Naibu Waziri TAMISEMI Mhe. Deo Ndejembi amesema katika mwaka wa fedha 2021/22, TARURA ilitenga jumla ya kiasi cha Shilingi Milioni 200 kwa ajili ya kuchonga na kuweka barabara kwa kiwango cha Changarawe yenye urefu wa kilomita 2.7, kujenga makalavati 9, mifereji yenye urefu wa kilomita 1.9 katika mji wa Mombo wilayani Korogwe mkoani Tanga.

Ndejembi ameeleza hayo leo Juni 14, 2023 Bungeni Jijini Dodoma wakati akijibu swali la Mheshimiwa Timotheo Paul Mzava Mbunge wa Jimbo la Korongwe vijijini aliyetaka kujua ni lini serikali itatekeleza ahadi zake za kujenga barabara za lami katika mji wa mombo.

‘‘katika mwaka wa fedha 2022/23 Serikali imetenga jumla ya shilingi milioni 400 kwaajili ya kurengeneza barabara yenye urefu wa kilometa 2.84 kwa kiwango cha changarawe ujenzi wa makalavati  23 na ujenzi wa mifereji urefu wa kilometa 2.46 na utekelezaji wa kazi hizi unaendelea na umefikia asilimia 56’’amesema Ndejembi.

‘Barabara za Mombo Mjini zitaanza kujengwa kwa kiwango cha lami mara baada ya kuziimarisha kwa kiwango cha changarawe na ujenzi wa mifereji kulingana na upatikanaji wa fedha’ aliongezea Ndejembi.

Aidha, amesema Serikali itaendelea kuipa kipaumbele barabara hiyo na kuendelea kutekeleza ahadi hii lakini pia kutafuta fedha kwa mwaka wa fedha 2023/2024 unaoanza mwezi Julai.

Mji Mdogo wa Mombo una barabara zenye urefu wa jumla ya kilomita 28.4. Kati ya hizo kilomita 0.45 ni tabaka la lami, changarawe kilomita 5 na udongo kilomita 22.95.

TARURA imeendelea kutenga fedha za matengenezo ya sehemu korofi na matengenezo ya muda maalum kwa barabara za Mombo Mjini ili kuhakikisha barabara hizi zinapitika majira yote ya mwaka.

Share To:

Post A Comment: