Serikali imewataka Vijana wanaojishughulisha na Biashara za Mitandao nchini kuwa walinzi Wakuu wa mifumo ya kidijitali kwa kupambana vikali na matapeli wa mtandaoni, kwani vitendo vyao vinaharibu uaminifu ambao ndio nguzo kuu ya uchumi wa sasa na wa baadaye.
Bondia mashuhuri kutoka Marekani mwenye rekodi ya kushika mikanda yote minne ya dunia katika uzito wake ukiwemo wa welterweight, Terence “Bud” Crawford, ametua nchini Tanzania leo Mei 24, 2026, kuanza “Royal Tour.”

Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) inaendesha semina kwa wamiliki na wahariri wa redio za kijamii zipatazo 50 toka Tanzania Bara na Zanzibar kuanzia tarehe 23 hadi 25,Mei 2026, Lengo kuu likiwa ni kukuza uelewa juu ya majukumu ya TADB pamoja na kuonesha fursa zinazopatikana katika benki hiyo.

 


Na. OWM TAMISEMI, 

Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa ( OWM – TAMISEMI) Bw. Sospeter Mtwale, amesema Serikali imejipanga kuhakikisha biashara ya kaboni nchini inatekelezwa kwa uwazi, uwajibikaji na ushirikishwaji wa jamii ili kuwanufaisha wananchi na Taifa kwa ujumla. 

Bw. Mtwale amesema hayo  katika Kikao cha Makatibu Wakuu cha kupokea taarifa ya makubaliano ya uendeshaji wa biashara ya kaboni kilichofanyika tarehe 22 Mei 2026 katika ukumbi wa Best Western. Kikao hiki ni utekelezaji wa maagizo ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliyoyatoa wakati wa ufunguzi wa mkutano wa ALAT jijini Dodoma mwaka 2025, ambapo alielekeza kuwa wadau muhimu washirikishwe kabla ya Halmashauri kusaini mikataba ya biashara ya kaboni ili kuwepo uelewa wa pamoja.

“Serikali inatarajia mikataba yote ya biashara ya kaboni izingatie sheria, kanuni na taratibu pamoja na kuhakikisha uhifadhi wa mazingira unaenda sambamba na maendeleo ya wananchi,” amesema Bw. Mtwale.

Bw. Mtwale   amesisitiza umuhimu wa kuwepo kwa mifumo madhubuti ya ufuatiliaji ili biashara hiyo iwe na tija kwa jamii na Taifa.

Katika kikao hicho, wataalam wamejadili makubaliano yanayotarajiwa kufanywa kati ya Halmashauri za Uvinza na Tanganyika pamoja na kampuni ya Carbon Tanzania Limited kwa ajili ya biashara ya kaboni katika misitu ya Masito, Tongwe Mashariki na Tongwe Magharibi yenye zaidi ya hekta 683,000.

Katika utekelezaji wa maagizo hayo,  wizara na taasisi mbalimbali zimeshiriki, zikiwemo Ofisi ya Makamu wa Rais – Mazingira, Ofisi ya Waziri Mkuu-TAMISEMI Wizara ya Fedha, Kituo cha Taifa cha Ufuatiliaji na Tathmini ya Kaboni, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Wizara ya Maliasili na Utalii, uongozi kutoka mikoa ya Katavi na Kigoma pamoja na wadau wengine muhimu.









NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

Serikali imesema mafanikio yaliyofikiwa na kiwanda cha kuunganisha magari aina ya Howo kinachomilikiwa na Saturn Corporation Limited ndani ya kipindi cha miaka miwili ni ushahidi wa ukuaji wa sekta ya viwanda nchini, huku uzalishaji, ajira na mapato ya Serikali vikiongezeka kwa kasi.
Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

TANZANIA inatarajiwa kupokea ujumbe mkubwa wa viongozi wa elimu ya juu kutoka Malaysia, wakiwemo viongozi kutoka Wizara ya Elimu ya Malaysia, Education Malaysia Global Services (EMGS), pamoja na wawakilishi wa vyuo vikuu tisa.







>Sheria Isichague Chama

NA OSCAR ASSENGA, TANGA

Katibu Mkuu wa Chama cha NLD, Doyo Hassan Doyo, amesema mjadala unaoendelea kuhusu hatua zinazochukuliwa na Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa umeonyesha jinsi baadhi ya Watanzania wanavyotoa hukumu za haraka bila kutafakari misingi ya sheria.

Doyo alisema kumekuwa na mtazamo kwamba Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa inalenga zaidi vyama vya upinzani, huku ukweli ukiwa ni kwamba taasisi hiyo inasimamia sheria bila kuangalia itikadi ya chama husika.



Akizungumza wakati wa ziara ya chama hicho mkoani Tanga, alisema hatua zilizochukuliwa hivi karibuni dhidi ya baadhi ya viongozi wa kisiasa zinatokana na matamshi yaliyotafsiriwa kuwa na viashiria vya uvunjifu wa sheria za vyama vya siasa.

“Sheria iko wazi. Chama au kiongozi anayekiuka taratibu anaweza kupewa adhabu ya faini, kusimamishwa shughuli au hata kuchukuliwa hatua nyingine za kisheria. Hii siyo kwa chama fulani pekee,” alisema.





Alieleza kuwa baada ya viongozi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kutoa kauli zilizozua mjadala, Ofisi ya Msajili iliwaandikia barua ya kutaka maelezo. Hatua hiyo, kwa mujibu wa Doyo, ilitafsiriwa vibaya na baadhi ya wananchi pamoja na wanaharakati waliodai kuwa upinzani unaonewa.

Hata hivyo alisema hali hiyo imebadilika baada ya mmoja wa viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) naye kuandikiwa barua kufuatia matamshi yake ya kisiasa.

“Watu walidhani sheria inafanya kazi kwa upande mmoja, lakini sasa imeonekana wazi kuwa anayevunja sheria ndiye anayechukuliwa hatua, bila kujali anatoka chama gani,” alisema.

Doyo alisema vyama vya siasa vinapaswa kutambua kuwa vimesajiliwa kwa mujibu wa sheria na hivyo vina wajibu wa kuendesha shughuli zake ndani ya mipaka ya kisheria.

Alionya kuwa siasa zisizo na nidhamu zinaweza kupelekea uvunjifu wa amani na kuhatarisha usalama wa Taifa.

“Ukianza kufanya siasa nje ya sheria, maana yake unaondoka kwenye misingi ya kisiasa na kinachofuata ni migogoro na vurugu. Taifa haliwezi kujengwa kwa misingi ya shinikizo na vitisho,” alisema.








Aidha, aliitaka Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa kuendelea kusimamia sheria kwa uthabiti bila kuogopa presha za kisiasa kutoka kwa wanasiasa au wanaharakati.

Kwa mujibu wa Doyo, uwepo wa taasisi imara zinazotekeleza sheria kwa haki ndiyo msingi wa kulinda amani na utulivu wa nchi.

Katika ziara hiyo ya NLD iliyoanzia Pangani na kuelekea Lushoto, chama hicho kimesema kinaendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kuheshimu sheria, taratibu na kanuni za kisiasa ili kuimarisha demokrasia na mshikamano wa Taifa.

 


WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema jamii inapaswa kurejea katika misingi ya malezi ya pamoja na uwajibikaji wa kijamii ili kujenga kizazi chenye maadili, kinachoheshimu viongozi, wazazi pamoja na taasisi za jamii.

“Tunataka kujenga jamii inayoguswa na changamoto za wengine. Maadili mema yanaanzia kwenye malezi ya familia na jamii kwa ujumla,” amesema Dkt. Mwigulu.

Dkt. Mwigulu amesema hayo leo Jumapili, Mei 24, 2026 aliposhiriki Ibada ya Pentekoste katika Kanisa Kuu la KKKT Usharika wa Iringa Mjini iliyoongozwa na Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Iringa, Dkt. Blaston Gavile.

Amesema Serikali itaendelea kushirikiana na taasisi za dini katika kuimarisha huduma za kijamii, malezi ya maadili na utekelezaji wa miradi ya maendeleo inayogusa maisha ya wananchi.

“Ushirikiano kati ya Serikali na taasisi za dini ni jambo kubwa sana katika maendeleo ya nchi yetu. Shule nyingi kongwe na taasisi mbalimbali za huduma zilianzishwa na taasisi za dini kabla hata ya Serikali kuendelea kuzijenga na kuzisimamia,” amesema Dkt. Mwigulu.

Aidha, Waziri Mkuu amesema kuanzia mwaka 2028 Serikali itaanza rasmi utekelezaji wa elimu ya lazima ya miaka 10 kwa watoto wote wa Kitanzania kuanzia elimu ya awali hadi kidato cha nne kwa lengo la kuongeza ujuzi na kuwajengea vijana uwezo wa kujitegemea.

“Hatusemi shule ya msingi iwe miaka 10, tunasema elimu ya lazima kwa mtoto wa Kitanzania iwe miaka 10 ili watoto wetu wapate maarifa na ujuzi wa kutosha kwa maisha yao ya baadaye,” amesema.

Dkt. Mwigulu amesema hatua hiyo pia inalenga kupunguza changamoto za watoto kuacha shule katika umri mdogo pamoja na kukabiliana na changamoto za ndoa za utotoni kwa kuhakikisha watoto wanabaki shuleni kwa muda mrefu zaidi.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amepongeza KKKT Dayosisi ya Iringa kwa kuendelea kuwahudumia watoto yatima na watu wenye mahitaji maalum huku akieleza kuwa Serikali inaendelea kufanya maboresho ya sera na mifumo ya utoaji wa huduma kwa makundi hayo.

Amesema Serikali imeanza kufanya marekebisho ya mfumo wa utoaji wa mikopo kwa watu wenye ulemavu ili hata mtu mmoja mmoja aweze kunufaika badala ya kulazimika kuunda vikundi.

“Tunataka kujenga mfumo unaowatambua watu wenye mahitaji maalum kwa utu wao na kuhakikisha wanapata huduma na msaada stahiki bila usumbufu,” amesema.

Kwa upande wake, Askofu wa KKKT Dayosisi ya Iringa, Dkt. Blaston Gavile amepongeza kazi kubwa inayofanywa na Waziri Mkuu katika kusikiliza na kutatua changamoto za wananchi pamoja na kuendelea kusimamia maendeleo ya Taifa kwa karibu.

“Hakika kwa kipindi hiki kifupi tangu kuteuliwa kwako tumeona moyo wako wa kuwatumikia Watanzania. Umetenga muda wako kusikiliza kero za wananchi na kuzitatua kwa busara, uelewa na hekima kubwa,” amesema Dkt. Gavile.

Aidha, amesema KKKT inaunga mkono maono ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayolenga kujenga uchumi imara, huduma bora za jamii na maendeleo endelevu kwa Watanzania wote.

Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) imeteketeza kilogramu 504.36 za dawa za kulevya aina ya heroin katika kiwanda cha saruji cha Dangote kilichopo mkoani Mtwara. Uteketezaji huo umefanyika kufuatia amri ya Mahakama Kuu Masijala Ndogo ya Mtwara baada ya kukamilika kwa hatua za kisheria dhidi ya watuhumiwa waliohusika na dawa hizo.

 ▪️Asema mradi huo utafungua fursa mpya za uchumi na kupunguza msongamano wa magari mjini Iringa

▪️Aagiza wakandarasi kuwalipa kwa wakati wadaiwa wao

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali itaendelea kuwekeza katika miradi ya kimkakati ya miundombinu ili kuboresha usafiri, kuongeza ufanisi wa uchukuzi na kufungua fursa mpya za maendeleo ya kiuchumi nchini.

“Barabara hii ni muhimu kwa uchumi wa Mkoa wa Iringa na Taifa kwa ujumla. Itasaidia kupunguza msongamano wa magari, kuongeza biashara na kuchochea ukuaji wa mji wa Iringa,” amesema Dkt. Nchemba.

Amesema hayo leo Jumamosi, Mei 23, 2026 wakati akikagua maendeleo ya ujenzi wa Barabara ya Mchepuo ya Mji wa Iringa (Iringa Municipal Bypass) yenye urefu wa kilomita 7.3 inayojengwa kwa kiwango cha lami mkoani Iringa.

Mradi huo unaotekelezwa na kampuni ya SINOHYDRO Corporation Limited kwa usimamizi wa TANROADS kupitia kitengo chake cha TECU, unagharimu shilingi bilioni 41.6.

Akizungumza baada ya kupokea taarifa ya utekelezaji wa mradi huo, Waziri Mkuu amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kutekeleza miradi mikubwa ya barabara nchini kwa lengo la kuimarisha uchumi na kurahisisha huduma za usafiri na uchukuzi.

Amesema barabara hiyo itakuwa suluhisho la kudumu la msongamano wa magari katika mji wa Iringa hususan katika eneo la mlima wa Ipogoro ambalo limekuwa likikumbwa na ajali na changamoto za usafiri kutokana na ongezeko kubwa la idadi ya watu, magari na vyombo vingine vya usafiri.

“Ndugu zangu wana Iringa, Mheshimiwa Rais amejipambanua kuwa ni Rais wa matokeo. Akisema jambo analitekeleza, na ndiyo maana mnaendelea kuona miradi mikubwa ya barabara ikitekelezwa karibu kila kona ya nchi,” amesema.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amewataka wakandarasi wanaotekeleza miradi ya Serikali kuhakikisha wanawalipa kwa wakati wakandarasi wadogo, mafundi na vibarua wanaoshiriki katika utekelezaji wa miradi hiyo.

“Kadri wanavyopata fedha, wawalipe wale wanaotekeleza mradi pamoja nao. Sio vizuri mradi ukamilike wakati wengine waliotoa huduma wanadai malipo yao,” amesema.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Ujenzi, Mhandisi Godfrey Kasekenya amesema mradi huo ni sehemu ya utekelezaji wa mkakati wa Serikali wa kujenga barabara za mchepuo katika miji mikubwa ili kupunguza msongamano wa magari na kuongeza ufanisi wa usafiri wa mizigo nchini.

Amesema Serikali pia inaendelea kutekeleza miradi mingine ya barabara za mchepuo katika maeneo mbalimbali nchini ikiwemo Dodoma, Mbeya, Morogoro, Mwanza, Arusha na Tanga.

Awali akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa mradi huo, Kaimu Meneja wa TANROADS Mkoa wa Iringa, Mhandisi Hosea Machaka amesema utekelezaji wa mradi umefikia asilimia 38.5 huku kazi mbalimbali zikiendelea ikiwemo ulipuaji wa miamba, ujazaji wa kifusi, ujenzi wa makalavati pamoja na ujenzi wa njia za mchepuo.

Amesema wananchi 186 walioathiriwa na mradi huo wamelipwa fidia yote yenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 4.6, hatua iliyosaidia kuondoa changamoto za upatikanaji wa eneo la mradi.

Naye Mbunge wa Iringa Mjini, Fadhili Ngajilo amesema wananchi wa Iringa wameupokea mradi huo kwa matumaini makubwa kutokana na mchango wake katika kuboresha usafiri na kuchochea ukuaji wa shughuli za kiuchumi katika mji huo.









 ▪️Aonya dhidi ya vitendo vya uchochezi, kujiteka na propaganda zinazolenga kuwagombanisha Watanzania

▪️Asema Serikali imejikita kusikiliza wananchi na kutatua kero zao badala ya mijadala ya uchaguzi

▪️Awataka wananchi kuendelea kulinda mshikamano na utulivu wa Taifa


WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amevitaka vyombo vya ulinzi na usalama kuendelea kuwa macho dhidi ya vitendo vinavyolenga kuvuruga amani ya nchi huku akisisitiza kuwa Serikali itaendelea kusimamia usalama wa wananchi na mali zao.

“Kuweni macho na njama za aina hii, shughulikeni na waovu wa aina hii. Mliweza lile la Kibiti, mliweza lile la Amboni na mambo mengine mengi mmeweza. Kuweni macho kuhakikisha michezo ya aina hiyo haifanikiwi huku mkihakikisha usalama wa raia wetu na mali zao unaendelea kulindwa,” amesema Dkt. Mwigulu.

Dkt. Mwigulu amesema hayo leo Jumamosi, Mei 23, 2026 alipozungumza na wananchi wa Manispaa ya Iringa katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika viwanja vya Kichangani mkoani Iringa.

Amesema amani ni msingi wa maendeleo ya Taifa na kwamba Watanzania wanapaswa kuendelea kulinda mshikamano wa kitaifa na kukataa vitendo vya uchochezi vinavyoweza kusababisha migawanyiko ya kisiasa, kidini au kijamii.

“Amani ni msingi wa maendeleo ya taifa letu. Kila mwananchi ana wajibu wa kuhakikisha nchi yetu inaendelea kuwa salama na yenye mshikamano,” amesema.

Aidha, Waziri Mkuu amesema zipo njama mbalimbali zinazolenga kuwagombanisha Watanzania kupitia siasa, dini na taarifa za upotoshaji huku akiwataka wananchi kuwa makini na watu wanaowachochea kufanya vitendo vinavyohatarisha usalama wa nchi.

“Tupuuze na wala tusiwe na ushirika na mtu anayekutuma kuvunja amani wakati yeye hayupo hapo na anajua yeye hataathirika,” amesema.

Kadhalika, Dkt. Mwigulu amesema baadhi ya matukio yanayoendelea kujitokeza nchini yakiwemo madai ya watu kujiteka au kushambuliwa yanapaswa kutazamwa kwa umakini mkubwa kwa kuwa baadhi yake yanaweza kuwa sehemu ya njama za kuwagawa Watanzania na kuichonganisha Serikali na wananchi wake.

“Hizi ni ajenda maalum. Hii ni michezo ambayo inalenga kutengeneza hasira na kuwafanya watu wachukiane,” amesema.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema Serikali imejikita zaidi katika kutatua changamoto za wananchi na kusukuma maendeleo badala ya kuendelea kujadili siasa za uchaguzi muda mfupi baada ya uchaguzi mkuu kumalizika.

“Taifa linapotakiwa kupiga hatua, tujadili namna ya kutatua kero za wananchi badala ya kutumia muda mwingi kujadili uchaguzi,” amesema.

Amesema yeye binafsi ameendelea kufanya ziara mbalimbali za kusikiliza wananchi, kupokea changamoto zao na kuhakikisha Serikali inazitatua kwa wakati ili wananchi waendelee na shughuli zao za maendeleo.

“Watu wanahitaji kusikilizwa, wanahitaji kutatuliwa changamoto zao na wanahitaji maendeleo. Hiyo ndiyo kazi ambayo Serikali imepewa na wananchi,” amesema.

Aidha, Dkt. Mwigulu amesema Tanzania imeendelea kuwa mfano wa mshikamano na uvumilivu wa kidini na kijamii barani Afrika kutokana na misingi iliyoasisiwa na viongozi waasisi wa Taifa.

“Hii ndiyo nchi ambayo Mungu ametupatia na Baba wa Taifa ameturithisha. Tukatae vibaraka wanaotaka kuligawa Taifa letu,” amesema.

Waziri Mkuu pia amewaomba viongozi wa dini, wazee wa mila, viongozi wa kisiasa na wananchi kwa ujumla kuendelea kuhubiri amani, mshikamano na uzalendo ili taifa liendelee kuwa salama na lenye umoja.






NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

MKUU wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila amesema uzingatiaji wa viwango katika uzalishaji wa bidhaa na huduma ni msingi muhimu wa kulinda afya za wananchi, kukuza biashara, kuimarisha viwanda vya ndani na kujenga uchumi endelevu wa taifa.
Arusha

Tume ya Madini imeanza rasmi kutumia Mfumo Jumuishi wa Kodi za Ndani (IDRAS) unaolenga kurahisisha utoaji wa huduma, kuongeza ufanisi wa utendaji na kuongeza ukusanyaji wa mapato ya Serikali katika sekta ya madini.

Mbunge wa Jimbo la Gairo, Ahmed Shabiby, ameupongeza Wakala wa Vipimo Tanzania (WMA) kwa kazi kubwa inayofanya katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma na bidhaa zenye vipimo sahihi, hatua ambayo amesema imeendelea kuimarisha ulinzi wa maslahi ya walaji pamoja na wafanyabiashara nchini.

Akichangia leo Mei 22,bungeni Dodoma wakati wa mjadala wa Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda na Biashara kwa mwaka wa fedha 2026/2027, Shabiby amesema  WMA imeendelea kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi mkubwa huku ikishirikiana kikamilifu na wadau mbalimbali kuhakikisha mfumo wa usimamizi wa vipimo nchini unakuwa imara na wa kuaminika.

Shabiby amesema  WMA imekuwa mstari wa mbele kutoa ushirikiano wa karibu kila inapohitajika, jambo lililochangia kuongezeka kwa ufanisi katika usimamizi wa vipimo nchini na kuimarisha imani ya wananchi kwa taasisi hiyo.. Aidha, amempongeza Afisa Mtendaji Mkuu wa WMA, Alban Kihulla, kwa uongozi wake wenye weledi, uwajibikaji na ushirikiano mzuri katika kusimamia majukumu ya wakala huo muhimu kwa maendeleo ya sekta ya biashara na viwanda.

Hata hivyo, mbunge huyo ameitaka WMA kuongeza umakini zaidi katika kudhibiti ubora wa bidhaa za chuma, hususan nondo zinazozalishwa na baadhi ya viwanda nchini, akieleza kuwa bado kuna changamoto ya uwepo wa bidhaa zisizokidhi viwango vya vipimo vinavyotakiwa.

Amesema baadhi ya viwanda vinavyoendeshwa na wawekezaji wa ndani na nje ya nchi vinaendelea kuzalisha nondo zenye upungufu wa vipimo, hali inayoweza kuhatarisha usalama wa majengo pamoja na maisha ya wananchi. “Tusibaki kwenye kutoa faini pekee. Viwanda vinavyotengeneza nondo zisizokidhi vipimo vinapaswa kuchukuliwa hatua kali ikiwemo kufungiwa, ili kulinda usalama wa wananchi na kuhakikisha ubora wa ujenzi nchini,” amesema  Shabiby. Ameongeza kuwa usimamizi madhubuti wa vipimo vya bidhaa za ujenzi ni msingi muhimu katika kukuza sekta ya viwanda, kulinda miundombinu na kuhakikisha maendeleo endelevu ya taifa.

 Wakala wa Vipimo Tanzania umeendelea kusimamia matumizi sahihi ya vipimo nchini kwa mujibu wa Sheria ya Vipimo Sura ya 340, ikiwa ni jitihada za kuhakikisha wananchi wanapata bidhaa sahihi kulingana na thamani ya fedha wanazolipa.

Washiriki wa mafunzo ya kuwajengea uwezo wadau wa Tasnia ya Maziwa mkoani Mbeya wamepata fursa ya kujifunza kwa vitendo kupitia ziara maalum zilizofanyika katika kiwanda cha maziwa cha Chuo Kikuu Cha Sayansi na Teknolojia Mbeya (MUST) pamoja na shamba la ng’ombe wa maziwa la Gereza la Songwe, ikiwa ni sehemu ya kuimarisha uelewa wao kuhusu uzalishaji, uchakataji na usimamizi wa ubora wa maziwa.

 Serikali kupitia Wakala wa Vipimo (WMA) imeendelea kuimarisha huduma za uhakiki wa vipimo nchini kwa kukamilisha ujenzi wa Kituo cha Kisasa cha Uhakiki kilichopo eneo la Misugusugu, mkoani Pwani, ambacho kimegharimu jumla ya shilingi bilioni 7.3.

Kituo hicho kilichojengwa katika eneo lenye ukubwa wa hekta 2.4 ni sehemu ya utekelezaji wa mkakati wa Serikali wa kusogeza karibu huduma za vipimo kwa wananchi na wadau wa kibiashara, sambamba na kuimarisha miundombinu ya kitaifa ya udhibiti wa ubora wa vipimo.

Kwa mujibu wa taarifa iliyowasilishwa Bungeni, kituo hicho kitahusika na uhakiki wa vifaa mbalimbali vinavyotumika katika sekta za nishati na maji, ikiwemo matenki ya magari yanayosafirisha vimiminika, mita mpya za umeme pamoja na dira za maji kabla ya kufungwa kwa watumiaji.

Lengo kuu la uhakiki huo ni kuhakikisha kuwa vifaa hivyo vinakidhi viwango vilivyowekwa kitaifa na kimataifa, na hivyo kuhakikisha usahihi wa vipimo, kulinda haki za watumiaji na wauzaji, pamoja na kuongeza ufanisi katika usimamizi wa rasilimali za umma.

Hata hivyo, WMA imebainisha kuwepo kwa changamoto mbalimbali zinazokwamisha utekelezaji wake, ikiwemo mwitikio hafifu kutoka kwa baadhi ya wazabuni wa mita za umeme kushindwa kutekeleza takwa la kisheria la kuwasilisha mita hizo kwa ajili ya uhakiki kabla ya kusambazwa kwa taasisi nunuzi.

Changamoto nyingine ni malimbikizo ya muda mrefu ya madai ya malipo ya huduma za uhakiki wa dira za maji kutoka kwa baadhi ya kampuni zilizopewa zabuni, hali inayoweza kuathiri uendelevu wa huduma na ufanisi wa taasisi hiyo.

Akizungumza Bungeni, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo, Mariam Ditopile, amesema kamati yake imebaini hatua nzuri zilizofikiwa na WMA katika kuboresha huduma zake, ikiwemo ujenzi wa kituo hicho cha kisasa cha Misugusugu.

Ditopile amesema kuwa kamati imepongeza juhudi za Serikali katika kuimarisha miundombinu ya uhakiki wa vipimo, lakini pia imesisitiza umuhimu wa kuongeza ufuatiliaji wa wazabuni ili kuhakikisha wanazingatia matakwa ya kisheria kabla ya kusambaza vifaa kwa wananchi.

Aidha, alibainisha kuwa changamoto ya malimbikizo ya madeni ya huduma za uhakiki inapaswa kushughulikiwa kwa haraka ili kuepusha athari katika uendeshaji wa taasisi na utekelezaji wa majukumu yake ya msingi.

Kamati hiyo pia imeitaka Serikali kuendelea kuimarisha usimamizi wa sekta ya vipimo ili kuhakikisha vifaa vyote vinavyotumika nchini vinakuwa sahihi na vinakidhi viwango vilivyowekwa, hatua itakayosaidia kuongeza ufanisi katika sekta mbalimbali za uchumi.

Kwa ujumla, ujenzi wa Kituo cha Misugusugu unatajwa kuwa hatua muhimu katika mageuzi ya sekta ya vipimo nchini, ukiwa na lengo la kuongeza uwazi, usahihi na ulinzi kwa watumiaji wa huduma mbalimbali za kijamii na kiuchumi.


 


Ofisi ya Makamu wa Rais inatarajiwa kuzindua Programu ya Kitaifa ya Mageuzi ya Kimkakati ya Mazingira Endelevu Tanzania katika kilele cha Siku ya Mazingira Duniani (WED) ambapo kitaifa itafanyika jijini Dodoma, Juni 5, 2026.

Akizungumza katika uzinduzi wa usafi wa Mazingira kuelekea siku hiyo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni alisema lengo ni kuhakikisha Tanzania inakuwa nchi ya mfano duniani katika suala la Uhifadhi na Utunzaji wa Mazingira.

Alisema Programu hiyo inalenga kutekeleza Dira, 2050 hususan nguzo ya tatu kuhusu Uhifadhi wa Mazingira na Ustahimilivu wa Mabadiliko ya Tabianchi ikiwa na lengo la kupanda miti bilioni 2 kwa mwaka, kuimarisha Biashara ya Kaboni, Uanzishaji wa Bustani za Kijani katika Miji na shughuli zingine za Kijani.

“Pia program hii inatarajia kuongeza ajira zinazoweza kufikia zaidi ya elfu ishirini na tano (25,000) ifikapo 2030 kupitia sekta za taka, misitu, kaboni na nishati safi,”alisema Mhe. Masauni.

Alifafanua kuwa tukio hilo ni sehemu ya juhudi za Kitaifa na Kimataifa za kulinda mazingira, kupambana na athari za mabadiliko ya tabianchi na kujenga jamii yenye afya na ustahimilivu.

Aidha, alileza Dira, 2050 imeweka maono ya Taifa kuwa hadi kufikia mwaka 2050 Tanzania iwe kinara katika matumizi endelevu ya rasilimali, Taifa linalotumia taka kama malighafi kwa manufaa ya kiuchumi na Taifa kinara katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi kwa kuimarisha ustahimilivu na uendelevu wa mazingira.

“Juhudi zinahitajika ili kutekeleza shughuli za mazingira kwa njia jumuishi inayohusisha makundi yote ya kijamii bila kujali jinsia au umri. Kwa jiji la Arusha, tafiti za mwaka 2020 zinaonesha kuwa jiji linazalisha takribani tani 550 za taka ngumu kwa siku, ambapo zaidi ya asilimia 60 ya taka hizo zinaweza kurejelezwa ikiwa zitadhibitiwa vizuri kupitia uchumi rejeshi,"aliongeza.

"Kwa ngazi ya Kitaifa, Tanzania inakadiriwa kupoteza takribani hekta 469,420 za misitu kila mwaka kutokana na shughuli mbalimbali zisizo endelevu ikiwa ni pamoja na matumizi makubwa ya kuni na mkaa, kilimo kisicho endelevu, ufugaji holela pamoja na shughuli nyingine za kibinadamu zinazosababisha uharibifu wa mazingira hali inayochangia kuongezeka kwa gesi joto, kuharibu vyanzo vya maji na kuhatarisha usalama wa bioanuwai,".

Alieleza Upandaji wa miti yenye matumizi mbalimbali una mchango mkubwa katika kufyonza gesi ya kaboni, kupunguza mmomonyoko wa udongo, kuhifadhi vyanzo vya maji, kutoa matunda pamoja na kuongeza kipato kwa wananchi kupitia bishara ya Kaboni na kuongeza ustahimilivu dhidi ya athari za Mabadiliko ya Tabianchi.

"Matumizi ya nishati safi ya kupikia ni hatua muhimu katika kupunguza utegemezi wa kuni na mkaa ambao umeendelea kuwa miongoni mwa sababu kuu za uharibifu wa misitu nchini.

“Kuimarisha upatikanaji na matumizi ya nishati safi kama vile gesi asilia, umeme, biogas na teknolojia bora za kupikia kutasaidia kupunguza kasi ya ukataji miti, kupunguza uzalishaji wa gesi joto na kuboresha afya za wananchi hususan wanawake na watoto ambao huathirika zaidi na moshi unaotokana na matumizi ya nishati isiyosafi," alisisitiza.

Naye Mkuu wa Wilaya Arusha Mhe. Joseph Mkude alisema kila mmoja ana wajibu wa kutunza na kuhifadhi mazingira na kuzingatia matumizi ya nishati safi ya kupikia na kusema taasisi nyingi zinatekeleza agizo hilo.

Amesema  arusha imekuwa ikifanya kila jitihada kuhakikisha jiji hilo linakuwa safi na kushirikisha jamii yote kutambua umuhimu wa utunzaji wa mazingira ndio maana wanafunzi wamepewa kipaumbele.





Mtandao wa Wamiliki wa Nyumba za Upataji Nafuu nchini, Tanzania Network for Voice of Sober House Tanzania, umemkabidhi tuzo ya shukrani Kamishna Jenerali wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA), Aretas Lyimo, kwa kutambua mchango wake mkubwa katika mapambano dhidi ya dawa za kulevya hususan katika eneo la usimamizi, uratibu na uwezeshaji wa nyumba za upataji nafuu nchini.


Na Mwandishi Wetu - Dar es Salaam


Tume ya Taifa ya Mipango kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa UNDP leo Mei 22, imefanya mjadala uliyowakutanisha wadau wa maendeleo, sekta binafsi, asasi za kiraia, watafiti na taasisi za elimu ya juu kujadili hatua mbalimbali na afua zinazoweza kutumika ili kukabiliana na athari za mgogoro wa ukanda wa Ghuba.

Akifungua mjadala huo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji Mhe. Prof. Kitila Mkumbo amesema kuwa Serikali itaendelea kuchukua hatua madhubuti na za kimkakati ili kupunguza athari zinazotokana na mgogoro wa Ghuba kiuchumi na kwa wananchi.

Mhe. Mkumbo amesema hayo leo Mei, 22 jijini Dar es Salaam katika mjadala wa kitaalamu ulioandaliwa na Tume ya Taifa ya Mipango kwa kushirikiana na Umoja wa Mataifa UNDP kwa lengo la kujadili athari, uhimilivu na fursa zinazotokana na mgogoro huo.

Akitaja hatua hizo, Prof. Mkumbo amesema kuwa ni pamoja na kufuatilia kwa karibu bei na upatikanaji wa mafuta, chakula, mbolea na usafiri, kulinda kaya zilizo katika mazingira hatarishi, kuimarisha akiba na usambazaji wa biadhaa muhimu.

“tutahakikisha wananchi wanaendelea kupata chakula cha kutosha na mbolea kwa bei himilivu, vile vile tutaendelea kufanya uthibiti wa gharama za nishati, ikiwa ni pamoja na kutumia fursa za maliasili tulizonazo kama Gesi asilia, madini, utalii na fursa ya miundombinu ya usafiri kuimarisha uchumi wa taifa” amesema Prof. Mkumbo.

Hatua hizo, zinalenga kukabiliana na athari kama vile kupanda kwa bei ya mafuta, usafirishaji na mbolea kunakoweza kuathiri maisha ya wananchi, uzalishaji na bajeti ya Serikali, hivyo Serikali itaendelea kuchukua hatua za haraka ili kuwalinda.

Aidha, Mheshimiwa Waziri ameeleza kuwa pamoja na changamoto hizo, mgogoro huo wa Ghuba unatoa fursa ya kipekee ya kiuchumi kwa Tanzania na bara la Afrika kwa ujumla, hasa katika kuvutia uwekezaji mpya kwenye sekta ya nishati.

"Mgogoro huu unatoa mwanya mkubwa wa uwekezaji katika miundombinu ya mafuta, ikiwemo ujenzi wa viwanda vya kikanda vya kusafisha na kuchakata mafuta (regional refineries)," amesema Prof. Mkumbo.

Awali akimkaribisha Mhe. Waziri, Katibu Mkuu Ofisi ya Rais-Mipango na Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango Dkt. Tausi Kida alieleza kuwa mkutano huo unahusisha wadau wa maendeleo, sekta binafsi, asasi za kiraia, watafiti na taasisi za elimu ya juu kujadili hatua mbalimbali na afua zinazoweza kutumika ili kukabilia na athari za mgogoro huo.

Majadiliano hayo yalihudhuriwa na Mratibu Mkaazi wa Umoja wa Mataifa Bi. Susan Namondo na Mwakalishi Mkaazi wa Umoja wa Mtaifa, na Mwakilishi Mkazi wa UNDP Tanzania Bw. Shigeki Komatsubaram.