Na Oscar Assenga, TANGA

WAZIRI Mkuu Dkt Mwigulu Nchemba amefanya ziara ya kutembelea utekelezaji wa mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki unaotekelzwa eneo la Chongoleani Jijini Tanga huku akiridhishwa na kasi ya utekelezaji wake unaoendelea kwa kuzingatiwa viwango vilivyowekwa.

Nchemba aliyasema hayo wakati akizungumza katika ziara yake eneo la Chongoleani Jijini Tanga linapoishia Bomba la Mafuta ambalo litasafirisha mafuta kutoka Hoima nchini Uganda hadi eneo la Chongoleani licha ya kuwepo kwa changamoto zilizojitokeza wakati wa utekelezaji wake.

Alisema kwamba kwamba mradi huo wa kimkakati ambao utagharimu Dola za Marekani Bilioni 5.65 ni kielelezo cha Undugu Kati ya Tanzania na Uganda ambapo mradi huo umefikia asilimia 81 ya utekelezaji wake

Ambapo alisema changamoto hizo ni pamoja na mlipuko wa ugonjwa wa Uviko 19 pamoja na mtikisiko wa uchumi wa dunia lakini akabainisha kuwa hatua zilizochukuliwa zimewezesha mradi huo kuendelea bila kuathiri ubora na malengo yake.
"Mradi umepiga hatua lakini wakati wa utekelezaji wa mradi huu kulikuwepo na changamoto ikiwemo dunia kupita kwenye misikusuko ya kiuchumi na mabadilio ya sera za kiuchumi lakini umeendelea kutekelezwa kwa kasi jambo ambalo linaendelea kuipa heshima nchi yetu pamoja na ndugu zetu tunaotekeleza mradi huo kwa pamoja "Alisema

Mradi huo wa EACOP una urefu wa takribani Kilomita 1,444 ukianzia Hoima nchini Uganda hadi Chongoleani Tanzania na unatarajiwa kusafirisha mafuta ghafi kutoka maeneo ya uzalishaji ya Uganda hadi kwenye Kituo cha Kuhifadhi na Kusafirisha mafuta eneo la Chongoleani Jijini Tanga.

Alisema kwamba mradi huo unatajwa kuwa miongoni mwa miradi mikubwa ya kimkakati katika ukanda wa Afrika Mashariki ukilenga kuchochea ukuaji wa uchumi na kuongeza ajira kwa wananchi pamoja na

Aidha Waziri Mkuu huyo aliwatahadharisha watu wanaoanzisha makampuni na kuyaita ya wazawa huku yakiwa yanamilikiwa na wageni ili kunufaika na fursa ya “Loal Content” ya ushirikishwaji wa watanzania mradi kwamba watakapogundulika watafungiwa na hawatafanya kazi tena hapa nchini kwani hivyo ni kuwatapeli watanzania na kuwaibia fursa

Awali akizungumza katika ziara hiyo,Naibu Waziri wa Nishati Salome Makamba alisema kwamba katika mradi huo ulianza mwaka 2022 na unatarajiwa kukamilika Julai 2026 huku akieleza Serikali kwa kushirikiana na EACOP imekamilisha zoezi la kuthamini na utwaaji wa ardhi ya mradi.

Alisema kwamba hadi kufikia Januari 2026 Jumla ya Sh. Bilioni 35.06 zimetumika kulipa stahiki ya fidia kwa wananchi 9,869 kati ya wananchi 9,927 sawa na asilimia 96.4 kwa wanaopisha eneo la mradi na mkoani Tanga wananchi 1,688 wamefidiwa na kulipwa Jumla ya Bilioni 10.49.

Aidha alisema wananchi 294 wamenufaika kwa kujengewa nyumba 340 za makazi mbadala na wameshakabidhiwa nyumba zao hapa Tanga walionufaika ni wananchi 43.

Alisema kwamba wananchi wa Mkoa wa Tanga waliopatiwa udhamani wa chakula ni 1,200 huku wananchi 191 wameshiriki mafunzo ya ufugaji wa kuku,nyuki na ujasiriamali ili kuongeza kipato.

Makamba alisema katika mkoa huo miundombinu iliyojengwa ni pamoja na kituo kimoja cha Afya na kituo kimoja cha kupunguza mgandamizi wa mafuta ghafi kilichopo Handeni,Matenki Mawili ya Kuhifadhia Mafuta yaliyopo Tanga na Gati ya kupakia mafuta na kituo kikuu cha kuongeza ulinzi wa bomba la mafuta.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Tanga Balozi,Dkt Batilda Burian alisema wana Tanga wanamshukruu Rais kwa jinsi ambavyo maono yake na Rais wa Uganda Yoweri Museveni kwamba mradi umekuwa mzuri na shughuli zimekwenda vizuri na wananchi wa Tanga wamepata ajira.

Alisema pia kwa waliopitiwa na mradi waliweza kupata fidia bila kuwepo kwa changamoto yoyote lakini waliweza kusaidiwa na mashamba yaliyoguswa waliweza kulimiwa huku akiwashukuru EACOP kuna maeneo walikwenda kwa sababu walikwenda na utaalamu wakarudi kumueleza kuna changamoto ya uharibifu wa panya wa mazao iliwasaidia nao kuwaeleza wizara na hivyo kuondosha changamoto hiyo.

Mkuu wa Mkoa alisema kwamba zaidi vijana wa Tanga wameweza kushirikiana na wahandisi na wanashukuru mradi upo salama na hawajapata changamoto yoyote ya watu kupata madhara na suala la mazingira kwa sababu mradi umekwenda kwenye bahari wamehakikisha maeneo yenye uoto asili waliweza kuzingatia na hata kuchepusha ili wasiharibu na wanazingatia mazingira ya bahari.





Na Hadija Bagasha - Tanga


Imeelezwa kuwa ongezeko la mifarakano na kuvunjika kwa ndoa nyingi kwenye jamii imekuwa chanzo kikuu cha mmomonyoko wa maadili kwa watoto wengi na kwamba changamoto za kifamilia zimekuwa zikiathiri kwa kiasi kikubwa makuzi ya watoto na kuwaingiza katika hatari ya kuharibika kitabia na hata kuathirika kisaikolojia.


Kauli hiyo imetolewa na Mchungaji Ibrahim Joram wakati wa mahafali ya nne ya Chuo cha Theolojia na uongozi cha Eclea Kampasi ya Tanga, ambapo alisisitiza kuwa athari za kuvunjika kwa ndoa haziishii kwenye mgawanyiko wa mali au makazi, bali huacha alama ya kudumu katika nafsi za watoto.

Kwa mujibu wa mchungaji huyo, watoto wanaokulia katika mazingira yenye migogoro ya mara kwa mara au wazazi waliotengana hukosa msingi imara wa malezi na mwongozo wa karibu kutoka kwa pande zote mbili za wazazi ambapo hali hiyo huwafanya baadhi yao kukosa upendo, uangalizi na haki ya msingi ya kusikilizwa na kueleweka, jambo linaloweza kuwafanya watafute faraja au uthibitisho nje ya familia, wakati mwingine kujiingiza katika makundi au matendo yasiyofaa.


Kwa upande wake Katibu mkuu wa huduma ya Eclea Tanzania Reverine Mdimi, alieleza kuwa watoto wengi baada ya wazazi kutengana hujikuta wakikumbwa na msongo wa mawazo, hasira, huzuni au kukosa mwelekeo sahihi wa maisha hivyo bila msaada wa karibu wa wazazi, walezi au jamii, watoto hao huweza kujiingiza katika mienendo mibaya inayoweza kuharibu mustakabali wa maisha yao.


Wakizungumza katika mahafali hayo, wachungaji waliwataka wazazi kujijenga kiimani na kiroho ili kuimarisha misingi ya ndoa na familia na kwamba imani thabiti humsaidia mzazi kuwa na uvumilivu, busara na uwezo wa kusuluhisha migogoro kwa njia ya mazungumzo badala ya kuishia katika kuvunjika kwa ndoa.


Naye mchungaji Joas Stephano wa makanisa ya pentecoste motomoto aliwahimiza wanandoa kutafuta ushauri wa kitaalamu na wa kiroho mapema wanapokumbana na changamoto, ili kulinda ustawi wa watoto wao.


Kwa upande wa taasisi za elimu ya dini, wachungaji hao walibainisha kuwa mafunzo yanayotolewa katika Chuo cha Eclea hayalengi tu masomo ya kitheolojia, bali pia yanatoa elimu ya maisha.


"Eclea inatoa masomo rasmi yanayohusika na mambo kama hayo moja msamaha na maridhiano, mbili ndoa na malezi bora ni mafunzo tunayoyatoa kwa kina zaidi pamoja na kutoa ushauri wa kijinsia kwa maana tunawashauri watu namna gani bora ya kutatua migogoro ya kifamilia hasa kwenye eneo hili la ndoa na familia, "akisisitiza Mchungaji Mdimi.


Walieleza kuwa viongozi wa dini wanaohitimu masomo ya kidini wanatarajiwa kuwa mwanga katika jamii, wakifundisha si tu neno la Mungu, bali pia misingi ya malezi bora, maadili na utatuzi wa migogoro ya kifamilia.


Mahafali hayo yalikuwa fursa ya kuwakumbusha wahitimu kuwa huduma yao kwa jamii inapaswa kuanzia katika kuimarisha familia, ambayo ndiyo msingi wa taifa lolote huku Wachungaji wakiwahimiza wahitimu kuwa mabalozi wa amani na maridhiano, wakisaidia kurejesha matumaini kwa familia zinazokumbwa na misukosuko na kulinda kizazi dhidi ya athari za kuvunjika kwa ndoa.


Kuvunjika kwa ndoa ni changamoto inayoweza kuzuilika endapo wazazi watachukua hatua za makusudi kujenga upendo, mawasiliano na imani ndani ya familia. Ni wito kwa jamii nzima kusimama pamoja kulinda maadili ya watoto, kwani mustakabali wa taifa huanzia katika uimara wa familia.
















 MKUU wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo ameamsha shangwe baada ya kufanikiwa kumaliza mgogoro wa ardhi wa muda mrefu ulihusu eneo lililotengwa na Serikali kwa ajili ya maakaburi kuvamiwa na kujengwa nyumba za makazi ya watu.


Eneo lilovamiwa lipo Kimani Mtaa wa Kinyamwezi, Kata ya Pugu, Ilala Jijini Dar es Salaam ambapo wakazi wa eneo hilo walimtuhumu Elizabeth Mwakapangala kuliuza huku akifukua makaburi bila ya kufuata sheria.

Mpogolo akizungumza na wananchi wa eneo hilo katika mkutano wa hadhara uliofanyika Februari 13, 2026 ambao ulihudhuriwa na baadhi ya wajumbe wa kamati ya ulinzi na usalama pamoja na Mkurugenzi wa Jiji la Dar es Salaam, Elihuhuruma Mabelya alisema eneo hilo lilitengwa na Serikaali kwa ajili ya makaburi.

“Eneo hili lenye ramani ya upimaji namba E' 351\96, ya mwaka 2000, Kiwanja Na. 423 Kitalu N Pugu Mwakanga Kata ya Pugu Halmashauriya Jiji la Dar es Salaam lilitengwa kwa matumizi ya makaburi kwa mujibu wa mipango miji, lakini baadhi ya yetu yaani Mama Elizabeth alifungua kesi ya ardhi namba 202/2020 kati yake Elizabeth Mwakapangala ambaye alikuwa msimamizi wa mirathi ya Saidi Shomari Loko akiipeleka Halmashauri ya Jiji, Mamlaka ya Viwanja vya Ndege (TAA) na Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mahakamani,” alisema Mpogolo.

Mpogolo akisoma hukumu katika mkutano huo iliyotolewa na Mhe. Jaji A. M. Msafiri aliyesikiliza kesi hiyo ilielekeza mlalamikaji Bi Elizabeth alipwe fidia na siyo kuuza eneo la makaburi wala kufukua makaburi ya watu na kutupa mabaki ya miili hiyo dampo kama alivyofanya.

Aidha, Mhe. Jaji Msafiri alitoa muongozo mzuri kwa mlalamikaji wa namna ya kupata haki yake ya fidia na kueleza kuwa Mahakama haina mamlaka ya kufuta ramani ya mipango miji iliyoandaliwa na Serikali au kuhoji mamlaka ya Rais ya kutwaa ardhi kwa manufaa ya umma.

Mpogolo alisema kufuatia hukumu hiyo mlalamikaji hakuwa na haki ya kuuza eneo hilo wala kuhamisha makaburi na nikinyume na katazo la Sheria ya Mipango Miji katika Kifungu cha 3 (e) cha sheria hiyo.

Akisisitiza katika mkutano huo Mpogolo alisema uhamishaji wa makaburi upo kwa mujibu wa sheria za nchi na kueleza kuwa mtu yeyote hawezi akatoka na maamuzi ya kikao cha familia na kwenda kuhamisha mwili wa mtu aliyezikwa kwenye kaburi husika ni lazima afuate utaratibu uliopo kisheria na miiko ya dini zetu.

Alisema mlalamikaji Elizabeth anapaswa kufuata utaratibu wa kisheria ili pate haki yake na si vinginevyo.

Mpogolo alisema awali mlalamikaji alisimamishwa kufanya chochote kwenye eneo hilo analodai ni lake lakini hakufuata maelekezo na sasa Serikali imekata rufaa uamuzi wa Mahakama na kuhusu kufukua Makaburi na kutupa mabaki ya miili wanakwenda kushughulika naye kwa mujibu sharia.

Aidha Wananchi hao wamedai kuwa eneo lenye mgogoro lilitengwa kwa ajili ya maziko, kama walivyoelekezwa na serikali ya mtaa na watu waliohamishwa kutoka Kipawa kupisha upanuzi wa Uwanjani wa Ndege wa Mwalimu Nyerere.

Leo amefika akiwa na Mkurugenzi wa Jiji la Dar es Salaam, Elihuhuruma Mabelya kwa lengo la kuwasikiliza wananchi hao na kuamuru kuwa wananchi hao wawe ma amani na waendelee na shughuli zao ambazo zimepangiwa na serikali kwa eneo hilo.

Akizungumza Mama Elizabeth, amekanusha madai hayo akieleza kuwa hajawahi kufukua makaburi hayo na kwamba eneo hilo siyo eneo la Makaburi na ni mali yake halali ambalo anazo nyaraka zote baada ya kushinda kesi mahakamani tarehe 20 Oktoba 2022.






Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu tarehe 14 Februari 2026 imetembelea Chuo cha Bahari Dar es Salaam (DMI) kwa ziara ya kikazi yenye lengo la kujua shughuli zinazofanywa na Chuo katika utekelezaji wa majukumu yake ya kitaifa.  


Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mwenyekiti wa Kamati Mhe. Moshi Kakoso aliipongeza menejimenti na watumishi wa DMI kwa juhudi kubwa katika kuzalisha wataalamu wanaochangia katika sekta ya bahari na usafiri wa majini. Aliahidi kuchukua hatua kuhusu changamoto na maoni yaliyotolewa na wajumbe wa Kamati na wabunge wengine ili kuhakikisha chuo kinaendelea kustawi na kufikia malengo yake ya kimkakati.  

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Uchukuzi Mhe. David Kihenzile alibainisha kuwa Serikali ya Awamu ya Sita imejikita katika kuboresha sekta ya usafiri wa majini kupitia ujenzi, ukarabati, na upanuzi wa bandari. Amesema jitihada hizo zinategemea nguvu kazi yenye ujuzi mkubwa, na kwamba DMI ni kitovu cha kuzalisha wataalamu watakaoiwezesha sekta hiyo kukua kwa kasi.  

Akizungumzia kuhusu Uchumi wa Buluu, Naibu Waziri alisema Serikali inaendeleza matumizi endelevu ya rasilimali za bahari na maziwa makuu kwa ajili ya kukuza uchumi wa taifa. Alisisitiza kuwa DMI ina wajibu wa kuzalisha wataalamu, kufanya tafiti, na kutoa ushauri wa kitaalamu utakaosaidia nchi kunufaika zaidi na rasilimali hizo. Aidha, aliongeza kuwa mafanikio ya sekta ya bahari na rasilimali za majini yanategemea kwa kiasi kikubwa wataalamu wanaotoka DMI.

Mkuu wa Chuo, Prof. Tumaini Gurumo, katika taarifa yake alieleza kuwa licha ya mafanikio yaliyopatikana, bado kuna uhitaji wa kuboresha miundombinu ya kufundishia na kujifunzia, pamoja na kuendelea kuwasomesha waalimu nje ya nchi.


Aliongeza kuwa chuo katika kuliona hilo kimeanza kutekeleza mpango wa upanuzi wa huduma zake katika Mikoa ya Dar es Salaam, Pwani, Lindi, Mwanza, Simiyu na Pemba ili kukidhi mahitaji ya  elimu na mafunzo ya bahari.

Alibainisha kuwa DMI inaendelea kunufaika kupitia ushirikiano na taasisi mbalimbali za kimataifa na sekta binafsi, ambao  huchukua wanafunzi na kuwapa mafunzo kwa vitendo kwa kutumia meli zao na kubadilishana uzoefu wa kitaaluma.  

Prof. Gurumo vilevile aliishukuru Serikali kwa kuendelea kukiwezesha chuo kutimiza majuku yake ikiwa ni pamoja na kukipatia vifaa vya kisasa vya kufundishia kama vile mitambo ya  kisasa ya mafunzo kwa vitendo (simulators), ambavyo vimeongeza ubora wa mafunzo unaoendana  na maendeleo ya teknolojia ya usafiri wa majini.  

Wajumbe wa Kamati walikipongeza chuo kwa mchango wake katika kukuza sekta ya bahari na kusema kuwa wameona umuhimu wa chuo hicho kuwezeshwa kwa miundombinu bora, meli ya mafunzo na vifaa vya kisasa ili kuimarisha uzalishaji wa wataalamu kwa maendeleo ya Uchumi wa Buluu.






Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi amesema ujenzi wa Kiwanda cha Kutengeneza Nguzo za Zege cha TCPM Tabora kinachomilikiwa na Shirika la Umeme Tanzania - TANESCO kupitia kampuni tanzu ya TCPM haukusudii kuathiri wala kudhoofisha uwekezaji wa sekta binafsi bali unaongeza uzalishaji wa nguzo za zege ili kukidhi mahitaji yaliyopo ambayo bado hayajatosheleza uhitaji wa nguzo hizo nchini.

Ameeleza hayo Februari 15, 2026 wakati akikagua mradi wa ujenzi wa Kiwanda cha Kutengeneza Nguzo za Zege cha TCPM Tabora, ambao umefikia asilimia 95 ya utekelezaji. Kiwanda hicho kitakuwa na uwezo wa kuzalisha wastani wa nguzo za zege 120 kwa siku.

“Kiwanda hiki si tishio kwa sekta binafsi; kinakuja kuongeza nguvu katika kazi ambazo tayari zilikuwa zinafanywa na sekta binafsi ya kuzalisha nguzo za zege,” amesema Ndejembi.

Ndejembi amefafanua kuwa TANESCO kwa mwaka 2025 ilikuwa na uhitaji wa nguzo za zege 80,000, lakini zilizopatikana kupitia sekta binafsi ni nguzo 40,000 jambo lililosababisha kutokufikiwa kwa malengo ya mahitaji hayo.

Ameeleza kuwa pamoja na Serikali kujenga kiwanda hicho, bado kuna fursa kwa sekta binafsi kuwekeza katika viwanda vya nguzo za umeme kutokana na mpango wa TANESCO wa kuendelea kufanya maboresho kwa kuondoa nguzo za miti na kutumia nguzo za zege katika usambazaji wa umeme nchini.

Aidha, Ndejembi ameitaka Bodi na Menejimenti ya TANESCO kusimamia kikamilifu ukamilishaji wa kiwanda hicho ili mitambo itakapowashwa iweze kufanya kazi kwa ufanisi na ubora kulingana na mpango na malengo ya Kiwanda hicho.

Kadhalika, amewataka wafanyakazi waliopata ajira na watakaoajiriwa kutunza miundombinu na mitambo ya kiwanda hicho pamoja na kuweka mpango madhubuti na endelevu wa uendeshaji ili kuepusha hasara zinazoweza kujitokeza.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Lazaro Twange amesema utekelezaji wa mradi wa kiwanda hicho cha nguzo za zege, kinachomilikiwa na Serikali kwa asilimia 100, hadi kukamilika kwake utagharimu Shilingi bilioni 7.9.

Twange ameeleza kuwa ujenzi wa kiwanda hicho upo katika hatua za mwisho za ukamilishaji, ambapo kufikia tarehe 20 Februari 2026 mkandarasi atakuwa amekamilisha kazi zote, tayari kwa kuanza uzalishaji.