Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Daniel Mushi, amesema upatikanaji wa mabasi ya watumishi yatasaidia sana katika kuweka mazingira salama na wezeshi ya utendaji.
Amesema hatua hiyo inaonesha dhamira ya dhati ya Serikali katika kujali watumishi na kuboresha mazingira ya kazi.
Amesisitiza kuwa watumishi ni nguzo kuu ya kufikia malengo kwani ndio watekekezaji wa mipango na maono wizara hivyo, Wizara inaendelea kuweka mazingira stahiki na jumuishi kwa watumishi wote.
"Rais wetu amesisitiza kazi iende sambamba na kujali utu, na hivi ndio tunatekeleza kauli mbiu ya Kazi na Utu tunasonga mbele kwa kuweka mazingira yanayovutia utendaji kwa watumishi" amesema Prof. Mushi.
Prof. Mushi amewahimiza watumishi kutumia mabasi hayo na kuyatunza ili yaweze kurahisisha utendaji kazi na kutumika kwa muda mrefu.Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimaliwatu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Edith Rwiza amesema ununuzi wa mabasi matatu (3) mapya kwa ajili ya usafiri wa watumishi ni hatua muhimu ya kuboresha mazingira ya kazi kwa Wizara.
Akizungumza jijini Dodoma Aprili 28, 2026 katika uzinduzi wa mabasi ya watumishi, Mkurugenzi huyo amesema mabasi hayo yamenunuliwa na Wizara kwa kushirikiana na Mradi wa Kuimarisha na Kuboresha Elimu ya Awali na Msingi Tanzania Bara (BOOST) kwa zaidi ya Shilingi milioni 500 kwa lengo la kuwezesha watumishi katika safari za kila siku za kwenda kazini na kurudi nyumbani pamoja na ziara za kikazi.
"Kabla ya hatua hii, watumishi walilazimika kutumia kati ya shilingi 10,000 hadi 15,000 kwa siku kufika ofisini hali iliyoleta ugumu wa maisha na kupunguza morali ya kazi" amesema Dkt. Rwiza
Mkurugenzi Rwiza amesema upatikanaji wa mabasi haya ni sehemu ya jitihada za wizara kuhakikisha watumishi wanafanya kazi katika mazingira bora na yenye ufanisi.
Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikalin na Afya (TUGHE), Bw. Moshi Kisinga ameushukuru uongozi wa Wizara hiyo kwa kununua magari kwa ajili ya watumishi.
"Kwa niaba ya watumishi wenzangu tumepokea magari haya kwa furaha na hakika tumeondokana na changamoto kubwa ya usafiri", amesema Kisinga.
Ametoa rai kwa watumishi kufanya kazi kwa juhudi na maarifa akisisitiza uwajibikaji katika majukumu ya kila siku.

Dkt. Kiruswa aongoza ujumbe wa Tanzania katika kongamano la kikanda
Mbibo: Ushirikiano wa kimataifa ni chachu ya mafanikio Sekta ya Madini
📍 Addis Ababa, Ethiopia
Serikali ya Tanzania imesisitiza umuhimu wa matumizi endelevu ya madini muhimu (critical minerals) kama nyenzo kuu ya kuchochea maendeleo ya viwanda na kukuza uchumi Barani Afrika.
Hayo yameelezwa na Naibu Waziri wa Madini, Dkt. Steven Kiruswa, Aprili 28, 2026, wakati wa kongamano la Kikanda lililofanyika Makao Makuu ya Tume ya Umoja wa Mataifa ya Uchumi Afrika (UNECA) jijini Addis Ababa.
Dkt. Kiruswa amesema Afrika ina nafasi ya kimkakati duniani kutokana na utajiri wa madini muhimu yanayotumika katika teknolojia za nishati safi, akitaja madini ya lithiamu, kobalti na nikeli kuwa nguzo muhimu katika uzalishaji wa betri za magari ya umeme na mifumo ya nishati jadidifu. Amesema hali hiyo inaifanya Afrika kuwa mhimili muhimu katika mabadiliko ya uchumi wa dunia kuelekea matumizi ya nishati safi.
Aidha, Dkt. Kiruswa ameongoza ujumbe wa Tanzania katika Kongamano hilo, ambapo ameeleza dhamira ya Serikali ya Tanzania ya kuhakikisha rasilimali za madini zinasimamiwa kwa manufaa ya wananchi kupitia Sera na Mikakati inayolenga uongezaji thamani wa madini ndani ya nchi, ajira na ukuaji jumuishi wa uchumi.
Awali, Aprili 27, 2026, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Msafiri Mbibo, alisema Afrika ina fursa kubwa ya kunufaika na ongezeko la mahitaji ya madini hayo duniani, lakini akasisitiza umuhimu wa kuhakikisha uwekezaji unaendana na misingi ya uendelevu na uwajibikaji.
Alibainisha changamoto zinazoikabili sekta ya madini kuwa ni pamoja na uchimbaji usio rasmi, uharibifu wa mazingira na ushirikishwaji mdogo wa jamii, akisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya serikali, sekta binafsi na wadau wa maendeleo ili kukabiliana nazo.
Pamoja na Mambo mengine, Mbibo aliongeza kuwa Tanzania itaendelea kuimarisha ushirikiano wa kikanda na kimataifa sambamba na kuhamasisha matumizi ya teknolojia za kisasa katika shughuli za uchimbaji ili kuongeza tija na kupunguza athari kwa mazingira.
Kongamano hilo limewakutanisha mawaziri, wataalamu na wadau wa sekta ya madini kutoka nchi mbalimbali za Afrika na nje ya bara hilo, likilenga kujadili namna bora ya kuhakikisha madini muhimu yanachangia kikamilifu maendeleo ya viwanda na ustawi wa jamii.
Miongoni mwa washiriki mashuhuri ni Hailemariam Desalegn na Habtamu Tegegne, ambao kwa pamoja wamesisitiza umuhimu wa ushirikiano wa kikanda ili Afrika inufaike ipasavyo na rasilimali zake za madini.
Na Oscar Assenga, Tanga
Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Dkt. Balozi Batilda Burian, amesema mkoa huo umeanza mkakati maalum wa kukuza na kutangaza utalii wa fukwe pamoja na fursa za uwekezaji zilizopo, ili kuongeza mchango wake katika uchumi wa Taifa.
Akizungumza leo, amesema ameita wadau mbalimbali kwa ajili ya kujadili na kuweka mikakati ya pamoja ya kuitangaza Tanga, akibainisha kuwa mkoa huo umejaliwa kuwa katika ukanda wa Bahari ya Hindi wenye maeneo mengi yenye fursa za kiuchumi na utalii.
Ametaja baadhi ya maeneo hayo kuwa ni pamoja na Kipumbwi (Pangani), Ushongo, Kwale (Mkinga) na maeneo ya Raskazone jijini Tanga, ambapo kuna mradi wa kuboresha fukwe unaofadhiliwa na Benki ya Dunia.
Amesema mradi huo utakapokamilika utafungua fursa za michezo ya maji, matembezi ya boti, kuogelea pamoja na shughuli za kijamii kama harusi.
Aidha, amesema mkoa umeanza kushirikiana na Kampuni ya Makazi Solution pamoja na wadau wa Zanzibar ili kujifunza na kubadilishana uzoefu wa namna ya kuendeleza utalii wa fukwe.
Timu ya wataalamu inatarajiwa kwenda Zanzibar kukutana na Wizara ya Utalii na wadau wengine ili kuimarisha ushirikiano huo.
“Tunajifunza kutoka Zanzibar, ambako maeneo kama Nungwi na Paje yalianza kidogo lakini sasa yamekua vituo vikubwa vya utalii. Sasa ni wakati wa Tanga kuchukua nafasi hiyo,” amesema.
Kwa upande wa uwekezaji, Dkt. Burian ameeleza kuwa mradi wa Kipumbwi Satellite City, unaotekelezwa kwa ushirikiano na Halmashauri ya Pangani na Makazi Solution, unalenga kutoa fursa kwa wananchi na wawekezaji kupata viwanja na kuendeleza eneo hilo.
Amesema eneo la Kipumbwi lina umuhimu mkubwa kimkakati, likiwa kilomita 3 kutoka bandari ya Kipumbwi, kilomita 80 kutoka Tanga, kilomita 60 kutoka Zanzibar kwa njia ya bahari, na kilomita 180 kutoka Dar es Salaam. Pia ujenzi wa barabara ya Tanga–Pangani–Saadani–Bagamoyo unatarajiwa kufungua zaidi ukanda huo wa pwani.
Mbali na fukwe, mkoa wa Tanga una vivutio vingi vya utalii ikiwemo Mapango ya Amboni, Hifadhi ya Taifa ya Saadani, Hifadhi ya Taifa ya Mkomazi, Milima ya Usambara (Lushoto), pamoja na urithi wa kihistoria kama makaburi ya vita ya kwanza ya dunia na Kisiwa cha Toten.
Ameongeza kuwa Tanga pia ni kitovu cha utamaduni wa Kiswahili, likiwa na historia ya muziki wa taarab, vyakula vya asili, pamoja na kuwa chimbuko la lugha ya Kiswahili, ambapo mwanazuoni mashuhuri Sheikh Shaban Robert alizaliwa katika eneo hilo.
Kwa sasa, amesema mkoa unapokea wageni kutoka ndani na nje ya nchi, hususan kutoka Kenya, Ujerumani, Uholanzi na Uswisi, wanaovutiwa na historia, mazingira asilia na utamaduni wa Tanga.
Dkt. Burian amesema jitihada hizo zinaunga mkono azma ya Rais Samia Suluhu Hassan ya kuitangaza Tanzania kupitia kampeni ya Royal Tour na kuongeza idadi ya watalii.
Kwa upande wa uchumi, amesema mkoa wa Tanga kwa sasa unachangia takribani shilingi trilioni 9.8 katika pato la taifa, na una mpango wa kuongeza mchango huo na kufikia nafasi ya pili kitaifa baada ya Dar es Salaam ifikapo mwaka 2028.
Amehitimisha kwa kusema kuwa Tanga ni eneo sahihi kwa uwekezaji na utalii, akiwakaribisha wawekezaji na watalii kutoka ndani na nje ya nchi kuja kutumia fursa zilizopo.

Na, Mwandishi Wetu, Muleba – Kagera
KAIMU Mganga Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Bw. Salum Kimbau amesema maandalizi ya Mpango wa Afya Moja kwa mkoa wa Kagera utaunufaisha mkoa huo kwa kuzingatia malengo yake ya kuboresha uratibu na utekelezaji wa Dhana ya Afya ya Moja na kuendelea kutatua changamoto zilizopo na zenye mwingiliano kati ya binadamu, wanyama na mazingira
Amezungumza hayo wakati akifungua kikao kazi cha wataalamu wa masuala ya Afya Moja kutoka sekta mbalimbali zikiwemo za afya, mifugo, mazingira, wanyamapori na kilimo ambao wamekutana katika Halmashauri ya Wilaya ya Muleba mkoani Kagera kwa siku tano kuanzia tarehe 27 Aprili hadi 01 Mei, 2026 ili kuandaa Mpango huo utakaotumika kubaini rasilimali zitakazosaidia kutatua changamoto na vihatarishi vya afya ya binadamu, wanyama na mazingira.

Bw. Kimbau amesema kuwa, mkoa utanufaika kwa uwepo wa Mpango huo kwani utaongeza tija katika kutatua changamoto zinazokabili sekta hizo hususan katika kuendelea kutatua changamoto za mwingiliano wa magonjwa kutoka kwa wanyama kwenda kwa binadamu na binadamu kwenda kwa wanyama.
“Tunashukuru kuufikia mkoa wetu wa Kagera, tunajua kuwa asilimia 75 ya magonjwa yanatokana na mwingiliano ulipo kati ya wanyama na binadamu, hivyo kuandaliwa kwa mpango kutasaidia utekelezaji wa Dhana ya Afya Moja kwa kushirikiana pamoja, hivyo utatusaidia kutatua changamoto zilizopo na kuwa na jamii salama,” alisema Bw. Kimbau

Aliongezea kuwa ufanisi wa mpango huu unategemea ushirikishwaji wa sekta zote zinazohusika ili kuleta matokeo chanya.
Naye Mratibu wa Maafa kutoka Idara ya Menejimenti ya Maafa sehemu ya Afya Moja kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Bi. Valentina Sanga amesema kuwa, Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kushirikiana na Shirika lisilo la Serikali la CIHEB Tanzania kupitia Mradi wa Usalama wa Afya Duniani imeratibu maandalizi ya uwepo wa mpango huo huku akisihi kuunganisha nguvu ya pamoja katika kuhakikisha utekelezaji wake unaleta matunda yanayotarajiwa.

Aidha, aliwasihi wataalamu wa Masuala ya Afya Moja kutumia fursa hiyo kuja na Mpango utakaoinufaisha Kagera, kwa kuzingatia ni miongoni mwa Mikoa inayokumbwa na majanga ya mlipuko mengine yakichangiwa na mwingiliano wa wanyama na binadamu.

“Dhana ya Afya Moja (One Health) inatoa fursa ya kutambua uhusiano wa karibu kati ya afya ya binadamu, wanyama, na mazingira. Inasisitizwa kuendelea kujifunza zaidi dhana hii ili kutatua changamoto zilizopo zikiwemo za milipuko ya magonjwa na kuweza kuyakabili endapo yanatokea katika maeneo yetu,” alisisitiza Bi. Valentina

Aliongezea kuwa, Mpango huo utasaidia kutatua changamoto za masuala ya kiafya zinazotokea katika Halmashauri za mkoa wa Kagera, kujiandaa na kukabili majanga hayo ili kuwa na jamii salama kwa maendeleo ya Taifa kwa ujumla.

Kwa upande wake Mwakilishi wa Shirika la CIHEB Tanzania, Bw. Mark Lwakatare alisema mradi wa Usalama wa Afya Duniani utaendelea kushirikiana na mikoa husika katika kuimairisha utekelezaji wa dhana ya Afya Moja ili nchi iweze kukabiliana na vihatarishi vya majanga mbalimbali.

“Mradi huu unashirikiana na Serikali kuboresha na kuimarisha utekelezaji wa afua mbalimbali kupitia dhana ya Afya Moja nchini, hivyo mradi utaendelea kushirikiana katika kujiandaa na kukabili athari katika afya ya binadamu, manyama na mazingira,” alisisitiza Lwakatare.
Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania (TCDC) kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa mkoa wa Njombe,Kamati ya Michezo ya Meimosi, Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) imeshiriki zoezi la upandaji miti lililofanyika katika eneo la Ofisi ya Mkuu wa mkoa wa Njombe.
Katika zoezi hilo Mkuu wa mkoa wa Njombe Mhe. Anthony Mtaka awewahimiza Wafanyakazi na wananchi kuhakikisha kuwa wanapanda miti yenye kuleta faida hususan miti ya matunda ili kusaidia upatikanaji wa kipato cha mtu mmojammoja na Taifa kwa ujumla.
" Kumekuwa na tabia ya watu wengi kupanda miti kwaajili ya kivuli tu, pasipo faida yoyote, vi vizuri sasa tukapanda miti yenye kuleta faida kubwa kama vile miti ya matunda, amesema Mtaka.
Zoezi hilo lilihudhuriwa na Viongozi mbalimbali akiwemo Katibu Tawala wa mkoa wa Njombe, Rais wa Shirikisho la Wafanyakazi Tanzania (TUCTA), Mwenyekiti wa Kamati ya Meimosi na Watumishi wa Serikali kutoka Wizara na Taasisi mbalimbali.

Na. Josephine Majura na Saidina Msangi, WF, Dodoma.
Taasisi kongwe ya dini ya kiislamu ya Twariqa Tulqadirya Arazakia Jailania Tanzania yenye makao yake makuu mkoani Arusha, imedhamiria kufanya sensa ya watu na mali za taasisi hiyo ili kupata Idadi sahihi ya waumini wake.
Lengo la zoezi hilo ni kuweza kufanya kazi kwa Ufanisi na kuyafahamu makundi mbali mbali yaliyomo katika taasisi hiyo yakiwemo makundi ya Viongozi Vijana,Wanawake,Walemavu,Yatima,Wajane na Wagane ili waweze kupatiwa huduma stahiki katika Mikoa yote ya Tanzania .
Akizungumza na Vyombo vya Habari mkoani Arusha Mwenyekiti wa Twariqa Taifa Shekhe Mubaraka Salim Gahran amesema kuwa taasisi hiyo ilifanya sensa ya kitwariqa mnamo mwaka 1932,ambapo imepita kipindi kirefu bila zoezi hilo kufanyika hali ambayo inapelekea tasisi kushindwa kuwa na Idadi kamili ya watu pamoja na mali zilizopo sasa.
Shekhe Gahrani amesema kuwa pia Ofisi yake imeona ni vema kufanya uhakiki wa mali zilizopp kwa kuwa tangu kiongozi wao Daruweshi Mti Mkavu alipofariki takribani mwaka mmoja na nusu kuna baadhi ya vitu wanapaswa kuviweka sawa ili kuhakiki mali zote na kuepusha migogoro isiyo ya lazima ndani yao ikiwa ni pamoja na watu binafsi kujimilikisha mali za taasisi hiyo nchini.
"Hii ni sensa ya kawaida ya kitwariqa na inawahusu wanatwariqa wa Daraweshi Mti Mkavu na tunataka kuhakiki kila kitu kuanzia Idadi ya Waridi wetu waliopata Ijaza,Elimu zao za kawaida,kufahamu haya yote itatuwezesha sisi Viongozi kujua mahitaji yao na tuna watu wa aina gani na tunawahudumiaje na kwa namna gani bila kusahau migogoro isiyo ya lazima na isielewele vinginevyo.Alisisitiza Shekhe Gahran
Nae katibu mkuu wa twariqa Taifa shekhe Haruna Hussein Lotha ameiomba serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kuwapa Ushirikiano wakati wa zoezi hilo ili kufanya zoezi hilo kutekelezwa kwa utulivu na kwa kufuata taratibu.
Shekhe Haruna Hussein amesema kuwa tangu wameingia madarakani hawajui idadi ya waumini wao,majengo wala mali walizonazo ili kuwasaidia kujua mapungufu yaliyopo na kisha kuboresha kwa kuwa kazi ya dini ni kujenga Imani za watu na kuwahudumia kiroho.
"Taasisi yetu imekuwa ikishirikiana na serikali yetu kila eneo hivyo tunatazamia kuwa mashirikiano haya yatakuwa endelevu na pia tumetumia vyombo vya habari ni kuhakikisha jamii inaendelea kupata taarifa kwa wakati na zoezi litakapoanza katika mikoa yote ya Tanzania,liwe rahisi "Amesisitiza Katibu Lotha
Na Mwandishi wetu- DODOMA
Katibu Tawala Mkoa wa Dodoma, Dkt. Khatibu Kazungu, amesema Ofisi yake ikishirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu Idara ya Menejimenti ya Maafa ipo katika hatua ya kuanzisha Kituo cha Operasheni ya Dharura katika Mkoa ikiwa ni utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Usimamizi wa Maafa ya mwaka 2004.
Dkt. Kazungu ameyasema hayo leo tarehe 27 Aprili,2026 jijini Dodoma kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma wakati akifungua mafunzo ya siku nne ya kujiandaa na kukabiliana na maafa kwa Timu ya kukabiliana na dharura ya Mkoa ambayo yameandaliwa na Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Idara ya Menejimenti ya Maafa pamoja na uanzishaji wa kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura cha Mkoa.
Aidha, Dkt. Kazungu ameshukuru ujio wa elimu hiyo ndani ya Mkoa wa Dodoma akisema itasaidia kuwajenga kielimu Maafisa wa Mkoa ili waweze kupeleka elimu katika ngazi za Wilaya.
"Elimu hii itasaidia kuongeza ujuzi na weledi kwa Maafisa wa Mkoa kwani majanga haya yamekuwa na madhara mengi kwa jamii," alisema Dkt. Kazungu.
Pia, alisisitiza ukusanyaji wa taarifa kwa wakati na kabla ya majanga ili kurahihisisha kuyakabili pamoja na kuboresha mawasiliano ya karibu baina ya wananchi na Maafisa wa Mkoa.
"Lazima kuwepo ushirikiano baina yetu na Wananchi ili tuweze kupambana na maafa ndani ya Mkoa wetu wa Dodoma," alisisitiza.
Awali Kaimu Mkurugezi Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu, Kanali Selestine Masalamadu aliupongeza Mkoa wa Dodoma kwa kuwa tayari kupokea elimu ya maafa na majanga na kusema kuwa Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Idara hiyo ina jukumu la kuratibu shughuli za Kuzuia, Kupunguza Athari, Kujiandaa, Kukabiliana na Kurejesha hali baada ya maafa.
![]() |
Vilvile, alisema kuwa Ofisi inaendelea kuratibu uanzishaji na uendeshaji wa Vituo vya Operesheni na Mawasiliano ya Dharura vya Mikoa pamoja na Timu za kukabiliana na dharura , ikiwa ni utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Usimamaizi wa Maafa ya Mwaka 2004, Sheria ya Usimamaizi wa maafa Na. 6 ya mwaka 2022 na kanuni zake.
“Lengo la mafunzo haya ni kuimarisha uwezo wa Mkoa kuratibu shughuli za usimamaizi wa maafa ili kupunguza madhara wakati wa dharura. Mafunzo haya yatawajengea uwezo washiriki katika maandalizi, uratibu wa taarifa, mwitikio wa haraka, usimamizi rasilimali na utoaji wa huduma kwa waathirika,” alifafanua Kanali Masalamadu.
Aidha, alibainisha kwamba kila Mkoa unatakiwa kuwa na chumba maalum kwa ajili ya kuratibu shughuli za maafa na dharura huku akihimiza kuharakishwa kwa upatikanaji wa chumba chenye sifa stahiki kuwezesha uanzishwaji kamili wa Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura Mkoa wa Dodoma.
MWISHO















