodoma.

Mhe. Kakoso amesema kuwa, katika jimbo lake kuna eneo ambalo TARURA imejenga daraja ambapo kila mwaka wananchi walikuwa wakipoteza maisha kutokana na kukosekana kwa daraja la uhakika, lakini tangu daraja hilo lijengwe hakuna taarifa za vifo tena.

“Katika Jimbo langu kuna sehemu ambayo toka nchi ipate uhuru haijawahi kuwa na barabara lakini TARURA imejenga barabara katika eneo hilo na sasa wananchi wananufaika nayo,” ameeleza Mhe. Kakoso.

Naye, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Florent Kyombo amesema licha ya Serikali kufanya vizuri katika ujenzi wa miundombinu ya barabara katika majiji, ameishauri TARURA kufanya mgao mzuri wa rasilimali fedha ili na maeneo mengine yenye uhitaji yanufaike na ujenzi wa miundombinu hiyo ya barabara.

Kwa upande wake, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu -TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amewahakikishia wajumbe wa kamati hizo kuwa, maoni yote yaliyowasilishwa na wajumbe wa kamati hizo yamepookelewa na yatafanyiwa kazi na wataalam ili kuongeza ufanisi katika ujenzi wa miundombinu ya barabara na hatimaye wananchi kunufaika na miundombinu hiyo.

Katika kukabiliana na majanga, Mtendeji Mkuu wa TARURA Mhandisi Victor Seff amesema kupitia dirisha la majanga (Crisis Management Window) Tanzania imeidhinishiwa mkopo wa nyongeza wa Dola za Kimarekani Milioni 100  kwa ajili ya kurejesha miundombinu iliyoharibiwa na mvua za elnino na kimbunga hidaya cha mwaka 2024, ambapo Dola Milioni 30 ni kwa ajili ya barabara za wilaya na Dola Milioni 70 ni kwa ajili ya barabara za kitaifa.












Na Munir Shemweta, WANMM ARUSHA

 

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo amewasisitiza wananchi wenye maeneo ya ardhi, kuhakikisha wanayaendeleza kabla serikali haijaanza kuchukua hatua.

 

Dkt. Akwilapo ametoa kauli hiyo leo tarehe 11 Februari 2026 wakati akifungua Kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) kinachoendelea jijini Arusha.

 

Akwilapo amesema kumekuwa na tabia kwa baadhi ya wananchi kununua maeneo ya ardhi na kuyahifadhi kwa muda mrefu kama mtaji kwa lengo la kupata faida baadaye.

 

"Bado natafakari  nifanye nini maana sheria ipo, usipoendeleza eneo lako ndani ya miaka mitatu unaweza kunyang'anywa na wengi wanafanya ardhi kama mtaji. Nadhani kuna taasisi maalum za kukuza mitaji, kama vile Soko la Hisa la Dar es Salaa na UTT-AMIS, tumieni hizo taasisi. Huku ardhi tutapishana maneno". Amesema Dkt Akwilapo.

 

Sheria ya Ardhi Sura Namba 113 kifungu cha 49 inaeleza wazi kuwa mmiliki wa ardhi asiyeendeleza eneo lake katika kipindi cha miaka mitatu serikali inaweza kulichukua eneo lake kutokana na kushindwa kuliendeleza.

 

Kupitia kikao hicho cha Baraza la wafanyakazi, Mhe. Dkt Akwilapo amewataka waendelezaji milki nchini  likiwemo Shirika la Nyumba la Taifa, kuhakikisha wananchi wanapata nyumba bora na za gharama nafuu ili watanzania waweze kuwa na tabasamu.

 

Amewaasa watumishi wa NHC kuzingatia utu, maadili, uwazi na uaminifu wakati wote wa kutekeleza majukumu yao huku wakiachana na ile dhana ya kuuliza watapata kitu gani ndani ya shirika na badala yake wajiulize watalifanyia nini shirika hilo.

 

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Baraza la wafanyakazi la NHC ambaye pia ndiye Mkurugenzi Mkuu wa Shirika hilo, Bw. Hamad Abdallah amesema shirika lake limekuwa likifanya jitihada mbalimbali za kuhakikisha linaboresha maslahi ya watumishi. 

 

Kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi cha Shirika la Nyumba la Taifa kilichoanza leo tarehe 11 Februari 2026 kinatarajiwa kuhitimishwa Alhamisi tarehe 12 Februari 2026. Kikao hicho pamoja na mambo mengine kinajadili Mizania na Bajeti ya NHC kwa mwaka wa fedha 2026/2027.










Katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha, Dk. Toba Alnason Nguvila, amewasistiza watumishi wa Umma kufanya kazi kwa kufuata Sheria, taratibu na kanuni kwa kuzingatia kiwango cha juu cha Maadili ya Utumishi wa Umma, ili kufikia lengo la Serikali la kuwahudumia wananchi.

Dkt.Nguvila ametoa wito huo, wakati akizungumza na baadhi ya watumishi wa Umma mkoa wa Arusha, kwenye hafla fupi ya mapokezi yake, iliyofanyika kwenye ukumbi wa Mikutano Ofisi ya Mkuu wa Mkoa huo, leo Februari 10, 2026, muda mfupi baada ya kupokelewa ofisini hapo, tayari kwa kuanza kutekeleza majukumu yake kwa washifa huo.

Amewasisitiza watumishi hao, kila mmoja kwa nafasi yake kuzingatia kuwa, mkoa huo ni mkoa wa Utalii hivyo wanalo jukumu la kuhakikisha wadau wa utalii wanafanya kazi kwenye mazingira rafiki, yasiyo na vikwazo vya aina yoyote huku akisisitiza kuto kuvumilia vikwazo vya kiutendaji wala urasimu unaokwamisha wawekezaji katika sekta ya utalii. 

"Sisi watalamu tunapaswa kuwa kichocheo cha kuiimarisha sekta ya utalii, kwa kuwa kila wilaya ina vivutio vyake, hivyo si busara kwa baadhi ya watendaji kuweka urasimu usio wa lazima unaoweza kudhoofisha sekta hiyo, sitavumilia urasimu wala migogoro inayokwamisha wawekezaji katika sekta ya utalii". Amesema Dkt.Nguvila

Aidha, amewaagiza Wakurugenzi wa Halmashauri zote, kutenga bajeti ya kutekeleza shughuli za utalii kwenye maeneo yao, kubuni vyanzo vya mapato pamoja na kusimamia ukusanyaji wa mapato, ikiwa ni pamoja na kutoka maofisini na kuwafuata wananchi ili kubaini changamoto zao na kuzitatua kwa haraka.

Katika kutekeleza maelekezo ya Serikali, Dkt.Nguvila ameataka viongozi hao, kuwa na kampeni maalumu ya kutoa elimu na usajili sambamba na kuhamasisha wananchi kujiunga na mpango wa Bima ya Afya kwa wote, ili ili kufikia lengo la Serikali ya awamu ya sita ya kila mwananchi kujiunga na Bima hiyo, itakayowawezesha kupata huduma za matibabu wanapougua.

Awali, Dkt.Nguvila amemshukuru Mhe.Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kumuanini na kumteua kuwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha na ameahidi kushirikiana na watalamu wa ngazi zote katika kuwahudumi wananchi.

















Na Oscar Assenga,MUHEZA

MKURUGENZI Bonde la Maji la Pangani Segule Segule amewaonya watu ambao wanao kuchukua maji chini ya ardhi,juu ya ardhi bila kufuata utaratibu uliowekwa kisheria ikiwemo kuwa vibali kuacha mara moja kwani wakiwafikia watawakamata.

Segule aliyasema hayo wakati wa Mkutano Mkuu wa Uchaguzi wa Jumuiya ya Maji Mto Zigi uliofanyika mjini Muheza ambapo alisema iwe mtu binafasi au taasisi huku akiwashauri wafuate utaratibu na kuchukua vibali na vibali vyao vinawaeleza kitu gani wanapaswa kufanya.

Aliwaeleza wadau wa Jumuiya hiyo kuwa Bonde la Mto Pangani linasimamia vyanzo vilivyopo chini ya ardhi kupitia visima na katika eneo hilo watu wengi hawana ufahamu au wengine wanaelewa lakini hawafuati utaratibu uliowekwa

Aidha alisema watu hawana ufahamu wa kutosha katika eneo la visima kwamba ukipewa ridhaa na Mkurugenzi wa Halmshauri ukipewa hatia na Wizara ya Ardhi juu ya kutumia ardhi na unaporaka kutumia rasilimali maji lazima upate kibali kutoka kwenye Bonde husika na katika Kanda ya Kaskazini anayetaka kutimia maji kutoka chini ya ardhi lazima apate kibali kuyoka Bonde la Pangani.

Aidha alisema kwamba Serikali imefanya kwa nia njema na sio kuweka ugumu watu wasitumie lakini wasiposimamiana katika hilo ipo siku maji yote yatachafuliwa na yanaweza yasiwepo.

Alieleza kwamba wao hawatoi vibali pekee bali wanaratibu wachimbaji kujua wana utaalamu wa kutosha wanaanza kuratibu kwenye utafiti huyo anayefanya utafiti je ana taaluma hiyo mpaka wanapotoa kibali cha kuchimbiwa visima wanauhakika wanakuwa ni watu sahihi wanaotumia utaalamu sahihi hivyo uchimbahji wake hauwezi kuleta madhara kwenye jmii husika,

Awali akizungumza wakati akifungua mkutano huo kwa niaba ya Mkuu wa wilaya ya Muheza, Katibu Tawala wa wilaya hiyo serikali inatambua ushirikishwaji wa wadau mbalimbali katika usimamizi na uhifadhi na uendelezaji wa rasimali za maji na mazingira.

Alisema lengo kuu katika juhudi hizo ni kuhakikisha rasilimali za maji zinazopatikana kwa wingi ikiwemo ubora unaokubalika na kwa uendelevu wa matumizi ya maji kwa sasa na vizazi vijavyo.

“Niwapongeze viongozi mliomaliza muda wenu kwa kazi nzuri na kubwa mlioifanya na kusimamia uendeshaji wa jumuiya ikiwemo usimamizi wa vyanzo vya maji”Alisema

Aliongeza kwa athari za mabadiliko ya tabia ya nchi na hali ya hewa hapa nchini ikiwemo Muheza joto kali mvua hazinyeshi hayo yote yamebadilika kutokana na uharibifu wa mazingira unaoendelea.

Alisisitiza utunzaji wa mazingira ni jambo muhimu ambalo limeendelewa kupewa kipaumbele na Rais na hata alipoazimisha siku ya kuzaliwa alipanda miti hivyo kupitia jumuya hiyo waendelee kuwahamasisha watu wapande miti katika kila sikukuu zao muhimu ikiwemo kuzaliwa.

Hata hivyo alieleza kwamba kuna umuhimu wa Jumuiya hizo kuendelea kujengewa uwezo ili kuweza kutunza mazingira ikiwemo mafunzo ya mara kwa mara ili waweze kuendana na kazi na mazingira kipindi cha sasa.