Serikali imesema kuwa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Msalato jijini Dodoma unatarajiwa kukamilika na kuanza kutumika ndani ya mwezi Septemba mwaka huu, hatua inayotarajiwa kuimarisha usafiri wa anga na kulipa hadhi zaidi jiji la Dodoma ambalo ni Makao Makuu ya nchi.

Akizungumza wakati alipotembelea na kuona maendeleo ya mradi huo, Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), alisema ujenzi wa uwanja huo umefikia hatua za mwisho ambapo miundombinu mikubwa ikiwemo njia ya kuruka na kutua ndege pamoja na maeneo ya maegesho ya ndege imekamilika kwa kiwango kikubwa.

Mhe. Balozi Omar, alisema mradi huo ulianza kutekelezwa mwaka 2022 kwa ushirikiano kati ya Serikali ya Tanzania, Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) na Mfuko wa Afrika Growing Together Fund (AGTF), ukiwa na lengo la kujenga uwanja wa kisasa utakaoendana na mahitaji ya Mji Mkuu wa nchi.

“Dodoma ni makao makuu ya nchi, hivyo ilikuwa muhimu kuwa na uwanja wa ndege wa kisasa unaoweza kukidhi ongezeko la shughuli za kiuchumi, kiserikali na kijamii,” alisema Mhe. Balozi Omar.

Aliongeza kuwa, Kwa mujibu wa taarifa ya utekelezaji wa mradi huo iliyotolewa na watalaamu, sehemu ya kwanza inayohusisha miundombinu ya uwanja imefikia asilimia 86.73 ya utekelezaji, huku sehemu ya pili inayohusisha majengo muhimu ikiwemo jengo la abiria, mnara wa kuongozea ndege na jengo la zimamoto ikiwa imefikia asilimia 75.1.

“Uwanja huu utakuwa miongoni mwa viwanja vikubwa nchini, ukiwa na njia ya kuruka na kutua ndege yenye urefu wa kilomita 3.6 na upana wa mita 60, pamoja na maegesho makubwa ya ndege yatakayowezesha kuhudumia ndege nyingi kwa wakati mmoja” aliongeza Mhe. Balozi Omar.

Aidha Mhe. Balozi Omar, alisema Kukamilika kwa Uwanja huo kunatarajiwa kuufungua zaidi mji wa Dodoma kwa safari za ndani na kimataifa, huku ukiongeza mvuto wa uwekezaji, kuimarisha nafasi ya Tanzania katika sekta ya usafiri wa anga katika ukanda wa Afrika Mashariki, kwa kuwa jengo la abiria litakuwa na uwezo wa kuhudumia abiria milioni 1.5 kwa mwaka, jambo linalotarajiwa kuongeza uwezo wa Dodoma kupokea wageni wa ndani na nje ya nchi pamoja na kuchochea ukuaji wa uchumi.

Mradi huo pia unahusisha ujenzi wa mnara wa kisasa wa kuongozea ndege wenye urefu wa mita 56.2, jengo la zimamoto la kiwango cha kimataifa, majengo ya kuzalisha umeme na jengo la hali ya hewa lenye vifaa vya kisasa vya usimamizi wa usafiri wa anga.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Ujenzi, Mhe. Godfrey Kasekenya (Mb) alisema kuwa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Msalato ni miongoni mwa miradi muhimu ya kimkakati na ya kielelezo inayotekelezwa nchini chini ya uongozi wa Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Alisema mradi huo umebuniwa kwa mtazamo wa muda mrefu, ukiwa na uwezo wa kupanuliwa hatua kwa hatua kulingana na ongezeko la mahitaji ya usafiri wa anga nchini.

“Uwanja huu umejengwa kwa viwango vya kisasa vya kimataifa na unatarajiwa kuwa miongoni mwa viwanja vya ndege vya kisasa zaidi nchini mara utakapoanza kutumika” alisema Mhe. Kasekenya

Alisisitiza kuwa Serikali imejipanga kuhakikisha kazi zilizobaki zinakamilika kwa wakati ili ahadi ya kuanza kwa shughuli za uwanja huo mwezi Septemba itimie, huku akibainisha kuwa mradi huo ni sehemu ya jitihada za kuimarisha miundombinu ya usafiri na kukuza uchumi wa Taifa kupitia uwekezaji mkubwa wa kimkakati.

Katika Ziara hiyo Waziri wa Fedha Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar, aliambatana na Naibu Mawaziri wake, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), Mhe. Laurent Luswetula, Katibu Mkuu Wizara ya Fedha ambaye pia ni Mlipaji Mkuu wa Serikali, Dkt. Natu El-maamry Mwamba, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Bw. Nsubili Joshua, Kaimu Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha ambaye pia ni Kamishna wa Idara ya Fedha za Nje, Bw. Rished Bade, Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi Balozi Mhandisi Aisha Amour pamoja na wataalam mbalimbali kutoka Wizara ya Fedha, Wizara ya Ujenzi wakiwemo Wakala wa Barabara nchini (Tanroads).

 

Na Mwandishi Wetu, Pretoria

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Dkt. Abdulmajid Mussa Nsekela, ametunukiwa Shahada ya Uzamivu (PhD) kutoka Chuo Kikuu cha Afrika Kusini (UNISA), hatua inayotafsiriwa kama ushahidi wa namna taaluma, utawala bora na uongozi wa kimkakati vinavyoweza kuibadilisha taasisi ya kifedha na kuleta matokeo chanya ya biashara.

Dkt. Nsekela alihitimu shahada hiyo Juni 12, 2026, baada ya kukamilisha utafiti uliochambua uhusiano kati ya utawala wa makampuni na ufanisi wa kifedha wa benki za Afrika Mashariki, huku ukitathmini athari za uvujaji wa taarifa katika utendaji wa taasisi za fedha.

Utafiti huo umebainisha kuwa mifumo imara ya utawala, uwazi katika utoaji wa taarifa na udhibiti wa taarifa nyeti huongeza imani ya wawekezaji, kuimarisha utendaji wa kifedha na kuweka msingi wa ukuaji endelevu wa taasisi.
Akizungumza baada ya kutunukiwa shahada hiyo, Dkt. Nsekela alisema kujifunza ni safari endelevu inayowasaidia viongozi kufanya maamuzi bora na kuimarisha utendaji wa taasisi wanazoongoza.

"Usimamizi makini wa makampuni si suala la nadharia pekee, bali ni msingi wa utendaji bora na mafanikio endelevu katika sekta ya fedha. Safari hii imeniongezea maarifa yatakayochangia zaidi katika kuendeleza taasisi na sekta yetu," alisema.

Mafanikio hayo ya kitaaluma yanakuja wakati Benki ya CRDB ikiendelea kushuhudia ukuaji mkubwa chini ya uongozi wake tangu alipoteuliwa mwaka 2018. Katika kipindi hicho, bei ya hisa za benki imeongezeka kutoka Sh95 hadi kufikia takribani Sh3,000 kwa hisa, huku faida baada ya kodi ikiongezeka kutoka Sh bilioni 64.1 hadi Sh bilioni 728.6 mwaka 2025.
Benki hiyo pia imefanikiwa kuharakisha mageuzi ya kidijitali, ambapo zaidi ya asilimia 98 ya miamala yake hufanyika kupitia majukwaa ya kidijitali. Idadi ya wateja imeongezeka na kufikia zaidi ya milioni 7.2 wanaohudumiwa kupitia matawi, mawakala, ATM, SimBanking na huduma za intaneti.

Katika kipindi hicho, CRDB imepanua shughuli zake nje ya mipaka ya Tanzania kwa kuimarisha uwepo wake Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, sambamba na kufungua ofisi ya uwakilishi Dubai ili kuvutia mitaji na kuimarisha ushirikiano wa kimkakati katika masoko ya kimataifa.
Mwenyekiti wa Bodi ya Benki ya CRDB, Profesa Neema Mori, alisema mafanikio ya Dkt. Nsekela yanaonesha namna taaluma na uongozi makini vinavyoweza kuleta mageuzi makubwa ndani ya taasisi za biashara.

Alisema Benki ya CRDB imeendelea kuwa mfano wa mafanikio yanayojengwa katika misingi ya utawala bora, ubunifu na maamuzi yanayotokana na matumizi sahihi ya taarifa.

Mafanikio ya Dkt. Nsekela yanatoa funzo kwa viongozi wa biashara barani Afrika kuhusu umuhimu wa kuwekeza katika maarifa na kujifunza kila wakati ili kujenga taasisi imara, zenye ushindani na uwezo wa kuhimili mabadiliko ya mazingira ya biashara duniani

 


Na.Ashura Mohamed - Arusha 

Katika kuhakikisha kuwa Uchumi wa wakazi wa mkoa wa Arusha  unaimarika  wananchi wa mkoa huo hususani Vijana  wametakiwa kuhakikisha kuwa wanachangamkia fursa mbali mbali za kiuchumi ili kunufaika na ujio wa mashindano ya kimataifa ya Afcon 2027.

Akizungumza kwa niaba ya mkuu wa Wilaya ya Arusha Mjini bw.Jospeh Mkude,wakati wa Kongamano la Vijana  la Engutoto Youth Summit kuhusu Mashindano ya AFCON 2027,Wakili Irene Ndosi ambaye ni Katibu Tarafa Suye  amesema kuwa ujio wa Afcon ni neema kubwa kwa wakazi wa mkoa wa Arusha ambapo mbali na kupata burudani ya mpira wa miguu lakini pia ni fursa kwa makundi yote kuongeza uchumi wao.

"Fursa zitaanzia kuanzia watu wa chini kabisa boda boda,watu wa usafirishaji mpaka wanawake watengeneza shanga,kila mtu achukue nafasi hiyo kuleta mabadiliko chanya  kwenye uchumi wake binafsi na familia yake na mkoa  kwa ujumla,pia tuwe tayari kujaza eneo la  uwanja wa Afcon kwasababu mashindano haya ni yakipekee na yanashirika nchi tatu ambazo ni Tanzania,Kenya na Uganda."Amesitiza Ndosi 

Aidha Hamza Juma Njiku ni Diwani wa Kata ya Engutoto amesema kuwa kongamano hilo ni muhimu kwa kuwa limewakutananisha vijana na wadau mbal8 mbali katika kuonyesha fursa zilizopo kuelekea mashindano hayo ya Afcon.

"Sisi katika kata yetu fursa za Afcon zimetugusa moja kwa moja kwa kuwa tunajengewa Uwanja mkubwa mzuri wa Mazoezi kwaajili ya mashindano hayo ambapo utakuwa na uwezo wa kuchukuwa watu 5000 waliokaa,maegesho ya magari 500 na mabasi mawili kwaajili ya zile timu ambazo zitaingia kufanya mazoezi,ila uwanja ukikamilika na mashindano kumalizika utatumika kwaajili ya ligi kuu na michuano mbali mbali."Amesema Diwani Njiku

Kwa Upande wake Mwenyekiti wa Umoja wa Chama cha Mapinduzi (UVCCM),Kata ya Engutoto ambaye ndio muandaaji wa Kongamano Engutoto Youth Summit,bw.Ibzan  Michael Ruheta  amesema kuwa  kongamano hili si jukwaa la kisiasa bali ni jukwaa linalokutanisha watu wote kujadili fursa za AFCON kuelekea mwaka 2027. 

Bw.Ruheta  amesema kuwa Mashindano ya AFCON hayatahuishwa na Tanzania peke yake bali ushirikiano na  mataifa mengine wakiwemo Kenya pamoja na Uganda,hivyo kama Watanzania ni wajibu wao  kuamka na kuhakikisha tunaitumia nafasi hiyo ipasavyo.

"Ndugu mgeni rasmi, kama unavyojua nchi yetu imepata fursa ya kuandaa mashindano haya ya AFCON,hivyo kama viongozi mliopo katika nafasi za maamuzi, ni vizuri kujipanga kwa kushirikiana na wadau mbalimbali na taasisi mbalimbali zilizopo nchi yetu kwa kikisha fursa hizi tunazipata kwa wakati, vijana waheshimiwe, wasikilizwe na kero zao zitatuliwe ili nchi yetu inufaike."Amefafanua  Mwenyekiti huyo

Kongamano la Engutoto Youth  Summit lenye kauli mbiu ya "Unlocking 2027 AFCON Opportunity" limeandaliwa na Vijana wa Chama Cha Mapinduzi Kata ya Engutoto,na limekusudia kuwajengea vijana uwezo wa kunufaika na fursa za michezo hiyo kubwa ya kimataifa ambapo limefanyika katika Chuo cha Uhasibu Arusha(IAA) na kukutanisha Vijana Zaidi ya 1000 ili kuonesha nyanja mbali mbali ambazo vijana wanaweza kunuifa nazo.








 Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba amemuagiza Waziri wa Maji kwenda Mkoa wa Mwanza kushughulikia mara moja changamoto ya upatikanaji wa maji inayowakabili wananchi wa mkoa huo na kuhakikisha huduma hiyo inarejea kwa haraka.


Dkt. Mwigulu ametoa maelekezo hayo leo, Jumapili Juni 14, 2026, wakati akizungumza, kusikiliza na kutatua changamoto za wananchi wa Tarafa ya Kiomboi katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika Uwanja wa Shule ya Msingi Lulumba, Wilaya ya Iramba mkoani Singida.

Amesema amepokea taarifa kuhusu changamoto ya maji katika Mkoa wa Mwanza na tayari amemuelekeza Waziri mwenye dhamana ya maji kwenda eneo husika kusimamia upatikanaji wa suluhisho la haraka.

“Nimemtuma Waziri aende haraka Mwanza akasimamie jambo lile mpaka maji yapatikane. Sisi watu wa Singida tunataka tupate maji toka Mwanza. Simiyu tunataka tupate maji toka Mwanza. Dodoma tunataka tupate maji toka Mwanza. Tabora, wengine wameshaanza kupata maji toka Mwanza. Leo kuja kuambiwa Mwanza, pale pale lilipo Ziwa Victoria, pana shida ya maji. Hili ni jambo ambalo haliwezi kueleweka, na wala hatuwezi kulielewa,” amesema Dkt. Mwigulu.

Amesema hakuna sababu ya wananchi kuendelea kukosa huduma hiyo wakati chanzo cha maji kinajulikana na miundombinu ya mradi ipo.

“Hatutaki ngonjera za maneno. Hawa wanasema si bomba limekuwaje, hawa wanasema si umeme umekuwaje. Chanzo sisi tunajua kiko pale, hatuna shida ya chanzo cha maji, na mradi upo, na maji yapo. Haya mambo mengine ni ya ngonjera, mimi sitaki kuyasikia,” amesema.

Waziri Mkuu amewataka wataalamu wa sekta ya maji pamoja na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kufanya kazi kwa pamoja na kuhakikisha wananchi wanapata huduma hiyo kwa haraka.

“Mkuu wa Mkoa awatafute wataalamu wake, awatafute TANESCO na wataalamu wa maji. Wachimbe kiini cha tatizo na wakeshe mpaka wananchi wapate maji. Kunapopambazuka kesho nipate majawabu kwamba maji yamepatikana,” amesema.

Juni 9, 2026, Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Mwanza (MWAUWASA) ilitoa taarifa kwa umma kuhusu upungufu wa huduma ya maji uliosababishwa na hitilafu za umeme zilizokuwa zikijitokeza mara kwa mara.

Wakati huohuo, Dkt. Mwigulu amesema Serikali imejipanga kuhakikisha changamoto ya upatikanaji wa maji katika Tarafa ya Kiomboi na maeneo mengine ya Wilaya ya Iramba inapata ufumbuzi wa kudumu kupitia utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maji pamoja na uwekezaji mkubwa unaoendelea kufanywa katika sekta hiyo nchini.

Amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeweka kipaumbele maalum katika sekta ya maji kwa kutekeleza miradi ya kimkakati inayolenga kuongeza upatikanaji wa maji safi na salama kwa wananchi.

“Niwahakikishie kwamba hili ni eneo ambalo Mheshimiwa Rais ameliwekea kipaumbele cha hali ya juu kwa sababu maji ni uhai, maji ni maisha. Tulihangaika kupata chanzo cha uhakika cha maji na sasa kimepatikana, hatua mbalimbali zinaendelea ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma hiyo kwa uhakika,” amesema.

Aidha, amesema Serikali inaendelea na utekelezaji wa mpango wa Gridi ya Taifa ya Maji pamoja na kuimarisha uwezo wa uchimbaji wa visima, ujenzi wa mabwawa na upimaji wa vyanzo vya maji ili kukabiliana na changamoto ya maji katika maeneo mbalimbali nchini.

Dkt. Mwigulu ambaye pia ni Mbunge wa Iramba Magharibi amesema Serikali inaendelea na usanifu wa barabara ya Kiomboi–Kisiriri–Sibiti kwa lengo la kuijenga kwa kiwango cha lami na kuboresha mawasiliano kati ya wananchi wa maeneo hayo na maeneo jirani.

Aidha, amesema usanifu wa barabara ya Kitusha–Galangala–Kisana–Kinampanda–Kisiriri umekamilika, huku Serikali ikiendelea na maandalizi ya utekelezaji wa miradi mingine ya barabara katika Wilaya ya Iramba ili kurahisisha shughuli za kijamii na kiuchumi.

Pia amesema usanifu wa daraja la kuunganisha eneo la Hospitali ya Kiomboi na maeneo ya Meli pamoja na Iguguno umekamilika na hatua zinazofuata ni kumpata mkandarasi kwa ajili ya kuanza utekelezaji wa mradi huo.

Sambamba na hilo, Dkt. Mwigulu amesema Serikali inaendelea na maandalizi ya kuanzisha Chuo Kikuu katika eneo la Kiomboi baada ya eneo lililotengwa kuridhiwa na wataalamu husika.

“Hapa Kiomboi tutakuwa na Chuo Kikuu. Eneo limekaguliwa na kuridhiwa na hatua za utekelezaji zinaanza,” amesema.

Amesema pindi ujenzi wake utakapokamilika, Chuo Kikuu hicho kinatarajiwa kuanza kwa awamu ya kwanza kwa uwezo wa kuhudumia wanafunzi takribani 10,000.




 






Na Mwandishi Wetu, Muheza

Mkuu wa Wilaya ya Muheza mkoani Tanga, Ayoub Sebabili, amewahimiza wananchi kujitokeza kwa wingi katika shughuli za mapokezi ya Mwenge wa Uhuru 2026, akisema ushiriki mkubwa wa wananchi utasaidia wilaya hiyo kufanya vizuri katika mashindano ya Kitaifa ya Mwenge wa Uhuru.

Sebabili ametoa wito huo wakati wa zoezi la Jogging lililoandaliwa kama sehemu ya maandalizi ya mapokezi ya Mwenge wa Uhuru, ambapo aliwashukuru wananchi kwa kujitokeza kwa wingi na kushiriki shughuli hiyo.

Alisema Mwenge wa Uhuru unatarajiwa kuwasili wilayani Muheza Juni 23, 2026 ukitokea Wilaya ya Mkinga na kupokewa katika eneo la Kilapura, huku ukitarajiwa kulala katika Uwanja wa Jitegemee.

"Niwashukuru kwa namna mlivyojitokeza leo. Ushiriki wenu unaonyesha dhamira ya kuhakikisha Muheza inafanya vizuri katika mapokezi ya Mwenge wa Uhuru. Kila mmoja wetu awe balozi wa kuhamasisha wananchi wengine kujitokeza kwa wingi," alisema Sebabili..

Kwa upande wake, Mratibu wa Mwenge wa Uhuru Wilaya ya Muheza alisema maandalizi yanaendelea vizuri na kuwa viongozi katika ngazi zote wamepewa jukumu la kuhamasisha wananchi wa makundi mbalimbali, wakiwemo vijana, wanawake, wazee na watu wenye ulemavu kushiriki kikamilifu katika shughuli hizo.

Alisema Mwenge wa Uhuru utapitia maeneo mbalimbali ya wilaya hiyo kwa ajili ya kuzindua na kukagua miradi ya maendeleo pamoja na kutoa ujumbe wa umoja, uzalendo na mshikamano wa kitaifa.

Kwa mujibu wa ratiba iliyopangwa, Mwenge wa Uhuru utaanzia Kata ya Mlingano kabla ya kuelekea Machemba kwa uzinduzi wa mradi na ukaguzi wa banda la lishe litakaloonyesha juhudi za Halmashauri ya Muheza katika kupambana na utapiamlo, malaria na maambukizi ya Virusi vya Ukimwi.

Baadaye utaelekea katika Shule ya Venance Mabeyo na Kata ya Mpapayu kwa ajili ya uzinduzi wa miradi mbalimbali ya maendeleo.

Katika Kata ya Genge, Mwenge wa Uhuru utazindua maabara katika Shule ya Sekondari Chief Mang'enya iliyojengwa kwa nguvu za wananchi na kuweka jiwe la msingi katika mradi wa madarasa mapya kwa ajili ya maandalizi ya wanafunzi wa Kidato cha Kwanza mwaka 2027.

Mratibu huyo alisema pia kutakuwa na shughuli za Klabu ya Wapinga Rushwa pamoja na programu mbalimbali za elimu kwa jamii.

Katika Kata za Magila na Majengo, Mwenge wa Uhuru utatembelea kikundi kilichonufaika na mkopo wa asilimia 10 wa Halmashauri unaotolewa kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu, ambapo kikundi hicho kimepata Sh25 milioni kwa ajili ya shughuli za maendeleo ya kiuchumi.

Aidha, katika eneo la Mikwamba kutakuwa na maonesho ya fursa za zabuni kupitia PPRA, yakilenga kuhamasisha vikundi maalumu kushiriki katika zabuni zinazotengwa kwa makundi hayo.

Ratiba hiyo itahitimishwa kwa shughuli mbalimbali katika Kata ya Tongwe na eneo la Mpaa, ikiwemo uzinduzi wa daraja la karavati, uzinduzi wa Jengo la Havest Inn na mkesha wa Mwenge wa Uhuru katika Uwanja wa Jitegemee.

Viongozi hao wamewataka wananchi kuzingatia amani, utulivu na usalama katika kipindi chote cha shughuli hizo, huku wakisisitiza kuwa vitendo vya uhalifu na uvunjifu wa amani havitavumiliwa.

Akizungumza katika hafla hiyo, Katibu Tawala wa Wilaya (DAS) wa Muheza, Mohamed Mfaki, aliwashukuru wananchi kwa ushirikiano wao katika maandalizi ya mapokezi ya Mwenge wa Uhuru na kuwataka kuendelea kushiriki kikamilifu.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Muheza, Dk Juma Mhina, alisema wilaya hiyo imejipanga kufanya vizuri zaidi mwaka huu na inalenga kushika nafasi ya kwanza kitaifa katika mapokezi ya Mwenge wa Uhuru


Alisema maandalizi yaliyoanza mapema chini ya usimamizi wa Mkuu wa Wilaya yanalenga kuongeza ushiriki wa wananchi na kuhakikisha shughuli zote zinafanyika kwa mafanikio makubwa.

"Malengo yetu ni kuona wananchi wanajitokeza kwa wingi katika shughuli zote za Mwenge wa Uhuru. Tunataka Muheza iwe mfano wa mafanikio na ushirikiano katika mapokezi ya Mwenge wa Uhuru 2026," alisema Dk Mhina.


 


Na OWM - TAMISEMI, Dar es Salaam


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) Mhe. Prof. Riziki Shemdoe ametaka Mkandarasi kampuni ya China Railways and Bridges Corporation (CRBC) inayojenga barabara tisa (9) za lami zenye urefu wa kilometa 5.42 kukamilisha ujenzi wa barabara saba (7) zilizosalia ifikapo Agosti 14, 2026, barabara hizo zinajengwa kupitia Mradi wa Uboreshaji wa Jiji la Dar es Salaam Awamu ya Pili (DMDP II) katika kata za Sinza, Mburahati, Mabibo na Makurumla wilayani Ubungo.

Prof. Shemdoe ametoa maelekezo hayo Juni 13, 2026 Katika Manispaa ya Ubungo jijini Dar es Salaam wakati wa ziara yake ya kikazi ya kukagua ujenzi wa barabara 23 zenye urefu wa kilometa 52.37 zinazojengwa wilayani Ubungo katika kata 11 kupitia utekelezaji wa Mradi wa Uboreshaji wa Jiji la Dar es Salaam Awamu ya Pili (DMDP II).

Prof. Shemdoe amesitiza kuwa, mkandarasi huyo anayesuasua katika ujenzi wa barabara hizo kwa kisingizio cha lami kuchelewa kufika kutokana na vita ya Mashariki ya Kati, hatopewa muda wa nyongeza wa kukamilisha ujenzi wa barabara hizo iwapo atashindwa kukamilisha ifikapo Agosti 14, 2026 kwa mujibu wa mkataba.

“TARURA hakuna kumuongezea muda mkandarasi huyu, atafute lami popote atakapoipata na afanye kazi usiku na mchana kukamilisha barabara hizi 7 zilizosalia ili kuwaondolea adha wananchi,” amesisitiza Prof. Shemdoe.

Katika kuhakikisha barabara zinakamilika kwa wakati, Prof. Shemdoe ameitaka TARURA na Mshauri Elekekezi (NIMETA Consult (T) kumshauri mkandarasi CRBC kwa kuangalia uwezekano wa kukabidhi baadhi ya barabara hizo kwa mkandarasi mwingine (sub contract) ili ujenzi ukamilike kwa wakati.

Aidha, Prof. Shemdoe amemuelekeza Mtendaji Mkuu wa TARURA Mhandisi Victor Seff kumuondoa Mkuu wa Kitengo cha Fedha na Uhasibu Bw. Evans Mgeusa anayesimamia Fedha za Miradi ya Benki ya Dunia kwa kitendo cha kuchelewesha malipo na kumleta mwingine ambaye atafanya kazi kwa weledi na wakati.

Sanjari na hilo, Prof. Shemdoe amemuelekeza Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu - TAMISEMI Bw. Adolf Ndunguru kuwaondoa Wahasibu Bw. Julius Bashuta na Mbwana Mkembe wa kitengo hicho cha Fedha na Uhasibu kinachosimamia  fedha za miradi ya Benki ya Dunia, na kuwaleta wengine ambao watafanya kazi vizuri na kwa uaminifu. 

Akizungumzia jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita, Prof. Shemdoe amempongeza Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwezesha utiaji saini wa mikataba minne ya ujenzi wa barabara za wilaya ya Ubungo yenye thamani ya shilingi bilioni 77, 457,169,172.73 kupitia Mradi wa Uboreshaji wa Jiji la Dar es Salaam Awamu ya Pili (DMDP II).

Kwa upande wake Mkazi wa Sinza Bw. Jawa Waziri amemshukuru Prof. Shemdoe kwa kufanya ziara ya ukaguzi wa barabara ya mtaa wake wa Sinza Lion na kumpongeza kwa kumuelekeza mkandarasi CRBC kukamilisha kwa wakati barabara hiyo ambayo imekuwa ni kero kwa wakazi wa eneo hilo.

Na Abdu Madenge, WAF – Dar es Salaam

Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Dkt. Seif Shekalaghe, ametoa wito kwa wadau wa maendeleo kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuboresha afya ya uzazi kwa kutoa msaada wa kifedha, kiufundi na rasilimali nyingine muhimu, huku akisisitiza dhamira ya Serikali ya kutokomeza au kupunguza kwa kiwango kikubwa vifo vya akina mama wajawazito na watoto wachanga vinavyoweza kuzuilika.
Nilipoanzisha biashara yangu, nilikuwa na matumaini makubwa. Nilikuwa nimewekeza akiba yangu, muda wangu, na nguvu zangu zote kwenye mradi huo. Niliamini kwamba kwa kufanya kazi kwa bidii, mafanikio yangekuja haraka. Lakini mambo hayakwenda kama nilivyotarajia.

Kuanzia mwezi wa kwanza hadi wa sita, biashara yangu ilihangaika kupata faida ya kutosha. Wateja walikuwa wachache na mauzo hayakufikia kiwango nilichokuwa nimekitarajia. 

Wakati huo huo, washindani wangu walionekana kufanya vizuri zaidi kila siku. Kwa kweli nilianza kuwa na wasiwasi.

Kila mwisho wa mwezi nilipokagua hesabu zangu, niliona faida ndogo sana au wakati mwingine kutokuwepo kabisa. 

Nilijiuliza kama nilikuwa nimefanya uamuzi sahihi wa kuanzisha biashara hiyo. Kilichoniumiza zaidi ni kuona watu wakiniambia kwamba biashara yangu isingeweza kushindana na zile ambazo tayari zilikuwa zimejijengea jina sokoni.

Kadri miezi ilivyopita, shinikizo liliongezeka.

Kulikuwa na nyakati nilifikiria kufunga biashara na kutafuta jambo lingine la kufanya. Nilihisi kama juhudi zangu zote zilikuwa zinaenda bure.

Lakini sikuwa tayari kukata tamaa. Badala ya kuacha, nilianza kutafuta njia za kuboresha huduma zangu.SOMA ZAIDI.
Kwa miaka mingi, kulikuwa na mtu mmoja ambaye alikuwa amechukua nafasi ya pekee moyoni mwangu. Tulijuana vizuri na tulikuwa marafiki wa karibu. 

Tulizungumza mara kwa mara, tulicheka pamoja, na mara nyingi tulisaidiana katika mambo mbalimbali ya maisha. Kadri muda ulivyopita, hisia zangu kwake zilianza kukua.

Lakini kulikuwa na tatizo moja. Sikuwahi kumwambia ukweli. Niliogopa kwamba nikifungua moyo wangu, ningeharibu urafiki wetu. 

Nilihofia kukataliwa na kupoteza mtu ambaye tayari alikuwa muhimu sana maishani mwangu. Hivyo niliamua kunyamaza.

Miezi iligeuka miaka huku nikificha hisia zangu. Kila nilipomwona akiwa na watu wengine, nilihisi wivu kidogo, lakini sikuwa na ujasiri wa kusema chochote. 

Kwa kweli hali ile ilinichosha.
Kulikuwa na nyakati nilitaka kumweleza kila kitu, lakini kila nilipopata nafasi, hofu ilinishinda.

Nilianza kuamini kwamba labda hisia zile zingebaki siri yangu milele. Kadri muda ulivyopita, nilijaribu kuendelea na maisha. SOMA ZAIDI.