📌Fedha za ndani sh.bilioni 15 kutumika


Katika juhudi za kuhakikisha kuwa Tanzania inafikia asilimia 80 ya matumizi ya nishati safi ya kupikia ifikapo 2034, Serikali katika mwaka wa fedha 2026/2027 itasambaza mifumo ya nishati safi ya kupikia katika taasisi 300 zinazolisha watu zaidi ya 100.

Hayo yamesemwa na Mtaalam kutoka Kitengo cha Nishati Safi ya Kupikia, Wizara ya Nishati, Bw. Omari Khalifa wakati wa Maonesho ya Kimataifa ya Biashara (SabaSaba) yanayoendelea katika Viwanja vya Mwl.Nyerere jijini Dar es Salaam.

Khalifa amesema mpango huo utatekelezwa katika bajeti ya mwaka huu wa fedha kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) ambapo  jumla ya shilingi bilioni 15 ambazo ni fedha za ndani zimetengwa kwa ajili ya utekelezaji wa mpango huo.

Ameeleza kuwa mifumo itakayofungwa inajumuisha gesi ya LPG, majiko banifu, mkaa mbadala pamoja na majiko ya umeme  kwa lengo la kuboresha huduma za upishi, kulinda mazingira na kuimarisha afya ya watumiaji.

Katika utekelezaji wa mpango huo kampuni mbalimbali zinazotoa huduma ya mifumo ya nishati safi ya kupikia zitafaidika kupitia fursa zitakazotangazwa na  REA  huku taasisi hiyo ikisimamia usimikaji wa mifumo hiyo katika taasisi zitakazokidhi vigezo vilivyowekwa.







 

 Mwenyekiti wa Taifa Group na mfanyabiashara mashuhuri, Bw. Rostam Azizi, ametunukiwa Tuzo ya Juu ya Heshima ya Chemba ya Taifa ya Biashara Tanzania (TNCC) kwa kutambua mchango wake katika kukuza uwekezaji, kuunda ajira, kuboresha huduma za jamii na kuchochea maendeleo ya uchumi wa Taifa.

Tuzo hiyo ilikabidhiwa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Nchemba, aliyekuwa mgeni rasmi katika Kongamano la Biashara na Uwekezaji la Mwaka 2026 lililoandaliwa na TNCC katika Hoteli ya Johari Rotana, Dar es Salaam.

Akizungumza katika kongamano hilo, Dkt. Mwigulu alisema Serikali itaendelea kuimarisha mazingira ya biashara na uwekezaji kupitia maboresho ya sera, sheria, kanuni na mifumo ya utoaji huduma ili kuiwezesha sekta binafsi kuwa injini ya ukuaji wa uchumi na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

"Ajenda ya sekta binafsi ni ajenda ya Taifa. Hatuwezi kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 bila sekta binafsi yenye nguvu na inayoshirikiana kwa karibu na Serikali," amesema.

Aliongeza kuwa Serikali itaendelea kushughulikia mapendekezo ya sekta binafsi ili kuondoa vikwazo vya biashara na kuongeza ushindani wa bidhaa na huduma za Tanzania katika masoko ya kikanda na kimataifa.

Kupitia uwekezaji wake katika sekta mbalimbali, Bw. Rostam Azizi amechangia uundaji wa maelfu ya ajira, kukuza uwekezaji na kuboresha huduma za jamii, hatua zilizochangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya uchumi wa Taifa.

Akizungumza baada ya kupokea tuzo hiyo, Bw. Rostam Azizi aliishukuru Serikali na TNCC kwa kutambua mchango wake, akisema tuzo hiyo ni motisha ya kuendelea kushiriki katika maendeleo ya Taifa.

"Ninapokea tuzo hii kwa heshima kubwa.

Naihusisha na juhudi za pamoja kati ya sekta binafsi na Serikali katika kujenga uchumi imara. Nawapongeza pia wadau wote waliotunukiwa tuzo mbalimbali leo kwa mchango wao katika kuimarisha sekta binafsi na kukuza uchumi wa Taifa," amesema.

Katika hafla hiyo, Waziri Mkuu pia alikabidhi tuzo mbalimbali kwa wadau wengine, akiwemo Bi. Emma Kawawa, Bw. David Mwaibula, Bw. Imani Kajula, Bw. Elibariki Mmasi na Bi. Mercy Emmanuel Sila, kwa mchango wao katika kuendeleza sekta binafsi, kuboresha mazingira ya biashara na kuimarisha shughuli za TNCC.


Na Mwandishi Wetu


Dar es Salaam. Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imeendelea kutoa huduma mbalimbali kwa waandishi wa habari, wadau wa sekta ya habari na wananchi kupitia banda lake lililopo katika Kijiji cha Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwenye Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba).


Huduma zinazotolewa ni pamoja na ugawaji wa vitambulisho vya ithibati kwa waandishi wa habari waliokidhi vigezo kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, usajili wa waandishi wa habari, marekebisho ya taarifa za usajili pamoja na utoaji wa elimu kuhusu majukumu na huduma mbalimbali zinazotolewa na Bodi hiyo.


JAB imesema ushiriki wake katika maonesho hayo unalenga kusogeza huduma karibu na wananchi na wadau wa sekta ya habari, ili kurahisisha upatikanaji wa huduma pamoja na kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa ithibati na usajili wa waandishi wa habari nchini.


Bodi hiyo imewahimiza waandishi wa habari na wadau wengine kutumia fursa ya maonesho hayo kupata huduma kwa haraka na kwa ukaribu, huku ikieleza kuwa huduma hizo zinaendelea kutolewa pia katika Makao Makuu ya JAB.


Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam yanaendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, Barabara ya Kilwa, yakihusisha taasisi mbalimbali za umma na binafsi zinazowasilisha huduma na bidhaa zao kwa wananchi.




















Share this

 


Awataka wakuu wa mikoa kuendeleza kampeni za usafi


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) Mhe. Prof. Riziki amewapongeza Maafisa Afya wa Mikoa na Halmashauri nchini kwa kupunguza mlipuko wa kipindupindu kutoka maambukizi ya watu 12,000 hadi 700 kwa mwaka 2025/26, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa malengo waliyojiwekea mwaka jana.

Prof. Shemdoe ametoa pongezi hizo Juni 01, 2026 jijini Arusha, wakati  akifungua mkutano wa mwaka wa tathmini ya utekelezaji wa afua za afya na usafi wa mazingira nchini, unaofanyika katika Ukumbi wa Mkutano wa Kimataifa (AICC).

“Niwapongeze kwa utekelezaji wa lengo la kupunguza mlipuko wa ugonjwa wa kipindupindu mlilojiwekea mwaka jana, mmefanikiwa kupunguza kiwango cha mlipuko kutoka kesi 12,000 hadi 700, sasa niwaombe mwaka huu muweke lengo la kuendelea kutokomeza mlipuko wa ugonjwa huu,” amesema Prof. Shemdoe.

Sanjari na hilo, Prof. Shemdoe amewasisitiza Wakuu wa Mikoa, Maafisa Afya wa Mikoa na Halmashauri kuwahimiza wananchi kufanya mazoezi ili kuepukana na magonjwa yasiyoambukizwa kama shinikizo la damu, kisukari, magonjwa ya moyo, kiharusi, pumu, ambayo yanasababisha vifo na kuathiri nguvu kazi ya taifa.

Aidha, Prof. Shemdoe amewataka Wakuu wa Mikoa nchini kuendelea na kampeni ya kufanya usafi kila jumamosi ya mwisho wa mwezi kwani kampeni hiyo itaendelea kuimarisha hali ya usafi, kupunguza na kuondoa kabisa changamoto uwepo ya magonjwa ya milipuko ikiwepo kipindupindu.

Prof. Shemdoe ametumia fursa hiyo, kumshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uongozi wake na namna anavyowekeza katika sekta ya afya na mazingira, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa maono yake ya kutaka kila mtanzania awe na afya bora.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mhe. CPA Amos Makalla amemhakikishia Prof. Shemdoe kuwa, mkoa wake umejipanga ipasavyo katika utekelezaji wa miradi ya afya, na kuongeza kuwa ofisi yake itaendelea kushirikiana na wataalam wa afya katika kukabiliana na magonjwa ya milipuko.

Naye, Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu - TAMISEMI anayeshughulikia Afya Prof. Tumaini Nagu amesema mkutano huo umelenga kutathmini mpango kazi wa mwaka 2025/26 waliojiwekea maafisa afisa afya kuanzia ngazi ya mikoa hadi Mamlaka za Serikali za Mitaa, pamoja na kuandaa mpango kazi wa mwaka wa fedha 2026/27. 

Akifafanua malengo la mkutano huo, Mkurugenzi wa Afya,Ustawi wa Jamii na Lishe wa Ofisi ya Waziri Mkuu -TAMISEMI Dkt. Rashid Mfaume amesema kuwa, malengo ya mkutano huo ni kutathmini maendeleo ya utekelezaji wa afua ya afya na usafi wa mazingira katika ngazi ya Mikoa na Halmashauri kwa kuzingatia viashiria vya kitaifa na malengo ya kisekta.

Akizungumza kwa niaba ya washiriki wa mkutano huo, Mwenyekiti wa Maafisa Afya wa Halmashauri Bw. Fanuel Nyadwike amemuahaidi Prof. Shemdoe kuwa, watatumia mkutano huo kutathmini utekelezaji wa shughuli za mwaka uliopita wa 2025/26, kubadilishana uzoefu na kujifunza mbinu bora za kuboresha huduma za afya na usafi wa mazingira kwa mwaka 2026/27. 

Mkutano huo wa mwaka huu wa 2026 umebeba kaulimbiu isemayo “Kuimarisha Mifumo Jumuishi na Endelevu ya Afya na Usafi wa Mazingira ili Kujenga Jamii Stahimilivu yenye Afya Bora”.












Mkurugenzi wa Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB), Bw. Asangye Bangu, amewataka waendesha maghala kuzingatia uadilifu, uwajibikaji na utoaji wa huduma bora ili kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala.

Akifungua kikao maalumu cha waendesha maghala kilichofanyika mjini Morogoro Julai 1, 2026, Bangu, amesema waendesha ghala wanapaswa kuendana na wakati kwa kuwa waadilifu, kutoa huduma zenye viwango vya juu na kuhakikisha mfumo wa stakabadhi za ghala unaendelea kuwa na tija kwa wakulima, wafanyabiashara na wananchi kwa ujumla.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Waendesha ghala Tanzania, Abdulikarim amesema kikao hicho kimeandaliwa kwa lengo la kuongeza uelewa kuhusu masuala mbalimbali ya kiutendaji, kujadili changamoto zinazowakabili pamoja na kutafuta suluhisho la kuboresha maslahi ya waendesha ghala kutokana na kupanda kwa gharama za maisha na uendeshaji wa shughuli zao.

Ameongeza kuwa maazimio na maelekezo yaliyotolewa katika kikao hicho yatawasaidia waendesha ghala kuongeza ufanisi wa kazi zao na kuendelea kutoa huduma bora kwa wadau wote wa sekta ya kilimo.