Na Mwandishi wetu

Katika dunia inayokabiliwa na changamoto kubwa za mabadiliko ya tabianchi, ongezeko la uchafuzi wa mazingira na kupungua kwa rasilimali asilia, hadithi ya Tanzania inajitokeza kama mfano wa matumaini, uthabiti na maamuzi ya kimkakati. Maadhimisho ya miaka 40 ya Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) si tukio la kawaida—ni kielelezo cha dhamira ya Taifa kulinda uhai wake huku likiendeleza uchumi wake.



‎Serikali kupitia Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) imeanza utekelezaji wa mradi wa Uboreshaji Miundombinu ya Miji Tanzania (TACTIC) unaolenga kukuza uchumi na kuboresha maisha ya wananchi katika Halmashauri ya Mji wa Korogwe mkoani Tanga.

‎Hayo yameelezwa na Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Korogwe, Bw.  Burhan Ngulungu ambapo amesema kuwa takribani shilingi Bilioni 19 kupitia mradi wa TACTIC zitatumika katika ujenzi wa barabara za lami Km 10.4 na mifereji ya maji ya mvua itakayosaidia kuondoa maji katikati ya mji na kupeleka eneo la mto Pangani.

‎"Kuna barabara itaunganisha stendi ya Kijazi na soko la Kilole, hivyo barabara ikikamilika licha ya kupendezesha mji, wananchi pia wataweza kupata huduma za usafiri na usafishaji, mazingira bora ya kufanyia biashara kwa wajasiriamali na wafanyabiashara na pia kuongeza mapato ya halmashauri ya mji wa Korogwe", amesema.

‎Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Korogwe mjini CPA. Charles Njama amesema mradi huo unaotarajiwa kujenga barabara katika kata za Bagamoyo, Mgombezi, Mtonga, Manundu, Masuguru na Magunga unakwenda kuleta tabasamu la kudumu kwa wananchi wa Korogwe.

‎"Tunamshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa mradi huu, barabara ya NMB-Magunga ni muhimu kwa wananchi wa Korogwe, Handeni, Lushoto na maeneo mengine kwasababu inapeleka wagonjwa hospitali ya Magunga, ikikamilika kwa kiwango cha lami itasaidia wagonjwa kufika hospitali bila usumbufu", amesema.

‎Naye, Mhandisi Charles Kamugisha Mratibu mradi wa TACTIC Korogwe Mji, ameeleza kuwa mradi unatarajiwa kukamilika tarehe 23 Januari, 2027 ambapo unahusisha ujenzi wa barabara ya NMB-Magunga Km 2.7, Bagamoyo-Mgombezi-Kibo Km 6.5, Kijazi Bus Stand-Kilole sokoni Km 1.2 pamoja na mifereji ya maji ya mvua Km 1.43 fedha za mkopo nafuu toka Benki ya Dunia. 

‎Vilevile, Mhandisi Zakayo Magoro Meneja wa TARURA wilaya ya Korogwe amesema kuwa TARURA ina mtandao wa barabara za lami Km 16.1 kupitia mradi wa TACTIC zitaongezeka hadi kufikia Km 26.5 ambapo zikikamilika zitapendezesha mji, thamani ya ardhi itapanda na itapunguza gharama za matengenezo ya mara kwa mara. 

‎Naye, Bw. Mohamed Dachi mkazi wa kata ya Mgombezi ambaye ni mkulima ameishukuru serikali kwa ujenzi wa barabara ya Bagamoyo hadi Kibo ambapo ikikamilika itaongeza fursa za kibiashara na kiuchumi kwani watasafirisha mazao yao sokoni kwa urahisi.

‎Bw. Salmin Sadala mkazi wa kata ya Manundu ambaye ni mfanyabiashara ndogondogo amesema kuwa baada ya kukamilika kwa mradi huo licha ya mji wa Korogwe kupendeza pia taa zikiwekwa watafanya biashara hadi usiku na kuchochea kukua kwa shughuli za kiuchumi kwa wananchi.

Kituo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Binafsi (PPP Centre) kimesema mafanikio ya utekelezaji wa ajenda ya ubia nchini yameongeza kwa kiasi kikubwa thamani ya miradi ya maendeleo, huku kikitoa wito wa kufanyiwa maboresho kwa Sheria ya Utumishi wa Umma ili kuongeza uwajibikaji na kulinda maslahi ya walipa kodi.

Naibu Waziri wa Nishati,Mhe. Salome Makamba ametembelea Ubalozi wa Tanzania nchini Misri, ambapo alipokelewa na Balozi wa Tanzania nchini humo, Richard Makanzo.

Katika mazungumzo yao, Balozi Makanzo alieleza majukumu mbalimbali yanayotekelezwa na ubalozi huo, pamoja na kuainisha fursa zilizopo katika sekta mbalimbali ikiwemo afya, kilimo, umeme, uchukuzi na biashara. 

Balozi Makanzo alieleza kuwa ushirikiano kati ya Serikali za Tanzania na Misri katika sekta hizo unalenga kuwanufaisha wananchi na kuimarisha mahusiano ya kidiplomasia kati ya nchi hizo mbili.

Mhe. Salome alimpongeza Balozi Makanzo kwa kazi nzuri anayoifanya pamoja na timu yake, hususan katika kuendeleza mahusiano si tu kati ya Tanzania na Misri, bali pia na balozi za nchi nyingine zilizopo nchini humo.

 Mhe. Salome yupo nchini Misri kwa ajili ya kushiriki mkutano wa East African Power Pool, utakaofanyika Aprili 29, 2026 jijini Cairo. 

Mkutano huo utajadili masuala muhimu ya sekta ya nishati miongoni mwa nchi wanachama, ikiwemo uunganishaji wa gridi za taifa na biashara ya umeme baina ya nchi hizo.

Mkutano huo umetanguliwa na vikao vya wataalamu kutoka sekta ya nishati katika nchi wanachama, vikilenga kuweka msingi wa majadiliano ya viongozi.










Wajumbe wa Bodi ya Chuo cha Maji (Water Institute) wakiongozwa na Mwenyekiti wa Bodi hiyo Dr. Maulid J. Maulid wamekutana Aprili 28, 2026 jijini Dar Es Salaam kwa kikao cha 46 cha Bodi hiyo kujadili masuala ya kimkakati yanayolenga kuimarisha utoaji wa huduma za kitaaluma na miradi ya maendeleo itakayoboresha ufundishaji na ujifunzaji.

 Na Farida Mangube Morogoro


Bodi ya Maji ya Bonde la Wami-Ruvu imewatoa hofu wakazi wa Manispaa ya Morogoro kuwa maji ya Bwawa la Mindu ni salama, kwani kemikali iliyomwagika haikufikia chanzo cha maji.

Wasiwasi huo ulizuka kufuatia ajali ya lori lililokuwa likisafirisha kemikali aina ya sulphur kuacha njia na kugonga miti mita 300 kutoka bwawa la Mindu mtaa wa mikoroshini Kata ya Mindu barabara kuu ya Morogoro–Iringa.

Mkurugenzi wa Bonde la Maji bonde la Wami-Ruvu, Mhandisi Elibariki Mmasi, amesema hatua za haraka zilizochukuliwa na wataalamu zilisaidia kuzuia kemikali hiyo kusambaa hadi kwenye chanzo cha maji.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Morogoro (MORUWASA), CPA Sais Kyejo, amesema uchunguzi wa awali umebaini kuwa hakuna madhara yaliyobainika katika ubora wa maji yanayosambazwa.

“Wananchi waendelee kutumia maji bila hofu,” amesema Kyejo.

Naye Meneja wa Kanda ya Kati wa Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali, Bi Magdalena Mtenga, amesema hadi sasa hakuna madhara yaliyoripotiwa kwa wananchi, licha ya kemikali hiyo kuwa hatarishi endapo itashughulikiwa bila tahadhari.

Ameeleza kuwa sulphur ina sifa ya kuwaka na hata kulipuka, pamoja na kusababisha muwasho wa ngozi au koo, lakini hali hiyo haikutokea wakati wa operesheni ya kuiondoa katika eneo la ajali.

Taasisi mbalimbali zikiwemo Bonde la Wami-Ruvu, MORUWASA, Baraza la Taifa la Usimamizi wa Mazingira (NEMC) pamoja na Jeshi la Zimamoto na Uokoaji zilishiriki kuondoa kemikali hiyo kwa usalama.

Meneja wa NEMC Kanda ya Morogoro na Rufiji, Arnold Mapinduzi, amesema kemikali hiyo itateketezwa kwa mujibu wa sheria ili kulinda mazingira.

Ajali hiyo ni ya tatu ndani ya mwezi mmoja kuhusisha usafirishaji wa kemikali aina ya sulphur Barabara kuu ya Morogoro - Iringa hali inayochochea haja ya kuimarisha usalama wa usafirishaji wa kemikali hatarishi.





 


Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi,Patrobas Katambi ameitaka Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kuzingatia mambo 10 vya msingi huku akisisitiza nidhamu, haki, weledi na uadilifu katika utekelezaji wa majukumu na wajibu wa wizara wa kulinda raia na mali zao.

Ametoa maagizo hayo makati akifungua Kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi ambacho kimefanyika leo,jijini Dodoma ambapo kilihudhuriwa na Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Ally Senga Gugu,Wakuu wa Idara na Vitengo wa wizara,Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza, CGP Jeremiah Katungu, Kamishna Jenerali wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, CGF John Masunga, Kamishna wa Fedha na Lojistiki wa Jeshi la Polisi, CP Liberatus Sabas, Kamishna wa Jeshi la Polisi Zanzibar, CP Kombo Khamis Kombo,Wawakilishi wa Idara ya Uhamiaji, Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa(NIDA) na wawakilishi wa watumishi wa wizara.

“Naomba tuzingatie yafuatayo; Moja, kusimamia na kuhakikisha mpango mkakati, mipango dira, dhima na majukumu ya wizara yanatekelezwa kwa ufanisi ili kufikia malengo ya Serikali ya Awamu ya Sita ya Dkt. Samia Suluhu Hassan, mbili, kuzingatia miongozo mbalimbali ya kisera ya Kitaifa, Kikanda na Kimataifa.

Tatu;kuhakikisha watumishi wote wanaostahili wanapandishwa vyeo kwa wakati.” amesema Waziri Katambi

Katika hotuba yake hiyo ya kufungua Baraza,Waziri Katambi ametaja agizo lingine la nne kuwa ni kulipa madai ya wastaafu, uhamisho, likizo, stahiki, madeni na madai mbalimbali ya watumishi kwa wakati ili kuipunguzia serikali malimbikizo ya madeni.

Tano ni kuhakikisha watumishi wa wizara wanatekeleza majukumu yao kwa kuzingatia sheria, haki, maadili na taratibu bila kutumia madaraka au mamlaka yao vibaya ili kuhakikisha kwamba   dhana ya uwajibikaji na utawala bora inaendelea kuzingatiwa na kuleta tabasamu ambalo  Rais wa nchi, Dkt.Samia Suluhu Hassan amekusudia.

Sita ni ufanisi na utendaji utakaosaidia uwajibikaji na nidhamu kazini, utekelezaji kwa wakati  na tathmini ambayo itapima malengo na kufuatilia kile ambacho tunakifanya na kupima malengo kama yamefikiwa kwa kuyafanyia tathmini na kufuatilia eneo gani linastahili marekebisho.

Saba ni kuzingatia maslahi na haki za watumishi ikiwemo pia kuwapa fursa ya mafunzo ili kuwaongezea ujuzi na weledi, huku akisisitiza haitakiwi kufanya kazi kwa kujuana, kuviziana wala kwa kutegena,ambapo aliwataka kufanya kazi kwa mujibu wa sheria na mahusiano yaliyo mema na tija kwa taifa.

Nane ni mafunzo huku akisisitiza wale wanaostahili kwenda mafunzo ikiwa ni programu fupi,warsha,ujuzi au weledi huku akikisitiza lizingatiwe kwa kuwa linaongeza ufanisi na kurahisisha majukumu 

Tisa ni kuzingatia usalama na maadili ya kazi na Kumi  ni kuimarisha mawasiliano ya ndani ya taasisi ili kuweza kurahisisha utendaji kazi katika kuwahudumia wananchi, ikiwemo mahusiano kati ya ofisi moja na nyingine, ikiwemo masuala ya kuandikiana barua pepe kati ya ofisi moja na nyingine akisisitiza kuwepo mazungumzo kwanza ya ana kwa ana ili kuweza kurahisisha maamuzi ambayo baadae wayaweke katika maandishi ambapo pia alisisitiza utunzaji wa siri.

Waziri Katambi alimalizia kwa kusisitiza uwepo utaratibu wa kufanya tathmini ya bajeti na rasilimali zilizopo ili kuleta matokeo chanya katika kuwahudumia wananchi ikiwemo ulinzi wa mali na maisha yao.

NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

SERIKALI ya Belarus imeendelea kutoa fursa za ufadhili wa masomo kwa wanafunzi wa Tanzania, hususan katika fani ya tiba kwa mwaka wa masomo 2026/2027, hatua inayotokana na kuimarika kwa ushirikiano kati ya nchi hizo mbili.

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Daniel Mushi, amesema upatikanaji wa mabasi ya watumishi yatasaidia sana katika kuweka mazingira salama na wezeshi ya utendaji.

Amesema hatua hiyo inaonesha dhamira ya dhati ya Serikali katika kujali watumishi na kuboresha mazingira ya kazi.

Amesisitiza kuwa watumishi ni nguzo kuu ya kufikia malengo kwani ndio watekekezaji wa mipango na maono wizara hivyo, Wizara inaendelea kuweka mazingira stahiki na jumuishi kwa watumishi wote.

"Rais wetu amesisitiza kazi iende sambamba na kujali utu, na hivi ndio tunatekeleza kauli mbiu ya Kazi na Utu tunasonga mbele kwa kuweka mazingira yanayovutia utendaji kwa watumishi" amesema Prof. Mushi.

Prof. Mushi amewahimiza watumishi kutumia mabasi hayo na kuyatunza ili yaweze kurahisisha utendaji kazi na kutumika kwa muda mrefu.

Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimaliwatu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Edith Rwiza amesema ununuzi wa mabasi matatu (3) mapya kwa ajili ya usafiri wa watumishi ni hatua muhimu ya kuboresha mazingira ya kazi kwa Wizara.

Akizungumza jijini Dodoma Aprili 28, 2026 katika uzinduzi wa mabasi ya watumishi, Mkurugenzi huyo amesema mabasi hayo yamenunuliwa na Wizara kwa kushirikiana na Mradi wa Kuimarisha na Kuboresha Elimu ya Awali na Msingi Tanzania Bara (BOOST) kwa zaidi ya Shilingi milioni 500 kwa lengo la kuwezesha watumishi katika safari za kila siku za kwenda kazini na kurudi nyumbani pamoja na ziara za kikazi.

"Kabla ya hatua hii, watumishi walilazimika kutumia kati ya shilingi 10,000 hadi 15,000 kwa siku kufika ofisini hali iliyoleta ugumu wa maisha na kupunguza morali ya kazi" amesema Dkt. Rwiza

Mkurugenzi Rwiza amesema upatikanaji wa mabasi haya ni sehemu ya jitihada za wizara kuhakikisha watumishi wanafanya kazi katika mazingira bora na yenye ufanisi.

Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikalin na Afya (TUGHE), Bw. Moshi Kisinga ameushukuru uongozi wa Wizara hiyo kwa kununua magari kwa ajili ya watumishi.

"Kwa niaba ya watumishi wenzangu tumepokea magari haya kwa furaha na hakika tumeondokana na changamoto kubwa ya usafiri", amesema Kisinga.

Ametoa rai kwa watumishi kufanya kazi kwa juhudi na maarifa akisisitiza uwajibikaji katika majukumu ya kila siku.



Dkt. Kiruswa aongoza ujumbe wa Tanzania katika kongamano la kikanda

Mbibo: Ushirikiano wa kimataifa ni chachu ya mafanikio Sekta ya Madini


📍 Addis Ababa, Ethiopia 

Serikali ya Tanzania imesisitiza umuhimu wa matumizi endelevu ya madini muhimu (critical minerals) kama nyenzo kuu ya kuchochea maendeleo ya viwanda na kukuza uchumi Barani Afrika.

Hayo yameelezwa na Naibu Waziri wa Madini, Dkt. Steven Kiruswa, Aprili 28, 2026, wakati wa kongamano la Kikanda lililofanyika Makao Makuu ya Tume ya Umoja wa Mataifa ya Uchumi Afrika (UNECA) jijini Addis Ababa.

Dkt. Kiruswa amesema Afrika ina nafasi ya kimkakati duniani kutokana na utajiri wa madini muhimu yanayotumika katika teknolojia za nishati safi, akitaja madini ya lithiamu, kobalti na nikeli kuwa nguzo muhimu katika uzalishaji wa betri za magari ya umeme na mifumo ya nishati jadidifu. Amesema hali hiyo inaifanya Afrika kuwa mhimili muhimu katika mabadiliko ya uchumi wa dunia kuelekea matumizi ya nishati safi.

Aidha, Dkt. Kiruswa ameongoza ujumbe wa Tanzania katika Kongamano hilo, ambapo ameeleza dhamira ya Serikali ya Tanzania ya kuhakikisha rasilimali za madini zinasimamiwa kwa manufaa ya wananchi kupitia Sera na Mikakati inayolenga uongezaji thamani wa madini ndani ya nchi, ajira na ukuaji jumuishi wa uchumi.

Awali, Aprili 27, 2026, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Msafiri Mbibo, alisema Afrika ina fursa kubwa ya kunufaika na ongezeko la mahitaji ya madini hayo duniani, lakini akasisitiza umuhimu wa kuhakikisha uwekezaji unaendana na misingi ya uendelevu na uwajibikaji.

Alibainisha changamoto zinazoikabili sekta ya madini kuwa ni pamoja na uchimbaji usio rasmi, uharibifu wa mazingira na ushirikishwaji mdogo wa jamii, akisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya serikali, sekta binafsi na wadau wa maendeleo ili kukabiliana nazo.

Pamoja na Mambo mengine, Mbibo aliongeza kuwa Tanzania itaendelea kuimarisha ushirikiano wa kikanda na kimataifa sambamba na kuhamasisha matumizi ya teknolojia za kisasa katika shughuli za uchimbaji ili kuongeza tija na kupunguza athari kwa mazingira.

Kongamano hilo limewakutanisha mawaziri, wataalamu na wadau wa sekta ya madini kutoka nchi mbalimbali za Afrika na nje ya bara hilo, likilenga kujadili namna bora ya kuhakikisha madini muhimu yanachangia kikamilifu maendeleo ya viwanda na ustawi wa jamii.

Miongoni mwa washiriki mashuhuri ni Hailemariam Desalegn na Habtamu Tegegne, ambao kwa pamoja wamesisitiza umuhimu wa ushirikiano wa kikanda ili Afrika inufaike ipasavyo na rasilimali zake za madini.



Na Oscar Assenga, Tanga

Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Dkt. Balozi Batilda Burian, amesema mkoa huo umeanza mkakati maalum wa kukuza na kutangaza utalii wa fukwe pamoja na fursa za uwekezaji zilizopo, ili kuongeza mchango wake katika uchumi wa Taifa.

Akizungumza leo, amesema ameita wadau mbalimbali kwa ajili ya kujadili na kuweka mikakati ya pamoja ya kuitangaza Tanga, akibainisha kuwa mkoa huo umejaliwa kuwa katika ukanda wa Bahari ya Hindi wenye maeneo mengi yenye fursa za kiuchumi na utalii.

Ametaja baadhi ya maeneo hayo kuwa ni pamoja na Kipumbwi (Pangani), Ushongo, Kwale (Mkinga) na maeneo ya Raskazone jijini Tanga, ambapo kuna mradi wa kuboresha fukwe unaofadhiliwa na Benki ya Dunia. 

Amesema mradi huo utakapokamilika utafungua fursa za michezo ya maji, matembezi ya boti, kuogelea pamoja na shughuli za kijamii kama harusi.

Aidha, amesema mkoa umeanza kushirikiana na Kampuni ya Makazi Solution pamoja na wadau wa Zanzibar ili kujifunza na kubadilishana uzoefu wa namna ya kuendeleza utalii wa fukwe.

 Timu ya wataalamu inatarajiwa kwenda Zanzibar kukutana na Wizara ya Utalii na wadau wengine ili kuimarisha ushirikiano huo.

“Tunajifunza kutoka Zanzibar, ambako maeneo kama Nungwi na Paje yalianza kidogo lakini sasa yamekua vituo vikubwa vya utalii. Sasa ni wakati wa Tanga kuchukua nafasi hiyo,” amesema.

Kwa upande wa uwekezaji, Dkt. Burian ameeleza kuwa mradi wa Kipumbwi Satellite City, unaotekelezwa kwa ushirikiano na Halmashauri ya Pangani na Makazi Solution, unalenga kutoa fursa kwa wananchi na wawekezaji kupata viwanja na kuendeleza eneo hilo.

Amesema eneo la Kipumbwi lina umuhimu mkubwa kimkakati, likiwa kilomita 3 kutoka bandari ya Kipumbwi, kilomita 80 kutoka Tanga, kilomita 60 kutoka Zanzibar kwa njia ya bahari, na kilomita 180 kutoka Dar es Salaam. Pia ujenzi wa barabara ya Tanga–Pangani–Saadani–Bagamoyo unatarajiwa kufungua zaidi ukanda huo wa pwani.

Mbali na fukwe, mkoa wa Tanga una vivutio vingi vya utalii ikiwemo Mapango ya Amboni, Hifadhi ya Taifa ya Saadani, Hifadhi ya Taifa ya Mkomazi, Milima ya Usambara (Lushoto), pamoja na urithi wa kihistoria kama makaburi ya vita ya kwanza ya dunia na Kisiwa cha Toten.

Ameongeza kuwa Tanga pia ni kitovu cha utamaduni wa Kiswahili, likiwa na historia ya muziki wa taarab, vyakula vya asili, pamoja na kuwa chimbuko la lugha ya Kiswahili, ambapo mwanazuoni mashuhuri Sheikh Shaban Robert alizaliwa katika eneo hilo.

Kwa sasa, amesema mkoa unapokea wageni kutoka ndani na nje ya nchi, hususan kutoka Kenya, Ujerumani, Uholanzi na Uswisi, wanaovutiwa na historia, mazingira asilia na utamaduni wa Tanga.

Dkt. Burian amesema jitihada hizo zinaunga mkono azma ya Rais Samia Suluhu Hassan ya kuitangaza Tanzania kupitia kampeni ya Royal Tour na kuongeza idadi ya watalii.

Kwa upande wa uchumi, amesema mkoa wa Tanga kwa sasa unachangia takribani shilingi trilioni 9.8 katika pato la taifa, na una mpango wa kuongeza mchango huo na kufikia nafasi ya pili kitaifa baada ya Dar es Salaam ifikapo mwaka 2028.

Amehitimisha kwa kusema kuwa Tanga ni eneo sahihi kwa uwekezaji na utalii, akiwakaribisha wawekezaji na watalii kutoka ndani na nje ya nchi kuja kutumia fursa zilizopo.




Na, Mwandishi Wetu, Muleba – Kagera

KAIMU Mganga Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Bw. Salum Kimbau amesema maandalizi ya Mpango wa Afya Moja kwa mkoa wa Kagera utaunufaisha mkoa huo kwa kuzingatia malengo yake ya kuboresha uratibu na utekelezaji wa Dhana ya Afya ya Moja na kuendelea kutatua changamoto zilizopo na zenye mwingiliano kati ya binadamu, wanyama na mazingira


Amezungumza hayo wakati akifungua kikao kazi cha wataalamu wa masuala ya Afya Moja kutoka sekta mbalimbali zikiwemo za afya, mifugo, mazingira, wanyamapori na kilimo ambao wamekutana katika Halmashauri ya Wilaya ya Muleba mkoani Kagera kwa siku tano kuanzia tarehe 27 Aprili hadi 01 Mei, 2026 ili kuandaa Mpango huo utakaotumika kubaini rasilimali zitakazosaidia kutatua changamoto na vihatarishi vya afya ya binadamu, wanyama na mazingira.





Bw. Kimbau amesema kuwa, mkoa utanufaika kwa uwepo wa Mpango huo kwani utaongeza tija katika kutatua changamoto zinazokabili sekta hizo hususan katika kuendelea kutatua changamoto za mwingiliano wa magonjwa kutoka kwa wanyama kwenda kwa binadamu na binadamu kwenda kwa wanyama.


“Tunashukuru kuufikia mkoa wetu wa Kagera, tunajua kuwa asilimia 75 ya magonjwa yanatokana na mwingiliano ulipo kati ya wanyama na binadamu, hivyo kuandaliwa kwa mpango kutasaidia utekelezaji wa Dhana ya Afya Moja kwa kushirikiana pamoja, hivyo utatusaidia kutatua changamoto zilizopo na kuwa na jamii salama,” alisema Bw. Kimbau



Aliongezea kuwa ufanisi wa mpango huu unategemea ushirikishwaji wa sekta zote zinazohusika ili kuleta matokeo chanya.


Naye Mratibu wa Maafa kutoka Idara ya Menejimenti ya Maafa sehemu ya Afya Moja kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Bi. Valentina Sanga amesema kuwa, Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kushirikiana na Shirika lisilo la Serikali la CIHEB Tanzania kupitia Mradi wa Usalama wa Afya Duniani imeratibu maandalizi ya uwepo wa mpango huo huku akisihi kuunganisha nguvu ya pamoja katika kuhakikisha utekelezaji wake unaleta matunda yanayotarajiwa.

Aidha, aliwasihi wataalamu wa Masuala ya Afya Moja kutumia fursa hiyo kuja na Mpango utakaoinufaisha Kagera, kwa kuzingatia ni miongoni mwa Mikoa inayokumbwa na majanga ya mlipuko mengine yakichangiwa na mwingiliano wa wanyama na binadamu.

“Dhana ya Afya Moja (One Health) inatoa fursa ya kutambua uhusiano wa karibu kati ya afya ya binadamu, wanyama, na mazingira. Inasisitizwa kuendelea kujifunza zaidi dhana hii ili kutatua changamoto zilizopo zikiwemo za milipuko ya magonjwa na kuweza kuyakabili endapo yanatokea katika maeneo yetu,” alisisitiza Bi. Valentina

Aliongezea kuwa, Mpango huo utasaidia kutatua changamoto za masuala ya kiafya zinazotokea katika Halmashauri za mkoa wa Kagera, kujiandaa na kukabili majanga hayo ili kuwa na jamii salama kwa maendeleo ya Taifa kwa ujumla.

Kwa upande wake Mwakilishi wa Shirika la CIHEB Tanzania, Bw. Mark Lwakatare alisema mradi wa Usalama wa Afya Duniani utaendelea kushirikiana na mikoa husika katika kuimairisha utekelezaji wa dhana ya Afya Moja ili nchi iweze kukabiliana na vihatarishi vya majanga mbalimbali.



“Mradi huu unashirikiana na Serikali kuboresha na kuimarisha utekelezaji wa afua mbalimbali kupitia dhana ya Afya Moja nchini, hivyo mradi utaendelea kushirikiana katika kujiandaa na kukabili athari katika afya ya binadamu, manyama na mazingira,” alisisitiza Lwakatare.


Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania (TCDC) kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa mkoa wa Njombe,Kamati ya Michezo ya Meimosi, Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) imeshiriki zoezi la upandaji miti lililofanyika  katika eneo la Ofisi ya Mkuu wa mkoa wa Njombe.

Katika zoezi hilo Mkuu wa mkoa wa Njombe Mhe. Anthony Mtaka awewahimiza Wafanyakazi na wananchi kuhakikisha kuwa wanapanda miti yenye kuleta faida hususan miti ya matunda ili kusaidia upatikanaji wa kipato cha mtu mmojammoja na Taifa kwa ujumla.

" Kumekuwa na tabia ya watu wengi kupanda miti kwaajili ya kivuli tu, pasipo faida yoyote, vi vizuri sasa tukapanda miti yenye kuleta faida kubwa kama vile miti ya matunda, amesema Mtaka.

Zoezi hilo lilihudhuriwa na Viongozi mbalimbali akiwemo Katibu Tawala wa mkoa wa Njombe, Rais wa Shirikisho la Wafanyakazi Tanzania (TUCTA), Mwenyekiti wa Kamati ya Meimosi na Watumishi wa Serikali kutoka Wizara na Taasisi mbalimbali.