Tamasha la Pasaka ‘Mtoko na Christina Shusho

Na Mwandishi Wetu

WAZIRI Mkuu wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Nchemba, anatarajiwa kuwa mgeni rasmi Aprili 5, 2026, siku ya Jumapili ya Pasaka, katika tamasha la ‘Mtoko na Christina Shusho Pasaka’ litakalofanyika katika Ukumbi wa Mlimani City, jijini Dar es Salaam ambapo wananchi wataruhusiwa kuingia bure.

Kauli mbiu ya tamasha hilo ni “Ushindi wa Milele.”

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam Machi 30, 2026, Meneja wa msanii wa muziki wa injili Christina Shusho, Humphrey Gatimu, amesema maandalizi ya tamasha hilo yamekamilika kwa asilimia 100 na kusisitiza kuwa wananchi wote wanakaribishwa kushiriki bila malipo yoyote.

Amesema tamasha hilo litawakutanisha waimbaji mbalimbali wa muziki wa injili akiwemo Rose Muhando, Joel Lwaga, The Voice, Bella Kombo, Ambwene Mwasongwe, Neema Gospel Choir, Paul Clement na wengine wengi.
“Milango ya ukumbi itafunguliwa rasmi saa nane mchana, hivyo tunawaomba wananchi kujitokeza kwa wingi na kuwahi mapema ili kuepuka changamoto ya kukosa nafasi ndani,” amesema Gatimu.
Aidha, Gatimu amebainisha kuwa matarajio ya waandaaji ni kupanua wigo wa tamasha hilo mwakani kwa kulipeleka katika mikoa mitatu tofauti, huku wakiahidi kuweka wazi maeneo hayo wakati utakapofika.
Kwa upande wake, mwimbaji wa nyimbo za injili, Shusho amesema tamasha hilo ambalo hufanyika kila mwaka kipindi cha Pasaka, limekuwa jukwaa muhimu la kuwakutanisha wasanii wa muziki wa injili, waumini pamoja na familia kwa lengo la kusherehekea sikukuu hiyo na kuinua vipaji vipya.
Amesema mafanikio ya tamasha hilo yanatokana na amani iliyopo nchini Tanzania, akimshukuru Mungu kwa kumpatia kibali cha kufanya tamasha pamoja na viongozi wa serikali kwa kuendelea kudumisha utulivu na maendeleo ya taifa.
“Tunawahimiza watu kufika mapema ili waweze kushiriki kikamilifu ibada ya sifa na kuabudu pamoja nasi, kwani kuna mambo mengi mazuri yameandaliwa kwa ajili ya kumtukuza Mungu,” amesema Shusho.
Naye mwimbaji kutoka kundi la The Voice, Obedi Mark amesema tamasha hilo limekuwa chachu kwa wasanii wengi kukuza vipaji vyao sambamba na kueneza ujumbe wa injili kupitia muziki.
Kwa upande wake mwanakwaya wa kwaya ya Mt Cecilia Makuburi, Joseph Atanasi amesema wao kama kwaya watashiriki kikamilifu katika tamasha hilo wakiwa wamejiandaa vyema kuendelea kumsifu Mungu kupitia uimbaji.
 

Na.Mwandishi Wetu

TUME ya Ushindani (FCC) Kanda ya Nyanda za Juu Kusini imeadhimisha Wiki ya Haki za Mlaji Duniani kwa kutoa msaada wa vifaa tiba katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya, ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za kuboresha huduma za afya kwa wananchi.

Shughuli hiyo imefanyika tarehe 31 Machi, 2026 ambapo FCC imekabidhi vifaa tiba vinne vya Oxygen Flow Meter vitakavyosaidia wagonjwa wanaohitaji huduma ya hewa tiba, hususan wale wanaopata changamoto ya kupumua.

Akizungumza wakati wa hafla ya makabidhiano hayo, Mkuu wa FCC Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, Bw.Dickson Mbanga, amesema kuwa tukio hilo ni sehemu ya kuadhimisha Wiki ya Haki za Mlaji Duniani pamoja na kutimiza miaka mitatu tangu kuanzishwa kwa ofisi hiyo katika ukanda huo.

Mbanga ameeleza kuwa FCC imeona ni vyema kutumia maadhimisho hayo kwa kutoa mchango wa kijamii utakaoleta tija moja kwa moja kwa wananchi, hasa katika sekta ya afya ambayo ni nyeti na muhimu kwa ustawi wa jamii.

 "Vifaa hivyo vitasaidia kuongeza uwezo wa hospitali katika kuhudumia wagonjwa wanaohitaji msaada wa hewa tiba, hivyo kupunguza changamoto zinazoweza kujitokeza wakati wa utoaji wa huduma hizo."amesema Bw.Mbanga

Kwa upande wake, akipokea vifaa hivyo kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya, Muuguzi Kiongozi Ndg. Petro Seme ametoa shukrani za dhati kwa FCC kwa msaada huo muhimu.

Seme amesema kuwa vifaa hivyo ni vya kisasa na vina uwezo wa kuhudumia wagonjwa wawili kwa wakati mmoja, jambo ambalo litarahisisha upatikanaji wa huduma ya hewa tiba na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma kwa wagonjwa.


Katibu Mkuu-Mipango na Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango Dkt Tausi M. Kida ametoa wito kwa watendaji wa Tume hiyo kufanya kazi kwa weledi, ubunifu na ushirikiano ili kuishi dhana ya kufanya kazi isivyokawaida ili kuyafikia matarajio ya Taifa jumuishi, lenye ustawi, haki na linalojitegemea.

‎Dkt Kida ametoa wito huo leo jijini Dar es Salaam wakati akifungua Mkutano wa Baraza la Wafanyakazi wa Tume ya Taifa ya Mipango.

Aidha, amesisitiza ‎kuwa Serikali ya awamu ya sita chini ya Mheshimiwa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan inayo matarajio makubwa kwa Tume ya kuhakikisha inatekeleza ipasavyo majukumu yake kwa weledi, ari na kuzingatia utu.

‎Mkutano huo, umeongozwa na kauli mbiu isemayo: Utumishi Imara ni Msingi wa Utekelezaji wa Dira 2050.





 

Mabadiliko ya bei za mafuta nchini kwa mwezi Aprili 2026 yamechangiwa kwa kiasi kikubwa na vita inayoendelea kati ya Marekani kwa kushirikiana na Israeli dhidi ya Irani iliyoanza tarehe 28 Februari 2026, mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) imesema jana.

“Kushambuliwa kwa visima vya mafuta, maghala ya kuhifadhi mafuta na viwanda vya kusafisha mafuta (refineries) pamoja na Irani kufunga Lango la Hormuz linalopitisha takriban asilimia 20 ya mafuta yanayosafirishwa kwenda kwenye masoko mbalimbali duniani, imeathiri hali ya uzalishaji mafuta kwenye nchi za Mashariki ya Kati ambako Tanzania inaagiza kwa kiasi kikubwa; imeongeza gharama za usafirishaji kutokana na kukosekana kwa meli za kusafirisha mizigo na imeongeza gharama za bima za meli za mizigo kutokana na vita,” imeeleza taarifa iliyosambazwa kwenye vyombo vya habari jana.

Kwa mwezi Aprili 2026, gharama za kuagiza mafuta (premiums) katika Bandari ya Dar es Salaam zimeongezeka kwa wastani wa asilimia 15.3 kwa mafuta ya petroli na asilimia 10.8​ kwa mafuta ya dizeli na hakuna mabadiliko ya gharama kwa mafuta ya taa.

EWURA imesema ongezeko hilo ni janga la kidunia na Tanzania kama sehemu hiyo inachukua hatua mbalimbali kuhakikisha usalama wa upatikanaji wa mafuta nchini na bei himilivu ili kupunguza madhara ya kiuchumi na kijamii. Kutokana na hali hiyo, EWURA imewashauri wananchi kutumia mafuta kwa uangalifu na ufanisi mkubwa.

 


Na Mwandishi Wetu - Ifakara, Morogoro


Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) imetumia shilingi bilioni 25 kujenga Kituo cha Kupoza Umeme 1x20MVA, 220/33kv pamoja na njia za kusambaza Umeme katika Wilaya ya Kilombero, hatua ambayo imeboresha upatikanaji wa umeme na kuondoa changamoto ya kukatika kwa nishati hiyo katika wilaya za Kilombero, Ulanga na Malinyi.


Hayo yameelezwa leo Jumanne Machi 31, 2026 wakati wa ziara ya Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) waliotembelea mradi huo kujionea utekelezaji wake na tija yake kwa maendeleo ya kiuchumi na kijamii katika ukanda wa Morogoro Kusini.

"Fursa za uwekezaji wilayani hapa zimeongezeka baada ya kukamilika kwa kituo hiki, ninatoa wito kwa wawekezaji kujitokeza kwa wingi kwani tunao umeme wa uhakika na toshelevu," amebainisha Wakili Kyoba. 

Amesema kuimarika kwa huduma ya umeme kumechochea ukuaji wa shughuli za kiuchumi, hususan katika sekta za viwanda, uchimbaji madini, kilimo na huduma za kijamii.

Kwa upande wake, Meneja wa Usimamizi wa Miradi ya Kusambaza Umeme kutoka REA, Mhandisi Deogratius Nagu, amesema gharama za mradi huo zinahusisha pia usimikaji wa mashine umba (transfoma) pamoja na mifumo yake ya uendeshaji, udhibiti na ulinzi, ujenzi wa njia za kusafirisha umeme za msongo wa kilovolti 33 zenye urefu wa kilometa 70 pamoja na gharama za mshauri elekezi.

Mhandisi Nagu amebainisha kuwa, kituo hicho ni cha kisasa, kikiwa na teknolojia kutoka nchi mbalimbali ikiwemo transfoma kutoka Bulgaria, mifumo ya udhibiti na ulinzi kutoka Hispania pamoja na mifumo ya switching (switchgears) kutoka Ujerumani.

“Kituo hiki kimeondoa changamoto ya upatikanaji wa umeme katika wilaya za Kilombero na Ulanga na kuwezesha wananchi kuendeleza shughuli za uzalishaji na kuongeza thamani ya mazao,” alisema Nagu.

Naye Mwenyekiti wa TEF, Deodatus Balile, amesema uwekezaji huo unaonesha matumizi sahihi ya rasilimali za umma na mchango wa REA katika kusambaza huduma ya umeme vijijini.

"Tumeshuhudia uwekezaji mkubwa uliofanywa na Serikali kupitia REA, ni fursa ya maendeleo kwa wananchi ni muhimu tukachangamkia Uwepo wa umeme wa uhakika kujiletea maeendeleo," amesema Balile.

Balile amesema REA imeonyesha mfano wa kipekee kwenye utekelezaji wa majukumu yake na kwamba kazi iliyokwishakamilika ni kubwa na manufaa yake yanaonekana na ametoa wito kwa Taasisi zingine za Serikali kuiga mfano huo.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti, baadhi ya wanufaika wa mradi huo wameeleza namna ambavyo Mradi huo umekuwa mkombozi kwao.

Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Kilimo Ifakara, Setina Ngailo, amesema huduma ya umeme imeimarika na kuondoa changamoto ya kukatika kwa umeme iliyokuwa ikiathiri shughuli za shule.

Kwa upande wake, Msimamizi wa Hospitali ya Kansa ya Good Samaritan, Father Charles Masawe, amesema upatikanaji wa umeme wa uhakika umeongeza ufanisi katika utoaji wa huduma za afya kwa kupunguza utegemezi wa jenereta.

Naye Meneja wa Kiwanda cha Kukoboa Mpunga cha Bezelengule, Enos Machumu, amesema uzalishaji umeongezeka kwa kiasi kikubwa kufuatia kuboreshwa kwa huduma ya umeme, hali iliyorejesha wateja na kulinda mitambo dhidi ya uharibifu.

Kwa ujumla, mradi huo unatajwa kuwa kichocheo muhimu cha maendeleo ya kiuchumi na kijamii katika ukanda wa Morogoro Kusini, huku serikali ikiendelea na juhudi za kusambaza umeme katika vitongoji vilivyobaki ili kuhakikisha upatikanaji wa huduma hiyo kwa wananchi wote.

 Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi, Hassan Saidy amewataka Watumishi wa Wakala kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi ili kuhakikisha ndani ya muda uliopangwa wanafikisha umeme kwenye vitongoji vyote vya Tanzania Bara.


Ametoa maelekezo hayo Machi 30, 2026 Makao Makuu ya REA, Jijini Dodoma wakati wa kikao kazi na Watumishi wote, ambapo amesema baada ya kusaini Mradi mkubwa wa HEP II (B); Mradi wa kusambaza umeme kwenye vitongoji 9,009 tarehe 17 Januari, 2026 na kuongeza kuwa kazi iliyombele ya kila Mtumishi ni kuhakikisha vitongoji hivyo vinafikishiwa umeme katika kipindi cha miaka mitatu yaani hadi 2029.

Awali ilielezwa kuwa Mradi huo wa HEP II (B) ni muendelezo wa jitihada za Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) za kuhakikisha upatikanaji wa huduma ya umeme kwa Wananchi wote wa Tanzania Bara.

Mhandisi Saidy amesema kukamilika kwa Mradi huo wa HEP II (B) pamoja na miradi mingine inayoendelea kutafanya jumla ya vitongoji ambavyo tayari vitakuwa vimefikishiwa umeme kuwa takriban 51,000 kufanya vitongoji vitakavyobakia bila umeme na bila kuwa katika mradi wowote kuwa taklibani 13,000 ambavyo vimepangwa kuanza kusambaziwa umeme ifikapo mwaka 2030 kama ilivyoelekezwa katika Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya Mwaka 2025 – 2030.

Mradi huo unatarajiwa kutoa manufaa ya moja kwa moja kwa Wananchi kwa kuongeza upatikanaji wa huduma ya umeme vitongojini; kuboresha huduma za kijamii hususan katika sekta za afya, elimu na maji; kuwezesha matumizi ya umeme katika shughuli za uzalishaji na kuongeza kipato cha Wananchi pamoja na kuchochea ukuaji wa uchumi wa maeneo ya vitogojini pamoja na kuimarisha ustawi wa jamii.

Aidha; Mhandisi, Saidy aliongoza Watumishi wa REA katika zoezi la kuchagua Viongozi wa TUGHE tawini hapo ambapo kwa kauli moja Watumishi waliwachagua Viongozi wao katika ngazi tofauti kama ifuatavyo: – Mwenyekiti wa Tawi ni Bwana Swalehe Kiloza, Katibu wa Tawi ni Mhandisi, Annet Malingumu; Mjumbe wa Halmashauri ya Tawi ni Bwana Issa Sabuni na Mwakilishi wa Kundi la Vijana, Mhandisi, Issac Sanga.

Viongozi wengine ni pamoja na Wajumbe wa Kamati ya Wanawake ya Tawi la TUGHE REA ni kama ifuatavyo: – Mwenyekiti ni Bi. Wilhelmina Cheyo; Katibu ni Bi. Ruth Emmanuel; Mweka Hazina ni Bi. Aveline Wilfred; Wajumbe Kamati ya Wanawake ni Bi. Happiness Ndunguru na Mhandisi, Bertha Mwaituka.

Vilevile Watumishi wa REA pia walichagua Viongozi kwa upande wa Klabu ya Michezo ya REA ambapo itaongozwa na Bwana Selemani Mtunzy kama Mwenyekiti na Mwenyekiti Msaidizi ni Bwana Samwel Sumwa; Katibu ni Bwana Praygod Ng’hunda; Mweka Hazina ni Bwana Daniel Kisaka wakati Wajumbe wa Kamati Tendaji kwa upande wa Wanaume atakuwa Mhandisi, Thomas Mmbaga na kwa upande wa Wanawake atakuwa Bi. Beatrice Shelukindo.

Wakati huo huo Watumishi wa REA walishiriki kwenye zoezi la kuchagua Viongozi wa Chama cha Kijamii cha Wafanyakazi (REA Social Club) chenye lengo la kusaidiana wakati wa raha na changamoto mbalimbali. Viongozi wa Chama hicho waliochaguliwa ni kama ifuatavyo: Mwenyekiti ni Bwana Elias Gunzer; Katibu ni Bi. Theresia Mang’ung’ula; Mweka Hazina ni Bwana Shukuru Malebeto; Wajumbe wa Kamati Tendaji ni Bwana Pastory Mwijage na Bi. Emmy Chali.


WAKALA wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu nchini (ADEM) kwa kushirikiana na Taasisi ya Elimu Tanzania (TET) wamefanya warsha maalumu ya kuhakiki Matini ya uendeshaji wa Jumuiya za Kujifunza za walimu na viongozi wa elimu (JzK), ikiwa ni hatua muhimu ya kukusanya maoni ya wadau kwa ajili ya kuboresha nyenzo hiyo.

 


Na Carlos Claudio, Dodoma.


Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali imegawa vifaa vya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) vyenye thamani ya jumla ya Shilingi milioni 769 kwa shule za msingi na sekondari 19 zilizopo katika mikoa tisa nchini, ikiwemo Kusini Unguja (Zanzibar), Dodoma, Iringa, Ruvuma, Arusha, Geita, Kilimanjaro, Mbeya na Mtwara.


Akizungumza katika hafla ya ugawaji wa vifaa hivyo iliyofanyika jijini Dodoma, Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Wanu Hafidh Ameir, alisema hatua hiyo ni sehemu ya juhudi za Serikali za kuendelea kuimarisha sekta ya elimu kwa kuzingatia matumizi ya teknolojia za kisasa.


Alisema matumizi ya vifaa hivyo yataongeza uelewa kwa wanafunzi kwa kuwapa fursa ya kujifunza kwa vitendo na kuona, hasa katika masomo ya sayansi na teknolojia. Aidha, alieleza kuwa walimu watanufaika kwa kutumia mbinu bunifu za ufundishaji, kuandaa maudhui kwa ufanisi na kufuatilia maendeleo ya wanafunzi kwa urahisi kupitia mifumo ya kidijitali.


“Serikali inaendelea kutekeleza mageuzi makubwa katika sekta ya elimu kama yalivyoainishwa katika Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014 (Toleo la 2023) pamoja na mitaala iliyoboreshwa, kwa lengo la kuboresha ubora wa elimu na kuandaa rasilimali watu yenye ujuzi unaokidhi mahitaji ya sasa na ya baadaye,” alisema Ameir.


Alitaja baadhi ya hatua zinazoendelea kuchukuliwa kuwa ni pamoja na utekelezaji wa elimu ya lazima ya miaka 10, kuanzishwa kwa mkondo wa elimu ya amali unaolenga kuwapatia wanafunzi stadi za ufundi na ujasiriamali, pamoja na kuimarisha matumizi ya teknolojia za kidijitali katika ufundishaji, ujifunzaji na usimamizi wa elimu.


Aidha, aliongeza kuwa Serikali imeandaa na kuanza kutekeleza Mkakati wa Kitaifa wa Matumizi ya Teknolojia za Kidijitali katika Elimu, sambamba na miongozo mbalimbali ikiwemo mwongozo wa matumizi ya TEHAMA katika shule na vyuo vya ualimu pamoja na mwongozo wa matumizi ya Akili Unde (AI) katika elimu.


Kwa upande mwingine, alisema katika mwaka wa fedha 2025/2026, Serikali imeanzisha madarasa janja matano na kufunga mbao janja 422 katika shule za sekondari, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuboresha mazingira ya ujifunzaji nchini.


Naye Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Caroline Nombo, alisema Serikali inaendelea kuchukua hatua madhubuti za kuboresha elimu kwa kuzingatia mahitaji ya karne ya 21, hususan kwa kuimarisha matumizi ya teknolojia za kidijitali.


Alisema ugawaji wa vifaa hivyo ni sehemu ya utekelezaji wa sera ya elimu pamoja na mkakati wa TEHAMA katika sekta hiyo, na ni ushahidi wa dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha walimu na wanafunzi wanapata nyenzo bora za kufundishia na kujifunzia.


Profesa Nombo alisisitiza kuwa vifaa hivyo vitachangia kwa kiasi kikubwa kuboresha ubora wa elimu, kuongeza ufanisi wa ufundishaji na ujifunzaji, pamoja na kuwawezesha wanafunzi kupata ujuzi wa kidijitali unaohitajika katika dunia ya sasa.








 


Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais na Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) imeweka mikakati madhubuti ya kuimarisha mfumo wa usimamizi wa taka kwa kuandaa Mkakati wa Taifa wa usimamizi wa Taka (2025 - 2030) ambao unalenga kupunguza uzalishaji wa taka kwa kutumia dhana ya uchumi rejeshi.

 

Katika kuhakikisha mnyororo wa usimamizi wa taka unaimarika, Serikali inahamasisha wadau hususan sekta binafsi kuwekeza katika matumizi ya teknolojia za kisasa za kuchakata taka, uwekezaji katika viwanda vya urejelezaji na kuimarisha mifumo ya ukusanyaji wa taka ili kufikia malengo ya kupunguza au kuondoa taka katika Mazingira kwa kuigeuza kuwa malighafi ya uzalishaji wa bidhaa anuwai zinazofaa kwa matumizi mbalimbali.

 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni ameyasema hayo katika maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Taka Sifuri, Viwanja vya Mnazi Mmoja, jijini Dar es Salaam, Machi 30,  2026.

 

Amesema Siku ya Kimataifa ya Taka Sifuri  huadhimishwa kila mwaka Machi 30 kwa lengo la kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa kupunguza matumizi ya bidhaa zinazopelekea kuzalisha taka, kutumia tena bidhaa kabla ya kugeuzwa taka na kuchakata taka kwa kurejeleza  ili kuepuka uchafuzi wa mazingira.

 

“Kauli mbiu ya kimataifa kwa mwaka huu inatoa hamasa ya "KUWEZESHA TAKA SIFURI KWENYE SEKTA YA CHAKULA" ikiwa na lengo la kuhimiza matumizi endelevu ya vyakula  na kupunguza taka zitokanazo na sekta hii. Kwa upande wa Tanzania, kauli mbiu ya Kitaifa inahimiza kutambua  "TAKA NI FURSA" ikisisitiza kuwa taka si uchafu bali ni malighafi yenye thamani, endapo itasimamiwa na kuchakatwa vyema.”

 

“Uzalishaji wa taka umekuwa changamoto kubwa kwa nchi za Ugaibuni na Africa, hususani katika miji mikubwa kama Dar es Salaam, Mwanza na Arusha na takwimu zinaonesha takribani kiasi cha tani zaidi ya millioni 7 za taka ngumu huzalishwa nchini kwa mwaka ambapo wastani wa asilimia 45 hadi 50 tu hukusanywa na kutupwa dampo.

 

Aidha, amesema asilimia 50 hadi 55 hubaki kwenye mazingira na kuzagaa kwenye mito na mifereji ya maji taka na mitaro ya maji ya mvua. Hata hivyo, matokeo ya Sensa ya Taifa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022 yanaonesha kuwa, asilimia 40 ya kaya zinachoma taka ngumu na asilimia 22 ya kaya zinatumia njia ya ukusanyaji sahihi wa mara kwa mara.

 

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Dkt. Immaculate Sware amesema ni wakati sasa wa kubadili mtazamo kuwa taka si uchafu tu bali ni rasilimali yenye thamani.

 

Amesema mabaki ya chakula yanaweza kuzalisha mbolea na nishati, plastiki inaweza kurejelezwa na kuwa bidhaa mpya, na chuma chakavu kinaweza kurejelezwa na kuzalisha bidhaa nyingine.

 

“Ninatoa wito kwa kila mmoja wetu kuanzia maeneo ya makazi, biashara na viwandani kuchukua hatua madhubuti za kupunguza uzalishaji wa taka, kuchambua taka katika vyanzo vyake na kuimarisha utamaduni wa kuchakata taka.”


Katika kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia, Wakala wa Vipimo (WMA) imetoa misaada ya vifaa vya ujenzi wa jiko la kisasa katika Kituo cha kulelea watoto wenye mahitaji maalumu Cha RAHMAN ORPHANAGE CENTER kilichopo Chang'ombe jijini Dodoma.

Akizungumza baada ya kutoa misaada hiyo Meneja wa WMA Mkoa wa Dodoma Said Ibrahimu amesema suala la mazingira safi ya kupikia ni haki ya kila mmoja ndio maana wameamua kama Wakala kutoa misaada hiyo itakayowezesha upishi wa kisasa katika mazingira safi na salama ikiwemo usalama wa chakula kwani kituo hicho wamekuwa wakipika kwa kutumia kuni na mazingira ya Nje ambayo sio salama kwa afya ya watoto hao.

"tunamuunga mkono Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha nishati safi ya kupikia inakuwa katika mazingira safi na salama ndio maana leo kwa niaba ya wafanyakazi wa WMA tumekabidhi Sementi, Marumaru na vifaa vingine vitakavyosaidia ujenzi wa jiko hilo, "amesema Meneja Said

Kadhalika, Mkurugenzi wa kituo hicho Bi. Rukia Abdallah ameishukuru WMA kwa misaada hiyo itakayokwenda kuboresha mazingira ya mapishi katika Kituo hicho chenye idadi ya watoto 120 huku akiomba wadau wengine kujitokeza kuchangia kituo hicho ikiwemo suala la usafiri ili watoto hao waweze kutembelea maeneo mbalimbali kwa ajili ya kujifunza zaidi.

Mmoja wa watoto wanaolelewa katika Kituo hicho Hazra Ramadhan ameipongeza Wakala wa Vipimo kwa kuona umuhimu wa kuwasaidia na kuwaomba kuendelea kuwakumbuka kila mara ili waweze kutimiza malengo yao.







NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

SEKTA binafsi imeelezwa kuwa nguzo muhimu katika kufanikisha malengo ya Mpango wa Nne wa Maendeleo (FYDP IV), huku Serikali ikisisitiza umuhimu wa kuongeza ushiriki wake katika uwekezaji wa nishati ili kufikia uzalishaji wa megawati 70,000 ifikapo mwaka 2050.

 


Na Joseph Mahumi, WF

Kampuni ya tathmini ya nchi kukopa na kulipa mikopo ya Fitch Ratings, imeithibitisha Tanzania kuendelea kuwa ‘B+’ huku likidumisha mtazamo wa “Stable Outlook”. Hatua hiyo inaashiria imani ya Kampuni hiyo katika mwenendo wa uchumi wa nchi pamoja na uthabiti wake wa kifedha katika kipindi cha kati.

Kwa mujibu wa tathmini hiyo, Tanzania inaendelea kunufaika na ukuaji mzuri wa pato la taifa (GDP) , kiwango cha chini cha mfumuko wa bei, deni kuendelea kuwa himilivu ikilinganishwa na nchi nyingine zinazofanana.

Mwenendo mzuri wa uchumi umepelekea upatikanaji wa fedha za nje kupitia programu za Shirika la Fedha la Kimataifa - IMF ikiwemo Extended Credit Facility (ECF) inayohusisha upatikanaji wa mkopo nafuu kwa ajili ya kuimarisha uchumi wa nchi kupitia sekta za uzalishaji na huduma za jamii na Resilience Sustainability Facility (RSF) ya kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi. 

Ripoti hiyo pia imeeleza kuwa ushindi wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika uchaguzi wa Oktoba 2025 unatarajiwa kuendeleza sera za kiuchumi, jambo litakalosaidia utekelezaji wa mipango ya mageuzi ya uchumi na kuendelea kuweka mazingira wezeshi kwa wawekezaji.

Kwa upande wa ukuaji wa uchumi, Fitch inatarajia Tanzania kuendelea kuwa na kasi ya ukuaji wa asilimia 6 mwaka 2026 na 2027, juu ya wastani wa nchi zilizo katika kundi la ‘B’ ambapo Ukuaji huo utachangiwa na sekta za kilimo na madini pamoja na uwekezaji mkubwa katika miundombinu, ikiwemo mradi wa reli ya kisasa ya Standard Gauge Railway na bomba la mafuta ghafi la Afrika Mashariki (EACOP).

Kwa upande wa sera za fedha za umma, Fitch inakadiria nakisi ya bajeti kubaki karibu asilimia 3 ya Pato la Taifa katika miaka ya fedha 2026 na 2027, huku ukusanyaji wa mapato ukiendelea kuimarika kutoka asilimia 14.2 ya Pato la Taifa mwaka wa fedha 2021 hadi asilimia 15.9 mwaka wa fedha 2025.

Ripoti hiyo inaonesha kuwa Mapato ya utalii (travel exports) yalifikia dola za Marekani bilioni 4.4 mwaka 2025, sawa na asilimia 25 ya mauzo yote ya bidhaa na huduma nje ya nchi. 

Hata hivyo, hali hii itafidiwa kwa kiasi na kuongezeka kwa thamani ya mauzo ya dhahabu ya Tanzania nje ya nchi, ambayo yalifikia dola za Marekani bilioni 4.7 mwaka 2025 (sawa na asilimia 27 ya jumla ya mauzo ya bidhaa na huduma nje ya nchi).

Aidha, deni la serikali linatarajiwa kushuka hadi asilimia 47 ya Pato la Taifa ifikapo mwaka 2027, likisaidiwa na ukuaji wa uchumi na nidhamu ya matumizi ya Serikali.

Tathmini hiyo pia imepongeza jitihada za Serikali katika kuboresha usimamizi wa fedha za umma, ikiwemo kupunguza madeni ya wazabuni na marejesho ya VAT katika miaka ya karibuni ambapo Kufikia Desemba 2025, kiasi kilichothibitishwa cha madeni hayo kilipungua hadi asilimia 0.2 ya Pato la Taifa (GDP), kutoka asilimia 1.2 mwishoni mwa Desemba 2022, hatua inayochangia kuongeza uwazi na ufanisi wa kifedha.

“Ninawapongeza Viongozi wa Wizara Taasisi zake zote waliofanikisha kazi ya kusimamia sekta hii ya uchumi na fedha, tunafarijika kuona matokeo haya ambayo ni muhimu kwa maendeleo ya nchi yetu kwani tutaendelea kuaminika katika masoko ya fedha na dhamana ya Kimataifa” alisema Dkt. Natu El-maamry Mwamba, Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha

Kwa ujumla, uthibitisho wa daraja la ‘B+’ na mtazamo thabiti unaashiria kuwa Tanzania inaendelea kujenga msingi imara wa uchumi, huku ikiongeza imani ya wawekezaji wa ndani na kimataifa katika uwezo wa nchi kusimamia uchumi wake na kukabiliana na mishtuko ya nje.