
.............
TUME ya Ushindani (FCC) imekutana na wadau wa uzalishaji wa ndani wa saruji kwa lengo la kujadili hali ya uzalishaji wa bidhaa hiyo pamoja na namna ya kulinda soko na maslahi ya mlaji.





.............
TUME ya Ushindani (FCC) imekutana na wadau wa uzalishaji wa ndani wa saruji kwa lengo la kujadili hali ya uzalishaji wa bidhaa hiyo pamoja na namna ya kulinda soko na maslahi ya mlaji.













Na OWM - TAMISEMI, Dodoma
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu Mhe. Selemani Kakoso ameipongeza Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini (TARURA) kwa kujenga miundombinu ya barabara iliyookoa maisha ya wananchi katika maeneo mbalimbali ambayo awali kuharibika kwa miundombinu hiyo kulisababisha vifo vya wananchi.
Mhe. Kakoso amesema hayo leo Februari 11, 2026 wakati wa kikao cha mafunzo kwa wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu, yaliyohusu uboreshaji wa Mtandao wa Barabara za Wilaya, Mikakati, Changamoto na Fursa kwa Maendeleo ya Taifa yaliyofanyika katika Ukumbi wa Anne Makinda Bungeni Jijini Dodoma.
Mhe. Kakoso amesema kuwa, katika jimbo lake kuna eneo ambalo TARURA imejenga daraja ambapo kila mwaka wananchi walikuwa wakipoteza maisha kutokana na kukosekana kwa daraja la uhakika, lakini tangu daraja hilo lijengwe hakuna taarifa za vifo tena.
“Katika Jimbo langu kuna sehemu ambayo toka nchi ipate uhuru haijawahi kuwa na barabara lakini TARURA imejenga barabara katika eneo hilo na sasa wananchi wananufaika nayo,” ameeleza Mhe. Kakoso.
Naye, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Florent Kyombo amesema licha ya Serikali kufanya vizuri katika ujenzi wa miundombinu ya barabara katika majiji, ameishauri TARURA kufanya mgao mzuri wa rasilimali fedha ili na maeneo mengine yenye uhitaji yanufaike na ujenzi wa miundombinu hiyo ya barabara.
Kwa upande wake, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu -TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amewahakikishia wajumbe wa kamati hizo kuwa, maoni yote yaliyowasilishwa na wajumbe wa kamati hizo yamepookelewa na yatafanyiwa kazi na wataalam ili kuongeza ufanisi katika ujenzi wa miundombinu ya barabara na hatimaye wananchi kunufaika na miundombinu hiyo.
Katika kukabiliana na majanga, Mtendeji Mkuu wa TARURA Mhandisi Victor Seff amesema kupitia dirisha la majanga (Crisis Management Window) Tanzania imeidhinishiwa mkopo wa nyongeza wa Dola za Kimarekani Milioni 100 kwa ajili ya kurejesha miundombinu iliyoharibiwa na mvua za elnino na kimbunga hidaya cha mwaka 2024, ambapo Dola Milioni 30 ni kwa ajili ya barabara za wilaya na Dola Milioni 70 ni kwa ajili ya barabara za kitaifa.
Na Munir Shemweta, WANMM ARUSHA
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo amewasisitiza wananchi wenye maeneo ya ardhi, kuhakikisha wanayaendeleza kabla serikali haijaanza kuchukua hatua.
Dkt. Akwilapo ametoa kauli hiyo leo tarehe 11 Februari 2026 wakati akifungua Kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) kinachoendelea jijini Arusha.
Akwilapo amesema kumekuwa na tabia kwa baadhi ya wananchi kununua maeneo ya ardhi na kuyahifadhi kwa muda mrefu kama mtaji kwa lengo la kupata faida baadaye.
"Bado natafakari nifanye nini maana sheria ipo, usipoendeleza eneo lako ndani ya miaka mitatu unaweza kunyang'anywa na wengi wanafanya ardhi kama mtaji. Nadhani kuna taasisi maalum za kukuza mitaji, kama vile Soko la Hisa la Dar es Salaa na UTT-AMIS, tumieni hizo taasisi. Huku ardhi tutapishana maneno". Amesema Dkt Akwilapo.
Sheria ya Ardhi Sura Namba 113 kifungu cha 49 inaeleza wazi kuwa mmiliki wa ardhi asiyeendeleza eneo lake katika kipindi cha miaka mitatu serikali inaweza kulichukua eneo lake kutokana na kushindwa kuliendeleza.
Kupitia kikao hicho cha Baraza la wafanyakazi, Mhe. Dkt Akwilapo amewataka waendelezaji milki nchini likiwemo Shirika la Nyumba la Taifa, kuhakikisha wananchi wanapata nyumba bora na za gharama nafuu ili watanzania waweze kuwa na tabasamu.
Amewaasa watumishi wa NHC kuzingatia utu, maadili, uwazi na uaminifu wakati wote wa kutekeleza majukumu yao huku wakiachana na ile dhana ya kuuliza watapata kitu gani ndani ya shirika na badala yake wajiulize watalifanyia nini shirika hilo.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Baraza la wafanyakazi la NHC ambaye pia ndiye Mkurugenzi Mkuu wa Shirika hilo, Bw. Hamad Abdallah amesema shirika lake limekuwa likifanya jitihada mbalimbali za kuhakikisha linaboresha maslahi ya watumishi.
Kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi cha Shirika la Nyumba la Taifa kilichoanza leo tarehe 11 Februari 2026 kinatarajiwa kuhitimishwa Alhamisi tarehe 12 Februari 2026. Kikao hicho pamoja na mambo mengine kinajadili Mizania na Bajeti ya NHC kwa mwaka wa fedha 2026/2027.
Katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha, Dk. Toba Alnason Nguvila, amewasistiza watumishi wa Umma kufanya kazi kwa kufuata Sheria, taratibu na kanuni kwa kuzingatia kiwango cha juu cha Maadili ya Utumishi wa Umma, ili kufikia lengo la Serikali la kuwahudumia wananchi.
Dkt.Nguvila ametoa wito huo, wakati akizungumza na baadhi ya watumishi wa Umma mkoa wa Arusha, kwenye hafla fupi ya mapokezi yake, iliyofanyika kwenye ukumbi wa Mikutano Ofisi ya Mkuu wa Mkoa huo, leo Februari 10, 2026, muda mfupi baada ya kupokelewa ofisini hapo, tayari kwa kuanza kutekeleza majukumu yake kwa washifa huo.
Amewasisitiza watumishi hao, kila mmoja kwa nafasi yake kuzingatia kuwa, mkoa huo ni mkoa wa Utalii hivyo wanalo jukumu la kuhakikisha wadau wa utalii wanafanya kazi kwenye mazingira rafiki, yasiyo na vikwazo vya aina yoyote huku akisisitiza kuto kuvumilia vikwazo vya kiutendaji wala urasimu unaokwamisha wawekezaji katika sekta ya utalii.
"Sisi watalamu tunapaswa kuwa kichocheo cha kuiimarisha sekta ya utalii, kwa kuwa kila wilaya ina vivutio vyake, hivyo si busara kwa baadhi ya watendaji kuweka urasimu usio wa lazima unaoweza kudhoofisha sekta hiyo, sitavumilia urasimu wala migogoro inayokwamisha wawekezaji katika sekta ya utalii". Amesema Dkt.Nguvila
Aidha, amewaagiza Wakurugenzi wa Halmashauri zote, kutenga bajeti ya kutekeleza shughuli za utalii kwenye maeneo yao, kubuni vyanzo vya mapato pamoja na kusimamia ukusanyaji wa mapato, ikiwa ni pamoja na kutoka maofisini na kuwafuata wananchi ili kubaini changamoto zao na kuzitatua kwa haraka.
Katika kutekeleza maelekezo ya Serikali, Dkt.Nguvila ameataka viongozi hao, kuwa na kampeni maalumu ya kutoa elimu na usajili sambamba na kuhamasisha wananchi kujiunga na mpango wa Bima ya Afya kwa wote, ili ili kufikia lengo la Serikali ya awamu ya sita ya kila mwananchi kujiunga na Bima hiyo, itakayowawezesha kupata huduma za matibabu wanapougua.
Awali, Dkt.Nguvila amemshukuru Mhe.Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kumuanini na kumteua kuwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha na ameahidi kushirikiana na watalamu wa ngazi zote katika kuwahudumi wananchi.