Vyuo vikuu nchini vinapaswa kuifanya agenda ya umataifishaji kuwa sehemu ya mikakati yake ya msingi kwa kuijumuisha katika ufundishaji, utafiti, ubunifu na huduma kwa jamii ili kuongeza ushindani wa kimataifa, kupanua fursa za elimu na ajira kwa vijana pamoja na kuchochea maendeleo ya kiuchumi.

Hayo yamesemwa na Makamu Mkuu wa Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela Prof. Maulilio Kipanyula wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Kitaifa wa Kuimarisha Mikakati ya Umataifishaji wa Elimu ya Juu Juni 19, 2026 katika kampasi ya NM-AIST jijini Arusha, ukiwakutanisha wataalamu wa sekta ya elimu kutoka ndani na nje ya Tanzania kujadili mustakabali wa elimu ya juu nchini.

Prof. Kipanyula ameeleza kuw umataifishaji wa elimu ya juu una mchango mkubwa katika kuongeza ubora wa elimu na tafiti, kuvutia wanafunzi na wataalamu kutoka mataifa mbalimbali, kuimarisha ushirikiano wa kimataifa na kuwaandaa wahitimu wenye uwezo wa kushindana katika soko la ajira la dunia.

Aidha, aliipongeza Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) kwa kuandaa mkutano huo na kutambua mchango wa Mradi wa TANZIE katika kuimarisha uwezo wa taasisi za elimu ya juu kupitia ushirikiano kati ya vyuo vikuu vya Tanzania na Ulaya.

Kwa upande wake, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Mzumbe, Prof. William Mwegoha, amesema mkutano huo unatoa jukwaa muhimu la kujadili masuala ya sera, rasilimali fedha na ushirikiano wa kimataifa, huku ukitarajiwa kutoa mapendekezo yatakayosaidia kuimarisha utekelezaji wa agenda ya umataifishaji nchini.

Mkutano huo umeandaliwa na Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) kupitia Mradi wa TANZIE unaofadhiliwa na Umoja wa Ulaya, kwa lengo la kuimarisha ushirikiano wa kimataifa na kuongeza uwezo wa taasisi za elimu ya juu nchini.

Na.Alex Sonna-DODOMA

Shirika la Viwango Tanzania (TBS) limepongezwa kwa mafanikio makubwa yaliyopatikana katika kipindi cha miaka 50 tangu kuanzishwa kwake, huku likitakiwa kuendelea kwenda sambamba na maendeleo ya teknolojia na mabadiliko ya soko la dunia ili kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania kimataifa.

Pongezi hizo zimetolewa na Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga,wakati wa maadhimisho ya kilele cha miaka 50 ya shirika hilo yaliyofanyika katika ofisi zake zilizopo Njedengwa jijini Dodoma, sambamba na uzinduzi wa kitabu kinachoelezea historia, mafanikio na mchango wa taasisi hiyo katika kukuza ubora wa bidhaa na huduma nchini.

Waziri Kapinga amesema TBS imekuwa nguzo muhimu katika kulinda afya na usalama wa wananchi kupitia usimamizi wa viwango vya bidhaa mbalimbali, huku ikichangia kwa kiasi kikubwa ukuaji wa sekta za uzalishaji, biashara na viwanda nchini.

Ameeleza kuwa katika kipindi hiki ambacho dunia inaendelea kubadilika kwa kasi kupitia teknolojia na ubunifu, TBS inapaswa kuwa na dhana ya kujitegemea zaidi kwa kuimarisha mifumo ya kisasa ya utoaji huduma na kuongeza uwezo wake wa kitaalamu ili kukidhi mahitaji ya soko la ndani na nje ya nchi.

"Tunapoadhimisha miaka 50 ya TBS, tunashuhudia mchango mkubwa wa taasisi hii katika kujenga imani ya bidhaa za Tanzania. Hata hivyo, ni muhimu kuendelea kuwekeza katika teknolojia, ubunifu na ushirikiano na sekta binafsi ili kuhakikisha bidhaa zetu zinakidhi viwango vya kimataifa," amesema Kapinga.

Aidha, Waziri huyo amesisitiza umuhimu wa TBS kuendelea kufanya kazi kwa karibu na sekta binafsi ili kuongeza ubora wa bidhaa zinazozalishwa nchini na kusaidia kutafsiri kwa vitendo maono ya Tanzania ya kuwa taifa lenye uchumi wa viwanda unaozalisha bidhaa zenye ushindani mkubwa katika masoko ya kikanda na kimataifa.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Dkt. Ashura Katunzi,amesema  maadhimisho hayo  ni fursa ya kutathmini mafanikio yaliyofikiwa na kuweka mikakati mipya ya kuifanya taasisi hiyo kuwa ya kisasa zaidi na yenye uwezo mkubwa wa kukabiliana na changamoto za karne ya 21.

Dkt. Katunzi amesema TBS itaendelea kuimarisha maabara za kisasa, kuongeza matumizi ya teknolojia za kidijitali na kuwekeza katika rasilimali watu ili kuhakikisha huduma za viwango zinakuwa bora zaidi, za haraka na zenye kuaminika.

"TBS inatambua kuwa dunia inabadilika kwa kasi kubwa, huku teknolojia na mazingira ya biashara vikibadilika, hivyo shirika hilo linapaswa kuendelea kuwa imara, bunifu na lenye uwezo wa kujibu changamoto mpya zinazoibuka."aamesema Dkt. Katunzi

Amebainisha kuwa kwa kipindi cha nusu karne, TBS imekuwa mhimili muhimu wa maendeleo ya viwanda na biashara nchini kwa kuhakikisha bidhaa zinazozalishwa na kuuzwa zinazingatia viwango vinavyotakiwa, jambo ambalo limeongeza imani ya walaji na kufungua fursa za biashara katika masoko mbalimbali duniani.

Naye Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo, Mariam Ditopile Mzuzuri, amesema TBS imekuwa mhimili muhimu katika kulinda maslahi ya walaji, kuimarisha ushindani wa bidhaa za Tanzania na kuchochea ukuaji wa sekta za uzalishaji nchini.

 Ditopile amesema ipo haja ya kufanyika kwa mapitio ya kina ya Sera ya Ubora wa Bidhaa ili iweze kuakisi mabadiliko makubwa yaliyotokea katika nyanja za sayansi, teknolojia, biashara na uzalishaji tangu sera hiyo ilipoanzishwa.

"Tunapoipongeza TBS kwa mafanikio ya miaka 50, ni muhimu pia kuangalia mbele na kufanya maboresho yatakayoiwezesha taasisi hii kuendelea kuwa nguzo ya maendeleo ya viwanda, biashara na kilimo katika mazingira ya sasa ya kiteknolojia," amesema Ditopile.

Ditopile amesema imejijengea rekodi ya kuwa taasisi muhimu katika kuhakikisha bidhaa zinazozalishwa, kuuzwa na kutumiwa nchini zinakidhi viwango vinavyotakiwa kwa ajili ya kulinda afya, usalama na maslahi ya watumiaji.

Naye Katibu Mkuu wa Shirikisho la Viwango Afrika (ARSO), Dkt. Hermogene Nsengimana, amesema Julai 2026 Tanzania itakuwa nchi ya saba barani Afrika kupata Alama ya Ubora ya Afrika (Africa Quality Mark) kwenye bidhaa zake.

Amesema kwa hatua hiyo, Tanzania itaungana na Rwanda, Togo, Senegal, Ethiopia, Nigeria na Zimbabwe katika nchi zinazotumia alama hiyo ya ubora inayolenga kuimarisha viwango vya bidhaa barani Afrika.

Amesema Shirikisho la Viwango Afrika limekwisharatibu na kuoanisha takribani viwango 2,600 vinavyolenga sekta za kipaumbele ikiwemo usindikaji wa mazao ya kilimo, sekta ya magari, dawa na bidhaa za afya, usafirishaji na ugavi, pamoja na nguo na bidhaa za ngozi.

Ameeleza kuwa kwa sasa takribani bidhaa 500 katika ngazi ya Afrika zinapitiwa ili kupata Alama ya Ubora ya Afrika, hatua itakayosaidia kurahisisha biashara ndani ya Eneo Huru la Biashara la Afrika (AfCFTA).

Amesema bidhaa za Tanzania ambazo kwa sasa zinabeba alama ya TBS, zitapata fursa ya kuwekewa alama ya ubora ya Afrika, jambo litakaloongeza ushindani na upatikanaji wa masoko katika nchi mbalimbali za bara hilo.

 


Chuo cha Uhasibu Arusha (IAA) kinaendelea kuwaandaa wanafunzi na walimu kushiriki kikamilifu katika kutangaza Tanzania, vitutio vyake vya Utalii pamoja na chuo hicho kupitia Mashindano ya AFCON yanayotarajiwa kufanyika mwaka 2027.

Hayo yamesemwa na Meneja wa Kampasi ya Dodoma (IAA), Prof. Epaphra Manamba leo tarehe 19 Juni 2026; wakati akizungumza katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayofanyika katika Viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma.

“Ukizungumzia Arusha unazungumza Utalii, makao makuu ya IAA ni Arusha na sisi IAA tuna programu ya utalii na ukarimu; kwa hiyo wanafunzi wetu watashiriki kikamilifu kufanyia kazi yale waliyojifunza katika eneo la utalii na ukarimu kuanzia kuwapokea wageni mbalimbali, kutangaza nchi yetu na vivutio vyake na chuo chetu pia,” amesema Prof. Manamba.

 Aidha, Prof. Manamba amesema IAA inatambua umuhimu wa elimu katika maendeleo ya nchi na itahakikisha inaendelea kuandaa wataalam wa fani mbalimbali ambao watakuwa na uwajibikaji jumuishi kwa ajili ya kushiriki kujenga uchumi jumuishi kuendana na Dira ya Maendeleo ya Taifa ya 2050.

Katika hatua nyingine Prof. Manamba amesema dirisha la maombi kwa ngazi ya Cheti (Certificate), Stashahada (Diploma)  na Shahada ya Uzamili (Master’s Degree ) limefunguliwa, hivyo akatoa wito kwa watu wenye sifa na vigezo vya kujiunga na IAA katika kutuma maombi yao ili waweze kupata elimu bora inayojibu mahitaji ya wakati ya soko la ajira.

Naye Bw. Justine Kitaja ambaye ni mhitimu wa IAA Shahada ya kwanza na Shahada ya Uzamili  ameipongeza IAA kwa ubunifu wa kutoa shahada ya uzamili kwa mwaka mmoja kupitia mfumo mseto (masomo ya darasani na kwa njia ya mtandao/Blended and Physical classes); jambo linalosaidia kuokoa muda na kuwawezesha wanafunzi kusoma  huku wakiendelea na majukumu yao ya kazi na familia.