•Aitaka kamati iliyoshiriki majadiliano ya awali kujadiliana tena

Na OWM - TAMISEMI, Kibaigwa


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amemshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan na Kampuni ya Barrick - Twiga Minerals kwa kupeleka tabasamu mashuleni kupitia majadiliano waliyoyafanya ambayo yalipelekea Barrick kuchangia zaidi ya shilingi bilioni 70 za kitanzania ambazo zimewezesha ujenzi wa madarasa, mabweni na matundu ya vyoo katika shule za sekondari 132 nchini. 

Prof. Shemdoe ametoa pongezi hizo kwa Mhe. Rais na Kampuni ya Barrick - Twiga Minerals Julai 02, 2026 akiwa katika Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Kibaigwa iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Kongwa, wakati wa hafla ya uzinduzi wa mradi wa miundombinu ya shule za kidato cha tano na sita, ambao unaofadhiliwa kupitia ushirikiano wa Serikali na Kampuni ya Barrick - Twiga Minerals. 

“Nampongeza sana Mhe. Rais kwa kuwaona Barrick kama wadau muhimu, na nawashukuru na kuwapongeza Barrick kwa kuleta fedha za kuwekeza kwenye sekta hii muhimu ya elimu,” ameeleza Prof. Shemdoe.

Prof. Shemdoe amefafanua kuwa, ni chini ya uongozi makini wa Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ndipo yalipoanzishwa majadiliano kati ya Serikali na Kampuni ya Barrick ya kuimarisha ushirikiano katika kuchangia maendeleo ya jamii kupitia uwekezaji wa sekta ya elimu, na kuongeza kuwa majadiliano hayo yalipelekea kupatikana kwa zaidi ya bilioni 70 za kitanzania ziloizotumika kwenye ujenzi wa madarasa, mabweni na matundu ya vyoo.

Aidha, Prof. Shemdoe ameelekeza kamati iliyoshiriki kwenye majadiliano ya awali ya mwaka 2023 na Kampuni ya Barrick - Twiga Minerals kurejea tena kwenye majadiliano mengine na kampuni hiyo, ili awamu awamu ya pili ya mradi huo ikikamilika zipatikane fedha nyingine za kuendelea kujenga miundombinu bora ya elimu.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Kampuni ya Barrick - Twiga Minerals Bi Penina Kituku ambaye ni Meneja wa Fedha amesema kuwa, uwekezaji wa zaidi ya shilingi bilioni 70 za kitanzania walioufanya una maana kubwa kwa jamii na unakwenda moja kwa moja kuboresha mazingira ya ufundishaji na ujifunzaji, ikiwa ni pamoja kutoa fursa kwa wanafunzi kusoma katika mazingira bora na salama.

Naye, Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI anayeshughulikia elimu Bw. Atupele Mwambene,amesema kwamba mradi huo ulianzishwa kwa lengo la kuongeza fursa za upatikanaji wa elimu kwa wanafunzi wenye ufaulu mzuri ambao wanajiunga na kidato cha tano, na kuongeza kuwa afua ambazo zimetekelezwa nchi nzima mpaka hivi sasa ni ujenzi wa madarasa 1090, mabweni 270 na matundu ya vyoo 1640.

Akizungumza kwa niaba ya wakazi wa Kibaigwa, Bw. Alex Sailemi amesema kuwa, wakazi wa Kibaigwa wanayo sababu ya kuishukuru Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan  pamoja na Kampuni ya Barrick kwa kujengewa miundominu ya madarasa, mabweni na matundu ya vyoo katika Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Kibaigwa.















 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI), Profesa Riziki Shemdoe akizindua jiwe la msingi la ujenzi wa madarasa sita na mabweni mawili katika Shule ya Sekondari Kibaigwa, mkoani Dodoma. Kushoto ni Meneja wa Fedha wa Barrick nchini, Penina Kituku.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI), Profesa Riziki Shemdoe akizindua jiwe la msingi la ujenzi wa madarasa sita na mabweni mawili katika Shule ya Sekondari Kibaigwa, mkoani Dodoma.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI), Profesa Riziki Shemdoe, akiwa pamoja na ujumbe kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI) na viongozi wa Mkoa wa Dodoma, wakikagua maendeleo ya mradi wa ujenzi wa madarasa na mabweni katika Shule ya Sekondari ya Wasichana Kibaigwa, mkoani Dodoma.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI), Profesa Riziki Shemdoe, akiwa pamoja na ujumbe kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI) na viongozi wa Mkoa wa Dodoma, wakikagua maendeleo ya mradi wa ujenzi wa madarasa na mabweni katika Shule ya Sekondari ya Wasichana Kibaigwa, mkoani Dodoma.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI), Profesa Riziki Shemdoe, akiwa pamoja na ujumbe kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI) na viongozi wa Mkoa wa Dodoma, wakikagua maendeleo ya mradi wa ujenzi wa madarasa na mabweni katika Shule ya Sekondari ya Wasichana Kibaigwa, mkoani Dodoma.
Muonekano wa sehemu ya majengo katika Shule ya Sekondari ya Wasichana Kibaigwa, mkoani Dodoma.
Muonekano wa sehemu ya majengo katika Shule ya Sekondari ya Wasichana Kibaigwa, mkoani Dodoma.
Muonekano wa sehemu ya majengo katika Shule ya Sekondari ya Wasichana Kibaigwa, mkoani Dodoma.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI), Profesa Riziki Shemdoe, akiwa pamoja na ujumbe kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI) na viongozi wa Mkoa wa Dodoma, wakikagua maendeleo ya mradi wa ujenzi wa madarasa na mabweni katika Shule ya Sekondari ya Wasichana Kibaigwa, mkoani Dodoma.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI), Profesa Riziki Shemdoe akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi wa awamu ya pili ya mpango wa Barrick–Twiga Future Forward Education Program katika Shule ya Sekondari ya Wasichana Kibaigwa, mkoani Dodoma.
Meneja Mkazi wa Barrick nchini, Dkt. Melkiory Ngido akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya uzinduzi wa awamu ya pili ya mradi wa Barrick–Twiga Future Forward Education Program uliozinduliwa Kibaigwa, mkoani Dodoma, na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI), Profesa Riziki Shemdoe.
Meneja Mkazi wa Barrick nchini, Dkt. Melkiory Ngido (kulia) akipeana mkono na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI), Profesa Riziki Shemdoe, baada ya uzinduzi wa awamu ya pili ya mpango wa Barrick–Twiga Future Forward Education Program unaotekelezwa nchini kote kwa lengo la kuboresha miundombinu katika shule za sekondari zenye madarasa ya Kidato cha Tano na Sita.
Meneja wa Fedha wa Barrick nchini, Penina Kituku, akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi wa awamu ya pili ya mpango wa Barrick–Twiga Future Forward Education Program uliofanyika katika Shule ya Sekondari ya Wasichana Kibaigwa, mkoani Dodoma.

***
Kampuni ya Barrick, inayofanya shughuli zake kwa ubia na Serikali kupitia Twiga Minerals, imeahidi kwamba kupitia programu yake ya Barrick-Twiga Future Forward Education Program itaendelea kufanya kazi na Serikali ya Awamu ya Sita kwenye sekta ya elimu kwa kuboresha miundombinu ya elimu, kuwezesha mazingira rafiki ya kusomea kwa ajili ya kuchochea maendeleo ya taifa kwenye sekta hiyo.

Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya uzinduzi wa kitaifa wa mradi huo wa awamu ya pili, Meneja Mkazi wa Barrick nchini, Dkt. Melkiory Ngido, amesema kwamba baada ya makubaliano na Serikali mwaka 2023, kampuni hiyo ya Barrick ilikubali kutoa zaidi ya Tsh bilioni 70 kwa ajili ya ujenzi wa madarasa, mabweni na matundu ya vyoo katika shule za sekondari nchini kote.

“Mradi huu wa Barrick-Twiga Future Forward Education Program unalenga kuwekeza kwa Watanzania kwa kuweka mbele maslahi ya jamii kwa kutoa kipaumbele kwenye uboreshaji wa miundombinu kwenye sekta ya elimu ambayo itatengeneza mazingira bora zaidi ya kujifunza na kufundishia kwa pande zote, walimu na wanafunzi,” amesema Dkt. Ngido.

Aliongeza kwamba programu hiyo leo imezinduliwa kwa kujengwa madarasa sita na mabweni mawili ambayo yote kwa pamoja yana madawati na vitanda kwa ajili ya wanafunzi wa kike wa Kidato cha Tano na Sita wa Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Kibaingwa, mkoani Dodoma.

Amesema kwamba mradi huo unalenga kujenga madarasa 1,090, majengo ya maliwato na vyoo 1,640 na mabweni 270 katika shule 161 nchini kote ili kusaidia kuwapatia malazi wanafunzi takribani 190,000 wa Kidato cha Tano na Sita.

Alifafanua kwamba kampuni hiyo ya Barrick ni mdau mkubwa kwenye sekta ya elimu baada ya hivi karibuni kuingia makubaliano na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) na kutoa ufadhili wa Tsh bilioni 25 kwa ajili ya kufanya tafiti, uzalishaji wa wanataaluma na kuwezesha sekta ya madini kupata wataalamu wa kutosha wenye maarifa.

“Tangu mwaka 2020, baada ya Twiga Minerals kuundwa, Barrick imekuwa ikishirikiana na Serikali katika kuendeleza sekta ya madini ili iweze kuleta tija na maendeleo endelevu kwa nchi yetu,” amesema Dkt. Ngido.

Naye, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI), Profesa Riziki Shemdoe, amesema kwamba sekta ya elimu ina mchango mkubwa sana kwenye maendeleo ya taifa na ustawi wa watu wake, na ni muhimu miundombinu hiyo itunzwe na kulindwa kwa maslahi ya vizazi vijavyo.

“Nachukua nafasi hii kuwashukuru sana kampuni ya Barrick kwa fedha hizi za uwekezaji kwenye sekta ya elimu na nina imani yangu wataendelea kutusaidia baada ya awamu hii ya pili kukamilika, na ni kwa sababu mazungumzo ya awali aliyafungua Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, na mimi jukumu langu ni kuendeleza tu juhudi za Rais,” amesisitiza.

Kwa upande wake, Meneja wa Fedha wa Barrick, Penina Kituku, amesema kwamba uwekezaji huo kwenye sekta ya elimu ni muhimu kwa ajili ya kufungua milango ya elimu kwa Watanzania kwa kuboresha mazingira ya kusomea na kujifunzia.

“Tunajivunia kama Barrick kuwa kwenye safari hii ya maendeleo ya elimu hapa nchini na ni ahadi tutaendelea kushirikiana na Serikali katika kufanikisha watoto wa Kitanzania wanapata elimu katika mazingira bora na rafiki zaidi,” amesema Kituku.

Kampuni hiyo ya Barrick inaendesha migodi ya Bulyanhulu uliopo Kahama, Shinyanga, North Mara uliopo Tarime, Mara, na Buzwagi uliopo Kahama ambao upo kwenye hatua za mwisho za kufungwa.

Kampuni hiyo ya Barrick wiki hii ilitoa gawio la Serikali la Tsh 221,907,320,687 kwa Serikali ya Tanzania na kutunukiwa tuzo ya nafasi ya kwanza kwa kuongoza kutoa gawio kubwa mwaka huu kwa makampuni ambayo Serikali ina hisa, pamoja na kupata Tuzo ya Rais ya Mlipa Kodi Bora nchini.


Back To Top