Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete akizungumza na Wanataaluma ya Menejimenti ya Taarifa, Kumbukumbu na Nyaraka (hawapo pichani) wakati alipokuwa akifunga kikao kazi cha Mafunzo maalum ya kuwajengea uwezo wa kiutendaji Wanataaluma hao leo tarehe 12 Februari, 2026 Mjini Njombe.
Na Antonia Mbwambo, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora-Njombe
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete amewataka wanataaluma ya Menejimenti ya Taarifa, Kumbukumbu na Nyaraka kuzingatia maadili ya utendaji kazi kutokana na dhamana kubwa waliyonayo kwa maslahi mapana ya Taifa.
Mhe. Kikwete ameyasema hayo leo tarehe 12, Februari, 2026 alipokuwa akifunga kikao kazi cha mafunzo maalum ya kuwajengea uwezo wa kiutendaji wanataaluma ya Menejimenti ya Taarifa, Kumbukumbu na Nyaraka mkoani Njombe.
“Tambueni dhamana yenu ni kubwa sana kwa maslahi ya Taifa letu. Ni vizuri utaalamu wenu uzingatie maadili ya utendaji kazi ili kuepuka kuvuja kwa siri na kuepusha madhara yanayoweza kujitokeza kutokana na siri kuvuja,” amesisitiza Mhe. Kikwete.
Amesema kaulimbiu ya kikao kazi hicho isemayo “Kumbukumbu Sahihi leo, Maamuzi Sahihi kesho; Tunza siri kwa heshima ya Taifa” inaakisi kikamilifu mwelekeo wa Serikali katika kusimamia rasilimaliwatu na mifumo ya utendaji kazi na umuhimu wa kutunza siri kwa heshima ya Taifa. Na kuongeza kuwa hilo halina ubishi kwamba siri za nchi hii zinatakiwa kulindwa kwa wivu mkubwa. Hivyo, wataalamu wa kada hiyo wanalo jukumu kubwa la kuhakikisha kwa namna yoyote ile mtu yoyote haruhusiwi kuikanyaga taaluma hiyo wala kuvujisha siri.
Mhe. Kikwete amesema Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora ndio msimamizi wa Chama cha Wanataaluma hao (TRAMPA), hivyo itaendelea kuhakikisha Nyaraka za serikali zinabaki salama kwa kuendelea kutoa miongozo mbalimbali pamoja na kusimamia utekelezaji wake.
Amewapongeza waajiri waliotenga bajeti na kuwaruhusu watumishi wao kushiriki kikao kazi hicho huku akimuagiza Katibu Mkuu-UTUMISHI kuwaandikia barua waajiri wote serikalini kutenga bajeti ya ushiriki wa watumishi walio chini yao kwani vikao hivyo ni muhimu katika kukua kitaaluma.
Aidha, amesema Serikali itaendelea kushirikiana na TRAMPA katika kutekeleza majukumu yake ya kitaaluma na kiutumishi ikiwemo kuhamasisha matumizi ya mifumo ya kidijitali katika usimamizi wa Kumbukumbu na Nyaraka, hususani katika Ofisi za Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, ili kuongeza ufanisi, usalama wa taarifa,Uwajibikaji na upatikanaji wa kumbukumbu kwa wakati.
“Kwenye hili Mkurugenzi wa Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa ninakuagiza kushirikiana na TRAMPA kuzitambua na kuziorodhosha halmashauri ambazo zinazorota katika kukamilisha hili ili ziweze kupewa msukumo kwa maandishi,” ameongeza Waziri Kikwete.
Akizungumza kabla ya kumkaribisha Waziri Kikwete kuhitimisha kikao kazi cha wanataaluma hao, Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Mhe. Antony Mtaka alimshukuru Mhe. Kikwete kwa kuwapa heshima wanataaluma hao na wenyeji wa Mkoa wa Njombe kwa kufika mwenyewe kuhitimisha kikao kazi hicho.
Mhe. Mtaka amewaasa watumishi hao kuthamini kazi walizo nazo kwa kutekeleza majukumu yao kwa bidii, nidhamu na uadilifu kwani watu wengi wanatafuta kazi usiku na machana lakini hawapati.
Naye Mwenyekiti wa TRAMPA, Bi. Devotha Mrope amesema mada mbalimbali zimewasilishwa katika kikao kazi hicho ili kuwajengea uwezo wa kiutendaji wanataaluma hao.
Amesema takribani wanataaluma wa Menejimenti ya Taarifa, Kumbukumbu na Nyaraka 1900 wameshiriki kikao kazi hicho cha siku 4.

Mwenyekiti wa chama cha TRAMPA Bi. Devotha Mrope akitoa taarifa fupi ya kikao kazi cha Mafunzo maalum ya kuwajengea uwezo wa kiutendaji Wanataaluma ya Menejimenti ya Taarifa, Kumbukumbu na Nyaraka (hawapo pichani) kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (hayupo pichani) kabla ya Waziri huyo kufunga kikao hicho leo tarehe 12 Februari, 2026 Mini Njombe.

Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Mhe. Antony Mtaka akitoa neno la shukrani kabla ya kumkaribisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete kufunga kikao kazi cha Mafunzo maalum ya kuwajengea uwezo wa kiutendaji Wanataaluma hao leo tarehe 12 Februari, 2026 Mini Njombe.
Wanataaluma ya Menejimenti ya Taarifa, Kumbukumbu na Nyaraka wakimsikiliza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (hayupo pichani) walipokuwa katika kikao kazi cha Mafunzo maalum ya kuwajengea uwezo wa kiutendaji Mjini Njombe leo tarehe12 Februari, 2026

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete akisaini Kitabu cha wageni baada ya kuwasili katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Njombe alipokuwa akifunga kikao kazi cha Mafunzo maalum ya kuwajengea uwezo wa kiutendaji Wanataaluma hao leo tarehe 12 Februari, 2026 Mjini Njombe.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (kulia) akiteta jambo na Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Mhe. Antony Mtaka (kushoto) wakati waziri huyo akifunga kikao kazi cha Mafunzo maalum ya kuwajengea uwezo wa kiutendaji Wanataaluma hao leo tarehe 12 Februari, 2026 Mini Njombe
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete akiwa katika picha ya pamoja na Kamati ya Usalama ya mkoa wa Njombe baada ya waziri huyo kufunga kikao kazi cha Mafunzo maalum ya kuwajengea uwezo wa kiutendaji Wanataaluma hao leo tarehe 12 Februari, 2026 Mini Njombe.
Wanataaluma ya Menejimenti ya Taarifa, Kumbukumbu na Nyaraka wakimsikiliza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (hayupo pichani) walipokuwa katika kikao kazi cha Mafunzo maalum ya kuwajengea uwezo wa kiutendaji Mjini Njombe leo tarehe12 Februari, 2026

























