Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule (kushoto) akifurahia jambo na Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Dkt. John Mduma, baada ya kufungua kikao kazi cha madaktari na watoa huduma za Afya kutoka mikoa ya Kigoma, Tabora, Singida na Dodoma kuhusu namna ya kufanya tathmini za ulemavu utokanao na ajali na magonjwa.

NA K-VIS BLOG/KHALFAN SAID, DODOMA

MKUU wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Rosemary Senyamule amesema hivi sasa wafanyakazi wanao uhakika wa kinga na kipato kutokana na majanga yanayosababishwa na ajali, magonjwa na vifo kutokana na kazi kufuatia uwepo wa Mfuko wa Fidia kwa wafanyakazi (WCF).

Mhe. Senyamule ameyasema hayo jijini Dodoma Septemba 26, 2022 wakati akifungua mafunzo ya tathmini za ulemavu uliosababishwa na ajali na magonjwa yatokanayo na kazi kwa madaktari wa mikoa ya Dodoma, Singida, Tabora na Kigoma.

“WCF ndio inayobeba jukumu la gharama zote pindi Mfanyakazi anapoumia, kuugua ama kufariki kutokana na kazi.” Alifafanua.

Aidha Waajiri nao wanapata muda zaidi wa kushughulikia uzalishaji na uendelevu wa biashara zao na hivyo kuongeza tija inayopelekea kuongezeka kwa pato la taifa.

Alisema uwepo wa Mfuko wa Fidia ni hatua muafaka katika mazingira ya sasa ambapo serikali ya awamu ya sita chini ya uongozi mahiri wa Mhe. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inaendelea na kazi ikiwemo ya kujenga uchumi na hivyo kuwa na ongezeko kubwa la maeneo ya uzalishaji.

“Katika hali ya kawaida ongezeko litakwenda sambamba na ongezeko la matukio na athari zinazotokana na ajali na magonjwa yatokanayo na kazi hivyo jukumu la WCF sio kulipa Fidia pekee bali pia kushirikiana na wadau katika kubuni na kuendeleza mbinu za kupunguza au kuzuia ajali na magonjwa yatokanayo na kazi.” Alisisitiza.

Aliwaasa washiriki kuwa waadilifu wanapotekeleza jukumu hilo la kufanya tathmini ya ulemavu utokanao na ajali au magonjwa yatokanayo na kazi ili WCF iweze kutoa fidia stahiki na kwa wakati.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Dkt. John Mduma, amesema Mfuko unajivunia kufanya vizuri katika uboreshaji wa mifumo ya kielektroniki ya utoaji huduma pamoja na punguzo la kiwango cha uchangiaji kwa sekta binafsi kutoka asilimia 0.6% hadi 0.5% vilevile punguzo kubwa la riba (interest) kwa madeni ya michango ya nyuma.

Alisema Maboresho hayo yanalenga kukuza uzalishaji ambapo sasa Waajiri wa Sekta binafsi wamepewa nafuu kubwa ya kuelekeza nguvu katika uzalishaji mali, huku WCF ikiendelea kulinda nguvukazi ya Taifa.

“Kama unavyofahamu tayari kuna mabadiliko makubwa sana ya uboreshaji wa mazingira ya uwekezaji na biashara hapa nchini ndani ya kipindi cha Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mhe. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, na sisi kama Mfuko tayari tumejipanga kuhakikisha tunaendelea kutoa huduma bora wakati wote.” Alisema Dkt. Mduma.

Ameishukuru Serikali na taasisi zake kwa namna inavyosaidia katika kuhakikisha Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi unaweka misingi imara katika kutekeleza majukumu yake ipasavyo.

Aliwakumbusha Waajiri kutumia fursa hii adhimu ya punguzo iliyowezeshwa na Serikali sikivu ya Awamu ya Sita Ili kuongeza uzalishaji na hivyo kuchochea maendeleo ya kiuchumi.

Akizungumzia kuhusu mafunzo hayo ya alisema yameandaliwa na WCF kama sehemu ya hatua muhimu kuuwezesha kutekeleza vyema jukumu la kufanya tathmini sahihi na hatimaye Fidia stahiki pindi mfanyakazi anapoumia au kuugua kutokana na kazi.

Uelimishaji wa aina hii ni moja ya mikakati ya kuondoa changamoto ambazo zinaukabili Mfuko mpaka sasa, kwani Mfuko unatambua umuhimu wa Mafunzo haya kwa Wataalamu ili kuwawezesha kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi na uweledi wa hali ya juu na hatimaye kusaidia Mfuko kutimiza lengo lake la kutoa fidia stahiki na kwa wakati.


Share To:

Post A Comment: