Na.Mwandishi Wetu

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda, amesema Tuzo ya Taifa ya Mwalimu Nyerere ya Uandishi Bunifu imeendelea kuonyesha mafanikio makubwa, ambapo tangu kuanzishwa kwake Watanzania 27 wamefanikiwa kushinda katika nyanja mbalimbali za uandishi bunifu.

Amesema mafanikio hayo yanaonyesha namna tuzo hiyo inavyoibua na kutambua vipaji vya waandishi bunifu nchini, huku idadi ya washiriki ikiongezeka kila mwaka kutoka ndani na nje ya Tanzania.

Prof. Mkenda amebainisha kuwa Serikali imewekeza takribani Shilingi milioni 800 kwa ajili ya kuchapisha vitabu vilivyoshinda tuzo hizo na kuvisambaza katika shule za Tanzania Bara na Zanzibar, hatua inayolenga kuwafikia wasomaji wengi zaidi na kuhamasisha utamaduni wa kusoma.

Aidha, Waziri Mkenda amesema tuzo hizo zimeendelea kukua na kuvutia washiriki kutoka mataifa mbalimbali, jambo linaloonyesha kuongezeka kwa hadhi yake na umuhimu wa uandishi bunifu katika kukuza fasihi na lugha ya Kiswahili.

Ameongeza kuwa tuzo hizo zimekuwa jukwaa la kuwahamasisha vijana na waandishi kutumia vipaji vyao katika kutengeneza kazi zenye ubunifu na maudhui yanayoweza kuelimisha na kujenga jamii.

“Tuzo hii sasa imeingizwa rasmi katika orodha ya tuzo za uandishi bunifu duniani, ukiitafuta mtandaoni utaona tarehe 13 Aprili ni siku ya kutoa Tuzo ya Mwalimu Nyerere ya Uandishi Bunifu,” amesema Prof. Mkenda.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Kitaifa ya Tuzo ya Taifa ya Mwalimu Nyerere ya Uandishi Bunifu, Prof. Penina Mlama, amesema dirisha la kuwasilisha miswada ya kazi za ubunifu limefunguliwa rasmi leo, Agosti 19, 2026, na litafungwa Novemba 30, mwaka huu.

Ameeleza kuwa waandishi bunifu wanatakiwa kutumia kipindi cha takribani miezi mitatu kuwasilisha miswada yao, huku matangazo yenye vigezo na taratibu za kushiriki yakitolewa kupitia mitandao ya kijamii ya tuzo hiyo pamoja na mitandao ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia na Taasisi ya Elimu Tanzania.

Prof. Mlama amesema mshiriki anatakiwa kuwa raia wa Tanzania, kazi iwe imeandikwa kwa Kiswahili na kila mwandishi anaruhusiwa kuwasilisha andiko moja tu katika nyanja atakayochagua. Aidha, mswada unaowasilishwa unatakiwa kuwa haujawahi kuchapishwa popote.

Amefafanua kuwa miswada iliyowahi kushika nafasi ya kwanza hadi ya 10 katika miaka iliyopita haitaruhusiwa kuwasilishwa tena, ingawa waandishi waliowahi kushika nafasi hizo wanaweza kushiriki kwa kuwasilisha miswada mipya. Pia, miswada iliyowahi kushinda tuzo nyingine haitazingatiwa katika ushindani wa mwaka huu.

Kwa upande wa vigezo mahususi, tamthilia ya jukwaani inapaswa kutumia vionjo vya sanaa za maonyesho za Tanzania, iwe na muda wa dakika 40–60, isiwe na maonyesho zaidi ya sita na wahusika wasiozidi sita. Ushairi unatakiwa kuwa na mashairi yasiyopungua 50 wala kuzidi 60, huku kila shairi likiwa na beti zisizozidi 15.

Kwa riwaya, urefu unatakiwa kuwa kati ya maneno 60,000 na 100,000, wakati hadithi za watoto zinatakiwa kuwa na kati ya maneno 250 na 500 kwa hadithi moja. Prof. Mlama amesisitiza kuwa kazi zinazowasilishwa zinapaswa kuwa na mawazo asilia ya mwandishi na kujikita katika masuala muhimu ya jamii.


Na Mwandishi Wetu - Tanga


Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC) inaendelea kushiriki katika Maonesho ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu yanayofanyika katika Viwanja vya Usagara jijini Tanga, ikitumia jukwaa hilo kutoa elimu kwa wananchi kuhusu matumizi salama ya mionzi na fursa zinazotokana na teknolojia ya nyuklia katika kuchochea maendeleo ya Taifa.

Maonesho hayo, yanayoratibiwa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, yanawakutanisha taasisi za Serikali, taasisi za elimu na utafiti, wabunifu, wanafunzi, wataalamu pamoja na wadau mbalimbali wa sekta ya elimu, sayansi na teknolojia.

Katika banda la TAEC, wananchi, wanafunzi na wadau mbalimbali wanaendelea kupata elimu kuhusu jukumu la Tume la kusimamia na kudhibiti matumizi salama ya mionzi nchini, pamoja na mchango wa teknolojia ya nyuklia katika sekta mbalimbali zikiwemo afya, kilimo, mifugo, maji, viwanda, migodi, utafiti na nishati.

Ushiriki wa TAEC katika maonesho hayo pia unatoa fursa kwa wanafunzi na vijana kufahamu taaluma mbalimbali zinazohusiana na teknolojia ya nyuklia na umuhimu wa kujikita katika masomo ya sayansi, teknolojia, uhandisi na hisabati (STEM) ili kujenga kizazi cha wataalamu kitakachosaidia Taifa kutumia kikamilifu fursa zinazotokana na maendeleo ya sayansi na teknolojia.

Akifungua rasmi maonesho hayo Agosti 18, 2026, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda, alisisitiza umuhimu wa elimu, ujuzi, sayansi, teknolojia na ubunifu katika kujenga uchumi wa kisasa na kuongeza uwezo wa Taifa kutumia maarifa na teknolojia katika kutatua changamoto mbalimbali za maendeleo.

Katika muktadha huo, ushiriki wa TAEC unaunga mkono juhudi za Serikali za kuhakikisha sayansi na teknolojia zinatumika moja kwa moja katika kuleta maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Teknolojia ya nyuklia ina matumizi mapana yenye manufaa kwa wananchi, ikiwemo katika uchunguzi na tiba ya magonjwa, kuongeza tija katika kilimo na mifugo, usimamizi wa rasilimali za maji, shughuli za viwandani na migodini, utafiti wa kisayansi pamoja na sekta ya nishati.

Wananchi wanaotembelea banda la TAEC pia wanapata nafasi ya kuzungumza moja kwa moja na wataalamu, kuuliza maswali na kupata ufafanuzi kuhusu usalama wa mionzi, udhibiti wa vyanzo vya mionzi na matumizi ya teknolojia ya nyuklia kwa madhumuni ya amani na maendeleo.

TAEC itaendelea kutoa elimu na kuhamasisha matumizi salama ya mionzi na teknolojia ya nyuklia kwa maendeleo endelevu ya Taifa.

“Mionzi kwa Matumizi Salama na Teknolojia ya Nyuklia kwa Maendeleo ya Taifa.”

SERIKALI imeonya kuwa mtu au taasisi itakayobainika kuharibu au kutenda kosa dhidi ya Miundombinu Muhimu ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (CII) atakabiliwa na adhabu kali kwa mujibu wa Sheria ya Makosa ya Mtandao ya mwaka 2015.

Kaimu Mkurugenzi wa Udhibiti wa Bidhaa Bandia wa Tume ya Ushindani (FCC), Bw.Salvatory Chuwa, akiwasilisha mada  wakati wa Mkutano wa   Maafisa Biashara katika Kikao cha Tatu cha Wizara ya Viwanda na Biashara na Maafisa Biashara, kilichofanyika kwa siku mbili  jijini Dodoma.

Na Mwandishi Wetu

Tume ya Ushindani (FCC) imetoa elimu  kwa Maafisa Biashara kwa lengo la kuwaongezea uelewa kuhusu masuala ya ushindani katika biashara, udhibiti wa bidhaa bandia pamoja na umuhimu wa kumlinda mlaji dhidi ya bidhaa na huduma zisizokidhi viwango.

Semina hiyo imelenga kuwajengea uwezo Maafisa Biashara ambao wana nafasi muhimu katika kusimamia shughuli za biashara katika maeneo yao, ili waweze kutambua changamoto zinazohusiana na ushindani usio wa haki, bidhaa bandia na vitendo vinavyoweza kuwaathiri walaji.

Akitoa mada kuhusu udhibiti wa bidhaa bandia, wakati wa Mkutano wa  Maafisa Biashara nchini katika Kikao cha Tatu cha Wizara ya Viwanda na Biashara na Maafisa Biashara, kilichofanyika kwa siku mbili  jijini Dodoma.

Kaimu Mkurugenzi wa Udhibiti wa Bidhaa Bandia wa FCC, Bw. Salvatory Chuwa, ameeleza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano kati ya FCC na Maafisa Biashara katika kukabiliana na biashara ya bidhaa bandia.

"Bidhaa bandia zina madhara makubwa kwa uchumi, wafanyabiashara wanaofuata sheria na walaji, hivyo ni muhimu kwa Maafisa Biashara kuwa na uelewa wa kutosha kuhusu namna ya kubaini na kutoa taarifa kuhusu bidhaa zinazodhaniwa kuwa bandia."amesema Bw.Chuwa

Amesisitiza kuwa udhibiti wa bidhaa bandia unahitaji ushirikiano wa karibu kati ya taasisi za Serikali, wafanyabiashara na wananchi, huku akiwataka Maafisa Biashara kutumia nafasi zao kuelimisha wafanyabiashara na walaji kuhusu madhara ya bidhaa bandia.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Tafiti, Miungano ya Makampuni na Uraghibishi wa FCC, Bi. Zaytun Kikula, ametoa mada kuhusu masuala ya ushindani, akieleza umuhimu wa kuwepo kwa mazingira ya biashara yenye ushindani wa haki kwa ajili ya kukuza uchumi na kuwapa wafanyabiashara fursa sawa katika soko.

Bi.Kikula amebainisha kuwa ushindani wenye tija husaidia kuongeza ubunifu, kuboresha ubora wa bidhaa na huduma pamoja na kuwapa walaji fursa ya kupata bidhaa bora kwa bei shindani.

Aidha, amewataka Maafisa Biashara kushirikiana na FCC katika kutoa elimu kwa wafanyabiashara kuhusu sheria za ushindani na kuhakikisha kuwa vitendo vinavyoweza kuzuia au kupotosha ushindani vinatambuliwa na kuchukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria.

Semina hiyo ni sehemu ya jitihada za FCC za kuimarisha uelewa wa wadau kuhusu wajibu wa kulinda ushindani katika soko, kudhibiti bidhaa bandia na kuhakikisha haki za walaji zinalindwa.

FCC imeendelea kusisitiza kuwa ushirikiano wa wadau mbalimbali, hususan Maafisa Biashara, ni muhimu katika kujenga soko lenye ushindani wa haki, bidhaa salama na mazingira bora ya biashara kwa manufaa ya wafanyabiashara, walaji na uchumi kwa ujumla.

Kaimu Mkurugenzi wa Udhibiti wa Bidhaa Bandia wa Tume ya Ushindani (FCC), Bw.Salvatory Chuwa, akiwasilisha mada  wakati wa Mkutano wa   Maafisa Biashara katika Kikao cha Tatu cha Wizara ya Viwanda na Biashara na Maafisa Biashara, kilichofanyika kwa siku mbili  jijini Dodoma.

Mkurugenzi wa Tafiti, Miungano ya Makampuni na Uraghibishi wa FCC, Bi. Zaytun Kikula, akiwasilisha mada  wakati wa Mkutano wa   Maafisa Biashara katika Kikao cha Tatu cha Wizara ya Viwanda na Biashara na Maafisa Biashara, kilichofanyika kwa siku mbili  jijini Dodoma.

 Maafisa Biashara nchini wakifatilia mada mbalimbali kutoka kwa wataalamu wa Tume ya Ushindani (FCC) katika Kikao cha Tatu cha Wizara ya Viwanda na Biashara na Maafisa Biashara, kilichofanyika kwa siku mbili  jijini Dodoma.

 Maafisa Biashara nchini wakifatilia mada mbalimbali kutoka kwa wataalamu wa Tume ya Ushindani (FCC) katika Kikao cha Tatu cha Wizara ya Viwanda na Biashara na Maafisa Biashara, kilichofanyika kwa siku mbili  jijini Dodoma.

 



✅YAFUNGUA MILANGO YA UWEKEZAJI KWA SAUDI ARABIA


Shirika la Madini la Taifa( STAMICO) limefanya mazungumzo na ujumbe wa wafanyabiashara kutoka Serikali ya Saudi Arabia kuelezea fursa za uwekezaji zilizopo katika mnyororo wa rasilimali madini kwa manufaa ya watanzania.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO Dkt. Venance Mwasse katika Mkutano uliofanyika Agosti 18 2026 jijini Dar es Salam

Dkt Mwasse, amesema STAMICO inaendelea kufungua milango kwa wawekezaji kulingana na Sheria na taratibu za Serikali ili kuhakikisha inaleta manufaa kwa wote.

Amesema Shirika linazingatia misingi ya kujiendesha kibiashara na kwa uwazi ili kuzuia mianya ya urasimu na kuhakikisha inatoa matokeo yenye tija kwa haraka.

STAMICO, ni Shirika sahihi kuingia nalo ubia kwa kuwa lina wataalam wenye ujuzi na uzoefu wa kutosha, ushirika mzuri na jamii inayozunguka miradi na uwezo wa kushirikiana na taasisi zingine.

Naye, Abdulrahman Al Thobaity Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyabiashara wa Saudia Tanzania, ameshukuru kwa taarifa za fursa za uwekezaji na ushirikiano waliopata kutoka STAMICO.

Kwa upande wa wataalam meneja wa Utafiti Bw Frederick Mangasini Ametumia nafasi hiyo kuonesha fursa za uwekezaji katika miradi mbalimbali ikiwemo ya dhahabu, makaa ya mawe, shaba (copper) na uendelezaji wa wachimbaji wadogo

STAMICO inaendelea kujiimarisha na kuweka mazingira wezeshi ya uwekezaji kwa maslahi ya taifa.










 


Na Munir Shemweta, Tanga

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo, amesema Wizara yake iko tayari kutoa hati miliki za ardhi kwa maeneo yatakayotumika katika shughuli za utafiti, elimu ya ujuzi na ubunifu nchini.

Dkt. Akwilapo ameyasema hayo leo, Agosti 18, 2026, wakati wa uzinduzi wa Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu kwa mwaka 2026, inayoendelea viwanja vya Usagara jijini Tanga.

Amesema, Wizara ya Ardhi iko tayari kushirikiana na taasisi za elimu na utafiti kwa kuhakikisha maeneo yanayotumika katika shughuli hizo yanapatiwa hati miliki ili kuwezesha utekelezaji wa tafiti na ubunifu kwa ufanisi.

“Nichukue fursa hii kuipongeza Wizara ya Elimu, sambamba na kuwashukuru wahadhiri na wakufunzi wote kwa kazi nzuri ya kuandaa vijana katika kazi za ujuzi na ubunifu. Wizara yangu iko tayari kutoa hati miliki katika maeneo ya utafiti,” amesema Dkt. Akwilapo.

Akizungumzia Maonesho ya wiki ya kitaifa ya elimu, ujuzi na ubunifu nchini, Dkt. Akwilapo amepongeza kazi inayofanywa na taasisi za elimu, akisema Tanzania imepiga hatua kubwa katika matumizi ya teknolojia na ubunifu.

“Nipongeze ubunifu pamoja na maonesho. Kwa kweli yamefana sana, na ubunifu mliouonesha ni wa hali ya juu. Nawapongeza kwa yote mnayoyafanya katika taasisi zenu,” amesema.

Dkt. Akwilapo, ambaye aliwahi kuwa katika Wizara ya Elimu, ameeleza kuwa, mabadiliko yaliyofanyika katika sekta hiyo yanaonesha kuwa Tanzania imepiga hatua kubwa, hususan katika mabadiliko ya mitaala na kuibua vipaji vya vijana.

“Mimi nilikuwa Wizara ya Elimu na nilivyoiacha siyo ilivyo sasa. Mmepiga hatua kubwa, mmebadilisha. Tulivyoiacha siyo ilivyo leo. Mmerekebisha mtaala wa Amali na Sera, na matokeo yake tunayoyaona sasa, ambapo vijana wa kidato cha kwanza na cha pili wanaonesha uwezo wao,” amesema.

Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu kwa mwaka 2026 imezinduliwa rasmi na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Adolf Mkenda, ikiwa na lengo la kuendeleza ujuzi, ubunifu na matumizi ya teknolojia miongoni mwa vijana na jamii kwa ujumla.

Kaulimbiu ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu mwaka 2026 ni: “Elimu, Ujuzi na Ubunifu: Njia ya Kufikia Dira ya 2050.”





Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Queen Sendiga, amekabidhi wasanii hao T-shirt rasmi za Manyara Tanzanite Marathon, ikiwa ni sehemu ya maandalizi kuelekea tukio hilo ambalo limeendelea kupata mwitikio kutoka kwa wadau mbalimbali.


Na Mwandishi Wetu, Manyara


Manyara Tanzanite Marathon 2026 inatarajiwa kuwa na burudani ya aina yake baada ya wasanii maarufu nchini, Dully Sykes, Banana Zoro na Mr Blue, kuthibitisha kushiriki na kutumbuiza katika tukio hilo litakalofanyika Agosti 22, 2026 mjini Babati, mkoani Manyara.


Ushiriki wa wasanii hao umewezeshwa na kampuni ya Mati Super Brands Ltd kupitia kinywaji chake cha Tanzanite Royal Gin, hatua inayoongeza ushiriki wa sekta binafsi katika kufanikisha mbio hizo zinazolenga kuunganisha michezo, burudani na shughuli za kijamii.



Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Queen Sendiga, amekabidhi wasanii hao T-shirt rasmi za Manyara Tanzanite Marathon, ikiwa ni sehemu ya maandalizi kuelekea tukio hilo ambalo limeendelea kupata mwitikio kutoka kwa wadau mbalimbali.


Manyara Tanzanite Marathon 2026 imebeba kaulimbiu “Hatua Moja Okoa Maisha”, ikiwa na lengo la kukusanya Shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi wa wodi maalumu ya kuwahudumia watoto njiti wanaozaliwa kabla ya wakati.



Ujio wa Dully Sykes, Banana Zoro na Mr Blue unatarajiwa kuongeza hamasa kwa wanariadha, vikundi vya jogging na wananchi watakaoshiriki au kujitokeza kushuhudia mbio hizo. Burudani hiyo pia inalenga kuwapa washiriki na watazamaji uzoefu wa kipekee huku ikihamasisha jamii kuunga mkono kampeni ya kuokoa maisha ya watoto njiti..



Mchango wa Mati Super Brands Ltd kupitia Tanzanite Royal Gin unaendelea kuonesha nafasi ya sekta binafsi katika kusaidia shughuli zenye manufaa kwa jamii. Ushiriki huo unatarajiwa kuongeza mvuto wa marathon na kuwafikia watu wengi zaidi kupitia michezo na burudani.


Kwa ujumla, Manyara Tanzanite Marathon 2026 inatarajiwa kuwa jukwaa linalounganisha michezo, burudani, utalii na uwajibikaji kwa jamii, huku kila hatua ya washiriki ikilenga kuchangia upatikanaji wa huduma bora kwa watoto njiti mkoani Manyara.






Na Mwandishi Wetu.


Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Queen Sendiga, amezindua rasmi vifaa maalum (KIT) vitakavyotumiwa na washiriki wa Manyara Tanzanite Marathon 2026, huku idadi ya watu waliojiandikisha kushiriki mbio hizo za hisani ikifikia 2,200.


Uzinduzi wa KIT hiyo, inayojumuisha T-shirt, kofia na namba za washiriki, umefanyika Agosti 17, 2026, mjini Babati, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya mwisho kuelekea mbio hizo zinazotarajiwa kufanyika Agosti 22, 2026.


Manyara Tanzanite Marathon 2026 imeandaliwa ikiwa na lengo la kuchangisha fedha zitakazosaidia kuboresha huduma za afya kwa watoto njiti katika Mkoa wa Manyara, hususan katika maeneo yanayohitaji miundombinu na huduma bora zaidi kwa watoto wanaozaliwa kabla ya muda.






Kaulimbiu ya mbio hizo mwaka huu ni “Hatua Moja, Okoa Maisha ya Mtoto,” inayolenga kuhamasisha wananchi, taasisi, kampuni na wadau mbalimbali kushiriki katika tukio hilo huku wakitoa mchango wa moja kwa moja katika kuboresha maisha ya watoto njiti.


Akizungumza katika uzinduzi huo, RC Sendiga amehimiza wananchi na wadau mbalimbali kuendelea kujitokeza kwa wingi kushiriki mbio hizo, akieleza kuwa mwitikio wa watu 2,200 waliojisajili hadi sasa ni ishara ya namna jamii inavyoguswa na ajenda ya kuboresha afya na ustawi wa watoto.


Idadi hiyo ya washiriki inatarajiwa kuongezeka kadri siku ya mbio inavyokaribia, huku waandaaji wakiendelea kutoa wito kwa watu ambao bado hawajajisajili kutumia fursa hiyo kushiriki katika tukio lenye lengo la kuchangia ustawi wa watoto na maendeleo ya afya mkoani Manyara.





Mbali na kushiriki katika mbio hizo, tukio hilo limeandaliwa pia kwa namna inayolenga kukuza utalii wa ndani na kuifanya Manyara kuwa sehemu ya kuvutia kwa wageni kutoka ndani na nje ya Tanzania. Washiriki watakaokuwa wamechagua kifurushi kinachojumuisha ziara ya utalii watapata fursa ya kutembelea Hifadhi ya Taifa ya Tarangire baada ya kumalizika kwa mbio.


Uhusiano kati ya mbio hizo na utalii unalenga kuwapa washiriki uzoefu mpana zaidi, huku ukiendelea kutangaza vivutio vya utalii vilivyopo mkoani Manyara na kuchochea shughuli za kiuchumi zinazotokana na utalii.


Manyara Tanzanite Marathon imeendelea kujijenga kama moja ya matukio yanayounganisha michezo, afya, utalii na uwajibikaji kwa jamii. Kupitia mbio hizo, waandaaji wanatarajia kuhamasisha watu kutoka makundi mbalimbali kushiriki katika jitihada za kuchangia huduma za afya kwa watoto njiti.






Kwa mwaka 2026, msisitizo umewekwa katika kaulimbiu “Hatua Moja, Okoa Maisha ya Mtoto,” huku fedha zitakazopatikana kupitia mbio hizo zikilenga kusaidia ujenzi na uboreshaji wa huduma kwa watoto njiti katika Mkoa wa Manyara.


Uzinduzi wa KIT hiyo umeongeza hamasa kuelekea Agosti 22, ambapo Babati inatarajiwa kuwa kitovu cha tukio hilo litakalowakutanisha washiriki, wadau wa afya, taasisi, wafanyabiashara, watalii na wananchi kwa ujumla katika hatua ya pamoja ya kuokoa maisha ya watoto njiti.