Na Beatus Maganja


Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania - TAWA imepokea tuzo ya mshindi wa pili wa jumla kwenye maonesho ya 11 ya utalii na biashara almaarufu "TANGA TRADE FAIR" yaliyokuwa yakifanyika katika viwanja vya shule ya sekondari usagara Mkoani Tanga kuanzia Mei 28, 2024 mpaka Juni 06, 2024.

Sambamba na tuzo hiyo, TAWA pia imetunukiwa vyeti vitatu kwa ushindi na pongezi kwa kushiriki na kufanikisha maonesho hayo.

Tuzo na vyeti hivyo vilitolewa Juni 06, 2024 na Mkuu wa Mkoa wa Tanga Mhe. Dkt. Batilda Buriani ambaye alikuwa mgeni rasmi wakati wa hafla ya kuhitimisha maonesho hayo kwa Mwaka 2024 ambapo taasisi mbalimbali za Serikali na zisizo za Serikali zilishiriki.

Licha ya kujikusanyia tuzo na vyeti mbalimbali vya pongezi, TAWA pia imepongezwa kwa kufanikisha uwepo wa wanyamapori hai ambao walikuwa kivutio kikubwa na hamasa ya watu wengi kuhudhuria na kushiriki katika maonesho hayo.

TAWA imeshiriki kikamilifu maonesho hayo ya biashara na utalii yaliyokuwa na kauli mbiu *"Kufungua fursa za kiuchumi kupitia ushirikiano wa Sekta za Umma na Binafsi"* ikiwa ni utekelezaji wa mpango mkakati wa kuunga mkono jitihada za Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania za kukuza na kutangaza Utalii wa nchi yetu.


Aidha TAWA imetumia maonesho hayo kunadi fursa mbalimbali za utalii na uwekezaji zilizosheheni katika taasisi hiyo ikiwa ni pamoja na kutoa elimu ya uhifadhi kwa maelfu ya wananchi waliohudhuria katika maonesho hayo.

Share To:

OKULY BLOG

Post A Comment: