Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi, Dkt. James Mataragio, ameielekeza Mamlaka ya Udhibiti Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA) kuongeza kasi ya utafiti wa awali katika maeneo mapya ya mafuta na gesi asilia ili kuvutia wawekezaji na kuongeza mapato ya taifa.

Akizungumza leo Februari 26, 2026, wakati wa Mkutano wa Tano wa Baraza la Wafanyakazi uliofanyika mkoani Morogoro, Dkt. Mataragio amesema juhudi hizo zitachochea uwekezaji, kupanua ushiriki wa wazawa na kuimarisha utekelezaji wa majukumu ya msingi ya taasisi hiyo.

Amesisitiza kuwa ni muhimu kwa PURA kuendelea kutambua na kuendeleza maeneo mapya ya miradi, kuyatangaza kwa wawekezaji pamoja na kusimamia kikamilifu majukumu yake kama yalivyoainishwa katika malengo ya kuanzishwa kwake.

Miongoni mwa majukumu hayo ni kusimamia na kufuatilia shughuli za utafutaji na uzalishaji wa mafuta na gesi asilia kwa kuzingatia sheria na taratibu, kuishauri Serikali kuhusu masuala ya mkondo wa juu wa mafuta na gesi, pamoja na kutangaza vitalu vilivyowazi kwa ajili ya uwekezaji ili kuongeza ugunduzi wa rasilimali hizo nchini.

Dkt. Mataragio amesema hatua hizo zitasaidia kuongeza mchango wa sekta ya mafuta na gesi katika ukuaji wa uchumi wa taifa na kuimarisha usimamizi wa rasilimali kwa manufaa ya Watanzania.







Tume ya Ushindani (FCC) imesema itaendelea na mchakato wa marekebisho ya sheria zake kwa lengo la kuimarisha ulinzi wa walaji, kudhibiti bidhaa bandia na kuhakikisha kunakuwepo ushindani wa haki unaochochea ukuaji wa uchumi na ajira nchini.

Hayo yamesemwa na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, Khadija Ngasongwa, wakati akifungua semina ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari iliyofanyika jijini Dar es Salaam.
Ngasongwa amesema marekebisho hayo yanalenga kumlinda mlaji dhidi ya bidhaa zisizo na ubora, matangazo ya upotoshaji pamoja na vitendo vinavyokwenda kinyume na misingi ya ushindani wa haki sokoni.
Amesema moja ya vipaumbele vya Tume hiyo ni kuimarisha udhibiti wa bidhaa bandia zinazoingia sokoni, akibainisha kuwa bidhaa hizo huathiri afya za wananchi, hupunguza mapato ya Serikali na kuwanyima wafanyabiashara halali fursa ya kukuza biashara zao.
“Jukumu letu ni kuhakikisha uchumi unakua kwa misingi ya ushindani wa haki. Matokeo yake ni kuongezeka kwa uwekezaji na ajira kwa wananchi,” alisema Ngasongwa.
Aidha, amesema FCC itaendelea kukutana mara kwa mara na waandishi wa habari pamoja na wadau mbalimbali kwa lengo la kutoa taarifa sahihi kuhusu majukumu yake na kusikiliza changamoto za wananchi ili kuzipatia ufumbuzi kwa wakati.
Katika hatua nyingine, amesema kuna maboresho yanayofanyika kupitia TANOGA — muunganiko wa taasisi za Serikali za udhibiti pamoja na mawakala wa forodha — kwa lengo la kuimarisha usimamizi wa bidhaa zinazoingia nchini.
Ngasongwa ameongeza kuwa taasisi hizo zinaelekea kuingia katika mfumo wa kidijitali utakaopunguza mwingiliano wa moja kwa moja kati ya watumishi na wateja, hatua itakayosaidia kuongeza uwazi, kupunguza urasimu na kudhibiti mianya ya vitendo visivyo vya kiadilifu.
FCC imeahidi kuendelea kushirikiana na taasisi nyingine za Serikali pamoja na sekta binafsi ili kuhakikisha mazingira ya biashara nchini yanabaki kuwa salama, yenye ushindani wa haki na yenye manufaa kwa wananchi.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani (FCC), Khadija Ngasongwa, akizungumza wakati akifungua semina ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari iliyoandaliwa na Tume hiyo, iliyofanyika jijini Dar es Salaam jana, Februari 24, 2026.
Makamu wa Mwenyekiti wa Chama cha Waandishi Habari Mkoa wa Dar ea Salaam (DARPC) Mary Geofrey akitoa maelezo kuhusiana na semina ya FCC itavyochochea ushindani wa soko ,jijini Dar es Salaam.
Semanina ikiendelea 
Picha pamoja ya wafanyakazi wa FCC na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC Khadija Ngasongwa katika Semina ya Waandishi wa Habari jijini Dar es Salaam.
Picha pamoja ya waandishi wa Habari na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC Khadija Ngasongwa katika Semina ya Waandishi wa Habari jijini Dar es Salaam.



Victoria Falls, Zimbambwe 

Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika – SADC) imeeleza kuvutiwa na mikakati ya Tanzania katika kuharakisha matumizi ya nishati safi ya kupikia, hususan hatua ya kuondoa kodi na kutoa ruzuku kwa vifaa kama mitungi ya gesi na majiko banifu, pamoja na kampeni za uhamasishaji kwa wananchi.

Akizungumza katika mdahalo wa Mawaziri kuhusu Nishati endelevu katika maadhimisho ya Wiki ya Nishati Endelevu ya SADC inayofanyika Victoria Falls, Zimbabwe (23–27 Februari 2026), Naibu Waziri wa Nishati Mhe. Salome Makamba amesema Tanzania inalenga kufikia asilimia 80 ya matumizi ya nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034, huku Mpango Mahsusi wa Taifa wa Nishati ukilenga asilimia 75 ifikapo 2030.

Mhe. Salome amesema Serikali imeweka mkazo kwa taasisi zinazohudumia zaidi ya watu 100 zikiwemo magereza, kambi za jeshi, shule na masoko makubwa  kwa kuzifungia mifumo ya nishati safi ya kupikia, hatua iliyotajwa kuwa ya ubunifu na yenye matokeo chanya.

Aliongeza kuwa Tanzania imefikisha umeme katika vijiji vyote 12,318 vya Tanzania Bara, na kuongeza upatikanaji wa umeme hadi asilimia 85.5. Uwezo wa uzalishaji umefikia megawati 4,437 na unatarajiwa kuongezeka hadi megawati 8,000 ifikapo 2030.

Kwa upande wake Katibu Mtendaji wa SADC, Mhe. Elias Magosi aliipongeza Tanzania kwa kuongoza juhudi za kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia katika Ukanda, hivyo kuchochea mabadiliko chanya ya kijamii, kiuchumi na kimazingira katika ngazi zote za maendeleo

Maadhimisho hayo yalifunguliwa rasmi na Makamu wa Rais wa Zimbabwe, Constantino Chiwenge amesisitiza umuhimu wa nchi za Afrika kutumia rasilimali za nishati jadidifu kama chachu ya maendeleo ya kiuchumi.









Kwa masikitiko makubwa na huzuni nzito, tumepokea taarifa ya kifo cha Mwadhama Polycarp Cardinali Pengo, Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam.
Marehemu alikuwa mchungaji mwaminifu na kiongozi mwenye hekima na busara, aliyeilitumikia Kanisa na Taifa kwa uaminifu mkubwa, akiacha alama isiyofutika katika mioyo ya wengi.
Kwa niaba yangu binafsi na kwa niaba ya Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira (TRAMEPRO), ninawasilisha salamu za rambirambi kwa Kanisa Katoliki, familia ya marehemu, waumini wote, na Watanzania wote walioguswa na msiba huu mkubwa katika Kanisa na Taifa letu.
Tunamwomba Mwenyezi Mungu ailaze roho ya marehemu mahali pema peponi, apumzike kwa amani ya milele.
“Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo alikuwa kama sisi, nasi tutakuwa kama yeye; hivyo tujiandae.”
Imetolewa na:
Boniventura Mwalongo
Katibu Mkuu – TRAMEPRO
 
 


Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) na Mamlaka ya Udhibiti wa Nafaka na Mazao Mchanganyiko (COPRA) zimeagizwa kuwa na mkakati wa kuwawezesha wakulima kuanzia uzalishaji ukusanyaji hadi  uuzaji ili kuleta tija na bei nzuri ya Mazao.

Vilevile  Serikali imetoa rai kwa wakulima na wafanyabiashara kuwa waaminifu na kuunga mkono Mfumo wa Stakabadhi za Ghala kwa kuimarisha upatikanaji wa pembejeo, mbegu, teknolojia, na masoko ya uhakika ili kuongeza thamani ya mazao ya kilimo, kulinda maslahi ya wakulima, kuongeza ajira na kuimarisha uchumi wa nchi.

Hayo yameelezwa Februari 25, 2026 na Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe.Judith Kapinga (Mb), wakati wa  kufunga msimu wa Mauzo ya Mfumo wa Stakabadhi za Ghala kwa msimu wa 2025/2026 na kufungua msimu mpya wa 2026/2027, hafla iliofanyika mkoani Simiyu.

Aidha ameiagiza, WRRB kutoa elimu  na kuwahamasisha wakulima, wafanyabiashara, wasimamizi wa ghala, na wadau wengine muhimu kutumia Mfumo huo ili kuongeza uelewa na kuboresha ushiriki wao pamoja na wale wenye maghala ambayo hayajakidhi vigezo  ili  wafanikiwe kutoa huduma bora na kuongeza ufanisi wa utendaji kazi wa  mfumo huo.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe. Anamringi Macha amesema kufunga na kufungua Msimu wa Mauzo ya Mazao katika Mkoa huo kumekuwa ni chachu na hamasa kwa Wananchi kwa kuwa wameelewa maana na faida za kuendelea kutumia Mfumo huo. 

Mkurugenzi wa WRRB, Bw. Asangye Bangu, amesema msimu wa 2025/2026 umerekodi mauzo ya zaidi ya tani milioni 1.1 za mazao, ikiwa ni ongezeko la 43% kutoka msimu uliopita. Wakulima wamejipatia Shilingi trilioni 2.4, huku korosho, mbaazi, na ufuta yakiongoza mauzo hayo. 

Aidha, Mfumo umepanuka kutoka wilaya 65 hadi 114, huku idadi ya waweka mali ikipanda kutoka 224 hadi 788, hali iliyoziongezea Halmashauri mapato ya ushuru kufikia Shilingi bilioni 65 na kuzalisha ajira zaidi ya 11,430 rasmi na zisizo rasmi na kuongeza leseni za maghala kufulia 286.

Katika msimu wa 2026/2027, WRRB  imelenga kuingiza sekta za mifugo, ngozi, na mwani kwenye mfumo wa stakabadhi za ghala na inahimiza Sekta binafsi kuanzisha Maghala bora yanayohamishika.

Nao Watumiaji  wa  Mfumo huo katika Mkoa wa Simiyu Bw. Daud Mpina  na Mariam Litwina wananufaika na Mfumo huo kwa kuuza Mazao yao katika Mnada kwa uwazi  kwa bei nzuri na kupata fedha kwa wakati na wameiomba Serikali kuendelea kuboresha Mfumo huo.

 


Serikali imesema itaendelea kuimarisha malezi ya watoto na utoaji wa mafunzo ya ustawi wa jamii kwa wananchi ili kupunguza changamoto za misongo ya mawazo, migogoro ya kifamilia na matatizo ya kisaikolojia, sambamba na kujenga jamii yenye maadili mema, ustawi imara na uwezo wa kukabiliana na changamoto za maisha ya kila siku.

Akizungumza wakati wa ziara yake katika Taasisi ya Ustawi wa Jamii Kampasi ya Kisangara wilayani Mwanga mkoani Kilimanjaro, Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi amesema Serikali inatambua umuhimu wa taasisi hiyo katika kutoa wataalamu na elimu kwa jamii kuhusu malezi, makuzi na maendeleo ya watoto pamoja na ustawi wa familia. Amesema hali hiyo inachangia kujenga jamii yenye utulivu na maendeleo endelevu.

“Serikali inaendelea kuweka mkazo katika eneo la malezi ya watoto na utoaji wa elimu ya ustawi wa jamii kwa wananchi kwa sababu tunaamini kuwa familia imara ndiyo msingi wa jamii imara. Kupitia mafunzo haya tunalenga kupunguza misongo ya mawazo, kuimarisha afya ya akili na kuhakikisha watoto wanalelewa katika mazingira salama na yenye maadili mema.” alisema Mahundi.

Aidha, amesema Wizara itaendelea kushirikiana na Taasisi hiyo pamoja na wadau wengine kuhakikisha elimu hiyo inawafikia wananchi wengi zaidi, kuimarisha uwezo wa wataalamu wa ustawi wa jamii ili watoe huduma bora zinazokidhi mahitaji ya jamii na kusaidia kukabiliana na changamoto zinazojitokeza katika familia na jamii kwa ujumla.

Kwa upande wake, Katibu Tawala Wilaya ya Mwanga Mpapalike Mfaume amepongeza mchango wa Taasisi hiyo katika kutoa elimu na mafunzo kwa wananchi, akisema hatua hiyo imekuwa na manufaa makubwa katika kuimarisha ustawi wa jamii na kusaidia kupunguza changamoto za kijamii katika wilaya hiyo.

“Tutaendelea kuimarisha ushirikiano wetu na Taasisi ya Ustawi wa Jamii Kampasi ya Kisangara ili kuhakikisha wananchi wetu wanaendelea kupata elimu na huduma za ustawi wa jamii, kwa kuwa tunaamini taasisi hii ni nguzo muhimu katika kusaidia kujenga jamii yenye ustawi, maadili mema na maendeleo endelevu,” alisema Mpapalike

Awali, akisoma taarifa ya Taasisi hiyo Meneja wa Taasisi ya Ustawi wa Jamii Kampasi ya Kisangara Dkt. Leah Mwaisango amesema chuo kinaendelea kutoa mafunzo ya ngazi mbalimbali za taaluma ya ustawi wa jamii pamoja na mafunzo maalum kwa jamii, hatua inayolenga kuongeza uelewa wa masuala ya malezi, makuzi ya watoto, ustawi wa familia na huduma za kijamii ili kujenga jamii yenye ustawi na maendeleo.

“Taasisi imeendelea kutekeleza jukumu lake la kutoa mafunzo kwa wanafunzi na jamii kwa ujumla, lengo likiwa ni kuzalisha wataalamu wenye ujuzi na kuwajengea uwezo wananchi ili waweze kukabiliana na changamoto za kijamii, kuimarisha malezi ya watoto na kuchangia maendeleo ya jamii na Taifa kwa ujumla,” alisema Dkt. Leah.

Ziara hiyo ni sehemu ya juhudi za Serikali za kuimarisha taasisi zake na kuhakikisha zinaendelea kutoa mchango mkubwa katika kukuza ustawi wa jamii, malezi bora ya watoto na afya ya akili, ikiwa ni pamoja na kuhakikisha wananchi wanapata elimu na huduma zinazowawezesha kuishi maisha yenye ustawi na tija.