Na Mwandishi wetu ..Arusha

Baada ya kupita miaka 42 tangu kufariki kwa aliyekuwa Waziri Mkuu wa zamani, Hayati Edward Moringe Sokoine, wananchi mkoani Arusha wameendelea kukumbuka na kuthamini mchango wake, wakisisitiza umuhimu wa uwajibikaji, mapambano dhidi ya rushwa na kilimo cha kufa na kupona.

Wakizungumza wakati wa maandalizi ya misa ya kumbukizi itakayofanyika Aprili 12 katika eneo la Monduli Juu, wananchi hao walisema Sokoine alijitofautisha kwa uongozi wa vitendo ulioweka mbele maslahi ya taifa.

Baadhi ya viongozi wa chama cha wazee wanaume Tanzania Joseph Laitatei makamu wa Rais wa chama hicho alisema Sokoine alikuwa kiongozi aliyesimamia haki bila kuyumba na hakuvumilia vitendo vya rushwa. Kwa upande wake, Cloud Gwangu alieleza kuwa kiongozi huyo alihamasisha kwa nguvu sera ya kilimo cha kufa na kupona, akilenga kujenga taifa linalojitegemea kwa uzalishaji.

Naye Abel Mollel Mwenyekiti  wa wilaya wa chama hicho alisisitiza kuwa uwajibikaji wa Sokoine unapaswa kuwa somo kwa viongozi wa sasa, huku Geoge Mwakalukwa akimtaja kama mfano wa uongozi wa uadilifu usio na hofu.

Aidha viongozi wa Chama cha Wazee Wanaume Tanzania wameipongeza familia ya Sokoine kwa kuendelea kuuenzi na kuudumisha kumbukumbu ya kiongozi huyo kila mwaka, wakieleza kuwa hatua hiyo inasaidia kizazi cha sasa na kijacho kujifunza misingi ya uongozi bora.

Katika kuenzi uzalendo wa Hayati Edward Moringe Sokoine, baadhi ya wananchi wameeleza namna walivyoguswa na uongozi wake wa kujitolea kwa taifa.

Akizungumza, Cloud Gwandu, mkazi wa Arusha, amesema Sokoine alikuwa kiongozi wa vitendo aliyethamini maslahi ya wananchi kuliko yake binafsi.

“Uzalendo wake ulikuwa wa kweli, alipambana na rushwa bila kuogopa na alihakikisha rasilimali za taifa zinawanufaisha wananchi wote. Viongozi wa sasa wanapaswa kujifunza kutoka kwake,” amesema Gwandu.

Ameongeza kuwa msisitizo wa Sokoine kwenye kilimo cha kufa na kupona ulikuwa sehemu ya uzalendo wake, kwani aliamini taifa lenye chakula cha kutosha lina uhuru wa kweli.

Kwa mujibu wa Gwandu, mfano wa Sokoine unaendelea kuwa somo muhimu kwa kizazi cha sasa katika kujenga uongozi wenye uwajibikaji na uadilifu.

Hayati Sokoine alifariki dunia Aprili 12 mwaka 1984 kufuatia ajali ya gari iliyotokea Dumila mkoani Morogoro.

Wananchi hao wameeleza kuwa licha ya kupita kwa muda mrefu, bado taifa lina kila sababu ya kuuenzi na kuutumia urithi wa Sokoine kama mwongozo wa kujenga uongozi bora, unaozingatia uwajibikaji, kupinga rushwa na kukuza kilimo kwa maendeleo endelevu.

















Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Dkt. Fabian Madele, akihutubia wadau mbalimbali wa Sekta ya Mifugo, wakati wa warsha ya utambulisho wa Mradi wa Jenga Kesho Iliyo Bora (BBT) ya Unenepeshaji wa Mbuzi na Kondoo, uliyofanyika katika Ukumbi wa Chuo cha Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) - Kongwa, Aprili 9, 2026 Dodoma.

Mtaalam wa Ufuatiliaji na Tathmini wa Mradi wa Jenga Kesho Iliyo Bora (BBT) ya Unenepeshaji wa Mbuzi na Kondoo, ambaye ni Mchumi Mwandamizi Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI), Bw. Tumsime Mutta (aliyesimama), akielezea Mpango Mkakati wa Mradi, wakati wa warsha ya utambulisho wa Mradi huo, uliyofanyika katika Ukumbi wa Chuo cha Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) - Kongwa, Aprili 9, 2026 Dodoma.

Mtaalam wa Ufuatiliaji na Tathmini wa Mradi wa Jenga Kesho Iliyo Bora (BBT) ya Unenepeshaji wa Mbuzi na Kondoo, ambaye ni Mchumi Mwandamizi Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI), Bw. Tumsime Mutta (aliyesimama), akielezea Mpango Mkakati wa Mradi, wakati wa warsha ya utambulisho wa Mradi huo, uliyofanyika katika Ukumbi wa Chuo cha Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) - Kongwa, Aprili 9, 2026 Dodoma.

Mchungaji wa kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Ndg. Jeremia Nyato (aliyesimama), akitoa Ushauri wa namna ya kuwashawishi vijana kukimbilia fursa za unenepeshaji Mifugo, wakati wa warsha ya utambulisho wa Mradi wa Jenga Kesho Iliyo Bora (BBT) ya Unenepeshaji wa Mbuzi na Kondoo, uliyofanyika katika Ukumbi wa Chuo cha Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) - Kongwa, Aprili 9, 2026 Dodoma.

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Dkt. Fabian Madele (katikati), akijibu hoja mbalimbali za wadau wa Sekta ya Mifugo, wakati wa warsha ya utambulisho wa Mradi wa Jenga Kesho Iliyo Bora (BBT) ya Unenepeshaji wa Mbuzi na Kondoo, uliyofanyika katika Ukumbi wa Chuo cha Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) - Kongwa, Aprili 9, 2026 Dodoma, kulia ni Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Kongwa ambaye ni Afisa Tarafa ya Kongwa, Bw. Jerimia.

Picha ni baadhi ya wadau wa Sekta ya Mifugo wakimsikiliza Mgeni Rasmi ambaye ni Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Dkt. Fabian Madele (hayupo pichani), wakati wa warsha ya utambulisho wa Mradi wa Jenga Kesho Iliyo Bora (BBT) ya Unenepeshaji wa Mbuzi na Kondoo, uliyofanyika katika Ukumbi wa Chuo cha Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) - Kongwa, Aprili 9, 2026 Dodoma.

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Dkt. Fabian Madele (aliyekaa katikati), akiwa kwenye picha ya pamoja na wadau wa Sekta ya Mifugo, wakati wa warsha ya utambulisho wa Mradi wa Jenga Kesho Iliyo Bora (BBT) ya Unenepeshaji wa Mbuzi na Kondoo, uliyofanyika katika Ukumbi wa Chuo cha Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) - Kongwa, Aprili 9, 2026 Dodoma.

....

Wizara ya Mifugo na Uvuvi inayotekeleza Mradi wa miaka mitano wa Jenga Kesho Iliyo Bora (BBT) ya Unenepeshaji wa Mbuzi na Kondoo katika eneo la Kituo cha Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI) iliyopo Wilayani Kongwa, imepanga kuwawezesha vijana 200 wa Kitanzania kupata Mafunzo hayo ikiwa na lengo la kuongeza ushiriki wa vijana na wanawake katika ujasiliamali wa Biashara ya Mifugo.

Akizungumza leo Aprili 9, 2026 Wilayani Kongwa Jijini Dodoma kwa Niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, wakati wa warsha ya utambulisho wa Mradi huo, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Dkt. Fabian Madele, amesema mradi huo wenye thamani ya takribani shilingi Billioni 81, unalenga kuwawezesha vijana kupitia shughuli za unenepeshaji wa mbuzi na kondoo kibiashara, uzalishaji wa malisho na mbegu za malisho, uchakataji wa vyakula vya mifugo, pamoja na matumizi ya teknolojia za kisasa.

"Walengwa wakuu wa mradi huu ni vijana, ambao kupitia utekelezaji wake watapata ujuzi na uzoefu wa vitendo katika mnyororo mzima wa thamani wa mazao ya mifugo, hususan mbuzi, na kupitia mafunzo haya, vijana wetu watajengewa uwezo wa kuingia kwenye biashara za kisasa za mifugo na hivyo kujiongezea kipato pamoja na kuchangia ukuaji wa uchumi wa taifa." Amesema Dkt. Madele

Aidha, Dkt. Madele amesema baada ya vijana kupata ujuzi huo, matarajio ya Serikali ni kuwa vijana wataweza kujiajiri wenyewe, kuanzisha biashara zao, na kuwa sehemu ya suluhisho la changamoto ya ajira nchini, ambapo vijana watakaonufaika watakuwa na fursa ya kupatiwa mikopo isiyo na dhamana kwa ajili ya kuendeleza biashara zao baada ya mafunzo.

Vilevile, Dkt. Madele amebainisha kuwa matokeo ya kuwepo kwa Mradi huo ni kutokana na uongozi madhubuti wa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi mahiri wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kutambua kwa kina changamoto ya ukosefu wa ajira miongoni mwa vijana, ndiyo maana Mheshimiwa Rais amechukua juhudi za makusudi kuhakikisha fedha hizo zinapatikana kwa ajili ya kuboresha maisha ya vijana kupitia miradi yenye tija kama huo wa BBT.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Ufuatiliaji na Tathmini Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Ndg. Daudi Mayeji, amesema Mradi huo hautaishia kwa vijana waliopo Dodoma tu bali kwa vijana kutoka maeneo mbalimbali ya nchi, ambapo Mpango huo utamuwezesha kijana kuhudumia Mbuzi 100 kwa pamoja.

Pia, Ndg. Mayeji amesema Mradi huo unategemea ndani ya miaka mitano kutoa Mafunzo kwa vijana takriban 1750 na Serikali tayari imeshatenga eneo la hekta 2000 kwa ajili ya kupanda Malisho ya Mifugo.

Naye, Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Kongwa, ambaye ni Afisa Tarafa ya Kongwa, Ndg. Jeremiah Kabebwa ameishukuru Wizara kwa kuwaletea Mradi wenye fursa kwa vijana ambapo ameihakikishia Wizara kuwa Ofisi ya Mkuu wa Wilaya itahakikisha vijana wote wanaichangamkia fursa hiyo ili kuweza kujikwamua kiuchumi.

 


Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi amekutana na kufanya mazungumzo na Kampuni ya Equinor Tanzania AS pamoja na Shell Exploration and Production Tanzania Ltd kuhusu utekelezaji wa uchimbaji wa gesi ya LNG katika mikoa ya kusini, leo tarehe 10 Aprili 2026, jijini Dar es Salaam.

Katika kikao hicho, Waziri alikutana na viongozi wa makampuni hayo, akiwemo Menno Bax, Mkurugenzi Mtendaji na Mwenyekiti wa Shell Exploration and Production Tanzania Ltd, pamoja na Hilde Merete Nafstad, Makamu wa Rais na Meneja wa Nchi wa Utafutaji na Uzalishaji wa Kimataifa (EPI) wa Equinor Tanzania AS.

Mazungumzo hayo pia yaliwashirikisha Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi, Dkt. James Mataragio, na Kamishna wa Mafuta na Gesi kutoka Wizara ya Nishati, Goodluck Shirima.

Makampuni haya yanajihusisha na utafiti, uchimbaji na uendelezaji wa gesi asilia baharini, pamoja na kushiriki katika maandalizi na utekelezaji wa mradi wa gesi iliyoyeyushwa (LNG) nchini Tanzania.














 RAIS SAMIA AAGIZA VIJANA WANUFAIKE NA FURSA ZA UCHUMI WA KIDIJITALI

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ameiagiza Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais – Maendeleo ya Vijana kuhakikisha vijana wananufaika kikamilifu na fursa zitokanazo na ukuaji wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA).

Akizungumza leo Ijumaa Aprili 10, 2026 katika ukumbi wa Jakaya Kikwete Convention Centre jijini Dodoma, mara baada ya kuzindua minara 758 ya mawasiliano pamoja na maunganisho ya mkongo wa taifa katika wilaya 85, Rais Samia amesema hatua hiyo ni muhimu katika kukuza ajira na ubunifu kwa vijana.

Amesema serikali inapaswa kuhakikisha miundombinu ya mawasiliano iliyopo inatumika ipasavyo kuwawezesha vijana kuongeza ujuzi wa kidijitali na kushiriki katika shughuli za kiuchumi.

“Ni muhimu kuhakikisha vijana wetu wanapata fursa za kunufaika na uchumi wa kidijitali kupitia ubunifu, ajira na matumizi sahihi ya teknolojia,” alisema.

Rais Samia pia amesisitiza umuhimu wa kuwezesha kampuni changa (start-up) zinazomilikiwa na vijana kwa kuwapatia mitaji ili ziweze kukua na kuongeza ushindani katika soko la ajira na biashara.

Aidha, amewataka wadau wa sekta binafsi kushirikiana na serikali katika kukuza ubunifu na uwekezaji katika TEHAMA, akieleza kuwa vijana ndio chachu ya maendeleo ya uchumi wa kisasa unaotegemea maarifa na teknolojia.

Katika hatua nyingine, Rais Samia ameelekeza kulindwa kwa miundombinu ya mkongo wa taifa wa mawasiliano ili kuhakikisha inaendelea kutoa manufaa yaliyokusudiwa kwa taifa.

Amesisitiza kuwa, utekelezaji wa maagizo hayo utasaidia kuhakikisha hakuna kijana anayebaki nyuma katika safari ya kuelekea uchumi wa kidijitali na jumuishi nchini.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani (FCC) Bi. Khadija Ngasongwa amewataka watumishi wa FCC kufanya kazi kwa ushirikiano, bidii, upendo pamoja na ubunifu katika utendaji ili kuboresha utoaji huduma kwa wananchi.

 Mbunge wa Bunda Mjini, Ester Bulaya, ameishauri Serikali kuweka historia mpya kwa kutunga sheria maalum itakayolinda miundombinu ya nchi, akisisitiza umuhimu wa kuhakikisha uwekezaji mkubwa unaofanywa katika miradi ya maendeleo unadumu kwa muda mrefu na kuwa na tija kwa vizazi vya sasa na vijavyo.

Akichangia mjadala wa makadirio ya mapato na matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa mwaka wa fedha 2026/2027 bungeni mjini Dodoma, Bulaya amemuomba Waziri Mkuu  Dkt Mwigulu Nchemba, kuchukua hatua madhubuti kwa kuanzisha mfumo wa kisheria utakaolinda barabara, madaraja pamoja na miradi mingine mikubwa ya kimkakati.

Bulaya alisisitiza kuwa ni wakati sasa kwa Taifa kuweka utamaduni wa kutenga fedha mahsusi kwa ajili ya matengenezo na ulinzi wa miundombinu, badala ya kusubiri miradi iharibike ndipo hatua zichukuliwe. Alibainisha kuwa mara nyingi Serikali imekuwa ikitumia fedha nyingi kujenga miradi mipya, lakini juhudi za kuitunza na kuilinda zimekuwa hazipewi uzito unaostahili.

“Lazima kama Taifa, kwenye dira yetu ya maendeleo, tuanze kuwa na utamaduni wa kuweka fedha za kulinda miradi ya nchi hii. Hii itasaidia kuhakikisha uwekezaji unaofanywa unadumu na kuwanufaisha wananchi kwa muda mrefu,” alisema Bulaya.

Aidha, mbunge huyo alieleza kuwa kasi ya maendeleo inayoshuhudiwa nchini chini ya uongozi wa Rais, Samia Suluhu Hassan, inapaswa kuambatana na mikakati thabiti ya kuhakikisha ubora wa miradi hiyo unadumishwa. Alionya kuwa bila kuwepo kwa mfumo madhubuti wa ulinzi na matengenezo, baadhi ya miradi inaweza kupoteza thamani yake mapema na hivyo kuisababishia nchi hasara.

Bulaya alisisitiza pia dhana ya “kupanga ni kuchagua”, akihimiza Serikali kuweka vipaumbele vinavyolenga kulinda uwekezaji mkubwa unaofanywa katika sekta ya miundombinu. Kwa mujibu wake, ni bora kutumia rasilimali kidogo kulinda kilichopo kuliko kutumia fedha nyingi kujenga upya miradi iliyoharibika.

Katika hatua nyingine, alionya kuwa iwapo hoja hiyo haitapatiwa majibu ya kuridhisha na Serikali, yuko tayari kuchukua hatua zaidi za kibunge ili kuhakikisha suala la ulinzi wa miundombinu linapewa uzito unaostahili.


 Na Munir Shemweta, WANMM NAIROBI



Serikali ya Tanzania imesisitiza umuhimu wa kuunganisha maendeleo ya kikanda, mipango miji pamoja na miundombinu kama nyenzo muhimu ya kuchochea ukuaji wa uchumi na ujumuishaji wa kikanda Barani Africa.

Akizungumza katika mjadala wa kitaalamu uliofanyika sambamba na Kongamano la Pili la Miji Afrca (2nd Africa Urban Forum) jijini Nairobi, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo ameeleza kuwa, kanda za maendeleo zina mchango mkubwa katika kurahisisha biashara, usafirishaji na kuunganisha nchi zisizo na bandari na masoko ya kimataifa.

‘’Tanzania imekuwa mstari wa mbele katika kuendeleza kanda mbalimbali tangu miaka ya 1970 ambazo zimechangia kwa kiasi kikubwa kukuza uchumi wa nchi na ukanda wa Afrika Mashariki na Kati’’. amesema

Kwa mujibu wa Dkt Akwilapo, Kanda ya Kati imeendelea kuwa mhimili muhimu wa usafirishaji, ikiunganisha Bandari ya Dar es Salaam na nchi za Rwanda, Burundi, Uganda na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo kupitia reli, barabara na njia za majini.

Ameongeza kuwa, ongezeko la kasi la ukuaji wa miji limeongeza mahitaji ya miundombinu na huduma, huku mahitaji ya usafiri yakiongezeka mara nne ndani ya kipindi cha miaka 20 iliyopita. ‘’Hali hii imeifanya serikali kuongeza uwekezaji katika sekta ya miundombinu na mipango miji ili kukidhi mahitaji hayo’’. ameeleza

Aidha, amesema uwepo Bandari ya Dar es Salaam, Reli za TRC pamoja na ile ya TAZARA umeendelea kuwa kichocheo kikubwa cha biashara ya kikanda, huku usafiri wa majini katika Maziwa Makuu ukichangia kuimarisha uhusiano wa kiuchumi kati ya nchi jirani.

Katika hatua nyingine, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo ameeleza kuwa, Serikali ya Tanzania inaendelea kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayolenga kuboresha miundombinu na makazi, sambamba na kuhimiza ushiriki wa sekta binafsi kupitia ubia na serikali.

Akihitimisha taarifa yake katika mjadala wa kitaaluma, Dkt Akwilapo amezitaka nchi za Africa kuimarisha ushirikiano wa kikanda, mipango miji na miundombinu, akieleza kuwa, hatua hiyo itasaidia kukuza biashara, kuvutia uwekezaji, kuboresha maisha ya wananchi na kupunguza pengo la maendeleo kati ya mijini na vijijini.

Kongamano la pili la Miji Africa limebeba kauli mbiu isemayo “Adequate Housing for All: Advancing Socio-Economic and Environmental Transformation Towards the Realization of Agenda 2063,” ambapo kupitia kongamano hilo kumekuwa na mijadala inayohusisha Mawaziri, Mameya na Wataalamu mbalimbali, lengo likiwa kuimarisha ushirikiano wa kikanda na kimataifa katika sekta ya maendeleo ya miji.



Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akizungumza katika Mjadala wa Kitaalamu unaofanyika sambamba na Kongamano la Pili la Miji Africa (2nd Africa Urban Forum) jijini Nairobi, Kenya.


Sehemu ya washiriki katika Mjadala wa Kitaalamu uliofanyika sambamba na Kongamano la Pili la Miji Africa (2nd Africa Urban Forum) jijini Nairobi, Kenya ambapo Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo alishiriki. ( PICHA ZOTE NA WIZARA YA ARDHI).

 


Waziri wa Maji, Mhe. Jumaa Aweso (Mb), amewataka watumishi wa Sekta ya Maji nchini kuongeza bidii, weledi na uwajibikaji ili kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi. Amesisitiza kuwa upatikanaji wa maji safi na salama ni nguzo muhimu ya maendeleo ya jamii na uchumi kukua hivyo kila mtumishi anapaswa kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi na kujituma.

Akizungumza na Menejimenti ya Wizara ya Maji na RUWASA katika ukumbi wa Wizara ya Maji Mtumba, jijini Dodoma, Mhe. Aweso amebainisha kuwa mafanikio yanategemea mshikamano na ushirikiano wa dhati miongoni mwa watumishi. Amesisitiza  kuwa viongozi wanapaswa kuwa mfano bora kwa kuzingatia maadili ya kazi, uwazi na uwajibikaji, sambamba na kuimarisha mawasiliano katika  taasisi.

 Waziri Aweso amepongeza  menejimenti kwa kazi nzuri na ushirikiano katika suala la   ukaguzi wa kazi za Sekta ya Maji na kueleza , ni  mafanikio hayo yanaonyesha matumizi sahihi ya rasilimali za umma pamoja na usimamizi imara wa miradi ya maendeleo. Amewataka watumishi kuendeleza viwango hivyo na kujipambanua zaidi katika utendaji wao.

Amehimiza matumizi ya ubunifu pamoja na utekelezaji wa mkakati madhubuti wa kukabiliana na changamoto zilizopo, kukamilisha miradi kwa wakati na kuhakikisha huduma ya maji inawafikia wananchi wote. Amesema  kuwa Serikali itaendelea kuweka mazingira wezeshi ili kuongeza ufanisi katika sekta.

Katika hatua nyingine, ameipongeza  RUWASA kwa juhudi kubwa za kushughulikia changamoto za wananchi kwa wakati, hatua inayochangia kuimarisha imani ya wananchi na kuboresha huduma ya maji  vijijini.

 Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji,  Mhandisi Mwajuma Waziri, amewataka watumishi kuendelea kufanya kazi kwa bidii, kushirikiana kwa karibu na kuweka mbele maslahi ya wananchi ili kuhakikisha huduma ya maji inaboreshwa na kuwa endelevu kwa manufaa ya sasa   na kizazi  kijacho.

 

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akiongea na Waandishi wa Habari kuhusu Miradi ya Maendeleo na Fursa za Vijana kwa Mwaka 2025/26, Jijini Dodoma.



Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) imeendelea kuongoza katika utoaji wa huduma za matibabu ya moyo katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kusini mwa Jangwa la Sahara, kwa kufanya zaidi ya upasuaji 3,000 wa tundu dogo kila mwaka.

Mkurugenzi Mtendaji wa taasisi hiyo, Dkt. Peter Kisenge, amesema mafanikio hayo yametokana na uwekezaji mkubwa wa Serikali katika sekta ya afya, pamoja na kuimarika kwa rasilimali watu, vifaa tiba na miundombinu ya kisasa.

Akizungumza na waandishi wa habari Aprili 9, 2026 jijini Dodoma, amesema Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) iliyoanzishwa mwaka 2015 kwa ajili ya huduma za kibingwa bobezi, tafiti na mafunzo, imefanikiwa kupunguza utegemezi wa wagonjwa kwenda nje ya nchi kwa matibabu ya moyo.

Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO), magonjwa ya moyo yanaongoza kwa kusababisha vifo duniani, yakigharimu maisha ya watu milioni 17.9 kila mwaka, huku asilimia 75 ya vifo hivyo vikitokea katika nchi zenye kipato cha chini na cha kati.

Dkt. Kisenge amesema Tanzania ni miongoni mwa nchi chache barani Afrika zilizoanzisha hospitali maalum za moyo kutokana na uwekezaji mkubwa unaohitajika.

Ameongeza kuwa JKCI hufanya zaidi ya upasuaji 3,000 wa tundu dogo kila mwaka pamoja na zaidi ya upasuaji mkubwa 800 wa kufungua kifua. Pia hutoa huduma za upasuaji tata kama TAVI, pamoja na upasuaji maalum kwa watoto ikiwemo Ozaki na Truncus.

Mafanikio hayo yameifanya Tanzania kuwa kitovu cha utalii wa matibabu, huku wagonjwa kutoka ndani na nje ya Afrika wakija kupata huduma katika taasisi hiyo.

Katika kusogeza huduma karibu na wananchi, JKCI imeanzisha matawi sita katika maeneo ya Tazara (Temeke), Kawe, Oysterbay, Kariakoo, Chato na Arusha. Hali hii imeongeza idadi ya wagonjwa kutoka wastani wa 400 kwa siku mwaka 2022 hadi zaidi ya 1,100 mwaka 2025.

Aidha, taasisi hiyo imepanua huduma za upasuaji kwa watoto kupitia ufadhili wa Serikali na wadau, ambapo mamia ya watoto wamefanyiwa upasuaji bila malipo.

Kwa upande wa teknolojia, JKCI inatumia mifumo ya kisasa ikiwemo DOZEE kwa ufuatiliaji wa wagonjwa pamoja na mfumo wa miadi kwa njia ya mtandao uliopunguza msongamano na muda wa kusubiri huduma.

Taasisi hiyo pia imeanza maandalizi ya kuanzisha huduma za upandikizaji wa moyo, zikitarajiwa kuanza ifikapo mwaka 2030.

Zaidi, Serikali imewekeza katika maabara ya kisasa inayotumia teknolojia ya akili mnemba na roboti, hatua iliyopunguza muda wa majibu ya vipimo kutoka saa tatu hadi saa moja.

JKCI pia imeingia makubaliano ya ushirikiano na nchi mbalimbali za Afrika katika kuboresha huduma na kujenga uwezo wa wataalamu wa afya. Aidha, imeanzisha mkutano wa kimataifa wa magonjwa ya moyo (CardioTan) unaowakutanisha wataalamu kutoka zaidi ya nchi 40 duniani.

Kupitia huduma za tiba mkoba, taasisi hiyo imewafikia wananchi zaidi ya 35,000 katika mikoa mbalimbali nchini.

Katika mwaka 2025 pekee, JKCI ilitoa huduma kwa wagonjwa 252,915 huku wagonjwa 2,710 wakifanyiwa upasuaji, wakiwemo 836 waliopata upasuaji mkubwa wa moyo.

Mbunge wa Jimbo la Kisarawe, Dkt. Selemani Jafo,akichangia makadirio ya mapato na matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zake kwa mwaka wa fedha 2026/27  leo Aprili 9,2026 bungeni jijini Dodoma.

Na.Alex Sonna-DODOMA

Mbunge wa Kisarawe, Dkt. Selemani Jafo, amedhamiria kuwasilisha hoja binafsi bungeni itakayolenga kuishauri Serikali kuanzisha mpango maalum wa mikataba ya ajira za muda mfupi kwa vijana ili kupunguza changamoto ya ukosefu wa ajira nchini.

Akichangia makadirio ya mapato na matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zake kwa mwaka wa fedha 2026/27 bungeni, Jafo alisema mpango huo unaweza kuwa na mfumo wa Ajira za muda (part time employment) utakaodumu kwa kipindi cha miaka mitatu mitatu hadi ifikapo mwaka 2050  ambapo vijana watapata ajira za mikataba na kujipatia uzoefu wa kazi.

Alimpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, kwa juhudi kubwa za kuongeza fursa za ajira kwa vijana tangu aingie madarakani, akisema serikali imefanya kazi kubwa katika kuwawezesha wananchi, lakini bado kuna haja ya kuja na mikakati mipya ya kukabiliana na wimbi la vijana wasio na ajira.

Jafo alibainisha kuwa changamoto ya ajira bado ni kubwa, huku akitoa mfano wa vijana wengi waliopo kwenye shughuli zisizo rasmi kama bodaboda, baadhi yao wakiwa na elimu ya juu ikiwemo stashahada,  shahada na kuendelea. Alipendekeza mpango maalum utakaolenga wahitimu hao ili kuwapa nafasi ya kupata ajira za muda na mikataba ya miaka mitatu.

Kwa mujibu wa mapendekezo yake, kila mwaka vijana 50,000 wanaweza kuingizwa kwenye mpango huo, ambapo asilimia 20 wawe wahitimu wa stashahada na asilimia 80 wawe wahitimu wa shahada na kuendelea. Aidha, alipendekeza malipo ya kujikimu ya Shilingi 500,000 kwa wenye stashahada na Shilingi 700,000 kwa wahitimu wa shahada.

Alisema gharama ya utekelezaji wa mpango huo inakadiriwa kufikia Shilingi bilioni 396, huku akisisitiza kuwa mpango huo utasaidia kukuza ujuzi wa vijana, kuongeza uzoefu wa kazi na kupunguza tatizo la ajira nchini.

Pia alipendekeza asilimia 10 zitoke katika mapato ya ndani ya kila Halmashauri, 10 ya gawio la Serikali kutoka kwenye mashirika ya umma, na fedha zingine zitokane na kubana maeneo mengine ya matumizi ya kawaida ya serikali(Recurrent Expenditure) ili zitumike kufadhili mpango huo. Aidha, alishauri mpango huo usimamie kupitia serikali za mitaa na Taasisi za Umma ili kurahisisha upatikanaji wa ajira katika halmashauri mbalimbali na Taasisi hizo za Umma.

Jafo alisisitiza kuwa mpango huo, kama utapitishwa, utaisaidia Serikali kuongeza wigo wa ajira na kuwawezesha vijana wengi zaidi kunufaika na fursa za kiuchumi nchini.

 



Na  OWM-SBUU -Morogoro


Serikali imezindua Kikosi Kazi cha Taifa cha Ufuatiliaji, Tathmini na Utoaji Taarifa (ME&R National Task Force) kwa lengo kuratibu utekelezaji wa Mwongozo Jumuishi wa Ufuatiliaji na Tathmini katika kusimamia utendaji wa shughuli za Serikali.

Kauli hiyo imetolewa leo tarehe 09 Aprili, 2026 na Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Dkt. James Kilabuko  wakati akifungua Kikao Kazi Cha Kikosi Kazi cha Taifa cha Ufuatiliaji, Tathmini na Utoaji Taarifa (ME&R National Task Force) kilichofanyika mkoani Morogoro.

Dkt. Kilabuko amesema, Ufuatiliaji na Tathmini ni dhana muhimu ya usimamizi inayotumika kwa lengo la kuhakikisha uwajibikaji na uwazi katika utekelezaji wa afua za maendeleo.

“Kikosi Kazi hiki kitakuwa chombo cha kitaalamu cha kusaidia kuratibu utekelezaji wa Mwongozo Jumuishi wa U&Tc, kuoanisha mifumo ya kitaifa ya utendaji, kuimarisha ubora wa takwimu na taarifa za Serikali na  kuandaa mapendekezo ya sera na maboresho ya kiutendaji” alisema Naibu Katibu Mkuu huyo.

 


Na Oscar Assenga, TANGA

Chama cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Tanga kimetoa maelekezo kwa Halmashauri ya Jiji la Tanga kuhakikisha maeneo ya kukusanyia taka katika soko la Mgandini yanaboreshwa kwa kujazwa kifusi ikiwemo kurekebisha barabara za ndani ili kuimarisha usafi.

Agizo hilo lilitolewa na Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Tanga Rajab Abdurhaman wakati wa ziara yake ambapo alisisitiza umuhimu wa kuhakikisha maji ya mvua yanaelekezwa ipasavyo kwenye mifereji ili kuepusha mafuriko na uharibifu wa miundombinu.

Ziara hiyo ilikuwa ni kufuatilia utekelezaji wa maagizo aliyoyatoa awali kuhusu kuboresha usafi wa soko hilo ambapo viongozi wa Jiji hilo walianza kuyafanyia kazi ikiwemo kuondosha uchafuzi uliokuwepo awali.

Awali, wakati wa ziara yake ya kukagua hali ya usafi, Mwenyekiti huyo hakuridhishwa na mazingira ya soko hilo na kutoa muda wa mwezi mmoja kwa uongozi wa Jiji kuhakikisha hali ya usafi inaboreshwa.

Akizungumza baada ya kufanya ziara ya ufuatiliaji, Rajab aliwapongeza Mstahiki Meya pamoja na viongozi wa Jiji kwa kuchukua hatua na kuanza kutekeleza maelekezo hayo ya CCM.

“Hatuhitaji viongozi wa kulalamika, tunahitaji viongozi wanaochukua hatua kutatua changamoto za wananchi. Mlichokifanya ni kutimiza wajibu wenu,” alisema.

Alisema kuwa hali ya uchafu iliyokuwepo awali haikuwafurahisha viongozi wala wafanyabiashara, hivyo hatua zilizochukuliwa zinaonesha uwajibikaji wa uongozi.

Hata hivyo Mwenyekiti Rajab alisisitiza kuwa atarejea kukagua maendeleo hayo baada ya wiki mbili na kuonya kuwa hataki kusikia visingizio badala ya utekelezaji.

“Ndani ya mwezi mmoja kuanzia Aprili 9 hadi Mei 9, tunatarajia kuona kazi imeanza. Hatutaki hadithi, tunataka vitendo,” alisisitiza.

Aidha, alieleza kuwa Jiji la Tanga ni taswira ya mkoa huo, hivyo linapaswa kuwa safi na lenye mpangilio mzuri.

Alikumbusha kuwa zamani Tanga ilikuwa mji unaojulikana kwa usafi na ustaarabu, hivyo ipo haja ya kurejesha hali hiyo.

Kuhusu huduma za vyoo katika soko hilo, Mwenyekiti alieleza kutoridhishwa na hali iliyopo, akibainisha kuwa choo kilichopo hakitoshelezi mahitaji kutokana na idadi kubwa ya watumiaji.

Alisema kuwa hali hiyo inasababisha baadhi ya watu kulazimika kujisaidia katika maeneo yasiyofaa, jambo linalohatarisha afya za wananchi na wafanyabiashara.

Alisisitiza umuhimu wa Jiji kutafuta suluhisho la kudumu, ikiwemo kuboresha mfumo wa maji taka ili kuendana na ongezeko la watumiaji.

Hata hivyo, aliwapongeza viongozi kwa kuanza mpango wa kujenga choo kipya chenye matundu 12 kitakachosaidia kupunguza changamoto hiyo, hasa katika kipindi hiki ambacho soko linatarajiwa kujengwa upya.

Pia alizungumzia changamoto ya msongamano wa magari yanayoleta bidhaa sokoni hapo, akielekeza kuwepo kwa utaratibu maalum wa magari kuingia na kushusha mizigo kwa mpangilio ili kupunguza msongamano na kuboresha usafi.


Alipendekeza magari yapaki katika maeneo maalum yaliyo nje ya soko, kisha yaingie kwa zamu kushusha bidhaa.

Katika hatua nyengine alisisitiza umuhimu wa kujenga mifereji ya maji ili kuzuia maji ya mvua kutuama au kuingia sokoni, hali inayochangia uchafu na uharibifu wa mazingira.


Alimalizia kwa kuwataka viongozi wa Jiji kuwa karibu na wananchi na kushughulikia changamoto zao kwa vitendo, akibainisha kuwa wananchi hao ndio chanzo cha mapato ya Jiji kupitia kodi.

Kwa upande wake, Naibu Meya Khalid Rashid alisema kuwa Jiji lina mpango wa kuboresha miundombinu ya ndani ya soko, ikiwemo njia za kupita ili kuondoa changamoto ya matope wakati wa mvua. Alibainisha kuwa kazi hiyo inatarajiwa kuanza ndani ya wiki moja.

Mwisho.