Wafugaji nchini wanatarajiwa kunufaika na biashara ya kisasa ya mifugo baada ya Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) kuanza kuingiza mifugo katika Mfumo wa Stakabadhi za Ghala, utakaounganisha taarifa za mifugo kidijitali na kuwawezesha wanunuzi kushindana kwa uwazi kupitia Soko la Bidhaa Tanzania (TMX).

Akizungumza katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), Mkurugenzi Mtendaji wa WRRB, Bw. Asangye Bangu, amesema baada ya mafanikio ya kusimamia bidhaa 18 za mazao ya kilimo kupitia mfumo huo, sasa bodi imepanua huduma zake kwa kujumuisha mifugo.

Amesema hatua hiyo inatokana na mahitaji ya wafugaji waliokuwa wakihoji kwa nini mfumo huo unawanufaisha wakulima pekee huku sekta ya mifugo ikibaki nje.

"Tumekuja na bidhaa mpya ambazo zimeongezwa kwenye mfumo, na kubwa zaidi tumewafikia wafugaji. Tulikuwa tunasimamia bidhaa 18 za mazao ya kilimo, lakini sasa tumeingia rasmi kwenye bidhaa za mifugo," amesema.

Bw. Bangu amesema WRRB inalenga kuunganisha biashara ya mifugo na TMX, ambapo taarifa za kila mnyama zitawekwa kidijitali ili wanunuzi waweze kuzifikia kwa urahisi, kushindana kwa uwazi na kufanya maamuzi ya ununuzi kwa kutumia taarifa sahihi badala ya makadirio.

Ameeleza kuwa mfumo huo utatumia taarifa zinazopatikana kupitia hereni za utambuzi wa mifugo zilizozinduliwa na Rais Samia Suluhu Hassan, ambazo zina namba maalumu zinazobeba taarifa za kila mnyama.

"Tunafahamu Mheshimiwa Rais Samia miaka miwili iliyopita alizindua uwekaji wa hereni kwenye mifugo. Sisi kama WRRB tunapiga hatua zaidi kwa kutumia taarifa zilizopo kwenye hereni hizo kuingiza mifugo kwenye Mfumo wa Stakabadhi za Ghala. Hereni hiyo ndiyo itakuwa msingi wa stakabadhi kwa kuwa ina namba na taarifa zote za mnyama," amesema.

Amefafanua kuwa mfumo huo utawanufaisha wafugaji wanaojishughulisha na unenepeshaji wa mifugo kwa kuwa mifugo yao itahifadhiwa katika maeneo maalumu yatakayokuwa yanatambulika kama ghala, huku wafugaji wakipewa stakabadhi zitakazowawezesha kupata mikopo kutoka taasisi za fedha.

Kwa mujibu wa Bangu, WRRB tayari imefikia makubaliano na Benki ya NBC ambayo imekubali kutoa mikopo kwa wafugaji watakaoweka mifugo yao kwenye ghala.

"Wengi wanauliza ghala litakuwaje. Kwa upande wa mifugo, zizi ndilo litakuwa ghala. Mifugo itatunzwa katika maeneo maalumu yenye chakula na huduma za matibabu, huku mfugaji akiwa na stakabadhi inayomwezesha kupata fedha bila kulazimika kuuza mifugo yake mapema," amesema.

Bangu amesema hatua nyingine muhimu ni kuondoa utaratibu wa kupanga bei kwa kutazama mwonekano wa mnyama pekee, badala yake mifugo itapimwa kwa uzito ili bei iweze kuamuliwa kwa kuzingatia kilo halisi za mnyama.

"Leo hii kwenye minada mingi ng'ombe anapimwa kwa macho, anaonekana mnene au mwembamba ndipo bei inawekwa. Sisi tunataka mifugo ipimwe kwa uzito ili bei iwe ya haki kwa mfugaji na mnunuzi. Hii itakuwa mkombozi mkubwa kwa wafugaji na pia itarahisisha upatikanaji wa taarifa zinazohitajika katika masoko ya ndani na kimataifa," amesema.

Serikali imewaagiza wazalishaji wote nchini kutumia alama ya 'Made in Tanzania' ili kuongeza imani kwa bidhaa zinazozalishwa nchini na kuimarisha ushindani wake katika masoko ya kimataifa.

Agizo hilo limetolewa  na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Immanuel Nchimbi, kwenye kilele cha Usiku wa Jubilei ya Dhahabu (Miaka 50) ya Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TANTRADE), uliofanyika Ukumbi wa Mlimani City, Dar es Salaam. Sherehe hizo zilienda sambamba na utoaji wa tuzo kwa washirika muhimu wa mamlaka hiyo. Udhibiti wa Viwango na Huduma za Kifedha.

Aidha, Makamu wa Rais amezitaka taasisi zinazosimamia viwango na huduma za kifedha kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi ili kuhakikisha bidhaa za Tanzania zinakidhi viwango vya kimataifa. Alisema matumizi ya alama ya 'Made in Tanzania' yataongeza utambulisho wa bidhaa zenye ubora na kuimarisha heshima ya taifa katika biashara za kimataifa.

 "Nazipongeza taasisi za fedha kwa kutoa mikopo yenye masharti nafuu kwa viwanda vidogo na vya kati, akisema hatua hiyo imeendelea kupunguza changamoto za upatikanaji wa mitaji kwa wajasiriamali na kuchochea ukuaji wa uzalishaji nchini."amesema Balozi Nchimbi

Amesema Serikali itaendelea kuweka sera rafiki, kuboresha miundombinu na kuimarisha sekta binafsi ili kujenga uchumi wa viwanda wenye ushindani. Ameongeza kuwa maadhimisho ya Jubilei ya Dhahabu ya TANTRADE ni fursa ya kutathmini mafanikio yaliyopatikana, ikiwemo kuongezeka kwa viwanda, uzalishaji, ajira na upanuzi wa masoko ya bidhaa za Tanzania duniani.

Kwa upande wake Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Judith Kapinga (Mb), amesisitiza kuwa manufaa makubwa ya rasilimali zilizopo nchini yatapatikana Tanzania itakapowekeza katika kuchakata na kuzalisha bidhaa za mwisho zenye ubora wa juu badala ya kuuza malighafi ghafi nje ya nchi.

Waziri Kapinga amebainisha kuwa hatua hiyo itafungua masoko mapya, itaongeza thamani ya mauzo ya nje, na kuinua uchumi wa wananchi kwa ujumla.

Mhe. Kapinga ameeleza kuwa, ili kujenga uchumi imara wa viwanda na wenye ushindani, kuna haja ya kubadili mtazamo wa kibiashara kwa kuhakikisha mazao ya kilimo, mifugo, uvuvi, misitu na madini yanageuzwa kuwa bidhaa zilizofungashwa vizuri na kukidhi viwango vya kimataifa.

Amesisitiza kuwa uwekezaji mkubwa katika teknolojia za kisasa una mchango mkubwa katika kuongeza kiwango cha uzalishaji, kuboresha ubora wa bidhaa zinazotengenezwa nchini, kupunguza gharama za uendeshaji, na kuzipa bidhaa za Tanzania uwezo mkubwa wa kushindana katika soko la kimataifa.



Kukamilika kwa ujenzi wa Daraja la Upinde la Mawe katika Mto Mmbaga, Wilaya ya Ngorongoro, kunatarajiwa kufungua fursa za kijamii na  kiuchumi kwa kurahisisha usafiri na usafirishaji, kuboresha upatikanaji wa huduma za kijamii pamoja na kuchochea biashara kwa wakazi wa eneo hilo na maeneo jirani.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa daraja hilo katika mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka 2026, Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa, Wazo Michael Mwang'onda, amesema kuwa mradi huo umeondoa adha ya muda mrefu iliyokuwa ikiwakabili wananchi wa maeneo hayo, hususan kipindi cha msimu wa mvua ambapo ilikuwa changamoto kubwa kuvuka Mto Mmbaga. 

Amesisitiza kuwa, Serikali ya awamu ya sita imeendelea kuboresha miundombinu ya barabara kwa kuwekeza kwa kiwango kikubwa katika ujenzi wa barabara na madaraja ili kuimarisha miundombinu na kuharakisha maendeleo ya kijamii na kiuchumi nchini.

"Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan alitambua changamoto zilizokuwa zinawakabili wananchi wa eneo Oldonyosambu na majirani zake na kuelekeza fedha zitolewe kwa ajili ya ujenzi wa daraja hili, ambalo sasa limekuwa mkombozi kwa jamii, tuendelee kulitunza na kulitulitumia kwa usafirishaji wa watu na bidhaa, kupanua fursa za biashara na kuimarisha shughuli za kiuchumi kwa maendeleo yetu na Taifa letu," Amesema Mwang'onda.

Mwang'onda amesisitiza kuwa, Serikali itaendelea kutekeleza miradi ya maendeleo katika maeneo mbalimbali nchini huku akiwahimiza wananchi kuendelea kudumisha amani na utulivu, ambayo ni msingi wa maendeleo endelevu.

Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Ngorongoro, Yanick Ndoinyo, alipokea kwa furaha kukamilika kwa daraja hilo akisema linahudumia kata za Sale, Pinyinyi na Oldonyosambu kupitia Masusu hadi Jema

Alimshukuru Rais Dk,Samia Suluhu Hassan kwa kusikiliza na kutatua changamoto za wananchi wa Ngorongoro kwa kutoa fedha za Mfuko wa Barabara  zilizowezesha ujenzi wa daraja hilo, akieleza kuwa ni hatua muhimu katika kuboresha mawasiliano, usafiri na maisha ya wananchi wa wilaya hiyo.









Mkemia Mkuu wa Serikali, Dkt. Fidelice Mafumiko, akisaini kitabu cha wageni alipowasilikwemye viwanja vya maonyesho vya Mwalimu Nyerere vilivyopo Barabara ya Kilwa Dar es Salaam Julai 6, 2026.
SHIRIKA la Viwango Tanzania (TBS) limeendelea kutumia Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) kutoa elimu na kuwahamasisha wajasiriamali kuthibitisha ubora wa bidhaa zao ili kukidhi matakwa ya sheria za viwango na kuongeza ushindani wa bidhaa hizo katika soko la ndani na nje ya nchi.
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

Matumizi ya kemikali katika uchakataji wa ngozi yanatarajiwa kupungua kufuatia ubunifu wa Shirika la Utafiti na Maendeleo ya Viwanda Tanzania (TIRDO) wa kubuni dawa ya asili inayotokana na mimea, teknolojia inayolenga kulinda mazingira, afya za watumiaji na kuongeza ushindani wa bidhaa za ngozi za Tanzania katika masoko ya ndani na kimataifa.
 

Na.Mwandishi Wetu-Geneva 

Tanzania imetoa wito wa kuimarishwa kwa ushirikiano wa kimataifa ili kuhakikisha maendeleo ya kasi ya Akili Unde (AI) yanasimamiwa kupitia mifumo ya kimataifa iliyo jumuishi, yenye uwazi na usawa, ikitahadharisha kuwa nchi zinazoendelea hazipaswi kuachwa nyuma wakati teknolojia hiyo ikiendelea kubadili uchumi na jamii.

Akizungumza mbele ya zaidi ya wajumbe 190 wanaowakilisha serikali, mashirika ya kimataifa, sekta binafsi na jamii ya teknolojia duniani katika mdahalo wa Kimataifa kuhusu Utawala wa Akili Unde (Global Dialogue on AI Governance), Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Angellah Kairuki (Mb), aliwasilisha dira ya Tanzania ya kutumia Akili Unde kama kichocheo cha maendeleo ya taifa huku ikiimarisha mifumo ya kuhakikisha matumizi yake yanakuwa ya kuwajibika.

Waziri alisema Tanzania inaichukulia Akili Unde kuwa nguzo muhimu ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 na kichocheo muhimu cha uchumi wa kidijitali unaochipukia. Alieleza kuwa Serikali inaendelea kutekeleza mageuzi ya kina ya sera na mifumo ya udhibiti ili kuweka mazingira imara yanayochochea ubunifu huku yakilinda haki za wananchi na kujenga imani ya umma.

“Tanzania inaamini kuwa Akili Unde ina uwezo wa kuleta mageuzi katika sekta za kilimo, afya, elimu, huduma za kifedha na utawala wa umma,” alisema Mhe. Kairuki. “Hivyo, matumizi yake yanapaswa kuwa salama, jumuishi na yalenge kuhakikisha wananchi wote wananufaika.”

Alieleza hatua zinazotekelezwa kuimarisha utawala wa Akili Unde, ikiwemo kuandaa mifumo ya udhibiti, kuboresha mifumo ya usimamizi wa data, kuimarisha ulinzi wa faragha na usalama wa mtandao, pamoja na kuandaa miongozo ya kitaifa ya matumizi ya Akili Unde katika sekta za kimkakati kama elimu na afya.

Waziri pia alieleza uwekezaji unaoendelea wa Serikali katika miundombinu ya kidijitali, akitaja upanuzi wa Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano (NICTBB) pamoja na maendeleo ya Miundombinu ya Umma ya Kidijitali (Digital Public Infrastructure – DPI) kuwa msingi muhimu wa kupanua mawasiliano ya kidijitali na kuwezesha wananchi wengi zaidi kupata huduma zinazotumia Akili Unde nchini kote.

Mbali na mageuzi ya ndani ya nchi, Mhe. Angellah Kairuki alisisitiza kuwa utawala madhubuti wa Akili Unde unahitaji ushirikiano endelevu wa kimataifa.

Alithibitisha dhamira ya Tanzania ya kuendelea kushirikiana kwa karibu na Umoja wa Kimataifa wa Mawasiliano (ITU), Umoja wa Afrika (AU), Umoja wa Mawasiliano Afrika (ATU), Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) ili kuendeleza mifumo ya kidijitali inayoweza kushirikiana, inayorahisisha ubunifu, biashara na huduma za kuvuka mipaka huku ikilinda mamlaka ya nchi na usalama wa data.

Akihitimisha hotuba yake, Waziri Kairuki alitoa wito wa kuimarishwa kwa ushirikiano wa kimataifa katika uhamishaji wa teknolojia, maendeleo ya ujuzi, ushirikiano wa tafiti, ubunifu na uwekezaji katika miundombinu ya kidijitali. Alisisitiza kuwa kuziba pengo la kidijitali kutahitaji hatua za pamoja ili kuhakikisha manufaa ya Akili Unde yanagawanywa kwa usawa kati ya nchi zilizoendelea na zinazoendelea.

Mdahalo wa Kimataifa kuhusu Utawala wa Akili Unde unawakutanisha watunga sera, viongozi wa serikali, wataalamu wa teknolojia na wadau wa sekta binafsi kutoka duniani kote kwa lengo la kujenga mifumo ya kimataifa ya utawala wa Akili Unde na kujadili namna teknolojia hiyo inavyoweza kuchangia maendeleo jumuishi na endelevu.

 Taasisi ya Tiba ya Mifupa na Ubongo (MOI) imesema itaendelea kuimarisha tafiti zinazolenga kuzalisha afua za matibabu zinazozingatia mazingira na vinasaba vya Watanzania, ili kuboresha huduma za matibabu ya magonjwa ya mifupa na mfumo wa fahamu.

Akizungumza na waandishi wa habari Mkurugenzi Mtendaji wa MOI, Balozi Dkt. Mpoki Ulisubisya, Jijini Dar es Salaam Julai 6, 2026, kwenye Maadhimisho ya Miaka 50 ya Maonesho ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba).

Amesema mara nyingi tiba zinazotumika hutokana na matokeo ya tafiti zilizofanyika katika nchi zilizoendelea pamoja na baadhi ya nchi za bara la Afrika, ambapo afua hizo zinaweza kuwa zimezingatia watu wenye vinasaba tofauti, hivyo wao wameona umuhimu wa kufanya tafiti zitakazozalisha afua zinazokidhi mazingira ya Tanzania.

Aidha, amesema MOI imetimiza miaka 30 tangu kuanzishwa kwake na imeendelea kujikita katika maeneo makuu matatu ambayo ni kutoa huduma kwa wagonjwa wa mifumo ya ubongo na mifupa, kufundisha huduma hizo kwa wananchi na wataalam katika ngazi ya shahada ya kwanza, shahada ya pili na ubobezi, pamoja na kufanya tafiti.

Pia amesema taasisi hiyo imeweza kutoa mafunzo kwa wananchi na wataalam kutoka ndani na nje ya Tanzania, hususan katika ukanda wa Afrika Mashariki, Kati, Kusini na Magharibi, ikiwa ni sehemu ya kuimarisha huduma za afya katika kanda hiyo.




 



Na Mwandishi Wetu
TUME ya Nguvu za Atomiki Tanzania (TAEC) imesema Serikali imeanza maandalizi ya kuanzisha mpango wa kuzalisha umeme wa nyuklia, huku ikisisitiza kuwa utekelezaji wa mradi huo utafuata kikamilifu viwango vya kimataifa vya usalama ili kulinda wananchi, mazingira na kuhakikisha matumizi salama ya teknolojia hiyo.

Akizungumza na waandishi wa habari katika banda la TAEC kwenye Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Mkurugenzi Mkuu wa TAEC, Prof. Najat Kassim Mohammed, amesema Tanzania ipo katika hatua za awali za maandalizi kabla ya kuingia rasmi katika awamu ya kwanza ya utekelezaji wa mpango huo.

Alisema Serikali inaendelea kuimarisha mfumo wa kisheria, sera na taasisi zitakazosimamia matumizi ya teknolojia ya nyuklia ili kuhakikisha uzalishaji wa umeme unafanyika kwa kuzingatia viwango vya usalama vinavyokubalika kimataifa, sambamba na kujenga uelewa wa wananchi kuhusu matumizi ya nishati hiyo.

Prof. Najat alisema TAEC tayari imewaalika wataalamu wa kimataifa kufanya tathmini ya utayari wa Tanzania katika kutekeleza mpango huo.

Alieleza kuwa endapo tathmini hiyo itaridhisha, nchi itapata kibali cha kuendelea na hatua inayofuata ya utekelezaji.

Aidha, alisema Serikali inalenga ndani ya kipindi cha miaka saba kuanza kuzalisha umeme wa nyuklia, hatua inayotarajiwa kuongeza upatikanaji wa nishati ya uhakika, kuimarisha ukuaji wa uchumi na kuchochea maendeleo ya sekta ya viwanda.

Akizungumzia upatikanaji wa malighafi, Prof. Najat amesema Tanzania ina akiba ya madini ya Urani, ambayo ndiyo malighafi muhimu katika uzalishaji wa nishati ya nyuklia kuongeza kuwa madini ya urani lazima yachakatwe kwa teknolojia maalumu kabla ya kutumika kama mafuta ya nyuklia.

Alieleza kuwa katika hatua za mwanzo, urani itakayochimbwa nchini itasafirishwa kwenda nje ya nchi, ikiwemo Urusi, kwa ajili ya kuchakatwa, kisha kurejeshwa Tanzania kwa matumizi ya kuzalisha umeme.

Prof. Najat alisema mradi wa uchimbaji wa madini ya urani unatarajiwa kuanza katika eneo la Mkuju, mkoani Ruvuma, huku shughuli za utafiti zikiendelea katika maeneo mengine ili kubaini akiba zaidi zenye uwezo wa kuchimbwa kibiashara.

Pamoja na hayo, aliwataka wananchi kujenga uelewa sahihi kuhusu teknolojia ya nyuklia na kuondoa hofu zisizo na msingi, akisisitiza kuwa Serikali inatekeleza mpango huo kwa kuzingatia miongozo na viwango vya kimataifa vinavyolenga kuhakikisha usalama wa watu, mazingira na miundombinu.

Alisema matumizi ya teknolojia ya nyuklia yana mchango mkubwa katika maendeleo ya taifa, siyo tu katika uzalishaji wa umeme, bali pia katika sekta za afya, kilimo, viwanda na utafiti wa kisayansi.

 


KAMPUNI ya mawasiliano ya Airtel Tanzania imeendelea kuimarisha mchango wake katika maendeleo ya jamii kwa kuunganisha ajenda za afya, ustawi wa wafanyakazi na uhifadhi wa mazingira kupitia udhamini wake wa mbio za ‘Great Ruaha Marathon 2026’, zilizofanyika hivi karibuni ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Ruaha.

Ikiwa Mdhamini Rasmi kutoka sekta ya Mawasiliano, Airtel ilishiriki pamoja na mamia ya wakimbiaji katika tukio ambalo limeendelea kujijengea sifa kama moja ya mbio za kipekee nchini zinazochanganya michezo, utalii na juhudi za kuhifadhi mfumo wa ikolojia wa Mto Mkuu wa Ruaha.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo mkoani Iringa, Mkurugenzi wa Rasilimali Watu wa Airtel Tanzania, Bi. Stellah Kibaja, alisema ushiriki wa kampuni hiyo unaonyesha dhamira yake ya kuleta mchango chanya kwa jamii, hatua inayokwenda sambamba na shughuli zake za kibiashara.

"Airtel tunaamini kuwa mahusiano imara hayajengwi kupitia mtandao wetu pekee, bali kupitia watu, uzoefu wa pamoja na jamii zinazounganishwa na lengo moja. Ndiyo maana tunajivunia kuwa sehemu ya Great Ruaha Marathon, tukio linaloendana na maadili yetu ya kuhamasisha afya bora, kuunga mkono jamii na kushiriki katika mipango yenye manufaa ya kudumu," alisema Bi. Kibaja.

Katika kuonyesha mfano wa uongozi unaoshiriki kwa vitendo, Airtel iliwashirikisha wafanyakazi 20 katika mbio hizo, wakiwemo wajumbe watatu wa Kamati ya Utendaji ya kampuni hiyo.

Bi. Kibaja alibainisha kuwa kampuni hiyo inaamini afya ya wafanyakazi ndio msingi mkuu wa mafanikio ya taasisi yoyote inayotaka kupiga hatua.

"Watu wenye afya hujenga timu imara, timu imara hujenga biashara zenye mafanikio, na biashara zenye mafanikio huchangia zaidi maendeleo ya jamii. Uongozi hauonekani kwenye vikao pekee, bali pia katika kushiriki bega kwa bega na wafanyakazi na kuhamasisha wengine kupitia matendo," alisisitiza.

Aliongeza kuwa Airtel imeendelea kuwekeza katika programu za ustawi wa wafanyakazi zinazolenga kuimarisha afya ya mwili, akili na uwiano kati ya kazi na maisha binafsi, hatua inayosaidia kuongeza tija kazini na kuboresha huduma kwa wateja.

Mbali na michezo, Mkurugenzi huyo alieleza kuwa Airtel inaunganisha mamilioni ya Watanzania kila siku kupitia huduma za sauti, intaneti, intaneti ya nyumbani (Airtel Smart Box) na Airtel Money, huku ikizidi kupanua mtandao wake hadi vijijini.

"Mawasiliano ni zaidi ya kuunganisha watu; ni kufungua fursa. Iwe ni mwanafunzi anayesoma mtandaoni, mkulima anayepokea malipo kupitia Airtel Money, au mfanyabiashara anayekuza biashara yake kidijitali, kila muunganisho una nafasi ya kuboresha maisha ya Watanzania," alisema.

Akifunga maelezo yake kabla ya kuanza kwa mbio hizo, Bi. Kibaja aliwataka washiriki kuona mbio hizo kama jukwaa la kipekee la kuleta mabadiliko.

"Haijalishi unamaliza wa kwanza au wa mwisho. Kilicho muhimu ni kwamba umechagua kuwekeza katika afya yako, kuunga mkono uhifadhi wa mazingira na kuwa sehemu ya harakati zinazozalisha mabadiliko chanya kwa jamii," alihitimisha.

Mbio za Great Ruaha Marathon zimeendelea kukua na kuwa jukwaa muhimu linalovutia ushiriki wa sekta binafsi nchini katika kuhamasisha afya, kukuza utalii endelevu, na kuimarisha uhifadhi wa ikolojia ya Mto Mkuu wa Ruaha ambao ni uti wa mgongo wa hifadhi hiyo na nishati nchini.
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, amewaalika wafanyabiashara wa Ufaransa kuwekeza Tanzania, akisisitiza kuwa mazingira mazuri ya uwekezaji yaliyopo nchini yanatoa fursa kubwa za kukuza biashara, kuzalisha ajira, kuhamisha teknolojia na ujuzi, pamoja na kuharakisha ujenzi wa uchumi wa viwanda wenye manufaa kwa Tanzania na Ufaransa.
Na Mwandishi Wetu

CHUO cha Benki Kuu ya Tanzania (BOT Academy) kimewahimiza Watanzania, hususani wahitimu wa elimu mbalimbali na watumishi wa sekta ya fedha, kujiunga na programu zake za mafunzo ya muda mrefu na muda mfupi zinazolenga kuwajengea ujuzi wa vitendo unaokidhi mahitaji ya soko la ajira na sekta ya fedha.
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

MAMLAKA ya Elimu Tanzania (TEA) imeeleza kuwa imejikita katika kutafuta rasilimali zitakazowezesha utekelezaji wa Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2023, kwa kuwekeza nguvu katika maeneo matatu ya kipaumbele ambayo ni ujenzi wa miundombinu kwa elimu ya lazima ya miaka 10, maendeleo ya mkondo wa amali pamoja na matumizi ya nishati safi na uhifadhi wa mazingira shuleni.
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

WAFANYABIASHARA na wananchi kwa ujumla wametakiwa kutumia Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) kutembelea banda la Tume ya Ushindani (FCC) ili kupata huduma mbalimbali za papo kwa papo pamoja na elimu kuhusu ulinzi wa mlaji, ushindani wa biashara na udhibiti wa bidhaa bandia.
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

TAASISI ya Elimu Tanzania (TET) imesema ushiriki wake katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba) unalenga kuelimisha wananchi kuhusu maboresho ya mitaala, kuhamasisha elimu jumuishi na kusogeza karibu huduma za vitabu vya kiada na ziada kwa wananchi.

 






>Asema kasi ya maendeleo chini ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, amani, uchumi, afya, maji na miundombinu vimemshawishi kubadili msimamo wa kisiasa.

Baada ya zaidi ya miaka 30 ya kuwa mwanasiasa wa upinzani, aliyekuwa Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Wilaya ya Tanga, Rashid Jumbe, amefanya uamuzi mkubwa wa kisiasa kwa kujiunga na Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Jumbe, ambaye kwa muda mrefu alikuwa mmoja wa viongozi mashuhuri wa Chadema mkoani Tanga, amesema uamuzi wake umetokana na kuridhishwa na utekelezaji wa miradi ya maendeleo pamoja na juhudi za Serikali ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan katika kuimarisha amani, umoja na ustawi wa wananchi.

Akizungumza wakati wa hafla ya kumpokea ndani ya CCM iliyoongozwa na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Tanga, Rajab Abdurhaman, Jumbe alisema hakufanya uamuzi huo kwa papara, bali baada ya kutafakari kwa kina na kujiridhisha kuhusu mwelekeo wa maendeleo ya taifa.


"Nilikuwa mpinzani kwa zaidi ya miaka 30, lakini leo nimeamua kuhitimisha safari hiyo. Kilichonishawishi zaidi ni kazi kubwa inayofanywa na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan katika kuwaletea Watanzania maendeleo na kuhakikisha amani ya nchi inalindwa," alisema.

Alieleza kuwa pia amevutiwa na utekelezaji wa falsafa ya 4R inayosisitiza maridhiano, ustahimilivu, mageuzi na kujenga upya, akisema imeongeza mshikamano na kuimarisha mazingira ya maendeleo nchini.



Akizungumzia Mkoa wa Tanga, Jumbe alisema mabadiliko yanayoonekana katika sekta mbalimbali ni ushahidi wa dhamira ya Serikali ya kuufungua mkoa huo kiuchumi.

Alitaja kuongezeka kwa shughuli katika Bandari ya Tanga, ujenzi wa bandari kavu pamoja na utekelezaji wa miradi mingine ya kimkakati kuwa miongoni mwa hatua zilizochochea ukuaji wa uchumi na kuongeza fursa za biashara.


"Nimekuwa nikipaza sauti kwa miaka mingi nikitaka Tanga ifunguliwe kiuchumi. Leo naona hilo limefanyika. Mizigo imeongezeka bandarini, bandari kavu zimejengwa na shughuli za biashara zinaendelea kukua," alisema.

Katika sekta ya afya, Jumbe alisema maboresho yaliyofanyika katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Tanga Bombo, upatikanaji wa dawa na vifaa tiba pamoja na ujenzi wa zahanati katika kata na mitaa mbalimbali vimempa imani kuwa Serikali inaendelea kuboresha huduma kwa wananchi.

Aidha, alisema upanuzi wa huduma za maji na umeme pamoja na utekelezaji wa mpango wa Bima ya Afya kwa Wote ni miongoni mwa hatua zinazoonyesha dhamira ya Serikali ya kuinua maisha ya Watanzania.




"Nilijiuliza ni hoja gani itanifanya nibaki upinzani wakati maendeleo yanaonekana wazi. Tanga ina amani, huduma zinaimarika na wananchi wanaendelea kunufaika na miradi ya maendeleo," alisema.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Tanga, Rajab Abdurhaman, alisema chama hicho kinaendelea kuimarisha umoja na mshikamano ili kuongeza uwezo wake wa kusimamia maendeleo na kuwatumikia wananchi.



Alisema tangu alipopewa dhamana ya kuongoza CCM mkoani humo, ameweka mkakati wa kuimarisha chama kupitia ushirikiano na wanachama pamoja na kuwakaribisha viongozi kutoka vyama vingine vya siasa.

Rajab alisema mkakati huo umeendelea kuzaa matunda, akieleza kuwa kujiunga kwa Rashid Jumbe ni ishara ya kuongezeka kwa imani ya baadhi ya viongozi wa upinzani kwa juhudi za maendeleo zinazotekelezwa na Serikali.


"Jumbe alikuwa mmoja wa viongozi wakubwa wa upinzani katika Wilaya ya Tanga. Tuliahidi kwamba tutamshawishi aje kushirikiana nasi katika kujenga chama na kuwaletea wananchi maendeleo, na leo tumefanikiwa," alisema.