Na. Gideon Gregory, Dodoma.
Waziri wa nchi ofisi ya Rais TAMISEMI Mohamed Mchengerwa amewaelekeza wakuu wa mikoa na makatibu tawala wa mikoa kuteua shule maalumu ambayo itakuwa nguzo ya kusambaza mifumo ya TEHAMA katika shule mbalimbali katika maeneo yao.

 

Mchengerwa ameyasema hayo leo Februari 7,2024Jijini Dodoma wakati akizindua mfumo wa ufundishaji mubashara kati ya Shule ya Sekondari Kibaha Mkoa wa Pwani na Shule ya Sekondari ambapo amesema kuwa mfumo huo utaenda kutatua changamoto ya uhaba wa walimu kwa baadhi ya shule nchini.

 

“Hakikisheni Kila mkoa lazima Mteue shule kama walivyofanya hapa Dodoma, na kwa Mkoa wa Pwani kama walivyofanya kule Kibaha, na wakuu wa mikoa mingine waanze kuteua shule moja ambayo itakuwa nguzo katika shule mikoa husika kwenda kulitekeleza mara moja,”amesema

 

Waziri Mchengerwa amesema kuwa uanzishwaji mfumo huo ni moja ya jitihada za serikali ya awamu ya sita chini ya ungozi wa Rais Samia wa kwenda kupunguza uhaba wa walimu nchini.

 

“Ufundishaji mubashara utasaidia katika kupunguza changamoto ya uhaba wa walimu na kuongeza ufahamu na maarifa kwa wanafunzi wanaosoma katika shule mbalimbali katika ngazi ya awali, msingi na sekondari.”amesema Mhe.Mchengerwa.

 

Kwa upande wao walimu wa shule ya sekondari Dodoma wameipongeza serikali kwa kubuni mfumo huo na kuongeza kuwa utaenda kuwapungizia mzigo wa kumaliza mada.

 

Nao baadhi ya wanafunzi wa shule hiyo wamesema kuwa mfumo huo unaenda kuwaongezea wigo mpana wa kujifunza zaidi hasa kwa vitendo tofauti na ilivyokuwa hapo awali pia utawaongezea maarifa ya kujifunza vitu vingi kutoka kwa wanafunzi wenzao kwa njia ya kidigitali.

Share To:

Post A Comment: