Na John Walter-Manyara

Mkuu wa Wilaya ya Babati Lazaro Twange kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Manyara Charles Makongoro Nyerere   amekabidhi zawadi mbalimbali za Krismasi  zilizotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan katika Kituo cha kulelea watoto yatima na waishio katika mazingira magumu cha Manyara Holistic Center (MAHOCE)  kilichopo kata ya Bagara Mjini Babati.

Zawadi zilizokabidhiwa kutoka kwa Mhe.Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan kituoni hapo  ni pamoja na Kilo 100 za Mchele, Mbuzi wawili, Maharage, Mafuta ya kupikia, viungo vya kupikia, pamoja na vitu vingine ambavyo jumla yake ni shilingi Milioni moja.

Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa, Mkuu wa Wilaya ya Babati, amemshukuru Mhe.Rais Dkt Samia Suluhu Hassan  kwa msaada huo alioutoa kwa watoto hao  huku akiwakumbusha wengine wenye mapenzi mema kuwakumbuka watu wenye mahitaji.

Kwa Upande wake afisa Maendeleo wa kituo Felista Massay  amemshukuru Rais Dkt.Samia pamoja na uongozi wa Mkoa wa Manyara kwa kutambua umuhimu wa kutoa msaada huo kwa watoto hao na ametoa wito kwa Jamii kujumuika kuiga Mfano wa viongozi kujumuka na watoto hao kwa kuwasaidia katika mahitaji mbalimbali.

Amesema kituo kinahudumia watoto 85 ambao wanasoma katika shule za Msingi, Sekondari, vyuo vya kati, vyuo vya ufundi stadi na vyuo vikuu.

Share To:

Post A Comment: