Nchi za Tanzania na Norway zimejipanga kuimarisha ushirikiano baina ya nchi hizo ili kukuza uchumi huku mkakati mkubwa ukiwekwa katika kuimarisha sekta ya kilimo ili kuifanya nchi ya Tanzania kufikia malengo ya kukuza sekta hiyo kufikia asilimia 10 kwa mwaka 2030.


Hayo yamezungumwa jana Jijini Dar es salaam wakati kikao baina ya Waziri wa Norway anayeshughulikia masuala ya Ushirikiano wa Maendeleo ya Kimataifa na nchi za Nordic, Mhe. Anne Beathe Tvinnereim na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Liberata Mulamula aliyeongozana na Waziri wa Maendeleo ya Jamii,Wanawake,Jinsia na Makundi Maalum Mh. Dr. Doroth Gwajima pamoja na Naibu Waziri wa Kilimo Mh.Anthony Mavunde.



Nchi za Tanzania na Norway zinashirikiana katika masuala ya elimu, afya, kilimo, uwekezaji, miundombinu, nishati, madini, tehama, utafiti, maboresho kwenye mifumo ya ukusanyaji wa kodi, uchangiaji wa bajeti kuu ya Serikali, misitu, demokrasia, haki za binadamu, usawa wa jinsia, utunzaji wa mazingira na ukuzaji wa sekta ya biashara.


Akizungumza katika mkutano huo Waziri Balozi Mulamula alieleza kuwa Tanzania inathamini ushirikiano uliopo baina yake na Norway kwa kusimamia miradi ya maendeleo iliyo kwenye makubaliano na kuongeza maeneo mapya ya ushirikiano kwa lengo la kujenga uchumi wa Wananchi.


“Norway ni mshirika wa maendeleo wa Tanzania wa muda mrefu na imesaidia kujenga uwezo katika maeneo mbalimbali ya kiutendaji ikiwemo uboreshaji wa mazingira wezeshi ya uwekezaji na biashara, usimamizi wa mfumo wa ulipaji kodi,” alisema Balozi Mulamuala.


Kadhalika, Serikali ya Norway imeongeza muda wa miaka mitano ya utekelezaji wa makubaliano ya majadiliano ya kisiasa yaliyoingiwa kati yake na Tanzania yanaendelea ili kuimarisha ushirikiano katika maeneo ya kipaumbele ya Serikali ya awamu ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan.


Kwa upande wake Waziri Dkt. Doroth Gwajima alieleza kuwa Tanzania ipo tayari kushirikiana na Norway katika utekelezaji wa pendekezo la mpango wa miaka mitano wa kujenga usawa na uwezo kwa wanawake, vijana na makundi maalum unaotegemewa kuinua uchumi na kuwawezesha kuajiriwa na kujiajiri katika kazi rasmi.


Mpango huo pia umezingatia umuhimu wa afya ya uzazi kuwa agenda muhimu ili kuyafikia Malengo ya Mpango wa Maendeleo Endelevu.


Naibu Waziri wa Kilimo, Mhe. Anthony Mavunde alieleza kuwa kupitia sekta ya kilimo Tanzania inayo nia ya kushirikiana na Norway katika masuala ya kujenga uwezo katika vyuo vya kilimo na taasisi zake ili kuwezesha tafiti za sekta hiyo kwa lengo la kuinua uwezo binafsi wa kuzalisha mbegu za mazao, kusimamia usalama wa chakula nchini, kujenga mabwawa na kuimarisha miradi ya umwagiliaji.


Maeneo mengine ya ushirikiano ni pamoja na upatikanaji wa mbolea kwa gharama nafuu, uimarishaji na ujenzi wa miundominu ya kilimo ili kujenga uwezo wa kuzalisha kwa mwaka mzima badala ya kusubiri msimu wa mvua kama ilivyosasa.


Vilevile Wizara ya Kilimo imeandaa mpango wa miradi ya kilimo kwa Wanawake na Vijana itakayotekelezwa katika mikoa ya Mbeya na Dodoma ambapo mradi huo utatumia jumla ya ekari 69,000 hivyo, kupitia ushirikiano uliopo Tanzania ina dhamira ya dhati ya kushirikiana na Norway ili kuyafikia malengo ya uzalishaji yaliyowekwa katika kufanya kilimo cha biashara na kulifikia soko la kimataifa.


Naye Mhe. Tvinnereim ameeleza kuwa Norway imejenga uwezo mkubwa katika masuala ya uzalishaji wa mbegu hivyo itaendelea kushirikiana na Tazania katika eneo hilo na maeneo mengine yaliyoelezwa na mawaziri walioshiriki mazungumzo hayo kwa lengo la kuondoa umasikini, kuongeza nafasi za ajira na kujenga uwezo wa kiuchumi kwa wananchi.

Share To:

Post A Comment: