Na Heri Shaaban (Dar es Salaam)

Mkuu wa Wilaya ya Ilala Edward Mpogolo, amewasilisha Taarifa ya utekelezaji wa Ilani ya chama cha Mapinduzi CCM ya Desemba 2025 mpaka FEBRUARY 2026 kwa wajumbe wa Halmashauri Kuu ya ccm wilaya ya Ilala. 

Akiwasilisha taarifa hiyo Mkuu wa Wilaya Edward Mpogolo, amesema Halmashauri hiyo imejipanga kujenga vyumba vya madarasa kwa ajili ya kupokea wanafunzi  65000 ambapo Halmashauri hiyo imeweka fedha nyingi sekta ya Elimu. 

Alisema miradi yote Ilala imekamilika kwa asilimia 89 changamoto ilikuwa katika vyumba vya madarasa kwa sasa wanaenda kuitatua changamoto ndani ya wilaya Ilala. 

"Leo nimewasilisha taarifa ya utekelezaji wa Ilani katika taarifa hii tumeelekeza shilingi bilioni 80 kuelekezwa katika miradi mbalimbali ya maendeleo katika fedha  shilingi bilioni  347 zilizotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan ambapo natumia fursa hii kumpongeza Rais kwa kushusha Neema Ilala inaenda kuwa ya kisasa" amesema Mpogolo .

Katika hatua nyingine aliagiza viongozi wa ngazi ya kata kusimamia vikundi vya mikopo ya Serikali ya asilimia kumi ambayo inatolewa ngazi ya Halmashauri wakishirikiana Umoja wanawake UWT Wilaya ya Ilala katika kuratibu vikundi hivyo .

Akizungumzia migogoro ya ardhi ndani ya wilaya Ilala  ameagiza viongozi wa chama na Serikali kushirikiana pamoja katika kutatua changamoto hizo.

Alitumia fursa hiyo kuwapongeza Wajumbe wa Halmashauri Kuu wilaya ya Ilala wakiongozwa na Madiwani na Wabunge kwa kufanya kazi kwa kushirikiana 

Wakati huohuo Mkuu wa Wilaya Edward Mpogolo amesema Wenyeviti wa Serikali za mitaa 159 wa Wilaya ya Ilala hivi karibuni wanatarajia kukabidhiwa Vitamburisho vyao vya kazi  hivyo aliwataka wavute subira taratibu zote zimekamilika 

Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi CCM Wilaya ya Ilala Said Sidde alitumia fursa hiyo kumpongeza mkuu wa Wilaya Edward Mpogolo pamoja na Katibu Tawala Wilaya Charangwa Selemani na Watendaji wote kwa kuleta maendeleo makubwa Ilala. 

Mwenyekiti Side alisema Ilala wana mahusiano mazuri kati ya chama na Serikali katika utendaji wao wa kazi kila jambo wanashirikiana pamoja kujenga Serikali. 

Meya wa Halmashauri ya jiji la Dar es Salaam Nurudini sheta ameomba Wajumbe wa Halmashauri Kuu wilaya waweze kupatiwa mafunzo kwa ajili ya kuwajengea uwelewa kila mjumbe aweze kufanya kazi kwa Weledi.

















Wananchi Wilayani Kwimba na maeneo jirani, wameishukuru Taasisi ya Doris Mollel (Doris Mollel Foundation) kwa kuleta  mabadiliko makubwa katika Wilaya ya Kwimba, Mwanza, baada ya kufadhili na kusimamia ujenzi wa jengo la kisasa la Kimataifa la kuwahudumia Watoto wanaozaliwa kabla ya wakati (njiti) katika Hospitali ya Wilaya ya Kwimba, jengo linalosogeza huduma hizi muhimu karibu na wananchi kwa mara ya kwanza.

Mkuu wa Wilaya ya Kwimba Mhe. Ng’wilabuzu Ludigija ameridhishwa na utekelezaji wa mradi huo unaofadhiliwa na Taasisi ya Doris Mollel , akieleza kuwa jengo hilo litakuwa na mchango mkubwa katika kuokoa maisha ya Watoto.

Mkazi wa Kwimba, Joyce Emmanuel James, ameishukuru Taasisi ya Doris Mollel Foundation kwa kujenga jengo hilo, akieleza changamoto walizokuwa wanapitia kabla ya uwepo wa huduma hizo karibu.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) nchini Tanzania, Dkt. Alex Ntale Gasasira, ametambua uwekezaji huo na kusisitiza umuhimu wa uwepo wa huduma hizi karibu na jamii, akieleza kuwa mfumo huo unaendana na miongozo ya WHO inayosisitiza umuhimu wa Mama na Mtoto kuwa pamoja wakati wa matibabu.

Jengo hilo la kimataifa linalotarajiwa kuzinduliwa tarehe 28 Februari 2026 ,limefadhiliwa na kujengwa na Taasisi ya Doris Mollel (DMF) kwa lengo la kuboresha huduma za Watoto wachanga na kuleta matumaini mapya kwa Familia za Kwimba na maeneo ya jirani na limegharimu takribani Bil. 2.125 kwa kushirikiana na Taasisi ya Keep A Child Alive na Jhpiego.


















Meneja wa Ukaguzi wa Sekta za Umma, kutokea Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Bi. Rosemary Ruganuza,amezitaka taasisi za sekta ya umma kutumia kwa usahihi Mfumo Jumuishi wa Usimamizi wa Kodi za Ndani (IDRAS) ili kuongeza uwazi, uwajibikaji na ufanisi katika ukusanyaji na usimamizi wa mapato ya Serikali.

Kauli hiyo ameitoa leo Februari 25 Jijini Dodoma wakati akifungua mafunzo ya mfumo wa IDRAS yaliyoandaliwa na Idara ya Walipakodi Wakubwa wa TRA kwa taasisi za umma.

Bi. Ruganuza amesema matumizi sahihi ya mfumo huo yatasaidia taasisi za umma kutekeleza majukumu yao ya kikodi kwa wakati, kwa usahihi na kwa kuzingatia sheria na kanuni za kodi.

Amesema IDRAS ni sehemu ya mageuzi ya kidijitali yanayolenga kurahisisha huduma za kikodi, kupunguza makosa ya kibinadamu na kuongeza ufuatiliaji wa taarifa za walipakodi kwa njia ya kielektroniki.

“Matumizi sahihi ya IDRAS yataimarisha uwajibikaji, kuongeza uwazi na kuhakikisha majukumu ya kikodi yanatekelezwa kwa wakati na kwa usahihi. Ni wajibu kwa kila taasisi kuwa balozi wa ndani ya eneo lake la kazi,” asema Bi. Ruganuza.

 

-Ahimiza Mshikamano katika kujenga Tanzania Imara

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Clement Sangu amesisitiza umuhimu wa kudumisha mahusiano mema ili kuimarisha umoja wa Taifa na kuchochea maendeleo endelevu nchini.



Wapiga Kura 127,632 walioandikishwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura watashiriki katika uchaguzi wa kuchagua Mbunge katika Jimbo la Peramiho lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Songea, Mkoa wa Ruvuma na Kata ya Shiwinga iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi Mkoa wa Songwe.

 

Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji wa Rufaa Mhe. Jacobs Mwambegele ameyasema hayo leo Februari 25, 2026 mjini Songea Mkoani Ruvuma wakati akisoma risala maalum kuhusu uchaguzi katika jimbo na kata husika utakao fanyika kesho Februari 26, 2026 na kusema kuwa jumla ya vituo 373 vya Kupigia Kura vitatumika.

 

“Kati yao wapiga kura 120,780 ni wa Jimbo la Peramiho na wapiga kura 6,852 wapo katika kata ya shiwinga na jumla ya vituo 373 vya Kupigia Kura vitatumika, ambapo vituo 354 vipo Jimbo la Peramiho na vituo 19 vipo katika Kata ya Shiwinga Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi,”amesema Jaji Mwambegele.

 

Aidha, amesema kwa uchaguzi mdogo wa ubunge Jimbo la Peramiho vyama vya siasa 15 vimesimamisha wagombea na  kwa upande wa uchaguzi mdogo wa udiwani katika Kata ya Shiwinga vyama vya siasa nane (08) vimesimamisha  wagombea.

 

“Natumia fursa hii kuvikumbusha Vyama vya Siasa vinavyoshiriki uchaguzi kesho Februari 26, 2026 kuzingatia wajibu wao wa kuweka mawakala katika vituo vyote vya zoezi la kupiga, kuhesabu na kujumlishia kura. Wasimamizi wa uchaguzi katika Jimbo na Kata husika, wamekamilisha taratibu zinazoweka mazingira yanayowawezesha mawakala wa vyama vya siasa kufuatilia mchakato mzima wa uchaguzi,”alisema Jaji Mwambegele.

 

Amesema, mawakala hao, wanawajibika katika kulinda maslahi ya vyama na wagombea wao. Hivyo, wanapaswa kuzingatia Sheria, Kanuni, taratibu za Uchaguzi na maelekezo ya Tume katika utekelezaji wa majukumu yao vituoni.

 

Jaji Mwambegele amesema vituo vitafunguliwa saa 01:00 asubuhi na kufungwa saa 10:00 jioni na kwamba ifikapo muda wa kufunga kituo saa 10:00 kamili jioni, kama wapiga kura bado wapo kwenye mistari, mlinzi wa kituo atasimama nyuma ya mtu wa mwisho na zoezi la upigaji kura litaendelea hadi wapiga kura walio kwenye mstari watakapomalizika.

 

“Baada ya kumaliza kupiga kura, mpiga kura anatakiwa kuondoka eneo la kituo cha kupigia kura; na Mpiga kura awapo kituoni, anatakiwa kufuata maelekezo yote atakayopewa na karani mwongozaji wapiga kura,”amesema Jaji Mwambegele.

 

Kwa mpiga kura ambaye ameandikishwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura na taarifa zake zipo katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura lililopo katika kituo husika, lakini amepoteza kadi yake au kadi yake imeharibika, ataruhusiwa kupiga Kura kwa kutumia moja wapo ya vitambulisho cha Taifa NIDA, Leseni ya udereva au Pasi ya kusafiria (Passport).


Dar es Salaam, 23 Februari 2026 — Waziri wa Madini, Anthony Mavunde, amepongeza kwa ushirikiano wa kimkakati kati ya Benki ya CRDB na Tume ya Madini, akieleza kuwa mpango maalum wa kifedha uliozinduliwa leo kwa ajili ya wachimbaji wadogo ni hatua ya kihistoria itakayobadili kabisa mfumo wa upatikanaji wa mitaji katika sekta ya madini nchini.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa huduma hizo na utiaji saini wa Mkataba wa Makubaliano (MOU) uliofanyika katika hoteli ya Johari Rotana, Waziri Mavunde alisema sekta ya madini imeendelea kukua kwa kasi, ikichangia asilimia 10 ya Pato la Taifa na zaidi ya asilimia 56 ya mapato ya fedha za kigeni kupitia mauzo ya nje yanayozidi dola za Marekani bilioni 5 kwa mwaka.
“Sekta ya madini sasa ni injini ya uchumi wetu. Tunachokishuhudia leo ni daraja linalounganisha maono ya Serikali na nguvu ya mtaji kutoka sekta ya fedha. Ushirikiano huu unaenda moja kwa moja kumgusa mchimbaji mdogo na kumwinua katika uchumi rasmi. Benki ya CRDB hakika mmeonyesha kuwa ni Benki kiongozi katika kuleta suluhisho stahiki kwa sekta mbalimbali. Tunawashukuru sana,” alisema Waziri Mavunde.

Alisisitiza kuwa chini ya uongozi wa Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, Serikali imekuwa ikitekeleza mageuzi ya kisera, kiusimamizi na kisheria ili kuhakikisha sekta ya madini inawanufaisha Watanzania wengi zaidi, hususan wachimbaji wadogo. Alieleza kuwa azma ya Serikali ni kuona uchimbaji hauishii kwenye kuuza mawe ghafi, bali unapanuka hadi kwenye uchakataji na uongezaji thamani ndani ya nchi.
Mpango uliozinduliwa na Benki ya CRDB unaleta mageuzi makubwa katika mfumo wa dhamana kwa kutambua dhamana mbadala zinazotokana moja kwa moja na shughuli za uchimbaji. Kwa mara ya kwanza katika sekta ya benki nchini, leseni halali za uchimbaji, mikataba ya mauzo ya dhahabu, na akiba ya dhahabu iliyohifadhiwa katika viwanda vya kusafisha pamoja inatambuliwa kama dhamana zinazokubalika kwa ajili ya mikopo.

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela, alisema mpango huo ni mfumo kamili wa kifedha unaogusa mnyororo mzima wa thamani wa sekta ya madini kuanzia uchimbaji, uchakataji, uhifadhi, usafirishaji hadi biashara na masoko ya ndani na nje ya nchi.
“Huu ni muundo mpya wa kifedha unaotambua uhalisia wa sekta ya madini. Tumekubali dhamana zinazotokana na shughuli halisi za wachimbaji badala ya mali zisizohusiana na sekta.

 Hii itafungua milango kwa maelfu ya wachimbaji wadogo waliokuwa nje ya mfumo rasmi wa kifedha,” alisema Nsekela.
Alieleza kuwa mpango huo unajumuisha mikopo ya mtaji kwa ajili ya uendeshaji wa shughuli za uchimbaji, mikopo ya ununuzi wa mitambo na vifaa vya kisasa, mikopo inayodhaminiwa na dhahabu, huduma za bima za migodi na wafanyakazi kupitia CRDB Insurance, pamoja na akaunti maalum za miamala ya madini na dhahabu zitakazorahisisha ufuatiliaji na uwazi wa biashara.

Kwa upande wake Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi CRDB, Donald Mmari, alimweleza Waziri wa Madini kuwa Bodi imeweka miongozo ya kimkakati inayolenga kuhakikisha sekta ya madini inakua kwa kuzingatia misingi ya uendelevu, uwajibikaji na uchumi shirikishi.
“Tunataka kuona wachimbaji wadogo wanapanda ngazi kutoka uchimbaji wa jadi hadi kutumia teknolojia bora, kupata masoko rasmi na kushiriki katika uongezaji thamani. Ukuaji wa sekta ya madini lazima uwe endelevu na wenye manufaa kwa jamii,” alisema Dkt. Mmari.

Benki ya CRDB ni miongoni mwa taasisi chache za kifedha zilizowekeza kwa kiwango kikubwa zaidi katika sekta ya madini nchini. Hadi kufikia mwishoni mwa mwaka jana, Benki hiyo imetoa mikopo yenye thamani ya jumla ya shilingi bilioni 186 katika sekta ya madini, ambapo shilingi bilioni 136 zimetolewa kwa wachimbaji wakubwa na shilingi bilioni 50 kwa wachimbaji wadogo.  

Akizungumza kwa niaba ya wachimbaji, Rais wa Chama cha Wachimbaji Madini Tanzania (FEMATA), John Bina alisema mpango huo umeleta matumaini mapya kwa wachimbaji wadogo waliokuwa wakikabiliwa na changamoto ya kukosa dhamana zinazokubalika na taasisi za fedha.
“Leo tunashuhudia mwanzo wa zama mpya. Wachimbaji wadogo tumepewa heshima ya kutambuliwa kama washirika halali wa maendeleo. Tunaishukuru sana Benki ya CRDB kwa kutuletea suluhisho hii, na tunawaahidi tutaendelea kushirikiana nao pamoja na Serikali kuhakikisha tunatumia fursa hii kwa uwajibikaji,” alisema.

Mkataba wa Makubaliano uliosainiwa kati ya Benki CRDB na Tume ya Madini unatarajiwa kuimarisha urasimishaji wa wachimbaji, kuongeza upatikanaji wa mitaji nafuu, kukuza ajira kwa vijana na wanawake katika maeneo ya migodi, pamoja na kuongeza mapato ya Serikali kupitia uwazi wa miamala na ufuatiliaji wa kidijitali.

WANANCHI wa Kata ya Mzenga na Mafizi wamepongeza hatua ya Mbunge wao, Dkt. Selemani Jafo, kusimamia binafsi ujenzi wa Daraja la Kitomondo hadi usiku, wakisema imeongeza kasi na uwajibikaji kwa mkandarasi.

Akizungumza kwa niaba ya wananchi wa Mafizi, mmoja wa wazee wa eneo hilo, Ramadhani Zungwe amesema si jambo la kawaida kwa kiongozi kubaki kijijini hadi usiku akihakikisha kazi inafanyika kama ilivyopangwa.

“Ameonyesha mfano wa kujitoa kwa ajili ya maendeleo yetu. Hii inatupa matumaini mapya,” amesisitiza Zungwe.

Msukumo huo umefuatia maelekezo aliyoyatoa Dkt. Jafo wiki iliyopita kwa mkandarasi, kampuni ya Neloyt Tanzania Limited, akitaka ifikapo tarehe 24 nguzo za daraja hilo ziwe tayari zimemwagwa.

Tangu wakati huo, kazi imekuwa ikiendelea kwa kasi kubwa, huku Dkt. Jafo mwenyewe akishuhudia hatua za ujenzi zinavyopiga hatua.

Naye, Diwani wa Kata ya Mafizi, Mhe. Bora Mayage, amekiri kuwa usimamizi wa karibu wa mbunge huyo umeleta matokeo chanya.

Amesema kasi ya awali ya mkandarasi haikuwa ya kuridhisha, lakini kwa sasa mabadiliko yanaonekana wazi na nguzo za zege tayari zimesimama.

Mbali na hayo, Dkt. Jafo amemtaka mkandarasi kuhakikisha ifikapo Machi 5 zoezi la umwagaji wa slab linakamilika, akiahidi kushiriki pamoja na viongozi wa kata hizo mbili katika hatua hiyo muhimu.

Ameweka bayana kuwa hatokuwa tayari kuona wananchi wake wanaendelea kuteseka wakati Rais, Mhe.Dkt. Samia Suluhu Hassan ameshatoa pesa ya kukamilisha daraja hilo.

Daraja la Kitomondo linatajwa kuwa kiungo muhimu kwa wakazi wa Mzenga na Mafizi, likirahisisha shughuli za kijamii na kiuchumi zikiwemo usafiri wa wanafunzi, wafanyabiashara na wagonjwa.

Kukamilika kwake kunatarajiwa kufungua ukurasa mpya wa maendeleo kwa wananchi wa maeneo hayo.