WAKUU wa Wilaya na Wakurugenzi wa
halmashauri zote saba za mkoa wa Singida wamesaini mikataba maalum kwa ajili ya
kushughulikia kikamilifu suala la kuboresha lishe katika maeneo yao ikiwa ni
utekelezaji wa Agizo la Rais Samia Suluhu Hassan alilolitoa hivi karibuni
Jijini Dodoma.
Mikataba hiyo inayohusu usimamizi
madhubuti wa kuboresha masuala ya lishe katika jamii, imesainiwa na Wakuu wa
Wilaya pamoja na Wakurugenzi wa halmashauri mbele ya Mkuu wa Mkoa wa Singida,
Peter Serukamba.
“Hivi karibuni, Rais wetu Mama
Samia alituita Dodoma na kutuagiza kuongeza jitihada katika kuhamasisha
utekelezaji wa shughuli za lishe bora." alisema kisha akaendelea;
Nami nimewaita nyie Ma-DC na
Ma-DED ili kusaini mikataba hii kwa ajili ya kusimamia lishe bora kwenye maeneo
yenu. Nasisitiza, atakayeshindwa jukumu hili atakuwa ametafuta ugomvi na
Serikali"
Pamoja na kusimamia huko,
Serukamba aliwataka Wakurugenzi wa halmashauri zote kuhakikisha wanatenga
1,000/- kwa kila mtoto kwenye bajeti ya mwaka kwa ajili ya utekelezaji wa mpango
wa lishe bora.
“Suala la lishe na afua za lishe
tulipe kipaumbele cha kwanza. Tukifanikiwa kuifanya jamii yetu kuwa na lishe
bora; hasa kwa watoto wa mwaka mmoja hadi mitano, tutakuwa tumeweka jiwe la
msingi kwenye kizazi kijacho," alisema kisha akaendelea;
Tunaweza tukawa tunajiuliza kwa
nini watoto wetu wanafeli sana mitihani tukadhani walimu hawafundishi kumbe
sababu mojawapo ni madhara ya kutopata lishe bora; hasa kutoka kwa mama
anapopata mimba," alifafanua.
Wadau mbalimbali wanasema kuwa
utiaji saini mikataba hiyo ya kusimamia lishe bora kwa Wakuu wa Wilaya na
Wakurugenzi wa halmashauri, umekuja wakati muafaka ambapo Serikali inatekeleza
Programu Jumuishi ya Taifa juu ya Malezi, Makuzi na Maendeleo ya Awali ya Mtoto
(PJ-MMMAM) ya miaka mitano iliyoanza Januari 2021.
Mmoja wa wadau hao, Mganga Mkuu
wa mkoa wa Singida, Dk Victorina Ludovick alisema kuwa chini ya Programu
hiyo ya Taifa inayoshughulika na masuala mtambuka; ikiwemo afya bora, lishe,
malezi yenye mwitikio, fursa za ujifunzaji wa awali na ulinzi na usalama ni
muhimu kwa maendeleo na makuzi ya mtoto chini ya miaka minane.
"Ni dhahiri suala la
udumavu, ukondefu na uzito pungufu kwa kundi hilo litakuwa historia. Hivi sasa
takwimu zinaonesha udumavu kwa watoto walio chini ya miaka mitano limepungua
kwa asilimia 10 katika kipindi cha miaka minane iliyopita. Naamini chini ya
juhudi hizi zilizopewa msisitizo na Rais mwenyewe, changamoto hii inaenda
kwisha” alisema.
Hata hivyo, Utafiti wa Kitaifa wa
hali ya lishe nchini mwaka 2018, unaonesha kuwa asilimia 29.8 ya watoto wenye
umri chini ya miaka mitano mkoani Singida wana tatizo la udumavu, asilimia 5
wanakabiliwa na ukondefu na asilimia 15 ya watoto hao wana uzito mdogo.
Daktari bingwa mshauri wa
magonjwa ya Wanawake na Watoto hospitali ya Rufaa mkoa wa Singida, Dk Suleiman
Muttani anasema pamoja na sababu nyingine, mara nyingi udumavu, ukondefu na
uzito pungufu kwa mtoto ni matokeo ya lishe duni na huleta homa za mara kwa
mara.
“Lishe duni ni chanzo kikubwa cha
magonjwa na vifo kwa watoto wadogo. Hudumaza ukuaji wa kimwili na kiakili
lakini pia hupunguza uwezo wa mtoto kufanya vizuri shuleni na ufanisi wa kazi
katika maisha ya utu uzima.
Ndio maana msisitizo mkubwa wa
lishe bora huwekwa kwa mtoto katika siku 1,000 za mwanzo; yaani tangu mimba kutungwa”
alifafanua.
Baadhi ya wazazi na walezi
wanasema kuwa cha muhimu ni kwa wataalamu wa afya, lishe na wadau wengine
kuendelea kutoa elimu kwa jamii; hususan Vijijini juu ya umuhimu wa lishe bora
hasa kwa akinamama wajawazito, wanaonyonyesha na wenye watoto walio na umri
chini ya miaka mitano.
Kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa, Tanzania ni miongoni mwa nchi ambazo asilimia 43 ya watoto wapo kwenye hatari ya kutofikia hatua timilifu za ukuaji kutokana na viashiria kama vile utapiamlo, umasikini na kukosekana kwa uhakika wa chakula.
Post A Comment: