Mkuu wa Mkoa wa Arusha John Mongella amekitaka chuo cha Ufundi Arusha kifundishe kwa vitendo zaidi, ubunifu na wanafunzi kuwa na uwezo wa kutoa suluhu za changamoto katika jamii.

Ameyasema hayo alipokuwa akiweka jiwe la msingi katika hospitali ya chuo hicho.

Amesema hospitali hiyo itasaidia sana kutoa wataalamu wanaoweza kutumia vizuri vifaa tiba kwani kwa sasa vingi vinaharibika kwa kukosa wataalumu wa kuvitumia.

Jamii inakiamini chuo hicho kwa kutoa wanafunzi wazuri katika vitendo hivyo waendelee na kasi hiyo na kuwa mfano wa kuigwa katika nchi.

Aidha, amewashauri watoe wanafunzi wenye sifa za kuweza kushindana katika soko la ajira la Afrika kwani kwasasa dunia ni kijiji.

Amesisitiza kuwa, Mkoa wa Arusha unamkakati wa kuhakikisha unakuwa kinara wa kutoa huduma bora za afya.

Nae, Mkuu wa Chuo cha Ufundi Arusha Dkt. Musa Chacha amesema hospitali hiyo imejengwa kwa mapato ya ndani na mpaka kukamilika kwake itagharimu Bilioni 1.4.

Amesema ujenzi upo katika hatua za mwisho kwa 92% na wanatarajia utakamilika ifikapo mwisho wa mwezi Novemba, 2022.

Hospitali ya chuo cha ufundi Arusha inajengwa kwa lengo la kusaidia wanafunzi wanaofanya masomo kwa vitendo na hata pia itatoa huduma kwa wananchi.
Share To:

Post A Comment: