Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Adolf Mkenda ameishukuru Serikali ya Finland kwa namna ambavyo imekuwa ikishirikiana na Serikali ya Tanzania katika kuendeleza sekta ya elimu, Sayansi na Teknolojia hususan ushirikiano kati ya Vyuo Vikuu vikuu na ufadhili wa miradi kupitia Taasisi.

Waziri Mkenda ameeleza hayo jijini Dodoma alipokutana na Waziri wa Finland anaeshughulikia masuala ya Uchumi Mhe. Mika Lintila na ujumbe wake.

Amesema kwa sasa nchi ya Tanzania inafanya mapitio ya Sera ya elimu ya mwaka 2014 na mabadiliko ya mitaala kwa kuhakikisha elimu inatoa ujuzi bila kuathiri ubora katika taaluma.

” Finland mnafanya vizuri sana kwenye elimu ninaomba ushirikiano uliopo uendelee hasa katika kipindi hiki ambacho tunafanya mabadiliko makubwa ya mfumo wa elimu,” amesema Mkenda

Amesema Serikali pia inaweka utaratibu wa kuwezesha watanzania wengi kwenda kusoma katika vyuo vya nje ikiwemo Sweden ili kupata uzoefu zaidi.

Kwa upande wake Waziri Mika Lintila amemuhakikishia Waziri Mkenda kuwa ushirikiano wa muda mrefu baina Tanzania na Finland tangu mwaka 1962 utaendelea na kwakuwa uchumi unategemea sana elimu hivyo umuhimu wa kushirikiana katika eneo hili pamoja na teknolojia upo na utaendelea.

Share To:

Post A Comment: