Kukamilika kwa ujenzi wa Barabara ya kutoka Longido - Samia Longido Girls Kijiji cha Oltepesi, Kata ya Orbomba, kunatarajiwa kuwa kichocheo cha ukuaji wa uchumi wa Wilaya ya Longido kwa kuboresha usafiri, mawasiliano, biashara na fursa za uwekezaji.
Hayo yameselwa na Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa, Wazo Michael Mwang'onda, wakati akiweka Jiwe la Msingi mradi wa barabara yenye urefu wa kilometa 0.84, mradi unaogharimu kiasi cha shilingi milioni 395.
" Kukamilika kwa barabara hiyo itarahisisha usafiri wa wananchi, kuboresha upatikanaji wa huduma za kijamii na kufungua fursa mpya za shughuli za kiuchumi kwa wakazi wa eneo hilo, hivyo mkandarasi unatakiwa kukamilisha kazi zilizobaki kwa kuzingatia viwango vya ubora vilivyowekwa". Amebainisha Mwang'onda
Meneja wa Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) Wilaya ya Longido, Mhandisi Lawrence Msemo, amesema barabara hiyo ina urefu wa jumla wa kilometa 0.84, ambapo awamu ya kwanza yenye urefu wa kilometa 0.3.
Ameeleza kuwa mradi huo ulianzishwa kwa lengo la kuboresha upatikanaji wa huduma katika Shule ya Sekondari ya Wasichana Longido Girls, huku kazi zilizobaki zikihusisha ujenzi wa mifereji ya maji.
Kwa mujibu wa Msemo, barabara hiyo inaunganisha Mji wa Longido na Shule ya Sekondari ya Wasichana Longido Girls, ambayo ni shule muhimu ya Mkoa wa Arusha, hivyo itarahisisha usafiri kwa wanafunzi, walimu na wananchi wa maeneo jirani.
Baadhi ya wananchi walieleza kufurahishwa na utekelezaji wa mradi huo. Mkazi wa eneo hilo, Losiana Lomayan, alisema barabara hiyo itachochea ukuaji wa uchumi wa wilaya, huku mwanafunzi Salome John akiishukuru Serikali kwa kuwajengea barabara ya lami.
Naye Naibu Waziri wa Madini, Dk. Stephen Kiruswa, ameipongeza Serikali kwa kuendelea kuboresha miundombinu ya barabara katika Wilaya ya Longido kulingana na bajeti zilizotengwa.





















































