RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan, akizungumza kwenye maadhimisho ya sherehe za Mei Mosi Kitaifa 2023 Mjini Morogoro.


Na Mwandishi Wetu, Morogoro


RAIS Samia Suluhu Hassan, ameagiza Waajiri kuwasilisha michango ya wafanyakazi kwenye mifuko ya hifadhi ya jamii mara moja ili wapate stahiki na haki zao.


Akihutubia kwenye maadhimisho ya sherehe za Mei Mosi Kitaifa 2023 Mjini Morogoro, Rais Samia amemuagiza Waziri Mkuu Kassim Majaliwa kushughulikia suala la waajiri wa kutopeleka michango katika mifuko ya jamii na michango ya bima za afya ya wafanyakazi wao.


“Waziri Mkuu amesema akitoka hapa anaenda kuitisha mkutano wa waajiri lazima walie michango ya wafanyakazi hasa wale ambao serikali imewapa wao hawawasilishi …Malimbikizo yote ya bima ya afya yalipwe ndani ya siku 60 kama kuna mtu analimbikiza alipe ndani ya siku 60 ziwe zimelipwa waajiriwa waweze kupata haki zao,”amesisitiza Rais Samia.


Aidha, Rais Samia amerudisha nyongeza za mshahara za kila mwaka ambazo zilikuwa zimesitishwa kwa muda mrefu.


“Lakini niseme pia kuna nyongeza za mishahara ambazo muda mrefu zilisitishwa, nimeona mwaka huu tuzirudishe. Kwa hiyo wafanyakazi wote mwaka huu nyongeza za kila mwaka zitakuwepo na itakuwa hivyo kila mwaka, nashukuru TUCTA mwaka huu wamenielewa hawakuja na mdomo mkali unaotoa moto mara hii wamekuwa wapole, kutokana na yaliyofanyika,”amesema.


Kadhalika, Rais Samia amesema serikali kwa mwaka 2022/23 imeendelea kuimarisha Wakala wa Usalama na Afya Mahala pa Kazi (OSHA) kwa kuongeza wafanyakazi 18 na kununua magari 13 huku Idara ya Kazi chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu yamenunuliwa magari 17 na mchakato wa kuongeza wafanyakazi unaendelea ili taasisi hizo zifanye kazi kwa ufanisi.

Share To:

OKULY BLOG

Post A Comment: