Mkurugenzi wa VETA Kanda ya Kati Dodoma, John Mwanja akitoa taarifa kwa Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Daniel Chongolo (wa pili kushoto) kuhusu ujenzi wa Chuo cha Ufundi Stadi Veta Wilaya ya Ikungi mkoani Singida wakati wa ziara yake ya kikazi ya kutembelea miradi ya maendeleo aliyoifanya Februari 28, 2023. 

Na Dotto Mwaibale, Singida

MKURUGENZI Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi, Justice Kijazi amesema moja ya mafanikio makubwa waliyoyapata katika kipindi cha miaka miwili tangu aingie madarakani Rais Samia Suluhu Hassan ni ujenzi wa Chuo cha Ufundi Stadi cha Veta na akatumia nafasi hiyo kuwapongeza Veta Kanda ya Kati kwa ujenzi wa viwango vya hali ya  juu wa chuo hicho wilayani humo.

Kijazi alizungumza hayo mwishoni mwa wiki wakati wa utoaji wa taarifa ya mafanikio ya Serikali ya Awamu ya Sita katika kipindi cha miaka miwili tangia aingie madarakani Rais Samia Suluhu Hassan na kumpongeza kwa mambo makubwa ya maendeleo yaliyofanyika katika wilaya hiyo na mkoa wa Singida kwa ujumla.

Kijazi alisema ujenzi wa chuo hicho ni fahari kwa wilaya hiyo kwani kitaanza kutoa mafunzo ya ufundi wa aina mbalimbali kwa vijana wa wilaya hiyo na za jirani jambo ambalo litawasaidia kujiajiri na kuajiriwa katika maeneo tofauti kulingana na fani zao za ufundi watakazo kuwa wamejifunza.

"Tulikuwa na changamoto kubwa ya vijana wetu wanaomaliza elimu ya msingi na sekondari kwenda kupata elimu ya ufundi nje ya wilaya yetu lakini kukamilika kwa ujenzi wa chuo cha Veta hapa Ikungi kunakwenda kuondoa changamoto hiyo," alisema Kijazi.

Kijazi alisema anampongeza Rais Samia kwa kutoa fedha nyingi kwa ajili ya ujenzi wa chuo hicho ambacho kitakuwa mkombozi kwa wana Ikungi na wilaya jirani ambacho kimejengwa na Veta Kanda ya Kati Dodoma.

Mkurugenzi wa VETA Kanda ya Kati John Mwanja akizungumzia ujenzi wa chuo hicho alisema Chuo cha Ufundi Stadi cha Wilaya ya Ikungi chenye umiliki wa Hati namba: 2218- SGD  kimejengwa  katika  Kijiji  cha Muungano,Kata  ya Unyahati  wilayani  Ikungi  katika  mkoa  wa Singida kwenye eneo lenye ukubwa wa ekari 50.

Alisema Mradi huo  ulianza mnamo mwezi Machi, 2020 ukisimamiwa na chuo cha VETA Singida na ulipaswa kutekelezwa kwa muda wa miezi sita hata hivyo, haukuweza kukamilika kwa wakati kutokana na changamoto kadhaa zilizojitokeza na baadaye mradi kusimama kwa muda wa mwaka mmoja.

Alisema Mkurugenzi Mkuu wa VETA Februari 28/2022 alihamishia majukumu ya usimamizi wa Ujenzi wa chuo hicho  kutoka Chuo cha VETA Singida kwenda ofisi ya  Mkurugenzi wa VETA Kanda ya kati ambaye hadi sasa ndiye anaendelea na usimamizi wa ujenzi huo ambao unatekelezwa kwa  mfumo wa “Force Account”.

Akizungumzia utekelezaji wa ujenzi huo alisema unahusisha jumla ya majengo 17 ambayo ni Jengo moja la utawala, Majengo manne  ya karakana, jengo moja la madarasa mawili makubwa, majengo mawili  ya mabweni  (Wasichana na Wavulana), Bwalo la chakula na Jiko, Majengo Matatu  ya vyoo (Wasichana Wavulana  na  Watumishi),  nyumba  mbili  (2)  za  watumishi,  jengo  la  umeme,  Jengo  la  bohari  na kibanda cha mlinzi. Kwa wastani hatua ya ujenzi hadi sasa imefikia asilimia 96%.

Alisema  chuo kitakapokamilika, kitaendesha mafunzo ya kozi ndefu na fupi na kuwa ya muda mrefu yatachukua muda wa miaka miwili hadi mitatu ambayo  yatatolewa katika fani zipatazo sita katika awamu ya kwanza mara chuo kitakapokamilika ambazo ni Uhazili na Kompyuta (Secretarial and Computer Application), Ushonaji (Design Sewing and Cloth Technology), Uashi (Masonry and Bricklaying), Umeme wa Majumbani (Electrical Installation), Ufundi Magari (Motor Vehicle Mechanics) na Uchomeleaji Vyuma (Welding and Metal Fabrication). 

Alisema chuo  kitakuwa  na  uwezo  wa  kudahili  wanafunzi  240  wa  kozi  ndefu  na  uwezo  wa  kuchukua wanafunzi 144 wa bweni  (wasichana 64 na wavulana 80).

Alisema pia, kutakuwa na mafunzo ya muda mfupi (Short Courses) yatakayochukua muda wa mwezi mmoja hadi miezi sita (6); kwa wastani mafunzo hayo yanakadiriwa kudahili wanafunzi wapatao 250 hadi 900 kwa mwaka kutegemeana na mahitaji ya jamii na shughuli za kiuchumi za eneo hilo.

  Mwanja, alisema ujenzi wa chuo hicho ulianza katika bajeti ya 2019/2020 ambapo hadi sasa Sh.bilioni 2.3 zimeshatumika katika ujenzi huo ambao utakamilika Aprili mwaka huu.

Mwanja alisema Serikali imetoa Sh.milioni 259 ili kukamilisha ujenzi wa chuo hicho na kwamba kitaanza kutoa mafunzo ya kozi ndefu kwa wanafunzi 240 na wa kozi fupi kati wanafunzi 250 hadi 900 kwa mwaka.

Alisema faida ya chuo hicho mara kitakapokamilika kinatarajiwa kuhudumia wakazi wapatao 343,985 wa Wilaya ya Ikungi na wakazi wapatao  1,754,370  wa Mkoa  wa  Singida.

Alisema katika kutekeleza mradi huo VETA imekumbana na changamoto mbali mbali kama kupanda  kwa bei  ya  vifaa vya  ujenzi  wakati wakiendelea  na  utekelezaji wa  mradi,  hali iliyopelekea  pesa iliyotengwa  kutokidhi  mahitaji halisi  ya  mradi kutokana  na  bei za  vifaa kupanda zaidi ya matarajio ya awali.

Alitaja changamoto nyingine waliyokumbana nayo ni uwezo mdogo wa kiuchumi wa mafundi waliowatumia hivyo kupelekea kushindwa kuwalipa vibarua wao kwa wakati na kupelekea baadhi yao kuacha kazi, hivyo kupelekea kuchelewa kwa utekelezaji wa mradi.

Mwanja alitumia nafasi hiyo kutoa shukrani za dhati kwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuimarisha mafunzo ya ufundi stadi nchini kwa kutoa fedha za miradi ya maendeleo ikiwemo ujenzi wa vyuo vipya vya Veta na uboreshaji wa vyuo vya zamani na kuwa wao wakiwa na dhamana ya kusimamia Veta wataendelea kuunga mkono jitihada za Serikali na kuhakikisha Veta inakuwa juu siku zote kwa kutoa mafunzo bora na sio bora mafunzo kwa mustakabari wa Taifa la Tanzania.        

Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Daniel Chongolo, akiwa katika ziara yake ya kikazi mkoani hapa hivi karibuni alihimiza vijana kujiunga na vyuo vya ufundi ili kupata mafunzo ya ufundi yatakayo wasaidia kupata ajira pamoja na kujiajiri na aliiomba Veta ianze kutoa mafunzo hayo ya ufundi kuanzia shule za sekondari lengo likiwa ni kuwaanda kujua umuhimu wa ufundi na faida zake.

Alisema lengo la Serikali ni kujenga vyuo vya Veta katika kila wilaya hapa nchini na kuwa katika miaka mitatu mfululizo imekuwa ikitoa mafunzo hayo bure ambapo aliiomba Veta kujikita zaidi katika uhamasishaji wa vijana kujiunga katika vyuo hivyo.

Aidha Chongolo alihimiza  kila mtu kujifunza walau fani moja ya ufundi bila kujali elimu aliyonayo ambayo haimzuii mtu kuwa na ujuzi mwingine akijitolea mfano yeye ambaye ni fundi mahiri wa kuchomelea vyuma lakini sasa ni Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM)

           Muonekano wa baadhi ya majengo ya Chuo cha Ufundi Veta Wilaya ya Ikungi.    

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauriya Wilaya ya Ikungi, Justice Kijazi (kushoto) akitoa taarifa ya wilaya hiyo ya mafanikio ya kipindi cha miaka miwili ya Rais Samia tangu aingie madarakani.  

Share To:

dotto mwaibale

Post A Comment: