Kundi la 16 la wananchi wanaohama kwa hiari kutoka eneo la Hifadhi ya Ngorongoro kwenda Kijiji cha Msomera limeondoka leo tarehe 14 Novemba, 2022 baada ya kuagwa na mkuu wa Wilaya ya Ngorongoro Mhe. Raymond Mangwala.


Kwa mujibu wa Naibu Kamishna wa Uhifadhi NCAA, Needpeace Wambuya, kundi linalohama katika awamu hii linajumuisha kaya 32 zenye wananchi 187 pamoja na Mifugo 1,038.

Naibu Kamishna Wambuya ameeleza kuwa zoezi la kuhamisha wananchi waliojiandikisha kuhama kwa hiari kwenda Kijiji cha Msomera lililoanza mwenzi Juni, 2022 hadi tarehe 14 Novemba, 2022 linapoagwa kundi la 16, Jumla ya kaya 489 zenye watu 2,629 na mifugo 14,094 zimeshahamia Kijiji cha Msomera kwa ajili ya kupisha shughuli za Uhifadhi katika eneo la Ngorongoro.

Wambuya amebainisha kuwa hadi kufikia tarehe 10/11/2022 jumla ya kaya 1, 524 zenye watu 8,715 na migugo 32,842 zimeshaandikishwa kuhama kwa hiari katika eneo la Hifadhi ya Ngorongoro.

Akiwaaga wananchi hao Mkuu wa Wilaya ya Ngorongoro Mhe. Raymond Mangwala amesema

“Msomera mnakohamia kuna Maisha bora kuliko mazingira mnayotoka, zoezi hili la wanaojiandikisha kwa hiari litaendelea kuzingatia misingi ya utawala bora, uwazi, na ushirikishwaji wa wananchi wa tarafa ya Ngorongoro”

Mhe. Mangwala ameongeza kuwa kundelea kujitokeza kwa wanachi wengi ni ishara njema katika kustawisha uhifadhi na ikolojia ya eneo la Ngorongoro kwa kuwa shughuli nyingi za kibinadamu zinapungua na pia wananchi wananufaika kwenda kufanya shughuli za kijamii na kuongeza uchumi wao katika eneo la msomera lililotengwa na serikali ambapo tayari kuna huduma zote muhimu za kijamii.

Bi. Mosoni Laizer kutoka kata ya Olbalbal amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan na Serikali yake kwa kuwafuta machozi kwa kuondokana na hali ngumu ya kuishi na wanyamapori katika eneo moja na kuathiri Maisha yao na Watoto hasa wanapoenda shule.

“Ndani ya Hifadhi Maisha yetu ni magumu sana, Mhe Rais na serikali yake wametufuta machozi, baada ya kutuhamisha tumepewa fidia ya mali zetu na Rais wetu mpendewa ametuongezea pesa ya ziada ili tukaishi vizuri maeneo tunayohamia” ameongeza Bi. Mosoni Laizer.



Share To:

Post A Comment: