Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (LAAC) imesikitishwa na kutotumika kwa majengo ya Hospitali ya Manispaa ya Bukoba kutokana na kukosa usajili.

 

Kauli hiyo imetolewa na Makamu Mwenyekiti wa Kamati, Mheshimiwa Stansalau Mabula wakati Kamati hiyo ilipotembelea na kukagua mradi wa ujenzi wa hospitali hiyo.

 

Alisema licha ya kwamba majengo manne kati ya sita yamekamalika tangu mwaka 2021 lakini majengo hayo hadi sasa hayajaanza kutumika kutokana na kuchelewa kuomba usajili kutoka Zahanati kuwa Hospitali ya Wilaya.

 

“Kamati  hii inakagua thamani ya fedha na kuona kama imefanya kazi iliyokusudiwa, lakini kama majengo yamekamilika lakini hayatumiki thamani yake bado haionekani,” alisema.

 

Alisema kwa tathimini iliyofanywa na Kamati mpaka sasa majengo hayo yanatumika kwa asilimia 10 tu ya malengo yalikusudiwa ya kujenga hospitali hiyo.

 

“Miaka mitatu nyuma mliomba fedha mletewe hospitali ya wilaya, lakini pamoja na kumaliza majengo toka mwaka 2021, mwaka jana Desemba ndio mlipeleka maombi ya kusajili Hospitali ya Wilaya kutoka kwenye zahanati.

 

“Vifaa vimepelekwa na MSD (Bohari ya Dawa), tunajisikiaje kama hatutavitumia kwa wakati, vitaharibika, wiki mbili zijazo wataleta vingine vyenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 400, vitaharibika,” alisema

 

Aliutaka watendaji wa Manispaa hiyo wawe na uchungu na fedha za Serikali zinazopelekwa kwa ajili ya kuweka miundombinu na kuwawapelekea wananchi  huduma bora. 

 

Aidha, kamati iliagiza kufanyika marekebisho iliyoyainisha katika majengo ya hospitali hiyo ikiwemo sakafu hasa katika chumba cha upasuaji.

 




Share To:

Post A Comment: