NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

SERIKALI ya Belarus imeendelea kutoa fursa za ufadhili wa masomo kwa wanafunzi wa Tanzania, hususan katika fani ya tiba kwa mwaka wa masomo 2026/2027, hatua inayotokana na kuimarika kwa ushirikiano kati ya nchi hizo mbili.

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Daniel Mushi, amesema upatikanaji wa mabasi ya watumishi yatasaidia sana katika kuweka mazingira salama na wezeshi ya utendaji.

Amesema hatua hiyo inaonesha dhamira ya dhati ya Serikali katika kujali watumishi na kuboresha mazingira ya kazi.

Amesisitiza kuwa watumishi ni nguzo kuu ya kufikia malengo kwani ndio watekekezaji wa mipango na maono wizara hivyo, Wizara inaendelea kuweka mazingira stahiki na jumuishi kwa watumishi wote.

"Rais wetu amesisitiza kazi iende sambamba na kujali utu, na hivi ndio tunatekeleza kauli mbiu ya Kazi na Utu tunasonga mbele kwa kuweka mazingira yanayovutia utendaji kwa watumishi" amesema Prof. Mushi.

Prof. Mushi amewahimiza watumishi kutumia mabasi hayo na kuyatunza ili yaweze kurahisisha utendaji kazi na kutumika kwa muda mrefu.

Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimaliwatu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Edith Rwiza amesema ununuzi wa mabasi matatu (3) mapya kwa ajili ya usafiri wa watumishi ni hatua muhimu ya kuboresha mazingira ya kazi kwa Wizara.

Akizungumza jijini Dodoma Aprili 28, 2026 katika uzinduzi wa mabasi ya watumishi, Mkurugenzi huyo amesema mabasi hayo yamenunuliwa na Wizara kwa kushirikiana na Mradi wa Kuimarisha na Kuboresha Elimu ya Awali na Msingi Tanzania Bara (BOOST) kwa zaidi ya Shilingi milioni 500 kwa lengo la kuwezesha watumishi katika safari za kila siku za kwenda kazini na kurudi nyumbani pamoja na ziara za kikazi.

"Kabla ya hatua hii, watumishi walilazimika kutumia kati ya shilingi 10,000 hadi 15,000 kwa siku kufika ofisini hali iliyoleta ugumu wa maisha na kupunguza morali ya kazi" amesema Dkt. Rwiza

Mkurugenzi Rwiza amesema upatikanaji wa mabasi haya ni sehemu ya jitihada za wizara kuhakikisha watumishi wanafanya kazi katika mazingira bora na yenye ufanisi.

Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikalin na Afya (TUGHE), Bw. Moshi Kisinga ameushukuru uongozi wa Wizara hiyo kwa kununua magari kwa ajili ya watumishi.

"Kwa niaba ya watumishi wenzangu tumepokea magari haya kwa furaha na hakika tumeondokana na changamoto kubwa ya usafiri", amesema Kisinga.

Ametoa rai kwa watumishi kufanya kazi kwa juhudi na maarifa akisisitiza uwajibikaji katika majukumu ya kila siku.



Dkt. Kiruswa aongoza ujumbe wa Tanzania katika kongamano la kikanda

Mbibo: Ushirikiano wa kimataifa ni chachu ya mafanikio Sekta ya Madini


📍 Addis Ababa, Ethiopia 

Serikali ya Tanzania imesisitiza umuhimu wa matumizi endelevu ya madini muhimu (critical minerals) kama nyenzo kuu ya kuchochea maendeleo ya viwanda na kukuza uchumi Barani Afrika.

Hayo yameelezwa na Naibu Waziri wa Madini, Dkt. Steven Kiruswa, Aprili 28, 2026, wakati wa kongamano la Kikanda lililofanyika Makao Makuu ya Tume ya Umoja wa Mataifa ya Uchumi Afrika (UNECA) jijini Addis Ababa.

Dkt. Kiruswa amesema Afrika ina nafasi ya kimkakati duniani kutokana na utajiri wa madini muhimu yanayotumika katika teknolojia za nishati safi, akitaja madini ya lithiamu, kobalti na nikeli kuwa nguzo muhimu katika uzalishaji wa betri za magari ya umeme na mifumo ya nishati jadidifu. Amesema hali hiyo inaifanya Afrika kuwa mhimili muhimu katika mabadiliko ya uchumi wa dunia kuelekea matumizi ya nishati safi.

Aidha, Dkt. Kiruswa ameongoza ujumbe wa Tanzania katika Kongamano hilo, ambapo ameeleza dhamira ya Serikali ya Tanzania ya kuhakikisha rasilimali za madini zinasimamiwa kwa manufaa ya wananchi kupitia Sera na Mikakati inayolenga uongezaji thamani wa madini ndani ya nchi, ajira na ukuaji jumuishi wa uchumi.

Awali, Aprili 27, 2026, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Msafiri Mbibo, alisema Afrika ina fursa kubwa ya kunufaika na ongezeko la mahitaji ya madini hayo duniani, lakini akasisitiza umuhimu wa kuhakikisha uwekezaji unaendana na misingi ya uendelevu na uwajibikaji.

Alibainisha changamoto zinazoikabili sekta ya madini kuwa ni pamoja na uchimbaji usio rasmi, uharibifu wa mazingira na ushirikishwaji mdogo wa jamii, akisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya serikali, sekta binafsi na wadau wa maendeleo ili kukabiliana nazo.

Pamoja na Mambo mengine, Mbibo aliongeza kuwa Tanzania itaendelea kuimarisha ushirikiano wa kikanda na kimataifa sambamba na kuhamasisha matumizi ya teknolojia za kisasa katika shughuli za uchimbaji ili kuongeza tija na kupunguza athari kwa mazingira.

Kongamano hilo limewakutanisha mawaziri, wataalamu na wadau wa sekta ya madini kutoka nchi mbalimbali za Afrika na nje ya bara hilo, likilenga kujadili namna bora ya kuhakikisha madini muhimu yanachangia kikamilifu maendeleo ya viwanda na ustawi wa jamii.

Miongoni mwa washiriki mashuhuri ni Hailemariam Desalegn na Habtamu Tegegne, ambao kwa pamoja wamesisitiza umuhimu wa ushirikiano wa kikanda ili Afrika inufaike ipasavyo na rasilimali zake za madini.



Na Oscar Assenga, Tanga

Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Dkt. Balozi Batilda Burian, amesema mkoa huo umeanza mkakati maalum wa kukuza na kutangaza utalii wa fukwe pamoja na fursa za uwekezaji zilizopo, ili kuongeza mchango wake katika uchumi wa Taifa.

Akizungumza leo, amesema ameita wadau mbalimbali kwa ajili ya kujadili na kuweka mikakati ya pamoja ya kuitangaza Tanga, akibainisha kuwa mkoa huo umejaliwa kuwa katika ukanda wa Bahari ya Hindi wenye maeneo mengi yenye fursa za kiuchumi na utalii.

Ametaja baadhi ya maeneo hayo kuwa ni pamoja na Kipumbwi (Pangani), Ushongo, Kwale (Mkinga) na maeneo ya Raskazone jijini Tanga, ambapo kuna mradi wa kuboresha fukwe unaofadhiliwa na Benki ya Dunia. 

Amesema mradi huo utakapokamilika utafungua fursa za michezo ya maji, matembezi ya boti, kuogelea pamoja na shughuli za kijamii kama harusi.

Aidha, amesema mkoa umeanza kushirikiana na Kampuni ya Makazi Solution pamoja na wadau wa Zanzibar ili kujifunza na kubadilishana uzoefu wa namna ya kuendeleza utalii wa fukwe.

 Timu ya wataalamu inatarajiwa kwenda Zanzibar kukutana na Wizara ya Utalii na wadau wengine ili kuimarisha ushirikiano huo.

“Tunajifunza kutoka Zanzibar, ambako maeneo kama Nungwi na Paje yalianza kidogo lakini sasa yamekua vituo vikubwa vya utalii. Sasa ni wakati wa Tanga kuchukua nafasi hiyo,” amesema.

Kwa upande wa uwekezaji, Dkt. Burian ameeleza kuwa mradi wa Kipumbwi Satellite City, unaotekelezwa kwa ushirikiano na Halmashauri ya Pangani na Makazi Solution, unalenga kutoa fursa kwa wananchi na wawekezaji kupata viwanja na kuendeleza eneo hilo.

Amesema eneo la Kipumbwi lina umuhimu mkubwa kimkakati, likiwa kilomita 3 kutoka bandari ya Kipumbwi, kilomita 80 kutoka Tanga, kilomita 60 kutoka Zanzibar kwa njia ya bahari, na kilomita 180 kutoka Dar es Salaam. Pia ujenzi wa barabara ya Tanga–Pangani–Saadani–Bagamoyo unatarajiwa kufungua zaidi ukanda huo wa pwani.

Mbali na fukwe, mkoa wa Tanga una vivutio vingi vya utalii ikiwemo Mapango ya Amboni, Hifadhi ya Taifa ya Saadani, Hifadhi ya Taifa ya Mkomazi, Milima ya Usambara (Lushoto), pamoja na urithi wa kihistoria kama makaburi ya vita ya kwanza ya dunia na Kisiwa cha Toten.

Ameongeza kuwa Tanga pia ni kitovu cha utamaduni wa Kiswahili, likiwa na historia ya muziki wa taarab, vyakula vya asili, pamoja na kuwa chimbuko la lugha ya Kiswahili, ambapo mwanazuoni mashuhuri Sheikh Shaban Robert alizaliwa katika eneo hilo.

Kwa sasa, amesema mkoa unapokea wageni kutoka ndani na nje ya nchi, hususan kutoka Kenya, Ujerumani, Uholanzi na Uswisi, wanaovutiwa na historia, mazingira asilia na utamaduni wa Tanga.

Dkt. Burian amesema jitihada hizo zinaunga mkono azma ya Rais Samia Suluhu Hassan ya kuitangaza Tanzania kupitia kampeni ya Royal Tour na kuongeza idadi ya watalii.

Kwa upande wa uchumi, amesema mkoa wa Tanga kwa sasa unachangia takribani shilingi trilioni 9.8 katika pato la taifa, na una mpango wa kuongeza mchango huo na kufikia nafasi ya pili kitaifa baada ya Dar es Salaam ifikapo mwaka 2028.

Amehitimisha kwa kusema kuwa Tanga ni eneo sahihi kwa uwekezaji na utalii, akiwakaribisha wawekezaji na watalii kutoka ndani na nje ya nchi kuja kutumia fursa zilizopo.




Na, Mwandishi Wetu, Muleba – Kagera

KAIMU Mganga Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Bw. Salum Kimbau amesema maandalizi ya Mpango wa Afya Moja kwa mkoa wa Kagera utaunufaisha mkoa huo kwa kuzingatia malengo yake ya kuboresha uratibu na utekelezaji wa Dhana ya Afya ya Moja na kuendelea kutatua changamoto zilizopo na zenye mwingiliano kati ya binadamu, wanyama na mazingira


Amezungumza hayo wakati akifungua kikao kazi cha wataalamu wa masuala ya Afya Moja kutoka sekta mbalimbali zikiwemo za afya, mifugo, mazingira, wanyamapori na kilimo ambao wamekutana katika Halmashauri ya Wilaya ya Muleba mkoani Kagera kwa siku tano kuanzia tarehe 27 Aprili hadi 01 Mei, 2026 ili kuandaa Mpango huo utakaotumika kubaini rasilimali zitakazosaidia kutatua changamoto na vihatarishi vya afya ya binadamu, wanyama na mazingira.





Bw. Kimbau amesema kuwa, mkoa utanufaika kwa uwepo wa Mpango huo kwani utaongeza tija katika kutatua changamoto zinazokabili sekta hizo hususan katika kuendelea kutatua changamoto za mwingiliano wa magonjwa kutoka kwa wanyama kwenda kwa binadamu na binadamu kwenda kwa wanyama.


“Tunashukuru kuufikia mkoa wetu wa Kagera, tunajua kuwa asilimia 75 ya magonjwa yanatokana na mwingiliano ulipo kati ya wanyama na binadamu, hivyo kuandaliwa kwa mpango kutasaidia utekelezaji wa Dhana ya Afya Moja kwa kushirikiana pamoja, hivyo utatusaidia kutatua changamoto zilizopo na kuwa na jamii salama,” alisema Bw. Kimbau



Aliongezea kuwa ufanisi wa mpango huu unategemea ushirikishwaji wa sekta zote zinazohusika ili kuleta matokeo chanya.


Naye Mratibu wa Maafa kutoka Idara ya Menejimenti ya Maafa sehemu ya Afya Moja kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Bi. Valentina Sanga amesema kuwa, Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kushirikiana na Shirika lisilo la Serikali la CIHEB Tanzania kupitia Mradi wa Usalama wa Afya Duniani imeratibu maandalizi ya uwepo wa mpango huo huku akisihi kuunganisha nguvu ya pamoja katika kuhakikisha utekelezaji wake unaleta matunda yanayotarajiwa.

Aidha, aliwasihi wataalamu wa Masuala ya Afya Moja kutumia fursa hiyo kuja na Mpango utakaoinufaisha Kagera, kwa kuzingatia ni miongoni mwa Mikoa inayokumbwa na majanga ya mlipuko mengine yakichangiwa na mwingiliano wa wanyama na binadamu.

“Dhana ya Afya Moja (One Health) inatoa fursa ya kutambua uhusiano wa karibu kati ya afya ya binadamu, wanyama, na mazingira. Inasisitizwa kuendelea kujifunza zaidi dhana hii ili kutatua changamoto zilizopo zikiwemo za milipuko ya magonjwa na kuweza kuyakabili endapo yanatokea katika maeneo yetu,” alisisitiza Bi. Valentina

Aliongezea kuwa, Mpango huo utasaidia kutatua changamoto za masuala ya kiafya zinazotokea katika Halmashauri za mkoa wa Kagera, kujiandaa na kukabili majanga hayo ili kuwa na jamii salama kwa maendeleo ya Taifa kwa ujumla.

Kwa upande wake Mwakilishi wa Shirika la CIHEB Tanzania, Bw. Mark Lwakatare alisema mradi wa Usalama wa Afya Duniani utaendelea kushirikiana na mikoa husika katika kuimairisha utekelezaji wa dhana ya Afya Moja ili nchi iweze kukabiliana na vihatarishi vya majanga mbalimbali.



“Mradi huu unashirikiana na Serikali kuboresha na kuimarisha utekelezaji wa afua mbalimbali kupitia dhana ya Afya Moja nchini, hivyo mradi utaendelea kushirikiana katika kujiandaa na kukabili athari katika afya ya binadamu, manyama na mazingira,” alisisitiza Lwakatare.


Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania (TCDC) kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa mkoa wa Njombe,Kamati ya Michezo ya Meimosi, Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) imeshiriki zoezi la upandaji miti lililofanyika  katika eneo la Ofisi ya Mkuu wa mkoa wa Njombe.

Katika zoezi hilo Mkuu wa mkoa wa Njombe Mhe. Anthony Mtaka awewahimiza Wafanyakazi na wananchi kuhakikisha kuwa wanapanda miti yenye kuleta faida hususan miti ya matunda ili kusaidia upatikanaji wa kipato cha mtu mmojammoja na Taifa kwa ujumla.

" Kumekuwa na tabia ya watu wengi kupanda miti kwaajili ya kivuli tu, pasipo faida yoyote, vi vizuri sasa tukapanda miti yenye kuleta faida kubwa kama vile miti ya matunda, amesema Mtaka.

Zoezi hilo lilihudhuriwa na Viongozi mbalimbali akiwemo Katibu Tawala wa mkoa wa Njombe, Rais wa Shirikisho la Wafanyakazi Tanzania (TUCTA), Mwenyekiti wa Kamati ya Meimosi na Watumishi wa Serikali kutoka Wizara na Taasisi mbalimbali.

 


Na. Josephine Majura na Saidina Msangi, WF, Dodoma.


Serikali imeeleza kuwa iko tayari kushirikiana na Hispania katika maeneo ya kipaumbele ikiwemo kukuza uchumi endelevu, ujenzi wa miundombinu, mapambano dhidi ya mabadiliko ya tabianchi, na kuendeleza rasilimali watu, kwa lengo la kuchochea maendeleo jumuishi nchini.

Hayo yalielezwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), alipokutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Hispania chini, Mhe. Paloma Serra Robles, aliyefika kwa ajili kujitambulisha na kuwasilisha masuala mbalimbali ya ushirikiano kati ya Tanzania na Hispania, katika ukumbi wa mikutano wa Waziri wa Fedha, Treasury Square, Dodoma.

Mhe. Balozi Omar alisema dhamira ya Serikali ni kuendelea kushirikiana na Hispania katika kutafuta rasilimali za kifedha kwa ajili ya miradi mingine ya maendeleo yenye maslahi mapana kwa Taifa, lengo likiwa ni kuchochea ukuaji wa uchumi na huduma bora kwa jamii.

‘‘Uhusiano uliopo kati ya Tanzania na Hispania ni wa muda mrefu, ambapo kampuni za Hispania zimekuwa zikiwekeza nchini katika sekta mbalimbali, ikiwemo utalii, pamoja na kutekeleza miradi ya maendeleo na zitaendelea kuja kuwekeza nchini kwa kuwa mwelekeo wa Serikali ya Hispania ni kuongeza ushirikiano wa pamoja wenye mandeleo endelevu ikiwemo kuunganisha kampuni za Tanzania na kampuni za Hispania’’, alisema Mhe. Balozi Omar.

Pia Mhe. Omar alitoa wito kwa kampuni na wawekezaji kutoka Hispania kuja kuwekeza nchini Tanzania na kuwa Serikali itaendelea kuboresha mazingira ya kufanya biashara na kutoa vivutio mbalimbali vya kikodi na uwekezaji vinavyoendana na ukubwa wa miradi, ikilenga kukuza ushirikiano.

Aliishukuru Hispania kwa kufadhili utekelezaji wa miradi mbalimbali nchini, ikiwemo kutoa mkopo wa masharti nafuu wa Dola za Marekani milioni 30 kwa ajili ya utekelezaji wa Mradi wa Uendelezaji wa Bonde la Msimbazi, jijini Dar es Salaam ambao unatarajiwa kuleta mabadiliko katika kukabiliana na changamoto za mafuriko, kuimarisha hifadhi ya mazingira, na kukuza ustahimilivu wa miundombinu ya jiji hilo dhidi ya majanga ya asili.

Akizungumza kuhusu uchumi wa Tanzania Mhe. Omar alisema kuwa uchumi umeendelea kuimarika kwa kasi baada ya Pato la Taifa (GDP) kukua hadi kufikia asilimia 6.4 katika robo ya tatu ya mwaka 2025, ikilinganishwa na asilimia 6.1 katika kipindi kama hicho mwaka uliopita.

Aliongeza kuwa mfumuko wa bei umesalia kuwa tulivu kwa wastani wa asilimia 3.5 hadi kufikia Desemba 2025, ndani ya malengo ya kitaifa ya kati ya asilimia 3 na 5, huku kikiwa chini ya viwango vya ukomo vilivyowekwa na Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC).

Utulivu huo wa bei za bidhaa na huduma unatajwa kuwa kigezo muhimu kinachojenga imani kwa wawekezaji na kutoa fursa pana kwa washirika wa maendeleo kuendelea kuwekeza nchini kutokana na mazingira tabiri ya uchumi mkuu.

Alisisitiza kuwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, chini ya uongozi wa Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, itaendelea kuimarisha ushirikiano wa pande hizo mbili kwa ajili ya maendeleo na ustawi wananchi na kumpongeza kwa kuteuliwa kwake kuwa Balozi wa nchi hiyo.

Kwa upande wake Balozi wa Hispania nchini, Mhe. Paloma Serra Robles, ameeleza dhamira ya nchi yake kuendelea kuisaidia Tanzania katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo katika sekta tofauti zikiwemo miundombinu ya usafirishaji na miradi ya kijamii yenye tija kwa wananchi.

Alisema nchi hiyo imesaidia katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ikiwemo wa uendelezaji wa bonde la msimbazi ambao kukamilika kwake kutaleta tija kwa wakazi wa Dar es Salaam.

Kikao hicho pia kilihudhuriwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mlipaji Mkuu wa Serikali, Dkt. Natu El -maamry Mwamba, Kamishna Msaidizi Idara ya Usimamizi wa Madeni,  Bw. Omary Khama, Kamishna Msaidizi Idara ya Fedha za Nje, Bw. James Msina pamoja na Wataalamu kutoka Wizara ya Fedha na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano Wa Afrika Mashariki.



Taasisi kongwe ya dini ya kiislamu ya Twariqa Tulqadirya Arazakia Jailania Tanzania yenye makao yake makuu mkoani Arusha, imedhamiria kufanya sensa ya watu  na mali za taasisi hiyo ili kupata Idadi sahihi ya waumini wake.

Lengo la  zoezi hilo ni kuweza kufanya kazi kwa Ufanisi na kuyafahamu makundi  mbali mbali yaliyomo katika taasisi hiyo yakiwemo  makundi ya Viongozi Vijana,Wanawake,Walemavu,Yatima,Wajane na Wagane ili waweze kupatiwa huduma stahiki katika Mikoa yote ya Tanzania .

Akizungumza na Vyombo vya Habari mkoani Arusha Mwenyekiti wa Twariqa Taifa Shekhe  Mubaraka Salim Gahran amesema kuwa taasisi hiyo  ilifanya sensa ya kitwariqa  mnamo mwaka 1932,ambapo imepita kipindi kirefu bila zoezi hilo kufanyika hali ambayo inapelekea tasisi kushindwa kuwa na Idadi kamili ya watu  pamoja na mali zilizopo sasa.

Shekhe  Gahrani amesema kuwa  pia Ofisi yake imeona  ni vema kufanya uhakiki wa mali zilizopp kwa kuwa tangu kiongozi wao  Daruweshi Mti Mkavu alipofariki takribani mwaka mmoja na nusu  kuna baadhi ya vitu wanapaswa kuviweka sawa ili kuhakiki mali zote na kuepusha migogoro isiyo ya lazima ndani yao ikiwa ni pamoja na watu binafsi kujimilikisha mali za taasisi hiyo nchini.

"Hii ni sensa ya kawaida ya kitwariqa na inawahusu wanatwariqa wa Daraweshi Mti Mkavu na tunataka kuhakiki  kila kitu kuanzia Idadi ya Waridi wetu waliopata Ijaza,Elimu zao za kawaida,kufahamu haya yote itatuwezesha sisi  Viongozi kujua mahitaji yao na tuna watu wa aina gani na tunawahudumiaje na kwa namna gani bila kusahau migogoro isiyo ya lazima  na isielewele vinginevyo.Alisisitiza Shekhe Gahran 

Nae katibu mkuu wa twariqa Taifa shekhe  Haruna Hussein Lotha ameiomba serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kuwapa Ushirikiano wakati wa zoezi hilo ili kufanya zoezi hilo kutekelezwa kwa utulivu na kwa kufuata taratibu.

Shekhe Haruna Hussein amesema kuwa tangu wameingia madarakani hawajui idadi ya waumini wao,majengo wala mali walizonazo ili kuwasaidia kujua mapungufu yaliyopo na kisha kuboresha kwa kuwa kazi ya dini ni kujenga Imani za watu na kuwahudumia kiroho.

"Taasisi  yetu imekuwa ikishirikiana  na serikali yetu kila eneo hivyo tunatazamia kuwa mashirikiano haya  yatakuwa endelevu na  pia tumetumia vyombo vya habari ni kuhakikisha jamii inaendelea  kupata taarifa kwa wakati na zoezi litakapoanza katika mikoa yote ya Tanzania,liwe rahisi "Amesisitiza Katibu Lotha


Na Mwandishi wetu- DODOMA



Katibu Tawala  Mkoa wa Dodoma, Dkt. Khatibu Kazungu, amesema Ofisi yake ikishirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu Idara ya Menejimenti ya Maafa ipo katika hatua ya kuanzisha Kituo cha Operasheni ya Dharura katika Mkoa ikiwa ni utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Usimamizi wa Maafa ya mwaka 2004.

Dkt. Kazungu ameyasema hayo leo tarehe 27 Aprili,2026 jijini Dodoma kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma wakati akifungua  mafunzo ya siku nne ya  kujiandaa na kukabiliana na maafa kwa Timu ya kukabiliana na dharura ya Mkoa ambayo yameandaliwa na Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Idara ya Menejimenti ya Maafa pamoja na  uanzishaji wa kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura cha Mkoa.

Aidha, Dkt. Kazungu ameshukuru ujio wa elimu hiyo ndani ya Mkoa wa  Dodoma  akisema  itasaidia kuwajenga kielimu Maafisa wa Mkoa ili waweze kupeleka elimu katika ngazi za Wilaya.

"Elimu hii itasaidia kuongeza ujuzi na weledi kwa Maafisa wa Mkoa kwani majanga haya yamekuwa na madhara mengi kwa jamii," alisema Dkt. Kazungu.

Pia, alisisitiza  ukusanyaji wa taarifa kwa wakati na kabla ya majanga ili kurahihisisha  kuyakabili pamoja na kuboresha mawasiliano ya karibu baina ya wananchi na Maafisa wa Mkoa.

"Lazima kuwepo ushirikiano baina yetu na Wananchi ili tuweze kupambana na maafa ndani ya Mkoa wetu wa Dodoma," alisisitiza.


Awali Kaimu Mkurugezi Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu, Kanali Selestine Masalamadu aliupongeza Mkoa wa Dodoma kwa kuwa tayari kupokea elimu ya maafa na majanga na kusema kuwa  Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Idara hiyo ina jukumu la kuratibu shughuli za Kuzuia, Kupunguza Athari, Kujiandaa, Kukabiliana na Kurejesha hali baada ya maafa.

Vilvile, alisema kuwa Ofisi inaendelea kuratibu uanzishaji na uendeshaji wa Vituo vya Operesheni na Mawasiliano ya Dharura vya Mikoa  pamoja na Timu za kukabiliana na  dharura , ikiwa ni utekelezaji wa  Sera ya Taifa ya Usimamaizi wa Maafa ya Mwaka 2004, Sheria ya Usimamaizi wa maafa Na. 6 ya mwaka 2022 na kanuni zake.

“Lengo la mafunzo haya ni kuimarisha uwezo wa Mkoa kuratibu shughuli za usimamaizi wa maafa ili kupunguza madhara wakati wa dharura. Mafunzo haya yatawajengea uwezo washiriki katika maandalizi, uratibu wa taarifa, mwitikio wa haraka, usimamizi rasilimali na utoaji wa huduma kwa waathirika,” alifafanua Kanali Masalamadu.

Aidha, alibainisha kwamba kila Mkoa unatakiwa kuwa na chumba maalum kwa ajili ya kuratibu shughuli za maafa na dharura huku akihimiza kuharakishwa kwa upatikanaji wa chumba chenye sifa stahiki kuwezesha uanzishwaji kamili wa Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura Mkoa wa Dodoma.




MWISHO