Mkuu wa Mkoa wa Arusha Paul Makonda amekutana na kuzungumza na Wakuu wa Mikoa ya Mwanza Mhe. Said Mtanda na Mhe. Nurdin Babu na kujadiliana nao mambo Mbalimbali kuhusu Maendeleo ya Mikoa yao.

Viongozi hao waliofika mkoani Arusha kwa shughuli mbalimbali, wamesifu Maandalizi makubwa yaliyofanyika kuelekea maadhimisho ya siku ya wafanyakazi duniani yanayotarajiwa kufanyika Jumatano hii kwenye Viwanja vya Sheikh Amri Abeid Mjini Arusha.

Viongozi hao walioambatana na baadhi ya wasaidizi wao walipata fursa pia ya kujionea shughuli mbalimbali za sanaa zinazoendelea Mjini Arusha kama sehemu ya Shamra shamra za kuelekea kwenye Sherehe za Wafanyakazi.

Wakizungumza na Wananchi waliojitokeza kushuhudia maonesho mbalimbali ya sanaa kuelekea Mei Mosi, Mhe Mtanda amemtaja Mhe. Makonda kama Kiongozi wa Kupigiwa Mfano kutokana na Umahiri na Ubunifu wake katika Uongozi na namna anavyojitoa kushughulikia masuala ya wananchi.

Wakuu hao pia wamesifu namna ambavyo Arusha Imebadilika katika muda mfupi tangu kuteuliwa kwa Mhe. Makonda kuwa Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mwishoni mwa Mwezi Machi.

Shamrashamra Mbalimbali zinaendelea Mjini Arusha kuelekea sherehe za Mei Mosi suala ambalo limeamsha hisia za watu wengi wanaojitokeza kwenye Viunga vya Jiji la Arusha ili kujionea shughuli mbalimbali za sanaa kutoka kwa vikundi vya Ngoma, dansi na Kikundi cha vijana wa kucheza na Pikipiki Maarufu kama dede.















Share To:

Post A Comment: