Na. Benny Mwaipaja, Dodoma
Na. Benny Mwaipaja, Dodoma
Waziri wa Nishati Mhe. Deogratius Ndejembi amewaagiza Watumishi wa Wizara hiyo kufanya kazi kwa bidii ili kutimiza Vipaumbele vya Serikali katika Sekta ya Nishati ikiwemo kufikia Megawati 8000 ifikapo 2030.
Mhe. Ndejembi ameyasema hayo tarehe 18 Novemba 2025 wakati akizungumza na watumishi wa Wizara mara baada ya kuwasili Katika Wizara Mji wa Serikali Mtumba Jijini Dodoma.
Amesema watumishi wa Wizara ya Nishati ndio watendaji wakuu na wenye dhamana ya kuhakikisha kwamba malengo ya Serikali yaliyowekwa yanatimia kwa kufanya kazi kwa bidii , kuwataka watumishi kuchambua kwa kina hotuba ya Mhe Rais ili kuweza kufikia vipaumbele kwa wakati na kuyoa huduma bora kwa wananchi wa Tanzania.
Pia amesisitiza watumishi kutumia siku mia moja za Mhe. Rais kama kipimo na kielelezo cha kutathmini uelekeo wa malengo ya Serikali.
“Sisi kama viongozi wenu tunategemea zaidi ushirikano kutoka kwenu ninyi wataalamu wa hapa Wizara ya Nishati ili tuweze kukamilisha Vipaumbele vya Mhe. Rais alivyoviweka katika sekta yetu kwasababu tunatakiwa tuanze kwa kukimbia na sio kutembea“ amesema Mhe. Ndejembi.
Nae Naibu Waziri wa Nishati Mhe. Salome Makamba amewataka watumishi kushirikiana kwa pamoja na viongozi wa Wizara hiyo ili kuendesha Sekta ya Nishati kwa pamoja, na kuongeza kuwa anatambua kwamba maswala mengi ya sekta ya Nishati yameshafanyika tayari mpaka sasa.
Amesema Serikali imeshafikisha Megawat 4000 za kiwango cha kuzalisha Umeme, hivyo ni jukumu letu kukamilisha miradi iliyokuwa inaendelea na kuongeza vyanzo vingine vya uzalishaji umeme ili kufikia megawati 8,000 ifikapo 2030.
Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati Mha. Felchesmi Mramba amewashukuru viongozi hao na amewataka watumishi wa Wizara ya Nishati kutoa ushirikiano kwa viongozi hao sambamba na kutekeleza majukumu yao kwa wakati ili kuweza kutekeleza Vipaumbele vya Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan ifikapo mwaka 2030.
Waziri wa Madini Anthony Mavunde amewataka Watumishi wa Wizara ya Madini na Taasisi zake kutambua kwamba maelekezo yaliyotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Hassan kuhusu kutumia fedha za ndani zinazotokana na rasilimali kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maendeleo ni agizo linaloigusa Wizara ya Madini moja kwa moja.
Ameyasema hayo Novemba 18, 2025 wakati akizungumza na Watumishi wa Wizara ya madini na taasisi zake Makao Makuu ya Wizara Mtumba, mapema baada ya kuapishwa Ikulu ya Chamwino Dodoma na Rais Dkt. Samia Hassan.
‘’Mapato ya ndani aliyoyaelekeza Mhe. Rais yanatugusa sisi Sekta ya Madini moja kwa moja. Dkt. Samia anataka uongozi unaogusa watu hivyo tuendelee kuongeza kasi. Lakini Katibu Mkuu nitapenda maelekezo aliyoyasema wakati akihutubia Bunge, haya ya leo na yale yaliyoahidiwa kwenye Ilani ya Uchaguzi yamfikie kila mtumishi,’’ amesisitiza Mavunde.
Mhe. Mavunde ameeleza kuwa Rais. Dkt.Samia Suluhu Hassan amekuwa na imani kubwa na Wizara ya Madini hususan kutokana na mapato yanayotokana na rasilimali madini kuendesha uchumi wa nchi na hivyo kumtaka kila mtumishi kutumia nafasi yake kuhakikisha sekta ya madini inagusa maisha ya kila mwananchi kwa manufaa ya jamii na taifa.
Akielezea kuhusu programu ya Mining for A Brighter Tommorrow (MBT), Mhe. Mavunde amesema kuwa mradi huo utatekelezwa kikamilifu kama ulivyopangwa kwa lengo la kuwawezesha wachimbaji vijana na wanawake kuchimba kwa tija. Kupitia mradi wa MBT Wizara imepanga kuwawezesha vijana na wanawake kwa kuwapatia maeneo ya kuchimba na teknolojia ili kuwarahisishia shughuli zao.
Pia, ametumia fursa hiyo kumshukuru Dkt. Samia kwa kumuamini na kumrejesha tena kuitumika wizara hiyo pamoja na kuwashukuru watumishi wote na wadau wote wa Sekta ya madini kwa ushirikiano mkubwa waliompatia katika kipindi cha miaka miwili aliyohudumu katika wizara hiyo na kueleza kwamba, kwake mlango uko wazi kwa ajili ya kupokea maoni na mapendekezo yanayojenga kwa lengo la kuendelea kuboresha Sekta ya Madini.
Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Madini Dkt. Steven Kiruswa Dkt. Kiruswa ameshukuru Rais Samia kwa kumuamini kuendelea kuhudumu katika Wizara ya Madini na kuwashukuru watendaji wote kwa ushirikiano waliompatia na kuwapongeza watumishi kwa kazi wanayofanya hususan kuendelea na ukusanyaji wa maduhuli ya Serikali.
‘’Mhe. Rais ametoa mwelekeo, hivyo tunapaswa kutekeleza yale tuliyoagizwa, tuliwaacha na mchango wa asilimia 10.1 matamanio ni kufikia asilimia 15 – 20 ifikapo mwaka 2030’’ amesema Dkt. Kiruswa.
Naye, Katibu Mkuu Wizara ya Madini Eng. Yahya Samamba amewapongeza viongozi hao kwa kuchaguliwa tena katika Wizara ya Madini na kuahidi kuendelea kuwapa ushirikiano wa utendaji kazi kuanzia ngazi ya chini mpaka juu.
Pamoja na mambo Kamishna wa Madini Dkt.AbdulRahman Mwanga kwa pamoja amewapongeza hao kwa kuchaguliwa tena na kuahidi ushirikiano
*#Vision 2030: Madini ni Maisha na Utajiri*
Na WAF, Dodoma
Waziri wa Afya, Mhe. Mohamed Mchengerwa, amewataka watendaji wa Wizara ya Afya kufanya kazi kwa bidii, weledi na uadilifu na kuacha kufanya kazi kwa mazoea ili kuleta tija na ufanisi kwa wananchi.
Mhe. Mchengerwa ametoa wito huo leo, Novemba 18, 2025, alipokutana na Menejimenti ya Wizara mara baada ya kuwasili rasmi kuanza majukumu yake mapya ya kazi kwenye wizara hiyo.
Amesema huu ni wakati wa watumishi kuongeza juhudi na kuto bweteka, ili kuendelea kusukuma maendeleo ya Sekta ya Afya mbele.
“Nawasisitiza watumishi wote kuacha kufanya kazi kwa mazoea Tubadilike na kutekeleza majukumu kwa ufanisi ili kuhakikisha Taifa letu linasonga mbele katika Sekta ya Afya,” amesema Mhe. Mchengerwa.
Aidha, Waziri Mchengerwa amewataka watumishi wote kufuata maadili ya kazi na kusimamia kwa umakini maelekezo yanayotolewa, ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora za afya.












.jpg)
.jpg)
.jpg)
.jpg)