Mheshimiwa Ridhiwani Kikwete akifurahia michango ya wakazi hao

Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Makazi na MBUNGE wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete amewataka wananchi wa Jimbo hilo kujikita kwenye kilimo cha pamba ambacho kitawakwamua kiuchumi.

Ametoa rai hiyo alipokuwa akizungumza na wakazi wa Vijiji vya  Kilemela, Hondogo na Lupungwi katika kata ya Mandera ambapo alisema ni wakati sasa wananchi kuona umuhimu wa zao hilo la biashara.

"Siwaambii mkatoe mihogo mliyopanda shambani ili mlime pamba, ila nawashauri kufufua kilimo cha zao hili ambacho kitawasaidia kuinuka kiuchumi kutokana na uboreshaji wa mazingira ya soko ulivyo sasa" amesema.

Kikwete amesema miaka ya nyuma zao hilo lilikuwa likilimwa kwa wingi katika kata hiyo na maeneo mengine ya Halmashauri ya Chalinze na baadae mwamko ulipingua kutokana na soko na kwakua sasa mazingira yameboreshwa ni vema kulima zao hilo ambalo litawainua kiuchumi.

Awali Ofisa kilimo wa Halmashauri ya Chalinze Jovin Bararata alisema mbegu ya zao hilo, pembejeo  na dawa zinatolewa bure huku mbolea ikitolewa kwa ruzuku na mazingira ya soko yameboreshwa kutokana kuwepo kwa kiwanda cha uchakataji katika Kata ya Mandera.

Bararata amesema ni vema wananchi wakachangamkia fursa ya uwepo wa kiwanda hicho badala ya kuwaachia wakulima kutoka mikoa mingine.

Ofisa kilimo huyo amewashauri wakulima kuzingatia kuwatumia Maofisa ugani  kwa ushauri wa kilimo ili walime kwa kufuata kanuni za kilimo na kupata mafuno mengi.

Katika hatua nyingine Kikwete amewaelekeza wataalamu kuhakikisha wanasimamia utekelezaji wa miradi kwa weledi ili fedha zinazotengwa zikamalize vikwazo kwa wananchi.
Share To:

Post A Comment: