Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Juma Homera ameagiza kukamatwa mara moja wa Askari wa TANAPA waliohusika kuwapiga wananchi wa Kata ya Imalilo Mkuu huyo wa mkoa amefika na kuzungumza na Wananchi juu ya tukio hilo ambapo baada ya kuwasikiliza Wananchi RC Homera amelaani vikali kitendo kilichofanywa na Askari hao na ameliagiza Jeshi la Polisi kuwakamata ndani ya saa 24 na kuwatia mbaroni Askari hao waliohusika.

Homera amesema Serikali haijawahi kumtuma Askari kupiga au kunyanyasa Raia bali jukumu la Askari ni kulinda Raia na mali zake. 

"Wale wannachi wote ambao walijeruhiwa kwa kupigwa na Askari hawa wa TANAPA Serikali imewapa mkono wa pole wa shilingi milioni moja kwa kila mwananchi aliyejeruhiwa " Alisema Homera

Kwa upande wake Waziri wa Maliasili na Utalii Mohamed Mchengerwa amekabidhi Tsh. milioni tano kwa ajili ya Wananchi watano wa Kijiji cha Mwanavala Kata ya Imalilo Songwe Wilaya ya Mbarali Mkoani Mbeya kama pole baada ya kujeruhiwa na Askari wa TANAPA May 6,2023.

Sambamba na hilo Waziri Mchengerwa amemuagiza pia Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii kuwachukulia hatua za kinidhamu Askari wote waliohusika na tukio hilo.

Askari wanne tayari wamekamatwa kuhusiana na tukio hili uchunguzi ukikamilka watafikishwa Mahakamani.

 Swala hili liliibuka Bungeni mara baada ya Mbunge wa Jimbo la Mbarali Fransis Mtega kutaka bunge kusitisha shughuli zake na kujadili hoja ya dharura juu ya Wananchi kupigwa na Askari wa TANAPA, hoja ambayo ilimfanya Waziri Mkuu Kasimu Majaliwa kuiagiza Wizara ya Maliasili na Utalii kufika eneo husika mara moja na kushughulikia tatizo hilo.
Share To:

Post A Comment: