Na Mathias Canal, Ikungi-Singida


Mbunge wa Jimbo la Singida Mashariki Mhe. Miraji Mtaturu amesema serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt Samia Suluhu Hassan inaendelea kuboresha Miundombinu mbalimbali kwenye shule ya Msingi Ikungi Mchanganyiko ili kurahisisha ujifunzaji na ufundishaji kwa watoto wenye mahitaji maalum ili kuweza kuongeza kiwango cha elimu.

Mbunge Mtaturu amesema hayo April 16, 2023 wakati akizungumza na watoto wenye mahitaji Maalumu baada ya kukagua miradi ya ujenzi wa Bwalo la chakula, Mabweni Mawili ya Wasichana na Wavulana katika shule ya msingi mchanganyiko Ikungi ambapo serikali ya Rais Dkt. Samia imepeleka fedha Shilingi Milioni 300 kwa ajili ya ujenzi wa miradi hiyo.

Mtaturu aliihakikishia kamati ya shule pamoja na walimu wa shule hiyo kuwa kupitia ofisi yake ataendelea kutatua changamoto mbalimbali kwa makundi yenye uhitaji ili kuboresha upatikanaji wa elimu kwa watoto hao.

“Nimshukuru Rais Samia ametuletea Milioni 300 kwaajili ya miradi ya ujenzi wa bwalo na Mabweni na nimekagua yamejengwa vizuri kwa hiyo niwahakikishie kuwa serikali itaendelea kuboresha mazingira ya kujifunzia na ufundishaji kwenye shule zenye watoto wenye mahitaji Maalum ikiwemo hii Ikungi Mchanganyiko ambayo hata mimi nilisoma hapa”Alisema Mtaturu.


Ameongeza kuwa ili kuwa na elimu bora ni vyema idadi ya wanafunzi ipungue kwenye shule hiyo ya Ikungi Mchanganyiko ambapo amesema kuwa ujenzi wa shule ya Mbwanjiki utasaidia kupunguza idadi hiyo jambo ambalo litasaidia kutoa elimu bora na yenye tija.


Naye Mwalimu Mkuu wa shule hiyo Rachel Maliwa ameishukuru Serikali kwa kutenga fedha kwaajili ya ujenzi wa bwalo na mabweni ya wanafunzi hao ambapo amesema kuwa itawasaidia watoto hao ambao wanansoma katika shule ya msingi Mchanganyiko kuishi katika mazingira Mazuri wawapo shuleni.


Kwa upande Mwingine Mwalimu Manase Lingula alimuomba Mbunge Mtaturu kuwasemea bungeni juu ya mafunzo kwa walimu wenye ulemavu hasa wasioona ili yawarahisishie katika kuwafundisha watoto wenye mahitaji maalum katika shule hiyo.


Share To:

Post A Comment: