Na Imma Msumba ; Mbeya

Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa (NEC) Ndg. Ndele Mwaselela amesema kuwa ziara aliyoifanya kwa kata ishiri na mbili (22) za halmashauri ya wilaya ya Mbeya ipo kwa mjibu wa katiba ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na ni maelekezo ya vikaoa vya Halmashauri Kuu ya Taifa chini ya Mwenyekiti wa CCM Taifa Dkt.Samia Suluhu Hassan.

Mwaselela ametoa ufafanuzi huo leo tarehe 20 juni 2024 wakatika akizungumza na waandishi wa habari ofisi za CCM mkoa wa Mbeya, wakati akielezea mafanikio chanya ya ziara hiyo ambayo imefanyika kwa siku kumi ndani ya halmashauri ya Mbeya.

Amesema kwa mjibu wa katiba ya CCM ibara ya 97inaelekeza Mjumbe wa Halmashauri Kuu Taifa (M-NEC) kuwasilisha mbele ya kamati ya siasa taarifa ya kazi au ziara ambayo ameifanya na ndiyo kusudi la kufanyaa kazi ya ziara hiyo ya kusikiliza na kutatua kero za wananchi.

“Mhe. Rais ambaye ni Mwenyekiti wetu, ametupa maelekezo ya kututaka wasaidizi wake wote kuanzia wajumbe wa Halmashauri Kuu mpaka ngazi ya chini kwenda kusikiliza kero za wananchi na kuzitatua kwasababu kila mkoa kuna Serikali na ndiyo maana kwenye zaira hii niliambatana na watumishi wa Serikali idara zote” Mwaselela

Mwaselela amesema kuwa Serikali iliyopo madarakani ni ya CCM, ndiyo maana kamati ya siasa ya mkoa wa Mbeya ilikaa chini kukubaliana kuandaa ratiba ya kwamba Mwenyekiti wa CCM na M-NEC watakuwa na ziara ya kikazi ndani ya mwezi huu wa sita, lengo ni utekelezaji wa Ilani ya chama hicho na kuisimamia Serikali.  

“Ndugu Waandishi nimeona niwaeleze hayo ili kwenda kufafanulia umma na baadhi ya watu ambao hawafahamu majukumu ya M-NEC, mabadiliko ya katiba ya CCM ya mwaka 2022 imewapa nguvu Wajumbe wa Halmashauri Kuu taifa kusikiliza kero na kuzitatua, tofauti na kipindi cha hapo nyuma” Mwaselela.

Katika  mkutano huo na waandishi wa habari Mwaselela ameainisha mambo mbalimbali ambayo ni mafanikio ya ziara hiyo, ikiwa ni pamoja na wananchi kuishukuru serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa ya kusukuma maendeleo ya wananchi.

“Kwenye ziara hii kumekuwa na mafanikio makubwa sana, kwanza tumefahamu ni jinsi gani wananchi wanaimani kubwa na Mheshimiwa Rais na wanampenda kuliko kawaida, pili kumekuwa na msukumo mkubwa wa kumalizia baadhi ya miradi ya maendelea ambayo bado haijakalika na tatu wananchi walipata majibu ya serikali papo hapo kuhusu changamoto waliyoiwasilisha mbele ya mkutano wa hadhara” Mwaselela.

Aidha Mwaselela amesema bado kata kumi ili ahitimishe ziara kwa upande wa halmashauri ya Mbeya na baada ya hapo, atakwenda wilaya Chunya, Mbarali, Kyela, Rungwe, Busokelo na kumalizia halmashauri ya Jiji la Mbeya.

Share To:

Post A Comment: