Kamati ya Siasa ya Chama cha Mapinduzi Mkoa wa Arusha ikiongozwa na Mwenyekiti wake Thomas Loy Sabaya imeendelea na ziara yake ya kukagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo wilayani Monduli ambapo imekagua baadhi shule mpya zilizojengwa kupitia mradi wa Boost.
Kamati hiyo imekagua ujenzi wa shule mpya ya msingi Emairete ulioigharimu serikali zaidi ya shilingi milioni 480 ambao umetajwa kupunguza utoro kwa wanafunzi wa jamii ya kifugaji wilayani Monduli  kutokana na kuondoa adha ya kutembea umbali mrefu hali iliyokuwa moja ya sababu zilizosababisha wanafunzi hao wakatize masomo.
Amani Laizer ni mkazi wa Kijiji cha Emairete katika Kata ya Monduli juu ambapo anaeleza kuwa ujenzi wa shule hiyo umeondoa hatari kubwa ya wanafunzi hao kusombwa na maji nyakati za masika kutokana na jigrafia ya eneo hilo kuwa na makororngo makubwa ya kupitisha maji.
“Watoto walikuwa wanatembea zaidi ya kilomita saba maana kuna baadhi ya mito ambayo maji yalikuwa yanakwama na watoto walikuwa hawawezi kupita ila sasa tumejengewa shule ipo karibu,ila tunawapongeza serikali kwa ujenzi nzuri wa majengo ya kisasa hakika sisi kama wananchi tutakwenda kuhakikisha watoto wetu wanayatunza vyema” Aliongezea laizer
Ikumbukwe idadi kubwa ya wakazi wa wilaya ya Monduli ni jamii ya kifugaji wa kabila la kimasai waliokuwa wakikabiliwa na tatizo la utoro mashuleni kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo masuala ya kijiografia yaliyowafanya wanafunzi hao kutofika mashuleni.
Share To:

Post A Comment: