Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo, Mhe. Deodatus Mwanyika (Mb), ameeleza kuridhishwa kwake na hatua ya ujenzi wa jengo la kisasa la Vipimo na Viwango katika Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE) jijini Dar es Salaam.
Akizungumza Machi 12, 2026, Mhe. Mwanyika amebainisha kuwa mradi huo wa ghorofa 10 umefikia asilimia 93 ya utekelezaji wake, jambo linaloashiria usimamizi madhubuti na weledi katika ukamilishaji wa Jengo Jengo hilo ili kukidhi ongezeko la wanafunzi wanaodahiliwa kila mwaka.
Vilevile, Mwenyekiti huyo ametoa rai kwa uongozi wa chuo kuendelea kutoa na kuimarisha elimu ya kati (middle-level education) katika fani za biashara hususani ujasiliamali kwa kuwa ni nyenzo adhimu kwa wahitimu wanaojiandaa kuingia kwenye soko la ajira binafsi na
Kutasaidia kuongeza hadhi ya chuo na kuchochea ari ya wanafunzi wengi zaidi kujiunga na taasisi hiyo.
Amesema kuwa uimara wa chuo unategemea ubora wa mafunzo unayoyatoa na uwezo wake wa kuzalisha wataalamu wenye ushindani katika soko la ndani na nje ya nchi.
Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Dennis Londo (Mb), amefafanua kuwa mradi huo unatekelezwa kupitia bajeti ya Serikali ya mwaka wa fedha 2025/26 na unatarajiwa kuwa na uwezo wa kubeba zaidi ya wanafunzi 4,000 kwa wakati mmoja.
Aidha amebainisha kuwa Jengo hilo la Vipimo na Viwango litakuwa kitovu cha mafunzo ya masoko na nyanja mbalimbali za kibiashara ambazo zinahitajika kwa kiasi kikubwa kulingana na mwelekeo wa sasa wa uchumi wa viwanda.
Naye Mkuu wa Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE), Prof. Edda Lwoga, ameeleza kuwa mradi huo ulioanza Mei 25, 2023, umekuwa mhimili wa mabadiliko makubwa ya kitaaluma chuoni hapo. Alibainisha kuwa kukamilika kwa jengo hilo kutaongeza fursa za udahili kwa wanafunzi wengi wanaohitaji masomo ya biashara na ujasiriamali, ikiwemo kozi fupi ambazo zimekuwa na mahitaji makubwa kwa wadau wa sekta binafsi.

📍*Geita.*
Mwenyekiti wa Kamati ya TEITI, Balozi Wilson Masilingi, ametembelea Mgodi wa Dhahabu wa Geita Gold Mining Limited akiambatana na Menejimenti ya TEITI, kwa lengo la kujitambulisha na kufanya mazungumzo na menejimenti ya mgodi huo.
Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Balozi Masilingi alisema ziara hiyo imelenga kujenga na kuimarisha ushirikiano kati ya TEITI na wadau wa sekta ya uziduaji, hususan migodi mikubwa inayochangia maendeleo ya taifa.
Alisema kuwa aliteuliwa kusimamia taasisi hiyo muhimu na Mhe.Dkt.Samia Suluhu Hassan, Rais wa Tanzania, mwezi Januari mwaka huu, hivyo anaona ni muhimu kujitambulisha kwa wadau wakuu wa sekta hiyo ili kuimarisha ushirikiano katika utekelezaji wa majukumu ya TEITI.
“Utekelezaji wa shughuli za EITI nchini ni wa ushirikiano, hivyo nitashirikiana kikamilifu na wadau wote ili kuendeleza gurudumu la uwazi na uwajibikaji katika sekta ya uziduaji,” alisema Balozi Masilingi.
Katika ziara hiyo, menejimenti ya mgodi ilitoa maelezo kuhusu maendeleo yaliyofikiwa tangu kuanzishwa kwa mgodi huo, ikiwemo namna wanavyotekeleza sheria, kanuni na miongozo ya sekta ya madini pamoja na masharti ya leseni ya uchimbaji.
Aidha, ilielezwa kuwa mgodi huo umeendelea kutenga fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya Uwajibikaji kwa Jamii (CSR) katika halmashauri mbalimbali za Mkoa wa Geita, hatua inayochangia maendeleo ya jamii zinazouzunguka mgodi.
Pia ilibainishwa kuwa kwa sasa mgodi huo unaendeshwa kwa kiasi kikubwa na Watanzania na umeendelea kuongeza ajira kwa wananchi wa ndani ikilinganishwa na miaka ya awali ya uendeshaji wake.
Balozi Masilingi aliishukuru menejimenti ya mgodi kwa mapokezi mazuri waliompatia pamoja na utayari wao wa kuendeleza ushirikiano kwa manufaa ya sekta ya uziduaji na maendeleo ya taifa.
Kwa upande wake, Katibu Mtendaji wa TEITI, Bi. Mariam Mgaya, aliishukuru menejimenti ya mgodi kwa kuendelea kushirikiana na TEITI katika utekelezaji wa matakwa ya EITI pamoja na Sheria ya TEITA ya mwaka 2015, inayolenga kuimarisha uwazi na uwajibikaji katika sekta ya uziduaji.
Alisisitiza kuwa ushirikiano huo unapaswa kuendelezwa ili kuongeza uwazi na uwajibikaji katika usimamizi wa rasilimali za madini, mafuta na gesi asilia nchini.
Naye Meneja wa mgodi huo, Bw. Ashraf Suryaningrat, alisema Geita Gold Mining Limited itaendelea kushirikiana kikamilifu na TEITI katika kufanikisha lengo la uwazi na uwajibikaji katika sekta ya uziduaji, akibainisha kuwa mgodi huo ni miongoni mwa wadau wakubwa wa TEITI nchini.

Naibu Waziri wa Ujenzi Eng. Godfrey Kasekenya amemtaka mkandarasi JASCO anaejenga daraja la Kabalisi mita 40 na GEMEN anaejenga daraja la Sange mita 40 wilayani Ileje kuhakikisha ujenzi huo unakamilika ifikapo machi 30 mwaka huu.
Eng. Kasekenya amezungumzia umuhimu wa ujenzi huo kuendana na uwekaji wa taa katika madaraja hayo na kuhakikisha mitaro karibu na madaraja hayo inasakafiwa vizuri.
" Hakikisheni ujenzi wa madaraja haya unakidhi ubora uliosanifiwa ili kuwiana na barabara za lami zitakapojengwa", amesema Eng. Kasekenya.
Msimamizi wa ujenzi huo Eng. Jonas Matete kutoka Kitengo cha Usimamizi wa Barabara cha TANROADS (TECU), amesema atawasimamia Wakandarasi hao ili madaraja hayo yayojengwa sehemu zenye miinuko yakamilike kwa wakati na ubora na hivyo kuchochea fursa za kijamii na kiuchumi kwa wananchi
Madaraja ya Kabalisi na Sange yako katika barabara ya mkoa itokayo Ibungu- Kalembo-Kafwafwa hadi Kimo yenye urefu wa km 46.1 na inaunganisha wilaya ya Ileje mkoani Songwe na Rungwe mkoani Mbeya.
Zaidi ya shilingi bilioni 7.9 zimetumika katika ujenzi wa daraja la Kabalisi wakati shilingi bilioni 7 zikitumika kujenga daraja la Sange.
Na WMJJWM Dar Es Salaam
Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi, amezindua kamati maalum ya kuratibu na kuhamasisha michango kwa ajili ya kuwasaidia wanafunzi wenye mahitaji maalum.
Akizungumza baada ya kuzindua kamati hiyo Machi 11, 2026, Mkoani Dar Es salaam, Mahundi amesema uanzishwaji wa Kamati hiyo ni sehemu ya juhudi za serikali na wadau kuhakikisha wanafunzi wenye mahitaji maalum wanapata huduma na kuwa na mazingira bora ya kujifunzia na kuendeleza ndoto zao.
“Watoto wenye mahitaji maalum ni sehemu muhimu ya jamii yetu hivyo Serikali itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha wanapata fursa sawa za elimu, huduma na msaada unaowawezesha kufikia ndoto zao pia kamati hii itakuwa na jukumu la kuhamasisha jamii, taasisi na wadau mbalimbali kuchangia rasilimali zitakazosaidia kuboresha mahitaji ya wanafunzi hao ikiwemo vifaa vya kujifunzia, huduma za kijamii na mazingira rafiki ya elimu.,” amesema Mhe. Mahundi.
Naye Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Dar Es Salaam Lawrence Malangwa amesema ni muhimu ushirikiano wa jamii katika kuwasaidia watoto wenye uhitaji ili kuhakikisha hakuna mtoto anayekosa haki ya elimu kutokana na changamoto za maisha hiivyo tutasimamia vyema upatikananji wa vifaa na mtumizi kwa Watoto hao.
Kwa upande wake Mhazini wa Kamati ya Elimu Mama Tunu Pinda ameipongeza Wizara kwa kuendelea kuonesha dhamira ya dhati katika kutetea na kuimarisha ustawi wa makundi maalum nchini, akieleza kuwa hatua hiyo itachochea ari ya wadau wengi zaidi kujitokeza kusaidia wanafunzi wenye mahitaji.
Uzinduzi huo unatarajiwa kuwa chachu ya kuimarisha ushirikiano kati ya Serikali, wadau na jamii katika kuhakikisha wanafunzi wenye uhitaji wanapata msaada unaohitajika ili waweze kusoma na kufanikiwa kama watoto wengine.
Na Mwandishi Wetu Dar es Salaam.
Tume ya Ushindani (FCC) imesema wazalishaji wa vifaa vya ujenzi wana wajibu wa kumlinda mlaji kwa kuhakikisha wanazalisha na kuuza bidhaa zenye ubora unaolingana na thamani ya fedha anayolipa mnunuzi.
FCC imeeleza kuwa ni muhimu kwa wazalishaji kuzingatia viwango vinavyotakiwa katika uzalishaji wa vifaa vya ujenzi ili kuepusha uwepo wa bidhaa zisizo na ubora sokoni, ambazo zinaweza kusababisha hasara kwa watumiaji na kudhoofisha imani ya wananchi katika bidhaa hizo.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa semina kwa wazalishaji wa vifaa vya ujenzi kuelekea kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Mlaji Duniani, Mkurugenzi wa Udhibiti wa Mienendo ya Bidhaa Inayokatazwa na Sheria ya Ushindani wa FCC, Bi. Magdalena Utouh, kwa niaba ya Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, amesema ulinzi wa mlaji ni miongoni mwa majukumu makuu ya Tume hiyo.
Amesema FCC itaendelea kufuatilia mwenendo wa soko la bidhaa za ujenzi ili kuhakikisha haki za walaji zinalindwa na wananchi wanapata bidhaa salama na zenye ubora unaokidhi viwango vinavyotakiwa.
Bi. Utouh amewataka wazalishaji wa vifaa vya ujenzi kuendesha biashara zao kwa kuzingatia sheria na kanuni za ushindani wa haki, hatua ambayo itasaidia kujenga soko lenye ushindani wa kweli unaolinda maslahi ya walaji pamoja na kuchochea maendeleo ya sekta ya ujenzi nchini.
Ameeleza kuwa sekta ya ujenzi ni mhimili muhimu wa ukuaji wa uchumi wa taifa, hivyo uzalishaji wa vifaa vya ujenzi unapaswa kufanyika kwa kuzingatia viwango stahiki na thamani halisi ya fedha inayolipwa na mlaji.
“FCC ina jukumu la kufuatilia mwenendo wa ushindani katika soko ili kuhakikisha hakuna makubaliano ya kupanga bei miongoni mwa wafanyabiashara ambayo yanaweza kumuathiri mlaji,” amesema Bi.Magdalena
Amesema Tume haitavumilia vitendo vyovyote vinavyomuumiza mlaji, akisisitiza kuwa sheria na miongozo ya ushindani ipo wazi na wazalishaji wanapaswa kuizingatia kikamilifu.
Hata hivyo amesema mikutano na majadiliano kati ya FCC na wadau wa sekta ya ujenzi itaendelea kufanyika mara kwa mara ili kuimarisha ushindani wa soko na kuhakikisha walaji wanapata bidhaa na huduma bora.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Huduma za Wanachama wa Shirikisho la Wamiliki wa Viwanda Tanzania (CTI), Bi. Neema Mhondo, amesema sekta ya ujenzi ina mchango mkubwa katika kukuza uchumi wa nchi pamoja na kutoa ajira kwa wananchi.
Hata hivyo, amesema wazalishaji wa ndani wanakabiliwa na changamoto ya uwepo wa bidhaa bandia sokoni, hali inayofanya viwanda vya ndani kupata ugumu katika ushindani kutokana na gharama kubwa za uzalishaji na uendeshaji wa biashara.
Semina hiyo ya siku moja imefanyika Machi 11, 2026 katika Ukumbi wa Mikutano wa Ngorongoro katika Ofisi za FCC, Jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi wa Udhibiti wa Mienendo ya Bidhaa inayokatazwa na Sheria ya Ushindani wa FCC Bi.Magdalena Utouh akizungumza wakati akifungua Semina ya Wadau wa Uzalishaji wa Vifaa vya Ujenzi ,jijini Dar es Salaam.
Meneja wa Kumlinda Mlaji wa FCC Joshua Msoma akitoa mada kwa wadau wa uzalishaji wa vifaa vya Ujenzi ikiwa ni muendelezo wa FCC kukutana na wadau kuelekea maadhimisho ya Siku ya Mlaji Duniani,jijini Dar es Salaam. 
Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini wa FCC,Bi. Roberta Feruzi akitoa maelezo kuhusiana na Semina ya wadau uzalishaji wa vifaa vya Ujenzi ikiwa ni muendelezo wa FCC kukutana na wadau kuelekea maadhimisho ya Siku ya Mlaji Duniani,jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi wa Huduma za Wanachama wa CTI Neema Mhondo akizungumza kwa niaba ya wadau kuhusiana na semina ya Wadau wa Uzalishaji wa wa vifaa vya Ujenzi ,jijini Dar es Salaam.
Picha ya pamoja ya makundi mbalimbalj ya Mkurugenzi wa Udhibiti wa Mienendo ya Bidhaa inayokatazwa na Sheria ya Ushindani wa FCC Bi.Magdalena Utouh na Wadau wa Uzalishaji wa Vifaa vya Ujenzi ,jijini Dar es Salaam.














.jpeg)





