Mwenge wa Uhuru kitaifa-2023 umetembelea na kukagua Uhifadhi wa chanzo cha maji cha Ivumwe Wilaya ya Mbeya Mjini ambapo chanzo hicho kina uwezo wa kuzalisha maji lita milioni 29 kwa siku.


Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa- 2023 ameipongeza Bodi ya maji ya Bonde la Ziwa Rukwa kwa kuendelea kulinda na kuhifadhi chanzo hicho kwa upandaji wa miti 490 ambayo ni rafiki wa Mazingira.

Kwa upande Mheshimiwa Mhandisi Maryprisca Mahundi(Mb), Naibu Waziri wa Maji amesisitiza kuwa wakazi wa Kata ya Mwaikibete waendelea kutunza na kulinda chanzo cha maji pamoja na Mazingira kwa ujumla ili kuhakikisha huduma ya maji inakuwa endelevu.

Pia, Mhe. Mahundi ameendelea kusema kuwa katika kuboresha huduma ya maji kwenye jiji la Mbeya, Serikali kwa mwaka huu wa fedha inaendelea na utekelezaji wa mradi wa maji wa Mto Kiwira kwa gharama ya shilingi bilioni 117 ambapo mpaka sasa shilingi Bilioni 14.9 zimetolewa ikiwa ni malipo ya awali ya Mkandarasi. Kazi zinazoendelea ni ujenzi wa kambi ya Mkandarasi na usanifu wa kina wa mradi

Naye,Mbunge wa Jimbo la Mbeya Mjini na Spika wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt Tulia Ackson ameishukru Serikali kwa utekelezaji wa miradi ya maji ndani Jiji la Mbeya ukiwemo mradi wa maji wa Mto Kiwira. Aidha Spika wa Bunge amesema kuwa Chanzo cha Maji cha Ivumwe kinatumika kwa ajili ya usambazaji maji kwa wakazi wa mitaa ya Forest mpya, forest ya Zamani, Mwanjelwa, old airport, Iyela, Iyunga, Iwambi, Viwanda vya Coca-Cola, Veta pamoja na mtaa wa Nanenane.


Share To:

Post A Comment: