Na John Walter-Manyara

Mkuu wa Mkoa wa Manyara Makongoro Nyerere amezindua zoezi la  upandaji miti mkoani hapa huku akiagiza kila Mwananchi kuhakikisha anapanda mti na kuutunza katika eneo lake.

Amewataka wakuu wa wilaya, wakurugenzi pamoja na wakuu wa idara za mazingira kila mmoja kuhakikisha miti inapandwa kama muongozo unavyoelekeza.

Nyerere ameyasema hayo  leo Januari 27,2023 wakati akizindua  zoezi la upandaji wa miti katika kitongoji cha Sumbi, kijiji cha Nakwa kata ya Bagara Halmashauri ya mji wa Babati.

Mkuu wa mkoa amesema kuwa mkoa huo utaendelea kusimamia vyema Jitihada  za Serikali katika kutunza mazingira na kuweka msisitizo wa uhifadhi wa mazingira kwa wnanchi wote ili kuendelea kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabia nchi.

Pia ameeleza kuwa Serikali mkoani humo kwa kushirikiana na wadau mbalimbali imeendelea kuhamasisha upandaji miti kwa kupanda katika maeneo ya ofisi za Umma kama shule, hospitali, vituo vya afya na zahanati.

Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais na Ofisi ya Rais, TAMISEMI imeendelea kuratibu utekelezaji wa kampeni ya kitaifa ya upandaji na utunzaji wa miti inayotekelezwa nchini ambapo  kila Halmashauri inapaswa kupanda miti milioni 1.5 kila mwaka.

Kaulimbiu ya mwaka huu inasema Mazingira yetu, Tanzania Yetu, Nitaipenda daima" kauli hiyo inatabananisha kuwa uzuri wa nchi ni sambamba na kupanda miti na kutunza mazingira kwa ujumla.
Share To:

Post A Comment: