Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira na Muungano, Dk Selemani Jafo (kulia)akizindua Chama cha Bioteknolojia Tanzania (BST), katika Mkutano Mkuu uliofanyika katika Ukumbi wa Tume ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) jijini Dar es Salaam.


 Wanachama wa BST wakiwa katika picha ya pamoja na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira na Muungano, Dk Selemani Jafo baada ya kufungua Mkutano wao Mkuu na kuzindua chama.

Na Mwandishi Wetu, Dares Salaam 

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Suleiman Jafo amewataka watafiti na wataalamu waliojikita kwenye teknolojia ya bioteknolojia kufanya tafiti ambazo zitawezesha jamii kupata uelewa na kuondoa hofu iliyopo kuhusu teknolojia hiyo.

Waziri Jafo alisema hayo jana kwenye ufunguzi wa mkutano wa kwanza wa Chama cha Bioteknolojia Tanzania (BST) uliofanyika katika ukumbi wa Tume ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) jijini Dar es Salaam.

Dk Jafo alisema kumekuwa na mkakanganyiko kuhusu bidhaa zinazotokana na bioteknolojia hapa nchini, hivyo njia ya kuondoa hali hiyo ni vema watafiti wakafanya tafiti za kina ambazo zitaiwezesha Serikali kuchukua hatua stahiki.

Alisema taarifa zinaonesha bioteknolojia inatumika kwenye sekta ya afya, viwandani, kilimo na kwingineko ila upingaji au uungaji mkono umejikita katika kilimo hali ambayo inaibua malumbano kila kukicha.

“Sisi Serikali hatuna shida na tafiti kuhusu bioteknolojia, ila msukumo mkubwa utaonekana iwapo tafiti zitafanyika ili kuhakikisha kundi ambalo linapinga ua halina uelewa liweze kuelewa, kwani haiwezekani hata nguo ambazo tunavaa zinatoka na bioteknolojia, lakini wapo watu wanapinga, lazima elimu ya kutosha itolewe,” alisema.

Waziri Jafo alisema wapo watu ambao wanahusisha  bioteknolojia na masuala ya mabadiliko ya tabianchi yaliyopo kwa sasa, hivyo yote hayo ili kuondoa hiyo dhana tafiti na elimu ni muhimu.

Alisema wizara na serikali kwa ujumla wanasubiri maazimio ya BST katika eneo hilo la bioteknoloji, ili iangalie ni njia gani ya kwenda nayo kwa maslahi ya taifa.

“Naahidi kutoa ushirikiano BST kuhakikisha wananchi wanapata uelewa ili nchi isonge mbele kibiashara, kiuchumi na kijamii,” alisema.

Waziri Jafo alisema pamoja na ukweli kuwa bioteknolojia inahusisha sekta nyingi ila BST inajukumu kutoa elimu katika eneo la kilimo ambalo limekuwa likipigiwa kelele, hasa kwa kueleza faida na hasara zilizopo.

inapaswa kuwaelimi wananchi kwa kulinganisha aina ya kilimo kimoja na kingine cha ndani na cha nje ya nchi.

“Nchi kama China, India na nyingine ambazo zina watu wengi zina zinazalisha bidhaa zinazotokana na bioteknolojia, hivyo watafiti na watalaamu wakitumia mifano hiyo na kuwaweka sawa wananchi wanaweza kuelewa na kuimarisha kilimo hicho,”alisema.

Jafo alisema historia inaonesha bioteknolojia ilianza tangu karne ya 19 kwenye ‘Tissue Culture’ hivyo sio jambo geni na kwamba elimu ndio njia itakayoweza kuondoa hofu iliyopo.

Alisema Serikali ina sera ya mazingira ya mwaka 1997 ambayo ilikuwa na kasoro kidogo na kufanyiwa marekebisho mwaka 2021 na sera mpya ya mazingira iliyozinduliwa rasmi mwaka 2022.

Pia alisema ipo sera inayozungumzia bioteknolojia, hivyo ikitumika inavyopaswa itakuwa njia sahihi ya kufikisha elimu kwa jamii.

“Sera ya kilimo ya mwaka 2015 nayo inazungumzia jinsia gani mchakato  wa uangalizi wa kimazingira na bioteknolojia unavyokwenda sambamba katika kusimamia maendeleo ya nchi,” alisema.

Awali akizungumza kwenye mkutano huo wa kwanza wa Mwenyekiti wa BST, Profesa Peter Msolla alisema, matumizi ya bioteknolojia duniani yameleta manufaa makubwa kwenye sekta mbalimbali kama kilimo, afya, mifugo, viwanda na mazingira.

“Bioteknolojia imewezesha uzalishaji wa miche isiyo na vimelea vya magonjwa, mazao bora yasiyoshambuliwa na  visumbufu vya magonjwa na wadudu, pamoja na kupunguza gharama za uzalishaji.

Katika sekta ya afya imerahisisha utambuzi wa magonjwa kwa usahihi, pamoja na utengenezaji wa chanjo na dawa mpya na zenye ubora zaidi kukabili magonjwa sugu kwa mfano insulin kwa wagonjwa wa kisukari, homa ya ini (hepatitis B), saratani ya shingo ya kizazi, magonjwa ya kuhara kwa watoto, na chanjo za VVU/Ukimwi na Uviko-19,” alisema.

Alisema utafiti unaendelea wa kutumia teknolojia hiyo katika kuzuia au kutokomeza ugonjwa wa malaria.

Prof Msola alisema hali kama hiyo imeonekana kwenye  sekta ya mifugo kwa kurahisisha utambuzi wa magonjwa kwa usahihi, kuongeza uzalishaji wa aina bora za mifugo, pamoja na utengenezaji wa dawa na chanjo;

“Katika sekta ya viwanda bioteknolojia imeweza kuongeza ufanisi na tija katika kutengeneza bidhaa mbalimbali za vyakula, pamoja na madawa na kemikali kwa matumizi ya kilimo na viwandani bila kuharibu mazingira.

Katika sekta ya mazingira imechangia kuhifadhi au kuboresha mazingira kwa kupunguza kwa kiasi kikubwa matumizi ya viuatilifu na kubaini mbinu bora za kutambua, kuzuia na kusafisha sumu katika mazingira na kubadilisha taka za mashambani na viwandani kuwa mbolea na gesi,” alisema.

Alisema BST imebaini kuwa uelewa na ufahamu wa baadhi ya wadau kuhusu matumizi ya bidhaa zitokanazo na bioteknolojia ya kisasa (GMO) ni mdogo hali ambayo imesababisha ongezeko la taarifa zisizo sahihi kuhusu teknolojia hiyo na zenye kuleta hofu kwa jamii ya Watanzania.

Mwenyekiti huyo alisema baadhi ya wanasiasa na hasa wabunge wamekuwa na mashaka na wasiwasi juu ya matumizi ya bioteknolojia ya kisasa katika sekta ya kilimo, ingawa wanakubali kwa urahisi matumizi yake katika sekta ya afya.

Aidha, Msola alimpongeza Dk Jakaya Kikwete kwa kutunukiwa Tuzo ya Shujaa wa Bioteknolojia Tanzania kutokana na mchango wake mkubwa katika kuendeleza uvumbuzi wa teknolojia za kisasa ili hatimaye ziwanufaishe  wakulima na taifa letu kwa ujumla.

“Tuzo hiyo ilitolewa na Wakfu ya Teknolojia za Kilimo Afrika (African Agricultural Technology Foundation, AATF) iliyoko Nairobi-Kenya kupitia mradi wake wa Jukwaa la Bioteknolojia za Kilimo Afrika (OFAB),” alisema.

Alisema Kikwete alifanikishwa kurekebisha na kuridhia kanuni za matumizi salama ya bioteknolojia ya kisasa na hivyo kuwezesha nchi kufanya utafiti wa mahindi yanayostahimili ukame na bungua wa mahindi.

Pia aliwezesha utengenezaji, uwekezaji na uzinduzi wa maabara mahiri ya bioteknolojia ya kisasa kwenye kituo cha utafiti TARI-Mikocheni, Dar es Salaam.

“Hii iliwezesha utafiti wa kijenetiki ili kuzalisha mihogo inayostahilimi magonjwa, hususan batobato na michirizi kahawia. Maabara hii ilivutia watafiti na wanataaluma kutoka nchi mbalimbali za Afrika waliokuja kufanyia utafiti wao TARI-Mikocheni,” alisema.

Msola alisema Kikwete alikuza ushirikiano na nchi zinazotuzunguka katika kuendeleza bioteknolojia ya kisasa hususan dhidi ya magonjwa na wadudu waharibifu katika kilimo. “Yeye alitambua fika kwamba haya maadui wa uzalishaji katika kilimo hayana mipaka,” alisisitiza.

Share To:

dottomwaibale

Post A Comment: